Nafasi Ya Matangazo

October 15, 2024

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa akishuhudia mchezo kati ya Timu ya Taifa ya Tanzania ya Mpira wa Miguu (Taifa Stars) na Timu ya Taifa ya Congo wa kuwania nafasi ya kufuzu michuano ya AFCON 2025.

Viongozi wengine wanaoshuhudia mchezo unaochezwa kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa ni Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na Naibu Waziri Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Hamisi Mwinjuma.


Posted by MROKI On Tuesday, October 15, 2024 No comments
Naibu Waziri Nishati na Mbunge wa Viti Maalum Vijana Taifa, Mhe. Judith Kapinga amewahamasisha wananchi katika Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma kujitokeza kwa wingi katika zoezi  la kujiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ili waweze kuchagua viongozi watakaowaletea maendeleo. 

Mhe. Kapinga amesema hayo hivi karibuni wakati akifungua Mafunzo ya Matumizi ya Matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 kwa Viongozi, Watendaji na Wadau wa Wilaya ya Mbinga.

"Ni muhimu kila mmoja wetu akashiriki zoezi la kujiandikisha,  sio kujiandikisha wewe tu bali kuhamasisha na wengine kwenye eneo lako waweze kujiandikisha." Ameeleza Kapinga.

Amesema ili wananchi waweze kuweka viongozi imara watakaofaa kwenye jamii, ni lazima kuwe na watu wengi wa kuwapigia kura, hivyo ni vyema wananchi wakahamasishana ili kwenda kwa wingi  kujisajili kwenye daftari la kudumu la wapiga kura.

Aidha, ametoa rai kwa wananchi kuchagua viongozi  watakaowatumikia  kwa weledi na kutatua changamoto mbalimbali pale zinapojitokeza.
Posted by MROKI On Tuesday, October 15, 2024 No comments


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Mwenge wa Uhuru kutoka kwa Kiongozi wa mbio hizo kitaifa Ndugu Godfrey Eliakim Mzava  kwenye Kilele cha Maadhimisho Mbio za Mwenge wa Uhuru katika uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza tarehe 14 Oktoba, 2024.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameeleza kuwa maono na fikra za Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere zinaendelea kuishi, na Taifa la Tanzania linaendelea kujivunia amani, mshikamano na umoja.

Aidha, Rais Dkt. Samia amesema kuwa historia ya Mwalimu Nyerere haiwezi kutofautishwa na historia ya Mwenge wa Uhuru, ambayo ni Tunu ya Taifa ambayo Mwalimu Nyerere amewaachia Watanzania.
 
Rais Dkt. Samia ameyasema hayo wakati wa Kumbukizi ya Miaka 25 ya Kifo cha Hayati Mwalimu Nyerere na Maadhimisho ya Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru yaliyofanyika katika Uwanja wa CCM Kirumba.
 
Rais Dkt. Samia amewapongeza vijana walioshiriki mbio za Mwenge wa Uhuru za mwaka 2024 kwa kuzunguka nchi nzima kuhamasisha shughuli za maendeleo na kuwahimiza wananchi kufanya kazi kwa bidii, kuwajibika na kuwa wazalendo kwa Taifa lao.
 
Vilevile, ameeleza kuwa Serikali itafanyia kazi taarifa na mapendekezo yaliyowasilishwa na Kiongozi wa Mbio za Mwenge, Ndugu Godfrey Eliakim Mzava inayojumuisha changamoto, maombi na ushauri uliotolewa na wananchi kupokelewa na Mwenge wakati wa mbio hizo.
 
Kwa upande mwingine, Rais Dkt. Samia ametoa rai kwa vijana kuendelea kulinda Mwenge wa Uhuru ambayo ni Tunu ya Taifa na kuuenzi kwa kuendelea kufanya kazi kwa bidii.
 
Akizungumzia Maonesho ya Wiki ya Vijana, Rais Dkt Samia ametoa pongezi kwa vijana kwa ubunifu, ujuzi, uthubutu na utayari wao walioonesha kupitia kazi zao na amewahakikishia kuwa Serikali itaendelea kutatua changamoto zinazowakabili.
  
Katika kuchochea zaidi ubunifu wa vijana, Rais Dkt. Samia ameelekeza Halmashauri zote nchini kununua vifaa vinavyotumika kwenye vituo vya kutolea huduma za afya na kufundishia wanafunzi ambavyo vinazalishwa kwa ubora na vijana wabunifu hapahapa nchini.
 
Rais Dkt. Samia pia amerejea wito wake kwa wananchi kujiandikisha ili waweze kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ikiwa ni kuendana na dhamira ya Uhuru ya kuwawezesha wananchi kujiamulia mambo yao wenyewe, ikiwemo kwa kuwachagua viongozi wao.


 

Posted by MROKI On Tuesday, October 15, 2024 No comments

October 13, 2024








Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, ametoa wito kwa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) pamoja na jumuiya nyingine za chama hicho kuendelea kushindana kwa hoja na kuwa mfano bora wanapojadili masuala mbalimbali ya kitaifa. 

Akizungumza katika hafla ya kumaliza matembezi ya vijana kuadhimisha kumbukumbu ya Mwalimu Julius Nyerere, Balozi Nchimbi aliweka wazi kuwa nafasi ya CCM kushinda katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwezi Novemba inategemea sana juhudi za vijana hao.

Balozi Nchimbi, aliyekuwa akizungumza mbele ya vijana takriban 2,156 waliotembea kutoka Butiama, Mkoa wa Mara, hadi Nyamagana, Jijini Mwanza, alisisitiza umuhimu wa vijana wa CCM kuwa mstari wa mbele katika kutafuta kura kwa bidii.

Alieleza kuwa ushindi wa CCM hautapatikana kwa kubahatisha, bali kwa juhudi za makusudi na mipango ya kimkakati, huku akiwataka vijana hao kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha chama kinapata ushindi mkubwa.

“Vijana wa UVCCM, ninyi ni nguzo muhimu katika chama hiki. Ushindi wa CCM uko mikononi mwenu. Mnapaswa kushindana kwa hoja na kuhakikisha mnatafuta kura za CCM usiku na mchana. Tunataka ushindi wa aina ambayo wapinzani wetu hawajawahi kushindwa tangu chaguzi hizi zianze. Na baada ya hapo, tutawashukuru kwa ushiriki wao mzuri kwenye mchakato wa uchaguzi,” alisema Balozi Nchimbi.

Pamoja na kutoa wito huo kwa vijana, Nchimbi alitoa pongezi kwa UVCCM kwa kuandaa matembezi hayo, ambayo alisema yamekuwa na maana kubwa kwa Chama na Taifa zima.

Alieleza kuwa matembezi ya vijana yaliyoanza tarehe 9 Oktoba 2024 hadi 13 Oktoba 2024, yameleta faraja kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM. 

Alisema Rais Samia ni muumini wa falsafa za Mwalimu Nyerere, na hivyo matembezi hayo yamemgusa kwa namna ya kipekee.

“Nimefurahi sana kuona vijana wa UVCCM mmekuwa na ujasiri wa kuandaa matembezi haya. Mwalimu Nyerere alikuwa mfuasi wa falsafa zake mwenyewe, na mara ya kwanza alitembea kwa miguu kuunga mkono Azimio la Arusha. Kuanzia hapo, matembezi ya miguu yamekuwa ishara ya imani thabiti kwa jambo fulani. Kwa hatua hii, UVCCM mmefanya jambo kubwa sana ambalo limeleta faraja kwa Rais Samia na kwa wote tunaopenda historia ya nchi hii,” aliongeza.

Aidha, Balozi Nchimbi alisisitiza kuwa chini ya uongozi wa Rais Samia, Muungano wa Tanzania umekuwa na ustawi mkubwa, na amani imeendelea kudumu.

Alisema ni jukumu la vijana kuendeleza falsafa za Baba wa Taifa na kuhakikisha wanaendeleza mshikamano ndani ya chama na katika jamii kwa ujumla.

Katika ujumbe wake wa mwisho, aliwataka vijana hao kuzingatia wajibu wao wa kuhakikisha CCM inapata ushindi katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. 

Alisema kwa jitihada na ushirikiano kati ya vijana na wazee wa chama, ushindi wa chama hicho utakuwa wa kihistoria na wa kipekee.

“CCM ni chama cha wazee na vijana. Wazee ndio waanzilishi wa chama, lakini sasa nyinyi vijana ndio mna jukumu la kuhakikisha chama kinaendelea kushinda. Lazima tushirikiane kwa karibu kuhakikisha tunaleta ushindi mkubwa wa CCM kwenye uchaguzi huu ujao. Nina uhakika tutaweza kufanya hivyo,” alihitimisha Balozi Nchimbi.
Posted by MROKI On Sunday, October 13, 2024 No comments









Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia S. Hassan kwa usimamizi madhubuti wa sekta unaopelekea ukuaji wa haraka wa mchango wa sekta ya madini katika pato la Taifa.

Hayo yameelezwa leo Oktoba 13, 2024 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan wakati akifunga maonesho ya Saba ya Teknolojia ya Madini mkoani Geita.

Aidha Mh Rais Samia ameeleza katika mikakati ya kuimarisha uchumi wa nchi na upatikanaji wa fedha za kigeni Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imetenga kiasi cha shilingi Trilioni moja kwa ajili ya ununuzi wa dhahabu  kutoka kwa wachimbaji.

Rais, Dkt. Samia amesema kwamba  sekta ya madini imekuwa na mchango mkubwa katika kuliingizia taifa fedha za kigeni ambapo kwa mwaka wa fedha 2022/2023 ilichangia asilimia 56 ya fedha za kigeni.

Sambamba na hapo Rais , Dkt.Samia amesema kiasi cha shilingi 250 zimetengwa kama dhamana ya mikopo zitakazo wawezesha wanunuzi wa dhahabu kupata mtaji.

Rais Dkt. Samia amesema kuwa ,  kwa mwaka wa 2023 mauzo ya madini yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni mbili yaliuzwa katika masoko 44 na vituo mbalimbali vya uuzaji madini  vilivyopo sehemu mbalimbali nchini.

Akielezea kuhusu mwenendo wa biashara ya madini nchini kuanzia mwaka 2019 mpaka septemba 2024 , Dkt.Samia amesema kwa kipindi husika kiasi cha tani 20.8 za dhahabu zenye gharama ya shilingi trilioni 5.2 zimenunuliwa kutoka kwa wachimbaji na wafanyabiashara ya madini nchini.

Dkt.Samia ameeleza serikali inatambua mchango wa asilimia 40 kutoka kwa wachimbaji wadogo nchini, ambapo ametoa leseni 21 kwa vikuandi vya Vijana na wanawake  vikiwemo vikundi vya GEWOMA , Ushirika Madirisha na TEWOMA vinavyojihusisha na uchimbaji mdogo.

Naye , Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati , Dkt.Dotto Biteko ameipongeza wizara ya madini kwa juhudi mbalimbali inazofanya za mageuzi katika mnyororo wa thamani katika sekta ya madini hususan katika masuala uongezaji thamani madini na mpango ya kufanya utafiti wa kina kwa asilimia 50 ifikapo mwaka wa 2030.

Akielezea kuhusu mikakati iliyopo  ndani ya sekta ya madini , Waziri wa Madini , Mhe. Anthony Mavunde amesema katika kuimarisha uchimbaji wenye tija na uhakika Serikali itajenga Maabara kubwa mkoani Dodoma na Geita ili
 kuwawezesha wachimbaji wadogo kupeleka sampuli zao kwa ajili ya  uchunguzi wa sampuli za madini na miamba.

Waziri Mavunde amesema kuwa wizara inaendelea kuweka mipango mizuri katika ukusanyaji wa maduhuli ambapo kwa kipindi cha siku 90 cha mwaka wa 2024/2025 wizara kupitia Tume ya Madini imekusanya kiasi cha shilingi Bilioni 287 ambayo ni zaidi ya asilimia 106.

Akielezea kuhusu utekelezaji wa Sheria na Kanuni ndani ya Wizara, Waziri Mavunde amesema kuwa  wizara imekuwa ikizingatia taratibu zote za  utekelezaji wa Mpango wa Ushirikishwaji wa Jamii inayozunguka mgodi na Mpango wa Urudishaji kwa Jamii ambapo kwasasa ipo  na mpango mpya wa Mining for Brighter Tommorrow (MBT) utakao washirikisha vijana na wakina mama.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini Mhe. Constantine Kanyasu amemshukuru  Rais , Dkt.Samia kwa kupeleka fedha za miradi ya  maendeleo mkoani Geita katika sekta ya Afya,Maji, Barabara na  Elimu.

Pamoja na mambo mengine , Rais wa Shirikisho la Wachimbaji wadogo wa madini Tanzania (FEMATA) John Bina amemuomba Rais , Dkt. Samia kuifanya dira ya Vision2030 ya Madini ni Maisha na Utajiri kuwa kitaifa badala ya kisekta.

Kwa mara ya kwanza maonesho ya Saba ya Teknolojia ya madini yamefungwa leo rasmi na Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan.
Posted by MROKI On Sunday, October 13, 2024 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan akikabidhi Waziri wa Viwanda na Biashara Dkt. Selemani Jafo tuzo kwa niaba ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania ( TanTrade) kwa kutambua usimamizi bora na uratibu wa Maonesho ya biashara ndani na nje ya nchi na kutoa huduma ya kliniki ya biashara kipindi cha Maonesho ya 7 ya kitaifa ya Teknolojia ya Madini yaliyofanyika Viwanja vya EPZA Bombambili mjini Geita, maonesho hayo yamefingwa Leo Oktoba 13, 2024 ,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan akikabidhi Waziri wa Viwanda na Biashara Dkt. Selemani Jafo tuzo kwa niaba ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania ( TanTrade) kwa kutambua usimamizi bora na uratibu wa Maonesho ya biashara ndani na nje ya nchi na kutoa huduma ya kliniki ya biashara kipindi cha Maonesho ya 7 ya kitaifa ya Teknolojia ya Madini yaliyofanyika Viwanja vya EPZA Bombambili mjini Geita, maonesho hayo yamefingwa Leo Oktoba 13, 2024 , Kushoto ni Waziri wa Madini Anthony Mavunde.
Posted by MROKI On Sunday, October 13, 2024 No comments
 






WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema Serikali inaendelea na jitihada za kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya hali ya hewa nchini ambapo ifikapo mwishoni mwa mwaka huu, Tanzania itakuwa na Rada saba ikiwa ni kiwango kikubwa cha Rada katika nchi za Afrika Mashariki na Kati.
 
Amesema kuwa hatua hiyo ni mwendelezo Serikali za kufanya uwekezaji katika sekta ya hali ya hewa nchini kwa kufunga miundombinu ya kisasa ya hali hewa ili kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji wa taarifa za hali ya hewa.
 
Amesema hayo leo (Jumapili, Oktoba 13, 2024) wakati alipotoa tamko la kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Madhara ya Maafa, Jijini Mwanza.
 
“Nitumie fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa uwekezaji mkubwa katika eneo hili lakini pia kuendelea kutoa kipaumbele kwa makundi maalumu na kuweka mikakati thabiti inayolenga kuwawezesha vijana kiuchumi na kijamii. ”
 
Amesema kuwa maadhimisho ya mwaka huu yanatoa fursa ya kuimarisha ushirikiano wa kitaifa na kimataifa ili kuunganisha juhudi za kuwalinda watoto na vijana dhidi ya athari za majanga.
 
“Ili kuifikia adhma hiyo, katika ngazi ya Taifa tunapaswa, pamoja na mambo mengine, kuhakikisha kuwa tunatumia fursa hii kutoa mafunzo kwa jamii kuhusu mikakati ya kujikinga na maafa, hasa elimu ya hali ya hewa na jinsi ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi; kuandaa mikutano ya kujadili changamoto za maafa na kupanga mikakati ya pamoja. ”
 
Ameongeza kuwa mamlaka husika zinapaswa kuendesha kampeni za uhamasishaji kuhusu umuhimu wa elimu na mawasiliano ya hatari, pamoja na ushiriki wa jamii, kuandaa matukio ya utamaduni na michezo ili kuhamasisha jamii na kutoa elimu kwa njia ya burudani, kuendeleza tafiti kuhusu madhara ya maafa pamoja na  kutoa taarifa kwa umma ili kuongeza uelewa.
 
Aidha, Waziri Mkuu ameielekeza wizara yenye dhamana ya elimu na taasisi zake kuhakikisha wanaendelea kuimarisha mitaala ya elimu ili ijumuishe masuala ya usalama shuleni, kupunguza hatari, na uelewa wa majanga. “Vilevile, kuhakikisha mafunzo kwa walimu kuhusu mbinu za kufundisha masuala haya kwa wanafunzi yanaendelea kuimarisha. ”
 
Pia,  Mheshimiwa Majaliwa amezitaka mamlaka husika ziendelee kuhamasisha na kuwezesha matumizi ya mbegu zinazokomaa kwa muda mfupi pamoja na utunzaji wa chakula cha binadamu na malisho ya mifumo. “Imarisheni utoaji taaluma ya matumizi ya mbinu za kilimo cha kisasa kinazohitaji maji kidogo. ”
 
Awali, akipokea taarifa kuhusu maadhimisho ya Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru na Kumbukizi ya Miaka 25 ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius K. Nyerere, Mheshimiwa Majaliwa amesema ameridhishwa na hatua za maandalizi ya maadhimisho hayo.
 
Mgeni Rasmi katika maadhimisho hayo yatakayofanyika katika uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza, Oktoba 14, 2024 atakuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
 
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Ridhiwani Kikwete amesema kuwa maandalizi yamekamilika ambapo  pamoja na mambo mengine Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajia kushiriki katika ibada maalum ya kumuombea Baba wa Taifa itakayofanyika katika Kanisa Katoliki la Parokia ya Mtakatifu Fransisco Xavery Jijini Mwanza.
Posted by MROKI On Sunday, October 13, 2024 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipata maelezo kuhusu Maabara ya kisasa ya  dhahabu iliyopo katika Soko Kuu la Dhahabu Geita mara baada ya kuwasili Mkoani Geita tarehe 13 Oktoba, 2024.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipata maelezo kuhusu Maabara ya kisasa ya  dhahabu iliyopo katika Soko Kuu la Dhahabu Geita mara baada ya kuwasili Mkoani Geita tarehe 13 Oktoba, 2024.








Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimsikiliza Bw. Mussa Waziri kuhusu Maabara ya dhahabu iliyopo katika Soko Kuu la Dhahabu Geita mara baada ya kuwasili Mkoani Geita tarehe 13 Oktoba, 2024. 


Muonekano wa Soko Kuu la Dhahabu Geita lililopo Mkoani Geita. 
 

Posted by MROKI On Sunday, October 13, 2024 No comments
Bodi ya Bima ya Amana imeeleza kuwa jukumu lake kuu ni kuhakikisha wateja wa benki wanarudishiwa fedha zao pale benki inapopata changamoto au kufilisika, ili kuzuia hasara ya asilimia 100 kwa wananchi waliohifadhi fedha zao.

Mkurugenzi wa Bodi ya Bima ya Amana, Isack Kihwili, alibainisha hayo leo, Oktoba 12, 2024, katika Maonesho ya Teknolojia ya Madini yanayofanyika katika viwanja vya EPZ, Bombambili, Geita. Kihwili alisema bodi hiyo inatoa elimu kwa wananchi ili kuwafahamisha namna wanavyoweza kunufaika na ulinzi wa amana zao kupitia bodi hiyo.

"Sisi ni taasisi ya serikali yenye jukumu la kukinga amana za wateja, ambapo amana ni fedha ambazo watu wanahifadhi katika benki," alisema Kihwili.
Alifafanua kuwa ingawa Bodi ya Bima ya Amana haiwezi kulipa fidia ya asilimia 100, kiwango cha fidia kimewekwa kuwa shilingi milioni 7.5 kuanzia Februari 2023. Kiasi hiki kitatolewa kwa wateja wa benki ambayo imepata changamoto ya kufilisika.

"Utaratibu ni kwamba hatulipi asilimia 100 ya fidia, lakini kiwango kilichowekwa ni milioni 7 na laki 5. Iwapo mteja alikuwa na kiasi chochote kinachozidi kiwango hicho, atarudishiwa fedha zake hadi kufikia milioni 7.5 bila kujali hali ya benki husika," aliongeza Kihwili.

Alieleza kuwa endapo mteja alikuwa na kiasi cha chini ya milioni 7.5, atalipwa fedha zote kwa utaratibu uliowekwa. Kihwili alifafanua zaidi kuwa utaratibu huu unazingatia ridhaa ya serikali pamoja na uwezo wa mfuko wa Bima ya Amana katika kufidia wateja.

Akijibu swali la mmiliki wa Full Shangwe Blog, John Bukuku, kuhusu vigezo vilivyotumika kuweka kiwango hicho cha fidia, Kihwili alieleza kuwa kiwango hicho kimewekwa kwa kuzingatia uwezo wa mfuko na hali ya uchumi wa nchi.

"Kuanzia mwaka 2010 hadi mwaka 2022, kiwango cha fidia kilikuwa milioni 1.5, lakini kutokana na ukuaji wa uchumi na mfuko kuwa na uwezo wa kifedha zaidi, tumeongeza kiwango hicho mara tano hadi milioni 7.5," alisema Kihwili.

Pia alisisitiza kuwa si jambo jema kulipa fidia kwa asilimia 100 hata kama mfuko unaruhusu, kwani kuna hofu ya kuibuka kwa tatizo linaloitwa 'moral hazard,' ambapo watu hawatakuwa makini katika kufuatilia hali ya benki wanazoweka fedha zao.

Kihwili alihitimisha kwa kutoa wito kwa wananchi kufuatilia maendeleo ya benki wanazoweka fedha zao kila robo mwaka ili wawe na uhakika wa usalama wa amana zao.

Posted by MROKI On Sunday, October 13, 2024 No comments

October 12, 2024






Na Mwandishi Wetu
Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) imepokea ugeni kutoka nchini Sierra Leone kwa lengo la kujifunza mbinu bora za ujenzi wa barabara za mwendokasi (BRT) pamoja na daraja la Tanzanite. Ugeni huo ulitoka katika taasisi mbalimbali za Wizara ya Ujenzi ya Sierra Leone.

Kaimu Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Mhandisi Ephatar Mlavi, amesema wageni hao walitembelea ujenzi wa mradi wa BRT awamu ya 3 unaoanzia Gongolamboto hadi Posta. Wageni hao wamevutiwa na mradi huo kutokana na kwamba nchini kwao hawana mradi kama huo unaopunguza msongamano wa magari.

"Wageni wetu wamekuja kujifunza kutoka kwetu kwa kuwa wanataka kuboresha miundombinu ya barabara kwao. Wameona tunafanya vizuri katika ujenzi wa barabara za mwendokasi na madaraja, kama vile Daraja la Tanzanite na barabara za mzunguko zinazojengwa Dodoma, pamoja na upanuzi wa barabara kwenye miji ya Mbeya, Arusha, na Dar es Salaam," alisema Mha. Mlavi.

Aidha, wageni hao walitembelea Daraja la Tanzanite lililopo Salender, ambapo walijifunza kuhusu ujenzi wa madaraja yanayopita juu ya maji. Pia walijifunza jinsi TANROADS inavyotumia wahandisi wa ndani katika ujenzi wa miundombinu inayounganisha mikoa na maeneo muhimu kwa usafirishaji.

Mhandisi Mlavi aliongeza kuwa mafanikio ya TANROADS yanatokana na wataalam wenye weledi na ushirikiano mzuri kati ya watumishi wa Wakala huo, Serikali Kuu, na Wizara husika, huku akisisitiza umuhimu wa mipango madhubuti katika ujenzi wa miundombinu.

Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Barabara wa Sierra Leone, Mohamed Kallon, alisema wamejifunza mengi kutoka TANROADS, licha ya kuwa Wakala ya Tanzania ni mchanga zaidi tangu kuanzishwa kwake mwaka 2000, ikilinganishwa na yao iliyoanzishwa mwaka 1992, lakini bado hawajafanikiwa kujenga barabara za kiwango cha Tanzania.

Naye Muelimishaji Umma wa Serikali za Mitaa wa Sierra Leone, Bi. Martha Gbouma, alisema TANROADS imefanya kazi nzuri katika ujenzi wa barabara, na wamepanga kutumia elimu waliyopata kuboresha miundombinu ya barabara nchini kwao.

Mtaalam wa Usimamizi wa Mali za Barabara, Mha. Kingstone Gongera, alisema kuwa ameona jinsi matengenezo ya barabara yanavyofanyika kwa msaada wa Mfuko wa Barabara, jambo ambalo litawasaidia kuboresha utendaji wao nchini Sierra Leone.
Posted by MROKI On Saturday, October 12, 2024 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo