Nafasi Ya Matangazo

June 12, 2026








Na, mwandishi wetu - Arusha
SERIKALI imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuzingatia misingi ya uadilifu katika utumishi wa umma ili kuhakikisha utekelezaji wa majukumu na mipango ya maendeleo unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia maadili ya kazi.

Hayo yamesemwa hii leo (12 Juni, 2026) na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, wakati akifungua Mafunzo ya Kamati ya Uadilifu yaliyolenga kuwajengea uwezo wajumbe wa Kamati Maalum ya Menejimenti katika kusimamia masuala ya uadilifu katika ofisi hiyo.

“Uadilifu ni nguzo muhimu katika ufanikishaji wa majukumu na utekelezaji wa mipango ya maendeleo katika sehemu za kazi,” amesema Dkt. Yonazi.

Dkt. Yonazi amesema kuwa ni wajibu wa kila mtumishi wa umma kuhakikisha anazingatia maadili ya kazi na kulinda misingi ya uadilifu ili kuimarisha utendaji na kuongeza imani ya wananchi kwa Serikali.

Aidha, Dkt. Yonazi amesema mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha wajumbe kusimamia utekelezaji wa Mkakati wa Uadilifu kwa kuhakikisha unaingizwa katika mipango kazi na bajeti za mwaka za taasisi.

Vilevile, amebainisha kuwa Kamati za Uadilifu zina jukumu la kusimamia utekelezaji wa sera dhidi ya rushwa na kuhakikisha watumishi wanazingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma. 

“Kuna umuhimu wa kuimarisha uwazi na uwajibikaji pamoja na kuanzisha mifumo madhubuti ya kupokea na kushughulikia malalamiko ya wananchi kwa kuzingatia usiri.

Akiwasilisha mada ya masuala ya Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji (NACSAP IV) 2023-2030 Mkurugenzi kutoka Ofisi ya Rais Ikulu Bw. Andrew Massawe amesema, ni wajibu wa watumishi kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na kupinga vitendo vyote vinavyoashiria mazingira ya rushwa ili kuendelea kuhudumia wananchi, na Taifa kwa ujumla katika misingi sahihi ya utumishi wa umma.

“Tufanye kazi kwa uadilifu na kuzingatia masuala ya huduma bora kwa wateja, tusihudumie watu kama favor bali tutoe huduma kwa viwango bora vinavyotakiwa,”alisema Bw. Massawe
Posted by MROKI On Friday, June 12, 2026 No comments








Na Oscar Nkembo
Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Mhe. Naitapwaki Tukai, amewataka wachimbaji wa dhahabu kuzingatia usimamizi na matumizi salama ya Kemikali ili kuepukana na madhara ya kemikali yanayoweza kuathiri afya za wananchi na mazingira.

Mkuu wa Wilaya, Tukai amesema hayo Juni 12, 2026 wakati akifungua mafunzo ya usimamizi na matumizi salama ya Kemikali kwa wachimbaji wadogo wa Nzega na tabora yaliyoandaliwa na Ofisi ya Kanda ya Kati ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na kufanyika wilayani Nzega Mkoa wa Tabora.

“Inaumiza sana kupoteza nguvu kazi kwa uzembe wa kutozingatia mafunzo haya, Afya ni mtaji namba moja, tufanye uchimbaji tutumie kemikali kwa kuzingatia yale tunayoelekezwa na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ili tuweze kulinda afya za watu na mazingira” alisema Tukai.

Naye Meneja wa Kanda ya Kati ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Magdalena Mtenga, amesema Mamlaka inahakikisha inawawezesha wananchi kwenye shughuli zao wakiwa salama kiafya pamoja na Mazingira yao kwa kuhakikisha taratibu na kanuni za matumizi salama ya kemikali yanazingatiwa.

“Mamlaka imekuwa rafiki na taasisi wezeshi kwa wananchi ili kufanikisha shughuli zao huku wakiwa salama na kuayaacha mazingira yakiwa salama, Kemikali ni muhimu zinatusaidia kuingiza kipato binafsi na pato la Taifa lakini lazima tuzingatia usimamizi na matumizi salama ya hizo Kemikali ili zisilete madhara” alisema Mtenga.

Aidha, Wadau wa Kemikali wameipongeza Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kwa kuwekeza katika teknolojia ikiwemo mfumo wa wa usajili wa wadau wa kemikali kwani mfumo huo umekuwa mkombozi mkubwa kwao kwenye shughuli mbalimbali za usajili na upatikanaji wa vibali vya Kemikali.

“Mfumo wa usajili wa wateja wa kemikali umerahisisha sana kazi na kuokoa muda na fedha, kwa sababu huhitaji kwenda ofisini, bali kwa njia ya mtandao tu unaweka nyaraka
Posted by MROKI On Friday, June 12, 2026 No comments

June 11, 2026



Na, Mwandishi Wetu - Dodoma
KATIKA kuendelea kuimarika kwa sekta ya usimamizi wa maafa nchini na kuongezeka kwa hamasa ya kujifunza mifumo ya usimamizi wa maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura, wanafunzi wa Shahada ya Usimamizi wa Hatari za Maafa kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wamefanya ziara ya mafunzo kupitia Idara ya Usimamizi wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu).

Ziara hiyo imefanyika tarehe 10 na 11 Juni, 2026 iliyolenga kuwajengea uelewa kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa, ufuatiliaji wa vihatarishi mbalimbali, utoaji wa taarifa za tahadhari ya mapema pamoja na uratibu wa operesheni za dharura nchini.

Katika ziara hiyo, wanafunzi walitembelea Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kilichopo Ngome, Chumba cha Ufuatiliaji wa Mienendo ya Majanga na Tahadhari za Mapema kilichopo Mtumba pamoja na eneo la ujenzi wa Kituo Kikuu cha Taifa cha Usimamizi wa Maafa na Maghala ya Kuhifadhi Vifaa vya Dharura kilichopo Nzughuni, jijini Dodoma.

Akizungumza na wanafunzi hao, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Dkt. Jim Yonazi, aliwapongeza kwa uamuzi wao wa kujifunza kwa vitendo kuhusu masuala ya usimamizi wa maafa na kuonesha dhamira ya kuchangia maendeleo ya sekta hiyo nchini.

Dkt. Yonazi aliwahimiza wanafunzi kuendelea kujiongezea maarifa kupitia tafiti, ubunifu na uandishi wa machapisho mbalimbali kuhusu usimamizi wa hatari za maafa ili kuchangia katika kuimarisha uwezo wa Taifa wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa. 

Aidha, aliwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za elimu ya juu katika kukuza taaluma ya usimamizi wa maafa na kuahidi kutembelea Chuo Kikuu cha Dodoma siku zijazo kwa ajili ya kutoa mihadhara na kushiriki katika mijadala ya kitaaluma.

“Ziara yenu ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu ya juu na Serikali katika kujenga kizazi cha wataalamu wenye uelewa wa kina kuhusu usimamizi wa hatari za maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura. Aidha, inaonesha mafanikio ya uwekezaji uliofanywa na Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa, jambo ambalo limeendelea kuvutia wadau mbalimbali, watafiti na wanafunzi kutoka ndani na nje ya nchi kujifunza na kubadilishana uzoefu,”alisema Dkt. Yonazi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, aliwaeleza wanafunzi hao kuwa wamefanya jambo la msingi kwa kutenga muda wa kujifunza na kushuhudia kwa vitendo namna Serikali inavyotekeleza majukumu yake ya usimamizi wa maafa nchini.

Alisema kuwa mifumo iliyowekwa na Serikali katika ufuatiliaji wa vihatarishi, utoaji wa tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao dhidi ya madhara yatokanayo na maafa mbalimbali.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Bi. Jane Alfred Kikunya, ambaye aliongoza mafunzo hayo, alisema ameridhishwa na hamasa na ari kubwa iliyooneshwa na wanafunzi katika kujifunza masuala ya usimamizi wa maafa na tahadhari ya mapema.

Bi. Jane alieleza kuwa ujio wa wanafunzi hao unaonesha namna sekta ya usimamizi wa maafa inavyoendelea kupata umuhimu katika jamii na taasisi za elimu ya juu. Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kufungua milango kwa wanafunzi, watafiti na wadau mbalimbali wanaotaka kujifunza kuhusu mifumo ya ufuatiliaji wa majanga, uchambuzi wa vihatarishi, tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura kutembelea ofisi hiyo.

Kwa upande wake, Dkt. Japhet Ringo kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma ambaye aliambatana na wanafunzi hao, aliishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuwapatia wanafunzi fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa nchini.

Dkt. Ringo alisema kuwa ziara hiyo imekuwa darasa muhimu lililowawezesha wanafunzi kuunganisha maarifa ya kinadharia wanayojifunza darasani na utekelezaji halisi wa shughuli za usimamizi wa maafa katika ngazi ya Taifa.

Aliongeza kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kukuza tafiti, ubunifu na maendeleo ya taaluma ya usimamizi wa hatari za maafa ili kusaidia juhudi za Taifa za kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.


Posted by MROKI On Thursday, June 11, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akifuatilia Hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/2027, kupitia Televisheni ya Taifa (TBC1), Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 11 Juni, 2026. Bajeti hiyo ilikuwa ikisomwa Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, kwenye Bunge la 13, Mkutano wa tatu katika Kikao cha 48 Jijini Dodoma. 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipiga makofi pamoja na Wasaidizi wake mara baada ya Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar kumaliza kuwasilisha Hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/2027 kwenye Bunge la 13, Mkutano wa tatu katika Kikao cha 48 Jijini Dodoma. Rais Dkt. Samia alikuwa akifuatilia Hotuba ya Bajeti hiyo Kuu ya Serikali kupitia Televisheni ya Taifa (TBC1), Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 11 Juni, 2026.






Posted by MROKI On Thursday, June 11, 2026 No comments



Dodoma
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, amefanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Marvel Gold ya Australia, Timothy Strong, jijini Dodoma ambapo amepokea taarifa kuhusu maendeleo ya hatua za awali za mradi wa mgodi wa dhahabu unaoendelezwa katika Wilaya ya Hanang’, Mkoa wa Manyara.

Akizungumza katika kikao hicho, Strong amesema kuwa kampuni hiyo inaishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi yaliyowezesha kufanikisha uwekezaji huo.

Ameeleza kuwa baada ya kukamilisha hatua ya awali ya utafiti kwa kutumia teknolojia ya ndege nyuki (drones), kampuni imeingia katika hatua ya pili ya uchorongaji, huku awamu ya kwanza ya shughuli hizo ikitarajiwa kukamilika mwishoni mwa Julai 2026.

“Shabaha yetu ni kuanza mara moja shughuli za uchimbaji pindi ambapo taratibu zote zitakapokamilika kwa mafanikio,” amesema Strong.

Kwa upande wake, Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira bora na kuvutia uwekezaji unaochochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Waziri Mavunde ameipongeza Kampuni ya Marvel Gold kwa kasi ya utekelezaji wa mradi huo mpya wa dhahabu katika Mkoa wa Manyara, akieleza kuwa kukamilika kwake kutachochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika Wilaya ya Hanang’, Mkoa wa Manyara na Tanzania kwa ujumla.

“Ni matarajio yetu kwamba mradi huu utakuwa chachu ya maendeleo kwa wananchi wa Hanang’ na Mkoa wa Manyara, sambamba na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa Taifa. Serikali itaendelea kushirikiana na wawekezaji mbalimbali ili kuhakikisha sekta ya madini inaendelea kutoa mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa Tanzania,” amesema Waziri Mavunde.
Posted by MROKI On Thursday, June 11, 2026 No comments





Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Babati na Mkuu wa Wilaya ya Kiteto, Mheshimiwa Remidius Mwema, leo tarehe 10 Juni 2026, ameongoza kikao maalum cha Kamati ya Mwenge wa Uhuru Wilaya ya Babati kilicholenga kujadili na kuratibu maandalizi ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru mwaka 2026.

Kikao hicho kimewakutanisha viongozi na watendaji kutoka Halmashauri ya Mji wa Babati (Babati TC) pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Babati (Babati DC), ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa vikao vya maandalizi vinavyoendelea kufanyika kuelekea mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mhe. Mwema amepongeza juhudi na ushirikiano unaoendelea kuoneshwa na halmashauri zote mbili katika maandalizi ya tukio hilo muhimu la kitaifa. Aidha, amesisitiza umuhimu wa kufanya maandalizi ya kina na kwa wakati ili kuhakikisha shughuli zote zinazohusiana na mbio za Mwenge wa Uhuru zinafanyika kwa ufanisi na mafanikio makubwa katika wilaya nzima.

Kikao hicho ni sehemu ya mfululizo wa mikutano na vikao vya uratibu vinavyoendelea kufanyika kwa lengo la kuhakikisha Wilaya ya Babati inakuwa tayari kupokea na kushiriki kikamilifu katika mbio za Mwenge wa Uhuru 2026
Posted by MROKI On Thursday, June 11, 2026 No comments

June 10, 2026

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati wa Mkutano wake na wanahabari kuhusu Mwelekeo wa Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2026/27, katika Ukumbi wa Kambarage, Treasury Square jijini Dodoma, ambayo itasomwa Bungeni Dodoma Siku ya Alhamisi, tarehe 11 juni 2026, ambapo alisema Bajeti hiyo itakuwa ya kipekee kwa kuwa ndiyo bajeti ya kwanza kutumika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2026/27–2030/31) pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), akizungumza wakati wa Mkutano wake na wanahabari kuhusu Mwelekeo wa Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2026/27, katika Ukumbi wa Kambarage, Treasury Square jijini Dodoma, ambayo itasomwa Bungeni Dodoma Siku ya Alhamisi, tarehe 11 juni 2026, ambapo alisema Bajeti hiyo itakua ya kipekee kwa kuwa ndiyo bajeti ya kwanza itakayotumika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2026/27–2030/31) pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025. Wengine katika picha ni Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba (kushoto) na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bw. Elijah Mwandumbya.




Na Eva Valerian, WF, Dodoma
Serikali imesema Bajeti Kuu ya mwaka wa fedha 2026/27 ni ya kipekee kwa kuwa ndiyo bajeti ya kwanza itakayotumika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2026/27–2030/31) pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025.
 
Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mwelekeo wa Bajeti Kuu ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, katika Ukumbi wa Kambarage, Treasury Square jijini Dodoma, Bajeti ambayo itasomwa Bungeni Dodoma Siku ya Alhamisi, tarehe 11 juni 2026.
 
Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, Serikali inatarajia kutumia jumla ya shilingi trilioni 62.3 katika mwaka wa fedha 2026/27, ambapo sehemu kubwa ya fedha hizo itaelekezwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya kimkakati inayochochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.
 
“Fedha hizi zitaelekezwa katika kuendelea na ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), kuboresha mtandao wa barabara, kuimarisha huduma za maji, kuendeleza miradi ya nishati pamoja na uwekezaji katika rasilimali watu na maendeleo ya ujuzi,” alisema Mhe. Balozi Omar.
 
Aidha, alisema kuwa bajeti hiyo imeandaliwa kwa lengo la kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, kuongeza ajira, kuvutia uwekezaji na kuimarisha ustawi wa wananchi na Serikali inatarajia kukusanya mapato ya ndani ya shilingi trilioni 46.8 ili kugharamia sehemu kubwa ya matumizi yaliyopangwa katika bajeti hiyo.
 
Mhe. Balozi Omar aliongeza kuwa, kabla ya kuwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya mwaka 2026/27, Serikali itatoa tathmini ya utekelezaji wa Bajeti ya mwaka 2025/26, akibainisha kuwa ukusanyaji wa mapato ya ndani umeendelea kufanya vizuri na kufikia malengo yaliyowekwa.

Aliongeza kuwa, Serikali imeendelea kushirikisha wadau mbalimbali katika mchakato wa maandalizi ya bajeti kupitia Kamati ya Wataalam wa Maboresho ya Kodi (Task Force on Tax Reforms) pamoja na Kamati ya Ushauri ya Ngazi ya Juu ya ‘Think Tank’, hatua ambayo imeongeza uwazi na ushirikishwaji katika maamuzi ya sera za kodi.
 
“Upande wa maboresho ya kodi, Serikali imepokea jumla ya mapendekezo 727 kutoka kwa wadau mbalimbali wakiwemo sekta binafsi, taasisi za elimu, jumuiya za wafanyabiashara, mashirika yasiyo ya kiserikali na wananchi binafsi, ambapo kati ya mapendekezo hayo, 125 yalikubaliwa kama yalivyowasilishwa, 121 yalifanyiwa maboresho na kukubaliwa, huku 295 yakikataliwa baada ya kufanyiwa uchambuzi wa kina” alisema Mhe. Balozi Omar
 
Mhe Balozi Omar aliongeza kuwa, Lengo la maboresho hayo ni kukuza uchumi, kuongeza ajira, kupanua wigo wa kodi kwa kuvutia uwekezaji zaidi na wakati huo huo kupunguza mzigo wa kodi kwa walipakodi.
 
Mhe. Balozi Omar, alitumia fursa hiyo kuwapongeza waandishi wa habari kwa mchango wao mkubwa katika kuhabarisha umma kuhusu masuala ya maendeleo na kusisitiza umuhimu wa wananchi kuendelea kutimiza wajibu wao wa kulipa kodi kwa hiari na kwa wakati.
 
“Tunajenga Taifa letu kwa pamoja. Serikali itaendelea kuhakikisha fedha zinazokusanywa zinatumika kwa ufanisi na kuleta matokeo chanya kwa wananchi,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Alitumia fursa hiyo kuwataka Watanzania kufuatilia kwa makini uwasilishaji rasmi wa Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/27 utakaofanyika Bungeni jijini Dodoma Juni 11, 2026, akisema bajeti hiyo imeandaliwa kwa kuzingatia matarajio ya wananchi na mahitaji ya maendeleo ya taifa.


Posted by MROKI On Wednesday, June 10, 2026 No comments

Waziri wa Afya, Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa, ameitaka Bodi mpya ya Ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mt. Meru kuongoza kwa mtazamo wa mageuzi na kusukuma mbele mabadiliko yenye tija yatakayoboresha utoaji wa huduma za afya na matokeo ya afya kwa wananchi wa Mkoa wa Arusha na Tanzania kwa ujumla.
 
Akizungumza katika hafla rasmi ya uzinduzi wa Bodi ya Ushauri ya hospitali hiyo iliyofanyika leo katika Hoteli ya Kibo Palace jijini Arusha, Mheshimiwa Mchengerwa alisema sekta ya afya nchini inaingia katika hatua mpya ambapo mafanikio ya viongozi yatapimwa kwa matokeo halisi na mchango wao katika kuboresha maisha ya wananchi badala ya taratibu za kiutawala pekee.
 
“Leo si uzinduzi wa Bodi pekee. Ni uzinduzi wa matarajio mapya, kiwango kipya cha uongozi na sura mpya ya utoaji wa huduma za afya katika Arusha na Tanzania kwa ujumla,” alisema Mheshimiwa Mchengerwa. 

Waziri Mchengerwa aliwapongeza Mwenyekiti na Wajumbe wapya wa Bodi kwa kuteuliwa kushika nafasi hizo muhimu, akisisitiza kuwa uteuzi wao unaambatana na wajibu mkubwa wa kusimamia moja ya hospitali muhimu za rufaa nchini inayohudumia maelfu ya Watanzania wanaohitaji huduma bora, salama na za wakati.
 
KUSUKUMA MAGEUZI YA SEKTA YA AFYA
Mchengerwa alisisitiza dhamira ya Serikali ya kuharakisha mageuzi katika sekta ya afya na kuitaka Bodi hiyo kwenda zaidi ya majukumu ya kawaida ya usimamizi na kuwa chachu ya ubunifu, uwajibikaji na ubora wa taasisi.
 
“Sikuja Wizara ya Afya kusimamia mifumo iliyopo. Nimekuja kuharakisha mabadiliko,” alisema. Alieleza kuwa taasisi za afya zinapaswa kuongozwa kwa kuzingatia matokeo, kutumia takwimu katika kufanya maamuzi, kuweka mgonjwa katikati ya huduma, na kuwajibika katika kuhakikisha uwekezaji wa fedha za umma unaleta manufaa kwa wananchi.
 
Waziri Mchengerwa aliitaka Bodi kufuatilia kwa karibu utendaji wa hospitali, kuuliza maswali muhimu na kuhakikisha uongozi wa hospitali unaendelea kuzingatia maboresho yanayopimika katika utoaji wa huduma.
 
MSISITIZO WA MATOKEO YANAYOPIMIKA
Mojawapo ya ujumbe muhimu katika hotuba ya Waziri ulikuwa ni umuhimu wa usimamizi unaozingatia matokeo. Aliwahimiza wajumbe wa Bodi kuzingatia viashiria vya utendaji kama vile kupungua kwa vifo vya akina mama wajawazito, kuongezeka kwa kuridhika kwa wagonjwa, kupungua kwa muda wa kusubiri huduma, kuongezeka kwa mapato ya ndani ya hospitali, na kuboreshwa kwa ubora wa huduma.
 
“Hatupaswi kupima mafanikio kwa kiasi cha fedha kilichotumika. Tunapaswa kupima mafanikio kwa maisha yaliyookolewa,” alisema Mheshimiwa Mchengerwa.
 
Aidha, alisisitiza matumizi ya takwimu na ushahidi katika kufanya maamuzi na kuendesha maboresho endelevu katika shughuli zote za hospitali.
KUWEKA MGONJWA KATIKATI YA HUDUMA
 Waziri Mchengerwa alithibitisha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha wagonjwa wanabaki kuwa kitovu cha utoaji wa huduma za afya.

Alieleza kuwa uwepo wa majengo bora na vifaa vya kisasa pekee hauwezi kuifanya hospitali kuwa yenye mafanikio ikiwa wagonjwa hawapati huduma zenye utu, huruma na taaluma.
 
“Kipimo halisi cha mafanikio ya hospitali si ukubwa wa majengo yake. Ni kiwango cha imani ambacho wananchi wanakiweka katika hospitali hiyo,” alisema.
 
Mheshimiwa Mchengerwa alitoa wito wa kuboresha huduma kwa wagonjwa katika maeneo yote ya utoaji huduma ikiwemo mapokezi, maabara, maduka ya dawa, wodi na vitengo vya huduma za dharura.
 
KUKUMBATIA UBUNIFU WA KIDIJITALI.
Akizungumzia nafasi ya teknolojia katika mageuzi ya sekta ya afya, Waziri aliitaka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mt. Meru kuwa kinara wa ubunifu wa kidijitali katika huduma za afya.
 
Alitaja matumizi ya kumbukumbu za afya za kidijitali, huduma za tiba kwa njia ya mtandao (telemedicine), na mifumo ya kidijitali ya usimamizi wa dawa, fedha, vifaa tiba na huduma kwa wagonjwa kuwa miongoni mwa maeneo muhimu ya kupewa kipaumbele. 
 
“Hospitali ya karne ya 21 haiwezi kuendeshwa kwa mifumo ya karne iliyopita,” alisema.
 
KUIMARISHA USHIRIKIANO WA KIMKAKATI
Akigusia umuhimu wa Mkoa wa Arusha kama kitovu cha biashara, utalii, diplomasia na uwekezaji, Mheshimiwa Mchengerwa aliihimiza Bodi kujenga ushirikiano na sekta binafsi, taasisi za elimu ya juu, washirika wa maendeleo na taasisi za utafiti.
 
Alisema ushirikiano wa kimkakati unaweza kufungua fursa za rasilimali zaidi, utaalamu na teknolojia zitakazosaidia kuimarisha huduma za afya na kunufaisha jamii.
 
DHAMIRA YA KUBORESHA MATOKEO YA AFYA
Katika hitimisho la hotuba yake, Waziri Mchengerwa aliwakumbusha wajumbe wa Bodi kuwa maamuzi yao yana athari za moja kwa moja kwa wagonjwa na familia zinazotegemea hospitali hiyo kupata huduma.
“Kila uamuzi mnaoufanya unaweza kuokoa maisha. Kila ubunifu mnaouanzisha unaweza kuboresha huduma. Kila mfumo mnaouimarisha unaweza kurejesha matumaini ya wananchi,” alisema.
 
Mchengerwa alieleza imani yake kuwa chini ya uongozi wa Bodi mpya, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mt. Meru itaendelea kuwa mfano wa kitaifa wa ubora, ubunifu, uwajibikaji na mageuzi ya sekta ya afya kwa kuendana na Ajenda ya Mageuzi ya Afya Tanzania 2023–2030.
 
Waziri Mchengerwa alitangaza rasmi uzinduzi wa Bodi ya Ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mt. Meru, hatua inayofungua ukurasa mpya wa uongozi na mageuzi kwa moja ya taasisi muhimu zaidi za afya Kaskazini mwa Tanzania.

Posted by MROKI On Wednesday, June 10, 2026 No comments



WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuondoa vikwazo na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ili kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Ameyasema hayo leo (Jumatano, Juni 10, 2026), wakati akizindua ghala la forodha la kampuni ya Ciwaye Trading Co. Ltd Wilayani Chamwino mkoani Dodoma.

“Kama tunavyoheshimu sekta ya umma, tunatakiwa kuheshimu sekta binafsi kwa uzito ule ule, kama mataifa mengine yaliyoendelea, uchumi wa mataifa hayo nguzo yake ni sekta binafsi.”

Dkt. Mwigulu aliongeza kwa kusema “Kwa kuheshimu hilo, nimeona nije kuzindua mradi huu, kama ambavyo nimepita kwenye ziara kuzindua miradi ya Serikali, ndiyo maana nimeona na hapa nije mwenyewe.”

Aidha, ameeleza kuwa mradi huo una umuhimu mkubwa katika maendeleo ya nchi, hivyo hauna budi kulelewa.

“Ukubwa wa jambo hili haupimwi kwa majengo, bali kwa uthubutu na matokeo yanayoakisi Dira yetu ya maendeleo na maono ya Rais wetu ya kuhakikisha mradi kama huu unatoa matokeo yaliyokusudiwa.” Amesisitiza Waziri Mkuu Mwigulu.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa mradi huo unatazamwa na Serikali kama mradi wa kielelezo wa kutekeleza Dira 2050 na ndiyo maana Serikali imekuwa ikiboresha mazingira ya uwekezaji nchini, ikiwemo maboresho ya sheria za uwekezaji.

“Zimebadilishwa Sheria za uwekezaji ili kuhakikisha wazawa wananufaika na kuushika uchumi, zamani vivutio vya uwekezaji viliwanufaisha wageni, lakini sasa wazawa wanapata vivutio hivyo,” ameeleza Waziri Mkuu.

Ameongeza kuwa: “Mfano katika sekta ya uzalishaji, zamani miradi yote mikubwa ilikuwa inatekelezwa na wageni, lakini mabadiliko hayo ya sheria yamewezesha wazawa kutekeleza miradi mikubwa, na sasa wanaweza kuajiri wageni katika utekelezaji wa miradi hiyo.”

Waziri Mkuu Mwigulu amesema mkakati mwingine unaoenda sambamba na mabadiliko ya sheria, ni pamoja na kuondoa zaidi ya tozo 270 ili kuwapunguzia mzigo wafanyabiashara na walaji wa mwisho.

Akizungumzia utekelezaji wa mradi huo, Waziri Mkuu ameeleza kufurahishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wake, kwani umetekelezwa ndani ya muda mfupi lakini viwango vya ubora vimezingatiwa.

Amesema uamuzi wa kuanzisha ghala hilo mkoani Dodoma ni wa kimkakati kwani Dodoma ipo katikati ya nchi, ikiunganisha maeneo mengine ya nchi na fursa zilizopo katika maeneo hayo, ambapo amewataka wafanyakazi wa mradi huo kuwa waaminifu ili mradi uwe na faida endelevu, kwao binafsi na jamii.

Pia Waziri Mkuu Mwigulu amewahimiza Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhamasisha wawekezaji kuwekeza kwenye mikoa na maeneo yao kwa kuweka miundombinu inayochochea vyanzo vya mapato na kukua kwa uchumi.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Mwigulu ameuagiza Wakala wa Barabara za Mijini na Vijini (TARURA) kukaa kwa haraka na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na kufanya tathmini ya ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami ya kilometa 25 kuanzia Chamwino kwenda kituo cha treni cha Igandu ili kusaidia ufanisi wa ghala lililojengwa kwani barabara hiyo itaunufaisha mradi huo.
 
Kwa upande wake Meneja Masoko wa ghala hilo, Leroy Nelson amesema mradi huo umegharimu zaidi ya shilingi bilioni tatu ambapo utekelezaji wake umekamilika kwa asilimia 100.
Posted by MROKI On Wednesday, June 10, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo