Nafasi Ya Matangazo

June 24, 2026


Na Mwandishi Maalumu – Dodoma
Jumla ya watu 546 wamefanyiwa uchunguzi wa afya kwa kupimwa Namba Zao wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi wa afya iliyokuwa ikifanyika katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma.
Kupitia kambi hiyo iliyomalizika leo katika Viwanja vya Chinangali Park vilivyopo jijini Dodoma watu waliotembelea katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) walifanyiwa vipimo vya kuchunguza ugonjwa wa shinikizo la damu, kiwango cha sukari kwenye damu, uwiano wa urefu kwa uzito pamoja na mzunguko wa kiuno.
Aidha watu 192 walifanyiwa kipimo cha kuchunguza utendaji kazi wa moyo (Echocardiography – ECHO), huku watu 11 wakifanyiwa kipimo cha kuangalia mfumo wa umeme wa moyo (Electrocardiography – ECG).
Akizungumza wakati wa kuhitimisha kambi hiyo Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Daud Gwilenza alisema watu 94 wamepewa rufaa kwenda katika Taasisi hiyo kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
“Watu 82 tumewabaini kuwa na tatizo la shinikizo la juu la damu, huku watu 20 tumewabaini kuwa na tatizo la sukari. Baadhi ya watu hawa walikuwa tayari wanajua hali zao lakini wengine hawakuwa wanajua kama wana matatizo ya shinikizo la damu na sukari”, alisema Dkt. Daud.
Dkt. Daud aliongeza kuwa magonjwa mengine yaliyobainika kupitia kambi hiyo ni pamoja na kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo na kutanuka kwa moyo hali ambayo kwa kiasi kikubwa husababishwa na shinikizo la damu la muda mrefu.
“Jamii inapaswa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara, hii itatusaidia kulinda afya zetu na kuchukua hatua mapema tunapogundulika kuwa na magonjwa yasiyoambukiza ambayo kwa sasa yanaongezeka kwa kasi katika jamii yetu”, alisema Dkt. Daud.
Kwa upande wao wananchi waliopata huduma katika banda la JKCI waliishukuru Serikali kwa kuwezesha kufanyika kwa Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mkoani Dodoma jambo lililowapa fursa ya kufanyiwa uchunguzi wa afya bila gharama.
James Balilonga mkazi wa Dodoma alisema maonesho hayo yamemsaidia kutambua umuhimu wa kufanya uchunguzi wa afya hata pale mtu anapokuwa hana dalili za ugonjwa.
“Unapokutana na wataalamu wa afya na kupata elimu kuhusu umuhimu wa kuchunguza  afya unahamasika kuchukua hatua. Hili limekuwa fundisho kwangu kwamba siyo lazima nisubiri kuumwa ndipo nifanye uchunguzi wa afya”, alisema James.
Naye Doris Mwirezeyo alizitaka taasisi za afya kuanzia ngazi ya Wilaya kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kuchunguza afya mara kwa mara ili kuwasaidia wananchi kujikinga na magonjwa na kupata matibabu kwa wakati.
“Leo nimejifunza jambo muhimu, kama tungekuwa na utamaduni wa kupima afya mara kwa mara na kuzingatia mtindo bora wa maisha pengine tusingekuwa na wagonjwa wengi wenye matatizo ya moyo, elimu hii inapaswa kuwafikia wananchi hadi ngazi za chini ili waweze kujilinda”, alisema Doris.

Posted by MROKI On Wednesday, June 24, 2026 No comments
Na: Dkt. Reubeni Lumbagala 
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ni chombo muhimu nchini katika kuhakikisha mipango na mikakati ya maendeleo inatimizwa kikamilifu. Hii inatokana na ukweli kuwa mipango mingi ya maendeleo kama uboreshaji wa sekta za elimu, afya, maji, masoko, viwanda, umeme, barabara, makazi, biashara, inategemea upatikanaji wa raslimalifedha ili ziwezeshe utekelezaji wake.

TRA ina wajibu wa kukusanya kodi kutoka kwa walipakodi wake kama wafanyabiashara, wawekezaji, wafanyakazi na wajasiriamali mbalimbali. Mafanikio ya ukusanyaji kodi, ndiyo msingi wa kuiwezesha serikali kutimiza mipango yake ya maendeleo kwa ustawi na maendeleo ya wananchi.

Sasa TRA imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake. TRA imepata mafanikio makubwa sana hasa katika uongozi wa serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Rais Dk. Samia aliweka msingi wa serikali yake mapema kwa kuiagiza TRA iwajibike ipasavyo katika kukusanya mapato, lakini mapato hayo yasiwe ya dhuluma. Rais Dk. Samia anataka kila mwananchi mwenye sifa za kulipa kodi alipe.

Aprili 6, 2021, Rais Dk. Samia alipokuwa akiwaapisha makatibu wakuu na manaibu wao, alitoa maelekezo mahsusi kwa TRA. "Kukusanya kodi kwa mabavu havisaidii kwa muda mrefu. Nimepewa takwimu ya zile taskforce (vikosikazi vya kukusanya kodi) mlizoziunda lakini havisaidii, mnawatisha watu wanalazimika kufunga biashara."

"Tunazitaka kodi lakini kodi za dhuluma hapana. Kwa sababu hazitatufikisha mbali. Jinsi ya kurudisha wafanyabiashara, kutengeneza wigo wa kukusanya kodi, nafahamu uamuzi huu niliochukua tutayumba kwa miezi miwili, mitatu lakini baada ya muda tutarudi vizuri," amesema Rais Dk. Samia.

Msisitizo wa kuongeza mapato ulitokana na ukweli kuwa mipango mingi na mizuri aliyonayo Rais Dk. Samia kwa wananchi wake, haitaweza kufanikiwa kama TRA haitakusanya kodi kikamilifu ambayo ndiyo kichochea cha kufanikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Awali, TRA ilikuwa na utaratibu wa kufunga biashara na shughuli mbalimbali pale ambapo mlipakodi atashindwa kulipa kodi kwa wakati. 

Vilevile, katika makadirio ya kodi, baadhi ya wafanyabiashara walikuwa wakilalamikia kuwekewa makadirio makubwa tofauti na kiwango cha biashara zao. Hii iliweka uadui mkubwa kati ya TRA na walipakodi nchini.

MAGEUZI MAKUBWA YAMEONDOA UADUI KATI YA TRA NA WALIPAKODI

Kutokana na maelekezo ya Rais. Dk. Samia kwa TRA, uadui uliokuwepo awali kati ya TRA na walipakodi umeondoka. Hii inatokana na mtazamo chanya alioujenga Rais Dk. Samia kwa pande zote mbili. 

Kimsingi, pande zote mbili zinategemeana. TRA anamtegemea mlipakodi kwani pindi kodi inapolipwa ndipo inawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo inamnufaisha mlipakodi moja kwa moj.

Rais Dk. Samia akasisitiza pawepo na meza ya mazungumzo na makubaliano ya namna gani mlipakodi atalipa kodi pale ambapo atashindwa kulipa kwa wakati.

Aidha, Rais Samia akasisitiza kuwa kufunga biashara ni kummaliza kabisa mlipakodi kwani biashara yake itakapofungwa, ndipo atashindwa kabisa kulipa kodi kwani hatakuwa na shughuli ya kumuingizia kipato cha kuwezesha kulipa kodi na wala TRA haitaweza kupata kodi yake.

Kongole kwa Kamishna Mkuu wa TRA, Yusuph Mwenda, pamoja na wasaidizi wake nchi nzima wamefanyia kazi maelekezo ya Rais, na sasa tunashuhudia mafanikio ya kumalizika kwa uadui uliokuwepo awali.

Ni faraja kuona tunapoadhimisha miaka 30 ya TRA, kumejengeka uhusiano mzuri kati ya mlipakodi na mamlaka. Hakuna mabavu wala ubabe. Uhusiano mzuri uliopo umewezesha kuongezeka kwa mapato ya serikali.

Mathalani, mwezi Machi, 2026,  TRA wamefanikiwa kukusanya trilioni 3.58, na kimsingi, ongezeko la makusanyo yamewezesha hata bajeti ya mwaka 2026/2027, kutegemea mapato ya ndani kwa asilimia 74.2.

Maoni : 0620 800 462
Posted by MROKI On Wednesday, June 24, 2026 No comments

June 23, 2026






Na Benny Mwaipaja, Dodoma
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, limepitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

Akitangaza matokeo ya kura ya wazi iliyopigwa bungeni jijini Dodoma, Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azzan Zungu alisema kuwa kati ya kura hizo 393 zilizopigwa, kura 8 zimekataa kuunga mkono bajeti hiyo na wabunge wengine nane 8 hawakupiga kura kwa sababu hawakuwepo bungeni.

Akihitimisha hoja baada ya Bunge kupitisha Muswada wa Sheria kwa ajili ya kuidhinisha Serikali kuanza kutekeleza Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/2026 (zaidi ya shilingi trlilioni 62.33) kutoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina, Mhe. Spika Zungu alimpongeza Waziri wa Fedha, Mhe. Ballozi Khamis Mussa Omar (Mb) wasaidizi wake, watendaji wa Wizara kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya na Wabunge wote kwa michango yao yenye tija kwa Taifa.

“Kura zimepigwa na Serikali imeruhusiwa kuzitumia pesa kuanzia sasa, mkazitumie pesa hizi kama Kamati za Bunge zilivyoelekeza, kuhakikisha maslahi ya watu kwanza yanazingatiwa kabla ya mambo mengine. Bunge hili litaendelea kufuatilia utekelezaji wake na kuhakikisha kuwa miradi yote iliyoainishwa inazingatiwa na kuleta furaha kwa wananchi” alisisitiza Mhe. Zungu.

Kupitia kwa Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), Serikali ililiomba Bunge lipitishe Bajeti ya shilingi trilioni 62.33 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo katika Mwaka wa Fedha 2026/2027, ikiwa ni ongezeko la asilimia 10.3 ikilinganishwa na bajeti ya mwaka 2025/26. 

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, mapato yalitarajiwa kuwa shilingi trilioni 46.79 ambapo mapato ya kodi ni shilingi trilioni 36.99, mapato mengine ni shilingi trilioni 9.24 (ikijumuisha mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa shilingi trilioni 1.977) na misaada kutoka kwa washirika wa maendeleo shilingi bilioni 563.1.

Aidha aliongeza kuwa ili kuendana na dhamira ya kujitegemea katika uendeshaji wa Serikali na maendeleo, takribani robo tatu ya bajeti yote ya mwaka 2026/27, sawa na asilimia 74.2 itagharamiwa na mapato ya ndani.

Matumizi na uwekezaji katika mali zisizo za kifedha yalikadiriwa kuwa shilingi trilioni 54.50 pasipo kujumuisha malipo ya mtaji wa deni la Serikali ambapo kati ya kiasi hicho, stahiki za watumishi ikijumuisha michango ya pensheni ni shilingi trilioni 10.13.

“Gharama za bidhaa na huduma itakuwa shilingi trilioni 5.22, malipo ya riba ni shilingi trilioni 6.86, ruzuku shilingi trilioni 25.32, mafao na misaada ya kijamii shilingi trilioni 1.01, uwekezaji katika mali zisizo za kifedha shilingi trilioni 2.33 na gharama nyingine shilingi trilioni 3.63.” alisema Mhe. Balozi Omar

Aliongeza kuwa kulingana na makadirio ya mapato na matumizi hayo, kunajitokeza nakisi kwenye bajeti ya shilingi trilioni 7.71 na Serikali itaendelea kugharamia nakisi ya bajeti hiyo kwa kutumia mikopo kutoka vyanzo vya ndani na nje kwa kuzingatia Mkakati wa Muda wa Kati wa Kusimamia Deni la Serikali (2025/26 – 2027/28).

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, katika mwaka 2026/27, Serikali inatarajia kukopa jumla ya shilingi trilioni 15.54 ambapo kati ya kiasi hicho, mikopo ya ndani itakuwa shilingi trilioni 6.56, mikopo ya nje yenye masharti nafuu shilingi trilioni 6.55 na mikopo ya nje yenye masharti ya kibiashara shilingi trilioni 2.43.
Aidha, Serikali inakadiria kulipa malipo ya mtaji kwa mikopo iliyoiva shilingi trilioni 7.84.

Baada ya kupitishwa kwa bajeti hiyo, Bunge linatarajia kupokea, kujadili na kupitisha Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2026 ( The Finance Bill,2026) tarehe 24 Juni, 2026.

Mwisho
 
 
Captions

PIX : 1

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, akimpongeza Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

PIX:2

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), na Naibu Mawaziri wake, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) na Mhe. Laurent Luswetula (Mb) wakipongezwa na Wabunge mbalimbali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, baada ya wabunge hao kupitisha kwa kishindo makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali ya shilingi Trilioni 62.33 kwa mwaka 2026/2027, ambapo zaidi ya wabunge 385 sawa na asilimia 97.66 walipitisha kwa kura za ndio.

PIX:3

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, wakipongezana baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

PIX:4

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akipongezwa na Wafanyakazi wa Shule ya Awali na Msingi ya Mzigu ya mkoani Mwanza, baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

PIX: 5

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi waandamizi wa Wizara ya Fedha na Wizara ya Mipango na Uwekezaji, baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

PIX:6

Manaibu Katibu Wakuu wa Wizara ya Fedha, Bw. Elijah Mwandumbya (kushoto) na Bw. Joshua Nsubili, wakipongezana baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)
Posted by MROKI On Tuesday, June 23, 2026 No comments

June 22, 2026







Dodoma
Banda la Tume ya Madini limeendelea kuwa kivutio kikubwa kwa mamia ya wananchi wanaotembelea Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, huku wengi wakijitokeza kupata elimu kuhusu sekta ya madini, huduma zinazotolewa na Tume  pamoja na fursa zilizopo katika shughuli za utafutaji, uchimbaji na biashara ya madini.

Miongoni mwa waliotembelea banda hilo ni Lusajo Luena kutoka Dodoma, ambaye amesema elimu aliyoipata imemwezesha kuelewa taratibu za upatikanaji wa leseni za madini na wajibu wa wamiliki wa leseni katika kuendeleza maeneo yao ya uchimbaji.

"Kabla ya kufika hapa sikuwa na uelewa wa kina kuhusu namna leseni za madini zinavyotolewa na kusimamiwa. Leo nimepata elimu ya kutosha kuhusu taratibu mbalimbali na umuhimu wa kuzingatia sheria za madini," amesema Luena.

Kwa upande wake, Joyce Kitundu kutoka Dodoma amesema maelezo aliyopata katika banda hilo yamemsaidia kufahamu mchango mkubwa wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa taifa na namna Serikali inavyosimamia rasilimali za madini kwa manufaa ya wananchi.

"Nimejifunza kuwa sekta ya madini ni nguzo muhimu ya maendeleo ya nchi. Pia nimeelewa majukumu ya Tume ya Madini katika kusimamia shughuli za uchimbaji na biashara ya madini nchini," amesema Kitundu.

Naye Glory Daudi kutoka Kondoa amesema elimu aliyopata imefungua fursa mpya za uelewa kuhusu ushiriki wa vijana na wanawake katika shughuli mbalimbali zinazohusiana na sekta ya madini.

"Nimefurahishwa na elimu niliyopewa kuhusu fursa zilizopo kwenye sekta ya madini. Sasa nimeelewa kuwa si lazima mtu awe mchimbaji pekee, kwani kuna fursa nyingi za biashara na utoaji huduma zinazozunguka sekta hii," amesema Daudi.

Tume ya Madini inaendelea kutumia maonesho hayo kutoa elimu kwa umma kuhusu majukumu yake, huduma mbalimbali zinazotolewa pamoja na kuhamasisha ushiriki wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya madini ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.
Posted by MROKI On Monday, June 22, 2026 No comments
Na Adelina Johnbosco - MAELEZO
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara, ameipongeza Ofisi ya Msemaji Mkuu wa Serikali na kusema inafanya kazi kubwa ya kuzitangaza shughuli zinazotekelezwa na Serikali pamoja na kuwafikia wananchi.

Prof. Kahyarara amesema hayo Juni 22, 2026, alipotembelea banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na taasisi zake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea kwenye viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.

"Serikali ina shughuli nyingi zinazofanyika ikiwemo miradi mbalimbali, mipango na malengo kwa ajili ya maendeleo na maslahi ya wananchi, hata ukisema kila siku au kila wiki utoke na kitu kimoja lakini bado inakuwa haitoshi, lakini Ofisi ya Msemaji Mkuu wa Serikali inajitahidi kwa kufanya kazi kubwa kwani taarifa zinatolewa kuhusu yanayotekelezwa na Serikali kwa wananchi wake" ameongeza Prof. Kahyarara.

Kwa upande mwingine, ameipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kufikia hatua nzuri katika maandalizi ya AFCON 2027 pia na taifa kwa ujumla kuwa miongoni mwa nchi zilizochaguliwa kuwa mwenyeji wa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) yanayotarajiwa kufanyika nchini Tanzania mwaka 2027.

"Hii inaonesha jinsi gani Tanzania imefikia hatua ya juu katika michezo na imeaminika na ina uwezo wa kuhudumia wageni, lakini pia itakuwa fursa ya kuutangaza utamaduni wetu kwa mataifa mengine" - Prof. Kahyarara. 

Aidha, amesema Wizara ya Uchukuzi tayari imejipanga katika sekta zake za usafiri na usafirishaji kwa kuhakikisha inawahudumia wenyeji na wageni kabla, wakati na baadaya ya AFCON 2027.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026 na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi. Dkt.  Moses Kusiluka
Posted by MROKI On Monday, June 22, 2026 No comments
Afisa Usimamizi wa Fedha Mkuu, Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha, Bw. Abdul Dachi, akitoa elimu kwa wananchi wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Afisa Habari Mkuu, Wizara ya Fedha, Bi. Eva Valeria (kulia) na Afisa Habari, Wizara ya Fedha, Bw. Joseph Mahumi, wakimpa mwanafunzi wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP), Bi. Nice Justace, maelekezo wa namna ya kujiunga na mitandao ya kijamii ya Wizara ya Fedha, ikiwemo, Instagram (urt mof), Facebook (Wizara ya Fedha), LinkedIn (Ministry of Finance -Tanzania), Youtube – Hazina TV.
Afisa Usimamizi wa Fedha Mwandamizi, Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha, Bi. Grace Samwel, akitoa elimu kwa wanafunzi wa Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) kuhusu matumizi ya huduma rasmi za kifedha, walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Mchumi Daraja la Kwanza, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPU), Wizara ya Fedha, Bi. Anastazia Amandi, akitoa elimu kwa mwananchi kuhusu mafanikio ya Ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP), walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Maafisa wa Wizara ya Fedha, wakiendelea kutoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, kuhusu majukumu yanayotekelezwa na wizara hiyo, wakati wananchi hao walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, yenye kauli mbiu ‘Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Maendeleo Endelevu’, yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.
Maafisa wa Wizara ya Fedha, wakiendelea kutoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, kuhusu majukumu yanayotekelezwa na wizara hiyo, wakati wananchi hao walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, yenye kauli mbiu ‘Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Maendeleo Endelevu’, yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.
Na Saidina Msangi na Asia Singano, WF - Dodoma
Wizara ya Fedha imeendelea kutoa elimu kwa umma ili kuhakikisha wananchi wanapata ufafanuzi kuhusu masuala ya kodi, uchumi na sera mbalimbali za fedha na mchango wa kodi katika kugharamia huduma muhimu za kijamii kama vile miundombinu, elimu, afya, maji nishati na huduma nyingine muhimu.
 
Hayo yamebainishwa na Afisa Usimamizi wa Fedha Mkuu, Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha, Bw. Abdul Dachi, wakati akitoa elimu kwa wananchi kwenye  Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.
 
Bw. Dachi alisema kupitia Maonesho hayo, Idara imekuwa ikitoa taarifa kwa wananchi kwa lugha rahisi na inayoeleweka ili kuwawezesha kufahamu mchango wa Sera za Kodi na Uchumi katika maendeleo ya Taifa na ustawi wa jamii.
 
‘‘Miongoni mwa maeneo yanayotolewa elimu ni kuhusu mwenendo wa uchumi wa Taifa na namna Sera za Uchumi zinavyosaidia kudhibiti mfumuko wa bei, kuongeza fursa za ajira na kukuza uchumi kwa ujumla pamoja na namna hizo zinavyoandaliwa ili kuhakikisha mapato ya Serikali yanakusanywa kwa ufanisi na kwa kuzingatia maslahi ya Taifa,’’, alisema Bw. Dachi.
 
Aliongeza kuwa Serikali inatumia taarifa za takwimu na tafiti mbalimbali zinazosaidia katika upangaji wa bajeti na utekelezaji wa mikakati ya maendeleo ya muda mfupi na mrefu pamoja na usimamizi wa mikataba ya kikodi kati ya Tanzania na mataifa mengine na ushirikiano wa kikanda na kimataifa unaolenga kulinda maslahi ya Taifa katika sekta ya kodi.
 
Alifafanua kuwa wananchi wanapatiwa elimu kuhusu namna Wizara inavyofanya tafiti za kisera na kuandaa mapendekezo ya kitaalamu yanayosaidia Serikali kufanya maamuzi yenye tija kwa maendeleo ya nchi pamoja na namna Serikali inavyoshughulikia masuala ya kodi za kimataifa.
 
‘’Tumetumia fursa hii kueleza wananchi umuhimu wa sera za kodi na fedha katika kukuza uchumi na ustawi wa wananchi, mchango wa kodi katika maendeleo ya Taifa, pamoja na umuhimu wa uwazi na uwajibikaji katika mchakato wa utungaji wa sera nafasi ya Tanzania katika uchumi wa dunia na manufaa yanayotokana na ushirikiano wa kiuchumi na mataifa na taasisi mbalimbali za kimataifa’’, alifafanua Bw. Dachi.
 
Alisema kuwa ili kuhakikisha ujumbe unawafikia wananchi wengi zaidi, idara pia inatoa vipeperushi, vitabu vya elimu pamoja na mazungumzo ya ana kwa ana na wageni wanaotembelea Banda hatua inayochangia kuongeza uelewa wa umma na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na wananchi katika maendeleo ya Taifa.

Posted by MROKI On Monday, June 22, 2026 No comments

June 21, 2026





📍Dodoma
Tume ya Madini imeendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa leseni za madini nchini kwa lengo la kufuatilia maendeleo ya leseni hizo na kuhakikisha shughuli za utafutaji na uchimbaji wa madini zinafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Akizungumza katika Banda la Tume ya Madini kwenye Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park mkoani Dodoma, Mtakwimu kutoka Kurugenzi ya Leseni ya Tume ya Madini, Azihar Kashakara, amesema ukaguzi huo ni muhimu katika kuhakikisha wamiliki wa leseni wanatimiza masharti na wajibu unaotokana na leseni walizopewa.

Amesema kuwa, pamoja na kufuatilia maendeleo ya leseni, Kurugenzi ya Leseni ina jukumu la kutoa na kusimamia leseni za madini, kutafsiri na kusambaza takwimu za leseni, pamoja na kuwezesha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali yatokanayo na umiliki wa leseni hizo.

Kashakara ameeleza kuwa utoaji wa leseni za madini unazingatia masharti na vigezo vilivyowekwa kisheria, hivyo waombaji wanapaswa kuyatimiza ili kuwezesha upatikanaji wa leseni kwa wakati. 

Aidha, ametoa ufafanuzi kuhusu ada na tozo mbalimbali zinazohusiana na leseni za madini, sambamba na kueleza tofauti kati ya umiliki wa ardhi (Surface Rights) na umiliki wa haki za madini (Mineral Rights).

Tume ya Madini ni miongoni mwa taasisi zinazoshiriki Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma chini ya kaulimbiu isemayo, “Kuchochea Uwajibikaji kwa Huduma Endelevu.” 

Kupitia maonesho hayo, wananchi na wadau wa sekta ya madini wanapata fursa ya kuelimishwa kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na Tume ya Madini pamoja na mchango wake katika usimamizi endelevu wa rasilimali za madini kwa maendeleo ya taifa.
Posted by MROKI On Sunday, June 21, 2026 No comments
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na Waumini wa Kanisa Kuu Anglikana la Roho Mtakatifu Dodoma mara baada ya kushiriki Ibada ya jumapili katika kanisa hilo leo tarehe 20 Juni, 2026.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na Waumini wa Kanisa Kuu Anglikana la Roho Mtakatifu Dodoma mara baada ya kushiriki Ibada ya jumapili katika kanisa hilo leo tarehe 20 Juni, 2026.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akishiriki Ibada ya Jumapili katika Kanisa Kuu Anglikana la Roho Mtakatifu Dodoma leo tarehe 20 Juni, 2026. (kulia kwake ni Katibu wa Bunge Ndg. Baraka Leonard.
***********
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Watanzania kushirikiana na Serikali katika kutunza na kuhudumia vituo vya watoto wenye mahitaji maalumu na wasiojiweza badala ya kutegemea wahisani kutoka nje kwani mambo hayo yamepitwa na wakati.
 
Ametoa kauli hiyo leo Jumapili, Juni 21, 2026 katika harambee ya uchangiaji wa jengo la kitega uchumi cha kanisa la Anglika jijini Dodoma. “Mambo ya misaada yamepitwa na wakati na hata katika bajeti Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kusisitiza kuwa na bajeti ya nchi ambayo inategemea rasilimali za ndani ya nchi”.
 
Pia, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa rai halmashauri zote nchini ziandae orodha ya vituo vya kulelea watoto wenye mahitaji maalumu na wasiojiweza na kuona namna ya kuvisaidia ambapo amesisitiza si vema kuwaandikia watu hao barua za kwenda kuomba misaada pindi wanapofika kwenye ofisi za umma.
 
Waziri Mkuu amesema awali katika maeneo mbalimbali nchini ilizoeleka kuwa vituo vya kulelea watoto yatima na wenye mahitaji maalumu viliendeshwa kupitia misaada kutoka nje ya nchi dhana ambayo watu wanatakiwa kuachana nayo.
 
Kadhalika, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwahimiza Watanzania kuendelea kusimama katika mafundisho mbalimbali yanayotolewa na viongozi wa dini ikiwemo kuendeleza amani na umoja wa kitaifa.
 
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan analipongeza Kanisa la Anglikana Tanzania kwa kuendeleza mradi wa ujenzi wa kitega uchumi kwa sababu ukuaji wa uchumi ni miongoni mwa malengo muhimu ya maendeleo.
 
Awali, Katibu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Kasisi Canon Dkt. George Lawi alisema ili kuimarisha uwezo wa kifedha na kupunguza utegemezi, Kanisa la Anglikana Tanzania lilianzisha mradi wa kitega uchumi jijini Dodoma na kuhakikisha linakuwa na vyanzo endelevu vya mapato vitakavyowezesha utekelezaji wa majukumu ya kiroho na kijamii kwa ufanisi zaidi.
 
Alisema jengo hilo linatarajiwa kutoa huduma mbalimbali zikiwezo za hoteli, ofisi na hivyo kuchangia katika kukuza uchumi wa kanisa na Taifa kwa ujumla. Mradi huu umefikia hatua ya umaliziaji na umeshagharimu shilingi bilioni tatu na bado zinahitajika shilingi bilioni 1.5 ili kukamilisha na ndiyo sababu ya kufanya harambee leo.
 
Pia, Dkt. Lawi alitumia fursa hiyo kumuahidi Waziri Mkuu kuwa Kanisa Anglikana Tanzania litaendelea kuwa mshirika wa Serikali katika juhudi za kuwaletea wananchi maendeleo endelevu kupitia sekta za elimu, afya, uwezeshaji wa jamii na kukuza maadili mema.
 
Katika harambee hiyo zaidi ya shilingi bilioni moja zilipatikana, ambapo pia Kanisa Anglikana limempa Heshima ya Kikanisa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Lay Canon, mshauri wa mambo ya Kanisa baada ya kuridhishwa na utendaji wake.
Posted by MROKI On Sunday, June 21, 2026 No comments

June 20, 2026










Dar es Salaam
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema Serikali imejipanga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha madini ya kimkakati na shughuli za uongezaji thamani barani Afrika, huku akizitaka taasisi za sekta hiyo kutumia fursa zilizopo kuhakikisha nchi inahudumia masoko ya kikanda na kimataifa.

Mhe. Mavunde ameyasema hayo Juni 19, 2026, baada ya kufanya ziara katika Kituo cha African Minerals and Geoscience Centre (AMGC) kilichopo Kunduchi jijini Dar es Salaam, ambapo alipata fursa ya kutembelea maabara, kitengo cha ukataji, utengenezaji na usafishaji wa vito pamoja na  kuzungumza na viongozi pamoja na watumishi wa kituo hicho.

“Tumedhamiria kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha madini ya kimkakati barani Afrika. Tunayo nafasi kubwa kutokana na eneo letu la kijiografia na miundombinu iliyopo, hivyo ni lazima tutumie fursa hii kuhakikisha tunazihudumia nchi zote zinazotuzunguka na kuifanya Tanzania kuwa lango la huduma za madini katika ukanda huu,” amesema Waziri Mavunde.

Amesema Serikali kupitia Wizara ya Madini inaendelea kutekeleza programu ya *Mining for a Brighter Tomorrow*, inayolenga kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kiuchumi kupitia sekta ya madini.

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, programu hiyo itahusisha utoaji wa mafunzo ya kitaalamu katika vituo mbalimbali vya sekta ya madini ikiwemo AMGC, ambapo wanufaika watapatiwa maarifa pamoja na teknolojia na mashine ndogo zitakazowawezesha kujiajiri na kuongeza kipato chao.

“Tutawaleta vijana, kina mama na watu wenye ulemavu hapa AMGC wapatiwe mafunzo maalum, na baada ya hapo waweze kupata vifaa na mashine ndogo zitakazowawezesha kujiajiri na kuboresha maisha yao kupitia shughuli za madini,” ameeleza.

Katika ziara hiyo, Waziri Mavunde amesema amevutiwa na kiwango cha utaalamu kilichopo AMGC, hususan katika ukataji na utengenezajishaji wa madini ya vito, akisema dhana iliyokuwa imejengeka kuwa Tanzania haina wataalamu wa kutosha katika eneo hilo siyo sahihi.

“Kwa muda mrefu tuliaminishwa kwamba hatuna wataalamu wa kutosha katika ukataji wa madini ya vito, lakini leo nimeshangazwa kukutana na wataalamu wazawa wenye uwezo mkubwa wa kukata na kutengeneza vito kwa viwango vya kimataifa. Huu ni uthibitisho kwamba tuna rasilimali watu wenye uwezo wa kuipeleka Tanzania mbele zaidi,” amesema.

Aidha, Waziri Mavunde amesema hiyo ilikuwa ziara yake ya kwanza katika kituo hicho na kuahidi kukitangaza kimataifa ili kuvutia wawekezaji, wataalamu na wadau mbalimbali wa sekta ya madini kutoka ndani na nje ya Afrika.

“Niwahakikishie kwamba tutakitangaza kituo cha AMGC kimataifa ili Tanzania iwe kitovu cha uongezaji thamani wa madini barani Afrika. Pia nitarudi tena hapa kukutana na watumishi wote, kusikiliza changamoto zao na kujadiliana namna bora ya kukiendeleza kituo hiki,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa AMGC, Ibrahim Shaddad, amesema kituo hicho kinakabiliwa na changamoto ya uhaba wa watumishi, ambapo kwa sasa kina watumishi wa kudumu 17 na watumishi wa mikataba ya muda mfupi 12, hali inayokifanya kushindwa kutekeleza kikamilifu baadhi ya majukumu yake.

Aidha, Shaddad amemuomba Waziri wa Madini kusaidia katika upatikanaji wa fedha za uendeshaji wa kituo hicho, hususan kupitia nchi wanachama ambazo kwa mujibu wa sheria zinapaswa kuchangia gharama za uendeshaji, lakini baadhi yake zimekuwa zikichelewesha au kutotekeleza wajibu huo.

Shaddad amesema ucheleweshaji wa michango kutoka kwa baadhi ya nchi wanachama umeendelea kuathiri shughuli za kila siku za AMGC na kusababisha upungufu wa fedha za uendeshaji.

Ametaja Tanzania, Kenya, Angola na Sudan kuwa miongoni mwa nchi zinazowasilisha michango yao kwa wakati, huku baadhi ya nchi nyingine ikiwemo Msumbiji, Ethiopia, Comoro, Sudan Kusini na Uganda zikikabiliwa na changamoto ya kutowasilisha michango hiyo kwa wakati.

AMGC ni taasisi ya kikanda inayojihusisha na tafiti za jiolojia, huduma za maabara, mafunzo na maendeleo ya teknolojia za madini kwa nchi wanachama wa Afrika, na imeendelea kuwa moja ya taasisi muhimu katika kuendeleza sekta ya madini na kuongeza thamani ya rasilimali za madini barani Afrika. Uh
Posted by MROKI On Saturday, June 20, 2026 No comments

June 19, 2026




Na Adelina Johnbosco - MAELEZO
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, amesema benki hiyo itaendelea kuwa mdau mkubwa wa maendeleo ya michezo nchini kwa kushiriki kikamilifu kufanikisha mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) yanayotarajiwa kufanyika nchini Tanzania mwaka 2027.

Dkt. Nsekela ametoa kauli hiyo Juni 19, 2026, alipotembelea banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea kwenye viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.

Amesema CRDB iko tayari kushirikiana kwa karibu na wizara hiyo katika kuhakikisha maandalizi na utekelezaji wa AFCON 2027 unafanikiwa kwa kiwango kikubwa.

"Sisi CRDB tunaahidi kuwa na wizara hii bega kwa bega kila hatua pale tutakapohitajika. Ni wadau wakubwa wa michezo na sekta nyingine zilizo chini ya wizara hii, hivyo nawahakikishia kwamba tutashiriki kwa nguvu zote kuifanikisha AFCON 2027," amesema Dkt. Nsekela.

Mbali na ahadi hiyo, Dkt. Nsekela ameipongeza Wizara kwa namna ilivyojipanga katika kutoa huduma na elimu kwa wananchi kupitia maonesho hayo, akieleza kuwa ushiriki wa taasisi zote chini ya wizara hiyo umeongeza ufanisi wa utoaji huduma.

"Hii ni wizara inayogusa sekta nyingi muhimu. Mmefanya vizuri kushiriki maonesho haya pamoja na taasisi zenu zote ili mwananchi anapohitaji msaada asikwame, bali apate suluhisho kwa haraka na urahisi," ameongeza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu wa Wizara hiyo, Bi. Savera Salvatory, ameishukuru Benki ya CRDB kwa ahadi ya ushirikiano na kuipongeza kwa mchango wake katika maendeleo ya sekta ya michezo na maeneo mengine ya kijamii.

Bi. Savera amesema wizara itaendelea kuboresha huduma zake kwa wananchi na kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha sekta zilizo chini yake zinapiga hatua zaidi.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026.
Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments




Dodoma
Tume ya Madini imeendelea kuimarisha ukaguzi wa migodi nchini kupitia Kurugenzi ya Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kwa lengo la kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinafanyika kwa usalama, ufanisi na kwa kuzingatia uhifadhi wa mazingira, hatua inayolenga kuhakikisha rasilimali za madini zinanufaisha kizazi cha sasa na kijacho.

Akizungumza Juni 19, 2026, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, Afisa Mkaguzi wa Migodi wa Tume ya Madini, Rose Mika, amesema ukaguzi wa mara kwa mara unaofanyika katika migodi mikubwa, ya kati na midogo unalenga kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinaendeshwa kwa kuzingatia Sheria ya Madini pamoja na Kanuni za Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira za mwaka 2010.

Amesema ukaguzi huo husaidia kubaini mapema changamoto zinazoweza kuhatarisha usalama wa wafanyakazi na wananchi wanaoishi jirani na maeneo ya migodi, hivyo kuwezesha hatua stahiki kuchukuliwa kabla ya kutokea kwa madhara.

Rose amesema Tume ya Madini pia inaendelea kusimamia utekelezaji wa mipango ya usimamizi wa mazingira, ikiwemo kudhibiti uchafuzi wa maji, hewa na ardhi pamoja na kuhakikisha taka zinazotokana na shughuli za uchimbaji zinahifadhiwa na kushughulikiwa kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa.

Aidha, amesema Tume inafuatilia utekelezaji wa mipango ya kufunga migodi (Mine Closure Plans) ili kuhakikisha maeneo yaliyokwishafanyiwa uchimbaji yanarejeshwa katika hali salama na yenye tija baada ya shughuli hizo kukamilika.

Kwa mujibu wa Rose, hatua hiyo ni muhimu katika kuhakikisha ukuaji wa sekta ya madini unaenda sambamba na uhifadhi wa mazingira na ustawi wa jamii zinazozunguka maeneo ya migodi.

Mbali na ukaguzi wa migodi, Tume ya Madini inaendelea kusimamia matumizi ya baruti katika shughuli za uchimbaji, ikiwemo utengenezaji, uingizaji, usafirishaji na biashara yake kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizopo.

Katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, Tume ya Madini inaendelea kutoa elimu kwa wananchi na wadau kuhusu fursa mbalimbali zilizopo katika sekta hiyo na kuwahamasisha kushiriki katika shughuli za utafiti, uchimbaji, uchenjuaji, biashara ya madini pamoja na utoaji wa huduma kwenye migodi ya madini kwa kuzingatia matakwa ya sheria, ili kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo