Nafasi Ya Matangazo

March 13, 2026










Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imelipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa usimamizi na utekelezaji mzuri wa Mradi wa Uzalishaji Umeme kwa nguvu ya Jua wa Kishapu wenye uwezo wa Megawati 50 unaotekelezwa katika Mkoa wa Shinyanga.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgallu, mara baada ya Kamati kutembelea mradi huo tarehe 13 Machi, 2026 kwa lengo la kujionea maendeleo ya utekelezaji wake pamoja na ufanisi wa matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Mhe. Mgallu alisema mradi huo ni hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya nishati nchini kutokana na matumizi ya teknolojia ya nishati jadidifu.

“Tumetembelea mradi huu wa uzalishaji wa umeme kwa kutumia teknolojia ya jua na tunaona ni mapinduzi makubwa katika sekta ya nishati nchini. Hii ni hatua muhimu kwani kwa mara ya kwanza Tanzania inapata Megawati 50 za umeme kutoka kwenye nishati ya jua,” alisema Mhe. Mgallu.

Alisema Kamati imeridhishwa na namna fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo zimetumika ipasavyo na kufanikisha utekelezaji wa mradi huo kwa ufanisi.

“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, tumeridhishwa na matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya mradi huu. Tunaona wazi kuwa fedha hizo zimetumika vizuri katika utekelezaji wa mradi huu wenye thamani ya takribani shilingi bilioni 118,” alieleza.

Aidha, alisema mradi huo tayari umeanza kuchangia Megawati 50 katika Mfumo wa Gridi ya Taifa, hatua inayochangia kuongeza uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini pamoja na kuimarisha vyanzo mseto vya nishati.

“Utekelezaji wa mradi huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kunakuwa na vyanzo mbalimbali vya kuzalisha umeme. Hii inaongeza uhakika wa upatikanaji wa nishati ya umeme nchini,” alisema.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, alisema mradi wa Kishapu unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme katika Gridi ya Taifa.

“Mradi huu una awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme kwenye Gridi ya Taifa. Awamu ya pili itahusisha uzalishaji wa Megawati 100 zaidi na kufanya jumla ya Megawati 150 kutoka katika mradi huu,” alisema Mhe. Ndejembi.

Kamati hiyo imetoa Rai kwa Wizara ya Nishati na TANESCO  inaendelea kuendelea na  mikakati ya kuanza utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo ili kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini.
Posted by MROKI On Friday, March 13, 2026 No comments

March 12, 2026











Na Mwandishi wetu, Tabora
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeridhishwa na Ujenzi wa Kiwanda cha Zege kinachomilikiwa na kampuni tanzu ya TANESCO ya  kuzalisha nguzo za zege  kilichopo katika Mkoa wa Tabora wakati wa ziara yao ya kikazi Mkoani humo tarehe 12 Machi, 2026.

Akizungumza baada ya ziara hiyo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu ameeleza kuridhishwa na   hatua ya kukamilika kwa Kiwanda hicho kilichoanza uzalishaji  na kuwaelekeza Wizara ya Nishati  na TANESCO kukisimamia kiwanda hiko kiendelee kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kuzalisha faida.

"Kwa niaba ya Kamati tumeridhika na kazi kubwa iliyofanyika katika kiwanda hiki ambacho kimekamilika na uzalishaji umeanza, tunatoa rai kwa Wizara na TANESCO kuendelea kusimamia kiwanda hiki ili kiendelee kufanya kazi yake kwa ufanisi zaidi", alieleza Mhe. Mgallu

Alieleza kuwa uelekeo wa sasa ni kusambaza nguzo za zege hasa kwa maeneo yenye unyevu sambamba na maeneo yaliyo karibu na misitu pamoja na mikondo ya mito ya maji ambayo nguzo za miti huathirika kwa kiasi kikubwa haswa kwenye msimu wa mvua hivyo nguzo za zege zitakuwa msaada mkubwa katika mazingira kama hayo na  kuboresha upatikanaji wa huduma ya umeme.

“Kama mnavyofayahamu kwa sasa uelekeo ni kusambaza nguzo za zege badala ya nguzo za miti hasa katika maeneo ambayo yana asili ya unyevu, maeneo karibu na mito ya maji ama visiwa ambapo nguzo za miti huathiriwa na mazingira hayo”, aliongeza. 

Naye Mhe. Deogratius Ndejembi Waziri wa Nishati alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hiko umekamilika mwaka huu na kuanza uzalishaji wake rasmi Februari, 2026 ambapo mpaka sasa wastani wa nguzo zinazozalishwa ni 80 hadi 120 kwa siku ambapo mpaka sasa gharama ya shilingi bilioni 6.4 imeshatumika katika hatua zote hadi uzalishaji ulipoanza ambapo kiasi cha shilingi bilioni 1.4 bado hazijalipwa kwa mkandarasi ambaye bado yupo kwenye kipindi cha uangalizi.

“Kiwanda hiki kilianza uzalishaji rasmi mwezi Februari mwaka huu ambapo kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha nguzo 80 hadi 120, mpaka sasa ujenzi wa kiwanda hiki hadi uzalishaji ulipoanza imetumia gharama ya shilingi bilioni 6.4 ambapo bado kuna billioni 1.6 bado haijalipwa kwa mkandarasi kwa kuwa yupo kwenye kipindi cha uangalizi”, aliongeza Mhe. Ndejembi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange ameeleza kuwa kukamilika kwa kiwanda hiko kunaenda kuleta mageuzi makubwa kwani nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo Shirika bado linaendelea kuikuza sekta  na kuwa na utoshelevu wa nguzo zenyewe kwa matumizi ya wananchi. 

“Baada ya kukamilika kwa ujenzi wa kiwanda na kuanza uzalishaji ambapo kwa hali ilivyo ya matumizi ya nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo kama Shirika tutahakikisha tunaisimamia sekta hii ili kuendelea kuwapatia wateja wetu huduma ya umeme wa uhakika”, alisema Bw. Twange. 

Ziara hiyo ya kamati ya kudumu ya bunge ya nishati na madini inalenga kufanya ukaguzi wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Shirika katika maeneo mbalimbali nchini ili kujionea ufanisi wake.
Posted by MROKI On Thursday, March 12, 2026 No comments
Waziri Mkuu, Dkt, Mwigulu Nchemba akifunga Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili  ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji kwenye ukumbi wa Kambarage - Hazina jijini Dodoma, Machi  11, 2026.
Washiriki wa Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili  ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji wakimsikiliza Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba alipofunga mkutano huo kwenye ukumbi wa Kambarage - Hazina jijini Dodoma, Machi 11, 2026.
Washiriki wa Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili  ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji wakimsikiliza Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba alipofunga mkutano huo kwenye ukumbi wa Kambarage - Hazina jijini Dodoma, Machi 11, 2026.
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Wakuu wa Mikoa na watendaji wao katika mikoa yote nchini wajipange kutoa taarifa kuhusu uwekezaji na ukuzaji wa biashara kwenye mikoa yao kila wanapotoa taarifa kwa viongozi wa kitaifa.
 
“Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala na Wakurugenzi wa Halmashauri mbebe jukumu la kuwa mabalozi wa kwanza wa uwekezaji katika maeneo yenu kwa kutambua na kutangaza fursa mbalimbali zilizopo katika maeneo yenu.”
 
“Tubebe hili jukumu, kila Mkuu wa Mkoa anapotoa taarifa atapaswa aseme ameongeza uwekezaji kwa kiasi gani, amekuza biashara kwa kiasi gani na katika kuongeza biashara mpya
 
Ametoa wito huo leo jioni (Jumatano, Machi 11, 2026) wakati akifunga Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (Mkumbi II) uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage, HAZINA, jijini Dodoma.
 
Amesema mapendekezo yote yaliyowasilishwa na washiriki wa mkutano huo ambao ni Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa pamoja na Wakurugenzi yaandaliwe katika mfumo wa mkakati wa utekelezaji ili kuwezesha utekelezaji wake kwa ufanisi.
 
“Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alishasema isiwepo sheria inayoleta kikwazo katika utendaji kazi wa serikali. Haya tuliyoyabaini, tuyaweke kwenye majedwali na kubainisha lipi ni kikwazo na lipi limefanyika. Leteni hayo mapendekezo.”
 
“Kuhusu suala la utitiri wa taasisi za udhibiti na kodi, andaeni mapendekezo mahsusi na yawasilishwe kwa Waziri wa Fedha ili yaweze kuingizwa katika Muswada wa Sheria ya Fedha (Finance Bill) wa mwaka huu. Hatua hii inalenga kuwa sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha mazingira ya uwekezaji nchini,” amesema.
 
Pia amezitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa zihakikishe zinaondoa urasimu katika kuanzisha biashara mpya au viwanda vipya katika maeneo yao. “Kufanya hivyo, kutasaidia kuchochea upatikanaji wa ajira mpya kwa vijana, kukuza kipato kwa wawekezaji na wafanyabiashara pamoja na kukuza pato la Taifa.”
 
Amezitaka mamlaka hizo ziweke mikakati ya kushughulikia changamoto mbalimbali zikiwemo za tozo zisizo rafiki kwa sekta binafsi. “Ni dhahiri kuwa Serikali pekee haiwezi kufanikisha malengo haya bila ushiriki mpana na madhubuti wa sekta binafsi,” amesema.
 
Mapema, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo aliwashukuru Wakuu wa Mikoa yote kwa ushirikiano wao na jinsi walivyolipa kipaumbele suala la uwekezaji kwenye maeneo yao.
 
Alisema ofisi yake kwa kushirikiana na Waziri wa Nchi, OWM – TAMISEMI wanaandaa nyenzo za kushindanisha mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa (Ease of Doing Competitive Business) katika kuvutia uwekezaji na kulinda biashara.
 
“Kupitia hii kila mkoa utapimwa jinsi wanavyowezesha biashara na kuvutia uwekezaji ili kuona wanakuza vipi biashara katika maeneo yao. Na watapimwa ufanisi wao kila mwaka mara moja,” alisema.
 
Naye, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar aliwaeleza washiriki wa mkutano huo kwamba matarajio ya Serikali kwenye utekelezaji wa DIRA 2050 unaendana na MKUMBI II kwenye maeneo yao.
 
“Uchumi wa nchi yetu kwa sasa ni dola za Marekani bilioni 100 tukichanganya uzalishaji wa bidhaa zetu zote, huduma na biashara za ndani na za nje angalau kwa hesabu za mwaka jana. Katika miaka 25 ijayo, tunataka tufikie dola za Marekani trilioni moja, maana yake tukue zaidi ya mara 10.”
 
“Ili tufike huko hatupaswi kwenda kama ilivyo sasa, tunapaswa kubadilika sana na tuongeze bidii siyo tu uchumi ukue bali uwe wa kisasa pia,” alisema.
 
Posted by MROKI On Thursday, March 12, 2026 No comments

March 11, 2026






Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Ndg. Asha-Rose Migiro,leo tarehe 11 Machi 2026 amefanya mazungumzo jijini Dodoma na Balozi Parfait Onanga-Anyanga, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika na Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa iliyopo Addis Ababa (UNOAU).

Balozi Onanga-Anyanga yupo nchini Tanzania kwa nafasi yake kama
Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe.António Guterres.

Kikao hicho ni sehemu ya mashauriano ya Mjumbe huyo na wadau mbalimbali wa kitaifa kwa lengo la kubadilishana mawazo kuhusu mustakabali wa kisiasa kufuatia Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025, pamoja na juhudi pana za kuimarisha amani, demokrasia na mshikamano wa kitaifa nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Ndg. Asha-Rose Migiro alisisitiza dhamira ya muda mrefu ya Tanzania katika kuendeleza utawala wa kidemokrasia, ushiriki wa kisiasa kwa njia ya amani na kuheshimu utawala wa sheria.

Alibainisha kuwa Tanzania inaendelea kuongozwa na misingi ya Mkataba wa Umoja wa Afrika wa Demokrasia, Uchaguzi na Utawala Bora, pamoja na viwango vya kimataifa vilivyowekwa katika Tamko la kimataifa la Haki za Binadamu na Mkataba wa kimatifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa.

Katibu Mkuu pia alieleza kuhusu mageuzi ya kisheria katika Tume ya Uchaguzi na taasisi nyingine yaliyofanyika kwa lengo la kuimarisha mfumo wa uchaguzi, ikiwa ni pamoja na kutungwa kwa sheria mpya za uchaguzi mwaka 2024 na hatua mbalimbali zilizolenga kuongeza uwazi, uwajibikaji na imani ya wananchi katika mchakato wa uchaguzi.

Mazungumzo hayo pia yaligusia matukio ya vurugu yaliyojitokeza katika baadhi ya maeneo nchini wakati na baada ya uchaguzi, ambayo yalisababisha upotevu wa maisha na uharibifu wa mali, ikiwemo mashambulizi dhidi ya ofisi za CCM. Ilibainishwa kuwa hatua stahiki zilichukuliwa kurejesha hali ya utulivu na amani nchini.

Pande zote mbili zilisisitiza umuhimu wa kuendelea kwa mazungumzo na maridhiano miongoni mwa wadau wa kitaifa. Hali kadhalika Katibu Mkuu wa CCM alimthibitishia Balozi Onanga-Anyanga kuwa Tanzania itaendeleza uhusiano wake na jumuiya ya kimataifa katika kuimarisha amani, usalama na maendeleo jumuishi.

CCM imepongeza ushirikiano madhubuti uliopo kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa na kuthibitisha dhamira yake ya kustawisha umoja wa kitaifa, utulivu na demokrasia katika Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.
Posted by MROKI On Wednesday, March 11, 2026 No comments

March 09, 2026





Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Asha-Rose Migiro, leo Jumatatu,Machi 9,2026, amefungua rasmi mafunzo maalum ya Uongozi na Utawala Bora kwa viongozi na watendaji waandamizi wa Chama yanayofanyika katika Ukumbi wa Mount Royal, Mkoani Iringa.

Mafunzo hayo ya siku nne yameandaliwa na Jitegemee Holdings Company Limited (JHCL) kwa kushirikiana na Taasisi ya Wakurugenzi Tanzania (IoDT), na yanawaleta pamoja wajumbe wa Bodi, Menejimenti ya Jitegemee Holdings pamoja na viongozi waandamizi wa CCM.

Akifungua mafunzo hayo, Dkt. Migiro amesema kuwa uongozi na utawala bora ni msingi muhimu wa kuimarisha taasisi na kuendeleza maendeleo ya Taifa, akisisitiza kuwa mafunzo hayo yanaendana na utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa 2025 pamoja na maono ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Aidha, amewataka washiriki kutumia fursa ya mafunzo hayo kujenga uwezo wa kiuongozi na kuhakikisha maarifa watakayopata yanatumika kuimarisha utendaji wa taasisi wanazoziongoza.





Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa Serikali itachukua hatua kali ikiwemo kufilisiwa kwa yeyote anatakayebainika kuhujumu wakulima kwa kuwauzia pembejeo zisizokuwa na ubora zikiwemo mbegu.
 
Ameyasema hayo leo Jumapili, Machi 08, 2026 alipozungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Laela A wilayani Sumbawanga, Rukwa. Amesisitiza kuwa watu hawatovumiliwa kwa kuwa wana lengo la kuliingiza Taifa katika njaa.
 
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo baada ya Mbunge wa Viti Maalumu, Sylvia Sigula kuishukuru Serikali kwa kuwapatia ruzuku ya pembejeo ila ameiomba Serikali kuwatatulia changamoto ya kuuziwa mbegu zisizokuwa na ubora jambo linalosababisha wakulima kupata hasara kwani kilimo ndio uchumi wa Rukwa.

ameiagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufanya uchunguzi wa kina kuhusu matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo katika baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Rukwa kufuatia taarifa za kuchelewa kwa utekelezaji wa miradi hiyo.

Ametoa agizo hilo leo Jumapili (Machi 8, 2026) wakati akizungumza na mamia ya wananchi wa Laela mkoani Rukwa baada ya kupokea taarifa za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika eneo hilo.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali haitavumilia kuona miradi ya maendeleo ikicheleweshwa wakati fedha zake tayari zimetolewa kwa ajili ya kuwahudumia wananchi.

 “Kamanda wa TAKUKURU nifanyie uchunguzi wa kina, senti mpaka senti, yeyote aliyehusika kwenye hii fedha hapa nipe taarifa hiyo ili niweze kufanya maamuzi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameonesha kutoridhishwa na kuchelewa kwa utekelezaji wa baadhi ya miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa shule za sekondari, madarasa pamoja na miundombinu mingine ya elimu katika eneo hilo.
 
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde amesema wizara amekuwa ikifanya uchunguzi na kuchukua hatua pale inapobaini kuwepo kwa pembejeo zisizokuwa na ubora na tayari kuna mtu mmoja amekamatwa mkoani humo.
Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu,Pwani
Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) wameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kusambaza miundombinu ya gesi asilia kwenye kaya takribani 1000 na shule moja  ambapo mradi huo umefadhiliwa na Serikali kwa asilimia 100 kupitia REA.

Hayo yamezungumzwa leo Machi 8, 2026 na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF)  Bw. Deodatus Balile wakati wa Ziara ya TEF Kutembelea mradi uliofadhiliwa na REA wa ujenzi wa miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia kwenye nyumba za makazi mkoa wa Pwani

Bw. Balile amesema kupitia mradi huo Serikali imepunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa Nishati nyingine kama mkaa wa kawaida, kuni, na mafuta ya taa na nishati gesi asilia sasa inakua ni chanzo cha nishati ya kupikia.

"REA imefanya kazi kubwa sana ya kufadhili mradi huu, hivyo basi mradi huu utaboresha kiwango cha maisha ya walengwa wa mradi kwa kuokoa gharama na muda wa kupika, mazingira safi afya bora na uwezeshaji wa wanawake kuongezeka, " Amesema Bw. Balile.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Mradi kutoka REA,  Mha. Emmanuel Yessaya amesema kuwa Wakala ulitenga Fedha kwa ajili ya kufadhili mradi ya usambazaji wa gesi asilia kupitia Mfuko wa Nishati Vijijini (REF) ambapo takribani kaya 1000 pamoja na taasisi moja zimenufaika kwa kusambaziwa miundombinu ya gesi asilia kwa ajili ya kupikia majumbani katika mkoa wa Lindi na Pwani.

Mha.Yessaya ameongeza kuwa, Mradi huo ni wa kimkakati kwa ajili ya kupunguza gharama za nishati ya kupikia, kulinda afya za wananchi na kupunguza athari za kimazingira zitokanazo na ukataji wa misitu kwa ajili ya nishati ya kupikia kwa wananchi wanaoishi Vijijini na kwenye vijiji miji.

Kwa upande wake Mhandisi wa mradi huo kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Mha. Anthony Karomba, amesema kuwa mradi huo wa kuunganisha wateja wa majumbani kwenye mtandao wa gesi asilia umegharamikiwa kwa fedha nyingi na Serikali kupitia REA na hivyo amewasihi wananchi kuendelea kuilinda miundombinu hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi wa Kata ya Kisemvule wameishukuru Serikali kupitia REA kwa kusambaza miundombinu ya gesi asilia ya kupikia katika miji yao. Wameeleza kuwa mradi umenufaisha kaya zao kwa kuokoa gharama, kuongeza muda wa kufanya shughuli za kuzalisha mali, imelinda mazingira, imeboresha afya zao na kuimarisha usawa wa kijinsia kwenye shughuli za kiuchumi.



Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments
Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu akiwa anamfariji mtoto wa yatima wa kituo cha Caring from Childhood to Youth kilichopo katika kijiji cha Bumilayinga,wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu akiwa akikabidhi zawadi  katika kituo cha watoto yatima cha Caring from Childhood to Youth kilichopo katika kijiji cha Bumilayinga,wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake.
Na Fredy Mgunda, Mufindi
Wanawake wahifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kutoka Shamba la Miti Sao Hill wametembelea na kuwafariji watoto wanaolelewa katika Kituo cha Kulelea Watoto Yatima cha Caring from Childhood to Youth kilichopo katika kijiji cha Bumilayinga, wilayani Mufindi mkoani Iringa.

Ziara hiyo imefanyika ikiwa ni sehemu ya shughuli za kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, ambapo wanawake hao walionyesha upendo na mshikamano kwa watoto hao kwa kutumia muda kuzungumza nao pamoja na walezi wao na kusikiliza changamoto wanazokabiliana nazo.

Akizungumza kwa niaba ya wanawake hao, Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu, alisema licha ya majukumu yao ya kulinda na kuhifadhi rasilimali za misitu, wanatambua pia umuhimu wa kushiriki katika shughuli za kijamii zinazogusa maisha ya watu moja kwa moja.

Alisema vitendo hivyo vinasaidia kuimarisha upendo, mshikamano na ushirikiano ndani ya jamii, huku vikiwapa watoto walioko katika mazingira magumu matumaini na ari ya kuendelea kupambana ili kufikia malengo yao ya maisha.

Kwa upande wake, Meneja wa Kituo cha Caring from Childhood to Youth, Bw. Ponsiano Mfikwa, aliwashukuru wanawake hao kwa kuwatembelea na kuwakumbuka watoto hao, akisema ujio wao umeleta faraja kubwa kwa watoto pamoja na walezi wao.

Alisema msaada huo ni ishara ya moyo wa upendo na unatoa mfano mzuri kwa jamii kuendelea kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu ili waweze kukua katika malezi bora.

Naye Diwani wa Kata ya Sao Hill ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga, Mhe. Stephen Msigwa, aliwapongeza wanawake wahifadhi kwa juhudi zao katika kulinda na kuhifadhi rasilimali za misitu pamoja na kushiriki katika shughuli za kijamii.

Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba akizungumza katika Mji wa Laela, Halmashauri ya wilaya ya Sumbawanga wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba iliyoanza jana mkoani Rukwa.
***************
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema wananchi wa Mkoa wa Rukwa wataanza kupata umeme wa gridi kuanzia mwezi mei mwaka huu mara utakapokamilika mradi wa usafirishaji umeme wa msongo wa kV 400 kutokea mkoani Iringa.

Ameyasema hayo tarehe 8 Machi 2026, katika Mji wa Laela, Halmashauri ya wilaya ya Sumbawanga wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba iliyoanza jana mkoani Rukwa.

“Kwa maelekezo ya Rais, Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan na maelekezo yako, tunaendelea kuhakikisha inapofika mei 2026 tunawasha umeme kupitia mradi wa TAZA. Hali ya mradi inaenda vizuri na kama kila kitu kitakwenda kama kilivyo, itakapofika mwezi wa tano mwaka huu hatimaye Mkoa huu wa Rukwa utanufaika na umeme wa gridi.” Amesema Mhe.Salome

Ameeleza kuwa, kwa sasa mkoa wa Rukwa unapata umeme kutoka nchini Zambia kupitia mashirikiano ya biashara ya umeme katika nchi za Ukanda wa Kusini mwa Afrika (Southern Africa Power Pool) ambayo yanawezesha nchi wanachama kuuza au kununua umeme pale kunapokuwa na uhitaji ili kukidhi mahitaji ya wananchi.

 Ameongeza kuwa, kutokana na nchi kuwa na umeme wa kutosha, kazi zinazoendelea ili kuweza kuutumia umeme huo ipasavyo ni ujenzi wa miundombinu imara ya usafirishaji na usambazaji umeme itakayowezesha kufikisha huduma hiyo kwa wananchi wengi.

Kuhusu Nishati Safi ya Kupikia, amesema jitihada mbalimbali zinaendelea ili kuweza kufikia asilimia 80 ya wananchi wanaotumia Nishati Safi ya Kupikia ifikapo 2034 ikiwemo ya kusambaza majiko banifu na mitungi ya gesi kwa bei ya ruzuku.

Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Palamagamba J. Kabudi, ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa 26 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Jumuiya ya Madola (CFAMM) uliofanyika Machi 8, 2026 jijini London, Uingereza akimwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.).

Akichangia mjadala, Prof. Kabudi amesema Jumuiya ya Madola inapaswa kubaki kuwa jukwaa muhimu la kushughulikia changamoto za maendeleo na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa (multilateralism) katika kipindi cha sasa chenye changamoto za kisiasa, kiuchumi na kimazingira.

Katika masuala ya uchumi, Prof. Kabudi amesisitiza umuhimu wa kuimarisha biashara na uwekezaji kati ya nchi wanachama kwa kujifunza kutoka mifano ya ushirikiano wa kikanda kama Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA). 

Amesema jukwaa la biashara na uwekezaji la Jumuiya ya Madola litasaidia kupunguza vikwazo vya biashara na kuongeza biashara kati ya nchi wanachama.

Vilevile amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika madini muhimu na kuimarisha miundombinu ya kidijitali ili kuhamasisha uwekezaji, uhamishaji wa teknolojia na matumizi ya huduma za serikali mtandaoni. Hatua hizo, amesema zitasaidia kupunguza pengo la kidijitali na kuongeza fursa za kiuchumi kwa vijana.

Kwa upande wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Shirley Ayorkor Botchwey, amewaimiza nchi wanachama kuimarisha ushirikiano kukabiliana na mabadiliko ya mazingira ya kimataifa. 

Amesema mkutano huo ni fursa ya kujadili mikakati ya kukuza biashara, uwekezaji na kukabiliana na changamoto kama mabadiliko ya tabianchi na changamoto za kiuchumi.

Mkutano wa CFAMM unawakutanisha Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka nchi 56 za Jumuiya ya Madola ikiwa ni jukwaa muhimu la kujadiliana masuala ya kimataifa yanayoathiri maendeleo ya nchi wanachama.
Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments

March 08, 2026

Wanawake kutoka Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Leo tarehe 08 Machi, 2026 wameshiriki katika maadhimisho ya siku wanawake duniani ambayo kimkoa yamefanyika katika uwanja wa shule ya msingi Mbande iliyopo katika halmashauri ya wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma.








Posted by MROKI On Sunday, March 08, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo