Nafasi Ya Matangazo

May 20, 2026










MKuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila ametoa ahadi ya milioni 50 kwa Dar City Basket Team endapo itafunzu mtanange huko Rwanda kufikia hatua ya nusu fainali.

RC Chalamila ameyasema hayo leo Mei 20, 2026 katika uwanja wa ndege wa Mwalimu JK Nyerere Terminal 3 wakati akiiaga team hiyo kuelekea Kigali Rwanda kwenye mashindano.

Aidha RC Chalamila ametoa rai kwa wakazi wa Mkoa huo endapo watabaini kuna kijana anakipaji cha basket ball,wamlete ofisini kwake ili aweze kuendelezwa kipaji hicho pamoja na kumuunganisha na wachezaji nguli wa Dar City Basket Ball.

Vilevile RC Chalamila amesema Rais wa team hiyo Ndg Hashimu Thabit akirudi toka Rwanda uandaliwe utaratibu wa kukutana na Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wote wa Mkoa huo kuona namna ya kuwa na uwanja mkubwa wa kisasa wa Basket Ball  katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Kwa upande wa Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe Edward Mpogolo amesema Dar City ni team ya kimataifa na inafanya vizuri ni ya kihistoria toka Tanzania ipate uhuru hivyo anaitakia kila kheri.

Mwisho RC Chalamila amemshukuru Rais Dkt Samia kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya michezo kwa kuwa michezo ni afya lakini pia michezo ni uchumi.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments



Freetown- Sierra Leone
Tanzania imesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa Kikanda katika kuongeza thamani Madini ya Almasi, uwazi katika usimamizi wa rasilimali madini na kuimarisha mchango wa Sekta ya Madini katika maendeleo ya uchumi wa nchi wanachama Zinazozalisha Madini ya Almasi Afrika (ADPA).

Hayo yalibainishwa  Mei 19, 2026   mjini Freetown, Sierra Leone, na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo, ambaye anaongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki  katika Mkutano wa 11 wa Kawaida  wa Kamati ya  Wataalam  wa umoja huo.

Mkutano huo unawakutanisha wataalam kutoka nchi wanachama wa ADPA kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha usimamizi, biashara na maendeleo ya sekta ya almasi barani Afrika.

 Aidha, katika mkutano huo, wajumbe walijadili taarifa ya mwaka ya Mkurugenzi Mtendaji wa ADPA ya mwaka 2025, utekelezaji wa bajeti na taarifa za fedha za mwaka 2025 pamoja na taarifa ya ukaguzi wa nje wa hesabu kwa kipindi cha 2023–2024. Aidha, masuala ya msamaha wa madeni, daftari la hatari, maendeleo ya uwezo wa taasisi na uanachama wa ADPA katika Shirika la Viwango Duniani (ISO) yalipata nafasi ya kujadiliwa kwa lengo la kuimarisha ufanisi wa taasisi hiyo.

Vilevile, mkutano ulipokea taarifa za maendeleo kuhusu maandalizi ya Mkutano wa Almasi na maadhimisho ya miaka 20 ya ADPA, mapitio ya mkakati wa mawasiliano na masoko, utekelezaji wa ukaguzi wa ndani wa miaka 2023–2025 pamoja na mapendekezo ya sera ya usimamizi wa utendaji kazi.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing pamoja na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing pamoja na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing, Ujumbe Maalumu kwenda kwa Rais wa China Mhe. Xi Jinping mara baada ya mazungumzo, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi wa Chama cha Mapinduzi  (CCM) na Serikali kwenye picha na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing pamoja na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments





Kibaha, Pwani 
CCM leo imekuwa mwenyeji wa mkutano kati ya Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) na Vyama Sita Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika uliofanyika katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS), Kibaha.

Mkutano huo chini ya wenyeji wa Chama Cha Mapinduzi, ulikuwa sehemu ya ziara ya kikazi ya Komredi Liu Haixing, Mjumbe wa Kamati Kuu na Waziri wa Idara ya Mambo ya Nje wa CPC kutoka China.

Katika mkutano huo, viongozi wa vyama vya ukombozi kutoka ANC, FRELIMO, MPLA, SWAPO na ZANU-PF walijadiliana na CPC kuhusu kuimarisha mshikamano, kubadilishana uzoefu wa kiuongozi na kusukuma ajenda ya maendeleo ya kisasa kwa ustawi wa wananchi wao.

Viongozi hao pia walishiriki uzinduzi wa Kituo cha Tafiti kuhusu Fikra za Xi Jinping juu ya Ujamaa wenye Maono ya Kichina katika Zama Mpya, hatua inayolenga kuimarisha ushirikiano wa kielimu na maendeleo kati ya CCM na CPC.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments








Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar Dkt. Habiba Hassan Omar, amefanya ziara katika Ofisi za Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) na kukagua maandalizi ya Maonesho ya Jubilei ya Miaka 50 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (Sabasaba). Katika ziara hiyo, Katibu Mkuu alieleza kuridhishwa kwake na hatua zilizofikiwa hadi sasa na kufafanua umuhimu wa ushiriki wa wadau katika maonesho hayo makubwa.

Aidha, Dkt. Habiba alipata nafasi ya kuzungumza na Kamati ya Kitaifa ya Ulinzi na Usalama, ambayo inaratibu masuala ya kiusalama wakati wa kipindi chote cha maonesho. Mazungumzo hayo yalilenga kuhakikisha maandalizi ya Sabasaba yanakwenda sambamba na viwango vya usalama na uratibu wa kitaifa.

Kwa upande wa TanTrade, Mkurugenzi Mkuu Dkt. Latifa M. Khamis alieleza hatua zilizofikiwa katika maandalizi, ikiwemo uandaaji wa maeneo ya maonesho na programu maalum zitakazofanyika wakati wa maonesho ili kuonesha upekee wa Maonesho ya Jubilei ya Miaka 50 tofauti na yaliyopita. Maonesho haya yanatarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 28 Juni hadi 13 Julai 2026 katika Uwanja wa Maonesho wa Mwalimu J.K. Nyerere, Barabara ya Kilwa, Dar es Salaam
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya uteuzi wa Majaji wa Mahakama ya Rufani. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Moses Kusiluka, walioteuliwa kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani ni:-

(i) Mhe. Abdi Shaaban Kagomba – Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania,
        Kanda ya Dodoma;
(ii) Mhe. Yohane Bokobora Masara – Jaji wa Mahakama Kuu ya                         Tanzania, Kanda ya Arusha;
(iii) Mhe. Immaculata Kajetan Banzi – Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu         ya Tanzania, Kanda ya Kagera;
(iv) Mhe. Rabia Hussein Mohamed – Jaji wa Mahakama Kuu ya                         Zanzibar;

(v) Mhe. Cyprian Phocas Mkeha – Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
        Tanzania, Divisheni ya Biashara, Dar es Salaam;
(vi) Mhe. Yose Joseph Mlyambina – Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
        Tanzania, Divisheni ya Kazi, Dar es Salaam;
(vii) Mhe. Imani Daud Aboud – Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania,                 Kanda ya Dodoma;
(viii)Mhe. Mzee Ibrahim Ibrahim – Jaji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar;            na.
(ix) Mhe. Juliana Laurent Masabo – Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu             ya Tanzania, Kanda ya Dodoma.

Aidha, uapisho wa Majaji wateule wa Mahakama ya Rufani utafanyika kwa tarehe itakayopangwa baadaye.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments
KAMPUNI ya mawasiliano ya simu ya Airtel Tanzania na kampuni ya teknolojia ya Huawei zimethibitisha upya dhamira yao ya kuendelea kuimarisha huduma za mawasiliano nchini kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa na ubunifu vilivyojadiliwa katika Kongamano la Huawei Mini Mobile World Congress (Mini MWC).

Kampuni hizo zimesema ushirikiano wao unaendelea kulenga kuharakisha mageuzi ya kidijitali, kupanua huduma za mtandao na kuboresha uzoefu wa wateja kupitia suluhisho za kisasa za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa kongamano hilo lililofanyika Tanzania Mei 12, 2026, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, Charles Kamoto, alisema ushirikiano huo unaendelea kuwa sehemu muhimu katika kusaidia ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.

“Ni furaha kubwa kushiriki nanyi leo tunapojadili mustakabali wa sekta ya mawasiliano, mageuzi ya kidijitali na fursa zinazoendelea kujitokeza ndani ya soko letu na ukanda mzima,” alisema.

Mkutano huo uliwakutanisha viongozi na wataalamu wa kiufundi kutoka kampuni zote mbili kujadili teknolojia za baadaye zinazolenga kuboresha utoaji wa huduma na kuimarisha miundombinu ya mawasiliano nchini Tanzania.

Miongoni mwa maeneo ya kimkakati yaliyojadiliwa ni pamoja na ukuaji wa huduma za intaneti ya simu na majumbani, matumizi ya mitandao msingi inayotumia Akili Unde (AI), maendeleo ya teknolojia ya microwave pamoja na mifumo ya kisasa ya usafirishaji wa taarifa kwa njia ya kidijitali.

Kupitia ushirikiano huo, Airtel Tanzania na Huawei pia walijadili matumizi ya teknolojia za kisasa za wireless na AI zinazolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za mtandao, kuboresha uthabiti wa huduma, kuongeza uzoefu wa wateja na kupunguza matumizi ya nishati katika mifumo ya mawasiliano.

Kamoto alisema matumizi ya teknolojia za kizazi kijacho yataongeza matumizi ya data, kusaidia ukuaji endelevu wa biashara na kuiweka Airtel katika nafasi ya kuwa kampuni kinara wa mawasiliano ya kidijitali nchini.

“Tunaendelea kuwa na malengo makubwa na dhamira thabiti katika kusukuma mbele dira ya Airtel kupitia ubunifu na ujumuishaji,” alisema.

Kwa upande wake, Huawei ilisema ushirikiano wake na Airtel Tanzania utaendelea kuwa nguzo muhimu katika safari ya mageuzi ya kidijitali nchini Tanzania.

Kampuni hiyo pia iliipongeza menejimenti ya Airtel Tanzania kwa kushiriki katika majadiliano ya kimkakati yanayolenga kukuza sekta ya mawasiliano nchini na kuhamasisha matumizi ya teknolojia mpya zinazoibukia.

Mini MWC ni jukwaa maalum linaloandaliwa na Huawei Tanzania kwa ajili ya kuwapa wadau fursa ya kujionea teknolojia bunifu zinazooneshwa katika Kongamano la Kimataifa la Mobile World Congress linalofanyika kila mwaka mjini Barcelona, Hispania.

Jukwaa hilo pia linawawezesha wadau wa sekta ya mawasiliano kujadili mwenendo wa teknolojia mpya pamoja na matumizi yanayoongezeka ya Akili Unde (AI) katika kuboresha huduma za mawasiliano nchini.

Baadhi ya viongozi wa Huawei waliohudhuria kongamano hilo ni pamoja na Rais wa Idara ya Bharti Group Key Account, Jack Huang, pamoja na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Mauzo wa Huawei Tanzania, Galving Gao.

Kongamano hilo limefanyika wakati ambapo sekta ya mawasiliano nchini Tanzania inaendelea kushuhudia ukuaji mkubwa wa huduma za intaneti, matumizi ya huduma za kidijitali na ongezeko la matumizi ya data kutokana na mahitaji yanayoongezeka ya huduma bora na nafuu za mtandao.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments

MONACO - Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo ya Taifa kupitia sekta mbalimbali kwa kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 81 wa Michezo ya Majeshi Duniani (81st CISM General Assembly) uliofanyika nchini Monaco kuanzia tarehe 1 hadi 9 Mei 2026.

Mkutano huo wa kimataifa uliwakutanisha viongozi wa kijeshi na wadau wa michezo kutoka zaidi ya nchi 130 duniani kwa lengo la kuimarisha mshikamano, diplomasia ya michezo na amani kupitia kaulimbiu ya “Friendship Through Sport.”
Benki ya CRDB, ikiwa miongoni mwa wadau wakubwa wa maendeleo nchini, imeendelea kuunga mkono jitihada za vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na michezo ya majeshi, hatua inayoimarisha ushirikiano wake na taasisi za Serikali katika kukuza ustawi wa askari na familia zao.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Brigedia Jenerali Saidi Hamisi Saidi, akisaidiana na Luteni Kanali Penina Anthony Igwe. Kutoka CRDB, ujumbe unajumuisha Meneja wa Kitengo cha Wateja Maalum, Crispin Sichalwe pamoja na Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma, Emmanuel Tupeligwe.
Akizungumza kwenye mkutano huo, Sichalwe alisema CRDB imeendelea kutoa huduma maalum za kifedha kwa wanajeshi ndani na nje ya nchi, ikiwemo mikopo nafuu, bima na huduma za kifedha zinazowafikia popote walipo.

“Tunatambua mchango mkubwa wa majeshi katika usalama wa Taifa, hivyo tunahakikisha wanapata huduma bora na za haraka kupitia kitengo chetu maalum,” alisema.
Kwa upande wake, Tupeligwe alisisitiza kuwa CRDB itaendelea kushirikiana kwa karibu na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kupitia elimu ya fedha na huduma zinazowafikia wanajeshi hata wakiwa katika maeneo ya mbali au majukumu ya kimataifa.

Aidha, benki hiyo imeendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kimkakati na JWTZ ili kuhakikisha wanajeshi wanapata huduma bora za kifedha kwa urahisi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika maendeleo na usalama wa Taifa.

Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments



Na Mwandishi wetu, Njombe
Serikali imetangaza kuwa Mkoa wa Njombe unatarajiwa kuwa kitovu kipya cha uwekezaji wa madini nchini baada ya kugunduliwa kwa madini adimu ya Rare Earth Elements (REE) ya aina mbili ambayo ni Neodymium Nd na Praseodymium Pr yenye mahitaji makubwa katika teknolojia za kisasa duniani.

Akizungumza katika kijiji cha Mkiu Wilaya ya Ludewa, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Mhandisi Lucas Mlekwa, amesema utafiti wa madini hayo unaendelea kufanywa na kampuni ya Hongji Mining Co. Ltd kwa kushirikiana na wazawa, huku soko kubwa la madini hayo likiwa nchini China kutokana na ukuaji wa haraka wa sekta ya viwanda na teknolojia.

Amesema madini ya REE yanatumika katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, mitambo ya kuzalisha umeme wa upepo pamoja na vifaa mbalimbali vya kielektroniki vinavyotumika duniani kote.

“Mkoa wa Njombe unaendelea kufungua ukurasa mpya wa maendeleo kupitia rasilimali hizi muhimu ambazo zina mchango mkubwa katika mapinduzi ya teknolojia ya kijani duniani,” amesema Mhandisi Mlekwa.

Ameeleza kuwa kampuni hiyo tayari imekamilisha awamu ya kwanza ya utafiti na sasa ipo katika awamu ya pili ya uchunguzi wa kina kabla ya kuanza uzalishaji rasmi katika eneo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 280.
Kwa mujibu wa Mhandisi Mlekwa, zaidi ya shilingi bilioni moja tayari zimelipwa kama fidia kwa wananchi waliopisha mradi huo, huku tathmini ya athari kwa mazingira (EIA) ikiwa katika hatua za mwisho kukamilishwa kabla ya shughuli za uzalishaji kuanza.

Akizungumzia utekelezaji wa mradi huo, Mkurugenzi wa Hongji Mining Co. Ltd, Yahya Mohamed, amesema kampuni imechagua kutumia teknolojia ya In Situ Leaching ambayo inapunguza athari kwa mazingira kwa kutohusisha uchimbaji mkubwa wa mashimo ya wazi wala migodi ya chini ya ardhi.

Amesema matumizi ya teknolojia hiyo yatawezesha uchimbaji endelevu huku yakilinda mazingira na jamii zinazozunguka eneo la mradi.

“Tunataka kuona wananchi wa Njombe wanakuwa sehemu ya mafanikio ya mradi huu kupitia ajira, fursa za biashara na ongezeko la mapato ya kiuchumi,” amesema Mohamed.

Mradi huo unatarajiwa kuongeza mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa Mkoa wa Njombe, kuchochea uwekezaji mpya pamoja na kuiwezesha Tanzania kunufaika zaidi na soko la kimataifa la madini adimu ambalo linaendelea kukua kwa kasi duniani.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo