Nafasi Ya Matangazo

January 04, 2026

Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam
Jumla ya Wapiga Kura 20,851 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki katika uchaguzi wa kuchagua madiwani katika Kata ya Kirua Vunjo Magharibi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi Mkoa wa Kilimanjaro na Kata ya Mindu iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro Mkoa wa Morogoro.
 
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele leo Januari 04, 2026 wakati akisoma risala maalum kuhusu uchaguzi katika Kata hizo utakao fanyika Januari 05,2026 na kusema kuwa jumla ya vituo 55 vya Kupigia Kura vitatumika.
 
Aidha, amesema jumla ya wagombea watano (5) kutoka katika vyama vya siasa vinne (4) wanawania nafasi wazi za udiwani katika maeneo hayo na kuvipongeza vyama vya siasa na wagombea waliojitokeza kushiriki katika uchaguzi huo.
 
“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho Januari 05,2026 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Majimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.
 
Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.
 
Jaji Mwambegele amesema vituo vitafunguliwa saa 01:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni. Ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapiga kura bado wapo kwenye mistari, mlinzi wa kituo atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapiga kura walio kwenye mstari watakapomalizika.
 
“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpiga kura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura; na Mpiga kura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapiga kura,”alisema Jaji Mwambegele.
 
Kwa mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi yake au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga Kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, Leseni ya udereva au Pasi ya kusafiria (Passport).
Posted by MROKI On Sunday, January 04, 2026 No comments

January 02, 2026



Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akisikiliza maelezo kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa mazingira Dar es salaam,  (DAWASA), Mhandisi Mkama Bwire (kulia) alipokagua maendeleo ya ujenzi wa Bwawa la Maji la Kidunda mkoani Morogoro, Januari 2, 2026. Wa tano kulia  ni Waziri wa Maji, Jumaa Aweso na wa tatu kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima. 
Muonekano wa hatua  iliyofikiwa ya ujenzi wa Bwawa   la Maji la Kidunda mkoani Morogoro ambalo Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba alikagua ujenzi wake, Januari 2, 2026. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
02 Januari, 2026
***********
WAZIRI MKUU Dkt Mwigulu Nchemba ameiagiza Wizara ya Maji kuhakikisha mradi wa Bwawa la Maji Kidunda hausimami na unakamilika kwa wakati ili uanze kutoa huduma ya maji kwa wananchi.

Ametoa wito huo leo (Ijumaa, Januari 02, 2026) wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa bwawa hilo lililopo Wilaya ya Morogoro, mkoani Morogoro. 

Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Dkt. Mwigulu amesema kuwa mradi huo unaakisi maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha anakabiliana na changamoto ya upungufu wa maji hasa kutokana na mabadiliko ya tabianchi.

“Kiongozi wetu anaona mbali; aliamua kuutekeleza mradi huu katika kipindi ambacho kulikuwa na utekelezaji wa miradi mingine mikubwa na ya kimkakati iliyotumia fedha nyingi. Serikali inachukua hatua ili kukabiliana na changamoto za Watanzania.”

Wakati huohuo, Dkt. Mwingulu ameiagiza Wizara ya Maji wahakikishe wanaandaa jedwali litakalomsaidia mkandarasi katika utekelezaji wa mradi huo ili uweze kukamilika kwa wakati.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema kuwa kukamilika kwa mradi huo utakaogharimu shilingi bilioni 366 kutasaidia kuzalisha takribani megawati 20 za umeme. Amesema mbali na kutoa huduma ya maji, mradi huo utawezesha ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilomita 72.

Ameongeza kuwa mradi huo utasaidia kuhifadhi lita bilioni 190 za maji zitakasaidia matumizi ya nyumbani hasa kipindi cha ukame wakati kina cha mto Ruvu kinapopungua.

Naye, Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo amesema mradi huo utasaidia katika sekta ya kilimo kwani eneo kubwa linalozunguka bwawa hilo ni zuri kwa ajili ya shughuli za kilimo hivyo wizara itawezesha kilimo cha umwagiliaji katika maeneo hayo.
Posted by MROKI On Friday, January 02, 2026 No comments

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amtembelea na kumjulia hali, Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mohamed Gharib Bilal, katika makazi yake Masaki Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 02 Januari 2026.
Posted by MROKI On Friday, January 02, 2026 No comments


Na Abdala Sifi WMJJWM - Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe, Dkt Samia Hassan Suluhu ametoa zawadi kwa Watoto wanaolelewa katika makao mbalimbali nchini kwa lengo la kuwapa faraja na upendo msimu huu wa sikukuu.
 
Zawadi hizo zimetolewa na Kamishna Msaidizi wa Ustawi wa Jamii wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maalum, Mussa Mkamate kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. John Jingu. 

Akikabidhi zawadi hizo tarehe 01 Januari, 2026 Kamishna Mkamate amesema zawadi hizo zimetolewa na Rais kwa lengo la kuwapa faraja na upendo watoto na kusherehekea kwa furaha sikukuu za mwisho wa mwaka.  

Amesema kuwa kwa kutambua umuhimu wa matunzo ya Watoto Rais Samia ametoa zawadi hizo katika vituo vya vinavyotoa huduma ya malezi ya Watoto ambavyo ni Kijiji cha Matumaini pamoja na Kituo cha KISEDET vilivyopo Mkoani Dodoma . 

“Napenda kukabidhi zawadi hizi zikiwemo mchele, maharage, sukari  vinywaji pamoja na mbuzi ambazo zimetolewa na Mheshimiwa Rais, kwa lengo la kuwatakia heri watoto hawa na kusherekea vyema mwaka mpya”amesema Mkamate.

Aidha ameongeza kwamba jamii inapaswa kuwalea na kuwatunza watoto kwa kuwapa mahitaji yao ya msingi, kudumishi amani na upendo katika familia ili kuepusha migogoro ambayo ndiyo imekuwa miongoni mwa sababu za kutelekeza watoto. 

Naye Msimamizi wa Kituo cha Kijiji cha Matumaini Vicent Bosseli amemshukuru Rais Samia kupitia Wizara pamoja na Ofisi ya Mkuu  Mkoa wa Dodoma kwa kutoa zawadi hizo kwa ajili ya watoto kwani zitaleta faraja katika kusheherekea Sikukuu ya Mwaka mpya kwa watoto hao.
Posted by MROKI On Friday, January 02, 2026 No comments

January 01, 2026

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela, ametembelea Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB iliyopo Dubai, Falme za Kiarabu, ikiwa ni hatua muhimu kuelekea uzinduzi rasmi wa ofisi hiyo unaotarajiwa kufanyika mapema Januari 2026.

Katika ziara hiyo, Nsekela alipokea taarifa ya kina kuhusu utekelezaji wa shughuli za ofisi tangu ilipoanza kazi rasmi Oktoba 2025, akiongozwa na Mwakilishi wa CRDB Bank Dubai, Jackson Kehengu. Taarifa hiyo ilieleza mafanikio ya awali katika kujenga mahusiano na wawekezaji, wafanyabiashara wakubwa, na washirika wa kifedha, ambao wameonesha kuvutiwa kwa kiwango kikubwa na upanuzi wa Benki ya CRDB katika Mashariki ya Kati.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Nsekela alisema Dubai ni kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji duniani, hasa katika kipindi cha baada ya janga la UVIKO-19 na mabadiliko ya kiuchumi yaliyoshuhudiwa katika miaka ya karibuni. Alisema Benki ya CRDB imeona fursa ya kimkakati ya kuunganisha wafanyabiashara na wawekezaji kati ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Afrika Mashariki.

“Benki ya CRDB kwa miaka mingi imekuwa mdau muhimu katika kuwezesha biashara na uwekezaji Tanzania na Afrika Mashariki, hususan Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo,” alisema Bw. Nsekela. “Ofisi ya Dubai inalenga kuimarisha daraja hili la kifedha kati ya Mashariki ya Kati na Afrika Mashariki.”

Nsekela alieleza kuwa Benki inajivunia hatua hii kubwa ambayo inaleta mchango chanya kwa uchumi wa Tanzania na ukanda mzima wa Afrika Mashariki. Alitoa shukrani kwa Serikali ya Tanzania kwa sera bora zilizowezesha hatua hiyo, na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa sera zake nzuri za diplomasia ya uchumi zilizoimarisha mazingira ya uwekezaji na ushirikiano kimataifa.

Aidha, aliishukuru Ubalozi wa Tanzania UAE, Benki Kuu ya Tanzania, Malamka ya Usimamizi wa Huduma za Fedha Dubai (DFSA), pamoja na Kituo cha Kimataifa cha Huduma za Fedha Dubai (DIFC) ambapo ofisi hizo zipo, kwa ushirikiano wao katika kufanikisha kuanzishwa kwa ofisi hiyo.


Akizungumza kuhusu fursa za kiuchumi, Nsekela alisema thamani ya biashara kati ya Tanzania na UAE sasa imezidi dola za Marekani bilioni 2.2, jambo linaloonesha nafasi kubwa ya kuvutia mitaji na uwekezaji zaidi.

Alitoa wito kwa wafanyabiashara na wawekezaji kutumia Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai kama lango la kupata huduma za kifedha, ushauri wa uwekezaji, na kuunganishwa na fursa mbalimbali nchini Tanzania na Afrika Mashariki, pamoja na Falme za Kiarabu.

Nsekela aliongeza kuwa pamoja na kuvuka mipaka hadi nje ya bara la Afrika, Benki hiyo itaendelea na mkakati wake wa kupanua wigo wa huduma zake katika nchi za ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati, na bara la Afrika kwa ujumla.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Mawasiliano na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa (kulia), na Mkurugenzi Mwakilishi wa Benki ya CRDB Dubai, Jackson Kehengu alipotembelea Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya uzinduzi rasmi wa ofisi hiyo unaotarajiwa kufanyika mapema mwezi huu.
Posted by MROKI On Thursday, January 01, 2026 No comments





Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeendelea kuvunja rekodi yake yenyewe ya makusanyo kwa kukusanya kodi kiasi cha Sh. Trilioni 4.13 kwa mwezi Desemba pekee sawa na ufanisi wa asilimia 102.9 wa lengo la kukusanya Sh. Trilioni 4.01.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam tarehe 01.01.2026 Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda amesema katika kipindi cha Oktoba hadi Desemba TRA imekusanya kiasi cha Sh.  Trilioni 9.8 sawa na ufanisi wa asilimia 101.45 ya lengo la kukusanya Sh. Trilioni 9.66.

Amesema makusanyo hayo ni sawa na ukuaji wa asilimia 12.26 toka Sh. Trilioni 8.73 zilizokusanywa katika kipindi kama hicho mwaka 2024/2025 ambapo ongezeko la makusanyo hayo ya kodi limetokana na kuongezeka kwa ulipaji kodi kwa hiari nchini.

Kamishna Mkuu Mwenda amesema tangu kuanza kwa mwaka wa fedha 2025/2026 TRA imevuka malengo ya makusanyo kwa kila mwezi jambo ambalo limesababishwa na uhimilivu wa shughuli za uchumi uliojengwa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan. 

"Mhe. Rais amejenga uhimilivu wa shughuli za uchumi ambao umeonyesha matokeo katika makusanyo ya kodi na miongozo ambayo tumekuwa tukipewa na Serikali ya awamu ya sita imeonyesha kuwa na matunda" amesema Mwenda. 

Amesema kuwa wastani wa makusanyo kwa mwezi katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2025/2026 umefikia Sh. Trilioni 3.13 ambacho ni kiasi cha juu kabisa ukilinganisha na Wastani wa Sh. Trilioni 2.75 kwa kipindi kama hicho mwaka 2024/2025.

Ametaja sababu nyingine zilizoongeza makusanyo kuwa ni kuendeleza ushirikiano na wafanyabiashara pamoja na vyama vya wafanyabiashara, kuendelea kuboresha mahusiano na Walipakodi na kuendelea kusimamia utendaji mzuri, nidhamu na kuchochea ubunifu. 

Kuendelea kuhimiza utatuzi wa migogoro ya kikodi kwa njia ya majadiliano na makubaliano ya nje ya mahakama nako kumeongeza mapato maana katika kipindi cha Oktoba hadi Desemba 2025 kulikuwa na makubaliano maalum 42 yenye thamani ya kodi ya Sh. Bilioni 9.4.

"Kuendelea kufuatilia kwa karibu hali ya ufanyaji biashara nchini kwa kusimamia kikamilifu uzalishaji wa viwandani pamoja na kuendelea kuhimiza matumizi ya mashine za kielekitroniki (EFD) nchini na kuwa na mifumo ya kisasa ya kunusanyaji wa kodi kumechangia mafanikio haya" amesema Mwenda. 

Kamishna Mkuu Mwenda amesema ufanisi wa mapato uliofikiwa na TRA ni kiashiria chanya katika kuhakikisha kuwa lengo la makusanyo kwa mwaka wa fedha 2025/2026 la Sh. Trilioni 36.06 linafikiwa.

Amesema TRA imeweka lengo la kuhakikisha kuwa sehemu ya makusanyo ya Mapato kwenye pato la Taifa kwa mwaka 2025/2026 inakuwa ni zaidi ya asilimia 14.1 today kwenye kiwango cha asilimia 13.7 kilichorekodiwa mwaka 2024/2025.
Posted by MROKI On Thursday, January 01, 2026 No comments

December 30, 2025






Hombolo - Dodoma
Kuelekea Mwaka Mpya 2026, Wakala wa Nishati Vijijini (REA), imewagusa Watanzania wenye mahitaji mbalimbali kwa kutoa mkono wa faraja na kuwatakia heri ya mwaka Mpya ujao.

Zoezi la kuwapatia mahitaji walemavu limeongozwa na Bi. Judith Abdalah kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA mha. Hassan Saidy ambapo REA imetoa mahitaji mbalimbali kwa Kikundi cha Walemavu wa Ukoma waliopo Kata ya Hombolo jijini Dodoma. 

Akiwasilisha salamu za REA, Bi. Abdalah amewataka walemavu wa Ukoma kuishi kwa upendo na amani na kusisitiza kuwa, REA itaendelea kuwashika mkono kwa kuwapatia mahitaji mbalimbali ili wakue kiuchumi na kijamii. 

Halikadhalika, Swalehe Kibwana Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi Tawi la REA (TUGHE), amesema zoezi hilo la kuwafikia na kuwasaidia wahitaji mbalimbali ni endelevu na REA itaendelea kutoa mahitaji kwao hususan kwa walemavu wa ukoma waliopo Hombolo. 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kikundi cha Wanawake na Samia mkoa wa Dodoma Bi. Fatuma Madudu ameishukuru REA kwa kufika Hombolo na kuwasaidia walemavu wa ukoma katika sehemu hiyokwa kuwapatia mahitaji mbalimbali. 

Naye, Katibu wa Walemavu Hombolo ametoa rai kwa wadau mbalimbali kujitokeza kuwashika mkono Walemavu wa ukoma na kuwapatia mahitaji mbalimbali ikiwemo chakula ili nao waweze kufurahia sikukuu ya kuukaribisha Mwaka Mpya wa 2026.
Posted by MROKI On Tuesday, December 30, 2025 No comments
Mbunge wa Jimbo la Mtumba Mh. Anthony Mavunde leo amekabidhi awamu ya kwanza ya madawati 2700 kwa ajili ya Shule za Sekondari za Jiji la Dodoma kufuatia maelekezo ya Mh. Rais Dkt. Samia S. Hassan kutaka kukamilika kwa miundombinu ya madarasa na upatikanaji wa madawati ya kuwapokea wanafunzi wapya wa kidato cha Kwanza Januari 2026.

Mbunge Mavunde amelipongeza Jiji la Dodoma kwa hatua za makusudi za kuhakikisha upatikanaji wa madawati ya kutosha zaidi ya 2713 ili wanafunzi wasome katika mazingira bora.

“Hii ni hatua kubwa katika kuboresha sekta ya Elimu ndani ya Jiji la Dodoma kwa kuweka mazingira bora ya kusomea ya wanafunzi wetu”Alisema Mavunde

Akizungumza katika hafla hiyo fupi,Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mh. Jabir Shekimweri amesema ni wajibu wa watu wote kuyatunza madawati hayo ili yawafae wanafunzi wengi kwa siku zijazo.

Naye Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Dkt. Fredrick Sagamiko amesema Jiji la Dodoma limejipanga kuhakikisha wanafunzi wote wanasoma katika mazingira rafiki na kwamba hatua ya utoaji wa madawati 800 leo ni hatua ya kwanza ya kukamilisha madawati 2713 ili kuwafikia kundi kubwa la wanafunzi wa Jiji la Dodoma.






Posted by MROKI On Tuesday, December 30, 2025 No comments
Mkazi wa Shehia ya Migombani katika jimbo la Fuoni akipiga kura leo kumchagua Mbunge wa jimbo hilo. 
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele akiwa na mkazi wa Shehia ya Fuoni aliyekua akihakiki jina lake kabla ya kuingia kupiga kura leo. 
Mjumbe wa Tume, Mhe. Magdalena Rwebangira akizungumza mmoja wa wasimamizi wa viuo vya kupigia Kura katika jimbo la Fuoni Mjini Zanzibar leo. 
Mkazi wa Shehia ya Migombani katika jimbo la Fuoni akipiga kura leo kumchagua Mbunge wa jimbo hilo katika kituo cha Skuli ya Raudha B. 


Mwenyekiti wa Tume na Mjumbe wa Tume hiyo wakizungumza na Mawakala katika moja ya vituo vya kupigia Kura. 



Wananchi wa Jimbo la Fuoni na Siha pamoja na Kata tano za Tanzania bara wamejitokeza kwawingi kupiga kura leo Desemba 30,2025 katika Uchaguzi mdogo uliofanyika katika majimbo yao.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele leo Desemba 30,2025 ametembelea na kushuhudia zoezi la upigaji kura katika Jimbo la Fuoni lililopo Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini Magharibi, Tanzania Zanzibar na kusema zoezi hilo linakwenda vizuri na wananchi wamejitokeza kwa wingi licha ya asubuhi kuwa na mvua.
 
Aidha, Jaji Mwambegele amesema katika Jimbo la jimbo la Siha lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Siha, Mkoa wa Kilimanjaro, Tanzania Bara ambako nako uchaguzi wa Mbunge unafanyika zoezi hilo linakwenda vizuri.
 
Jaji Mwambegele amesema, uchaguzi mdogo huo unahusisha pia, kata tano za Tanzania Bara ambazo ni Chamwino iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Mkoa wa Morogoro; Mbagala Kuu iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam; na Nyakasungwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa, Mkoa wa Mwanza.
 
Kata nyingine ni Kata ya Masoko iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Mkoa wa Mbeya; na kata ya Ndono iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, Mkoa wa Tabora.
 
Mwenyekiti huyo wa Tume katika ziara hiyo aliambatana na Mjumbe wa Tume Mhe. Magdalena Rwebangira.
Posted by MROKI On Tuesday, December 30, 2025 No comments
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na baadhi ya wafanyabiashara wa soko la Bunju B, alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa soko  hilo pamoja na ujenzi wa Kituo cha Mabasi, Jijini Dar es Salaam, Desemba 29, 2025. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na wakazi wa Bunju B wakati alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Soko pamoja na Kituo cha Mabasi, Bunju B jijini Dar es Salaam, Desemba 29, 2025.
***************
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa maelekezo ya kuboreshwa kwa miundombinu ya Soko na Stendi ya Bunju wilayani Kinondoni ili kuwezesha wafanyabiashara na wananchi kuendesha shughuli zao kwa ufanisi na kuongeza fursa za kiuchumi katika eneo hilo.

Katika ziara yake ya kikazi Bunju, Waziri Mkuu alisema soko hilo bado ni jipya na linapaswa kuendeshwa kwa kuzingatia uhalisia wa biashara. Alisisitiza kuwa tozo na ushuru vinapaswa kwenda sambamba na hatua ya ukuaji wa soko.

“Hili ni soko jipya, lazima tulipe nafasi likue. Tozo na ushuru viendane na uhalisia wa biashara ili wafanyabiashara wetu waweze kuimarika na kuongeza kipato,” alisema Waziri Mkuu.

Serikali imetambua kuwa meza, vibanda na bidhaa za wafanyabiashara wadogo ndizo mitaji na ofisi zao, hivyo viongozi wa Serikali za Mitaa wameagizwa kuhakikisha wanazingatia mazingira ya soko kabla ya kutoza ushuru au kuchukua hatua zinazoweza kudhoofisha shughuli za kiuchumi za wananchi.

“Meza hizi, vibanda hivi na bidhaa hizi ndizo mitaji ya wafanyabiashara wetu. Hatuwezi kuzichukulia kama vitu vya kawaida; lazima tuzilinde,” alisisitiza Dkt. Nchemba.

Akizungumza katika ziara hiyo, Waziri Mkuu alionyesha kuwa utekelezaji wa miradi ya masoko na miundombinu ya usafiri ni sehemu ya maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuendelea kuboresha mazingira ya biashara, kuongeza ajira na kuinua uchumi wa wananchi katika maeneo ya mijini na vijijini.

“Maelekezo haya tunayoyatekeleza ni sehemu ya dhamira ya Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha wananchi wanapata mazingira bora ya kufanya kazi na kujipatia kipato,” alisema Waziri Mkuu.

Kuhusu Stendi ya Bunju, Waziri Mkuu alisema Serikali imepokea maoni ya wananchi kuhusu mpangilio wa usafiri na athari zake kwa gharama za maisha, hususan kwa abiria wanaolazimika kubadilisha magari zaidi ya moja. Ameelekeza mamlaka husika kufanya tathmini ya mpangilio huo ili kulinda maslahi ya wananchi bila kuathiri utoaji wa huduma za usafiri.

Aidha, katika hatua za awali za uendeshaji wa soko hilo, Waziri Mkuu ameagiza mamlaka husika zizingatie kupunguza au kuahirisha ushuru kwa kipindi maalum ili kutoa nafasi kwa wafanyabiashara kujiimarisha na kuvutia wateja. Amesema Serikali imejipanga kutenga fedha katika bajeti ijayo kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya masoko, ikiwemo barabara za kuingia sokoni, maeneo ya maegesho na mazingira rafiki yatakayochochea biashara na maendeleo ya maeneo yanayoyazunguka masoko hayo.

Akihitimisha ziara hiyo, Waziri Mkuu aliwataka wananchi wa Jiji la Dar es Salaam kuwa makini na wageni wanaowapangisha nyumba zao, akibainisha kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakikodi nyumba kwa bei ndogo kisha kuzikodisha tena kwa bei kubwa, huku wengine wakizikodisha kwa watu wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu vinavyohatarisha amani na usalama wa jamii.

“Wananchi wawe makini na wageni wanaowapangisha nyumba. Wengine wanazitumia vibaya nyumba hizo na kuhatarisha amani na usalama wa jamii,” alionya.

Katika ziara hiyo, Waziri Mkuu aliambatana na viongozi wengine wakiwemo Waziri wa Maji, Jumaa Aweso; Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Dkt. Jafar Seif; Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, pamoja na viongozi wengine wa Serikali.
Posted by MROKI On Tuesday, December 30, 2025 No comments

December 29, 2025

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele leo Desemba 29,2025 amesoma risala maalum kuhusu uchaguzi wa ubunge katika jimbo la Siha lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Siha, Mkoa wa Kilimanjaro, Tanzania Bara na Jimbo la Fuoni lililopo Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini Magharibi, Tanzania Zanzibar unaotaraji kufanyika Desemba 30,2025.
 
Jaji Mwambegele amesema, uchaguzi mdogo huo utahusisha pia, kata tano za Tanzania Bara. Kata hizo ni;            Chamwino iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Mkoa wa Morogoro; Mbagala Kuu iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam; na Nyakasungwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa, Mkoa wa Mwanza.
 
Nyingine ni Kata ya Masoko iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Mkoa wa Mbeya; na kata ya Ndono iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, Mkoa wa Tabora.
 
Aidha, amesema jumla ya wagombea 33 kutoka katika vyama vya siasa 17 wanawania nafasi wazi za ubunge na udiwani katika maeneo niliyoyataja. Kati ya wagombea 33, wagombea 21 sawa na asilimia 63.64 ni wanaume na wagombea 12 sawa na asilimia 36.36 ni wanawake. Kwa namna ya pekee, Tume inavipongeza vyama vilivyoshiriki na wagombea waliojitokeza kushiriki.
 
Jaji Mwambegele amesema, jumla ya Wapiga Kura 218,024 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki katika uchaguzi huo na jumla ya vituo 556 vya Kupigia Kura vitatumika.
 
“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho tarehe 30 Desemba, 2025 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Majimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.
 
Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.
 












Posted by MROKI On Monday, December 29, 2025 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo