Nafasi Ya Matangazo

May 14, 2026






Na Mwandishi wetu, Dodoma
Wizara ya Madini imetoa siku tatu kwa wachimbaji na wanunuzi wa madini ya jasi kuwasilisha mchanganuo wa gharama za uzalishaji ili kupata suluhisho litakalowanufaisha pande zote katika biashara ya madini hayo.

Agizo hilo limetolewa leo Mei 14, 2026 jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, wakati wa kikao kati ya wachimbaji wa madini ya jasi na wanunuzi zikiwemo kampuni za saruji na wazalishaji wa gypsum kilichofanyika katika ukumbi wa Makao Makuu ya Tume ya Madini.

Dkt. Kiruswa amesema Serikali inahitaji kila upande kuwasilisha kwa kina changamoto zinazoukabili ili kufanya uchambuzi utakaosaidia kufikia muafaka wenye manufaa kwa wachimbaji, wanunuzi na watumiaji wa mwisho.

“Tunataka kila upande uainishe vitu vinavyouumiza upande mmoja na vinavyoubeba upande mwingine ili baada ya uchambuzi huo tupate suluhisho la pamoja,” amesema Dkt. Kiruswa.

Aidha, ameahidi Serikali kuyafanyia kazi malalamiko kuhusu tozo mbalimbali zinazotozwa na baadhi ya halmashauri ambazo zimeelezwa kuwa zinaongeza gharama za uzalishaji na biashara ya madini ya jasi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wachimbaji Wadogo wa Madini ya Jasi Mkoa wa Lindi, Salum Kassim, amesema bei ya madini hayo haijawahi kuongezeka tangu mwaka 2016 licha ya kupanda kwa gharama za uzalishaji ikiwemo mafuta, vipuri vya mitambo na mishahara ya wafanyakazi.

Amesema hali hiyo imeathiri uzalishaji na kufanya wachimbaji wengi kushindwa kupata faida kutokana na biashara hiyo.

Katika mapendekezo yao, wachimbaji wamependekeza bei ya tani moja ya jasi kwa Dar es Salaam na Pwani iongezwe kutoka shilingi 110,000 hadi 150,000, Mkoa wa Mtwara kutoka shilingi 75,000 hadi 95,000, Mkuranga kutoka shilingi 95,000 hadi 130,000 huku eneo la Kiranjeranje bei ikipendekezwa kuongezeka kutoka shilingi 60,000 hadi 75,000 kwa tani.

Kwa mujibu wa Kassim, marekebisho ya bei yatasaidia kufufua uzalishaji wa madini hayo na kuboresha maisha ya wachimbaji ambao kwa sasa wanakabiliwa na changamoto kubwa za uendeshaji.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa Manunuzi wa kampuni ya Dangote Cement Limited, Halima Kuchwa, ametoa tahadhari kuwa ongezeko la gharama za malighafi linaweza kuathiri bei ya saruji sokoni na hatimaye kumgusa mtumiaji wa mwisho.

Madini ya jasi ni miongoni mwa malighafi muhimu inayotumika katika uzalishaji wa saruji, gypsum na bidhaa nyingine za ujenzi nchini. Tanzania ina maeneo kadhaa yenye uzalishaji wa jasi ikiwemo Lindi, Mtwara, Pwani na Mkuranga. Kwa miaka ya hivi karibuni, wachimbaji wadogo wamekuwa wakilalamikia kupanda kwa gharama za uzalishaji huku bei ya soko ikibaki ileile kwa muda mrefu, hali inayodaiwa kupunguza tija na kuathiri uzalishaji wa madini hayo.
Posted by MROKI On Thursday, May 14, 2026 No comments










Na Mwandishi Wetu, Singida
Kamati ya Kitaifa  ya Ufungaji Migodi imeendelea na vikao vyake kwa siku mbili katika Mgodi wa dhahabu wa Shanta uliopo mkoani Singida kwa lengo la kujadili na kupitia Mpango wa Ufungaji wa Mgodi huo ili kuhakikisha unazingatia matakwa ya Sheria ya Madini, Sura 123 na Kanuni za Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira katika kufunga mgodi huo.

Akiongoza kikao hicho kilichowakutanisha wataalam kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Wizara ya Maji, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Madini, Tume ya Matumizi Endelevu ya Ardhi, Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Tume ya Madini pamoja na viongozi wa Wilaya, Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Ufungaji Migodi, Dkt. Abubakary Salama amesema  migodi mikubwa na ya kati inalazimika kisheria kuandaa mipango ya ufungaji migodi.

Amesema  kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Madini Sura ya 123 pamoja na Kanuni ya 206 ya Kanuni za Madini (Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira) za Mwaka 2010, wamiliki wa migodi wanapaswa kuandaa mpango wa ufungaji mgodi na kuuwasilisha kwa Mkaguzi Mkuu wa Migodi kwa ajili ya mapitio ya kitaalam kabla ya kuidhinishwa na Kamati ya Kitaifa ya Ufungaji Migodi.

Kwa upande wake, Mshauri Mwelekezi  kutoka kampuni ya MTL Consulting Company Limited, John Bosco Tindyebwa, amesema  kampuni hiyo imefanikiwa kuandaa na kuwasilisha Mpango wa Ufungaji wa Mgodi wa Singida Gold Mine unaomilikiwa na Shanta Mining Company kwa ajili ya mapitio ya kitaalam na uidhinishaji wa Kamati hiyo.

Ameongeza kuwa kampuni ya MTL itaendelea kushirikiana kwa karibu na Tume ya Madini, Shanta Mining Company pamoja na wadau wengine muhimu wa sekta ya madini ili kuhakikisha mpango huo unazingatia viwango vinavyotakiwa, kulinda mazingira na kuacha manufaa endelevu kwa jamii zinazozunguka mgodi huo baada ya shughuli za uchimbaji kukamilika.

Naye Meneja Mkuu wa Mgodi wa dhahabu wa Singida, Juma Kisonda, ameihakikishia Kamati kuwa mgodi huo unaendelea kuzingatia masuala ya usalama, afya na utunzaji wa mazingira, akisisitiza kuwa uongozi wa mgodi utatekeleza maelekezo yote yatakayotolewa na Kamati ya Kitaifa ya Ufungaji Migodi ili kuhakikisha ufungaji wa mgodi unafanyika kwa kuzingatia viwango vinavyokubalika kitaifa na kimataifa.
Posted by MROKI On Thursday, May 14, 2026 No comments




Na Mwandishi wetu, 
Dodoma
Watumishi wapya 37 wa Tume ya Madini wametakiwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, uwajibikaji na uzalendo katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuimarisha usimamizi wa Sekta ya Madini na kuongeza mchango wake katika Pato la Taifa. Wito huo umetolewa wakati wa ufunguzi wa mafunzo elekezi kwa waajiriwa hao kabla ya kuripoti katika vituo vyao vya kazi mbalimbali nchini.

Akizungumza katika Ofisi za Tume ya Madini Makao Makuu jijini Dodoma, Meneja wa Utawala wa Tume ya Madini, Jacob Mnyenyelwa, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimaliwatu na Utawala, Nsajigwa Kabigi, amesema watumishi hao wanapaswa kuzingatia maadili ya kazi, weledi na uwazi wanapotoa huduma kwa wananchi na wadau wa sekta ya madini.

Amesema wananchi wana matarajio makubwa kutoka katika Sekta ya Madini, hivyo watumishi wapya wanapaswa kuwa mfano bora wa uadilifu, ubunifu na uzalendo ili kuhakikisha rasilimali madini zinasimamiwa kwa manufaa ya Taifa. 

Amesisitiza kuwa utendaji wenye maadili utaongeza imani ya wananchi na wawekezaji katika sekta hiyo muhimu ya uchumi.

Mafunzo hayo yamewashirikisha wahandisi, mafundi sanifu pamoja na afisa TEHAMA, yakilenga kuwajengea uwezo kuhusu majukumu yao, misingi ya utumishi wa umma, mawasiliano ya kikazi na taratibu za utendaji ndani ya Tume ya Madini kabla ya kuanza majukumu rasmi.

Tume ya Madini imeendelea kuimarisha rasilimaliwatu kwa kuajiri wataalam wenye ujuzi mbalimbali ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuongeza ufanisi wa usimamizi wa shughuli za utafiti, uchimbaji na biashara ya madini nchini, hatua inayotarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu ya Taifa.
Posted by MROKI On Thursday, May 14, 2026 No comments



Na Mwandishi Wetu, Shinyanga
Mkoa wa Shinyanga umeendelea kuimarisha nafasi yake kama kitovu muhimu cha sekta ya madini nchini, huku uchimbaji wa dhahabu na almasi ukitajwa kuwa nguzo kuu ya ukuaji wa uchumi wa mkoa huo na chanzo kipya cha fursa za uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani ya madini.

Akizungumza mkoani Shinyanga, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa huo, Mhandisi Noel Odera, amesema mkoa umebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi za madini zikiwemo dhahabu, almasi, madini ya ujenzi pamoja na madini ya viwandani kama chokaa, hali inayochochea shughuli za kiuchumi, ajira kwa wananchi na ongezeko la mapato ya Serikali.

Amesema shughuli za uchimbaji zinaendelea kwa kasi katika maeneo mbalimbali ya mkoa, zikihusisha wachimbaji wadogo, wa kati na migodi mikubwa, ikiwemo migodi ya El-Illari na Williamson Diamond iliyopo Wilaya ya Kishapu katika eneo la kimbaritiki linalozalisha sehemu kubwa ya almasi nchini.

Kwa mujibu wa Mhandisi Odera, utafiti mpya umeibua matumaini ya ongezeko la uzalishaji baada ya wachimbaji wadogo kugundua almasi katika eneo la Ng’wapangabule kwenye mwamba unaofanana na kimbaritiki, hatua inayofungua fursa mpya za uwekezaji na utafiti wa kina wa kijiolojia.

Ameeleza kuwa uzalishaji wa dhahabu unaendelea kuimarika katika maeneo ya Mwakitoryo, Nyandolwa, Mwanubi, Ishinabulandi na Mwazezema ambapo wachimbaji wadogo na wa kati wameendelea kuchangia ukuaji wa sekta hiyo kupitia ajira, kipato binafsi na mapato ya Serikali.

Mbali na uchimbaji, amesema Shinyanga ina mazingira rafiki kwa uwekezaji katika viwanda vya kisasa vya uchenjuaji wa dhahabu vinavyotumia teknolojia za Carbon in Pulp (CIP) na Carbon in Leach (CIL), vitakavyosaidia kuongeza thamani ya madini kabla ya kuuzwa na kuwapa wachimbaji huduma bora za uchenjuaji.

Aidha, amesema mkoa una fursa kubwa za uwekezaji katika viwanda vya utengenezaji wa bidhaa zitokanazo na almasi ikiwemo vito vya thamani na mapambo, hatua itakayoongeza thamani ya madini ndani ya nchi na kuimarisha uchumi wa viwanda.

Mhandisi Odera ameongeza kuwa uwepo wa malighafi za kutosha kama chokaa umeifanya Shinyanga kuwa eneo lenye uwezo mkubwa wa uwekezaji katika viwanda vya saruji, vitakavyosaidia kukuza sekta ya ujenzi, kuongeza ajira na kuimarisha maendeleo ya kijamii.

Amesema masoko ya madini yanaendelea kuimarika ambapo kwa sasa kuna wanunuzi wakubwa 19 wa dhahabu na almasi wanaofanya biashara mkoani humo, hali inayorahisisha biashara ya madini kwa wachimbaji na kuongeza uwazi wa biashara hiyo.

Amehitimisha kwa kuwahimiza wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kutumia fursa zilizopo Shinyanga kwa kuwekeza katika uchimbaji, utafiti wa madini na viwanda vya kuongeza thamani, akisisitiza kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki ili sekta ya madini ichangie zaidi maendeleo endelevu ya taifa na ustawi wa wananchi.
Posted by MROKI On Thursday, May 14, 2026 No comments

May 13, 2026

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Erica E. Yegella amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa fursa ya ajira mpya takriabani 259 katika kipindi cha mwezi Januari na Mei 2026.

Katika kipindi cha mwezi Januari, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ilifanikiwa kupangiwa ajira mpya takribani 111 kwenye kada tofauti tofauti ikiwemo elimu msingi na sekondari, afya, ujenzi, maendeleo ya jamii, utawala, na mawasiliano.

Mnamo mwezi Aprili 2026, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ilipangiwa ajira mpya 118 kwenye kada tofauti tofauti ikiwemo elimu msingi na sekondari, afya, ujenzi, na uhasibu.

Mwezi Mei, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ilipangiwa ajira mpya 30 mahususi kwa ajili ya watu wa kada ya afya pekee, wakataosaidia jitihada za utoaji huduma muhimu za afya katika zahanati na vituo vya afya vilijengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya.

Bi. Yegella amesema ajira mpya zilizotolewa kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kupitia Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, ni jambo ambalo anapaswa kupongezwa sana Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kukubali ombi la kuongeza watumishi katika Halmashauri.

"Katika kipindi cha miezi mitano pekee, Rais ameruhusu Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kupangiwa ajira mpya zaidi ya 250. Tunamshukuru sana kwa hili. Hii ni fursa kwa vijana wa kitanzania pamoja Halmashauri kwani itasaidia kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma muhimu za kijamii," ameeleza Bi. Yegella.
Posted by MROKI On Wednesday, May 13, 2026 No comments

May 11, 2026

Serikali kupitia Bohari ya Dawa (MSD) itaendelea kununua dawa zinazozalishwa na wawekezaji wa ndani ili kuimarisha uzalishaji wa ndani wa bidhaa za afya na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje ya nchi.

Hayo yamesemwa Waziri wa Afya, Mohammed Mchengerwa leo Mei 11 2026 akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 Bungeni, Jijini Dodoma.

“Serikali imejipanga kuhakikisha MSD inanunua kwanza dawa zinazozalishwa ndani ya nchi zilizokidhi viwango vya Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) kabla ya kwenda kununua kutoka nje ya nchi, hatua inalenga kukuza viwanda vya ndani, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi wa Taifa” amesema Waziri Mchengerwa

Amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi, ikiwemo kuboresha upatikanaji wa ardhi, miundombinu muhimu pamoja na kuratibu uwekezaji katika sekta ya dawa na bidhaa za afya ili kuvutia uwekezaji zaidi nchini.
Waziri Mchengerwa amesema Serikali imeendelea kuimarisha upatikanaji wa bidhaa za afya nchini kwa kutoa Shilingi trilioni 1.4 kupitia MSD ili kuhakikisha wananchi wanapata dawa na bidhaa muhimu za afya kwa wakati.

“Upatikanaji wa bidhaa muhimu za afya umeongezeka kutoka asilimia 58 mwaka 2021/22 hadi asilimia 88 mwezi Machi 2026” amesema Waziri Mchengerwa.

Amesema kuwa Wizara ya Afya itaendelea kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi pamoja na kuwawekea mazingira rafiki na wezeshi, ikiwemo upatikanaji wa ardhi na miundombinu muhimu, ili kuwavutia kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya bidhaa za afya na kupunguza utegemezi.

Waziri Mchengerwa amesisitiza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya, dawa salama na huduma zenye ubora bila kuachwa nyuma.
Posted by MROKI On Monday, May 11, 2026 No comments





Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), ameshiriki Mkutano wa Dharura wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Siasa, Ulinzi, na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC-MCO), uliofanyika  tarehe 10 Mei, 2026, Jijini Nairobi, Kenya.

Mkutano huo uliolenga kuimarisha misingi ya amani, umeongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. George Chaponda, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Jamhuri ya Malawi.

Katika mazungumzo hayo, Mawaziri wamejadili  changamoto mbalimbali za kiusalama zinazoikabili kanda hiyo ikiwemo  Vurugu zinazoendelea nchini Afrika Kusini dhidi ya raia wa nchi nyingine za Afrika.

Kwa Upande wake Mwenyekiti Dkt. Chaponda amewahakikishia wajumbe wa mkutano huo kuwa mapendekezo yote yaliyofikiwa yatafanyiwa kazi kwa haraka na kwa ufanisi. Hatua hii ni sehemu ya mikakati ya SADC kuhakikisha kuwa Kanda ya Kusini mwa Afrika inasalia kuwa kisiwa cha amani, utulivu, na ushirikiano wa kiuchumi.
Posted by MROKI On Monday, May 11, 2026 No comments

May 10, 2026


Na. Mwandishi Wetu, Ismani 
Wagombea 17 wameteuliwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kugombea ubunge Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa.

Uteuzi huo umefanywa kwa niaba ya Tume na Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Ismani, Ndugu. Caroline Angwen Otieno leo tarehe 10 Mei, 2026. 

Wagombea walioteuliwa na vyama vyao kwenye mabano ni Ndugu. Emmanuela Kaganda Mtatifikolo (CCM), Ndugu. Farida Issa Mwapungu (MAKINI), Ndugu. Asha Athumani Chuma (UPDP), Ndugu. Protas Shaibu Mgimbila (CCK), Ndugu. Fidelis Daud Mtikile (SAU), Ndugu. Hadija Husen Makawa (ADA-TADEA) Ndugu. Zavely Raurent Seleleka (UDP) na Ndugu. Subira Majuto Kalolo (NLD).

Wengine ni Ndugu. Bernard George Mwingira (DP), Ndugu. Burton Emilyo Chetenge (NCCR-Mageuzi), Ndugu. Mbalinga Christian Thomas (N.R.A), Ndugu. Mark Isdory Mhemela (AAFP), Ndugu.  Nassim Yahaya Upete (CUF), Ndugu. Mwaka Lameck Mgimwa (TLP), Ndugu. Asma Abdallah Othman (UMD), Ndugu. Maimuna Martin Lumato (ADC) na Ndugu. Daudi Issa Masasi (CHAUMMA). 

Akizungumza baada ya uteuzi huo, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo, Ndugu. Caroline Angwen Otieno amesema kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Tume, 

Kampeni kwa ajili ya uchaguzi mdogo wa Jimbo la Ismani pamoja na kata 12 za Tanzania Bara zitaanza kesho tarehe 11 hadi 31 Mei, 2026 na uchaguzi utafanyika siku ya Jumatatu tarehe 01 Juni, 2026.

Baada ya hatua hii ya uteuzi, kinachofuata ni kubandika fomu za uteuzi eneo la wazi kwa ajili ya kuwapa fursa ya kuweka pingamizi wale wanaoruhusiwa kuweka pingamizi kwa mujibu wa sheria. 

Baada ya saa 24 kupita na endapo hakutakuwa na pingamizi wagombea hao 17 wataendelea na kampeni kuanzia kesho tarehe 11 hadi 31 Mei, 2026 na uchaguzi utafanyika tarehe 01 Juni, 2026, amesema. 

Kata 12 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi mdogo wa Udiwani ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu. 

Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.


















Posted by MROKI On Sunday, May 10, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo