Nafasi Ya Matangazo

March 15, 2026









Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imefanya ziara ya ukaguzi katika Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Mpomvu kilichopo mkoani Geita tarehe 15 Machi 2026, ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya Nishati inayolenga kuimarisha upatikanaji wa umeme nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu amesema ziara hiyo imelenga kukagua maendeleo ya miradi ya nishati pamoja na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa na Serikali unaleta matokeo yaliyokusudiwa kwa wananchi.

“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini tuna jukumu la kuisimamia Wizara ya Nishati ili kuhakikisha inatekeleza majukumu yake kikamilifu. Tumeridhishwa na uwekezaji uliofanywa katika kituo hiki ambacho kina mchango mkubwa katika kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na shughuli za kiuchumi,” amesema Mhe. Mgallu.

Ameongeza kuwa Kituo hicho kina uwezo wa kupokea na kusambaza takribani megawati 90, huku jitihada zikiendelea kuboresha miundombinu ya usambazaji wa umeme ikiwemo mpango wa kuongeza laini maalum kwa ajili ya Mgodi wa dhahabu wa Geita (GGM).

“Mahitaji ya umeme ya mgodi wa GGM yanatarajiwa kufikia takribani megawati 70 ifikapo mwaka 2035 kutoka megawati 36 zinazotumika kwa sasa, hivyo ni muhimu kuendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa umeme ili kukidhi mahitaji hayo,” ameongeza.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya umeme katika Mkoa wa Geita kutokana na ukuaji mkubwa wa shughuli za kiuchumi na kijamii hususan katika sekta ya madini.

“Kituo hiki kina mchango mkubwa katika kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Geita pamoja na maeneo ya jirani ikiwemo Biharamulo na Ngara mkoani Kagera, Sengerema mkoani Mwanza na Kakonko mkoani Kigoma,” amesema Mhe. Salome. 

Naibu Waziri wa Nishati  ameongeza kuwa  Kituo cha Mpomvu kimegharimu takribani shilingi bilioni 50, uwekezaji ambao umeongeza uwezo wa usambazaji wa umeme katika eneo hilo linalokua kwa kasi kiuchumi ambapo mahitaji ya sasa ya umeme yamefikia Megawati 73.64. 

Awali, Mkoa wa Geita ulikuwa ukipokea umeme kutoka Mkoa wa Shinyanga wenye uwezo wa takribani megawati 4 pekee, kiwango ambacho hakikukidhi mahitaji ya umeme yaliyokuwa yakiongezeka kutokana na shughuli za kiuchumi hususan uchimbaji wa madini.

Kituo cha Kupokea na Kupoza umeme cha  Mpomvu kilianza kujengwa mwaka 2019 na kukamilika mwaka 2020, kabla ya kuzinduliwa rasmi mwaka 2022 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Posted by MROKI On Sunday, March 15, 2026 No comments







Na Eleuteri Mangi, Rombo, Kilimanjaro
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imeridhishwa na kazi ya uimarishaji wa mpaka wa Kimataifa kati ya Tanzania na Kenya ambapo Km 564 sawa asilimia 75 tayari zimewekewa alama kati ya km 758 za mpaka mzima wa nchi kavu.

Akizungumza wakati wa ziara ya kamati hiyo eneo la Holili, wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Mhe. Timotheo Mzava amesema kazi ya kuweka alama kwenye mipaka sio kazi ndogo na kuipongeza wizara ya ardhi kwa kazi kubwa iliyofanya.

“Kipekee kwenye mpaka huu, ukisimama hapa unaona mpaka kule juu unaona alama zimewekwa, hii ni kazi kubwa imefanyika, nawapongeza wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya”, amesema Mzava.

Aidha, Kamati imeitaka Serikali kukamilisha kazi ya uimarishaji mpaka huo wa kimataifa kati ya Tanzania na Kenya huku ikitarajia kuona mipango ya kifedha na bajeti inayoonesha mwelekeo na nia ya dhati ya kukamilisha kazi hiyo kwenye bajeti ya sasa na inayokuja katika  mwaka wa fedha 2026/2027.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Kaspar Mmuya amewataka wataalamu wa Wizara ya ardhi  kuendelea kutoa elimu kwa wananachi wa maeneo ya mipakani kwa lugha ile ile ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili waelewe na kuwa sehemu ya ulinzi wa mipaka ya nchi.

“Dhana kubwa hata kwenye Katiba ya nchi inasema, hata mwananchi mwenyewe ana dhamana ya kulinda mipaka ya nchi yake. Ndiyo maana unapofanya kazi ya uimarishaji wa mipaka na ukiishi kwenye mipaka hii tunawahusisha wananchi kwa kutoa elimu kuwa wana dhamana ya kuilinda mipaka ya nchi yao”, amesisitiza Naibu Waziri Mmuya. 

Naye Mkuu wa Wilaya ya Rombo Mhe. Raymond Mwangwala ameiambia kamati hiyo ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii kuwa mpaka wa nchi hizo mbili uko  salama na wananchi wanaendelea na shughuli zao za kiuchumi na wana uhusiano mzuri na kuweka wazi kuwa wote walishiriki vizuri kwenye zoezi la kuweka alama kwenye mipaka.

Mpaka wa Tanzania na Kenya umekuwa ni eneo la mfano wa kuigwa kwenye ukanda wa Afrika kwa mujibu wa Taasisi ya Uimarishaji wa Mipaka Afrika inayojulikana kama African Union Border Program.
Posted by MROKI On Sunday, March 15, 2026 No comments

March 14, 2026

Na Wizara ya Madini
Kabla ya mwaka 2019, biashara ya madini ya dhahabu na vito nchini Tanzania, hususan kwa wachimbaji wadogo na wafanyabiashara, ilifanyika bila kuwepo kwa maeneo rasmi ya kukutana. Hali hiyo ilisababisha kutokuwepo kwa uwazi katika bei, udanganyifu katika vipimo na ubora wa madini, uwepo wa dhahabu bandia, pamoja na vitendo vya utoroshaji wa madini nje ya nchi, jambo lililosababisha wachimbaji na wafanyabiashara kupata hasara na Serikali kukosa mapato stahiki.

Mageuzi makubwa yalianza mwaka 2019 baada ya kufanyika marekebisho ya Sheria ya Madini mwaka 2017, ambayo yalipelekea kuanzishwa kwa soko la kwanza la Madini Geita likifutiwa na Chunya. Hatua hiyo iliweka msingi wa uwazi, usalama na uhakika wa biashara ya madini. Leo, Tanzania ina masoko 44 ya madini na vituo vidogo vya ununuzi wa madini 120 nchi nzima. 

Masoko haya yamekuwa mkombozi mkubwa kwa wachimbaji na wafanyabiashara kwa kuwapatia mahali salama pa kuuza, bei elekezi na ulinzi dhidi ya udanganyifu huku Serikali ikipata mapato yake stahiki.
Uwepo wa masoko ya madini na vituo vidogo vya ununuzi wa madini umepelekea wimbi kubwa la watanzania kuingia kwenye uchumi wa madini, hususan uchimbaji mdogo huku mifumo rafiki, uwazi na uhakika wa kisheria wa kuchimba na kufanya biashara vimeifanya Tanzania kuwa chaguo bora kwa wachimbaji wadogo barani Afrika na wageni kufika kujifunza.  

Tayari nchi kama Zambia, Malawi, Burundi, Uganda, Kenya na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo zimefika kujifunza kuhusu mfumo huo na hivi karibuni nchi ya Bukinafaso ilifika kujifunza.

Takwimu zinaonesha wazi mafanikio ya mfumo huo kabla na baada ya masoko kuanzishwa ambapo mwaka 2018/19 mauzo ya madini kupitia mfumo wa masoko yalifikia shilingi bilioni 8 kwa mwaka, ambapo awali fedha hizo zilipotea. 

Mwaka wa 2021/22 mapato kupitia masoko pekee yalifikia shilingi bilioni 264.09 na mwaka 2023/24 biashara ya thamani yenye shilingi trilioni 2.095 na trilioni 1.926 mtawalia ilifanyika kupitia masoko hayo. Hali hiyo inaonesha mwenendo chanya na endelevu wa mapato ya Serikali kupitia masoko ya madini.

Mathalani, Mkoa wa kimadini Chunya, uwepo wa masoko ya Madini umeongeza chachu ya uzalishaji wa dhahabu ambapo Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Kimadini Chunya Mhandisi Laurent Mayalla akizungumza na Madini Diary anasema kuna ongezeko la shughuli za madini ambazo zimeleta mageuzi makubwa na hivyo kuchochea ukuaji wa sekta nyingine. Anasema uzalishaji wa madini ya dhahabu hivi sasa umefikia kilo 300 kwa mwezi kutoka kilo 5 zilizokuwa zikizalishwa kabla ya masoko.

Kupitia kodi na tozo mbalimbali, mapato haya yanarejea kwa wananchi kwa kugharamia huduma za jamii na miradi ya maendeleo jambo linaloifanya rasilimali  hii kuwa nguzo muhimu ya uchumi wa taifa kwa ujumla, na hii ndiyo tafsiri nyingine ya kauli kwamba: madini ni maisha na madini ni utajiri, uchumi na maendeleo.
Masoko ya Madini  Yachochea Maendeleo ya Halmashauri
Kutokana na umuhimu wa miundombinu hii, Serikali za Mitaa zimeendelea kuwekeza kwenye miundombinu ya masoko kutokana na manufaa yanayoonekana wazi kwa wananchi. Masoko yamezalisha ajira lukuki kwa vijana kupitia biashara, usajili na huduma mbalimbali. Mfano mdogo ni pale unapofika sokoni, unakutana na makundi ya vijana wakiwa na dhahabu mikononi, wakipokea kutoka kwa wachimbaji na wafanyabiashara kwa ajili ya kusajiliwa ili kuuzwa. Taswira hii inaonesha wazi kuwa masoko ya madini yameunda mnyororo mzima wa thamani, unaogusa wachimbaji, wafanyabiashara, vijana na Serikali kwa ujumla.

Kwa ujumla, masoko ya madini yamebadilisha taswira ya sekta kutoka biashara ya dhahabu na vito kiholela kwenda mfumo wa uwazi, unaosimamiwa kwa karibu na Serikali ambapo kila shilingi ya Tanzania inayoingia inaonekana. Si ajabu kuwa nchi nyingi za afrika zimekuja kujifunza uzoefu wa Tanzania na hii ndiyo tafsiri halisi kwamba madini ni maisha na madini ni utajiri.

Pia, ndiyo tafsiri kwamba Serikali inasikiliza na inapokaa mezani na wadau inachukua hatua kwa vitendo. kupitia Sera, mabadiliko ya mifumo na uanzishaji wa masoko ya madini, Serikali imehakikisha sekta ya madini inafikika kwa wachimbaji wadogo na wafanyabiashara, huku ikileta matokeo yanayoonekana wazi katika uwazi wa biashara, ongezeko la ajira na mapato ya taifa na usimamizi madhubuti.

Kwa mafanikio haya, masoko ya madini yanaendelea kudhihirisha kuwa rasilimali za madini si tu chanzo cha mapato, bali pia ni daraja la fursa, ajira na maendeleo kwa watanzania wengi.
Posted by MROKI On Saturday, March 14, 2026 No comments

March 13, 2026










Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imelipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa usimamizi na utekelezaji mzuri wa Mradi wa Uzalishaji Umeme kwa nguvu ya Jua wa Kishapu wenye uwezo wa Megawati 50 unaotekelezwa katika Mkoa wa Shinyanga.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgallu, mara baada ya Kamati kutembelea mradi huo tarehe 13 Machi, 2026 kwa lengo la kujionea maendeleo ya utekelezaji wake pamoja na ufanisi wa matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Mhe. Mgallu alisema mradi huo ni hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya nishati nchini kutokana na matumizi ya teknolojia ya nishati jadidifu.

“Tumetembelea mradi huu wa uzalishaji wa umeme kwa kutumia teknolojia ya jua na tunaona ni mapinduzi makubwa katika sekta ya nishati nchini. Hii ni hatua muhimu kwani kwa mara ya kwanza Tanzania inapata Megawati 50 za umeme kutoka kwenye nishati ya jua,” alisema Mhe. Mgallu.

Alisema Kamati imeridhishwa na namna fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo zimetumika ipasavyo na kufanikisha utekelezaji wa mradi huo kwa ufanisi.

“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, tumeridhishwa na matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya mradi huu. Tunaona wazi kuwa fedha hizo zimetumika vizuri katika utekelezaji wa mradi huu wenye thamani ya takribani shilingi bilioni 118,” alieleza.

Aidha, alisema mradi huo tayari umeanza kuchangia Megawati 50 katika Mfumo wa Gridi ya Taifa, hatua inayochangia kuongeza uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini pamoja na kuimarisha vyanzo mseto vya nishati.

“Utekelezaji wa mradi huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kunakuwa na vyanzo mbalimbali vya kuzalisha umeme. Hii inaongeza uhakika wa upatikanaji wa nishati ya umeme nchini,” alisema.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, alisema mradi wa Kishapu unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme katika Gridi ya Taifa.

“Mradi huu una awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme kwenye Gridi ya Taifa. Awamu ya pili itahusisha uzalishaji wa Megawati 100 zaidi na kufanya jumla ya Megawati 150 kutoka katika mradi huu,” alisema Mhe. Ndejembi.

Kamati hiyo imetoa Rai kwa Wizara ya Nishati na TANESCO  inaendelea kuendelea na  mikakati ya kuanza utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo ili kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini.
Posted by MROKI On Friday, March 13, 2026 No comments

March 12, 2026











Na Mwandishi wetu, Tabora
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeridhishwa na Ujenzi wa Kiwanda cha Zege kinachomilikiwa na kampuni tanzu ya TANESCO ya  kuzalisha nguzo za zege  kilichopo katika Mkoa wa Tabora wakati wa ziara yao ya kikazi Mkoani humo tarehe 12 Machi, 2026.

Akizungumza baada ya ziara hiyo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu ameeleza kuridhishwa na   hatua ya kukamilika kwa Kiwanda hicho kilichoanza uzalishaji  na kuwaelekeza Wizara ya Nishati  na TANESCO kukisimamia kiwanda hiko kiendelee kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kuzalisha faida.

"Kwa niaba ya Kamati tumeridhika na kazi kubwa iliyofanyika katika kiwanda hiki ambacho kimekamilika na uzalishaji umeanza, tunatoa rai kwa Wizara na TANESCO kuendelea kusimamia kiwanda hiki ili kiendelee kufanya kazi yake kwa ufanisi zaidi", alieleza Mhe. Mgallu

Alieleza kuwa uelekeo wa sasa ni kusambaza nguzo za zege hasa kwa maeneo yenye unyevu sambamba na maeneo yaliyo karibu na misitu pamoja na mikondo ya mito ya maji ambayo nguzo za miti huathirika kwa kiasi kikubwa haswa kwenye msimu wa mvua hivyo nguzo za zege zitakuwa msaada mkubwa katika mazingira kama hayo na  kuboresha upatikanaji wa huduma ya umeme.

“Kama mnavyofayahamu kwa sasa uelekeo ni kusambaza nguzo za zege badala ya nguzo za miti hasa katika maeneo ambayo yana asili ya unyevu, maeneo karibu na mito ya maji ama visiwa ambapo nguzo za miti huathiriwa na mazingira hayo”, aliongeza. 

Naye Mhe. Deogratius Ndejembi Waziri wa Nishati alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hiko umekamilika mwaka huu na kuanza uzalishaji wake rasmi Februari, 2026 ambapo mpaka sasa wastani wa nguzo zinazozalishwa ni 80 hadi 120 kwa siku ambapo mpaka sasa gharama ya shilingi bilioni 6.4 imeshatumika katika hatua zote hadi uzalishaji ulipoanza ambapo kiasi cha shilingi bilioni 1.4 bado hazijalipwa kwa mkandarasi ambaye bado yupo kwenye kipindi cha uangalizi.

“Kiwanda hiki kilianza uzalishaji rasmi mwezi Februari mwaka huu ambapo kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha nguzo 80 hadi 120, mpaka sasa ujenzi wa kiwanda hiki hadi uzalishaji ulipoanza imetumia gharama ya shilingi bilioni 6.4 ambapo bado kuna billioni 1.6 bado haijalipwa kwa mkandarasi kwa kuwa yupo kwenye kipindi cha uangalizi”, aliongeza Mhe. Ndejembi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange ameeleza kuwa kukamilika kwa kiwanda hiko kunaenda kuleta mageuzi makubwa kwani nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo Shirika bado linaendelea kuikuza sekta  na kuwa na utoshelevu wa nguzo zenyewe kwa matumizi ya wananchi. 

“Baada ya kukamilika kwa ujenzi wa kiwanda na kuanza uzalishaji ambapo kwa hali ilivyo ya matumizi ya nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo kama Shirika tutahakikisha tunaisimamia sekta hii ili kuendelea kuwapatia wateja wetu huduma ya umeme wa uhakika”, alisema Bw. Twange. 

Ziara hiyo ya kamati ya kudumu ya bunge ya nishati na madini inalenga kufanya ukaguzi wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Shirika katika maeneo mbalimbali nchini ili kujionea ufanisi wake.
Posted by MROKI On Thursday, March 12, 2026 No comments
Waziri Mkuu, Dkt, Mwigulu Nchemba akifunga Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili  ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji kwenye ukumbi wa Kambarage - Hazina jijini Dodoma, Machi  11, 2026.
Washiriki wa Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili  ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji wakimsikiliza Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba alipofunga mkutano huo kwenye ukumbi wa Kambarage - Hazina jijini Dodoma, Machi 11, 2026.
Washiriki wa Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili  ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji wakimsikiliza Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba alipofunga mkutano huo kwenye ukumbi wa Kambarage - Hazina jijini Dodoma, Machi 11, 2026.
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Wakuu wa Mikoa na watendaji wao katika mikoa yote nchini wajipange kutoa taarifa kuhusu uwekezaji na ukuzaji wa biashara kwenye mikoa yao kila wanapotoa taarifa kwa viongozi wa kitaifa.
 
“Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala na Wakurugenzi wa Halmashauri mbebe jukumu la kuwa mabalozi wa kwanza wa uwekezaji katika maeneo yenu kwa kutambua na kutangaza fursa mbalimbali zilizopo katika maeneo yenu.”
 
“Tubebe hili jukumu, kila Mkuu wa Mkoa anapotoa taarifa atapaswa aseme ameongeza uwekezaji kwa kiasi gani, amekuza biashara kwa kiasi gani na katika kuongeza biashara mpya
 
Ametoa wito huo leo jioni (Jumatano, Machi 11, 2026) wakati akifunga Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (Mkumbi II) uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage, HAZINA, jijini Dodoma.
 
Amesema mapendekezo yote yaliyowasilishwa na washiriki wa mkutano huo ambao ni Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa pamoja na Wakurugenzi yaandaliwe katika mfumo wa mkakati wa utekelezaji ili kuwezesha utekelezaji wake kwa ufanisi.
 
“Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alishasema isiwepo sheria inayoleta kikwazo katika utendaji kazi wa serikali. Haya tuliyoyabaini, tuyaweke kwenye majedwali na kubainisha lipi ni kikwazo na lipi limefanyika. Leteni hayo mapendekezo.”
 
“Kuhusu suala la utitiri wa taasisi za udhibiti na kodi, andaeni mapendekezo mahsusi na yawasilishwe kwa Waziri wa Fedha ili yaweze kuingizwa katika Muswada wa Sheria ya Fedha (Finance Bill) wa mwaka huu. Hatua hii inalenga kuwa sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha mazingira ya uwekezaji nchini,” amesema.
 
Pia amezitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa zihakikishe zinaondoa urasimu katika kuanzisha biashara mpya au viwanda vipya katika maeneo yao. “Kufanya hivyo, kutasaidia kuchochea upatikanaji wa ajira mpya kwa vijana, kukuza kipato kwa wawekezaji na wafanyabiashara pamoja na kukuza pato la Taifa.”
 
Amezitaka mamlaka hizo ziweke mikakati ya kushughulikia changamoto mbalimbali zikiwemo za tozo zisizo rafiki kwa sekta binafsi. “Ni dhahiri kuwa Serikali pekee haiwezi kufanikisha malengo haya bila ushiriki mpana na madhubuti wa sekta binafsi,” amesema.
 
Mapema, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo aliwashukuru Wakuu wa Mikoa yote kwa ushirikiano wao na jinsi walivyolipa kipaumbele suala la uwekezaji kwenye maeneo yao.
 
Alisema ofisi yake kwa kushirikiana na Waziri wa Nchi, OWM – TAMISEMI wanaandaa nyenzo za kushindanisha mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa (Ease of Doing Competitive Business) katika kuvutia uwekezaji na kulinda biashara.
 
“Kupitia hii kila mkoa utapimwa jinsi wanavyowezesha biashara na kuvutia uwekezaji ili kuona wanakuza vipi biashara katika maeneo yao. Na watapimwa ufanisi wao kila mwaka mara moja,” alisema.
 
Naye, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar aliwaeleza washiriki wa mkutano huo kwamba matarajio ya Serikali kwenye utekelezaji wa DIRA 2050 unaendana na MKUMBI II kwenye maeneo yao.
 
“Uchumi wa nchi yetu kwa sasa ni dola za Marekani bilioni 100 tukichanganya uzalishaji wa bidhaa zetu zote, huduma na biashara za ndani na za nje angalau kwa hesabu za mwaka jana. Katika miaka 25 ijayo, tunataka tufikie dola za Marekani trilioni moja, maana yake tukue zaidi ya mara 10.”
 
“Ili tufike huko hatupaswi kwenda kama ilivyo sasa, tunapaswa kubadilika sana na tuongeze bidii siyo tu uchumi ukue bali uwe wa kisasa pia,” alisema.
 
Posted by MROKI On Thursday, March 12, 2026 No comments

March 11, 2026






Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Ndg. Asha-Rose Migiro,leo tarehe 11 Machi 2026 amefanya mazungumzo jijini Dodoma na Balozi Parfait Onanga-Anyanga, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika na Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa iliyopo Addis Ababa (UNOAU).

Balozi Onanga-Anyanga yupo nchini Tanzania kwa nafasi yake kama
Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe.António Guterres.

Kikao hicho ni sehemu ya mashauriano ya Mjumbe huyo na wadau mbalimbali wa kitaifa kwa lengo la kubadilishana mawazo kuhusu mustakabali wa kisiasa kufuatia Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025, pamoja na juhudi pana za kuimarisha amani, demokrasia na mshikamano wa kitaifa nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Ndg. Asha-Rose Migiro alisisitiza dhamira ya muda mrefu ya Tanzania katika kuendeleza utawala wa kidemokrasia, ushiriki wa kisiasa kwa njia ya amani na kuheshimu utawala wa sheria.

Alibainisha kuwa Tanzania inaendelea kuongozwa na misingi ya Mkataba wa Umoja wa Afrika wa Demokrasia, Uchaguzi na Utawala Bora, pamoja na viwango vya kimataifa vilivyowekwa katika Tamko la kimataifa la Haki za Binadamu na Mkataba wa kimatifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa.

Katibu Mkuu pia alieleza kuhusu mageuzi ya kisheria katika Tume ya Uchaguzi na taasisi nyingine yaliyofanyika kwa lengo la kuimarisha mfumo wa uchaguzi, ikiwa ni pamoja na kutungwa kwa sheria mpya za uchaguzi mwaka 2024 na hatua mbalimbali zilizolenga kuongeza uwazi, uwajibikaji na imani ya wananchi katika mchakato wa uchaguzi.

Mazungumzo hayo pia yaligusia matukio ya vurugu yaliyojitokeza katika baadhi ya maeneo nchini wakati na baada ya uchaguzi, ambayo yalisababisha upotevu wa maisha na uharibifu wa mali, ikiwemo mashambulizi dhidi ya ofisi za CCM. Ilibainishwa kuwa hatua stahiki zilichukuliwa kurejesha hali ya utulivu na amani nchini.

Pande zote mbili zilisisitiza umuhimu wa kuendelea kwa mazungumzo na maridhiano miongoni mwa wadau wa kitaifa. Hali kadhalika Katibu Mkuu wa CCM alimthibitishia Balozi Onanga-Anyanga kuwa Tanzania itaendeleza uhusiano wake na jumuiya ya kimataifa katika kuimarisha amani, usalama na maendeleo jumuishi.

CCM imepongeza ushirikiano madhubuti uliopo kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa na kuthibitisha dhamira yake ya kustawisha umoja wa kitaifa, utulivu na demokrasia katika Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.
Posted by MROKI On Wednesday, March 11, 2026 No comments

March 09, 2026





Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Asha-Rose Migiro, leo Jumatatu,Machi 9,2026, amefungua rasmi mafunzo maalum ya Uongozi na Utawala Bora kwa viongozi na watendaji waandamizi wa Chama yanayofanyika katika Ukumbi wa Mount Royal, Mkoani Iringa.

Mafunzo hayo ya siku nne yameandaliwa na Jitegemee Holdings Company Limited (JHCL) kwa kushirikiana na Taasisi ya Wakurugenzi Tanzania (IoDT), na yanawaleta pamoja wajumbe wa Bodi, Menejimenti ya Jitegemee Holdings pamoja na viongozi waandamizi wa CCM.

Akifungua mafunzo hayo, Dkt. Migiro amesema kuwa uongozi na utawala bora ni msingi muhimu wa kuimarisha taasisi na kuendeleza maendeleo ya Taifa, akisisitiza kuwa mafunzo hayo yanaendana na utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa 2025 pamoja na maono ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Aidha, amewataka washiriki kutumia fursa ya mafunzo hayo kujenga uwezo wa kiuongozi na kuhakikisha maarifa watakayopata yanatumika kuimarisha utendaji wa taasisi wanazoziongoza.





Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo