Nafasi Ya Matangazo

February 20, 2026








Na Mwandishi Wetu,
 Morogoro
Elimu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia imeendelea kuwafikia wananchi katika soko la Mahindi na vijiwe vya bodaboda waliopo Mikese Morogoro  lengo likiwa ni kuhakikisha watu wanaachana na matumizi ya nishati isiyo safi ya kupikia kama vile kuni na mkaa.

Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF) inaendelea na  kampeni endelevu ya nishati safi ya kupikia  ambapo tarehe 19 Februari 2026 kampeni hiyo iliwafikia wananchi katika Kata ya Mikese, wilaya ya Morogoro vijijini.

 Timu ya uhamasishaji imekuwa ikizungumza na wananchi na wafanyabiashara ili kubaini nishati wanayotumia na kuwapatia elimu ya umuhimu wa kuhamia katika nishati safi.

Baadhi ya wananchi wameeleza kuwa wanahitaji kutumia gesi zaidi wanapopika hivyo wameomba Serikali kuweka gharama rafiki  za ununuzi wa nishati hiyo.
Posted by MROKI On Friday, February 20, 2026 No comments





Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imefanya Ziara yake leo kwa kutembelea miradi ya umeme na imeipongeza Serikali ya Mhe. Samia Suluhu Hassan, uongozi na wafanyakazi wa TANESCO kwa kazi na hali ya uzalishaji wa umeme, ambapo sasa nchi ina uwezo wa kuzalisha jumla ya megawati 4,400.

Kwenye Ziara hiyo iliyofanyika Februari 20,2026  ambapo ilitembelea Kituo cha Kusafirisha Umeme kwenda Zanzibar cha Ras Kilomoni na Kituo cha kuzalisha Umeme kwa Gesi Asilia cha Kinyerezi I na II.

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, amesema kumekuwa na maendeleo makubwa katika eneo la uzalishaji wa umeme, na sasa TANESCO inaendelea na jitihada za kujenga njia za kusafirisha umeme, ikiwemo ya kutoka bwawa la Julius Nyerere hadi Chalinze, kisha Kinyerezi hadi Mkuranga, eneo lenye viwanda vingi vya uzalishaji.

“Tunaipongeza sana TANESCO kwa utekelezaji wa miradi ya umeme. Ile hali ya kukatika kwa umeme imepungua, na sasa hakuna mgao. Kamati inashauri kuwa nguvu kubwa sasa itumike katika kuhakikisha umeme unamfikia mlaji wa mwisho, hususani katika maeneo ya viwanda na migodi,” alifafanua Mhe. Subira.

Naye Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, kwa niaba ya Katibu Mkuu, Mhe. Innocent Luoga, amesema wamepokea maagizo ya Kamati kuhusu maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2030 nchi iweze kuzalisha jumla ya megawati 8,000.

“Hivi sasa mahitaji ya umeme yameendelea kuongezeka, hasa katika shughuli za uzalishaji. Serikali kupitia TANESCO, inahakikisha umeme unawafikia wananchi, na lengo ni kuwaunganishia umeme takribani wananchi milioni 1.7 kwa mwaka.”

Kwenye ziara hii Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeahidi kutoa ushirikiano wa hali ya juu ili kuweza kufikia malengo na mipango inayotekelezwa hapo mbeleni.






Posted by MROKI On Friday, February 20, 2026 No comments



Watendaji katika Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) wametakiwa kutekeleza kwa vitendo maelekezo ya Viongozi Wakuu wa Kitaifa yanayolenga kuendeleza sekta ya mafuta na gesi asilia, ikiwemo agizo la kuhakikisha mazungumzo ya Mradi wa Kuchakata Gesi kuwa Kimiminika (LNG) yanakamilika kwa wakati ili utekelezaji wake uanze.

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema hayo tarehe 20 Februari, 2026 jijini Mwanza wakati akifunga kikao kazi cha menejimenti ya TPDC kilicholenga kujadili mipango na bajeti ya Shirika kwa mwaka 2026/2027 pamoja na kufanya tathmini ya utendaji kazi wa Shirika.

“Maelekezo mengine yaliyotolewa ni pamoja na kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2030 ujenzi wa Bomba la Kusafirisha Gesi Asilia kutoka Kinyerezi hadi Chalinze unakamilika, pamoja na kuharakisha ujenzi wa vituo vya Gesi Asilia Iliyoshindiliwa (CNG) katika mikoa ya Morogoro na Dodoma. Haya ni maelekezo ya kimkakati yanayohitaji mshikamano, umakini na kasi ya utekelezaji kutoka TPDC na wadau wake, na utekelezaji wa maelekezo haya utafanyiwa tathmini,” amesema Mhe. Salome.

Aidha, Mhe. Salome amelitaka Shirika hilo kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa mafuta ya kutosha, ikiwemo kwa kujenga miundombinu ya hifadhi ya mafuta, kuimarisha shughuli za utafutaji, uzalishaji na usambazaji wa gesi asilia viwandani, kwenye taasisi, majumbani na kwenye magari, pamoja na kukamilisha miradi ya kimkakati ukiwemo wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

Kuhusu utekelezaji wa Ajenda ya Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia, Mhe. Salome amepongeza jitihada za TPDC katika miradi ya usambazaji wa gesi asilia kama nishati safi ya kupikia katika mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na Dar es Salaam, na kulitaka Shirika hilo kuongeza kasi ili kufikia mikoa mingine.

Vilevile ameipongeza TPDC kwa mchango wake katika kuchochea matumizi ya CNG na hivyo kupunguza foleni katika vituo vya kujaza gesi kwenye magari. Amesema juhudi za TPDC pia zimeonekana kupitia ujenzi wa kituo mama cha CNG katika Barabara ya Sam Nujoma, Dar es Salaam, ambacho kinaendelea kuchochea wawekezaji binafsi kuanzisha vituo vyao kutokana na uhakika wa upatikanaji wa gesi. Pia amepongeza utoaji wa idhini kwa kampuni binafsi kuwekeza katika biashara ya CNG.

Katika hatua nyingine, TPDC pia imetakiwa kutokubaki nyuma katika matumizi ya teknolojia na mageuzi ya kidijitali, ikiwemo matumizi ya Akili Mnemba (Artificial Intelligence – AI), mifumo ya kidijitali na uchambuzi wa takwimu kwani Serikali inatarajia TPDC ijipambanue kidijitali ili kurahisisha utoaji wa huduma, kupunguza urasimu, kuongeza uwazi katika manunuzi, kupunguza gharama za uendeshaji na kuongeza faida.

“Jambo jingine kubwa kwenu TPDC, mnapaswa wakati wote mjiridhishe kuhusu ushirikishwaji wa wazawa kwa kuhakiki uhalali wa kampuni za wazawa, si kwa usajili tu hapa nchini bali kwa uhalisia wa umiliki wa kampuni hizo. Nasisitiza pia umuhimu wa uwajibikaji kwa jamii (CSR), kwani miradi ya mafuta na gesi inapaswa kuleta manufaa yanayoonekana kwa jamii zinazozunguka maeneo ya miradi. Tayari mmeanza kufanya vizuri katika eneo hili, lakini mnapaswa kuongeza juhudi,” amesema Mhe. Salome.

Naye, mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Mafuta na Gesi Asilia), Mhandisi Antelimi Raphael  ameipongeza TPDC kwa kikao hicho cha kujitathmini, akisema ni hatua muhimu katika kuendeleza Shirika.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mussa Makame, alisema kikao hicho kililenga kujadili mipango na bajeti ya Shirika kwa mwaka 2026/2027. Pia kililenga kufanya tathmini ya utendaji kazi ili kubaini changamoto na kuzitatua, hivyo kuiwezesha miradi kuendelea kwa kasi iliyokusudiwa.

Kikao hicho pia kilienda sambamba na mafunzo mbalimbali ikiwemo ya uongozi.



Posted by MROKI On Friday, February 20, 2026 No comments







Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde leo Februari 20, 2026 ameongoza kikao cha kutatua Mgogoro kati ya Wachimbaji Wadogo wa duara No 15 na Uongozi wa Mgodi wa ILILIKA uliopo Nyarugusu Mkoani Geita. 

Baada ya kusikiliza pande zote mbili kupitia wawakilishi wao, Waziri Mavunde  amesema ili kufikia muafaka wa mgogoro huo na kuhakikisha haki inapatikana, ameelekeza kupimwa kwa sampuli ya mawe yanayolalamikiwa na pia kutaka uwepo wa mashahidi wengi zaidi wa pande zote ili kupata taarifa sahihi kisha kuendeleza kikao hicho ili haki ipatikane pale inapostahili.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Katibu Mtendaji Tume ya Madini Mhandisi Ramadhan Lwamo, Afisa Madini Mkazi Geita Mkoa Wa Geita  Samweli Shoo,  Msimamizi wa Mgodi wa Ililika Bi. Salma Mipawa pamoja na wachimbaji waki wakilishwa na Bw. Geofrey Mushi.
Posted by MROKI On Friday, February 20, 2026 No comments



 

Posted by MROKI On Friday, February 20, 2026 No comments


 

Posted by MROKI On Friday, February 20, 2026 No comments



⚫Ni za wakulima wa kahawa AMCOS ya Mwika Kinyamvuo

⚫Akagua ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amemuagiza Mrajisi wa Vyama vya Ushirika mkoa wa Kilimanjaro ahakikishe Chama cha Ushirika Mkoa wa Kilimanjaro (KNCU) kinalipa kwa mkupuo mmoja sh. milioni 400 ambazo chama hicho kinadaiwa na wakulima.

Ametoa agizo hilo leo (Ijumaa, Februari 20, 2026) aliposimama kusalimia wananchi katika eneo la Chekereni ambapo mkazi wa eneo hilo, Bi. Glory Sam kutoka Chama cha Mwika Kinyamvuo AMCOS alieleza malalamiko yake mbele ya Waziri Mkuu akitaja kusikitishwa na KNCU kuuza kahawa yao msimu wa mwaka 2021/2022 lakini hadi sasa hawajalipwa.

“Tuliuza kahawa yetu kwa zaidi ya shilingi milioni 600 lakini mpaka sasa tumelipwa shilingi milioni 200 pekee. Kwa kipindi chote hicho tumekuwa tukidai milioni 400 bila mafanikio.”

Dkt. Mwigulu amemtaka Mrajis ahakikishe kuwa hadi kufikia tarehe 25 Februari, 2026 Bodi hiyo iwe imekaa kikao na iamue ni mali gani zinauzwa ili kuweza kuwalipa kwa mkupuo wakulima hao.

“Tafuta kimojawapo kiuzwe, shilingi milioni 400 ipatikane na hawa watu walipwe mara moja.  Hatuwezi kukaa na jambo moja miaka yote, kama kuna chama hakiwezi kulipa watu mnakaa nacho cha nini? Wananchi wanaumia, tabia ya kuzoea shida, matatizo na machozi ya watu hatuwezi kuivumilia.”

“Jambo limekaa miaka mitano mnataka likae miaka mingapi, upuuzi huu sitaki kusikiliza mnalipa lini? Jumatano ijayo mkae mtoke na majibu, tafuteni mtakachouza muwalipe watu pesa zao,” amesisitiza.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amekagua mradi wa ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi inayojengwa katika Kata ya Ng’ambo kwenye manispaa hiyo.

Mradi huo ambao hadi kukamilika kwake unatarajiwa kugharimu sh. bilioni 6.59, hadi sasa ujenzi wake umefikia asilimia 55 ya katika majengo ya huduma za wagonjwa wa nje, huduma za mama na mtoto kwa miundombinu ya sakafu ya chini na ya kwanza.
Posted by MROKI On Friday, February 20, 2026 No comments



WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewaagiza watendaji wanaosimamia sekta ya elimu kuanzia sasa waanze kujenga shule zitakazokidhi mahitaji ya mtaala mpya wa elimu ifikapo mwaka 2028.

“Tulikuwa na vikao hivi karibuni, niliagiza ujenzi wa shule za sekondari nchini kuanzia sasa hivi uzingatie kuna madarasa 10 na shule zinapoenda kujengwa pawe na eneo la kutosha kujenga yote 10 au tuamue kujenga madarasa matatu kwenye yale saba yaliyokuwepo,” amesema.

Ametoa agizo hilo leo (Ijumaa, Februari 20, 2026) wakati akizungumza na wananchi wa Mabogini mara baada ya kukagua ujenzi wa barabara ya Spencon - Mabogini - Kahe hadi Chekereni wilayani Moshi, mkoani Kilimanjaro. Alikuwa akijibu ombi la Mbunge wa Moshi Vijijini, Morris Makoi ambaye aliomba kata hiyo ipatiwe sekondari.

Amesema mabadiliko ya mtaala wa elimu yanajumuisha miaka sita ya elimu ya msingi na miaka minne ya elimu ya sekondari. “Zamani tulizoea kusema kila kata iwe na shule ya sekondari lakini tuendako sasa itabidi kila kijiji kiwe na shule ya sekondari ili kumudu mahitaji hayo mapya.”

“Kama tuna bajeti ya kujenga majengo ya elimu, tuanze kuzingatia mitaala mipya. Kati ya mwaka 2026 na 2027, tunapaswa kuongeza madarasa 39,000 kwa maana kwamba tuna vijiji 13,000 na kila shule moja ya msingi itabidi iongezwe madarasa matatu.”

"Tunaposema kuanzia mwaka kesho, mwaka kesho wa bajeti hauko mbali. Ni miezi minne ijayo sababu mwaka mpya wa fedha unaanza Julai, mwaka huu. Na mwaka kesho, darasa la sita na la saba wataunganishwa na kufanya mtihani mmoja ili kujiandaa kuanza elimu ya lazima,” amesema.

Mapema, akielezea hoja kuhusu ujenzi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 31.25, Dkt. Mwigulu aliwaelekeza viongozi wa mkoa na wilaya wafuate utaratibu wa kuomba barabara hiyo ipandishwe hadi kutoka TARURA na kwenda TANROADS ili ijengwe kwa kiwango cha lami. 

RC na DC, TARURA na TANROADS fanyeni mchakato wa kuipandisha hadhi ya TANROADS ili ijengwe kw amara moja. Kwa muundo wake, barabara hii ni Bypass, kwa hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza msongamano katikati ya mji wa Moshi na pia itasaidia kutoa huku mazao ya wakulima.”

Barabara ya Spencon - Mabogini - Kahe hadi Chekereni inapita katikati ya vijiji 12 ambavyo ni Mabogini, Chekereni, Mtakuja, Oria, Miwaleni, Kahe, Mwangaria, Ngasini, Ngasini B, Soko, Kyomu na Gona. 
 
Kwa mujibu wa taarifa ya ujenzi iliyosomwa mbele ya Waziri Mkuu, barabara hiyo ambayo itagharimu sh. bilioni 7.2, iko chini ya mtandao wa barabara wa TARURA Wilaya ya Moshi na inapita katika majimbo matatu ya Moshi Manispaa, Moshi Vijijini na Vunjo. Aidha, inapita katika kata tatu za Kahe Magharibi, Kahe Mashariki na Mabogini. 

Ujenzi wa barabara hiyo utasaidia kuimarisha shughuli za usafiri na usafirishaji na kuchochea uchumi kwenye maeneo yaliyo pembezoni mwa barabara hii kutokana na uwepo wa maeneo ya kilimo cha mpunga na mbogamboga. 
Posted by MROKI On Friday, February 20, 2026 No comments

Mwadhama Polycarp Cardinal Pengo 
 

Posted by MROKI On Friday, February 20, 2026 No comments

February 19, 2026

Na.Sophia Kingimali.
Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Immaculate Semesi, amesema taasisi hiyo imepokea maabara tembezi ya kisasa yenye thamani ya Sh. milioni 715 itakayosaidia kuimarisha usimamizi na utekelezaji wa Sheria ya Mazingira nchini. 

Akizungumza leo Februari 19,2026 jijini Dar es salaam wakati wa makabidhiano ya gari hilo, Dkt. Semesi amesema mradi huo ulioanza mwaka 2020 na unaotarajiwa kukamilika Juni mwaka huu, 

"Mradi huu umewezesha upatikanaji wa miundombinu muhimu ikiwemo maabara hiyo inayotoa majibu ya papo kwa papo (real time) wakati wa ukaguzi wa mazingira,hivyo kifaa hicho kitapima viwango vya kelele, mitetemo, ubora wa maji, hali ya hewa, udongo pamoja na metali nzito kama zebaki, hivyo kurahisisha utoaji wa maamuzi ya haraka dhidi ya vitendo vya uchafuzi wa mazingira",Amesema Dkt Semesi.

Aidha Dkt. Semesi, ameongeza kuwa matumizi ya maabara hayo yatapunguza gharama na muda uliokuwa ukitumika kusafirisha sampuli kwenda maabara nyingine zilizoidhinishwa, ambapo gharama ya kipimo kimoja ilikuwa inaweza kufikia kati ya Sh milioni 5 hadi 10 kulingana na aina ya sampuli amesema kwa sasa NEMC itaweza kufanya uchunguzi ndani ya muda mfupi na kuchukua hatua stahiki mara moja, hali itakayoongeza ufanisi katika kulinda mazingira.

Aidha, amesema baraza lina kanda 13 nchini na matarajio ni kupata angalau magari 12 zaidi ya maabara tembezi ili kuimarisha huduma katika mikoa yote na kuhakikisha ukaguzi unafanyika kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi huo, Paul Kalokola, amesema maabara hiyo pia ina vifaa vya kisasa ikiwemo droni kwa ajili ya kufikia maeneo magumu na yaliyofichika, hatua itakayowezesha upimaji wa kisayansi kufanyika popote nchini na kusaidia maamuzi yanayotegemea ushahidi wa kitaalamu.

Naye Meneja wa Programu za Mazingira na Hali ya Hewa kutoka Ubalozi wa Sweden, Stephen Mwakifwamba, amesema jumla ya mradi huo ulikuwa na thamani ya dola milioni tatu za Marekani na ulijumuisha pia uboreshaji wa sheria na kanuni za mazingira pamoja na kuzitafsiri kwa Kiswahili ili ziweze kueleweka kwa wananchi hivyo ameishauri NEMC kuhakikisha vifaa hivyo vinatunzwa na kufanyiwa matengenezo ya mara kwa mara ili viweze kudumu na kutoa huduma kwa muda mrefu.

Serikali ya Sweden imeahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuimarisha uhifadhi wa mazingira kwa maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi.

Maabara hiyo imenunuliwa kupitia mradi wa miaka mitatu uliofadhiliwa na Serikali ya Sweden kupitia Shirika la Maendeleo la Sweden (Sida), uliolenga kujenga uwezo wa taasisi za serikali na binafsi katika kusimamia mazingira.

Posted by MROKI On Thursday, February 19, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo