Nafasi Ya Matangazo

April 18, 2026

Uamuzi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC),kuongeza safari za treni za SGR kutoka safari mbili  hadi nne kati ya Dar es Salaam na Morogoro si jambo la kawaida tu la ratiba bali ni ishara kubwa ya mabadiliko ya kiuchumi, kimkakati na kiutendaji.
 
Mosi,  Ongezeko la mahitaji ya abiria (Demand-driven decision), kuongeza safari maana yake ni kwamba, Idadi ya abiria imeongezeka sana na huduma ya SGR imekubalika na wananchi. Kwa mfano, tayari SGR imeonyesha mafanikio makubwa kwa kubeba mamilioni ya abiria na kurahisisha usafiri

Tafsiri yake ni kwamba, TRC haiongezi safari bila sababu bali ni muitikio wake kwa soko.

Pili, Kuboresha upatikanaji wa huduma (Service accessibility), awali safari mbili zilikuwa hazimpi nafasi abiria kuwa na machaguo ya safari   hivyo ilikuwa kwamba

abiria akikosa  treni ya asubuhi ama jioni basi atasubiri muda mrefu.
Kuongeza treni hizo kufikia nne, kunampa machaguo mengi zaidi kwa abiria,  ikiwemo urahisi wa kupanga safari kulingana na muda wa kazi/shughuli husika.

Aidha, hii inaifanya reli, kuwa rafiki kwa wafanyakazi na kuwa  mbadala halisi wa mabasi na magari binafsi

Tatu, kuongezeka kwa ufanisi wa matumizi ya miundombinu, kama inavyofahamika, SGR ni uwekezaji mkubwa wa serikali (mabilioni ya fedha), hivyo kuuongeza safari za treni kati ya Jiji la Dar Es Salaam na Mkoa wa Morgoro, kunamaanisha kwamba, treni zinatumika muda mwingi zaidi na kwamba miundombinu haikai muda mwingi bila kutumika (idle)

Nne, athari chanya kiuchumi, kuwa na Safari nyingi zaidi  ni sawasawa na harakati nyingi zaidi za watu na hii  inasabaisha biashara kuongezeka kati ya Dar es salaam na Morogoro. Aidha ni fursa za ajira (moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja), Ukuaji wa miji, wakati tunaangalia matokeo ya kuongeza treni kati ya maeneo hayo mawili, SGR tayari inachochea biashara, ajira na utalii

Tano,. Kupunguza msongamano wa barabara na gharama za usafiri, kuwa na Safari nyingi za treni kuna maana kubwa sana kufanya barabaara kupumua kwa maana kwamba zinapunguza mabasi barabarani, zinapunguza ajali na uchakavu wa barabara lakini pia zinatoa usafiri wa haraka na wa gharama nafuu. Treni hubeba maelfu ya watu kwa safari moja tofauti na mabasi.

Sita, hatua kuelekea huduma ya “high-frequency rail system”, kuongeza safari ni hatua ya kuelekea mfumo wa kisasa wa reli (kama metro/intercity advanced systems).

Ratiba zinazokaribiana ni ishara kuwa: TRC inaelekea kwenye mfumo wa reli wa kisasa unaofanana na nchi zilizoendelea.
 
Kuongezeka kwa safari kutoka mbili  hadi nne,  kunamaanisha kuwa Mahitaji ya huduma yameongezeka, wananchi wana imani na SGR, uchumi unaanza kunufaika, na huduma inakuwa ya kisasa zaidi na rafiki kwa mtumiaji.


Posted by MROKI On Saturday, April 18, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula , amesema uandishi wa habari usiozingatia maadili unaweza kuhatarisha umoja wa kitaifa, amani na utulivu wa jamii.

Akizungumza na waandishi wa habari  ambao ni wanachama wa JUMIKITA, TADIO na TBN, leo Ijumaa Aprili 17, 2026 jijini Dar es Salaam, Kipangula alisema waandishi wa habari wanapaswa kutambua uzito wa nafasi yao katika jamii, hasa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya kijamii, kisiasa na kiuchumi, ambapo taarifa wanazozitoa zina athari kubwa kwa mwenendo wa jamii.

Alifafanua kuwa amani ni hali ya kutokuwepo kwa migogoro au vurugu, huku utulivu ukimaanisha usalama na uhakika wa maisha ya wananchi bila hofu, akibainisha kuwa hali hizi mbili haziwezi kudumu bila uwepo wa umoja wa kitaifa unaojengwa juu ya mshikamano wa wananchi bila kujali tofauti zao.
“Pale ambapo uandishi hauzingatii maadili, unaweza kuchochea migawanyiko, kupotosha ukweli na hatimaye kuvuruga mshikamano wa kitaifa. Hivyo, ni muhimu kwa waandishi wa habari kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji,” alisema Kipangula.

Alibainisha kuwa waandishi wa habari wana wajibu wa msingi wa kukusanya, kuchakata na kusambaza taarifa sahihi, pamoja na kusaidia kuunda mitazamo ya wananchi kwa njia inayochangia maridhiano na maendeleo ya jamii.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia Kanuni za Maadili ya Taaluma ya Uandishi wa Habari, akibainisha kuwa maadili hayo yanahimiza ukweli, usawa, uwazi na heshima kwa haki za binadamu, mambo ambayo ni msingi wa kulinda amani, kuimarisha utulivu na kukuza umoja wa kitaifa.
Posted by MROKI On Saturday, April 18, 2026 No comments

April 17, 2026

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa akijibu maswali bungeni jijini Dodoma leo Aprili 17, 2026.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa akisalimiana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) Mhe. Ridhiwani Kikwete bungeni jijini Dodoma leo Aprili 17, 2026. Kulia ni Naibu Waziri wa Maji Mhe. Mhandisi Kundo Mathew.
******************
Serikali imesema itaendelea kuimarisha juhudi za kuhakikisha wananchi wanapata uelewa wa kutosha na kushiriki kikamilifu katika biashara ya kaboni ili kunufaika kiuchumi huku wakichangia uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
 
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa amesema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu Mhe. Josephine Kapoma aliyetaka kujua Serikali ina mkakati gani wa kufikisha elimu kwa wananchi kuhusu biashara ya kaboni.
 
Akijibu swali hilo bungeni jijini Dodoma leo Aprili 17, 2026, Mhe. Kwagilwa alisema Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais na Kituo cha Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC) zimeweka mikakati mbalimbali ya kufikisha elimu kwa wananchi.
 
Alitaja mikakati hiyo kuwa ni kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu dhana, faida na fursa zilizopo katika biashara hiyo kupitia vyombo vya habari na kutoa mafunzo kwa viongozi wa ngazi za mikoa, halmashauri na vijiji ili waweze kuwa mabalozi wa elimu kwa jamii zao kuhusu utekelezaji wa miradi ya kaboni na manufaa yake.
 
“Tangu kupitishwa kwa Kanuni na Mwongozo wa Biashara ya Kaboni tumetoa elimu kwa viongozi mbalimbali pamoja na kushirikiana na wadau wa maendeleo, asasi za kiraia na sekta binafsi katika kutoa elimu na kujenga uwezo kwa jamii kuhusu namna ya kuanzisha na kunufaika na miradi ya kaboni,” alisema Mhe. Kwagilwa.
 
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Kwagilwa alisema kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinashirikiana katika kutekeleza miradi ya mazingira na kunufaisha wananchi wa pande zote mbili za Muungano.
 
Alisema hayo wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Jimbo la Amani Mhe. Abdul Yussuf Maalim aliyetaka kufahamu Zanzibar inanufaika vipi na biashara ya kaboni.
 
Akiendelea kujibu swali hilo, Mhe. Kwagilwa alisema pamoja na kushirikiana katika biashara ya kaboni pia Serikali zote mbili zinashirikiana katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
 
Ikumbukwe kuwa biashara ya kaboni ni mfumo wa kifedha unaoruhusu nchi, taasisi au miradi kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kupata faida kwa kuuza au kubadilishana hati za kaboni ambazo hutolewa unapofanikiwa kupunguza au kufyonza hewa ya kaboni.
Posted by MROKI On Friday, April 17, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Arusha
WANANCHI wa Kijiji cha Losimingor, wilayani Monduli mkoani Arusha, wanatarajiwa kunufaika kiuchumi na kijamii kupitia utekelezaji wa Mradi wa Kujenga Ustahimilivu wa Bioanuai za Misitu ya Mazingira Asilia dhidi ya Athari za Mabadiliko ya Tabianchi (BUREFOBI), unaolenga kuunganisha uhifadhi wa mazingira na maendeleo ya wananchi.

Mradi huo unatekelezwa katika vijiji vinavyopakana na Msitu wa Hifadhi ya Mazingira Asilia Essimingor, ukiwa na lengo la kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi huku ukiboresha maisha ya jamii kupitia miradi ya maendeleo endelevu.

Losimingor ni miongoni mwa vijiji sita vinavyonufaika na mradi huo, ambapo utekelezaji wake unatarajiwa kuleta mageuzi ya kiuchumi kupitia shughuli mbalimbali ikiwamo uimarishaji wa majosho ya mifugo, sekta inayobeba maisha ya wananchi wengi wa eneo hilo.

Mbali na ufugaji, mradi huo pia unafungua fursa mpya za kipato kupitia utalii shirikishi, ambapo jamii itanufaika moja kwa moja kwa kushiriki katika shughuli za utalii, ikiwemo kuanzishwa kwa kituo cha jamii cha kuuza bidhaa za utalii. Hatua hiyo inalenga kupanua wigo wa ajira na kupunguza utegemezi wa moja kwa moja wa rasilimali za misitu.

Akizungumza Aprili 16,2026 wakati wa ziara ya timu ya mradi wilayani Monduli, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Mwalimu Happiness Laizer, alisema halmashauri imejipanga kikamilifu kuhakikisha utekelezaji wa mradi unakuwa na tija kwa wananchi.

“Halmashauri ya Monduli inajivunia kuwa miongoni mwa wanufaika wa mradi huu. Tunaahidi tutatimiza wajibu wetu kikamilifu kadri tutakavyoelekezwa na wasimamizi wa mradi,” alisema.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Someni Mteleka, alisema ziara hiyo inalenga kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa miradi na kuhakikisha manufaa yaliyokusudiwa yanawafikia wananchi.

Alisisitiza kuwa TFS itaendelea kushirikiana na halmashauri za wilaya ili kuhakikisha miradi hiyo inaleta matokeo chanya kwa jamii, huku ikiimarisha uhifadhi endelevu wa misitu.

Naye mwakilishi wa Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Getrude Lyatuu, alisema ushirikiano kati ya taasisi hiyo na TFS utaendelea kuimarishwa ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa ufanisi na ushirikishwaji mpana wa jamii.

Alibainisha kuwa lengo kuu ni kuhakikisha makundi yote ya wananchi, wakiwemo wanawake na vijana, yanapata fursa sawa za kunufaika na miradi hiyo.

Ziara ya timu ya mradi inaendelea katika Mkoa wa Manyara, ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo pamoja na tathmini ya athari zake kwa wananchi na mazingira

Posted by MROKI On Friday, April 17, 2026 No comments





Na Mwandishi Wetu, Singida
Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), imeendesha mafunzo maalum kwa wachimbaji wadogo wa madini yenye lengo la kuongeza uelewa kuhusu uchimbaji salama, wenye tija na unaozingatia utunzaji wa mazingira.

Mafunzo hayo yamelenga kuwajengea wachimbaji uwezo katika matumizi ya teknolojia bora za uchimbaji, usimamizi wa afya na usalama migodini, uongezaji thamani wa madini pamoja na kuimarisha biashara ya madini kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za sekta ya madini.

Akifungua mafunzo hayo yaliyofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa huo, Mhandisi Sabai Nyansiri, amesema Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wachimbaji wadogo ili kuhakikisha sekta ya madini inachangia kikamilifu maendeleo ya wananchi na uchumi wa Taifa kwa ujumla.

Ameongeza kuwa mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuwawezesha wachimbaji wadogo kuongeza tija, kipato na kuendesha shughuli zao kwa kuzingatia misingi ya usalama, uhifadhi wa mazingira na uendelevu wa rasilimali madini.
Posted by MROKI On Friday, April 17, 2026 No comments
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Utalii, Biashara na Kilimo, Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Mhe. Dkt. Mohammed Ali Suleiman akizungumza wakati wa ziara ya mafunzo katika kituo cha kuhakiki vipimo Misugusugu, mkoani Pwani, Aprili 16, 2026.
Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Utalii, Biashara na Kilimo ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, wakiwa katika ziara ya mafunzo, Kituo cha vipimo Misugusugu, mkoani Pwani, Aprili 16, 2026.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo, Bw. Alban Kihulla akifafanua jambo kwa Wajumbe wa Kamati ya Utalii, Biashara na Kilimo ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, wakati wa ziara yao ya mafunzo katika Kituo cha Vipimo Misugusugu, mkoani Pwani, Aprili 16, 2026.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA), Bw. Alban Kihulla akiwaeleza Wajumbe wa Kamati ya Utalii, Biashara na Kilimo ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, namna Wakala hiyo inavyohakiki dira za maji, wakati wa ziara yao ya mafunzo katika Kituo cha Vipimo Misugusugu, mkoani Pwani, Aprili 16. 2026.

Wajumbe wa Kamati ya Utalii, Biashara na Kilimo ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, wakiwa katika ziara ya mafunzo, Kituo cha vipimo Misugusugu, mkoani Pwani, Aprili 16, 2026.
Wajumbe wa Kamati ya Utalii, Biashara na Kilimo ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, wakiwa katika ziara ya mafunzo, Kituo cha vipimo Misugusugu, mkoani Pwani, Aprili 16, 2026.
Wajumbe wa Kamati ya Utalii, Biashara na Kilimo ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, wakiwa katika ziara ya mafunzo, Kituo cha vipimo Misugusugu, mkoani Pwani, Aprili 16, 2026.
****************
Na Veronica Simba - WMA
Kamati ya Utalii, Biashara na Kilimo ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar, imekiri kuvutiwa na utendaji kazi wa Wakala wa Vipimo (WMA) Tanzania Bara na kuahidi kuweka mikakati ya makusudi itakayoisaidia Mamlaka inayosimamia vipimo nchini humo (ZAWEMA) kutekeleza majukumu yake kwa kiwango hicho au zaidi.

Akizungumza na waandishi wa habari mapema leo Aprili 16, 2026 baada ya ziara ya mafunzo katika Kituo cha Vipimo Misugusugu, mkoani Pwani, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. Mohammed Ali Suleiman, amesema Wakala wa Vipimo upande wa Tanzania Bara wamepiga hatua kubwa kiutendaji hivyo kuna kila sababu ya Zanzibar kufuata mfano huo.

“Tumeona wenzetu wamefanya kazi kubwa na wana vipimo vya kisasa ambavyo vinawawezesha kuhakiki mathalani kiwango cha maji anachotumia mteja ndicho anacholipia, halikadhalika kwenye umeme pamoja na vipimo vingine.”

Mhe. Dkt. Suleiman ameongeza kuwa, Kamati yake itaishauri Wizara ya Biashara ambayo ndiyo inayoisimamia Mamlaka ya Vipimo Zanzibar, kuweka mikakati ya makusudi ili kuiwezesha kutekeleza majukumu yake kikamilifu kwa manufaa ya wananchi.

Amesema wataishauri Serikali kuhakikisha ZAWEMA, ambayo ndiyo Mamlaka ya Vipimo kwa upande wa Zanzibar, kwanza inakuwa Mamlaka huru lakini pia ipate mitambo ya kisasa ya uhakiki vipimo na pia ishirikiane kwa ukaribu na WMA ili iweze kutekeleza majukumu yote kwa ufanisi.

“Ukiangalia, Kituo hiki cha Misugusugu kinaipatia Serikali ya Tanzania mapato makubwa sana. Ni muhimu Serikali yetu iwezeshe ZAWEMA kufanya kazi kwa karibu na WMA ili kupata mafanikio kama hapa,” amesisitiza Mhe. Dkt. Suleiman.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Bw. Alban Kihulla, amesema anaamini kwamba, kupitia ziara hiyo ya mafunzo kwa Kamati kutoka Baraza la Wawakilishi, jukumu la uhakiki na ukaguzi wa vipimo linaenda kuwa bora zaidi kwa pande zote mbili; Zanzibar na Tanzania Bara.

“Niwahakikishie tu kwamba tutaendelea kushirikiana na wenzetu wa Zanzibar ili kuhakikisha Mtoa Huduma analindwa lakini pia Mpokeaji Huduma analindwa.”

Akidadavua zaidi kuhusu ushirikiano uliopo kati ya WMA na ZAWEMA, Mtendaji Mkuu amesema Taasisi hizo mbili zilikwishasaini Hati ya Ushirikiano (MoU) kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo kushiriki kwenye mikutano ya kikanda na kimataifa pamoja na katika kaguzi za vipimo hususan katika bidhaa zilizofungashwa.

Amesema kuwa, WMA wakiwa ndiyo wenyeji katika ziara hiyo, wamewaonesha wageni wao utendaji kazi katika maeneo mbalimbali ikiwemo uhakiki wa tenki za kusafirishia mafuta, uhakiki wa mita za umeme pamoja na uhakiki wa dira za maji.

Wakala wa Vipimo Tanzania imekuwa ikipokea wageni mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuja kujifunza kuhusu majukumu ya uhakiki wa vipimo.

Aidha, kwa sasa, Wakala wa Vipimo Tanzania ndiye Mwenyekiti wa Jukwaa la Kikanda linaloratibu masuala ya kivipimo (legal metrology) kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADCMEL).   
Posted by MROKI On Friday, April 17, 2026 No comments

April 16, 2026



Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa - Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI), Ndg. Rabia Abdalla Hamid, amefanya Kikao kazi na Kansela wa Chama Cha Kikomunisti (CPC), Ubalozi wa China nchini Tanzania Ndg. Xu Sujiang leo tarehe 16.04.2026, Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba, Dar es Salaam.

Lengo la kikao hicho ni kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha uhusiano na itikadi za vyama hivyo.
Posted by MROKI On Thursday, April 16, 2026 No comments


Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema Serikali inaendelea na Marekebisho ya Mfumo wa Kidigitali wa  Leseni za Utafiti wa Madini utakaosimamia hatua zote za utoaji na usimamizi wa leseni hizo.

Amesema mfumo huo utahusisha utoaji wa leseni, uwasilishaji wa taarifa za kila robo mwaka, utoaji wa hati za makosa, na hata kufutwa kwa leseni pale inapobidi bila kuhitaji uingiliaji wa moja kwa moja wa binadamu.

“Baada ya mfumo huu kukamilika, hamtaniona tena natangaza kufuta leseni. Leseni itajiondoa yenyewe kupitia mfumo huu. Mfumo utakuletea taarifa zote muhimu, utakukumbusha muda wa kuwasilisha taarifa, utatoa hati za makosa pale inapobidi, na hatimaye utafuta leseni wenyewe moja kwa moja endapo masharti hayatatekelezwa,” amesisitiza Waziri Mavunde.

Mhe. Mavunde ameyasema hayo Aprili 16, 2026, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Morning Trumpet kinachorushwa na runinga ya UTV. Ameongeza kuwa leseni za utafiti ni msingi muhimu wa kuibua migodi mikubwa na ya kati, na kwamba maeneo yanayoshikiliwa bila kuendelezwa yanaikosesha Serikali mapato, ajira, pamoja na fursa katika mnyororo mzima wa thamani wa Sekta ya Madini.

Ameeleza hayo kufuatia uamuzi wake wa Aprili 15, 2026, wa kuielekeza Tume ya Madini kufuta leseni 40 za utafiti wa madini zenye jumla ya eneo la kilomita za mraba 900 (sawa na hekari 188,163), baada ya wamiliki wake kushindwa kutekeleza masharti ya leseni licha ya kupewa hati za makosa.

Aidha, Waziri Mavunde amesema Serikali imejipanga kuimarisha usimamizi wa Sheria ya Madini kwa kuondoa tabia ya mazoea iliyokuwepo kwa muda mrefu, akisisitiza kuwa sekta hiyo inahitaji wawekezaji wenye dhamira ya dhati ya kuendeleza rasilimali za madini kwa manufaa ya taifa.

“Sekta ya Madini kuchangia asilimia 10.1 kwenye pato la taifa si jambo dogo. Tanzania tumepiga hatua kubwa. Fikiria kama tafiti kwenye leseni hizi zingekamilika tungekuwa na migodi mingapi mikubwa na ya kati?” amehoji.

Katika hatua nyingine, ametoa wito kwa vijana wanaopenda kuingia katika sekta ya madini kujiunga na kuanzisha vikundi rasmi ili waweze kufikiwa kwa urahisi na Serikali kupitia programu maalum ya Mining For A Brighter Tomorrow, inayolenga kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kupata leseni, mitaji na vifaa vya uchimbaji.
Posted by MROKI On Thursday, April 16, 2026 No comments

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, akimpongeza na kumshukuru Mkurugenzi Mkuu wa Viwanja vya Ndege (TAA) Bw. Abdul Mombokaleo kwa kujitolea computer zenye thamani ya shilingi milioni 170 kama mchango wake yeye na Alumni  wengine kwa kuboresha elimu ya Sayansi katika shule hiyo.

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, akupewa maelezo juu ya  mradi wa jengo la maabara ya TEHAMA ambayo  ni ‘Smart Class’ alipokuwa Mgeni rasmi katika  Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (KSS) kama mgeni rasmi, katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani.
Sehemu ya wahitimu wa kidato cha sita katika Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (K katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani.

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, akiwatambulisha baadhi ya Alumni walio katika kamati ya   mradi wa ujenzi wa  jengo la maabara ya TEHAMA ambayo  ni ‘Smart Class’ katika  Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (KSS) kama mgeni rasmi, katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani. Kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Viwanja vya Ndege (TAA) Bw. Abdul Mombokaleo, akifuatiwa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO Nchini Prof. Hamisi Malebo.

(Picha na Habari na Issa Michuzi)

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, akikagua na kupewa maelezo juu ya  maabara ya TEHAMA ambayoni ‘Smart Class” na Mkuu wa Shule hiyo alipokuwa Mgeni rasmi katika n Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (KSS) kama mgeni rasmi, katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani.
*************
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, amehudhuria Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (KSS) kama mgeni rasmi, katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani.
 
Akiwa katika mahafali hayo, Dkt. Kikwete amezindua harambee ya kuchangia ujenzi wa jengo la ghorofa la maabara ya TEHAMA na masomo mengine, ambalo linatarajiwa kugharimu shilingi bilioni 3.
 
Amesema ujenzi huo ni muhimu katika kuendeleza ubunifu na uwezo wa wanafunzi katika masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM).
 
 
Aidha, Dkt. Kikwete amekubali kuwa mlezi wa kamati ya kukusanya michango kwa ajili ya mradi huo mkubwa ambao kwa sasa umefikia hatua ya msingi.
 
Pia, Rais Mstaafu ameishukuru jumuiya ya wanafunzi wa zamani (alumni) wa shule hiyo, wakiuongozwa na  Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Bw. Abdul Mombokaleo, kwa kuchangia kompyuta zenye thamani ya Shilingi Milioni 170 kwa ajili ya “Darasa Janja” (Smart Class) lililoanzishwa shuleni hapo.
 
Darasa hilo litakuwa ni kituo cha mafunzo kwa wanafunzi wa shule hiyo na shule nyingine zitakazounganishwa kupitia mfumo wa mtandao, ambapo mwalimu anaweza kufundisha madarasa yaliyoko nje ya Kibaha kwa wakati mmoja kwa njia ya kidigitali.
 
Katika ziara yake, Dkt. Kikwete alipata fursa ya kutembelea na kukagua Darasa Janja hilo, akipokea maelezo kutoka kwa Mkuu wa Shule kuhusu namna teknolojia hiyo inavyotumika kuboresha mbinu za ufundishaji na ujifunzaji shuleni hapo.
 
Shule ya Sekondari Kibaha, inayomilikiwa na Shirika la Elimu Kibaha na kusimamiwa na Kurugenzi ya Hud uma za Elimu, ilianzishwa mwaka 1965 kupitia ushirikiano kati ya Serikali ya Tanganyika ya wakati huo na nchi za Nordic – Denmark, Finland, Norway, na Sweden. Wakati inaanzishwa, shule ilikuwa na wanafunzi 110 wa Kidato cha Kwanza na 60 wa Kidato cha Tano.
 
Kwa sasa, shule hiyo ya bweni kwa wavulana ina uwezo wa kuchukua zaidi ya wanafunzi 800 na imeendelea kuwa miongoni mwa taasisi kongwe na zenye heshima kubwa katika sekta ya elimu nchini.
 
Dkt. Kikwete ni miongoni mwa alumni mashuhuri wa Shule ya Sekondari Kibaha, alikosoma zaidi ya miaka 60 iliyopita. Wengine waliopitia shule hiyo ni pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mkurugenzi Mkuu wa ATCL Bw. Peter Ulanga, Balozi Lazaro Nyalandu, Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO Nchini Prof. Hamisi Malebo, Mkurugenzi Mkuu wa Viwanja vya Ndege Bw. Abdul Mombokaleo, na Mwenyekiti Mstaafu wa CHADEMA Mhe. Freeman Mbowe, miongoni mwa wengine wengi.
 
Aidha, kwa kutambua mchango mkubwa wa alumni wake, Shule ya Sekondari Kibaha inaendelea kuimarisha ushirikiano na wadau wa elimu ili kuhakikisha inaendelea kuwa kinara katika utoaji wa elimu ya ubora nchini.
Posted by MROKI On Thursday, April 16, 2026 No comments

April 15, 2026




Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndg. Asha-Rose Migiro, leo tarehe 15 Aprili 2026 amefanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Malawi, Mhe. Lazarus Chakwera, katika Ofisi za CCM Lumumba, jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalijikita katika hali ya kisiasa nchini pamoja na matukio ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

Mhe. Chakwera yupo nchini Tanzania kwa ziara maalum katika nafasi yake kama Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mhe. Shirley Ayorkor Botchwey. 

Kikao hicho ni sehemu ya mashauriano yake na wadau mbalimbali wa kitaifa kwa lengo la kubadilishana mawazo kuhusu maendeleo ya kisiasa baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba 2025, pamoja na juhudi zinazoendelea za kuimarisha amani, demokrasia na mshikamano wa kitaifa nchini Tanzania.
Posted by MROKI On Wednesday, April 15, 2026 No comments



Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde ameielekeza Tume ya Madini kufuta jumla ya leseni 40 za utafiti wa madini ambao wameshindwa kuendeleza leseni hizo kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa rasilimali za madini na kuondoa wamiliki wasiotekeleza masharti ya leseni, huku akionya kuwa Serikali haitavumilia uzembe unaokwamisha maendeleo ya Sekta ya Madini pamoja na uchumi kwa ujumla.

Waziri Mavunde ametangaza uamuzi huo leo Aprili 15, 2026 jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari, akieleza kuwa leseni hizo zimefutwa baada ya wamiliki wake kushindwa kuziendeleza licha ya kupewa hati za makosa na muda wa kurekebisha kasoro zilizobainika na kwamba zitarudishwa Serikalini kwa ajili ya  kuweka utaratibu wa kugawa kwa wachimbaji wadogo,wawekezaji walio na utayari na makundi ya Wanawake na Vijana kupitia Programu ya Mining for A Brighter Tomorrow-MBT. 

Amesema kuwa, tathmini ya kina iliyofanywa na Wizara ya Madini imeonesha uwepo wa ukiukwaji mkubwa wa masharti ya leseni, ikiwemo baadhi ya wamiliki kuhodhi maeneo bila kuyaendeleza, kushindwa kulipa ada stahiki, kutotekeleza wajibu wa ushirikishwaji wa Watanzania (Local Content), pamoja na kushindwa kutekeleza miradi ya uwajibikaji kwa jamii (CSR).

“Wapo waliokuwa wanamiliki leseni lakini hawafanyi uwekezaji wowote unaoonekana, wala kuthibitisha matumizi ya fedha katika kuendeleza maeneo yao. Hali hii hairuhusiwi kuendelea,” amesema Mavunde. 

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, vitendo vya kuhodhi leseni vimekuwa chanzo kikubwa cha migogoro na kuchochea uchimbaji holela, hali inayohatarisha usalama wa wananchi, mazingira na mapato ya Serikali.

“Hizi leseni 40 ni sawa na eneo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 900 sawa na  hekari  188,163” amesisitiza Mavunde.

Katika hatua nyingine, Serikali kupitia Tume ya Madini imetoa hati za makosa kwa leseni nyingine 43, zikiwemo leseni 40 za utafutaji na tatu za uchimbaji wa kati, huku wamiliki wake wakitakiwa kurekebisha kasoro ndani ya siku 30.

Waziri Mavunde amesisitiza kuwa endapo masharti hayo hayatatekelezwa ndani ya muda uliowekwa, leseni hizo zitafutwa na maeneo husika kutolewa kwa wawekezaji wengine wenye uwezo wa kuyaendeleza. 

Akizungumzia mwenendo wa matukio ya mlipuko wa maeneo yenye madini ya dhahabu “gold rush” katika maeneo mbalimbali nchini, Waziri Mavunde ametoa onyo kali kwa watu wanaovamia maeneo yenye leseni halali wakidai kufuata taarifa za uwepo wa madini.

Ameeleza kuwa uchimbaji wowote bila leseni ni kinyume cha sheria na hautavumiliwa, akibainisha kuwa vitendo hivyo vimesababisha migogoro kati ya wachimbaji na wamiliki halali, pamoja na uharibifu wa mazingira na hatari za kiafya.

Waziri Mavunde amebainisha kuwa Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kukabiliana na hali hiyo, ikiwemo, kudhibiti usalama wa wananchi na mali zao, kuzuia migogoro ya kimiliki, kulinda mazingira dhidi ya uchimbaji holela pamoja na kudhibiti milipuko ya magonjwa katika maeneo yenye msongamano mkubwa wa wachimbaji.

Aidha, Waziri Mavunde amekemea tabia inayoongezeka ya baadhi ya wachimbaji wadogo kuvamia maeneo yenye leseni halali, akieleza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote watakaokiuka sheria.

“Kuanzia sasa ni marufuku kuvamia maeneo ya leseni kwa sababu yoyote ile. Serikali haitasita kuwachukulia hatua kali wote watakaohusika,” amesisitiza Waziri Mavunde.

Hatua ya kufuta leseni 40 inaashiria msimamo thabiti wa Serikali wa kuendeleza Sekta ya Madini dhidi ya uzembe na vitendo visivyo halali, huku ikifungua ukurasa mpya wa uwajibikaji na ushindani wa haki katika matumizi ya rasilimali za taifa.
Posted by MROKI On Wednesday, April 15, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo