Nafasi Ya Matangazo

May 15, 2026





Na Mwandishi wetu,Dodoma
Vituo vya kutolea huduma za afya vimetakiwa kuboresha maoteo ya uagizaji wa dawa na kuzingatia mwenendo wa magonjwa katika maeneo yao ili kuhakikisha bidhaa za afya zinapatikana wakati wote na kuondokana na changamoto ya wananchi kukosa bidhaa hizo wanapohitaji huduma.

Kauli hiyo imetolewa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dkt. Thomas Rutachunzibwa, leo Mei 15, 2026 Jijini Dodoma wakati akifungua kikao kazi cha wateja na wadau wa Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya Dodoma inayohudumia Mikoa ya Dodoma, Singida pamoja na Halmashauri ya Kiteto ya Mkoa wa Manyara.

“MSD inafanya kazi kubwa ya kuhakikisha bidhaa muhimu za afya zinapatikana, zinatunzwa na kusambazwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini. Ni muhimu kwa vituo vya afya kufanya maoteo sahihi ya mahitaji yao ili kuondoa malalamiko ya wananchi kuhusu ukosefu wa dawa,” amesema Dkt. Rutachunzibwa.

Amesema serikali inaendelea kuweka kipaumbele kuhakikisha nidhaa za afya ziinapatikana wakati wote ili wananchi waendelee kupata huduma bora za afya.

Dkt. Rutachunzibwa amewataka watendaji wa sekta ya afya Halmashuari za Wilaya kushirikiana na wafamasia pamoja na wataalam wa maabara kupanga mahitaji ya dawa na kuhakikisha bidhaa hizo zinatengewa bajeti pamoja na kuwepo fedha za manunuzi.

“Kwa nini tuwe na dawa zinaharibika kutokana na kuagiza bidhaa nyingi kuliko mahitaji halisi wakati bado kuna wananchi wanahitaji huduma hizo? Ni muhimu kuboresha maoteo na kuagiza dawa kulingana na mwenendo wa magonjwa katika maeneo husika,” amesisitiza.

“Asitokee mtu mmoja anatengeneza oda na kuleta dawa ambazo hazihitajiki na kufanya tuwe na dawa zinazokwenda kuharibika bila matumizi,” amesema Dkt. Rutachunzibwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ugavi na Uendeshaji wa MSD, Hassan Ibrahim, amesema ushirikiano na mawasiliano ya karibu kati ya wadau wa sekta ya afya ni muhimu katika kuhakikisha changamoto za mnyororo wa ugavi zinatatuliwa kwa wakati.

“Tunatamani tuwe tunaongea lugha moja katika kutatua changamoto za mnyororo wa ugavi wa bidhaa za afya ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora,” amesema Hassan.

Naye Meneja wa MSD Kanda ya Dodoma, Mwanashehe Jumaa, amesema jukumu kubwa la MSD ni kuhakikisha bidhaa za afya zinapatikana kwa wakati kwa wateja wake kupitia ushirikiano wa karibu na wadau wa mnyororo wa ugavi.

Amesema vikao hivyo vinasaidia kupata mrejesho kutoka kwa wateja na kujadili namna bora ya kuboresha upatikanaji wa bidhaa za afya.

Kwa upande wake, Katibu wa Afya wa Wilaya ya Chamwino, Loveness Raphael, amepongeza utaratibu wa MSD wa kukutana mara kwa mara na wadau wa sekta ya afya kwa kuwa unasaidia kujadili changamoto na kuweka mikakati ya kuboresha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba kwa wananchi.
Posted by MROKI On Friday, May 15, 2026 No comments






Na Mwandishi Wetu, Shinyanga
Kuanzishwa kwa masoko ya madini ya almasi na dhahabu mkoani Shinyanga kumechochea kwa kasi ongezeko la uzalishaji, biashara na mapato ya Serikali, huku wachimbaji na wafanyabiashara wakinufaika na kusogezewa huduma karibu nao.

Akizungumza katika Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Shinyanga, Mthaminishaji wa Madini ya Almasi, Shikimayi Muyinza, amesema uzalishaji wa almasi umeongezeka kwa kiwango kikubwa kutokana na kuibuka kwa machimbo mapya pamoja na uwepo wa masoko rasmi ya madini yaliyorahisisha biashara na kuongeza uwazi.

Amesema awali uzalishaji ulitegemea zaidi eneo la Maganzo karibu na Mwadui, lakini tangu mwaka jana machimbo mapya ya Ng’wapangabule yameongeza uzalishaji kwa kiasi kikubwa kutokana na kuongezeka kwa wachimbaji wadogo.

Kwa mujibu wa Muyinza, mwezi Aprili 2026 pekee karati 6,177 za almasi zilinunuliwa sokoni, tofauti na hapo awali ambapo uzalishaji haukuwa ukifikia hata karati 1,000 kwa mwezi.

“Hili ni ongezeko kubwa sana. Sasa tunapata kati ya karati 3,000 hadi 6,000 kwa mwezi kutokana na vyanzo vipya vya uchimbaji na masoko ya madini,” amesema.

Ameeleza kuwa masoko ya madini yameongeza ufanisi wa huduma kwa kutoa uthaminishaji wa haraka na wa uwazi, ambapo wachimbaji husajiliwa, madini hupimwa na kupatiwa ushauri wa thamani kabla ya kuingia kwenye mauzo.

Muyinza amefafanua kuwa tofauti na dhahabu, bei ya almasi hutegemea sifa nne muhimu ambazo ni ukubwa, umbo, rangi na ubora wa ndani wa jiwe, hivyo kila almasi huwa na thamani yake ya kipekee.

Kwa upande wake, Mhandisi wa Migodi na Msimamizi wa Masoko Mkoa wa Shinyanga, Gerald Kabeho, amesema mfumo wa masoko ya madini umeondoa urasimu uliokuwepo awali na kurahisisha upatikanaji wa huduma zote muhimu ndani ya muda mfupi.

Naye Mkurugenzi wa Mwabu General Trading, Samweli Sita, amesema masoko hayo yamewaondolea wafanyabiashara changamoto ya kutafuta wanunuzi kwani sasa wauzaji na wanunuzi hukutana moja kwa moja sokoni na kufanya biashara kwa uwazi.

Aidha, amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuanzisha masoko ya madini nchini, hatua aliyosema imeongeza fursa za biashara, kuimarisha uchimbaji halali na kukuza sekta ya madini kwa wachimbaji wadogo na wakubwa.

Takwimu zinaonesha kuwa mafanikio hayo pia yameongeza makusanyo ya Serikali ambapo kuanzia Julai hadi Aprili mwaka wa fedha 2025/2026, Mkoa wa Shinyanga umekusanya shilingi bilioni 35.2, sawa na asilimia 110 ya lengo la shilingi bilioni 32, ikiashiria mchango mkubwa wa masoko ya madini katika kukuza uchumi wa taifa.
Posted by MROKI On Friday, May 15, 2026 No comments






Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Waziri wa Maliasili na Utalii, Ashatu Kijaji ametembelea banda la Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika maonesho ya Wizara ya Maliasili na Utalii yanayoendelea kwenye viunga vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Dodoma.

Mhe. Dkt. Kijaji, akiambatana na viongozi mbalimbali wa wizara hiyo, alifanya ziara hiyo mara baada ya kuwasilisha bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni mapema leo.

Katika ziara hiyo, Waziri alipata fursa ya kujionea na kupata maelezo kuhusu shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazotekelezwa kupitia sekta ya misitu nchini, ikiwemo uhifadhi wa misitu, utalii wa mazingira, uzalishaji wa mazao ya misitu pamoja na mchango wa sekta hiyo katika kukuza uchumi wa taifa.

Aidha, banda la TFS limeendelea kuvutia wadau mbalimbali wanaotembelea maonesho hayo kutokana na ubunifu na maonesho ya shughuli za uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.

Pamoja na mambo mengine, banda hilo pia linatoa huduma ya tiba ya kudungwa na nyuki (Api-Therapy) bure kwa wananchi wanaotembelea maonesho hayo. Huduma hiyo ni sehemu ya juhudi za TFS kuelimisha Watanzania kuhusu manufaa ya uhifadhi wa mazingira kupitia matumizi ya tiba za asili zinazotokana na rasilimali za misitu.

Kwa mujibu wa Mhifadhi wa TFS ambaye ni Afisa Nyuki kutoka Hifadhi ya Mazingira Asilia ya Vikindu, Brenda Mwakipesile alisema huduma hiyo inalenga kusaidia kuimarisha kinga ya mwili, kupunguza maumivu ya viungo, kuboresha mzunguko wa damu pamoja na kusaidia afya ya akili.

“Tumeileta huduma hii bure kwa wananchi ili kuwaonesha kuwa uhifadhi wa misitu hauishii kwenye miti pekee, bali pia unaweza kuzaa tiba za asili ambazo ni salama na zenye manufaa ya kiafya,” alisema Mhifadhi Brenda.

Katika maonesho hayo, viongozi mbalimbali waliotembelea banda la TFS leo pia walipata huduma ya kudungwa na nyuki kama sehemu ya kujionea kwa vitendo huduma hiyo ya tiba asilia, kama wanavyoonekana pichani.
Posted by MROKI On Friday, May 15, 2026 No comments


 

Posted by MROKI On Friday, May 15, 2026 No comments


Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Serikali imeipongeza Benki ya CRDB Bank Plc kwa juhudi zake za kuhamasisha uwekezaji nchini kupitia elimu ya fedha, uwekezaji wa hisa na uwezeshaji wa kiuchumi unaolenga kuwajenga vijana kuwa wawekezaji wa baadaye.

Pongezi hizo zimetolewa jana jijini Arusha na Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omar wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB iliyofanyika sambamba na Mkutano Mkuu wa 31 wa mwaka wa benki hiyo katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Semina hiyo ilikuwa na kaulimbiu isemayo “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa” na iliwakutanisha viongozi wa serikali, wanahisa, wataalamu wa masoko ya mitaji pamoja na vijana kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri Omar alisema vijana wanapaswa kushiriki kikamilifu katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji badala ya kutegemea ajira pekee.

“Kaulimbiu ya mwaka huu imebeba ujumbe mkubwa wa kimkakati kwa taifa letu. Vijana hawapaswi kuishia kutafuta ajira pekee, bali wanastahili kushiriki katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji,” alisema Waziri Omar.

Aidha, aliipongeza benki hiyo kwa hatua ya kufungua Ofisi ya Uwakilishi Dubai, akisema hatua hiyo imeongeza hadhi ya Tanzania katika sekta ya fedha na uwekezaji kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema benki hiyo itaendelea kuwawezesha vijana kupitia huduma za kifedha, ubunifu na programu za maendeleo ya ujasiriamali.

Alisema kupitia CRDB Bank Foundation na programu ya IMBEJU, maelfu ya vijana na wafanyabiashara wadogo wamefikiwa kwa mafunzo, mitaji na ushauri wa biashara.

“Tunaamini vijana wa leo si wateja tu wa benki yetu, bali ni wawekezaji, wabunifu na viongozi wa uchumi wa kesho,” alisema Dkt. Nsekela.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Neema Mori alisema uwekezaji katika hisa ni njia muhimu ya kujenga ustawi wa kifedha wa muda mrefu kwa vijana na familia za Kitanzania.

Profesa Mori alisema mafanikio ya Benki ya CRDB yanaonyesha namna uwekezaji wa muda mrefu unavyoweza kuleta matokeo chanya kwa wanahisa.

Alibainisha kuwa ndani ya miaka mitatu iliyopita thamani ya hisa za benki hiyo imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 253, huku bei ya hisa ikifikia wastani wa Sh2,800 kutoka Sh460 mwaka 2023.

Aidha, alisema bodi ya wakurugenzi inapendekeza gawio la Sh90 kwa kila hisa kutokana na matokeo mazuri ya kifedha ya mwaka 2025, ikiwa ni ongezeko la asilimia 38 ikilinganishwa na mwaka uliopita.

Profesa Mori aliwahamasisha wazazi kuanza kuwawekezea watoto wao hisa mapema ili kuwajengea msingi imara wa maisha ya kifedha ya baadaye.

Benki ya CRDB ni miongoni mwa taasisi kubwa za kifedha Afrika Mashariki na Kati, ikiwa na zaidi ya wateja milioni sita katika nchi za Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo pamoja na ofisi ya uwakilishi Dubai, Falme za Kiarabu.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, semina inayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), ambapo alitoa wito kwa Taasisi za Fedha nchini kupunguza riba na gharama nyingine za mikopo ili kuwawezesha wananchi wakiwemo vijana kupata mitaji ya kuwekeza kwenye shughuli zao za kiuchumi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).









Posted by MROKI On Friday, May 15, 2026 No comments

May 14, 2026






Na Mwandishi wetu, Dodoma
Wizara ya Madini imetoa siku tatu kwa wachimbaji na wanunuzi wa madini ya jasi kuwasilisha mchanganuo wa gharama za uzalishaji ili kupata suluhisho litakalowanufaisha pande zote katika biashara ya madini hayo.

Agizo hilo limetolewa leo Mei 14, 2026 jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, wakati wa kikao kati ya wachimbaji wa madini ya jasi na wanunuzi zikiwemo kampuni za saruji na wazalishaji wa gypsum kilichofanyika katika ukumbi wa Makao Makuu ya Tume ya Madini.

Dkt. Kiruswa amesema Serikali inahitaji kila upande kuwasilisha kwa kina changamoto zinazoukabili ili kufanya uchambuzi utakaosaidia kufikia muafaka wenye manufaa kwa wachimbaji, wanunuzi na watumiaji wa mwisho.

“Tunataka kila upande uainishe vitu vinavyouumiza upande mmoja na vinavyoubeba upande mwingine ili baada ya uchambuzi huo tupate suluhisho la pamoja,” amesema Dkt. Kiruswa.

Aidha, ameahidi Serikali kuyafanyia kazi malalamiko kuhusu tozo mbalimbali zinazotozwa na baadhi ya halmashauri ambazo zimeelezwa kuwa zinaongeza gharama za uzalishaji na biashara ya madini ya jasi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wachimbaji Wadogo wa Madini ya Jasi Mkoa wa Lindi, Salum Kassim, amesema bei ya madini hayo haijawahi kuongezeka tangu mwaka 2016 licha ya kupanda kwa gharama za uzalishaji ikiwemo mafuta, vipuri vya mitambo na mishahara ya wafanyakazi.

Amesema hali hiyo imeathiri uzalishaji na kufanya wachimbaji wengi kushindwa kupata faida kutokana na biashara hiyo.

Katika mapendekezo yao, wachimbaji wamependekeza bei ya tani moja ya jasi kwa Dar es Salaam na Pwani iongezwe kutoka shilingi 110,000 hadi 150,000, Mkoa wa Mtwara kutoka shilingi 75,000 hadi 95,000, Mkuranga kutoka shilingi 95,000 hadi 130,000 huku eneo la Kiranjeranje bei ikipendekezwa kuongezeka kutoka shilingi 60,000 hadi 75,000 kwa tani.

Kwa mujibu wa Kassim, marekebisho ya bei yatasaidia kufufua uzalishaji wa madini hayo na kuboresha maisha ya wachimbaji ambao kwa sasa wanakabiliwa na changamoto kubwa za uendeshaji.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa Manunuzi wa kampuni ya Dangote Cement Limited, Halima Kuchwa, ametoa tahadhari kuwa ongezeko la gharama za malighafi linaweza kuathiri bei ya saruji sokoni na hatimaye kumgusa mtumiaji wa mwisho.

Madini ya jasi ni miongoni mwa malighafi muhimu inayotumika katika uzalishaji wa saruji, gypsum na bidhaa nyingine za ujenzi nchini. Tanzania ina maeneo kadhaa yenye uzalishaji wa jasi ikiwemo Lindi, Mtwara, Pwani na Mkuranga. Kwa miaka ya hivi karibuni, wachimbaji wadogo wamekuwa wakilalamikia kupanda kwa gharama za uzalishaji huku bei ya soko ikibaki ileile kwa muda mrefu, hali inayodaiwa kupunguza tija na kuathiri uzalishaji wa madini hayo.
Posted by MROKI On Thursday, May 14, 2026 No comments










Na Mwandishi Wetu, Singida
Kamati ya Kitaifa  ya Ufungaji Migodi imeendelea na vikao vyake kwa siku mbili katika Mgodi wa dhahabu wa Shanta uliopo mkoani Singida kwa lengo la kujadili na kupitia Mpango wa Ufungaji wa Mgodi huo ili kuhakikisha unazingatia matakwa ya Sheria ya Madini, Sura 123 na Kanuni za Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira katika kufunga mgodi huo.

Akiongoza kikao hicho kilichowakutanisha wataalam kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Wizara ya Maji, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Madini, Tume ya Matumizi Endelevu ya Ardhi, Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Tume ya Madini pamoja na viongozi wa Wilaya, Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Ufungaji Migodi, Dkt. Abubakary Salama amesema  migodi mikubwa na ya kati inalazimika kisheria kuandaa mipango ya ufungaji migodi.

Amesema  kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Madini Sura ya 123 pamoja na Kanuni ya 206 ya Kanuni za Madini (Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira) za Mwaka 2010, wamiliki wa migodi wanapaswa kuandaa mpango wa ufungaji mgodi na kuuwasilisha kwa Mkaguzi Mkuu wa Migodi kwa ajili ya mapitio ya kitaalam kabla ya kuidhinishwa na Kamati ya Kitaifa ya Ufungaji Migodi.

Kwa upande wake, Mshauri Mwelekezi  kutoka kampuni ya MTL Consulting Company Limited, John Bosco Tindyebwa, amesema  kampuni hiyo imefanikiwa kuandaa na kuwasilisha Mpango wa Ufungaji wa Mgodi wa Singida Gold Mine unaomilikiwa na Shanta Mining Company kwa ajili ya mapitio ya kitaalam na uidhinishaji wa Kamati hiyo.

Ameongeza kuwa kampuni ya MTL itaendelea kushirikiana kwa karibu na Tume ya Madini, Shanta Mining Company pamoja na wadau wengine muhimu wa sekta ya madini ili kuhakikisha mpango huo unazingatia viwango vinavyotakiwa, kulinda mazingira na kuacha manufaa endelevu kwa jamii zinazozunguka mgodi huo baada ya shughuli za uchimbaji kukamilika.

Naye Meneja Mkuu wa Mgodi wa dhahabu wa Singida, Juma Kisonda, ameihakikishia Kamati kuwa mgodi huo unaendelea kuzingatia masuala ya usalama, afya na utunzaji wa mazingira, akisisitiza kuwa uongozi wa mgodi utatekeleza maelekezo yote yatakayotolewa na Kamati ya Kitaifa ya Ufungaji Migodi ili kuhakikisha ufungaji wa mgodi unafanyika kwa kuzingatia viwango vinavyokubalika kitaifa na kimataifa.
Posted by MROKI On Thursday, May 14, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo