Nafasi Ya Matangazo

March 28, 2026

Sehemu ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA) wakiimba wimbo wa ‘Mshikamano Daima’ kabla ya kuanza kikao cha 37 cha Baraza hilo, kilichofanyika Machi 27, 2026 jijini Dodoma.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA), Alban Kihulla akifungua kikao cha 37 cha Baraza la Wafanyakazi wa Wakala hiyo kilichofanyika Machi 27, 2026 jijini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Sekta ya Afya (TUGHE), Ngazi ya Taifa, Rugemalira Rutatina akizungumza wakati wa kikao cha 37 cha Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA) kilichofanyika Machi 27, 2026 jijini Dodoma.
Baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA), wakichangia hoja mbalimbali wakati wa kikao cha 37 cha Baraza hilo kilichoketi Machi 27, 2026 jijini Dodoma.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA), Alban Kihulla (katikati) akiongoza kikao cha 37 cha Baraza la Wafanyakazi wa Wakala hiyo kilichoketi Machi 27, 2026 jijini Dodoma. Kulia ni Katibu wa Baraza, Meckytidicy Ngonyani na kushoto ni Katibu Msaidizi, Fadhil Msane.



Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA) wakiimba wimbo wa ‘Mshikamano Daima’ baada ya kuhitimisha kikao cha 37 cha Baraza hilo kilichofanyika Machi 27, 2026 jijini Dodoma.
***************
Na Mwandi wa WMA – DODOMA
Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA), Alban Kihulla amewataka watendaji wa Wakala hiyo kuanza ukaguzi wa mazao ya shamba na kupambana zaidi na ufungashaji wa mazao hayo kwa mtindo wa lumbesa.

Akifungua Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa WMA, Machi 27, 2026 jijini Dodoma, Kihulla amewasisitiza wajumbe wa Baraza hilo kufikisha ujumbe huo kwa watumishi wote katika maeneo yao kuanza kutekeleza jukumu hilo kikamilifu.

“Lakini tunapotekeleza majukumu haya, tuhakikishe haki katika biashara na kulinda mapato ya Serikali,”ametahadharisha.

Amesema kuwa katika kipindi cha kuanzia Julai 2025 hadi Machi 2026, WMA imepata mafanikio mbalimbali katika utekelezaji wa majukumu yake ya kumlinda mlaji kupitia uhakiki wa vipimo lak
ini pia kumekuwepo na changamoto kadhaa.
Akidadavua, amesema mafanikio yaliyopatikana yametokana na juhudi, weledi na ushirikiano wa watumishi wote wa Wakala hivyo amewapongeza kwa kazi nzuri wanayoendelea kufanya.

“Pamoja na mafanikio hayo, bado tunakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na ongezeko la wigo wa majukumu yetu katika kumlinda mtoa huduma pamoja na mpokea huduma,” ameeleza.

Mtendaji Mkuu Kihulla amebainisha baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na jukumu la uhakiki wa vipimo vinavyotumika kupima muda wa maongezi pamoja na uhakiki wa mita za maji na vilevile lumbesa; suala ambalo liliungwa mkono na Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Sekta ya Afya (TUGHE), Ngazi ya Taifa, Rugemalira Rutatina ambaye pia alishiriki mkutano huo, akisema yako malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi katika maeneo hayo hivyo yanapaswa kushughulikiwa.

Kihulla amesisitiza kuwa hata viongozi wakuu wa Wizara akiwemo Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga wameielekeza WMA kupambana na ufungashaji mazao ya shamba kwa mtindo wa lumbesa ili kuwalinda wakulima.

Katika hatua nyingine, Mtendaji Mkuu amewahimiza wafanyakazi wote wa WMA kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na uzalendo akiwataka kutambua kuwa kazi wanayofanya ina mchango mkubwa katika kulinda haki za wananchi pamoja na kukuza biashara ya ushindani na haki, ikiwemo pia kuongeza mapato ya Serikali.

“Kwahiyo, niwaombe sana mkawasisitize watumishi waliopo katika vituo vyenu kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na weledi na kubwa zaidi kujiepusha na vitendo vya rushwa.”

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la WMA, Isaac Birahi aliushukuru Uongozi wa Wakala hiyo kwa kuendelea kuweka mazingira mazuri ya ufanyaji kazi kwa watumishi na kuomba hali hiyo iendelee kwa viwango vya juu zaidi.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Sera na Mipango, Nelson Ruturagala, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango na Bajeti katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 16, 2026 alisema kuwa Wakala imefanikiwa kutekeleza Mpango Kazi wake kwa wastani wa zaidi ya asilimia 91.62

Akidadavua, aliyataja maeneo ya utekelezaji yaliyochangia kufikia wastani huo kuwa ni katika usimamizi wa vipimo, ukaguzi, uhakiki wa bidhaa zilizofungashwa zinazoingia nchini pamoja na ada kutokana na utolewaji wa huduma.

Katika kikao hicho cha 37, wajumbe wa baraza walipata pia fursa ya kujadili Mpango na Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027.
Posted by MROKI On Saturday, March 28, 2026 No comments








Na Mwandishi Wetu, Kahama
Naibu Waziri wa Nishati Mh. Salome Makamba amekabidhi vitendea kazi vya usafiri kwa TANESCO Mkoa wa Shinyanga kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi na kutatua changamoto zao kwa haraka.

Akizungumza leo tarehe 27, Machi 2026 wakati wa hafla ya kukakabidhi vitendea kazi hivyo iliyofanyika katika Manispaa ya Kahama Mkaoni Shinyaga Mhe. Salome amesema  hatua hiyo ya kukabidhi vitendea kazi hivyo ni kuyaishi maono ya Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma za Umeme wa uhakika.

Amesema vitendea kazi  hivyo vinakwenda kuongeza ufanisi katika utendaji kazi kwa watumishi wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga na kuwawezesha kutatua changamoto za wateja kwa wakati. 

“Kupitia vyombo hivi vya usafiri vitakwenda kuleta mabadiliko makubwa katika kumfikia mteja kwa haraka na kumhudumia, niwaombe mvitumie kutatua changamoto zao kwa wakati “ amesema Salome.

Aidha Mhe. Salome ametumia nafasi hiyo kuwataka wakazi wa Manispaa ya Kahama kuchangamkia matumizi ya Nishati safi ya umeme kupikia kwani Nishati ya umeme ni nafuu salama na rafiki kwa mazingira.

“Niwaombe wakina mama wa Kahama tuchangamkie matumizi ya nishati safi ya kupikia ya umeme, TANESCO wameleta majiko hapa unapika kwa urahisi na haraka zaidi”.

Hata hivyo Mhe. Salome amesema Serikali kupitia Shirika la Umeme TANESCO inaendelea kwa kasi kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katika Manispaa ya Kahama kutokana na kuendelea kukua kwa Mji huo ambapo mpaka sasa tayari zaidi ya  Shilingi milioni 600 zimetengwa kwa ajili ya kujenga laini mpya ya umeme itakayo wahudumia wakazi wa Manispaa ya Kahama.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga Mhandisi Benson Mbigili amesema wamepokea vitendea kazi mbalimbali ikiwemo Magari manne (4), Bajaji moja (1)  pamoja na Pikipiki nne (4). 


Mha. Benson ameipongeza Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania TANESCO kwa kuwezesha vitendea kazi hivyo ambavyo kwa sasa wanakwenda kuvitumia kufikisha huduma kwa wananchi kwa haraka zaidi.

Amesema kupitia Magari hayo sasa yatawasaidia kuwafikia wateja wapya katika maeneo yote hasa yale korofi ambapo kabla ya Magari hayo ilikuwa changamoto kuwafikia na kuwaahidi wananchi kuendelea kutoa huduma bora na ya uhakika kila wakati.

“Tunaishukuru Serikali kupitia Shirika la umeme Tanzania TANESCO kwa kutupa vitendea kazi hivi ambavyo kwa sasa tunakwenda kuvitumia kufikisha huduma kwa wananchi kwa haraka zaidi.

Aidha amesema TANESCO Mkoa wa Shinyanga inaendelea kwa kasi kubwa kuhamasisha matumizi ya Nishati safi ya kupikia kwa umeme ili wananchi waweze kuelewa umuhimu wa kutumia nishati hiyo kupikia.
Posted by MROKI On Saturday, March 28, 2026 No comments

March 27, 2026








Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) zimethibitisha azma ya kuendeleza ushirikiano katika kukuza sekta binafsi, uwekezaji na uchumi endelevu kwa manufaa ya pande zote mbili.

Hayo yameelezwa katika mazungumzo kati ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb), na Mkurugenzi wa IFC Kanda ya Afrika Mashariki, Mary Porter Peschka, yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Kombo amepongeza mchango mkubwa wa IFC katika kuimarisha sekta ya fedha nchini, hususan kupitia usaidizi kwa benki za NMB, CRDB na NBC. Amesema ushirikiano huo umeongeza upatikanaji wa mikopo na mitaji, na kuwa msaada muhimu kwa wajasiriamali wadogo na wa kati.

Aidha, Serikali imetambua mchango wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) katika maendeleo ya miundombinu, ikiwemo huduma za ushauri kwa miradi ya kimkakati kama mradi wa mabasi yaendayo haraka (BRT) jijini Dar es Salaam. Amesema ushiriki wa shirika hilo katika sekta za kilimo-biashara na viwanda pia umechangia kuongeza thamani ya mazao na kufungua fursa za ajira kwa Watanzania.

Mhe. Kombo amesisitiza kuwa Serikali inaendelea kuipa kipaumbele sekta binafsi kama injini ya ukuaji wa uchumi, kwa lengo la kuendeleza viwanda na kuongeza thamani ya bidhaa ili kufikia malengo ya maendeleo ya taifa ifikapo mwaka 2050.

Kwa upande wake, Bi. Peschka ameipongeza Tanzania kwa utekelezaji mzuri wa miradi inayofadhiliwa na IFC, na kueleza kuwa shirika hilo litaendelea kushirikiana na nchi katika kukuza matumizi ya teknolojia na kuandaa wataalamu watakaoongeza tija katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda, kilimo na miradi ya kimkakati.
Posted by MROKI On Friday, March 27, 2026 No comments




Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam 
Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imeanza kutekeleza ujenzi wa barabara Kilomita 42.78 kwa kiwango cha lami kupitia mradi wa Uendelezaji Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II) katika kata za Mjimwema, Kibada, Kigamboni, Vijibweni na Somangila zilizopo Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni.

Hayo yameelezwa na Kaimu Meneja wa TARURA wilaya ya Kigamboni, Mhandisi Edgar Tumsifu ambapo amesema kuwa mradi huo unaogharimu shilingi Bilioni 110 utekelezaji wake umefikia asilimia 30 huku tayari umeshaanza kuleta matokeo kwani barabara zilizokuwa na changamoto zimeshaanza kufanyiwa kazi na zikikamilika wananchi watanufaika na miundombinu hiyo.

"Tunaishukuru serikali ya Awamu ya Sita chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea mradi huu, TARURA Kigamboni tuna mtandao wa barabara Km 1035 kati ya hizo barabara za lami ni Km 10 lakini kupitia DMDP II imetuletea Km 42.78 kwahiyo tutakuwa na zaidi ya Km 50 za barabara za lami mpaka kufikia mwezi Agosti mwaka huu", amesema.

Ameeleza kuwa barabara hizo zikikamilika zitasaidia kupunguza uharibifu wa vyombo vya usafiri, pia kuna baadhi ya barabara ambazo ni 'bypass' zikikamilika zitasaidia wakazi wa Kigamboni wanaoelekea maeneo ya Kivukoni au darajani kufika kwa urahisi na haraka. 

"Leo tumetembelea barabara zenye urefu wa Km 10.48 zilizopo kata ya Kibada ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 68, mkandarasi anaendelea na ujenzi wa mitaro na njia za waenda kwa miguu, barabara hizi zikikamilika zitasaidia kupunguza foleni katika maeneo haya", amesema.

Amesema kazi zitakazofanyika katika mradi wa DMDP II ni ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, njia za waenda kwa miguu, vituo vya daladala, taa za barabarani na mifereji ya maji ya mvua zaidi ya Km 80.

Aidha, amewaomba wananchi wawe watulivu katika kipindi cha mpito cha ujenzi mara baada ya shughuli za ujenzi kukamilika mitaa yote itapendeza na kuwa safi na salama na pia wawe walinzi wa miundombinu hiyo wasitupe taka kwenye mitaro wala wasipitishe magari yenye uzito mkubwa.

Naye, Mwenyekiti wa mtaa wa Kichangani kata ya Kibada, Bw. Nassoro Chande amesema ubovu wa barabara uliokuwepo awali ulikwamisha shughuli zao za kiuchumi na kijamii lakini kwa sasa hali ya kiuchumi itaimarika kufuatia kuendelea kwa ujenzi wa barabara hizo ambazo kwa sasa watu wengi wanajenga maeneo hayo na kufanya thamani ya ardhi kupanda.

Bw. Frank Mwakipageme ambaye ni mfanyabiashara eneo la Shangwe kata ya Kibada amesema kuwa adha kubwa waliyokuwa wanaipata ni maji kujaa hasa kipindi cha mvua kwasababu eneo hilo kuna bonde lakini sasa wamepata nafuu baada ya kutengenezewa mitaro na wanafanya biashara zao bila shida na ameiomba serikali iendelee kuwaboreshea miundombinu ili kuzifikia huduma za kijamii kwa urahisi. 

Bw. Albano Nditi mkazi wa mtaa wa Kiziza ameishukuru serikali kwa kuwaboreshea miundombinu na ameomba waongezewe alama za barabarani na matuta na pia ameomba wananchi wenzake wailinde miundombinu hiyo kwa kuwa wastaarabu na kutotupa takataka kwenye mifereji.
Posted by MROKI On Friday, March 27, 2026 No comments


Mradi wa kuimarisha jamii pamoja na mifumo ikolojia katika kuhimili mabadiliko ya tabianchi ukanda wa misitu ya miombo umepanga kutumia Shilingi Bilioni 2.6 kwa mwaka 2025/26-2026/27 kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za mradi huo.
 
Akifungua kikao cha kamati tendaji ya Mradi huo Machi 27, 2026 Jijini Dodoma, Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Balozi Baraka Luvanda amesema mradi huo unatekelezwa katika misitu ya miombo Tanzania Bara na Maeneo Kame Zanzibar.
 
Amesema mradi huo unatekelezwa na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais-Zanzibar, Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo-Zanzibari, na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).
 
“Mradi huu umekusudia kuboresha na kuimarisha mazingira wezeshi ili kukuza matumizi ya teknolojia za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika sekta za kipaumbele hapa nchini” amesema Balozi Luvanda.
 
Mhe. Balozi Luvanda amebainisha kuwa mradi huo pia utaongeza mnyororo wa thamani ya mazao yasiyokuwa ya misitu, mbogamboga na malisho ya mifugo kwa ukanda wa maeneo ya miombo kwa Tanzania Bara na upande wa Zanzibar.
 
Amesema dhamira ya Ofisi ya Makamu wa Rais ni kuhakikisha inaongeza furs ana wigo wa upatikanaji wa miradi ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi nchini  kujenga uwezo kwa jamii zenye changamoto ya rasilimali fedha na uelewa mdogo wa mbinu za uzalishaji wa mazao.
 
Kwa upande wake Mratibu wa Mradi, Bw. James Chuyi amesema mradi huo unatekelezwa katika Mikoa saba iliyopo katika Halmashauri saba nchini kutoka upande wa Tanzania Bara na Zanzibar.
 
Ameitaja Mikoa hiyo kuwa ni Tabora (Sikonge), Rukwa (Nkasi), Katavi (Mpanda), Kaskazini Unguja (Kaskazini B), Kusini Unguja (Kusini), Kaskazini Pemba (Micheweni) na Kusini Pemba (Chakechake).
 
Mradi wa kuimarisha jamii na mifumo ikolojia katika kuhimili mabadiliko ya tabianchi ukanda wa misitu ya miombo unatekelezwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2025-2029 na unafadhiliwa wa Mfuko wa Dunia wa Mazingira (GEF) kupitia usimamizi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO).
Posted by MROKI On Friday, March 27, 2026 No comments








Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, leo tarehe 26 Machi 2026 amewasili Jijini Malabo nchini Guinea ya Ikweta, ambapo anamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi 
na Serikali wa Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki, utakaofanyika kuanzia tarehe 27 hadi 29 Machi 2026.

Katika Mkutano huo, Tanzania itapata fursa ya kuwasilisha vipaumbele vyake vya Kitaifa pamoja na kuchangia kuunda mwelekeo wa mikakati mipya ya jumuiya hiyo, inayoelekea kutimiza miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.

Ushiriki wa Tanzania katika Mkutano huo ni mwendelezo wa jitihada za kuendelea kushiriki kikamilifu katika majukwaa ya kikanda na kimataifa, na kudhihirisha mchango wa nchi katika mijadala ya maendeleo na ushirikiano wa kimataifa.

Aidha, Makamu wa Rais anatarajiwa kufanya mazungumzo ya pande mbili na viongozi mbalimbali wanaoshiriki Mkutano huo kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kimaendeleo.
Posted by MROKI On Friday, March 27, 2026 No comments

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira, akipiga makofi baada ya kuweka jiwe la msingi katika ofisi ya CCM Mkoa wa Geita. Kulia ni wajumbe wa Kamati ya Siasa Mkoa. 



Na Mwandishi Wetu, Geita
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira, amesema Chama kitaendelea kusimama imara kuwaletea maendeleo Watanzania kwa kuwa ndilo jukumu lake la msingi.

Aidha, amewataka wana CCM kutambua kuwa uchaguzi una gharama na moja ya gharama zake ni hasira hususani kwa walioshindwa, hivyo wasikubali hasira iwapeleke katika hasara.

Wasira ameyasema hayo leo Machi 26, 2026 alipozungumza baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo la ofisi za Chama Mkoa wa Geita ambalo ujenzi wake unatarajiwa kutumia sh bilioni 1.5.

“Chama chetu madhumuni yake ni mengi lakini kubwa ni kukamata dola, lakini watu wanatuuliza nyinyi mnataka kukamata dola ya nini, ukisoma katiba yetu nendeni mkasome madhumuni ni pamoja na kukamata dola, madhumuni makubwa kuliko yote ni kuhakikisha wananchi wanapata maendeleo, hiyo ndiyo kazi kubwa ya chama chetu.

“Sasa mnataka maendeleo ya Mkoa wa Geita lakini nyinyi ofisi yenu ya wasimamizi wa maendeleo mmejibanza kwenye vibanda, mnaweza kuulizwa maendeleo gani hayo yanayoweza kuletwa na chama hakina hata anuani.

“Kwa hiyo uko uhusiano kati ya jengo hili na wajibu wetu wa kusimamia maendeleo na tunasimamia maendeleo ndio maana tunataka dola, maana dola inatoza kodi tunajenga zahanati, dola inatoza kodi tunajenga chuo, dola inatoza kodi tunajenga miradi mingi ya maendeleo,” alisema.

Wasira alisema mtu yeyote ambaye anasema hakuna maendeleo yaliyofanyika huenda ana matatizo binafsi kwa kuwa kazi kubwa yenye kuonekana imefanyika. 

“Hatumtukani lakini na yeye naye tunadhani ana matatizo ya kufikiri kwa sababu vitu tunavyofanya vinaonekana. 

“Nimetoka Mwanza saa nne nimefika Geita saa tano kwa daraja lile la Magufuli kama lisingekuwepo ningefika hapa saa saba maana ningesubiri feri (kivuko) lakini tunafanya na hayo tunayoyafanya ndiyo ynayoeleza ukuu wa CCM katika kutekeleza majukumu yake ya kusaidia maendeleo ya watu na viongozi wetu wanachaguliwa na watu wenyewe,” alisema Wasira akitoa mfano wa sehemu ya maendeleo yaliyofanyika.

Mbali na hilo, Wasira alisema kunapofanyika uchaguzi ni muhimu kuvumilia hususan kwa wale ambao wamekosa nafasi ya kufikia malengo yao ya kisiasa.

“Ninataka niwaombe wanachama waliopo hapa wajitahidi sana kuwa na kifua kipana maana uchaguzi una gharama na ghamarama yake nyingine ni hasira tu, ukishindwa unakasirika sana, hiyo nayo ni hasara, unaweza ukakasirika lakini ukasirike kidogo tu maana ukikasirika sana presha ikipanda unaweza ukaugua halafu hasira ikageuka kuwa hasara.

“Kwa hiyo mambo ya uchaguzi haya yakipita tuwe tunakubali kwamba yamepipita yalivyopita sasa turudi pamoja tujenge chama chetu tujiimarishe,” aliwaeleza.
Posted by MROKI On Friday, March 27, 2026 No comments

March 26, 2026





Na Mwandishi Maalum, Dar es Salaam
Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius John Ndejembi ameutaka Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) kuhakikisha kuwa maghala yote makubwa ya usambazaji wa mafuta yanapata bidhaa hiyo kwa wakati, ili kuimarisha upatikanaji wake nchini.

Hayo yamesemwa  leo Machi 26, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa kikao chake na viongozi wa PBPA, Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) na kampuni ya TIPER kwa lengo la kujadili hali ya upokeaji wa mafuta yanayoingia nchini.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Ndejembi ameielekeza PBPA kuweka mfumo madhubuti wa upangaji wa ratiba ya ushushaji wa mafuta (sequencing) ili kuhakikisha maghala yote makubwa yanayohusika na usambazaji yanapata mafuta kwa usawa na kwa wakati.

 Amesema hatua hiyo itasaidia kupunguza changamoto za upatikanaji wa mafuta katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Aidha, ameeleza kuwa Serikali imekubaliana kuharakisha ushushaji wa meli za mafuta zinazoingia nchini, hususan kwa ajili ya matumizi ya ndani, ili kuhakikisha upatikanaji wa mafuta unaendelea kuwa wa uhakika na salama.

Ameongeza kuwa Serikali imefanya mazungumzo na Tanzania International Petroleum Reserves Limited (TIPER), na kuelekeza kuwepo kwa utaratibu mzuri wa kupanga ushushaji wa mafuta ili wasambazaji wote wapate huduma kwa usawa.

Waziri Ndejembi amewaasa Watanzania kutokuwa na taharuki kuhusu upatikanaji wa mafuta, akisisitiza kuwa nchi ina akiba ya kutosha. 

Vilevile, Mhe. Ndejembi,  ameitaka EWURA kuhakikisha kuwa mafuta yote yanayotoka kwenye maghala yanafika kwa walengwa na kutumika ipasavyo, huku vituo vya mafuta vikihimizwa kuuza bidhaa kulingana na mahitaji halisi ya soko.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio,  Mtendaji Mkuu wa PBPA, Bw. Erasto Simon, Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Andilile pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa TIPER, Bw. Mohamed Mohamed na wataalam mbalimbali wa sekta ya mafuta.
Posted by MROKI On Thursday, March 26, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo