Nafasi Ya Matangazo

May 27, 2026








Mtwara
Mkoa wa Mtwara umeendelea kujidhihirisha kuwa kitovu muhimu cha uwekezaji katika sekta ya chumvi kutokana na uwepo wa fukwe zinazofaa kwa uzalishaji, maboresho ya mazingira ya biashara na ongezeko la uzalishaji linalofikia takribani tani 90 kwa majaruba manne katika baadhi ya maeneo ya uzalishaji.

Kutokana na hatua hiyo, wachimbaji na wazalishaji wa chumvi wameanza kunufaika na fursa mpya za kiuchumi kupitia kuongezeka kwa uzalishaji, ajira na upanuzi wa maeneo ya uzalishaji.

Akizungumza katika mahojiano maalum, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mtwara, Winnifrida Mrema, amesema sekta ya chumvi mkoani humo inaendelea kukua kwa kasi kutokana na kuimarika kwa shughuli za uzalishaji pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa katika uchakataji wa chumvi.

Amesema maboresho hayo yanalenga kuongeza ubora wa chumvi kwa matumizi ya majumbani, viwandani na mifugo, huku yakichochea ajira kwa wananchi wa maeneo yanayozunguka mashamba ya chumvi.

“Mtwara ina mazingira rafiki kwa uzalishaji wa chumvi na Serikali inaendelea kuhamasisha uwekezaji katika sekta hii ili kuongeza mapato kwa wananchi na taifa kwa ujumla,” amesema Mrema.

Katika Kijiji cha Mnete, Kata ya Nalingu Halmashauri ya Mtwara Vijijini, msimamizi wa mashamba ya chumvi, Salum Amani, amesema mashamba hayo yanamilikiwa na Zamda Khatibu na yana leseni mbili za uvunaji chumvi pamoja na majaruba 24 yanayotumika kwa uzalishaji.

Amesema kwa sasa wanaendelea na shughuli za usafishaji wa majaruba baada ya msimu wa mvua ili kuruhusu maji ya chumvi kuingia tayari kwa uzalishaji mpya.

Kwa mujibu wa Salum, uzalishaji wa chumvi hutegemea hali ya hewa, ambapo jua kali huwezesha chumvi kukauka ndani ya siku 30, huku hali ya baridi ikifanya mchakato huo kuchukua hadi siku 40.

“Kwa kawaida majaruba manne huzalisha takribani tani 90 za chumvi kwa msimu mmoja, huku shughuli hizi zikitoa ajira kwa wafanyakazi tisa katika eneo hili,” amesema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wazalishaji Chumvi Mkoa wa Mtwara na  Mwenyekiti wa Kamati ya Chumvi kupitia  FEMATA, Khalfan Nassoro, amesema kupunguzwa kwa gharama ya ada ya pango ya leseni za chumvi  kutoka Shilingi 45,000 hadi Shilingi 20,000 kumeongeza uwezo wa wazalishaji kupanua maeneo ya uzalishaji.

Amesema hatua hiyo imeongeza matumaini kwa wawekezaji na wachimbaji wadogo, huku akisisitiza kuwa mazingira bora ya uwekezaji yataifanya Mtwara kuwa kitovu kikuu cha uzalishaji wa chumvi nchini.

Nassoro amesema pia ukuaji wa sekta hiyo unaweza kuchochea ujenzi wa viwanda vya kuongeza thamani ya chumvi na hivyo kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa.
Posted by MROKI On Wednesday, May 27, 2026 No comments




Mtwara
Mkoa wa Mtwara umeendelea kujidhihirisha kama kitovu muhimu cha uwekezaji wa madini nchini kutokana na uwepo wa rasilimali nyingi za madini ya viwandani, vito na madini mkakati, huku mapato ya Serikali kupitia sekta hiyo yakiongezeka kwa kasi katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mtwara, Winnifrida Mrema, amesema mkoa huo unafahamika zaidi kwa uwepo wa madini ya chokaa yanayotumika kuzalisha saruji katika Kiwanda cha Saruji cha Dangote, jambo linalochangia kukuza uchumi wa mkoa na kuimarisha shughuli za viwanda nchini.

Amesema Mkoa wa Mtwara pia una utajiri wa madini mengine ya viwandani yakiwemo chuma, shaba, kinywe, ulanga pamoja na madini ya mchanga mzito (heavy mineral sands), ambayo ni miongoni mwa madini mkakati yanayohitajika kwa kiwango kikubwa duniani katika utengenezaji wa teknolojia mbalimbali ikiwemo magari ya umeme.

Aidha, amesema Bandari ya Mtwara imeendelea kuwa kiungo muhimu cha biashara na usafirishaji wa madini na bidhaa za viwandani, ambapo hutumika kusafirisha saruji ya Dangote kwenda Zanzibar na Visiwa vya Comoro, sambamba na usafirishaji wa makaa ya mawe kutoka mikoa ya Ruvuma na Njombe kuelekea masoko ya China, India na Dubai.

Kwa upande wa uwekezaji, Mrema amesema Mkoa wa Mtwara una fursa kubwa katika uchimbaji na uchakataji wa madini ya dhahabu, shaba pamoja na vito, hususan green garnet, huku akiwahimiza wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kutumia fursa hizo kuwekeza katika sekta ya madini.

Pia amesema Serikali inaendelea kuwahamasisha wawekezaji kushirikiana na wachimbaji wadogo wa madini ya viwandani, dhahabu na vito kwa kuwapatia mitaji, mafunzo na msaada wa kitaalam ili kuongeza uzalishaji na kuboresha shughuli zao za uchimbaji.

Akizungumzia mapato ya Serikali, Mrema amesema makusanyo kupitia sekta ya madini mkoani humo yameongezeka kutoka shilingi bilioni 1.85 mwaka 2021/22 hadi shilingi bilioni 5.95 mwaka 2023/24, kabla ya kufikia shilingi bilioni 7.55 mwaka 2024/25, hatua inayoonesha ukuaji mkubwa wa sekta hiyo na mchango wake katika uchumi wa taifa.

Naye Fundi Sanifu Madini kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mtwara, Nurah Juma, amesema madini ya ujenzi kama mawe na kokoto yanayochimbwa katika kijiji cha Chipite wilayani Masasi yameendelea kuwa mhimili muhimu wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika mikoa ya Mtwara na Lindi.

Amesema kokoto zinazozalishwa katika eneo hilo zinatumika katika ujenzi wa barabara, majengo, upanuzi wa Bandari ya Mtwara na viwanja vya ndege, pamoja na ujenzi wa Bandari mpya ya Kisiwa Mgao, hali inayochangia upatikanaji wa vifaa vya ujenzi vyenye ubora na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa kusini.
Posted by MROKI On Wednesday, May 27, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu

BABATI — Mahakama ya Mwanzo Wilaya ya Babati mkoani Manyara imesitisha kusikiliza kesi ya jinai namba 291 ya mwaka 2026 iliyofunguliwa na aliyekuwa Mbunge wa Babati Mjini, Paulina Gekul, inayomkabili Brayton Lucas (17), baada ya kujiridhisha kuwa mshtakiwa huyo ni mtoto mwenye umri wa chini ya miaka 18 na hivyo shauri hilo linapaswa kusikilizwa katika Mahakama ya Watoto kwa mujibu wa sheria.

Uamuzi huo ulitolewa baada ya Wakili wa upande wa utetezi, Thadei Lister, kuiomba mahakama kujiridhisha kuhusu umri wa mshtakiwa kwa kuwasilisha nyaraka mbalimbali ikiwemo cheti cha kuzaliwa kilichoonesha kuwa Brayton alizaliwa Novemba 12, 2008 na kwa sasa ana umri wa miaka 17 na miezi sita, tofauti na taarifa zilizokuwa katika hati ya mashtaka zilizomtaja kuwa na miaka 19.

Katika shauri hilo, Paulina Gekul alidai kuwa Brayton Lucas, ambaye alikuwa akichunga mifugo yake, alihusika katika wizi wa mbuzi 15 wenye thamani ya shilingi milioni tatu, kosa linalodaiwa kufanyika chini ya kifungu cha 268 cha sheria ya wizi wa mifugo. Kesi hiyo ilikuwa na jumla ya watuhumiwa watatu.

Mahakama pia ilielezwa kuwa mtoto huyo alikuwa amechanganywa katika shauri moja na watuhumiwa watu wazima, jambo ambalo upande wa utetezi ulidai ni kinyume na sheria zinazolinda haki za mtoto.

 Baada ya kupitia nyaraka zilizowasilishwa, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Babati, Ahmed Mgodo, alisema mahakama imejiridhisha kuwa Brayton Lucas ni mtoto na hivyo haina mamlaka ya kuendelea kusikiliza kesi hiyo. Kutokana na uamuzi huo, mahakama ilisimamisha shauri hilo dhidi ya mshtakiwa huyo na kuagiza polisi kuandaa hati mpya ya mashtaka kwa mujibu wa sheria zinazohusu watoto.

Brayton Lucas alipatiwa dhamana huku washtakiwa wawili wengine wakiendelea kushikiliwa. Wakili Thadei Lister amesema wako tayari kuendelea kumtetea mtoto huyo iwapo atafikishwa katika Mahakama ya Watoto.

Akizungumza nje ya mahakama, Wakili Thadei alisema Brayton ni mwanafunzi wa kidato cha nne ambaye alitoweka akiwa Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha na wazazi wake walikuwa wakimtafuta kwa kipindi cha miezi mitatu kabla ya kupata taarifa kuwa amekamatwa Babati kwa tuhuma za wizi.

Mama mzazi wa Brayton alisema mtoto wake alitakiwa kuwa shuleni baada ya kumaliza kidato cha nne na tayari alikuwa amepangiwa shule, lakini aliondoka nyumbani bila kutoa taarifa na baada ya juhudi za muda mrefu za kumtafuta walipata taarifa kuwa alikuwa Babati akifanya kazi.
Wakati huo huo, Diwani wa Kata ya Maruvango Wilaya ya Arumeru Mashariki, Digna Nassari, amesema taarifa za kupotea kwa mtoto huyo zilikuwa zimetolewa polisi miezi mitatu kabla ya kufunguliwa kesi dhidi yake na Paulina Gekul.

Aidha, Digna amesema Brayton ni miongoni mwa watoto 16 kutoka kata hiyo waliotoroka shule, huku akisisitiza umuhimu wa jamii kushirikiana kuhakikisha watoto wanarudi katika mfumo wa elimu na kupata ulinzi unaostahili
Posted by MROKI On Wednesday, May 27, 2026 No comments

May 25, 2026








Nkanda - Ludewa
Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijni (REA), unaendelea kutekeleza miradi mbalimbali pamoja na kuwasimamia kwa karibu wakandarasi wote waliopewa na watakaopewa zabuni ya kutekeleza miradi ili kuhakikisha kuwa miradi hiyo inakamilika kwa wakati na kwa ubora uliopangwa ili iweze kuwanufaisha wananchi.

Hayo yamebainishwa leo Mei 25, 2026 na Wajumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), wakati wa hafla ya kukagua miradi, kutembelea na kuwasha umeme kitongoji cha Nkanda kilichopo wilaya ya Ludewa mkoani Njombe mradi uliokuwa unatekelezwa na Suma Jkt Electric Company Ltd. 

Mha. Ahmed Chinemba amesema kuwa, mradi wa kupeleka umeme katika vitongoji vya mwambao wilayani Ludewa unatekelezwa na mkandarasi M/S SUMAJKT ELECTRIC COMPANY LTD kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 3.2 ili wananchi wa mwambao wapate huduma ya umeme. 

"Mradi huu umelenga kuongeza shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa kitongoji cha nkanda ukiwa na chachu ya kutoa fursa za kibiashara kwa kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi, kurahisiha upatikanaji wa huduma za kijamii na uwekezaji wa viwanda vidogo vidogo kama mashine za kusaga, mashine za kuchana mbao pamoja na mashine za kuchomelea," Amesema Mha.  Chinemba.

Kwa upande wake, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Suma JKT Brigedia Jenerali Shija Lupi, ameishukuru REA kwa kuwapatia kazi hiyo ya kufikisha umeme katika maeneo ya mwambao kikiwemo kitongoji hicho cha Nkanda ambapo kazi imekamilika kwa ubora. 

"Sisi Suma JKT tumefanisha kufikisha umeme kwenye mazingira magumu kama haya ambayo yalikuwa na changamoto nyingi lakini tumefanikiwa na sasa tunaona matunda yake, " Amesema Brigedia Jenerali Lupi.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, Mha. Deogratius Nagu amesema katika kitongoji cha Nkanda takribani shilingi milioni 450 zimetolewa na Serikali kupitia REA ili kufikisha huduma ya umeme katika kitongoji hicho. 

Aidha, amewataka wananchi wa Nkanda kuchangamkia fursa ya uwepo wa umeme kwa kuhakikisha wanafanya wiring katika nyumba zao na kuunganisha umeme kwa wingi ili wanufaike na umeme huo katika kitongoji chao.

Naye, Mwakilishi wa Mbunge wa Jimbo hilo Bw. Stanslaus Gowele amesema ujio wa umeme maeneo ya mwambao yanakwenda kuongeza chachu ya Maendeleo kiuchumi na kijamii kwa wananchi hao.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wanufaika wa mradi huo wameeleza namna ambavyo Mradi huo umekuwa mkombozi kwao.
Posted by MROKI On Monday, May 25, 2026 No comments





LINDI
Wilaya  ya Ruangwa mkoani Lindi imeendelea kushuhudia mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii kufuatia kuongezeka kwa shughuli za uchimbaji madini katika Mgodi wa Namungo unaomilikiwa na kampuni ya Elianje Limited, huku wachimbaji wadogo na wananchi wa maeneo yanayouzunguka mgodi huo wakinufaika kupitia ajira, biashara na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Ukuaji wa shughuli za uchimbaji katika mgodi huo umechangia kuboresha huduma za maji, elimu, afya na miundombinu, hali iliyobadili maisha ya wananchi ambao miaka michache iliyopita walikabiliwa na changamoto kubwa za kiuchumi na kijamii.

Akizungumza kwa niaba ya Afisa Madini Mkazi wa Lindi, Mhandisi Dickson Joram amesema hali ya wachimbaji na wananchi wa Namungo imebadilika kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na mwaka 2019 alipowasili katika eneo hilo.

Amesema wakati huo shughuli za uchimbaji zilikuwa katika kiwango cha chini, huku wachimbaji wengi wakitumia njia duni za uzalishaji na kushindwa kumudu mahitaji muhimu ya kila siku.
“Wachimbaji wengi walikuwa wanapitia kipindi kigumu sana. Ulipowatembelea ilibidi wakati mwingine uwaachie fedha za chakula au kuwasaidia mahitaji muhimu. Lakini leo Namungo imebadilika kwa kiasi kikubwa; wananchi wanajitegemea na wanaendesha shughuli kubwa kupitia sekta ya madini,” amesema.

Kwa upande wake, Afisa Uhusiano wa kampuni ya Elianje Limited, Joseph Shayo amesema kampuni hiyo ilianza shughuli za utafiti na uchimbaji mwaka 2020 na tangu wakati huo imekuwa ikihakikisha jamii inayouzunguka mgodi inanufaika moja kwa moja kupitia utekelezaji wa miradi ya kijamii.

Amesema kampuni imefanikiwa kuchimba visima na kusambaza maji katika Kijiji cha Tongwe na Kitongoji cha Namungo, huku maboresho ya huduma hiyo yakiendelea katika maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama.

Mbali na huduma ya maji, amesema kampuni imejenga shule ya awali, kuboresha madarasa, kujenga vyoo vya kisasa pamoja na kushiriki katika ujenzi wa shule ya msingi katika Kitongoji cha Namungo ili kupunguza adha ya watoto kutembea umbali mrefu kufuata huduma za elimu.

Shayo amesema mgodi huo pia umechangia uboreshaji wa barabara zinazounganisha vijiji na kata jirani sambamba na kusaidia shule mbalimbali kwa kutoa vifaa vya elimu ikiwemo kompyuta na mashine za uchapishaji.

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Chingumbwa, Kata ya Mbekenyela wilayani Ruangwa, Abdallah Manjakali amesema uwepo wa mgodi huo umefungua fursa nyingi za ajira, biashara na huduma za kijamii ambazo hapo awali zilikuwa changamoto kubwa kwa wananchi.

“Leo wananchi wengi wanapata kipato na maisha yameimarika. Pia kampuni imenunua gari la wagonjwa linalowahudumia wananchi bure wakati wa dharura bila kuchangishwa fedha yoyote,” amesema.

Manjakali ameongeza kuwa ushirikiano uliopo kati ya mgodi na vijiji vinavyouzunguka unapaswa kuwa mfano kwa wawekezaji wengine wa sekta ya madini, huku akizitaka kampuni zenye leseni ambazo bado hazijaanza uzalishaji kuharakisha uwekezaji ili wananchi waweze kunufaika na rasilimali zilizopo katika maeneo yao.
Posted by MROKI On Monday, May 25, 2026 No comments








Na Benny Mwaipaja, Congo, Brazaville
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amewasili nchini Congo, Brazzaville, amabako atashiriki Mkutano Mkuu wa 61 wa mwaka 2026 wa Bodi ya Magavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) na Mkutano Mkuu wa 52 wa Mwaka wa Mfuko wa Maendeleo wa Benki hiyo (ADF), uliopangwa kufanyika kuanzia tarehe 25 hadi 29 mwaka 2026, katika Mji Mkuu wa Congo, Brazaville.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Brazaville, Maya Maya, Mhe. Balozi Omar, alilakiwa na Balozi wa Tanzania nchini Congo, Brazaville, Mhe. Said Juma Mshana.

Katika msafara huo, Mhe. Balozi Omar, ambaye ni Gavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, ameambatana na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mlipaji Mkuu wa Serikali ambaye pia katika Muundo wa Benki ya Maendeleo ya Afrika ni Gavana Mbadala wa Benki hiyo (Alternative Governor), Dkt. Natu El-maamry Mwamba na Naibu Katibu Mkuu ambaye pia ni Kamishna wa Fedha za Nje, Bw. Rished Bade.

Zaidi ya wajumbe 3,000 kutoka nchi mbalimbali za Afrika na Kimataifa, wanatarajiwa kuhudhuria Mkutano Mkuu huo, Utakaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Kintélé, wakiwemo Marais na Wakuu wa Serikali za Afrika, Mawaziri wa Fedha, Magavana wa Mabenki Kuu, washirika wa maendeleo, wawakilishi wa sekta binafsi, viongozi wa asasi za kiraia, wasomi, taasisi za utafiti, NGOs, na wadau wengine.

Kauli mbiu ya mwaka huu ni: “Kuhamasisha Ufadhili wa Maendeleo ya Afrika kwa Wingi katika Dunia Iliyogawanyika”. Kauli hii inasisitiza umuhimu wa kuziba pengo la kifedha linalokua kwa mahitaji ya maendeleo ya Afrika, hasa katika mazingira ya kisiasa na kiuchumi duniani yanayobadilika kwa kasi.

Mkutano pia utajadili masuala mtambuka kama mageuzi ya kidijitali, uimarishaji wa taasisi na utawala bora. Haya yote yanalingana na utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), Mkataba wa Paris wa Mabadiliko ya Tabianchi, Ajenda 2063 ya Umoja wa Afrika, na Mikakati Mikuu Mitano ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (High 5s).
Posted by MROKI On Monday, May 25, 2026 No comments







Dodoma
Timu ya mchezo wa netiboli ya Ofisi ya Makamu wa Rais nchini Tanzania Bara, imeibuka kidedea kwa kutwaa ubingwa wa ligi ya daraja la tatu baada ya kushinda mechi zake zote kwenye ligi hiyo iliyofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.

Mabingwa hao walidhihirisha umahiri wao baada ya mchezo wa kwanza kuwafunga timu ya Chamwino HQ, na katika mchezo wa pili waliwashinda JKT Makutupora kwa magoli 41-24.

Awali Katibu Msaidizi wa Chama cha Netiboli Mkoa wa Dodoma (CHANEDO), Bi. Maimuna Kitete, amesema ligi hiyo ilishirikisha timu tatu pekee baada ya nyingine kushindwa kushiriki kutokana na changamoto mbalimbali, ambapo bingwa ajikusanyia magoli mengi ya kufunga 103 na kufungwa 33; huku mshindi wa pili JKT Makutupora alimaliza kwa magoli ya kufunga 48 na kufungwa 50 na mshindi wa tatu Chamwino HQ alifunga 18 na kufungwa 103.

Bi. Maimuna amesema timu mbili ya Makamu wa Rais na JKT Makutupora zimefanikiwa kupanda daraja hadi la pili, na watashiriki  kwenye mashindano hayo yanayotarajia kufanyika mkoani Tanga baadaye mwezi Oktoba.

Akifunga ligi hiyo mgeni rasmi, Bi. Itika Mwankenja, Mjumbe kutoka Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI), pamoja na uchache wa timu amewapongeza washiriki wote walioshiriki kwenye ligi hiyo, ambapo wamecheza kwa amani, nidhamu na upendo mkubwa tofauti na mashindano mengine.

Bi. Itika amezitaka timu zilizopanda daraja kuhakikisha wanapeperusha vyema bendera ya CHANEDO kwa kufanya vizuri katika mashindano ya daraja la pili, kwa kuendelea kufanya mazoezi kwa bidii, kujifunza mambo mapya na kusikiliza mafunzo kutoka kwa makocha wao.

“Ninawapongeza sana wachezaji mmecheza kwa nidhamu kubwa, tofauti kabisa na mashindano mengine tuendelee na nidhamu hii, mmemaliza mechi mkakumbatiana na kupeana mikono, hadi na makocha wenu wamefanya vivyo hivyo, nawapongeza viongozi wa CHANEDO kwa kuandaa ligi hii, maana mchezo wa netiboli hauchuji tuendelee kuuenzi, na ninatamani sana kuona mkoa wa Dodoma unatoa wachezaji wengi wa timu ya Taifa, najua mpo na mkifanya vizuri mtatokea na mnawalimu wazuri pia” alisisitiza Bi. Itika.

Hatahivyo, amezitaka timu zijitokeze kwa wingi kushiriki kwenye kombe la CHANEDO litakalofanyika baadaye mwezi Juni 2026
Posted by MROKI On Monday, May 25, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu

MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Pwani, Mariam Ibrahim, ameendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Ameyasema hayo leo alipokuwa mgeni rasmi katika mashindano ya “Mkali wa Chapati” yaliyofanyika Wilaya ya Mkuranga, Mkoa wa Pwani ambapo amefafanua mashindano hayo ni sehemu ya juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati safi chini ya uongozi wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.

“Mashindano haya ni sehemu ya juhudi za kumuunga mkono Rais Dk.Samia Suluhu Hassan katika kampeni ya matumizi ya nishati safi kwa wananchi. Hakika Rais Samia ni kiongozi imara ambaye ameweka mbele maslahi ya wananchi pamoja na utunzaji wa mazingira,” amesema Mariam Ibrahim.

Aidha amewataka wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kuachana na matumizi ya majiko ya mkaa na badala yake kutumia nishati safi kama gesi ili kupunguza ukataji wa miti na kulinda mazingira.

Pia amesema kutakuwa na mashindano mengine yajayo yakiwemo ya upishi wa pilau na nyama choma, yenye lengo la kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi pamoja na kukuza mshikamano wa kijamii.
Katika hatua nyingine, amewaomba wananchi wa wilaya hiyo kuendelea kushikamana na kushirikiana katika shughuli mbalimbali za kijamii kwa maendeleo ya jamii yao.

Wakati huo huo  amemshukuru Mbunge wa Jimbo la Mkuranga Abdallah Ulega, kwa kufanikisha mashindano hayo pamoja na shughuli zote zilizofanyika siku hiyo.

“Maandalizi na mafanikio ya mashindano hayo yametokana na juhudi za Mbunge Abdallah Ulega kwa kushirikiana na wananchi wa Mkuranga,”amesema.








 

Posted by MROKI On Monday, May 25, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo