Nafasi Ya Matangazo

June 02, 2026






Na mwandishi wetu, Morogoro
SERIKALI imeendelea kuimarisha mifumo ya uratibu, kujiandaa na kukabiliana na maafa ili kuhakikisha misaada ya kibinadamu inayotolewa inawafikia walengwa kwa wakati, ufanisi na kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.

Hayo yameelezwa leo tarehe 02 Juni, 2026 na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Kanali Selestine Masalamado, wakati wa ufunguzi wa warsha ya zoezi la uigaji la uratibu wa utoaji wa misaada ya kibinadamu na usafirishaji wakati wa dharura, mkoani Morogoro.

Amesema utoaji wa misaada ya kibinadamu na usafirishaji wa dharura ni nguzo muhimu zinazowezesha kuokoa maisha ya wananchi walioathiriwa na maafa, kupunguza mateso ya waathirika na kuharakisha urejeshaji wa hali za kawaida katika maeneo yaliyoathirika.

“Kwa kutambua umuhimu huo, Serikali imeendelea kuimarisha mifumo ya uratibu, kujiandaa na kukabiliana na maafa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuhakikisha misaada inawafikia walengwa kwa wakati, ufanisi na kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya utoaji wa huduma za kibinadamu,” amesema.

Vilevile, amelishukuru Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), washirika wote waliohusika katika utekelezaji wa Mradi wa Field-Based Preparedness Project (FBPP), ambapo katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, mradi huo umechangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha uwezo wa taifa katika sekta ya utoaji wa misaada ya kibinadamu na usafirishaji.

Amesema Tanzania imefanikiwa kuanzisha Kikosi Kazi cha Kitaifa cha Uratibu wa utoaji wa misaada ya kibinadamu na usafirishaji wa dharura mwezi Julai 2025, ambacho kimekuwa jukwaa muhimu la uratibu na ushirikiano baina ya taasisi za serikali na wadau wa kibinadamu.

“Zoezi hili la uigaji limeandaliwa kama jukwaa la kitaifa la kujifunza, kupima na kuboresha mifumo yetu ya uratibu wa shughuli za usafirishaji na utoaji wa misaada ya kibinadamu.”alieleza 

Katika hatua nyingine, Kanali Masalamado amesisitiza umuhimu wa kuendelea kujumuisha masuala ya uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa tabianchi katika mipango na shughuli za usafirishaji wa misaada ya kibinadamu ili kuhakikisha kuwa hatua tunazochukua leo hazisababishi changamoto mpya kwa vizazi vijavyo.

Naye Naibu Mkurugenzi wa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) Bi. Christine Mendese amesema, Shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali katika kukabiliana na changamoto za maafa kwa kutoa misaada ya kibinadamu ili kuwa na jamii stahimilivu dhidi ya majanga hususan katika  kuzuia na kukabiliana na majanga mbalimbali.
Kwa upande wake Mratibu wa Maafa mkoa wa Pwani Bi.Roseline ameshukuru uwepo wa warsha hiyo itakayosaidia kuongeza uelewa katika masuala la utoaji wa misaada ya kibinadamu kwa waathirika wa maafa.
“Warsha hii imekuja wakati sahihi kwa kuzingatia mikoa ndiyo inaratibu masuala ya maafa kwa ngazi za Halmashauri zetu, tunashukuru kwa niaba ya ofisi ya mkoa kwa namna wadau mlivyoleta warsha hii na kutujengea uwezo, hii itaongeza tija katika masuala ya logistics wakati wa maafa na kusaidia kuwa na mwelekeo sahihi na kuepuka  changamoto wakati wa kutekeleza majukumu ya logistics wakati wa maafa,” alisema Kimaro.
Posted by MROKI On Tuesday, June 02, 2026 No comments

June 01, 2026

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Wadau wa sekta ya habari nchini wamesema mfumo wa ithibati ya Waandishi wa Habari umechangia kurejesha heshima, uwajibikaji na weledi katika taaluma ya habari, huku ukisaidia kuweka utaratibu unaotambua umuhimu wa elimu, maadili na viwango vya kitaaluma katika utekelezaji wa majukumu ya kihabari.

Wakizungumza katika mahojiano tofauti, jijini Dar es Salaam wadau hao wameeleza kuwa hatua zinazochukuliwa na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) katika kusimamia ithibati wa Waandishi wa Habari zimeongeza uelewa kuhusu umuhimu wa taaluma hiyo na kuhamasisha uzingatiaji wa maadili na viwango vya kitaaluma.

Mwandishi wa Habari wa AYO TV, Bakari Chijumba, amesema mfumo wa ithibati umeongeza heshima ya taaluma ya habari na kusaidia kupunguza changamoto zilizokuwa zikijitokeza kutokana na baadhi ya watu kufanya kazi za habari bila kuwa na taaluma husika.

“Kwa muda mrefu kulikuwa na watu waliokuwa wakifanya kazi za uandishi wa habari bila kuwa na taaluma husika. Wakati mwingine hali hiyo ilisababisha upotoshaji wa taarifa na ukiukwaji wa maadili ya taaluma. Uwepo wa ithibati umeweka utaratibu unaosaidia kuhakikisha wanaofanya kazi hii wanazingatia viwango vya kitaaluma,” amesema Chijumba.

Kwa upande wake, Mtangazaji wa TBC1, Alice Shayo, amesema uhuru wa vyombo vya habari unapaswa kwenda sambamba na uwajibikaji na uzingatiaji wa maadili ya taaluma.

“Uhuru wa vyombo vya habari una mipaka yake. Mwandishi wa habari anapaswa kufahamu namna ya kukusanya, kuchakata na kusambaza taarifa kwa kuzingatia maadili na miongozo ya taaluma,” amesema Shayo.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Torch Media, James Salvatory, amesema mfumo wa ithibati umechangia kurejesha heshima ya taaluma ya habari kwa kuweka bayana kuwa uandishi wa habari ni taaluma inayohitaji elimu, ujuzi na weledi kama zilivyo taaluma nyingine.

“Ithibati imeongeza hamasa kwa wataalamu wa habari na kuonesha wazi umuhimu wa taaluma hii katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla,” amesema Salvatory.
Kwa upande wake, Afisa Habari Mkuu, Neema Mbuja, amesema taaluma ya habari inahitaji elimu, ujuzi na kuongozwa na kanuni na maadili maalumu ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora ya habari.

“Mara nyingi baadhi ya watu walikuwa wakidhani kuwa kujua kusoma na kuandika pekee kunatosha kuwa mwandishi wa habari, jambo ambalo si sahihi. Taaluma ya habari ina misingi, maadili na miongozo inayopaswa kufuatwa ili kuhakikisha huduma bora ya habari inatolewa kwa wananchi,” amesema Mbuja.

Wadau hao wameeleza kuwa kuendelea kuimarishwa kwa mfumo wa ithibati kutasaidia kukuza uaminifu wa umma kwa vyombo vya habari, kuimarisha uwajibikaji wa waandishi na kuongeza hadhi ya taaluma ya habari nchini.
Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, amewasili leo nchini Ufaransa kwa ziara ya kikazi ya kushiriki na kuongoza vikao vya Bodi ya Global Partnership for Education (GPE), taasisi ya kimataifa inayojihusisha na maendeleo ya elimu duniani, ambako anahudumu kama Mwenyekiti wa Bodi.

Mhe. Kikwete alipokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Charles de Gaulle na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe. Saidi Othman Yakubu, pamoja na watumishi wa Ubalozi wa Tanzania nchini humo.

Katika nafasi yake kama Mwenyekiti wa Bodi ya GPE, Mhe. Kikwete anaongoza juhudi za kimataifa zinazolenga kuimarisha upatikanaji wa elimu bora, jumuishi na yenye usawa kwa watoto katika nchi zinazoendelea. GPE ni ushirikiano wa kimataifa unaozileta pamoja serikali, mashirika ya maendeleo, sekta binafsi, asasi za kiraia na wadau wengine wa elimu ili kusaidia nchi zenye kipato cha chini na cha kati kuboresha mifumo yao ya elimu.

Kupitia ushirikiano huo, GPE hutoa msaada wa kifedha na kiufundi kwa nchi washirika ili kuongeza upatikanaji wa elimu ya msingi na sekondari, kuboresha ubora wa ufundishaji na ujifunzaji, kuimarisha usawa wa kijinsia katika elimu, pamoja na kuhakikisha watoto walio katika mazingira magumu wanapata fursa ya elimu.

Uongozi wa Mhe. Kikwete katika GPE umeendelea kuimarisha mchango wa Afrika na nchi zinazoendelea katika mijadala ya kimataifa kuhusu elimu, huku ukisisitiza umuhimu wa elimu kama nyenzo muhimu ya maendeleo endelevu na ustawi wa jamii.

Wakati wa ziara yake nchini Ufaransa, Mhe. Kikwete anatarajiwa kuongoza vikao mbalimbali vya Bodi ya GPE pamoja na kushiriki majadiliano ya kimkakati kuhusu mustakabali wa elimu duniani.
Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments

 

Ofisi ya Rais – TAMISEMI imetangaza rasmi uchaguzi wa wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na Kidato cha Tano pamoja na Vyuo vya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa mwaka 2026.

👉 BOFYA HAPA KUONA ORODHA YA WANAFUNZI 

Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa akizindua  maonesho ya mazingira katika Viwanja vya Jakaya Kikwete jijini Dodoma ambayo ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake ni Juni 05, 2026
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa akikagua mabanda ya maonesho katika Viwanja vya Jakaya Kikwete jijini Dodoma ambayo ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake ni Juni 05, 2026
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa akikagua mabanda ya maonesho katika Viwanja vya Jakaya Kikwete jijini Dodoma ambayo ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake ni Juni 05, 2026
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa Juni mosi, 2026 akiwasili katika Viwanja vya Jakaya Kikwete jijini Dodoma kufungua maonesho ya mazingira ambayo ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake ni Juni 05, 2026. Anayempokea ni Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Balozi Baraka Luvanda.
Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments




Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe (Mb) amekutana na Balozi wa Australia nchini Tanzania anayemaliza muda wake, Mhe. Jenny Da Rin kwa madhumuni ya kumuaga. 

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam, tarehe 1 Juni, 2026, Mhe. Dkt. Maghembe alimpongeza Balozi Jenny kwa kumaliza muda wake wa uwakilishi nchini kwa mafanikio na kwa mchango wake mkubwa katika kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Australia.

Kwa upande wake, Balozi Jenny Da Rin aliishukuru Serikali kwa ushirikiano iliyompatia na kusisitiza umuhimu wa Watanzania kutumia fursa za elimu na semina zinazotolewa na Australia, akieleza kuwa maarifa na ujuzi unaopatikana kupitia programu hizo zinachangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya Tanzania, hususan katika sekta ya madini.

Aidha, Balozi Jenny aliihakikishia Serikali ya Tanzania kuwa Serikali ya Australia itaendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta ya kilimo, ikiwemo tafiti, usimamizi wa rasilimali maji, kuongeza uzalishaji wa mazao na utekelezaji wa programu mbalimbali za maendeleo ya kilimo.
 
Vile vile, alielezea dhamira yake ya kuendeleza kuhamasisha wawekezaji na wafanyabiashara wa Australia kuja kuwekeza nchini, huku akisisitiza umuhimu wa kutafuta suluhisho la baadhi ya changamoto zinazowakabili wawekezaji kwa manufaa ya nchi zote mbili.
Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu
Waandishi wa Habari watakaoshiriki Tuzo za Uandishi wa Habari na Makala za Maendeleo (Samia Kalamu Awards - SKA) 2026 wamelazimika kukidhi sharti la kuwa na ithibati kutoka Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), hatua inayolenga kuimarisha weledi, uwajibikaji na ushindani wa haki katika taaluma hiyo.

Akizindua rasmi mchakato wa kupokea kazi za kushindanishwa, Jumapili Tarehe 31 Mei, 2026, jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa SKA, Mha. Peter Mwasalyanda, amesema maandalizi ya mwaka huu yanazingatia maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kutambua mchango wa Waandishi wa Habari za maendeleo nchini.
Mwasalyanda amesema ili kuhakikisha uadilifu, uwazi na ushindani wa haki, maandalizi ya tuzo hizo yanahusisha pia Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kama mdau muhimu katika kusimamia weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari.

“Tuzo hizi zinalenga kutambua, kuthamini na kuhamasisha uzalishaji wa maudhui ya ndani yenye ubora, yanayochangia kuelimisha, kuhabarisha na kuburudisha, na kuimarisha taswira chanya ya Taifa kupitia habari za maendeleo,” amesema.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema tofauti na msimu wa kwanza wa tuzo hizo, mwaka huu washiriki wanapaswa kuhakikisha wamekidhi sharti la ithibati.

“Mtakumbuka Msimu wa kwanza wa Samia Kalamu mambo ya JAB hayakuwepo, kwa hiyo waandishi walishiriki wote bila kujali vigezo vya Ithibati lakini mwaka huu kuna hiki kigezo cha kuwa na ithibati kwa hiyo niwashauri basi wote wanaoshiriki kwenye hizi tuzo wahakikishe wanakuwa na ithibati, wamethibitishwa na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari.” Amesema Wakili Kipangula na kuongeza;
“Ni muhimu sana kwa sababu ni takwa la kisheria na kitu ambacho hatuwezi kukikwepa. Nawahamasisha tushiriki wote kwa sababu isionekane ni tuzo za watu fulani tu, kila mmoja awasilishe kazi zake,” amesema Kipangula.

Kwa mujibu wa vigezo vya ushiriki vilivyotangazwa, Waandishi wa Habari wa Tanzania Bara wanatakiwa kuwa wamethibitishwa na JAB, huku kwa Zanzibar washiriki wakitakiwa kuwa na kitambulisho cha Mwandishi wa Habari (Press Card).

Tuzo hizo zimeanza kupokea kazi kuanzia Mei 31 hadi Juni 30, 2026 na zinatarajiwa kutolewa kati ya Oktoba na Desemba mwaka huu.

Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments
Wananchi wa Kijiji cha Mkungugu jimbo la Ismani katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa wakiwa katika foleni ya kupiga kura ya kumchagua Mbunge wao katuika uchaguzi mdogo uliyofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwananchi Mkazi wa wa Kijiji cha Kihongorota katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa, Angelista Mwenda akipiga kura katika uchaguzi mdogo wa Ubunge jimbo la Ismani uliofanyika leo Juni 01, 2026.  
Mwananchi Mkazi wa wa Kijiji cha Kihongorota katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa, Angelista Mwenda akipiga kura katika uchaguzi mdogo wa Ubunge jimbo la Ismani uliofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akipita kuingia katika kituo cha Kura cha Ofisi ya Kijiji Mtera katika jimbo la Ismani Wilaya ya Iringa mkoani Iringa kukagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Ismani lililofanyika leo Juni 01, 2026. 
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akizungumza na Mawakala katika moja ya vituo alivyotembelea.
MWENYEKITI wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele amesema zoezi la upigaji Kura wa Ubunge katika jimbo la Isman  katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara limekwenda vizuri.
 
Mwenyekiti huyo wa Tume Jaji Mwambegele amesema hayo leo Juni 01,2026 akiwa katika ofisi za Kijiji Igingilanyi Wilayani Iringa mara baada ya kutembelea na kukagua zoezi la upigaji Kura linavyoendelea katika vituo vya kupigia Kura vya jimbo la Isimani ambako kunafanyika uchaguzi mdogo wa ubunge.
 
Amesema mwitikio wa wananchi wa Ismani katika kujitokeza kupiga kura umekua mkubwa na hata katika Kata nyingine 12 ambazo nazo zinachagua Madiwani hii leo wamejitokeza kwa Wingi.
 
Mwenyekiti huyo wa Tume Jaji Mwambegele ameshudia upigaji kura kwa baadhi yavituo vilivyopo katika vijiji vya   Igingilanyi, Mkungugu, Kihongorota na Migori.
 
Kata 12 zilofanya uchaguzi leo ni Mzimuni iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Halmashauri ya Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji Kasulu.
 
Nyingine ni Kata ya Kala iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akikagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Iringa mkoani Iringa hii leo Juni 01,2026. 

Wananchi wakiwa katika mistari tayari kuingia vituoni kupiga Kura. 

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akikagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Iringa mkoani Iringa hii leo Juni 01,2026. 

Wananchi wakiwa katika mistari tayari kuingia vituoni kupiga Kura. 

Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe 


Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema jumla ya wanafunzi 246,197 wakiwemo wasichana 114,102 na wavulana 132,095 waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano mwaka 2026 wanatakiwa kuripoti shuleni kuanzia Julai 04, 2026 hadi Julai 31, 2026 kwakuwa muhula wa kwanza wa masomo utaanza Julai 06, 2026. 

Prof. Shemdoe amesema hayo leo Juni 01, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi Ndogo ya Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Magogoni Jijini Dar es Salaam, wakati akitoa taarifa kwa umma kuhusu wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya elimu ya ufundi kwa mwaka 2026.

“Wanafunzi 172,114 sawa na asilimia 69.9 wakiwemo wasichana 85,987 na wavulana 86,127 wenye sifa wamechaguliwa kujiunga na kidato cha tano katika shule  za sekondari za Serikali 856 zikiwemo shule za bweni 825, kutwa 25 na kutwa na bweni sita (06),” amefafanua Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amesema jumla ya wanafunzi 74,083 sawa na asilimia 30.1  wakiwemo wasichana 28,115 na wavulana 45,968 wamechaguliwa kujiunga na vyuo vya Ufundi.

“Wanafunzi 3,144 wakiwemo wasichana 1,170 na wavulana 1,974 wamechaguliwa kujiunga na fani mbalimbali katika vyuo 04 vya elimu ya ufundi, vyuo hivyo ni Chuo cha Ufundi cha Arusha (ATC), Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT), Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST) na Chuo cha Maendeleo ya Maji (WMDI),” ameeleza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amesisitiza kwamba, uchaguzi wa wanafunzi wa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya elimu ya ufundi umefanyika kwa kuzingatia ufaulu na nafasi zilizopo katika shule; hivyo, hakutakuwa na fursa ya kufanya mabadiliko yoyote ya Shule kutokana na ukosefu wa nafasi.  

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi zilizotumika kujenga miundombinu bora ya shule za kidato cha tano na vyuo vya kati ambayo itatumika kuwahudumia wanafunzi 246,197 waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya elimu ya ufundi mwaka 2026.
Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments

May 31, 2026






Mpwapwa
Mkoa wa Dodoma leo umepokea Mwenge wa Uhuru 2026 katika Uwanja wa Shule ya Msingi Mtera iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa, ukitokea Mkoa wa Iringa.

Akizungumza katika hafla ya mapokezi hayo, Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma, Dkt. Khatibu Kazungu, amesema Mwenge wa Uhuru utakimbizwa umbali wa kilomita 1,595.3 katika wilaya zote saba (7) na halmashauri nane (8) za Mkoa wa Dodoma, ambapo utapitia, kuzindua, kuweka mawe ya msingi na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo yenye thamani ya jumla ya Shilingi 23,243,056,418.58.

Dkt. Kazungu alipokea Mwenge huo kutoka kwa Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Bi. Doris Kalasa, na kueleza kuwa Mkoa wa Dodoma una miradi mikubwa ya kimkakati itakayopitiwa na Mwenge wa Uhuru mwaka huu.

Amesema mafanikio hayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ameendelea kuuletea Mkoa wa Dodoma fedha nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali.

“Tunamshukuru na kumpongeza Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuupatia Mkoa wa Dodoma rasilimali za kutosha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Miradi hii ya kimkakati imeendelea kuufungua Mkoa wa Dodoma kiuchumi, kuimarisha huduma za kijamii na kuufanya kuwa kivutio muhimu kwa uwekezaji na utalii,” amesema Dkt. Kazungu.

Aidha, ameeleza kuwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma wanathamini mchango wa Mwenge wa Uhuru katika kuhamasisha umoja, mshikamano na uzalendo miongoni mwa Watanzania.

“Katika mazingira ya amani na umoja wa kitaifa, Taifa letu linaendelea kustawi, kuvutia wawekezaji na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Hakuna Taifa linaloweza kufanikiwa kiuchumi bila kuwepo kwa amani na mshikamano wa Wananchi wake,” alisisitiza.

Dkt. Kazungu ameongeza kuwa wananchi pamoja na viongozi wa Mkoa wa Dodoma wameendelea kuzingatia na kutekeleza ujumbe wa kudumu wa Mwenge wa Uhuru unaohimiza uzalendo, uwajibikaji na ushiriki wa wananchi katika maendeleo ya Taifa, sambamba na kaulimbiu ya mwaka huu isemayo:

“Tanzania ni yetu sote, tushikamane kwa pamoja kuleta maendeleo.” 
Posted by MROKI On Sunday, May 31, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo