Nafasi Ya Matangazo

June 29, 2026









Na Mwandishi Wetu – Dar es Salaam
SERIKALI imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuhakikisha Watu Wenye Ulemavu wanapata nafasi sawa katika nyanja zote za maendeleo, ikiwa ni pamoja na kijamii, kiuchumi na kisiasa, kupitia sera, sheria na mipango jumuishi inayotekelezwa nchini.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt. Jim Yonazi wakati wa ufunguzi wa kikao kazi kilichowakutanisha viongozi wa vyama vya Watu Wenye Ulemavu na mashirika yasiyo ya kiserikali kujadili utekelezaji wa sera, sheria na miongozo ya ujumuishaji nchini.

Amesema hatua kubwa zimeendelea kuchukuliwa katika kuhakikisha hakuna mwananchi anayeachwa nyuma, ambapo Sera ya Taifa ya Watu Wenye Ulemavu ya mwaka 2004 pamoja na Sheria Na. 9 ya mwaka 2010 zimekuwa msingi muhimu wa utekelezaji wa haki na usawa kwa kundi hilo.

“Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa kila sera, mpango na huduma inayotekelezwa nchini inazingatia ujumuishaji wa Watu Wenye Ulemavu tangu hatua ya upangaji, utekelezaji, ufuatiliaji hadi tathmini, ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma,” amesema Dkt. Jim Yonazi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa mawasiliano bora na uratibu imara kati ya Serikali, vyama vya Watu Wenye Ulemavu na mashirika yasiyo ya kiserikali, akibainisha kuwa ushirikiano huo ni msingi muhimu wa kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa shughuli za maendeleo.

Amesema ujumuishaji si jukumu la sekta moja pekee, bali ni wajibu wa kila taasisi, kila sekta na kila mdau wa maendeleo. “Tunapaswa kufanya kazi kwa pamoja ili kuhakikisha huduma zote zinamfikia kila mwananchi kwa usawa,” alisisitiza.

Dkt. Yonazi pia ametoa wito wa kuimarishwa kwa mifumo ya mawasiliano inayowezesha Watu Wenye Ulemavu kupata taarifa kwa urahisi, ikiwemo matumizi ya lugha ya alama, maandishi ya Breli, teknolojia saidizi na mifumo mingine jumuishi.

“Serikali inatambua mchango mkubwa unaotolewa na vyama vya Watu Wenye Ulemavu pamoja na mashirika yasiyo ya kiserikali katika kutoa huduma za utetezi wa haki, elimu kwa umma, mafunzo ya kujenga uwezo, uwezeshaji kiuchumi, huduma za afya, elimu jumuishi na ushauri wa kitaalamu,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Yonazi amesema kuwa pamoja na jitihada ambazo Serikali imeendelea kuzichukua, bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazohitaji ushirikiano wa wadau wote.
Amesema changamoto hizo ni pamoja na uelewa usioridhisha kuhusu masuala ya ujumuishaji katika baadhi ya sekta, utekelezaji usiofanana wa sera na sheria, pamoja na changamoto za upatikanaji wa huduma jumuishi zinazokidhi mahitaji ya Watu Wenye Ulemavu.

“Kutokana na hali hiyo, kikao hiki ni muhimu sana kwa kuwa kinatoa fursa ya kujadili kwa kina namna bora ya kuimarisha ujumuishaji wa huduma katika sekta zote.”

Awali, Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA), Bi. Tungi Mwanjala, ameiomba Serikali kuendelea kuangalia uwezekano wa kuwatambua watoto wa wazazi wenye ulemavu ili waweze kunufaika na fursa mbalimbali za maendeleo, ikiwemo kupata mikopo ya elimu ya juu kwa urahisi.

Bi.Mwanjala ameeleza kuwa, Serikali imepiga hatua kubwa kwa kukamilisha muongozo na mfumo wa utambuzi wa watu wenye ulemavu, lakini bado kuna haja ya kupanua utambuzi huo kwa watoto wa wazazi wenye ulemavu.

"Tunashukuru Serikali kwa kukamilisha muongozo na mfumo wa kutambua watu wenye ulemavu. Hata hivyo, tunaomba pia watoto wetu watambuliwe kupitia mfumo maalumu utakaowezesha kupata vitambulisho, jambo litakalowarahisishia kupata mikopo ya elimu ya juu na fursa nyingine za maendeleo ikiwamo ajira kwa kuzingatia utaratibu uliopo," amesema.
Posted by MROKI On Monday, June 29, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Ikiwa ni takribani miaka 30 imepita tangu ianzishwe Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Julai 1, 1996, Mamlaka hiyo inajivunia maendeleo, uwazi, mageuzi na mabadiliko chanya ya kimifumo yaliyofanyika ambayo yamekuwa chachu ya kufikia malengo ya Mamlaka hiyo na maendeleo ya taifa kwa ujumla.

Akizungumza kuhusiana na mafanikio hayo, Juni 28, 2026, Jijini Dodoma, Meneja wa Elimu kwa Mlipakodi wa TRA,  Paul Walalaze, anasema imekuwa ni miaka 30 ya mafanikio mengi na Mamlaka inajivunia utendajikazi na ushirikiano mkubwa wanaoupata kutoka kwa walipakodi na wananchi katika ujenzi wa taifa.

"Kama ambavyo TRA inawajibika kukusanya kodi, katika miaka hii 30, tumeweza kuongeza makusanyo kutoka shilingi bilioni 531 kwa mwaka wa fedha 1996/1997 hadi trilioni 32 mwaka 2025/2026, ongezeko hili ni kubwa na ndiyo maana serikali inafanya mambo makubwa ya kimaendeleo kwa wananchi wake, kwani fedha za kufanya hayo zipo," amesema Walalaze.

Aidha, Walalaze anasema, TRA imefanikiwa kuwafikia wanafunzi, walipakodi na wananchi wengi kuwapa elimu ya kodi. 

"TRA tunakwenda walipo wadau wetu, yaani shuleni, vyuoni, sehemu za kazi, viwandani na kwenye biashara ili kuwapa elimu. Pia tunashirikiana na taasisi za elimu kufundisha masuala ya kodi, kutumia vipeperushi, vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, hii yote ni kuhakikisha kila raia anakuwa na uelewa wa masuala ya kodi na ashiriki katika kulipa kodi," amesema.

Sambamba na hilo, Meneja huyo wa Elimu ya Mlipakodi, anasisitiza kuwa, Mamlaka ya Mapato imeimarisha matumizi ya teknolojia katika utendaji na usimamizi wa kodi ili kufikia malengo yaliyowekwa.

"Kwa kiwango kikubwa sana, Mamlaka imehama kutoka kwenye matumizi ya karatasi na sasa tupo kidijitali zaidi. Mathalani, usajili wa walipakodi, malipo ya kodi, utoaji wa risiti, masuala ya forodha na mengine mengi yanafanyika kwa njia ya mtandao."

"Tulipoanza kutumia teknolojia, baadhi walikuwa na hofu, lakini leo, walipakodi wenyewe wanafurahia kwani hawana ulazima wa kufikia katika ofisi za TRA kuhudumiwa, wanafanya shughuli zao kule kule walipo, na Mamlaka inapata taarifa zao," amesema.

Katika hatua nyingine, Walalaze anasema, katika miaka 30, Mamlaka inajivunia kuongezeka uwazi na uwajibikaji ambao umekuwa nyenzo muhimu ya kufikia malengo na maendeleo.

"Sasa hivi hakuna janjajanja, utendajikazi na shughuli za kikodi zinafanyika kwa uwazi, na uwazi huu umeongeza uwajibikaji na uadilifu kwa watendaji wa Mamlaka na walipakodi pia," amesisitiza.

Vilevile, Mamlaka imefanikiwa kujenga uhusiano mzuri kati yake na walipakodi. Anasisitiza kuwa, kumekuwa na mafanikio ya kujenga uhusiano mzuri ambao umekuwa chachu ya ongezeko la makusanyo ya kodi, kwani meza ya mazungumzo ipo na inatumika vyema kufikia muafaka wa ulipaji kodi.

"Eneo la uhusiano mzuri limefanikiwa sana hasa kufuatia maelekezo ya Mheshimiwa Rais wetu, Dk. Samia Suluhu Hassan ambaye anasisitiza majadiliano yachukue nafasi na kuachana na matumizi ya mabavu katika ukusanyaji wa kodi, na hapa niseme tumefanikiwa sana, na tija yake imeakisi katika ongezeko la mapato," amesema Walalaze.

Mafanikio mengine, ni kuimarika kwa mazingira ya biashara na uwekezaji. Walalaze anasisitiza kuwa wafanyabiashara na wawekezaji ni mashahidi wa namna Mamlaka ilivyoweka mazingira mazuri ya ufanyikaji wa shughuli za biashara na uwekezaji, na hili limesaidia kuongezeka kwa idadi ya wafanyabiashara ambao ni chachu ya kukuza uchumi na maendeleo nchini.

Kwa mwaka wa fedha 2026/2027, TRA inapaswa kukusanya shilingi trilioni 36.99 ili kufanikisha bajeti nzima ya serikali ya shilingi trilioni 62.33, hivyo TRA inahimiza walipakodi na wananchi kwa ujumla kutimiza wajibu wa kulipa kodi kwa hiari ili kufikia malengo ya serikali ya kukuza uchumi na kuboresha ustawi wa wananchi.

Ikumbukwe kuwa, Julai 1, 2026, Rais Dk. Samia atatoa tuzo kwa walipakodi mahiri kwa mwaka wa fedha 2024/2025, ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wa walipakodi katika ujenzi wa taifa na kujenga motisha kwa walipakodi kuendelea kulipa kodi.

Sambamba na hilo, Walalaze ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi, Julai 2, katika uwanja wa KMC Complex, ambapo kutakuwa na mechi ya kirafiki kati ya timu ya TRA United na URA FC kutoka Uganda, ikiwa ni mwendelezo wa maadhimisho ya miaka 30 ya mafanikio kwa kuzingatia TRA inashirikiana na mamlaka nyingine za ukusanyaji kodi za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. Katika mechi hiyo, hakuna kiingilio, yaani ni bure.
Posted by MROKI On Monday, June 29, 2026 No comments

June 28, 2026

Na Neema Chalila Mbuja, Bagamoyo
IMEELEZWA  kuwa ni muhimu kwa maeneo yenye Malikale kuenziwa na kutangazwa ili  historia yake irithishwe kwa vizazi vijavyo.

Hayo yamesemwa leo Juni 28, 2026 mjini Bagamoyo na Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Kale, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Cristowaja Ntandu wakati wa kuhitimisha ziara ya Menejimenti ya wizara hiyo na taasisi zake waliokuwa wakitembelea maeneo ya Malikale na namna watakavyotumia fursa ya ujio wa Michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON -2027) kunadi Malikale kuvutia watalii.

Ameyataja maeneo ya Malikale ambayo wajumbe wa Menejimenti wameyatembelea kuwa ni pamoja na mabaki ya Magofu ya Kaole, Ngome Kongwe eneo la Bagamoyo na eneo la njia ya msafara wa watumwa kutoka Kigoma Ujiji hadi Bagamoyo ambalo ndio lililokuwa  Soko la Watumwa kwa Afrika Mashariki.

Awali akizungumza wakati wa ziara hiyo,  Kamishna wa Kanda ya Mashariki wa Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA) John Nyamuhanga amesema kuna haja ya kuhakikisha kuwa TANAPA inanadi historia ya nchi yetu ili kuongeza idadi ya watalii hadi kufikia milioni nane ifikapo mwaka 2030.

Amesema jamii inapaswa kurithishwa utalii wa Malikale na kuendelea kutoa mafunzo kwa jamii na  wanafunzi ili kujenga uelewa wa pamoja kuhusu urithi wa Malikale uliopo.

Menejimenti ya Wizara ya Maliasili na Utalii imehitimisha ziara yake ya kutembelea maeneo ya Malikale na kuafikiana kutumia vema uwepo wa Malikale kuitangaza Tanzania kwa  kutumia fursa ya ujio wa AFCON na matukio mengine makubwa kutangaza utalii. 












Posted by MROKI On Sunday, June 28, 2026 No comments

June 26, 2026

Na Mwandishi Wetu, Dodoma 
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambayo ni miongoni mwa taasisi chini ya Wizara ya Fedha imejipanga kuhakikisha kuwa bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 inafanikiwa kikamilifu katika utekelezaji wake.

Hayo yameelezwa na Meneja wa Elimu kwa Mlipakodi wa TRA, Paul Walalaze, Juni 26, 2026, Jijini Dodoma.

Walalaze amesema, bajeti nzima ni shilingi trilioni 62.33, ila TRA ina jukumu kuhakikisha inafanikisha makusanyo ya shilingi trilioni 36.99, ili mipango mizuri iliyowekwa na serikali katika kukuza maendeleo na ustawi wa wananchi ifanikiwe.

"TRA inaendelea kusimamia mkakati wa utiifu wa hiari kupitia utoaji wa elimu kwa walipakodi kwa kutumia vyombo vya habari, mitandao ya kijamii na mlango kwa mlango. Kimsingi, wananchi wakielimishwa ipasavyo juu ya umuhimu wa kulipa kodi na namna kodi hizo zinavyoweza kuleta maendeleo, hawana shida wanalipa, na ndiyo maana TRA tumeimarisha sana elimu ya mlipakodi na matunda yake tumeyaona," amesema Walalaze.

Aidha, Walalaze amesema, mkakati mwingine ambao umeonyesha matokeo chanya na utaendelea kuimarishwa ni kuhimiza mifumo ya kieletroniki ya ukusanyaji mapato na kufuatilia miamala ya malipo.

"Malipo yanapofanyika kieletroniki yanakwenda moja kwa moja panapohusika na kuepusha mianya ya upotevu wake. Hili limehimizwa sana katika bajeti ya mwaka huu, na TRA tunalisimamia hili kikamilifu," amesema.

Katika hatua nyingine, Walalaze amesema, TRA imejipanga kuhakikisha maeneo yote ya forodha yanaimarishwa ili Mamlaka ipate mapato yake ambayo ni chachu ya maendeleo kwa wananchi. Hii ina maana kwamba, TRA itasimamia kikamilifu kazi za forodha kama bandarini na mipakani.

"Maeneo yote ya forodha kama bandarini na mipakani yataimarishwa, na kila bidhaa inayopaswa kulipiwa kodi, italipiwa kwa mujibu wa sheria za kodi. Hii litaijengea uwezo Mamlaka kupata mapato ili kuiwezesha serikali kufanikisha mipango ya maendeleo kwa wananchi," amesisitiza.

Mikakati mingine ambayo TRA imejipanga nayo ni pamoja na kuongeza usajili wa walipakodi wapya hasa wa sekta isiyo rasmi ikiwa ni mpango wa kujumuisha sekta zote yaani sekta rasmi na isiyo rasmi katika ujenzi wa Taifa.

Vilevile, kutumia teknolojia za malipo na mifumo ya kidijitali ili kufuatia biashara ambazo hapo awali hazikuwa kwenye mifumo ya kikodi inayotambulika na serikali.

Mikakati mingine ni kuongeza ushirikiano baina ya TRA na wafanyabiashara bila kusahau utoaji wa elimu mahsusi juu ya mabadiliko ya sheria za fedha ili kujenga uelewa wa pamoja kwa walipakodi na wananchi kwa ujumla.

Halikadhalika, Walalaze amesema, TRA inapoadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1996, inavijunia mwamko mkubwa walionao wananchi katika kulipa kodi kwa hiari. 

Sambamba na hilo, Mamlaka inajivunia namna serikali inavyotumia vyema kodi zinazokusanywa katika kuboresha huduma za jamii, kukuza maendeleo na ustawi wa wananchi, huku mapato ya ndani yakitegemewa kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwa asilimia 74.2 katika bajeti ya mwaka 2026/2027, jambo ambalo ni la kihistoria katika nchi yetu.

Kimsingi, TRA imepata mafanikio makubwa katika utendajikazi wake hasa baada ya kufuata maelekezo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ambaye ameonya matumizi ya mabavu katika ukusanyaji wa kodi huku akihimiza uwepo wa mazungumzo pindi mlipakodi anapokwama kulipa kodi kwa wakati.
Posted by MROKI On Friday, June 26, 2026 No comments

June 25, 2026













Na, Mwandishi Wetu – Dodoma
SERIKALI imesema itaendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali ambayo yamekuwa yakigharimu maisha ya watu, kuharibu mali na kurudisha nyuma maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewa hii leo 25 Juni, 2026 na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko, wakati akifunga Jukwaa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa lililojadili Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na Madhara ya El Niño Jijini Dodoma.

Amesema Tanzania imeendelea kukabiliwa na matukio ya maafa yanayosababisha athari kubwa kwa wananchi na uchumi wa Taifa, hali inayolazimu kuwepo kwa maandalizi madhubuti ya kukabiliana na changamoto hizo kabla hazijatokea.

“Nchi yetu imekuwa ikishuhudia matukio ya majanga ambayo yamekuwa yakisababisha maafa na kuathiri mfumo wa kawaida wa maisha ya jamii. Majanga hayo yamesababisha vifo, ulemavu wa kudumu, upotevu wa mali na uharibifu wa miundombinu,” amesema Dkt. Kilabuko.

Amesema kufuatia taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ya Aprili 28, 2026 kuhusu uwezekano wa kujitokeza kwa hali ya El Niño, Ofisi ya Waziri Mkuu imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura kwa ajili ya kuzuia na kukabiliana na madhara yanayoweza kutokea kuanzia Agosti 2026 hadi Juni 2027.

Kwa mujibu wa Dkt. Kilabuko, rasimu hiyo imejadiliwa na wadau mbalimbali ili kuiboresha kwa kuzingatia uzoefu uliopatikana wakati wa matukio ya El Niño yaliyowahi kutokea nchini, hususan ya mwaka 2023/2024.

Amesema ushirikishwaji wa wadau ni hatua muhimu itakayoiwezesha Serikali kuwa na mpango shirikishi na unaotekelezeka katika kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali endapo maafa yatatokea.

“Ni vema kushiriki kikamilifu na kutoa maoni yetu huku tukijielekeza kwenye athari tarajiwa na hatua za kuchukua ili kuwa na mpango thabiti utakaoiwezesha Serikali na wadau kuchukua hatua stahiki za kuzuia au kupunguza madhara,” amesema.

Aidha, ameeleza imani yake kuwa jukwaa hilo litatoa mchango mkubwa katika kuimarisha ufanisi wa usimamizi wa maafa nchini na kuongeza uwezo wa taasisi mbalimbali kukabiliana na changamoto za majanga.

Dkt. Kilabuko amesisitiza kuwa usimamizi wa maafa haupaswi kuonekana kama jukumu la taasisi chache pekee, bali unapaswa kujumuishwa katika mipango ya maendeleo na utekelezaji wa shughuli za kila siku za wizara, taasisi na mamlaka za serikali za mitaa.

Amesema hatua hiyo itasaidia kujenga jamii yenye uwezo wa kuhimili majanga na kulinda maendeleo yaliyopatikana nchini dhidi ya athari zinazoweza kusababishwa na hali ya El Niño na majanga mengine.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala amesema kuwa,Jukwaa hilo ni muhimu na lipo kisheria hivyo litumike kwa manufaa na kuzingatia umuhimu wake.

Aidha alitumia nafasi hiyo kuzikumbusha kamati za maafa ngazi zote kuendelea kujiandaa na kukabiliana na maafa pindi yanapotokea kwa kuendelea kuweka mipango madhubuti ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza hasa yale ya uharibifu wa miundombinu na kuepuka madhara mengine kwa jamii na Taifa kwa Ujumla.
Posted by MROKI On Thursday, June 25, 2026 No comments
IMG_6244.JPG
Benki ya NMB imetangaza udhamini wa Sh milioni 150 kufanikisha msimu wa nane wa Mashindano ya Kombe la Mkuu wa Majeshi—CDF Cup 2026—yatakayofanyika Dar es Salaam kuanzia Julai 6 hadi 17.

Mashindano hayo yatahusisha michezo 13 na timu kutoka Kamandi ya Makao Makuu ya JWTZ, Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu, Kamandi ya Jeshi la Anga, Kamandi ya Jeshi la Wanamaji, Kamandi ya Jeshi la Akiba na Kamandi ya Jeshi la Kujenga Taifa.

Mkuu wa Idara ya Wateja Binafsi wa Benki ya NMB, Aikansia Muro, alisema udhamini huo unaendeleza ushirikiano wa benki hiyo na majeshi katika kukuza michezo, kuimarisha ushindani na kujenga umoja, afya thabiti na mshikamano miongoni mwa washiriki.

Mashindano yatafunguliwa Julai 6 katika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, huku yakitarajiwa kutoa jukwaa la kukuza vipaji, kuimarisha utimamu wa mwili na afya ya akili pamoja na kujenga mahusiano mema kwa washiriki.

Mkuu wa Idara ya Wateja Binafsi wa Benki ya NMB, Aikansia Muro (kushoto), akikabidhi hundi mfano ya udhamini wa Sh milioni 150 kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya CDF Cup 2026, Brigedia Jenerali Saidi Hamis Saidi (katikati), jijini Dar es Salaam.

Mashindano hayo yatafanyika kuanzia Julai 6 hadi 17, yakishirikisha timu za kijeshi katika michezo 13.
IMG_6259.JPG
IMG_6246.JPG

IMG_6247.JPG

IMG_6248.JPG

IMG_6250.JPG

IMG_6251.JPG

IMG_6253.JPG

IMG_6254.JPG

IMG_6255.JPG

IMG_6257.JPG

IMG_6258.JPG

IMG_6245.JPG
Posted by MROKI On Thursday, June 25, 2026 No comments
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hania Bwahama akimuelezea Mshiriki wa mkutano mkuu wa tatu wa Kimataifa wa kikanda PEN-PLUS (ICPPA 2026) kutoka nchini Nigeria Mya Nyon vifaa vinavyotumika wakati wa upasuaji wa moyo alipotembelea banda la JKCI lililopo katika mkutano huo unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) kilichopo jijini Dar es Salaam.
Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Alex Msoka akimuelezea Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu kwa Umma Dkt Rahma Hingora kuhusu kampeni ya Jua Namba Zako inayofanywa na Taasisi hiyo alipotembelea banda la JKCI wakati wa mkutano mkuu wa tatu wa Kimataifa wa kikanda PEN-PLUS (ICPPA 2026) unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) kilichopo jijini Dar es Salaam.
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hania Bwahama akimuelezea mtaalamu wa afya kutoka nchini Afrika Kusini Roylah Rykiel kuhusu huduma za upasuaji wa moyo zinazotolewa na Taasisi hiyo wakati wa mkutano mkuu wa tatu wa Kimataifa wa kikanda PEN-PLUS (ICPPA 2026) unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) kilichopo jijini Dar es Salaam.
**************
Watalaamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wameshiriki katika mkutano mkuu wa tatu wa Kimataifa wa kikanda PEN-PLUS (ICPPA 2026) ili kujadili changamoto mbalimbali zinazokwamisha mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza na kufikia maamuzi ya pamoja yatakayosaidia kufanikisha malengo ya afya kuelekea dira 2050.
Akizungumza wakati wa mkutano huo  Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Alex Msoka alisema mkutano huo umesaidia kuwakutanisha wadau mbalimbali  kutoka nchi za Afrika  kujadili kwa pamoja na kuweka mikakati ya kukabiliana na magonjwa hayo.
Dkt. Msoka alisema magonjwa yasiyoambukiza yanaongezeka kwa kasi katika Bara la Afrika jambo linalohitaji hatua za haraka na ushirikiano wa wadau mbalimbali katika kuyadhibiti.
“JKCI kama mdau katika mkutano huu tunashiriki kikamilifu katika kujadili changanmoto zilizopo na kutafuta suluhisho zake ili kuimarisha utoaji wa elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza kwani takwimu zinaonesha kuwa asilimia 35 ya vifo nchini vinatokana na magonjwa hayo”, alisema Dkt. Msoka.
Dkt. Msoka alisema kupitia mkutano huo JKCI imeweka banda la maonesho kuwaonesha wataalamu kutoka nchi washiriki wa mkutano huo huduma inazozitoa na namna ambavyo imeleta mabadiliko makubwa katika matibabu ya moyo Afrika Mashariki na Kati.
“Kumekuwa na changamoto nyingi zinazotokana na mtindo usiofaa wa maisha katika ukanda wetu kama vile kutokufanya mazoezi, matumizi ya pombe kupita kiasi na kutokufuata lishe bora, hizi ni miongoni mwa sababu kuu zinazochangia magonjwa yasiyoambukiza, hivyo sisi kama JKCI tunaendelea kupambana na magonjwa hayo katika jamii yetu”, alisema Msoka.
Baadhi ya washiriki wa mkutano huo waliotembelea banda la JKCI walipongeza jitihada za Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuboresha huduma za afya hususani huduma bingwa bobezi za magonjwa ya moyo.
“Huduma zinazotolewa na JKCI ni huduma za kiwango cha juu, naiomba Serikali iendelee kutoa elimu kwa wananchi wake hususani walioko vijijini ili wanapokumbana na changamoto za magonjwa ya moyo waweze kupata huduma kwa wakati”, alisema Padri Cosmas Mgina wa Kanisa la Anglikana Tanzania Dayosisi ya Dar es Salaam.
Kwa upande wake Daktari kutoka nchini Ghana Wallace Ollen alisema JKCI imekuwa mfano wa kuigwa barani Afrika kwa kutoa huduma za kibingwa bobezi za matibabu ya magonjwa ya moyo na mishipa ya damu.
“Naipongeza JKCI kwani upatikanaji wa huduma za matibabu ya moyo Barani Afrika umekuwa msaada mkubwa kwa wananchi wetu kwa kuwa sasa hatuna sababu ya kusafiri kwenda mataifa mengine kama India kupata matibabu bingwa ya moyo”, alisema Dkt. Ollen.
Posted by MROKI On Thursday, June 25, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo