Nafasi Ya Matangazo

February 12, 2026









Na WMJJWM – Arusha
‎Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mheshimiwa Dkt. Dorothy Gwajima, amepongeza mchango wa sekta binafsi na mashirika yasiyo ya kiserikali katika kuimarisha ustawi wa jamii, hususan watoto, vijana na familia, wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi ya SOS Children’s Villages Tanzania iliyofanyika Ngaramtoni, wilayani Arumeru mkoani Arusha.
‎Dkt. Gwajima amesema ameridhishwa na utekelezaji wa programu zinazolenga malezi chanya, ulinzi wa mtoto, maendeleo ya awali ya mtoto (ECD) na uwezeshaji wa kiuchumi kwa vijana na familia, akisisitiza kuwa jitihada hizo zinaendana na sera na miongozo ya Taifa. Amesema malezi bora na mazingira salama kwa watoto ni msingi wa kujenga Taifa imara.
‎Aidha, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali, mashirika ya kiraia na jamii katika kuhakikisha utekelezaji wa programu za maendeleo una matokeo endelevu, huku akiwataka wadau kuendelea kuzingatia mipango ya Taifa, hususan katika kukomesha ukatili dhidi ya wanawake na watoto.
‎Katika ziara hiyo, Waziri Gwajima ameshiriki kukabidhi pikipiki 15 zenye thamani ya shilingi milioni 40 kwa vijana wanufaika wa miradi ya SOS Children’s Villages Tanzania, akibainisha kuwa hatua hiyo inalenga kuwawezesha vijana kujitegemea kiuchumi kupitia ajira binafsi na ujasiriamali.
‎Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Mhe. Seleman Msumi, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuimarisha ustawi wa watoto, vijana na familia, akipongeza mchango wa SOS Children’s Villages Tanzania katika malezi, ulinzi wa mtoto na uwezeshaji wa vijana wilayani humo.
‎Naye Mkurugenzi wa SOS Children’s Villages Tanzania,  Thomas Kipng’ili, amesema kupitia Mradi wa Arusha Re-Innovation uliotekelezwa kwa miaka minne, shirika limewafikia vijana zaidi ya 1,000, ambapo 229 waliwezeshwa mitaji. Amesema mradi huo pia umewezesha walezi wa malezi mbadala 450, watoto 3,538 na familia 1,211 katika Halmashauri za Jiji la Arusha, Arusha DC, Meru na Karatu. Jumla ya shilingi milioni 173.5 zilitolewa kuwawezesha wanufaika 121, hatua iliyosaidia kuboresha ustawi wa watoto 346 waliokuwa katika mazingira hatarishi.
Posted by MROKI On Thursday, February 12, 2026 No comments



Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt.Asha-Rose Migiro, leo, Alhamis, Februari 12, 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Namibia hapa nchini, Mheshimiwa Gabriel Pandureni Sinimbo.

Mazungumzo hayo yamefanyika katika Ofisi Ndogo ya CCM, Lumumba, jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo yao, wamejadili masuala mbalimbali yenye lengo la kuendelea kuimarisha uhusiano wa kihistoria na urafiki wa kidugu kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha SWAPO, pamoja na uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Namibia.
Posted by MROKI On Thursday, February 12, 2026 No comments

February 11, 2026







Mtuhumiwa wa makosa nane ya kikodi Bw. Matondo Kilugala Malanda, mmiliki wa kampuni ya Matondo Breweries Investment Limited, iliyopo Wilaya ya Bukombe amefikishwa katika Mahakama Kuu mkoani Geita na kusomewa mashtaka nane ya kikodi yanayomkabili.

Mtuhumiwa huyo alifikishwa mbele ya Mahakama kuu Geita tarehe 10 Februari, 2026, ambapo shauri lake lilisikilizwa  na hakimu Mkazi Mhe. Cleofas Waane.

Akizungumza kuhusu shauri hilo, Wakili wa Serikali Bw. Emmanuel Cheneko amesema mtuhumiwa huyo anakabiliwa na makosa nane ya kikodi, ikiwemo kuanza uzalishaji bila kuwa na leseni halali, matumizi ya stempu bandia, kukutwa na bidhaa zinazopaswa kulipiwa ushuru wa bidhaa bila kulipiwa ushuru huo, pamoja na kushindwa kuandaa na kuwasilisha ritani za ushuru wa bidhaa kama inavyotakiwa kisheria.

Aidha, Meneja wa Idara ya Upelelezi wa Kodi Kanda ya Ziwa, Bw. Joel Mbilinyi, amewakumbusha wazalishaji wa pombe kali kuwa pamoja na kupata usajili kutoka BRELA, wanapaswa pia kupata leseni ya uzalishaji kutoka TRA kwa mujibu wa sheria, ili kuepuka kuchukuliwa hatua za kisheria.
Posted by MROKI On Wednesday, February 11, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Dennis Londo akizungumza na wafanyakazi wa FCC wakati alipotembelea Taasisi hiyo kwa ajili ya kujua majukumu ,jijini Dar es Salaam.
**************
Na Mwandishi Wetu 
Waziri wa Viwanda na Biashara Dennis Londo amesema Tume ya Ushindani (FCC) iendelee na majukumu  ya kusimamia ushindani katika kujenga imani ya walaji kwani sehemu ya huduma ndio wananchi wanapokutana na serikali

Londo aliyasema hayo wakati alipotembelea Tume ya Ushindani Jijini Dar es Salaam,amesema kuwa ushindani katika soko unajenga imani ya walaji kupata huduma zilizo bora na kufanya kuchangia uchumi wa nchi.

Amesema imani ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ni kuona Taasisi ya  FCC inaendelea kulinda ushindani nchini kwa taratibu na sheria zilizowekwa katika kuhakikisha walaji wanakuwa wa kwanza kutoa taarifa sahihi za huduma wanazozipata.

Aidha amesema kuwa katika kuhakikisha  wanalinda soko za bidhaa za ndani kwani Tanzania inafikiwa na mataifa mbalimbali hivyo bidhaa hizo zikitoka zikawa chini ya viwango kunafanya nchi kuathirika na kushindwa kupata fedha za kigeni.

Hata hivyo amesema kuwa wafanyakazi FCC kuendelea kutoa huduma bora ambazo zitachochea uwekezaji wa viwanda vitavyofanya kuendelea kuongeza ajira kwa vijana wa kitanzania.

Amesema matamanio ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kuona tija inaendelea kuongezeka katika malengo ya kukua kiuchumi na Dira ya Taifa 2050.

"Nina imani na FCC na Wizara tutaendelea kushirikiana katika kuwafikisha watanzania kwenye kupata huduma bora katika ushindani wa soko wenye uwazi bidhaa za ndani na nje ya nchi".amesema Londo 

Nae Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC) Khadija Ngasongwa amesema FCC imejipanga vyema kuendelea kushirikiana na  katika kutekeleza majukumu kwa mujibu wa sheria ili kuendelea kutoa huduma zenye tija kwa mlaji na Taifa kwa ujumla hususan katika masuala ya Ushindani, Udhibiti wa Bidhaa Bandia na Kumlinda Mlaji kwa lengo la kukuza ustawi wa uchumi jumuishi.

Khadija anesema  katika kutekeleza majukumu yetu kwa mujibu wa mamlaka tuliyopewa kisheria, Tume ya Ushindani (FCC) hufanya kazi kwa karibu na Wizara ya Viwanda na Biashara, Idara, Taasisi za Serikali, Wadau wa Maendeleo na Sekta Binafsi kwa kuzingatia dira na miongozo mbalimbali ya kisera, kitaifa na kimataifa ili kuhakikisha inatekeleza jukumu lake kama chombo cha usimamizi wa utendaji wa ufanisi wa uchumi wa soko kwa kulinda na kushajiisha uzingatiwaji wa misingi ya ushindani wa haki, kumlinda mlaji na kudhibiti bidhaa bandia katika soko la Tanzania Bara. 

Majukumu haya kwa pamoja yanalenga kulifanya soko kuwa shindani, salama na walaji wanajenga uaminifu katika bidhaa zinazoletwa sokoni na hivyo mazingira ya biashara kuchangia ukuaji endelevu na jumuifu katika uchumi na ustawi wa mtu mmoja mmoja.

Amesema FCC ina jukumu la kusimamia Ushindani katika Soko la Tanzania Bara kwa kuhakikisha kuwa inadhibiti makubaliano yanayofifisha Ushindani, matumizi mabaya ya nguvu ya soko na miungano ya kampuni inayolenga kuimarisha hodhi ya soko. Tume imepewa mamlaka ya kisheria ya kufanya uchunguzi endelevu (Inquisitorial Procedure) katika kushughulikia ukiukwaji wa Sheria ya Ushindani ambapo huweza kutoa maamuzi dhidi ya ukiukwaji huo, ikihusisha pia masuala ya kumlinda mlaji.

Aidha, FCC imepata mafanikio makubwa baada ya Marekebisho ya Sheria ya Ushindani  ambapo sasa Sheria hiyo inaweza kufanya maamuzi dhidi ya ukiukwaji wa mashauri yanayohusiana na masuala ya kumlinda mlaji badala ya masuala hayo kufanywa na mahakama pekee.

Aidha amesema  majukumu mengine wanayotekeleza ni pamoja na kuchunguza na kuchukua hatua kwa wafanyabiashara wanaobainika kujihusisha na uingizaji nchini, uuzaji, uzalishaji, usafirishaji na uhifadhi wa bidhaa bandia.

 Amesema FCC inatoa elimu au uraghibishi wa Ushindani  kushajiisha utekelezaji wa Sheria ya Ushindani kwa njia ya mashauriano na maelekezo kwa Taasisi za Umma bila kutumia taratibu za kisheria zenye adhabu mbalimbali. 

Hata hivyo Kaimu Mkurugenzi Mkuu amesema FCC inajukumu la kumlinda mlaji dhidi ya mbinu na mienendo kandamizi na hadaifu katika soko, na hivyo kutoa elimu kuhusu haki na wajibu wa mlaji kupitia vyombo vya habari, tovuti na mitandao yake ya kijamii, kutathmini na kusajili mikataba ya walaji inayoandaliwa na upande mmoja na hushughulikia malalamiko ya walaji wa bidhaa na huduma katika soko.

 Amesema  FCC imewezesha na kuimarisha uwekezaji baada ya kuongeza kizingiti cha ulazima wa kuiarifu FCC kuhusu kusudio la kuunganisha shughuli za kibiashara kutoka Shilingi milioni 800 hadi bilioni 3.5 ambapo kampuni za wajasiriamali wadogo na wa kati ambazo thamani ya jumla ya rasilimali zao haifiki kizingiti hicho cha Shilingi bilioni 3.5, zinaweza kuunganisha shughuli zao za kibiashara bila ulazima wa kuomba kibali kutoka FCC. 

Kwa hatua hiyo FCC tumewezesha ukuaji wa biashara ndogo na za kati ambazo zimeweza kuunganisha shughuli zao na kukuza kiwango cha mitaji ya SMEs na kuziwezesha kukopesheka na utafutaji wa teknolojia zaidi, ili kuweza kushiriki zaidi katika uwekezaji na biashara nchini.

 Katika hatua hiyo FCC ya Miungano ya kampuni  imekuwa ikileta faida kubwa katika uchumi wa soko ikiwa ni pamoja na kukuza mitaji ya kampuni husika, kuingia sokoni kwa wawekezaji wapya, kupatikana kwa teknolojia bora za uzalishaji, kuongezeka kwa uzalishaji na tija, kuwezesha upatikanaji wa uchaguzi wa bidhaa na huduma na hivyo kuwezesha bidhaa kupatikana kwa bei za ushindani na kuongeza mapato ya Serikali kwa njia ya kodi.

 Khadija amesema FCC imesogeza huduma karibu kwa kufungua Ofisi za Kanda katika Kanda ya Ziwa (Mwanza), Kanda ya Kaskazini (Arusha) na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini (Mbeya) pamoja na Ofisi ya Tanga.  Baada ya kufungua Ofisi hizo, FCC sasa tuna jumla ya Ofisi sita ikiwa ni pamoja na Dar es Salaam na Dodoma. Ofisi hizi zinawezesha usimamizi madhubuti wa Sheria ya Ushindani pamoja na Sheria ya Alama za Bidhaa kwa ufanisi zaidi.

Khadija amesema FCC imepata Cheti cha Ithibati ya utoaji wa huduma zenye viwango kimataifa, “ISO CERTIFIED 9001:2015” na usimamizi mzuri wa misingi ya Ushindani, kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara na uwekezaji ni jambo tunaloliangalia kwa karibu sana na kuliimarisha na kuwapa wawekezaji imani ya kuwekeza nchini kutokana na FCC kuaminika na kuwa miongoni mwa vyombo vya kusimamia uchumi wa soko, kwa kuhakikisha urahisi wa wawekezaji kuingia na kutoka sokoni bila vikwazo, na kwa kuhakikisha sheria, taratibu na kanuni za ushindani, kumlinda mlaji na kudhibiti bidhaa bandia zinasimamiwa vyema katika soko.

Mwenyekiti wa FCC Dkt.Aggrey Mlimuka akizungumza kuhusiana na majukumu yao kuishauri Taasisi yao katika utoaji huduma ,jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu FCC Khadija Ngasongwa akitoa maelezo kuhusisiana na Majukumu ya Taasisi hiyo kwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara  Dennis Londo wakati alipotembelea Taasisi hiyo jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Wafanyakazi  wakimsikiliza Naibu Waziri wakati alipotembelea ofisi hiyo jijini Dar es Salaam. 
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Dennis Londo akiwa katika picha ya pamoja na makundi ya muundo wa FCC ,jijini Dar es Salaam.

Posted by MROKI On Wednesday, February 11, 2026 No comments

February 10, 2026



Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi amesema kuwa Serikali inatambua jitihada za wabunifu wa nyenzo mbalimbali zinazosaidia kupunguza gesijoto inayotokana na matumizi ya mafuta kwenye vyombo vya moto.
 
Amesema hayo wakati mkutano na wadau kutoka Jumuiya ya Vyombo vya Moto vitumiavyo Umeme Tanzania (TAEMA) pamoja na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) jijini Dar es Salaam kwa lengo la kujadiliana na kuweka mikakati ya namna bora ya kuifanyia huduma hiyo iwe endelevu.
 
Dkt. Muyungi alitoa wito kwa wadau hao kuendelea kuongeza wigo wa huduma ya usafirishaji kwa kutumia magari ya umeme kwa kuwa hivi sasa Tanzania imeanza kuzalisha umeme wa kutosha hususan kutoka Bwawa la Nyerere. 
 
“Tunawahitaji sana ninyi wadau wa sekta hii ya usafirishaji wa vyombo vya moto vya umeme, mtumie fursa ya upatikanaji wa umeme wa uhakika kwani mtasaidia katika kupunguza uzalishaji wa gesijoto,” alisisitiza.
 
Aidha, Dkt. Muyungi alipongeza mchango wa COSTECH katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi hususan kupitia tafiti zake ikiwemo Programu ya Utafiti wa Mabadiliko ya Tabianchi.
 
Pamoja na hayo alitoa wito kwa Tume hiyo kuwekeza kwenye teknolojia ya kukabiliana na maabdiliko ya tabianchi kuhakikisha inakuwa chanzo cha maarifa ya kukabiliana na changamoto hiyo.
Posted by MROKI On Tuesday, February 10, 2026 No comments
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (wa pili kulia) akilisha Samaki katika bwawa la kufugia nyumbani kwa Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Peter Pinda alipomtembelea nyumbani kwake Dodoma, Februari 10, 2026.
Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Peter Pinda akilisha Samaki katika bwawa la kufugia, wa pili kulia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni alipomtembelea nyumbani kwake Dodoma Februari 10, 2026. Wa mwisho kushoto ni Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Hassan Mitawi.
Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Peter Pinda akilisha Samaki katika bwawa la kufugia, wa pili kulia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni alipomtembelea nyumbani kwake Dodoma Februari 10, 2026. Wa mwisho kushoto ni Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Hassan Mitawi.
Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Peter Pinda (katikati) akizungumza na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (kushoto) alipomtembelea nyumbani kwake Dodoma, Februari 10, 2026. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Hassan Mitawi. 
Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Peter Pinda (katikati) akizungumza na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (kushoto) alipomtembelea nyumbani kwake Zuzu- Dodoma, Februari 10, 2026. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Hassan Mitawi. 
Posted by MROKI On Tuesday, February 10, 2026 No comments
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akiongoza kikao cha Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027), Katika ukumbi wa mikutano wa 
Ofisi ndogo ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam. Kikao hicho kimelenga kupitia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika maandalizi ya michuano hiyo mikubwa itakayofanyika mwaka 2027 katika nchi za Tanzania, Kenya na Uganda. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Paul Makonda akizungumza katika kikao cha Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027), Katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ndogo ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam. Kikao hicho kimeongozwa na Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba.
****************
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amekutana na Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) kwa ajili ya kupitia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika maandalizi ya michuano hiyo mikubwa itakayofanyika mwaka 2027 katika nchi za Tanzania, Kenya na Uganda.
 
Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amefanya kikao hicho leo Jumanne (Februari 10, 2026) Ofisi ndogo ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam.
 
Katika mazungumzo hayo, Waziri Mkuu amepongeza kazi kubwa inayofanywa na kamati hiyo, akieleza kuridhishwa na kasi na mwelekeo wa maandalizi yanayoendelea. 
 
“Maendeleo yaliyofikiwa hadi sasa yanaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuhakikisha Tanzania inakuwa mwenyeji bora wa michuano hiyo”.
 
Waziri Mkuu amesisitiza kuwa ni muhimu kuwepo kwa ushirikishwaji wa sekta zote, “mawaziri, makatibu wakuu pamoja na watendaji wengine hakikisheni mnazishirikisha sekta zetu kila mmoja katika eneo lake, tunataka kuona matokeo chanya katika michuano hii”.

 

Aidha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewataka wajumbe wa kamati hiyo kuhakikisha kila mmoja anasimamia kikamilifu eneo lake la uwajibikaji, ili hatua zote za maandalizi zikamilike kwa muda uliopangwa na kwa viwango vinavyokubalika.
Posted by MROKI On Tuesday, February 10, 2026 No comments

Dar es Salaam, Februari 10, 2026: Katika hatua inayoonesha mwelekeo mpya wa michezo ya kubahatisha nchini, PigaBet imezindua kampeni ya “SHINDA BODA” inayolenga si burudani pekee, bali pia kuwawezesha wachezaji—hasa vijana—kujipatia mtaji wa kujiajiri na kujiongezea kipato kupitia ushindi wa pikipiki mpya kila wiki.

Kampeni hiyo inawapa wachezaji wawili kila wiki fursa ya kushinda boda boda, zawadi ambayo kwa wengi imekuwa nyenzo muhimu ya kujiajiri au kuongeza kipato cha kila siku. Kupitia mfumo wa PigaPoints, kila mchezaji anayeshiriki michezo ya PigaBet ikiwemo Sports Betting, Casino na Aviator hujikusanyia pointi kwa kila bet au raundi, hali inayoongeza nafasi yake ya kuingia kwenye droo ya ushindi.

Akizungumza kuhusu dira ya kampeni hiyo, Meneja Masoko wa PigaBet, Arthur Kazora, alisema kampeni ya Shinda Boda inalenga kuwafanya wachezaji waone thamani ya muda na ushiriki wao.

“Tumelenga kumwezesha mchezaji kubadili ushindi kuwa fursa ya maisha. Boda si zawadi tu, ni chombo cha ajira, ni mtaji na ni mwanzo wa safari ya kujitegemea kiuchumi,” alisema Kazola.

Tofauti na kampeni nyingi za awali, Shinda Boda imebuniwa kuunganisha burudani, ushindi na uwezeshaji wa kiuchumi. Wachezaji hawazuiliwi na mchezo mmoja pekee, bali wanaruhusiwa kucheza michezo mbalimbali ndani ya jukwaa la PigaBet, jambo linalowawezesha kukusanya pointi zaidi na kuongeza nafasi ya ushindi.

PigaBet pia imeendelea kuvutia wachezaji kwa promosheni zinazolinda na kuongeza thamani ya mchezaji, ikiwemo 10% Cashback kila Jumatatu kwa bet zilizopotea, Win Boost hadi 1000%, pamoja na huduma ya 2UP na Cashout, vinavyompa mchezaji udhibiti zaidi wa michezo yake.

Kwa kutambua nguvu ya mitandao ya kijamii, kampeni hiyo pia imefungua milango kwa content creators kupitia PigaBet Content Creator Challenge, itakayoratibiwa na mshirika wao WAKA.WIN. Kupitia mpango huo, wabunifu wa maudhui watapata nafasi ya kunufaika kifedha kwa kushiriki kikamilifu katika kuhamasisha kampeni.

Wadau wa michezo ya kubahatisha na vijana kwa ujumla wamehimizwa kujisajili kupitia www.pigabet.co.tz na kushiriki kampeni hiyo, huku PigaBet ikisisitiza umuhimu wa kucheza kwa uwajibikaji kwa watu wenye umri wa miaka 18 na kuendelea.

Kwa mtazamo mpya unaoangazia ajira na uwezeshaji, Shinda Boda imejipambanua kama kampeni inayotazama mbali zaidi ya ushindi wa muda mfupi, na kuweka msingi wa matumaini mapya kwa vijana wanaotafuta fursa za kujikwamua kiuchumi.

Posted by MROKI On Tuesday, February 10, 2026 No comments



 

Posted by MROKI On Tuesday, February 10, 2026 No comments

February 09, 2026




Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amekutana na kufanya mazungumzo na Bw.Frederic Van de vyver Mkuu wa Jeune Afrique Media Group, kampuni inayoongoza ya habari ya ki-panafrika yenye makao yake makuu jijini Paris, Ufaransa. 

Katika mazungumzo yao yaliyofanyika katika Ofisi ya Msajili wa Hazina, wamejadiliana ni kwa namna gani wanaweza wakafanya kazi pamoja katika fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo nchini.

Bw. Mchechu alimhakikishia Bw. De vyver kuwa Tanzania ina mazingira mazuri ya uwekezaji na kwamba atapata ushirikiano wa kutosha.

 “Kwa upande wa sekta ya umma utapata ushirikiano wa kutosha kutoka kwa Ofisi ya Msajili wa Hazin ana kwa upande wa sekta binafsi utapata ushirikiano kutoka kwa CEOrt,” alisema Bw. Mchechu.

Kwa upande wake Bw. De vyver alieleza dhamira yake ya kuimarisha ushirikiano na Tanzania.

“Lazima tutafute namna bora ya kushirikiana,” alisema.
Posted by MROKI On Monday, February 09, 2026 No comments

February 06, 2026



WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Februari 6, 2026 ameahirisha Mkutano wa Pili wa Bunge la 13 jijini Dodoma na kutumia fursa hiyo kuwaasa Watanzania wote kuwa na matumizi chanya ya mitandao ya kijamii na kuifanya kuwa nyenzo muhimu ya kujielimisha, kuendeleza biashara na kueneza ujumbe wa mshikamano.

Pia, Mheshimiwa Dkt. Nchemba ameiagiza Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum iweke kipaumbele cha kutoa elimu ya malezi bora katika kijamii kwa kushirikiana wadau mbalimbali wakiwemo Viongozi wa Asasi za Kiraia na Mashirika yasiyo ya Kiserikali.

Waziri Mkuu amesema suala la amani, usalama na utulivu ni jukumu la kila Mtanzania na linahitaji juhudi za pamoja katika nyanja mbalimbali, hivyo wote wanawajibika kuepuka masuala yote yanayochochea uvunjifu wa amani ikiwemo matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii.

Aidha, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa rai kwa Watanzania wote kuendelea kulinda Tunu za Taifa kwa kuwa ni wajibu wa kila raia kuziheshimu na kuziendeleza ili kuleta mshikamano na kuimarisha heshima ya Taifa.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuwawezesha wananchi kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuongeza upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya biashara ndogo za kati na kampuni changa.

“Tarehe 05 Februari, 2026 nilishiriki kwenye tukio muhimu la uzinduzi wa utoaji mitaji yenye thamani ya shilingi bilioni 200 ili kuwawezesha wakulima, wafugaji, wavuvi, wafanyabiashara, maafisa usafirishaji, wasanii na kampuni changa za vijana kuongeza mitaji, kukuza biashara na kuchangia ajira na ukuaji wa uchumi.”

Pia, Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kutoa mikopo mingine yenye masharti nafuu kupitia mifuko mbalimbali na kunufaisha wafanyabiashara wadogo, wajasiriamali na kampuni changa kwa kuwatambua na kuwasajili wafanyabiashara wadogo zaidi ya milioni moja na kuwapatia mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 707.4 kutoka taasisi za fedha za NMB, DCB na TCB.

Vilevile, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa rai kwa Watanzania kuendelea kutumia taasisi za kifedha zilizo rasmi na kuepuka taasisi zisizokuwa na usajili . “Hakuna benki yenye masharti mabaya kuliko yale ambayo baadhi ya Watanzania wanayapata kwenye kausha damu. Tusiziogope taasisi rasmi ili kujiepusha na matatizo ambayo yamekuwa yakijitokeza kwenye baadhi ya taasisi ambazo hazijasajiliwa.”
Posted by MROKI On Friday, February 06, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo