Nafasi Ya Matangazo

May 02, 2026

Na Mwandishi Wetu

Manyara. Kampuni ya Mati Super Brands Ltd imeibuka kinara katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yaliyofanyika kimkoa mwaka 2026, baada ya kuonesha ubunifu wa hali ya juu na ushindani uliovutia katika vipengele mbalimbali vya sherehe hizo.

Katika tukio hilo lililofanyika kwa shamrashamra kubwa, kampuni hiyo ilitwaa ushindi wa jumla, ikiibuka bora katika maandamano ya miguu, ubunifu wa magari pamoja na uandaaji wa banda bora, hatua iliyowavutia waamuzi na washiriki wengine.
Akizungumza wakati wa kukabidhi tuzo hizo Mei 1, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, aliipongeza Mati Super Brands Ltd kwa ubunifu na kujituma kwake, akisema imeonesha mfano bora wa ushiriki wa sekta binafsi katika kuadhimisha siku hiyo muhimu kwa wafanyakazi.

“Tumeshuhudia ushindani wa hali ya juu mwaka huu, lakini Mati wamejitofautisha kwa ubunifu, mpangilio na ujumbe waliouwasilisha. Hii ni ishara ya kampuni inayojali wafanyakazi na maendeleo ya jamii,” alisema Sendiga.

Kufuatia ushindi huo, kampuni hiyo ilikabidhiwa kombe la ubingwa wa jumla pamoja na cheti cha pongezi, ikiwa ni kutambua mchango wake katika kuhamasisha ari ya kazi na ubunifu katika maadhimisho ya Mei Mosi.

Kwa niaba ya kampuni, Afisa Rasilimali Watu wa Mati Super Brands Ltd, Doreen Mushi, alipokea tuzo hizo na kueleza kuwa ushindi huo ni matokeo ya mshikamano na jitihada za wafanyakazi wa kampuni hiyo.

Alisema kampuni itaendelea kuwekeza katika ubunifu na kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza tija na kuchangia maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

“Ushindi huu unatupa motisha ya kufanya zaidi. Tutazidi kubuni na kuboresha shughuli zetu ili kuendana na mahitaji ya soko na dira ya maendeleo ya taifa,” alisema Mushi.

Naye Mwenyekiti wa Makampuni ya Mati, David Mulokozi, alibainisha kuwa kampuni hiyo inaendelea kuwekeza katika sekta ya kilimo kwa kuzingatia mwelekeo wa serikali wa kuimarisha uzalishaji kupitia teknolojia za kisasa.

Alifafanua kuwa kampuni hiyo imeanza kuzalisha vifaa vya kisasa ikiwemo ndege nyuki (drones) za kunyunyizia dawa mashambani, hatua inayolenga kurahisisha kazi kwa wakulima, kupunguza gharama na kuongeza tija katika uzalishaji.

“Tunataka kuona mkulima wa Tanzania anatumia teknolojia za kisasa ili kuongeza uzalishaji na kipato. Hii ndiyo dira yetu kama kampuni,” alisema Mulokozi.

Maadhimisho ya mwaka huu yamebeba kaulimbiu isemayo “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” ikisisitiza umuhimu wa ajira bora na mazingira rafiki ya kazi katika kufikia maendeleo ya muda mrefu ya taifa.

Ushindi wa Mati Super Brands Ltd katika maadhimisho hayo umeendelea kudhihirisha nafasi ya sekta binafsi katika kukuza uchumi, kuhamasisha ubunifu na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia ajira na maendeleo ya kilimo.
Posted by MROKI On Saturday, May 02, 2026 No comments

May 01, 2026






Na Mwandishi wetu, Njombe
Watumishi wa Tume ya Madini kwa kushirikiana na Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe wameshiriki kikamilifu katika Maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) yaliyofanyika kitaifa Mei 1, 2026 katika Viwanja vya Lunyanywi, Halmashauri ya Mji wa Njombe.

Maadhimisho hayo yanayofunguliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, yanahusisha wafanyakazi kutoka sekta mbalimbali nchini waliokusanyika kuenzi mchango wa wafanyakazi katika maendeleo ya taifa pamoja na kujadili ustawi wao na kuboresha mazingira ya kazi.

Watumishi wa Tume ya Madini wameshiriki katika maandamano rasmi pamoja na taasisi nyingine za umma na binafsi, wakionesha mshikamano wa wafanyakazi wa Sekta ya Madini katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kukuza uchumi kupitia rasilimali madini.

Kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu isemayo, “Kazi zenye staha ni nguzo imara kwa maendeleo endelevu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” imelenga kuhamasisha ajira zenye heshima, kulinda haki za wafanyakazi na kuimarisha mchango wao katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya muda mrefu ya nchi.

Maadhimisho ya Mei Mosi hufanyika kila mwaka duniani kote kama jukwaa la kutambua mchango wa wafanyakazi katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii pamoja na kuhimiza mazingira bora na salama ya kazi.
Posted by MROKI On Friday, May 01, 2026 No comments








Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Watumishi wa Tume ya Madini wameaswa kuzingatia weledi, uwajibikaji na mshikamano katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuendeleza mafanikio ya Tume pamoja na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa taifa.

Akizungumza leo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) yaliyofanyika kimkoa katika Viwanja vya Jamhuri jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala wa Tume ya Madini, Nsajigwa Kabigi, amesema mafanikio yaliyopatikana yanapaswa kulindwa kwa kuongeza bidii, nidhamu na uwajibikaji kazini.

Kabigi amesema Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amewapongeza watumishi wote wa Tume waliopo Dodoma, wale walioshiriki maadhimisho ya kitaifa mkoani Njombe pamoja na watumishi waliopo katika mikoa mbalimbali ya kimadini nchini kwa juhudi zao katika kutekeleza majukumu ya kazi.

“Tumeaswa kuendelea kudumisha mshikamano, upendo na kufanya kazi kwa bidii ili kuendelea kuiweka Tume ya Madini katika nafasi ya juu ya utendaji,” amesema Kabigi.

Ameeleza kuwa Tume ya Madini imeendelea kufanya vizuri katika utekelezaji wa majukumu yake, akisisitiza kuwa ni wajibu wa kila mtumishi kuhakikisha taasisi inaendelea kuwa kinara katika ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali kutoka sekta ya madini.

Aidha, amesema waajiri wataendelea kulinda haki za wafanyakazi mahali pa kazi, huku akisisitiza kuwa watumishi wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na bidii ili kufikia malengo ya sekta ya madini na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Katika maadhimisho hayo ya Mei Mosi mkoani Dodoma, maandamano ya wafanyakazi yalianzia Viwanja vya Bunge na kuhitimishwa katika Viwanja vya Jamhuri, ambapo yalipokelewa rasmi na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule.
Posted by MROKI On Friday, May 01, 2026 No comments

April 30, 2026

Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk akizungumza wakjati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika Mkoani Morogoro. Mafunzo hayo yamefungwa leo tarehe 30 Aprili, 2026 na yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026.
Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk akizungumza wakjati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika Mkoani Morogoro. Mafunzo hayo yamefungwa leo tarehe 30 Aprili, 2026 na yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa rufani Jacobs Mwambegele akiwa katika ufungaji wa mafunzo hayo. 

Na. Mwandishi Wetu, Morogoro
Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi imetoa wito kwa watendaji wa uchaguzi kuhakikisha wanatumia muda wao kusoma Katiba, sheria za uchaguzi, kanuni na maelekezo ya Tume ili waweze kusimamia uchaguzi kwa weledi.
 
Wito huo umetolewa na Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk Mkoani Morogoro leo tarehe 30 Aprili, 2026 wakati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026.
 
Mafunzo hayo ni sehemu ya mchakato wa maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge kwenye Jimbo la Ismani Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika tarehe 01 Juni, 2026.
 
“Natumia nafasi hii kuendelea kuwasisitiza kuhusu umuhimu wa kutenga sehemu ya muda wenu kusoma Katiba, sheria na maelekezo mbalimbali yanayotolewa na Tume ili yawaongoze katika kusimamia uchaguzi utakaokuwa huru na wa haki,” amesema Jaji Mbarouk.
 
Amewataka watendaji hao wa uchaguzi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na weledi ili kufanikisha uchaguzi huo mdogo ambao unafanyika kujaza nafasi wazi ya mbunge na madiwani.
 
 “Jukumu lililopo mbele yetu ni kubwa na muhimu, linahitaji umakini na kujituma. Ni matazamio ya Tume kwamba, baada ya kupatiwa mafunzo haya, mtatekeleza majukumu yenu kwa ufanisi na weledi mkizingatia ratiba ya utekelezaji ili kufanikisha uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Ismani na Kata 12 za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika tarehe 01 Juni, 2026,” amesema Jaji Mbarouk.
 
Amesisitiza kuwa ili ufanisi uwepo ni muhimu watendaji hao wazingatie sifa na uwezo wakati wa kuteua na kuajiri watendaji wa vituo vya kupigia kura kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni.
 
“Kuhusu ajira za watendaji wa vituo, tunayo imani kuwa mtateua na kuajiri watendaji wenye sifa na uwezo wa kufanya kazi hii muhimu kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni. Kazi ambayo inahitaji umahiri, umakini na weledi katika kuitekeleza.,” amesema Jaji Mbarouk.
 
Amewataka watendaji hao kuhakikisha kuwa mafunzo ya watendaji wa vituo yanafanyika kwa ufanisi na weledi katika tarehe zilizopangwa kwenye ratiba ya utekelezaji wa shughuli za uchaguzi.
 
Ameongeza kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo ili waweze kufahamu majukumu yao na kuyatekeleza ipasavyo wakati wa uchaguzi.
 
Mafunzo hayo yamewahusisha Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu.
 
Kata 12 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi wa Udiwani ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu.
 
Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.

Sehemu ya watendaji wa uchaguzi katika jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania bara wakisikiliza hotuba ya kufunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika mkoani Morogoro kuanzia tarehe 28 hadi 30 Aprili, 2026. 

Sehemu ya watendaji wa uchaguzi katika jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania bara wakisikiliza hotuba ya kufunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika mkoani Morogoro kuanzia tarehe 28 hadi 30 Aprili, 2026. 

Sehemu ya watendaji wa uchaguzi katika jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania bara wakisikiliza hotuba ya kufunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika mkoani Morogoro kuanzia tarehe 28 hadi 30 Aprili, 2026. 
Posted by MROKI On Thursday, April 30, 2026 No comments

April 29, 2026









Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) leo tarehe 29.04.2026 imezindua awamu ya pili ya kupokea mawazo bunifu kutoka kwa Umma katika kuongeza wigo wa kodi na kuboresha huduma za kodi nchini.

Akizindua awamu hiyo ya pili ya kupokea mawazo bunifu kutoka kwa Umma katika kuongeza wigo wa kodi na kuboresha huduma  jijini Dar es Salaam, Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda amesema lengo la kuwashirikisha wananchi kutoa mawazo yao ni kutaka maboresho yanayofanywa na TRA pamoja na ubunifu utokane na wananchi wenyewe.

Amesema TRA ni chombo cha wananchi kinachokusanya kodi kwa wananchi kwaajili ya wananchi hivyo ni hatua muhimu kuwashirikisha kutoa mawazo yao ya ubunifu ikiwa ni awamu ya pili huku awamu ya kwanza ikitajwa kuwaibua wabunifu 9 kati ya 106 waliofika kwenye hatua ya pili kutoka wabunifu 5,681 waliowasilishq mawazo yao.

Kamishna Mkuu Mwenda amesema awamu ya pili ya Tuzo imeboreshwa kwa kiasi kikubwa kwa kuweka Kamati huru itayoratibu kazi zote zitakazotumwa na waombaji ambayo haihusishi watumishi wa TRA huku zawadi zitakazotolewa nazo zikiwa zimeboreshwa.

Amesema mshindi wa kwanza atajipatia Sh. Milioni 50, washindi wawili wa Pili watapata milioni 30 kila mmoja, washindi wa nafasi ya tatu wawili watapata Sh. Milioni 20 kila mmoja huku washindi wengine 15 wakipatiwa Sh. Milioni 10 kila mmoja ambapo washiriki ambao wazo lao litafika hatua ya pili watapatiwa Sh. Laki moja kwa kila mmoja wao.

Kukusu maeneo ya kipaumbele yatakayozingatiwa kwenye bunifu hizo amesema miongoni mwake ni Upanuzi wa wigo wa kodi hususan katika sekta isiyo rasmi, urahisishaji wa ukadiriaji na ulipaji wa kodi kwa wafanyabiashara wadogo, Maboresho ya huduma za Kidijitali, Maboresho ya utatuzi wa migogoro ya kikodi na matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa kodi. 

Kamishna Mkuu Mwenda amewahakikishia wote wanaotarajia kuwasilisha mawazo yao ya ubunifu kuwa matarajio yao yatafikiwa hivyo wajitokeze kwa wingi kutuma mawazo bunifu.

Awali akimkaribisha Kamishna Mkuu, Naibu Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Mcha Hassan Mcha mawazo bunifu yatakayotolewa yanatarajiwa kuongeza ufanisi katika masuala ya kodi na kutatua baadhi ya changamoto ikizingatiwa kuwa changamoto za kodi zinahitaji ushirikishwaji na matumizi ya teknolojia katika utatuzi wake.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utafiti na Mipango Dkt. Ephraim Mdee amesema awamu hii  wamefanya Maboresho makubwa kwa vigezo na zawadi zinazotolewa na hiyo ni baada ya kupata uzoefu katika awamu ya kwanza sambamba na maoni ya wadau mbalimbali. 
Posted by MROKI On Wednesday, April 29, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo