Nafasi Ya Matangazo

April 16, 2026


Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema Serikali inaendelea na Marekebisho ya Mfumo wa Kidigitali wa  Leseni za Utafiti wa Madini utakaosimamia hatua zote za utoaji na usimamizi wa leseni hizo.

Amesema mfumo huo utahusisha utoaji wa leseni, uwasilishaji wa taarifa za kila robo mwaka, utoaji wa hati za makosa, na hata kufutwa kwa leseni pale inapobidi bila kuhitaji uingiliaji wa moja kwa moja wa binadamu.

“Baada ya mfumo huu kukamilika, hamtaniona tena natangaza kufuta leseni. Leseni itajiondoa yenyewe kupitia mfumo huu. Mfumo utakuletea taarifa zote muhimu, utakukumbusha muda wa kuwasilisha taarifa, utatoa hati za makosa pale inapobidi, na hatimaye utafuta leseni wenyewe moja kwa moja endapo masharti hayatatekelezwa,” amesisitiza Waziri Mavunde.

Mhe. Mavunde ameyasema hayo Aprili 16, 2026, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Morning Trumpet kinachorushwa na runinga ya UTV. Ameongeza kuwa leseni za utafiti ni msingi muhimu wa kuibua migodi mikubwa na ya kati, na kwamba maeneo yanayoshikiliwa bila kuendelezwa yanaikosesha Serikali mapato, ajira, pamoja na fursa katika mnyororo mzima wa thamani wa Sekta ya Madini.

Ameeleza hayo kufuatia uamuzi wake wa Aprili 15, 2026, wa kuielekeza Tume ya Madini kufuta leseni 40 za utafiti wa madini zenye jumla ya eneo la kilomita za mraba 900 (sawa na hekari 188,163), baada ya wamiliki wake kushindwa kutekeleza masharti ya leseni licha ya kupewa hati za makosa.

Aidha, Waziri Mavunde amesema Serikali imejipanga kuimarisha usimamizi wa Sheria ya Madini kwa kuondoa tabia ya mazoea iliyokuwepo kwa muda mrefu, akisisitiza kuwa sekta hiyo inahitaji wawekezaji wenye dhamira ya dhati ya kuendeleza rasilimali za madini kwa manufaa ya taifa.

“Sekta ya Madini kuchangia asilimia 10.1 kwenye pato la taifa si jambo dogo. Tanzania tumepiga hatua kubwa. Fikiria kama tafiti kwenye leseni hizi zingekamilika tungekuwa na migodi mingapi mikubwa na ya kati?” amehoji.

Katika hatua nyingine, ametoa wito kwa vijana wanaopenda kuingia katika sekta ya madini kujiunga na kuanzisha vikundi rasmi ili waweze kufikiwa kwa urahisi na Serikali kupitia programu maalum ya Mining For A Brighter Tomorrow, inayolenga kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kupata leseni, mitaji na vifaa vya uchimbaji.
Posted by MROKI On Thursday, April 16, 2026 No comments

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, akimpongeza na kumshukuru Mkurugenzi Mkuu wa Viwanja vya Ndege (TAA) Bw. Abdul Mombokaleo kwa kujitolea computer zenye thamani ya shilingi milioni 170 kama mchango wake yeye na Alumni  wengine kwa kuboresha elimu ya Sayansi katika shule hiyo.

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, akupewa maelezo juu ya  mradi wa jengo la maabara ya TEHAMA ambayo  ni ‘Smart Class’ alipokuwa Mgeni rasmi katika  Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (KSS) kama mgeni rasmi, katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani.
Sehemu ya wahitimu wa kidato cha sita katika Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (K katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani.

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, akiwatambulisha baadhi ya Alumni walio katika kamati ya   mradi wa ujenzi wa  jengo la maabara ya TEHAMA ambayo  ni ‘Smart Class’ katika  Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (KSS) kama mgeni rasmi, katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani. Kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Viwanja vya Ndege (TAA) Bw. Abdul Mombokaleo, akifuatiwa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO Nchini Prof. Hamisi Malebo.

(Picha na Habari na Issa Michuzi)

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, akikagua na kupewa maelezo juu ya  maabara ya TEHAMA ambayoni ‘Smart Class” na Mkuu wa Shule hiyo alipokuwa Mgeni rasmi katika n Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (KSS) kama mgeni rasmi, katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani.
*************
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatano, Aprili 15, 2026, amehudhuria Mahafali ya 59 ya Shule ya Sekondari Kibaha (KSS) kama mgeni rasmi, katika hafla iliyofanyika shuleni hapo, Tumbi, Kibaha Mji, mkoani Pwani.
 
Akiwa katika mahafali hayo, Dkt. Kikwete amezindua harambee ya kuchangia ujenzi wa jengo la ghorofa la maabara ya TEHAMA na masomo mengine, ambalo linatarajiwa kugharimu shilingi bilioni 3.
 
Amesema ujenzi huo ni muhimu katika kuendeleza ubunifu na uwezo wa wanafunzi katika masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM).
 
 
Aidha, Dkt. Kikwete amekubali kuwa mlezi wa kamati ya kukusanya michango kwa ajili ya mradi huo mkubwa ambao kwa sasa umefikia hatua ya msingi.
 
Pia, Rais Mstaafu ameishukuru jumuiya ya wanafunzi wa zamani (alumni) wa shule hiyo, wakiuongozwa na  Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Bw. Abdul Mombokaleo, kwa kuchangia kompyuta zenye thamani ya Shilingi Milioni 170 kwa ajili ya “Darasa Janja” (Smart Class) lililoanzishwa shuleni hapo.
 
Darasa hilo litakuwa ni kituo cha mafunzo kwa wanafunzi wa shule hiyo na shule nyingine zitakazounganishwa kupitia mfumo wa mtandao, ambapo mwalimu anaweza kufundisha madarasa yaliyoko nje ya Kibaha kwa wakati mmoja kwa njia ya kidigitali.
 
Katika ziara yake, Dkt. Kikwete alipata fursa ya kutembelea na kukagua Darasa Janja hilo, akipokea maelezo kutoka kwa Mkuu wa Shule kuhusu namna teknolojia hiyo inavyotumika kuboresha mbinu za ufundishaji na ujifunzaji shuleni hapo.
 
Shule ya Sekondari Kibaha, inayomilikiwa na Shirika la Elimu Kibaha na kusimamiwa na Kurugenzi ya Hud uma za Elimu, ilianzishwa mwaka 1965 kupitia ushirikiano kati ya Serikali ya Tanganyika ya wakati huo na nchi za Nordic – Denmark, Finland, Norway, na Sweden. Wakati inaanzishwa, shule ilikuwa na wanafunzi 110 wa Kidato cha Kwanza na 60 wa Kidato cha Tano.
 
Kwa sasa, shule hiyo ya bweni kwa wavulana ina uwezo wa kuchukua zaidi ya wanafunzi 800 na imeendelea kuwa miongoni mwa taasisi kongwe na zenye heshima kubwa katika sekta ya elimu nchini.
 
Dkt. Kikwete ni miongoni mwa alumni mashuhuri wa Shule ya Sekondari Kibaha, alikosoma zaidi ya miaka 60 iliyopita. Wengine waliopitia shule hiyo ni pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mkurugenzi Mkuu wa ATCL Bw. Peter Ulanga, Balozi Lazaro Nyalandu, Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO Nchini Prof. Hamisi Malebo, Mkurugenzi Mkuu wa Viwanja vya Ndege Bw. Abdul Mombokaleo, na Mwenyekiti Mstaafu wa CHADEMA Mhe. Freeman Mbowe, miongoni mwa wengine wengi.
 
Aidha, kwa kutambua mchango mkubwa wa alumni wake, Shule ya Sekondari Kibaha inaendelea kuimarisha ushirikiano na wadau wa elimu ili kuhakikisha inaendelea kuwa kinara katika utoaji wa elimu ya ubora nchini.
Posted by MROKI On Thursday, April 16, 2026 No comments

April 15, 2026




Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndg. Asha-Rose Migiro, leo tarehe 15 Aprili 2026 amefanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Malawi, Mhe. Lazarus Chakwera, katika Ofisi za CCM Lumumba, jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalijikita katika hali ya kisiasa nchini pamoja na matukio ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

Mhe. Chakwera yupo nchini Tanzania kwa ziara maalum katika nafasi yake kama Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mhe. Shirley Ayorkor Botchwey. 

Kikao hicho ni sehemu ya mashauriano yake na wadau mbalimbali wa kitaifa kwa lengo la kubadilishana mawazo kuhusu maendeleo ya kisiasa baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba 2025, pamoja na juhudi zinazoendelea za kuimarisha amani, demokrasia na mshikamano wa kitaifa nchini Tanzania.
Posted by MROKI On Wednesday, April 15, 2026 No comments



Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde ameielekeza Tume ya Madini kufuta jumla ya leseni 40 za utafiti wa madini ambao wameshindwa kuendeleza leseni hizo kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa rasilimali za madini na kuondoa wamiliki wasiotekeleza masharti ya leseni, huku akionya kuwa Serikali haitavumilia uzembe unaokwamisha maendeleo ya Sekta ya Madini pamoja na uchumi kwa ujumla.

Waziri Mavunde ametangaza uamuzi huo leo Aprili 15, 2026 jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari, akieleza kuwa leseni hizo zimefutwa baada ya wamiliki wake kushindwa kuziendeleza licha ya kupewa hati za makosa na muda wa kurekebisha kasoro zilizobainika na kwamba zitarudishwa Serikalini kwa ajili ya  kuweka utaratibu wa kugawa kwa wachimbaji wadogo,wawekezaji walio na utayari na makundi ya Wanawake na Vijana kupitia Programu ya Mining for A Brighter Tomorrow-MBT. 

Amesema kuwa, tathmini ya kina iliyofanywa na Wizara ya Madini imeonesha uwepo wa ukiukwaji mkubwa wa masharti ya leseni, ikiwemo baadhi ya wamiliki kuhodhi maeneo bila kuyaendeleza, kushindwa kulipa ada stahiki, kutotekeleza wajibu wa ushirikishwaji wa Watanzania (Local Content), pamoja na kushindwa kutekeleza miradi ya uwajibikaji kwa jamii (CSR).

“Wapo waliokuwa wanamiliki leseni lakini hawafanyi uwekezaji wowote unaoonekana, wala kuthibitisha matumizi ya fedha katika kuendeleza maeneo yao. Hali hii hairuhusiwi kuendelea,” amesema Mavunde. 

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, vitendo vya kuhodhi leseni vimekuwa chanzo kikubwa cha migogoro na kuchochea uchimbaji holela, hali inayohatarisha usalama wa wananchi, mazingira na mapato ya Serikali.

“Hizi leseni 40 ni sawa na eneo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 900 sawa na  hekari  188,163” amesisitiza Mavunde.

Katika hatua nyingine, Serikali kupitia Tume ya Madini imetoa hati za makosa kwa leseni nyingine 43, zikiwemo leseni 40 za utafutaji na tatu za uchimbaji wa kati, huku wamiliki wake wakitakiwa kurekebisha kasoro ndani ya siku 30.

Waziri Mavunde amesisitiza kuwa endapo masharti hayo hayatatekelezwa ndani ya muda uliowekwa, leseni hizo zitafutwa na maeneo husika kutolewa kwa wawekezaji wengine wenye uwezo wa kuyaendeleza. 

Akizungumzia mwenendo wa matukio ya mlipuko wa maeneo yenye madini ya dhahabu “gold rush” katika maeneo mbalimbali nchini, Waziri Mavunde ametoa onyo kali kwa watu wanaovamia maeneo yenye leseni halali wakidai kufuata taarifa za uwepo wa madini.

Ameeleza kuwa uchimbaji wowote bila leseni ni kinyume cha sheria na hautavumiliwa, akibainisha kuwa vitendo hivyo vimesababisha migogoro kati ya wachimbaji na wamiliki halali, pamoja na uharibifu wa mazingira na hatari za kiafya.

Waziri Mavunde amebainisha kuwa Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kukabiliana na hali hiyo, ikiwemo, kudhibiti usalama wa wananchi na mali zao, kuzuia migogoro ya kimiliki, kulinda mazingira dhidi ya uchimbaji holela pamoja na kudhibiti milipuko ya magonjwa katika maeneo yenye msongamano mkubwa wa wachimbaji.

Aidha, Waziri Mavunde amekemea tabia inayoongezeka ya baadhi ya wachimbaji wadogo kuvamia maeneo yenye leseni halali, akieleza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote watakaokiuka sheria.

“Kuanzia sasa ni marufuku kuvamia maeneo ya leseni kwa sababu yoyote ile. Serikali haitasita kuwachukulia hatua kali wote watakaohusika,” amesisitiza Waziri Mavunde.

Hatua ya kufuta leseni 40 inaashiria msimamo thabiti wa Serikali wa kuendeleza Sekta ya Madini dhidi ya uzembe na vitendo visivyo halali, huku ikifungua ukurasa mpya wa uwajibikaji na ushindani wa haki katika matumizi ya rasilimali za taifa.
Posted by MROKI On Wednesday, April 15, 2026 No comments

April 14, 2026

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) ikiongozwa na Mwenyekiti wa Tume, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele leo Aprili 14, 2026 amekutana na kuzungumza na mjumbe maalum Jumuiya ya Madola (Commonwealth) Rais wa zamani wa Malawi Mhe.Lazarus McCarthy Chakwera ambaye alitembelea ofisi za Tume Njedengwa jijini Dodoma. Ziara hiyo maalum ya mjumbe huyo wa Jumuia ya Madola ililenga kuangalia namna Uchaguzi Mkuu wa 2025 ulivyofanyika. (Picha na INEC).







Posted by MROKI On Tuesday, April 14, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Dodoma 
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, ametoa maelekezo ya haraka kutatua mgogoro kati ya Kikundi cha Isunda (wamiliki wa leseni), wamiliki wa mashamba na wamiliki wa maduara katika kijiji cha Busulwagili, wilayani Kahama, Mkoani Shinyanga.

Maelekezo hayo yametolewa Aprili 14, 2026, katika ukumbi wa Tanzanite, Makao Makuu ya Madini, Dodoma, wakati wa kikao kilichowakutanisha wadau hao ili kusikiliza hoja na kupata suluhisho la uhalali wa umiliki na uzalishaji.

Amekiagiza Kikundi cha Isunda kusitisha mara moja shughuli zote za kuendelea na uchimbaji hadi wawasilishe muhtasari wa kikao utakaonesha makubaliano ya wazi kuhusu haki waliyopewa kwanza wenye maduara kuwekeza kabla mwekezaji mwingine kuendelea na uwekezaji kama ambavyo Kanuni ya 18A ya Haki Madini inavyoeleza.

Amefafanua kuwa Sheria ya Haki za Madini (kifungu 18A) inataka kama mwenye Leseni kaingiza wachimbaji wameweka maduara siku atakapopata  mwekezaji mwingine awape kwanza haki ya kwanza ya uwekezaji wenye maduara na si vinginevyo.

"Leseni ni kwa shughuli za uchimbaji pekee, siyo upangishaji, ukiukwaji wa taratibu wowote hautavumiliwa" amesema Mhe. Mavunde Ameongeza kuwa wamiliki wa leseni na maduara watalazimika kuingia mikataba rasmi ya ushirikiano kabla ya kuanza uchimbaji, ili kuzuia migogoro.

Hata hivyo, Waziri ameonya uongozi wa Kikundi  kuacha kutoa taarifa zisizo sahihi zinazoleta taharuki  kwa jamii inayopelekea migogoro kati ya wachimbaji wadogo na wamiliki wa leseni.

Aidha, ameielekeza Tume ya Madini Tanzania kutosaini mkataba wowote wa kiufundi hadi ijiridhishe, kuwa hakuna mgogoro kati ya wamiliki wote wa leseni na wachimbaji wa maduara .

" Itapelekwa timu ya wataalamu katika kila duara kutathmini uzalishaji, mrabaha wa Serikali na kuhakikisha uwazi na uwajibikaji." amesema Mhe. Waziri.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Madini, Dkt.Steven Kiruswa amesema kuwa ufumbuzi wa kudumu unategemea majadiliano ya uwazi yanayozingatia sheria, haki na maslahi ya pande zote.
Posted by MROKI On Tuesday, April 14, 2026 No comments
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali inatambua na kuthamini mchango wa wafanyakazi wa sekta ya umma na sekta binafsi katika kukuza uchumi na maendeleo ya Taifa.
 
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu ameyasema hayo jana jioni Aprili 13, 2026 jijini Dodoma katika Hafla ya Maandalizi ya Mei Mosi, 2026 ambayo Kitaifa inafanyika mkoani Njombe.
 
Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema Serikali inaendelea kuwaenzi wafanyakazi nchini kutokana na umuhimu wao mkubwa kwa Taifa.
 
Katika hafla hiyo ya awali, kiashi cha shilingi bilioni 1.105 kimekusanywa ambapo Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu alisema fedha hizo zitausaidia mkoa mwenyeji kukamilisha shughuli za maandalizi kwa ajili ya tukio hilo.
 
Mheshimiwa Waziri Mkuu aliongeza kwa kulipongeza Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (TUCTA) kwa ubunifu wa kuhakikisha maadhimisho ya Mei Mosi yanaacha alama katika mkoa mwenyeji.
 
“Wenzetu TUCTA wamekuja na ubunifu kwamba shughuli za Mei Mosi zinaacha alama katika mkoa husika kwa kutekeleza miradi mbalimbali kama walivyofanya katika maadhimisho ya mwaka 2025 mkoani Singida kwa kujenga uwanja wa Bombadia mkoani humo, uwanja ambao sasa umekuwa na manufaa makubwa kwa Wanasingida, na Njombe nako wamejiandaa kuacha alama kubwa.”  Alisema Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba.
 
Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mheshimiwa Deus Clement Sangu alisema maandalizi ya maonesho ya Mei Mosi mwaka huu yanaendelea vizuri akisisitiza kuwa kwa siku zilizosalia, maandalizi yote yatakamilika ndani ya wakati.
 
Naye Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mheshimiwa Anthony Mtaka alisema maadhimisho hayo ni fursa kubwa si tu kwa kwa mkoa wa Njombe, bali kwa mikoa yote ya kanda ya Nyanda za Juu Kusini kwani ugeni wa watu wasiopungua elfu tano unatarajiwa kushiriki sherehe za Mei Mosi Kitaifa mkoani humo.
 
Naye Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (TUCTA), Tumaini Nyamhokya alishukuru na kupongeza kuimarika ushirikiano kati ya Serikali na Vyama vya Wafanyakazi, akisema ushirikiano huo umechangia kuwepo kwa utulivu miongoni mwa wafanyakazi nchini.
Posted by MROKI On Tuesday, April 14, 2026 No comments

April 13, 2026

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba  akihutubia mkutano wa hadhara katika uwanja wa  Shule ya Msingi Boys iliyopo Mvumi Misheni kwenye jimbo la Mvumi, Dodoma, Aprili 12, 2026. 
Wananchi wakimsikiliza Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba alipohutubia mkutano wa hadhara katika uwanja wa  Shule ya Msingi Boys iliyopo Mvumi Misheni katika jimbo la Mvumi Dodoma, Aprili 12, 2026. 

 *************
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amekagua ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami ya Ntyuka–Mvumi–Kikombo yenye urefu wa kilomita 76 pamoja na kipande cha barabara ya Chololo–Mapinduzi (Makao Makuu ya TPDF) yenye urefu wa kilomita 5, katika Jimbo la Mvumi, Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma.

Mradi huu unaotekelezwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) unafadhiliwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ukiwa na lengo la kuboresha miundombinu ya usafiri, kuimarisha muunganiko kati ya Wilaya ya Dodoma Mjini na Chamwino, pamoja na kurahisisha upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii ikiwemo Hospitali ya Mvumi Mission.
 
Katika hatua ya utekelezaji, mradi huu unafanyika kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza yenye urefu wa kilomita 25 (ikiwemo Ntyuka–Mvumi–Makulu na Kikombo–Chololo–Mapinduzi) imefikia utekelezaji wa asilimia 80.9, na inatekelezwa na Mkandarasi M/s China Henan International Corporation Company Ltd kwa gharama ya shilingi bilioni 38.199.

Awamu ya pili yenye urefu wa kilomita 53 (Ntyuka–Mvumi Hospitali–Kikombo) imeanza kutekelezwa na Mkandarasi China First Highway Engineering Co. Ltd, ikiwa imefikia asilimia 5.2 ya utekelezaji kwa sasa, kwa gharama ya shilingi bilioni 98.488.

Aidha, mradi huu umeendelea kutoa ajira kwa Watanzania ambapo zaidi ya wafanyakazi 500 wamehusishwa katika awamu zote mbili za ujenzi.
 
Vilevile, Serikali imeendelea kulipa fidia kwa wananchi waliopisha mradi ambapo hadi sasa kiasi cha shilingi bilioni 7.6 kimeshalipwa kwa wananchi 756 katika sehemu ya kwanza ya mradi, huku zoezi la uthamini likiendelea kwa sehemu iliyobaki.
 
Taarifa ya utekelezaji wa mradi huo iliwasilishwa kwa Waziri Mkuu na Mhandisi Jefferson Nko, ambapo alieleza hatua zilizofikiwa pamoja na changamoto na mikakati ya kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.
 
Akizungumza baada ya kupokea taarifa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema: “Ndicho Mhe. Rais anataka kuwaachia alama ya kudumu wakazi wa eneo hili, hii ni barabara muhimu sana kwa kuwa nimepita nimeona hili ni eneo la uzalishaji.”
 
Mheshimiwa Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa wakandarasi kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo ili ukamilike kwa wakati na ubora unaotakiwa kulingana na makubaliano ya mkataba.
 
Aidha, Waziri Mkuu alitoa maagizo kwa Meneja wa Mradi kuhakikisha malipo kwa wafanyakazi wote wanaoshiriki katika mradi huo, ikiwemo wakandarasi wa ndani, mafundi na vibarua, yanafanyika kwa wakati.

“Meneja wa Mradi simamia na hakikisha mafundi na vibarua wanalipwa kwa wakati fedha zinapotoka. Tunapokamilisha mradi wale wote waliohusika kufanya kazi walipwe malipo yao mara moja,” alisisitiza.
Posted by MROKI On Monday, April 13, 2026 No comments

April 12, 2026





Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, amekutana na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kiarabu ya Sahara (SADR), Mhe. Brahim Ghali. Katika mazungumzo hayo, aliwasilisha salaam za Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mazungumzo hayo yalifanyika tarehe 9 Aprili 2026 katika makazi rasmi ya Mhe. Ghali, Kambi ya Ausserd, Tindouf, Algeria. Balozi Migiro alisisitiza kuwa msimamo wa Tanzania na CCM wa kuunga mkono haki ya watu wa Saharawi kujitawala ni wa muda mrefu. Alieleza kuwa msingi wake uliwekwa tangu enzi za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Kwa upande wake, Mhe. Ghali alimshukuru Rais Dkt. Samia kwa salaam na kwa kutuma uwakilishi kwenye maadhimisho ya miaka 50 ya SADR yaliyofanyika tarehe 8 Aprili 2026 katika Kambi ya Ausserd. Pia aliomba salamu zake zifikishwe kwa Rais, CCM na Watanzania.

Aliongeza kuwa watu wa Saharawi wanathamini mchango wa Mwalimu Nyerere katika kuhamasisha mshikamano wa Afrika na dunia. Alisema mshikamano huo umeendelea kuimarisha harakati za SADR, chini ya uongozi wa Chama cha Polisario, katika kudai haki ya kujitawala.
Posted by MROKI On Sunday, April 12, 2026 No comments





Na Mwandishi wetu, Dodoma
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imepatiwa mafunzo maalum kuhusu Sheria, Kanuni na Miongozo ya Sekta ya Madini, kwa lengo la kuongeza uelewa hususan juu ya tofauti kati ya Haki ya Ardhi na Haki ya Madini.

Mafunzo hayo yamefanyika katika Ukumbi wa Tanzanite, Makao Makuu ya Tume ya Madini, jijini Dodoma.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema kuwa umiliki wa haki ya madini na haki ya ardhi ni mambo mawili tofauti kisheria, na kwamba mwenye leseni ya madini haruhusiwi kuanza shughuli za uchimbaji bila kufikia makubaliano na mmiliki wa ardhi husika.

Amefafanua kuwa, kwa mujibu wa Sheria, leseni ya madini inaweza kutolewa katika eneo lolote, lakini utekelezaji wake unahitaji ridhaa au makubaliano na mwenye haki ya ardhi. Hata hivyo, iwapo makubaliano hayatapatikana, Waziri ana mamlaka ya kuruhusu shughuli za uchimbaji kuendelea kwa kuzingatia sheria.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgalu, ameipongeza Wizara ya Madini kwa kuandaa mafunzo hayo, akieleza kuwa yameongeza uelewa na kuwajengea wabunge uwezo wa kusimamia vyema sekta hiyo.

Wasilisho kuhusu haki ya madini na haki ya ardhi limetolewa na Mkurugenzi wa Huduma za Sheria kutoka Wizara ya Madini, Dkt. Arnold Gisase, ambaye ameeleza kuwa mtu anaweza kumiliki haki ya madini bila kuwa mmiliki wa ardhi, na kwamba umiliki wa ardhi pekee haumruhusu mtu kufanya shughuli za madini bila leseni husika.

Dkt. Gisase pia amebainisha changamoto zinazojitokeza, ikiwemo uelewa mdogo wa wananchi kuhusu haki na wajibu wao, kutokuelewa taratibu za uthamini na fidia, ucheleweshaji wa malipo ya fidia, pamoja na baadhi ya wamiliki wa ardhi kudai kuwa sehemu ya umiliki wa leseni za madini.

Naye, Mwanasheria kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Method Akilimali, amesisitiza kuwa fidia kwa mmiliki wa ardhi lazima ilipwe kabla ya kuanza kwa shughuli za utafiti au uchimbaji.

Ameongeza kuwa sheria inamtaka mmiliki wa leseni kurejesha eneo katika hali yake ya awali baada ya shughuli za madini kukamilika. Aidha, ameeleza kuwa ardhi yote nchini ni mali ya umma chini ya usimamizi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama mdhamini.

Amesema pia fidia inapaswa kulipwa ndani ya miezi sita; kuchelewa hulazimu kulipwa riba, na endapo itazidi miaka miwili tangu uthamini kufanyika, tathmini hiyo hupoteza uhalali.

Akizungumzia muundo wa leseni, Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amesema zipo aina kuu tatu za leseni ambazo ni leseni ya utafiti, uchimbaji mdogo na uchimbaji mkubwa ambapo kwa leseni ya uchimbaji mdogo Mtanzania pekee mwenye umri wa kuanzia miaka 18 ndiyo anaruhusiwa kuomba.

Mhandisi Lwamo amesema leseni kubwa na ya kati inaruhusiwa kuombwa na mtu yoyote na kwa sasa kuna mfumo wa kuomba leseni bila kufika ofisi za madini.

Mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha wabunge kuelewa kwa kina masuala ya kisheria na kiutendaji katika sekta ya madini ili kuboresha usimamizi na maamuzi yenye tija kwa maendeleo ya taifa.
Posted by MROKI On Sunday, April 12, 2026 No comments

April 11, 2026

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko (wapili kulia) akishiriki kuimba Wimbo wa Wafanyakazi wakati wa ufunguzi wa Barala la Wafanyakazi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi lililokutana leo Aprili 11, 2026 mkoani Morogoro. Wengine pichani ni Mwenyekiti wa Baraza hilo na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa INEC, Ramadhani Kailima (wapili kushoto), Katibu wa Baraza, Livini Avith (kulia) na Kulia ni mtumishi wa Tume, Rose Tengu. 
Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi wakishiriki kuimba Wimbo wa Wafanyakazi wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Barala la Wafanyakazi  INEC lililokutana leo Aprili 11, 2026 mkoani Morogoro. 
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko akizungumza wakati wa kufungua baraza la Wafanyakazi la INEC. 
Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi INEC ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume, Ndg. Ramadhani Kailima akizungumza katika kikao hicho cha Baraza. 
****************
Na Mwandishi Wetu, Morogoro
Watumishi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia katiba, sheria, kanuni  na taratibu na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania.
 
Hayo yamesemwa leo Aprili 11, 2026 na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt Jimmy Yonaz wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, katika kikao kilichoketi Mkoani Morogoro.
 
“Napenda kuwaasa, kuzingatia katiba, sheria, kanuni  na taratibu mnapotekeleza majukumu ya Tume na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania,”alisema Dkt Kilabuko.
 
Dkt. Kilabuko amesema, taasisi ina malengo yake, upo uwezakano wa kuepusha migogoro ya ndani na nje ya taasisi inayoweza kuathiri utekelezaji wa majukumu ya Tume kwa ufanisi.
  
Mapema akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi INEC ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume, Ndg. Ramadhani Kailima alisema kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025.
 
“Tume imekamilisha Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 ambao ulifanyika tarehe 29 Oktoba, 2025.  Kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025. Taarifa hiyo baada ya kukamilika, itawasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,”alisema Kailima.
 
Aidha, amesema Tume ipo katika maandalizi ya uchaguzi mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Isimani mkoani Iringa kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Mhe. William Lukuvi pamoja na uchaguzi wa udiwani katika Kata mbalimbali nchini ambazo madiwani wake walifariki.
 
Katika Kikao hicho cha siku moja pia kilitumika kwa kufanya uchaguzi wa Katibu wa Baraza hilo ambapo wajumbe walimchagua Ndg. Mwitaru Keboya kuwa Katibu mpya wa Baraza akichukua nafasi ya Ndg. Livini Avith ambaye amemaliza muda wake.
Katibu Mpya wa baraza la Wafanyakazi INEC, Ndg. Mwitaru Keboya akizungumza. 
Katibu wa Baraza aliyemaliza muda wake, Ndg. Livini Avith akizungumza. 

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi INEC wakifuatilia agenda mbalimbali katika mkutano huo. 

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi INEC wakifuatilia agenda mbalimbali katika mkutano huo. 

Mwenyekiti wa TUGHE tawi la INEC, Ndg. Juvenile Kaiza akizungumza.

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi INEC wakifuatilia agenda mbalimbali katika mkutano huo. 
Posted by MROKI On Saturday, April 11, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo