Nafasi Ya Matangazo

May 18, 2026


 

Posted by MROKI On Monday, May 18, 2026 No comments



Na, Mwandishi wetu - Pwani
Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge, amekutana na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, katika ziara maalum ya kutembelea, kukagua na kutoa elimu katika Kituo cha Maarifa cha Mdaula kilichopo Chalinze, Mkoa wa Pwani.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 18 Mei, 2026 ambapo Dkt. Yonazi alipata fursa ya kupokea taarifa ya maendeleo ya Mkoa wa Pwani, hususan katika utekelezaji wa Afua za masuala ya UKIMWI hasa huduma na mipango inayohusu WAVIU (Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI).

Taarifa hiyo ilieleza hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali pamoja na wadau wa maendeleo katika kuboresha huduma za afya na ustawi wa jamii kwa wananchi wa mkoa huo.

Aidha kwa upande wake amesema Serikali kwa sasa imeongeza bajeti katika hutuma za VVU na UKIMWI ii kungeza ufanisi zaidi katika kuwahudumia wananchi.

Zahanati ya Mdaula ilianza kutoa huduma za afya mwezi Oktoba mwaka 2022, ikiwa ni pamoja na huduma za wagonjwa wa nje, huduma za mama na mtoto, uzazi pamoja na huduma za chanjo kupitia kliniki tembezi. Kwa sasa, zahanati hiyo ina tawi dogo lililopo kandokando ya barabara ambalo linatoa huduma za maarifa ya jamii kwa wananchi na wasafiri wanaopita katika eneo hilo.

Tawi hilo lilifanyiwa maboresho na Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) kupitia Mradi wa SATTF uliokuwa unasimamiwa na TANROADS wakati wa utekelezaji wa ujenzi wake. Maboresho hayo yamelenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa elimu na huduma zinazohusiana na mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI pamoja na huduma nyingine za afya ya jamii.
Posted by MROKI On Monday, May 18, 2026 No comments

 


Posted by MROKI On Monday, May 18, 2026 No comments



Na Mwandishi Wetu, Tabora
Uongozi wa Soko la Madini Nzega mkoani Tabora umempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuanzisha masoko ya madini nchini, hatua iliyotajwa kuleta mapinduzi makubwa katika biashara ya madini kwa kuongeza uwazi, usalama na ufanisi wa shughuli za kibiashara.

Akizungumza katika Soko la Madini Nzega, Katibu wa Soko hilo na mfanyabiashara wa madini, Revocatus Chungu, amesema kuanzishwa kwa masoko rasmi kumewasaidia wafanyabiashara kupata maeneo salama na yenye utaratibu mzuri wa kufanya biashara, tofauti na hapo awali ambapo walikosa mifumo thabiti na kukumbwa na changamoto ikiwemo utapeli kutoka kwa watu wa kati.

Ameeleza kuwa kupitia masoko hayo, biashara za madini sasa zinafanyika kwa uwazi zaidi, Serikali ikiongeza ukusanyaji wa mapato huku wananchi wanaojishughulisha na sekta hiyo wakinufaika moja kwa moja na shughuli za madini.

Chungu ameongeza kuwa masoko ya madini yamerahisisha taratibu za biashara, kuharakisha huduma kwa wafanyabiashara pamoja na kuongeza ajira na kuchochea ukuaji wa uchumi wa wananchi katika maeneo yanayozunguka masoko hayo.

Kwa upande wake, mfanyakazi wa kampuni ya Banjul Limited, Hussein Sadala, ameipongeza Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Tabora kwa ushirikiano wanaoutoa kwa wadau wa sekta ya madini, akisema hali hiyo imeongeza uwazi na kurahisisha shughuli za biashara.

Amesema uwepo wa masoko ya madini umeondoa changamoto ya kutafuta wateja kwani wanunuzi na wauzaji sasa hukutana moja kwa moja katika soko rasmi, jambo linaloongeza uaminifu, ushindani wa haki na ufanisi wa biashara ya madini nchini.
Posted by MROKI On Monday, May 18, 2026 No comments
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, akizungumza na waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Kondoa Mjini, Jimbo la Kondoa, Dayosisi ya Dodoma leo tarehe 17 Mei, 2026. 

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amewahimiza wananchi kuendelea kuiombea Tanzania ili amani, umoja na mshikamano wa kitaifa viendelee kuimarika sambamba na nchi kuendelea kupiga hatua za maendeleo katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Amesema hayo leo Jumapili, Mei 17, 2026 aliposhiriki ibada katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Kondoa Mjini, Jimbo la Kondoa, Dayosisi ya Dodoma.

Ibada hiyo iliongozwa na Msaidizi wa Askofu wa Dayosisi ya Dodoma, Stanley Makasi Tabulu pamoja na Mchungaji Kiongozi wa Usharika wa Kondoa Mjini na Mkuu wa Jimbo la Kondoa KKKT, Eliezer Mbwambo.

Waziri Mkuu amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anaendelea kushirikiana na taasisi za dini nchini akitambua mchango wake katika kujenga jamii yenye maadili, umoja na maendeleo.

“Ujumbe wake kwa wananchi wa Kondoa ni kwamba tuendelee kuiombea nchi yetu ili iendelee kuwa ya amani na kuendelea kupiga hatua za maendeleo,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopo kwenye Ilani ya Uchaguzi ikiwemo ujenzi wa daraja la kuingia Kondoa Mjini pamoja na daraja la barabara ya kuelekea Hanang.

“Tumebeba jambo la daraja la kuingia hapa Kondoa Mjini… hilo tutaanza nalo. Lakini la pili ni daraja la kuelekea Hanang ambalo na lenyewe kero yake ni kubwa sana,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea na maandalizi ya utekelezaji wa mfumo wa elimu ya lazima wa miaka 10 unaotarajiwa kuanza mwaka 2028.

“Hatutakuwa na jambo linaloitwa mtoto amemaliza darasa la saba. Tunaenda kuondoa mfumo wa kuishia darasa la saba ili elimu ya lazima iwe miaka 10,” amesema.

Amesema utekelezaji wa mfumo huo unahitaji ushiriki na hamasa kutoka kwa Watanzania wote kutokana na umuhimu wa mabadiliko hayo katika sekta ya elimu nchini.

Kwa upande wake, Msaidizi wa Askofu wa Dayosisi ya Dodoma, Stanley Makasi Tabulu ameishukuru Serikali kwa kuendelea kushirikiana na taasisi za dini nchini.

“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa ushirikiano na sisi watu wa imani na viongozi wa dini,” amesema.

Aidha, amesema kanisa linaendelea kumuombea Waziri Mkuu pamoja na viongozi wa Serikali ili waendelee kulitumikia taifa kwa hekima na uadilifu.
Posted by MROKI On Monday, May 18, 2026 No comments

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, akizungumza na wananchi waliojitokeza katika mkutano wake wa hadhara alioufanya katika Uwanja wa shule ya msingiKambi ya Nyasa, Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma leo tarehe 17 Mei, 2026.
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, akizungumza na wananchi waliojitokeza katika mkutano wake wa hadhara alioufanya katika Uwanja wa shule ya msingiKambi ya Nyasa, Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma leo tarehe 17 Mei, 2026.

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, akizungumza na Ndg. Mursali Mustafa Issa ambaye ni mlemavu wa viungo katika Uwanja wa shule ya msingiKambi ya Nyasa, Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma leo tarehe 17 Mei, 2026 alipokuwa akifanya Mkutano wa hadhara na wananchi wa Wilaya hiyo.

*************
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha miradi yote ya maendeleo iliyopungua kasi ya utekelezaji inaanza tena kutekelezwa kwa kasi inayotakiwa ili wananchi waendelee kunufaika na huduma za kijamii na kiuchumi.


Amesema hayo leo Jumapili, Mei 17, 2026, alipowahutubia wananchi wa Wilaya ya Chemba katika Viwanja vya Shule ya Msingi Kambi ya Nyasa, akiwa katika ziara ya kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi.

Dkt. Mwigulu amesema baadhi ya miradi ilipungua kasi baada ya Serikali kuelekeza nguvu kubwa katika kukamilisha miradi ya kimkakati ya kitaifa iliyokuwa imefikia hatua za mwisho, ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, reli ya kisasa pamoja na Daraja la Kigongo–Busisi.

 “Kilichosababisha baadhi ya miradi kupungua kasi haikuwa uzembe wala kupuuza. Ilikuwa ni mkakati wa kukamilisha miradi iliyokuwa imekaribia kukamilika ili ianze kutumika,” amesema.

Amesema Serikali sasa imeweka kipaumbele katika kuhakikisha miradi yote iliyokuwa imepungua kasi inaanza tena kutekelezwa, huku miradi ambayo mikataba yake tayari imesainiwa ikitengewa fedha za kuanza kazi.

Kuhusu Mradi wa Bwawa la Farkwa, Dkt. Mwigulu amesema mradi huo, unaokadiriwa kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 312, utaanza kutekelezwa mara baada ya kukamilika kwa taratibu za kimanunuzi.

“Tunapoanza bajeti mpya naamini mtakuwa mmeanza kuona mkandarasi akiwa eneo la mradi kutekeleza mradi huo wa kihistoria,” amesema.

Amesema Serikali imeelekeza miradi mipya ya maji ibuniwe kwa namna itakayotoa huduma ya maji kwa matumizi ya nyumbani, mifugo na shughuli za kilimo.

Aidha, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta za afya, elimu, maji na nishati, hatua ambayo imebadili kwa kiwango kikubwa maisha ya wananchi.

Katika sekta ya afya, amesema Serikali imejenga hospitali za wilaya zaidi ya 100, vituo vya afya zaidi ya 600 na zahanati zaidi ya 2,700, sambamba na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa vya uchunguzi katika hospitali za rufaa na za kanda.

Katika sekta ya elimu, amesema Serikali imejenga shule za amali 103, zikiwemo shule 29 za mkondo wa uhandisi, pamoja na kuendelea kuongeza miundombinu ya shule za msingi na sekondari nchini.

Kuhusu nishati, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imejipanga kumaliza changamoto ya kukatika kwa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa Gridi Imara wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 1.1. 

“Mkiona umeme unakatika katika baadhi ya maeneo siyo upungufu wa umeme tena. Changamoto ipo kwenye uimara wa gridi kutokana na ongezeko kubwa la matumizi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameagiza viongozi na watendaji kuacha vitendo vya ukamataji usio na msingi pamoja na kushikilia vitendea kazi vya wananchi kwa makosa madogo.

 “Haya mambo ya kushikilia vitendea kazi vya wananchi tuachane nayo. Mtu anafanya shughuli yake ya kujitafutia kipato halafu mnachukua kitendea kazi chake; hiyo ni kuua mtaji na maisha ya familia yake,” amesema.

Amesema Serikali itaendelea kulinda haki za wananchi na kuhakikisha sheria hazitumiki kuwaonea wananchi au kuwanyima fursa za kufanya shughuli halali za uzalishaji.

Aidha, amesema Serikali inaendelea na hatua za kuifuta sheria ya kutaifisha mali ambayo imekuwa ikitumika vibaya katika baadhi ya maeneo na kusababisha wananchi kupoteza mali zao isivyo halali.
Posted by MROKI On Monday, May 18, 2026 No comments

May 16, 2026





Na Mwandishi wetu, Tabora
Serikali imewataka wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza katika sekta ya madini mkoani Tabora ili kuchochea ukuaji wa uchumi, kuongeza ajira na kuinua kipato cha wananchi, kufuatia uwepo wa rasilimali nyingi za madini ambazo bado hazijatumika ipasavyo.

Akizungumza mkoani humo, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Tabora, Fatuma Kyando, amesema mkoa huo ni miongoni mwa maeneo yenye utajiri mkubwa wa madini nchini ukiwa na dhahabu, vito, chuma, chokaa pamoja na madini mengine yenye thamani kubwa kiuchumi, hali inayotoa fursa pana za uwekezaji katika uchimbaji, uchenjuaji na uongezaji thamani wa madini.

Amesema Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia mitaji mipya, huku akisisitiza kuwa uwekezaji unaozingatia sheria, kanuni na miongozo ya nchi utawezesha wananchi na Taifa kunufaika zaidi na rasilimali hizo.

Amewataka wawekezaji kuchangamkia fursa za utafiti, uchimbaji, uchenjuaji, uuzaji na uongezaji thamani wa madini.

Kyando amesema bado kuna upungufu wa mitambo ya kisasa ya uchimbaji na uchenjuaji madini, akibainisha kuwa kwa sasa mkoani Tabora kuna mitambo minne pekee inayomilikiwa na sekta binafsi, kiwango ambacho hakikidhi mahitaji ya wachimbaji waliopo.

Kutokana na hali hiyo, amewahimiza wawekezaji kuwekeza katika teknolojia za kisasa zitakazoongeza ufanisi wa uzalishaji, kuboresha usalama migodini na kuongeza mapato kwa wachimbaji pamoja na Serikali.

Ameongeza kuwa eneo la uongezaji thamani lina fursa kubwa zaidi kupitia uwekezaji katika uchakataji wa mawe kwa ajili ya utengenezaji wa tiles, kokoto, paving blocks na bidhaa nyingine za ujenzi, hatua itakayochochea viwanda vya ndani na kuongeza thamani ya madini kabla ya kuuzwa.

Aidha, amesema bado kuna maeneo mengi yenye madini ambayo hayajafanyiwa utafiti wa kina, hivyo uwekezaji katika tafiti za madini unahitajika ili kugundua maeneo mapya ya uchimbaji na kupanua wigo wa shughuli za madini mkoani humo.

Kyando pia amesisitiza umuhimu wa kuanzishwa kwa maabara ya kisasa ya upimaji wa sampuli za madini ndani ya Mkoa wa Tabora ili kupunguza gharama na muda kwa wachimbaji wanaolazimika kufuata huduma hizo nje ya mkoa.

Amehitimisha kwa kuzitaka kampuni na wawekezaji binafsi kutumia fursa zilizopo katika biashara na huduma mbalimbali zinazohusiana na sekta ya madini, akieleza kuwa hatua hiyo itaimarisha uchumi wa mkoa wa Tabora na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika maendeleo ya Taifa.
Posted by MROKI On Saturday, May 16, 2026 No comments










Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi, Dkt. Asha-Rose Migiro, kwa nyakati tofauti amekutana na kufanya mazungumzo na mabalozi wawili wanaoziwakilisha nchi zao katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mazungumzo hayo yamefanyika katika ofisi ndogo ya makao makuu  CCM, Lumumba, jijini Dar es salaam.
Mabalozi hao ni Mheshimiwa Yordenis Despaigne Vera, Balozi wa Jamhuri ya Cuba na Mheshimiwa Vu Thanh Huyen, Balozi wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Viet Nam, wote wenye makaazi yao nchini Tanzania.

Mazungumzo hayo yalijikita katika kuendeleza na kuimarisha ushirikiano wa kihistoria kati ya CCM na vyama rafiki vya CPC–Cuba na CPV–Viet Nam, hususan katika maeneo ya uongozi, mshikamano wa vyama vya siasa na maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizi mbili.

Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa CCM, Dkt Migiro, alifanya mazungumzo na Mheshimiwa Susan Ngongi Namondo, Mwakilishi Mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania, ambapo walijadiliana vipaumbele vya maendeleo ya jamii katika utekelezaji wa baadhi ya maeneo yaliyomo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025–2030 ambayo yanawiana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,  na Malengo ya Maendeleo ya Kimataifa (SDGs).
Posted by MROKI On Saturday, May 16, 2026 No comments







Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Riziwan Kikwete, amewataka viongozi wanaochipukia nchini kutumia elimu na mafunzo ya uongozi waliyoipata kwa manufaa ya taifa na jamii kwa ujumla.

Waziri Kikwete ametoa kauli hiyo leo Mei 15, 2026 aliposhiriki Mahafali ya Tisa ya Wahitimu wa Kozi za Uongozi yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam, ambapo pia aligawa vyeti kwa wahitimu wa programu mbalimbali za uongozi.

Kozi hizo zimehusisha mafunzo ya Wanawake Viongozi, Viongozi Wanaochipukia pamoja na kozi za uongozi katika madaraja tofauti kwa lengo la kukuza uwezo wa viongozi katika taasisi za umma na binafsi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Kikwete amesema nidhamu na uadilifu ni msingi muhimu wa maendeleo ya taifa na kwamba viongozi wakizingatia maadili hayo wataweza kuleta mabadiliko chanya nchini na barani Afrika kwa ujumla.

“Nidhamu na uadilifu vikizingatiwa ipasavyo vitaweza kuiponya Tanzania na Afrika kwa ujumla,” amesema Waziri Kikwete.

Aidha, amesema kozi hizo zinazoendeshwa na Taasisi ya Uongozi kwa kushirikiana na Vyuo vya Aalto cha Finland na Yale cha Marekani zina mchango mkubwa katika kuandaa kizazi cha viongozi wenye uwezo, weledi na maadili ya uongozi bora.
Posted by MROKI On Saturday, May 16, 2026 No comments

May 15, 2026





Na Mwandishi wetu,Dodoma
Vituo vya kutolea huduma za afya vimetakiwa kuboresha maoteo ya uagizaji wa dawa na kuzingatia mwenendo wa magonjwa katika maeneo yao ili kuhakikisha bidhaa za afya zinapatikana wakati wote na kuondokana na changamoto ya wananchi kukosa bidhaa hizo wanapohitaji huduma.

Kauli hiyo imetolewa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dkt. Thomas Rutachunzibwa, leo Mei 15, 2026 Jijini Dodoma wakati akifungua kikao kazi cha wateja na wadau wa Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya Dodoma inayohudumia Mikoa ya Dodoma, Singida pamoja na Halmashauri ya Kiteto ya Mkoa wa Manyara.

“MSD inafanya kazi kubwa ya kuhakikisha bidhaa muhimu za afya zinapatikana, zinatunzwa na kusambazwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini. Ni muhimu kwa vituo vya afya kufanya maoteo sahihi ya mahitaji yao ili kuondoa malalamiko ya wananchi kuhusu ukosefu wa dawa,” amesema Dkt. Rutachunzibwa.

Amesema serikali inaendelea kuweka kipaumbele kuhakikisha nidhaa za afya ziinapatikana wakati wote ili wananchi waendelee kupata huduma bora za afya.

Dkt. Rutachunzibwa amewataka watendaji wa sekta ya afya Halmashuari za Wilaya kushirikiana na wafamasia pamoja na wataalam wa maabara kupanga mahitaji ya dawa na kuhakikisha bidhaa hizo zinatengewa bajeti pamoja na kuwepo fedha za manunuzi.

“Kwa nini tuwe na dawa zinaharibika kutokana na kuagiza bidhaa nyingi kuliko mahitaji halisi wakati bado kuna wananchi wanahitaji huduma hizo? Ni muhimu kuboresha maoteo na kuagiza dawa kulingana na mwenendo wa magonjwa katika maeneo husika,” amesisitiza.

“Asitokee mtu mmoja anatengeneza oda na kuleta dawa ambazo hazihitajiki na kufanya tuwe na dawa zinazokwenda kuharibika bila matumizi,” amesema Dkt. Rutachunzibwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ugavi na Uendeshaji wa MSD, Hassan Ibrahim, amesema ushirikiano na mawasiliano ya karibu kati ya wadau wa sekta ya afya ni muhimu katika kuhakikisha changamoto za mnyororo wa ugavi zinatatuliwa kwa wakati.

“Tunatamani tuwe tunaongea lugha moja katika kutatua changamoto za mnyororo wa ugavi wa bidhaa za afya ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora,” amesema Hassan.

Naye Meneja wa MSD Kanda ya Dodoma, Mwanashehe Jumaa, amesema jukumu kubwa la MSD ni kuhakikisha bidhaa za afya zinapatikana kwa wakati kwa wateja wake kupitia ushirikiano wa karibu na wadau wa mnyororo wa ugavi.

Amesema vikao hivyo vinasaidia kupata mrejesho kutoka kwa wateja na kujadili namna bora ya kuboresha upatikanaji wa bidhaa za afya.

Kwa upande wake, Katibu wa Afya wa Wilaya ya Chamwino, Loveness Raphael, amepongeza utaratibu wa MSD wa kukutana mara kwa mara na wadau wa sekta ya afya kwa kuwa unasaidia kujadili changamoto na kuweka mikakati ya kuboresha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba kwa wananchi.
Posted by MROKI On Friday, May 15, 2026 No comments






Na Mwandishi Wetu, Shinyanga
Kuanzishwa kwa masoko ya madini ya almasi na dhahabu mkoani Shinyanga kumechochea kwa kasi ongezeko la uzalishaji, biashara na mapato ya Serikali, huku wachimbaji na wafanyabiashara wakinufaika na kusogezewa huduma karibu nao.

Akizungumza katika Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Shinyanga, Mthaminishaji wa Madini ya Almasi, Shikimayi Muyinza, amesema uzalishaji wa almasi umeongezeka kwa kiwango kikubwa kutokana na kuibuka kwa machimbo mapya pamoja na uwepo wa masoko rasmi ya madini yaliyorahisisha biashara na kuongeza uwazi.

Amesema awali uzalishaji ulitegemea zaidi eneo la Maganzo karibu na Mwadui, lakini tangu mwaka jana machimbo mapya ya Ng’wapangabule yameongeza uzalishaji kwa kiasi kikubwa kutokana na kuongezeka kwa wachimbaji wadogo.

Kwa mujibu wa Muyinza, mwezi Aprili 2026 pekee karati 6,177 za almasi zilinunuliwa sokoni, tofauti na hapo awali ambapo uzalishaji haukuwa ukifikia hata karati 1,000 kwa mwezi.

“Hili ni ongezeko kubwa sana. Sasa tunapata kati ya karati 3,000 hadi 6,000 kwa mwezi kutokana na vyanzo vipya vya uchimbaji na masoko ya madini,” amesema.

Ameeleza kuwa masoko ya madini yameongeza ufanisi wa huduma kwa kutoa uthaminishaji wa haraka na wa uwazi, ambapo wachimbaji husajiliwa, madini hupimwa na kupatiwa ushauri wa thamani kabla ya kuingia kwenye mauzo.

Muyinza amefafanua kuwa tofauti na dhahabu, bei ya almasi hutegemea sifa nne muhimu ambazo ni ukubwa, umbo, rangi na ubora wa ndani wa jiwe, hivyo kila almasi huwa na thamani yake ya kipekee.

Kwa upande wake, Mhandisi wa Migodi na Msimamizi wa Masoko Mkoa wa Shinyanga, Gerald Kabeho, amesema mfumo wa masoko ya madini umeondoa urasimu uliokuwepo awali na kurahisisha upatikanaji wa huduma zote muhimu ndani ya muda mfupi.

Naye Mkurugenzi wa Mwabu General Trading, Samweli Sita, amesema masoko hayo yamewaondolea wafanyabiashara changamoto ya kutafuta wanunuzi kwani sasa wauzaji na wanunuzi hukutana moja kwa moja sokoni na kufanya biashara kwa uwazi.

Aidha, amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuanzisha masoko ya madini nchini, hatua aliyosema imeongeza fursa za biashara, kuimarisha uchimbaji halali na kukuza sekta ya madini kwa wachimbaji wadogo na wakubwa.

Takwimu zinaonesha kuwa mafanikio hayo pia yameongeza makusanyo ya Serikali ambapo kuanzia Julai hadi Aprili mwaka wa fedha 2025/2026, Mkoa wa Shinyanga umekusanya shilingi bilioni 35.2, sawa na asilimia 110 ya lengo la shilingi bilioni 32, ikiashiria mchango mkubwa wa masoko ya madini katika kukuza uchumi wa taifa.
Posted by MROKI On Friday, May 15, 2026 No comments






Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Waziri wa Maliasili na Utalii, Ashatu Kijaji ametembelea banda la Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika maonesho ya Wizara ya Maliasili na Utalii yanayoendelea kwenye viunga vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Dodoma.

Mhe. Dkt. Kijaji, akiambatana na viongozi mbalimbali wa wizara hiyo, alifanya ziara hiyo mara baada ya kuwasilisha bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni mapema leo.

Katika ziara hiyo, Waziri alipata fursa ya kujionea na kupata maelezo kuhusu shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazotekelezwa kupitia sekta ya misitu nchini, ikiwemo uhifadhi wa misitu, utalii wa mazingira, uzalishaji wa mazao ya misitu pamoja na mchango wa sekta hiyo katika kukuza uchumi wa taifa.

Aidha, banda la TFS limeendelea kuvutia wadau mbalimbali wanaotembelea maonesho hayo kutokana na ubunifu na maonesho ya shughuli za uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.

Pamoja na mambo mengine, banda hilo pia linatoa huduma ya tiba ya kudungwa na nyuki (Api-Therapy) bure kwa wananchi wanaotembelea maonesho hayo. Huduma hiyo ni sehemu ya juhudi za TFS kuelimisha Watanzania kuhusu manufaa ya uhifadhi wa mazingira kupitia matumizi ya tiba za asili zinazotokana na rasilimali za misitu.

Kwa mujibu wa Mhifadhi wa TFS ambaye ni Afisa Nyuki kutoka Hifadhi ya Mazingira Asilia ya Vikindu, Brenda Mwakipesile alisema huduma hiyo inalenga kusaidia kuimarisha kinga ya mwili, kupunguza maumivu ya viungo, kuboresha mzunguko wa damu pamoja na kusaidia afya ya akili.

“Tumeileta huduma hii bure kwa wananchi ili kuwaonesha kuwa uhifadhi wa misitu hauishii kwenye miti pekee, bali pia unaweza kuzaa tiba za asili ambazo ni salama na zenye manufaa ya kiafya,” alisema Mhifadhi Brenda.

Katika maonesho hayo, viongozi mbalimbali waliotembelea banda la TFS leo pia walipata huduma ya kudungwa na nyuki kama sehemu ya kujionea kwa vitendo huduma hiyo ya tiba asilia, kama wanavyoonekana pichani.
Posted by MROKI On Friday, May 15, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo