
Na Mwandishi wetu, Dodoma
Wanawake nchini Tanzania wanaojishughulisha na mnyororo wa thamani madini wameshauriwa kufanya shughuli za madini katika mwamvuli mmoja utakaowatambulisha kulingana na huduma zitolewazo ndani ya Sekta ya Madini ikiwemo Uchimbaji, Uchenjuaji, Uongezaji thamani.
Rai hiyo imetolewa leo Aprili 22, 2026 na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati akizungumza na wanawake wanaojihusisha za shughuli za madini katika mnyororo mzima wa thamani madini nchini.
Waziri Mavunde amesema kuwa, ni wakati sasa wa kutengeneza jukwaa moja litakalobeba vyama vyote ambapo itakuwa rahisi kuwafikia kwa pamoja na kwa wakati mmoja tofauti na ilivyosasa.
Waziri Mavunde amesema, katika nyanja ya uongezaji thamani madini , Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan ametoa shilingi bilioni 30 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Kituo cha mafunzo ya Uongezaji thamani madini (TGC) ambacho ni fursa kwa Wanawake walio katika mstari wa uongezaji thaman madini.
Aidha, Waziri Mavunde ameeleza kuwa, Mpango wa Ushirikishwaji kwa Wazawa (Local Content) una fursa mbalimbali ambapo kila mwaka utengwa kiasi cha trilioni 5.1 kwa ajili ya manunuzi na huduma za migodini , hivyo kupitia jukwaa moja ndani ya vyama husika ni rahisi kuingia katika mnyororo huo.
Waziri Mavunde amefafanua kuwa kupitia Programu maalum ya (MBT) , inakuja na mpango maalum wa kuwawezesha Wanawake, Vijana na Watu wenye uhitaji maalum kwa kuwapatia leseni , vifaa na mashine na kuwapatia mafunzo maalum ya uchimbaji na uchenjuaji madini.
Pamoja na mambo mengine , Waziri amewapongeza wachimbaji wanawake na wachimbaji wadogo wote kwa mchango wanatoa katika sekta ya madini, ambapo umepelekea kuchangia Pato la Taifa kwa asilimia 10.1.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini Wanawake Tanzania(TAWOMA) Semeni Malale ameipongeza Wizara ya Madini na taasisi zake kwa Juhudi mbalimbali inazofanya za kuwawezesha wachimbaji wanawake nchini.
Vyama vilivyoshiriki mkutano huo ni pamoja na TAWOMA, Chama cha Wanawake Wachimbaji Madini ya Viwanda (TWIMMI), Muungano wa Wanawake wanaojihusisha na Uchimbaji Madini(WIMA) na Chama cha Wanawake Wachimbaji na Waongezaji thamani ya madini Tanzania (WIMO).





























































