Nafasi Ya Matangazo

August 07, 2026


Na Neema Chalila Mbuja
WIZARA ya Maliasili na Utalii imevunja rekodi ya kupokea  wageni zaidi ya 17,000  kwa siku kwenye  Maonesho ya mwaka huu ya Wakulima, Wafugaji  na Wavuvi maarufu  lama NANE NANE yanayoendelea kitaifa kwenye Viwanja vya John Malecela, Nzuguni Jijini Dodoma.

Makundi makubwa ya wananchi, wanafunzi na wadau mbalimbali wa uhifadhi na wanyamapori wamefurika kwenye banda l Wizara ya Maliasili na Utalii kwa ajili ya kuona wanyama aina mbalimbali waliopo kwenye bustani ya wanyamapori kwa lengo la kutangaza utalii wa ndani. 

Idadi hiyo inafanya banda la Wizara ya Maliasili na Utalii kuvunja  rekodi ya kutembelewa na wananchi wengi ambapo Bi. Amina Saleh  mmoja wa wananchi waliotembelea bustani ya wanyama anasema wamefurahishwa sana na ujio wa wanyamapori hao kwani hajawahi kuwaona wanyama ana kwa ana zaidi ya kwenye picha.

Tembo Mary aliyekuwa kwenye bustani hiyo ya Maonesho ya wanyamapori amekuwa kivutio kwa wanafunzi wengi na wananchi kwa ujumla kutokana na historia yake na usikivu alionao ambapo mwanafunzi Collins Msemwa wa Kato Victoria Academy anasema kuwa ziara hiyo ya shule imehamasisha wanafunzi wengi kupenda wanyamapori na kujifunza kwa kina tabia za wanyamapori hao.

Mamlaka ya Usimamizi wa  Wanyamapori Tanzania (TAWA) ambayo ndiyo msimamizi wa wanyamapori imefanikiwa kuleta wanyama Kama  Tembo, Simba, Nyumbu, Pofu, Ngiri maarufu Kama Kasongoyeye, Duma, Chatu, ndege Karani, Mbuni, ndege Korongo (Crane) ambaye ni alama ya nchi ya Uganda, na ndege Mwali (White Perican bird) mbalimbali waliopo kwenye bustani ya NANE NANE.






Posted by MROKI On Friday, August 07, 2026 No comments
Muonekano wa eneo utakapotekelezwa Mradi wa Bwawa la Farkwa, ujezi unatarajiwa kuanza Oktoba, 2026, katika Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma.
Na Adelina Johnbosco – MAELEZO
Tatizo la uhaba wa maji katika baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Dodoma linaelekea kupata ufumbuzi wa kudumu kufuatia ujenzi wa Mradi wa Bwawa la Farkwa utakaoanza kujengwa Oktoba mwaka huu.

Bwawa hilo litakalojengwa wilayani Chemba, kata ya Farkwa mkoani Dodoma litakuwa na uwezo wa kuzalisha lita milioni 128 kwa siku na kuhifadhi lita bilioni 390 na linatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 22.

Bwawa hili litahudumia hasa wilaya za Chemba, Bahi, Chamwino na maeneo mengine ndani na maeneo ya karibu na mkoa wa Dodoma, lengo ni kutokomeza kabisa upungufu wa maji ndani ya mkoa huo.

Ujenzi wa bwawa la Farkwa utatekelezwa na Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) kwa gharama ya Shilingi bilioni 163.43 hadi kukamilika kwake.

Aidha, jumla ya Shilingi bilioni 8.5 zimelipwa kama fidia kwa wananchi kutoka katika vijiji viwili vya Mombose na Bubutole waliopisha ujenzi.

“Tuliambiwa tunahamishwa na kulipwa, mwaka 2017 tathmini ilifanyika katika maeneo yetu, ila ukiwa bado hujapokea kitu mkononi unaona kama haiwezekani, lakini mwaka 2019 tukalipwa fidia zetu, tukaanza maisha mapya na yenye matumaini zaidi katika kijiji cha Sankwaleto kwenye makazi mapya” Bi. Rahma Petro, mkazi wa Farkwa

Hadi hapa, tayari inaonekana Dodoma yenye ukijani wakati wote, iwe mvua iwe jua, hakuna tena ukame katika mkoa huu pale mradi huu utakapokuwa umekamilika, yale yaliyokuwa yanasubiriwa kufanyika wakati wa kipindi cha mvua pekee yatafanyika pia kipindi cha kiangazi.

“Tumeajiandaa kwa vingi kwa kweli, kijamii na kiuchumi, tutalima kilimo cha umwagiliaji, tutafuga samaki na mengine mengi, ni furaha tupu. Hii ilikuwa ni hadithi ya muda mrefu ambayo tumezaliwa tukaikuta kutoka kwa wazee wetu, hakika leo inatimia” Bw. Suleiman Gawa, mkazi wa Farkwa

Akiwa katika eneo utakapotekelezwa mradi huo, hivi karibuni, Bw. David Manyama, Mhaidrojiolojia ambaye ni mtaalam wa maji chini ya ardhi kutoka Wizara ya Maji, amebainisha uwepo wa maji ya akiba kwa watumiaji kutokana na wingi wa lita za maji utaokaozalishwa na bwawa hilo.

“Mradi huu unaanza mwezi Oktoba, 2026, maandalizi yako tayari na baada ya kukamilika kwa mradi, si kwamba utaondoa kero ya maji tu bali hata kuchochea miradi mbali mbali ya kiuchumi kama vile kilimo cha umwagiliaji kisichosubiri msimu, ufugaji wa samaki na itakuwa ongezeko la maji katika hifadhi ya pori la akiba Swagaswaga Chemba, wanyama hifadhini watapata maji ya kunywa ya kutosha tofauti na hali ilivyo kwa sasa” Bw. David Manyama, Mhaidrojiolojia

Mradi huu mwisho wake ni kuleta maji, lakini suala la ajira wakati na baada ya mradi ni vitu vinavotegemewa pakubwa. Mwenyekiti wa kijiji chenye makazi mapya cha Sankwaleto, akaongea kuhusu wazawa kupata fursa mbalimbali kutokana na mradi huo.

“Kama kiongozi tumeshashirikishwa na kuhakikishiwa kwamba, sisi wazawa tutapewa kipaumbele katika fursa mbalimbali zinazotokana na huu mradi ikiwemo ajira wakati na baada ya ujenzi, hivyo nawasihi vijana na wakazi wenzangu wa hapa kuwa tayari, tusikubali kukaa kinyonge katika kuchangamkia fursa katika hizi” Bw. Khalifa Salum, mwenyekiti wa kijiji chenye makazi mapya Sankwaleto

Si nyumba na umiliki wa ardhi pekee kwenye maeneo ya makazi mapya waliohamia wananchi waliopisha mradi, bali shule na zahanati vimejengwa kwa ajili ya kuwahudumia.

“Kijiji cha Sankwaleto kimejengwa shule ya msingi na imeshaanza kazi, kuna nyumba za walimu na wanafunzi wote waliokuwa wakisoma kule kwenye vijiji vya zamani wako kwenye shule mpya wanaendelea na masomo, hakuna kilichosimama, pia zahanati inayowahudumia wananchi, kwa kweli tunashukuru sana” – Bi. Agnes Msote, Diwani wa kata ya Farkwa

Kukamilika kwa Bwawa la Farkwa kunatarajiwa kuimarisha usalama wa maji katika jiji la Dodoma na kuchangia kwa kiasi kikubwa maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi katika mkoa huo.

Juhudi hizo zinaendana na azma ya Serikali ya kuimarisha upatikanaji wa huduma za maji nchini kwa kuzingatia usimamizi endelevu wa rasilimali za maji na upatikanaji wake maeneo yote hasa katika maeneo ya vijijini pamoja na kuhakikisha juhudi za kufikisha huduma za maji katika vijiji vyote nchini linatimia ili kumtua mwanamke ndoo kichwani.
Posted by MROKI On Friday, August 07, 2026 No comments

August 06, 2026

Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Ndugu Aggrey Mwanri, akiwa ameambatana na wajumbe wengine wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, amepokelewa Makao Makuu ya CCM, jijini Dodoma, leo tarehe 6 Agosti 2026. Mapokezi hayo yaliyoandaliwa na CCM Mkoa wa Dodoma, yamehudhuriwa na wanachama, makada na viongozi mbalimbali wa CCM, akiwemo Makamu Mwenyekiti Mstaafu wa CCM (Bara), Mzee Philip Japhet Mangula.







Posted by MROKI On Thursday, August 06, 2026 No comments



Dodoma
Tume ya Madini imeendelea kuimarisha ukaguzi wa migodi nchini ili kuhakikisha shughuli zote za uchimbaji zinafanyika kwa kuzingatia sheria, usalama wa wafanyakazi, afya kazini na utunzaji wa mazingira, hatua inayolenga kujenga sekta ya madini yenye tija na endelevu.

Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma, Mjiolojia na Mkaguzi wa Migodi kutoka Tume ya Madini, Paschal Juma, amesema Kurugenzi ya Ukaguzi wa Migodi na Mazingira chini ya Mkurugenzi wake, Mhandisi Hamisi Kamando, ina jukumu la kusimamia na kufuatilia shughuli zote za uchimbaji ili kuhakikisha zinazingatia Sheria ya Madini, kanuni, sera na miongozo mbalimbali ya sekta hiyo.

Amesema Kurugenzi hiyo hufanya ukaguzi wa usalama na afya mahali pa kazi, hufuatilia utekelezaji wa mipango ya usimamizi wa mazingira, urejeshaji wa maeneo yaliyochimbwa pamoja na mipango ya ufungaji migodi kwa kuzingatia viwango vinavyolinda mazingira na kuhakikisha rasilimali za madini zinatumika kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Aidha, amesema Kurugenzi hiyo hupitia na kuidhinisha mipango ya uchimbaji, taarifa za utendaji wa migodi na usanifu wa miundombinu ya migodi, huku ikisimamia matumizi salama ya baruti kwa mujibu wa Sheria ya Baruti, Sura ya 45, na kanuni zake.

Paschal amesema Tume ya Madini inatumia Maonesho ya Nanenane kama jukwaa la kutoa elimu kwa wananchi, wachimbaji na wadau wa sekta kuhusu matumizi sahihi ya vifaa vya kujikinga, mbinu salama za uchimbaji, utunzaji wa mazingira pamoja na uhifadhi na matumizi salama ya baruti.

Amesisitiza kuwa elimu hiyo inalenga kuongeza uelewa wa wadau, kuimarisha uzingatiaji wa sheria na viwango vya usalama, kupunguza ajali migodini na kuendeleza sekta ya madini inayochangia ukuaji wa uchumi wa taifa kwa njia endelevu.
Posted by MROKI On Thursday, August 06, 2026 No comments

August 05, 2026






Dodoma
Kampuni ya CDICD Group Limited imeendelea kuimarisha mnyororo wa thamani katika Sekta ya Madini kwa kuchakata madini ya black granite na kuzalisha bidhaa mbalimbali za ujenzi zinazouzwa katika soko la ndani na nje ya nchi, hatua inayochochea ukuaji wa viwanda, kuongeza ajira na kukuza mauzo ya bidhaa zenye thamani.

Akizungumza jijini Dodoma kwenye Maonesho ya Nane Nane, Meneja wa CDICD, Shija Shimba, amesema kampuni hiyo imewekeza katika kiwanda cha kisasa cha uchakataji wa black granite kinachobadilisha mawe ghafi kuwa bidhaa mbalimbali zikiwemo countertops za majiko, paving stones, slabs za ujenzi na headstones zinazotumika katika makaburi.

Amesema shughuli za uchimbaji na uchakataji zinafanyika katika kijiji cha Manyemba, wilayani Chamwino mkoani Dodoma, ambapo kampuni imejikita katika kuongeza thamani ya madini kabla ya kuyapeleka sokoni.

Kwa mujibu wa Shimba, uwekezaji huo umeiwezesha CDICD kupanua masoko yake ndani na nje ya Tanzania. Mbali na kuuza bidhaa zilizochakatwa nchini, kampuni pia husafirisha black granite blocks kwenda China na nchi nyingine kwa ajili ya uchakataji zaidi katika viwanda vya nchi hizo.

Amesema kampuni huzalisha wastani wa tani 270 za black granite kwa wiki, huku bidhaa zake zikisambazwa kupitia vituo vya mauzo vilivyopo Dodoma na Victoria, Kinondoni jijini Dar es Salaam, pamoja na mikoa mbalimbali nchini.

Shimba amesema uwekezaji huo pia umefungua fursa za ajira kwa vijana kati ya 90 na 100 wanaofanya kazi katika maeneo mbalimbali, ikiwemo uendeshaji wa mitambo, udereva, uchomeleaji na shughuli nyingine za uzalishaji.

Ameongeza kuwa CDICD ilianza shughuli zake mwaka 2014 na imeendelea kupanua shughuli za uchimbaji wa black granite katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Chamwino, kabla ya kuhamishia shughuli zake Manyemba, ambako inaendelea na uzalishaji na uchakataji wa madini hayo kwa sasa.
Posted by MROKI On Wednesday, August 05, 2026 No comments






Na: Mwandishi Wetu
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, ameipongeza Halmashauri ya wilaya ya Songwe kwa kufanikisha miradi mingi ya maendeleo yenye tija kwa wananchi.

Chatanda ametoa pongezi hizo, Agosti 3, wilayani Songwe, katika ziara maalum ya viongozi wa UWT Taifa kukagua shughuli mbalimbali mkoani Songwe.

Amesema kuwa, serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, imejikita katika kutatua kero za wananchi kupitia miradi ya maendeleo.

"Nimejionea kwa macho kazi nzuri zimefanyika Songwe, mmegusa maisha ya wananchi, fedha za mikopo ya asilimia kumi zinafika kwa vijana, wanawake na wenye mahitaji maalum, hakika Songwe mmeonyesha mfano mzuri wa kuigwa," amesema Chatanda.

Akiwa Songwe, Chatanda na wajumbe wa Jumuiya hiyo, walipata fursa ya kutembelea kikundi cha wanawake cha 'Mama ni Nguzo' kinachojishughulisha na uchimbaji na uchenjuaji wa madini ya dhahabu. Kikundi hiki kimenufaika na mkopo wa shilingi milioni 100.

Aidha, walitembelea kikundi cha waponda kokoto Saza ambacho kimeonyesha uaminifu wa kurejesha mkopo wote wa shilingi milioni 23 waliokopeshwa awali huku uongozi wa Halmashauri ukijipanga kuwakopesha gari aina ya fuso ili kubeba mawe na hatimaye waweze kukuza mradi wao.

Katika hatua nyingine, wajumbe hao walitembelea mradi wa ujenzi wa Soko la Madini la CPA. Cecilia Kavishe, ambapo ujenzi wake umefikia asilimia 99.

Sanjari na hilo, wametembelea mradi wa ujenzi wa nyumba ya Katibu wa UWT wilaya, huku wakipongeza hatua nzuri iliyofikiwa.

Ziara hiyo ya siku tatu mkoani humo ni mahsusi kwa ajili ya kukagua uhai wa Chama, Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025-2030. 

Vilevile, kufanya mikutano ya ndani, kuongea na wanachama na wananchi kuwapongeza kwa kuendelea kuwa na imani na Chama hicho katika kuwatumikia.

Katika ziara hiyo, Chatanda ameambatana na viongozi wengine wakiwemo Ellen Bogohe (MNEC), Mjumbe wa Baraza Kuu la UWT Taifa Flora Magambe na Mbunge wa Viti Maalum, Dk. Catherine Joakim.
Posted by MROKI On Wednesday, August 05, 2026 No comments








Na Neema Chalila Mbuja, Dodoma
WAGENI mbalimbali wameendelea kumiminika kwenye Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii kwenye Maonesho ya Maadhimisho ya Siku ya Wakulima Duniani (NANE NANE), kujionea shughuli mbalimbali za uhifadhi na wanyamapori zinazofanywa na Wizara.

Miongoni mwa wageni waliotembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii ni pamoja na Wakuu wa Wilaya na Makatibu Tawala mbalimbali ambapo waliipongeza Wizara kwa ushiriki wa Maonesho hayo ya NANE NANE kwani wamekuwa wakichagiza uwepo wa wananchi wengi wanaokuja kufanya utalii wa ndani wa kuona wanyamapori.

Makatibu Tawala hao ni pamoja na Katibu Tawala wa Wilaya ya Kongwa Sozi Ngate, Katibu Tawala wa Wilaya ya Dodoma Mjini Sakina Mbugi, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kondoa Christina Kalekezi na Wakuu  wa Wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri na Mpwapwa Dkt. Sophia Kizigo.

Viongozi hao wamesema kila mwaka Wizara ya Maliasili na Utalii imekuwa ikipokea wageni wengi hususani wananchi na wanafunzi wanaotembelea banda lake kujifunza elimu kuhusu uhifadhi, wanyamapori, malikale, misitu na nyuki.

Katika hatua nyingine Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii Imepokea wananfunzi zaidi ya elfu moja waliofika kwa ajili ya kupata wa elimu na kuona wanyamapori hai ambapo wengi wao wamevutiwa na mnyama  Ngiri maarufu kama Kasongoyeye ambaye  ana umaarufu mkubwa kutokana na tabia yake na kutokuwa na woga.
Posted by MROKI On Wednesday, August 05, 2026 No comments






Na Neema Chalila Mbuja, Dodoma
BALOZI wa Tanzania nchini Italia na Mwakilishi Mkazi  wa Shirika la Chakula na Kilimo la  Umoja wa Mataifa (FAO), Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) na Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa (WFP),  Mhe. Mbarouk  Nassoro Mbarouk leo Agosti 04, 2026,  ametembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii  na kusema kuwa nchi ya Italia ina nafasi kubwa ya kuleta watalii wengi nchini.

Mhe. Balozi Mbarouk amesema Tanzania inafanya vizuri kwenye kutangaza utalii na vivutio vyake  na kuipongeza Wizara kwa kazi nzuri inayoifanya.

Katika hatua nyingine Wizara ya Maliasili na Utalii  imepokea ugeni wa Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Rajab Mruma ambaye ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kubuni mbinu za kutafuta utatuzi wa  changamoto za wanyamapori hai kuingia kwenye makazi ya wananchi kwa kujenga  uzio ili kuzuia uharibifu unaoweza kutokea.

Aidha, Mhe Jaji Mruma ametembelea bustani ya wanyamapori  hai iliyoko kwenye Maonesho ya Nane  Nane yanayoendelea Jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya kutangaza utalii wa ndani kwa wananchi.
Posted by MROKI On Wednesday, August 05, 2026 No comments

August 04, 2026






Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe kupitia programu ya Polisi Jamii limeendelea kuonesha mshikamano na jamii baada ya kuwatembelea wakina mama waliojifungua, watoto na wagonjwa mbalimbali katika kituo cha afya cha Tnduma kilichopo Wilaya ya Momba, ambapo walikabidhi mahitaji mbalimbali na kuwasaidia kulipia gharama ndogo za matibabu. Hatua hiyo imelenga kuimarisha mahusiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi pamoja na kuhamasisha ushirikiano katika kudumisha amani, usalama na malezi bora ya watoto.

Akiongoza ziara hiyo Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Songwe, Kamishna Msaidizi wa Polisi Maria Kway, tarehe 04 Agosti 2026, alisema kuwa malezi bora ndiyo msingi wa kujenga taifa lenye maadili na usalama, hivyo aliwataka wakina mama kuhakikisha watoto wanapata haki zao za msingi, uangalizi unaostahili na kulindwa dhidi ya aina zote za ukatili, ikiwemo unyanyasaji wa kimwili, kisaikolojia na kijinsia. 

Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuzuia uhalifu na kulinda ustawi wa jamii.

Mwisho wananchi wamehimizwa kutumia elimu hiyo kwa kuwalea watoto katika mazingira salama, kuripoti matukio ya ukatili na uhalifu kwa wakati kwenye vyombo vya dola, pamoja na kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kudumisha amani, usalama na maendeleo ya jamii kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Posted by MROKI On Tuesday, August 04, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo