Nafasi Ya Matangazo

August 20, 2026

NnnMkuu wa Wilaya ya Kiteto akagua miradi ya elimu yenye thamani ya Shilingi bilioni 1.37

Mkuu wa Wilaya ya Kiteto, Mhe. Remidius Mwema,tarehe 17 Agosti 2026  alifanya ziara ya ukaguzi wa miradi mbalimbali katika sekta ya elimu yenye thamani ya jumla ya Shilingi bilioni 1.37, katika Kata za Partimbo, Engusero na Laiseri.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mwema pia alizungumza na wananchi kwa kusikiliza na kutatua kero mbalimbali,akiwa katika Kata ya Laiseri, Mhe. Mwema alishuhudia mapokezi makubwa na bashasha kutoka kwa wananchi kufuatia hatua ya Serikali kutegua kitendawili cha muda mrefu cha ukosefu wa shule ya sekondari katika kata hiyo.

Serikali tayari imeanza ujenzi wa Shule Mpya ya Sekondari Laiseri, ambayo itakuwa shule ya kwanza ya sekondari katika kata hiyo.Mapema akizungumza na wananchi, Mhe. Mwema alisema:

_“Serikali imekata kiu kwa wananchi wa Kata ya Laiseri kufuatia hitaji la shule ya sekondari. Tambueni kwamba vijiji na kata zote zina usawa kimtazamo linapokuja suala la maendeleo ya wananchi, sasa Serikali imetekeleza kwa vitendo. Wito wetu kwenu ni kuendelea kutoa ushirikiano katika kipindi chote cha utekelezaji wa mradi huu,”Alisema.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mwema alitembelea na kukagua maendeleo ya miradi ifuatayo:

Ujenzi wa Shule Mpya ya Sekondari Mbeli – Kata ya Partimbo, wenye thamani ya Shilingi milioni 584.

Ujenzi wa Bweni katika Shule ya Sekondari Engusero, wenye thamani ya Shilingi milioni 204.

Ujenzi wa Shule Mpya ya Sekondari Laiseri, wenye thamani ya Shilingi milioni 584.

Miradi hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuhakikisha wananchi wa maeneo yote wanapata huduma bora za elimu.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Wilaya amesema hakuna Kijiji au kata ambayo inasahaulika linapokuja suala la maendeleo, Ujenzi wa Sekondari Laiseri ilikuwa ni hitaji muhimu na muda mrefu kwa wananchi wa kata  Laiseri, leo Serikali imetekeleza hitaji hili kubwa na itaendelea kugusa maisha ya Wananchi wote Wilayani Kiteto.






 


Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Tanga.
Ajali ya moto iliyotokea usiku wa Agosti 14, 2026, Barabara ya 12, Jijini Tanga, ambayo iliteketeza maduka 12 ya wafanyabiashara, imewaibua Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani humo, ambapo wamefika eneo la ajali na kuwapa mkono wa pole wafanyabiashara hao.

Akizungumzia suala hilo, Agosti 18, 2026, Meneja TRA mkoa wa Tanga, CPA Castro John, amesema wameguswa na tukio hilo la moto kwani wafanyabiashara ni wadau muhimu katika ulipaji kodi nchini.

"Wafanyabiashara wameunguliwa karibu vitu vyao vyote, tumekuja kuwapa pole na kuonyesha mshikamano, pia tumekuja kuwapa kiasi cha fedha kidogo kama kianzio kutokana na wengi wao kupoteza mali zao zote," amesema CPA John.

Ameongeza kuwa, TRA inawajibika si tu kukusanya kodi lakini pia kuwalea wafanyabiashara waweze kustawi na kukua kibiashara, hivyo, wanapopata majanga ya aina hiyo, wanalo jukumu la kuwashika mkono.

"TRA ina jukumu la kukusanya kodi lakini pia kuhakikisha wafanyabiashara wanastawi. Tutawaita waje ofisini tuongee nao na kuona tunawasaidiaje ili wapate unafuu wa kodi," amesema.

Katika hatua nyingine, Katibu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara mkoani humo, Ismail Masoud, amempongeza Meneje TRA mkoa na Kamishna Mkuu kwa kuthibitisha kwa vitendo kuwa wafanyabiashara ni familia moja na TRA.

Pia, ameatoa wito kwa wafanyabiashara wote wa Mkoa wa Tanga kuendelea kulipa kodi kwani kodi hizo ndizo zimesaidia hata kupata misaada hiyo.

Kwa upande wa wafanyabiashara hao, wameushukuru uongozi wa TRA kwa kuwafariji na kuwapa mkono wa pole kwani wapo katika kipindi kigumu kutokana na wengi wao kupoteza mali zao zote.
Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments




Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Ndugu Aggrey Mwanri, amekutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi wa Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) nchini Tanzania, Ndugu Xu Sujiang, huku akisisitiza dhamira ya CCM ya kuendelea kuimarisha uhusiano wa kihistoria na wa kimkakati kati ya vyama hivyo viwili.

Kikao hicho kimefanyika leo Agosti 20,2026 katika Makao Makuu ya CCM, Dodoma, ambapo Ndugu Xu ametumia nafasi hiyo kuaga rasmi kabla ya kuhitimisha majukumu yake nchini Tanzania
Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments



Na, Mwandishi wetu – Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu–Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi, amewataka wananchi kuzingatia tahadhari na maelekezo yanayotolewa na wataalamu na mamlaka husika ili kupunguza madhara yanayotokana na majanga na maafa.

Prof. Kabudi ametoa wito huo tarehe 19 Agosti, 2026 wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Watoa Huduma za Misaada ya Kibinadamu Duniani yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

“Ushiriki wa wananchi ni muhimu katika kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya majanga, huku akiwataka kuendelea kufuata taarifa na maelekezo rasmi kutoka kwa wataalamu na mamlaka zinazohusika na masuala ya maafa.”

Katika hatua nyingine, alisema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema na kujenga ustahimilivu wa jamii ili kuongeza uwezo wa wananchi kukabiliana na majanga na kupunguza madhara yanayotokana na matukio hayo.

Alisema uwezo wa nchi katika kukabiliana na majanga kwa ufanisi unategemea uwepo wa mifumo madhubuti, uratibu na ushirikiano wa karibu na wenye tija kati ya Serikali na wadau wa huduma za kibinadamu.

Prof. Kabudi pia alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake katika kusimamia masuala ya kibinadamu na ustawi wa wananchi.

“Kupitia uongozi wa Rais Dkt. Samia, Serikali imeendelea kuhakikisha wananchi wanaokumbwa na changamoto za majanga wanapata msaada na faraja wakati wa dharura.”

Prof. Kabudi aliwataka watoa huduma za kibinadamu kuwekeza zaidi katika kuwawezesha wananchi kwa elimu na taarifa sahihi kuhusu vihatarishi vinavyowazunguka, pamoja na hatua za kuchukua kabla, wakati na baada ya janga.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Dkt. James Kilabuko, amesema maadhimisho ya siku hiyo yanatoa fursa ya kutambua na kuthamini mchango wa watoa huduma za kibinadamu ambao hujitolea kwa moyo wa huruma, ujasiri na mshikamano katika kuokoa maisha na kupunguza madhara.

Alisema ni muhimu kuendelea kuimarisha ushirikiano na mshikamano miongoni mwa Serikali, wadau wa huduma za kibinadamu na jamii katika kuhakikisha kuwa msaada unapatikana kwa wakati na unawafikia wale wanaouhitaji.

“Ni muhimu kuhakikisha kuwa katika kila hatua ya utoaji wa huduma za kibinadamu, maisha, usalama na utu wa mwanadamu vinaendelea kuwa kiini cha hatua tunazochukua.”
=MWISHO=
Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments

August 19, 2026






Na. Mwandishi Wetu - Shinyanga
SERIKALI imesema itaendelea kuongeza nguvu katika mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU), kwa kuboresha vituo vya huduma, kuwezesha vikundi na kuimarisha ushirikiano na wadau, ili kuhakikisha Tanzania inafikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dk. Jim Yonazi, wakati wa ziara yake mkoani Shinyanga, ambapo alitembelea vikundi mbalimbali vya vijana vinaoishi na Maambukizi ya VVU pamoja na Kituo cha Maarifa Kahama kilichopo Kagongwa mkoani humo.

Dk. Yonazi amesema juhudi zinazofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau zimeanza kuzaa matunda, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza kasi katika utoaji wa elimu, upimaji, ushauri nasaha, pamoja na huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.

“Lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma karibu nao, lakini vilevile wanapata elimu inayowasaidia katika mapambano dhidi ya UKIMWI
na maambukizi ya UKIMWIi,” amesema.

Amesema Serikali imeendelea kuboresha huduma hizo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa wakati, huku akiwataka wadau kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha afua za kukabiliana na VVU.

Dkt. Yonazi amepongeza Mkoa wa Shinyanga kwa kufikia malengo ya kimataifa ya 95-95-95, akisema hatua hiyo ni ishara ya mafanikio katika jitihada za kupunguza maambukizi mapya na madhara yatokanayo na VVU.

“Serikali imeamua kwa makusudi kabisa kuongeza nguvu yake. Ndiyo maana imeanzisha Mfuko wa Mfadhili, na asilimia 70 ya fedha hiyo inakwenda katika Mfuko wa UKIMWI ili kusaidia afua mbalimbali na kuondokana na utegemezi,” amesema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Mhe. Mbona Mahita, alisema mkoa huo bado una kiwango cha maambukizi ya VVU kilicho juu ya wastani wa kitaifa, ambapo Shinyanga ina asilimia 5.6 ikilinganishwa na asilimia 4.4 ya kitaifa.

Mahita alisema Serikali imeendelea kuongeza elimu kuhusu VVU katika ngazi mbalimbali, kuanzia kaya hadi jamii, ili wananchi wawe na uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kujikinga na maambukizi.

“Shinyanga ni business hub kwa Kanda ya Ziwa. Movement za watu mara kwa mara ni kubwa. Watu wanaoingia na kutoka ni wengi, ndiyo maana tumeshuka mpaka kwenye ngazi za kijamii katika utoaji wa elimu,” alisema.

Awali, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Dk. Honoratha Rutatinisibwa, alisema mkoa huo una vituo 374 vinavyotoa huduma za afya, ambapo vituo 120, sawa na asilimia 32, vinatoa huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.

Dkt. Rutatinisibwa amesema, kwa mujibu wa utafiti wa maambukizi ya VVU uliofanyika mwaka 2023, kiwango cha maambukizi mkoani Shinyanga ni asilimia 5.6, ikilinganishwa na wastani wa kitaifa wa asilimia 4.4.

Akizungumzia huduma zinazotolewa katika Kituo cha Maarifa Kahama kilichopo Kagongwa, Mratibu wa Kudhibiti Maambukizi ya VVU, Homa ya Ini na Magonjwa ya Ngono Kahama, Dkt. Herry Silvester, amesema kituo hicho kinatoa huduma za tiba na matunzo, pamoja na huduma maalumu kwa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi.

Amesema makundi hayo ni pamoja na madereva wa masafa marefu, mabinti na wanawake vijana, ambao wamekuwa wakifikiwa kupitia huduma za upimaji, elimu na ushauri nasaha.
Posted by MROKI On Wednesday, August 19, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu
Ushirikiano baina ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), umeelezwa kuwa na manufaa mengi yenye mchango wa kukuza maendeleo baina ya nchi hizo mbili. 

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu (MCC), Mary Chatanda, Agosti 18, 2026.

Chatanda amesema, ziara ya siku mbili ya Rais Felix Tshisekedi wa DRC Kongo nchini Tanzania ni kielelezo cha uhusiano mzuri ambao hauishii kuwa urafiki wa kawaida bali nyenzo ya kushirikiana katika kukuza uchumi na maendeleo.

"Rais Dk. Samia na mwenzake Tshisekedi wamekubaliana kushirikiana katika kuboresha sekta za uchukuzi, madini, nishati, uwekezaji, biashara, barabara, bandari, usafiri wa majini, jambo linaloongeza kasi ya ukuaji uchumi," amesema.

Aidha, Chatanda amehimiza uzingatiaji wa maslahi ya wananchi katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa nchi zote.

"Wananchi wetu wanapaswa kunufaika na fursa za uchumi katika sekta za ushirikiano, ili maendeleo yawe jumuishi kwa serikali na wananchi wake," amesisitiza.

Katika hatua nyingine, Chatanda amempongeza Rais Dk. Samia kwa kuendelea kuifungua nchi kwa kuhimiza diplomasia ya kiuchumi kwa kushirikiana na mataifa mbalimbali duniani.

"Nampongeza Rais wetu Dk. Samia kwa namna anavyoshirikiana na mataifa mengine, kwa kufanya hivyo, tunaongeza wigo wa kupata fursa za biashara na uwekezaji," ameongeza.
Posted by MROKI On Wednesday, August 19, 2026 No comments

August 18, 2026








Na. Mwandishi Wetu, Mwanza
Serikali imedhamiria kuendelea kuimarisha afua za masuala ya UKIMWI nchini kwa kuboresha mazingira ya utekelezaji wa shughuli hizo, huku ikihimiza ushirikiano na wadau mbalimbali katika kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, alipotembelea na kujionea utekelezaji wa shughuli zinazotekelezwa na vikundi vya watu wanaoishi na Maambukuzi ya Virusi vya UKIMWI katika Wilaya ya Nyamagana, Jijini Mwanza.

Akiwa katika ziara hiyo, Dkt. Yonazi amesema Serikali imeendelea kuboresha mazingira na kutenga bajeti inayosaidia kuratibu na kutekeleza afua za masuala ya UKIMWI nchini, huku ikishirikiana na wadau mbalimbali.

“Ushirikiano ni muhimu sana kwani, tunaamini unauwezo wa kutuvusha katika mapambano dhidi ya VVU, ambapo tumeendelea kuunganisha nguvu pamoja katika mapambano hayo,” alisema Dkt. Yonazi.

Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu, yenye dhamana ya kuratibu shughuli zote za Serikali, ikiwemo masuala ya UKIMWI, itaendelea kuhakikisha vifaa na huduma zinatolewa kwa wakati na ubora kwa WAVIU, huku kanuni na taratibu za afya zikizingatiwa.

Dkt. Yonazi Ametumia jukwaa hilo kuiasa jamii kuendelea kupima afya ili kujitambua na kuchukua hatua za mapema endapo mtu atabainika kuwa na maambukizi ya VVU, ili aweze kuishi kwa tahadhari na kuwalinda wengine.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Ndugu Balandya Elikana, amesema kuwa mkoa umechukuwa hatua madhubuti kuimarisha mapambano dhidi ya UKIMWI kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya afya na kamati za utekelezaji wa mikakati ya kuzuia maambukizi, huku wakihimiza upatikanaji wa huduma bora na elimu kwa jamii. 

“Jamii inaendelea kuhamasishwa kuhusu upimaji wa afya kwa hiari na matumizi sahihi ya njia za kujikinga na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI pamoja na kuendelea kushirikiana kwa karibu na mashirika na wadau wa afya ili kuboresha huduma za kinga na tiba,” alisema Elikana

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dkt. Kheri Kagya, akiwasilisha taarifa ya hali ya UKIMWI mkoani humo, amesema Mkoa wa Mwanza una kiwango cha maambukizi ya VVU cha asilimia 4.7, ikilinganishwa na kiwango cha kitaifa cha asilimia 4.4, kwa mujibu wa matokeo ya Utafiti wa Kitaifa wa THIS 2022/2023.

Alisema kwa mujibu wa taarifa ya DHIS2 Annual Report ya mwaka 2025/2026, Mkoa wa Mwanza unakadiriwa kuwa na idadi ya watu wanaoishi na VVU (WAVIU) 112,685.

“Mkoa, kwa kushirikiana na wadau, umeendelea kutoa elimu ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya VVU kwa kuhamasisha matumizi sahihi ya kondomu. Katika kipindi cha mwaka 2025/2026, Mkoa ulisambaza jumla ya kondomu 2,265,772 katika jamii, hususani sehemu za kulala wageni, sehemu za kuuzia vileo (baa), kumbi za starehe na kwenye mikusanyiko mbalimbali,” alisema.
Posted by MROKI On Tuesday, August 18, 2026 No comments

August 16, 2026

Na: Dk. Reubeni Lumbagala 
Katika maisha ya kawaida ya mwanadamu, kuna kuweka malengo ili kufikia mafanikio. Inapotokea malengo yametimia, moyo hujaa furaha kwani mlango wa kufanikiwa unakuwa umefunguka.

Haya ndiyo yaliyotokea kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Kwa TRA, mwaka wa fedha 2026/2027 umeanza vizuri. Hii ni kufuatia Mamlaka hiyo kukusanya shilingi trilioni 3.245 kwa mwezi Julai, 2026, ambapo makusanyo hayo ni sawa na asilimia 109 ya lengo la kukusanya trilioni 2.971 kwa mwezi huo.

Ni kwamba; mwaka mpya wa fedha huanza Julai 1 ya kila mwaka. Hivyo mwezi wa kwanza wa mwaka mpya wa fedha ni kuanzia Julai 1 hadi 31. Kwa malengo ambayo TRA ilijiwekea, ni kukusanya shilingi trilioni 2.971, lakini lengo hilo limetimia na kuzidi, ambapo zimekusanywa shilingi trilioni 3.245. 

Kimsingi, bajeti iliyopitishwa na bunge kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ni shilingi trilioni 62.33, ambapo asilimia 74 ya fedha hizo zinategemewa kukusanywa kupitia mapato ya ndani (own sources).

Katika fedha hizo, TRA inawajibika kukusanya shilingi trilioni 41.08, sawa na asilimia 67 ya bajeti nzima katika kipindi cha Julai 1, 2026 hadi Juni 30, 2027.

Akiwa katika hafla ya Uwekezaji wa Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya TRA, Kizimkazi, Zanzibar, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Omar, ameipongeza TRA kwa kufanikiwa kukusanya shilingi trilioni 3.245 kwa mwezi Julai, 2026.

Naye, Kamishna Mkuu wa TRA, CPA Yusuph Mwenda, amesema wanaendelea kuwahudumia vyema walipakodi na kutatua changamoto zao ili Mamlaka ifanikishe malengo.

"Kutokana na usimamizi wako mzuri Mheshimiwa Waziri wa Fedha na ushirikiano na walipakodi, tunakuhakikishia tutavuka lengo hilo na kupitia, ishara inaonyesha kwamba tumeanza mwaka wa fedha kwa nguvu kubwa na tuna imani tutafikia na kuvuka malengo tuliyowekewa," amesema CPA Mwenda.

MAMBO YA KUZINGATIA KATIKA SAFARI YA UKUSANYAJI MAPATO WENYE TIJA

Mosi, kufanya malipo kwa njia za kieletroniki. Moja ya mabadiliko ya sheria za kodi ni pamoja na kuhimiza malipo ya kieletroniki ili kuendana na uchumi wa kidijitali unaoachana na matumizi ya fedha taslimu (cashless economy). Ni muhimu kufanya malipo kwa njia za kieletroniki kama simu na benki.

Pili, kudai na kutoa risiti halali ya kieletroniki. Ni muhimu kwa mnunuaji kudai risiti pale anapofanya malipo na muuzaji nae atoe risiti halali ya kieletroniki (EFD), ili serikali ipate kodi yake halali. Mmoja kati ya hawa wawili au wote wawili wasipotimiza wajibu wao, serikali itakosa mapato, na hivyo kushindwa kutimiza kikamilifu malengo ya kuwahudumia wananchi.

Tatu, kuwa waaminifu katika kurekodi taarifa za mauzo. Muuzaji anapaswa kuandika taarifa sahihi za mauzo ili Mamlaka iwe na taarifa sahihi za mwelekeo wa biashara au shughuli za uzalishaji zinazofanyika. Kwa mabadiliko ya sheria za kodi yaliyofanyika, udanganyifu katika uandishi wa taarifa za mauzo, adhabu yake ni mhusika kulipa mara mbili ya kiwango kilichofanyiwa udanganyifu.

Nne, kuboresha uhusiano baina ya walipakodi na TRA. Pamoja na mafanikio katika eneo la uhusiano, bado suala hili linapaswa kuhimizwa kwani walipakodi ndiyo waliobeba hatma ya maendeleo ya nchi yetu. Namna yeyote ya kuwapuuza, ni kuikosesha serikali mapato na kuua shughuli zao za uzalishaji ambazo zinachangia kutoa ajira na kuongeza mapato ya nchi.

Tano, kutoa makadirio ya kodi yanayoendana na kiwango cha biashara. Wakati mwingine, mfanyabiashara anaweza kufunga baishara pale anapokadiriwa kiwango kikubwa zaidi ya uwezo wa biashara yake. Hivyo basi, ukadiriaji kodi unapaswa kumwezesha mfanyabiashara kukua na si kumrudisha nyuma.

Sita, ajenda ya kujitegemea iwe ni ajenda ya kitaifa na si ya viongozi. Mwelekeo wa serikali ni kujitegemea kibajeti. Ajenda hii imefungamanishwa na ulipaji kodi wa hiari na wa kizalendo. Katika safari ya maendeleo ya nchi yetu wananchi na walipakodi kwa ujumla, tuone fahari kulipa kodi kwani kodi hizo ndizo zitakazotujengea heshima ya kujitegemea na kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na ya kimkakati nchini.

Saba, kutoa elimu endelevu ya kodi kwa walipakodi na wananchi. Elimu ya kodi izidi kutolewa ikizingatiwa serikali imefanya mabadiliko makubwa ya sheria za kodi. Elimu ya kodi itolewe kwa wanafunzi wa shule za msingi, sekondari na vyuo. Klabu za kodi ziimarishwe katika taasisi za elimu nchini. Pia, elimu hiyo itolewe sehemu za wazi kama sokoni, vituo vya mabasi ili kujenga uelewa mkubwa kwa wananchi. Pia, TRA iwafuate wafanyabiashara kule walipo kuwapa elimu ya kodi.

Ni faraja kuona mwaka mpya wa fedha umeanza kwa kishindo cha makusanyo yaliyozidi malengo yaliyowekwa. Nchi yetu itaendelea kupiga hatua kubwa za maendeleo endapo wananchi tutalipa kodi kwa uaminifu. Hakuna mwingine wa kutuletea maendeleo katika nchi yetu - ni sisi wenyewe tunawajibika, hivyo kodi zetu zitaamua maendeleo yetu. 

Mungu Ibariki Tanzania.

0620800462.
Posted by MROKI On Sunday, August 16, 2026 No comments

August 14, 2026







Na Mwandishi Wetu, Tanga
Katika kuhakikisha wafanyabiashara wanakuwa na uelewa wa kutosha kuhusiana na mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka 2026/2027, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Tanga, imetoa mafunzo kwa wafanyabiashara mkoani humo.

Mafunzo hayo yametolewa Agosti 12, 2026, katika Ukumbi wa YDCP Jijini Tanga. Katika mafunzo hayo, wafanyabiashara wamejengewa uwezo juu ya mabadiliko mbalimbali ya sheria za kodi yaliyofanyika ili kuiwezesha TRA kutekeleza majukumu waliyopangiwa na serikali kuu.

Akifungua mafunzo hayo, Meneja wa TRA mkoa wa Tanga, CPA. Castro John, amesema sheria zaidi ya 15 za kodi zimefanyiwa mabadiliko, hivyo wanalo jukumu la kutoa elimu kwa wafanyabiashara.

"Niwashukuru wafanyabiashara wa Tanga kwa kujitokeza kupata elimu hii muhimu kwani wafanyabiashara wanapokuwa na uelewa wa mabadiliko haya, basi utekelezaji wa ulipaji kodi utakuwa mwepesi," amesema CPA John.

Maofisa mbalimbali kutoka TRA Makao Makuu waliwaelimisha wafanyabiashara hao mabadiliko ya sheria mbalimbali za kodi ambazo utekelezaji wake una mchango wa moja kwa moja katika kufanikisha mipango mbalimbali ya kodi.

Naye, Afisa Elimu ya Mlipakodi na Mawasiliano kutoka TRA Makao Makuu, Hamisi Sanze, alitoa mada juu ya Sheria ya Kodi ya Mapato, amesema, serikali imedhamiria kuinua sekta ya madini ili iendelee kuchangia pato la taifa. 

Amesema, katika sura ya 332, serikali imetoa msamaha wa kodi ya mapato kwa mmiliki wa leseni ya uchimbaji wa madini (Mining licence) au leseni maalum ya uchimbaji madini.

Pia amesema, katika kuendelea kuweka mazingira wezeshi kwa sekta hiyo, Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) Sura 148 imeeleza kuwa, bidhaa na huduma zinazoangizwa au kununuliwa na mwenye leseni ya madini au leseni maalum ya madini zitapata msamaha wa kodi.

Aidha, msamaha huo utatumika kwa bidhaa na huduma zinazotumika katika ujenzi wa mradi wa madini na utakoma uzalishaji wa madini utakapoanza.

Katika hatua nyingine, Sanze amesema, kwa mujibu wa Sheria ya Ushuru wa Bidhaa, Sura 147; inafafanua kuwa, watoa huduma za mitandao wasio wakazi, wanatakiwa kujisajili, kupata TIN, kutoza, kuwasilisha ritani na kulipa ushuru wa bidhaa kwa huduma zinazotolewa.

Kwa upande wake, Afisa Mkuu Msimamizi wa Kodi, Salim Bakari, amesema kwa mujibu wa Sheria za Usimamizi wa Kodi, Sura ya 438 ni kwamba, mtu anayepaswa kulipa kodi kutokana na ajira, biashara na uwekezaji anatakiwa kuomba Namba ya Utambulisho wa Mlipakodi (TIN) ndani ya siku 15 tangu aanze shughuli hizo. 

Aidha, kifungu cha 73(4) kinaeleza, Kamishna Mkuu wa TRA, amepewa mamlaka ya kuuza bidhaa zilizokamatwa ambazo zinaharibika haraka kwa njia ya mnada au mauzo ya moja kwa moja

Sambamba na hilo, amesema kifungu cha 95, kinatoa onyo kwa mtu anayehusika kurekodi taarifa za uongo au zisizo sahihi kwenye vitabu vya hesabu, rejesta au mifumo, kwani kwa kufanya hivyo, atapaswa kulipa adhabu mara mbili ya kodi aliyokwepa au aliyopunguza kulipa.

Halikadhalika, Bakari, amewakumbusha wafanyabiashara wa Jiji la Tanga kuwa, serikali imetoa msamaha wa kodi kwa kipindi cha mwaka mmoja kwa mfanyabiashara anayeanza biashara kwa mtaji usiozidi milioni 200.

Pia, amewakumbusha, malipo ya ada za shule, utalii, tozo, bidhaa, huduma, ununuzi wa magari, mashamba, viwanja, yafanyike kieletroniki ili kuongeza ufanisi wa ukusanyaji mapato ya serikali.

Akihitimisha mafunzo hayo, Meneja Msaidizi Ukaguzi na Ufuatiliaji TRA mkoa wa Tanga, Daniel Ramadhani, amewasisitiza wafanyabiashara kulipa kodi kwa uaminifu mkubwa kwani ndizo zinazowezesha serikali kutoa huduma nzuri kama elimu, afya, maji, miundombinu, umeme kwa wananchi wake.

Pia, ametoa wito kwa wafanyabiashara na walipakodi kwa ujumla, kuwasilisha changamoto zao ili zifanyiwe kazi kwani wapo kwa ajili ya kuwahudumia.

Ikumbukwe kuwa, bajeti ya mwaka 2026/2027, TRA inapaswa kukusanya shilingi trilioni 41.80 ambayo ni sawa na asilimia 67 ya bajeti nzima ya shilingi trilioni 62.33. Bajeti hii ndiyo bajeti ya kwanza kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.
Posted by MROKI On Friday, August 14, 2026 No comments

August 13, 2026

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemjulia hali, Mama Fatma Karume,Mjane wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, ambaye anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Lumumba Zanzibar. Tarehe 13 Agosti 2026.


Posted by MROKI On Thursday, August 13, 2026 No comments
Mwenyekiti wa TASWA, Amir Mhando.
CHAMA cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), kimeandaa kampeni maalumu ijulikanayo kama ‘AFCON Kitaa 2027’, ambayo itazinduliwa rasmi Oktoba 30, 2026 jijini Dar es Salaam.

Kampeni hiyo ni mahususi kwa wanataaluma ya habari kwa ajili ya Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON), zitakazofanyika nchini mwaka 2027 na itahusisha matukio ambayo TASWA itayafanya kuelekea fainali hizo, ambazo Tanzania itaandaa kwa ubia na nchi za Kenya na Uganda.

Taarifa iliyotolewa na TASWA leo Agosti 13, 2026 na kusainiwa na Mwenyekiti wa wake, Amir Mhando imesema,Kampeni ya AFCON Kitaa 2027 itawafikia makundi yote katika jamii ili kuwapa hamasa ya kuchangamkia fursa za kufanyika ka
Wa michusno hiyo nchini.

"Kampeni ya AFCON Kitaa 2027 inatarajia kufikia makundi mbalimbali kuanzia wanahabari, wanamichezo, wanasiasa, wafanyabiashara, watumishi wa umma, wajasiriamali, vijana, wanawake na wanafunzi kuyataja kwa uchache, lengo Watanzania wote tuimbe wimbo mmoja kwamba AFCON 2027 ni fursa ya kitaifa," imesema sehemu ya taarifa hiyo.

Pia kuelekea uzinduzi rasmi wa AFCON Kitaa 2027, TASWA itaendesha warsha na makundi ya wanahabari kwa awamu tofauti, ikiwa ni mwendelezo wa mpango wake iliouanzisha Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam ujulikanayo kama Mustakabali wa Uandishi wa Habari za Michezo 'The Future Of Sports Journalism’.

Makundi hayo ni waandishi wa habari chipukizi, waandishi wa habari waandamizi, wachambuzi wa habari za michezo, wahariri wa habari za michezo. Pia itakutana na viongozi wa michezo wa sasa na wa zamani, lengo ikiwa ni kutazama mwelekeo wa uandishi wa habari za michezo na pia ujio wa AFCON Kitaa 2027.

Aprili 24, 2026 TASWA ilianza Awamu ya Kwanza ya Mpango wa Mustakabali wa Uandishi wa Habari za Michezo kwa kuendesha warsha iliyohusisha wanahabari chipukizi, wahariri wa habari za michezo na waandishi magwiji wa habari za michezo, ambapo mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwemo masuala ya rushwa kwenye michezo iliyotolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Posted by MROKI On Thursday, August 13, 2026 No comments

August 12, 2026

 

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Asha-Rose Migiro, amefungua rasmi Tawi la CCM Kibuteni, Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja, leo tarehe 12 Agosti 2026.

Tawi hili lina historia kubwa tangu nyakati za ASP na TANU, na ni jambo la kujivunia kuona sasa lina sura mpya inayokwenda sambamba na mahitaji na hadhi ya Chama.

Dkt. Migiro amewahimiza viongozi na wanachama kuhakikisha Tawi hilo linakuwa kituo cha uhai wa Chama, mshikamano, mafunzo, vikao na utekelezaji wa shughuli za Chama.

Pia, Katibu Mkuu amewashukuru wana-CCM wa Kibuteni kwa mapokezi mazuri, upendo na zawadi.




Posted by MROKI On Wednesday, August 12, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo