Nafasi Ya Matangazo

July 12, 2026



 

Posted by MROKI On Sunday, July 12, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu.
Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imezindua rasmi Mwongozo wa Kisheria wa Utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa Waandishi wa Habari Wakongwe, hatua inayolenga kutambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari waliolitumikia Taifa kwa muda mrefu na kwa utumishi uliotukuka katika maendeleo ya sekta ya habari nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo, Julai 11, 2026, wakati wa maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika katika Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Kupitia hotuba yake iliyosomwa na Dkt. Egbert Mkoko, Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Bw. Tido Mhando, alisema mwongozo huo umeandaliwa kwa kuzingatia mamlaka iliyopewa Bodi chini ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 pamoja na Kanuni zake, ili kuweka utaratibu wa utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa waandishi wa habari wakongwe waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya taaluma hiyo.

Alisema mwongozo huo unawahusu waandishi wa habari ambao wakati Sheria ya Huduma za Habari ilipoanza kutumika mwaka 2016 walikuwa na umri wa miaka 50 au zaidi na walikuwa tayari wametoa mchango mkubwa katika sekta ya habari, lakini hawakupata fursa ya kujiendeleza hadi kufikia sifa za kitaaluma zinazohitajika kwa mujibu wa sheria.

"Mwongozo huu unalenga kuhifadhi historia ya tasnia ya habari, kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe na kuhakikisha uzoefu wao unaendelea kuwa sehemu ya urithi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini," ilieleza sehemu ya hotuba ya Mwenyekiti.

Bw. Mhando alisisitiza kuwa mwongozo huo hauondoi wala haupunguzi masharti ya msingi yaliyowekwa na Sheria ya Huduma za Habari kuhusu sifa za kupata ithibati kwa waandishi wa habari, bali unaweka utaratibu wa kutekeleza mamlaka ambayo sheria imeipa Bodi kuhusu utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa watu wenye utumishi uliotukuka na waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya sekta ya habari.

Aidha, aliipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuendelea kuiwezesha Bodi kutekeleza majukumu yake na kuimarisha ushirikiano unaolenga kukuza weledi, uwajibikaji na maadili katika taaluma ya uandishi wa habari.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alisema uzinduzi wa mwongozo huo ni hatua muhimu katika utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari na unaonesha dhamira ya Bodi ya kuimarisha viwango vya taaluma huku ikitambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe waliolitumikia Taifa kwa uaminifu, uzalendo na weledi.

Sambamba na uzinduzi huo, JAB iliendesha mdahalo uliowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya habari kujadili maendeleo ya sekta ya habari nchini, utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari pamoja na mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mwaka mmoja wa utekelezaji wa mfumo wa utoaji wa ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo vya sheria.

Posted by MROKI On Sunday, July 12, 2026 No comments

July 11, 2026

Mkurugenzi wa Sera na Mipango kutoka Wizara ya Nishati,Petro Lyatuu ametembelea banda la Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA ) katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba)leo  Julai 11 2026.



Posted by MROKI On Saturday, July 11, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Mkurugenzi Mtendaji wa Wasafi Media, Nasib Abdul maarufu Diamond Platnumz, amesema utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari unaweka mazingira bora ya kukuza uwekezaji katika sekta ya habari kwa kuhakikisha vyombo vya habari vinaendeshwa kwa kuzingatia sheria, weledi na viwango vya taaluma.

Diamond alitoa kauli hiyo tarehe 11 Juni, 2026 alipotembelea Banda la Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), kufuatia mwaliko wa Bodi hiyo ili kujionea huduma na elimu inayotolewa kwa waandishi wa habari pamoja na wananchi.

Alisema uwekezaji katika sekta ya habari unahitaji nidhamu, maono, subira na uongozi unaozingatia sheria, akibainisha kuwa usimamizi unaofanywa na JAB unasaidia wawekezaji kuelewa matakwa ya kisheria na namna ya kuyazingatia bila kuhisi kuwa biashara zao zinakwamishwa.

"Utekelezaji na usimamizi wa Sheria ya Huduma za Habari unaonesha ni kwa kiwango gani Serikali inaunga mkono uwekezaji wa vijana katika sekta ya habari. Kazi ya Bodi si kuzuia watu kufanya biashara, bali kuwaelekeza kufuata matakwa ya sheria na kuwahamasisha kuongeza elimu na kukidhi vigezo vinavyotakiwa," alisema Diamond.

Aliongeza kuwa utekelezaji wa sheria unahitaji busara, maarifa na uwezo wa kuwaelimisha wadau ili waelewe mabadiliko ya taratibu bila kujenga hofu au kuona kuwa wanawekewa vikwazo.

"Kazi hii inahitaji busara na maarifa ya kuwafundisha watu, kuwaelekeza na kuwafanya waelewe taratibu mpya pasipo kuona kwamba wameharibiwa biashara zao. Nimeona Bodi ina timu nzuri inayounga mkono maono ya uongozi wake katika kusimamia sekta hii," alisema Diamond.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alimpongeza Diamond kwa uwekezaji wake katika sekta ya habari na kwa Wasafi Media kuendelea kuzingatia matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari.

Alisema JAB itaendelea kushirikiana na wamiliki wa vyombo vya habari na wadau wengine kuhakikisha sheria inatekelezwa kwa njia inayokuza weledi, uwajibikaji na maendeleo ya sekta ya habari, huku ikitoa elimu na ushauri unaowawezesha wadau kutekeleza matakwa ya sheria kwa ufanisi.

Ziara ya Diamond katika Banda la JAB ilikuwa sehemu ya maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika ndani ya Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, ambapo Bodi imekuwa ikitoa huduma za ithibati, elimu kuhusu Sheria ya Huduma za Habari na ushauri kwa waandishi wa habari, wamiliki wa vyombo vya habari na wananchi.
Posted by MROKI On Saturday, July 11, 2026 No comments
 



Dar es Salaam
Mjiolojia kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Abbas Mruma, amesema Tanzania inaendelea kujijengea nafasi muhimu duniani kutokana na kuwa na hifadhi kubwa ya madini muhimu ya kimkakati, yakiwemo graphite, lithium na rare earth elements, ambayo ni nguzo muhimu katika maendeleo ya teknolojia za kisasa na nishati safi.

Mruma ameyasema hayo wakati akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Stanslaus Muyungi, alipotembelea banda la Tume ya Madini katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Amesema mahitaji ya madini ya lithium yanaendelea kuongezeka kwa kasi duniani kutokana na matumizi yake katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, simu za mkononi, kompyuta mpakato (laptops) na vifaa vingine vya kisasa vya kielektroniki.

Amefafanua kuwa nchini Tanzania, madini ya lithium yanapatikana zaidi katika maeneo ya Dodoma na Ikungi, mkoani Singida.

Akizungumzia madini ya graphite, Mruma amesema Tanzania ndiyo nchi inayoongoza barani Afrika kwa kuwa na hifadhi kubwa ya madini hayo, ambayo ni malighafi muhimu katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme pamoja na matumizi mengine mbalimbali ya viwandani.

Aidha, amesema Tanzania pia ina hifadhi kubwa ya madini ya rare earth elements katika Ukanda wa Afrika Mashariki, yanayopatikana katika eneo la Ngualla mkoani Songwe na Wigu mkoani Morogoro.

Baada ya kupokea maelezo hayo, Dkt. Richard Stanslaus Muyungi ameipongeza Tume ya Madini kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu rasilimali za madini na fursa zilizopo katika sekta hiyo.

Amesema elimu hiyo ina mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa rasilimali za madini, fursa za uwekezaji na nafasi ya sekta ya madini katika kukuza uchumi na maendeleo endelevu ya Taifa.
Posted by MROKI On Saturday, July 11, 2026 No comments

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe, akitoa maelekezo kwa watumishi wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali wakati alipotembelea banda la Mamlaka katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) Julai 8,2026.
Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Aretas Lyimo, akisaini kitabu cha wageni wakati aipotembelea banda la Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) Julai 8,2026.
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe, akisaini kitabu cha wageni wakati aipotembelea banda la Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) Julai 8,2026.
*********
Na. Judith Meingarai
Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Aretas Lyimo, ameipongeza Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) kwa mchango wake mkubwa katika kuimarisha mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini kupitia uchunguzi wa kitaalamu wa sampuli, matumizi ya teknolojia za kisasa pamoja na utoaji wa ushahidi wa kisayansi unaosaidia kuimarisha ushindi wa kesi mahakamani.

Akizungumza wakati alipotembelea banda la GCLA katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Kamishna Jenerali Lyimo alisema ushirikiano kati ya DCEA na GCLA umeendelea kuimarika na kuwa nguzo muhimu katika kutekeleza majukumu ya taasisi hizo kwa ufanisi.

Alisema sampuli zote zinazowasilishwa GCLA kwa ajili ya uchunguzi hupimwa kwa wakati na kwa usahihi, jambo linalowezesha wataalamu wa Mamlaka hiyo kutoa ushahidi wenye weledi mahakamani na hivyo kuongeza kiwango cha mafanikio katika kesi zinazohusu dawa za kulevya.

"Ushirikiano wetu na GCLA ni wa mfano. Majibu ya uchunguzi tunayapata kwa wakati pamoja na ushahidi wa kitaalamu unaotolewa na Wakemia mahakamani umechangia kwa kiwango kikubwa kushinda kesi mbalimbali zinazohusu dawa za kulevya," alisema Lyimo.

Aidha, aliipongeza GCLA kwa kuendelea kuwekeza katika vifaa na teknolojia za kisasa zinazowezesha kubaini aina mbalimbali za dawa za kulevya na kemikali husika, akieleza kuwa uwezo huo umeifanya Tanzania kuwa na mfumo imara wa uchunguzi wa kisayansi unaokidhi mahitaji ya sasa.

Alibainisha kuwa duniani kuna zaidi ya aina 1,430 za dawa za kulevya na kwamba uwezo wa GCLA wa kuzitambua na kuzichunguza kwa usahihi ni mchango mkubwa katika kuimarisha utekelezaji wa sheria na utoaji wa haki.

Kamishna Jenerali Lyimo pia aliwataka wafanyabiashara na wananchi kuhakikisha wanajiridhisha kuhusu kemikali zilizomo kwenye bidhaa wanazoingiza au kuuza nchini kwa kushirikiana na GCLA, pamoja na taasisi nyingine za udhibiti, ili kuepuka kujikuta wakikiuka sheria bila kufahamu.

"Baadhi ya wafanyabiashara wamejikuta wakikamatwa kwa kuuza bidhaa walizodhani ni salama, lakini baadaye kubainika kuwa zina kemikali zinazohusiana na dawa za kulevya. Ni muhimu kupata ushauri na uhakiki wa kitaalamu kabla ya kuingiza au kusambaza bidhaa hizo," alisisitiza.

Wakati huo huo, mmoja wa wananchi waliotembelea banda la GCLA, Pasehsi Anthony mkazi wa Mbezi, Dar es Salaam, alisema elimu aliyoipata imemsaidia kuelewa kwa undani mchango wa Mamlaka hiyo katika mfumo wa haki jinai nchini.

Alisema kabla ya kutembelea banda hilo hakuwa akifahamu kuwa dawa zote za kulevya zinazokamatwa nchini lazima zipitie uchunguzi wa kisayansi katika maabara za GCLA ili kuthibitisha aina ya dawa husika kabla ya ushahidi huo kutumika mahakamani.

"Leo nimegundua kuwa GCLA ina jukumu kubwa zaidi kuliko nilivyokuwa nikifahamu. Uchunguzi wake wa kisayansi unasaidia kuthibitisha ukweli mahakamani na kuhakikisha haki inatendeka. Nawahamasisha wananchi wote watembelee banda hili ili wapate elimu muhimu kuhusu huduma zinazotolewa na taasisi hii," alisema Anthony.

Kupitia ushiriki wake katika Maonesho ya Sabasaba, GCLA inaendelea kutumia jukwaa hilo kutoa elimu kwa wananchi kuhusu huduma zake mbalimbali, ikiwemo uchunguzi wa kisayansi wa dawa za kulevya, kemikali, bidhaa, mazingira na vielelezo vya jinai, sambamba na kuhamasisha matumizi salama ya kemikali kwa maendeleo na usalama wa taifa.


Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kuthibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Aretas Lyimo (Katikati), akiwa na Mkurugenzi wa Huduma za Taasisi, Evaclotida Kapinga (wa nne kutoka kushoto) pamoja na watumishi wa Mamlaka katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) Julai 8,2026.
Posted by MROKI On Saturday, July 11, 2026 No comments

July 10, 2026


Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia Mradi wa Urejeshaji Endelevu wa Mazingira na Hifadhi ya Bayoanuai Tanzania imewezesha urejeshaji wa hekta milioni 3.3 za ardhi na misitu iliyoharibiwa hadi kufikia mwezi Desemba 2024.
 
Hayo yamebainishwa Julai 9, 2026 Mkoani Morogoro na Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais, Abdllah Hassan Mitawi wakati ufunguzi wa warsha ya kujenga uwezo kikosi-kazi cha taifa cha urejeshaji wa mazingira ya ardhi na misitu iliyoharibika.
 
Amebainisha kuwa Tanzania imebarikiwa utajiri mkubwa wa mifumo ikolojia ambapo takribani hekta milioni 48 ni misitu, ambapo hata hivyo pamoja na wingi wa rasimali hizo kumekuwepo na changamoto za uharibifu wa mazingira, ambapo tafiti zimeonesha kuwa takribani hekari 469,000 za misitu hupotea kila mwaka.
 
Mitawi amesema urejeshaji wa Ardhi ya Misitu iliyoharibiwa ni sehemu ya ajenda muhimu ya maendeleo endelevu ya Tanzania, kutokana na hatua hiyo Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kisera na kimkakati kwa kushirikiana na wadau.
 
Amesema mwa juhudi hizo ni utekelezaji wa Mkakati wa AFR100, unaolenga kurejesha hekta milioni 100 za ardhi  na misitu iliyoharibika barani Afrika kufikia mwaka 2030 ambapo mkakati huo unachangia malengo ya kidunia ya kurejesha hekari milioni 350 za ardhi na misitu duniani kote.
 
Amefafanua kuwa katika kuchangia jitihada za kimataifa na malengo ya uhifadhi mazingira kitaifa, mwaka 2018, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliahidi kurejesha hekta milioni 5.2 za maeneo ya ardhi na misitu iliyoharibika kufikia mwaka 2030 chini ya mkakati wa AFRI100.
 
Kwa mujibu wa Mitawi amesema mwaka 2024 Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia mradi wa Urejeshaji Endelevu wa Mazingira na Hifadhi ya Bayoanuai Tanzania (SLR) ilikamisheni Kituo cha Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC) kufanya tathmini ya utekelezaji wa ahadi hiyo ili kubaini hatua iliyofikiwa.
 
Ameeleza utekelezaji wa ahadi hiyo inaongozwa na na Mkakati wa Taifa wa Urejeshaji wa Ardhi na Misitu iliyoharibiwa (2023–2033); Mpango Kabambe wa Taifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022 – 2032); Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024 -2034) na Programu ya Mageuzi ya Usimamizi wa Mazingira kuelekea Dira2050.
 
”Nichukue fursa hii kuwajulisha wajumbe wa kikosi-kazi hiki mchukue jambo hili kwa umakini na uzito unaostahili, kwakuwa Serikali na wadau wote wa masuala ya urejeshaji na hifadhi wa mazingira watategemea sana maoni, ushauri na mapendekezo yenu” amesema Mitawi.
Kaimu Meneja wa Vyanzo vya Mbegu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Dk Fortunata Senya alisema Serikali imeandaa Mkakati wa Taifa wa Urejeshaji wa Mandhari ya Misitu wa mwaka 2023–2030 ili kuhakikisha lengo la kurejesha hekta milioni 5.2 linafikiwa.
 
Alisema mafanikio ya mpango huo hayawezi kupatikana kwa juhudi za Serikali pekee, bali yanahitaji ushiriki mpana wa wadau mbalimbali wakiwamo taasisi za utafiti, sekta binafsi, mashirika ya maendeleo na wananchi.
 
Kwa upande wake, Mtafiti wa Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI), Joshua Maguzu alisema taasisi hiyo inaendelea kufanya tafiti zinazolenga kubaini aina sahihi za miti zinazofaa kupandwa katika maeneo mbalimbali ya nchi kulingana na hali ya udongo na tabianchi.
 
 
Alisema matokeo ya tafiti hizo yanawasaidia wataalamu na wananchi kuchagua miche inayostawi vizuri katika maeneo husika, hatua inayoongeza mafanikio ya urejeshaji wa mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.




Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu, Arusha
WIZARA ya Maliasili na Utalii imepongeza hatua kubwa iliyofikiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika kujiandaa kupokea wageni wa mashindano ya AFCON 2027, baada ya Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki, Bw. Daniel Pancrasi, kujionea maendeleo makubwa yaliyofanyika katika eneo la utalii la Ziwa Duluti, Arusha.

Bw. Pancrasi alitoa pongezi hizo alipofanya ukaguzi wa maandalizi ya miundombinu na huduma zinazotekelezwa na TFS, akisema ameridhishwa na uwekezaji mkubwa uliofanywa hususan katika maeneo ya malazi, huduma za chakula na kuboresha mazingira ya utalii kwa viwango vinavyoweza kupokea wageni wa kimataifa wakati wa AFCON.

“Hongereni sana TFS. Kwa muda mrefu mmekuwa mkituletea taarifa mbalimbali kuhusu maandalizi haya, lakini leo nimejionea mwenyewe kazi kubwa iliyofanyika. Hakika nimefurahishwa sana. Nitakuwa shahidi katika vikao mbalimbali kwamba TFS haisemi tu kwa maneno, bali inafanya kazi kwa vitendo,” alisema Bw. Pancrasi huku akisisitiza kuwa maandalizi hayo yanaonesha dhamira ya Serikali kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na fursa za kiuchumi zitakazotokana na AFCON 2027.

Alisema maboresho yaliyofanyika Ziwa Duluti yanaongeza hadhi ya vivutio vya utalii vya Tanzania na kuweka mazingira bora ya kuwahudumia wageni kutoka mataifa mbalimbali watakaowasili nchini wakati wa mashindano hayo.

Awali, Mkuu wa Dawati la Utalii wa TFS, Mhifadhi Mkuu, PCO Someni Mteleka, alisema maboresho yanayotekelezwa katika Ziwa Duluti ni sehemu ya mkakati mpana wa TFS wa kuandaa vivutio vya utalii vinavyosimamiwa na wakala huo ili viwe tayari kupokea idadi kubwa ya wageni wakati wa AFCON 2027.

Mteleka alisema uwekezaji unaoendelea unalenga kuboresha ubora wa huduma za malazi, migahawa, mapokezi ya wageni na shughuli mbalimbali za utalii wa asili, sambamba na kuhakikisha wageni wanapata huduma zinazokidhi viwango vya kimataifa.

Aliongeza kuwa TFS inaendelea kutekeleza maagizo ya Serikali ya kutumia AFCON 2027 kama jukwaa la kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia vivutio vya utalii, huku Ziwa Duluti likiwa miongoni mwa maeneo yaliyopangwa kuwa kitovu cha mapumziko na burudani kwa wageni watakaofika nchini.

Ziara ya Bw. Pancrasi imeongeza matumaini kuwa kasi ya maboresho inayoendelea katika vivutio vya utalii vinavyosimamiwa na TFS itaifanya Tanzania kuwa tayari kupokea maelfu ya wageni wa AFCON 2027, huku Ziwa Duluti likitajwa kuwa mfano wa namna uwekezaji wa kimkakati unavyoweza kubadilisha vivutio vya utalii kuwa bidhaa zinazoweza kushindana katika soko la kimataifa.

Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments
Wananchi wanaotembelea banda la Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) wanapata fursa ya kujifunza mchango wa mashamba ya miti ya kupandwa katika kukuza uchumi wa viwanda na biashara ya mazao ya misitu nchini.

Katika banda hilo, TFS inaonesha jinsi mashamba ya miti yanavyotoa malighafi kwa viwanda mbalimbali vinavyozalisha mbao, samani, karatasi na bidhaa nyingine za misitu, huku yakichangia uhifadhi wa mazingira na kuongeza ajira.

Mbali na hilo, wageni wanapata nafasi ya kujionea uzalishaji wa mianzi na kufahamu matumizi yake katika ujenzi, utengenezaji wa samani, bidhaa za ubunifu na uhifadhi wa mazingira.

Wataalamu wa TFS pia wanatoa elimu kuhusu mbinu bora za upandaji na utunzaji wa miti, uvunaji endelevu, pamoja na taratibu za kufanya biashara ya mazao ya misitu kwa kuzingatia sheria na kanuni.

Kupitia maonesho hayo, TFS inawahimiza wananchi, wawekezaji na wafanyabiashara kutembelea banda lake ili kupata ushauri wa kitaalamu, kufahamu fursa zilizopo katika sekta ya misitu na kushiriki katika kukuza uchumi wa Taifa kupitia matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.




Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Maridhiano baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Alliance For Change and Transparency (ACT-Wazalendo) kuelekea uundwaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) Zanzibar, umepongezwa kwani umezingatia maslahi ya nchi ambayo ni muhimu kuliko maslahi binafsi ya wanasiasa.

Hayo yameelezwa na Mbunge wa Viti Maalum CCM na Mwenyekiti Taifa wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mary Chatanda, Julai 9, 2026, Jijini Dodoma.

Akitoa maoni yake baada ya kumalizika hafla hiyo ya Tamko la Pamoja la Maridhiano ya Kisiasa baina ya vyama hivyo, Chatanda amesema, Wazanzibar wameshasahau siasa za chuki, kipaumbele chao sasa ni umoja, mshikamano na maendeleo.

"Wazanzibar ni watu rahimu sana, wao wanataka amani, mshikamano na maendeleo na kitendo cha vyama hivi viwili kufikia muafaka, ni ishara ya ukomavu wa kisiasa na kuzingatia maslahi ya nchi," amesema Chatanda.

Aidha, amesema maridhiano hayo yana maana kubwa katika kuhakikisha SUK inaundwa kwa ukamilifu wake kwani SUK ndiyo mwelekeo wa siasa za Zanzibar katika uundwaji wa serikali. 

Sambamba na hilo, amesema ni muhimu kwa wananchi na wanasiasa wa Zanzibar kumpa ushirikiano Rais Dk. Hussein Mwinyi ambaye amejipambanua kuwa kiongozi mchapakazi, msikivu na mpenda maendeleo kwa wananchi wake.

"Wazanzibar wana Rais mchapakazi na mwenye maono makubwa ya maendeleo, wananchi wanapaswa kumpa ushirikiano na kuhakikisha Zanzibar inasonga mbele kwa kasi," amesisitiza.

Katika hafla hiyo, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amesisitiza kuwa, maridhiano hayo si udhaifu bali ni ukomavu wa kisiasa na unafungua ukurasa mpya wa umoja, amani, utulivu na mshikamano kwa maendeleo ya wananchi wa Zanzibar.

"Uungwana hautufunzi kiburi na kutosikilizana. Wananchi wetu hawahitaji vurugu wala mivutano ya kisiasa isiyoisha. Wananchi wetu wanahitaji amani, usalama na utulivu," amesema Rais Dk. Samia
Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments
Serikali imeanza utekelezaji wa bajeti mpya kwa mwaka wa fedha 2026/2027. Yale yaliyopangwa na serikali na kujadiliwa na Bunge na hatimaye yakaafikiwa katika bajeti hiyo, yameanza kufanyiwa kazi ili kufanikisha mipango ya maendeleo.

Wizara ya Fedha kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekuja na mabadiliko mbalimbali ya kodi. Mabadiliko haya yamelenga kuleta mageuzi, ufanisi na hatimaye kuongeza mapato bila kumuumiza mlipakodi ambaye ni mdau muhimu katika mipango ya maendeleo. 

Kwahiyo, kutokana na mabadiliko hayo, TRA pamoja na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA), wameratibu mafunzo kwa wahasibu, wakaguzi, wataalamu wa fedha na washauri wa kodi ili kuwajengea uwezo wa mabadiliko hayo ili ukusanyaji kodi ufanyike kwa ufanisi.

Hivyo basi, baada ya kupata mafunzo hayo, watakuwa na jukumu la kwenda kwa walipakodi na wananchi kuwaelimisha juu ya mabadiliko hayo ili kujenga uelewa wa pamoja ili yale yaliyopangwa yaweze kutimia.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Julai 8, 2026, Jijini Dar es Salaam, Meneja wa Elimu kwa Mlipakodi, CPA Paul Walalaze, ambaye alimwakilisha Kamishna Mkuu wa TRA, amesema wataalamu hao wanapaswa kunolewa ili kutambua mabadiliko ya sheria za kodi ili kuongeza tija.

"Mafunzo haya yameandaliwa ili kuwajengea uwezo wa kutekeleza vyema majukumu yenu lakini mkawasaidie walipakodi pia ili tija ipatikane," amesema CPA Walalaze.

Katika hatua nyingine, CPA Walalaze amesema, mabadiliko hayo yamehusisha Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), Sheria ya Kodi ya Mapato, Sheria ya Ushuru wa Bidhaa na Sheria ya Usajili wa Vyombo vya Moto.

Mabadiliko mengine ni Sheria ya Usimamizi wa Kodi, Sheria ya Ushuru wa Stempu, Sheria ya Uingizaji wa Bidhaa Nchini na Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ikumbukwe kuwa, mkakati wa serikali ni kuhakikisha nchi inajitegemea kibajeti kwa asilimia kubwa kwa kuimarisha ukusanyaji kodi. Tayari, katika bajeti hii ya 2026/2027, asilimia 74.2 ni mapato ya ndani. Jambo hili, linatoa dira ya kufanikiwa mipango ya maendeleo kwani makusanyo ya kodi ndiyo msingi wa kufanikisha mipango hiyo.





Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments

Makatibu Wakuu wanaosimamia sekta za Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wamekutana jijini Arusha kukamilisha maandalizi ya Mkutano wa 20 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa (Transport, Communications and Meteorology Sectoral Council – TCM), unaotarajiwa kufanyika Julai 10, 2026.

Mkutano huo wa ngazi ya Makatibu Wakuu umejadili na kupokea taarifa ya wataalamu waliokutana kuanzia Julai 6 hadi 8, 2026, kuhusu utekelezaji wa maamuzi ya mkutano uliopita wa TCM pamoja na maendeleo ya miradi na programu za kikanda zinazolenga kuimarisha miundombinu, kurahisisha shughuli za usafiri na biashara na kuongeza ushirikiano kati ya nchi wanachama.

Miongoni mwa masuala muhimu yaliyojadiliwa ni maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya barabara, reli, usafiri wa anga na majini, uboreshaji wa Vituo vya Huduma kwa Pamoja Mipakani (One Stop Border Posts – OSBPs), pamoja na kuimarisha mifumo ya ubadilishanaji wa taarifa za hali ya hewa.

Akifungua mkutano huo, Naibu Katibu Mkuu wa Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki anayesimamia Sekta za Miundombinu, Uzalishaji, Jamii na Siasa, Bw. Andrea Aguer Ariik, alibainisha kuwa EAC inaendelea kupiga hatua kubwa katika kuendeleza miundombinu ya uchukuzi na mawasiliano, hatua ambazo zinachangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi na maendeleo ya kijamii katika ukanda.

“Hadi sasa tumepiga hatua tunazostahili kujivunia. Kwa mfano, takribani kilomita 15,000 za mtandao wa reli zinatumika na kuendelea kujengwa katika nchi wanachama, hususan Tanzania na Kenya, hatua hii itachochea muunganiko wa kikanda na kurahisisha mwingiliano wa watu na bidhaa,” alisema Bw. Ariik.

Mkutano wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa ni jukwaa muhimu la kufanya maamuzi ya kisera yanayolenga kuimarisha mtangamano wa kikanda kupitia maendeleo ya miundombinu ya kisasa, usafiri salama na wenye ufanisi, pamoja na huduma bora za mawasiliano na hali ya hewa kwa manufaa ya wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo umeongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dkt. Charles Msonde, akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi – Zanzibar, Mhandisi Ali Said Bakari, Mkurugenzi Mtendaji TCAA, Dkt. Jabiri Kuwe Bakari, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASHICO), Bw. Eric B. Hamissi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Ladislaus Benedict Chang’a, pamoja na maafisa wengine waandamizi kutoka wizara na taasisi mbalimbali za Serikali.





Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments

July 09, 2026

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akepeana mkono wa maridhiano na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman baada ya utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026. 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman pamoja na Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, Amani Abeid Karume wakishuhudia utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026. Kushoto anaye saini ni Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo- Zanzibar Omary Ally Shehe pamoja na Naibu Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM- Zanzibar Dkt. Mohammed Said Dimwa
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman pamoja na Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, Amani Abeid Karume wakishuhudia utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026. Kushoto anaye saini ni Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo- Zanzibar Omary Ally Shehe pamoja na Naibu Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM- Zanzibar Dkt. Mohammed Said Dimwa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Ikulu Zanzibar kabla ya kuhudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, tarehe 09 Julai, 2026. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi wakati wakiwasili katika viwanja vya Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kuhudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, tarehe 09 Julai, 2026. 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026. 







Posted by MROKI On Thursday, July 09, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo