Nafasi Ya Matangazo

July 09, 2026

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akepeana mkono wa maridhiano na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman baada ya utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026. 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman pamoja na Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, Amani Abeid Karume wakishuhudia utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026. Kushoto anaye saini ni Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo- Zanzibar Omary Ally Shehe pamoja na Naibu Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM- Zanzibar Dkt. Mohammed Said Dimwa
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman pamoja na Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, Amani Abeid Karume wakishuhudia utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026. Kushoto anaye saini ni Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo- Zanzibar Omary Ally Shehe pamoja na Naibu Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM- Zanzibar Dkt. Mohammed Said Dimwa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Ikulu Zanzibar kabla ya kuhudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, tarehe 09 Julai, 2026. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi wakati wakiwasili katika viwanja vya Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kuhudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, tarehe 09 Julai, 2026. 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026. 







Posted by MROKI On Thursday, July 09, 2026 No comments
Mwandishi Mwandamizi wa Gazeti la Daily News, Leonard Wilfred Mwakalabela amefariki dunia.

Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Magazeti la Serikali (TSN) Bi. Aisha Dachi imesema Mwakalebela amefikwa na umauti Julai 08, 2026. 
Posted by MROKI On Thursday, July 09, 2026 No comments

July 08, 2026




Dar es Salaam
Serikali imesema mageuzi yanayoendelea kutekelezwa katika sekta ya madini chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yameifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye mazingira bora ya uwekezaji barani Afrika, huku ikiwakaribisha wawekezaji kuwekeza katika utafiti, uchimbaji, uchenjuaji, uchakataji na uongezaji thamani wa madini.

Kauli hiyo imetolewa leo, Julai 8, 2026, na Naibu Waziri wa Madini, Mhe. Dkt. Steven Kiruswa, wakati akifungua Kongamano la Madini lililofanyika katika Ukumbi wa Dome, ndani ya Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF), maarufu Sabasaba.

Dkt. Kiruswa amesema maboresho ya sera, sheria na mifumo ya usimamizi wa sekta ya madini yameongeza uwazi, uwajibikaji na ushiriki wa sekta binafsi, hatua zilizochochea ongezeko la uwekezaji, ajira na mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Amesema Tanzania imejaliwa kuwa na rasilimali nyingi za madini mengi, ikiwemo dhahabu, almasi, tanzanite, nikeli, kinywe (graphite), nobium, madini adimu (Rare Earth Elements), pamoja na madini ya viwandani na ujenzi. 

Amebainisha kuwa Dira ya  Maendeleo ya Taifa 2050 imeweka msisitizo katika kuimarisha tafiti za kijiolojia kwa kutumia teknolojia za kisasa ili kufungua maeneo mapya ya uwekezaji.

“Serikali haiwaaliki wawekezaji kuja kuchimba madini pekee, bali pia kuwekeza katika tafiti za kijiolojia, teknolojia za uchenjuaji, uchakataji, uongezaji thamani wa madini na viwanda vinavyotumia madini kama malighafi,” amesema Dkt. Kiruswa.

Aidha, amesema Serikali imeendelea kuboresha sheria na kanuni za madini ili kuongeza ushiriki wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta hiyo kupitia matumizi ya bidhaa na huduma zinazotolewa na kampuni za wazawa. 

Ameongeza kuwa utekelezaji wa Programu ya Mining for Brighter Tomorrow (MBT) unaendelea kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalum kunufaika na fursa zinazotokana na sekta ya madini.

Dkt. Kiruswa amesema kongamano hilo linatarajiwa kufungua fursa mpya za biashara na uwekezaji, huku akiwakaribisha wadau kushiriki Mkutano wa Kimataifa wa Madini utakaofanyika Novemba 19 hadi 21, 2026, katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, kwa lengo la kuendelea kuitangaza Tanzania kama kitovu cha uwekezaji wa madini barani Afrika.

Akitoa mada kuhusu usimamizi wa leseni na biashara ya madini, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini wa Tume ya Madini, CPA Venance Kasiki, amesema Tume inaendelea kusimamia utoaji wa leseni za utafutaji, uchimbaji, uongezaji thamani na biashara ya madini kwa kuzingatia Sheria ya Madini, ili kuhakikisha rasilimali za madini zinawanufaisha Watanzania na Taifa kwa ujumla.

Amesema utoaji wa leseni unazingatia vigezo mbalimbali, ikiwemo sifa za waombaji, usajili wa kampuni na matumizi ya mifumo ya kielektroniki katika kupokea na kuchakata maombi. 

Ameongeza kuwa wamiliki wa leseni wanawajibika kutekeleza mipango ya uchimbaji iliyoidhinishwa, kulinda mazingira, kuajiri na kuwaendeleza Watanzania, pamoja na kutekeleza wajibu wa uwajibikaji kwa jamii zinazozunguka maeneo ya migodi.

CPA Kasiki amesema Serikali inaendelea kuimarisha utekelezaji wa Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania (Local Content), zinazolenga kuwawezesha Watanzania kushiriki kikamilifu katika usambazaji wa bidhaa na huduma ndani ya mnyororo wa thamani wa sekta ya madini. 

Amesema fursa hizo zinajumuisha usafirishaji, ujenzi, teknolojia, huduma za ulinzi, huduma za chakula na huduma za kifedha.

Amesisitiza kuwa usimamizi madhubuti wa leseni za madini pamoja na utekelezaji wa Kanuni za Local Content ni nguzo muhimu katika kuongeza mapato ya Serikali, kuvutia uwekezaji, kuimarisha viwanda vya uongezaji thamani na kuhakikisha wananchi wananufaika zaidi na rasilimali za madini.

Vilevile, amewahimiza Watanzania kutumia fursa zinazopatikana katika sekta ya madini kwa kuwekeza katika viwanda vinavyozalisha bidhaa na vifaa vinavyotumika migodini pamoja na kutoa huduma mbalimbali zinazohitajika katika shughuli za uchimbaji na uongezaji thamani wa madini.

Awali, Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita, Mohamed Jumanne, amesema sekta ya madini imeendelea kutoa ajira kwa maelfu ya vijana na kuchangia ukuaji wa uchumi wa maeneo yenye shughuli za uchimbaji. 

Amesema Serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano katika masuala ya ulinzi na usalama ili shughuli za uchimbaji zifanyike kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo, hatua itakayochochea maendeleo endelevu ya sekta hiyo na kuongeza mchango wake kwa uchumi wa Taifa.





Posted by MROKI On Wednesday, July 08, 2026 No comments
Muonekano wa sasa wa makutano ya Barabara ya Mzunguko Dodoma (Dodoma Outer Ring Road) katika eneo la Nala, jijini Dodoma, ambayo tayari yameanza kutumika.
Mhandisi Morice Mlay kutoka kampuni Mshauri wa Mradi wa Ujenzi wa Barabara ya Mzunguko Dodoma (Dodoma Outer Ring Road) ya Inter-Consult Ltd, akikagua moja ya barabara ya mzunguko katika eneo la Nala, ambayo tayari imeanza kutumika.

Mradi huo ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati ya miundombinu unaolenga kuboresha huduma za usafiri na usafirishaji, kupunguza msongamano wa magari katikati ya Jiji la Dodoma, pamoja na kufungua fursa mpya za uwekezaji na shughuli za kiuchumi kwa wananchi.
Na Adelina Johnbosco – MAELEZO
Barabara za Mzunguko Jijini Dodoma imechangia kwa kiasi kikubwa kuondoa msongamano wa magari katikati ya jiji, hususan magari makubwa ya mizigo ya ndani na yanayokwenda nchi za nje.

Mradi huu wa barabara ya njia nne kwa kiwango cha lami una urefu wa jumla ya kilometa 112.3 huku sehemu ya kwanza (lot 1) yenye kilometa 52.3 ikiwa imekamilika kwa asilimia 93.3.

Barabara hii imeunganisha barabara kuu za mikoa minne, bandari kavu Ihumwa - Morogoro, Veyula - Arusha, Nala - Singida na Matumbulu – Iringa ambako sehemu ya pili ya ujenzi (lot 2) inaanzia.

Shughuli za usafiri na usafirishaji tayari zimeanza katika barabra hiyo, watumiaji wanashuhudia urahisi wa safari kutokana na kutokuwepo foleni.

 “Imeturahisishia sana, inafanya safari iwe fupi kutokana na ukweli kwamba njia hii haina foleni hata kidogo kama kule mjini kati, mwanzoni kutoka Ihumwa hadi Nala ilikuwa tunatumia takribani saa na nusu hata zaidi, lakini kwa sasa tunatumia dakika 45 hadi 48 kwa safari hiyo hiyo” Bw. Simon Ndamanyilu, dereva lori

Akitoa ufafanuzi kuhusu barabara hiyo hivi karibuni, Mhandisi Morice Mlay, kutoka kampuni ya mzawa ya  Inter-Consult Ltd (Mhandisi Mshauri wa Mradi), amesema barabara hiyo tayari imeanza kutumika na inatarajiwa kuzinduliwa rasmi Oktoba, 2026 ambapo itakuwa imekamilika kabisa.

“Ujenzi sehemu ya kwanza umefikia ukingoni, bado baadhi ya vitu vichache sana ikiwemo taa za barabarani na umaliziaji wa njia za watembea kwa miguu, magari mengi yanapita na yanapata urahisi kwa sababu hakuna foleni kwenye njia hii, mfano magari yanatoka moja kwa moja kutoka eneo la mzunguko wa Ihumwa hadi Nala ile barabara inayounganisha barabara ya Iringa bila kusimama popote” ametanabaisha Mha. Mlay

Barabara hiyo ya njia nne yenye njia mbili kila upande, zimetenganishwa na uwazi katikati kwa ajili ya matumizi mengine pindi itakapohitajika kuongeza miundombinu mingine au uboreshaji.

“Kuna baadhi ya watu wanashangaa kuhusu hili tuta lililoachwa katikati, hili ni kwa ajili ya matumizi ya baadaye mfano ujenzi wa barabara za mwendo kasi au kitu chochote kitakachoamuliwa kufanyika, lengo kuu ni kuepuka kutobomoa barabara kwa ajili ya kufanya kitu kipya” – Mha. Mlay 

Baadhi ya wananchi jijini Dodoma wanaonesha furaha yao kutokana na uwepo wa barabara hiyo mpya inayopitisha magari mengi hasa magari makubwa ya mizingo kwenda ndani na nje ya nchi kwa wakati mmoja. Kwa mujibu wa Mha. Mlay, yapo magari yanayoelekea nchini Rwanda, Congo na Burundi kupitia barabara ya mzunguko.

Katika eneo la Nala ambako kuna mojawapo ya makutano ya barabara hiyo na sehemu ya maegesho ya magari, wakazi wa maeneo hayo wamepata fursa ya kufanya biashara kutokana na uwepo wa watu wengi kwa wakati mmoja.

"Kituo hiki yanapitisha na kusimama magari ya kila aina, hii ni tofauti na mwanzo, magari yakisimama hapa watu wanashuka na wengine wanakuwa wamesubiria kupanda, wengine ni madereva wa magari makubwa, kwa hiyo lazima watahitaji kupata mahitaji kutoka kwetu hasa chakula, hii ni furaha kwetu" Mary John, mama ntilie

Tamanio la wengi ni kuona barabara inaanza kazi rasmi kwani kwao ni tegemeo mojawapo la njia ya kuongeza kipato.

"Kama kwa sasa nauza bidhaa zangu kwa kiwango ambacho naona kinafaa, nawaza kwamba barabara hii ikianza kutumika rasmi magari yataongezeka, yataegeshwa kwa wingi zaidi na watu watakuwa wengi kuliko hivi" amesema Bi. Veronica Alfred, muuza nafaka eneo la Nala.

Mussa Rajab mkazi wa Nala na mkuli eneo hilo, akiwawakilisha wabeba mizigo wenzake, anasema uwepo wa sehemu ya kisasa ya kuegesha magari umefanya kazi yao kuwa rahisi na kukuza kipato.

“Mwanzoni eneo hili halikuwepo, hivyo kusimama kwa magari hapa ilitegemea udharura wa dereva hapo na sisi tunavizia kubeba mizigo japo kwa uchache sana, siku hizi magari yanasimama na mizigo inateremshwa hivyo tunabeba na kupata riziki” – Bw. Rajab

Mradi huu kipande cha kwanza utagharimu shilingi bil. 100.84 hadi kukamilika kwake, na unatarajiwa kuwa mwarobaini wa msongamano wa magari katikati ya jiji pia kukuza uchumi wa mkoa wa Dodoma, mikoa ya jirani na nchi kwa ujumla.
Posted by MROKI On Wednesday, July 08, 2026 No comments

July 07, 2026

Na Dk. Reubeni Lumbagala 
Kuna umuhimu mkubwa kwa Watanzania kubadili mtizamo kuhusiana na lugha ya Kiswahili. Hii ina maana kuwa, tusiiangalie lugha ya Kiswahili katika muktadha wa mawasiliano pekee. Hapana. 

Ni kwamba, twende mbele zaidi, yaani tukifanye Kiswahili kuwa bidhaa ya kuuza na kuingiza fedha, kuongeza ajira, hatimaye kukuza uchumi na maendeleo ya mama Tanzania badala ya Kiswahili kubaki kama chombo cha mawasiliano na kupiga soga.

Kiswahili kimepiga hatua kubwa sana na kupata heshima kubwa ulimwenguni. Tuna kila sababu ya kujivunia lugha hii adhimu na adimu, ambayo tunapaswa kuifungamanisha na mikakati ya ukuzaji uchumi kwa maendeleo endelevu.

Ni hivi: Lugha ya Kiswahili imevuka mipaka. Kwa sasa, Kiswahili si lugha ya Tanzania au Afrika Mashariki pekee bali ni lugha ya Afrika na ya dunia. 

Kiswahili sasa kimepata heshima kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO). UNESCO imeichagua Julai 7, ya kila mwaka, kuwa "Siku ya Kiswahili Duniani".

Na kwa mwaka huu, maadhimisho hayo, yanafanyika Jijini Paris, nchini Ufaransa, yalipo makao makuu ya UNESCO, ambapo Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amehudhuria maadhimisho hayo, kumuwakilisha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Kwa hakika, kuna mwamko mkubwa wa watu kujifunza Kiswahili ulimwenguni. Aidha, Kiswahili sasa kinafundishwa katika shule na vyuo mbalimbali ulimwenguni, jambo linaloendelea kuongeza thamani yake. Kukibidhaisha Kiswahili kunahusisha  kuingiza fedha kupitia lugha hiyo. Sasa, tunawezaje kutengeneza fedha kupitia lugha ya Kiswahili?

Kwanza, kupitia ajira ya kufundisha Kiswahili. Wapo vijana wengi wahitimu wa vyuo na vyuo vikuu waliosomea somo la Kiswahili. Hawa wanaweza kutumika kufundisha Kiswahili kwa wageni wanaopenda kujifunza lugha hii.

Aidha, kupitia shughuli hiyo, vijana hao wataingiza fedha na serikali kunufaika kupitia kuongeza fursa za ajira kwa wananchi wake na kupata kodi kupitia mishahara ya walimu hao, jambo litakalochangia katika kukuza uchumi.

Pili, kuuza matini za Kiswahili. Wataalamu wa Kiswahili wanaweza kuingiza fedha kupitia kuandika na kuuza vitabu vya Kiswahili vilivyo katika muundo wa nakala laini na nakala ngumu (soft and hard copies). Mauzo hayo, yatawezesha kujenga uchumi wa nchi yetu na kukuza maendeleo.

Tatu, kukifungamanisha Kiswahili na sanaa ya filamu na tamthiliya za nje. Serikali ishirikiane na wandaaji wa filamu na tamthiliya za nje kama Korea, Uturuki, India na wengineo katika kutafsiri filamu na tamthiliya hizo kwa kutumia Kiswahili. 

Hii itaongeza fursa za ajira kwa 'waingizaji wa sauti za Kiswahili' katika tamthiliya hizo na hivyo kuwezesha wahusika hao kupata kipato. Jambo hili natamani liendelee kufanyika kwa ukubwa zaidi ya linavyofanyika sasa.

Jambo muhimu, ni wataalamu wetu wa Kiswahili kuwa na umahiri katika lugha nyingine za kimataifa kama Kiingereza, Kifaransa, Kichina, Kijerumani, Kiarabu, Kikorea, kutaja kwa uchache ili waweze kuwa walimu mahiri wa kufundisha wanafunzi wa kigeni na kuongeza mawanda ya kupata fursa za kufundisha lugha hiyo ulimwenguni.

Kimsingi, hata safari ya miaka 25 ijayo, kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050, Kiswahili kina nafasi ya kuchangia kufanikisha mipango mingi ya kiuchumi kwa kutumia fursa zilizopo katika kukibidhaisha kama nilivyoeleza katika nyanja ya uchumi.
Mungu Ibariki Tanzania.
Maoni: 0620 800 462.

Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments




Na Dk. Reubeni Lumbagala 
Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, anatambulika kimataifa katika nyanja mbalimbali kutokana na utendajikazi wake uliotukuka. Miongoni mwa maeneo yanayomtambulisha kwa upekee ni pamoja na kuwa Kinara wa Afya ya Uzazi ya Mama na Mtoto barani Afrika.

Ni heshima ya kipekee aliyoipata kutokana na mageuzi makubwa yaliyofanyika katika sekta ya afya, ambapo matunda yake yameonekana hasa katika kupungua kwa vifo vya mama na mtoto wakati wa kujifungua.

Kwa wadhifa huu, Rais Dk. Samia anao wajibu wa kuhakikisha nchi zote 54 za barani Afrika na Tanzania ikiwemo, zinaendea kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa kiwango kikubwa.

Hii inatokana na ukweli kuwa, kundi la mama na mtoto ni wadau muhimu katika juhudi za maendeleo. Ni kundi ambalo linapaswa kuhakikishiwa usalama wa maisha na kamwe uzazi usio tishio la usalama wao.

Juhudi za kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa sehemu kubwa zinahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali hasa katika kubadilishana uzoefu, teknolojia na uwekezaji wa miundombinu bora ya afya na vifaa tiba vya kisasa.

Kwa kutumia ushirikiano baina ya sekta ya umma na binafsi (Public and Private Partnership - PPP), juhudi na mapambano ya kupunguza vifo vya mama na mtoto zitafanikiwa kwa kiwango kikubwa.

Ili jambo hili liwe halisi, Julai 02, 2026, Rais Dk. Samia alifanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Sera, Uhusiano na Ushirikiano na Serikali (PGRP), Divisheni ya Afrika na India kutoka Taasisi ya Gates, Bi. Caty Fall Sow ambaye aliambatana na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam. 

Haya yamefanyika ikiwa ni mwendelezo wa harakati chanya za uboreshaji wa afya ya uzazi ya mama na mtoto Tanzania na Afrika kwa ujumla.

"Bi. Sow alimpongeza Rais Samia kwa kuteuliwa kwake kuwa Bingwa wa Umoja wa Afrika wa Afya ya Mama, Mtoto Mchanga na Mtoto, na akathibitisha upya dhamira ya Taasisi ya Gates ya kuunga mkono juhudi zinazoongozwa na Waafrika za kumaliza vifo vinavyoweza kuzuilika vya akina mama na watoto," ilieleza Taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu.

Aidha, taarifa imesisitiza kuwa pande zote mbili zimejadili namna ya kuimarisha ushirikiano zaidi katika maeneo ya afya ya mama na mtoto, chanjo, lishe, kuimarisha mifumo ya huduma na kudhibiti magonjwa.

Naye, Rais Dk. Samia amesema, "Dhamira yetu ni kuhakikisha kila mama na kila mtoto anapata huduma bora za afya na nafasi ya kuishi maisha yenye afya na matumaini".

Taasisi ya Gates ni mdau mkubwa wa uimarishaji wa masuala ya afya barani Afrika, jambo linalosaidia kuimarika kwa huduma za afya na kuwezesha kufanikiwa kwa mipango ya serikali ya kuwahudumia wananchi wake.

Kutokana na kazi kubwa aliyonayo Rais Dk. Samia ya kusaidia mafanikio ya masuala ya afya ya uzazi ya mama na mtoto barani Afrika, Juni 02, 2026, alimteua Bi. Ummy Mwalimu kuwa Mshauri wa Rais - Masuala ya Afya ya Uzazi ya Mama na Mtoto.

Maoni: 0620 800 462.
Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments
Na Dk. Reubeni Lumbagala 
Malezi bora ya watoto yanapaswa kutiliwa mkazo ili kujenga jamii yenye watu wenye maadili, nidhamu, uzalendo na uwajibikaji katika maisha yao.

Wazazi wamepata baraka ya kupata watoto kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Watoto hao wanapaswa kuendelea kuwa baraka kwa kuhakikisha wanapata malezi na matunzo muhimu.

Katika miaka ya karibuni, kumekuwa na kulegalega malezi ya watoto. Baadhi ya wazazi na walezi ambao ndiyo wadau wa kwanza wa kusimamia malezi ya watoto wamekuwa walipambana na matunzo ya watoto huku wakisahau malezi yao.

Wazazi na walezi wanahangaika kutafuta fedha za kuwapatia watoto wao mahitaji muhimu kama vyakula, mavazi, mahitaji ya shule ili wafurahie maisha. Hili ni jambo zuri na la kupongezwa na kila mtu.

Changamoto inayokuja ni pale wazazi na walezi wanapojitahidi kutoa matunzo na kusahau suala la malezi ambalo ni la muhimu sana.

Julai 02, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dk. Batilda Buriani alitoa somo zuri la malezi kwa wazazi na walezi. 

Ni kwamba, Dk. Buriani alitoa somo hilo alipomwakilisha Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dk. Dorothy Gwajima, katika kilele cha Maadhimisho ya Mtoto wa Afrika na Kampeni ya Kitaifa ya Maadili na Malezi Chanya Kwa Watoto yenye kaulimbiu isemayo "Mtoto ni Malezi; Msingi wa Familia Bora kwa Taifa Imara".

Katika hafla hiyo, Balozi Dk. Buriani alisema, "Wazazi wanatakiwa kutenga muda kuwafuatilia watoto, kuwapa malezi bora, malezi si hiari bali ni wajibu kwa wazazi na walezi".

Kimsingi, Dk. Buriani alihimiza juu ya wazazi na walezi kutenga muda wa kufuatilia watoto wao na kuwalea watoto kwa misingi ya imani za dini zao.

Hivyo basi, wazazi na walezi wazingatie ushauri huu chanya uliotolewa. Wazungumze na watoto wao kutambua changamoto zao ili kuzitafutia ufumbuzi kwa ustawi wao. Pia, wafuatilie maendeleo ya kitaaluma ya watoto wao shuleni ili wafanye vizuri zaidi katika masomo yao.

Sanjari na hilo, wazazi na walezi wasimamie suala la mafundisho ya dini kwa watoto wao ili wawe na hofu ya Mungu na mwenendo mwema unaokubalika katika jamii na mbele za Mungu.

Naamini, haya yakifanyiwa kazi, tutajenga kizazi chenye maadili mazuri ambayo ni chachu ya maendeleo kuanzia ngazi ya familia, jamii na taifa kwa ujumla, na hili litafanya hata utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya mwaka 2050 kuwa rahisi.

Maoni: 0620 800 462.
Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments
Na Dk. Reubeni Lumbagala
Miongoni mwa haki za msingi za mfanyakazi serikalini au sekta binafsi ni pamoja na kulipwa mafao yake kwa wakati pindi anapostaafu utumishi wake.

Mafao hayo yanatokana na michango aliyochangia katika mifuko ya hifadhi ya jamii kutoka kwenye makato ya mshahara wake pamoja na michango ya mwajiri wake.

Kwahiyo, mfanyakazi anapomaliza muda wa utumishi wake eidha kwa kustaafu kwa hiari au kwa lazima, mifuko ya hifadhi ya jamii inapaswa kumlipa mafao yake ili kuendeleza maisha mengine, kwani maisha lazima yaendelee hata baada ya kustaafu.

Kwa muda mrefu, kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya wastaafu kucheleweshewa kulipwa mafao yao, ambayo kama nilivyoeleza awali ni haki yao ya msingi na si hisani. Kwa ufupi, wanastahili kulipwa bila usumbufu wowote.

Kucheleweshewa mafao ya wastaafu kumesababisha usumbufu mkubwa kwa wastaafu, na hata kuwasababishia msongo wa mawazo kwa kujiuliza kwani kustaafu ni kosa la jinai hadi kusumbuka kiasi hicho? 

Ni faraja kuona kuwa, sasa kero hiyo ya kuchelewa kulipwa kwa mafao ya wastaafu inakuwa historia nchini.

Mwezi Aprili, 2026, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeanzisha kaulimbiu isemayo "Tunalipa Jana" yenye malengo ya kuharakisha malipo ya mafao ya wastaafu kwa wakati mara tu mfanyakazi anapostaafu.

Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Fortunatus Magambo, amesema mfuko huo umejizatiti kuhakikisha wastaafu wanalipwa mafao yao kwa wakati ili kufurahia utumishi wao.

"Tunapoanza kumsajili mwanachama, tunahakikisha taarifa zake zinakuwa sahihi na zinahuishwa kila inapobidi. Lengo letu ni kwamba anapofikia umri wa kustaafu asiwe na changamoto yoyote ya malipo. Tunataka alipwe siku ya kustaafu. Hiyo ndiyo tafsiri halisi ya kaulimbiu yetu ya Tunalipa Jana, amesema Magambo.

Katika hatua nyingine, Magambo ameishukuru serikali chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kulipa deni la shilingi trilioni nne kwa Mfuko huo, jambo lililoimarisha ukwasi na uendelevu wa kulipa mafao.

Kwa hakika, mkakati wa PSSSF wa kulipa mafao ya wastaafu mara tu wanapostaafu ni jambo la kupongezwa. 

Wapo baadhi ya wastaafu kwa kuchelewa kulipwa mafao yao, wamejiingiza katika mikopo yenye riba kubwa, jambo linaloathiri mafao yao kwani wanapokuja kulipwa, hujikuta wakilipa deni kubwa linalochukua asilimia kubwa mafao yao. 

Kwa hili la kumlipa mstaafu kwa wakati, kutaleta utulivu wa akili, kustamwezesha mstaafu kutumia fedha zake kadri ya mipango yake aliyonayo na kufurahia utumishi wake na kuona kustaafu ni heshima na si mateso au adhabu. Sitakosea kusema PSSSF mmeutendea haki msemo wenu wa "Kesho Yako, Kipaumbele Chetu".

Maoni : 0620 800 462.
Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments





Na Mwandishi Wetu, Afrika Kusini
Waziri wa Maji, Jumaa Aweso pamoja na ugeni wake, wapo nchini Afrika Kusini, ikiwa ni ziara ya kikazi yenye lengo la kushirikiana na wadau mbalimbali katika kufanikisha udhibiti wa upotevu wa maji ili kuongeza kasi ya usambazaji wa huduma ya maji kwa wananchi.

Ziara hiyo iliyoanza Julai 6, 2026, imelenga kushiriki kikao kazi na wataalamu wa masuala ya teknolojia zenye uwezo wa kudhibiti upotevu wa maji, ili wananchi waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza kwa matumizi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.

Ikumbukwe kuwa, upotevu wa maji ni miongoni mwa changamoto inayoikabili Wizara ya Maji, ambayo imesababisha kupotea kwa maji mengi na kuzikosesha mapato mamlaka za maji katika wilaya mbalimbali nchini. 

Kimsingi, moja ya kipaumbele cha Wizara ya Maji kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ni kupambana na upotevu wa maji. Hivyo ziara hiyo, ni mkakati wa kufanikisha kipaumbele hicho.

Katika ziara hiyo, Aweso ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara, Mhandisi Mwajuma Waziri, Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, James Bwana pamoja na wataalamu wengine wa wizara hiyo.

Pamoja na masuala ya maji, Julai 7, akiwa nchini humo, Aweso pamoja na ugeni wake wameshiriki kikamilifu hafla ya maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani. 

Katika hafla hiyo, amezindua Kituo cha Utamaduni wa Kiswahili Tanzania (Tanzania Kiswahili Cultural Center) ikiwa ni mkakati wa kufundisha lugha ya Kiswahili kwa wageni ili kuendelea kukuza lugha hiyo na utamaduni wa Kitanzania ulimwenguni.
Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments

Waziri Mkuu, Dkt Mwigulu Nchemba akizcheza bao na Balozi wa Tanzania nchini Ufaranza, Saidi Othman Yakubu alipomwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye kilele cha maadhimisho ya miaka mitano ya Kiswahili Duniani kwenye ukumbi wa Makao Mkuu ya Shirika la Umoja wa Mataifa  la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) jijini Paris, Ufaransa, Julai 7, 2026. 

**************

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuna haja ya kutafuta mbinu mpya ya kukieneza Kiswahili baada ya kuwa kimepata hadhi ya kimataifa.
 
Kadiri Kiswahili kinavyoendelea kupata hadhi ya kimataifa, ni muhimu sasa kuanza kutazama hatua inayofuata ya kukieneza duniani. Mataifa mengi yamefanikiwa kueneza lugha na utamaduni wao kupitia vituo vya utamaduni vilivyoanzishwa katika nchi mbalimbali duniani,” amesema.
 
Ametoa wito huo leo (Jumanne, Julai 7, 2026) wakati akizungumza na washiriki waliohudhuria kilele cha Maadhimisho ya Tano ya Siku ya Kiswahili Duniani kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi za makao makuu ya UNESCO jijini Paris, Ufaransa. 
 
“Serikali itaendelea kuimarisha matumizi ya Kiswahili ndani na nje ya nchi kupitia elimu, tafiti, uchapishaji, tafsiri, teknolojia za kidijiti na diplomasia ya lugha. Tutaendelea kushirikiana na UNESCO, nchi mbalimbali, vyuo vikuu, taasisi za kimataifa na wadau mbalimbali katika kuendeleza lugha hii kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” amesema.
 
Waziri Mkuu ambaye alikuwa mgeni rasmi kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema sasa hivi Kiswahili kimeshatambulika kuwa lugha rasmi ya EAC na SADC. “Kiswahili ndiyo utambulisho wetu wana jumuiya ya Afrika Mashariki. Mtu akiongea Kiswahili anajulikana kuwa anatokea Tanzania, Burundi, Congo au Sudan Kusini. Na pia kimekuwa moja ya lugha rasmi za Umoja wa Afrika (AU),” amesema.
 
“Si hivyo tu, sasa hivi Kiswahili kinatambulika kuwa ni lugha rasmi ya mikutano mikubwa ya UNESCO kutokana na pendekezo lililopitishwa kwa kaulimoja Novemba, 2025 wakati wa Mkutano Mkuu wa 43 wa UNESCO, uliofanyika Samarkand, Uzbekistan.”
 
Amesema kwa mujibu wa wataalamu wa lugha, Kiswahili kinazungumzwa na watu kati ya milioni 300 hadi milioni 500 na idadi hiyo inaendelea kuongezeka kutokana na matumizi yake katika elimu, biashara, vyombo vya habari, teknolojia ya habari na mawasiliano pamoja na mitandao ya kijamii.
 
“Hali hiyo inaonesha kwamba Kiswahili siyo mali ya Watanzania pekee bali ni urithi wa Afrika na zawadi ya Afrika na dunia. Kiswahili kinaunganisha watu, Kiswahili kinaunganisha biashara, Kiswahili kinaunganisha jamii,” amesisitiza.
 
Mapema, Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO, Prof. Khaled El-Enany aliwaeleza washiriki wa maadhimisho hayo kwamba shirika lake limesaidia kufadhili uandaaji wa kamusi ya Kifaransa kwenda Kiswahili.
 
“Mbali na matumizi ya kawaida kwa watalii au watu wanaojifunza lugha, tunatarajia kwamba uwepo wa kamusi hiyo na nyaraka nyingine kutasaidia kuongeza fursa kwa walimu na wanafunzi wanaojifunza Kifaransa na Kiswahili,” amesema.
 
Amesema uzuri wa Kiswahili ni lugha ambayo imekuwa ikiendelea kukua na kuvuka mipaka bila kupoteza uasili wake na imeunganisha watu bila kulazimika kuvuka mipaka ya nchi zao.
 
Akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki hao, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda alisema Tanzania ina lugha za makabila zaidi ya 150 katika maeneo mbalimbali lakini wananchi wake wameweza kuunganishwa na lugha moja ya Kiswahili.
 
Alisema wakati jijini Paris, Ufaransa wakiadhimisha kilele cha maadhimisho hayo na kongamano la pili lililoandaliwa na UNESCO kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, nchi nyingine tatu za Uingereza, Algeria na Burundi nazo pia leo zimeadhimisha makongamano kama hayo.
 
Awali, Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Bw. Saidi Othman Yakub alisema maadhimisho hayo ya tano ambayo yanafanyika sambamba na Kongamano la Pili la Siku ya Kiswahili Duniani, yamevutia washiriki zaidi ya 300 kutoka nchi 16 duniani. 
 
Amezitaja nchi hizo kuwa ni Comoro, Tanzania, Ujerumani, Marekani, Canada, Uingereza, Italia, Luxembourg, Sweden, Ubelgiji, Austria, Uturuki, Misri, Kenya, Uganda na wengi kutoka Tanzania.
 
“Tangu tarehe 4 Julai hadi leo tarehe 7 Julai, 2026 tumeshuhudia shughuli mbalimbali zilizolenga kuendeleza na kukitangaza Kiswahili duniani. Shughuli hizo zilijumuisha matembezi ya hamasa katika mitaa maarufu ya Jiji la Paris, hafla za vyakula vya Kiswahili kwa Diaspora, kongamano kuhusu nafasi ya Kiswahili katika biashara na uchumi, semina na warsha mbalimbali hapa UNESCO.
 
Amesema waliandaa pia tamasha la Usiku wa Mswahili lililofanyika chini ya Mnara wa Eiffel kandokando ya Mto Seine, maonesho ya filamu na chakula pamoja na kazi za Kiswahili.
Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments

July 06, 2026

 

Familia ya ASAS imetangaza Kwa masikitiko makubwa kifo cha Al Haj Mzee Jaffer Abri (ASAS), ambaye amefariki leo asubuhi mjini Istanbul, Uturuki.

Kwa mujibu wa taarifa ya Familia hiyo, Swala ya Janaza pamoja na mazishi yamefanyika mjini Istanbul baada ya Swala ya Alasiri, kwa mujibu wa taratibu za Kiislamu.

Tunamuomba Mwenyezi Mungu (SWT) amsamehe madhambi yake, amrehemu kwa rehema Zake zisizo na mipaka, amjaalie Pepo ya Jannatul Firdaus, na awape subira, faraja na nguvu familia, ndugu, jamaa na wote walioguswa na msiba huu mzito.

Posted by MROKI On Monday, July 06, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akimjulia hali Sheikh Rashid Hamad Othman, Kaka mkubwa wa Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha ACT Wazalendo, Mhe. Othman Masoud Othman, anayepatiwa matibabu katika Hospitali ya Aga Khan Jijini Dar es Salaam. Akiwa hospitalini hapo Mhe. Rais Dkt. Samia pia alijulishwa kuhusu kuwepo kwa Mchezaji wa Timu ya Yanga Pacome Zouzoua katika chumba jirani, ambapo alipata muda wa kumtembelea na kumpa pole kufuatia majeraha aliyopata katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya JKT Tanzania katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo hivi karibuni.



 

Posted by MROKI On Monday, July 06, 2026 No comments

July 05, 2026





Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo leo Julai 5, 2026 ametembelea na kuzungumza na wataalam waliopo kwenye banda la Wakala wa Nishati Vijijini (REA) wakati wa maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es salaam 

Akiwa katika banda la REA, Mbibo alielezwa kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya nishati safi ya kupikia na umeme vitongojini iliyotekelezwa na inayotekelezwa na REA katika maeneo hayo.
Posted by MROKI On Sunday, July 05, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo