Nafasi Ya Matangazo

March 06, 2026


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amelipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa kusimamia na kukamilisha mradi wa kupeleka umeme wa gridi mkoani Kigoma na hivyo kuokoa takribani shilingi bilioni 58 zilizokuwa zikitumika kila mwaka kwa ajili ya ununuzi wa mafuta na matengenezo ya vipuri vya majenereta ya kuzalisha umeme.

Mhe. Salome ametoa pongezi hizo tarehe 6 Machi 2026 mara baada ya kutembelea mradi wa ujenzi wa kituo kikubwa cha Kupoza umeme cha Kidahwe kilichopo mkoani Kigoma pamoja na kituo cha kupoza umeme cha kigoma mjini na kituo cha muda cha Kidahwe.

“Niwapongeze TANESCO kwa kufikisha umeme wa gridi Kigoma hasa baada ya kukamilisha mradi  kutoka Nyakanazi hadi Kigoma na kwa kuamua kutumia fedha zenu za ndani shilingi bilioni tano kukamilisha kituo cha muda cha Kidahwe ambacho kwa sasa kinapeleka umeme Kigoma wakati ujenzi wa kituo kikubwa cha umeme Kidahwe ukiendelea,” amesema Mhe. Salome

Amesema kituo kipya cha umeme cha Kidahwe kitakuwa na uwezo wa megawati 192 na hivyo kitaimarisha zaidi hali ya upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Kigoma ambao kwa sasa unapata takribani megawati 30.

Ameongeza kuwa kituo hicho kinatarajiwa kukamilika mwezi Novemba mwaka huu na kitasaidia pia kuimarisha hali ya umeme katika mikoa ya Magharibi, kuendesha Treni ya Mwendo Kasi (SGR) pamoja na kuchochea biashara ya umeme na nchi jirani za Magharibi mwa Tanzania.

Kutokana na uwepo wa umeme wa kutosha mkoani Kigoma, Mhe. Salome amewakaribisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza katika mkoa huo.

 Aidha, amewaasa wananchi kulinda miundombinu ya umeme akieleza kuwa Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anaendelea kutoa fedha nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya nishati nchini hivyo wananchi wanao wajibu wa kuilinda na kuithamini.

Awali, Mratibu wa Mradi wa Kusafirisha umeme wa msongo wa kilovolti 400 kutoka Nyakanazi hadi Kigoma, Mhandisi Ramadhan Uwessu, alisema kuwa ujenzi wa kituo kipya cha Kidahwe unaenda sambamba na upanuzi wa kituo cha Nyakanazi ili kukiwezesha kusafirisha umeme wa msongo wa kV 400 kutoka Nyakanazi hadi Kidahwe.

Ameongeza kuwa kituo hicho pia kitapokea umeme kutoka njia ya Tabora kwa msongo wa kV 132, kutoka Sumbawanga kwa msongo wa kV 400 pamoja na umeme utakaozalishwa kutoka mradi wa Malagarasi.

Amesema mradi huo umefikia asilimia 47 ya utekelezaji na unagharimu takribani shilingi bilioni 434 zilizotolewa na Serikali ya Tanzania, Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) pamoja na Mfuko wa Maendeleo wa Watu wa Korea Kusini (EDCF).







Posted by MROKI On Friday, March 06, 2026 No comments


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amemwagiza Kamishna Jenerali wa Uhamiaji nchini amsake kokote alipo mkandarasi wa kampuni ya Tunnel Sadd Ariana na kumnyang'anya hati yake ya kusafiria kwa kushindwa kutekeleza mradi wa ujenzi wa bwawa katika mradi wa umwagiliaji wa Ziwa Eyasi.

“Huyu mtu amelipwa fedha na Serikali, lakini amepata wapi ujasiri wa kutufungulia kesi mahakamani wakati amekusanya vifaa tu na hajaanza kazi? Hii haikubaliki, ni dharau kwa nchi. Nimemwagiza Kamishna wa Uhamiaji, huyu mkandarasi atafutwe popote alipo, anyang'anywe pasi yake ya kusafiria, asiende kokote.”

Ametoa agizo hilo leo (Ijumaa, Machi 6, 2026) wakati akizungumza na wananchi na viongozi mbalimbali kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Mazingira mjini Karatu, mkoani Arusha. 

Waziri Mkuu amesema mkandarasi huyo alipaswa kujenga mradi huo wenye thamani ya sh. bilioni 21 na akalipwa malipo ya awali ya sh. bilioni tatu lakini hajafanya kazi. “Ipo michezo ya wakandarasi hasa wale wanaotaka walipwe kwenye akaunti za kwao. Nilishatoa maelekezo kwamba kuanzia sasa, fedha zilipwe katika akaunti zao kwenye benki za hapa Tanzania,” amesema.


Mapema, Waziri Mkuu aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa skimu za umwagiliaji katika Bonde la Eyasi, lililopo kilometa 50 kutoka mjini Karatu.

Amesema mradi huo ni miongoni mwa miradi 780 ya umwagiliaji inayoendelea kujengwa nchi nzima. “Mradi huu ni kama miradi inayoendelea kujengwa kule Isimani na Msingi. Miradi hii siyo ya serikali bali ni kwa ajili ya mashamba ya Watanzania walioko vijijini. Serikali haitavumilia uzembe, wizi na udokozi katika miradi ya maendeleo inayotekelezwa kwa fedha za walipakodi.”

Kwa mujibu wa taarifa ya mradi iliyowasilishwa, mradi huo unaotekelezwa na Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, utagharimu sh. bilioni 38.4. Hadi sasa utekelezaji wake umefikia asilimia 30 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Novemba, mwaka huu.

Kukamilika kwa mradi huo kutanufaisha zaidi ya wakulima 2,500 kutoka skimu za Mang’ola Barazani, Maleckchand, Laghangareri, Mbuga Nyekundu, Jobaji na Dumbechand, zenye zaidi ya hekta 5,000.

Aidha, utekelezaji wa mradi huo utasaidia kupunguza kwa kiwango kikubwa upotevu wa maji unaotokea katika mifereji ya asili, hatua itakayoongeza ufanisi wa matumizi ya maji na kuimarisha uzalishaji wa mazao katika eneo hilo.
Posted by MROKI On Friday, March 06, 2026 No comments








Na Mwandishi wetu, Dodoma
Wanawake wa Tume ya Madini wamefanya tukio la kibinadamu lililogusa mioyo ya watu wengi kwa kulipia gharama za matibabu kwa wagonjwa wenye uhitaji maalum katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), Kitengo cha Usafishaji Damu (Dialysis) iliyopo jijini Dodoma.

Msaada huo umetolewa kupitia ziara waliyoifanya hospitalini hapo ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, ambayo kilele chake ni  tarehe 08 Machi, mwaka huu. Wanawake hao wamejumuika na kuwatia moyo wagonjwa waliokumbwa na changamoto za kifedha, wakiwemo waliokuwa wakipatiwa matibabu ya figo.

Akizungumza kwa niaba ya wanawake wa Tume ya Madini, Kamishna wa Tume ya Madini, Mhandisi Theonestina Mwasha, amesema:

“Tunatambua kila mtu ana mahitaji mbalimbali, lakini nashukuru kwa michango iliyotolewa na Tume ya Madini kufanikisha kulipia baadhi ya gharama kwa wagonjwa kumi na wanne (14) waliokuwa wakikabiliwa na changamoto za kifedha katika kupata matibabu ya figo. Huu ni wakati wa kuwatia moyo na kuonyesha upendo wetu kwa wenzetu.” amesema.

Mhandisi Mwasha amesisitiza kuwa wanawake wana wajibu wa kuwa walezi na kuendeleza msaada kwa wananchi wenye mahitaji zaidi.

“Kutoa ni akiba ya baadaye, sio kwa familia zetu tu, bali kwa jamii kwa ujumla,” ameongeza.

Kwa upande wake, Kamishna wa Tume ya Madini, Dkt. Theresia Numbi, amesema msaada huu ni njia ya kugusa maisha ya wananchi na kurudisha tabasamu miongoni mwa wagonjwa, huku akibainisha gharama kubwa ya matibabu ya figo nchini.

Wakati huohuo akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo, Mkurugenzi wa Huduma za Uuguzi kutoka Hospitali ya Benjamin Mkapa, Mwanaidi Makao ameshukuru kwa msaada huo, akisema:

“Sio rahisi kusafisha damu kila mara kwa wagonjwa wetu kwa sababu gharama ni kubwa. Tunashukuru kwa kutuunga mkono na kuwasaidia wenye uhitaji.”

Naye Daktari bingwa wa hospitali hiyo, Dkt. Sabina Mmbali, amefafanua kuwa asilimia 60 ya wagonjwa wa figo  wanatumia bima za afya, huku asilimia 40 ya  wengine wakilipia matibabu kwa uwezo wao wenyewe. Matibabu ya figo hutakiwa kufanywa mara tatu kwa wiki.

“Msaada huu ni faraja kubwa kwa wagonjwa wetu, na tumefurahi sana,” amesema Dkt. Mmbali.

Wananchi wengi wameshuhudia tukio hilo na kupongeza jitihada za wanawake wa Tume ya Madini, wakisema kwamba ni ishara ya utu na mshikamano kwa kijamii.
Posted by MROKI On Friday, March 06, 2026 No comments

March 05, 2026


Na Mwandishi Wetu-Wizara ya Madini
Katika juhudi za Tanzania kuendelea kujidhihirisha kimataifa kupitia Sekta ya Madini, wanawake wa Kitanzania wameendelea kung’ara katika majukwaa ya madini barani Afrika na duniani. 

Hivi karibuni, katika Kongamano la African Mining Indaba nchini Afrika Kusini, Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wanawake Afrika (AWIMA) lilitoa tuzo kwa wanawake hodari wa sekta ya madini barani Afrika, ambapo wanawake wawili wa Tanzania walishinda vipengele tofauti. 

Mshindi mwingine ni Eng. Rose Mayembe, aliyeibuka mshindi wa pili katika kipengele cha Leading Woman in Large-Scale Mining akitanguliwa na mshindi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na wa tatu kutoka Afrika Kusini.

 Eng. Rose Mayembe  ni nani na ametoka wapi?

Akizungumza katika mahojiano maalum na Madini Diary, Rose anasema yeye ni mhandisi na mtaalamu mwelekezi wa masuala ya kimazingira na jamii, uchimbaji endelevu, na mabadiliko ya tabianchi. 

Safari yake katika madini ilianza takribani miaka 12 iliyopita aliposhiriki katika utekelezaji wa hatua za kufunga na baada ya kufunga mgodi mkubwa wa uchimbaji dhahabu wa Golden Pride Project (GPP) uliokuwa unamilikiwa na kampuni ya Resolute Mining Wilayani Nzega, Tabora. 

Uzoefu huo ulimfundisha umuhimu wa kuzingatia mipango ya kimazingira na kijamii mapema, ili kupunguza madhara kwa jamii na mazingira. 

“Hapo ndipo niliona umuhimu wa kuingiza fikra za mabadiliko ya tabianchi na ubunifu tangu mwanzo wa mradi,” anasema Rose.

Tuzo ya African  Mining Indaba na GGA
Katika Mining Indaba, Rose alitambuliwa mshindi wa pili wa Leading Woman in Large-Scale Mining in Africa. Anasema tuzo hiyo ni heshima kubwa, kwani majukwaa kama hayo hujumuisha Serikali, wawekezaji, kampuni kubwa, na wataalamu kutoka duniani kote. Anasema  ushindi huo unaonyesha uwezo wa wanawake wa kitanzania kushindana na kuongoza katika shughuli za uchimbaji mkubwa. Rose anasisitiza, “kwa wanawake, tuzo hii ni ishara ya kuvunja glass ceiling na kuthibitisha tunaweza kuwa mezani pa maamuzi, kusukuma mbele ajenda ya madini yenye uwajibikaji, ushindani wa kimataifa, na ushiriki wa wanawake na vijana,” anasema.

Mbali na tuzo hiyo, mwaka 2025, Rose alipata tuzo ya Global Advocacy Award (GAA) katika kipengele cha Nishati Safi na Uchimbaji Endelevu (Clean Energy & Sustainable Mining), ikitambua mchango wake katika SDG 7 (Affordable and Clean Energy)  iliyotolewa wakati wa Global Advocacy Forum Awards (GAF 2025) London, Uingereza.

Safari ya Kazi na mchango wake Sekta ya Madini

Kwa sasa, Rose anafanya kazi katika miradi ya kitaifa na kimataifa, akichangia uzoefu wake katika hatua zote za maisha ya mgodi: usanifu wa migodi, uendeshaji migodi, kufunga mgodi na baada ya kufungwa (post-closure). Lengo lake ni kuhakikisha sekta ya madini inaleta mapato, inalinda mazingira, inaheshimu haki za binadamu, na kuchangia maendeleo endelevu ya jamii.

 “Nilipoanza kuzungumza kwa takwimu na maandalizi ya kitaalamu, niliona nafasi ya uongozi si cheo bali ni uwezo wa kuathiri maamuzi na tangu hapo sikuwahi tena kujiona kama mshiriki wa pembeni bali kama sehemu ya mwelekeo wa Sekta,’’ anasema.


Nini kilimfikisha  alipo?
Anapoulizwa kilichomfikisha alipo anasema ilikuwa ni uamuzi wa ndani na aliamini kutokusubiri ili kuthibitishwa na wengine katika sekta ambayo imezoea sauti flani na kwamba aligundua ubora wa hoja unazidi sauti ya anayezungumza.  

Nini kilichomfanya atambulike?
Anasema anaamini kinachomtofautisha ni uwezo wake wa kuunganisha taaluma tofauti katika mtazamo mmoja wa kimkakati, akiangalia Sekta ya Madini si tu kama shughuli za uchimbaji bali kama mfumo unaogusa uhandisi, mazingira, jamii, fedha, na sera. “Uzoefu wangu katika hatua zote za maisha ya mgodi kuanzia feasibility, design, operations hadi closure na post-closure na umenipa  uwezo wa kuona picha kubwa na kutoa mwelekeo unaozingatia uendelevu tangu mwanzo wa mradi,’’anasisitiza.

Anasema zaidi, mtazamo wa mabadiliko ya tabianchi na haki za binadamu kama sehemu ya maamuzi ya kimkakati, umemfanya kuunganisha uchumi, mazingira, na jamii katika mfumo mmoja unaotekelezeka.

Wanawake Wachimbaji Tanzania

Mhandisi Rose anasema  wanawake katika Sekta ya madini wakiwemo  wachimbaji na wataalamu wanaofanya kazi na sekta, wanahitaji zaidi kuaminiwa na kupewa nafasi ya kuongoza. Anasema changamoto si  uwezo ni nafasi. ‘’Tunahitaji kushirikishwa katika maamuzi ya kimkakati, bodi na sera, si kubaki katika utekelezaji pekee,’’ anaeleza.


Anaizungumziaje Sekta ya Uchimbaji   Mdogo?

Mhandisi Rose anashauri kuanza na uwezeshaji wa wachimbaji wadogo, kuwarasimisha, kuwezesha upatikanaji wa mitaji, elimu ya biashara, na mafunzo ya lazima ya mazingira na usalama. Anasisitiza mwongozo rahisi wa EIA na ufuatiliaji wa kitaalamu ambao anasema unaweza kuboresha sekta hiyo bila kuongeza mzigo wa kisheria. Anasema lengo ni kujenga sekta ya uchimbaji mdogo endelevu, salama, na yenye ushindani wa muda mrefu.

Wito kwa Watanzania, wanawake na Wasichana.

Anatoa wito kwa watanzania, hususan wasichana na wanawake, akisema sekta ya madini ni fursa ya ubunifu na uongozi, si sekta ya jinsia. “Jiwekezeni katika elimu, jengeni ujuzi, na msijitenge katika meza za maamuzi. 

Uwezo hauna jinsia. Madini ni chachu ya maendeleo, lakini maendeleo ya kweli yanakuja pale tunaposhirikisha wanawake na vijana kikamilifu. 

"Naamini kizazi kijacho cha wanawake hakitaomba nafasi, kitakuwa sehemu ya mwelekeo wa sekta hii,” anasema Rose.
Posted by MROKI On Thursday, March 05, 2026 No comments


Na John Mapepele
Waziri wa Afya, Mohammed Mchengerwa, amesema kuwa ushirikiano madhubuti kati ya Serikali na Washirika wa Mfuko wa Pamoja wa Afya (Health Basket Fund) umeendelea kuwa chachu ya maboresho makubwa katika utoaji wa huduma za afya nchini.
 
Akizungumza katika mkutano wa nchi washirika wa Mfuko huo Machi 2, 2026 jijini Dar es Salaam Mhe. Mchengerwa alianza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuiwezesha Tanzania kufikia hatua ya kufanya majadiliano muhimu kuhusu mustakabali wa sekta ya afya. Alisisitiza kuwa pale washirika wa sekta ya afya wanapoungana kwa uwazi, dhamira na malengo ya pamoja, maisha ya wananchi huboreshwa kwa haraka zaidi.
 
“Mkutano huu si wa kawaida. Ni wakati wa kimkakati wa kuimarisha ushirikiano na kuthibitisha upya wajibu wetu wa pamoja wa kutoa huduma bora za afya kwa Watanzania,” alifafanua.
 
Mfuko wa Pamoja wa Afya Waimarisha Huduma za Msingi nchini
 
Waziri Mchengerwa alieleza kuwa tangu kuanzishwa kwa Mfuko wa Pamoja wa Afya mwaka 1999, zaidi ya dola za Marekani bilioni 1.3 zimechangishwa kusaidia utekelezaji wa mipango ya kimkakati ya sekta ya afya. Asilimia 90 ya fedha hizo zimeelekezwa katika huduma za Afya ya Msingi zinazosimamiwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa.
 
Alibainisha kuwa kuanzia mwaka 2017, fedha za Mfuko zilianza kupelekwa moja kwa moja katika zaidi ya vituo 7,345 vya afya kupitia utaratibu wa ufadhili wa moja kwa moja kwa Vituo vya Afya, hatua iliyoongeza uwazi na ufanisi katika matumizi ya rasilimali.
 
“Kwa pamoja tumeimarisha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba muhimu, tumepunguza vifo, na kuongeza uzazi salama katika Vituo vya Afya. Mageuzi haya yameweka msingi imara wa mfumo wa afya wenye ustahimilivu,” alisisitiza.
Katika hatua nyingine, Mhe. Mchengerwa alisema Tanzania ipo katika kipindi cha mageuzi makubwa, huku lengo kuu likiwa utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote. Alifafanua kuwa wakati bima hiyo ikipanua ulinzi wa kifedha kwa wananchi, Mfuko wa Pamoja wa Afya unabaki kuwa mhimili wa kuhakikisha huduma bora na zenye usawa zinapatikana kwa wote.
 
Aidha, Waziri huyo alitoa wito kwa washirika kuunga mkono utekelezaji wa Mkakati wa Kitaifa wa Afya Kidijitali uliounganishwa, akisisitiza umuhimu wa kuwa na mfumo mmoja wa kitaifa unaounganisha taarifa zote za afya.
 
“Huwezi kusimamia usichokiona, na huwezi kuboresha usichokipima. Mfumo wa kidijitali uliounganishwa ni mageuzi ya utawala, ufanisi na uaminifu,” alisema.
 
Akizungumzia dira ya muda mrefu, Mhe. Mchengerwa alisema Tanzania inalenga kupunguza utegemezi mkubwa wa bidhaa za afya kutoka nje kwa kuwekeza katika uzalishaji wa ndani wa dawa, vifaa tiba na teknolojia za afya.
 
“Hili si suala la uchumi pekee, bali ni suala la usalama wa afya ya taifa. Mfumo imara wa afya lazima uunganishe ustahimilivu wa kifedha, kidijitali, rasilimali watu pamoja na uzalishaji na ugavi,” alifafanua.
 
Waziri huyo alieleza kuwa mandhari ya maendeleo duniani yanabadilika, huku nchi zikielekea kwenye ushirikiano wa thamani ya pande zote na uendelevu wa muda mrefu.
 
“Tunaamini mustakabali wa ushirikiano haujengwi juu ya utegemezi, bali ubunifu wa pamoja na uwekezaji. Ushirikiano wenye busara haufiche changamoto; hujifunza kutoka kwake na hubuni mifumo bora zaidi,” alisema.
 
Alikiri kuwepo kwa changamoto ya upatikanaji wa fedha kwa wakati, akieleza kuwa Serikali inafanya kazi kwa karibu na Wizara nyingine ikiwa ni pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI  na Wizara ya Fedha ili kuondoa vikwazo vya kiutendaji na kuimarisha uwazi katika usimamizi wa fedha.

Akizungumza  kwa niaba ya timu ya mabalozi walioshiriki katika kikao hicho, Mheshimiwa Elke Wisch, Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) na Mratibu wa Wadau wa Mfuko wa Pamoja wa Afya alimshukuru Rais Samia kwa kazi kubwa katika kuokoa vifo vya mama wajawazito na mtoto wakati wa kujifungua.
 
Mhe. Wisch aliihakikishia Serikali ya Tanzania kuendelea kuchangia katika sekta ya afya.
 
Aidha, walisifu juhudi zilizofikiwa  katika kuimarisha huduma bora za afya katika kipindi kifupi cha Serikali chini ya Rais Samia.
Posted by MROKI On Thursday, March 05, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akizungumza wakati wa hafla ya kuzindua rasmi Huduma ya Mikopo Midogo ya Makazi, iliyoanzishwa na Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini ili kuwawezesha kumiliki makazi bora, katika hafla iliyofanyika katika hoteli ya Serena, jijini jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akikata utepe kuasharia  kuzindua rasmi Huduma ya Mikopo Midogo ya Makazi, iliyoanzishwa na Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini ili waweze  kumiliki makazi bora, hafla iliyofanyika katika hoteli ya Serena, jijini jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC), Bw. Elibariki Ndossi, akizungumza jambo wakati akimkaribisha Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (Hayupo pichani), kuzindua rasmi Huduma ya Mikopo Midogo ya Makazi, iliyoanzishwa na Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini ili waweze kumiliki makazi bora, hafla iliyofanyika katika hoteli ya Serena, jijini jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wadau wa sekta ya makazi na benki, wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (Hayupo pichani), wakati akizindua rasmi Huduma ya Mikopo Midogo ya Makazi, iliyoanzishwa na Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini kwa lengo la kuwawezesha kumiliki makazi bora, hafla iliyofanyika katika hoteli ya Serena, jijini jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wadau wa sekta ya makazi na benki, wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (Hayupo pichani), wakati akizindua rasmi Huduma ya Mikopo Midogo ya Makazi, iliyoanzishwa na Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini kwa lengo la kuwawezesha kumiliki makazi bora, hafla iliyofanyika katika hoteli ya Serena, jijini jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wadau wa sekta ya makazi na benki, wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (Hayupo pichani), wakati akizindua rasmi Huduma ya Mikopo Midogo ya Makazi, iliyoanzishwa na Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini kwa lengo la kuwawezesha kumiliki makazi bora, hafla iliyofanyika katika hoteli ya Serena, jijini jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (Katikati aliyeketi), akiwa katika ya pamoja na viongozi wa Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) pamoja na watumishi wa Shirika hilo, baada ya kuzindua rasmi Huduma ya Mikopo Midogo ya Makazi, iliyoanzishwa na Shirika hilo kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini kwa lengo la kuwawezesha kumiliki makazi bora, hafla iliyofanyika katika hoteli ya Serena, jijini jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (Katikati aliyeketi), akiwa katika ya pamoja na viongozi wa Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) pamoja wadau mbalimbali wa sekta ya nyumba na benki, baada ya kuzindua rasmi Huduma ya Mikopo Midogo ya Makazi, iliyoanzishwa na Shirika hilo kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini kwa lengo la kuwawezesha kumiliki makazi bora, hafla iliyofanyika katika hoteli ya Serena, jijini jijini Dar es Salaam.
*****************
Na Benny Mwaipaja, Dar es Salaam
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mshamu Ali Munde (Mb), amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za fedha likiwemo Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) ili kuiwezesha sekta ya fedha kupata mikopo yenye gharama nafuu, hatua itakayosaidia jamii ya kipato cha chini kumiliki makazi bora.

Mhe. Munde amesema hayo Jijini Dar es Salaam, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akizindua rasmi huduma ya mikopo midogo ya makazi jijini Dar es Salaam, iliyoanzishwa na Shirika la Mikopo ya Nyumba Tanzania (TMRC) kwa kushirikiana na Shirika la Habitat for Humanity International, iliyokusudiwa kuziwezesha taasisi za fedha kupata ukwasi wa shilingi bilioni 30, ili ziweze kutoa mikopo midogo ya nyumba, kwa wananchi wenye kipato cha chini kwa lengo la kuwawezesha kumiliki makazi bora.

“Serikali inaunga mkono mipango kama hii inayolenga kukabiliana na changamoto za makazi, hasa kwa wananchi wa kipato cha chini ambao hukumbwa na vikwazo vikubwa zaidi vya kupata mikopo rasmi kwa kutokuwa na rehani inayohitajika kutokana na kipato chao kuwa kidogo au kisicho rasmi” alisema Mhe. Munde.

Alisema kuwa huduma hizo zinaunga mkono juhudi za Serikali za kuongeza upatikanaji wa nyumba bora na nafuu zinazokidhi matarajio ya wananchi wa kipato cha chini, na kusaidia Serikali katika kuwahudumia wananchi wake katika sekta ya makazi.

Wakizungumza wakati wa uzinduzi huo rasmi wa huduma ya mikopo midogo ya makazi, Mkurugenzi Mtendaji wa TMRC, Bw. Elibariki Ndossi, amesema lengo kuu ni kuwawezesha Watanzania  kupata makazi bora huku Mkurugenzi wa Mikopo ya Nyumba kutoka Habitat for Humanity Tanzania, Bw. Daniel Mhina, akiweka wazi kuwa kupitia mradi huo wananchi hawatalazimika kuwa na dhamana isiyohamishika ili kupata mkopo.

Walisema kuwa hatua hiyo inafuatia utafiti uliofanywa na taasisi hizo, unaoonesha kuwa ni takribani asilimia 3 tu ya Watanzania wanaopata huduma za mikopo ya nyumba, hali inayochangiwa na wengi kushindwa kumudu masharti na viwango vya mikopo hiyo.

Tangu kuanzishwa kwa TMRC mwaka 2010, taasisi hiyo imechangia uwezeshaji wa mikopo ya nyumba kutoka shilingi bilioni 76.7 hadi kufikia shilingi bilioni 745 mwaka 2025.
Posted by MROKI On Thursday, March 05, 2026 No comments






Makatibu Wakuu wa Nchi Wanachama za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wanaosimamia masuala ya mtangamano wamekutana katika Makao Makuu ya Jumuiya hiyo jijini Arusha, ikiwa ni muendelezo wa maandalizi ya Mkutano wa 25 Wakuu wa Nchi Wanachama wa EAC utakaofanyika tarehe 7 Machi 2026 jijini Arusha.
 
 
Kikao hicho cha Makatibu Wakuu ambacho ni sehemu ya Mkutano Maalum wa 59 wa Baraza la Mawaziri wa EAC, pamoja na masuala mengine umepokea na kujadili agenda na taarifa mbalimbali zilizowasilishwa na mkutano wa Ngazi ya Wataalamu uliofanyika tarehe 2 hadi 3 Machi 2026. Agenda na taarifa hizo zitawasilishwa na kujadiliwa kwenye Mkutano wa Mawaziri utakaofanyika tarehe 5 Machi 2026 jijini Arusha.
 
Akifungua mkutano huo Dkt. Caroline W. Karugu, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki nchini Kenya, na Mwenyekiti wa mkutano huo, ameeleza kuwa Jumuiya imeendelea kupiga hatua kubwa ya maendeleo huku ikizingatia ustawi wa watu wake kwa kuwezesha shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo biashara na uwekezaji na utoaji wa huduma za kijamii. 
 
Aliongeza kusema kuwa licha ya kujivunia mafanikio hayo yanayotokana na uongozi imara wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya, juhudi zaidi zinahitajika katika kuendelea kuibua na kutekeleza mikakati itakayosaidia kutatua changamoto mpya zinazoibuka ambazo zinaweza kukwamisha utekelezaji wa programu mbalimbali za Jumuiya. 
 
Amebainisha baadhi ya mikakati hiyo kuwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ya uchukuzi na mawasiliano ambayo itachagiza kasi ya ukuaji wa uchumi jumuishi na kuongeza uzalishaji wa bidhaa na huduma katika Jumuiya. 
 
Miongoni mwa agenda zilizopokelewa na kujadiliwa katika mkutano huo ni pamoja na; uzinduzi wa Mkakati wa Saba wa Maendeleo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (2026/27 – 2030/31), uteuzi wa Katibu Mkuu wa Jumuiya, uondoshwaji wa vikwazo vya biashara visivyo vya kiforodha (NTB’s), hali na utaratibu wa utoaji wa michango ya Jumuiya kutoka nchi wanachama, uteuzi wa Majaji wa Mahakama ya Jumuiya na Mkataba wa Ulinzi wa Pamoja wa EAC. 
 
Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo umeongozwa na Balozi Stephen P. Mbundi Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki akiambatana na Viongozi wengine Waandamizi wa Serikali wakiwemo Bw. Elia Mwandumbya Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bw. Aristides Mbwasi Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Viwanda na Biashara,  Mhe. Samwel M. Maneno Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wakurugenzi na Maafisa waandamizi wa Serikali.
Posted by MROKI On Thursday, March 05, 2026 No comments

March 04, 2026







Na Eleuteri Mangi, WANMM- Bariadi, Simiyu
Serikali kupitia Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeanzisha Kliniki Maalumu ya Wanawake “Samia Ardhi Kliniki” hatua inayoweka mazingira rafiki kwa wanawake wengi kumiliki ardhi kisheria sambamba na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na maendeleo. 

Wanawake wa Mkoa wa Simiyu ambao ni miongoni mwa wanufaika wa kliniki hiyo wameishukuru Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kuwapelekea Samia Ardhi Kliniki inayoendelea kuwahudumia wanawake na kutatua changamoto zinazowakabili katika umiliki wa ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Kliniki hiyo Machi 4, 2026 mjini Bariadi, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anamringi Macha amesema, Kliniki hiyo imekuja muda muafaka kwa kuwa itasaidia wanawake wa mkoa huo kumiliki ardhi. 

Pia Mkuu wa Mkoa Mhe. Macha ametoa wito kwa wanawake katika mkoa huo kujitokeza kwa wingi katika wiki ya Samia Ardhi Kliniki ili kupata elimu, ushauri na huduma mbalimbali za Sekta ya Ardhi ikiwemo kupimiwa maeneo yao na kupata Hati Miliki zao. 

Pamoja na uwepo wa Sera na Sheria zinazolinda haki za wanawake, takwimu zinaonesha kuwa takribani asilimia 28 pekee ya wanawake nchini ndio wenye hati miliki katika maeneo mbalimbali nchini.

Akitoa taarifa ya utendaji kazi wakati wa ufunguzi wa Kliniki hiyo, Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Simiyu Bw. Denis Masami amesema, hadi kufikia tarehe 4 Machi 2026 wametoa jumla ya Hati 198 na kuweka bayana kuwa, kliniki hiyo inayotarajiwa kuhitimishwa Machi 7, 2026 ni sehemu ya kuelekea maadhimisho Siku ya Kimataifa ya Wanawake ambayo huadhimishwa kila mwaka Machi 08.

Ameongeza kuwa, Mkoa wa Simiyu una lengo la kutoa hati 3,000 kwa mwaka 2025/2026 ambapo hadi sasa wametoa jumla ya hati 1,441 sawa na asilimia 48 ya lengo ambapo kati ya hati hizo 403 ni za wanawake sawa na asilimia 28 ya hati zote zilizotolewa katika mkoa huo.

Kwa upande wake Bi. Stela Manyonyi kutoka Wilaya ya Busega mkoani Simiyu ameahidi kuitumia hati aliyoipata katika shughuli za maendeleo kwa kuchukulia mkopo wa kuendeleza biashara zake.

Kaulimbiu ya maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake mwaka huu ya  inahimiza "Haki sawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kifikia Dira 2050" huku Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi ikisisitiza kuwa “Mwanamke; Haki Yako, Miliki Ardhi Sasa’’.
Posted by MROKI On Wednesday, March 04, 2026 No comments
Makatibu Wakuu wa Vyama Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika, wakiongozwa na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, kwenye Kikao cha Bodi ya Wadhamini wa Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS), kilichoketi leo tarehe 4 Machi 2026, Kibaha, mkoani Pwani. 

Wajumbe wengine waliohudhuria kikao hicho ni; Katibu Mkuu wa Chama cha ANC (Afrika Kusini), Fikile Mbalula, Katibu Mkuu wa Chama cha FRELIMO (Msumbiji), Chakil Felizardo Passadas Aboobacar, Katibu Mkuu wa Chama cha ZANU-PF (Zimbabwe), Jacob Francis Nzwindamilimo Mudenda, Chama cha SWAPO (Namibia), kimewakilishwa na Mjumbe wa Kamati Kuu, Dkt. Samuel Abraham Peyavali Mushelenga na Chama cha MPLA (Angola) kimewakilishwa na Mjumbe wa Kamati Kuu, Frederico Toth Jorge De Miranda.






Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, (katikati), akiwa kwenye picha ya pamoja na  Katibu Mkuu wa Chama cha ANC (Afrika Kusini), Fikile Mbalula (kulia pichani) pia Katibu Mkuu wa Chama cha FRELIMO (Msumbiji), Chakil Felizardo Passadas Aboobacar (kushoto pichani), kabla ya kuanza Kikao cha Bodi ya Wadhamini wa Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS), kilichoketi leo tarehe 4 Machi 2026, Kibaha, mkoani Pwani. Wajumbe wa kikao hicho ni Makatibu wa Vyama Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika. Vyama vingine ni SWAPO (Namibia), ZANU - PF (Zimbabwe) na MPLA (Angola).


Posted by MROKI On Wednesday, March 04, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo