Nafasi Ya Matangazo

March 30, 2026




Na Mwandishi Wetu, Mwanza
Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba, amewataka watendaji wa Tume ya Madini hususan Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kuimarisha usimamizi wa mazingira katika shughuli za uchimbaji madini kwa kufanya kaguzi za mara kwa mara, hasa katika kipindi hiki cha msimu wa mvua, ili kuzuia ajali zinazoweza kusababisha madhara makubwa ikiwemo vifo.



Mhandisi Samamba ametoa wito huo wakati akifungua Kikao cha Pili cha Baraza la Pili la Wafanyakazi wa Tume ya Madini kilichofanyika jijini Mwanza, kilichowakutanisha viongozi mbalimbali wakiwemo Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo, Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, viongozi kutoka Wizara ya Madini, Ofisi ya Kamishna wa Kazi,  TUGHE pamoja na wakurugenzi, mameneja na wawakilishi wa Ofisi za Maafisa Madini Wakazi kutoka mikoa mbalimbali nchini.

Amesisitiza kuwa usalama wa wachimbaji unapaswa kuwa kipaumbele cha kwanza kwa watendaji wote wa sekta ya madini, akieleza kuwa uhai wa mchimbaji mmoja una thamani kubwa kwa Taifa.

“Ni wajibu wenu kuhakikisha maeneo yote ya uchimbaji yanakaguliwa mara kwa mara na migodi yenye vihatarishi vya ajali inafungwa mara moja, lengo likiwa ni kuhakikisha Watanzania wananufaika na rasilimali za madini bila kuhatarisha maisha yao,” amesema Mhandisi Samamba.

Katika hatua nyingine, amewataka watendaji wa Tume ya Madini kuongeza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya madini kuanzia uchimbaji, uchenjuaji hadi biashara ya madini, hatua itakayosaidia kuongeza uwazi, kudhibiti mianya ya rushwa na kuhakikisha Serikali inapata mapato stahiki.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuzingatia maadili na uadilifu kazini ili kuendelea kujenga taswira chanya ya Tume ya Madini mbele ya wananchi na wadau wa sekta hiyo.

Akizungumzia mafanikio ya ukusanyaji wa maduhuli, Mhandisi Samamba ameipongeza Tume ya Madini kwa kuvuka malengo ya makusanyo ambapo kuanzia Julai 2025 hadi Machi 24, 2026 imekusanya zaidi ya shilingi trilioni moja, sawa na zaidi ya asilimia 111 ya lengo la kipindi husika.

Ameeleza kuwa kasi hiyo inaipa Tume matumaini ya kuvuka lengo la kukusanya shilingi trilioni 1.2 ifikapo Juni mwaka huu katika kipindi cha mwaka wa fedha 2025/2026, fedha zitakazochochea maendeleo ya huduma za jamii ikiwemo umeme, maji, barabara, shule na sekta nyingine muhimu kwa wananchi.

Ameongeza kuwa kumekuwepo na ongezeko la uzalishaji wa madini ya dhahabu kutoka tani 54.06 zenye thamani ya shilingi trilioni 7.004 katika kipindi cha  mwaka wa fedha 2022/2023 hadi tani 66.88 zenye thamani ya shilingi trilioni 12.265 katika kipindi cha mwaka wa fedha 2024/2025 na kusisitiza kuwa katika kipindi cha mwezi Julai 2025 hadi Februari 2026 jumla ya tani 46.24 zenye thamani ya shilingi trilioni 11.726 zilizalishwa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo, amesema mafanikio ya Tume yanaonekana wazi kupitia ongezeko la makusanyo ya maduhuli kutoka shilingi bilioni 360 mwaka wa fedha 2017/2018 hadi kufikia shilingi trilioni 1.072 mwaka 2024/2025, hali inayoonesha mchango mkubwa wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Naye Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, ameishukuru Wizara ya Madini kwa kuendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi kupitia uboreshaji wa maslahi pamoja na kuongeza vitendea kazi ikiwemo magari na kompyuta zilizogawiwa katika Ofisi za Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa ili kuongeza ufanisi wa utendaji kazi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mwakilishi wa Kamishna wa Kazi, Betty Mtega pamoja na Katibu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Mkoa wa Dodoma, Samwel Nyungwa, wameipongeza Tume ya Madini kwa kuimarisha utaratibu wa vikao vya Baraza la Wafanyakazi vinavyotoa fursa kwa watumishi kushiriki kikamilifu kutoa maoni ya maboresho ya rasimu ya bajeti kabla ya kuwasilishwa rasmi.






Posted by MROKI On Monday, March 30, 2026 No comments


Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema makaa ya mawe yana nafasi ya kimkakati katika kuharakisha mageuzi ya uchumi wa Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda, akibainisha kuwa rasilimali hiyo si tu chanzo cha nishati bali pia ni mhimili wa kuongeza thamani ya madini na malighafi nyingine za viwandani. 

Amesema kupitia matumizi sahihi ya makaa ya mawe, nchi inaweza kupunguza utegemezi wa bidhaa za nje, kuongeza uzalishaji wa ndani na kuimarisha mnyororo wa thamani katika sekta mbalimbali ikiwemo  nishati, viwanda na madini.


Akizungumza leo Machi 30, 2026 katika kikao na wadau wa makaa ya mawe kilichofanyika katika Ukumbi wa Tume ya Madini, Jijini Dodoma, Mhe. Mavunde amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kusikiliza na kutatua changamoto za wadau ili kuhakikisha sekta hiyo inakua kwa kasi na ufanisi zaidi.

“Makaa ya mawe ni mhimili muhimu katika maendeleo ya viwanda. Tunahitaji kuongeza uzalishaji na kuhakikisha matumizi yake yanaongeza thamani ndani ya nchi,” ameeleza Mhe. Mavunde

lKatika kikao hicho, Waziri Mavunde amepokea changamoto mbalimbali kutoka kwa wachimbaji na wafanyabiashara, ikiwemo gharama za uzalishaji, usafirishaji na upatikanaji wa masoko na kuahidi kuwa Serikali itazifanyia kazi ili kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.

Aidha, amesisitiza kuwa upangaji wa bei elekezi utafanyika kwa ushirikishwaji wa wadau wote ili kulinda maslahi ya sekta.

Wadau wa makaa ya mawe wameipongeza hatua hio ya Waziri Mavunde na kueleza kuwa Serikali kwa kuwashirikisha katika majadiliano, wakieleza kuwa hatua hiyo imeongeza imani na uwazi katika uendeshaji wa sekta hiyo huku wakiahidi kuongeza uzalishaji wa makaa ya mawe ili kukidhi mahitaji ya ndani na kuongeza mapato ya Taifa kupitia Sekta ya Madini.

Katika kuimarisha uratibu na mshikamano wa sekta, Mhe. Mavunde amewahimiza wadau wa makaa ya mawe kuanzisha chama chao (association) kitakachowaunganisha ili kurahisisha shughuli zao na kushughulikia changamoto kwa pamoja kwa ufanisi zaidi.

Katika hatua ya kuimarisha viwanda vya ndani, Waziri Mavunde amesema kuwa Kampuni ya A1 Steels Tanzania LTD imepanga kujenga Kiwanda cha kuzalisha chuma jijini Dodoma na kwamba kiwanda hicho kinatarajiwa kutumia takribani tani 20,000 za makaa ya mawe kwa mwaka, hatua inayotarajiwa kuongeza mahitaji ya rasilimali hiyo na kufungua fursa zaidi za uzalishaji kwa wachimbaji wa ndani
Mradi huo unatarajiwa kuchochea ajira, kuongeza thamani ya madini na kuimarisha mchango wa sekta ya viwanda katika uchumi wa Taifa.

Kikao hicho kimeonesha dhamira ya Serikali ya kuifanya Sekta ndogo ya makaa ya mawe kuwa injini ya maendeleo ya viwanda nchini, huku ushirikiano kati ya Serikali na wadau ukiendelea kuwa nguzo muhimu ya mafanikio ya sekta hiyo. 






Posted by MROKI On Monday, March 30, 2026 No comments
Na Joseph Mahumi, WF
Kampuni ya tathmini ya nchi kukopa na kulipa mikopo ya Fitch Ratings, imeithibitisha Tanzania kuendelea kuwa ‘B+’ huku likidumisha mtazamo wa “Stable Outlook”. Hatua hiyo inaashiria imani ya Kampuni hiyo katika mwenendo wa uchumi wa nchi pamoja na uthabiti wake wa kifedha katika kipindi cha kati.

Kwa mujibu wa tathmini hiyo, Tanzania inaendelea kunufaika na ukuaji mzuri wa pato la taifa (GDP) , kiwango cha chini cha mfumuko wa bei, deni kuendelea kuwa himilivu ikilinganishwa na nchi nyingine zinazofanana.

Mwenendo mzuri wa uchumi umepelekea upatikanaji wa fedha za nje kupitia programu za Shirika la Fedha la Kimataifa - IMF ikiwemo Extended Credit Facility (ECF) inayohusisha upatikanaji wa mkopo nafuu kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa nchi kupitia sekta za uzalishaji na huduma za jamii na Resilience Sustainability Facility (RSF) ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Ripoti hiyo pia imeeleza kuwa ushindi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi wa Oktoba 2025 unatarajiwa kuendeleza sera za kiuchumi, jambo litakalosaidia utekelezaji wa mipango ya mageuzi ya uchumi na kuendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji.

Kwa upande wa ukuaji wa uchumi, Fitch inatarajia Tanzania kuendelea kuwa na kasi ya ukuaji wa asilimia 6 mwaka 2026 na 2027, juu ya wastani wa nchi zilizo katika kundi la ‘B’ ambapo Ukuaji huo utachangiwa na sekta za kilimo na madini pamoja na uwekezaji mkubwa katika miundombinu, ikiwemo mradi wa reli ya kisasa ya Standard Gauge Railway na bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

Kwa upande wa sera za fedha za umma, Fitch inakadiria nakisi ya bajeti kubaki karibu asilimia 3 ya Pato la Taifa katika miaka ya fedha 2026 na 2027, huku ukusanyaji wa mapato ukiendelea kuimarika kutoka asilimia 14.2 ya Pato la Taifa mwaka wa fedha 2021 hadi asilimia 15.9 mwaka wa fedha 2025.

Ripoti hiyo inaonesha kuwa Mapato ya utalii (travel exports) yalifikia dola za Marekani bilioni 4.4 mwaka 2025, sawa na asilimia 25 ya mauzo yote ya bidhaa na huduma nje ya nchi.

Hata hivyo, hali hii itafidiwa kwa kiasi na kuongezeka kwa thamani ya mauzo ya dhahabu ya Tanzania nje ya nchi, ambayo yalifikia dola za Marekani bilioni 4.7 mwaka 2025 (sawa na asilimia 27 ya jumla ya mauzo ya bidhaa na huduma nje ya nchi).

Aidha, deni la serikali linatarajiwa kushuka hadi asilimia 47 ya Pato la Taifa ifikapo mwaka 2027, likisaidiwa na ukuaji wa uchumi na nidhamu ya matumizi ya Serikali.

Tathmini hiyo pia imepongeza jitihada za Serikali katika kuboresha usimamizi wa fedha za umma, ikiwemo kupunguza madeni ya wazabuni na marejesho ya VAT katika miaka ya karibuni ambapo Kufikia Desemba 2025, kiasi kilichothibitishwa cha madeni hayo kilipungua hadi asilimia 0.2 ya Pato la Taifa (GDP), kutoka asilimia 1.2 mwishoni mwa Desemba 2022, hatua inayochangia kuongeza uwazi na ufanisi wa kifedha.

“Ninawapongeza Viongozi wa Wizara Taasisi zake zote waliofanikisha kazi ya kusimamia sekta hii ya uchumi na fedha, tunafarijika kuona matokeo haya ambayo ni muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu kwani tutaendelea kuaminika katika masoko ya fedha na dhamana ya Kimataifa” alisema Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha

Kwa ujumla, uthibitisho wa daraja la ‘B+’ na mtazamo thabiti unaashiria kuwa Tanzania inaendelea kujenga msingi imara wa uchumi, huku ikiongeza imani ya wawekezaji wa ndani na kimataifa katika uwezo wa nchi kusimamia uchumi wake na kukabiliana na mishtuko ya nje.
Posted by MROKI On Monday, March 30, 2026 No comments
Ofisi ya Afisa Madini Mkazi – Mbogwe inapenda kutoa ufafanuzi kwa umma na vyombo vya habari kuhusu tukio la ajali lililotokea katika Mgodi wa Dhahabu wa Msasa (Msasa Gold Mine) uliopo katika Kijiji cha Msasa, Runzewe, Wilaya ya Bukombe, Mkoa wa Geita.

Mgodi wa Msasa unamilikiwa na Khadija Mkopi Mohamed, Amani Jackonia Mkaga, Boaz Lucas Nkise na Fadhili Victor Malema, ukiwa na jumla ya leseni 17 za uchimbaji zilizotolewa tarehe 22 Oktoba 2025.

Shughuli za uchimbaji zilianza kushika kasi mwezi Novemba 2025, na hadi sasa mgodi unakadiriwa kuwa na maduara takribani 2,000 pamoja na zaidi ya watu 20,000 wanaojihusisha na shughuli za uchimbaji na utoaji huduma mbalimbali.

Mnamo Jumapili tarehe 29 Machi 2026 majira ya saa 4:00 asubuhi, katika eneo la Area A kulitokea mpasuko wa ardhi ulioathiri maduara manne (4) yenye namba KO 46A, 47A, 48A na 49A. Maduara hayo yalikuwa yamesimamishwa uzalishaji kufuatia maelekezo ya wakaguzi wa mgodi yaliyotolewa tarehe 27 Machi 2026 ili kufanyiwa ukarabati wa kiusalama. 

Mpasuko huo ulisababisha maduara hayo kutitia ardhini, hali inayohusishwa na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini na kusababisha kulegea kwa udongo na miamba.

Ni muhimu kufahamu kuwa, wakati tukio linatokea hapakuwa na shughuli zozote za uzalishaji katika eneo husika kwani watendakazi wote walikuwa tayari wameondolewa kupisha ukarabati. Shughuli za ukaguzi katika mgodi huo hufanyika kila siku kupitia Ofisi ya Ukaguzi wa Mgodi inayoongozwa na Mkaguzi Mkuu wa Mgodi akisaidiwa na takribani wakaguzi 200 waliopo muda wote katika eneo la mgodi, chini ya usimamizi wa karibu wa Ofisi ya Afisa Madini Mkazi – Mbogwe, Mkaguzi Mkuu wa Migodi Tanzania pamoja na taasisi nyingine za Serikali kwa mujibu wa sheria.

Baada ya kubainika dalili za hatari, wakaguzi wa mgodi walichukua hatua za haraka kuwaondoa mafundi waliokuwa chini ya ardhi pamoja na watu waliokuwa jirani na eneo hilo ambapo wote waliweza kutoka salama. Vikosi vya uokozi vilivyohusisha Ofisi ya Mgodi, Ofisi ya Madini, Kikosi cha Uokozi na Zimamoto, Jeshi la Polisi pamoja na vyombo vingine vya usalama vilifika mara moja katika eneo la tukio na kusimamisha shughuli zote za mgodi kwa muda, kuweka utepe wa tahadhari katika eneo lililoathirika na kudhibiti wananchi waliokuwa wakijaribu kusogea katika eneo la hatari. 

Ukaguzi wa kina unaendelea kufanywa ili kubaini hatua sahihi za ukarabati na kuandaa mpango salama wa kuendelea na shughuli za uchimbaji.

Hadi sasa, kwa mujibu wa taarifa ya pamoja ya timu ya uokozi, wakaguzi wa migodi na vyombo vya usalama, hakuna mtu aliyeripotiwa kupata majeraha wala kupoteza maisha kutokana na tukio hilo.

Tume ya Madini inawakumbusha wachimbaji na wananchi wote kuendelea kuzingatia taratibu za usalama migodini na kutoa taarifa mapema kwa Tume ya Madini au vyombo vya dola wanapoona dalili zozote za hatari ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kwa wakati.
Posted by MROKI On Monday, March 30, 2026 No comments


Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na wajasiriamali wadogo wanaofanya shughuli zao katika eneo la fukwe ya Coco "Coco Beach" jijini Dar es Salaam Machi 29, 2026 (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa ufafanuzi rasmi kuhusu hatma ya eneo la Coco Beach, akisisitiza kuwa halitauzwa kwa mwekezaji yeyote bali maboresho yatafanyika kwa manufaa ya wananchi waliopo katika eneo hilo.

Amesema hayo leo, Machi 29, 2026, alipotembelea eneo la Coco Beach jijini Dar es Salaam, ambapo alizungumza na wajasiriamali wadogo wanaofanya shughuli zao katika eneo hilo na kusikiliza kero zao mbalimbali.

“Coco Beach haiuzwi. La kwanza niwaondolee hofu—hapauzwi, wala hakuna mwekezaji mwingine zaidi yenu nyinyi wenyewe. Hakuna atakayekuja kutoa maelekezo zaidi ya yale yaliyotolewa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Hapa hapauzwi,” amesisitiza.

Aidha, Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaendelea kutekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kuhakikisha Watanzania wananufaika na maboresho yanayofanyika katika eneo hilo.

“Sisi wasaidizi wa Mheshimiwa Rais tutaendelea kuhakikisha Watanzania wanapata lile tabasamu la Mama ambalo amewaahidi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amewataka watendaji wa Manispaa ya Kinondoni, akiwemo Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi wa Halmashauri, Afisa Biashara pamoja na watendaji wengine, kubadili mtindo wa utendaji kazi kwa kuwafuata wananchi moja kwa moja badala ya kuwasubiri ofisini.

“Ninatoa agizo kwa Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi, Afisa Biashara pamoja na watendaji wengine—msikae ofisini tu. Tokeni mkazungumze na wananchi hawa moja kwa moja pale wanapokuwa na masuala yanayowahusu,” amesisitiza.

Kadhalika, Dkt. Mwigulu amewahimiza wajasiriamali wa eneo la Coco Beach kuunga mkono juhudi za Serikali katika maboresho yanayoendelea kufanyika, huku akisisitiza kuwa fursa zitakazotokana na maboresho hayo zitawanufaisha wao wenyewe.
Posted by MROKI On Monday, March 30, 2026 No comments

March 29, 2026

Utaratibu mpya wa kutoa mafuta kwenye vituo vya kuhifadhia mafuta ya Dizeli na Petroli kwenda sokoni uliowekwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), umetajwa kuharakisha utoaji wa mafuta kwenye vituo vya kuhifadhia kwenda sokoni.

Utaratibu huo wa kikodi unawataka wamiliki wa mafuta hayo kuyalipia kodi kabla ya kuyaingiza sokoni ili yanapoingizwa sokoni yanaendelea na taratibu za uuzwaji hali ambayo inarahisisha usambazaji na kuwafikishia wateja huduma ya mafuta kwa wakati.

Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda amefanya ziara kwenye baadhi ya vituo vya kuhifadhia mafuta ya vyombo vya moto jijini Dar es Salaam leo tarehe 29.03.2026 kikiwemo kituo cha Camel Oil, Moil Energies na Mount Meru na kujiridhisha namna utaratibu huo mpya unavyofanya kazi.

Akiwa katika ziara hiyo Kamishna Mkuu Mwenda amezungumza na wasimamizi wa vituo hivyo ambao wamemuhakikishia uwepo na mafuta ya kutosha kwenye viyuo hivyo na namna  utaratibu mpya wa TRA unavyorahisisha utoaji mafuta na kuweka udhibiti.

Amesema lengo la TRA kuweka utaratibu huo wa kulipia kodi mafuta kabla ya kuingia sokoni ni kuwezesha biashara ya mafuta ya Dizeli na Petroli kufanyika kwa urahisi na kuondoa changamoto zilizokuwepo huku akitoa wito kwa wafanyabiashara watakaokutana na chanagamoto kuwasiliana na TRA.

Aidha amesema TRA imejiwekea utaratibu wa kufanya kazi kwa saa 24 ili kuharakisha utolewaji wa huduma kwa walipakodi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti waratibu na wasimamizi wa vituo vya kuhifadhia mafuta akiwemo Omar Yusufu wa Mount Meru amesema utaratibu huo mpya wa TRA umeonyesha mafanikio makubwa kwa kusaidia uingizaji mafuta sokoni kwa urahisi.

Amesema wamekuwa wakisafirisha mafuta kwenda Rwanda, Burundi, Congo, Zambia na Malawi na kuwa wanayo mafuta ya kutosha huku wakisubiria shehena nyingine kuingia.

Omar Abeid kutoka Camel Oil amesema wanayo mafuta ya kutosha na wamekuwa wakiyauza kwa wateja wao kulingana na mahitaji ya miezi yote ambapo wateja wanaohitaji mafuta ya ziada hawapatiwi ili na wengine wapate huduma hiyo.

Kwa upande wa kituo cha Moil Energies Meneja wake hapa nchini Bw. Sanjar Rai amesema wao hawana upungufu wa mafuta na wanaendelea kutoa huduma zao kama kawaida na kuishukuru TRA kwa kuwapatia huduma kwa wakati.
Posted by MROKI On Sunday, March 29, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Balozi wa Italia nchini Tanzania Mheshimiwa Giuseppe Sean Coppola, na ujumbe kutoka DANIELI Group, Ikulu, Dar es Salaam tarehe 29 Machi, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amefanya mazungumzo na Balozi wa Italia nchini Tanzania, Mheshimiwa Giuseppe Sean Coppola, aliyemtembelea Ikulu, jijini Dar es Salaam.
 
Balozi huyo aliambatana na ujumbe kutoka Danieli Group, kampuni inayoongoza duniani katika teknolojia na uhandisi wa uzalishaji wa chuma, ambao wameonesha nia ya  kuchunguza uwezekano wa kuwekeza katika sekta ya chuma nchini Tanzania.
 
Katika mazungumzo hayo, ujumbe huo uliwasilisha nia ya kuanzisha mradi wa ujenzi wa kiwanda cha kisasa na kikubwa cha chuma mkoani Mtwara, kwa kushirikiana na mwekezaji mzawa.
 
Ushirikiano huu unatokana na majadiliano ya awali yaliyofanyika wakati wa Jukwaa la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Italia, pamoja na mashauriano ya kitaalamu yaliyofuata na taasisi za Tanzania, ikiwemo Mamlaka ya Maeneo Maalum ya Uwekezaji Tanzania (TISEZA) na wizara husika.
 
Mradi unaopendekezwa, ambao bado uko katika hatua ya awali ya uchambuzi, unakadiriwa kugharimu takribani Euro bilioni 1.5 (sawa na takribani Shilingi trilioni 4.2 za Kitanzania), na unatarajiwa kutekelezwa kwa awamu kulingana na tathmini zaidi na taratibu za uwekezaji.
 
Akizungumza katika kikao hicho, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan alikaribisha nia hiyo na kusisitiza dhamira ya Tanzania kuendeleza uwekezaji wa kimkakati unaoendana na vipaumbele vya taifa.
 
“Tanzania inaendelea kujijenga kama kituo shindani na cha kuaminika kwa uwekezaji, ikitegemea rasilimali zake asilia, nafasi yake ya kimkakati, pamoja na mageuzi yanayoendelea kuboresha mazingira ya biashara,” alisema.
 
Aliongeza kuwa, “Tunakaribisha ushirikiano unaoongeza thamani ya rasilimali zetu, unaozalisha ajira kwa wananchi wetu, na kuchangia dira yetu ya muda mrefu ya kujenga uchumi wa viwanda.”
 
Kwa upande wake, Balozi wa Italia alieleza kuwa ushirikiano huo unaakisi kuimarika kwa mahusiano ya kiuchumi kati ya Tanzania na Italia chini ya mifumo mipana ya ushirikiano wa maendeleo.
 
“Nia iliyooneshwa na Danieli Group ni sehemu ya juhudi pana za kuimarisha ushirikiano kati ya nchi zetu mbili, ikiwemo kupitia Mpango wa Mattei kwa Afrika,” alisema.
 
Aliongeza kuwa, “Mpango huu unalenga kukuza uwekezaji endelevu na wenye manufaa kwa pande zote, na Tanzania inaonekana kuwa mshirika muhimu katika muktadha huu.
 
Kwa sasa, tupo katika hatua ya kuangalia uwezekano na tunatarajia kuendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Tanzania kadri majadiliano yatakavyoendelea.”
 
Naye Mtendaji Mkuu wa Danieli Group, Bw. Giacomo Mareschi Danieli, alieleza sababu za kimkakati zilizoifanya kampuni hiyo kuvutiwa na Tanzania.
 
“Tunaona fursa kubwa nchini Tanzania, si tu kutokana na uwepo wa rasilimali kama gesi na madini ya chuma, bali pia kutokana na ukuaji wa soko na nafasi yake ya kimkakati katika ukanda huu,” alisema.
 
“Mtazamo wetu unalenga ushirikiano wa muda mrefu - kuleta teknolojia ya kisasa inayozingatia mazingira, huku tukishirikiana na wadau wa ndani kukuza ujuzi na kujenga uwezo endelevu wa viwanda. Hii ni hatua ya awali, na tumejipanga kuendelea na majadiliano ya kitaalamu ili kutathmini uwezekano wa mradi huu,” aliongeza.
 
Iwapo utatekelezwa, uwekezaji huu unaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa katika ajenda ya Tanzania ya kujenga uchumi wa viwanda chini ya Dira ya Taifa ya 2050, kwa kuimarisha uzalishaji wa ndani wa chuma, kupunguza uagizaji kutoka nje, kuongeza thamani ya rasilimali za ndani, na kutengeneza ajira kwa vijana.
 
Aidha, unaweza kuimarisha nafasi ya Tanzania kama kitovu cha uzalishaji wa chuma katika ukanda huu, hususan kwa nchi jirani zisizo na bandari, pamoja na kusaidia maendeleo ya miundombinu na usafirishaji katika ukanda wa Mtwara.
 
Mheshimiwa Rais Samia alimhakikishia Mheshimiwa Balozi na ujumbe wake kuwa Serikali itaendelea kuwa wazi kwa wawekezaji wenye sifa, wanaoleta si mtaji pekee bali pia teknolojia, ujuzi na dhamira ya muda mrefu katika maendeleo ya Tanzania.
 
Kikao hicho kimeonesha kuendelea kuimarika kwa mvuto wa Tanzania kama kituo cha uwekezaji, pamoja na dhamira ya pamoja ya pande zote mbili kuendelea kuchunguza fursa zitakazozalisha thamani endelevu ya kiuchumi na ukuaji shirikishi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Balozi wa Italia nchini Tanzania Mheshimiwa Giuseppe Sean Coppola pamoja na ujumbe kutoka DANIELI Group, Ikulu, Dar es Salaam tarehe 29 Machi, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Mkurugenzi na Mmiliki wa DANIELI Group Bw. Giacomo Mareschi-Danieli, Ikulu, Dar es Salaam tarehe 29 Machi, 2026.
Posted by MROKI On Sunday, March 29, 2026 No comments

March 28, 2026

Sehemu ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA) wakiimba wimbo wa ‘Mshikamano Daima’ kabla ya kuanza kikao cha 37 cha Baraza hilo, kilichofanyika Machi 27, 2026 jijini Dodoma.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA), Alban Kihulla akifungua kikao cha 37 cha Baraza la Wafanyakazi wa Wakala hiyo kilichofanyika Machi 27, 2026 jijini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Sekta ya Afya (TUGHE), Ngazi ya Taifa, Rugemalira Rutatina akizungumza wakati wa kikao cha 37 cha Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA) kilichofanyika Machi 27, 2026 jijini Dodoma.
Baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA), wakichangia hoja mbalimbali wakati wa kikao cha 37 cha Baraza hilo kilichoketi Machi 27, 2026 jijini Dodoma.

Baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA), wakichangia hoja mbalimbali wakati wa kikao cha 37 cha Baraza hilo kilichoketi Machi 27, 2026 jijini Dodoma.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA), Alban Kihulla (katikati) akiongoza kikao cha 37 cha Baraza la Wafanyakazi wa Wakala hiyo kilichoketi Machi 27, 2026 jijini Dodoma. Kulia ni Katibu wa Baraza, Meckytidicy Ngonyani na kushoto ni Katibu Msaidizi, Fadhil Msane.
Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA) wakiimba wimbo wa ‘Mshikamano Daima’ baada ya kuhitimisha kikao cha 37 cha Baraza hilo kilichofanyika Machi 27, 2026 jijini Dodoma.
***************
Na Mwandi wa WMA – DODOMA
Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA), Alban Kihulla amewataka watendaji wa Wakala hiyo kuanza ukaguzi wa mazao ya shamba na kupambana zaidi na ufungashaji wa mazao hayo kwa mtindo wa lumbesa.

Akifungua Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa WMA, Machi 27, 2026 jijini Dodoma, Kihulla amewasisitiza wajumbe wa Baraza hilo kufikisha ujumbe huo kwa watumishi wote katika maeneo yao kuanza kutekeleza jukumu hilo kikamilifu.

“Lakini tunapotekeleza majukumu haya, tuhakikishe haki katika biashara na kulinda mapato ya Serikali,”ametahadharisha.

Amesema kuwa katika kipindi cha kuanzia Julai 2025 hadi Machi 2026, WMA imepata mafanikio mbalimbali katika utekelezaji wa majukumu yake ya kumlinda mlaji kupitia uhakiki wa vipimo lak
ini pia kumekuwepo na changamoto kadhaa.
Akidadavua, amesema mafanikio yaliyopatikana yametokana na juhudi, weledi na ushirikiano wa watumishi wote wa Wakala hivyo amewapongeza kwa kazi nzuri wanayoendelea kufanya.

“Pamoja na mafanikio hayo, bado tunakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na ongezeko la wigo wa majukumu yetu katika kumlinda mtoa huduma pamoja na mpokea huduma,” ameeleza.

Mtendaji Mkuu Kihulla amebainisha baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na jukumu la uhakiki wa vipimo vinavyotumika kupima muda wa maongezi pamoja na uhakiki wa mita za maji na vilevile lumbesa; suala ambalo liliungwa mkono na Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Sekta ya Afya (TUGHE), Ngazi ya Taifa, Rugemalira Rutatina ambaye pia alishiriki mkutano huo, akisema yako malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi katika maeneo hayo hivyo yanapaswa kushughulikiwa.

Kihulla amesisitiza kuwa hata viongozi wakuu wa Wizara akiwemo Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga wameielekeza WMA kupambana na ufungashaji mazao ya shamba kwa mtindo wa lumbesa ili kuwalinda wakulima.

Katika hatua nyingine, Mtendaji Mkuu amewahimiza wafanyakazi wote wa WMA kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na uzalendo akiwataka kutambua kuwa kazi wanayofanya ina mchango mkubwa katika kulinda haki za wananchi pamoja na kukuza biashara ya ushindani na haki, ikiwemo pia kuongeza mapato ya Serikali.

“Kwahiyo, niwaombe sana mkawasisitize watumishi waliopo katika vituo vyenu kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na weledi na kubwa zaidi kujiepusha na vitendo vya rushwa.”

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la WMA, Isaac Birahi aliushukuru Uongozi wa Wakala hiyo kwa kuendelea kuweka mazingira mazuri ya ufanyaji kazi kwa watumishi na kuomba hali hiyo iendelee kwa viwango vya juu zaidi.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Sera na Mipango, Nelson Ruturagala, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango na Bajeti katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 16, 2026 alisema kuwa Wakala imefanikiwa kutekeleza Mpango Kazi wake kwa wastani wa zaidi ya asilimia 91.62

Akidadavua, aliyataja maeneo ya utekelezaji yaliyochangia kufikia wastani huo kuwa ni katika usimamizi wa vipimo, ukaguzi, uhakiki wa bidhaa zilizofungashwa zinazoingia nchini pamoja na ada kutokana na utolewaji wa huduma.

Katika kikao hicho cha 37, wajumbe wa baraza walipata pia fursa ya kujadili Mpango na Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027.
Posted by MROKI On Saturday, March 28, 2026 No comments









Na Mwandishi Wetu, Kahama
Naibu Waziri wa Nishati Mh. Salome Makamba amekabidhi vitendea kazi vya usafiri kwa TANESCO Mkoa wa Shinyanga kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi na kutatua changamoto zao kwa haraka.

Akizungumza leo tarehe 27, Machi 2026 wakati wa hafla ya kukakabidhi vitendea kazi hivyo iliyofanyika katika Manispaa ya Kahama Mkaoni Shinyaga Mhe. Salome amesema  hatua hiyo ya kukabidhi vitendea kazi hivyo ni kuyaishi maono ya Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma za Umeme wa uhakika.

Amesema vitendea kazi  hivyo vinakwenda kuongeza ufanisi katika utendaji kazi kwa watumishi wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga na kuwawezesha kutatua changamoto za wateja kwa wakati. 

“Kupitia vyombo hivi vya usafiri vitakwenda kuleta mabadiliko makubwa katika kumfikia mteja kwa haraka na kumhudumia, niwaombe mvitumie kutatua changamoto zao kwa wakati “ amesema Salome.

Aidha Mhe. Salome ametumia nafasi hiyo kuwataka wakazi wa Manispaa ya Kahama kuchangamkia matumizi ya Nishati safi ya umeme kupikia kwani Nishati ya umeme ni nafuu salama na rafiki kwa mazingira.

“Niwaombe wakina mama wa Kahama tuchangamkie matumizi ya nishati safi ya kupikia ya umeme, TANESCO wameleta majiko hapa unapika kwa urahisi na haraka zaidi”.

Hata hivyo Mhe. Salome amesema Serikali kupitia Shirika la Umeme TANESCO inaendelea kwa kasi kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katika Manispaa ya Kahama kutokana na kuendelea kukua kwa Mji huo ambapo mpaka sasa tayari zaidi ya  Shilingi milioni 600 zimetengwa kwa ajili ya kujenga laini mpya ya umeme itakayo wahudumia wakazi wa Manispaa ya Kahama.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga Mhandisi Benson Mbigili amesema wamepokea vitendea kazi mbalimbali ikiwemo Magari manne (4), Bajaji moja (1)  pamoja na Pikipiki nne (4). 


Mha. Benson ameipongeza Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania TANESCO kwa kuwezesha vitendea kazi hivyo ambavyo kwa sasa wanakwenda kuvitumia kufikisha huduma kwa wananchi kwa haraka zaidi.

Amesema kupitia Magari hayo sasa yatawasaidia kuwafikia wateja wapya katika maeneo yote hasa yale korofi ambapo kabla ya Magari hayo ilikuwa changamoto kuwafikia na kuwaahidi wananchi kuendelea kutoa huduma bora na ya uhakika kila wakati.

“Tunaishukuru Serikali kupitia Shirika la umeme Tanzania TANESCO kwa kutupa vitendea kazi hivi ambavyo kwa sasa tunakwenda kuvitumia kufikisha huduma kwa wananchi kwa haraka zaidi.

Aidha amesema TANESCO Mkoa wa Shinyanga inaendelea kwa kasi kubwa kuhamasisha matumizi ya Nishati safi ya kupikia kwa umeme ili wananchi waweze kuelewa umuhimu wa kutumia nishati hiyo kupikia.
Posted by MROKI On Saturday, March 28, 2026 No comments

March 27, 2026








Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) zimethibitisha azma ya kuendeleza ushirikiano katika kukuza sekta binafsi, uwekezaji na uchumi endelevu kwa manufaa ya pande zote mbili.

Hayo yameelezwa katika mazungumzo kati ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb), na Mkurugenzi wa IFC Kanda ya Afrika Mashariki, Mary Porter Peschka, yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Kombo amepongeza mchango mkubwa wa IFC katika kuimarisha sekta ya fedha nchini, hususan kupitia usaidizi kwa benki za NMB, CRDB na NBC. Amesema ushirikiano huo umeongeza upatikanaji wa mikopo na mitaji, na kuwa msaada muhimu kwa wajasiriamali wadogo na wa kati.

Aidha, Serikali imetambua mchango wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) katika maendeleo ya miundombinu, ikiwemo huduma za ushauri kwa miradi ya kimkakati kama mradi wa mabasi yaendayo haraka (BRT) jijini Dar es Salaam. Amesema ushiriki wa shirika hilo katika sekta za kilimo-biashara na viwanda pia umechangia kuongeza thamani ya mazao na kufungua fursa za ajira kwa Watanzania.

Mhe. Kombo amesisitiza kuwa Serikali inaendelea kuipa kipaumbele sekta binafsi kama injini ya ukuaji wa uchumi, kwa lengo la kuendeleza viwanda na kuongeza thamani ya bidhaa ili kufikia malengo ya maendeleo ya taifa ifikapo mwaka 2050.

Kwa upande wake, Bi. Peschka ameipongeza Tanzania kwa utekelezaji mzuri wa miradi inayofadhiliwa na IFC, na kueleza kuwa shirika hilo litaendelea kushirikiana na nchi katika kukuza matumizi ya teknolojia na kuandaa wataalamu watakaoongeza tija katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda, kilimo na miradi ya kimkakati.
Posted by MROKI On Friday, March 27, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo