Nafasi Ya Matangazo

May 06, 2025


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya uhamisho 
na uteuzi wa viongozi mbalimbali. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Moses Kusiluka, uhamisho na uteuzi huo ni kama ifuatavyo:

Rais amemhamisha kituo cha Kazi Mhe. Albert Gasper Msando kutoka Wilaya ya Handeni kwenda kuwa Mkuu wa Wilaya ya Ubungo mkoani Dar es Salaam.

Mhe. Japhari Mghamba Kubecha amehamishwa kutoka Wilaya ya Tanga kwenda kuwa Mkuu wa Wilaya ya Handeni mkoani Tanga. 

Aidha, Rais amemhamisha Mhe. Dadi Horace Kolimba kutoka Wilaya ya Karatu kwenda kuwa Mkuu wa Wilaya ya Tanga;

Rais Samia amemteua Ndg. Lameck Karanga Nganga kuwa Mkuu wa Wilaya ya Karatu. Kabla ya uteuzi huu, Bw. Nganga alikuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Karatu.

Naye Ndg. Bahati Migiri Mfungo ameteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Karatu. Kabla ya uteuzi huu, Bw. Mfungo alikuwa Afisa Tarafa ya Mbuguni, Wilayani Arumeru.

Pia amemteua Ndg. Lazaro Jacob Twange kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO). Kabla ya uteuzi huu, Bw. Twange alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Ubungo.

Katika uteuzi mwingine, Rais amemteua Ndg. Andrew William Massawe kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA). Bw. Massawe anachukua nafasi ya Jaji Mkuu Mstaafu  Mhe. Mohamed Chande Othman ambaye amemaliza muda wake. 
Posted by MROKI On Tuesday, May 06, 2025 No comments






Wakala wa Nishati Vijijini (REA), umepongezwa na Jeshi la Magereza kwa kuhamasisha, kuwezesha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa taasisi zinazohudumia watu zaidi ya 100 hapa nchini.

Hayo yemebainishwa na Mkuu wa Jeshi la Magereza mkoa wa Geita, ACP Jonam Mwakasagule wakati akizungumza na Bodi ya Nishati Vijijini (REB) mkoani Geita.

'Sisi kama Jeshi la Magereza tulikuwa tunapata shida sana hasa wakati tunatumia kuni kupika na kutupotezea muda mwingi  porini na kuepuka hatari za kupoteza maisha," Amesema ACP Mwakasagule. 

ACP Mwakasagule ameongeza kuwa, matumiz ya nishati safi katika jeshi hilo sasa yamepewa kipaumbe ili kujenga afya bora kwa kupunguza magonjwa ya macho na kifua yanayotokana na matumizi ya kuni wakati wa kupika chakula. 

Naye, Mjumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini Mha. Ahmed Chinemba amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais Samia wa Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024 - 2034).

"Mhe. Rais amesema taasisi zinazohudumia watu zaidi ya 100 ziachane na matumizi ya kuni na mkaa na kuanza kutumia nishati safi ya kupikia  ikiwemo gesi asilia, umeme, bayogesi na makaa ya mawe yaliyoboreshwa, ". Amesema Mha. Chinemba.

Aidha, Mha. Chinemba ameeleza kuwa REA kwa kushirikiana na STAMICO wapo mbioni kujenga kiwanda cha kuzalisha mkaa mbadala mkoani Geita ili kurahisisha upatikanaji wa mkaa mbadala katika maeneo hayo ikiwa ni sehemu ya uhamasishaji wa matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa watanzania.
Posted by MROKI On Tuesday, May 06, 2025 No comments



Na Mwandishi wetu, Dar Es Salaam
SERIKALI  imetoa Hati za Makosa kwa Kampuni  95 za Uchimbaji Mkubwa na wa Kati wa Madini kutokana na wamiliki wa leseni hizo kukiuka masharti ya Leseni  kama yalivyoainishwa kwenye Sheria ya Madini.

Akizungumza leo Mei 6, 2025 jijiini Dar es Salaam, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amesema kampuni hizo zinapaswa kujibu hoja ndani ya siku 30 la sivyo zitafutiwa leseni zao.

Hati hizo za makosa zimetolewa rasmi kuanzia Aprili 14, 2025 na muda wake utamalizika Mei 13 mwaka huu. 

 “Kama wanahoja walete majibu yao, tuyahakiki tukijiridhisha na hoja zao tutawaondolea makatazo kama hawana hoja tutawafutia leseni zao kwa  mujibu wa Sheria ya Madini Sura 123  ya  utoaji na ufutaji wa leseni za  madini na uchimbaji kifungu cha 63 na Kanuni zake, ambacho kinaeleza ukipewa leseni unapaswa uanze kazi ndani ya miezi 18.

Amesema, Serikali imetoa leseni kwa wachimbaji wa kati na wakubwa ambazo tangu kutolewa kwake hazifanyiwa kazi.

Zipo Kampuni tangu zimechukua leseni mwaka 2011 mpaka leo hazijaingiza hata koleo kwenye eneo miaka 14 sasa hazijaanza shughuli zozote, hatuwezi kuwa nchi ya namna hii.

Leseni 7 tu kati ya 95 ukiziweka pembeni zina mtaji wa Shilingi Trilioni 15 zimelala, sisi hatuwezi kuwa nchi ambayo  inatoa leseni kwa ajili ya kuchochea sekta ya madini kukua,halafu kuna watu wanachukua leseni wanakaa nazo hawafanyii kazi kwa kisingizio kuwa tupo kwenye mazungumzo na serikali  na sababu mbali mbali.

Leseni za madini zikitolewa zina masharti nyuma yake kwenye ile karatasi hakuna sharti linalosema mtu  ataanza uchimbaji wa madini nchini Tanzania akikamilisha mazungumzo na serikali, hiyo si sehemu ya sharti.

Masharti ni kwamba mwombaji anapopewa  leseni ni lazima aanze uchimbaji ndani ya miezi 18 vinginevyo awe na sababu ambazo zimeridhiwa na Waziri wa Madini kupitia Tume ya Madini, vinginevyo unapaswa kuanza uchimbaji ndani ya miezi 18.

Amesema na wale wote ambao  wamepata hati  ya makosa ambao wamejibu waende na barua ya ‘Commitment’ ya kueleza wataanza uchimbaji lini, ambao katika barua hiyo pia ikitokea ameshindwa kukidhi kile alichosema kwenye barua  sheria itafuata mkondo wake.

Kuna vitu kama nchi ni lazima tuchukue maamuzi magumu, hatuwezi kuifanya nchi yetu mtu anakuja anachukua leseni alafu akaitafutie mtaji, sheria inataka mtu yoyote anayekuja kufanya maombi ya leseni lazima atoe udhibitisho wa uwezo wa kifedha na kiufundi kabla ya kupata leseni,  sio nikupe ndio ukatafutie mtaji maana yake utakuwa umekiuka masharti ya sheri kwa kutoa taarifa ambazo sio sahihi wakati wa kuomba leseni.

Wale wote ambao hawatajibu ndani ya muda uliowekwa wasitegemee huruma yoyote, na wamekuwa ni mabingwa wakukimbilia mahakamani kuishtaki serikali katika hili Serikali imefuata taratibu zote kwa mujibu wa sheria inayowataka waliopata Leseni wote kufanya uendelezaji wa Leseni zao” Alisema Mavunde

Sekta ya Madini ni kati ya sekta zenye mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi hivyo shughuli za uchimbaji wa madini huchochea maendeleo makubwa ya kiuchumi. 
Posted by MROKI On Tuesday, May 06, 2025 No comments






Nyamguma Mahamud, Mwandishi wa Habari  kutoka Mlimani FM ameibuka kidedea katika Tuzo za Uandishi wa Habari za Samia Kalamu Awards 2025 kupitia kipengele cha habari za Nishati Safi ya Kupikia ambapo Wizara ya Nishati imetambua mchango wake kwa kumpa zawadi mbalimbali ili kuendelea kuhamasisha utoaji wa elimu ya Nishati Safi ya Kupikia.

Hafla ya utoaji wa Tuzo hizo imefanyika jijini Dar es Salaam huku mgeni rasmi akiwa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.  Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mohamud amekabidhiwa zawadi zake na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko.

Mshindi huyo amekabidhiwa fedha taslimu shilingi milioni tano, kompyuta mpakato, jiko linalotumia umeme kidogo na uniti za umeme za mwaka mzima.

"Tunatambua  masuala aliyoyaandika katika kuhamasisha nishati safi ya kupikia, kwahiyo tumemzawadia pia jiko la umeme la kisasa linalotumia umeme mdogo pamoja na umeme wa kutumia nyumbani kwake kwa mwaka mmoja," amesema Mha. Mramba

Amesema Tuzo ya Nishati Safi ya Kupikia ni kielelezo cha  kuunga mkono juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika  kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Samia Kalamu Awards  imeandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ikiwa na kaulimbiu ya "Uzalendo Ndio Ujanja'
Posted by MROKI On Tuesday, May 06, 2025 No comments

May 05, 2025


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa pamoja na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Mhe. Abdullah Bin Zayed Al Nahyan, wakishuhudia utiaji saini wa hati ya makubaliano kati ya Rais wa Chemba ya biashara,Viwanda na Kilimo(TCCIA) Vicent Minja na Waziri Msaidizi wa Masuala ya Uchumi na biashara UAE, Mh. Saeed Mubarak Al Hajeri wa Shirikisho la Vyama vya Biashara na Viwanda vya UAE na Chemba ya Biashara,Viwanda na Kilimo(TCCIA) kuhusu uanzishwaji wa Baraza la Pamoja la Biashara kati ya Umoja wa Falme za Kiarabu na Tanzania tarehe 05 Mei, 2025 Ikulu jijini Dar es Salaam.
Posted by MROKI On Monday, May 05, 2025 No comments
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele (kulia) akikagua mwenenedo wa uboreshaji Daftari katika Halamashauri ya Songea Vijijini. 
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele (shati la drafti) akiwa katika kituo cha shule ya Msingi Mahela katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma wakati akitembelea vituo mbalimbali vya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika mkoa huo jana. Kulia walio simama ni Afisa Mwandikishaji wa Jimbo la Mbinga Mjini, Ndg. Amina Hamisi Seif. (Picha na INEC).
Wananchi wakiangalia Daftari la awali la wapiga kura lililowekwa wazi.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele (kulia) akiwa katika kituo cha shule ya Msingi Mahela katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma wakati akitembelea vituo mbalimbali vya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika mkoa huo jana. Wapili Kulia ni Afisa Mwandikishaji wa Jimbo la Nyasa, Ndg. Khalid Khalifa. (Picha na INEC).

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele (Kushoto) akimkabidhi kadi ya Mpiga Kura Ndg. Acheni Maulid mkazi wa Mbamba Bay katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyasamkoani Ruvuma aliyefika katika kituo cha Shule ya msingi Mbamba bay kuboresha taarifa zake katika Daftari la Kudumu la Mpiga Kura. (Picha na INEC).
Mpiga Kura Ndg. Acheni Maulid mkazi wa Mbamba Bay katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa Mkoani Ruvuma akionesha aliyefika katika kituo cha Shule ya msingi Mbamba bay kuboresha taarifa zake katika Daftari la Kudumu la Mpiga Kura. (Picha na INEC).
Na Mwandishi Wetu, Ruvuma
Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, imewataka wananchi wa mikoa 15 inayotekeleza zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika mzunguko wa kwanza wa awamu ya pili kuzitumia siku chache zilizobaki katika mikoa yao kuhakikisha wanajitokeza kujiandikisha na kuhakiki taarifa zao ili wasijekosa haki yao ya msingi ya kupiga Kura katika uchaguzi ujao mwaka huu.
 
Hayo yamesema na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele wakati akitembelea vituo mbalimbali vya uboreshaji wa Daftari hilo katika Katika halsmahauri za Mkoa wa Ruvuma.
 
“Nawasihi wananchi wa mikoa 15 ambayo awamu ya pili ya Uboreshaji Daftari inafanyika wandelee kujitokeza kuja kuboresha, waendelee kujiandikisha lakini pia kuwaondoa wale ambao hawastahili kuwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, tumebakiwa na siku chache zinazotakiwa kuendelea na zoezi,” alisema Jaji Mwambegele.
 
Jaji Mwambegele amesema zoezi la uboreshaji wa wa awamu ya pili linakwenda sambamba na uwekaji wazi wa Daftari la awali la kudumu la wapiga Kura ambalo linatoa fursa kwa wananchi kukagua, kufanya marekebisho ya taarifa za wapiga kura na uwekaji wa pingamizi dhidi ya wapiga kura waliomo kwenye daftari ambao hawana sifa na litabandikwa katika vituo vyote vilivyotumika wakati wa uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya kwanza.
 
Akizungumzia kuhusu mwenendo wa zoezi hilo kwa ujumla Jaji Mwambegele amesema zoezi linakwenda vizuri na mwitikio wa wananchi ni mzuri kwani maeneo aliyotembelea katika mikoa ya Iringa, Njombe na Ruvuma wananchi wamejitokeza vituoni kujiandikisha, kuboresha taarifa zao pamoja na kutoa taarifa za watu waliopoteza sifa za kuwepo kwenye Daftari hilo.
 
“Kwa ujumla wake zoezi linakwenda vizuri na wananchi wengi wamejitokeza kwaajili ya kuboresha taarifa zao, wamejitokeza pia kwaajili ya kuboresha taarifa zao na pia, wale ambao hawastahili kuwepo katika Daftari la Kudumu la Wapiga kura wamefutwa,katika kila kituo nil;ichokwenda wameniambia kuhusu wale walio waandikisha, waboresha na wale waliowafuta,” alisema.
 
Uboreshaji wa Daftari unafanyika kwa mizunguko mitatu ambapo mzunguko wa kwanza unajumuisha mikoa 15, mzunguko wa pili utajumuisha mikoa 16 na mzunguko wa tatu utajumuisha vituo vya magereza na vyuo vya mafunzo.
 
Mikoa inayohusika kwenye mzunguko wa kwanza wa uboreshaji ni pamoja na Iringa, Geita, Kagera, Mara, Shinyanga, Mwanza, Simiyu, Rukwa, Tabora, Katavi, Kigoma, Ruvuma, Mbeya, Njombe na Songwe ambapo zoezi hilo lilianza kutekelezwa tangu Mei 1 na linataraji kukamilika Mei 7 mwaka huu.
 
Wakizungumza kwa nyakati tofauti Maafisa Waandikishaji kutoka Majimbo ya Nyasa, Ndg. Khalid Khalifa na yule wa Jimbo la Mbinga Mjini Ndg. Amina Hamisi Seif wamesema zoezi la Uboreshaji katika maeneo yao linakwenda vizuri na kuwahimiza wananchi kuendelea kujitokeza.
 
“Kwa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa tumekwisha andikisha wapiga kura wapya 436 na kuboresha taarifa za wapiga kura 415 wakati wapiga kura 68 wamepoteza sifa na kufutwa katika Daftari la Kudumu, bado tuzazo siku hivyo niombe kutumia fursa hii kuwataka wananchi waendelee kujitokeza,” alisema Khalifa.
 
Katika awamu ya pili ya uboreshaji, wapiga kura wapya 1,396,609 wataandikishwa, wapiga kura 1,092,383 wataboresha taarifa zao na wapiga kura 148,624 watafutwa kwenye Daftari kwa kukosa sifa za kuendelea kuwepo kwenye Daftari,” amesema Jaji Mwambegele.
 
Tume iliboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya kwanza kuanzia tarehe 20 Julai, 2024 na kukamilisha tarehe 25 Machi, 2025.
Posted by MROKI On Monday, May 05, 2025 No comments
Zitto Kabwe akizungumza na halaiki ya wananchi wa Kigoma mjini badaa ya kuchukua fomu.

Zitto Zuberi Ruyagwa Kabwe Kiongozi mstaafu wa ACT Wazalendo, Ndg. Zitto Zuberi Ruyangwa Kabwe  amejitosa kuwania kuteuliwa na chama chake kuwania Ubunge wa Jimbo la Kigoma Mjini katika uchaguzi Mkuu utakaofanyikia Mwezi Oktoba mwaka huu.
 
Zitto aliyepata kushika nafasi hiyo ya Ubunge kwa vipindi viliwi kuanzaia mwaka 2005 hadi 2015 akiwa ni Mbunge wa Kigoma Kusini naabaade kuamua kugombea jimbo la Kigoma Mjini akiwa na Chama cha Chadema na baadae kujiondoa uancahama alichukua fomu hioyo Mei 04,2025.
 
akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kata ya Bangwe Jimbo la Kigoma Mjini, Mei 04, 2025 ikiwa ni saa chache baada ya kuchukua fomu ya kugombea ubunge wa Jimbo la Kigoma Mjini.
 
Zitto ambaye ni Msomi wa masuala ya Uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ameamua kuchukua fomu ya kugombea Ubunge wa Jimbo la Kigoma Mjini.
Posted by MROKI On Monday, May 05, 2025 No comments



Na John Mapepele -Moshi
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa leo amekagua uharibifu wa  barabara ya Spencon- Fongagate- Mabogini- Chekereni hadi Kahe yenye urefu wa kilomita 31.25 na kuiagiza  Wakala ya Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) kuanza mara moja kujenga kwa kiwango cha lami. 

Akizungumza  kwa nyakati tofauti na wananchi wa Mabogini na  Kahe amesema Serikali inakwenda  kujenga kwa kiwango cha lami Ili ipitike katika kipindi chote cha mwaka ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi.

Aidha, amesema kukamilika kwa barabara hiyo kutarahisisha huduma ya usafiri kwa wananchi kwenda  kupata huduma ya afya na elimu.

" Kukamilika kwa barabara hii  kutasaidia wananchi wetu kufikisha mazao yao sokoni kwa maana ya Moshi Mjini  na maeneo mbalimbali nchini  hivyo kukuza kilimo cha mazao ya mpunga, mahindi na miwa ambayo yameonyesha kusitawi vema kwenye eneo hili" . Amefafanua Mhe. Mchengerwa 

Amesema katika awamu ya kwanza ya ujenzi wa barabara hiyo utahusisha ujenzi wa mitaro  mikubwa kwa pande zote mbili, madaraja na kuweka  mawe na kifusi ambapo utaifanye ipitike katika misimu yote ya mwaka.

Mkurugenzi Mtendaji Mkuu  wa TARURA,  Mhandisi Victor Seiff  amesema mradi wa ujenzi wa barabara hiyo hadi kukamilika kutagharimu takribani bilioni 45 ambapo awamu ya kwanza itagharimu jumla ya shilingi bilioni 7.

Pia Waziri Mchengerwa amezielekeza  Halmashauri zote nchini kukusanya mapato ya ndani na kuanza kutenga  10% kwa ajili ya ujenzi wa barabara.

Wakati huohuo amewaagiza wakuu wote wa mikoa na Wilaya kuendelea kulinda amani na kudhibiti vitendo vyovyote vinavyoweza  kusababisha uvunjifu wa amani.
Posted by MROKI On Monday, May 05, 2025 No comments



Waziri Mkuu na Mbunge wa Ruangwa, Kassim Majaliwa akitazama madini ya Graphite yaliyochenjuliwa na kufungashwa wakati alipotembelea mgodi wa Elianje Genesis  uliopo Namungo wilayani Ruangwa, Mei 4, 2025.  
Wafanyakazi wa mgodi wa  Elianje Genesis  uliopo Namungo wilayani Ruangwa wakitoka mgodini wakati Waziri Mkuu na Mbunge wa Ruangwa, Kassim Majaliwa alipotembelea mgodi huo, Mei 4, 2025.
Waziri Mkuu na Mbunge wa Ruangwa, Kassim Majaliwa akitazama madini aina ya Green Granie alipotembelea mgodi wa Elianje Genesis uliopo Namungo wilayani Ruangwa, Mei 4, 2025.  Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Zainab Telack. 
Waziri Mkuu na Mbunge wa Ruangwa , Kassim Majaliwa akisalimiana na  viongozi na watumishi wa mgodi wa Elianje Genesis uliopo  Namungo wilayani Ruangwa alipotembelea mgodi huo, Mei 4, 2025.  Kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Zainab Telack. 

Waziri Mkuu na Mbunge wa Ruangwa , Kassim Majaliwa akizungumza na wananchi katika Uwanja wa Namango wilayani Ruangwa, Mei 4, 2025
Wananchi wakimsikiliza Waziri Mkuuna Mbunge wa Ruangwa , Kassim Majaliwa  alipozungumza nao uwanja wa  Namungo wilayani Ruangwa, Mei 4, 2025. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
******************
WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeamua kuwekeza kwenye sekta ya madini ili kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata kipato na kujikwamua kiuchumi.

 

Amesema Serikali imenunua mitambo 15 ya kisasa ya uchenjuaji ambayo itasambazwa kwenye maeneo ya wachimbaji wadogo hivyo ametoa wito kwa wachimbaji hao kujiunga katika vikundi ili waweze kunufaika na fursa hiyo.

 

Ameyasema hayo leo Jumapili (Mei 04,2025) wakati akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye kijiji cha Chingumbwa kitongoji cha Namungo Wilaya ya Ruangwa Mkoani Lindi.

 

Kadhalika Mheshimiwa Majaliwa ametoa wito kwa Afisa Madini wa mkoa kuendelea na mpango wa kubaini maeneo yenye madini yatambulike na kisha kutoa leseni kwa wachimbaji wadogo ili waweze kufanya shughuli za uchimbaji.

 

 “Pamoja na hili tumeamua maeneo yote ya madini yaliyochukuliwa leseni na hayajaendelezwa kwa muda mrefu, tutayachukua, tutayapima upya na kuyagawa kwa wachimbaji wadogo.”

 

"Serikali yenu inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia imenunua ndege maalum ambayo itasaidia kufanya tafiti ya kujua aina ya madini yaliyopo na kiwango chake na sisi huku Lindi itakuja kuruka, Ruangwa na maeneo ya Nachingwea”.

 

Akizungumzia sekta ya barabara, Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Serikali inaendelea na mipango ya kuziboresha barabara mbalimbali katika wilaya ya Ruangwa ili kuziwezesha kupitika wakati wote na hivyo kuwafanya wakazi wa maeneo hayo kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi.

 

Naye Kaimu Meneja wa Tanesco Mkoa wa Lindi Emmanuel Sengwaji amesema kuwa Wataalam wa Idara ya Miradi mikubwa kutoka Tanesco wamefanya uhakiki wa mahitaji ya umeme katika mkoa wa Lindi kutokana na ongezeko la wawekezaji katika mkoa huo “Tuliomba tujengewe laini la gridi ya Taifa itakayotoa umeme kutoka Masasi hadi Ruangwa katika eneo la Kitandi ili umeme huo uweze kusambazwa maeneo ya uwekezaji ikiwemo kwenye migodi ya Namungo”.

Posted by MROKI On Monday, May 05, 2025 No comments

May 04, 2025

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Ndg. Ramadhani Kailima, akiwasaidia wananchi kuhakiki majina yao kabla ya kwenda kuboresha taarifa zao katika Kituo cha kuandikisha wapiga kura, Ofisi ya Kata ya Isevya, Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, wakati alipotembelea na kukagua vituo vya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya pili linalokwenda sambamba na uwekaji wazi wa Daftari la Awali la Wapiga Kura Mkoani Tabora, leo Mei 04, 2025. Picha na INEC
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Ndg. Ramadhani Kailima, akimkabidhi kadi ya mpiga kura Mwanafunzi wa Kidato cha Sita wa Shule ya Sekondari ya Milambo, Maboto Wambura, wakati alipokitembelea Kituo cha Kuandikisha Wapiga Kura katika shule hiyo iliyopo Kata ya Chemchem, Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, Mei 4, 2025. Picha na INEC
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Ndg. Ramadhani Kailima, akizungumza na wanafunzi wa shule ya sekondari ya wasichana Tabora, wakati alipotembelea Kituo cha Kujiandikisha Wapiga Kura kilichopo shuleni humo, Mei 04, 2025, ambapo pia aliwahamasisha wanafunzi wa shule hiyo na Sekondari ya Milambo zilizopo katika Hamlashauri ya Manispaa ya Tabora, wajitokeze kujiandikikisha kwa walio na sifa.  Picha na INEC.
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Ndg. Ramadhani Kailima (kulia), akizungumza na mwendesha kifaa cha ‘Bayometriki’ katika Kituo cha kuandikisha wapiga kura kilichopo Kata ya Isevya, Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, alipotembelea na kukagua vituo vya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya pili linalokwenda sambamba na uwekaji wazi wa Daftari la Awali la Wapiga Kura Mkoani Tabora, leo Mei 04, 2025. Katikati ni Mratibu wa Uandikishaji Mkoa wa Tabora, Elihuruma Nyella. Picha na INEC
***************
Na Mwandishi Wetu, Tabora.
MKURUGENZI wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi,Ndg Ramadhani Kailima amewataka wananchi wa Mkoa wa Tabora kujitokeza kuhakiki na kuboresha taarifa zao katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na uwekaji wazi wa Daftari la Awali la Wapiga Kura kwenye vituo walivyojiandikishia na kutazama daftari la awali lilolowekwa wazi na kutoa taarifa za wale waliokosa sifa kuwepo kwenye daftari hilo
 
Kailima amezungumza hayo Mei 4, 2025 wakati alipokuwa anatembelea na kukagua vituo katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora ambapo amesema wananchi wameonesha mwitikio mkubwa kwa kujitokeza kuhakiki taarifa zao.
 
Alisema Tume imeweka wazi daftari la awali la wapiga kura katika vituo vyote vilivyotumika kuandikisha na kuboresha taarifa za wapiga kura katika awamu ya pili hivyo wananchi wajitokeze kuhakiki taarifa zao na kutoa taarifa za wale ambao hawastahili kuwepo katika Daftari hilo.
 
“Wananchi endapo wataona katika Daftari ambalo tumeliweka katika kila kituo kuna mwananchi ambaye amekosa sifa kama vile kufariki basi wawe huru kwa kutumia fomu namba 5B kumuondoa huyo ambaye amekosa sifa za kuwepo kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura,” alisema Kailima.
 
Aliongeza kuwa, Mkoa wa Tabora unavituo vya kujiandikishia daftari la mpiga kura vipo 376 mkoa mzima. Hata hivyo, alisisitiza wananchi waendelee kujitokeza katika kuboresha taarifa zao wale ambao hawakuboresha taarifa zao katika awamu ya kwanza ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura basi ndio kipindi cha kafanya hivyo.
 
Aidha, tume inatoa nafasi kwa watu wote wenye changamoto ya kutoa kuona kusikia na kutoajua kusoma wanatakiwa kuja na watu wao wenye uwezo wa kuwasaidia ili waeze kujiandikasha kwenye Daftari la mpiga kura .
 
Kwa upande wake, Mratibu wa Uandikishaji Mkoa wa Tabora, Elihuruma Nyella alisema hali ya uandishikishaji katika Mkoa wa Tabora unaendelea vizuri na watu wanajitokea.
 
Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya pili unafanyika sambamba na uwekaji wazi wa Daftari la Awali la Wapiga Kura kuanzia Mei 01, 2025 na kukamilika tarehe 07, 2025 katika mikoa 15 ya mzunguko wa kwanza katika awamu ya pili ya uboreshaji.
Posted by MROKI On Sunday, May 04, 2025 No comments
Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM na Waziri Mkuu na Mbunge wa Ruangwa akizungumza na Wajumbe wa Mabaraza ya Chama cha Mapinduzi wilayani Ruangwa  kwenye Bwalo la Shule ya Msingi na Awali, Wonder Kids wilayani Ruangwa, Mei 3, 2025. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM na Waziri Mkuu na Mbunge wa Ruangwa akizungumza na Wajumbe wa Mabaraza ya Chama cha Mapinduzi wilayani Ruangwa  kwenye Bwalo la Shule ya Msingi na Awali, Wonder Kids wilayani Ruangwa, Mei 3, 2025. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Wajumbe wa Mabaraza ya Chama cha Mapinduzi wilaya ya Ruangwa  wakimsikiliza Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM  Mkuu na Mbunge wa Ruangwa, Kassim Majaliwa alipozungumza nao kwenye Bwalo la Shule ya Msingi na Awali Wonder Kids ya wilayani Ruangwa, Mei 3, 2025. 
Wajumbe wa Mabaraza ya Chama cha Mapinduzi wilaya ya Ruangwa  wakimsikiliza Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM  Mkuu na Mbunge wa Ruangwa, Kassim Majaliwa alipozungumza nao kwenye Bwalo la Shule ya Msingi na Awali Wonder Kids ya wilayani Ruangwa, Mei 3, 2025. 
***************
MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama Chama cha Mapinduzi, Waziri Mkuu na Mbunge wa Jimbo la Ruangwa, Kassim Majaliwa amesema kuwa Wilaya hiyo haina deni na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kutokana na kazi kubwa ya kimaendeleo iliyofanyika katika sekta mbalimbali.
Ameyasema hayo leo (Jumamosi, Mei 03, 2025) wakati akizungumza katika kikao kilichojumuisha wajumbe wa Mabaraza ya Jumuia za Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Ruangwa kilichofanyika katika Bwalo Shule ya Awali na Msingi ya Wonder Kids.
Waziri Mkuu amesema kuwa katika kipindi cha kuanzia mwaka 2010 hadi sasa ujenzi wa vituo vya afya umeongezeka kutoka vituo 2 hadi 12 hali inayowezesha kusogeza huduma za afya karibu na wananchi. “Tulikuwa na zahanati 22 lakini sasa zimefikia 35, na jitihada bado zinaendelea.
Aidha, Waziri Mkuu amesema kuwa kwa kutambua umuhimu wa sekta ya elimu, Wilaya hiyo imewezesha kujenga shule za sekondari 30 kutoka shule 16 za hapo awali.
Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa kwa sasa Serikali inatekeleza mradi mkubwa wa maji wa Nyangao - Ruangwa - Nachingwea ambao unajumuisha vijiji 34 vya Wilaya ya Ruangwa, vijiji 21 vya Wilaya ya Nachingwea na unatarajia kunufaisha wakazi 128,657.
Ameongeza kuwa Wilaya hiyo inaendelea na utekelezaji wa ujenzi wa barabara za ndani ya wilaya pamoja na ujenzi wa mradi mkubwa wa ujenzi wa barabara ya Nanganga-Ruangwa ambao upo mbioni kukamilika.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa, Hassan Ngoma ameipongeza Serikali kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika wilaya hiyo.
Mkuu huyo wa wilaya ametaja baadhi ya miradi kuwa ujenzi wa miundombinu ya barabara, vyumba vya madarasa, maji na vituo vya kutolea hiduma za afya.
Ametumia fursa hiyo kuwasisitiza wakazi wa wilaya hiyo kuendelea kuipa ushirikiano Serikali yao ambayo imejidhatiti kuendelea kuboresha huduma za kijamii.
Posted by MROKI On Sunday, May 04, 2025 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo