Nafasi Ya Matangazo

April 08, 2026

 


Na Shaban Juma, WAF – Dodoma
Serikali ya Tanzania inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kukuza utalii wa tiba, ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kuongeza uchumi wa sekta ya afya na mchango wake wa pato la Taifa.

Hayo yamesemwa leo Aprili 08, 2026, na Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Florence Samizi, bungeni jijini Dodoma, akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Dkt. Catherine Canute Joachim, katika Bunge la Kumi na Tatu, Mkutano wa Tatu, Kikao cha Nne.

Akijibu swali kwa niaba ya Waziri wa Afya,.Mhe. Mohamed Mchengerwa, Dkt. Samizi amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imewekeza zaidi kwenye uboreshaji wa miundombinu ya hospitali, ikiwemo kujenga majengo mapya na kukarabati yale yaliyochakaa.

Aidha, amesema Serikali inaendeleza upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa kama PET/CT Scan, Angio Suite, Cathlab, na CT Scan, sambamba na kuendeleza mafunzo ya kitaaluma kwa wataalamu wa afya ili kuhakikisha huduma zinakuwa za ubora wa kimataifa.

“Serikali pia inaanzisha huduma mpya za ubingwa bobezi na kuhakikisha hospitali zinapata ithibati za kimataifa, na kuzitangaza katika masoko ya kimataifa ili kuvutia wagonjwa kutoka nje ya nchi,” amesema Dkt. Samizi.

Takwimu zinaonyesha ukuaji wa utalii wa tiba: katika kipindi cha Julai 2025 hadi Februari 2026, wagonjwa 3,018 kutoka nje ya nchi walipatiwa huduma za ubingwa bobezi katika hospitali za rufaa za mikoa, kanda, maalum na taifa.

Aidha, Dkt. Samizi ameongeza kuwa Serikali inaendelea kuwekeza katika rasilimali watu kupitia Samia Health Super-specialization Program, ambapo wataalamu 1,483 wanafadhiliwa kusomea fani za ubingwa na ubingwa bobezi ndani na nje ya nchi, hatua inayolenga kuongeza ubora na uwezo wa hospitali zetu.



Posted by MROKI On Wednesday, April 08, 2026 No comments

April 07, 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum mbele ya kaburi la aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake, Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum mbele ya kaburi la aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake, Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akiweka Shada la Maua katika Kaburi la Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume mara baada ya Dua iliyofanyika katika Afisi Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kisiwandui Zanzibar leo tarehe 07 Aprili 2026, katika Siku ya Kumbukumbu ya (Karume Day).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akiweka Shada la Maua katika Kaburi la Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume mara baada ya Dua iliyofanyika katika Afisi Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kisiwandui Zanzibar leo tarehe 07 Aprili 2026, katika Siku ya Kumbukumbu ya (Karume Day).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum ya kumuombea aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake. Dua hiyo maalum imefanyika Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum ya kumuombea aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake. Dua hiyo maalum imefanyika Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.




Posted by MROKI On Tuesday, April 07, 2026 No comments

April 02, 2026

DODOMA
Kuelekea sikukuu ya Pasaka, Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, Bw. Pendolake Elinisafi, ameongoza ziara ya kutembelea kaya za watu wenye ulemavu wa macho wilayani Chamwino (Matembebora), akiongozana na Meneja Msaidizi Huduma kwa Walipa Kodi, Bw. John Njau, pamoja na watumishi wengine wa TRA Mkoa wa Dodoma, kwa lengo la kutoa faraja, upendo na kuwajengea matumaini, akisisitiza kuwa wao ni sehemu muhimu ya jamii inayothaminiwa.

Akizungumza kwa niaba ya wanakaya hao, Mwenyekiti Bw. Yeledi Cheleso ameishukuru TRA Dodoma kwa moyo wa kujali na msaada walioutoa, akieleza kuwa hatua hiyo imeongeza faraja na kuwapa nguvu mpya ya kuendelea na maisha.

Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii, Bi. Elizabeth, ameipongeza TRA kwa kuendeleza mshikamano na jamii, akibainisha kuwa juhudi hizo zinaimarisha ushirikiano kati ya taasisi na wananchi, hususan kwa makundi yenye uhitaji maalum.

Ziara hiyo imeacha ujumbe wa upendo na mshikamano, ikionesha dhamira ya TRA ya kuendelea kugusa maisha ya jamii sambamba na majukumu yake ya ukusanyaji wa mapato.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments




Na Saidi Saidi WMJJWM - Dodoma 
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe.Dkt. Dorothy Gwajima, ametoa wito kwa jamii na wazazi kushiriki kikamilifu katika malezi na ulinzi wa watoto, ili kuzuia ongezeko la watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani. 

Akizungumza na waandishi wa habari Aprili 01, 2026 jijini Dodoma kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mtoto anayeishi na kufanya kazi mtaani, yatakayofanyika Aprili 12, 2026 Jijini Dar Es Salaam yakiwa na Kaulimbiu isemayo “Malezi na Ulinzi wa Mtoto, Wajibu wetu Sote”.

Amesema ushiriki wa pamoja ni muhimu ili kuhakikisha watoto wanakua katika mazingira salama na yenye maadili mema huku akisisitiza jukumu la malezi si la wazazi pekee, bali ni la jamii nzima. 

Aidha, Waziri Gwajima ameeleza kuwa changamoto kama umasikini, migogoro ya kifamilia, na ukatili dhidi ya watoto zimekuwa zikichangia watoto wengi kukimbilia mitaani.

Ameibainisha pia mafanikio ya juhudi za Serikali katika kuwaokoa watoto wa mitaani kuwa zaidi ya watoto 5,000 wameunganishwa na familia zao tangu kuanza kwa kampeni ya kuwaokoa watoto wa mitaani mwaka 2025.

Vilevile, Serikali imeanzisha mifumo mbalimbali, ikiwemo madawati ya ustawi wa jamii katika vituo vya usafiri na makao ya watoto, ili kuhakikisha watoto waliookolewa wanapata huduma muhimu kama elimu, afya, na malezi bora.

Waziri Gwajima ametoa wito kwa Watanzania kushirikiana na Serikali kwa kutoa taarifa za ukatili dhidi ya watoto na kuhakikisha wanapata malezi bora. Amesisitiza kuwa watoto wa mitaani wanapaswa kulindwa na kupewa fursa sawa za maendeleo, akihitimisha kwa kusema kuwa ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha hakuna mtoto anayelazimika kuishi au kufanya kazi mitaani.

Waziri Gwajima ametumia nafasi hiyo pia kuwashukuru wadau wote wanaoshirikiana na Serikali katika kuhakikisha malezi ya watoto yanaimarishwa hususani shirika SoS Village na Railway Children.

Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Dodoma, mkuu wa wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wadau wote katika kukabiliana na changamoto ya watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani, akieleza hatua mbalimbali zilizofikiwa na mkoa wa Dodoma.

Shekimweri amesema mwaka 2024 hadi 2026 Serikali ya mkoa imewaunganisha watoto 293 na familia zao.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments


Na Mwandishi wa OMH,Dar es Salaam. 
Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH) imeanza zoezi la uchambuzi wa mipango na bajeti za taasisi na mashirika ya umma, likilenga kuimarisha mchango wa taasisi hizo katika utekelezaji wa Dira 2050.

Akizungumza kuhusu zoezi hilo, Alhamis, Aprili 2, 2026, Bw. Joseph Mwaisemba, Mkurugenzi Msaidizi wa Tathmini ya Mashirika yasiyo ya kibiashara (kwa upande wa mamlaka za udhibiti), alisema jumla ya watumishi 50 wa OMH wamekutana katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere kwa ajili ya kuchambua bajeti za taasisi na mashirika ya umma 252.

Alisema uchambuzi huo unalenga kuangalia namna taasisi hizo zilivyojipanga katika kutekeleza Dira 2050 sambamba na Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (FYDP IV).

“Tunachofanya hapa ni kuangalia kwa kina mipango ya taasisi na mashirika ya umma ili kuona namna inavyochangia utekelezaji wa Dira 2050 na mipango ya maendeleo ya taifa kwa ujumla,” alisema.

Aidha, alieleza kuwa zoezi hilo pia linahusisha uchambuzi wa mikakati ya taasisi hizo katika kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kutekeleza bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27.

Kwa mujibu wake, OMH inasimamia jumla ya taasisi 308, kati ya hizo 252 zinamilikiwa na serikali kwa hisa nyingi na 56 zinamilikiwa na serikali kwa hisa chache, huku jumla ya uwekezaji ukiwa ni Sh92.3 trilioni.

OMH pamoja na mashirika yake yaliyo chini yake yanatarajiwa kukusanya Sh1.8 trilioni kama mapato yasiyo ya kodi katika mwaka wa fedha 2026/27, ikiwa ni sehemu ya bajeti ya Serikali inayokadiriwa kufikia Sh62 trilioni.

“Hivyo basi, unaweza kuona namna ambavyo zoezi hili lilivyo muhimu katika kuhakikisha malengo ya Serikali yanafikiwa,” alisisitiza.

Kisheria, utekelezaji wa zoezi hilo la uchambuzi unaongozwa na matakwa ya kifungu cha 10(2)(c) cha Sheria ya Msajili wa Hazina, Sura ya 370, pamoja na kifungu cha 17(a) cha Sheria ya Bajeti, Sura ya 439, vinavyoitaka OMH kufanya uchambuzi wa mipango na bajeti za taasisi na mashirika ya umma yaliyo chini yake.

Kwa kuzingatia msingi huo wa kisheria, lengo la uchambuzi huo ni kuidhinisha mikakati na mipango ya mwaka ya taasisi na mashirika ya umma, na kuijumuisha katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo kwa ajili ya usimamizi madhubuti wa utekelezaji pamoja na upatikanaji wa rasilimali za kugharamia mipango hiyo.

Aliongeza kuwa katika uchambuzi huo, wataalamu wanapitia mipango ya matumizi ya rasilimali kwa kuangalia mgawanyo kati ya matumizi ya kawaida, miradi ya maendeleo, pamoja na michango ya taasisi katika bajeti kuu ya Serikali.

Maeneo makuu yanayopewa kipaumbele ni pamoja na tathmini ya namna taasisi zilivyojipanga kutekeleza miradi ya maendeleo kwa kutumia fedha za Serikali na zile zinazotokana na vyanzo vya ndani vya mashirika husika.

Baada ya kukamilika kwa uchambuzi huo, bajeti zitaingizwa katika mfumo wa mipango na bajeti wa Serikali (PlanRep), kabla ya OMH kuendelea na jukumu la kufuatilia utekelezaji wake kwa kila robo mwaka ili kuhakikisha malengo yaliyokubaliwa yanafikiwa.

Bw. Mwaisemba alitoa wito kwa taasisi na mashirika ya umma kushirikiana kikamilifu katika kuhakikisha rasilimali chache zilizopo zinatumika kwa ufanisi katika upangaji na usimamizi wa mipango.

“Ufanisi wa kila shirika katika kutekeleza majukumu yake utaakisi moja kwa moja mafanikio ya utekelezaji wa Dira 2050 pamoja na mipango ya maendeleo ya taifa,” alisisitiza.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akijibu maswali, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026.
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akisikiliza swali kutoka kwa Mbunge wa Viti Maalum Rose Tweve katika kipindi cha Masalı kwa Waziri Mkuu, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026. 
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba  akisikiliza swali kutoka kwa Mbunge wa Tunduru Kakazini, Ado Shaibu katika kipindi cha Maswalı kwa Waziri Mkuu, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akijibu maswali, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akijibu maswali, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026.
Mbunge wa Nachingwea, Fadhili Liwaka akimuuliza swali Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba katika Kipindi cha Masalı kwa Waziri Mkuu, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026. 
*********************
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amemuelekeza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) Profesa Riziki Shemdoe ahakikishe halmashauri zote ambazo bado hazijachukua viuadudu kwa ajili ya kutokomeza ugonjwa wa malaria ifikapo mwezi Mei zote ziwe zimeshakusanya dawa hizo ili ifikapo mwezi Juni waweze kutekeleza zoezi hilo.
 
Ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Aprili 2, 2026 wakati akijibu swali la Rose Tweve, Mbunge wa Viti Maalum katika kipindi cha Maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu. Mbunge huyo alitaka kujua tamko ya Serikali kuhusu baadhi ya halmashauri ambazo bado hazijatekeleza agizo la chukua viuadudu na kusababisha adha kwa Watanzania.
Kwa mujibu wa mbunge huyo Mwaka wa fedha 2025/2026 Serikali ilitoa kiasi cha shilingi bilioni 6.5 kwa ajili ya ununuzi wa lita 541,666 za viuadudu  ili ziweze kusambazwa katika halmashauri zote nchini, ambapo hadi sasa kuna baadhi hazijachukua dawa hizo huku wananchi wakiendelea kupoteza maisha kutokana na ugonjwa wa malaria.
 
“…Cha kusikitisha Mheshimiwa Waziri Mkuu kuna baadhi ya halmashauri hazijatekeleza agizo hilo na kusababisha adha kwa Watanzania kwani tatizo la maralia bado linaendelea kupoteza maisha ya Watanzania kwa sababisha vifo hususani kwa wanawake na watoto. Je nini tamko la Serikali kwa halmashauri hizi ambazo bado hazijatekeleza agizo hili?” alihoji.
 
“Ni kweli kumekuwepo agizo hilo la Serikali katika jitihada za kupambana na maralia kuhakikisha kwamba kunakuwepo na dawa hizo ambazo Serikali imezinunua kwa lengo la kupelekwa kwenye halmashauri zote nchini ili ziweze kuchukua hatua za kukabiliana na ugonjwa huo.”
 
Amesema suala hilo lilishajadiliwa ndani ya Serikali na kwamba ilihitajika yafanyike mafunzo katika ngazi za halmashauri kuhusu utekelezaji wa jambo hilo, kulikuwepo na angalizo la ratiba kwamba jambo hilo liweze kutekelezwa kuanzia mwezi Juni na kuendelea kwa kuwa ni kipindi ambacho maeneo mengi ya nchi yanakuwa hayana mvua.
 
Wakati huo huo, Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Sita imefanya jitihada kubwa za kuweza kuhakikisha kwamba mikoa ambayo haijaunganishwa kwa barabara za lami inaunganishwa ili kuweza kuhakikisha mawasiliano pamoja na biashara zinafanyika.
 
Waziri Mkuu amesema hadi sasa kuna mikoa michache ambayo bado kazi hiyo haijakamilika.  “Natambua kutoka Katavi kwenda Rukwa kulikuwa bado kuna eneo ambalo bado halijaunganishwa kwa lami lakini mkandarasi yuko site kwa ajili ya kuunganisha mkoa wa Rukwa na Katavi, Katavi kwenda Kigoma kulikuwa na sehemu bado haijaunganiishwa kwa lami fedha zipo zoezi hilo litakamilika.”
 
Ameyasema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Kisesa, Mussa Mbuga aliyetaka kujua ni upi mpango wa Serikali katika kuhakikisha barabara zote zinazounganisha mikoa nchini zinajengwa kwa kiwango cha lami ili kurahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa mbalimbali kwa ajili ya kuchochea ukuaji wa uchumi.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeandika historia nyingine ya mafanikio baada ya kuvuka malengo ya ukusanyaji mapato katika robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26, ikiashiria uimara wa mifumo ya kodi na juhudi za dhati za mageuzi ya kiutendaji.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamishna Mkuu wa Mamlaka hiyo Yusuf Mwenda, TRA imefanikiwa kukusanya jumla ya shilingi trilioni 9.31 katika kipindi cha Januari hadi Machi 2026, kiwango kinachozidi lengo la shilingi trilioni 8.75. 

“Hii ni sawa na ufanisi wa asilimia 106.4, ikiwa ni ishara tosha ya nidhamu ya ukusanyaji na kuimarika kwa mifumo ya usimamizi wa kodi nchini,”anasema Kamishna Mwenda kwenye taarifa hiyo.

Taarifa inasema kwa mwezi Machi pekee, TRA ilikusanya shilingi trilioni 3.58 dhidi ya lengo la trilioni 3.32, sawa na ufanisi wa asilimia 107.6. 

Takwimu hizi zinaonesha kasi ya kipekee ya ukusanyaji mapato, huku zikionesha pia mwitikio mzuri wa walipa kodi pamoja na juhudi za mamlaka katika kuziba mianya ya ukwepaji kodi.

Ukuaji wa mapato pia umeonekana kuwa wa kuridhisha, ambapo katika robo ya tatu ya mwaka huu wa fedha, TRA imepata ongezeko la asilimia 23.6 ikilinganishwa na makusanyo ya shilingi trilioni 7.53 katika kipindi kama hicho mwaka wa fedha 2024/25. 

Huu ni ushahidi wa wazi kuwa mageuzi yanayoendelea ndani ya mamlaka hiyo yanaanza kuzaa matunda yanayoonekana.

Uchambuzi wa mwenendo wa kila mwezi unaonesha kuwa Januari 2026 TRA ilikusanya trilioni 3.04 kwa ufanisi wa asilimia 106.7, Februari trilioni 2.69 kwa ufanisi wa asilimia 104.4, huku Machi ikiongoza kwa trilioni 3.58. Hali hii inaashiria uthabiti wa makusanyo kwa miezi yote mitatu ya robo ya tatu, bila kuyumba.

Wachambuzi wa masuala ya uchumi wanaeleza kuwa mafanikio haya yanachangiwa kwa kiasi kikubwa na matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa kodi, kuimarika kwa ushirikiano kati ya TRA na walipa kodi, pamoja na hatua kali dhidi ya wakwepa kodi. 

Aidha, elimu kwa walipa kodi imeendelea kusaidia kuongeza uelewa wa umuhimu wa kulipa kodi kwa hiari.

Mbali na mafanikio ya robo ya tatu, takwimu za kipindi cha miezi tisa kuanzia Julai 2025 hadi Machi 2026 zinaonesha kuwa TRA imekusanya jumla ya shilingi trilioni 28.005 dhidi ya lengo la trilioni 26.773, sawa na ukuaji wa asilimia 16.5. 

Hii inaashiria kuwa mamlaka ipo kwenye mstari sahihi wa kufikia na hata kuzidi malengo ya mwaka mzima wa fedha.

Katika hatua nyingine, ufanisi wa usimamizi wa sheria za kodi umeendelea kuimarika, ambapo uwiano wa gharama za ukusanyaji umebaki kuwa mdogo katika asilimia 2.41. 

Hii ina maana kuwa TRA inaendelea kutumia rasilimali chache kukusanya mapato makubwa zaidi, jambo linaloonesha ufanisi wa hali ya juu wa kiutendaji.

Aidha, mchango wa kodi katika pato la taifa umeongezeka hadi kufikia asilimia 14.1 kutoka asilimia 13.7, hatua inayodhihirisha jinsi mapato ya ndani yanavyozidi kuwa mhimili muhimu wa maendeleo ya uchumi wa nchi.
Wadau wa maendeleo wamepongeza mafanikio haya wakieleza kuwa yanaongeza imani kwa wawekezaji na washirika wa maendeleo, kwani yanaonesha uthabiti wa mifumo ya kifedha ya nchi.

Pia, mafanikio haya yanatarajiwa kusaidia serikali katika kugharamia miradi ya kimkakati bila kutegemea sana mikopo ya nje.

Hata hivyo, wataalam wanashauri kuwa pamoja na mafanikio haya, TRA inapaswa kuendelea kuboresha huduma kwa walipa kodi, kupunguza urasimu, na kuimarisha mifumo ya kidigitali ili kuongeza zaidi wigo wa walipa kodi na kuhakikisha uendelevu wa mafanikio haya.
Kwa ujumla, matokeo ya robo ya tatu yanaweka wazi kuwa TRA imepiga hatua kubwa katika ukusanyaji wa mapato, na kuifanya kuwa taasisi muhimu katika kuimarisha uchumi wa Tanzania. 

Kasi hii ikiendelezwa, basi matarajio ya kufikia malengo ya mwaka mzima wa fedha yanaonekana kuwa si ndoto bali ni jambo linalowezekana kwa asilimia kubwa.

Wachambuzi wa Masuala ya Kiuchumi wanashauri kuwa huu ni wakati muafaka kwa wadau wote kushirikiana zaidi na TRA ili kujenga taifa linalojitegemea kwa mapato yake ya ndani. 

Mafanikio haya si ya TRA pekee, bali ni ushindi wa kila Mtanzania anayetekeleza wajibu wake wa kulipa kodi kwa hiari na kwa wakati.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments
Ushirikiano baina ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Walipakodi umetajwa kuwezesha Mamlaka hiyo kuandika historia mpya kwa kukusanya kiasi cha shilingi trilioni 9.31 kwa kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26 sawa na ufanisi wa asilimia 106.4 ya lengo la kukusanya shilingi trilioni 8.75.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda April 1, 2026 imeeleza kuwa kwa mwezi Machi pekee TRA imekusanya shilingi trilioni 3.58 sawa na ufanisi wa asilimia 107.6 ya lengo la kukusanya shilingi trilioni 3.32.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa makusanyo hayo ya kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26, ni sawa na ukuaji wa asilimia 23.6 ikilinganishwa na kiasi cha shilingi trilioni 7.53 kilichokusanywa katika kipindi kama hicho mwaka wa fedha 2024/25. 

Kwa mujibu wa taarifa hiyo Ufanisi wa makusanyo kwa mwezi Machi unapelekea TRA kuweza kuandika rekodi mpya za kipekee katika ukusanyaji wa mapato nchini Wastani wa Makusanyo kwa mwezi katika kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26 umefikia shilingi trilioni 3.10 ambacho ni kiasi cha juu kabisa ukilinganisha na wastani wa shilingi trilioni 2.51  kwa kipindi kama hicho mwaka 2024/25.

TRA imeweza kurekodi Ukuaji chanya wa asilimia 23.6 katika kipindi cha Januari -Machi 2026, na imeweza kulifikia na kuvuka lengo la makusanyo kwa miezi 21 mfululizo kuanzia mwezi Julai 2024, mafanikio ambayo Mamlaka haijawahi yafikia toka ianzishwe hali ambayo imechagizwa na makusanyo ambayo yamechangiwa na ukaribu uliopo baina ya Mamlaka hiyo na Walipakodi.

Imeeleza kuwa Makusanyo yaliyokusanywa kwenye robo ya tatu ya Mwaka wa Fedha 2025/26 ni sawa na ukuaji wa asilimia 114.1 ukilinganisha na kiasi cha shilingi trilioni 4.35 kilichokusanywa katika kipindi kama hicho wakati Serikali ya Awamu ya Sita ilipoingia madarakani, mwaka 2020/21. 

Ushirikiano baina ya TRA na walipakodi umeiwezesha katika kipindi cha Julai, 2025 hadi Machi, 2026, kusajili walipakodi waруа 900,755 ambao ni ufanisi wa asilimia 131.36 wa kusajili walipakodi wapya 685,706 kufikia tarehe 31 Machi, 2026.

Pia imeelezwa kuwa katika kipindi cha robo ya tatu mahusiano na Viongozi wa vyama vya wafanyabiashara pamoja na wafanyabiashara wenyewe yaliimarishwa kwa kufanya mikutano na kuwasikiliza ili kutatua changamoto zao za kikodi ambapo TRA itaendelea kuboresha mahusiano na walipakodi kwenye Shughuli zote za Kiuchumi ili kuhamasisha ulipaji kodi wa hiari nchini.

Aidha TRA inapenda kuwahakikishia wananchi wote kuwa itaendelea kushirikiana na wananchi wote kwa ukaribu ili kuhakikisha kuwa lengo la makusanyo kwa mwaka huu wa fedha 2025/26 linafikiwa lote na hivyo kuiwezesha Serikali kuweza tekeleza mipango ya maendeleo kwa manufaa ya Taifa zima.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akifurahi jambo na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, wakati wakiagana mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican Aprili mosi, 2026.




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akisalimiana na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican,  April mosi, 2026.

Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kusimamia na kuratibu ushiriki wa Tanzania katika michezo ya kimataifa sambamba na kuharakisha maandalizi ya mashindano ya AFCON 2027 kwa lengo la kujenga urithi endelevu wa michezo, uchumi na heshima ya Taifa.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatano, Aprili 1, 2026) wakati akiwasilisha hotuba yake kuhusu Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma.

Amesema Tanzania inaendelea na maandalizi ya kuwa mwenyeji katika mashindano ya AFCON 2027, ambayo yanahusisha ujenzi na ukarabati wa viwanja pamoja na miundombinu wezeshi ikiwemo ujenzi wa Uwanja wa Arusha uliofikia asilimia 75.

“Ukarabati wa Uwanja wa Benjamin Mkapa umefikia asilimia 95; na ujenzi wa Uwanja wa Dodoma umefikia asilimia nne. Vilevile, Serikali imekamilisha ujenzi na ukarabati wa viwanja vya Meja Jenerali Isamuhyo, Gymkhana Club na Shule ya Sheria Tanzania kwa ajili ya mazoezi”.
 
Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea na ujenzi wa Viwanja vya Farasi, Gymkhana Annex na Leaders Club ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kuimarisha miundombinu ya michezo nchini.
 
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema mafanikio yanayoendelea kushuhudiwa katika sekta ya michezo yanatokana na uwekezaji wa kimkakati na uongozi thabiti wa Serikali.

“…Ninapenda kutumia fursa hii pia, kulipongeza Shirikisho la Mchezo wa Mpira wa Miguu Tanzania kwa uongozi, uratibu na usimamizi mzuri wa mchezo huo hapa nchini. Kupitia uongozi huo, kwa mara ya kwanza Tanzania imefanikiwa kuingiza vilabu vinne kwa pamoja katika hatua ya makundi ya mashindano ya Klabu Bingwa na Shirikisho Barani Afrika”.
 
Waziri Mkuu amevitaja vilabu hivyo kuwa ni Klabu ya Michezo Yanga (wananchi), Klabu ya Michezo Simba (wenye nchi), Klabu ya Michezo Azam (wana lambalamba) na Klabu ya Michezo Singida (wana kilemankundi).

Amesema kuwa mafanikio katika mchezo wa mpira wa miguu na michezo mingine kwa ujumla ni matokeo ya uwekezaji na hamasa inayotolewa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Mafanikio hayo, siyo tu yanaleta burudani kwa mashabiki, bali yanatoa fursa ya ajira na uwekezaji hapa nchini”.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha ushiriki wa wanafunzi katika michezo ili kuibua na kukuza vipaji vyao, ikiwa ni mkakati wa muda mrefu wa kujenga kizazi cha wanamichezo wenye ushindani kimataifa. 
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete leo April 1, 2026 akitia saini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Rais wa zamani wa Algeria, Jenerali Mstaafu Liamine Zeroual,  aliyefariki dunia mnamo Machi 28, 2026 akiwa na umri wa miaka 84 baada ya kuugua kwa muda mrefu. Pamoja naye ni Balozi wa Algeria nchini Mheshimiwa Ghalib Zermane.  Kitabu hicho kimefunguliwa nyumbani kwa Balozi Oysterbay jijini Dar es salaam.

Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete leo April 1, 2026 ametia saini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Rais wa zamani wa Algeria, Jenerali Mstaafu Liamine Zeroual,  aliyefariki dunia mnamo Machi 28, 2026 akiwa na umri wa miaka 84 baada ya kuugua kwa muda mrefu.
 
Jenerali Zeroual, aliyependwa na kuheshimikka sana, alichaguliwa kuwa rais mwaka 1995 katika kipindi kigumu cha vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Algeria. 

Alianzisha mageuzi ya kisiasa, ikiwa ni pamoja na kuratibu uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi.
 
Hata hivyo alijiuzulu mapema mwaka 1998 kabla ya kumaliza muhula wake wa miaka mitano ili kutoa nafasi kwa mpito wa kisiasa, na tangu hapo aliishi maisha ya faragha bila kujihusisha sana na siasa.
 
Hadi leo anakumbukwa kama kiongozi aliyetoa mchango muhimu katika kuiongoza Algeria katika kipindi cha mpito na changamoto kubwa za kisiasa na kiusalama.
 
Akiongea na Balozi wa Algeria nchini Mheshimiwa Ghalib Zermane, Dkt Kikwete alisema Algeria na Tanzania imekuwa rafiki wa karibu kwa muda mrefu, na kwamba viongozi wake wote waliopita wamefanya kazi kwa karibu na viongozi wa Tanzania kuanzia Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, hususan katika  ukombozi wa bara la Afrika, akiwataja viongozi hao kama Ahmed Ben Bella, Houari Boumédiène, Chadli Bendjedid,  Liamine Zéroual na Abdelaziz Bouteflika.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo