Nafasi Ya Matangazo

May 14, 2026





Na Mwandishi wetu, 
Dodoma
Watumishi wapya 37 wa Tume ya Madini wametakiwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, uwajibikaji na uzalendo katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuimarisha usimamizi wa Sekta ya Madini na kuongeza mchango wake katika Pato la Taifa. Wito huo umetolewa wakati wa ufunguzi wa mafunzo elekezi kwa waajiriwa hao kabla ya kuripoti katika vituo vyao vya kazi mbalimbali nchini.

Akizungumza katika Ofisi za Tume ya Madini Makao Makuu jijini Dodoma, Meneja wa Utawala wa Tume ya Madini, Jacob Mnyenyelwa, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimaliwatu na Utawala, Nsajigwa Kabigi, amesema watumishi hao wanapaswa kuzingatia maadili ya kazi, weledi na uwazi wanapotoa huduma kwa wananchi na wadau wa sekta ya madini.

Amesema wananchi wana matarajio makubwa kutoka katika Sekta ya Madini, hivyo watumishi wapya wanapaswa kuwa mfano bora wa uadilifu, ubunifu na uzalendo ili kuhakikisha rasilimali madini zinasimamiwa kwa manufaa ya Taifa. 

Amesisitiza kuwa utendaji wenye maadili utaongeza imani ya wananchi na wawekezaji katika sekta hiyo muhimu ya uchumi.

Mafunzo hayo yamewashirikisha wahandisi, mafundi sanifu pamoja na afisa TEHAMA, yakilenga kuwajengea uwezo kuhusu majukumu yao, misingi ya utumishi wa umma, mawasiliano ya kikazi na taratibu za utendaji ndani ya Tume ya Madini kabla ya kuanza majukumu rasmi.

Tume ya Madini imeendelea kuimarisha rasilimaliwatu kwa kuajiri wataalam wenye ujuzi mbalimbali ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuongeza ufanisi wa usimamizi wa shughuli za utafiti, uchimbaji na biashara ya madini nchini, hatua inayotarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu ya Taifa.
Posted by MROKI On Thursday, May 14, 2026 No comments



Na Mwandishi Wetu, Shinyanga
Mkoa wa Shinyanga umeendelea kuimarisha nafasi yake kama kitovu muhimu cha sekta ya madini nchini, huku uchimbaji wa dhahabu na almasi ukitajwa kuwa nguzo kuu ya ukuaji wa uchumi wa mkoa huo na chanzo kipya cha fursa za uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani ya madini.

Akizungumza mkoani Shinyanga, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa huo, Mhandisi Noel Odera, amesema mkoa umebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi za madini zikiwemo dhahabu, almasi, madini ya ujenzi pamoja na madini ya viwandani kama chokaa, hali inayochochea shughuli za kiuchumi, ajira kwa wananchi na ongezeko la mapato ya Serikali.

Amesema shughuli za uchimbaji zinaendelea kwa kasi katika maeneo mbalimbali ya mkoa, zikihusisha wachimbaji wadogo, wa kati na migodi mikubwa, ikiwemo migodi ya El-Illari na Williamson Diamond iliyopo Wilaya ya Kishapu katika eneo la kimbaritiki linalozalisha sehemu kubwa ya almasi nchini.

Kwa mujibu wa Mhandisi Odera, utafiti mpya umeibua matumaini ya ongezeko la uzalishaji baada ya wachimbaji wadogo kugundua almasi katika eneo la Ng’wapangabule kwenye mwamba unaofanana na kimbaritiki, hatua inayofungua fursa mpya za uwekezaji na utafiti wa kina wa kijiolojia.

Ameeleza kuwa uzalishaji wa dhahabu unaendelea kuimarika katika maeneo ya Mwakitoryo, Nyandolwa, Mwanubi, Ishinabulandi na Mwazezema ambapo wachimbaji wadogo na wa kati wameendelea kuchangia ukuaji wa sekta hiyo kupitia ajira, kipato binafsi na mapato ya Serikali.

Mbali na uchimbaji, amesema Shinyanga ina mazingira rafiki kwa uwekezaji katika viwanda vya kisasa vya uchenjuaji wa dhahabu vinavyotumia teknolojia za Carbon in Pulp (CIP) na Carbon in Leach (CIL), vitakavyosaidia kuongeza thamani ya madini kabla ya kuuzwa na kuwapa wachimbaji huduma bora za uchenjuaji.

Aidha, amesema mkoa una fursa kubwa za uwekezaji katika viwanda vya utengenezaji wa bidhaa zitokanazo na almasi ikiwemo vito vya thamani na mapambo, hatua itakayoongeza thamani ya madini ndani ya nchi na kuimarisha uchumi wa viwanda.

Mhandisi Odera ameongeza kuwa uwepo wa malighafi za kutosha kama chokaa umeifanya Shinyanga kuwa eneo lenye uwezo mkubwa wa uwekezaji katika viwanda vya saruji, vitakavyosaidia kukuza sekta ya ujenzi, kuongeza ajira na kuimarisha maendeleo ya kijamii.

Amesema masoko ya madini yanaendelea kuimarika ambapo kwa sasa kuna wanunuzi wakubwa 19 wa dhahabu na almasi wanaofanya biashara mkoani humo, hali inayorahisisha biashara ya madini kwa wachimbaji na kuongeza uwazi wa biashara hiyo.

Amehitimisha kwa kuwahimiza wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kutumia fursa zilizopo Shinyanga kwa kuwekeza katika uchimbaji, utafiti wa madini na viwanda vya kuongeza thamani, akisisitiza kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki ili sekta ya madini ichangie zaidi maendeleo endelevu ya taifa na ustawi wa wananchi.
Posted by MROKI On Thursday, May 14, 2026 No comments

May 13, 2026

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Erica E. Yegella amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa fursa ya ajira mpya takriabani 259 katika kipindi cha mwezi Januari na Mei 2026.

Katika kipindi cha mwezi Januari, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ilifanikiwa kupangiwa ajira mpya takribani 111 kwenye kada tofauti tofauti ikiwemo elimu msingi na sekondari, afya, ujenzi, maendeleo ya jamii, utawala, na mawasiliano.

Mnamo mwezi Aprili 2026, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ilipangiwa ajira mpya 118 kwenye kada tofauti tofauti ikiwemo elimu msingi na sekondari, afya, ujenzi, na uhasibu.

Mwezi Mei, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ilipangiwa ajira mpya 30 mahususi kwa ajili ya watu wa kada ya afya pekee, wakataosaidia jitihada za utoaji huduma muhimu za afya katika zahanati na vituo vya afya vilijengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya.

Bi. Yegella amesema ajira mpya zilizotolewa kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kupitia Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, ni jambo ambalo anapaswa kupongezwa sana Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kukubali ombi la kuongeza watumishi katika Halmashauri.

"Katika kipindi cha miezi mitano pekee, Rais ameruhusu Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kupangiwa ajira mpya zaidi ya 250. Tunamshukuru sana kwa hili. Hii ni fursa kwa vijana wa kitanzania pamoja Halmashauri kwani itasaidia kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma muhimu za kijamii," ameeleza Bi. Yegella.
Posted by MROKI On Wednesday, May 13, 2026 No comments

May 11, 2026

Serikali kupitia Bohari ya Dawa (MSD) itaendelea kununua dawa zinazozalishwa na wawekezaji wa ndani ili kuimarisha uzalishaji wa ndani wa bidhaa za afya na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje ya nchi.

Hayo yamesemwa Waziri wa Afya, Mohammed Mchengerwa leo Mei 11 2026 akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 Bungeni, Jijini Dodoma.

“Serikali imejipanga kuhakikisha MSD inanunua kwanza dawa zinazozalishwa ndani ya nchi zilizokidhi viwango vya Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) kabla ya kwenda kununua kutoka nje ya nchi, hatua inalenga kukuza viwanda vya ndani, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi wa Taifa” amesema Waziri Mchengerwa

Amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi, ikiwemo kuboresha upatikanaji wa ardhi, miundombinu muhimu pamoja na kuratibu uwekezaji katika sekta ya dawa na bidhaa za afya ili kuvutia uwekezaji zaidi nchini.
Waziri Mchengerwa amesema Serikali imeendelea kuimarisha upatikanaji wa bidhaa za afya nchini kwa kutoa Shilingi trilioni 1.4 kupitia MSD ili kuhakikisha wananchi wanapata dawa na bidhaa muhimu za afya kwa wakati.

“Upatikanaji wa bidhaa muhimu za afya umeongezeka kutoka asilimia 58 mwaka 2021/22 hadi asilimia 88 mwezi Machi 2026” amesema Waziri Mchengerwa.

Amesema kuwa Wizara ya Afya itaendelea kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi pamoja na kuwawekea mazingira rafiki na wezeshi, ikiwemo upatikanaji wa ardhi na miundombinu muhimu, ili kuwavutia kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya bidhaa za afya na kupunguza utegemezi.

Waziri Mchengerwa amesisitiza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya, dawa salama na huduma zenye ubora bila kuachwa nyuma.
Posted by MROKI On Monday, May 11, 2026 No comments





Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), ameshiriki Mkutano wa Dharura wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Siasa, Ulinzi, na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC-MCO), uliofanyika  tarehe 10 Mei, 2026, Jijini Nairobi, Kenya.

Mkutano huo uliolenga kuimarisha misingi ya amani, umeongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. George Chaponda, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Jamhuri ya Malawi.

Katika mazungumzo hayo, Mawaziri wamejadili  changamoto mbalimbali za kiusalama zinazoikabili kanda hiyo ikiwemo  Vurugu zinazoendelea nchini Afrika Kusini dhidi ya raia wa nchi nyingine za Afrika.

Kwa Upande wake Mwenyekiti Dkt. Chaponda amewahakikishia wajumbe wa mkutano huo kuwa mapendekezo yote yaliyofikiwa yatafanyiwa kazi kwa haraka na kwa ufanisi. Hatua hii ni sehemu ya mikakati ya SADC kuhakikisha kuwa Kanda ya Kusini mwa Afrika inasalia kuwa kisiwa cha amani, utulivu, na ushirikiano wa kiuchumi.
Posted by MROKI On Monday, May 11, 2026 No comments

May 10, 2026


Na. Mwandishi Wetu, Ismani 
Wagombea 17 wameteuliwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kugombea ubunge Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa.

Uteuzi huo umefanywa kwa niaba ya Tume na Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Ismani, Ndugu. Caroline Angwen Otieno leo tarehe 10 Mei, 2026. 

Wagombea walioteuliwa na vyama vyao kwenye mabano ni Ndugu. Emmanuela Kaganda Mtatifikolo (CCM), Ndugu. Farida Issa Mwapungu (MAKINI), Ndugu. Asha Athumani Chuma (UPDP), Ndugu. Protas Shaibu Mgimbila (CCK), Ndugu. Fidelis Daud Mtikile (SAU), Ndugu. Hadija Husen Makawa (ADA-TADEA) Ndugu. Zavely Raurent Seleleka (UDP) na Ndugu. Subira Majuto Kalolo (NLD).

Wengine ni Ndugu. Bernard George Mwingira (DP), Ndugu. Burton Emilyo Chetenge (NCCR-Mageuzi), Ndugu. Mbalinga Christian Thomas (N.R.A), Ndugu. Mark Isdory Mhemela (AAFP), Ndugu.  Nassim Yahaya Upete (CUF), Ndugu. Mwaka Lameck Mgimwa (TLP), Ndugu. Asma Abdallah Othman (UMD), Ndugu. Maimuna Martin Lumato (ADC) na Ndugu. Daudi Issa Masasi (CHAUMMA). 

Akizungumza baada ya uteuzi huo, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo, Ndugu. Caroline Angwen Otieno amesema kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Tume, 

Kampeni kwa ajili ya uchaguzi mdogo wa Jimbo la Ismani pamoja na kata 12 za Tanzania Bara zitaanza kesho tarehe 11 hadi 31 Mei, 2026 na uchaguzi utafanyika siku ya Jumatatu tarehe 01 Juni, 2026.

Baada ya hatua hii ya uteuzi, kinachofuata ni kubandika fomu za uteuzi eneo la wazi kwa ajili ya kuwapa fursa ya kuweka pingamizi wale wanaoruhusiwa kuweka pingamizi kwa mujibu wa sheria. 

Baada ya saa 24 kupita na endapo hakutakuwa na pingamizi wagombea hao 17 wataendelea na kampeni kuanzia kesho tarehe 11 hadi 31 Mei, 2026 na uchaguzi utafanyika tarehe 01 Juni, 2026, amesema. 

Kata 12 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi mdogo wa Udiwani ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu. 

Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.


















Posted by MROKI On Sunday, May 10, 2026 No comments

May 09, 2026






Na Mwajdishi wetu, Geita,
Waziri wa Madini, *Mheshimiwa Anthony Mavunde (Mb)* atoa wito kwa benki zote nchini kuchangamkia fursa kwenye sekta ya madini kwa kubuni na kutengeneza bidhaa maalum ya kuwawezesha wachimbaji wadogo kuwa na mitaji itakayoongeza tija kwenye shughuli zao.

Ameyasema hayo leo tarehe 09 Mei, 2026  alipokuwa akizindua Tawi la Benki ya Exim Mkoani Geita.

"Ninamshukuru kwa dhati *Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan* kwa namna anavyoendelea kuisimamia sekta ya madini. Maono na maelekezo yake ndiyo yanaifanya sekta ya madini kukua kwa kasi na kupelekea mchango wake kwenye Pato la Taifa kufikia asilimia 10.1"

"Nitoe wito kwa benki zote nchini, kufikiria kuwa na bidhaa maalum kwa ajili ya kuwawezesha wachimbaji wadogo pasipo kuathiri masharti ya Sheria ya Fedha. Niwaombe mtoke ofisini na muende migodini, mkawatembelee wachimbaji na kujionea fursa kubwa iliyopo kwenye sekta ya madini nchini", alisisitiza Mhe. Mavunde.

Aidha, Mheshimiwa Mavunde aliipongeza Benki ya Exim kwa kufungua Tawi Geita na kusisitiza kwamba ni uamuzi sahihi kwani Mkoa wa Geita umeendelea kuwa kinara katika makusanyo ya maduhuli ya Serikali na biashara ya madini nchini.

Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde alibainisha kuwa Serikali  ina mpango wa kuwawezesha wachimbaji na wafanyabiashara wa madini nchini kupitia mfuko wa dhamana ili kuwaongezea nguvu ya ushiriki wa kikamilifu kwenye sekta ya madini.

"Ni matamanio ya Serikali kuona kiasi kikubwa cha mzunguko wa fedha kwenye biashara ya madini zinabaki nchini ili kukuza uchumi wetu" aliongeza mhe. Mavunde.

Awali, akieleza maelezo mafupi ya benki, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania, *Bw. Jaffar Matundu* alieleza kuwa benki ya Exim ina mkakati wa kuwezesha biashara, ambao unaendana na dira ya Serikali ya kuinua uchumi kupitia rasilimali madini, na kuongeza kuwa Exim ipo tayari kutoa suluhisho la changamoto ya mitaji kwa wachimbaji wadogo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Geita akimwakilisha Mkuu wa Mkoa, *Mheshimiwa Hashim Komba* alimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuweka mazingira wezeshi ambayo yamerahisisha ufanyaji wa biashara na kuvutia wawekezaji mkoani Geita.
Posted by MROKI On Saturday, May 09, 2026 No comments





Posted by MROKI On Saturday, May 09, 2026 No comments

May 07, 2026



Maafisa tawala na Rasilimali Watu nchini  wametakiwa kutekeleza wajibu wao na kuleta furaha kwa watumishi wa umma ili kwa upande mwengine nao wapeleke furaha na neema kwa Watanzania . 

Hayo yamesema na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Manejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete wakati akizungum,a katika mkutano wa maafisa hao jiji i Arusha.

Kikwete, ameyasema hayo kufuatia maamuzi mbalimbali yanayofanywa na serikali ya awamu ya sita katika kuhakikisha maslahi ya Watumishi wa umma nchini yanaboreka. 

Uamuzi wa hivi karibuni wa Serikali kupandisha madaraja watumishi 219,042 ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha utumishi wa umma nchini Tanzania. 

Hatua hii ambayo imepata ridhaa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na ongezeko la mishahara ya watumishi wa umma (2025): +35.1% , Ongezeko la kima cha chini sekta binafsi (2025/26): +33.4% , ambapo Sekta mbalimbali zinakwenda athiriwa na maboresho haya ikiwemo afya, elimu, kilimo, mawasiliano, usafirishaji, nishati, viwanda, biashara, hoteli, michezo, uvuvi, baharini, madini ,utamaduni n.k 

Matokeo haya kitakwimu zinaonyesha kasi ya mageuzi ya kiutumishi chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ambayo inaonyesha uongozi wa kimkakati unaoweka mbele ustawi wa watumishi na ufanisi wa taasisi za umma.
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
 
Serikali imeendelea kuongeza fursa za elimu nchini kwa kusajili shule 671 zikiwemo shule 23 za awali, shule 401 za awali na msingi, shule 245 za sekondari pamoja na vyuo viwili vya ualimu katika jitihada za kuboresha upatikanaji wa elimu kwa watoto na vijana nchini.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Prof. Mkenda amesema Serikali imeendelea kuwezesha ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya elimu ikiwemo mabweni sita katika shule za sekondari, madarasa 128, bwalo la chakula, nyumba ya mwalimu pamoja na ukarabati wa shule mbili za sekondari ili kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani.

Aidha, amesema Serikali imeimarisha uthibiti ubora wa elimu kwa kufanya tathmini ya jumla katika asasi 8,067 zikiwemo shule za awali, msingi, sekondari, vyuo vya ualimu, vituo vya elimu nje ya mfumo rasmi pamoja na Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi.

Ameeleza kuwa asasi zilizobainika kuwa na changamoto mbalimbali zilipewa ushauri wa kitaalamu ili kuboresha utoaji wa elimu.

Katika kuhakikisha upatikanaji wa vitabu vya kiada unaimarika, Waziri huyo amesema Serikali imechapa na kusambaza nakala 4,845,490 za vitabu vya darasa la tano pamoja na nakala 6,887,325 za vitabu na viongozi vya walimu kwa wanafunzi wa kidato cha pili.

Kwa mujibu wa Prof. Mkenda, kwa masomo ya sanaa uwiano wa vitabu ni kitabu kimoja kwa wanafunzi watatu huku masomo ya sayansi yakifikia uwiano wa kitabu kimoja kwa mwanafunzi mmoja.

Vilevile, Serikali imechapa na kusambaza nakala 3,000 za vitabu vya darasa la tano na nakala 31,520 za vitabu vya kidato cha pili kwa wanafunzi wenye uoni hafifu kwa uwiano wa kitabu kimoja kwa mwanafunzi mmoja.

Kwa upande wa wanafunzi wasioona, amesema Serikali imechapisha na kusambaza nakala 9,600 za vitabu vya maandishi ya Breili kwa darasa la tano pamoja na nakala 8,362 za vitabu vya Breili kwa wanafunzi wa kidato cha pili ili kuhakikisha wanafunzi wenye mahitaji maalum wanapata haki sawa ya elimu. SOURCE: OKULY BLOG
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo