Nafasi Ya Matangazo

August 13, 2026

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemjulia hali, Mama Fatma Karume,Mjane wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, ambaye anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Lumumba Zanzibar. Tarehe 13 Agosti 2026.


Posted by MROKI On Thursday, August 13, 2026 No comments
Mwenyekiti wa TASWA, Amir Mhando.
CHAMA cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), kimeandaa kampeni maalumu ijulikanayo kama ‘AFCON Kitaa 2027’, ambayo itazinduliwa rasmi Oktoba 30, 2026 jijini Dar es Salaam.

Kampeni hiyo ni mahususi kwa wanataaluma ya habari kwa ajili ya Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON), zitakazofanyika nchini mwaka 2027 na itahusisha matukio ambayo TASWA itayafanya kuelekea fainali hizo, ambazo Tanzania itaandaa kwa ubia na nchi za Kenya na Uganda.

Taarifa iliyotolewa na TASWA leo Agosti 13, 2026 na kusainiwa na Mwenyekiti wa wake, Amir Mhando imesema,Kampeni ya AFCON Kitaa 2027 itawafikia makundi yote katika jamii ili kuwapa hamasa ya kuchangamkia fursa za kufanyika ka
Wa michusno hiyo nchini.

"Kampeni ya AFCON Kitaa 2027 inatarajia kufikia makundi mbalimbali kuanzia wanahabari, wanamichezo, wanasiasa, wafanyabiashara, watumishi wa umma, wajasiriamali, vijana, wanawake na wanafunzi kuyataja kwa uchache, lengo Watanzania wote tuimbe wimbo mmoja kwamba AFCON 2027 ni fursa ya kitaifa," imesema sehemu ya taarifa hiyo.

Pia kuelekea uzinduzi rasmi wa AFCON Kitaa 2027, TASWA itaendesha warsha na makundi ya wanahabari kwa awamu tofauti, ikiwa ni mwendelezo wa mpango wake iliouanzisha Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam ujulikanayo kama Mustakabali wa Uandishi wa Habari za Michezo 'The Future Of Sports Journalism’.

Makundi hayo ni waandishi wa habari chipukizi, waandishi wa habari waandamizi, wachambuzi wa habari za michezo, wahariri wa habari za michezo. Pia itakutana na viongozi wa michezo wa sasa na wa zamani, lengo ikiwa ni kutazama mwelekeo wa uandishi wa habari za michezo na pia ujio wa AFCON Kitaa 2027.

Aprili 24, 2026 TASWA ilianza Awamu ya Kwanza ya Mpango wa Mustakabali wa Uandishi wa Habari za Michezo kwa kuendesha warsha iliyohusisha wanahabari chipukizi, wahariri wa habari za michezo na waandishi magwiji wa habari za michezo, ambapo mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwemo masuala ya rushwa kwenye michezo iliyotolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Posted by MROKI On Thursday, August 13, 2026 No comments

August 12, 2026

 

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Asha-Rose Migiro, amefungua rasmi Tawi la CCM Kibuteni, Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja, leo tarehe 12 Agosti 2026.

Tawi hili lina historia kubwa tangu nyakati za ASP na TANU, na ni jambo la kujivunia kuona sasa lina sura mpya inayokwenda sambamba na mahitaji na hadhi ya Chama.

Dkt. Migiro amewahimiza viongozi na wanachama kuhakikisha Tawi hilo linakuwa kituo cha uhai wa Chama, mshikamano, mafunzo, vikao na utekelezaji wa shughuli za Chama.

Pia, Katibu Mkuu amewashukuru wana-CCM wa Kibuteni kwa mapokezi mazuri, upendo na zawadi.




Posted by MROKI On Wednesday, August 12, 2026 No comments


Dodoma
Jaribio la kwanza la Mbegu ya viazi mviringo lililotafitiwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) limeonesha mafanikio makubwa mkoani Dodoma katika shamba la Makamu wa Rais Mstaafu  Mhe. Dkt Philip Mpango lililopo Kijiji cha Mayamaya, Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.

Jaribio hilo lililochukua  siku 104 za majaribio shambani hadi kuvuna limedhihirisha kuwa zao la viazi mviringo linaweza kustawi katika mazingira ya  Mkoa wa Dodoma na kuufanya Mkoa huo kuwa na fursa mpya ya zao la chakula na biashara ambalo linaweza kuwasaidia wananchi wa mkoa huo kuondokana na umasikini.

Akiongelea  kuhusu jaribio hilo na matokeo yake,  Makamu wa Rais  Mstaafu Mhe. Dkt. Philip Mpango, ameishukuru TARI kwa kusimamia jaribio hilo ambalo kwa mara ya kwanza limeonyesha mafanikio  katika Kijiji cha Mayamaya na kuwataka wakazi wa Mkoa wa Dodoma kuchangamkia fursa ya kulima zao hilo pindi utafiti utakapokamilika.

“ Wakazi wa  Dodoma sasa tuanze kuchangamkia hii fursa na TARI wako tayari kutusaidia kwa kutupatia mbegu bora zinazofaa zaidi na hii itatusaidia chakula na kipato kwa ajili ya kusaidia watoto wetu kwenda shule. Dodoma sio nusu jangwa, ni maarifa tu ya kupata na kuvuna maji kwa ajili ya kuendeleza kilimo chetu, hatuwezi kuendelea kwa kutegemea mtama, mahindi, zabibu au alizeti pekee lazima tuongeze na mazao mengine” alisema Mhe. Dkt. Mpango.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TARI, Dkt. Thomas Bwana amemshukuru Mhe. Dkt. Mpango kwa kukubali TARI kuweka jaribio  la viazi mviringo katika shamba lake  lililopo katika Kijiji cha Mayamaya na kueleza kuwa  kwa sasa TARI imepanga kuweka majaribio ya zao hilo kwa wakulima wadogo wanaolima kwa kutegemea mvua.

Katika hatua nyingine Dkt. Bwane ameongeza kuwa  TARI itaendelea na majaribio ya utafiti wa mazao katika maeneo mbalimbali nchini  ili kuondoa dhana iliyojengeka ya  ikolojia  hii ni ya mazao Fulani pekee na kuwaomba wananchi hususan wakulima  kuwakaribisha TARI kuweka majaribio ya utafiti katika mashamba yao.

Kwa mujibu wa Mtafiti Kiongozi  wa zao la viazi mviringo kutoka kituo cha TARI - Uyole Dkt. Owekisha Kwigizila, mbegu hiyo  mpya ya TARI ina sifa ya kukomaa kwa muda mfupi wa takribani siku 90, kustahimili ukame na baadhi ya magonjwa pamoja na kuwa na uwezo wa kuzalisha tani 35 hadi 40 kwa hekta moja.

Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Mayamaya walioshiriki katika zoezi la uvunaji wa viazi hivyo wameonesha kustaajabishwa na kustawi kwa zao hilo katika Kijiji hicho cha Mayamaya na kueleza kuwa hiyo ni mara yao ya kwanza kuona zao hilo la viazi likilimwa  na kustawi Mkoani Dodoma na kuonyesha shauku kubwa ya kujaribu kulima zao hilo katika mashamba yao,

Utafiti huo wa zao la viazi Mkoani Dodoma bado unaendelea ili kukamilisha hatua zote muhimu kabla ya mbegu hiyo kuingizwa rasmi sokoni. Mafanikio hayo yanaendelea kuthibitisha kuwa Dodoma inaweza kuzalisha mazao mbalimbali ya chakula na biashara kupitia nguvu ya utafiti, ubunifu na teknolojia za kilimo  na kubadilisha maisha ya wakulima wa Mkoa wa Dodoma.
Posted by MROKI On Wednesday, August 12, 2026 No comments


 

Posted by MROKI On Wednesday, August 12, 2026 No comments

August 10, 2026



Kuelekea Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii nchini, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limewataka Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lyoto kutoa taarifa za uhalifu.

Wito huo umetolewa Agosti 10, 2026 na Polisi Kata ya Ilemi Mkaguzi wa Polisi Elibariki Mambuye wakati akizungumza na Walimu na Wanafunzi hao na kuwahimiza kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za uhalifu ili kuzuia vitendo hivyo katika jamii.

Aidha, Mkaguzi wa Polisi Mambuye amewaeleza Walimu na Wanafunzi wa Shule hiyo kuhusu Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii ambayo yatafanyika kitaifa Mkoani Mbeya yakiwa yamebeba kauli mbiu inayosema, Miaka 20 ya Polisi Jamii: Tushirikiane kuimarisha Amani, Usalama na Umoja wa Kitaifa.
Posted by MROKI On Monday, August 10, 2026 No comments

Timu ya mpira wa miguu ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya imeibuka bingwa wa mashindano ya mpira wa miguu kanda ya nyanda za juu kusini baada ya kuwafunga goli moja kwa bila Polisi Mkoa wa Songwe.


Akizungumza mara baada ya fainali hiyo iliyochezwa Agosti 10, 2026 Mkoani Rukwa, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Benjamin Kuzaga amesema kuwa ushindi huo umetokana na maandalizi mazuri ya timu, umoja na mshikamano.

Aidha, Kamanda Kuzaga amewapongeza wachezaji, benchi la ufundi na vikundi vya hamasa kwa kila mmoja kutimiza wajibu wake hadi kupata matokeo mazuri na kusisitiza nidhamu kuelekea maandalizi ya Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii ambapo timu hiyo itashindana na timu kutoka kanda nyingine.

Mashindano hayo ya kikanda yalifunguliwa rasmi Agosti 09, 2026 yalishirikisha timu za mpira wa miguu, mpira wa pete, riadha, kuvuta kamba na michezo mingine ya jadi ikijumuisha mikoa ya Rukwa (Mwenyeji), Mbeya, Songwe na Katavi ikiwa ni maandalizi ya Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii yatakayofanyika Agosti 25, 2026 Mkoani Mbeya yakibeba kauli mbiu inayosema, Miaka 20 ya Polisi Jamii: Tushirikiane kuimarisha Amani, Usalama na Umoja wa Kitaifa.






 

Posted by MROKI On Monday, August 10, 2026 No comments

Fundi Mussa Malale akielekeza jambo kwa msimamizi wake katika mradi wa ujenzi wa Uwanjha wa Ndege wa Kimataifa wa  Msalato Mkoani Dodoma.

Na Ssgt Mawazo Mtondo - DODOMA
Jeshi la Magereza linaendelea kutoa Programu mbalimbali za Urekebishaji kwa Wafungwa ili kuwapa ujuzi utakaowasaidia kujitegemea kwa kujiajiri au kuajiriwa pindi wamalizapo vifungo magerezani.

Magereza Tanzania Habari, tumefanya mahojiano na aliyekuwa mfungwa, Ndugu Mussa Malale, ambaye ni miongoni mwa wanufaika wa programu za urekebishaji zinazotekelezwa na Jeshi la Magereza.

Akizungumza katika mahojiano hayo, Ndg. Malale amesema kipindi chote alichokuwa gerezani alipewa mafunzo mbalimbali ya ufundi stadi, ikiwemo ufundi wa viyoyozi (Air Conditioning – AC), yaliyotolewa na wakufunzi wenye uzoefu na kumjengea ujuzi uliokuwa msingi wa mafanikio yake baada ya kumaliza kifungo.

Amesema baada ya kuachiliwa huru alianza kufanya kazi ya kuendesha gari la kubeba mchanga, lakini shughuli hiyo ilisimama baada ya gari kuharibika. Baadaye, rafiki yake alimshauri kutafuta kibarua katika mradi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege Mpya wa Msalato jijini Dodoma.

Malale, amesema alifanyiwa majaribio ya vitendo na kufanikiwa kuonesha uwezo wake, hatua iliyomwezesha kupata kibarua na kushiriki katika kazi za ufungaji wa viyoyozi katika mradi huo mkubwa, ambapo ametoa shukrani kwa Jeshi la Magereza kwa kumpatia ujuzi ambao hakuwa nao kabla ya kuingia gerezani.

Ushuhuda wa aliyekuwa Mfungwa, Ndg. Mussa Malale ni ushahidi wa mafanikio ya programu za urekebishaji zinazotekelezwa na Jeshi la Magereza, zinazowapa wafungwa elimu, mafunzo ya ufundi stadi na stadi za maisha zinazowawezesha kujitegemea, kupata ajira na kurejea katika jamii wakiwa raia wema wenye mchango chanya kwa maendeleo ya Taifa.

Usikose kufuatilia kampeni ya "MAGEREZA NURU YA MABADILIKO" kupitia kipindi cha Jambo Tanzania kinachorushwa na TBC kila siku kuanzia saa 12:00 asubuhi hadi saa 3:00 asubuhi, ili upate simulizi na ushuhuda wa mafanikio ya shughuli za urekebishaji zinazotekelezwa na Jeshi la Magereza.
Posted by MROKI On Monday, August 10, 2026 No comments

August 09, 2026



Na WMA - DODOMA.
Wakala wa Vipimo (WMA) umemhakikishia Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Mhe. Selemani Mwendwa kuwa utaongeza kasi ya utendaji kazi wa masuala ya vipimo katika wilaya hiyo ili kulinda uchumi wa wakulima na wafugaji.

Hakikisho hilo limetolewa jana Agosti 8, 2026 alipotembelea banda la WMA kwenye Maonesho ya 33 ya Wakulima Nane Nane, Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Dodoma, na kupatiwa elimu ya vipimo.

Meneja wa WMA Mkoa wa Singida, Bw.  Willie Amosi alisema kuwa "WMA itashirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya kuratibu na kutoa elimu ya vipimo katika maeneo mbalimbali ya Iramba kwa  lengo la kufikia wakulima wa mahindi, alizeti na pamba pamoja na wafugaji kwenye minada na masoko.

Aidha,  alimjulisha  Mkuu wa Wilaya kuwa WMA  itajipanga ili  kuanzisha Klabu za Vipimo (Vipimo Clubs) katika shule mbalimbali  za msingi na sekondari ikiwa ni mikakati ya kufika Tanzania nzima, hususan Tanzania Bara ambao ndiyo uwanda wa WMA. 

Vilevile, Meneja Amosi alisema kuwa WMA itaendelea  kushirikiana na ofisi ya Mkuu wa Wilaya ili wananchi wa Iramba waweze kuripoti moja kwa moja matumizi ya vipimo visivyo rasmi vinavyotumika katika masoko  na kwamba hatua za kisheria zitachukuliwa kwa uharaka

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya alisema:  
“Nimefurahishwa sana. Kama Serikali ya Wilaya tuko tayari kushirikiana na WMA ili kuhakikisha vipimo sahihi vinatumika na wananchi waweze kupata stahiki ya jitihada zao. Ningetamani Iramba iwe miongoni mwa   Wilaya zinazotumia vipimo sahihi katika sekta za kilimo.uvuvi pamoja na ufugaji.”

Wataalamu wa WMA walimkabidhi pia vipeperushi vyenye elimu ya vipimo ili vimsaidie kuendelea kujenga uelewa wa elimu ya vipimo.
Posted by MROKI On Sunday, August 09, 2026 No comments



Na WMA - DODOMA.
Kiongozi mstaafu wa Wakala wa Vipimo (WMA), aliyekuwa Mkurugenzi wa Huduma Saidizi Bw. Deogratius Aloyce Maneno amesema uwekezaji wa Serikali katika masuala ya vipimo ndiyo ufunguo wa kujenga uchumi imara na soko la haki.

Alisema hayo jana Agosti 8, 2026 alipotembelea banda la WMA kwenye Maonesho ya 33 ya Wakulima (Nane Nane), yaliyofanyika kitaifa katika Viwanja vya Dkt. John Malecela, Dodoma.

Baada ya kupokelewa na wataalamu wa WMA na kupewa maelezo ya maboresho mapya ya vifaa na elimu ya vipimo, Mkurugenzi Mstaafu alisema anajivunia kuona kazi aliyoshiriki kuianzisha ikiendelea na kukua.

“Nimefurahishwa sana kuona WMA imepiga hatua kubwa. Tulipoanza tulikuwa na changamoto za vifaa na uelewa, lakini leo naona vijana wanasimama wenyewe kutoa elimu. Hii ndiyo tija ya uwekezaji,” alisema.

Kutokana na uzoefu wake wa miaka mingi WMA, kiongozi huyo alitoa ushauri katika maeneo kadhaa ili kuboresha zaidi huduma za uhakiki wa vipimo.

 Kwanza, alisema kuwa ni jambo jema kutoa elimu kwa wafanyabiashara wakubwa. Hata hivyo alisisitiza kuwa "huu ni wakati wa kushuka ngazi hadi kwa mama lishe na wauuzaji wa sokoni maana ndio wanaoumia zaidi na vipimo visivyo rasmi,” alisema.

Pia, 'Bosi Deo' kama wengi wanavyomwita alitoa ushauri kwa wafanyabiashara kukumbatia teknolojia akisema kuwa “Dunia imebadilika. Tumieni mizani ya kidijitali zaidi na mifumo ya kutoa risiti. Hii itasaidia kuwa na rekodi na kupunguza ubadhilifu katika biashara.”

Aidha, alitoa ushauri kwa watendaji wa WMA kutokuogopa kutumia sheria inayoingoza Wakala kuwabana wale wanaokiuka maelekezo na taratibu halali za kivipimo. 

“WMA ina mamlaka. Itumieni. Mkikamata na kutoa faini kwa wale wanaokiuka, wengine watafuata sheria. Soko la haki linahitaji nidhamu.”

Kwa upande wake, Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa WMA, Bi. Veronica Simba, alimshukuru kiongozi huyo mstaafu kwa kuwa sehemu ya walioweka misingi imara ya utendaji kazi WMA.

“Tunajivunia alama ambayo wewe pamoja na wastaafu wengine mliiweka. Leo tunaendeleza dira yenu ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata kipimo sahihi. Milango yetu iko wazi kwa ushauri wako wakati wote,” alisema.

Wananchi waliokuwepo bandani walifurahishwa na uwepo wa kiongozi huyo mstaafu na kusema ni mfano mzuri wa watu kurejea kutoa uzoefu kwa vizazi vipya.

Wastaafu wengine waliotembelea banda la WMA kwenye Maonesho ya NaneNane ni pamoja na Bw. Evarist Masengo aliyekuwa Meneja wa WMA ngazi ya Mkoa na Bw. Joseph Maliti aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi. Wote walikiri kufurahishwa na maendeleo ya Wakala na waliupongeza Uongozi uliopo pamoja na wafanyakazi wote kwa ujumla.
Posted by MROKI On Sunday, August 09, 2026 No comments



Na WMA - DODOMA.
Meneja wa Fedha wa Wakala wa Vipimo  (WMA), Bw. Ibrahim Mbinga, amesema usimamizi mbovu wa vipimo ndiyo adui mkubwa wa mfuko wa mfanyabiashara, mkulima na mnunuzi.

Akizungumza na wadau katika banda la WMA kwenye Maonesho ya 33 ya Nane Nane, Dodoma, Agosti 8, 2026 Meneja huyo amefafanua jinsi vipimo visivyo rasmi vinavyosababisha upotevu wa fedha usioonekana.

Mbinga ameeleza kuwa majukumu ya WMA yanalenga kuokoa wafanyabiashara, wakulima na walaji. “Watu wengi wanafikiri kupima kwa ndoo au visado ni rahisi. Lakini ukweli ni kwamba unajipiga risasi mguuni. Kila kilo, kila lita iliyopotea ni shilingi iliyotoka mfukoni mwako,” alisema.

Akidadavua kuhusu hesabu ya fedha kwenye vipimo, alisema vipimo ni sawa na mfuko wa fedha. “Gunia la mahindi kilo 100 ukiuza kwa ndoo 18 badala ya mizani, unapoteza kilo 10. Kama gunia ni shilingi 100,000, umepoteza shilingi 10,000. Ukiuza magunia 10 kwa wiki, umepoteza shilingi 100,000. Kwa mwezi ni milioni 1.2. Hiyo pesa ingekuwa wapi?” aliuliza.

Akieleza zaidi, alisema kuwa wafanyabiashara wengi hulalamika kupata hasara lakini akafafanua kuwa 'unaponunua mafuta lita 19 badala ya 20, au mpunga kilo 18 badala ya 20, unalipa pesa kamili na kupata bidhaa pungufu. Hiyo ni hasara ya moja kwa moja."

Akizungumzia mikopo kutoka Benki kwa wafanyabiashara wakulima alisema "Benki leo haziombi tu dhamana bali zinataka rekodi. Mkulima anayetumia mizani iliyohakikiwa na kuwa na risiti anaaminika zaidi. Vipimo sahihi vinakupa historia ya biashara yako ambayo benki inaitaka."

Aidha, Mbinga pia aliwaelimisha wafanyabiashara wakulima kuepuka gharama za faini ambazo husababisha hasara.

Akifafanua, alisema "kutumia vipimo visivyo rasmi ni kosa kisheria. Unapokamatwa unalipa faini na wakati mwingine bidhaa inaweza kuzuiliwa hivyo ni hasara mbili kwa wakati mmoja.

Badala yake, aliwashauri kuwekeza kiasi kidogo cha pesa kununua mizani iliyohakikiwa na WMA ili kujiepusha  na faini inayoweza kukuletea hasara.

Katika hatua nyingine, Mbinga aliwashauri wafanyabiashara wakulima 'kujenga jina' ili kupata faida stahiki. "Mteja anapojua kuwa kwako anapata haki yake, atarudi tena na tena na ataleta wengine. Hiyo inakupunguzia gharama ya kutafuta wateja. Uaminifu unalipa," alisisitiza.

Meneja huyo wa Fedha, alihitimisha kwa kusisitiza kaulimbiu ya WMA isemayo "Pima kwa Haki, Pata Faida Halali" akidadavua kuwa mfanyabiashara  akiwekeza kwenye mizani iliyohakikiwa leo, baada ya miezi miwili atashangaa tofauti yake kwenye akaunti yake ya fedha. 

Mbinga amewataka wadau pia kutumia risiti na vitabu vya mauzo vinavyotokana na vipimo sahihi ili kufuatilia kwa urahisi mapato na matumizi.

Kwa upande wao, Wadau wameipongeza WMA kwa kuleta wataalamu wa fani mbalimbali katika banda la maonesho ya Nane Nane na kusema elimu ya kifedha imewapa uelewa mpya.
Posted by MROKI On Sunday, August 09, 2026 No comments

August 08, 2026

Na Mwandishi Wetu
JAMII ya Wandondi na Wandwewe, imetoa mwito wa kitaifa na kimataifa kwa watu wote wenye nia njema kuungana katika Dua Maalum kwa ajili ya Amani, Umoja, Maridhiano, Mshikamano na Ulinzi wa Maisha ya Binadamu.

Dua hiyo ni mwito wa pamoja unaolenga kuwakutanisha watu wa imani, mila, tamaduni na mitazamo mbalimbali katika kusimama kwa pamoja Na Mwandishi Wetu amani, utu, uhai, mshikamano na heshima kwa mwanadamu, bila kujali tofauti za dini, kabila, rangi, taifa, utamaduni, itikadi au hali ya kijamii.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Chifu Felix G. L. Mfunda, kwa niaba ya jamii ya Wandondi na Wandwewe amesema dua hiyo itafanyika  Agosti 12, 2026,  ambapo Misa Maalumu ya Kikatoliki itafanyika katika Kanisa Katoliki, Kigango cha Mhangazi, Parokia ya Kitanda, Namtumbo, Ruvuma. huku akitoa  mwito wa amani na maridhiano.

Aidha, kuanzia jioni ya Agosti 13 hadi mchana wa Agosti 14, 2026, kutafanyika dua, na shughuli za jadi zitakazoambatana na ngoma na sanaa mbalimbali za asili za Wandwele na Wandondi.

Jamii mbalimbali za Mkoa wa Ruvuma, zikiwemo Makumbo, Lizombe na Makiwa, zinatarajiwa kushiriki katika shughuli hizo zinazolenga kuenzi urithi wa tamaduni, kuimarisha undugu na mshikamano, pamoja na kukuza amani kati ya jamii.

Mfululizo huo utakamilishwa Agosti 16, 2026, kwa Dua Maalumu ya Kiislamu itakayofanyika jioni kwa ajili ya kuiombea Tanzania, Afrika na dunia nzima.
Ambapo  amesema Dunia ya leo inakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo migogoro, vita, chuki, migawanyiko ya kijamii, changamoto za kiuchumi, ukosefu wa usawa na athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Katika mazingira haya, tunapaswa kutambua kwamba amani si wajibu wa Serikali pekee; ni wajibu wa kila mwanadamu.Tunatoa mwito kwa viongozi wa kitaifa na kimataifa, viongozi wa dini, viongozi wa kimila, wasomi, vijana, wanawake, mashirika ya kiraia na wananchi wote kutumia nafasi zao kujenga madaraja ya maelewano badala ya kuta za migawanyiko.

“Tunasisitiza umuhimu wa mazungumzo, kusikilizana, kusameheana, kuheshimiana na kutafuta suluhu za amani katika kila tofauti inayojitokeza.”

Aidha amesema ulinzi wa maisha ni wajibu wa pamoja akifafanua maisha ya mwanadamu ni tunu kubwa na hayapaswi kuwekwa rehani kwa sababu ya tofauti za kisiasa, kidini, kikabila, kiuchumi, kijamii au kiitikadi.

Ameongeza kwa msingi huo, wanatoa mwito wa kuheshimiwa kwa utu wa binadamu, haki ya kuishi, usalama wa raia na ulinzi wa watoto, wanawake, wazee na makundi yote yaliyo katika mazingira hatarishi.

“Tunasisitiza tofauti zetu zisigeuke kuwa sababu ya kupoteza maisha ya watu.Kila jamii ina wajibu wa kulinda maisha na kujenga mazingira ambayo kila mwanadamu anaweza kuishi kwa usalama.

Pia amesema kuhusu amani, afya na ulinzi wa mazingira ni kwamba amani ya kweli haiwezi kutenganishwa na afya ya jamii, usalama wa chakula, maji safi, mazingira salama na matumizi endelevu ya rasilimali za asili.

“Uharibifu wa mazingira, ukataji wa misitu, uharibifu wa vyanzo vya maji, upotevu wa bayoanuai na athari za mabadiliko ya tabianchi vinaweza kuongeza changamoto za kijamii na kiuchumi na kuhatarisha maisha ya watu.

“Kwa hiyo, tunatoa mwito wa kuunganisha juhudi za amani, afya, mazingira na maendeleo endelevu kwa ajili ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.

Akieleza zaidi amesema katika dua kwa Watanzania ,Afrika na Dunia amefafanua Tanzania iendelee kuwa taifa la amani, umoja, mshikamano na utulivu na kwa Afrika ipate amani na utulivu wa kudumu.

Pia migogoro na vita duniani zipungue na hatimaye kumalizika na kuongeza viongozi wapate hekima, busara, uadilifu na moyo wa kuhudumia watu.Vijana wapate fursa za elimu, ajira, ubunifu, ujasiriamali na maendeleo.

Kwa watoto walindwe dhidi ya ukatili, unyanyasaji na mazingira yanayohatarisha maisha yao. Wanawake, wazee na makundi yaliyo katika mazingira magumu walindwe na kuheshimiwa.Wagonjwa na wote wanaokabiliwa na changamoto mbalimbali wapate faraja, matumaini na huduma stahiki na mazingira.

Kuhusu ujumbe kwa Watanzania amesema wanawakumbusha Umoja wetu ni nguvu yetu, amani yetu ni utajiri wetu, na maisha ya kila Mtanzania ni sehemu ya thamani ya Taifa letu.

“Tunapaswa kukataa chuki, uchochezi, ubaguzi, vurugu na lugha zinazogawa jamii. Badala yake, tujenge utamaduni wa kusikilizana, kuheshimiana, kusameheana, kusaidiana na kutatua tofauti zetu kwa njia za amani.

“Tanzania yenye amani na mshikamano ni msingi muhimu wa maendeleo ya watu wake na mchango mkubwa kwa amani ya Afrika na dunia.”

 


Posted by MROKI On Saturday, August 08, 2026 No comments




DODOMA
Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Aziza Swedi, amesema Maonesho ya Nanenane ni jukwaa muhimu la kuwaelimisha wananchi kuhusu Sekta ya Madini, kusikiliza maoni yao na kupata mrejesho unaosaidia kuboresha huduma na kuongeza thamani ya sekta hiyo.

Mhandisi Swedi amesema hayo baada ya kutembelea mabanda ya Taasisi za Wizara ya Madini katika kilele cha Maonesho ya Nanenane jijini Dodoma, akisisitiza umuhimu wa kuwashirikisha wananchi katika maendeleo ya sekta hiyo.

Amesema maonesho hayo yanawezesha Tume ya Madini kuwafikia wananchi moja kwa moja, kusikiliza changamoto zinazowakabili na kupata maoni ambayo yanaweza kutumika kuboresha utendaji na utoaji wa huduma.

“Kila swali na hoja inayotolewa na mwananchi ni muhimu, kwa sababu inatusaidia kutambua maeneo yanayohitaji maboresho na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma,” amesema Mhandisi Swedi.

Aidha, amesema ushiriki wa wananchi katika Maonesho ya Nanenane unaimarisha ushirikiano kati ya Serikali, taasisi zinazohusika na Sekta ya Madini na jamii, sambamba na kuwawezesha wananchi kupata uelewa kuhusu huduma, fursa na shughuli mbalimbali zinazopatikana katika sekta hiyo.

Katika ziara hiyo, Mhandisi Swedi ametembelea mabanda ya Tume ya Madini, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) na Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), ambako amepata fursa ya kujionea huduma na shughuli zinazotekelezwa na taasisi hizo.

Amewahimiza wananchi kutumia kikamilifu fursa inayotolewa na Maonesho ya Nanenane kwa kujifunza, kuuliza maswali na kutoa maoni kuhusu Sekta ya Madini.

Pia, amewakaribisha wananchi kufika katika ofisi za Tume ya Madini na taasisi nyingine zinazohusika na sekta hiyo ili kupata ufafanuzi na huduma zaidi kuhusu masuala ya madini.
Posted by MROKI On Saturday, August 08, 2026 No comments
Na WMA - DODOMA
WAKALA wa Vipimo  (WMA) umewataka wafanyabiashara na wananchi kuacha mara moja matumizi ya vipimo visivyo rasmi, ikiwemo ndoo, mafungu, visado na makopo, katika uuzaji wa mazao ya kilimo na mifugo na badala yake kutumia mizani iliyohakikiwa kwa mujibu wa sheria.

Wito huo umetolewa na Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihula, leo Agosti 8, 2026 wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 33 ya Kitaifa ya Siku ya Wakulima Nane Nane, yaliyokuwa yakifanyika katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, jijini Dodoma.

Kihula amesema matumizi ya vipimo visivyo rasmi yanaweza kusababisha kutokuwepo kwa usawa katika biashara na kuwaathiri wananchi kwa kuwafanya wasipate thamani halisi ya bidhaa wanazonunua au kuuza.

Amesema WMA imeendelea kutoa elimu kwa wananchi, wakulima, wafugaji na wafanyabiashara kuhusu matakwa ya Sheria ya Vipimo, Sura ya 340, ikiwemo namna ya kutambua vipimo vilivyohakikiwa na uwekaji wa alama sahihi kwenye bidhaa zilizofungashwa.

“Ili kuwa na soko lenye haki na kuongeza tija kuelekea Dira ya 2050, hakuna soko linaloweza kuwa la haki bila matumizi ya vipimo vilivyohakikiwa kwa mujibu wa sheria,” amesema Kihula.


Akizungumzia sekta ya kilimo, Kihula amewataka wakulima kuzingatia matumizi ya vipimo sahihi katika hatua zote za uzalishaji na biashara, kuanzia uandaaji wa mashamba hadi uvunaji, uhifadhi na uuzaji wa mazao.

Amesema matumizi ya vipimo sahihi katika kujua ukubwa wa eneo la shamba yanaweza kusaidia wakulima kupanga uzalishaji kwa usahihi badala ya kutegemea makadirio.

Aidha, amewataka kuhakikisha mazao yanapimwa kwa mizani iliyohakikiwa wakati wa kuuza ili mkulima aweze kupata thamani halisi ya bidhaa zake.

Kwa upande wa wafugaji, Kihula amewataka kuacha kuuza mifugo kwa kutegemea makadirio ya macho na badala yake kutumia mizani sahihi katika kubaini uzito wa mifugo kama vile ng'ombe, mbuzi, kondoo na kuku.

Amesema utaratibu huo unapaswa pia kuzingatiwa katika uuzaji wa bidhaa zinazotokana na mifugo, ikiwemo nyama na maziwa, ili kuhakikisha mnunuzi na muuzaji wanapata thamani inayolingana na kiasi cha bidhaa kinachouzwa.


Wakati huohuo, Kihula amewapongeza wavuvi kwa kuendelea kuonesha mfano mzuri katika matumizi ya vipimo na kuwataka kuendeleza utaratibu huo.

Amesema matumizi ya vipimo sahihi katika shughuli za uvuvi ni muhimu katika kuhakikisha biashara inafanyika kwa uwazi na kwa kuzingatia thamani halisi ya bidhaa.


Kihula amewataka wananchi kuwa mstari wa mbele kukataa kuhudumiwa kwa vipimo visivyo rasmi wanaponunua bidhaa kama vile viazi, bamia, vitunguu na nyanya, badala yake kusisitiza bidhaa hizo zipimwe kwa mizani iliyohakikiwa.

“Wananchi wasikubali kununua bidhaa kwa mafungu, visado au vipimo vingine visivyo rasmi. Wanapaswa kusisitiza kupimiwa kwa mizani iliyohakikiwa ili kuhakikisha wanapata kiasi sahihi cha bidhaa wanacholipia,” amesema.

Aidha, amewataka wananchi kutoa taarifa kwa WMA wanapobaini matumizi ya vipimo visivyo halali katika maeneo yao ili hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa.

Amesema ushirikiano wa wananchi, wafanyabiashara na taasisi za Serikali ni muhimu katika kujenga soko lenye haki, uwazi na linalozingatia matumizi ya vipimo sahihi kwa mujibu wa sheria.

Amesisitiza kuwa matumizi ya vipimo vilivyohakikiwa si suala la wafanyabiashara pekee, bali ni jambo linalomhusu kila mwananchi katika kuhakikisha anapata thamani halisi ya fedha anayolipa au mapato anayopata kutokana na bidhaa anazouza.



Posted by MROKI On Saturday, August 08, 2026 No comments




Na Neema Chalila Mbuja, DodomaRAIS  wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Agosti 8, 2026 amefunga rasmi Maonesho ya NANE NANE  yaliyokuwa yakifanyika kwenye Viwanja vya Dkt John Malecela  Nzuguni Dodoma na kuwapongeza Wizara ya Kilimo , Mifugo na Uvuvi kwa kazi nzuri liliyofanya kuwaunganisha wadau wa kilimo kwenye maonesho hayo.

Katika Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii maelfu ya wananchi wamefurika kwenye bustani ya wanyamapori hai ili kujionea wanyama mbalimbali.

Sambamba na hilo viongozi mbalimbali wa Wizara ya Maliasili na Utalii wametembelea banda la Wizara hiyo kwenye Viwanja vya NANE NANE kwa ajili ya kujionea shughuli mbalimbali zinazofanyika na taasisi na wadau wa   Malikale, Misitu na Nyuki, Utalii na Wanyamapori.

Wakiwa kwenye Maonesho hayo walipata fursa ya kuzungumza na wananchi na wadau na kueleza mustakabali wa sekta ya utalii sambamba na mikakati iliyojiwekea kwa ajili ya kutangaza sekta ya utalii hususani katika kipindi hiki cha kuelekea Michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027.






Posted by MROKI On Saturday, August 08, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo