Nafasi Ya Matangazo

February 20, 2025




Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa, ambaye pia ni Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mlezi wa CCM kwa Mikoa ya Kusini na Kaskazini Unguja, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, amesema kuwa CCM imejipanga kikamilifu kuhakikisha inaendelea kushika dola katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, kwa kuwa kazi iliyofanywa na Serikali inatosha kutangaza sera za ushindi.

Dkt. Tulia ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na Wanachama wa CCM katika Ukumbi wa CCM Hanyegwamchana, mara baada ya kuhitimisha ziara yake ya kikazi katika Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, leo tarehe 20 Februari 2025. Ziara hiyo ililenga kukagua miradi mbalimbali ya CCM pamoja na kuwaeleza wananchi kuhusu malengo ya CCM katika mkoa huo.

Aidha, Dkt. Tulia amewahimiza vijana wa CCM wenye sifa za kugombea nafasi mbalimbali za Uongozi kujitokeza kwa wingi, ili waweze kuonesha uwezo wao na kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa taifa. Amesisitiza kuwa CCM ina sera shirikishi zinazotoa fursa kwa kila mtu wakiwemo vijana, kushiriki katika Uongozi na maendeleo ya nchi.

“Ndani ya Chama hiki tunaunganishwa na imani yetu. Kipindi cha Uchaguzi si muda wa kunyoosheana vidole au kuoneshana ubaya, bali ni wakati muhimu wa kushikamana ili kupata ushindi wa kishindo. Hiyo ndiyo sera yetu kuu,” amesema Dkt. Tulia.
Posted by MROKI On Thursday, February 20, 2025 No comments






Na: Mwandishi Wetu, Dar
Maisha ya Watanzania wengi yamebadilika kutokana na kazi kubwa iliyofanywa na serikali kupitia Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu ( HESLB) katika kuwawezesha kufikia ndoto zao za kielimu na kimaisha baada ya kunufaika na mikopo ya elimu ya juu.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Dk. Bill Kiwia kwenye maadhimisho ya miaka 20 tangu kuanzishwa Bodi ya Mikopo yaliyofanyika Februari 15, 2025 kwenye viwanja vya Farasi, Oysterbay, jijini Dar es Salaam ambapo maadhimisho hayo yaliambatana na mbio za hisani ( HESLB Marathon).

Katika hotuba yake iliyojaa takwimu za kimafanikio kuhusiana na miongo miwili (miaka 20) tangu kuanzishwa Bodi ya Mikopo, Dk. Kiwia amesema wakati Bodi ya Mikopo inaanzishwa mwaka 2004, ni wanafunzi 48,000 pekee ndiyo waliokuwa wakinufaika, ambapo bajeti yake ilikuwa Bilioni 53.1. Aidha Kwa mwaka wa fedha 2024/2025, Bodi imetoa mikopo kwa wanafunzi 245,799 huku mikopo hiyo ikigharimu Bilioni 787, na kwa ujumla wake, katika miaka 20 ya Bodi, jumla ya wanufaika wote imefika 830,000 huku mikopo yote iliyotolewa ikigharimu Trilioni 8.2. 

"Kwa mwaka 2024/2025, shilingi Bilioni 787 zimetolewa kwa ajili ya wanafunzi 245,799 ambapo jumla ya mikopo iliyotolewa na Bodi tangu kuanzishwa kwake ni shilingi Trilioni 8.2 ambacho kimewezesha kusomesha wanafunzi 830,000 nchi nzima," amesisitiza Dk. Kiwia.

Mbio hizo za hisani za HESLB Marathon zilifana ambapo watu mbalimbali walijitokeza kushiriki huku wengi wakipongeza kazi nzuri zilizofanywa na Bodi ya Mikopo katika kipindi cha miaka 20 zilizowezesha vijana wengi kupata elimu ya juu.
Posted by MROKI On Thursday, February 20, 2025 No comments

February 19, 2025

Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Balozi Omari Ramadhani Mapuri akizungumza wakati akifunga mafunzo ya siku mbili kwa Waratibu wa Uandikishaji wa mkoa, Maafisa Waandikishaji, Maafisa Waandikishaji Wasaidizi ngazi ya Jimbo, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ugavi na Maafisa TEHAMA wa halmashauri yaliyoanza tarehe 18 hadi 19 Februari, 2025 Mkoani Morogoro . Zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Mpiga Kura mkoani humo linataraji kuanza Machi mosi 2025 na kufikia tamati Machi 07,2025 huku vituo vikitaraji kufunguliwa Saa 2:00 asubuhi na kufungwa Saa 12:jioni kwa siku zote saba.
Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Balozi Omari Ramadhani Mapuri akizungumza wakati akifunga mafunzo ya siku mbili kwa Waratibu wa Uandikishaji wa mkoa, Maafisa Waandikishaji, Maafisa Waandikishaji Wasaidizi ngazi ya Jimbo, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ugavi na Maafisa TEHAMA wa halmashauri yaliyoanza tarehe 18 hadi 19 Februari, 2025 Mkoani Morogoro . Zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Mpiga Kura mkoani humo linataraji kuanza Machi mosi 2025 na kufikia tamati Machi 07,2025 huku vituo vikitaraji kufunguliwa Saa 2:00 asubuhi na kufungwa Saa 12:jioni kwa siku zote saba.
Washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia hotuba za kufunga.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akiwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Ndg. Kailima R. K wakati wa kufunga mafunzo hayo. 
Mwenyekiti wa Mafunzo ambaye pia ni Afisa Mwandikishaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero, Ndg. Emmanuel Vuri akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo. 
Meza kuu ikimsikiliza Mwenyekiti wa mafunzo.

Mjumbe Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Magdalena Rwebangira akiwa wakati wa kufunga mafunzo hayo. Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Ndg. Kailima R. K akizungumza jambo na washiriki.

Washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia hotuba za kufunga.
******************
Na. Mwandishi Wetu
Watendaji wa uboreshaji wa Daftari; la Kudumu la Wapiga Kura wameaswa kutekeleza majukumu waliyopewa kwa kuzingatia sheria, kanuni, maelekezo na miongozo itakayotolewa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi.
 
Wito huo umetolewa na Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Balozi Omari Ramadhan Mapuri wakati akifunga mafunzo ya watendaji wa uboreshaji wa daftari mkoani Morogoro leo Februari 19, 2025.
 
“Mnapaswa kutekeleza majukumu mliyopewa kwa kuzingatia sheria, kanuni, maelekezo na miongozo itakayotolewa na Tume,” amewaasa watendaji hao ambao wamehudhuria mafunzo ya siku mbili. 
 
Balozi Mapuri ametoa wito kwa watendaji hao kuendelea kutumia muda wao wa ziada kusoma na kupitia maelekezo yote waliyopewa ili kuongeza uelewa zaidi kuhusu wajibu na majukumu yao wakati wa kutekeleza zoezi lililopo mbele yao.
 
Akifunga mafunzo kama hayo mkoani Tanga, Mjumbe wa Tume ambaye pia ni Jaji wa Mahakama Kuu, Asina Omari amewataka watendaji hao kusoma katiba na sheria ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
 
“Someni kwa makini Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sheria ya Uchaguzi, Kanuni za uboreshaji, Maelekezo na Miongozo yote inayotolewa na Tume ili kazi yenu ifanyike kwa unadhifu na haki,” amesema.
 
Jaji Asina amewakumbusha watendaji hao juu ya wajibu wao wa kuhamasisha wananchi wenye sifa ili wajitokeze kujiandikisha na kupata haki yao ya kikatiba itakayowawezesha kushiriki katika kuchagua viongozi wao kwenye uchaguzi mkuu utakoafanyika mwaka huu.
 
Uboreshaji wa Daftari  utafanyika mkoani Morogoro na kwenye Mkoa wa Tanga katika Halmashauri za Wilaya ya Bumbuli, Handeni, Pangani na Mkinga kwa siku saba kuanzia tarehe 01 hadi 07 Machi, 2025 ambapo vituo vitakuwa vinafunguliwa saa 02:00 asubuhi na kufungwa saa 12:00 jioni.
Posted by MROKI On Wednesday, February 19, 2025 No comments



Mjumbe wa Kamati kuu ya Halmashauri kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) taifa ambaye pia ni Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mlezi wa CCM Mikoa ya Kusini na Kaskazini Unguja, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, amewataka Wanachama wa Chama hicho kusimama kifua mbele katika kuyasema mazuri yanayofanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Dkt. Tulia ameyasema hayo leo tarehe 19 Februari, 2025 wakati akizungumza na Wana-CCM mara baada ya kuhitimisha ziara yake ya kikazi katika Mkoa wa Kaskazini Unguja iliyokuwa na lengo la kukagua miradi mbalimbali ya Chama hicho katika Mkoa huo.

Aidha, Dkt. Tulia amewasisitiza Wanachama wa Chama hicho kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura katika tarehe zilizopangwa ili kufanikisha ushindi wa kishindo katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025.

Dkt. Tulia amesisitiza umuhimu wa Wanachama hao kuendelea kuwa wamoja wakati wote na kuepuka kutengeneza makundi yasiyo na tija kwa Chama na taifa. Kufanya hayo itasaidia kuunga mkono kazi nzuri inayofanywa na Chama hicho chini ya Viongozi wao wakuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi, Rais wa Serikali ya Mapunduzi Zanzibar.

Sambamba na hayo, Dkt. Tulia ametoa mchango wa Shilingi Milioni tano (Tsh: 5,000,000/-) kwa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Kaskazini Unguja ili kuunga mkono ujenzi wa jengo la kitega Uchumi la Wanachama hao.


Posted by MROKI On Wednesday, February 19, 2025 No comments










Na Josephine Maxime- Dar es Salaa
           
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mheshimiwa Dkt. Doto Biteko ameagiza Mwanafunzi Mirabelle Msukari na Wenzake wa Shule ya Msingi Sun Rise iliyopo Wilayani Kinondoni jijini Dar es Salaam kupelekwa katika Mradi wa kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) ili kujifunza zaidi kwa Vitendo namna mradi huo unavyozalisha Umeme.

Mheshimiwa Biteko amesema  hayo leo Februari 18 kwa njia ya simu baada ya Naibu Waziri wa Nishati Mheshimiwa Judith Kapinga  kutembelea shule hiyo kwa lengo la kumpongeza mwanafunzi huyo ambaye video yake ilijizolea umaarufu kupitia mitandao ya kijamii ambapo  Mirabelle alielezea kwa ufanisi juu ya miradi mbalimbali ya umeme inayotekelezwa nchini ukiwemo mradi wa Julius Nyerere.

‘’Sisi tukupongeze na tumefurahi kwa umri wako unafuatilia masuala ya Nishati, sasa tutakupeleka kuliona Bwawa la Julius Nyerere uone Umeme unavyozalishwa ili uendelee kujifunza zaidi. Sisi tunatamani kukuona ukifanikiwa zaidi,” amesema Mhe. Biteko

Kwa Upande wake Naibu Waziri wa Nishati Mheshimiwa Judith Kapinga amesema Miradi hii ya kimkakati ambayo inatekelezwa nchini ni jitihada za Serikali chini ya  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa  Dokta Samia Suluhu Hassan ambaye ameonesha dhamira ya dhati  kuendeleza miradi ya umeme nchini ukiwemo mradi wa JNHPP ambao kwa sasa umefikia asilimia 99.8.

“Wakati Mheshimiwa Rais anaingia madarakani, Mradi wa Julius Nyerere ulikuwa asilimia 33, leo tunavyozungumza umefikia zaidi ya asilimia 99 na mashine nane tayari zimeingizwa kwenye gridi ya Taifa. Imebaki mashine moja pekee ambapo mradi uko mbioni kukamilika,” amesisitiza mheshimiwa Kapinga

Nae Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa wateja Bi. Irene Gowelle akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) , amesema wamepokea kwa vitendo agizo la Mheshimiwa Dkt. Biteko la kuhakikisha mwanafunzi huyo anafanya ziara katika Mradi wa Julius Nyerere ambapo pia amefafanua kuwa elimu na taarifa zinazotolewa na TANESCO zinawafikia walengwa kwa usahihi.

“Hatua hii inatupa nafasi ya kuona kwamba elimu na taarifa mbalimbali tunazozitoa zinawafikia moja kwa moja makundi mbalimbali i?wakiwemo  watoto na ndio maana mmeweza kuona Mirabelle akizungumza kwa ufasaha.
Sisi kama Shirika la Umeme tutaendelea kufanya hivyo” amefafanua Bi. Gowele.

Mwanafunzi huyo  licha ya pongezi ,amepewa zawadi mbalimbali ikiwemo Komputa Mpakato (Laptop) pamoja na fedha kiasi cha Shilingi Milioni Mbili.
Posted by MROKI On Wednesday, February 19, 2025 No comments








Na Mwandishi wetu,Dodoma
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, ameonya vikali wanachama wanaotafuta uteuzi wa udiwani, uwakilishi na ubunge kwa njia zisizo halali, akisisitiza kuwa chama hakitasita kuwaengua wale watakaokiuka Katiba, Kanuni na maadili ya CCM kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2025.

Akizungumza jijini Dodoma wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa makatibu wa matawi na kata kutoka Wilaya ya Dodoma, Balozi Nchimbi alisema baadhi ya wanachama wameanza kampeni kabla ya muda rasmi kwa kutumia mbinu kama kuanzisha mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs), kufadhili matukio ya kijamii kama kumbukumbu za misiba na sherehe za ndoa, pamoja na kushinikiza vikao vya chama kuwapitisha bila kupingwa.

“Tayari tumeshuhudia baadhi ya wabunge na madiwani wakitafuta mbinu za kuhakikisha wanapitishwa bila kupingwa. Wengine wanahamasisha matamko ya vikao, huku baadhi wakihudhuria matukio yenye lengo la kujitambulisha mapema kwa wapiga kura. Wapo wanaowapa posho wahudhuriaji wa mikutano wakiwa wamevaa sare za CCM ili kuonesha wanaungwa mkono. Tunawataka waache mara moja. CCM ina mfumo madhubuti wa kufuatilia mwenendo wa wanachama wake, na kumbukumbu hizi zote zinahifadhiwa. Wanaweza kushangaa majina yao yakiwekwa pembeni,” alisema.

Balozi Nchimbi aliwataka madiwani na wabunge walioko madarakani kuacha kupuuza majukumu yao kwa kisingizio cha maandalizi ya uchaguzi, akisema chama kitafanya tathmini kwa kila mgombea kulingana na utendaji wake, si kwa uwezo wa kutoa fedha kwa wapiga kura.

“Tumeshuhudia watu wakichaguliwa lakini wanakaa miaka mitano bila kufanya kazi kwa sababu wanajua wapiga kura wachache wa ndani ya chama watakaowarudisha tena madarakani. Mfumo wetu mpya unalenga kumchagua mgombea kwa misingi ya kazi zake, si kwa kutumia rushwa au mbinu za kificho. Tunataka ukichaguliwa ukafanye kazi kwa wananchi,” alisisitiza.

Alieleza kuwa mabadiliko ya Katiba ya CCM yaliyofanyika chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa CCM, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yalilenga kuongeza idadi ya wapiga kura katika kura za maoni ili kupata taswira pana ya maoni ya wananchi na kudhibiti mianya ya rushwa.

Aidha, Balozi Nchimbi alisema baadhi ya wanachama wanaotaka nafasi za uongozi wameanza kutumia mbinu mbalimbali kuhakikisha wanapitishwa bila kupingwa, jambo ambalo alisema halikubaliki ndani ya chama.

“Tumeanza kuona matukio ya baadhi ya wabunge na madiwani wakipitisha fomu ili watangazwe kuwa wagombea pekee. Wengine wanahamasisha vikao kutoa matamko kwamba wapitishwe bila kupingwa. Wapo wanaoandaa kumbukumbu za misiba, siku za kuzaliwa na hata sherehe za ndoa, lakini wahudhuriaji wanapewa posho na wamevaa sare za CCM ili ionekane kama mkutano wa kisiasa,” alisema.

Aliongeza kuwa CCM ina utaratibu wa kufuatilia mwenendo wa wanachama wake, na wale wote wanaoendesha kampeni za chinichini wataenguliwa mapema.

“Wengine wameanzisha NGOs kwa malengo ya kisiasa, wengine wanatumia mbinu za kuwachafua waliopo madarakani kwa sasa. Kwa wote hawa, tunasema waache mara moja. Wanapoteza muda na kutufanya tufikirie kuwaengua. Hatutavumilia mambo haya,” alionya.

Balozi Nchimbi aliwataka viongozi wa CCM katika ngazi zote kuhakikisha wanatenda haki kwa kusimamia Katiba na Kanuni za chama bila upendeleo.

“Mafunzo haya tunayotoa yanalenga kuwawezesha makatibu wa matawi na kata kujua dhamana yao ndani ya chama, majukumu yao na mipaka yao ya kazi. Ushindi wa CCM unategemea uimara wa mfumo wake, imani ya wanachama kwa chama, pamoja na utendaji wa Serikali yake chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” alisema.

Alihitimisha kwa kusisitiza kuwa chama hakitawavumilia wanaojihusisha na kampeni za chinichini na kwamba hatua kali zitachukuliwa dhidi ya watakaokiuka taratibu.
Posted by MROKI On Wednesday, February 19, 2025 No comments








Na Mwandishi wetu, Morogoro
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga ameielekeza Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli( PURA) kuendelea kuvutia  uwekezaji katika vitalu vilivyo wazi vya mafuta na gesi asilia ili kuongeza kiasi cha nishati hiyo nchini.

Mhe. Kapenga amesema hayo leo wilayani Morogoro, Mkoa wa Morogoro wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa PURA kinacholenga kujadili  masuala mbalimbali ikiwemoMpango na Bajeti ya Taasisi hiyo kwa mwaka  wa fedha 2025/26.

" Mkifanikiwa  kuvutia uwekezaji katika shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi, nchi itaongeza ugunduzi wa rasilimali hiyo muhimu ikiwa ni pamoja na kuogeza futi za ujazo wa gesi  inayopatikana nchini. 

Pia mkiendelea kuvutia uwekezaji kupitia Duru ya Tano ya kunadi vitalu itakayozinduliwa mwezi machi mwaka huu, pamoja na faida zilizopo, mtakuwa mmeendeleza jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuendelea kuifungua Tanzania kiuchumi na kuvutia uwekezaji zaidi."Amesema Kapinga

Amesema Wizara ya Nishati inatambua umuhimu wa tukio la Duru ya Tano ya kunadi vitalu vya utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini pamoja na kutambua kazi kubwa ambayo imeshafanyika kuelekea uzinduzi wa tukio hilo ambalo amesema kuwa ni muhimu katika 
 kuvutia uwekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini. 

“ Kwa muda mrefu sasa tumekuwa tukizungumzia ugunduzi wa futi za ujazo trilioni 57.54 pekee ni wakati sasa wa kufanya zaidi na zaidi ili tuweze kuongeza ugunduzi wa rasilimali hii muhimu kwa maendeleo ya Taifa." Amesisitiza Mhe.Kapinga

Katika kikao hicho cha  Baraza la Wafanyakazi,  ameupongeza uongozi wa PURA kwa kuendelea kuwashirikisha watumishi wake katika kujadili, kupanga na kupitisha mipango na Bajeti ya Taasisi kwenye Baraza la Wafanyakazi ikiwa ni utekelezaji pia wa Sheria ya Majadiliano ya Pamoja katika Utumishi wa Umma.

Amesema kufanyika kwa vikao hivyo ni ishara tosha ya utawala bora mahala pa kazi kwa kuwa watumishi wanapata fursa ya kuchangia mawazo yao kuhusu hali ya uendeshaji wa Taasisi hivyo kuendelea kuwa ni sehemu muhimu ya Taasisi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli( PURA) Mhandisi. Charles Sangweni, amesema duru ya tano (5) ya kunadi vitalu vya utafutaji wa mafuta na
gesi asilia nchini inatarajiwa kuzinduliwa mwezi Machi, 2025 Jijini Dar
es Salaam wakati wa Kongamano na Maonesho ya Petroli ya Nchi
Wanachama wa Afrika Mashariki (EAPCE’25).

Amesema PURA inaendelea kusimamia na kudhibiti shughuli za utafutaji, uendelezaji na uzalishaji wa gesi asilia katika vitalu mbalimbali nchini na Kuhakikisha watanzania wazawa wanashirikishwa katika miradi mbalimbali ya mkondo wa juu wa petroli nchini.




CAPTION

PICHA 1

Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga akizungumza na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli( PURA) wakati wa Kikao cha Baraza hilo  linalofanyika tarehe 18 na 19 Februari 2025, mkoani Morogoro.

PICHA 2

Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga akiteta jambo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli( PURA) Mhandisi. Charles Sangweni (kushoto). Kulia ni Katibu wa Baraza Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli ( PURA) Ebeneza Mollel,wakati wa Kikao cha Baraza hilo cha kujadili Mpango na Bajeti hilo linalofanyika tarehe 18 na 19 Februari 2025, mkoani Morogoro. 

PICHA 3

Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli( PURA) wakati wa Kikao cha Baraza hilo linalofanyika tarehe 18 na 19 Februari 2025, mkoani Morogoro. Kushoto Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli( PURA) Mhandisi. Charles Sangweni.
Posted by MROKI On Wednesday, February 19, 2025 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo