Nafasi Ya Matangazo

February 26, 2026





Na Mwandishi wetu, Manyara
MGODI wa Itracom Fertilizer Limited unaojihusisha na uchimbaji na uchakataji wa madini ya phosphate uliopo  katika eneo la Vilima Vitatu, Wilayani Babati mkoani Manyara, umechangia Shilingi Bilioni 1.29 katika mapato ya Serikali tangu kuanza kwa shughuli zake mwaka 2023.

Hayo yamebainishwa na Mjiolojia, Waziri Mkupe, akizungumza kwa niaba ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Manyara, Godfrey Nyanda, ambapo amesema mapato hayo yametokana na mrabaha na ada ya ukaguzi wa madini.

Amesema tangu kuanza kwa uzalishaji, mgodi huo umezalisha jumla ya tani 69,929 za madini ya phosphate zenye thamani ya Shilingi Bilioni 36.99, ambazo zimeuzwa katika soko la ndani na nje ya nchi, hususan Nala mkoani Dodoma na nchini Burundi.

Kwa mujibu wa Mkupe, mchango huo umeimarisha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali na kuchochea maendeleo ya jamii inayozunguka mgodi kupitia utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR).

Ameeleza kuwa tangu kuanza kwa shughuli zake, mgodi huo umechangia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa Shule ya Msingi Vilima Vitatu, nyumba za walimu, na upo katika hatua za awali za ujenzi wa bweni la shule ya sekondari ya wasichana.

Akifafanua kuhusu mauzo ya ndani, amesema kuanzia Desemba 16, 2023 hadi Februari 24, 2026, jumla ya tani 22,686 zenye thamani ya Shilingi bilioni 9.07 ziliuzwa kwenda Nala, Dodoma. Katika mauzo hayo, Serikali ilikusanya Shilingi milioni 90.74 kama mrabaha na kiasi kama hicho kama ada ya ukaguzi.

Kuhusu mauzo ya nje, amesema vibali 13 vilitolewa kwa ajili ya kusafirisha tani 47,243 za madini ya phosphate kwenda Burundi zenye thamani ya Shilingi Bilioni 27.92. Katika kipindi cha Septemba 4, 2024 hadi Februari 24, 2026, Serikali ilikusanya Shilingi milioni 837.64 kama mrabaha na Shilingi milioni 279.21 kama ada ya ukaguzi.

“Mgodi wa Itracom Fertilizer Limited umeendelea kudhihirisha kuwa sekta ya madini ya phosphate ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Manyara kwa kuongeza mapato ya Serikali, kutoa ajira na kuimarisha maendeleo ya jamii,” amesema Mkupe.

Aidha, amewahimiza Watanzania kuchangamkia fursa za uwekezaji zilizopo mkoani humo, akibainisha kuwa pamoja na madini ya phosphate, Mkoa wa Manyara una rasilimali nyingine zikiwemo dhahabu, moonstone, green tourmaline, amethyst, green aventurine, limestone, azurite, chumvi, muscovite mica, feldspar na quartz crystal.
Posted by MROKI On Thursday, February 26, 2026 No comments
   

Mbunge wa Jimbo la Kisarawe mkoani Pwani, Selemani Jafo, ameonesha kuridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi wa maji katika Kijiji cha Nyani, Kata ya Mafizi, akieleza kuwa hatua iliyofikiwa inaleta matumaini mapya kwa wananchi.

Mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya BROADWAYS ENGINEERING CO LTD una thamani ya shilingi milioni 402.8 na hadi sasa umefikia asilimia 70 ya utekelezaji, jambo linaloashiria kuwa upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wakazi wa eneo hilo si wa muda mrefu tena.

Kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji, mradi unahusisha ujenzi wa mnara wa tanki la maji lenye urefu wa mita 12 na uwezo wa kuhifadhi lita 50,000, pamoja na ujenzi wa vituo vitano vya kuchotea maji na ulazaji wa mtandao wa mabomba wenye urefu wa kilometa 16.167.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Dkt. Jafo alimpongeza mkandarasi kwa kufanya kazi kwa kasi na weledi mkubwa, akibainisha kuwa kampuni hiyo imeendelea na kazi hata kabla ya kupokea malipo yoyote, jambo alilolitaja kuwa ni uzalendo na kujitolea kwa maendeleo ya wananchi.

Kutokana na kasi hiyo, Jafo ameiiomba Wizara ya Maji kulipa kiasi cha shilingi milioni 279.1 kwa kazi zilizokamilika ili kumwezesha mkandarasi huyo kuendelea na hatua zilizobaki na kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.

Mbali na mkandarasi, mbunge huyo pia amempongeza Meneja wa RUWASA Wilaya ya Kisarawe, Mhandisi Evangelista Kahwili, kwa usimamizi makini wa miradi ya maji ndani ya jimbo hilo, akisema nidhamu na ufuatiliaji wa karibu umechangia mafanikio yanayoonekana.

Wananchi wa Nyani na maeneo ya jirani wanatarajia kunufaika na mradi huo mara utakapokamilika, huku wakieleza kuwa utapunguza adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta maji na kuboresha afya pamoja na shughuli za kiuchumi katika eneo hilo. 

Posted by MROKI On Thursday, February 26, 2026 No comments




Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimetoa salamu za rambirambi kwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddeus Ruwa’ichi OFMCap, kufuatia kifo cha Askofu Mkuu mstaafu wa Jimbo hilo, Mwadhama Polycarp Kadinali Pengo, aliyefariki dunia Februari 19, 2026, katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) alipokuwa akipatiwa matibabu.

Akizungumza Februari 26, 2026 baada ya kusaini kitabu cha maombolezo katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu, Dar es Salaam, Katibu Mkuu CCM, Dkt. Asha-Rose Migiro, alisema amewasilisha salamu za rambirambi kwa niaba ya Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Dkt. Migiro alisema marehemu Kadinali Pengo atakumbukwa kama mchungaji wa faraja na tumaini, kiongozi wa kiroho mwenye hekima, unyenyekevu na msimamo thabiti wa maadili. 

Alijipambanua si tu kwa huduma ya Kanisa, bali pia kwa mchango wake katika kuimarisha mshikamano wa kitaifa, maadili ya jamii, malezi ya vijana na uwajibikaji wa viongozi.

“Kadinali Pengo ameacha alama inayodumu ya utumishi wa Mungu, utumishi wa Taifa na utumishi wa jamii. Maisha na mafundisho yake yataendelea kuwa dira kwa vizazi vijavyo,” alisema Dkt. Migiro.

CCM imesema inaliombea Kanisa Katoliki na waumini wote wapate faraja katika kipindi hiki cha maombolezo na  Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.

Kwa mujibu wa ratiba ya mazishi, mwili wa marehemu utawasili Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu Februari 27, 2026 kwa ajili ya waumini kutoa heshima zao za mwisho, na Ibada ya Misa ya Mazishi itafanyika Februari 28, 2026 katika Kituo cha Hija Pugu, Dar es Salaam.
Posted by MROKI On Thursday, February 26, 2026 No comments

February 25, 2026




Na Heri Shaaban ,Dar es Salaam
Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo, amewasilisha Taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya chama cha Mapinduzi CCM ya Desemba 2025 mpaka FEBRUARY 2026 kwa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya ccm wilaya ya Ilala. 


Akiwasilisha taarifa hiyo Mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo, amesema Halmashauri hiyo imejipanga kujenga vyumba vya madarasa kwa ajili ya kupokea wanafunzi  65000 ambapo Halmashauri hiyo imeweka fedha nyingi sekta ya Elimu. 

Alisema miradi yote Ilala imekamilika kwa asilimia 89 changamoto ilikuwa katika vyumba vya madarasa kwa sasa wanaenda kuitatua changamoto ndani ya wilaya Ilala. 

"Leo nimewasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani katika taarifa hii tumeelekeza shilingi bilioni 80 kuelekezwa katika miradi mbalimbali ya maendeleo katika fedha  shilingi bilioni  347 zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan ambapo natumia fursa hii kumpongeza Rais kwa kushusha Neema Ilala inaenda kuwa ya kisasa" amesema Mpogolo .

Katika hatua nyingine aliagiza viongozi wa ngazi ya kata kusimamia vikundi vya mikopo ya Serikali ya asilimia kumi ambayo inatolewa ngazi ya Halmashauri wakishirikiana Umoja wanawake UWT Wilaya ya Ilala katika kuratibu vikundi hivyo .

Akizungumzia migogoro ya ardhi ndani ya wilaya Ilala  ameagiza viongozi wa chama na Serikali kushirikiana pamoja katika kutatua changamoto hizo.

Alitumia fursa hiyo kuwapongeza Wajumbe wa Halmashauri Kuu wilaya ya Ilala wakiongozwa na Madiwani na Wabunge kwa kufanya kazi kwa kushirikiana 

Wakati huohuo Mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo amesema Wenyeviti wa Serikali za mitaa 159 wa Wilaya ya Ilala hivi karibuni wanatarajia kukabidhiwa Vitamburisho vyao vya kazi  hivyo aliwataka wavute subira taratibu zote zimekamilika 

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Ilala Said Sidde alitumia fursa hiyo kumpongeza mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo pamoja na Katibu Tawala Wilaya Charangwa Selemani na Watendaji wote kwa kuleta maendeleo makubwa Ilala. 

Mwenyekiti Side alisema Ilala wana mahusiano mazuri kati ya chama na Serikali katika utendaji wao wa kazi kila jambo wanashirikiana pamoja kujenga Serikali. 


Meya wa Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam Nurudini sheta ameomba Wajumbe wa Halmashauri Kuu wilaya waweze kupatiwa mafunzo kwa ajili ya kuwajengea uwelewa kila mjumbe aweze kufanya kazi kwa Weledi. 
Posted by MROKI On Wednesday, February 25, 2026 No comments






Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeyapatia ufumbuzi malalamiko ya muda mrefu ya viwanja mbadala kwa wananchi wa jiji la Dodoma.

Suluhisho hilo linafuatia malalamiko ya takriban wananchi 4000 wa jiji la Dodoma wanaodai viwanja na halmashauri ya jiji la Dodoma kuwapa ahadi bila kutekeleza mpaka sasa.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 25 Februari 2026 na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo wakati akizungumza na wananchi wenye migogoro ya ardhi katika eneo la Mahomanyika lilopo kata ya Nzuguni jijini Dodoma.

Dkt Akwilapo amesema, eneo la Mahomanyika ni eneo la serikali hivyo lipangwe na kupimwa kwa ajili ya utatuzi wa migogoro ya meneo mbalimbali ya jiji la Dodoma pamoja na matumizi ya serikali.

"Eneo hili lenye mgogoro hapa Mahomanyika ni eneo la serikali hivyo lipangwe na kupimwa kwa ajili ya utatuzi wa migogoro na siyo ya hapa tu na mingine ya jiji la Dodoma na matumizi ya serikali" amesema.

Amesisitiza kuwa katika upangaji wa eneo hilo kipaumbele kiwe kutatua changamoto za wananchi wa jiji la Dodoma ambao kwa muda mrefu wamedai viwanja na jiji kuwaahidi bila ya kuwapatia.

Katika kufanikisha zoezi hilo, zimeundwa timu mbili kwa ajili ya upangaji na upimaji na pamoja na ile ya kushughulika na uhakiki wa wananchi wenye migogoro na kustahili kupatiwa  viwanja mbadala.

"Timu hizi zitaanza kazi mara moja na kazi hiyo itafanyika kwa muda wa siku sitini, miezi miwili kazi iwe imekamilika kila mtu kujua amepata nini na anaenda wapi" amesema.

Akigeukia uuzwaji viwanja 1,037 vilivyoingizwa kwenye mfumo wa TAUSI ili wananchi wapate viwanja vilivyopimwa katika eneo la Mahomanyika, Dkt. Akwilapo amuagiza Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma kuendelea na uuzaji viwanja kwa waombaji 352 pekee walioanza kulipa huku wale ambao hawajaanza kulipa maombi yao yasitishwe.

Eneo la Mahomanyika limekuwa na changamoto ya malalamiko ya muda mrefu kutoka kwa wananchi wakidai ni wamiliki wa asili wa maeneo hayo jambo lililosababisha kuundwa kwa Timu (Timu ya DC) ambayo ilishirikisha wananchi, Vyombo vya Usalama na Wataalam ambapo timu hiyo ilibaini eneo husika ni eneo la Serikali.
Posted by MROKI On Wednesday, February 25, 2026 No comments

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila leo Feb 25,2026 amekutana na Gavana wa Jimbo la Maniema-Congo DRC Mhe Mussa Kabwankubi Moise akiwa ameambatana na ujumbe wake alipomtembelea Ilala Boma Jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo yao wamekubaliana mashirikiano katika nyanja mbalimbali ikiwemo Uchumi na Masuala ya Kiusalama kati ya Mkoa wa Dar es Salaam na Jimbo la Maniema.

Aidha RC Chalamila amesema Congo na Tanzania ni majirani na ni marafiki wa muda mrefu ndiyo maana katika Mkoa wa Dar es Salaam wakongo ni wengi na wanajishughulisha na shughuli mbalimbali ikiwemo biashara

"Ukiangalia  kupitia Bandari ya Dar es Salaam mzigo unaokwenda Congo kitakwimu ni kiasi kikubwa kwa mwaka hivyo Mkoa unathamini sana wacongo" Alisema Chalamila










Posted by MROKI On Wednesday, February 25, 2026 No comments
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imetoa Tuzo za ubunifu kwa washindi 9 waliotoa mawazo bora zaidi yatakayosaidia kuendelea kuboresha huduma za kodi na kuongeza wigo wa kodi. 

Akikabidhi tuzo hizo, vyeti pamoja na hundi kwa washindi hao Februari 25.2026, Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar ameipongeza TRA kwa kuja na Tuzo hizo ambazo zitaongeza ukaribu na ushirikishwaji wa wananchi katika masuala ya ukusanyaji wa kodi. 

Mshindi wa jumla katika tuzo hizo ni Gabriel Mashenene ambaye amepatiwa hundi ya Sh. Milioni 50, washindi watatu wamepatiwa Sh. Milioni 30 kila mmoja huku washindi 5 wakipatiwa Sh. Milioni 20  kwa kila mmoja.










Posted by MROKI On Wednesday, February 25, 2026 No comments

 Na Mwandishi wetu, Ruvuma
Wapiga Kura 127,632 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki katika uchaguzi wa kuchagua Mbunge katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Mkoa wa Ruvuma na Kata ya Shiwinga iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi Mkoa wa Songwe.
 
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele ameyasema hayo leo Februari 25, 2026 mjini Songea Mkoani Ruvuma wakati akisoma risala maalum kuhusu uchaguzi katika jimbo na kata husika utakao fanyika kesho Februari 26, 2026 na kusema kuwa jumla ya vituo 373 vya Kupigia Kura vitatumika.
 
“Kati yao wapiga kura 120,780 ni wa Jimbo la Peramiho na wapiga kura 6,852 wapo katika kata ya shiwinga na jumla ya vituo 373 vya Kupigia Kura vitatumika, ambapo vituo 354 vipo Jimbo la Peramiho na vituo 19 vipo katika Kata ya Shiwinga Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi,”amesema Jaji Mwambegele.
 
Aidha, amesema kwa uchaguzi mdogo wa ubunge Jimbo la Peramiho vyama vya siasa 15 vimesimamisha wagombea na  kwa upande wa uchaguzi mdogo wa udiwani katika Kata ya Shiwinga vyama vya siasa nane (08) vimesimamisha  wagombea.
 
“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho Februari 26, 2026 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Jimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.
 
Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.
 
Jaji Mwambegele amesema vituo vitafunguliwa saa 01:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni na kwamba ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapiga kura bado wapo kwenye mistari, mlinzi wa kituo atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapiga kura walio kwenye mstari watakapomalizika.
 
“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpiga kura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura; na Mpiga kura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapiga kura,”amesema Jaji Mwambegele.
 
Kwa mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi yake au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga Kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, Leseni ya udereva au Pasi ya kusafiria (Passport).

Posted by MROKI On Wednesday, February 25, 2026 No comments

February 24, 2026

Taswira ya Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma mara baada ya kuzinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, tarehe 24 Februari, 2026.
Matukio mbalimbali yakimuonesha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alipozindua rasmi Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma tarehe 24 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Maafisa Askari, Watumishi wa umma na wageni mbalimbali waliohudhuria uzinduzi wa Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma tarehe 24 Februari, 2026.












 

Posted by MROKI On Tuesday, February 24, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo