Nafasi Ya Matangazo

February 04, 2026

Baada ya ufanisi mkubwa wa biashara kwa mwaka 2025 uliochangia kupata faida ya zaidi ya shilingi trilioni 1.04, Benki ya CRDB leo imezindua kampeni yake ya mwaka 2026 inayoitwa ‘Benki Kimpango Wako’ inayolenga kuboresha huduma kwa wateja kwa kupunguza muda wa kukamilisha muamala na kumruhusu mteja kujihudumia vile atakavyo, kwa muda wake akiwa mahali popote duniani.

Kampeni hiyo imezinduliwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela ambaye amewashukuru wateja, wawekezaji, wabia wa kimkakati pamoja na wadau wote kwa ujumla kwa imani waliyonayo kwa benki hiyo kubwa zaidi nchini.

“Mwaka jana tumepata faida kubwa kutokana na ushirikiano mkubwa tulioupata kutoka kwa wateja binafsi, wajasiriamali, taasisi, mashirika na serikali pamoja na wabia wetu. Ninyi ndiyo sababu ya uwepo wa Benki ya CRDB. Kila akaunti mliyofungua, mkopo mliouchukua, kila muamala mlioufanya, na kila mradi mlioutekeleza kupitia Benki ya CRDB vilitupa nguvu na ari ya kujituma zaidi. Ninaamini na kuomba ushirikiano huu uendelea mwaka huu pia,” amesihi Nsekela.

Mwaka 2025, Benki ya CRDB imepata faida ya shilingi trilioni 1.04 kabla ya Kodi sawa na ukuaji wa asilimia 33, huku faida baada ya kodi ikifika shilingi bilioni 725 likiwa ni ongezeko la asilimia 31 ikilinganishwa na mwaka 2024. Mizania yake nayo imeongezeka na kufika shilingi trilioni 22.2 sawa na ukuaji wa asilimia 33 na ndani ya kipindi hicho imetoa mikopo kiasi cha shilingi trilioni 13.7 sawa na ukuaji wa asilimia 32.6.
Ukuaji huo, Nsekela amesema unamaanisha uwezo mkubwa zaidi wa kufadhili miradi ya maendeleo, kusaidia kukuza mitaji ya biashara ndogo, za kati na kubwa, kuongeza uzalishaji, kutoa ajira mpya, na kuwawezesha vijana, wanawake na wajasiriamali kutimiza malengo yao ya kiuchumi.

Mafanikio haya yana akisi ushirikiano wa wadau wetu wote. Tutaendelea kutekeleza azma yetu ya kuboresha maisha ya watu wetu na uchumi wa Taifa letu pamoja na masoko mengine ambako benki yetu inatoa huduma. Sisi ni Benki Inayomsikiliza Mteja na kwa kufanya hivyo tunapata syluhisho la kila changamoto ya mteja,” amesema Nsekela.
Kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, kuongezeka kwa ushindani wa kibiashara na upangaji wa mikakati binafsi ya kiuchumi na maendeleo, Nsekela amesema wateja wanahitaji huduma za fedha ambazo ni rahisi, za haraka, na zinazoendana na mikakati waliyonayo ndio maana Benki ya CRDB imekuja na kampeni ya Benki Kimpango Wake ikikusudia na kuahidi kutoa kipaumbele kwa wateja na wadau wengine ambao ni sehemu ya mafanikio yake ya kibiashara.

Jitihada hizi za kuboresha na kuimarisha huduma kwa wateja na wadau wengine wa Benki ya CRDB, Nsekela amesema zilizanza mwaka jana pale walipofanya maboresho ya mfumo mkuu wa uendeshaji (core banking system) yakilenga kuiweka benki katika viwango vya kimataifa vya utoaji huduma na mapema mwaka huu wakazindua ofisi ya uwakilishi Dubai.
“Maboresho yetu ya mfumo mkuu wa uendeshaji wa yalilenga kubadilisha namna Benki inavyofanya kazi na jinsi mteja anavyopata huduma. Leo tunazindua kampeni tunayoiita Benki Kimpango Wako. Tunawahakikishia Watanzania na wateja wetu wengine popote duniani kuwa Benki yetu ya CRDB ni mbia wa uhakika na wa kutumainiwa katika upatikanaji wa huduma za fedha. Mwaka 2026 tunawaahidi huduma bora na za uhakika zaidi,” amesema Nsekela.

Uzinduzi wa kampeni ya Benki Kimpango Wako umefanyika katika kipindi muhimu kwa historia ya taifa wakati serikali ikianza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoelekeza kuwa uchumi wa Tanzania unapaswa kuwa jumuishi, wenye huduma za fedha zilizowafikia wananchi wengi zaidi, na taasisi za fedha kuwa nguzo ya ukuaji wa uchumi, ubunifu na ustawi wa jamii.
Ili kupata huduma za uhakika, wateja wanaweza kuhudumiwa katika tawi lolote la Benki ya CRDB iwe hapa Tanzania, nchini Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) au katika ofisi ya uwakilishi iliyopo Dubai au kupitia majukwaa tofauti ikiwamo Simbanking, huduma kwa njia ya intaneti au kwa CRDB Wakala. Huduma hizi zinapatikana pia hata kwa wale wanaofuata misingi ya dini kwani huhudumiwa kupitia dirisha la CRDB Al Barakah.

“Benki ya CRDB ni daraja la fursa kwa wananchi wote. Kampeni ya Benki Kimpango Wako inamkumbusha kila mdau kwamba Benki ya CRDB ni mshirika wa kutumainiwa katika safari ya maendeleo kwa mpango wa mteja katika muda wake,” amesisitiza Nsekela.
Posted by MROKI On Wednesday, February 04, 2026 No comments
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange akijibu maswali bungeni wakati wa Kikao cha Saba cha Mkutano wa Pili wa Bunge jijini Dodoma leo Februari 04, 2026.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (kulia) akizungumza na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange wakati wa kipindi cha maswali na majibu katika Kikao cha Saba cha Mkutano wa Pili wa Bunge jijini Dodoma leo Februari 04, 2026. Mbele ni Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Hamis Mwinjuma.
*******************
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesema katika kipindi cha mwaka 2020 hadi 2025 jumla ya miradi kumi ya kuhifadhji mazingira na kuhimili mabadiliko ya tabianchi yenye thamani ya takribani shilingi bilioni 97.6 imetekelezwa na kukamilika Zanzibar.
 
Hayo yamebainishwa bungeni jijini Dodoma leo Februari 04, 2026 na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange wakati akijibu swali la Mbunge wa Mtambwe Mhe. Rashid Habib Ali aliyetaka kufahamu Zanzibar inanufaikaje na fedha za mazingira zinazotolewa na wafadhili.
 
Mhe. Dkt. Dugange ameliarifu Bunge kuwa utekelezaji wa miradi ya mazingira umeleta manufaa kwa jamii kwa kuongeza kipato kupitia shughuli mbadala hivyo kuongeza uwezo wa jamii katika uhifadhi wa mazingira na kuhimili mabadiliko ya tabianchi
 
Akiendelea kujibu swali la mbunge huyo alifafanua kuwa utekelezaji wa miradi hiyo umechangia katika ukuaji wa uchumi kwa maendeleo endelevu na ustawi wa jamii kwa ujumla.
 
Mhe. Dkt. Dugange alisema Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikipokea fedha kutoka kwenye Mifuko ya Kimataifa ya Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi na wafadhili mbalimbali wakiwemo Mfuko wa Mazingira wa Dunia (GEF), Mfuko wa Mabadiliko ya tabianchi (GCF), Benki ya Dunia (WB) na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).
 
Aidha, alibainisha kuwa fedha zinazopatikana zimekuwa zikitumika kutekeleza miradi mbalimbali ya hifadhi ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi kwa Tanzania Bara na Zanzibar.
 
Hivyo, alisema Serikali imeendelea kuandaa miradi kwa ajili ya kutafuta fedha kupitia vyanzo mbalimbali ambapo hadi sasa jumla ya miradi mitatu yenye thamani ya takribani shilingi bilioni 62.6 ipo kwenye hatua za awali za maandalizi.
 
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri alisema fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya mazingira zinagawanywa kwa kuzingatia uwiano wa uhjtaji wa pande zote mbili za Muungano.
 
Alisema mkakati wa Serikali ni kuboresha maeneo yaliyoathiriwa na mabadiliko ya tabianchi hususan ya kwenye fukwe za bahari ambako maji huingia kwenye makazi ya wananchi na kuleta madhara.
 
Mhe. Dkt. Dugange alisema hayo wakati akijibu swali la nyongeza la Mhe. Ali aliyeuliza ni upi mgawanyo wa utekelezaji wa miradi Tanzania Bara na Zanzibar.
Posted by MROKI On Wednesday, February 04, 2026 No comments

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, Bungeni jijini Dodoma, Februari 4, 2026. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na Mbunge wa Bariadi Vijijini, Masanja Kadogosa, kwenye viwanja vya Bunge jijini Dodoma, Februari 4, 2026. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu) 
Posted by MROKI On Wednesday, February 04, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Rais wa Angola ambaye pia Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) Mhe. João Lourenço,
Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Mahama wa pili kutoka (kushoto), Waziri Mkuu wa Msumbiji Mhe. Maria Benvinda Levy wa kwanza (kushoto), Mwanzilishi Mwenza na Mwenyekiti Mtendaji wa GAIS na Rais Mstaafu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Akinwumi Adesina pamoja na Mwanzilishi na Mwenyekiti Mtendaji wa APCO Worldwide, Bi. Margery Kraus wa kwanza (kulia) mara baada ya uzinduzi rasmi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), uliofanyika Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu tarehe 03 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia katika uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu tarehe 03 Februari, 2026.
Posted by MROKI On Wednesday, February 04, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, kando ya Mkutano wa Dunia (WGS2026) hapa, Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.
  


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, mara baada ya mazungumzo kati yao, kando ya Mkutano wa Dunia (WGS2026) hapa, Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.  

Posted by MROKI On Wednesday, February 04, 2026 No comments

Tume ya Ushindani (FCC) imeweka mikakati mbalimbali ya kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi kwa wakati, kupitia matumizi ya mifumo ya kisasa katika utekelezaji wa majukumu yake.

Akizungumza wakati wa kikao kazi na watumishi wa Tume hiyo kwa lengo la kupanga mikakati ya utekelezaji wa majukumu, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa, amesema hatua hizo zinalenga kuongeza ufanisi wa huduma na kuwahudumia wananchi kwa viwango vya juu vya ubora.

Amesema FCC inaendelea kutekeleza dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha mazingira ya biashara nchini yanaboreshwa na kuwashirikisha wafanyabiashara kupitia mifumo rafiki na yenye ufanisi.

Ngasongwa amesema kuwa katika kipindi cha siku 100 za uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, FCC imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kusogeza huduma karibu na wananchi, ikiwemo kuanzisha Ofisi ya FCC Mkoa wa Tanga na Mipakani ili kuongeza wigo wa utoaji huduma na kuwafikia wananchi wengi zaidi, hususan wale waliopo maeneo ya pembezoni mwa nchi. 

Ameongeza kuwa FCC imeendelea kudumisha cheti hicho cha ubora kutokana na jitihada zake katika utoaji wa huduma kwa wananchi na wadau wa biashara kwa weledi na uwazi.

“Tuko hapa kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi kwa viwango vya ubora vinavyotambulika kimataifa, niwapongeze kwa kuendelea kushikilia Cheti cha Ithibati ya Ubora ISO 9001:2015,” amesema Ngasongwa.

Vilevile watumishi walipata nafasi ya kupitishwa na kujadili tathmini ya rasimu ya Mpango Mkakati Mpya wa Tume wa miaka mitano (Strategic Plan) 2026/27-2030/31 unaoakisi utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050. 

FCC ina utamaduni shirikishi katika kujadili mambo yahusuyo taasisi, ambapo watumishi wote kupitia ngazi mbalimbali hushirikishwa kwa ustawi wa taasisi. 

Kikao hicho kimefanyika Februari 02,2026 katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam.
Bw. Shalua Magandi, Mkurugenzi wa Huduma Saidizi akichangia mada wakati wa kikao kazi na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02,2026.Mwenyekiti wa Tughe Tawi la FCC, Bw. Emmanuel Ndyetabula akifuatilia kikao kazi cha Kaimu Mkurugenzi Mkuu na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02,2026.


Sehemu ya watumishi.




Picha za pamoja.

Posted by MROKI On Wednesday, February 04, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu, Singida
Wawekezaji wa ndani na nje ya Mkoa wa Singida wamehimizwa kujitokeza kuwekeza katika viwanda vya uchenjuaji na uongezaji thamani wa madini ili kunufaika na rasilimali zilizopo, kuongeza ajira na kukuza uchumi wa wananchi.

Wito huo umetolewa na Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Mhandisi Sabai Nyansiri, akisema mkoa huo una fursa kubwa ya uwekezaji katika sekta ya madini kutokana na ongezeko la shughuli za uchimbaji na mazingira bora ya uwekezaji yaliyowekwa na Serikali.

Akizungumza wakati wa ziara yake kwa wachimbaji wadogo katika Mgodi wa Matongo uliopo Kata ya Ikungi, Wilaya ya Ikungi, Mhandisi Nyansiri amesema Singida inaendelea kufanya vizuri katika uchimbaji wa madini ya dhahabu, shaba, madini ya ujenzi pamoja na jasi, hivyo kuwepo kwa viwanda vya uchenjuaji ni hatua muhimu ya kuongeza thamani ya madini hayo kabla ya kuuzwa.

Amesema uwekezaji katika viwanda vya uongezaji thamani wa madini utaongeza ajira kwa vijana na wanawake, kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa mkoa huo.

“Uwepo wa viwanda vya uchenjuaji na uongezaji thamani wa madini utaongeza ajira, mapato ya Serikali na kukuza uchumi wa kila mwananchi,” amesema.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha masoko ya madini na kuendeleza biashara rasmi ya madini, akibainisha kuwa hatua hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa ongezeko la mapato ya mkoa.

Ameeleza kuwa Mkoa wa Singida ulipangiwa kukusanya Shilingi Bilioni 30 kwa mwaka wa fedha 2025/2026, kutoka Shilingi Bilioni 24 mwaka wa fedha 2024/2025, na hadi kufikia Desemba 2025 tayari umefanikiwa kufikia asilimia 54 ya lengo hilo sawa na Shilingi Bilioni 16.

Mhandisi Nyansiri amesema mafanikio hayo yanatokana na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji na kutoa kipaumbele kwa wachimbaji wadogo wazawa.

Kwa upande wake, Meneja wa Mgodi wa Matongo, Japhet Madusa, ameishukuru Serikali kwa kutambua mchango wa wachimbaji wadogo katika maendeleo ya sekta ya madini na kuiomba iendelee kuwawezesha kwa kuwapatia vitendea kazi vya kisasa pamoja na kuboresha miundombinu ya barabara ili kurahisisha upatikanaji wa migodi.

Ameongeza kuwa mgodi huo unaendelea kushirikiana na jamii inayouzunguka kwa kutoa ajira kwa vijana wa eneo hilo, kuchangia vifaa vya ujenzi katika Shule ya Sekondari Matongo, Ofisi ya Kijiji cha Matongo pamoja na ujenzi wa ofisi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), hatua inayochangia maendeleo ya kijamii katika eneo hilo.




Posted by MROKI On Wednesday, February 04, 2026 No comments
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe. Makongoro Nyerere (Kulia) akipokea nyaraka kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa Waiala Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Bw. Frank Mugogo kuashiria kuanza kwa mradi wa kupeleka umeme kwenye vitongoji mkoani Rukwa
*****************
Na Mwandishi Wetu, Rukwa
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe. Makongoro Nyerere ameahidi kuipa kipaumbele miradi ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA)  ya kupeleka umeme kwenye vitongoji  156 vya Awamu ya Pili B (HEP 2B) inayotekelezwa mkoani humo.

RC Makongoro amebainisha hayo leo Februari 3, 2026 mara baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo iliyowasilishwa na Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa REA, Bw. Frank Mugogo sambamba na kumtambulisha mkandarasi kampuni ya M/s Dieynem Co Ltd atakayetekeleza mradi huo.

"Mimi natoa maelekezo sasa kwa watu wangu, mradi huu wa REA kwa miaka mitatu ijayo kuanzia sasa tutaipa kipaumbele na itakuwa ni ajenda ya kudumu katika kamati yangu ya usalama ya Mkoa ili kuhakikisha mradi unatekelezwa vyema na kwa ubora, " Amesisitiza RC Makongoro.

Aidha, RC Makongoro amemtaka mkandarasi wa mradi huo kuwasilisha taarifa ya mradi huo kila mwezi ili kupitia maendeleo ya mradi huo unavyoendelea kutekelezwa katika mkoa huo na kuwataka kufanya kazi kwa ubora na bidii ili iweze kukamilika kwa wakati.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa REA, Bw. Mugogo amesema kuwa mkoa wa Rukwa una jumla ya vitongoji 1,816, vitongoji vyenye umeme ni  1,508  na vitongoji ambavyo havina umeme ni 308.

"Kupitia mradi wa HEP 2B vitongoji 156 vinakwenda kupelekewa umeme kwa mkoa wa Rukwa na wateja wapatao 5,508 wataunganishiwa na huduma ya umeme. Gharama ya kuunganisha umeme ni shilingi 27,000 tu naomba mfahahamu na tuwaeleze wananchi katika maeneo ya mradi" Amesema Bw. Mugogo.

Kwa upande wake, Meneja wa Miradi wa Kampuni ya Dieynem Co. Ltd, Mha. Novatus Lyimo ameahidi kumaliza mradi huo kwa wakati na kuwataka wananchi kuchangamkia fursa za uwepo wa mradi huo katika maeneo yao ikiwemo kutumia fursa za ajira mbalimbali zitakazotolewa kipindi chote cha mradi.
Posted by MROKI On Wednesday, February 04, 2026 No comments
Matukio mbalimbali yaliyojiri kabla ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kufanya vikao na Viongozi mbalimbali pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiondoka eneo la mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Waziri wa Nchi, Umoja wa Falme za Kiarabu  Mhe. Dkt. Maitha Salem Al Shamsi muda mfupi kabla ya kufanya vikao na Viongozi mbalimbali pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiteta jambo na Rais wa Ethiopia Mhe. Aye Atske-Selassie kabla ya kufanya vikao na Viongozi mbalimbali pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Angola Mhe. João Lourenço kabla ya kufanya vikao na Viongozi mbalimbali pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Kossovo Mhe. Vjosa Osmani-Sadriu kabla ya kufanya vikao na Viongozi mbalimbali pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).

Posted by MROKI On Wednesday, February 04, 2026 No comments

February 03, 2026







Na Mwandishi wetu, Singida
Wadau wa sekta ya madini wakiwemo wachimbaji, wachenjuaji na wafanyabiashara wa madini mkoani Singida wamepongeza uwepo wa Soko la Madini Singida, wakisema limeleta mapinduzi makubwa katika biashara ya madini kwa kuimarisha uwazi, haki na ufanisi kupitia matumizi ya mfumo wa bei elekezi za kidigitali.

Akizungumza katika soko hilo, Mtaalam kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Mjiolojia Mbeleye David, amesema kuanzishwa kwa soko hilo kumeleta tija kubwa kwa wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini kwa kuweka mifumo inayowalinda dhidi ya udanganyifu wa ubora wa dhahabu na unyonyaji wa bei.

Amesema kabla ya kuanzishwa kwa masoko ya madini, mkoa wa Singida ulikuwa unaratibu kiasi kidogo cha uzalishaji, kati ya gramu 100 hadi 200 pekee, lakini kwa sasa kupitia masoko hayo umefanikiwa kuratibu uzalishaji unaoanzia kilo 50 hadi 60 kwa wachimbaji wadogo, hali inayoonesha ongezeko la ufanisi na imani ya wadau katika mfumo huo.

David ameeleza kuwa Serikali imeweka mfumo madhubuti wa bei elekezi unaolenga kumlinda mchimbaji mdogo dhidi ya kupunjwa kwa kuuza madini kwa bei duni.

 Amesema soko hilo limewekewa mashine ya kisasa ya X-Ray Fluorescence (XRF) kwa ajili ya kupima ubora wa dhahabu, hatua inayohakikisha madini yanauzwa kwa kuzingatia viwango sahihi vya ubora na thamani halisi.

Ameongeza kuwa, tofauti na awali ambapo bei elekezi ilitolewa kwa dhahabu ghafi pekee, kwa sasa soko linatumia ubao wa kidigitali unaoonesha bei elekezi za madini mbalimbali ikiwemo dhahabu, shaba na fedha, jambo lililoongeza uwazi na kuondoa mianya ya udanganyifu katika biashara ya madini.

“Teknolojia hii imeongeza uwazi na kurahisisha shughuli za masoko ikiwemo uthaminishaji wa madini na utoaji wa vibali vya kusafirisha madini ndani na nje ya nchi, ambazo sasa zinafanyika kwa wepesi na kwa haraka zaidi,” amesema David.

Kwa upande wake, mfanyabiashara wa madini, Abubakari Omary, amesema pamoja na mafanikio yaliyopo, elimu kuhusu matumizi ya bei elekezi inapaswa kuendelea kutolewa kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ili kuepusha sintofahamu na migogoro wakati wa kufanya biashara.

“Elimu ni msingi muhimu ili kila mdau aelewe haki na wajibu wake na kufanya biashara kwa kuzingatia bei halisi ya soko,” amesema Omary.

Aidha, wadau wamepongeza mfumo mpya wa masoko ya madini unaowawezesha wachimbaji wasio na leseni kujisajili na kuuza madini yao moja kwa moja katika masoko ya madini bila kulazimika kutumia leseni ya mfanyabiashara, hatua ambayo imeondoa kikwazo kikubwa kilichokuwepo awali.

Kwa ujumla, uwepo wa Soko la Madini Singida umetajwa kuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya sekta ya madini mkoani humo, kwa kuongeza uwazi na usalama wa biashara, pamoja na kuongeza mapato ya serikali kupitia kudhibiti na kuzuia utoroshaji wa madini.
Posted by MROKI On Tuesday, February 03, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo