Nafasi Ya Matangazo

April 26, 2026




Mkurugenzi wa Milki  Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Upendo Matotola, ameibuka mshindi miongoni mwa washindi wa Tuzo ya WIMA (Women in Management Africa) kwa mwaka 2026, kutokana na mchango wake mkubwa katika kukuza na kuimarisha sekta ya milki nchini.

Tuzo hiyo ni ushahidi wa uongozi wake mahiri, unaodhihirishwa na kujitolea kwake kuimarisha utendaji wa sekta ya milki pamoja na kuleta mabadiliko chanya yenye tija kwa jamii.

Mafanikio haya yanaakisi si tu ubora wake kitaaluma, bali pia mchango wake katika kusukuma mbele maono ya Afrika yenye ushirikishwaji mpana na maendeleo endelevu.

Dkt. Upendo alikabidhiwa tuzo hiyo mwishoni mwa wiki katika hafla maalum ya kuwapongeza na kuwatunza wanawake viongozi waliofanya vizuri katika nyanja mbalimbali za uongozi barani Afrika. Hafla hiyo iliendeshwa chini ya kaulimbiu isemayo, “Alama, uongozi na matokeo endelevu.”

Women in Management Africa (WIMA)ni taasisi ya bara la Afrika inayojikita katika kutambua, kusherehekea na kukuza wanawake viongozi bora wanaochangia mabadiliko ya sekta mbalimbali, kuboresha maisha ya jamii, na kuendeleza ukuaji wa Afrika katika ngazi ya kimataifa.
Posted by MROKI On Sunday, April 26, 2026 No comments

April 25, 2026





Na Mwandishi Wetu, Kahama
Serikali kupitia Tume ya Madini imesema itaendelea kutoa bei elekezi za madini ya dhahabu, shaba na fedha kila siku itakayotumika kwenye masoko na vituo vya ununuzi wa madini hatua inayolenga kuongeza uwazi katika biashara ya madini na kuwawezesha wachimbaji kuuza madini yao kwa bei halisi ya soko la dunia.

Akifunga mafunzo kwa Mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga mapema jana, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini, CPA Venance Kasiki alisema taarifa hizo za bei zitawasaidia wachimbaji kufanya maamuzi sahihi ya biashara na kuepuka hasara zitokanazo na madalali maarufu kama vishoka.

Alisema hapo awali baadhi ya wachimbaji walikuwa wakiuza madini bila kufahamu bei halisi ya soko la dunia, hali iliyosababisha kupoteza mapato na kuingia katika mikataba isiyo na manufaa. 

Alifafanua kuwa kwa sasa bei za madini hutolewa kila siku, hivyo mchimbaji ana uwezo wa kufanya uamuzi sahihi kabla ya kuuza madini yake.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kuimarisha mifumo ya uwazi katika biashara ya madini pamoja na kuwahamasisha wananchi kutoa taarifa za vitendo vya utoroshaji wa madini, ambapo watoa taarifa watapatiwa zawadi maalum.

CPA Kasiki alionya kuwa watakaobainika kujihusisha na utoroshaji wa madini watakabiliwa na hatua kali za kisheria ikiwemo kufunguliwa mashitaka, kutaifishwa madini, kulipa faini pamoja na kifungo kwa mujibu wa sheria.

Katika hatua nyingine, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia usalama migodini, akibainisha kuwa uchimbaji usiofuata taratibu hauwezi kuwa endelevu, huku akisisitiza kuwa uhai wa binadamu una thamani kubwa kuliko madini. 

Aliwahimiza wachimbaji kutumia maabara ya Tume ya Madini katika kupima sampuli ili kufanya maamuzi sahihi badala ya kutumia maabara zisizotambulika. 

Aidha, aliwakumbusha wamiliki wa leseni kufanya miradi endelevu kwa jamii zinazozunguka migodi ikiwa ni utekelezaji wa takwa la Kisheria la wajibu wa mwenye leseni kwa jamii (CSR).

Awali, Mkurugenzi  wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira, Mhandisi Hamisi Kamando alisema mwitikio wa washiriki ulikuwa mkubwa ambapo kati ya washiriki 400 waliotarajiwa, washiriki 370 walijitokeza, jambo linaloonesha hamasa kubwa ya wachimbaji kujifunza masuala ya usalama, afya na utunzaji wa mazingira.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa SHIREMA, Hamza Tandiko alisema mafunzo hayo yameongeza uelewa wa wachimbaji katika biashara ya madini, matumizi salama ya kemikali na baruti, uhifadhi wa mazingira pamoja na uchunguzi wa ajali migodini, akisisitiza umuhimu wa kuachana na uchimbaji wa kubahatisha na kuingia katika uchimbaji wa kisasa na wenye tija.
Posted by MROKI On Saturday, April 25, 2026 No comments

April 24, 2026







Na Mwandishi wetu, Kahama
Serikali imewataka Wakaguzi Wakuu wa Migodi pamoja na Mameneja wa Migodi nchini kuwa mabalozi wa utekelezaji wa sheria, kanuni za madini na kuwa wazalendo katika biashara ya madini ili kuongeza mchango wa sekta hiyo kwenye uchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa leo Aprili 24, 2026 wilayani Kahama, mkoani Shinyanga na Mtaalam kutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Biashara ya Madini – Tume ya Madini, Mhandisi Erasmina Massawe, kwenye mafunzo kwa Mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo yaliyowakutanisha washiriki kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga.

Mafunzo hayo yamelenga kuimarisha uelewa wa kitaalam, usimamizi bora wa migodi, uzingatiaji wa sheria na kanuni za madini pamoja na kukuza uchimbaji salama na endelevu.

Amesema mbali na kujifunza mbinu za kuimarisha usalama migodini, viongozi hao wanapaswa kuwa sehemu ya mikakati ya Serikali ya kuhakikisha biashara ya madini inafanyika kwa uwazi na kwa kuzingatia Sheria ya Madini na kanuni zake, hatua itakayosaidia kudhibiti vitendo vya utoroshaji wa madini.

Ameeleza kuwa Serikali kupitia Tume ya Madini imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha usimamizi wa biashara ya madini, ikiwemo uboreshaji wa mfumo wa biashara ya madini, uanzishwaji wa masoko na vituo vya ununuzi wa madini, uwepo wa Maafisa Migodi Wakazi katika maeneo ya uchimbaji pamoja na ujenzi wa ukuta wa Mirerani uliosaidia kudhibiti utoroshaji wa madini ya Tanzanite.

Aidha, amesema Serikali imeimarisha ulinzi na ufuatiliaji wa madini kwa kuweka wakaguzi katika maeneo muhimu kama viwanja vya ndege, bandari, mipakani na katika maeneo yote ya uzalishaji madini, sambamba na kusimamia utoaji wa vibali vya usafirishaji wa madini na utekelezaji wa Sheria ya kodi ikiwemo ondoleo la Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye baadhi ya shughuli za madini.

Akizungumzia uwezeshaji wa Watanzania kushiriki kikamilifu katika sekta hiyo, Mhandisi Massawe amesema maboresho ya Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini yameongeza kwa kiasi kikubwa ushiriki wa watanzania katika usambazaji wa bidhaa na  utoaji wa huduma mbalimbali migodini.

“Kwa sasa zipo fursa nyingi katika Sekta ya Madini ikiwemo huduma za chakula, ulinzi, vifaa kinga, huduma za kisheria, ujenzi na bima. Watanzania wanapaswa kuzitumia fursa hizi kujiongezea kipato na kukuza uchumi wa nchi,” amesisitiza.

Wakati huohuo amehimiza wadau wa madini nchini kutumia maabara bora ya Tume ya Madini iliyopo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kupimiwa madini yao na sampluli za madini ili kufanya biashara ya madini ya uhakika.

Mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za Serikali kuimarisha usimamizi wa uchimbaji mdogo na kuhakikisha rasilimali za madini zinaleta manufaa mapana kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.
Posted by MROKI On Friday, April 24, 2026 No comments

April 23, 2026










Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Imeelezwa kwamba Serikali kupitia Wizara ya Madini na Taasisi zake itaendelea kuwawezesha kwa kuwajengea uwezo  wanawake, vijana na watu wenye uhitaji maalum kwa kuwapatia  vifaa vya uchimbaji , mitambo ya uchorongaji miamba na kuwapatia maeneo ya leseni yaliyofanyiwa utafiti wa kina ili kuwaendeleza na uchimbaji bora na wenye tija bila kupoteza mitaji na muda.

Rai hiyo imetolewa leo Aprili 23, 2026 na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati akikabidhi  Pampu 10 za kutolea maji mgodini kwa Chama cha Wanawake wachimbaji Madini Tanzania (TAWOMA) kwenye Kongamano la fursa na mageuzi kwa wanawake katika  sekta ya madini nchini liliofanyika jijini Dodoma.

Waziri Mavunde amesema kwamba, kupitia Program wezeshi ya _Mining For A Brighter Tommorrow_ (MBT), itaendelea kuwawezesha wanakimama na vijana kwa kuwapatia leseni  zilizofanyiwa utafiti wa kina wa jiosayansi na mitambo ya kusaga mawe ili kuendelea kuwawezesha kuchimba kwa tija na uhakika.

Waziri Mavunde amesema kuwa, mpaka sasa wachimbaji wadogo wanachangia asilimia 40 katika makusanyo kwenye sekta ya madini ambayo ni mpaka mwezi April trilioni 1.1 

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) Dkt.Venance Mwase amesema , STAMICO itaendelea kuwawezesha wachimbaji wadogo katika makundi yote kwa kuwapatia mashine , 
kuwafanyia utafiti  lengo ni kufikia Dira ya 2030  inayosema Madini ni Maisha na Utajiri.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa TAWOMA Bi.Semeni Malale ameeleza kuwa kupitia mradi wa kimkakati wa Malkia wa Madini unaendelea kuwaunganisha wanawake na vijana nchini kwa kufungua fursa za uwezeshaji katika mikoa mbalimbali hususan katika suluhisho la kuongeza tija na kipato.

Malale ameongeza kuwa 
mpaka sasa mradi wa malkia wa madini umefanikiwa kuwaendeleza  kiuchumi wanawake 7000 katika mikoa 21 na vijana 120.

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Jabiri Shekimweri akimwakilisha Mkuu wa Mkoa ameipongeza  TAWOMA kwa kuwaingiza vijana wengi katika mnyororo wa thamani madini ambapo kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 ilionyesha idadi ya vijana katika taifa  kuwa na  asilimia 21 ya wakazi wote.

Washiriki wengine katika kongamano hilo ni pamoja na Tume ya Madini,Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) Benki ya CRDB, Azani , GF Truck.
Posted by MROKI On Thursday, April 23, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Kahama
Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuwawezesha Wakaguzi Wakuu wa Migodi pamoja na wachimbaji wadogo nchini ili kuimarisha usalama kazini, kulinda mazingira na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Wito huo umetolewa leo Aprili 23, 2026 wilayani Kahama, mkoani Shinyanga na Mkurugenzi wa Huduma za Leseni wa Tume ya Madini, Mhandisi Aziza Swedi, alipokuwa akifungua mafunzo kwa mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo.

Mafunzo hayo yanawakutanisha washiriki kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga yakilenga kuimarisha uelewa wa kitaalam, usimamizi bora wa migodi, uzingatiaji wa sheria na kanuni pamoja na kukuza uchimbaji salama na endelevu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Mhandisi Swedi amesema Wakaguzi Wakuu wa Migodi wanapaswa kupewa ushirikiano na mazingira wezeshi ili waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu, hatua itakayosaidia kuzuia ajali migodini, kulinda afya za wachimbaji na kuhifadhi mazingira yanayozunguka maeneo ya uchimbaji.

Amesema mafanikio ya jitihada za Serikali katika kuwawezesha wachimbaji wadogo yanategemea ushirikiano wa wadau wote, hususan mameneja na wakaguzi wa migodi ambao ni nguzo muhimu katika kusimamia uzingatiaji wa sheria, kanuni na viwango vya usalama.

“Serikali inalenga kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinaendelea kuchangia maendeleo ya Taifa huku zikifanyika kwa njia salama zisizoathiri mazingira, afya za wachimbaji na ustawi wa jamii,” amesema.

Aidha, amesema kupitia usimamizi madhubuti, nchi inaweza kufikia azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuongeza mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa kutoka asilimia 10 ya sasa hadi asilimia 12.5 ifikapo mwaka 2030.

Ameeleza kuwa wachimbaji wadogo tayari wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato yatokanayo na shughuli za madini, hali inayoonesha umuhimu wao katika uchumi wa Taifa, huku akiwataka wamiliki wa migodi kuhakikisha taarifa za uzalishaji na kumbukumbu muhimu zinatunzwa ipasavyo ili Serikali ipate mapato stahiki kwa wakati.

Mhandisi Swedi pia ameonya kuhusu athari za uchimbaji usiozingatia taratibu, akitaja matumizi holela ya kemikali hatarishi kama zebaki na sayanaidi pamoja na vumbi la silica kuwa chanzo cha magonjwa hatari ikiwemo silicosis, kifua kikuu na saratani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kutoka Tume ya Madini, Mhandisi Hamisi Kamando, amesema Wakaguzi Wakuu wa Migodi wanapaswa kuwasilisha taarifa za ukaguzi mara kwa mara ili kuiwezesha Serikali kubaini mapema vihatarishi vinavyoweza kusababisha ajali na kuchukua hatua za kinga kwa wakati.

Amesema bado kuna changamoto katika baadhi ya maeneo ya migodi ikiwemo ukiukwaji wa sheria, ukosefu wa kumbukumbu sahihi za uzalishaji, ukwepaji wa kodi na utoroshaji wa madini, hivyo mafunzo hayo yanalenga kuwajengea washiriki uwezo wa kuwa mabalozi wa uzingatiaji wa sheria na taratibu za sekta hiyo.

“Tunataka kuona wachimbaji wanaingia migodini salama na kurejea majumbani mwao salama kila siku. Uhai wa binadamu una thamani kubwa kuliko madini,” amesema Mhandisi Kamando.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini Mkoa wa Shinyanga (SHIREMA), Hamza Tandiko, amesisitiza umuhimu wa weledi kwa wachimbaji na utoaji wa taarifa sahihi za shughuli za uchimbaji, huku akipongeza mchango wa wakaguzi katika kupunguza ajali na madhara migodini.






Posted by MROKI On Thursday, April 23, 2026 No comments



Na Mwandishi wetu, Dodoma
Wanawake nchini Tanzania wanaojishughulisha na mnyororo wa thamani madini wameshauriwa kufanya shughuli za madini katika mwamvuli mmoja utakaowatambulisha kulingana na huduma zitolewazo ndani ya Sekta ya Madini ikiwemo Uchimbaji, Uchenjuaji, Uongezaji thamani.

Rai hiyo imetolewa leo Aprili 22, 2026 na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati akizungumza na wanawake wanaojihusisha za shughuli za madini katika mnyororo mzima wa thamani madini nchini.

Waziri Mavunde amesema kuwa, ni wakati sasa wa kutengeneza jukwaa moja litakalobeba  vyama vyote ambapo itakuwa rahisi kuwafikia kwa pamoja na kwa wakati mmoja tofauti na ilivyosasa.

Waziri Mavunde amesema, katika nyanja ya uongezaji thamani madini ,  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan ametoa shilingi bilioni 30 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Kituo cha mafunzo ya  Uongezaji thamani madini (TGC) ambacho ni fursa kwa Wanawake walio katika mstari wa uongezaji thaman madini.

Aidha, Waziri Mavunde ameeleza kuwa, Mpango wa  Ushirikishwaji kwa Wazawa (Local Content) una fursa mbalimbali ambapo kila mwaka utengwa kiasi cha trilioni 5.1 kwa ajili ya manunuzi na huduma za migodini , hivyo kupitia jukwaa moja ndani ya vyama husika ni rahisi kuingia katika mnyororo huo.

Waziri Mavunde amefafanua kuwa kupitia Programu maalum ya (MBT) , inakuja na mpango maalum wa kuwawezesha Wanawake, Vijana na Watu wenye uhitaji maalum kwa kuwapatia leseni , vifaa na mashine na  kuwapatia mafunzo maalum ya  uchimbaji na uchenjuaji madini.

Pamoja na mambo mengine , Waziri amewapongeza wachimbaji wanawake na wachimbaji wadogo wote  kwa mchango wanatoa katika sekta ya madini, ambapo  umepelekea kuchangia  Pato la Taifa kwa asilimia 10.1.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini Wanawake Tanzania(TAWOMA) Semeni Malale ameipongeza Wizara ya Madini na taasisi zake kwa Juhudi mbalimbali inazofanya za kuwawezesha wachimbaji wanawake nchini.

Vyama vilivyoshiriki mkutano  huo ni pamoja na  TAWOMA, Chama cha Wanawake Wachimbaji Madini ya Viwanda (TWIMMI), Muungano wa  Wanawake wanaojihusisha na Uchimbaji Madini(WIMA) na Chama cha Wanawake Wachimbaji na Waongezaji thamani ya madini Tanzania (WIMO).







Posted by MROKI On Thursday, April 23, 2026 No comments
Posted by MROKI On Thursday, April 23, 2026 No comments

April 22, 2026

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius J. Ndejembi (Mb.), akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 22 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Serikali imesema itaendelea kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa mafuta nchini licha ya changamoto za kimataifa zinazoathiri mnyororo wa usambazaji wa nishati hiyo , ikiwemo vita inayoendelea katika Ukanda wa Mashariki ya Kati.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma wakati wa uwasilishaji wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/27 ,Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Deogratius Ndejembi, alisema kuwa Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa za mafuta ya petroli kwa uhakika.

“Sambamba na kuimarika kwa upatikanaji wa umeme, nchi yetu pia imeendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa bidhaa za mafuta ya petroli licha ya changamoto za kimataifa zilizotokana na vita baina ya Marekani, Israel na Iran,” alisema Mhe. Ndejembi.

Alifafanua kuwa vita hiyo imesababisha athari kubwa katika usambazaji wa mafuta duniani, ikiwemo kufungwa kwa Mlango Bahari wa Hormuz ambao hupitisha zaidi ya asilimia 20 ya mafuta yote duniani, pamoja na kuathiri miundombinu ya uzalishaji na uhifadhi wa mafuta.

“Hali hii imeathiri kwa kiasi kikubwa nchi za Mashariki ya Kati ambako Tanzania inaagiza takribani asilimia 59 ya mafuta yake, huku asilimia 41 ikitoka India ambayo nayo hutegemea mafuta ghafi kutoka ukanda huo huo,” aliongeza.

Kutokana na hali hiyo, Waziri Ndejembi alisema Serikali imechukua hatua za haraka na za kimkakati ili kulinda usalama wa nishati nchini. Moja ya hatua hizo ni kuliwezesha Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuagiza mafuta ya kutosha kwa kipindi cha miezi mitatu ijayo.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa soko la mafuta duniani na iko tayari kuchukua hatua zaidi kulingana na mabadiliko yatakayotokea.
Posted by MROKI On Wednesday, April 22, 2026 No comments






Dodoma
Serikali imeendelea kuimarisha usimamizi wa utekelezaji wa wajibu wa kampuni kwa jamii (Corporate Social Responsibility – CSR) katika Sekta ya Madini, kufuatia kuwepo kwa mfumo maalum wa kisheria uliowekwa kupitia Kanuni za CSR za mwaka 2023 zinazolenga kuongeza uwazi, uwajibikaji na ushirikiano miongoni mwa wadau.

Akifungua kikao kazi cha wataalam kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI (OWM-TAMISEMI) kilichofanyika leo Aprili 22, 2026 jijini Dodoma kwa lengo la kujadili masuala mtambuka ya utekelezaji wa CSR, Kamishna wa Tume ya Madini, Dkt. Theresia Numbi, amesema kanuni hizo zilibuniwa mahsusi kupunguza migogoro iliyokuwa ikijitokeza kati ya Serikali za Mitaa na wamiliki wa leseni za madini kuhusu utekelezaji wa miradi ya CSR.

Dkt. Numbi amesema kuwa pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2018 hadi 2025, bado kuna changamoto zinazoathiri utekelezaji wa kanuni hizo, zikiwemo matarajio makubwa ya jamii zinazozunguka migodi kulinganisha na uwezo wa wachimbaji, uelewa mdogo wa kanuni kwa baadhi ya wamiliki wa leseni, pamoja na mivutano ya wadau mbalimbali wakiwemo wanasiasa na watendaji wa halmashauri.

Amesema kuna umuhimu wa kuandaliwa kwa jukwaa pana la kitaifa litakalowakutanisha wadau wote ili kujadili mafanikio, changamoto na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha utekelezaji wa miradi ya CSR nchini.

“Jukwaa hilo litawakutanisha wamiliki wa leseni za madini, watendaji wa halmashauri, waratibu wa CSR wa mikoa, Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa, pamoja na wadau kutoka OWM-TAMISEMI na Wizara ya Fedha,” amesema Dkt. Numbi.

Amesisitiza kuwa madini ni rasilimali isiyorejea, hivyo usimamizi madhubuti wa miradi ya CSR ni muhimu ili kuhakikisha jamii zinazozunguka migodi zinapata manufaa stahiki na kuchangia maendeleo ya taifa.

“Tusipojipanga vizuri kama taasisi za Serikali kusimamia utekelezaji wa miradi ya CSR, jamii hazitanufaika ipasavyo na hatimaye taifa litapoteza fursa muhimu za maendeleo,” ameongeza.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Serikali za Mitaa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Alfao Sanga, amesema uwepo wa Kanuni na Miongozo ya CSR umeleta mafanikio makubwa katika uratibu wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenye halmashauri mbalimbali nchini.

Ameeleza kuwa kwa mwaka wa fedha 2025/2026, hadi kufikia mwezi Februari 2026, miradi ya CSR yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 28 ilikuwa imetekelezwa katika sekta mbalimbali, ambapo Sekta ya Madini pekee imechangia takribani Shilingi bilioni 19.7.

Amesema mafanikio hayo yanaonesha mchango mkubwa wa Sekta ya Madini katika maendeleo ya jamii na ustawi wa wananchi wanaoishi maeneo yanayozunguka shughuli za uchimbaji.
Posted by MROKI On Wednesday, April 22, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo