Nafasi Ya Matangazo

July 10, 2026


Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia Mradi wa Urejeshaji Endelevu wa Mazingira na Hifadhi ya Bayoanuai Tanzania imewezesha urejeshaji wa hekta milioni 3.3 za ardhi na misitu iliyoharibiwa hadi kufikia mwezi Desemba 2024.
 
Hayo yamebainishwa Julai 9, 2026 Mkoani Morogoro na Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais, Abdllah Hassan Mitawi wakati ufunguzi wa warsha ya kujenga uwezo kikosi-kazi cha taifa cha urejeshaji wa mazingira ya ardhi na misitu iliyoharibika.
 
Amebainisha kuwa Tanzania imebarikiwa utajiri mkubwa wa mifumo ikolojia ambapo takribani hekta milioni 48 ni misitu, ambapo hata hivyo pamoja na wingi wa rasimali hizo kumekuwepo na changamoto za uharibifu wa mazingira, ambapo tafiti zimeonesha kuwa takribani hekari 469,000 za misitu hupotea kila mwaka.
 
Mitawi amesema urejeshaji wa Ardhi ya Misitu iliyoharibiwa ni sehemu ya ajenda muhimu ya maendeleo endelevu ya Tanzania, kutokana na hatua hiyo Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kisera na kimkakati kwa kushirikiana na wadau.
 
Amesema mwa juhudi hizo ni utekelezaji wa Mkakati wa AFR100, unaolenga kurejesha hekta milioni 100 za ardhi  na misitu iliyoharibika barani Afrika kufikia mwaka 2030 ambapo mkakati huo unachangia malengo ya kidunia ya kurejesha hekari milioni 350 za ardhi na misitu duniani kote.
 
Amefafanua kuwa katika kuchangia jitihada za kimataifa na malengo ya uhifadhi mazingira kitaifa, mwaka 2018, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliahidi kurejesha hekta milioni 5.2 za maeneo ya ardhi na misitu iliyoharibika kufikia mwaka 2030 chini ya mkakati wa AFRI100.
 
Kwa mujibu wa Mitawi amesema mwaka 2024 Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia mradi wa Urejeshaji Endelevu wa Mazingira na Hifadhi ya Bayoanuai Tanzania (SLR) ilikamisheni Kituo cha Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC) kufanya tathmini ya utekelezaji wa ahadi hiyo ili kubaini hatua iliyofikiwa.
 
Ameeleza utekelezaji wa ahadi hiyo inaongozwa na na Mkakati wa Taifa wa Urejeshaji wa Ardhi na Misitu iliyoharibiwa (2023–2033); Mpango Kabambe wa Taifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022 – 2032); Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024 -2034) na Programu ya Mageuzi ya Usimamizi wa Mazingira kuelekea Dira2050.
 
”Nichukue fursa hii kuwajulisha wajumbe wa kikosi-kazi hiki mchukue jambo hili kwa umakini na uzito unaostahili, kwakuwa Serikali na wadau wote wa masuala ya urejeshaji na hifadhi wa mazingira watategemea sana maoni, ushauri na mapendekezo yenu” amesema Mitawi.
Kaimu Meneja wa Vyanzo vya Mbegu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Dk Fortunata Senya alisema Serikali imeandaa Mkakati wa Taifa wa Urejeshaji wa Mandhari ya Misitu wa mwaka 2023–2030 ili kuhakikisha lengo la kurejesha hekta milioni 5.2 linafikiwa.
 
Alisema mafanikio ya mpango huo hayawezi kupatikana kwa juhudi za Serikali pekee, bali yanahitaji ushiriki mpana wa wadau mbalimbali wakiwamo taasisi za utafiti, sekta binafsi, mashirika ya maendeleo na wananchi.
 
Kwa upande wake, Mtafiti wa Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI), Joshua Maguzu alisema taasisi hiyo inaendelea kufanya tafiti zinazolenga kubaini aina sahihi za miti zinazofaa kupandwa katika maeneo mbalimbali ya nchi kulingana na hali ya udongo na tabianchi.
 
 
Alisema matokeo ya tafiti hizo yanawasaidia wataalamu na wananchi kuchagua miche inayostawi vizuri katika maeneo husika, hatua inayoongeza mafanikio ya urejeshaji wa mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.




Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu, Arusha
WIZARA ya Maliasili na Utalii imepongeza hatua kubwa iliyofikiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika kujiandaa kupokea wageni wa mashindano ya AFCON 2027, baada ya Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki, Bw. Daniel Pancrasi, kujionea maendeleo makubwa yaliyofanyika katika eneo la utalii la Ziwa Duluti, Arusha.

Bw. Pancrasi alitoa pongezi hizo alipofanya ukaguzi wa maandalizi ya miundombinu na huduma zinazotekelezwa na TFS, akisema ameridhishwa na uwekezaji mkubwa uliofanywa hususan katika maeneo ya malazi, huduma za chakula na kuboresha mazingira ya utalii kwa viwango vinavyoweza kupokea wageni wa kimataifa wakati wa AFCON.

“Hongereni sana TFS. Kwa muda mrefu mmekuwa mkituletea taarifa mbalimbali kuhusu maandalizi haya, lakini leo nimejionea mwenyewe kazi kubwa iliyofanyika. Hakika nimefurahishwa sana. Nitakuwa shahidi katika vikao mbalimbali kwamba TFS haisemi tu kwa maneno, bali inafanya kazi kwa vitendo,” alisema Bw. Pancrasi huku akisisitiza kuwa maandalizi hayo yanaonesha dhamira ya Serikali kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na fursa za kiuchumi zitakazotokana na AFCON 2027.

Alisema maboresho yaliyofanyika Ziwa Duluti yanaongeza hadhi ya vivutio vya utalii vya Tanzania na kuweka mazingira bora ya kuwahudumia wageni kutoka mataifa mbalimbali watakaowasili nchini wakati wa mashindano hayo.

Awali, Mkuu wa Dawati la Utalii wa TFS, Mhifadhi Mkuu, PCO Someni Mteleka, alisema maboresho yanayotekelezwa katika Ziwa Duluti ni sehemu ya mkakati mpana wa TFS wa kuandaa vivutio vya utalii vinavyosimamiwa na wakala huo ili viwe tayari kupokea idadi kubwa ya wageni wakati wa AFCON 2027.

Mteleka alisema uwekezaji unaoendelea unalenga kuboresha ubora wa huduma za malazi, migahawa, mapokezi ya wageni na shughuli mbalimbali za utalii wa asili, sambamba na kuhakikisha wageni wanapata huduma zinazokidhi viwango vya kimataifa.

Aliongeza kuwa TFS inaendelea kutekeleza maagizo ya Serikali ya kutumia AFCON 2027 kama jukwaa la kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia vivutio vya utalii, huku Ziwa Duluti likiwa miongoni mwa maeneo yaliyopangwa kuwa kitovu cha mapumziko na burudani kwa wageni watakaofika nchini.

Ziara ya Bw. Pancrasi imeongeza matumaini kuwa kasi ya maboresho inayoendelea katika vivutio vya utalii vinavyosimamiwa na TFS itaifanya Tanzania kuwa tayari kupokea maelfu ya wageni wa AFCON 2027, huku Ziwa Duluti likitajwa kuwa mfano wa namna uwekezaji wa kimkakati unavyoweza kubadilisha vivutio vya utalii kuwa bidhaa zinazoweza kushindana katika soko la kimataifa.

Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments
Wananchi wanaotembelea banda la Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) wanapata fursa ya kujifunza mchango wa mashamba ya miti ya kupandwa katika kukuza uchumi wa viwanda na biashara ya mazao ya misitu nchini.

Katika banda hilo, TFS inaonesha jinsi mashamba ya miti yanavyotoa malighafi kwa viwanda mbalimbali vinavyozalisha mbao, samani, karatasi na bidhaa nyingine za misitu, huku yakichangia uhifadhi wa mazingira na kuongeza ajira.

Mbali na hilo, wageni wanapata nafasi ya kujionea uzalishaji wa mianzi na kufahamu matumizi yake katika ujenzi, utengenezaji wa samani, bidhaa za ubunifu na uhifadhi wa mazingira.

Wataalamu wa TFS pia wanatoa elimu kuhusu mbinu bora za upandaji na utunzaji wa miti, uvunaji endelevu, pamoja na taratibu za kufanya biashara ya mazao ya misitu kwa kuzingatia sheria na kanuni.

Kupitia maonesho hayo, TFS inawahimiza wananchi, wawekezaji na wafanyabiashara kutembelea banda lake ili kupata ushauri wa kitaalamu, kufahamu fursa zilizopo katika sekta ya misitu na kushiriki katika kukuza uchumi wa Taifa kupitia matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.




Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Maridhiano baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Alliance For Change and Transparency (ACT-Wazalendo) kuelekea uundwaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) Zanzibar, umepongezwa kwani umezingatia maslahi ya nchi ambayo ni muhimu kuliko maslahi binafsi ya wanasiasa.

Hayo yameelezwa na Mbunge wa Viti Maalum CCM na Mwenyekiti Taifa wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mary Chatanda, Julai 9, 2026, Jijini Dodoma.

Akitoa maoni yake baada ya kumalizika hafla hiyo ya Tamko la Pamoja la Maridhiano ya Kisiasa baina ya vyama hivyo, Chatanda amesema, Wazanzibar wameshasahau siasa za chuki, kipaumbele chao sasa ni umoja, mshikamano na maendeleo.

"Wazanzibar ni watu rahimu sana, wao wanataka amani, mshikamano na maendeleo na kitendo cha vyama hivi viwili kufikia muafaka, ni ishara ya ukomavu wa kisiasa na kuzingatia maslahi ya nchi," amesema Chatanda.

Aidha, amesema maridhiano hayo yana maana kubwa katika kuhakikisha SUK inaundwa kwa ukamilifu wake kwani SUK ndiyo mwelekeo wa siasa za Zanzibar katika uundwaji wa serikali. 

Sambamba na hilo, amesema ni muhimu kwa wananchi na wanasiasa wa Zanzibar kumpa ushirikiano Rais Dk. Hussein Mwinyi ambaye amejipambanua kuwa kiongozi mchapakazi, msikivu na mpenda maendeleo kwa wananchi wake.

"Wazanzibar wana Rais mchapakazi na mwenye maono makubwa ya maendeleo, wananchi wanapaswa kumpa ushirikiano na kuhakikisha Zanzibar inasonga mbele kwa kasi," amesisitiza.

Katika hafla hiyo, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amesisitiza kuwa, maridhiano hayo si udhaifu bali ni ukomavu wa kisiasa na unafungua ukurasa mpya wa umoja, amani, utulivu na mshikamano kwa maendeleo ya wananchi wa Zanzibar.

"Uungwana hautufunzi kiburi na kutosikilizana. Wananchi wetu hawahitaji vurugu wala mivutano ya kisiasa isiyoisha. Wananchi wetu wanahitaji amani, usalama na utulivu," amesema Rais Dk. Samia
Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments
Serikali imeanza utekelezaji wa bajeti mpya kwa mwaka wa fedha 2026/2027. Yale yaliyopangwa na serikali na kujadiliwa na Bunge na hatimaye yakaafikiwa katika bajeti hiyo, yameanza kufanyiwa kazi ili kufanikisha mipango ya maendeleo.

Wizara ya Fedha kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekuja na mabadiliko mbalimbali ya kodi. Mabadiliko haya yamelenga kuleta mageuzi, ufanisi na hatimaye kuongeza mapato bila kumuumiza mlipakodi ambaye ni mdau muhimu katika mipango ya maendeleo. 

Kwahiyo, kutokana na mabadiliko hayo, TRA pamoja na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA), wameratibu mafunzo kwa wahasibu, wakaguzi, wataalamu wa fedha na washauri wa kodi ili kuwajengea uwezo wa mabadiliko hayo ili ukusanyaji kodi ufanyike kwa ufanisi.

Hivyo basi, baada ya kupata mafunzo hayo, watakuwa na jukumu la kwenda kwa walipakodi na wananchi kuwaelimisha juu ya mabadiliko hayo ili kujenga uelewa wa pamoja ili yale yaliyopangwa yaweze kutimia.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Julai 8, 2026, Jijini Dar es Salaam, Meneja wa Elimu kwa Mlipakodi, CPA Paul Walalaze, ambaye alimwakilisha Kamishna Mkuu wa TRA, amesema wataalamu hao wanapaswa kunolewa ili kutambua mabadiliko ya sheria za kodi ili kuongeza tija.

"Mafunzo haya yameandaliwa ili kuwajengea uwezo wa kutekeleza vyema majukumu yenu lakini mkawasaidie walipakodi pia ili tija ipatikane," amesema CPA Walalaze.

Katika hatua nyingine, CPA Walalaze amesema, mabadiliko hayo yamehusisha Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), Sheria ya Kodi ya Mapato, Sheria ya Ushuru wa Bidhaa na Sheria ya Usajili wa Vyombo vya Moto.

Mabadiliko mengine ni Sheria ya Usimamizi wa Kodi, Sheria ya Ushuru wa Stempu, Sheria ya Uingizaji wa Bidhaa Nchini na Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ikumbukwe kuwa, mkakati wa serikali ni kuhakikisha nchi inajitegemea kibajeti kwa asilimia kubwa kwa kuimarisha ukusanyaji kodi. Tayari, katika bajeti hii ya 2026/2027, asilimia 74.2 ni mapato ya ndani. Jambo hili, linatoa dira ya kufanikiwa mipango ya maendeleo kwani makusanyo ya kodi ndiyo msingi wa kufanikisha mipango hiyo.





Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments

Makatibu Wakuu wanaosimamia sekta za Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wamekutana jijini Arusha kukamilisha maandalizi ya Mkutano wa 20 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa (Transport, Communications and Meteorology Sectoral Council – TCM), unaotarajiwa kufanyika Julai 10, 2026.

Mkutano huo wa ngazi ya Makatibu Wakuu umejadili na kupokea taarifa ya wataalamu waliokutana kuanzia Julai 6 hadi 8, 2026, kuhusu utekelezaji wa maamuzi ya mkutano uliopita wa TCM pamoja na maendeleo ya miradi na programu za kikanda zinazolenga kuimarisha miundombinu, kurahisisha shughuli za usafiri na biashara na kuongeza ushirikiano kati ya nchi wanachama.

Miongoni mwa masuala muhimu yaliyojadiliwa ni maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya barabara, reli, usafiri wa anga na majini, uboreshaji wa Vituo vya Huduma kwa Pamoja Mipakani (One Stop Border Posts – OSBPs), pamoja na kuimarisha mifumo ya ubadilishanaji wa taarifa za hali ya hewa.

Akifungua mkutano huo, Naibu Katibu Mkuu wa Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki anayesimamia Sekta za Miundombinu, Uzalishaji, Jamii na Siasa, Bw. Andrea Aguer Ariik, alibainisha kuwa EAC inaendelea kupiga hatua kubwa katika kuendeleza miundombinu ya uchukuzi na mawasiliano, hatua ambazo zinachangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi na maendeleo ya kijamii katika ukanda.

“Hadi sasa tumepiga hatua tunazostahili kujivunia. Kwa mfano, takribani kilomita 15,000 za mtandao wa reli zinatumika na kuendelea kujengwa katika nchi wanachama, hususan Tanzania na Kenya, hatua hii itachochea muunganiko wa kikanda na kurahisisha mwingiliano wa watu na bidhaa,” alisema Bw. Ariik.

Mkutano wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa ni jukwaa muhimu la kufanya maamuzi ya kisera yanayolenga kuimarisha mtangamano wa kikanda kupitia maendeleo ya miundombinu ya kisasa, usafiri salama na wenye ufanisi, pamoja na huduma bora za mawasiliano na hali ya hewa kwa manufaa ya wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo umeongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dkt. Charles Msonde, akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi – Zanzibar, Mhandisi Ali Said Bakari, Mkurugenzi Mtendaji TCAA, Dkt. Jabiri Kuwe Bakari, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASHICO), Bw. Eric B. Hamissi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Ladislaus Benedict Chang’a, pamoja na maafisa wengine waandamizi kutoka wizara na taasisi mbalimbali za Serikali.





Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments

July 09, 2026

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akepeana mkono wa maridhiano na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman baada ya utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026. 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman pamoja na Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, Amani Abeid Karume wakishuhudia utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026. Kushoto anaye saini ni Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo- Zanzibar Omary Ally Shehe pamoja na Naibu Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM- Zanzibar Dkt. Mohammed Said Dimwa
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa na Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo Taifa Mhe. Othman Masoud Othman pamoja na Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, Amani Abeid Karume wakishuhudia utiaji saini wa ajenda zilizokubaliwa na pande zote mbili kwa ajili ya kufanyiwa kazi baada ya Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, tarehe 09 Julai, 2026. Kushoto anaye saini ni Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo- Zanzibar Omary Ally Shehe pamoja na Naibu Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM- Zanzibar Dkt. Mohammed Said Dimwa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Ikulu Zanzibar kabla ya kuhudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, tarehe 09 Julai, 2026. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi wakati wakiwasili katika viwanja vya Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kuhudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, tarehe 09 Julai, 2026. 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026. 







Posted by MROKI On Thursday, July 09, 2026 No comments
Mwandishi Mwandamizi wa Gazeti la Daily News, Leonard Wilfred Mwakalabela amefariki dunia.

Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Magazeti la Serikali (TSN) Bi. Aisha Dachi imesema Mwakalebela amefikwa na umauti Julai 08, 2026. 
Posted by MROKI On Thursday, July 09, 2026 No comments

July 08, 2026




Dar es Salaam
Serikali imesema mageuzi yanayoendelea kutekelezwa katika sekta ya madini chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yameifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye mazingira bora ya uwekezaji barani Afrika, huku ikiwakaribisha wawekezaji kuwekeza katika utafiti, uchimbaji, uchenjuaji, uchakataji na uongezaji thamani wa madini.

Kauli hiyo imetolewa leo, Julai 8, 2026, na Naibu Waziri wa Madini, Mhe. Dkt. Steven Kiruswa, wakati akifungua Kongamano la Madini lililofanyika katika Ukumbi wa Dome, ndani ya Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF), maarufu Sabasaba.

Dkt. Kiruswa amesema maboresho ya sera, sheria na mifumo ya usimamizi wa sekta ya madini yameongeza uwazi, uwajibikaji na ushiriki wa sekta binafsi, hatua zilizochochea ongezeko la uwekezaji, ajira na mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Amesema Tanzania imejaliwa kuwa na rasilimali nyingi za madini mengi, ikiwemo dhahabu, almasi, tanzanite, nikeli, kinywe (graphite), nobium, madini adimu (Rare Earth Elements), pamoja na madini ya viwandani na ujenzi. 

Amebainisha kuwa Dira ya  Maendeleo ya Taifa 2050 imeweka msisitizo katika kuimarisha tafiti za kijiolojia kwa kutumia teknolojia za kisasa ili kufungua maeneo mapya ya uwekezaji.

“Serikali haiwaaliki wawekezaji kuja kuchimba madini pekee, bali pia kuwekeza katika tafiti za kijiolojia, teknolojia za uchenjuaji, uchakataji, uongezaji thamani wa madini na viwanda vinavyotumia madini kama malighafi,” amesema Dkt. Kiruswa.

Aidha, amesema Serikali imeendelea kuboresha sheria na kanuni za madini ili kuongeza ushiriki wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta hiyo kupitia matumizi ya bidhaa na huduma zinazotolewa na kampuni za wazawa. 

Ameongeza kuwa utekelezaji wa Programu ya Mining for Brighter Tomorrow (MBT) unaendelea kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalum kunufaika na fursa zinazotokana na sekta ya madini.

Dkt. Kiruswa amesema kongamano hilo linatarajiwa kufungua fursa mpya za biashara na uwekezaji, huku akiwakaribisha wadau kushiriki Mkutano wa Kimataifa wa Madini utakaofanyika Novemba 19 hadi 21, 2026, katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, kwa lengo la kuendelea kuitangaza Tanzania kama kitovu cha uwekezaji wa madini barani Afrika.

Akitoa mada kuhusu usimamizi wa leseni na biashara ya madini, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini wa Tume ya Madini, CPA Venance Kasiki, amesema Tume inaendelea kusimamia utoaji wa leseni za utafutaji, uchimbaji, uongezaji thamani na biashara ya madini kwa kuzingatia Sheria ya Madini, ili kuhakikisha rasilimali za madini zinawanufaisha Watanzania na Taifa kwa ujumla.

Amesema utoaji wa leseni unazingatia vigezo mbalimbali, ikiwemo sifa za waombaji, usajili wa kampuni na matumizi ya mifumo ya kielektroniki katika kupokea na kuchakata maombi. 

Ameongeza kuwa wamiliki wa leseni wanawajibika kutekeleza mipango ya uchimbaji iliyoidhinishwa, kulinda mazingira, kuajiri na kuwaendeleza Watanzania, pamoja na kutekeleza wajibu wa uwajibikaji kwa jamii zinazozunguka maeneo ya migodi.

CPA Kasiki amesema Serikali inaendelea kuimarisha utekelezaji wa Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania (Local Content), zinazolenga kuwawezesha Watanzania kushiriki kikamilifu katika usambazaji wa bidhaa na huduma ndani ya mnyororo wa thamani wa sekta ya madini. 

Amesema fursa hizo zinajumuisha usafirishaji, ujenzi, teknolojia, huduma za ulinzi, huduma za chakula na huduma za kifedha.

Amesisitiza kuwa usimamizi madhubuti wa leseni za madini pamoja na utekelezaji wa Kanuni za Local Content ni nguzo muhimu katika kuongeza mapato ya Serikali, kuvutia uwekezaji, kuimarisha viwanda vya uongezaji thamani na kuhakikisha wananchi wananufaika zaidi na rasilimali za madini.

Vilevile, amewahimiza Watanzania kutumia fursa zinazopatikana katika sekta ya madini kwa kuwekeza katika viwanda vinavyozalisha bidhaa na vifaa vinavyotumika migodini pamoja na kutoa huduma mbalimbali zinazohitajika katika shughuli za uchimbaji na uongezaji thamani wa madini.

Awali, Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita, Mohamed Jumanne, amesema sekta ya madini imeendelea kutoa ajira kwa maelfu ya vijana na kuchangia ukuaji wa uchumi wa maeneo yenye shughuli za uchimbaji. 

Amesema Serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano katika masuala ya ulinzi na usalama ili shughuli za uchimbaji zifanyike kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo, hatua itakayochochea maendeleo endelevu ya sekta hiyo na kuongeza mchango wake kwa uchumi wa Taifa.





Posted by MROKI On Wednesday, July 08, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo