Nafasi Ya Matangazo

May 21, 2026


Njombe
Mkoa wa Njombe unatarajiwa kuwa kitovu kipya cha uchumi wa madini nchini kufuatia uwekezaji mkubwa katika miradi ya uchimbaji na uchakataji wa madini ya chuma inayolenga kufungua maelfu ya ajira, kukuza biashara za ndani na kuongeza mapato kwa wananchi wa Wilaya ya Ludewa.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Mhandisi Lucas Mlekwa, amesema tayari moja ya miradi mikubwa inayosimamiwa na Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) kwa kushirikiana na kampuni ya kigeni imepata Leseni Kubwa ya Uchimbaji wa Madini baada ya utafiti wa kina uliofanyika kati ya mwaka 2012 na 2013 kubaini uwepo wa zaidi ya tani milioni 126 za madini ya chuma.

Amesema tafiti hizo pia zimeonesha uwepo wa madini mengine yenye thamani kubwa yanayoambatana na chuma ikiwemo titanium na vanadium, hatua inayoongeza thamani ya kiuchumi ya mradi huo kwa Taifa.

“Kwa sasa tupo katika hatua za mwisho za kukamilisha makubaliano kati ya Serikali na wawekezaji, na tunatarajia ndani ya mwaka mmoja utekelezaji rasmi wa mradi utaanza,” amesema Mlekwa.

Kwa mujibu wa Mlekwa, mradi huo utahusisha shughuli kuu mbili ambazo ni uchimbaji wa madini pamoja na ujenzi wa kiwanda cha kisasa cha kuchakata chuma kitakachozalisha bidhaa mbalimbali zitakazotumika katika sekta ya ujenzi na viwanda nchini.

Ameeleza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo utaongeza ushiriki wa wazawa kupitia utekelezaji wa sera ya  Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini, ambapo wananchi watanufaika na fursa za ajira na biashara zikiwemo huduma za ulinzi, usafirishaji, ugavi wa vifaa vya ujenzi, huduma za migodini pamoja na shughuli nyingine za kiuchumi zinazozunguka miradi hiyo.

Aidha, amesema mradi wa chuma wa Maganga Matitu unaosimamiwa pia na NDC kwa ubia na kampuni ya kigeni umefikia hatua za mwisho za maandalizi baada ya mwekezaji kulipa zaidi ya Shilingi bilioni 4.2 kama fidia kwa wananchi waliopisha eneo la mradi huo, ambao una akiba inayokadiriwa kufikia tani milioni 45 za madini ya chuma.

Mlekwa ameongeza kuwa pamoja na miradi hiyo, Wilaya ya Ludewa itanufaika na utekelezaji wa mradi wa  Mchuchuma   wenye zaidi ya tani milioni 428 za makaa ya mawe kwa ajili ya uzalishaji wa umeme, unaotarajiwa kuimarisha upatikanaji wa nishati kwa shughuli za uchimbaji na viwanda vya chuma vitakavyojengwa wilayani Ludewa.

Amesema maendeleo hayo yataifanya Njombe kuwa miongoni mwa maeneo muhimu zaidi nchini katika sekta za madini, viwanda na nishati, huku yakitarajiwa kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa Taifa na maendeleo ya wananchi wa eneo hilo.
Posted by MROKI On Thursday, May 21, 2026 No comments
Mzee Peter Morisi Shirima akitia saini Hati ya Haki Miliki ya Kimila ya eneo alilofidiwa baada ya timu ya wataalamu kutoka iliyotumwa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba  kumaliza kwa njia ya maridhiano mgogoro wa ardhi  uliodumu kwa miaka 51 kati ya  Mzee huyo na Kanisa Katoliki Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, Mei 19, 2026. Wengine  kutoka kushoto ni Mkewe Juliana Anatoli, Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Rombo, Charles Daudi Mganga, Msaidizi wa Waziri Mkuu - Ardhi, Senso Magesa, Msaidizi wa Waziri Mkuu, Mahusiano, Asasi za Kiraia na Mashirika yasiyo ya  Kiserikali, Tryphone Mkorokoti na kulia ni Kamishina Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Kilimanjaro, Rehema Mdeedee. Tukio hilo lilifanyika kwenye ofisi ya kijiji cha Msaranga, Rombo. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Padri Amedeus Mtui, Wakili wa Askofu Rombo, Jimbo Katoliki Moshi akitia saini Hati ya Haki Miliki ya Kimila ya eneo la Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo baada ya timu ya wataalamu iliyotumwa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba kumaliza kwa njia ya maridhiano mgogoro  wa ardhi uliodumu kwa miaka 51 kati ya  Mzee Peter Morisi Shirima na Kanisa Katoliki Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, Mei 19, 2026. Wengine kutoka kushoto ni Paroko Parokia ya Mtimhoo, Padri Benedict Mwacha, Mke wa Mzee Peter,  Juliana Anatoli, Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Rombo, Charles Daudi Mganga, Msaidizi wa Waziri Mkuu - Ardhi, Senso Magesa, Msaidizi wa Waziri Mkuu, Uhusiano wa rami na Taasisi za Dini i, Tryphone Mkorokoti na kulia ni Kamishina Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Kilimanjaro, Rehema Mdee.Tukio hilo lilifanyika  katika Ofisi ya kijiji cha Msaranga wilayani Rombo.
Mzee Peter Morisi Shrima akipokea kutoka kwa Msaidizi wa Waziri Mkuu- Ardhi, Senso Magesa, Hati ya Haki Miliki ya Kimila  ya eneo alilofidiwa baada ya timu ya wataalamu iliyotumwa na Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kumaliza kwa njia ya maridhiano mgogoro  wa ardhiuliodumu kwa miaka 51 kati ya  Mzee huyo na Kanisa Katoliki Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, Mei 19, 2026.  Wengine kutoka kushoto ni Diwani wa Kata ya Kisale Msaranga, Aloyce Assenga, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilay ya Rombo, Charle Daudi Mganga na kulia ni Mwenyekiti wa Kijiji cha Msaranga, Fratei Shirima. Tukio hilo lilifanyika  katika Ofisi ya kijiji cha Msaranga wilayani Rombo.
Paroko wa Parokia ya Mtimhoo ya Jimbo Katoliki la Moshi wilayani Rombo, Padri Benedict Mwacha (kushoto) na WaKili wa Askofu Rombo, Jimbo Katoliki Moshi, Pandri  Amedeus Mtui wakipokea  kutoka kwa Msaidizi wa Waziri Mkuu - Ardhi, Senso Magesa, Hati ya Haki Miliki ya Kimila  ya eneo la Parokia hiyo baada ya timu ya wataalamu iliyotumwa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba  kumaliza kwa njia ya maridhiano mgogoro  wa ardhi uliodumu kwa miaka 51 kati ya  Mzee Peter Morisi Shirima na Kanisa Katoliki Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, Mei 19, 2026.  Wa pili kulia ni Diwani wa Kata ya  Kisale Msaranga, Aloyce Assenga. Tukio hilo lilifanyika  katika Ofisi ya kijiji cha Msaranga wilayani Rombo.
Mzee Peter Morisi Shirima   na Paroko wa Parokia ya Mtimhoo wa Jimbo Katoliki la Moshi, Padri Benedict Mwacha wakifurahia baada ya timu ya wataalamu iliyotumwa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba  kumaliza kwa njia ya maridhiano mğogoro wa ardhi  uliodumu kwa miaka 51 kati ya Mzee Peter Morisi Shirima na Parokia hiyo, kwenye Ofisi ya kijiji cha Msaranga wilayani Rombo,  Mei 19, 2026.
******************
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba ametatua mgogoro wa ardhi kati ya Parokia ya Mtimhoo ya Kanisa Katoliki Jimbo la Moshi na Mzee Peter Morisi wa Kijiji cha Msaranga, Wilaya ya Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, uliodumu kwa kipindi cha miaka 51.
 
Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokea malalamiko ya Mzee Peter Morisi alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Halmashauri ya Wilaya ya Rombo wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Kilimanjaro tarehe 17 Februari 2026 ambapo aliahidi kuwa Serikali ingetuma wataalamu wilayani humo kwa ajili ya kuchunguza na kutatua mgogoro huo.
 
Kufuatia maelekezo hayo, Waziri Mkuu alituma timu ya wataalamu kutoka Ofisi yake ambao walifika mkoani Kilimanjaro na kushirikiana na viongozi wa Mkoa pamoja na viongozi wa Kijiji cha Msaranga kutembelea eneo la mgogoro. Aidha, timu hiyo ilifanya vikao na familia iliyokuwa katika mgogoro, viongozi wa kijiji, viongozi wa Parokia ya Mtimhoo pamoja na viongozi wa Jimbo Katoliki la Moshi ambapo pande zote zilikubaliana kuwa maridhiano ndiyo njia sahihi ya kumaliza mgogoro huo.
 
Katika madai yake, Mzee Peter Morisi alieleza kuwa eneo lake lilichukuliwa kwa nguvu na Kanisa Katoliki na kwamba fidia aliyolipwa ilikuwa ndogo ikilinganishwa na ukubwa wa eneo lililotwaliwa. Kutokana na kutopata suluhisho kwa muda mrefu, aliamua kuwasilisha malalamiko yake kwa Waziri Mkuu wakati wa mkutano wa hadhara.
 
Timu ya wataalamu ilipitia nyaraka zote zilizowasilishwa na pande husika na kubaini kuwa Mzee Peter Morisi alipokea fidia ya shilingi 3,935.50 tarehe 16 Aprili 1980. Aidha, alipewa eneo jingine katika Kitongoji cha Kirachi, Kijiji cha Msaranga ili kupisha ujenzi wa shule na kanisa katika eneo lake la awali.
 
Katika hatua nyingine, timu hiyo ilikutana na Askofu wa Jimbo Katoliki la Moshi, Askofu Ludovick Minde ambaye alisisitiza kuwa Kanisa Katoliki lina utamaduni wa kutatua migogoro kwa njia ya maridhiano na kuwataka wahusika kuendelea na mazungumzo ya amani.
 
Askofu Minde alitoa shilingi milioni tano kama kifuta machozi kwa madhara ambayo Mzee Peter Morisi na familia yake wameyapitia katika kipindi chote cha kutafuta suluhisho la mgogoro huo. Aidha, alisema Kanisa halina kinyongo na mlalamikaji na litaendelea kushirikiana naye wakati wote.
 
Vilevile, Askofu Minde alimshukuru Waziri Mkuu kwa kutuma timu ya wataalamu kutoka Ofisini kwake na kumtakia heri katika utekelezaji wa majukumu yake ya uongozi.
 
Kwa upande wake, Mheshimiwa Waziri Mkuu naye alitoa shilingi milioni tano na kufanya jumla ya fedha zilizotolewa kwa Mzee Peter Morisi kuwa shilingi milioni kumi kwa lengo la kujenga maridhiano na kuimarisha mshikamano katika jamii.
 
Baada ya kufikiwa kwa maridhiano hayo, pande zote zilitia saini nyaraka za makubaliano zikikiri kuwa mgogoro huo umemalizika kwa njia ya maridhiano na kuahidi kusameheana pamoja na kuendelea kuishi kwa amani. Kila upande pia ulikabidhiwa Hati za Hatimiliki za Kimila kwa maeneo husika.
 
Akizungumza baada ya kukabidhiwa hati hizo na kusaini nyaraka za maridhiano, Mzee Peter Morisi aliishukuru Serikali kwa kumaliza mgogoro huo uliodumu kwa muda mrefu na kuahidi kushirikiana na Kanisa pamoja na wanakijiji wenzake bila kinyongo.
 
Naye Diwani wa Kata ya Kisale Msaranga, Mhandisi Mathias Assenga alisema mgogoro huo uliathiri mshikamano wa wananchi pamoja na uhuru wa kuabudu kwa kuwa ulihusisha eneo la kanisa linalotumiwa na waumini kwa ibada na shughuli nyingine za kidini.
 
Kwa upande wake, Padri Amadeus Mtui ambaye ni Wakili wa Baba Askofu wa Jimbo Katoliki la Moshi alimshukuru Waziri Mkuu kwa kutuma timu ya wataalamu ambayo imekuwa chachu ya kumalizika kwa mgogoro huo.
 
Baadhi ya viongozi walioshiriki katika mchakato wa maridhiano hayo ni pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Rombo, Charles Daudi Mganga, Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Kilimanjaro, Rehema Mdee pamoja na Diwani wa Kata ya Kisale Msaranga, Mhandisi Mathias Assenga.

Mzee wa Kijiji cha Msaranga, Andrea Peter Mkenda alisema kumalizika kwa mgogoro huo kutaleta amani, utulivu na kuimarisha mshikamano miongoni mwa wananchi hali itakayowapa nafasi nzuri ya kuendelea na shughuli zao za maendeleo.
Posted by MROKI On Thursday, May 21, 2026 No comments

May 20, 2026










MKuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila ametoa ahadi ya milioni 50 kwa Dar City Basket Team endapo itafunzu mtanange huko Rwanda kufikia hatua ya nusu fainali.

RC Chalamila ameyasema hayo leo Mei 20, 2026 katika uwanja wa ndege wa Mwalimu JK Nyerere Terminal 3 wakati akiiaga team hiyo kuelekea Kigali Rwanda kwenye mashindano.

Aidha RC Chalamila ametoa rai kwa wakazi wa Mkoa huo endapo watabaini kuna kijana anakipaji cha basket ball,wamlete ofisini kwake ili aweze kuendelezwa kipaji hicho pamoja na kumuunganisha na wachezaji nguli wa Dar City Basket Ball.

Vilevile RC Chalamila amesema Rais wa team hiyo Ndg Hashimu Thabit akirudi toka Rwanda uandaliwe utaratibu wa kukutana na Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wote wa Mkoa huo kuona namna ya kuwa na uwanja mkubwa wa kisasa wa Basket Ball  katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Kwa upande wa Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe Edward Mpogolo amesema Dar City ni team ya kimataifa na inafanya vizuri ni ya kihistoria toka Tanzania ipate uhuru hivyo anaitakia kila kheri.

Mwisho RC Chalamila amemshukuru Rais Dkt Samia kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya michezo kwa kuwa michezo ni afya lakini pia michezo ni uchumi.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments



Freetown- Sierra Leone
Tanzania imesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa Kikanda katika kuongeza thamani Madini ya Almasi, uwazi katika usimamizi wa rasilimali madini na kuimarisha mchango wa Sekta ya Madini katika maendeleo ya uchumi wa nchi wanachama Zinazozalisha Madini ya Almasi Afrika (ADPA).

Hayo yalibainishwa  Mei 19, 2026   mjini Freetown, Sierra Leone, na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo, ambaye anaongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki  katika Mkutano wa 11 wa Kawaida  wa Kamati ya  Wataalam  wa umoja huo.

Mkutano huo unawakutanisha wataalam kutoka nchi wanachama wa ADPA kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha usimamizi, biashara na maendeleo ya sekta ya almasi barani Afrika.

 Aidha, katika mkutano huo, wajumbe walijadili taarifa ya mwaka ya Mkurugenzi Mtendaji wa ADPA ya mwaka 2025, utekelezaji wa bajeti na taarifa za fedha za mwaka 2025 pamoja na taarifa ya ukaguzi wa nje wa hesabu kwa kipindi cha 2023–2024. Aidha, masuala ya msamaha wa madeni, daftari la hatari, maendeleo ya uwezo wa taasisi na uanachama wa ADPA katika Shirika la Viwango Duniani (ISO) yalipata nafasi ya kujadiliwa kwa lengo la kuimarisha ufanisi wa taasisi hiyo.

Vilevile, mkutano ulipokea taarifa za maendeleo kuhusu maandalizi ya Mkutano wa Almasi na maadhimisho ya miaka 20 ya ADPA, mapitio ya mkakati wa mawasiliano na masoko, utekelezaji wa ukaguzi wa ndani wa miaka 2023–2025 pamoja na mapendekezo ya sera ya usimamizi wa utendaji kazi.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing pamoja na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing pamoja na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing, Ujumbe Maalumu kwenda kwa Rais wa China Mhe. Xi Jinping mara baada ya mazungumzo, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi wa Chama cha Mapinduzi  (CCM) na Serikali kwenye picha na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing pamoja na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments





Kibaha, Pwani 
CCM leo imekuwa mwenyeji wa mkutano kati ya Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) na Vyama Sita Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika uliofanyika katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS), Kibaha.

Mkutano huo chini ya wenyeji wa Chama Cha Mapinduzi, ulikuwa sehemu ya ziara ya kikazi ya Komredi Liu Haixing, Mjumbe wa Kamati Kuu na Waziri wa Idara ya Mambo ya Nje wa CPC kutoka China.

Katika mkutano huo, viongozi wa vyama vya ukombozi kutoka ANC, FRELIMO, MPLA, SWAPO na ZANU-PF walijadiliana na CPC kuhusu kuimarisha mshikamano, kubadilishana uzoefu wa kiuongozi na kusukuma ajenda ya maendeleo ya kisasa kwa ustawi wa wananchi wao.

Viongozi hao pia walishiriki uzinduzi wa Kituo cha Tafiti kuhusu Fikra za Xi Jinping juu ya Ujamaa wenye Maono ya Kichina katika Zama Mpya, hatua inayolenga kuimarisha ushirikiano wa kielimu na maendeleo kati ya CCM na CPC.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments








Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar Dkt. Habiba Hassan Omar, amefanya ziara katika Ofisi za Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) na kukagua maandalizi ya Maonesho ya Jubilei ya Miaka 50 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (Sabasaba). Katika ziara hiyo, Katibu Mkuu alieleza kuridhishwa kwake na hatua zilizofikiwa hadi sasa na kufafanua umuhimu wa ushiriki wa wadau katika maonesho hayo makubwa.

Aidha, Dkt. Habiba alipata nafasi ya kuzungumza na Kamati ya Kitaifa ya Ulinzi na Usalama, ambayo inaratibu masuala ya kiusalama wakati wa kipindi chote cha maonesho. Mazungumzo hayo yalilenga kuhakikisha maandalizi ya Sabasaba yanakwenda sambamba na viwango vya usalama na uratibu wa kitaifa.

Kwa upande wa TanTrade, Mkurugenzi Mkuu Dkt. Latifa M. Khamis alieleza hatua zilizofikiwa katika maandalizi, ikiwemo uandaaji wa maeneo ya maonesho na programu maalum zitakazofanyika wakati wa maonesho ili kuonesha upekee wa Maonesho ya Jubilei ya Miaka 50 tofauti na yaliyopita. Maonesho haya yanatarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 28 Juni hadi 13 Julai 2026 katika Uwanja wa Maonesho wa Mwalimu J.K. Nyerere, Barabara ya Kilwa, Dar es Salaam
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya uteuzi wa Majaji wa Mahakama ya Rufani. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Moses Kusiluka, walioteuliwa kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani ni:-

(i) Mhe. Abdi Shaaban Kagomba – Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania,
        Kanda ya Dodoma;
(ii) Mhe. Yohane Bokobora Masara – Jaji wa Mahakama Kuu ya                         Tanzania, Kanda ya Arusha;
(iii) Mhe. Immaculata Kajetan Banzi – Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu         ya Tanzania, Kanda ya Kagera;
(iv) Mhe. Rabia Hussein Mohamed – Jaji wa Mahakama Kuu ya                         Zanzibar;

(v) Mhe. Cyprian Phocas Mkeha – Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
        Tanzania, Divisheni ya Biashara, Dar es Salaam;
(vi) Mhe. Yose Joseph Mlyambina – Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
        Tanzania, Divisheni ya Kazi, Dar es Salaam;
(vii) Mhe. Imani Daud Aboud – Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania,                 Kanda ya Dodoma;
(viii)Mhe. Mzee Ibrahim Ibrahim – Jaji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar;            na.
(ix) Mhe. Juliana Laurent Masabo – Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu             ya Tanzania, Kanda ya Dodoma.

Aidha, uapisho wa Majaji wateule wa Mahakama ya Rufani utafanyika kwa tarehe itakayopangwa baadaye.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments
KAMPUNI ya mawasiliano ya simu ya Airtel Tanzania na kampuni ya teknolojia ya Huawei zimethibitisha upya dhamira yao ya kuendelea kuimarisha huduma za mawasiliano nchini kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa na ubunifu vilivyojadiliwa katika Kongamano la Huawei Mini Mobile World Congress (Mini MWC).

Kampuni hizo zimesema ushirikiano wao unaendelea kulenga kuharakisha mageuzi ya kidijitali, kupanua huduma za mtandao na kuboresha uzoefu wa wateja kupitia suluhisho za kisasa za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa kongamano hilo lililofanyika Tanzania Mei 12, 2026, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, Charles Kamoto, alisema ushirikiano huo unaendelea kuwa sehemu muhimu katika kusaidia ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.

“Ni furaha kubwa kushiriki nanyi leo tunapojadili mustakabali wa sekta ya mawasiliano, mageuzi ya kidijitali na fursa zinazoendelea kujitokeza ndani ya soko letu na ukanda mzima,” alisema.

Mkutano huo uliwakutanisha viongozi na wataalamu wa kiufundi kutoka kampuni zote mbili kujadili teknolojia za baadaye zinazolenga kuboresha utoaji wa huduma na kuimarisha miundombinu ya mawasiliano nchini Tanzania.

Miongoni mwa maeneo ya kimkakati yaliyojadiliwa ni pamoja na ukuaji wa huduma za intaneti ya simu na majumbani, matumizi ya mitandao msingi inayotumia Akili Unde (AI), maendeleo ya teknolojia ya microwave pamoja na mifumo ya kisasa ya usafirishaji wa taarifa kwa njia ya kidijitali.

Kupitia ushirikiano huo, Airtel Tanzania na Huawei pia walijadili matumizi ya teknolojia za kisasa za wireless na AI zinazolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za mtandao, kuboresha uthabiti wa huduma, kuongeza uzoefu wa wateja na kupunguza matumizi ya nishati katika mifumo ya mawasiliano.

Kamoto alisema matumizi ya teknolojia za kizazi kijacho yataongeza matumizi ya data, kusaidia ukuaji endelevu wa biashara na kuiweka Airtel katika nafasi ya kuwa kampuni kinara wa mawasiliano ya kidijitali nchini.

“Tunaendelea kuwa na malengo makubwa na dhamira thabiti katika kusukuma mbele dira ya Airtel kupitia ubunifu na ujumuishaji,” alisema.

Kwa upande wake, Huawei ilisema ushirikiano wake na Airtel Tanzania utaendelea kuwa nguzo muhimu katika safari ya mageuzi ya kidijitali nchini Tanzania.

Kampuni hiyo pia iliipongeza menejimenti ya Airtel Tanzania kwa kushiriki katika majadiliano ya kimkakati yanayolenga kukuza sekta ya mawasiliano nchini na kuhamasisha matumizi ya teknolojia mpya zinazoibukia.

Mini MWC ni jukwaa maalum linaloandaliwa na Huawei Tanzania kwa ajili ya kuwapa wadau fursa ya kujionea teknolojia bunifu zinazooneshwa katika Kongamano la Kimataifa la Mobile World Congress linalofanyika kila mwaka mjini Barcelona, Hispania.

Jukwaa hilo pia linawawezesha wadau wa sekta ya mawasiliano kujadili mwenendo wa teknolojia mpya pamoja na matumizi yanayoongezeka ya Akili Unde (AI) katika kuboresha huduma za mawasiliano nchini.

Baadhi ya viongozi wa Huawei waliohudhuria kongamano hilo ni pamoja na Rais wa Idara ya Bharti Group Key Account, Jack Huang, pamoja na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Mauzo wa Huawei Tanzania, Galving Gao.

Kongamano hilo limefanyika wakati ambapo sekta ya mawasiliano nchini Tanzania inaendelea kushuhudia ukuaji mkubwa wa huduma za intaneti, matumizi ya huduma za kidijitali na ongezeko la matumizi ya data kutokana na mahitaji yanayoongezeka ya huduma bora na nafuu za mtandao.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments

MONACO - Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo ya Taifa kupitia sekta mbalimbali kwa kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 81 wa Michezo ya Majeshi Duniani (81st CISM General Assembly) uliofanyika nchini Monaco kuanzia tarehe 1 hadi 9 Mei 2026.

Mkutano huo wa kimataifa uliwakutanisha viongozi wa kijeshi na wadau wa michezo kutoka zaidi ya nchi 130 duniani kwa lengo la kuimarisha mshikamano, diplomasia ya michezo na amani kupitia kaulimbiu ya “Friendship Through Sport.”
Benki ya CRDB, ikiwa miongoni mwa wadau wakubwa wa maendeleo nchini, imeendelea kuunga mkono jitihada za vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na michezo ya majeshi, hatua inayoimarisha ushirikiano wake na taasisi za Serikali katika kukuza ustawi wa askari na familia zao.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Brigedia Jenerali Saidi Hamisi Saidi, akisaidiana na Luteni Kanali Penina Anthony Igwe. Kutoka CRDB, ujumbe unajumuisha Meneja wa Kitengo cha Wateja Maalum, Crispin Sichalwe pamoja na Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma, Emmanuel Tupeligwe.
Akizungumza kwenye mkutano huo, Sichalwe alisema CRDB imeendelea kutoa huduma maalum za kifedha kwa wanajeshi ndani na nje ya nchi, ikiwemo mikopo nafuu, bima na huduma za kifedha zinazowafikia popote walipo.

“Tunatambua mchango mkubwa wa majeshi katika usalama wa Taifa, hivyo tunahakikisha wanapata huduma bora na za haraka kupitia kitengo chetu maalum,” alisema.
Kwa upande wake, Tupeligwe alisisitiza kuwa CRDB itaendelea kushirikiana kwa karibu na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kupitia elimu ya fedha na huduma zinazowafikia wanajeshi hata wakiwa katika maeneo ya mbali au majukumu ya kimataifa.

Aidha, benki hiyo imeendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kimkakati na JWTZ ili kuhakikisha wanajeshi wanapata huduma bora za kifedha kwa urahisi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika maendeleo na usalama wa Taifa.

Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo