Nafasi Ya Matangazo

February 22, 2026


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele akizungumza leo Februari 22, 2026 na washiriki wa mafunzo ya makarani waongozaji wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Peramiho unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026. 

Na Waandishi wetu, Ruvuma na Songwe
Tume huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imewataka Makarani Waongozaji wapiga kura katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma kutekeleza majukumu yao bila woga kwa kufuata Sheria, Kanuni, maelekezo ya Tume.
 
Wito huo umetolewa na  Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele leo Februari 22, 2026 wakati akizungumza na washiriki wa mafunzo ya makarani waongozaji wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Peramiho unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026. 

“Nawasihi mnapokwenda kufanya kazi yenu mkawe wakarimu na wanyenyekevu katika kutekeleza shughuli zenu... .” amesema Jaji Mwambegele.

Jaji Mwambegele amewataka washiriki hao kutoa kipaumbele kwa wapiga kura wenye mahitaji maalum wakiwemo watu wenye ulemavu, wazee, wagonjwa, wajawazito na akina mama wanaonyonyesha watakaokwenda na watoto wao vituoni.

“Jambo lingine nawasihi mkatende kazi yenu bila kumuogopa mtu yeyote bali mkatekeleze majukumu yenu kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo ya Tume,” amesema Mhe. Jaji Mwambegele.
 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura klatika Jimbo la Peramiho 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura klatika Jimbo la Peramiho 
Katika hatua nyingine Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama Kuu Mhe. Asina Omari leo tarege 22 Februari, 2026 ametembelea mafunzo ya Makarani Waongozaji Wapiga Kura kwa ajili ya Uchaguzi mdogo wa Udiwani Kata ya Shiwinga, iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, Mkoani Songwe.
 
Mhe. Asina amewataka washiriki wa mafunzo hayo kufanya kazi kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo ya Tume kwani wao ndio taswira ya Tume katika kufanikisha uchaguzi huo.
 
Amesema pamoja na jukumu lao la kuwaongoza wapiga kura kutekeleza haki yao ya kupiga kura kwa urahisi, wanapaswa kutoa elimu ya mpiga kura kwa wapiga kura ambao hawatambui utaratibu wa kupiga kura kituoni.
 
“Mafunzo haya yana lengo la kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yenu. Hivyo, niwakumbushe mkatekeleze majukumu yenu kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo ya Tume” amesema Mhe. Asina na kuongeza….
 
“Kabla ya mafunzo mmeapa, viapo vyenu maana yake ni kwenda kutekeleza majukumu kwa uadilifu na kuzingatia weledi na kazi yenu ni zaidi ya kuwaongoza wapiga kura kwani mna jukumu la kutoa elimu ya mpiga kura”
 
Amesema katika kutekeleza majukumu yao wanapaswa kushirikiana na watendaji wa uchaguzi na wasimamizi wa vituo vya kupigia kura ili kuhakikisha wanatatua changamoto wanazokutana nazo wakati wa kutekeleza majukumu yao.
 
Akifungua mafunzo hayo, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Mbozi, Ndg. Danny Tweve amewakumbusha washiriki hao kuwa wamechaguliwa kutekeleza jukumu hilo la kitaifa kwa niaba ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi. Hivyo, wanapaswa kutoa huduma kwa wapiga kura kwa uaminifu na weledi mkubwa na kwa kuzingatia sheria za uchaguzi ili kufanikisha uchaguzi huo na kuwasaidia wapiga kura kutekeleza haki yao bila usumbufu.
 
Uchaguzi katika Jimbo la Peramiho, Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma na Udiwani katika Kata ya Shiwinga, Halmashauri ya Mbozi Mkoani Songwe umeapangwa kufanyika Februari 26,2026.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura katika Kata ya Shiwinga. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura katika Kata ya Shiwinga. 

Posted by MROKI On Sunday, February 22, 2026 No comments


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa wito kwa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Kampasi ya Tengeru ihakikishe inakuwa kitovu cha ubora wa kitaaluma na utafiti bunifu unaolenga kutatua changamoto halisi za dunia ya leo.

Ametoa wito huo leo (Jumapili, Februari 22, 2026) wakati akizungumza na viongozi wa mkoa wa Arusha, wanachuo na wakazi wanaoishi jirani na taasisi hiyo waliofika kushuhudia uwekaji wa jiwe la msingi katika hafla iliyofanyika kwenye Kampasi ya Tengeru, wilayani Arumeru, mkoani Arusha. 

“Tumeona tumeona chanjo ya samaki, tumeona mbolea inayozalishwa kwa kutumia mwani. Tumeona ndege nyuki ya kupanda mazao shambani, hii itaokoa muda wa unaotumika kupanda mazao. Hizi bunifu zote zinaundwa ili kurahisisha kazi kwani zinatatua mambo mengi kwenye shughuli za kila siku za maisha yetu,” amesema.

Aidha, ameitaka taasisi hiyo ihakikishe mafunzo yatakayotolewa, yanazingatia zaidi ujuzi wa vitendo, ubunifu na ujasiriamali ili wahitimu waweze kujiajiri, kuajiri wengine na kuwa sehemu ya suluhu ya changamoto ya ajira, badala ya kusubiri ajira serikalini pekee.

Ameutaka uongozi wa taasisi hiyo, kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, uhakikishe matumizi ya TEHAMA, mifumo ya kisasa ya kufundishia na kujifunzia, pamoja na usimamizi madhubuti wa rasilimali ili Kampasi hiyo iwe endelevu na shindani kimataifa.

Amewataka kwa wananchi wa Mkoa wa Arusha na mikoa jirani wakilinde na kukimiliki chuo kama rasilimali yao ya maendeleo kwa kushirikiana na Chuo katika kutoa huduma, mazingira rafiki na ushiriki wa kijamii.

Akisisitiza ukamilishaji wa hosteli hiyo, Waziri Mkuu amesema: “Kutokana na umuhimu wa hosteli hakikisheni hosteli hii inakamilika kwa wakati, kwa ubora unaokusudiwa, na inaanza kutoa huduma ili matunda ya uwekezaji huu yaanze kuonekana mapema kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.”

Amesema ujenzi wa hosteli hiyo unaakisi dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendeleza elimu ya juu na kuongeza nafasi za masomo katika nyanja ya sayansi kama nyenzo kuu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.



Kuhusu upatikanaji wa mikopo ya elimu ya juu, Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kuimarisha Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kwa kuongeza bajeti yake kutoka sh. bilioni 464 mwaka 2020/2021 hadi sh. bilioni 916.7 mwaka 2025/2026, hatua ambayo amesema imewezesha vijana wengi zaidi kutoka familia za kipato cha chini kupata fursa ya kujiendeleza kielimu.

“Hatua hiyo imewezesha idadi ya wanufaika kuongezeka kutoka 177,925 mwaka 2021/2022 hadi 252,773 mwaka 2025/2026 sawa na ongezeko la asilimia 42.1. Sambamba na hilo, Serikali imeboresha mifumo ya utoaji mikopo kwa kuzingatia vipaumbele vya Taifa katika sayansi, teknolojia, uhandisi, tiba na sasa kilimo cha kisasa.”

Akimkaribisha kuzungumza na hadhira hiyo, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda alisema chuo hicho ni cha kipekee kwa sababu kinahusika na utoaji wa masomo ya sayansi na teknolojia tu na pia kinatoa shahada za Uzamili na Uzamivu tu.

“Chuo hicho kinakidhi maelekezo ya Mheshimiwa Rais ya kutoa ufadhili kamili kwa wanafunzi wanaofanya vizuri sana. Hawa Serikali inawalipia gharama zote kwa asilimia 100. Mheshimiwa Rais pia alielekeza tuwapeleke kusoma nje ya nchi vijana waliofanya vizuri sana.”

“Tulianza na vijana 50. Kati yao, vijana 16 walikuja hapa Nelson Mandela kupata mafunzo maalum na sasa wako Afrika Kusini. Hawa vijana 34 waliokuja awamu ya pili, wanapatiwa mafunzo na wao ikifika Septemba wataenda Ireland kuanza masomo yao,” alisema wakati akielezea mpango huo.

Mapema, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo hicho, Balozi Maimuna Tarishi alisema ujenzi wa mabweni ya wanafunzi katika Kampasi ya Tengeru, unalenga kuongeza uwezo wa malazi wa wanafunzi kutoka 600 mwaka 2021 hadi 1,000 mwaka 2026. 

“Mradi unajumuisha jengo lenye ghorofa tatu katika mabawa matano ambalo lilikamilika litakuwa na vyumba 184. Kati ya hivyo, vyumba 160 ni self-contained, vyumba 20 ni  maalum kwa wanafunzi wa kike wenye watoto au mahitaji maalum na vinne vitakuwa kwa ajili ya matumizi mtambuka (common rooms).

Alisema mabawa matatu yako kwenye hatu ya umaliziaji na mawili yako kwenye hatua ya upauaji. “Ili kukamilisha ujenzi huu, zinahitajika sh. bilioni 1.88. Makadirio ya fedha hizo yako kwenye bajeti ya mwaka 2026/2027 na kama fedha yote itapatikana, tunatarajia ifikapo Desemba, 2026 majengo yote yatakuwa yamekamilika,” alisema.
Posted by MROKI On Sunday, February 22, 2026 No comments

Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Kampasi ya Tabora imefanya ziara ya kijamii katika Kituo cha Kulelea Wazee wenye Mahitaji Maalum kilichopo Ipuli, Manispaa ya Tabora. Ziara hiyo ilikuwa ni sehemu ya mikakati ya chuo kuimarisha ushirikiano na jamii.

Katibu Tawala wa Wilaya ya Tabora, Bi. Asha Churu, kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Kampasi ya Tabora, Dkt. Joseph Mbwillo, wameongoza timu  ya watumishi na wanachuo wa Kampasi ya Tabora kutembelea kituo hicho katika kujali na kusaidia wazee wenye mahitaji maalum.

Lengo kuu la ziara lilikuwa ni kuwapelekea misaada mbalimbali kwa wahitaji hao, ikiwa ni pamoja na mchele, maharage, mafuta ya kupikia na mafuta ya kujipaka, sabuni za kuogea na kufulia, nguo, sukari, mashuka pamoja na nguo katika kuboresha maisha ya wazee hao.

Pamoja na kutoa misaada hiyo, timu hiyo pia ilifanya kazi ya usafi wa mazingira ya makazi ya wazee pamoja na  zoezi la upandaji miti katika eneo hilo kwa lengo la kuimarisha ustawi wao na kuhifadhi mazingira kwa ujumla.

Ziara hii ni sehemu kuelekea kilele cha maadhimisho ya mika 25 ya chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kuonyesha mfano wa jamii inayojali na kuendeleza mazingira kwa manufaa ya wote.







Posted by MROKI On Sunday, February 22, 2026 No comments

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Leonard Akwilapo (wa pili kulia) akizungumza wakati wa kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga. Wa pili kushoto ni Waziri wa TAMISEMI Prof Riziki Shemdoe na kulia ni Naibu Waziri wa Mipango na Uwekezaji Dkt. Pius Chaya na Kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Muheza Ayubu Sebabili
********
Na Munir Shemweta, WANMM MUHEZA
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Leonard Akwilapo amewaongoza Mawaziri wenzake wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) pamoja na Ofisi ya Raisi Mipango na Uwekezaji katika kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga.

Kikao hicho kimefanyika tarehe 18 Februari 2026 katika ofisi ya Mkuu wa wilaya Muheza mkoa wa Tanga ikiwa ni utekelezaji wa masuala yaliyojitokeza wakati wa ziara ya Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba.

Mawaziri hao ni Prof. Riziki Shemdoe, Waziri wa TAMISEMI na Dkt. Pius Chaya, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji ambao kupitia kikao hicho, kilichohusisha pia wataalamu, viongozi hao walipata fursa ya kuwahoji wananchi walioguswa na migogoro hiyo ya mashamba ya uwekezaji ambayo yaliyofutiwa umiliki mwaka 2016.

Mashamba hayo ni Azimio/ Kilapula Geiglitz, Bwembwera, Kibaranga, Kihuhwi, Lewa pamoja na Saguras yaliyopo katika halmashauri ya wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga..
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Prof. Riziki Shemdoe (Wa pili kushoto) akizungumza katika kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga.

Naibu Waziri Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Dkt. Pius Chaya (Kulia) akisisitiza jambo wakati kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji kwenye wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga. Katikati ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo na kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Tanga Balozi Batilda Burian.

 

Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Muheza Dkt. Jumaa Mhina akizungumza wakati wa kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga. 


Baadhi ya wananchi walioguswa na mgogoro wa mashamba ya uwekezaji katika halmashauri ya Muheza mkoa wa Tanga wakielezea umiliki wao wa maeneo kwenye mashamba hayo mbele ya mawaziri wakati wa kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji tarehe 18 Februari 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)
Posted by MROKI On Sunday, February 22, 2026 No comments
Tanzania imeandika historia mpya katika sekta ya nishati baada ya kukamilika kwa ujenzi wa Mradi wa Kuzalisha Umeme kwa nishati ya jua ulioko Kishapu, mkoani Shinyanga mradi ambao ni mkubwa na wa kwanza wa aina yake nchini.

Akizungumza Februari 21, 2026 mara baada ya kukagua maendeleo ya mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema kukamilika kwa mradi huo ni ushahidi wa dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha upatikanaji wa huduma ya umeme ya uhakika kwa Watanzania.

“Hii ni historia mpya imeandikwa kwa nchi yetu. Tangu tupate uhuru, hatujawahi kuwa na mradi mkubwa wa aina hii ya umeme wa jua. Serikali kupitia Wizara ya Nishati na TANESCO imeandika historia, na leo mmeshuhudia hapa umeme ukizalishwa. Mpaka kufikia Machi 1, 2026 jumla ya Megawati 50 zitakuwa zimeunganishwa kwenye Gridi ya umeme ya Taifa,” alisisitiza Bw. Twange.

Bw. Twange ametumia fursa hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwezesha upatikanaji wa jumla ya Shilingi bilioni 118.6 kwa ushirikiano na Benki ya Maendeleo ya Ufaransa (AFD), fedha zilizowezesha utekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi huo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Mhe. Peter Masindi, amesema mradi huo ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa eneo hilo, hasa kwa vijana wanaojishughulisha na uchimbaji wa madini na shughuli za kilimo.

“Mradi huu umeleta ajira kwa wananchi wetu na umefungua ukurasa mpya wa maendeleo. Umeme wa uhakika utaongeza tija katika sekta za madini na kilimo, na kuchochea shughuli za kiuchumi na kijamii kwa wakazi wa Kishapu,” alisema Mhe. Masindi.

Naye Kaimu Meneja wa Kituo cha Kuzalisha Umeme Kishapu, Mhandisi Mariana Mrosso, alieleza kuwa kituo hicho kitaimarisha uthabiti wa Gridi ya Taifa na kuboresha ubora wa upatikanaji wa umeme, hususan kwa wateja wa maeneo ya mikoa ya Kanda ya Ziwa.

“Umeme unaozalishwa hapa utaongeza uwezo wa uzalishaji kwenye Gridi ya Taifa na kuboresha ufanisi wa huduma kwa wateja wetu hasa katika mikoa ya Kanda ya Ziwa,” alifafanua Mhandisi Mrosso.

Imeelezwa kuwa ifikapo Machi 1, 2026, megawati zote 50 zitakuwa zimeunganishwa kwenye Gridi ya Taifa. 

Wakati huo huo, TANESCO ipo katika hatua za mwisho za kumpata mkandarasi kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo, itakayozalisha megawati 100 kwa gharama ya Shilingi bilioni 200.4 za kitanzania.

Mradi wa Umeme wa Jua Kishapu unatajwa kuwa alama ya mabadiliko makubwa na hatua muhimu katika mwelekeo wa Tanzania kutumia matumizi ya nishati jadidifu katika uzalishaji wa umeme, hatua inayolenga kuimarisha usalama wa nishati zinazozalishwa nchini na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa Taifa.




Bvbbbb



Posted by MROKI On Sunday, February 22, 2026 No comments





Na Mwandishi wetu, Tabora
Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amezindua Kiwanda cha Rafiki Briquettes mkoani Tabora na kuielekeza Bodi ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kuongeza uzalishaji wa makaa ya mawe katika Mgodi wake wa Kiwira. Amesema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kupanua matumizi ya nishati safi ya kupikia na kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa.

Akizungumza Februari 21, 2026 wakati wa uzinduzi wa kiwanda hicho chenye uwezo wa kuzalisha tani 20 kwa siku, Waziri Mavunde, amesema kitasaidia kupunguza ukataji wa miti na kusaidia ukaushaji tumbaku mkoani Tabora. Ameongeza kuwa, uzinduzi huo ni utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuhusu matumizi ya nishati mbadala kwa ajili ya kukaushia tumbaku, na kuongeza kwamba, kiwanda  hicho kilichogharimu shilingi bilioni 3 kitawanufaisha wakulima wanaozalisha wastani wa tani 95,000 kwa mwaka ambao awali walitegemea kuni.

Waziri Mavunde amesema kutokana na akiba kubwa ya makaa ya mawe Kiwira, kutachangia kuongeza uzalishaji wa  nishati ya umeme.

 Amesisitiza kuwa matumizi ya nishati chafu yana athari kubwa kiafya na kimazingira, huku Serikali ikilenga kufikia zaidi ya asilimia 84 ya wananchi ifikapo mwaka 2034 kutumia nishati safi na salama.

*STAMICO Yabeba Agenda za Kitaifa za Uongezaji Thamani na Nishati Safi*
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa STAMICO, Dkt. Venance Mwasse, amesema uzinduzi wa kiwanda hicho unaendeleza ajenda za kitaifa za kuongeza thamani madini na kuhamasisha nishati safi ya kupikia. Amesema Shirika tayari lina kiwanda cha ubia cha kusafisha dhahabu cha Mwanza Precious Metals Refinery na sasa linazalisha na kusambaza Rafiki Briquettes kutoka makaa ya mawe ya Kiwira.

Ameongeza kuwa ujenzi wa kiwanda kingine unaendelea Dodoma na vingine vitano vinatarajiwa kujengwa katika mikoa mbalimbali ikiwemo Geita, hatua itakayofikisha jumla ya viwanda sita nchini. Amesisitiza kuwa briquettes hizo zimethibitishwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na zitasaidia kupunguza matumizi ya kuni na mkaa, huku kiwanda cha Tabora kikitarajiwa kutoa ajira 200 za moja kwa moja na zisizo rasmi.

*Balozi  Sirro Asisisitiza STAMICO Kuzalisha Briquettes Zenye Ubora*

Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya STAMICO, Balozi Simon Sirro, ameainisha umuhimu wa usimamizi mzuri wa Serikali na Wizara husika katika kuendesha shirika kwa ufanisi. Amesisitiza kuwa briquettes zinazozalishwa na STAMICO ni bora na zina soko, na kutoa wito wa kuongeza uzalishaji.

Aidha, ameeleza kuwa ili shirika liweze kujiendeleza, ni lazima kushindana na kampuni nyingine za uchimbaji madini na kuanzisha kampuni tanzu zenye ufanisi.  Amesema bodi ya STAMICO itaendelea kutekeleza maagizo ya Serikali, kuongeza mapato, na kutoa gawio kwa Serikali. 

*Kamati ya Bunge yapongeza ushiriki wa Stamico kwenye Nishati Safi*
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Subira Mgalu, ameipongeza Shirika la Madini Tanzania (STAMICO) kwa kuunga mkono agenda ya nishati safi ya kupikia na mafanikio ya sekta ya madini. Amesema kutokana na mwenendo mzuri wa sekta hiyo, Kamati itaendelea kuunga mkono juhudi za Wizara.

Ameeleza kuwa Serikali imefanikiwa kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia kutoka asilimia 6 hadi 27, na kumpongeza Waziri akisema, “Lakini Mhe. Waziri, tumeona namna unavyohamasisha uwekezaji huko duniani na sasa hapa unahamasisha matumizi ya nishati safi.”

Tukio la uzinduzi wa kiwanda hicho, limekwenda sambamba na kugawa vyeti kwa mawakala na makontena kwa mawakala Rafiki Briquettes katika mikoa mitano ya Tabora, Kigoma, Katavi, Rukwa na Singida. Pia, shirika hilo limesaini Mkataba wa Makubaliano na Chama Kuu cha Ushirika wa Tumbaku  Mkoa wa Tabora (WETCU) wa mashirikiano ya kuwaunganisha wakulima na STAMICO kutumia Rafiki Briquttes.
Posted by MROKI On Sunday, February 22, 2026 No comments

February 21, 2026








Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amezindua mradi wa kusambaza mifumo ya umeme jua visiwani unaolenga kuweka mifumo 20,000 ya umeme jua katika visiwa 120 kwa gharama ya Shilingi Bilioni 8 ambapo Rais, Dkt.Samia Suluhu Hassan ameweka ruzuku hadi ya asilimia 75 katika gharama za uunganishaji umeme.

Mhe. Salome Makamba amezindua mradi huo katika kisiwa cha Bezi wilayani Ilemela mkoani Mwanza ambapo  mradi huo unatekelezwa chini ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

"Maeneo ya visiwani na delta yana changamoto za kipekee, zikiwemo umbali kutoka Gridi ya Taifa, gharama kubwa za usafirishaji wa vifaa na mtawanyiko wa makazi unaoongeza gharama za usambazaji wa nishati ya umeme. Hata hivyo, changamoto hizi haziwanyimi wananchi haki ya kupata huduma ndio maana Serikali imekuja na mpango huu mahsusi wa matumizi ya mifumo ya umeme jua pamoja na gridi ndogo kama suluhisho la haraka la  kuwafikia wananchi wa visiwa na maeneo ya pembezoni." Amesema Mhe.Salome

Ameeleza kuwa hatua nyingine iliyochukuliwa na Serikali ili kurahisisha upatikanaji wa umeme katika maeneo kama hayo ya visiwa ni pamoja na kutoa ruzuku kwa mifumo ya umeme jua ili kuharakisha upatikanaji wa nishati safi, kupunguza utegemezi wa vyanzo visivyo endelevu kama dizeli, na kuhakikisha gharama za nishati zinakuwa nafuu.

Amesema mradi huo aliouzindua una mchango wa moja kwa moja katika kukuza Uchumi wa Buluu, ambao ni kipaumbele cha Taifa katika maeneo ya pwani na visiwa kwani mifumo ya umeme jua inayofungwa itawawezesha wavuvi kuongeza thamani ya samaki na dagaa kabla ya kupelekwa sokoni, jambo litakaloongeza mapato ya wananchi, Halmashauri pamoja na nchi, kuimarisha shughuli za ufugaji wa samaki (aquaculture), kilimo cha mwani, na huduma za utalii wa fukwe na visiwa, ambazo zote ni sehemu ya Uchumi wa Buluu. 

Mhe. Salome amemshukuru Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya nishati na kueleza kuwa Wizara itaendelea kusimamia kwa ukaribu utekelezaji wa miradi hiyo ili kuhakikisha ubora, uwazi na uwajibikaji vinazingatiwa katika kila hatua. 

Aidha, ameiagiza REA na TANESCO kuweka mifumo ya umeme kwa taasisi zinazotoa huduma muhimu kwa jamii kama vituo vya afya, mashule, vituo vya polisi ambavyo hadi sasa bado havijapata huduma hiyo.

Vilevile ameiagiza REA kuchochea matumizi ya nishati safi ya kupikia katika maeneo ya minada, stendi na masoko.Na katika kisiwa hicho cha Bezi wafanye  tathmini ya matumizi ya nishati safi katika soko la samaki na kuweka miundombinu ya nishati safi ya kupikia ili kuwalinda wakaangaji na wateja dhidi ya moshi wa kuni na mkaa ambao una athari kwa afya ya binadamu na mazingira. 

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amewaasa wananchi kutumia miradi ya umeme kama sehemu ya mabadiliko ya maisha  kwa kuhakikisha unatumika pia katika shughuli za kiuchumi.

Amesema Serikali inaendelea kuhakikisha miradi ya nishati jadidifu ikiwemo ya jua inakuwa na mchango mkubwa  katika gridi ya taifa na nje ya gridi huku moja ya mifano ukiwa ni mradi huo wa umeme  jua wa bei ya ruzuku uliozinduliwa pamoja na mradi wa Kishapu wa megawati 150.

Ameeleza kuwa, Serikali itaendelea kuhusisha sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi ya nishati lengo likiwa ni kufikisha megawati 8000 ifikapo 2030.

Kwa upande wake, Kaimu  Mkurugenzi Mkuu wa REA , Mhandisi Jones Olotu amesema mradi huo utakaotekelezwa katika mikoa nane kwa miaka miwili ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa nishati  (Energy Compact)  ambao moja ya azimio lake ni kufikisha huduma ya umeme kwa wananchi wote ifikapo 2030 na hii ukijumuisha kuunga wateja wapya takriban milioni 8.

Kwa Mkoa wa Mwanza amesema mradi utagusa visiwa 65 kwa gharama ya shilingi bilioni 4.8 ambapo Serikali tayari imetoa shilingi bilioni 3.3 na pesa iliyobaki wananchi watalipia kwa mfumo wa ruzuku.

Mikoa itakayonufaika na mradi wa kusambaza mifumo ya umeme jua visiwani unaolenga kuweka mifumo 20,000 ya umeme jua katika visiwa 120 ni Mwanza, Geita, Kagera, Mara, Rukwa, Lindi, Mtwara na Pwani.
Posted by MROKI On Saturday, February 21, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo