Nafasi Ya Matangazo

May 11, 2026






Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), ameshiriki Mkutano wa Dharura wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Siasa, Ulinzi, na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC-MCO), uliofanyika  tarehe 10 Mei, 2026, Jijini Nairobi, Kenya.

Mkutano huo uliolenga kuimarisha misingi ya amani, umeongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. George Chaponda, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Jamhuri ya Malawi.

Katika mazungumzo hayo, Mawaziri wamejadili  changamoto mbalimbali za kiusalama zinazoikabili kanda hiyo ikiwemo  Vurugu zinazoendelea nchini Afrika Kusini dhidi ya raia wa nchi nyingine za Afrika.

Kwa Upande wake Mwenyekiti Dkt. Chaponda amewahakikishia wajumbe wa mkutano huo kuwa mapendekezo yote yaliyofikiwa yatafanyiwa kazi kwa haraka na kwa ufanisi. Hatua hii ni sehemu ya mikakati ya SADC kuhakikisha kuwa Kanda ya Kusini mwa Afrika inasalia kuwa kisiwa cha amani, utulivu, na ushirikiano wa kiuchumi.
Posted by MROKI On Monday, May 11, 2026 No comments

May 10, 2026


Na. Mwandishi Wetu, Ismani 
Wagombea 17 wameteuliwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kugombea ubunge Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa.

Uteuzi huo umefanywa kwa niaba ya Tume na Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Ismani, Ndugu. Caroline Angwen Otieno leo tarehe 10 Mei, 2026. 

Wagombea walioteuliwa na vyama vyao kwenye mabano ni Ndugu. Emmanuela Kaganda Mtatifikolo (CCM), Ndugu. Farida Issa Mwapungu (MAKINI), Ndugu. Asha Athumani Chuma (UPDP), Ndugu. Protas Shaibu Mgimbila (CCK), Ndugu. Fidelis Daud Mtikile (SAU), Ndugu. Hadija Husen Makawa (ADA-TADEA) Ndugu. Zavely Raurent Seleleka (UDP) na Ndugu. Subira Majuto Kalolo (NLD).

Wengine ni Ndugu. Bernard George Mwingira (DP), Ndugu. Burton Emilyo Chetenge (NCCR-Mageuzi), Ndugu. Mbalinga Christian Thomas (N.R.A), Ndugu. Mark Isdory Mhemela (AAFP), Ndugu.  Nassim Yahaya Upete (CUF), Ndugu. Mwaka Lameck Mgimwa (TLP), Ndugu. Asma Abdallah Othman (UMD), Ndugu. Maimuna Martin Lumato (ADC) na Ndugu. Daudi Issa Masasi (CHAUMMA). 

Akizungumza baada ya uteuzi huo, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo, Ndugu. Caroline Angwen Otieno amesema kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Tume, 

Kampeni kwa ajili ya uchaguzi mdogo wa Jimbo la Ismani pamoja na kata 12 za Tanzania Bara zitaanza kesho tarehe 11 hadi 31 Mei, 2026 na uchaguzi utafanyika siku ya Jumatatu tarehe 01 Juni, 2026.

Baada ya hatua hii ya uteuzi, kinachofuata ni kubandika fomu za uteuzi eneo la wazi kwa ajili ya kuwapa fursa ya kuweka pingamizi wale wanaoruhusiwa kuweka pingamizi kwa mujibu wa sheria. 

Baada ya saa 24 kupita na endapo hakutakuwa na pingamizi wagombea hao 17 wataendelea na kampeni kuanzia kesho tarehe 11 hadi 31 Mei, 2026 na uchaguzi utafanyika tarehe 01 Juni, 2026, amesema. 

Kata 12 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi mdogo wa Udiwani ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu. 

Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.


















Posted by MROKI On Sunday, May 10, 2026 No comments

May 09, 2026






Na Mwajdishi wetu, Geita,
Waziri wa Madini, *Mheshimiwa Anthony Mavunde (Mb)* atoa wito kwa benki zote nchini kuchangamkia fursa kwenye sekta ya madini kwa kubuni na kutengeneza bidhaa maalum ya kuwawezesha wachimbaji wadogo kuwa na mitaji itakayoongeza tija kwenye shughuli zao.

Ameyasema hayo leo tarehe 09 Mei, 2026  alipokuwa akizindua Tawi la Benki ya Exim Mkoani Geita.

"Ninamshukuru kwa dhati *Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan* kwa namna anavyoendelea kuisimamia sekta ya madini. Maono na maelekezo yake ndiyo yanaifanya sekta ya madini kukua kwa kasi na kupelekea mchango wake kwenye Pato la Taifa kufikia asilimia 10.1"

"Nitoe wito kwa benki zote nchini, kufikiria kuwa na bidhaa maalum kwa ajili ya kuwawezesha wachimbaji wadogo pasipo kuathiri masharti ya Sheria ya Fedha. Niwaombe mtoke ofisini na muende migodini, mkawatembelee wachimbaji na kujionea fursa kubwa iliyopo kwenye sekta ya madini nchini", alisisitiza Mhe. Mavunde.

Aidha, Mheshimiwa Mavunde aliipongeza Benki ya Exim kwa kufungua Tawi Geita na kusisitiza kwamba ni uamuzi sahihi kwani Mkoa wa Geita umeendelea kuwa kinara katika makusanyo ya maduhuli ya Serikali na biashara ya madini nchini.

Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde alibainisha kuwa Serikali  ina mpango wa kuwawezesha wachimbaji na wafanyabiashara wa madini nchini kupitia mfuko wa dhamana ili kuwaongezea nguvu ya ushiriki wa kikamilifu kwenye sekta ya madini.

"Ni matamanio ya Serikali kuona kiasi kikubwa cha mzunguko wa fedha kwenye biashara ya madini zinabaki nchini ili kukuza uchumi wetu" aliongeza mhe. Mavunde.

Awali, akieleza maelezo mafupi ya benki, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania, *Bw. Jaffar Matundu* alieleza kuwa benki ya Exim ina mkakati wa kuwezesha biashara, ambao unaendana na dira ya Serikali ya kuinua uchumi kupitia rasilimali madini, na kuongeza kuwa Exim ipo tayari kutoa suluhisho la changamoto ya mitaji kwa wachimbaji wadogo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Geita akimwakilisha Mkuu wa Mkoa, *Mheshimiwa Hashim Komba* alimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuweka mazingira wezeshi ambayo yamerahisisha ufanyaji wa biashara na kuvutia wawekezaji mkoani Geita.
Posted by MROKI On Saturday, May 09, 2026 No comments





Posted by MROKI On Saturday, May 09, 2026 No comments

May 07, 2026



Maafisa tawala na Rasilimali Watu nchini  wametakiwa kutekeleza wajibu wao na kuleta furaha kwa watumishi wa umma ili kwa upande mwengine nao wapeleke furaha na neema kwa Watanzania . 

Hayo yamesema na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Manejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete wakati akizungum,a katika mkutano wa maafisa hao jiji i Arusha.

Kikwete, ameyasema hayo kufuatia maamuzi mbalimbali yanayofanywa na serikali ya awamu ya sita katika kuhakikisha maslahi ya Watumishi wa umma nchini yanaboreka. 

Uamuzi wa hivi karibuni wa Serikali kupandisha madaraja watumishi 219,042 ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha utumishi wa umma nchini Tanzania. 

Hatua hii ambayo imepata ridhaa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na ongezeko la mishahara ya watumishi wa umma (2025): +35.1% , Ongezeko la kima cha chini sekta binafsi (2025/26): +33.4% , ambapo Sekta mbalimbali zinakwenda athiriwa na maboresho haya ikiwemo afya, elimu, kilimo, mawasiliano, usafirishaji, nishati, viwanda, biashara, hoteli, michezo, uvuvi, baharini, madini ,utamaduni n.k 

Matokeo haya kitakwimu zinaonyesha kasi ya mageuzi ya kiutumishi chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ambayo inaonyesha uongozi wa kimkakati unaoweka mbele ustawi wa watumishi na ufanisi wa taasisi za umma.
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
 
Serikali imeendelea kuongeza fursa za elimu nchini kwa kusajili shule 671 zikiwemo shule 23 za awali, shule 401 za awali na msingi, shule 245 za sekondari pamoja na vyuo viwili vya ualimu katika jitihada za kuboresha upatikanaji wa elimu kwa watoto na vijana nchini.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Prof. Mkenda amesema Serikali imeendelea kuwezesha ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya elimu ikiwemo mabweni sita katika shule za sekondari, madarasa 128, bwalo la chakula, nyumba ya mwalimu pamoja na ukarabati wa shule mbili za sekondari ili kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani.

Aidha, amesema Serikali imeimarisha uthibiti ubora wa elimu kwa kufanya tathmini ya jumla katika asasi 8,067 zikiwemo shule za awali, msingi, sekondari, vyuo vya ualimu, vituo vya elimu nje ya mfumo rasmi pamoja na Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi.

Ameeleza kuwa asasi zilizobainika kuwa na changamoto mbalimbali zilipewa ushauri wa kitaalamu ili kuboresha utoaji wa elimu.

Katika kuhakikisha upatikanaji wa vitabu vya kiada unaimarika, Waziri huyo amesema Serikali imechapa na kusambaza nakala 4,845,490 za vitabu vya darasa la tano pamoja na nakala 6,887,325 za vitabu na viongozi vya walimu kwa wanafunzi wa kidato cha pili.

Kwa mujibu wa Prof. Mkenda, kwa masomo ya sanaa uwiano wa vitabu ni kitabu kimoja kwa wanafunzi watatu huku masomo ya sayansi yakifikia uwiano wa kitabu kimoja kwa mwanafunzi mmoja.

Vilevile, Serikali imechapa na kusambaza nakala 3,000 za vitabu vya darasa la tano na nakala 31,520 za vitabu vya kidato cha pili kwa wanafunzi wenye uoni hafifu kwa uwiano wa kitabu kimoja kwa mwanafunzi mmoja.

Kwa upande wa wanafunzi wasioona, amesema Serikali imechapisha na kusambaza nakala 9,600 za vitabu vya maandishi ya Breili kwa darasa la tano pamoja na nakala 8,362 za vitabu vya Breili kwa wanafunzi wa kidato cha pili ili kuhakikisha wanafunzi wenye mahitaji maalum wanapata haki sawa ya elimu. SOURCE: OKULY BLOG
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
Serikali imeendelea kuweka mikakati madhubuti ya kukuza ubunifu, utafiti na matumizi salama ya teknolojia ya kisasa ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.

Hatua hiyo inalenga kuongeza uwezo wa wananchi, taasisi za elimu pamoja na sekta mbalimbali kutumia teknolojia kwa tija na usalama zaidi.

Hayo yamebainishwa leo Mei 7,2026 bungeni Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Katika juhudi za kukuza ubunifu, Serikali itaendeleza Mfuko wa Kibiashara wa Ubunifu  kwa lengo la kusaidia mawazo ya wabunifu na tafiti zenye manufaa kuingia kwenye matumizi ya kibiashara. Kupitia mpango huo, vyuo vitano vya Maendeleo ya Wananchi vitawezeshwa kuanzisha vituo vya ubunifu vitakavyotoa nafasi kwa vijana na wabunifu kukuza teknolojia, ujasiriamali na ajira.

“Serikali imejipanga kuimarisha uthibiti na utafiti wa kimkakati katika matumizi ya teknolojia ya nyuklia ili kuhakikisha usalama wa wananchi pamoja na mazingira. Mkakati huo unalenga kuongeza matumizi salama ya teknolojia hiyo katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii ikiwemo afya, kilimo na viwanda.”amesema Prof.Mkenda.

Katika mwaka ujao wa utekelezaji, Serikali itaendelea kudhibiti matumizi ya mionzi nchini kwa kufanya ukaguzi katika vituo 900 vyenye vyanzo vya mionzi. Ukaguzi huo unalenga kuhakikisha usalama wa wagonjwa, wafanyakazi, jamii pamoja na mazingira dhidi ya athari zinazoweza kusababishwa na matumizi yasiyo salama ya mionzi.

Vilevile, Serikali itapima na kudhibiti viwango vya mionzi kwa wafanyakazi 2,110 wanaofanya kazi kwenye mazingira yenye vyanzo vya mionzi ili kuhakikisha afya zao zinalindwa na viwango vya usalama vinafuatwa wakati wote.

Hatua hizi zinaonesha dhamira ya Serikali ya kuendelea kuwekeza katika sayansi, teknolojia na ubunifu kama nyenzo muhimu ya kuharakisha maendeleo ya taifa na kuboresha maisha ya wananchi. SOURCE : Mzalendo Blog
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
 
Zaidi ya wanafunzi 3,021,177 wanatarajiwa kujiunga na elimu ya sekondari kidato cha kwanza ifikapo Januari 2028, kufuatia utekelezaji wa sera ya elimu ya lazima ya miaka 10 inayotekelezwa na Serikali kupitia Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Toleo la 2023.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Prof. Mkenda amesema idadi hiyo ya wanafunzi inatokana na wanafunzi waliopo darasa la tano na la sita mwaka 2026 ambao wanatarajiwa kuhitimu elimu ya msingi mwaka 2027 na kuanza sekondari mwaka 2028.

Amesema Serikali kupitia Ofisi ya Rais – TAMISEMI imeendelea na ujenzi wa miundombinu mbalimbali ikiwemo madarasa, maabara, karakana pamoja na ununuzi wa vifaa na kuajiri walimu wapya ili kuhakikisha wanafunzi hao wanapokelewa kwa wakati.

Aidha, amesema utekelezaji wa elimu ya lazima ya miaka 10 ni hatua ya kihistoria itakayoongeza upatikanaji wa elimu ya sekondari na kusaidia kuandaa vijana wenye ujuzi na maarifa yanayokidhi mahitaji ya maendeleo ya taifa na ajira.

Amefafanua kuwa chini ya mfumo mpya wa elimu, mtoto atamaliza elimu ya lazima akiwa na umri wa miaka 16 tofauti na mfumo wa awali ambapo mwanafunzi alimaliza darasa la saba akiwa na miaka 13, umri ambao hauwezi kumwezesha kuajiriwa au kujiajiri.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, Serikali pia imeendelea na maandalizi ya kuanzisha mkondo wa amali katika shule za sekondari ili kuwajengea wanafunzi ujuzi wa kujitegemea na kukabiliana na changamoto za ajira.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali inaendelea na mapitio ya Sheria ya Elimu Sura ya 353 ambapo tayari maoni ya wadau mbalimbali yamekusanywa na taarifa ya awali ya mapitio hayo imeandaliwa.

Sambamba na hilo, Serikali imeandaa viunzi mbalimbali vya kuimarisha sekta ya elimu ikiwemo Kiunzi cha Umahiri wa Walimu katika TEHAMA 2026 pamoja na Kiunzi cha Kitaifa cha Ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa teknolojia za kidijitali katika sekta ya elimu. Source: OKULY BLOG 

Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini unaendelea kuwa wa uhakika na bidhaa hiyo haiadimiki.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Janeth Mahawanga Bungeni jijini Dodoma, aliyetaka kujua hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kukabiliana na athari za migogoro ya kimataifa na kidunia zilizopelekea changamoto ya mafuta nchini.

“Hatua ya kwanza ambayo Serikali imechukua ni kuhakikisha bidhaa hii haiadimiki. Zipo nchi ambazo tayari matatizo yameshajitokeza ya bidhaa hiyo kuadimika, hata kama una fedha hupati mafuta,” amesema Dkt. Nchemba.

Waziri Mkuu amesema Serikali imeanza taratibu za kuweka ruzuku ili kupunguza makali ya athari zinazotokana na hali inayoendelea Mashariki ya Kati.

Aidha, amesema Serikali imekaa na kuwasikiliza wadau mbalimbali, wakiwemo wadau wa usafirishaji, kwa lengo la kujadiliana namna ya kudhibiti ongezeko la gharama za usafirishaji.

“Tulikubaliana na wasafirishaji kupunguza baadhi ya gharama zinazotokana na hatua zinazochukuliwa na Serikali ambazo kimsingi si za lazima. Mfano, ulikuwepo uratibu wa mabasi yote ya mikoani kupita kila stendi, tumesema hakuna ulazima wa basi kupita kila stendi,” amesema Waziri Mkuu.
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kusimamia sera, sheria na miongozo inayohusu afya na lishe ili kuhakikisha elimu inayotolewa kwa wananchi inalinda usalama wa afya za Watanzania.
 
Amesema hayo leo Alhamisi, Mei 7, 2026, wakati akijibu swali la Mbunge wa Hai, Mhe. Saashisha Mafuwe, katika kipindi cha Maswali kwa Waziri Mkuu Bungeni jijini Dodoma. Mbunge huyo alitaka kujua mpango wa Serikali wa kuweka utaratibu maalumu wa utoaji elimu ya lishe kwa watu wenye taaluma husika.
 
Akijibu swali hilo, Dkt. Mwigulu alisema Serikali itaendelea kuhakikisha elimu ya afya na lishe inayotolewa kwa wananchi inazingatia taaluma, ushahidi wa kitaalamu na usalama wa afya.
 
“Serikali itaendelea kusimamia miongozo iliyopo ili taarifa au elimu inayotolewa na wenye taaluma ya lishe iwe ya kweli na imethibitishwa kutokuwa na madhara kwa kile kinachoshauriwa,” alisema.
 
Aidha, Waziri Mkuu aliielekeza Wizara ya Afya pamoja na mabaraza yanayosimamia taaluma za afya kuendelea kufanya tathmini kuhusu uratibu wa leseni na vibali kwa watoa elimu ya afya na lishe nchini.
 
Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu alisema Serikali inaendelea kufuatilia athari za migogoro ya kimataifa katika sekta mbalimbali za uchumi, hususan upatikanaji na bei ya mafuta.
 
Amesema hayo alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Janeth Mahawanga, aliyetaka kujua hatua zinazochukuliwa na Serikali kukabiliana na athari za migogoro ya kimataifa zinazoathiri upatikanaji wa mafuta nchini.
 
Waziri Mkuu alisema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha bidhaa ya mafuta haipungui nchini na kupunguza athari za kupanda kwa gharama kwa wananchi.
 
“Mheshimiwa Spika, tayari kuna taratibu za namna ya kutekeleza zoezi hilo la ruzuku, ambapo zimekuwepo njia nyingi zinazotumika kwa ajili ya kuhakikisha tunapunguza makali ya madhara yanayotokana na kile kinachoendelea kule Mashariki ya Kati,” alisema.
 
Alisema Serikali pia imeendelea kushirikiana na wadau wa usafirishaji ili kudhibiti ongezeko la gharama za usafiri na usafirishaji.
 
“Tulizungumza na wadau wa usafirishaji na tukakubaliana kupunguza baadhi ya gharama walizokuwa wanazibeba. Kwa mfano, tulisema hakuna ulazima wa kila basi kupita kila stendi kama halina abiria wa kushusha,” alisema.
 
Aidha, alisema Serikali imepunguza baadhi ya taratibu za mizani kwa mabasi na magari ya usafirishaji ili kupunguza gharama za uendeshaji.
 
“Hata yale yanayotakiwa kupima uzito, tumepunguza vituo vya kupita kupima. Watapita kwenye mizani ya kwanza na ya mwisho kabla hawajamaliza safari,” alisema.
 
Alisema hatua hizo ni sehemu ya ruzuku zisizo za moja kwa moja zinazolenga kupunguza gharama ambazo zingebebwa na wananchi.
 
“Hizi ni njia mbalimbali za utoaji wa ruzuku zisizo za moja kwa moja ili kupunguza gharama ambazo zingebebwa na mwananchi,” alisema.
 
Waziri Mkuu alisema Serikali itaendelea kufuatilia mwenendo wa uchumi wa dunia na kuchukua hatua stahiki kuhakikisha huduma muhimu zinapatikana kwa wakati na kwa gharama nafuu kwa wananchi.
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (Kulia), akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule, katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.
Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule, akizungumza wakati akimkaribisha Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (hayupo pichani), kuhutubia kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.A
Mwenyekiti wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Taifa, Bw. Ernest Mtondo, akizungumza wakati wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.

Baadhi ya wafanyabiashara wadogo maarufu kama wamachinga wa Soko la Mwenge, wakisikiliza hotuba ya Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (hayupo pichani), wakati wa  Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ambao ulilenga pia kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.

Na. Joseph Mahumi, WF, Dar es Salaam
Serikali imewahakikishia wafanyabiashara wadogo maarufu kama wamachinga kuendelea kuboresha mazingira yao ya kufanyia biashara, ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kukuza uchumi jumuishi na kuongeza fursa za ajira nchini.

Ahadi hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akihutubia katika Mkutano Mkuu wa Baraza la Machinga uliofanyika katika Viwanja vya Mwenge, Kinondoni jijini Dar es Salaam, uliolenga kujadili mafanikio ya wamachinga katika siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania madarakani pamoja na kuweka mikakati ya kulijenga Taifa.

Mhe. Mhandisi Munde alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara wadogo ili waweze kukuza mitaji yao na hatimaye kupanda daraja na kuwa wafanyabiashara wakubwa.

“Tunataka kuwaona mnapiga hatua kutoka biashara ndogondogo hadi kuwa wawekezaji wakubwa na Serikali yenu inatambua mchango wenu katika uchumi na itaendelea kuwaunga mkono,” alisema Mhe. Mhandisi Munde.

Aidha Mhe. Mhandisi Munde, alisisitiza kuwa maoni na mapendekezo yatokanayo na mkutano huo yatasaidia kuboresha sera na mifumo ya biashara nchini, sambamba na utekelezaji wa falsafa ya 4Rs (Maridhiano, Ustahimilivu, Mabadiliko na Kujenga upya) inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita.

Aliongeza kuwa Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa kurasimisha sekta isiyo rasmi, hatua itakayowezesha wafanyabiashara kupata fursa zaidi za mikopo nafuu, mafunzo na huduma nyingine muhimu za kiuchumi ikiwemo maeneo mazuri zaidi ya kufanya biashara kwa utulivu.

“Ni muhimu mkakubali kufanya kazi katika maeneo mtakayotengewa ili kurahisisha Serikali yenu kuwekeza miundombinu na huduma muhimu katika maeneo hayo na Pia, taasisi kama TRA na benki zitaendelea kuboresha huduma zao ili ziwe rafiki kwa wafanyabiashara wadogo,” alisisitiza Mhe. Mhandisi Munde.

Aidha Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule, pongezi za dhati kwa Wizara ya Fedha pamoja na taasisi zake kwa ushirikiano mkubwa wanaoendelea kuutoa kwa wafanyabiashara wadogo, ikiwemo juhudi za Mamlaka ya Mapato Tanzania -TRA katika kuonyesha uwajibikaji na mafanikio makubwa ya ukusanyaji mapato.

“Kwa dhati nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa maono na jitihada zake za kufungua fursa za kiuchumi na kuimarisha miundombinu ya biashara, ikiwemo ujenzi wa masoko na maboresho ya maeneo ya biashara katika Wilaya ya Kinondoni, hasa kwa kutupa masoko zaidi ya 24 yakiwemo makubwa kama Tandale, na kuendelea kuboresha masoko mengine na kuongeza vibanda ili kuwawezesha wafanyabiashara wengi zaidi kufanya shughuli zao katika mazingira bora na salama” alisema Bw. Mtambule

Naye Mwenyekiti wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Taifa, Bw. Ernest Mtondo alisema kuwa, Wamachinga wanatambua na wanathamini juhudi za Serikali katika kuboresha mazingira ya biashara, pamoja na jitihada za kuimarisha zaidi mifumo ya hifadhi ya jamii kwa wajasiriamali hao.

Bw. Mtondo aliishukuru Wizara ya Fedha kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa kuanza kuweka mazingira rafiki ya biashara, ikiwemo ujenzi wa mahema katika maeneo maalum ambayo yatabeba zaidi ya wamachinga 300, hatua ambayo imeanza kuleta utulivu na heshima kwa shughuli za wamachinga.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Taifa, Bw. Joseph Mwanakijiji, amesema kuwa kuanzishwa kwa shirikisho hilo kumelenga kuwaunganisha wamachinga na wafanyabiashara ndogondogo nchini kote, huku likikuza ushirikiano thabiti kati yao na Serikali.

Bw. Mwanakijiji alisema kuwa kupitia SHIUMA, wamachinga wameanza kunufaika na fursa mbalimbali za kiuchumi ikiwemo upatikanaji wa mikopo kutoka taasisi za kifedha, pamoja na kupendekeza na kurasimisha maeneo rafiki ya biashara.

“Tayari kumekuwepo na maboresho makubwa ikiwemo ujenzi wa masoko maalum kama Machinga Complex Dodoma, kuimarika kwa mahusiano na Serikali, pamoja na kuboreshwa kwa mazingira ya biashara katika maeneo mbalimbali kama Mwenge na tunaahidi kuongeza ushirikiano na TRA katika ukusanyaji wa mapato pamoja na kuwahamasisha zaidi wamachinga kujiunga na mifuko ya hifadhi ya jamii kama NSSF ili kujenga ustawi wao wa baadaye” alisema Bw. Mwanakijiji.
Posted by MROKI On Thursday, May 07, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo