Nafasi Ya Matangazo

May 04, 2026

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SERIKALI imeanza kuvuna matokeo ya mageuzi ya kidijitali katika sekta ya habari baada ya Waandishi wa Habari 3,357 kuthibitishwa na kupatiwa ithibati ndani ya kipindi cha chini ya mwaka mmoja kupitia mfumo wa kisasa wa TAI HABARI.

Mafanikio hayo ni hatua kubwa katika kuimarisha weledi, uwajibikaji na usimamizi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini, kwa kuwa kwa mara ya kwanza sekta hiyo imeanza kuwa na mfumo rasmi, wa kidijitali na unaowezesha kuchakata maombi na kuhakiki waandishi wanaokidhi vigezo kwa mujibu wa sheria ya Huduma za Habari.

Akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa wizara hiyo, Mhe. Paul Christian Makonda, alisema kuanzia Julai 2025 hadi Aprili 2026, Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imepokea na kushughulikia jumla ya maombi 4,139 ya usajili kupitia mfumo huo wa TAI HABARI.

Kati ya maombi hayo, Waandishi wa Habari 3,357 waliokidhi vigezo vilivyoainishwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, wamepatiwa ithibati.
Katika hatua nyingine, Waziri Makonda alisema JAB imeshughulikia malalamiko 14 ya uvunjifu wa maadili ya taaluma ya habari, jambo linaloonesha kuanza kuimarika kwa mfumo wa uwajibikaji katika sekta hiyo.

Aidha, Mheshimiwa Makonda alisema Serikali kupitia JAB imeandaa mwongozo maalumu wa kisheria utakaowawezesha Waandishi wa Habari wakongwe walioathiriwa na mfumo wa ithibati kureiea katika mfumo rasmi, kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 ambayo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari.
Alisema kuwa sheria hiyo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari kwa kuweka mfumo wa kitaasis utakaosimamia sekta ya habari. 

“Mwongozo huu unaweka utaratibu wa kisheria wa kutambua na kuthibitisha umahiri wao kupitia tathmini maalumu ya uzoefu, weledi na maadili ya taaluma, na kuwawezesha kupata ithibati kwa mujibu wa sheria.” Alisema Mhe. Makonda

Hatua hii inalenga kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuhakikisha hata waandishi wa habari wenye uzoefu mkubwa
Posted by MROKI On Monday, May 04, 2026 No comments
Cosato Chumi 
Kambarage Wasira
Fatuma Kange 
Uchaguzi wa nafasi tatu za uwakilishi katika Bunge la Afrika Mashariki (EALA) umefanyika leo Mei 4, 2026 Bungeni jijini Dodoma. 

Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamewachagua wagombea watatu kuwa Wabunge wa Bunge la Jumuia ya Afrika Mashariki (EALA) katika uchaguzi uliofanyika leo Mei 04, 2026 wa kujaza nafasi tatu za Wabunge wa EALA.
 
Katika Uchaguzi huo wabunge 293 walishiriki kupiga kura hizo za ndio na NDIO na HAPANA na waliwachagua Fatma Kange, Cosato Chumi na Kambarage Wasira kuwa wabunge wa EALA.
 
Ndugu Kange alipata kura za NDIO 223 sawa na asilimia 76.1 huku  kura za HAPANA zikiwa 70.
 
Aidha wabunge 289 Sawa na asilimia 98.6 walimpa kura za NDIOndugu Cosato Chumi na kura nne zikisema HAPANA hivyo kutangazwa kuwa Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki.
 
Mtoto wa Mwanasiasa mkongwe wa Tanzania Steven Wasira Ndugu Kambarage Wasira alichaguliwa kuwa Mbunge wa Bunge la Jumuia ya Afrika Mashariki kwa kupata kura za NDIO 284 sawa na asilimia 96.9 huku kura tisa zikimkataa kwa HAPANA.

Bunge la Tanzania limetangaza kuwa uchaguzi mdogo wa kujaza nafasi tatu za uwakilishi katika Bunge la Afrika Mashariki (EALA) utafanyika Mei 4, 2026. Hatua hiyo inakuja kufuatia nafasi zilizoachwa wazi baada ya baadhi ya wabunge wa EALA kuchaguliwa kuingia katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Posted by MROKI On Monday, May 04, 2026 No comments
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Moses Manumbu akisikiliza mapigo ya moyo ya mwananchi aliyefika katika banda la JKCI Dar Group kwaajili ya kufanya uchunguzi wa afya wakati wa maonesho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi yaliyomalizika hivi karibuni Mkoani Njombe. Jumla ya watu 386 wamefanyiwa uchunguzi wa afya katika maonesho hayo.
Afisa Muuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mahawa Asenga akimpima shinikizo la damu na mapigo ya moyo mwananchi aliyefika katika banda la JKCI Dar Group kwaajili ya kufanya uchunguzi wa afya wakati wa maonesho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi yaliyomalizika hivi karibuni  Mkoani Njombe. Jumla ya watu 386 wamefanyiwa uchunguzi wa afya katika maonesho hayo.
Afisa Muuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Happiness Shirima akitoa elimu ya mtindo  bora wa maisha kujilinda na magonjwa ya moyo kwa wananchi wa Mkoa wa Njombe waliofika katika banda la JKCI Dar Group kwaajili ya kufanya uchunguzi wa afya wakati wa maonesho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi yaliyomalizika hivi karibuni Mkoani Njombe. Jumla ya watu 386 wamefanyiwa uchunguzi wa afya katika maonesho hayo.Picha na: JKCI
************
Na Mwandishi Maalumu – Njombe
Jumla ya watu 386 wamefanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi wa afya iliyofanywa  na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group.
Kambi hiyo ya siku sita ilifanyika kwenye maonesho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi yaliyomalizika hivi karibuni katika viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mwema Mkoani Njombe.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kuhitimisha kambi hiyo daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Moses Manumbu alisema kati ya watu 386 waliowahudumia 158 wamekutwa na matatizo mbalimbali ya moyo na kupewa rufaa kwaajili ya kufanyiwa uchunguzi zaidi.
“Baada ya kuwafanyia vipimo tumebaini watu wengi kuwa na matatizo ya shinikizo la juu la damu bila ya wao kujua lakini pia wengine tumewakuta na matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo na matatizo ya mishipa ya damu kuziba hivyo kuwapa rufaa kwaajili ya matibabu zaidi”, alisema Dkt. Moses.
Mtaalamu huyo wa magonjwa ya moyo alisema kwa upande wa watoto waliowahudumia waliwakuta na na matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo ambayo ni matundu na mishipa ya damu ya moyo kutokukaa katika mpangilio  wake na ugonjwa wa moyo unaosababishwa na bakteria wanaoshambulia valvu za moyo (Rheumatic Heart Diseases).
“Tunaendelea kuihamasisha jamii kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara na kujali afya zao kwani afya ndio mtaji wa maendelea, tukiwa na afya bora tutakuwa na uwezo wa kufanya kazi na kupata maendeleo”, alisema Dkt. Moses.
Kwa upande wake Bernadetha Kindu aliyefanyiwa uchunguzi wa afya katika banda la JKCI Dar Group alisema amekuwa akisumbuliwa na maumivu makali ya kichwa kwa muda mrefu bila ya kujua kama maumivu hayo ni dalili ya kuwa na ugonjwa wa shinikizo la juu la damu.
“Nawashauri wananchi wenzangu tukiona dalili zozote za ugonjwa tufike katika vituo vya afya kufanya uchunguzi, mimi nilichukulia kawaida na kutumia dawa bila ya ushauri wa daktari jambo ambalo halikuwa salama kwa afya yangu”, alisema Bernadetha.
Bernadetha alisema baada ya kuonana na daktari ameambiwa kuwa kutumia dawa bila kufanya uchunguzi wa afya kungeweza kumletea madhara makubwa kiafya lakini pia kuhatarisha maisha yake.
Naye Kazinja Ngoyai mkazi wa Songea alisema imekuwa rahisi kwake kufuata huduma bingwa bobezi za moyo katika Mkoa wa Njombe tofauti na angezifuata Dar es Salaam ingemgharimu na kuchukua muda wake mwingi.
“Tunaposikia fursa kama hizi tusiziache zipite, mfano mzuri ni mimi nimetumia masaa machache kutoka Songea hadi hapa kuja kupima moyo wangu lakini pia nimetumia gharama ndogo ya usafiri tofauti na ningezifuata Dar es Salaam”, alisema Ngoyai.
Posted by MROKI On Monday, May 04, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa William Samoei Ruto, anatarajiwa kuwasili nchini leo, tarehe 04 Mei, 2026, kwa ziara ya kitaifa ya siku mbili. 

Akiwa nchini, Rais Ruto atafanya mazungumzo ya ana kwa ana na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kabla ya viongozi hao kuongoza mazungumzo rasmi ya pamoja kati ya ujumbe wa Tanzania na Kenya, na kuzungumza na waandishi wa habari.

 Mazungumzo hayo yataangazia jitihada za kuimarisha ushirikiano wa kindugu na kimkakati kati ya Tanzania na Kenya katika biashara, uwekezaji, miundombinu, usafirishaji na maeneo mengine ya maslahi ya pamoja. 

Viongozi hao pia wanatarajiwa kushuhudia utiaji saini wa Hati za Makubaliano na Mikataba ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya, pamoja na kushiriki Jukwaa la Biashara litakalowakutanisha wafanyabiashara na wawekezaji kutoka nchi zote mbili. 

Aidha, siku ya Jumanne, tarehe 05 Mei, 2026, Rais Ruto anatarajiwa kuhutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mkoani Dodoma, ikiwa ni sehemu ya ziara yake. Siku hiyohiyo baadaye, atarejea nchini Kenya baada ya kuhitimisha ziara yake nchini.
Posted by MROKI On Monday, May 04, 2026 No comments

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya uteuzi wa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa ufundi na Umeme (TEMESA).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Moses Kusiluka, Bw. Kheri Abdul Mahimbali ameteuliwa kuwa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA).

Mahimbali aliwahi kuwa Naibu Katibu Kuu Wizara ya Nishati na Madini baadae kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Madini.


Posted by MROKI On Monday, May 04, 2026 No comments

May 03, 2026


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amempokea Ikulu jijini Dar es Salaam Rais wa Jamhuri ya Rwanda, Mheshimiwa Paul Kagame, aliyewasili nchini kwa ziara ya kikazi ya siku moja. 

Rais Dkt. Samia na mwenzake, Rais Kagame wamefanya mazungumzo ya ana kwa ana, na baadaye kuongoza mazungumzo rasmi ya uwili yaliyohusisha ujumbe wa nchi zote mbili, na kufuatiwa na mazungumzo na waandishi wa habari. 

Viongozi hao wamejadili hatua za kuimarisha ushirikiano katika biashara na uwekezaji, uchukuzi na miundombinu, nishati, ulinzi na usalama, uhamiaji, pamoja na uratibu wa misimamo ya nchi hizo mbili katika masuala ya kikanda na kimataifa. 

Akizungumza baada ya mazungumzo hayo, Rais Dkt. Samia amesema Tanzania na Rwanda zimeendelea kujenga uhusiano wa undugu, ujirani mwema na urafiki wa kihistoria, unaoakisi mshikamano wa muda mrefu kati ya wananchi wa pande zote mbili. Rais Dkt. Samia amesema biashara kati ya Tanzania na Rwanda imeendelea kukua na kufikia thamani ya shilingi bilioni 644 mwaka 2025. 

Amesema kuanzia mwaka 1990 hadi mwezi Machi, 2026, Mamlaka ya Uwekezaji Tanzania imesajili miradi 42 ya uwekezaji kutoka Rwanda yenye thamani ya dola za Marekani milioni 325.5, iliyozalisha ajira 2,225 kwa Watanzania. 

Pamoja na hatua hiyo, Rais Dkt. Samia amesema nchi zote mbili zimekubaliana kuongeza kasi ya kuondoa changamoto za kibiashara, ikiwemo vikwazo visivyo vya kikodi, ili kupanua biashara na uwekezaji, na kutumia kikamilifu fursa za soko la pamoja la Afrika Mashariki na Soko Huru la Biashara la Afrika.

Katika uchukuzi na miundombinu, Rais Dkt. Samia amesema takribani asilimia 70 ya shehena za Rwanda hupitia bandari za Tanzania, na kwamba Tanzania itaendelea kuweka mazingira bora ya kuhudumia shehena hizo, ikiwemo huduma maalum katika bandari, matumizi ya Bandari ya Dar es Salaam na Bandari ya Tanga, pamoja na maeneo ya kuhifadhi mizigo. 

Marais hao pia wamejadili uendelezaji wa miundombinu ya reli na barabara, ikiwemo mradi wa reli ya Isaka hadi Kigali, unaolenga kuharakisha usafirishaji wa bidhaa na kuongeza ufanisi wa biashara kati ya nchi hizo mbili. 

Katika nishati, viongozi hao wamejadili Mradi wa Umeme wa Maporomoko ya Rusumo, unaozihusisha Tanzania, Rwanda na Burundi, wenye uwezo wa kuzalisha megawati 80, pamoja na makubaliano ya kuuziana umeme kati ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Shirika la Umeme la Rwanda (REG), kwa ajili ya kuchochea shughuli za kiuchumi kwa manufaa ya nchi zote mbili. 

Kwa upande wake, Rais Paul Kagame amemshukuru Rais Dkt. Samia na Watanzania kwa mapokezi mazuri, akisema Tanzania ni mshirika muhimu wa Rwanda, hususan katika biashara na usafirishaji kupitia bandari zake zinazoiunganisha Rwanda na masoko ya kimataifa. 

Rais Kagame amesema Tanzania na Rwanda zinapaswa kuimarisha msingi imara wa uhusiano uliopo kwa kuendeleza ushirikiano katika maeneo ya kimkakati ili kukuza biashara, kuendeleza miradi ya pamoja na kusukuma mbele ajenda ya maendeleo ya nchi hizo mbili. 

Aidha, amesema Rwanda itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Tanzania katika kuimarisha ushirikiano ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Umoja wa Afrika na majukwaa mengine ya kimataifa, kwa manufaa ya wananchi wa nchi zote mbili. 

Ziara ya Rais Kagame nchini inadhihirisha nafasi muhimu ya Tanzania katika biashara na ushirikiano wa kikanda, kama mshirika wa karibu na lango la biashara kwa nchi jirani, huku makubaliano yaliyofikiwa yakitarajiwa kuongeza biashara, kurahisisha usafirishaji na kufungua fursa zaidi kwa wananchi wa nchi zote mbili.
Posted by MROKI On Sunday, May 03, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame akisaini Kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Rwanda uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mhe. Paul Kagame, tarehe 03 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame na ujumbe wake wakiwa katika mazungumzo na mwenyeji wake.
Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame akifuatilia kwa makini mazungumzo hayo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame kwenye mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame akizungumza na Waandishi wa Habari kufuatia Ziara yake ya Kikazi Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026.
Posted by MROKI On Sunday, May 03, 2026 No comments











Rais wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. Paul Kagame amewasili nchini kwa Ziara ya Kikazi ya siku moja yenye lengo la kuimarisha uhusiano wa uwili kati ya Tanzania na Rwanda.

Mhe. Rais Kagame anatarajia kukutana na kufanya mazungumzo  na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Inategemewa kwamba Ziara hii itadumisha mahusiano mazuri na ya kihistoria kati ya majirani hawa wawili. Ushirikiano huu umezidi kuimarika katika miaka ya hivi karibuni kwa kupitia Tume ya Kudumu ya Pamoja (JPC), ambapo Tanzania imeendelea kuwa miongoni mwa washirika wakuu watatu wa biashara wa Rwanda duniani, huku kiwango cha biashara kati ya nchi hizi kikiongezeka kila mwaka. 

Aidha, katika uwekezaji, kuanzia mwaka 1990 hadi Machi 2026, Tanzania imesajili miradi 42 ya uwekezaji kutoka Rwanda yenye thamani ya dola za Marekani milioni 325.53 na kuunda ajira 2,225 katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda, usafirishaji, huduma za kifedha, maliasili na utalii. 

Vilevile, wawekezaji wa Tanzania pia wamewekeza nchini Rwanda kupitia kampuni mbalimbali zikiwemo Bakhresa Group, Magodoro Dodoma, Discount Center, Jambo Plastic, Sagar Enterprises, Buffalo Travelling Tours, Maxcom Africa, Gasabo Grain Milling Company, LCM Delta Company na Metrex Integrated Consultancy.
Posted by MROKI On Sunday, May 03, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu, Njombe
Njombe. CRDB Bank Plc imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuunga mkono wafanyakazi na maendeleo ya taifa kwa kudhamini na kushiriki kikamilifu maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani kwa mwaka 2026 yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe.

Maadhimisho hayo yameongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, yakikusanya mamia ya wafanyakazi kutoka sekta mbalimbali, taasisi za umma na binafsi, pamoja na wadau wa maendeleo kwa lengo la kutambua mchango wa wafanyakazi katika kukuza uchumi wa nchi.
Kupitia ushiriki wake, CRDB imeungana na Watanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa kusherehekea nafasi ya wafanyakazi katika kuimarisha uzalishaji, ubunifu na ustawi wa jamii. Benki hiyo imekuwa miongoni mwa taasisi zinazoendelea kusisitiza umuhimu wa mazingira bora ya kazi na uwekezaji katika rasilimali watu kama msingi wa maendeleo endelevu.

Ujumbe wa benki hiyo katika maadhimisho hayo uliongozwa na Mkurugenzi wa Rasilimali Watu, Godfrey Rutasingwa, aliyeambatana na timu ya wataalamu kutoka makao makuu, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini pamoja na matawi mbalimbali ya mkoani Njombe.
Akizungumza pembeni mwa maadhimisho hayo, Rutasingwa alisema ushiriki wa CRDB katika Mei Mosi unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuthamini wafanyakazi wake na kuchangia ustawi wa jamii kwa ujumla.

Alibainisha kuwa CRDB imeendelea kuwekeza katika maendeleo ya wafanyakazi wake kupitia mafunzo endelevu, kuboresha mazingira ya kazi na kutoa motisha mbalimbali zinazolenga kuongeza tija na ubunifu kazini.

“Wafanyakazi ndio injini ya mafanikio ya taasisi yoyote. Ndiyo maana sisi kama CRDB tunaendelea kuhakikisha tunajenga mazingira rafiki yanayowawezesha kufanya kazi kwa ufanisi na ubunifu zaidi,” alisema.

Aidha, aliongeza kuwa benki hiyo itaendelea kushirikiana na serikali na wadau wengine katika kusaidia juhudi za kukuza uchumi jumuishi unaowanufaisha Watanzania wengi zaidi.
Maadhimisho ya mwaka huu yameongozwa na kaulimbiu isemayo “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” ikisisitiza umuhimu wa ajira zenye hadhi, haki na usawa katika kufikia malengo ya maendeleo ya muda mrefu.

Ushiriki wa CRDB katika tukio hilo umeendelea kudhihirisha nafasi ya sekta ya fedha katika kusaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi, huku benki hiyo ikiendelea kuwa mshirika muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi imara na shindani.
Posted by MROKI On Sunday, May 03, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo