Nafasi Ya Matangazo

May 03, 2026

Na Mwandishi Wetu, Njombe
Njombe. CRDB Bank Plc imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuunga mkono wafanyakazi na maendeleo ya taifa kwa kudhamini na kushiriki kikamilifu maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani kwa mwaka 2026 yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe.

Maadhimisho hayo yameongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, yakikusanya mamia ya wafanyakazi kutoka sekta mbalimbali, taasisi za umma na binafsi, pamoja na wadau wa maendeleo kwa lengo la kutambua mchango wa wafanyakazi katika kukuza uchumi wa nchi.
Kupitia ushiriki wake, CRDB imeungana na Watanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa kusherehekea nafasi ya wafanyakazi katika kuimarisha uzalishaji, ubunifu na ustawi wa jamii. Benki hiyo imekuwa miongoni mwa taasisi zinazoendelea kusisitiza umuhimu wa mazingira bora ya kazi na uwekezaji katika rasilimali watu kama msingi wa maendeleo endelevu.

Ujumbe wa benki hiyo katika maadhimisho hayo uliongozwa na Mkurugenzi wa Rasilimali Watu, Godfrey Rutasingwa, aliyeambatana na timu ya wataalamu kutoka makao makuu, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini pamoja na matawi mbalimbali ya mkoani Njombe.
Akizungumza pembeni mwa maadhimisho hayo, Rutasingwa alisema ushiriki wa CRDB katika Mei Mosi unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuthamini wafanyakazi wake na kuchangia ustawi wa jamii kwa ujumla.

Alibainisha kuwa CRDB imeendelea kuwekeza katika maendeleo ya wafanyakazi wake kupitia mafunzo endelevu, kuboresha mazingira ya kazi na kutoa motisha mbalimbali zinazolenga kuongeza tija na ubunifu kazini.

“Wafanyakazi ndio injini ya mafanikio ya taasisi yoyote. Ndiyo maana sisi kama CRDB tunaendelea kuhakikisha tunajenga mazingira rafiki yanayowawezesha kufanya kazi kwa ufanisi na ubunifu zaidi,” alisema.

Aidha, aliongeza kuwa benki hiyo itaendelea kushirikiana na serikali na wadau wengine katika kusaidia juhudi za kukuza uchumi jumuishi unaowanufaisha Watanzania wengi zaidi.
Maadhimisho ya mwaka huu yameongozwa na kaulimbiu isemayo “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” ikisisitiza umuhimu wa ajira zenye hadhi, haki na usawa katika kufikia malengo ya maendeleo ya muda mrefu.

Ushiriki wa CRDB katika tukio hilo umeendelea kudhihirisha nafasi ya sekta ya fedha katika kusaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi, huku benki hiyo ikiendelea kuwa mshirika muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi imara na shindani.
Posted by MROKI On Sunday, May 03, 2026 No comments

May 02, 2026










Na Mwandishi Wetu,Songwe
Tanzania imeanza rasmi Safari Mpya ya Kihistoria ikiingia kwenye ramani ya dunia kama Mzalishaji na Msambazaji wa kimkakati wa Gesi ya Helium. Hatua hiyo inafuatia baada ya kusainiwa kwa Mkataba wa Uchimbaji wa gesi hiyo baina ya Serikali na kampuni ya Helium One Global Limited kupitia Kampuni ya Ubia ya Songwe Helium Limited, katika hafla iliyofanyika Mei 2, 2026 Mkoani Songwe.

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Madini  Dkt. Steven  Kiruswa wakati akizungumza katika hafla  hiyo na kueleza kuwa, uzalishaji wa helium duniani kwa sasa unatawaliwa na nchi chache, hususan Marekani na Qatar, zinazochangia zaidi ya asilimia 75 ya uzalishaji wote, huku Urusi, Algeria, Canada, China na Poland zikichangia kwa kiwango kidogo. Ameongeza kuwa mahitaji ya gesi hiyo tayari yamevuka futi za ujazo bilioni 6 kwa mwaka na yanatarajiwa kuongezeka hadi zaidi ya bilioni 8.5 ifikapo mwaka 2030 ambapo kwa Tanzania kampuni za Helium One Global Limited na Noble Helium zimepiga hatua kubwa katika shughuli za utafiti wa gesi hiyo.

Ameeleza kuwa, mradi wa Southern Rukwa ni wa kimkakati unaoiwezesha Tanzania kuingia kwenye soko lenye thamani kubwa na ushindani mdogo na kuiweka katika nafasi ya kuathiri mwelekeo wa soko la helium duniani, huku ikitarajiwa kuwa sehemu ya suluhisho la uhaba wa gesi hiyo duniani na kueleza kwamba, uchimbaji wa helium utakwenda sambamba na gesi ambata kama hydrogen ambapo manufaa yake kimapato yatatenganishwa.

Aidha, Dkt. Kiruswa  amefafanua kwamba kupitia mkataba huo, Serikali itamiliki asilimia 17 ya hisa katika kampuni ya ubia ya  Songwe Helium Limited, hatua inayoiwezesha kushiriki moja kwa moja katika maamuzi ya kimkakati na kunufaika na mapato ya mradi kwa manufaa ya Taifa na wananchi.

‘’Huu ni utekelezaji halisi wa falsafa ya Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa rasilimali za nchi lazima ziwe chanzo cha ustawi wa taifa,’’ amesema Dkt. Kiruswa.

Akizungumzia manufaa mengine ya mradi huo amesema  utachangia ajira kwa vijana wa eneo husika na taifa kwa ujumla, fursa za kibiashara kwa wazawa kupitia huduma za ugavi, uboreshaji wa miundombinu, mapato kwa Serikali na fedha za kigeni na uboreshaji wa miundombinu muhimu kama  barabara na huduma za kijamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Helium One Global Limited, Lorna Blaisse amesema utiaji saini huo ni hatua muhimu kwa Tanzania na soko la helium duniani, akibainisha kuwa mradi una akiba yenye thamani kubwa na unaelekea kwenye uzalishaji wa kibiashara baada ya mafanikio ya  uchimbaji kisima mwaka 2024 ambacho kilipelekea ugunduzi wa helium katika kisima cha Itambula West-1.

‘’Katika upimaji wa kisima uliopanuliwa robo ya tatu ya 2024, kisima cha ITW-1 kilirekodi helium yenye mkusanyiko wa asilimia 5.5 hadi juu ya ardhi, na hadi asilimia 7.6 kutoka miamba ya Karoo iliyovunjika na miamba ya Basement iliyopasuka,’’ amesema

Amesema baada ya utiaji saini wa leseni ya uchimbaji, kampuni ya Songwe Helium Ltd itaendelea na hatua za uendeshaji kuelekea uzalishaji wa kwanza wa kibiashara wa heliamu.  Amezitaja hatua hizo kuwa ni pamoja na kukamilisha mipango ya maendeleo; mfumo wa usimamizi wa tathmini ya athari za mazingira na jamii; kubuni miundombinu, na kununua vifaa vya uchakataji na usafirishaji wa bidhaa.

Pia, ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano wake na kuridhia muundo wa ubia unaohakikisha nchi inanufaika na rasilimali zake, akibainisha dhamira ya kuzalisha helium ya Tanzania kwa uwajibikaji na ubora wa juu kwa soko la dunia.

Awali, akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Majadiliano ya Wizara ya Madini Prof. Sifuni Mchome amesema  kupitia utaratibu wa Serikali kumiliki hisa huru zisizohafifishwa thamani, Serikali inashiriki moja kwa moja katika miradi ya madini, inapata faida kupitia gawio, mrabaha,kodi  na tozo mbalimbali, inashiriki maamuzi ya kimkakati, kulinda mapato na maslahi ya wananchi kwa uwazi na uwajibikaji.

" Tulijadiliana kwa utaratibu mzuri bila kugombana na tumefika kwenye hatua ya kila mmoja apate, na leo tuko hapa kuweka wazi na kila mmoja ashuhudie," amesema Prof. Mchome.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Songwe  Mhe. Jabiri Makame amesema Mkoa huo ni wa kimkakati ukiwa na utajiri wa Madini mbalimbali yakiwemo ya rare earth elements ambao utafiti wake unaendelea.

" Tunaipongeza Wizara ya Madini kwa kutafsiri kwa vitendo. Kwetu sisi suala la kuwasaidia wawekezaji kutekeleza mradi Kwa mafanikio ni kipaumbele cha kwanza," amesema Mhe. Makame.

Helium ni gesi ya kipekee sana duniani kwa sababu haina mbadala wake na matumizi yake ni ya kimkakati kwa maisha ya kisasa ya binadamu; inatumika katika vifaa vya tiba kama MRI, uzalishaji wa vifaa vya kielektroniki na teknolojia za kidigitali;  sekta ya anga; ulinzi na tafiti za kisayansi, teknolojia za kisasa kama fibre optics  na quantum computing.

 Mradi huo unatekelezwa katika eneo la kilomita za mraba 480 ukiwa zaidi katika Mkoa wa Songwe Wilaya ya Momba na sehemu ndogo ikiingia Mkoa wa Rukwa.
Posted by MROKI On Saturday, May 02, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu

Manyara. Kampuni ya Mati Super Brands Ltd imeibuka kinara katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yaliyofanyika kimkoa mwaka 2026, baada ya kuonesha ubunifu wa hali ya juu na ushindani uliovutia katika vipengele mbalimbali vya sherehe hizo.

Katika tukio hilo lililofanyika kwa shamrashamra kubwa, kampuni hiyo ilitwaa ushindi wa jumla, ikiibuka bora katika maandamano ya miguu, ubunifu wa magari pamoja na uandaaji wa banda bora, hatua iliyowavutia waamuzi na washiriki wengine.
Akizungumza wakati wa kukabidhi tuzo hizo Mei 1, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, aliipongeza Mati Super Brands Ltd kwa ubunifu na kujituma kwake, akisema imeonesha mfano bora wa ushiriki wa sekta binafsi katika kuadhimisha siku hiyo muhimu kwa wafanyakazi.

“Tumeshuhudia ushindani wa hali ya juu mwaka huu, lakini Mati wamejitofautisha kwa ubunifu, mpangilio na ujumbe waliouwasilisha. Hii ni ishara ya kampuni inayojali wafanyakazi na maendeleo ya jamii,” alisema Sendiga.

Kufuatia ushindi huo, kampuni hiyo ilikabidhiwa kombe la ubingwa wa jumla pamoja na cheti cha pongezi, ikiwa ni kutambua mchango wake katika kuhamasisha ari ya kazi na ubunifu katika maadhimisho ya Mei Mosi.

Kwa niaba ya kampuni, Afisa Rasilimali Watu wa Mati Super Brands Ltd, Doreen Mushi, alipokea tuzo hizo na kueleza kuwa ushindi huo ni matokeo ya mshikamano na jitihada za wafanyakazi wa kampuni hiyo.

Alisema kampuni itaendelea kuwekeza katika ubunifu na kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza tija na kuchangia maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

“Ushindi huu unatupa motisha ya kufanya zaidi. Tutazidi kubuni na kuboresha shughuli zetu ili kuendana na mahitaji ya soko na dira ya maendeleo ya taifa,” alisema Mushi.

Naye Mwenyekiti wa Makampuni ya Mati, David Mulokozi, alibainisha kuwa kampuni hiyo inaendelea kuwekeza katika sekta ya kilimo kwa kuzingatia mwelekeo wa serikali wa kuimarisha uzalishaji kupitia teknolojia za kisasa.

Alifafanua kuwa kampuni hiyo imeanza kuzalisha vifaa vya kisasa ikiwemo ndege nyuki (drones) za kunyunyizia dawa mashambani, hatua inayolenga kurahisisha kazi kwa wakulima, kupunguza gharama na kuongeza tija katika uzalishaji.

“Tunataka kuona mkulima wa Tanzania anatumia teknolojia za kisasa ili kuongeza uzalishaji na kipato. Hii ndiyo dira yetu kama kampuni,” alisema Mulokozi.

Maadhimisho ya mwaka huu yamebeba kaulimbiu isemayo “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” ikisisitiza umuhimu wa ajira bora na mazingira rafiki ya kazi katika kufikia maendeleo ya muda mrefu ya taifa.

Ushindi wa Mati Super Brands Ltd katika maadhimisho hayo umeendelea kudhihirisha nafasi ya sekta binafsi katika kukuza uchumi, kuhamasisha ubunifu na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia ajira na maendeleo ya kilimo.
Posted by MROKI On Saturday, May 02, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo