Nafasi Ya Matangazo

June 08, 2026








Na, mwandishi wetu – Dar es Salaam
SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imeingia Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) na Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) yenye lengo la kuimarisha usimamizi wa maafa nchini kwa kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu.

Akizungumza mapema hii leo (08 Juni, 2026) katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Dkt. Jim Yonazi, amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa  Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kujenga mifumo madhubuti ya kiutendaji inayoongozwa na maarifa, sayansi na teknolojia ikiwemo matumizi ya Akili Unde (AI) katika kukabiliana na maafa.

Amesema makubaliano hayo yanatekeleza pia mapendekezo ya Mkutano wa Nane wa Umoja wa Mataifa wa Jukwaa la Dunia la Upunguzaji wa Vihatarishi vya Maafa uliofanyika Geneva, Uswisi, mwezi Juni 2025, na yanaashiria mabadiliko ya kimkakati katika namna Serikali inavyoshughulikia changamoto za maafa kutoka mfumo wa kusubiri majanga hadi mfumo wa kujikita katika kinga, maandalizi na tahadhari.

“Vyuo vikuu na taasisi za utafiti, ikiwemo Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam, zina jukumu muhimu la kuzalisha maarifa na suluhisho za kisayansi zitakazosaidia kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini,”amesema.

Ameongeza kuwa ili kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa makubaliano hayo, Serikali itaandaa Mpango Kazi wa utekelezaji pamoja na Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Usimamizi wa Maafa itakayobainisha maeneo ya kipaumbele yanayohitaji ufumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia.

Dkt. Yonazi amesisitiza kuwa mafanikio ya makubaliano hayo yatapimwa kwa matokeo halisi yatakayochangia kuongeza usalama wa wananchi, kulinda rasilimali za taifa na kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa.

Ushirikiano huo unaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoweka msisitizo katika matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nguzo kuu ya maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii.

Kwa upande wake Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam Prof.Preksedis Marco Ndomba amesema kuwa taasisi imeandika historia kwa kusaini hati ya ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu ambapo ameeleza kuwa mchakato huu ulianza muda mrefu na matunda yake yameanza kuonekana jambo ambalo ni mafanikio makubwa.

“Tunaahidi juu ya kufanikisha  makubaliano hayo kwa kuwa, uwezo huo tunao, utalaam upo wa kutosha kwa kushirikiana kwenye masuala ya viatarishi kitaifa ili kufanikisha adhima hii ya Serikali,” Alisema Profesa Ndomba.
Posted by MROKI On Monday, June 08, 2026 No comments
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu (mwenye suti), akiwa na Kiongozi Mkuu wa Buddha hapa nchini, Mchungaji Dkt.  Ilukuptiye  (kushoto) na Mchungani Xianhong, wakielekea eneo la sherehe za kuachimisha siku ya kuzaliwa ya dini hiyo, na uzinduzi wa Sanamu ya Golden Buddha Upanga jijini Dar es Salaam Juni 7, 2026.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu (mwenye suti), akiwa na Kiongozi Mkuu wa Buddha hapa nchini, Mchungaji Dkt.  Ilukuptiye  Pannasekara na viongozi wengine, wakati akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Sanamu ya Buddha kwenye temple la dini hiyo Upanga jijini Dar es Salaam, Juni 7, 2026.a



Na: Mwandishi wetu - Dar es Salaam, Juni 7, 2026
Kiongozi Mkuu wa dini ya Buddha nchini, Mchungaji Dkt. Ilukuptiye Pannasekara, amesifu ushirikiano ambao wanaupata sio tu kutoka katika dini zingine bali pia serikalini kwa ujumla.

Ametoa kauli hiyo wakati wa kusherehekea siku ya kuzaliwa kwa kiongozi wa dhehebu la Buddha duniani na uzinduzi wa sanamu ya dhahabu ya Buddha (Golden Buddha Statue) eneo la Upanga jijini Dar es Salaam Juni 7, 2026, ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu, akimwakilisha Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba.

Alisema, amekuwa akipata ushirikiano mkubwa kutoka dini nyingine hapa nchini na hivyo kuwafanya waumuni wa Buddha kujisikia furaha.

“Kutokana na mazingira hayo mazuri, tuna jumla ya miradi mitano  kwenye sekta za elimu, utalii na afya, miradin hii tayari mingine imeanza na mingine iko katika hatua mbalimbali.” Alisema.

“Hatuhitaji usaidizi wa fedha kutoka serikalini, tunahitaji ushirikiano, miradi hii mitano ni ya uhakika, italeta zaidi ya dola za kimarekani milioni 100 kwenye uchumi wa Tanzania, alisema Mchungaji Dkt. Pannasekara.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amewahakikishia kuwa Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wake, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kutoa ushirikiano kwa dini zote bila kuwepo kwa ubaguzi.

Amesema Muelekeo wa serikali inapoanza utekelezaji wa dira ya Maendeleo ya 2050 imefungua milango ya kidiplomasia ili kuwaalika wawekezaji kuwekeza hapa nchini.

“Kama serikali tumewahakikishia kuwa kupitia Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji tumewahakikishia kwamba watakapokuwa tayari tutawepeleka kwenye maeneo ya kimkakati ili kutekeleza miradi yao katika sekta za Utalii, Afya na Elimu.” Alisema.
Posted by MROKI On Monday, June 08, 2026 No comments
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, akizungumza na Watumishi wa Umma katika kikao kikao cha majumuisho na viongozi pamoja na watumishi wa umma kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa leo tarehe 7 Juni, 2026.

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amehitimisha ziara yake ya kikazi mkoani Iringa kwa kuwataka viongozi na watumishi wa umma kuendelea kusimamia haki, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi pamoja na kufuatilia utekelezaji wa maelekezo yote yaliyotolewa katika kutatua kero za wananchi.

Ametoa maelekezo hayo leo Jumapili (Juni 7, 2026) wakati akifunga ziara yake ya kikazi mkoani Iringa kwa kufanya kikao cha majumuisho na viongozi pamoja na watumishi wa umma kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imewekeza fedha nyingi katika sekta mbalimbali za maendeleo hivyo ni wajibu wa viongozi na watumishi kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na haki zao zinalindwa.

Amesema ameridhishwa na namna Mkoa wa Iringa ulivyoshughulikia changamoto mbalimbali za wananchi na kuwataka viongozi kuendelea kuwa mbele ya matukio kwa kusikiliza na kutatua kero kabla hazijafikia hatua kubwa.

“Nimeona viongozi wa Mkoa wa Iringa wako mbele ya matukio. Kila hoja iliyojitokeza tayari ilikuwa imepokelewa na hatua mbalimbali zilikuwa zimeanza kuchukuliwa. Huo ndiyo mwelekeo ambao Serikali inautaka,” alisema.

Waziri Mkuu aliwataka viongozi wa Mkoa huo kufuatilia moja baada ya nyingine kero zote zilizowasilishwa katika ziara yake na kuhakikisha wananchi wanapata mrejesho wa hatua zinazochukuliwa.

Alisema Serikali itaendelea kufanya tathmini ya utekelezaji wa maelekezo hayo na kwamba viongozi wa mikoa na halmashauri wanapaswa kuweka kumbukumbu za utekelezaji wa kila hoja iliyowasilishwa na wananchi.

Katika sekta ya afya, Dkt. Mwigulu alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha dawa muhimu na vifaa tiba vinapatikana kulingana na mahitaji ya maeneo husika pamoja na kuimarisha usimamizi wa fedha zinazotengwa kwa ajili ya huduma za afya.

Aidha, alizitaka halmashauri na taasisi za umma kuendelea kuwasaidia watu wenye ulemavu, wazee wasiojiweza na makundi mengine maalum kwa kutumia rasilimali zilizopo ili kuboresha ustawi wao.

Kwa upande wa miundombinu, Waziri Mkuu alielekeza kuharakishwa kwa utekelezaji wa miradi ya barabara iliyo katika hatua mbalimbali za maandalizi na utekelezaji huku akisisitiza ujenzi wa miundombinu yenye viwango vinavyoweza kuhimili changamoto za mazingira.

Pia aliwataka viongozi kuendelea kutatua migogoro ya ardhi kwa haki na kwa kuzingatia sheria pamoja na kuhimiza wananchi kurasimisha umiliki wa mali zao ili kuepusha migogoro inayoweza kujitokeza baadaye.

Akizungumzia utendaji wa watumishi wa umma, Dkt. Mwigulu alisema ni muhimu kuwatambua na kuwathamini watumishi wanaofanya kazi kwa uadilifu na ufanisi huku hatua stahiki zikichukuliwa kwa wale wanaoshindwa kutekeleza wajibu wao.

“Haki, uwajibikaji na huduma bora kwa wananchi lazima viwe msingi wa utendaji wetu. Wananchi wanatarajia kuona matokeo ya kazi zetu na ndiyo dhamira ya Serikali,” alisema.

Aidha, Waziri Mkuu aliwataka viongozi wa mkoa huo kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yote aliyoyatoa katika ziara hiyo ikiwemo migogoro ya ardhi, madai ya wananchi dhidi ya taasisi na kampuni mbalimbali, pamoja na masuala ya ustawi wa jamii yaliyowasilishwa katika mikutano ya hadhara.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James alisema ziara ya Waziri Mkuu imeimarisha ari ya uwajibikaji kwa viongozi na watumishi wa umma pamoja na kutoa mwelekeo wa kushughulikia changamoto zinazowakabili wananchi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo.

Posted by MROKI On Monday, June 08, 2026 No comments

June 07, 2026

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kinatarajia kuadhimisha Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu kuanzia Juni 9 hadi 11, 2026, katika Kampasi ya Mwalimu Julius Nyerere, huku Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, akitarajiwa kuwa mgeni rasmi.

Maadhimisho hayo yatakayowakutanisha watafiti, wabunifu, wanafunzi, sekta binafsi, taasisi za umma na wadau wa maendeleo, yanalenga kuonesha mchango wa utafiti na ubunifu katika kuharakisha maendeleo ya taifa na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Utafiti, Profesa Nelson Boniface, alisema maadhimisho ya mwaka huu yataongozwa na kaulimbiu isemayo: "Kutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania katika Kukuza Nishati Jadidifu, Mageuzi ya Kidijitali na Usalama wa Jamii."

Alisema kaulimbiu hiyo imechaguliwa kutokana na umuhimu wa madini katika maendeleo ya teknolojia za kisasa ikiwemo Akili Mnemba (AI), vituo vya kuhifadhi taarifa (Data Centres), magari ya umeme na nishati jadidifu.

“Tunataka kuonesha namna Tanzania inaweza kutumia rasilimali zake za madini kuchochea mageuzi ya kidijitali, kuimarisha usalama wa nishati na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi,” alisema Profesa Boniface.

Aliongeza kuwa maadhimisho hayo yatahusisha maonesho ya tafiti na ubunifu, mawasilisho ya kitaaluma, makongamano pamoja na majadiliano ya ushirikiano wa kimkakati yatakayowawezesha washiriki kubadilishana maarifa na kujenga mitandao ya kitaaluma na kibiashara.

Kwa mujibu wa UDSM, maadhimisho hayo yatatoa nafasi kwa watafiti na wabunifu kuonesha suluhisho mbalimbali za kisayansi na kiteknolojia zinazolenga kukabiliana na changamoto za maendeleo nchini katika sekta za madini, nishati, kilimo, afya na uchumi wa kidijitali.

Profesa Boniface alisema chuo kinaendelea kutumia maadhimisho hayo kama jukwaa la kuunganisha taaluma, ubunifu na maendeleo ya taifa kwa kuwafikia wananchi, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo.

"Utafiti na ubunifu ni msingi wa maendeleo endelevu. Tunawaalika Watanzania wote kushiriki katika Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu UDSM 2026 ili kujionea kazi na mafanikio ya watafiti na wabunifu wetu," alisema.
Posted by MROKI On Sunday, June 07, 2026 No comments

June 06, 2026






Dodoma 
Wizara ya Madini imekutana katika Bonanza la Michezo lililowashirikisha watumishi wa Wizara pamoja na taasisi zake zote, ikiwa ni utaratibu wa kawaida wa kukutana kila Robo Mwaka kwa lengo la kuimarisha ushirikiano, mshikamano na kufahamiana zaidi miongoni mwa watumishi.


Akizungumza katika bonanza hilo, lililofanyika Juni 6, 2026 katika Viwanja vya Shule ya Sekondari John Merlin, Mipango  jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, ameeleza umuhimu wa michezo na manufaa yake katika maisha ya kila siku, akibainisha kuwa michezo ni afya, burudani na ajira.

“Michezo ni afya kwa sababu inasaidia kujenga mwili imara na kukinga dhidi ya maradhi mbalimbali yasiyoambukiza. Afya inapokuwa imara, manufaa yake ni makubwa kwa mtu binafsi na taifa kwa ujumla,” amesema Dkt. Kiruswa.


Ameongeza kuwa michezo ni burudani kwa kuwa huwapa watu furaha, huondoa msongo wa mawazo na kuongeza amani ya moyo, hali inayochangia kuongeza ubora wa maisha na umri wa kuishi.

Kuhusu ajira, Dkt. Kiruswa amesema  katika nyakati za sasa michezo imekuwa sekta muhimu inayotoa ajira kwa wananchi wengi na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Vile vile, amependekeza katika mabonanza mengine Wizara kuangalia namna ambavyo michezo hiyo itawashirikisha watoto wa watumishi kama familia ya madini.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri amewapongeza watumishi wa Wizara ya Madini na taasisi zake kwa utendaji wao mzuri ulioiwezesha Wizara kuwa miongoni mwa wizara zenye utulivu na matokeo chanya katika utekelezaji wa majukumu yake.

 Amesema  hadi kufikia tarehe 5 Juni 2026, Wizara ilikuwa tayari imekusanya shilingi trilioni 1.27, na hivyo kuvuka lengo la shilingi trilioni 1.2 lililowekwa kwa Mwaka wa Fedha 2025/26.

Awali, akizungumza katika bonanza hilo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, amesema  bonanza hilo ni mwendelezo wa maelekezo ya viongozi wa Wizara ya kuhakikisha watumishi wanakutana mara kwa mara kwa ajili ya kuimarisha afya zao na kujikinga dhidi ya maradhi yasiyoambukiza.

“Siku za karibuni tumeshuhudia ongezeko la maradhi yasiyoambukiza ambayo yamekuwa na athari kubwa kwa wananchi. Hivyo, michezo ni sehemu muhimu ya kujenga afya bora,” amesema Eng. Samamba.

Ameongeza kuwa, Wizara inatambua watumishi wake kuwa ndiyo nguvu kazi kuu ya taasisi hiyo, hivyo itaendelea kuimarisha shughuli za michezo mahali pa kazi ili kukuza mshikamano, umoja na upendo miongoni mwa watumishi na kuongeza hatua hiyo itasaidia kuongeza ufanisi wa kazi na kuifanya Sekta ya Madini kuendelea kuchangia katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya nchi.

Watumishi wameshiriki katika michezo mbalimbali ikiwemo jogging, mpira wa miguu, Pete, riadha kufukuza Kuku, kukimbia na mayai, kukimbia na magunia, basketball, kuvuta kamba ambapo washindi wamepokea tuzo mbalimbali na medali.

Pia, wanamichezo walioshiriki Mashindano ya Mei Mosi  wamekabidhi vikombe viwili kufuatia ushindi walioupata wa mbio na pool table na hivyo kuishukuru Wizara kwa kuwapatia fursa ya kushiriki katika mashindano hayo.
Posted by MROKI On Saturday, June 06, 2026 No comments





Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba ametatua mgogoro wa ardhi uliodumu kwa miaka 41 kati ya Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Yohana  Mtume Nyololo wilayani Mufindi Mkoa wa Iringa na Familia ya   Yosefa Mgavilenzi ambaye ni msimamizi wa mirathi ya marehemu Michael Bakari Seveyage.

Akihutubia mkutano wa hadhara katika kata ya Igowole Mufindi Kusini, Waziri Mkuu alipokea malalamiko ya familia ya  Yosefa Mgavilenzi kuwa eneo lake lenye ukubwa wa ekari 107 limechukuliwa na Kanisa hilo bila fidia na aliomba Waziri Mkuu amsidie ili alipwe.

Mapema wiki hii Waziri Mkuu alituma timu ya wataalamu kutoka ofisi yake ambao walikwenda katika kata ya Nyololo na kufanya vikao vya maridhiano na viongozi wa Kanisa Katoliki, familia ya Yosefa, Wazee, viongozi wa Kata ya Nyololo na  kijiji  cha Nyololo Shuleni walioko madarakani na wastaafu pamoja na wananchi. 

Baada ya majadiliano yaliyochukuwa siku tatu pande mbili husika zilikubaliana kumaliza mgogoro kwa njia ya maridhiano ambapo Baba Askofu wa Jimbo la Mafinga, Vicent Mwagala alitoa shilingi milioni 20 kama fidia kwa familia ya Yosefa ambayo ilizipokea kwa moyo mkunjufu na kukubali kumaliza mgogoro huo.

Hati za maridhiano zilitiwa saini na Kanisa Katoliki Parokia ya Nyololo pamoja na familia ya marehemu Michael Bakari Seveyage leo Juni 5, 2026 katika kikao cha maridhiano kilichofanyika kwenye Ofisi ya Mtendaji wa Kata ya Nyololo wilayani Mufindi.

Paroko wa Parokia ya Yohana Mtume Nyololo alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hasan kwa sera yake ya maridhiano ambayo  imemuwezesha Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kuumaliza mgogoro uliodumu kwa miaka 41.

Alimshukuru Askofu wa Jimbo la Mafinga Vicent Mwagala kwa kutoa shilingi milioni 20 kama fidia kwa mlalamikaji hatua ambayo  imesaidia sana kufikia maridhiano  na alisisitiza kwamba mgogoro huo umeisha na sasa wataishi kwa amani kama jamii moja.

Mchungaji John Mbwiga ambaye ni Kiongozi wa familia ya mlalamikaji aliishukuru serikali kupitia kwa Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba aliyetuma timu ya watalaamu kutoka ofisini kwake ambao wamemaliza mgogoro huo ulioikosesha familia amani kwa miaka mingi na kwamba sasa wataishi kwa amani.

Mwenyekiti wa Kijiji Mstaafu wa kijiji cha Nyololo Shuleni, Jeremia Mngolage alliishukuru serikali hususan Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kazi anayofanya ya  kutatua migogoro mbalimbali katika jamii  kwa njia ya mardhiano.
Posted by MROKI On Saturday, June 06, 2026 No comments

June 05, 2026




Na Timothy Mwakyenda, Arusha
Mkurugenzi wa Idara ya Utalii kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Thereza Mugobi, amesema Maonesho ya Kimataifa ya Karibu-KiliFair 2026 yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuitangaza Tanzania kama kitovu cha utalii barani Afrika.

Maonesho hayo mbali na kutangaza utalii pia, yanatoa nafasi ya kuonesha vivutio mbalimbali vya utalii ikiwemo utalii wa misitu, kuimarisha ushirikiano wa wadau na kuvutia uwekezaji.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa maonesho hayo uliofanyika Juni 5, 2026 katika Viwanja vya Magereza mkoani Arusha, Dkt. Mugobi alisema Karibu-KiliFair imekuwa nyenzo muhimu ya kutangaza utajiri wa rasilimali za utalii zinazopatikana nchini na kufungua masoko mapya ya sekta hiyo.

Alisema maonesho hayo yanatoa fursa kwa taasisi za umma na sekta binafsi kuonesha bidhaa na huduma zao, kujenga mitandao ya kibiashara na kuimarisha ushirikiano unaochochea ukuaji wa sekta ya utalii.

“Karibu-KiliFair si maonesho ya kawaida bali ni uwekezaji wa kimkakati unaosaidia kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Tanzania, kuvutia wawekezaji wapya na kufungua masoko mapya ya bidhaa na huduma za utalii,” alisema Dkt. Mugobi.

Aliongeza kuwa maonesho hayo yanaendelea kuwakutanisha wadau wa utalii kutoka ndani na nje ya nchi, jambo linalochangia kuongeza mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Dkt. Mugobi alisema Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya utalii ikiwemo barabara, viwanja vya ndege na huduma za malazi ili kuongeza urahisi wa kufikia maeneo ya vivutio na kuboresha uzoefu wa watalii.

Pia alisisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia za kidijitali katika kuitangaza Tanzania kwenye masoko ya kimataifa, akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza mwonekano wa vivutio vya nchi na kuwafikia watalii wengi zaidi duniani.

Katika maonesho hayo, taasisi mbalimbali za umma na binafsi, ikiwemo Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), zinashiriki kutangaza huduma na fursa za uwekezaji zilizopo katika maeneo ya utalii wa mazingira na misitu ya hifadhi.

Karibu-KiliFair 2026 inaendelea kuthibitisha nafasi yake kama moja ya maonesho makubwa ya biashara ya utalii Afrika Mashariki, ikitoa jukwaa la kukuza ushirikiano, uwekezaji na utangazaji wa vivutio vinavyoifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa utalii barani Afrika.
Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Dodoma
WIZARA ya Madini imevuka lengo la ukusanyaji wa Maduhuli ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 baada ya kukusanya Sh trilioni 1.27 hadi Juni 5, 2026, dhidi ya lengo la Sh trilioni 1.2, huku ikitarajia kufikia Sh trilioni 1.3 ifikapo  Juni 30, 2026.

Kutokana na mafanikio hayo, watumishi wa Wizara hiyo na taasisi zake wametakiwa kuondokana na uzembe, kuongeza bidii na kufanya kazi kwa weledi ili kufikia lengo jipya la ukusanyaji wa Sh trilioni 1.4 lililowekwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Akizungumza katika kikao cha watumishi wote wa Wizara ya Madini na taasisi zake ambazo ni GST, TEITI, Tume ya Madini, STAMICO na TGC, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, amesema mafanikio yaliyopatikana yanapaswa kuwa chachu ya kuongeza juhudi katika usimamizi wa Sekta ya Madini kwa kuzingatia Sera, miongozo, kanuni na Sheria zilizowekwa.

Amesema watumishi wanapaswa kutambua kuwa wanapowahudumia wananchi wanatekeleza wajibu wenye thamani kubwa kwa taifa, hivyo wanapaswa kuwahudumia watu wote kwa usawa bila kujali itikadi, dini wala uraia wao.

“Wachache tuliokabidhiwa jukumu la kuhudumia sekta ya madini tunapaswa kuhakikisha watu wote wanahudumiwa kwa haki na uzalendo mkubwa ili kuendelea kujenga taifa letu,” amesema.

Amesema watumishi ndiyo injini ya Serikali katika sekta ya madini na kwamba mchango wao una nafasi muhimu katika kukuza uchumi wa nchi kupitia usimamizi bora wa rasilimali madini.

“Wito wangu ni kufanya kazi kwa bidii, weledi na kusimamia sera, miongozo, kanuni na sheria zilizowekwa ili sekta hii iendelee kutoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya taifa,” amesema.

Katibu Mkuu huyo amesema watumishi wanapaswa kujiepusha na vitendo vya rushwa, uvivu na uzembe ambavyo vinaweza kuharibu imani ya wananchi kwa wizara, taasisi zake na Serikali kwa ujumla.

“Tusiharibu imani ya wananchi kwa rushwa, uvivu na uzembe. Mtu mmoja anayepokea rushwa anaweza kuchafua kazi za watumishi wengi waadilifu. Tufanye kazi kwa uzalendo mkubwa ili kuhakikisha hakuna mtu au wachache miongoni mwetu wanaochafua taswira ya wizara, taasisi zetu na Serikali kwa ujumla,” amesema.

Amesema watumishi wanapaswa kuchagua kuwa mwangaza badala ya kuwa kivuli na kuendelea kuimarisha ushirikiano baina ya wizara na taasisi zake kwa kuwa wote ni timu moja yenye malengo yanayofanana.

“Kazi ya mwenzako ikichelewa, mafanikio yako pia yanachelewa. GST ikichelewa kutekeleza majukumu yake, Tume ya Madini nayo itaathirika. Tusaidiane kwa pamoja kufikia malengo yetu,” amesema.

Katika salamu za Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, watumishi wamepongezwa kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Aidha, imeelezwa kuwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini imepangiwa kukusanya Sh trilioni 1.4, lengo ambalo linahitaji watumishi kuongeza uwajibikaji, uadilifu na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao.
Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments











Na, mwandishi wetu – Mwanza
SERIKALI imezindua rasmi Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha Mkoa wa Mwanza, hatua inayolenga kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa na majanga katika mkoa huo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo leo tarehe 05 Juni, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa Said Mtanda, amesema kituo hicho ni nyenzo muhimu katika kufuatilia na kudhibiti matukio ya dharura kwa ufanisi zaidi. 

Amesema kupitia kituo hicho, mkoa unaweza kufuatilia matukio ya dharura kwa karibu, kukusanya na kuchambua taarifa kwa wakati pamoja na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau mbalimbali wa usimamizi wa maafa.

“Kupitia kituo hiki, taarifa muhimu zinafika kwa mamlaka husika kwa haraka ili kuwezesha maamuzi stahiki kufanyika kwa wakati,” anasema Mhe.Mtanda.

Ameongeza kuwa kituo hicho kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hatua inayorahisisha mtiririko wa taarifa na kuimarisha uratibu wa shughuli za kukabiliana na maafa kati ya ngazi ya mkoa na taifa.

Kwa mujibu wa Mhe. Mtanda, hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za serikali kujenga mfumo jumuishi wa usimamizi wa maafa wenye uwezo wa kutoa mwitikio wa haraka na wenye ufanisi katika kukabiliana na majanga.

Aidha, amewataka watumishi na viongozi kutumia mafunzo wanayopata kujenga uelewa, kubadilishana uzoefu na kuimarisha mshikamano wa kiutendaji ili kuboresha zaidi usimamizi wa maafa katika Mkoa wa Mwanza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, amesema kituo hicho kina umuhimu mkubwa kwa mkoa wa Mwanza na taifa kwa ujumla.

Amesema kituo hicho kinakuwa kitovu cha ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji wa taarifa za matukio ya dharura na maafa, ambapo kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hivyo kuwezesha upatikanaji wa taarifa kwa wakati na kufanya maamuzi ya haraka na sahihi.

“Kupitia kituo hiki, Serikali inaweza kufuatilia vihatarishi mbalimbali, kutoa tahadhari za mapema, kuratibu rasilimali za kukabiliana na maafa na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau wote wanaohusika na usimamizi wa maafa,”alisema.

Ameongeza kuwa, “Huu ni uwekezaji muhimu katika kuimarisha utayari wa mkoa na taifa kwa ujumla. Sambamba na hilo, timu ya mkoa ya kukabiliana na dharura tunayoizindua leo ndiyo nguzo kuu ya kukabiliana na matukio ya maafa kwa wakati.”

Vilevile amesema uzinduzi wa kituo hicho unakuja katika wakati muafaka ambapo serikali inaendelea kujiandaa na kuimarisha mifumo ya tahadhari ya mapema kufuatia taarifa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kuhusu uwezekano wa kutokea kwa hali mbaya ya hewa, ikiwemo athari zinazoweza kusababishwa na El Niño.
Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo