Nafasi Ya Matangazo

September 03, 2026


DODOMA
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Subira Mgalu (Mb.) imepatiwa mafunzo kuhusu usimamizi wa mikataba ya msaada wa kiufundi katika Sekta ya Madini, ikiwa ni pamoja na masharti ya kisheria yanayohusu umiliki wa leseni ndogo za uchimbaji wa madini.

Akizungumza kupitia mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye Ofisi za Makao Makuu ya Tume ya Madini jijini Dodoma mapema leo Mkurugenzi wa Huduma za Sheria wa Tume ya Madini, Francis Kayichile, kwa Niaba ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini amesisitiza kuwa mtu ambaye si raia wa Tanzania kupewa leseni ndogo ya uchimbaji madini ni kosa kwa mujibu wa Sheria ya Madini, Sura ya 123, kwa kuwa fursa ya kuomba na kumiliki leseni hizo imetengwa kwa Watanzania pekee.

Kayichile amesema Kifungu cha 64 kikisomwa pamoja na kifungu cha 9 (3) cha Sheria ya Madini, Sura ya 123, kinatoa fursa kwa Watanzania pekee kuwasilisha maombi ya leseni ndogo za uchimbaji madini, hivyo mtu asiye raia wa Tanzania hanufaiki na fursa hiyo.

Amesema pamoja na umiliki wa leseni kuwa kwa Watanzania, wamiliki wa leseni ndogo wanaweza kupata msaada wa kiufundi kutoka kwa wawezeshaji kwa kuzingatia sheria na kanuni zilizopo.


Aidha ameeleza kuwa kwa mujibu wa kanuni hizo mwenye leseni yenye msaada wa kiufundi amepatiwa  asilimia 30 ya faida baada ya kuondoa tozo zote za Serikali, bila kuzingatia gharama za uendeshaji wa mradi alizobeba mwezeshaji.

Ameongeza kuwa usimamizi wa mgodi, uingizaji wa vifaa na mitambo pamoja na ulinzi wa eneo na mali ni majukumu ya pamoja ya wahusika wa mkataba.

Kayichile amesema mkataba wa msaada wa kiufundi huwa na muda wa awali wa miaka mitatu na unaweza kuhuishwa, lakini kwa jumla muda wake haupaswi kuzidi miaka 12 au uhai wa mgodi unapoisha.

“Mikataba hiyo husajiliwa na Tume ya Madini na wahusika wana haki ya kufanya marekebisho  wakati wowote na pindi kunapofanyika marekebisho ya sheria  yanayoathiri masharti ya mkataba au pale inapobainika uwepo wa madini mapya katika eneo lenye leseni yenye msaada wa kiufundi” amesema.

Amesema Tume ya Madini inaendelea kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa mikataba hiyo, huku akisisitiza kuwa ukiukwaji wa masharti unaweza kusababisha hatua kuchukuliwa kwa mujibu wa Kifungu cha 74 cha Sheria ya Madini, Sura ya 123, ikiwemo kusitishwa au kufutwa kwa leseni.

Aidha, Kayichile amesema Serikali imefanya marekebisho ya Kanuni za Haki Madini kwa lengo la kulinda haki za wenye maduara waliopo ndani ya maeneo yenye leseni ndogo za uchimbaji madini.

Amesema kupitia Kanuni za Madini (Msaada wa Kiufundi) za mwaka 2025, hususan Kanuni ya 8(1)(h), mwenye leseni analazimika, kabla ya kuingia mkataba wa msaada wa kiufundi, kufanya makubaliano na wenye maduara au kuwalipa fidia kwa uwekezaji walioufanya katika eneo lenye leseni hiyo.

Kwa mujibu wa Kayichile, hatua hiyo inalenga kuhakikisha haki za Watanzania wanaomiliki leseni na wenye maduara zinalindwa, huku ikiweka mazingira ya ushirikiano katika shughuli za uchimbaji madini yanayozingatia sheria na kuhakikisha rasilimali za madini zinawanufaisha Watanzania wote.

Kikao hicho kilichoongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu (Mb.) kimeshirikisha pia watendaji wa taasisi zilizopo chini ya Wizara ya Madini.










Posted by MROKI On Thursday, September 03, 2026 No comments



Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Naibu Wasajili wa Mahakama nchini kuendelea kutekeleza majukumu yao ipasavyo huku wakilinda maslahi ya haki (Interest of Justice).

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 31 Agosti, 2026 alipokuwa akifungua Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Tuna wajibu wa kuendelea kutekeleza majukumu yetu kwa kulinda maslahi ya haki, kwa kutokufungwa kwa masharti ya kiufundi kupita kiasi hadi kukwamisha upatikanaji haki,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema kuwa, Wasajili wa Mahakama ndio 'injini' ya Mahakama. Hivyo, wana nafasi kubwa katika maendeleo ya Mhimili huo ambao mamlaka yake kwa mujibu wa Ibara ya 4 ni kutekeleza jukumu la utoaji haki.

“Kwa mujibu wa Ibara ya 107A(1), Mahakama ndio yenye kauli ya mwisho kwenye masuala ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano. Na ukiwa unaongozwa na kanuni kadhaa: mojawapo, kutenda haki kwa wote bila kujali hali ya mtu kiuchumi au kijamii, kutochelewesha haki bila kuwepo sababu ya msingi na kwamba itakuwa huru, italazimika tu kuzingatia sheria za nchi na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kama ambavyo Ibara ya 107A inavyoelekeza,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema, shughuli zote za umma huongozwa na kusimamiwa na sheria; hakuna shughuli yoyote ya umma ambayo haiongozwi na kusimamiwa na sheria. Na kwa sababu hiyo, Katiba inakuwa pia sheria, kwa mujibu wa ile Sheria ya Tafsiri za Sheria, sura ya kwanza ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Jaji Mkuu amewakumbusha Naibu Wasajili hao kuwa waadilifu ili wanapofanya maamuzi, watu waone kweli kwamba haki imetendeka. Amesisitiza, “Na katika hilo lazima tuwe waadilifu, tunapoacha kuwa waadilifu, tukiwa wazembe, tukiwa wavivu, uwezo wetu ukiwa mdogo, watu hawatatuheshimu.”

Vilevile, Mhe. Masaju amekemea vikali tabia ya baadhi ya watu kuingilia uhuru na maamuzi ya Mahakama huku akibainisha kuwa, Katiba imeiwekea ulinzi kwa Mahakama kupitia Ibara ya 30(2)(c) inayoelekeza kuhakikisha utekelezaji wa hukumu au amri ya Mahakama iliyotolewa katika shauri lolote la madai au la jinai.

Aidha, Ibara ya 30(2)(d) inatamka kulinda heshima, haki na uhuru wa watu wengine au faragha ya watu wanaohusika katika shauri lolote mahakamani, kuzuia kutoa habari za siri, au kulinda heshima na uhuru wa Mahakama.

“Ni lazima hukumu na amri za Mahakama zitekelezwe, ni Mahakama gani hiyo inaweza ikafanya maamuzi halafu yasitekelezwe, halafu ikabaki kuwa Mahakama?” amehoji Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, Katiba hiyo pia inaelekeza kwamba lazima Mahakama iheshimike; uhuru wake, mamlaka, na hadhi yake lazima vilindwe na viheshimiwe. Kwa hiyo, lazima kulinda sifa na haki au uhuru wa watu wengine, au maisha binafsi ya watu wanaohusika katika mashauri mahakamani, kuzuia kutoa habari za siri, kutunza heshima, mamlaka, na uhuru wa Mahakama.
Posted by MROKI On Thursday, September 03, 2026 No comments

September 02, 2026

Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC, Kenneth Simbaya (katikati) akiwa na Mwenyekiti wa Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA. Richard Mwaikenda pamoja na Makamu Mwenyekiti wa jukwa hilo, Sylivester Ngombaniza baada ya kufanya kikao cha pande hizo mbili.
Kutoka kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa JUWATA,Ngombaniza, Kaimu Afisa wa Fedha, Winfrida Madeni, Mwenyekiti wa JUWATA, Mwaikenda, Mkurugenzi Mtendaji wa UTPC, Simbaya na Afisa wa Programu UfutiliajiRasilimali, Andrew Malawiti.
Viongozi wa JUWATA na UTPC wakiwa katika kikao hicho.

Mwaikenda akimsikiliza kwa makini Simbaya wakati wa kikao hicho.
Mwaikenda akizungumza wakati wa kikao hicho.
Simbaya akiagana na viongozi wa JUWATA.
 ***************
JUKWAA Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) wamekubaliana kuimarisha ushirikiano katika kulinda uhuru wa vyombo vya habari, kutetea haki na maslahi ya waandishi wa habari pamoja na kuhakikisha jamii inapata habari sahihi na kwa wakati.

‎Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao cha pamoja cha viongozi wa JUWATA na UTPC kilichofanyika katika ofisi za UTPC zilizopo Barabara ya Aboud Jumbe, Mtaa wa Kazembo, eneo la Uzunguni jijini Dodoma.

Katika kikao hicho, viongozi hao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya habari, ikiwemo umuhimu wa kuwa na mshikamano miongoni mwa wadau wa habari katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili waandishi wa habari na vyombo vya habari nchini.

Aidha, walisisitiza umuhimu wa taasisi hizo kushirikiana katika kutetea uhuru wa vyombo vya habari, haki za waandishi wa habari na maslahi yao, huku wakitambua nafasi muhimu ya wanahabari katika kuhabarisha, kuelimisha na kuwajibika katika jamii.

Ushirikiano huo pia unalenga kuongeza nguvu katika kushughulikia changamoto zinazohusu mazingira ya kazi ya waandishi wa habari, pamoja na kujenga mahusiano mazuri kati ya wadau wa habari na taasisi mbalimbali zinazohusika na maendeleo ya sekta hiyo.

UTPC ina jumla ya Klabu 28 za Waandishi wa Habari zinazowakilisha waandishi wa habari kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, hivyo kuwa na mtandao mpana wa kuwafikia wanahabari katika maeneo mbalimbali nchini.

Kwa upande wa JUWATA, ujumbe uliongozwa na Mwenyekiti wake, Richard Mwaikenda, akifuatana na Makamu Mwenyekiti, Sylivester Ngombaniza, pamoja.

UTPC iliwakilishwa na Mkurugenzi Mtendaji, Kenneth Simbaya, pamoja na Afisa wa Programu wa Ufuatiliaji Rasilimali, Andrew Malawiti, Kaimu Afisa wa Fedha Winfrida Madeni na Afisa Msaidizi wa Programu, Edmund Kapungu.

Viongozi hao wameeleza umuhimu wa kuendeleza mawasiliano na ushirikiano wa karibu baina ya taasisi hizo kwa manufaa ya waandishi wa habari, vyombo vya habari na jamii kwa ujumla.

Wamesisitiza kuwa mshikamano wa wadau wa habari ni muhimu katika kujenga sekta imara, yenye weledi na inayoweza kutekeleza kwa ufanisi wajibu wake wa kuhabarisha umma na kulinda maslahi mapana ya jamii.
************
‎Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) limeanzishwa kihalali kwa kuzingatia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, likiwa na lengo la kupanua wigo kwa Wahariri wanaotimiza vigezo kuwa huru kujiunga na jukwaa hilo, ili kuongeza nguvu, umoja na ushirikiano katika kutetea na kulinda haki na maslahi ya Waandishi wa Habari pamoja na jamii kwa ujumla.

Katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku, JUWATA itazingatia Katiba na kanuni zake, sambamba na kufuata na kuheshimu Sheria za Nchi pamoja na taratibu zinazotawala tasnia ya Habari.

‎Kwa ufupi, JUWATA haijaasisiwa kwa lengo la kupambana, kushindana au kusigana na taasisi nyingine za Habari.

Badala yake, inalenga kujenga ushirikiano, mshikamano na mahusiano mema na taasisi za Habari za ndani na nje ya nchi, kwa manufaa ya Wahariri, Waandishi wa Habari na jamii kwa ujumla.

JUWATA inaamini kuwa umoja, ushirikiano na kuheshimiana ndiyo msingi wa kujenga tasnia imara, huru, yenye uwajibikaji na inayoweza kusimamia kwa ufanisi haki na maslahi ya Wadau wa Habari.
Posted by MROKI On Wednesday, September 02, 2026 No comments

September 01, 2026


Balozi wa Uingereza nchini Tanzania Mh.  Marianne Young amekutana na Waziri wa Madini, Mh. Anthony Mavunde, kwa na kufanya  mazungumzo kuhusu sekta ya madini nchini Tanzania na fursa za kuimarisha ushirikiano kati ya Uingereza na Tanzania.

Mkutano huo ulijadili kuhusu uwekezaji, uongezaji wa thamani, na kuhakikisha sekta hiyo inachangia katika ukuaji wa uchumi unaoshirikisha wote ulifanyika jijini Dodoma leo Septemba 1, 2026.





Tanzania na Uingereza zitaendelea kushirikiana katika maeneo yenye manufaa kwa pande zote mbili ili kudumisha ustawi wa mataifa yote mawili.
Posted by MROKI On Tuesday, September 01, 2026 No comments

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema jukumu kuu la Wizara ya Nishati ni kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika na wanapatiwa taarifa kwa wakati pindi changamoto zinapojitokeza.

Mhe. Makamba ameyasema hayo leo, tarehe 01 Septemba 2026, wakati akijibu Swali lanMhe. Exaud Silaoneka Kigahe, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini, aliyetaka kufahamu lini Serikali itabadilisha mkataba wa usambazaji wa umeme kwa wananchi kutoka Mwenga Power kwenda TANESCO, ili Mwenga Power ibaki kuwa mzalishaji wa umeme.

Akijibu swali hilo, Mhe. Makamba amesema utoaji na usimamizi wa leseni za uzalishaji na usambazaji wa umeme nchini ni jukumu la kisheria la Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), kwa mujibu wa Sheria ya Umeme ya mwaka 2008 na taratibu za utoaji wa leseni hizo.

“Jukumu namba moja la Wizara ya Nishati ni kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika na wanapata taarifa kwa wakati kunapotokea changamoto,” amesema Mhe. Makamba.

Ameeleza kuwa uamuzi wowote wa kubadili muundo wa leseni ya usambazaji umeme katika eneo hilo unapaswa kuzingatia matakwa ya sheria na taratibu zilizowekwa.

Hata hivyo, Mhe. Makamba amesema Serikali, kwa kutambua kuwa kumekuwa na malalamiko kuhusu ubora wa huduma inayotolewa na Mwenga Power, tayari taasisi zake za EWURA, TANESCO na REA zimeanza kufanya tathmini ya kina ili kubaini uwezekano wa kufanya mabadiliko hayo bila kuathiri uwekezaji uliopo.

Amesema tathmini hiyo itafanyika kwa haraka ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme yenye uhakika na inayokidhi mahitaji yao.

Aidha, akihitimisha, Mhe. Makamba amesema yupo tayari, pindi Vikao vya Bunge vitakapokamilika, kuongozana na Mhe. Exaud Silaoneka Kigahe, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini, kwenda kusikiliza na kufahamu kwa kina changamoto zinazowakabili wananchi katika eneo hilo.
Posted by MROKI On Tuesday, September 01, 2026 No comments


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) zimekubaliana kuondoa jambo la 15 la Maliasili ya mafuta, pamoja na mafuta yasiyochujwa ya motokaa na mafuta ya aina ya petroli na aina nyinginezo za mafuta au bidhaa, na gesi asilia katika orodha ya mambo ya Muungano.
 
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa wakati akijibu swali la Mbunge wa Mtambwe Mhe. Rashid Habib Ali Rashid aliyeuliza Serikali ina mpango gani wa kuondoa suala la Mafuta na Gesi kwenye orodha ya Masuala ya Muungano.
 
Akiendelea kujibu swali hilo, Mhe. Kwagilwa alisema kwa sasa, suala la Mafuta na Gesi Asilia linasimamiwa na kila upande ambapo SJMT imetunga Sheria ya Mafuta na Gesi Asilia ya Mwaka 2015 ambayo chini ya kifungu cha 11 imeanzisha Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA - Petroleum Upstream Regulatory Authority).

Aliongeza kuwa kwa upande wa Zanzibar, SMZ imetunga Sheria ya Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia, Namba 6 ya Mwaka 2016 iliyoanzisha Mamlaka ya Udhibiti, Utafutaji na Uendelezaji wa Mafuta na Gesi Asilia (ZPRA – Zanzibar Petroleum Regulatory Authority) na Kampuni ya Maendeleo ya Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar (ZPDC – Zanzibar Petroleum Development Corporation).

“Mheshimiwa Naibu Spika Kwanza niungane na Mheshimiwa mbunge ambaye amesema kwamba Baraza la Wawakilishi lilisharidhia na lilishawasilisha kutaka suala hili liondolewe na ndio maana Baraza la Wawakilishi limetunga sheria ya kuanzisha Mamlaka ya Udhibiti na hivyo linashughulikiwa katika kila upande hivyo halina hoja kinzani,” alifafanua Kwagilwa.

Pamoja na hayo, kila ongezeko au kuondolewa kwa masuala ya Muungano hupata nafasi ya kujadiliwa na kupata ridhaa ya Serikali zote mbili ya SJMT na SMZ na kupitia mchakato mahususi wa kikatiba.

Mabadiliko husika hupitia katika Baraza la Wawakilishi na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ibara ya 98(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inaruhusu Bunge kutunga sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti yoyote ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini kwa utaratibu maalumu ufuatao ulioainishwa na Katiba.
 
Posted by MROKI On Tuesday, September 01, 2026 No comments
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na Wananchi wa Mbuyuni, Moshi Mjini, waliojitokeza kumlaki akiwa katika ziara binafsi mkoani Kilimanjaro, leo tarehe 01 Septemba 2026.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi, amewasalimu Wananchi wa Mbuyuni, Wilayani Moshi waliokusanyika kumlaki akiwa katika ziara binafsi mkoani Kilimanjaro leo tarehe 01 Septemba 2026.
 
Akiwasalimu wananchi hao, Makamu wa Rais amewasihi kuendelea kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na yeye binafsi ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi. Amesema kwa imani ya maombi ataweza kumsaidia kwa hekima na utii Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 
Makamu wa Rais amesema ataendelea kutekeleza wajibu wake kwa uadilifu, umakini na kujituma, akisisitiza utayari wake wa kushirikiana na viongozi pamoja na wananchi.
 
Akizungumza kwa msisitizo, Makamu wa Rais amesema: “Hatawazingua Wana wala hatamzingua Mama,” kauli ambayo aliitoa pia mkoani Dodoma, kwa wananchi wa Chamwino, mara baada ya kuapishwa.
 
Awali, Makamu wa Rais aliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) ambapo alipokelewa na viongozi mbalimbali wa Serikali, Viongozi wa Dini na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Kilimanjaro.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi akisalimiana na Viongozi mbalimbali wakati alipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro, leo tarehe 01 Septemba 2026.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi akisalimiana na Viongozi mbalimbali wakati alipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro, leo tarehe 01 Septemba 2026.

Posted by MROKI On Tuesday, September 01, 2026 No comments


Kwa mara ya kwanza watalamu wa upasuaji wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na mwenzao kutoka Mradi wa Little Heart wa Shirika la Muntada lililopo nchini Uingereza Dkt. Ahmet Sasmazel wamemfanyia upasuaji wa moyo mtoto aliyezaliwa na mishipa miwili mikubwa ya damu inayotoka kwenye moyo kupishana (Nikaidoh Operation).


Upasuaji huo umefanyika kwa njia ya kufungua kifua kwa mtoto mwenye umri wa miaka miwili na mwezi mmoja kwa mafanikio makubwa.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii leo jijini Dar es Salaam Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Thabit Ramadhani alisema upasuaji huu ni wa kwanza kufanyika JKCI na Afrika Mashariki na Kati.

“Tumefanya upasuaji huu kwa umakini mkubwa, na sasa mtoto anaendelea vizuri, ameshatolewa katika chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU) na kupelekwa katika chumba cha ungalizi wa watoto (PICU)”, alisema Dkt. Thabit.

Dkt Thabit alisema mtoto huyo mbali na kuwa na mishipa mikubwa ya damu inayotoka kwenye moyo kupishana pia alikuwa na tundu kwenye moyo pamoja na uvimbe uliosababisha mshipa wa damu kusinyaa hivyo kuzuia damu kutoka kwenye moyo kwenda kwenye mwili na mapafu kwa mtiririko unaostahili.

 “Tatizo hili la mshipa wa damu unaopeleka damu kwenye mapafu kusinyaa ulisababishwa na kukandamizwa na uvimbe aliokuwa nao mtoto hivyo kutoruhusu damu kupita kwa urahisi, tumemuwekea mtoto mrija wa damu bandia ili kuwezesha damu kwenda kwenye mapafu”, alisema dkt. Thabit.

Kwa upande wake Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kutoka Mradi wa Little Heart wa Shirika la Muntada lililopo nchini Uingereza Dkt. Ahmet Sasmazel alisema mafanikio ya upasuaji huo yametokana na ushirikiano wa karibu uliokuwa ukifanywa na watalaamu wa JKCI.

“Tumepata matokeo mazuri ya upasuaji huu kwasababu ya uwepo wa vifaa tiba vya kisasa na watalaamu waliobobea ambao wana moyo wakuhudumia watoto kama hao na kujikita katika kuokoa maisha yao, waendelee kujifunza kwaajili ya matokeo mazuri zaidi ya baadaye”, alisema Ahmet.

Naye mama wa mtoto aliyefanyiwa upasuaji huo Witness Kibuga alisema mtoto wake aligundulika kuwa na tatizo la moyo akiwa na umri wa miezi saba na kuanza kuudhuria kliniki ya matibabu ya moyo hadi sasa alipofanyiwa upasuaji huo.

 “Namshukuru Mungu na watalaamu wote wa JKCI kwa kumfanyia upasuaji mtoto wangu ambaye kwa sasa anaendelea vizuri naomba waendelee na moyo wa kuwahuduma watoto wetu na kuokoa maisha yao kwani tunawategemea sana”, alisema Witness.
- Mwisho -

CAPTION

PICHA 2

Wataalamu wa upasuaji wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakimfanyia upasuaji wa moyo mtoto wa miaka miwili (Nikaidoh Operation) kwa kushirikiana na daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kutoka Uturuki Ahmet Sasmazel wa Mradi wa Liitle Aid wa Shirika la Muntada Aid jijini Dar es Salaam.

 

PICHA 2.

Mama wa mtoto Deus Mgonzo, Witness Kibuga akiwa na Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Idd Kimaro katika chumba cha ungalizi wa watoto (PICU) alipolazwa mtoto huyo jijini Dar es Salaam

Posted by MROKI On Tuesday, September 01, 2026 No comments

August 31, 2026

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) Mhe. Deus Sangu akiteta jambo na  Sheikh Mkuu wa Jumuiya ya Waithna’ashariyyah Tanzania (TIC) Sheikh Hemed Jalala (Kushoto) Pamoja na Mwenyekiti wa Taifa wa Jumuiyah ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) Sheikh Alhad Mussa Salum (Kulia) katika hafla ya kumbukizi ya mazazi ya Mtume Muhammad (Sallallahu Alayhi Wasallam) iliyofanyika Agosti 30,2026 katika uwanja wa Kigogo Posti, Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) Mhe. Deus Sangu akiteta jambo na  Sheikh Mkuu wa Jumuiya ya Waithna’ashariyyah Tanzania (TIC) Sheikh Hemed Jalala (Kushoto) Pamoja na Mbunge wa Jimbo la Kinondoni Mhe. Abbas Tarimba (Kulia) katika hafla ya kumbukizi ya mazazi ya Mtume Muhammad (Sallallahu Alayhi Wasallam) iliyofanyika Agosti 30,2026 katika uwanja wa Kigogo Posti, Jijini Dar es Salaam.
**************
Na: OWM (KAM), Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu ametoa wito kwa wananchi na Taasisi za dini kuendelee kushirikiana na Serikali katika kudumisha amani, upendo, umoja na mshikamano, akisisitiza kuwa misingi hiyo ni nguzo muhimu katika kujenga Taifa imara.

Aidha, pia amewasihi kuhusu suala la malezi bora na uadilifu kwa watoto na vijana ili kuepuka athari za mmomonyoko wa maadili pamoja na kutokomeza ukatili dhidi ya watoto, kwa lengo la kujenga kizazi kijacho chenye maadili na upendo.
 
Mhe. Sangu ametoa wito huo (Jumapili, Agosti 30, 2026) alipomwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba katika hafla ya kumbukizi ya mazazi ya Mtume Muhammad (Sallallahu Alayhi Wasallam) iliyofanyika katika uwanja wa Kigogo Posti, Jijini Dar es Salaam.

Amesema Serikali inatambua mchango wa Taasisi za Dini katika kuimarisha mshikamano wa kijamii; kukuza maadili ya uadilifu, uwajibikaji na upendo; kutoa huduma za kijamii kama vile elimu, afya na msaada wa kijamii pamoja na kuelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa amani na mshikamano wa kitaifa.

“Serikali inatambua nafasi ya Jumuiya ya Waithna’ashariyyah Tanzania (TIC), ikiongozwa na Sheikh Mkuu wa TIC Maulana Sheikh Hemed Jalala na taasisi zote za dini katika kuimarisha mahusiano mema, amani na utuivu,” amesema

Kadhalika, ametoa wito kwa waumini wa dini ya kiislamu kuyashika na kuyaishi kwa vitendo mafundisho na Maisha ya Mtume Mohammad (S.A.W) dini hususan katika kuimarisha maadili, upendo, amani na mshikamano katika jamii ili kujenga Taifa lente maadili mema na uwajibikaji.

Kwa upande mwengine, Waziri Sangu amewasilisha salamu za Sikukuu ya Maulid kutoka kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba na pia kuwapongeza kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kudumisha Amani, mshikamano na umoja wa kitaifa.

Pia, Sheikh Mkuu wa Jumuiya ya Waithna’ashariyyah Tanzania (TIC) Sheikh Hemed Jalala,ameishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa nia njema ya kushiriki katika Sherehe za Maulid, akisema ushiriki huo ni ishara ya ushirikiano mzuri kati ya Serikali na jamii. Aidha, upendo na Huruma ndo Mafunzo ya Mtume Muhammad (S.W.W) ampapo amezitaka taasisi zote za dini kuendeleza juhudi za kuwaleta pamoja waumini na wasiokuwa waumini kupitia mihadhara na shughuli mbalimbali za kidini zinazolenga kumuenzi na kumsifia Mtume Muhammad (S.W.W), huku akisisitiza umuhimu wa mshikamano na umoja katika jamii.
Posted by MROKI On Monday, August 31, 2026 No comments
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi, pamoja na familia yake wameungana na waumini mbalimbali katika kushiriki Ibada ya Misa Takatifu ya Jumapili, katika Kanisa Katoliki, Parokia ya Paulo wa Msalaba Jimbo Kuu Katoliki Dodoma. Tarehe 30 Agosti 2026.











Posted by MROKI On Monday, August 31, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo