Nafasi Ya Matangazo

June 06, 2026






Dodoma 
Wizara ya Madini imekutana katika Bonanza la Michezo lililowashirikisha watumishi wa Wizara pamoja na taasisi zake zote, ikiwa ni utaratibu wa kawaida wa kukutana kila Robo Mwaka kwa lengo la kuimarisha ushirikiano, mshikamano na kufahamiana zaidi miongoni mwa watumishi.


Akizungumza katika bonanza hilo, lililofanyika Juni 6, 2026 katika Viwanja vya Shule ya Sekondari John Merlin, Mipango  jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, ameeleza umuhimu wa michezo na manufaa yake katika maisha ya kila siku, akibainisha kuwa michezo ni afya, burudani na ajira.

“Michezo ni afya kwa sababu inasaidia kujenga mwili imara na kukinga dhidi ya maradhi mbalimbali yasiyoambukiza. Afya inapokuwa imara, manufaa yake ni makubwa kwa mtu binafsi na taifa kwa ujumla,” amesema Dkt. Kiruswa.


Ameongeza kuwa michezo ni burudani kwa kuwa huwapa watu furaha, huondoa msongo wa mawazo na kuongeza amani ya moyo, hali inayochangia kuongeza ubora wa maisha na umri wa kuishi.

Kuhusu ajira, Dkt. Kiruswa amesema  katika nyakati za sasa michezo imekuwa sekta muhimu inayotoa ajira kwa wananchi wengi na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Vile vile, amependekeza katika mabonanza mengine Wizara kuangalia namna ambavyo michezo hiyo itawashirikisha watoto wa watumishi kama familia ya madini.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri amewapongeza watumishi wa Wizara ya Madini na taasisi zake kwa utendaji wao mzuri ulioiwezesha Wizara kuwa miongoni mwa wizara zenye utulivu na matokeo chanya katika utekelezaji wa majukumu yake.

 Amesema  hadi kufikia tarehe 5 Juni 2026, Wizara ilikuwa tayari imekusanya shilingi trilioni 1.27, na hivyo kuvuka lengo la shilingi trilioni 1.2 lililowekwa kwa Mwaka wa Fedha 2025/26.

Awali, akizungumza katika bonanza hilo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, amesema  bonanza hilo ni mwendelezo wa maelekezo ya viongozi wa Wizara ya kuhakikisha watumishi wanakutana mara kwa mara kwa ajili ya kuimarisha afya zao na kujikinga dhidi ya maradhi yasiyoambukiza.

“Siku za karibuni tumeshuhudia ongezeko la maradhi yasiyoambukiza ambayo yamekuwa na athari kubwa kwa wananchi. Hivyo, michezo ni sehemu muhimu ya kujenga afya bora,” amesema Eng. Samamba.

Ameongeza kuwa, Wizara inatambua watumishi wake kuwa ndiyo nguvu kazi kuu ya taasisi hiyo, hivyo itaendelea kuimarisha shughuli za michezo mahali pa kazi ili kukuza mshikamano, umoja na upendo miongoni mwa watumishi na kuongeza hatua hiyo itasaidia kuongeza ufanisi wa kazi na kuifanya Sekta ya Madini kuendelea kuchangia katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya nchi.

Watumishi wameshiriki katika michezo mbalimbali ikiwemo jogging, mpira wa miguu, Pete, riadha kufukuza Kuku, kukimbia na mayai, kukimbia na magunia, basketball, kuvuta kamba ambapo washindi wamepokea tuzo mbalimbali na medali.

Pia, wanamichezo walioshiriki Mashindano ya Mei Mosi  wamekabidhi vikombe viwili kufuatia ushindi walioupata wa mbio na pool table na hivyo kuishukuru Wizara kwa kuwapatia fursa ya kushiriki katika mashindano hayo.
Posted by MROKI On Saturday, June 06, 2026 No comments





Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba ametatua mgogoro wa ardhi uliodumu kwa miaka 41 kati ya Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Yohana  Mtume Nyololo wilayani Mufindi Mkoa wa Iringa na Familia ya   Yosefa Mgavilenzi ambaye ni msimamizi wa mirathi ya marehemu Michael Bakari Seveyage.

Akihutubia mkutano wa hadhara katika kata ya Igowole Mufindi Kusini, Waziri Mkuu alipokea malalamiko ya familia ya  Yosefa Mgavilenzi kuwa eneo lake lenye ukubwa wa ekari 107 limechukuliwa na Kanisa hilo bila fidia na aliomba Waziri Mkuu amsidie ili alipwe.

Mapema wiki hii Waziri Mkuu alituma timu ya wataalamu kutoka ofisi yake ambao walikwenda katika kata ya Nyololo na kufanya vikao vya maridhiano na viongozi wa Kanisa Katoliki, familia ya Yosefa, Wazee, viongozi wa Kata ya Nyololo na  kijiji  cha Nyololo Shuleni walioko madarakani na wastaafu pamoja na wananchi. 

Baada ya majadiliano yaliyochukuwa siku tatu pande mbili husika zilikubaliana kumaliza mgogoro kwa njia ya maridhiano ambapo Baba Askofu wa Jimbo la Mafinga, Vicent Mwagala alitoa shilingi milioni 20 kama fidia kwa familia ya Yosefa ambayo ilizipokea kwa moyo mkunjufu na kukubali kumaliza mgogoro huo.

Hati za maridhiano zilitiwa saini na Kanisa Katoliki Parokia ya Nyololo pamoja na familia ya marehemu Michael Bakari Seveyage leo Juni 5, 2026 katika kikao cha maridhiano kilichofanyika kwenye Ofisi ya Mtendaji wa Kata ya Nyololo wilayani Mufindi.

Paroko wa Parokia ya Yohana Mtume Nyololo alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hasan kwa sera yake ya maridhiano ambayo  imemuwezesha Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kuumaliza mgogoro uliodumu kwa miaka 41.

Alimshukuru Askofu wa Jimbo la Mafinga Vicent Mwagala kwa kutoa shilingi milioni 20 kama fidia kwa mlalamikaji hatua ambayo  imesaidia sana kufikia maridhiano  na alisisitiza kwamba mgogoro huo umeisha na sasa wataishi kwa amani kama jamii moja.

Mchungaji John Mbwiga ambaye ni Kiongozi wa familia ya mlalamikaji aliishukuru serikali kupitia kwa Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba aliyetuma timu ya watalaamu kutoka ofisini kwake ambao wamemaliza mgogoro huo ulioikosesha familia amani kwa miaka mingi na kwamba sasa wataishi kwa amani.

Mwenyekiti wa Kijiji Mstaafu wa kijiji cha Nyololo Shuleni, Jeremia Mngolage alliishukuru serikali hususan Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kazi anayofanya ya  kutatua migogoro mbalimbali katika jamii  kwa njia ya mardhiano.
Posted by MROKI On Saturday, June 06, 2026 No comments

June 05, 2026




Na Timothy Mwakyenda, Arusha
Mkurugenzi wa Idara ya Utalii kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Thereza Mugobi, amesema Maonesho ya Kimataifa ya Karibu-KiliFair 2026 yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuitangaza Tanzania kama kitovu cha utalii barani Afrika.

Maonesho hayo mbali na kutangaza utalii pia, yanatoa nafasi ya kuonesha vivutio mbalimbali vya utalii ikiwemo utalii wa misitu, kuimarisha ushirikiano wa wadau na kuvutia uwekezaji.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa maonesho hayo uliofanyika Juni 5, 2026 katika Viwanja vya Magereza mkoani Arusha, Dkt. Mugobi alisema Karibu-KiliFair imekuwa nyenzo muhimu ya kutangaza utajiri wa rasilimali za utalii zinazopatikana nchini na kufungua masoko mapya ya sekta hiyo.

Alisema maonesho hayo yanatoa fursa kwa taasisi za umma na sekta binafsi kuonesha bidhaa na huduma zao, kujenga mitandao ya kibiashara na kuimarisha ushirikiano unaochochea ukuaji wa sekta ya utalii.

“Karibu-KiliFair si maonesho ya kawaida bali ni uwekezaji wa kimkakati unaosaidia kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Tanzania, kuvutia wawekezaji wapya na kufungua masoko mapya ya bidhaa na huduma za utalii,” alisema Dkt. Mugobi.

Aliongeza kuwa maonesho hayo yanaendelea kuwakutanisha wadau wa utalii kutoka ndani na nje ya nchi, jambo linalochangia kuongeza mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Dkt. Mugobi alisema Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya utalii ikiwemo barabara, viwanja vya ndege na huduma za malazi ili kuongeza urahisi wa kufikia maeneo ya vivutio na kuboresha uzoefu wa watalii.

Pia alisisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia za kidijitali katika kuitangaza Tanzania kwenye masoko ya kimataifa, akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza mwonekano wa vivutio vya nchi na kuwafikia watalii wengi zaidi duniani.

Katika maonesho hayo, taasisi mbalimbali za umma na binafsi, ikiwemo Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), zinashiriki kutangaza huduma na fursa za uwekezaji zilizopo katika maeneo ya utalii wa mazingira na misitu ya hifadhi.

Karibu-KiliFair 2026 inaendelea kuthibitisha nafasi yake kama moja ya maonesho makubwa ya biashara ya utalii Afrika Mashariki, ikitoa jukwaa la kukuza ushirikiano, uwekezaji na utangazaji wa vivutio vinavyoifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa utalii barani Afrika.
Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Dodoma
WIZARA ya Madini imevuka lengo la ukusanyaji wa Maduhuli ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 baada ya kukusanya Sh trilioni 1.27 hadi Juni 5, 2026, dhidi ya lengo la Sh trilioni 1.2, huku ikitarajia kufikia Sh trilioni 1.3 ifikapo  Juni 30, 2026.

Kutokana na mafanikio hayo, watumishi wa Wizara hiyo na taasisi zake wametakiwa kuondokana na uzembe, kuongeza bidii na kufanya kazi kwa weledi ili kufikia lengo jipya la ukusanyaji wa Sh trilioni 1.4 lililowekwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Akizungumza katika kikao cha watumishi wote wa Wizara ya Madini na taasisi zake ambazo ni GST, TEITI, Tume ya Madini, STAMICO na TGC, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, amesema mafanikio yaliyopatikana yanapaswa kuwa chachu ya kuongeza juhudi katika usimamizi wa Sekta ya Madini kwa kuzingatia Sera, miongozo, kanuni na Sheria zilizowekwa.

Amesema watumishi wanapaswa kutambua kuwa wanapowahudumia wananchi wanatekeleza wajibu wenye thamani kubwa kwa taifa, hivyo wanapaswa kuwahudumia watu wote kwa usawa bila kujali itikadi, dini wala uraia wao.

“Wachache tuliokabidhiwa jukumu la kuhudumia sekta ya madini tunapaswa kuhakikisha watu wote wanahudumiwa kwa haki na uzalendo mkubwa ili kuendelea kujenga taifa letu,” amesema.

Amesema watumishi ndiyo injini ya Serikali katika sekta ya madini na kwamba mchango wao una nafasi muhimu katika kukuza uchumi wa nchi kupitia usimamizi bora wa rasilimali madini.

“Wito wangu ni kufanya kazi kwa bidii, weledi na kusimamia sera, miongozo, kanuni na sheria zilizowekwa ili sekta hii iendelee kutoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya taifa,” amesema.

Katibu Mkuu huyo amesema watumishi wanapaswa kujiepusha na vitendo vya rushwa, uvivu na uzembe ambavyo vinaweza kuharibu imani ya wananchi kwa wizara, taasisi zake na Serikali kwa ujumla.

“Tusiharibu imani ya wananchi kwa rushwa, uvivu na uzembe. Mtu mmoja anayepokea rushwa anaweza kuchafua kazi za watumishi wengi waadilifu. Tufanye kazi kwa uzalendo mkubwa ili kuhakikisha hakuna mtu au wachache miongoni mwetu wanaochafua taswira ya wizara, taasisi zetu na Serikali kwa ujumla,” amesema.

Amesema watumishi wanapaswa kuchagua kuwa mwangaza badala ya kuwa kivuli na kuendelea kuimarisha ushirikiano baina ya wizara na taasisi zake kwa kuwa wote ni timu moja yenye malengo yanayofanana.

“Kazi ya mwenzako ikichelewa, mafanikio yako pia yanachelewa. GST ikichelewa kutekeleza majukumu yake, Tume ya Madini nayo itaathirika. Tusaidiane kwa pamoja kufikia malengo yetu,” amesema.

Katika salamu za Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, watumishi wamepongezwa kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Aidha, imeelezwa kuwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini imepangiwa kukusanya Sh trilioni 1.4, lengo ambalo linahitaji watumishi kuongeza uwajibikaji, uadilifu na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao.
Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments











Na, mwandishi wetu – Mwanza
SERIKALI imezindua rasmi Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha Mkoa wa Mwanza, hatua inayolenga kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa na majanga katika mkoa huo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo leo tarehe 05 Juni, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa Said Mtanda, amesema kituo hicho ni nyenzo muhimu katika kufuatilia na kudhibiti matukio ya dharura kwa ufanisi zaidi. 

Amesema kupitia kituo hicho, mkoa unaweza kufuatilia matukio ya dharura kwa karibu, kukusanya na kuchambua taarifa kwa wakati pamoja na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau mbalimbali wa usimamizi wa maafa.

“Kupitia kituo hiki, taarifa muhimu zinafika kwa mamlaka husika kwa haraka ili kuwezesha maamuzi stahiki kufanyika kwa wakati,” anasema Mhe.Mtanda.

Ameongeza kuwa kituo hicho kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hatua inayorahisisha mtiririko wa taarifa na kuimarisha uratibu wa shughuli za kukabiliana na maafa kati ya ngazi ya mkoa na taifa.

Kwa mujibu wa Mhe. Mtanda, hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za serikali kujenga mfumo jumuishi wa usimamizi wa maafa wenye uwezo wa kutoa mwitikio wa haraka na wenye ufanisi katika kukabiliana na majanga.

Aidha, amewataka watumishi na viongozi kutumia mafunzo wanayopata kujenga uelewa, kubadilishana uzoefu na kuimarisha mshikamano wa kiutendaji ili kuboresha zaidi usimamizi wa maafa katika Mkoa wa Mwanza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, amesema kituo hicho kina umuhimu mkubwa kwa mkoa wa Mwanza na taifa kwa ujumla.

Amesema kituo hicho kinakuwa kitovu cha ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji wa taarifa za matukio ya dharura na maafa, ambapo kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hivyo kuwezesha upatikanaji wa taarifa kwa wakati na kufanya maamuzi ya haraka na sahihi.

“Kupitia kituo hiki, Serikali inaweza kufuatilia vihatarishi mbalimbali, kutoa tahadhari za mapema, kuratibu rasilimali za kukabiliana na maafa na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau wote wanaohusika na usimamizi wa maafa,”alisema.

Ameongeza kuwa, “Huu ni uwekezaji muhimu katika kuimarisha utayari wa mkoa na taifa kwa ujumla. Sambamba na hilo, timu ya mkoa ya kukabiliana na dharura tunayoizindua leo ndiyo nguzo kuu ya kukabiliana na matukio ya maafa kwa wakati.”

Vilevile amesema uzinduzi wa kituo hicho unakuja katika wakati muafaka ambapo serikali inaendelea kujiandaa na kuimarisha mifumo ya tahadhari ya mapema kufuatia taarifa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kuhusu uwezekano wa kutokea kwa hali mbaya ya hewa, ikiwemo athari zinazoweza kusababishwa na El Niño.
Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments

Dodoma
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametembelea banda la Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika kilele cha Maonesho ya Siku ya Mazingira Duniani 2026 yanayofanyika jijini Dodoma. 

Mhe. Balozi Dkt. Nchimbi ametembelea banda la REA leo Juni 5, 2026 ambapo ameelezwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Wakala maeneo ya Vijijini na Mkurugenzi wa Nishati Jadidifu na Teknolojia Mbadala Mha. Advera Mwijage.

Halikadhalika, Mha. Mwijage amemueleza Mhe. Balozi Dkt. Nchimbi kuwa, kupitia miradi inayotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA), imesaidia kupunguza athari za uharibifu na uchafuzi wa mazingira.

Maonesho ya mwaka huu yamepambwa na kauli mbiu isemayo: Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania
Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Ilemela, Mhe. Tinnar Andrew Chenge, aliyetaka kujua, kigezo kinachotumiwa na Serikali katika kutoza Kodi ya Majengo kupitia Mfumo wa Mita za Luku, bungeni jijini Dodoma.
*************
Na. Jordan Mbwambo, WF, Dodoma
Serikali imefafanua vigezo vinavyotumika katika utozaji wa Kodi ya Majengo (Property Tax) kupitia Mfumo wa Mita za Umeme za LUKU, hatua inayolenga kurahisisha ukusanyaji wa kodi na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mapato ya ndani.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Tinnar Andrew Chenge, aliyetaka kujua kigezo kinachotumiwa na Serikali katika kutoza Kodi ya Majengo kupitia Mfumo wa Mita za LUKU.

“Kwa sasa Serikali inatumia viwango mfuto katika kutoza kodi ya majengo kupitia mita za umeme za LUKU. Vigezo vinavyotumika kutoza kodi ya majengo kupitia LUKU ni nyumba ya kawaida ambayo inatozwa shilingi 18,000 kwa mwaka au shilingi 1,500 kwa mwezi na nyumba ya ghorofa ambayo inatozwa shilingi 90,000 kwa kila sakafu kwa mwaka au shilingi 7,500 kwa kila sakafu kwa mwezi,” alisema Mhe. Luswetula.

Aidha, alisema kuwa nyumba za nyasi, udongo, majengo ya huduma za jamii, ibada pamoja na nyumba zinazoishi wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea hazitozwi Kodi ya Majengo isipokuwa pale majengo hayo yanapotumika kwa shughuli za biashara.

Mhe. Luswetula alisema kuwa utaratibu huo unalenga kuhakikisha mfumo wa utozaji kodi unaendelea kuwa rahisi, wenye ufanisi na unaozingatia makundi maalum yanayostahili msamaha kwa mujibu wa sheria.
Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akisikiliza maelezo kutoka kwa Mwanafunzi wa Shule ya Msingi Manyinga ya Mvomero, Morogoro, Jackline Eliabi kuhusu utumiaji wa taka katika kutengeneza bidhaa mbadala, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akisikiliza maelezo kutoka kwa Mwanafunzi wa Shule ya Msingi Manyinga ya Mvomero, Morogoro, Jackline Eliabi kuhusu utumiaji wa taka katika kutengeneza bidhaa mbadala, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akisikiliza maelezo kutoka kwa Mwanafunzi wa Shule ya Msingi Dumila Juu ya mkoani Morogoro, Alhad Yusuph kuhusu matumizi ya michezo katika kuhamasisha utunzaji mazingira, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akitembelea na kukagua mabanda mbalimbali ya maonesho kuhusu shughuli za uhifadhi mazingira, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akitembelea na kukagua mabanda mbalimbali ya maonesho kuhusu shughuli za uhifadhi mazingira, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akitembelea na kukagua mabanda mbalimbali ya maonesho kuhusu shughuli za uhifadhi mazingira, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwa na viongozi mbalimbali wakiwa katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete wakishiriki Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani tarehe 05 Juni 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwasili katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Mkoani Dodoma kushiriki Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, leo tarehe 05 Juni 2026.

Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Asha-Rose Migiro, leo Ijumaa Juni 5,2026 amefanya mazungumzo na Mheshimiwa Marianne Young, Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, katika Makao Makuu ya CCM, Dodoma.

Mazungumzo hayo yalihusu maeneo ya ushirikiano wa maendeleo kati ya Tanzania na Uingereza, kwa kuzingatia vipaumbele vilivyobainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2025–2030, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs).

Viongozi hao walijadili fursa za kuendeleza ushirikiano kwenye maendeleo ya kijamii na kiuchumi, hususan katika kuwawezesha vijana na wanawake kupitia elimu, ujuzi, ubunifu na uwekezaji.

CCM inaendelea kuthamini ushirikiano wa kimataifa unaochangia maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi wa Tanzania.







Posted by MROKI On Friday, June 05, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo