Nafasi Ya Matangazo

October 17, 2024

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Bw. Kailima Ramadhani akifafanua jambo wakati wa mafunzo ya siku moja kuhusu sharia za uchaguzi kwa Maafisa Wakuu wa Upelelezi wa Wilaya nchini. Mafunzo hayo yamefanyika leo Oktoba 17, 2024 jijini Dodoma. Pamoja nae ni Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini DCI Ramadhani Kingai. 
***********
Na Mwandishi wetu, Dodoma
Maafisa wa Polisi nchini wametakiwa kujenga  tabia ya kujikumbusha sheria mbalimbali ikiwemo zinazohusu masuala ya uchaguzi ili kuepuka kuyumbishwa na wanasiasa wanaoamua kupotosha yaliyomo katika sheria hizo kwa maslahi yao binafsi.
 
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Bw. Kailima Ramadhani wakati akifungua mafunzo ya Wakuu wa Upelelezi wa Wilaya nchini yaliyofanyika leo Oktoba 17, 2024 mkoani Dodoma.
 
Kailima amesema, mafunzo ya aina hii ni muhimu kwa kipindi hiki ambacho kuna Sheria Mpya mbili zinazosimamia masuala ya Uchaguzi. Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya mwaka 2024 na Sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Na. 2 ya mwaka 2024.
 
“Katika sheria zote mbili yapo mabadiliko makubwa katika maeneo mbalimbali ambayo ni muhimu sana kwenu kuyafahamu kipindi hiki ambacho uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga unaendelea na mwakani itakuwa ni uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani,” alisema Kailima.
 
Aliongeza, mafunzo hayo kuhusu sheria za uchaguzi yana umuhimu na maana kubwa katika maandalizi ya zoezi zima na mchakato wa kuelekea chaguzi zilizopo mbele yetu kama Taifa.
 
“Uelewa wenu kuhusu sheria hizi, utasaidia sana usimamiaji wa sheria na kuchukua hatua za udhibiti wa uvunjifu wa sheria hizo pamoja na sheria zingine ili watakaokiuka sheria hizo waweze kufunguliwa mashtaka ipasavyo na kuwatendea haki kwa kitakachoamuliwa na Mahakama,” alisisitiza Kailima.
 
Aliendelea kwa kusema kuwa, anaamini kuwa baada ya mada inayohusu sheria za uchaguzi kuwasilishwa wakuu hao wa upepelezi watakuwa mabalozi wa kuhamasisha wananchi kwenda kuboresha taarifa zao katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura pindi zoezi linapofanyika katika maeneo yao.
 
Lengo la mafunzo kwa maafisa hayo ni kuwajengea uelewa kuhusu haki za vyama, wananchi na makundi mengine katika vipindi vyote vya uchaguzi, kwa maana kabla ya uchaguzi Mkuu, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi.
 
Pamoja na masuala ya Sheria za uchaguzi, washiriki hao ambao ni Wakuu wa Upelelezi walipata kujua wajibu wa Jeshi la Polisi wakati wa uchaguzi, Bank Note Security features, utambuzi wa bidhaa bandia na hatimiliki, upelelezi sambamba na utafiti katika mapungufu ya kisheria.
Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini DCI Ramadhani Kingai (kulia) akifafanua jambo  akati wa mafunzo ya siku moja kuhusu sharia za uchaguzi kwa Maafisa Wakuu wa Upelelezi wa Wilaya nchini. Mafunzo hayo yamefanyika leo Oktoba 17, 2024 jijini Dodoma. Kulia kwake ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Bw. Kailima Ramadhani.
Mkurugenzi wa Huduma za Sheria, Bw. Selemani Mtibora akiwapitisha katika maeneo muhimu yaliyomo kwenye Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya mwaka 2024 na Sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Na. 2 ya mwaka 2024.

Mkurugenzi wa Daftari na Tehama wa INEC, Stanslaus Mwita akiwasilisha mada wakati wa mafunzo hayo. 
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Bw. Kailima Ramadhani (kushoto) akizungumza jambo na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini DCI Ramadhani Kingai wakati wa mafunzo ya siku moja kuhusu sheria za uchaguzi kwa Maafisa Wakuu wa Upelelezi wa Wilaya nchini. Mafunzo hayo yamefanyika leo Oktoba 17, 2024 jijini Dodoma. 

Washiriki wakifuatilia mada 


Washiriki mbalimbali ambao ni Wakuu wa Upelelezi Wilaya na Maofisa wengine mbalimbali wakishiriki katika mijadala kuhusu sheria za Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi. 





Posted by MROKI On Thursday, October 17, 2024 No comments
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Watumishi wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) wamehimizwa kujitokeza kwa wingi kujiandikisha kwenye daftari la Mpiga Kura, ili watumie haki yao kupiga kura na kuwachagua viongozi wa Serikali za Mitaa katika uchaguzi utakaofanyika tarehe 27 Novemba, 2024.

Kaulihiyo, imetolewa na Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Mhandisi Mohamed Besta, ambaye amewahimiza watumishi wa taasisi yake, ambao wapo kwenye mikoa yote ya Tanzania Bara kuhakikisha wanatumia fursa hiyo kutimiza haki yao ya msingi ya kikatiba ya kupiga kura katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Mha. Besta pia amehimiza kujitokeza kwa wingi siku ya uchaguzi, ili  wakachague viongozi wenye kusimamia maendeleo kama vile maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa.

“Naendelea kuhimiza kwa kuwa zimebaki siku chache basi watumishi wenzangu mhakikishe mnakwenda kujiandikisha na mwisho siku ya kupiga kura napo mkapige kura kwa kuchagua viongozi bora wenye kutuletea maendeleo katika maeneo yetu,” amesisitiza Mha. Besta.

Zoezi la uandikishaji wa wananchi katika Daftari la Mpiga Kura linaendelea nchi nzima ambapo lilianza tarehe 11 hadi 20 Oktoba, 2024, ambapo kaulimbiu ni “Serikali za Mitaa, Sauti ya Wananchi, Jitokeze kushiriki Uchaguzi” .
Posted by MROKI On Thursday, October 17, 2024 No comments

Na Mwandishi wetu, Dodoma 
Imeelezwa kwamba Wizara ya Madini kupitia Mpango wa Uchimbaji Madini wa Kesho yenye matumaini (MBT) kwa vijana watakaohitimu katika Kituo cha Jimolojia Tanzania (TGC)  kuwawezesha kwa kuwapatia vifaa na mashine za Uchongaji, Ukataji na Usafishaji madini ghafi zitakazo pelekea kuwa bidhaa bora zenye thamani ya juu.

Hayo yameelezwa leo Oktoba 16, 2024 na Waziri wa Madini Mhe.Anthony Mavunde wakati akitoa ufafanuzi kuhusu hoja zilizoibuliwa na wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini jijini Dodoma.

Waziri Mavunde amesema kuwa, Kituo cha TGC kinatoa mafunzo  kupitia vifaa vya kisasa hususan katika uongezaji thamani madini ya vito kwa Ukataji Uchongaji na Usafishaji, hivyo kwa Mwaka wa Fedha wa 2024/2025 wizara kupitia TGC chini ya Mpango wa MBT  itawapatia vifaa na mashine za kisasa kwa  wahitimu watakaomaliza masomo ili waweze kujiendeleza baada ya masomo kumalizika.

Waziri Mavunde amefafanua kuwa, lengo la wizara ni kuwa na KanziData inayoonesha maendeleo ya wahitimu katika kuendeleza ujuzi wa kiufundi na ubunifu walioupata na kuutumia katika  viwanda vya kuongeza thamani madini nchini.

Sambamba na hapo, Waziri Mavunde amesisitiza kuwa Mpango mwingine ni kuwepo kwa madini mengi ya vito  yaliyoongezewa thamani katika ubora mzuri wa muonekano, ukataji, rangi na uzito  ambayo yatawekwa katika vituo vya biashara ili kutanua masoko ya ndani ya nchi.

Kwa upande wake , Naibu Waziri wa Madini Dkt.Steven Kiruswa ameeleza kwamba , faida za Mpango wa MBT  kwa wahitimu wa TGC ni pamoja na kuwapatia fursa za masoko, kupata ujuzi wa kisasa kupitia vifaa, kukuza ujasiriamali na Kuchangia Maendeleo ya Sekta ya Madini kwa kuongeza thamani madini kabla ya kusafirisha nje ya nchi.

Awali , akiwasilisha taarifa kuhusu Utendaji Kazi wa Kituo cha TGC , Kaimu Mkuu wa Kituo Mhandisi Ally Maganga amesema kuwa, katika kipindi cha Oktoba 2023 mpaka Septemba 2024  jumla ya vipande vya madini ya vito 395 yenye jumla ya uzito wa carat 335.43 yalikatwa.

Aidha, jumla ya bidhaa 78 za urembo zilitengenezwa kwa kutumia metali za thamani ikiwemo dhahabu na fedha ambapo vinyago vya thamani madini 541 vilitengenezwa.

Akizungumza kwa niaba ya Mwenyekiti , Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini  Mhe.Kilumbe Ng'enda ameipongeza Wizara ya Madini na taasisi zake kwa kuratibu na kusimamia mipango mbalimbali inayopangwa ndani ya wizara kwa lengo la utekelezaji na kutoa matokeo chanya kwa sekta na taifa kwa ujumla.

Kituo cha TGC kilianzishwa Mwaka 2003 , kabla ya hapo kituo kilijulikana kama Arusha Gemstone Carving Center (AGCC).






Posted by MROKI On Thursday, October 17, 2024 No comments

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza, kwenye Mkutano wa Mwaka wa Wataalamu wa TEHAMA (TAIC,2024) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Dar es Salaam Oktoba 17, 2024. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza, kwenye Mkutano wa Mwaka wa Wataalamu wa TEHAMA (TAIC,2024) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Dar es Salaam Oktoba 17, 2024. 
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akifafanuliwa jambo na Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya QSOFT TECHNOLOGY Amali Bahanza, wakati alipomwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan kwenye Mkutano wa Mwaka wa Wataalamu wa TEHAMA (TAIC,2024) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Dar es Salaam Oktoba 17, 2024. Kushoto ni Waziri Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Jerry Silaa.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akifafanuliwa jambo na Waziri Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Jerry Silaa, kuhusu kadi maalum inayotumika kupata huduma mbalimbali za Serikali, alipomwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan kwenye Mkutano wa Mwaka wa Wataalamu wa TEHAMA (TAIC,2024) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Dar es Salaam Oktoba 17, 2024.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na wanafunzi wanaopata mafunzo ya komputa kwa ufadhili wa HUAWEI, kwenye Mkutano wa Mwaka wa Wataalamu wa TEHAMA (TAIC,2024) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Dar es Salaam Oktoba 17, 2024. 
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akifafanuliwa jambo na mtaalamu wa kutengeneza Roboti, Hassan Kassimu, wakati alipomwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan kwenye Mkutano wa Mwaka wa Wataalamu wa TEHAMA (TAIC,2024) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Dar es Salaam Oktoba 17, 2024. 
*************
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali inaendelea kutekeleza wa Mpango mkakati wa miaka mitano 2024/25 – 2029/30 wa Anga za juu utakaoiwezesha Tanzania kurusha satelaiti.
 
Amesema kuwa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam imepata mradi wa Utafiti wa kuwezesha urushaji wa satelaiti unaosimamiwa na Taasisi ya Umoja wa Mataifa ya masuala ya anga za juu ikishirikiana na Taasisi ya Anga za Juu ya Japan (JAXA).
 
Amesema hayo leo (Alhamisi Oktoba 17, 2024) alipomwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Kilele cha Kongamano la Nane la Mwaka la TEHAMA, lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, Dar es Salaam.
 
“Katika eneo hili Maandalizi ya utungwaji wa Sera, Sheria na uridhiwaji wa mikataba ya Kimataifa ya masuala ya anga za juu inaendelea”.
 
Mheshimiwa Majaliwa ameitaka Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari iwakusanye vijana wabunifu wenye uwezo wa kubuni teknolojia zenye manufaa kwa Taifa “Lakini simamieni hizi tafiti zenye kutoa matokeo na vijana hao waendelee kupewa fursa na kazi hizo ziingie kwa jamii na zianze kutumika”
 
Pia Mheshimiwa Majaliwa ameiagiza Wizara ya Mawasiliano, Habari na Teknolojia ya Habari isimamie na kuhakikisha ujenzi wa Vituo vya Ubunifu (Innovation Hubs) katika mikoa iliyokubalika unafanyika kama ilivyopangwa.
 
Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa mabadiliko ya kidijitali ni lazima na Safari hiyo haipaswi kumuacha mtu yeyote nyuma hususan kwenye mfumo wa kifedha jumuishi. “Kama mnakumbuka, Serikali katika mwaka 2020 ilizindua Mfumo wa N-Card ambao hadi kufikia sasa umefanikiwa kuwaunganisha wananchi wasiopungua milioni nne. Mfumo huo umesaidia sana kuokoa upotevu wa fedha katika vituo vya usafirishaji”
 
Ameongeza kuwa mfumo huo umesaidia kuongeza wigo wa ukusanyaji wa mapato. “Nitoe wito kwa Wizara kuhakikisha maeneo mengi ambayo Serikali imewekeza yanatumia mfumo wa N-card. Mfumo huo ni muhimu katika kuokoa upotevu wa fedha za Serikali na kuwasaidia wananchi kuacha kutembea na fedha taslimu na watumiefedha kwa njia ya kidijitali”
 
Katika hatua nyingine Mheshimiwa Majaliwa ameitaka Wizara ya Mawasiliano, Habari na Teknolojia ya Habari ihamasishe matumizi ya TEHAMA katika kutoa huduma, biashara na uzalishaji ili kuongeza uwazi, ufanisi na kuboresha maisha ya wananchi kiuchumi na kijamii;
 
Kwa Upande wake Waziri Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Jerry Silaa amesema kuwa Serikali imeendelea kuwekeza katika ujenzi wa miundombinu ya mawasiliano ambapo kwa mwaka fedha 2023/24 jumla ya urefu wa kilomita 1,592 za mkongo wa taifa zimejengwa na kufika katika wilaya 83.
 
“Pia umoja wa watoa huduma za mawasiliano (consortium of telecom operators) wameweza kujenga jumla ya kilomita 2,595 ambazo zinafanya mkongo wa taifa kuwa na kilomita 13,820. Wizara imehamisha shughuli zote zinazohusiana na ujenzi wa mkongo wa taifa wa mawasiliano na kituo cha kuhifadhia data (NIDC) kwenda katika Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL)”.

Naye, Mtendaji Mkuu wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Afrika (AUDA-NEPAD) Bi. Nardos Bekele-Thomas amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada anazozifanya katika kuhakikisha Tanzania inatumia ukuaji wa sekta ya TEHAMA katika kuchagiza Maendeleo Endelevu nchini.
Posted by MROKI On Thursday, October 17, 2024 No comments
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mhe. Dkt. Doto Biteko leo Oktoba 17, 2024 jijini Dar es salaam amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Nyumba, Huduma na Jumuiya za Mijini kutoka nchini  Misri, Mhe. Sherif EI Sherbiny.

Katika mazungumzo yao viongozi hao wamekubaliana kusimamia wakandarasi wa Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) ili kukamilisha mradi huo kwa wakati ambao hadi sasa umefikia asilimia 99 ya utekelezaji wake.

Aidha, Mhe.  EI Sherbiny ambaye ameteuliwa hivi karibuni katika nafasi hiyo akiwa nchini  atataembelea mradi wa JNHPP.



Posted by MROKI On Thursday, October 17, 2024 No comments

October 16, 2024







Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana (Mb) amekitaka Chuo cha Misitu Olmotonyi kilichopo Jijini Arusha kufanya Utafiti katika Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro Ili kubaini chanzo cha mimea vamizi na kutoa ushauri wa kitaalamu kwa lengo la kutatua changamoto hiyo inayolikumba eneo hilo.

Agizo hilo amelitoa leo Oktoba 16, 2024 alipofanya ziara ya kikazi Chuoni hapo na kuzungumza na Watumishi wa Chuo hicho katika kikao kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano Olmotonyi.

. "Kwa kuwa hapa tunatoa huduma ya Ushauri wa kitaaalamu na Utafiti wa Misitu na Uhifadhi naomba nielekeze muwasiliane na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) ili mfanye tafiti kuhusu namna ya kudhibiti mimea vamizi" alisema Mhe. Chana.

Aidha, katika hatua nyingine Mhe. Chana amekipongeza Chuo hicho kwa kuweza kubuni andiko la uanzishwaji wa miundombinu ya utalii na kuwasisitiza kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kufanikisha lengo hilo na kuwasisitiza kuendelea kuwajengea watumishi uwezo wa kitaalamu wapate masomo ya juu.

Naye, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii anayeshughulikia Masuala ya Utalii,  Nkoba  Mabula amekipongeza Chuo hicho kwa kuwa na maeneo maaalumu yanayoendeleza Utalii na kuahidi kufanya ziara Chuoni hapo kuona maeneo hayo na kutafuta namna ya kuyaendeleza Ili kuvutia Watalii zaidi.

Kwa Upande wake, Mkuu wa Chuo cha Misitu Olmotonyi,  Dkt Joseph Makero ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuendelea kukiboresha Chuo hicho pamoja kuongeza idadi ya Watumishi wanaopangiwa kituo cha kazi chuoni hapo.

Aidha, Dkt. Makero amesisitiza kuwa Chuo hicho kitaendelea kuipeperusha vyema Bendera ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuwaandaa vyema Wanafunzi wanaokidhi mahitaji ya soko la ajira na kuendelea kuhifadhi Maliasili na Kutangaza Utalii.

Kikao hicho kimehudhuriwa na baadhi ya Watumishi pamoja na Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii anayeshughulikia Masuala ya Utalii,  Nkoba  Mabula Mkurugenzi wa Utafiti na Mafunzo,Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Edward Kohi.
Posted by MROKI On Wednesday, October 16, 2024 No comments








WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa leo Oktoba  16, 2024 amemwakilisha Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika maziko ya Mzee Jeremiah Kusiluka ambaye ni Baba mzazi wa Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Moses Kusiluka yaliyofanyika katika kijiji cha Madihani, Makete mkoani Njombe.

Akitoa salamu za Mhe. Rais Dkt. Samia, Waziri Mkuu amesema  Mheshimiwa Rais Dkt. Samia ametoa wito kwa wanafamilia, ndugu na waombolezaji wawe watulivu katika kipindi hiki kigumu za msiba huo na waendelee kumuombea marehemu Mzee Jeremiah ili Mwenyezi Mungu amlaze mahali pema peponi. 

Aidha, Mhe. Majaliwa ametoa wito kwa wanafamilia, ndugu na waombolezaji kuyaenzi mema yote aliyoyafanya marehemu kipindi cha uhai wake. “Tuenzi yale yote mema aliyoyafanya mzee wetu Jeremiah wakati wa uhai wake, tukifanya hivyo tutakuwa tumetenda haki. ”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema kuwa Makamu wa Rais Dkt. Philip Isdor Mpango na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Mwinyi wanatoa pole kwa wanafamilia, ndugu na waombolezaji kutokana na msiba huo.
 
Akizungumza kwa Niaba ya Familia, Prof. Lughano Kusiluka ametoa shukrani kwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali kwa ujumla kwa kushiriki wake katika kumuaga Mzee Jeremiah. “Asanteni kwa kuja kushiriki nasi, tunawashukuru sana kwa kutuunga mkono kuja kushiriki nasi katika kumuaga mzee wetu, heshima hii ni kubwa na haielezeki. ”

Aliongeza kuwa Mzee Jeremiah alikuwa ni Baba imara na mwenye msimamo. “Mara zote alitusisitiza lazima tuheshimu watu tufanye kazi ili tuweze kuishi na alitukumbusha kuwa hapa katika kijiji cha Madihani, Kipahalo ni nyumbani kwetu. ” Alisema.

Kwa Upande wake Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Moses Kusiluka amesema kuwa Marehemu Mzee Jeremiah alikuwa ni mpenda maendeleo na watoto wake wote wamekuwa wakienzi msimamo huo. “Pamoja na kuwa mpenda maendeleo pia baba alikuwa mchaMungu na ameondoka akiwa mchaMungu. ”

Naye, Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema kutokana na historia ya mzee Jeremiah hasa kwenye malezi ya watoto wake inapaswa kusherehekea maisha yake kwa kuwa anakuwa shujaa wa Makete na Tanzania kwa ujumla. “Mafanikio ya watoto wake katika utumishi wa umma hayana kificho. ”
 
Viongozi walioshiriki msiba huo ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) William Lukuvi, Mkuu wa Mkoa wa Njombe Anthony Mtaka, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule.

Wengine ni Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonaz, Katibu  Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Antony Sanga, Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. John Jingu, Msajili wa Hazina Nehemia Kyando Mchechu
Posted by MROKI On Wednesday, October 16, 2024 No comments







Na Mwandishi wetu, Dodoma
Serikali kupitia Wizara ya Madini inarudisha minada ya ndani ya madini ya vito itakayofanyika katika maeneo ya uzalishaji hususan Mirerani, Mahenge, Tunduru, Dar es salaam, Arusha na Tanga na kimataifa itafanyika mji wa Bangkok na Jaipur nchini Thailand.

Hayo yamesemwa leo Oktoba 16, 2024 na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati akijibu hoja mbalimbali zilizoibuliwa na wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Nishati na Madini jijini Dodoma.

Waziri Mavunde amesema kuwa baada ya taratibu za marekebisho ya kisheria kukamilika juu ya uendeshaji wa minada hiyo wanatarajia ndani ya muda mfupi ujao kuanza taraibu za kuweka miundombinu ya kuanza minada ya ndani.

Waziri Mavunde amefafanua kuwa, uendeshaji wa maonesho na minada ya kimataifa nchini ni fursa muhimu ya kutangaza madini ya vito yanayozalishwa hususan kwenye masoko ya kimataifa ambayo ni njia mojawapo ya kuwafikisha watanzania katika masoko ya uhakika na upatikanaji wa bei nzuri na stahiki.

Waziri Mavunde ameieleza Kamati ya Nishati na Madini kuwa, Mpango wa kurejesha minada ya madini ya vito ni utekelezaji wa maagizo yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia  Suluhu Hassan  wakati wa ufunguzi wa kiwanda cha kusafisha dhahabu cha jijini Mwanza tarehe 13 Juni, 2024.

Kwa upande wake , Naibu Waziri wa madini Dkt.Steven Kiruswa amesema, kwa sasa wataalam wa Wizara ya Madini wamepata uzoefu mkubwa katika minada na maonesho ya kimataifa baada ya kujifunza namna biashara za kimataifa zinavyofanyika pamoja na matumizi ya teknolojia ya kisasa kwenye mnyororo mzima wa thamani madini katika nchi mbalimbali ikiwemo Marekani , India , Afrika Kusini na Thailand.

Awali, akiwasilisha taarifa kuhusu uboreshaji na utekelezaji wa Kanuni za Usimamizi wa Masoko na vituo, minada ya ndani na kimataifa ya madini ya vito kwa Kamati hiyo, Kaimu Mtendaji Tume ya Madini Mhandisi Ramadhani Lwamo amesema kuwa, minada hiyo itaendeshwa na Tume ya Madini kwa kushirikiana na Soko la Bidhaa la Tanzania (TMX) kupitia mfumo wa mauzo wa kielektroniki  ambapo usimamizi utahusisha shughuli za uthaminishaji na upangaji wa madini ili kuweza kupata bei nzuri kulingana na madini husika,akisisitiza kwamba lengo kuu ni kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara ya madini ya vito na usonara barani Afrika.

Mhandisi Lwamo ameongeza kuwa, minada ya vito itaifungamanisha Sekta ya Madini na Sekta nyingine za kiuchumi ikiwemo Utalii na biashara katika kipindi husika ikiwa ni pamoja na kuliingizia taifa fedha za kigeni.

Pamoja na mambo mengine, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini Dkt. David Mathayo ameendelea kumpongeza Waziri wa Madini na wasaidizi wake kwa kazi nzuri ya kuisongesha Sekta ya Madini katika ngazi ya kimataifa inayoleta tija katika uchumi wa nchi na hasa katika mkakati wa kurudisha hadhi na thamani ya madini ya vito yakiwemo madini ya Tanzanite ambayo ni madini yanayopatikana Tanzania peke yake.
Posted by MROKI On Wednesday, October 16, 2024 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo