Nafasi Ya Matangazo

June 22, 2026







Dodoma
Banda la Tume ya Madini limeendelea kuwa kivutio kikubwa kwa mamia ya wananchi wanaotembelea Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, huku wengi wakijitokeza kupata elimu kuhusu sekta ya madini, huduma zinazotolewa na Tume  pamoja na fursa zilizopo katika shughuli za utafutaji, uchimbaji na biashara ya madini.

Miongoni mwa waliotembelea banda hilo ni Lusajo Luena kutoka Dodoma, ambaye amesema elimu aliyoipata imemwezesha kuelewa taratibu za upatikanaji wa leseni za madini na wajibu wa wamiliki wa leseni katika kuendeleza maeneo yao ya uchimbaji.

"Kabla ya kufika hapa sikuwa na uelewa wa kina kuhusu namna leseni za madini zinavyotolewa na kusimamiwa. Leo nimepata elimu ya kutosha kuhusu taratibu mbalimbali na umuhimu wa kuzingatia sheria za madini," amesema Luena.

Kwa upande wake, Joyce Kitundu kutoka Dodoma amesema maelezo aliyopata katika banda hilo yamemsaidia kufahamu mchango mkubwa wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa taifa na namna Serikali inavyosimamia rasilimali za madini kwa manufaa ya wananchi.

"Nimejifunza kuwa sekta ya madini ni nguzo muhimu ya maendeleo ya nchi. Pia nimeelewa majukumu ya Tume ya Madini katika kusimamia shughuli za uchimbaji na biashara ya madini nchini," amesema Kitundu.

Naye Glory Daudi kutoka Kondoa amesema elimu aliyopata imefungua fursa mpya za uelewa kuhusu ushiriki wa vijana na wanawake katika shughuli mbalimbali zinazohusiana na sekta ya madini.

"Nimefurahishwa na elimu niliyopewa kuhusu fursa zilizopo kwenye sekta ya madini. Sasa nimeelewa kuwa si lazima mtu awe mchimbaji pekee, kwani kuna fursa nyingi za biashara na utoaji huduma zinazozunguka sekta hii," amesema Daudi.

Tume ya Madini inaendelea kutumia maonesho hayo kutoa elimu kwa umma kuhusu majukumu yake, huduma mbalimbali zinazotolewa pamoja na kuhamasisha ushiriki wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya madini ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.
Posted by MROKI On Monday, June 22, 2026 No comments
Na Adelina Johnbosco - MAELEZO
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara, ameipongeza Ofisi ya Msemaji Mkuu wa Serikali na kusema inafanya kazi kubwa ya kuzitangaza shughuli zinazotekelezwa na Serikali pamoja na kuwafikia wananchi.

Prof. Kahyarara amesema hayo Juni 22, 2026, alipotembelea banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na taasisi zake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea kwenye viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.

"Serikali ina shughuli nyingi zinazofanyika ikiwemo miradi mbalimbali, mipango na malengo kwa ajili ya maendeleo na maslahi ya wananchi, hata ukisema kila siku au kila wiki utoke na kitu kimoja lakini bado inakuwa haitoshi, lakini Ofisi ya Msemaji Mkuu wa Serikali inajitahidi kwa kufanya kazi kubwa kwani taarifa zinatolewa kuhusu yanayotekelezwa na Serikali kwa wananchi wake" ameongeza Prof. Kahyarara.

Kwa upande mwingine, ameipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kufikia hatua nzuri katika maandalizi ya AFCON 2027 pia na taifa kwa ujumla kuwa miongoni mwa nchi zilizochaguliwa kuwa mwenyeji wa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) yanayotarajiwa kufanyika nchini Tanzania mwaka 2027.

"Hii inaonesha jinsi gani Tanzania imefikia hatua ya juu katika michezo na imeaminika na ina uwezo wa kuhudumia wageni, lakini pia itakuwa fursa ya kuutangaza utamaduni wetu kwa mataifa mengine" - Prof. Kahyarara. 

Aidha, amesema Wizara ya Uchukuzi tayari imejipanga katika sekta zake za usafiri na usafirishaji kwa kuhakikisha inawahudumia wenyeji na wageni kabla, wakati na baadaya ya AFCON 2027.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026 na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi. Dkt.  Moses Kusiluka
Posted by MROKI On Monday, June 22, 2026 No comments
Afisa Usimamizi wa Fedha Mkuu, Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha, Bw. Abdul Dachi, akitoa elimu kwa wananchi wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Afisa Habari Mkuu, Wizara ya Fedha, Bi. Eva Valeria (kulia) na Afisa Habari, Wizara ya Fedha, Bw. Joseph Mahumi, wakimpa mwanafunzi wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP), Bi. Nice Justace, maelekezo wa namna ya kujiunga na mitandao ya kijamii ya Wizara ya Fedha, ikiwemo, Instagram (urt mof), Facebook (Wizara ya Fedha), LinkedIn (Ministry of Finance -Tanzania), Youtube – Hazina TV.
Afisa Usimamizi wa Fedha Mwandamizi, Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha, Bi. Grace Samwel, akitoa elimu kwa wanafunzi wa Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) kuhusu matumizi ya huduma rasmi za kifedha, walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Mchumi Daraja la Kwanza, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPU), Wizara ya Fedha, Bi. Anastazia Amandi, akitoa elimu kwa mwananchi kuhusu mafanikio ya Ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP), walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Maafisa wa Wizara ya Fedha, wakiendelea kutoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, kuhusu majukumu yanayotekelezwa na wizara hiyo, wakati wananchi hao walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, yenye kauli mbiu ‘Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Maendeleo Endelevu’, yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.
Maafisa wa Wizara ya Fedha, wakiendelea kutoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, kuhusu majukumu yanayotekelezwa na wizara hiyo, wakati wananchi hao walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, yenye kauli mbiu ‘Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Maendeleo Endelevu’, yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.
Na Saidina Msangi na Asia Singano, WF - Dodoma
Wizara ya Fedha imeendelea kutoa elimu kwa umma ili kuhakikisha wananchi wanapata ufafanuzi kuhusu masuala ya kodi, uchumi na sera mbalimbali za fedha na mchango wa kodi katika kugharamia huduma muhimu za kijamii kama vile miundombinu, elimu, afya, maji nishati na huduma nyingine muhimu.
 
Hayo yamebainishwa na Afisa Usimamizi wa Fedha Mkuu, Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha, Bw. Abdul Dachi, wakati akitoa elimu kwa wananchi kwenye  Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.
 
Bw. Dachi alisema kupitia Maonesho hayo, Idara imekuwa ikitoa taarifa kwa wananchi kwa lugha rahisi na inayoeleweka ili kuwawezesha kufahamu mchango wa Sera za Kodi na Uchumi katika maendeleo ya Taifa na ustawi wa jamii.
 
‘‘Miongoni mwa maeneo yanayotolewa elimu ni kuhusu mwenendo wa uchumi wa Taifa na namna Sera za Uchumi zinavyosaidia kudhibiti mfumuko wa bei, kuongeza fursa za ajira na kukuza uchumi kwa ujumla pamoja na namna hizo zinavyoandaliwa ili kuhakikisha mapato ya Serikali yanakusanywa kwa ufanisi na kwa kuzingatia maslahi ya Taifa,’’, alisema Bw. Dachi.
 
Aliongeza kuwa Serikali inatumia taarifa za takwimu na tafiti mbalimbali zinazosaidia katika upangaji wa bajeti na utekelezaji wa mikakati ya maendeleo ya muda mfupi na mrefu pamoja na usimamizi wa mikataba ya kikodi kati ya Tanzania na mataifa mengine na ushirikiano wa kikanda na kimataifa unaolenga kulinda maslahi ya Taifa katika sekta ya kodi.
 
Alifafanua kuwa wananchi wanapatiwa elimu kuhusu namna Wizara inavyofanya tafiti za kisera na kuandaa mapendekezo ya kitaalamu yanayosaidia Serikali kufanya maamuzi yenye tija kwa maendeleo ya nchi pamoja na namna Serikali inavyoshughulikia masuala ya kodi za kimataifa.
 
‘’Tumetumia fursa hii kueleza wananchi umuhimu wa sera za kodi na fedha katika kukuza uchumi na ustawi wa wananchi, mchango wa kodi katika maendeleo ya Taifa, pamoja na umuhimu wa uwazi na uwajibikaji katika mchakato wa utungaji wa sera nafasi ya Tanzania katika uchumi wa dunia na manufaa yanayotokana na ushirikiano wa kiuchumi na mataifa na taasisi mbalimbali za kimataifa’’, alifafanua Bw. Dachi.
 
Alisema kuwa ili kuhakikisha ujumbe unawafikia wananchi wengi zaidi, idara pia inatoa vipeperushi, vitabu vya elimu pamoja na mazungumzo ya ana kwa ana na wageni wanaotembelea Banda hatua inayochangia kuongeza uelewa wa umma na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na wananchi katika maendeleo ya Taifa.

Posted by MROKI On Monday, June 22, 2026 No comments

June 21, 2026





📍Dodoma
Tume ya Madini imeendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa leseni za madini nchini kwa lengo la kufuatilia maendeleo ya leseni hizo na kuhakikisha shughuli za utafutaji na uchimbaji wa madini zinafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Akizungumza katika Banda la Tume ya Madini kwenye Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park mkoani Dodoma, Mtakwimu kutoka Kurugenzi ya Leseni ya Tume ya Madini, Azihar Kashakara, amesema ukaguzi huo ni muhimu katika kuhakikisha wamiliki wa leseni wanatimiza masharti na wajibu unaotokana na leseni walizopewa.

Amesema kuwa, pamoja na kufuatilia maendeleo ya leseni, Kurugenzi ya Leseni ina jukumu la kutoa na kusimamia leseni za madini, kutafsiri na kusambaza takwimu za leseni, pamoja na kuwezesha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali yatokanayo na umiliki wa leseni hizo.

Kashakara ameeleza kuwa utoaji wa leseni za madini unazingatia masharti na vigezo vilivyowekwa kisheria, hivyo waombaji wanapaswa kuyatimiza ili kuwezesha upatikanaji wa leseni kwa wakati. 

Aidha, ametoa ufafanuzi kuhusu ada na tozo mbalimbali zinazohusiana na leseni za madini, sambamba na kueleza tofauti kati ya umiliki wa ardhi (Surface Rights) na umiliki wa haki za madini (Mineral Rights).

Tume ya Madini ni miongoni mwa taasisi zinazoshiriki Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma chini ya kaulimbiu isemayo, “Kuchochea Uwajibikaji kwa Huduma Endelevu.” 

Kupitia maonesho hayo, wananchi na wadau wa sekta ya madini wanapata fursa ya kuelimishwa kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na Tume ya Madini pamoja na mchango wake katika usimamizi endelevu wa rasilimali za madini kwa maendeleo ya taifa.
Posted by MROKI On Sunday, June 21, 2026 No comments
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na Waumini wa Kanisa Kuu Anglikana la Roho Mtakatifu Dodoma mara baada ya kushiriki Ibada ya jumapili katika kanisa hilo leo tarehe 20 Juni, 2026.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na Waumini wa Kanisa Kuu Anglikana la Roho Mtakatifu Dodoma mara baada ya kushiriki Ibada ya jumapili katika kanisa hilo leo tarehe 20 Juni, 2026.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akishiriki Ibada ya Jumapili katika Kanisa Kuu Anglikana la Roho Mtakatifu Dodoma leo tarehe 20 Juni, 2026. (kulia kwake ni Katibu wa Bunge Ndg. Baraka Leonard.
***********
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Watanzania kushirikiana na Serikali katika kutunza na kuhudumia vituo vya watoto wenye mahitaji maalumu na wasiojiweza badala ya kutegemea wahisani kutoka nje kwani mambo hayo yamepitwa na wakati.
 
Ametoa kauli hiyo leo Jumapili, Juni 21, 2026 katika harambee ya uchangiaji wa jengo la kitega uchumi cha kanisa la Anglika jijini Dodoma. “Mambo ya misaada yamepitwa na wakati na hata katika bajeti Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kusisitiza kuwa na bajeti ya nchi ambayo inategemea rasilimali za ndani ya nchi”.
 
Pia, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa rai halmashauri zote nchini ziandae orodha ya vituo vya kulelea watoto wenye mahitaji maalumu na wasiojiweza na kuona namna ya kuvisaidia ambapo amesisitiza si vema kuwaandikia watu hao barua za kwenda kuomba misaada pindi wanapofika kwenye ofisi za umma.
 
Waziri Mkuu amesema awali katika maeneo mbalimbali nchini ilizoeleka kuwa vituo vya kulelea watoto yatima na wenye mahitaji maalumu viliendeshwa kupitia misaada kutoka nje ya nchi dhana ambayo watu wanatakiwa kuachana nayo.
 
Kadhalika, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwahimiza Watanzania kuendelea kusimama katika mafundisho mbalimbali yanayotolewa na viongozi wa dini ikiwemo kuendeleza amani na umoja wa kitaifa.
 
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan analipongeza Kanisa la Anglikana Tanzania kwa kuendeleza mradi wa ujenzi wa kitega uchumi kwa sababu ukuaji wa uchumi ni miongoni mwa malengo muhimu ya maendeleo.
 
Awali, Katibu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Kasisi Canon Dkt. George Lawi alisema ili kuimarisha uwezo wa kifedha na kupunguza utegemezi, Kanisa la Anglikana Tanzania lilianzisha mradi wa kitega uchumi jijini Dodoma na kuhakikisha linakuwa na vyanzo endelevu vya mapato vitakavyowezesha utekelezaji wa majukumu ya kiroho na kijamii kwa ufanisi zaidi.
 
Alisema jengo hilo linatarajiwa kutoa huduma mbalimbali zikiwezo za hoteli, ofisi na hivyo kuchangia katika kukuza uchumi wa kanisa na Taifa kwa ujumla. Mradi huu umefikia hatua ya umaliziaji na umeshagharimu shilingi bilioni tatu na bado zinahitajika shilingi bilioni 1.5 ili kukamilisha na ndiyo sababu ya kufanya harambee leo.
 
Pia, Dkt. Lawi alitumia fursa hiyo kumuahidi Waziri Mkuu kuwa Kanisa Anglikana Tanzania litaendelea kuwa mshirika wa Serikali katika juhudi za kuwaletea wananchi maendeleo endelevu kupitia sekta za elimu, afya, uwezeshaji wa jamii na kukuza maadili mema.
 
Katika harambee hiyo zaidi ya shilingi bilioni moja zilipatikana, ambapo pia Kanisa Anglikana limempa Heshima ya Kikanisa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Lay Canon, mshauri wa mambo ya Kanisa baada ya kuridhishwa na utendaji wake.
Posted by MROKI On Sunday, June 21, 2026 No comments

June 20, 2026










Dar es Salaam
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema Serikali imejipanga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha madini ya kimkakati na shughuli za uongezaji thamani barani Afrika, huku akizitaka taasisi za sekta hiyo kutumia fursa zilizopo kuhakikisha nchi inahudumia masoko ya kikanda na kimataifa.

Mhe. Mavunde ameyasema hayo Juni 19, 2026, baada ya kufanya ziara katika Kituo cha African Minerals and Geoscience Centre (AMGC) kilichopo Kunduchi jijini Dar es Salaam, ambapo alipata fursa ya kutembelea maabara, kitengo cha ukataji, utengenezaji na usafishaji wa vito pamoja na  kuzungumza na viongozi pamoja na watumishi wa kituo hicho.

“Tumedhamiria kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha madini ya kimkakati barani Afrika. Tunayo nafasi kubwa kutokana na eneo letu la kijiografia na miundombinu iliyopo, hivyo ni lazima tutumie fursa hii kuhakikisha tunazihudumia nchi zote zinazotuzunguka na kuifanya Tanzania kuwa lango la huduma za madini katika ukanda huu,” amesema Waziri Mavunde.

Amesema Serikali kupitia Wizara ya Madini inaendelea kutekeleza programu ya *Mining for a Brighter Tomorrow*, inayolenga kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kiuchumi kupitia sekta ya madini.

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, programu hiyo itahusisha utoaji wa mafunzo ya kitaalamu katika vituo mbalimbali vya sekta ya madini ikiwemo AMGC, ambapo wanufaika watapatiwa maarifa pamoja na teknolojia na mashine ndogo zitakazowawezesha kujiajiri na kuongeza kipato chao.

“Tutawaleta vijana, kina mama na watu wenye ulemavu hapa AMGC wapatiwe mafunzo maalum, na baada ya hapo waweze kupata vifaa na mashine ndogo zitakazowawezesha kujiajiri na kuboresha maisha yao kupitia shughuli za madini,” ameeleza.

Katika ziara hiyo, Waziri Mavunde amesema amevutiwa na kiwango cha utaalamu kilichopo AMGC, hususan katika ukataji na utengenezajishaji wa madini ya vito, akisema dhana iliyokuwa imejengeka kuwa Tanzania haina wataalamu wa kutosha katika eneo hilo siyo sahihi.

“Kwa muda mrefu tuliaminishwa kwamba hatuna wataalamu wa kutosha katika ukataji wa madini ya vito, lakini leo nimeshangazwa kukutana na wataalamu wazawa wenye uwezo mkubwa wa kukata na kutengeneza vito kwa viwango vya kimataifa. Huu ni uthibitisho kwamba tuna rasilimali watu wenye uwezo wa kuipeleka Tanzania mbele zaidi,” amesema.

Aidha, Waziri Mavunde amesema hiyo ilikuwa ziara yake ya kwanza katika kituo hicho na kuahidi kukitangaza kimataifa ili kuvutia wawekezaji, wataalamu na wadau mbalimbali wa sekta ya madini kutoka ndani na nje ya Afrika.

“Niwahakikishie kwamba tutakitangaza kituo cha AMGC kimataifa ili Tanzania iwe kitovu cha uongezaji thamani wa madini barani Afrika. Pia nitarudi tena hapa kukutana na watumishi wote, kusikiliza changamoto zao na kujadiliana namna bora ya kukiendeleza kituo hiki,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa AMGC, Ibrahim Shaddad, amesema kituo hicho kinakabiliwa na changamoto ya uhaba wa watumishi, ambapo kwa sasa kina watumishi wa kudumu 17 na watumishi wa mikataba ya muda mfupi 12, hali inayokifanya kushindwa kutekeleza kikamilifu baadhi ya majukumu yake.

Aidha, Shaddad amemuomba Waziri wa Madini kusaidia katika upatikanaji wa fedha za uendeshaji wa kituo hicho, hususan kupitia nchi wanachama ambazo kwa mujibu wa sheria zinapaswa kuchangia gharama za uendeshaji, lakini baadhi yake zimekuwa zikichelewesha au kutotekeleza wajibu huo.

Shaddad amesema ucheleweshaji wa michango kutoka kwa baadhi ya nchi wanachama umeendelea kuathiri shughuli za kila siku za AMGC na kusababisha upungufu wa fedha za uendeshaji.

Ametaja Tanzania, Kenya, Angola na Sudan kuwa miongoni mwa nchi zinazowasilisha michango yao kwa wakati, huku baadhi ya nchi nyingine ikiwemo Msumbiji, Ethiopia, Comoro, Sudan Kusini na Uganda zikikabiliwa na changamoto ya kutowasilisha michango hiyo kwa wakati.

AMGC ni taasisi ya kikanda inayojihusisha na tafiti za jiolojia, huduma za maabara, mafunzo na maendeleo ya teknolojia za madini kwa nchi wanachama wa Afrika, na imeendelea kuwa moja ya taasisi muhimu katika kuendeleza sekta ya madini na kuongeza thamani ya rasilimali za madini barani Afrika. Uh
Posted by MROKI On Saturday, June 20, 2026 No comments

June 19, 2026




Na Adelina Johnbosco - MAELEZO
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, amesema benki hiyo itaendelea kuwa mdau mkubwa wa maendeleo ya michezo nchini kwa kushiriki kikamilifu kufanikisha mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) yanayotarajiwa kufanyika nchini Tanzania mwaka 2027.

Dkt. Nsekela ametoa kauli hiyo Juni 19, 2026, alipotembelea banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea kwenye viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.

Amesema CRDB iko tayari kushirikiana kwa karibu na wizara hiyo katika kuhakikisha maandalizi na utekelezaji wa AFCON 2027 unafanikiwa kwa kiwango kikubwa.

"Sisi CRDB tunaahidi kuwa na wizara hii bega kwa bega kila hatua pale tutakapohitajika. Ni wadau wakubwa wa michezo na sekta nyingine zilizo chini ya wizara hii, hivyo nawahakikishia kwamba tutashiriki kwa nguvu zote kuifanikisha AFCON 2027," amesema Dkt. Nsekela.

Mbali na ahadi hiyo, Dkt. Nsekela ameipongeza Wizara kwa namna ilivyojipanga katika kutoa huduma na elimu kwa wananchi kupitia maonesho hayo, akieleza kuwa ushiriki wa taasisi zote chini ya wizara hiyo umeongeza ufanisi wa utoaji huduma.

"Hii ni wizara inayogusa sekta nyingi muhimu. Mmefanya vizuri kushiriki maonesho haya pamoja na taasisi zenu zote ili mwananchi anapohitaji msaada asikwame, bali apate suluhisho kwa haraka na urahisi," ameongeza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu wa Wizara hiyo, Bi. Savera Salvatory, ameishukuru Benki ya CRDB kwa ahadi ya ushirikiano na kuipongeza kwa mchango wake katika maendeleo ya sekta ya michezo na maeneo mengine ya kijamii.

Bi. Savera amesema wizara itaendelea kuboresha huduma zake kwa wananchi na kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha sekta zilizo chini yake zinapiga hatua zaidi.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026.
Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments




Dodoma
Tume ya Madini imeendelea kuimarisha ukaguzi wa migodi nchini kupitia Kurugenzi ya Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kwa lengo la kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinafanyika kwa usalama, ufanisi na kwa kuzingatia uhifadhi wa mazingira, hatua inayolenga kuhakikisha rasilimali za madini zinanufaisha kizazi cha sasa na kijacho.

Akizungumza Juni 19, 2026, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, Afisa Mkaguzi wa Migodi wa Tume ya Madini, Rose Mika, amesema ukaguzi wa mara kwa mara unaofanyika katika migodi mikubwa, ya kati na midogo unalenga kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinaendeshwa kwa kuzingatia Sheria ya Madini pamoja na Kanuni za Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira za mwaka 2010.

Amesema ukaguzi huo husaidia kubaini mapema changamoto zinazoweza kuhatarisha usalama wa wafanyakazi na wananchi wanaoishi jirani na maeneo ya migodi, hivyo kuwezesha hatua stahiki kuchukuliwa kabla ya kutokea kwa madhara.

Rose amesema Tume ya Madini pia inaendelea kusimamia utekelezaji wa mipango ya usimamizi wa mazingira, ikiwemo kudhibiti uchafuzi wa maji, hewa na ardhi pamoja na kuhakikisha taka zinazotokana na shughuli za uchimbaji zinahifadhiwa na kushughulikiwa kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa.

Aidha, amesema Tume inafuatilia utekelezaji wa mipango ya kufunga migodi (Mine Closure Plans) ili kuhakikisha maeneo yaliyokwishafanyiwa uchimbaji yanarejeshwa katika hali salama na yenye tija baada ya shughuli hizo kukamilika.

Kwa mujibu wa Rose, hatua hiyo ni muhimu katika kuhakikisha ukuaji wa sekta ya madini unaenda sambamba na uhifadhi wa mazingira na ustawi wa jamii zinazozunguka maeneo ya migodi.

Mbali na ukaguzi wa migodi, Tume ya Madini inaendelea kusimamia matumizi ya baruti katika shughuli za uchimbaji, ikiwemo utengenezaji, uingizaji, usafirishaji na biashara yake kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizopo.

Katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, Tume ya Madini inaendelea kutoa elimu kwa wananchi na wadau kuhusu fursa mbalimbali zilizopo katika sekta hiyo na kuwahamasisha kushiriki katika shughuli za utafiti, uchimbaji, uchenjuaji, biashara ya madini pamoja na utoaji wa huduma kwenye migodi ya madini kwa kuzingatia matakwa ya sheria, ili kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments

Na Oscar Nkembo
Msimamizi wa Dawati la Ukaguzi wa Kemikali wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali Ofisi ya Kanda ya Kati, Suitbert Sinduhije amesema Mamlaka imedhibiti Kemikali ya Sulphur iliyomwagika eneo la Mikumi na amewataka Madereva kuzingatia mafunzo wanayopata huku akiwasihi Wananchi kutoa taarifa kwa Mamlaka pindi ajali za Kemikali zinapotokea.

Sinduhije amesema hayo Juni 18, 2026 baada ya kukamilisha zoezi la kuiondoa Kemikali iliyomwagika ikiwa inasafirishwa kwa njia ya barabara ambapo alisema.

“Tumepata Taarifa kuhusu Kemikali hii iliyomwagika tumefika kwaajili ya kudhibiti na hali ni shwari athari ndogo ndogo zilizosababishwa na vumbi la Kemikali hiyo ni kusikia muwasho mwishili na usoni ambapo kunywa maji mengi na kuosha eneo lililofikiwa na Kemikali inamuweka mwananchi salama kabisa, nawasihi Madereva kuzingatia mafunzo ambayo Mkemia Mkuu amewapa, pia nawaomba wananchi waendelee kutupa taarifa pindi matukio haya yanapotokea ili yakabiliwe kwa wakati bila madhara kwa wananchi” alisema Sinduhije.

Aggrey Kinzilizi na Yusta Komba ni wakazi wa Mikumi wanaofanya Biashara kando ya Barabara wamesema wamesikia muwasho sehemu zao za mwili baada ya vumbi la Kemikali hiyo kuwafikia.

“Magari yanapopita yanatibua ile Kemikali inakuja huku kiukweli ni kuwashwa mwanzo mwisho, Mkemia amefika akatueleza tunawe kwa maji mengi kwa sasa hamna tena ule muwasho, tunaomba hawa wanaosafirisha Kemikali wasiwe peke yao Mkemia wa Serikali awe anawafuatilia kwa nyuma ili changamoto hizi zisitukute” walisema wakazi hao wa Mikumi.
 
Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments

 

Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu haki za binadamu na utawala bora sambamba na kupokea na kushughulikia malalamiko mbalimbali katika Maonesho ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma leo Juni 18, 2026.

Akiongoza utoaji wa elimu hiyo, Kaimu Katibu Mtendaji wa THBUB ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Haki za Binadamu na utawala bora , Bi. Suzan P. Ndeona amefafanua kuhusu msingi wa kuanzishwa kwa Tume kwa mujibu wa Katiba, majukumu yake, pamoja na huduma mbalimbali zinazotolewa kwa wananchi.

Amesema Tume inaendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali katika jamii ikiwemo wanafunzi kupitia uanzishwaji wa vilabu vya haki za binadamu katika taasisi za elimu.

Akizungumzia mwitikio wa wananchi, Mchunguzi Mkuu Msaidizi wa THBUB, Bw. Botea Halfani amesema zaidi ya wananchi 35 wametembelea banda la Tume kupata elimu na kuwasilisha changamoto mbalimbali zinazowakabili ili zipatiwe ufumbuzi.

Amesema baadhi ya malalamiko yaliyopokelewa yanahusu mtoto kukosa matunzo kutoka kwa wazazi wake pamoja na mgogoro wa ardhi uliowasilishwa na mwananchi kutoka mkoani Manyara. Malalamiko hayo yamefanyiwa kazi na wahusika kuelekezwa katika mamlaka husika kwa hatua zaidi za utatuzi.

THBUB inaendelea kutumia maonesho hayo kama jukwaa la kuwafikia wananchi kwa karibu, kuwajengea uelewa kuhusu haki zao na kusikiliza changamoto zinazohusu haki za binadamu na utawala bora. Wananchi wote wanakaribishwa kutembelea banda la Tume ili kupata elimu, ushauri na huduma mbalimbali zinazotolewa.
Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments

June 18, 2026

Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, akizungumza wakati akifungua Kikao cha Jukwaa la Taifa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa kilicholenga kupitia na kuthibitisha Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa, Mwongozo wa Uendeshaji na Uratibu wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa, pamoja na Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS) jijini Dodoma.







Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SERIKALI imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kuongeza uwezo wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa, kufuatia kuongezeka kwa matukio yanayochochewa na mabadiliko ya tabianchi pamoja na vihatarishi vingine vya asili na kijamii.

Hayo yameelezwa leo Juni 18, 2026 jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, wakati akifungua Kikao cha Jukwaa la Taifa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa kilicholenga kupitia na kuthibitisha Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa, Mwongozo wa Uendeshaji na Uratibu wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa, pamoja na Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS).

Brigedia Jenerali Ndagala amesema kuwa katika miaka ya hivi karibuni Tanzania imekumbwa na matukio mbalimbali ya maafa yakiwemo mafuriko, ukame, maporomoko ya ardhi, upepo mkali, magonjwa ya mlipuko na ajali mbalimbali, hali ambayo imeathiri maisha ya wananchi, miundombinu, mazingira na shughuli za kiuchumi.

“Kwa kuzingatia hali hiyo, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuimarisha sera, mifumo, mikakati, mipango na nyenzo mbalimbali za usimamizi wa maafa ili kuhakikisha hatua zote za kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa zinafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya Mwaka 2022,” amesema.

Amesema kikao hicho ni hatua muhimu katika kuimarisha uratibu wa kitaifa wa usimamizi wa maafa kwa kuwa kinahusisha uthibitishaji wa nyenzo tatu muhimu zitakazochangia uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi wakati wa maafa na baada ya maafa.

Kwa mujibu wa Brigedia Jenerali Ndagala, Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa utaweka mfumo wa pamoja wa kitaifa wa kupanga na kuratibu shughuli za urejeshaji baada ya maafa, huku Mwongozo wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa ukiboresha utaratibu wa utoaji wa misaada ya fedha kwa waathirika. Aidha, Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS) utaimarisha ukusanyaji, uchambuzi, uhifadhi na matumizi ya taarifa za maafa kwa ajili ya kufanya maamuzi sahihi na kwa wakati.

“Nyenzo hizi zina mchango mkubwa katika utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya Mwaka 2022 kwa kuimarisha usimamizi wa taarifa, uratibu wa wadau, utoaji wa misaada na shughuli za urejeshaji hali baada ya maafa. Vilevile, zinachangia utekelezaji wa Mfumo wa Sendai wa Kupunguza Hatari za Maafa kwa kuimarisha uelewa wa hatari za maafa, usimamizi wa vihatarishi, uwekezaji katika ustahimilivu na kuimarisha hatua za kujiandaa na kujenga upya kwa ubora zaidi baada ya maafa,” amesisitiza.

Ameeleza kuwa mafanikio yanayoendelea kupatikana katika sekta ya usimamizi wa maafa nchini yanatokana na ushirikiano madhubuti kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, mashirika ya Umoja wa Mataifa, sekta binafsi na asasi za kiraia.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), Bi. Judith Bihondwa, amesema shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha uwezo wa jamii kukabiliana na maafa pamoja na kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.

Amesema ushirikiano huo utaendelea kulenga kuimarisha mifumo ya maandalizi, mwitikio na urejeshaji hali baada ya maafa kwa kuzingatia makundi yote ya jamii, hususan watoto na watu walio katika mazingira hatarishi.

Kikao hicho kimewakutanisha wadau mbalimbali wa usimamizi wa maafa kutoka taasisi za Serikali, mashirika ya Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na wadau wa maendeleo kwa lengo la kujadili na kuthibitisha nyenzo zitakazochangia kuimarisha usimamizi wa maafa na kuongeza ustahimilivu wa jamii nchini.
Posted by MROKI On Thursday, June 18, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo