Nafasi Ya Matangazo

July 24, 2026








Na. Mwandishi wetu - Dar es Salaam
Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu na Kusimamia Fedha za Mfuko wa Dunia nchini Tanzania (Tanzania National Coordinating Mechanism – TNCM), imeidhinisha rasmi Ombi la Tanzania la Ufadhili wa Mzunguko wa Nane wa Mfuko wa Dunia (Global Fund Grant Cycle 8 – GC8) kiasi cha dola za Marekani milioni 538.6 kwa ajili ya kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI, Kifua Kikuu (TB) na Malaria, pamoja na kuimarisha Mifumo Thabiti na Endelevu ya Afya (RSSH), katika kipindi cha utekelezaji kuanzia Januari 2027 hadi Desemba 2029.

Uidhinishaji huo umefanyika jijini Dar es Salaam katika kikao maalum cha TNCM kilichoongozwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa TNCM.

Dkt. Yonazi amesema kuwa, mchakato wa maandalizi ya Ombi la GC8 ulianza rasmi tarehe 13 Machi, 2026 na umeendelea kwa zaidi ya miezi minne, ukihusisha mashauriano ya kina, majadiliano ya kitaifa, upangaji wa vipaumbele, uandishi wa andiko, mapitio ya kitaalamu na uhakiki wa nyaraka za maombi. 

Aidha, alifafanua kuwa, mchakato huu umejengwa katika msingi wa ushirikishwaji mpana wa wadau, uwazi, uwajibikaji na umiliki wa kitaifa ambapo zaidi ya wadau 270 walishiriki kwa uwakilishi wa makundi mbalimbali, yakiwemo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara, Idara na Taasisi zake; Washirika wa Maendeleo, Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mashirika ya Kimataifa, Asasi za Kiraia, Sekta Binafsi, Mashirika ya Dini, watu wanaoishi na VVU, jamii zilizo katika hatari kubwa ya maambukizi na zilizoathiriwa na magonjwa hayo; pamoja na wataalamu wa sekta ya afya.

Dkt. Yonazi ameeleza kuwa uwekezaji wa Mfuko wa Dunia umeendelea kutoa mchango mkubwa katika juhudi za Serikali za kuboresha afya na ustawi wa Watanzania, na kusema utekelezaji wa GC8 utatoa fursa kwa Nchi kuendela kuzuia maambukizi mapya ya VVU, kuongeza upatikanaji wa dawa za kufubaza makali ya VVU (ARV), kuimarisha kinga, uchunguzi na matibabu ya Malaria, pamoja na kuboresha ugunduzi wa mapema na matibabu ya Kifua Kikuu.

“Kuidhinishwa kwa Ombi hili la Ufadhili ni matokeo ya kazi kubwa na ushirikiano wa wadau wetu ambao wamewekeza muda, utaalamu na rasilimali kuhakikisha kuwa vipaumbele vilivyoainishwa vinazingatia mahitaji ya nchi pamoja na sauti za jamii na makundi yanayoathiriwa na magonjwa hayo”.Alisema Dkt. Yonazi.

Aliongezea kuwa,hatua hiyo ni mafanikio muhimu yanayoonesha dhamira ya Tanzania ya kuendeleza mapambano dhidi ya magonjwa hayo matatu, sambamba na kujenga mfumo wa afya ulio imara, jumuishi na endelevu.

Dkt. Yonazi ameshukuru Sekretarieti ya Mfuko wa Dunia iliyopo Geneva (Global Fund Country Team), wajumbe wa TNCM pamoja na wadau wote walioshiriki katika maandalizi na ukamilishaji wa maombi hayo, amepongeza jitihada zao akisema zimekuwa na mchango muhimu kuwezesha kufikia hatua hii.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TNCM, Bw. Kent Pius, ametoa shukrani maalum kwa Mwenyekiti wa TNCM, Mfuko wa Dunia, wajumbe na wadau wote kwa ushirikiano na uwajibikaji mkubwa katika kuhakikisha kuwa zoezi hili limefanyika kwa ufanisi na ubora uliokusudiwa na kusema kuwa, hatua hii ni matokeo ya dhamira ya dhati na juhudi za pamoja. 

“TNCM itaendelea kuratibu ushirikiano kati ya Serikali, jamii, Asasi za Kiraia, Washirika wa Maendeleo, Sekta Binafsi na wadau wa kimataifa katika kuhakikisha uwekezaji wa Mfuko wa Dunia unachangia katika kufikia malengo ya Kitaifa na Kimataifa ya kutokomeza UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria kama vitisho vya afya ya jamii,” alisema Kent.
Posted by MROKI On Friday, July 24, 2026 No comments







Na Dk. Reubeni Lumbagala
Maji safi na salama ni hitaji muhimu la wananchi waishio mijini na vijijini. Serikali inalo jukumu la kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma hiyo ili kuwezesha kufanyika kwa shughuli za kijamii na kiuchumi kwa ufanisi na ubora.

Kutokana na uhitaji mkubwa wa raslimalifedha za kugharamia miradi ya maji, serikali inasisitiza ushirikiano baina ya sekta ya umma na binafsi (PPP).

Hilo linafanyika kwa nia njema ya kuharakisha usambazaji wa maji kwa wananchi. Watu binafsi, taasisi za dini, mashirika yasiyo ya kiserikali na wadau wa maendeleo, wanakaribishwa kuongeza nguvu ya usambazaji maji kwa wananchi. 

Aidha, wadau hao wanaweza kusaidia uchimbaji wa visima, kuanzisha miradi midogo na mikubwa ya maji, ili wananchi waweze kupata huduma hiyo kwa kuzingatia ukweli kuwa "Maji ni Uhai".

Kimsingi, serikali imekuwa ikipata ushirikiano mzuri kutoka sekta binafsi katika kugharamia miradi ya maji. Katika malengo na mikakati ya Wizara ya Maji katika bajeti ya mwaka 2026/2027, ni pamoja na kuhimiza ushirikiano baina ya sekta ya umma na binafsi katika kugharamia miradi ya maji.

Hakika, Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Tanga (Tanga Uwasa) imekuwa mfano mzuri wa kuigwa kwa kuishirikisha sekta binafsi kikamilifu katika kuongeza nguvu ya usambazaji maji kwa wananchi.

Ni hivi: Kupitia ubunifu wa kutafuta fedha mbadala (alternative financing), Tanga Uwasa kupitia Hatifungani ya Kijani, imefanikiwa kukusanya shilingi bilioni 53.12 kutoka kwa wananchi na wadau mbalimbali.

Fedha hizo zinatumika kuongeza mtandao wa usambazaji maji kwa wananchi waishio Jiji la Tanga na wilaya za Mkinga, Muheza na Pangani, huku wakitarajia kurejesha fedha hizo pamoja na gawio kwa wawekezaji wake.

Ubunifu huu unatokana na changamoto za kibajeti, ambapo kusubiri fedha kutoka serikali kuu pekee ni kuchelewesha maendeleo kwa wananchi kwani maji ni kiungo muhimu wa kuwezesha shughuli nyingi za kijamii na kiuchumi.

Hivyo basi, ipo haja ya mamlaka nyingine za maji, kuiga ubunifu huu wa Tanga Uwasa wa kutafuta fedha mbadala za kuwezesha usambazaji wa maji safi, salama na yenye kutosheleza kwa wananchi.

Mei 16, 2024, Tanga Uwasa iliorodheshwa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) kupitia ubunifu wake wa hatifungani ya miundombinu ya maji na utunzaji wa mazingira.

Katika hafla hiyo, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso alisema "Upatikanaji wa fedha kupitia Hatifungani kama hii ya Tanga, inasaidia juhudi za serikali na kuharakisha utoaji wa huduma bora ya maji kwa wananchi. Natoa rai kwa mamlaka nyingine za maji, kijifunza kupitia hatifungani ya Tanga Uwasa na kuiga mfano huu".

Hivi karibuni, Waziri wa Maji, Nishati na Madini wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Nadir Abdullatif, alitembelea mradi mkubwa wa maji unaofadhiliwa kwa fedha za Hatifungani ya Kijani ya Tanga Uwasa, kujifunza namna mamlaka hiyo ilivyofanikiwa kutumia fedha mbadala kugharamia miradi ya maji.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Tanga Uwasa, Mhandisi Geoffrey Hilly, amesema mafanikio ya utekelezaji wa miradi ya maji yamechangiwa na ushiriki wa sekta binafsi, hivyo serikali itaendelea kushirikiana nao bega kwa bega ili kufanikisha dhamira ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ya kumtua ndoo mama kichwani na kuongeza kasi ya maendeleo kupitia sekta ya maji.

Maoni: 0620 800 462.
Posted by MROKI On Friday, July 24, 2026 No comments






Na Mwandishi Wetu, Dar
Mkandarasi anayetekeleza mradi wa Maduka ya Biashara ya Maria Nyerere (Maria Nyerere Shopping Mall) ulio chini Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT), amehimizwa kuongeza kasi ya ujenzi ili mradi huo ukamilike kwa wakati.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa UWT Taifa, Mary Chatanda, Julai 22, 2026, Jijini Dar es Salaam, katika ziara ya Wajumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la UWT Taifa, kukagua uhai wa Chama na miradi ya Jumuiya hiyo.

Chatanda amesema, ipo haja ya mkandarasi huyo kuongeza kasi ya ujenzi, huku akimshauri kuongeza wakandarasi wengine ili kumsaidia baadhi ya kazi na kuongeza kasi ya ujenzi wa mradi huo.

"Mradi unakwenda vizuri, isipokuwa kwa mwenendo unavyokwenda na kwa muda tuliokubaliana huenda asikamilishe kwa wakati. Mkandarasi tunachomuhitaji aukamilishe mradi kwa mujibu wa tulivyokubaliana na kama kuna maeneo yeye hana uwezo wa kufanya, akabidhi kwa wakandarasi wengine (sub contractors) ili kazi ikamilike kwa wakati," amesema Chatanda.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti UWT Taifa, Zainabu Shomari, amesema mradi huo ni utekelezaji wa maagizo ya Chama wa kuzitaka Jumuiya zake kuwa na vitega uchumi.

"Chama kimeelekeza Jumuiya zake kujitegemea kiuchumi, kwahiyo, mradi huu ni utekelezaji wa maagizo na Chama na kwa hakika UWT tutafanikiwa kujitegemea," amesema Shomari.

Ikumbukwe kuwa, mradi wa Maria Nyerere Shopping Mall unatekelezwa eneo la Gerezani Jijini Dar es Salaam, ambapo unategemewa kuongeza mapato ili Jumuiya  hiyo iwe na uwezo wa kuendesha shughuli zake bila kutegemea uwezeshwaji kutoka Chama ngazi ya Taifa.

Pamoja na mradi huo, Kamati hiyo, ilipata fursa ya kukagua eneo lake lenye ukubwa wa hekta 8.2, lililopo mtaa wa Zogo, kata ya Zingiziwa, wilayani Ilala, ambapo linategemewa kuongeza uwekezaji wa Jumuiya hiyo.
Posted by MROKI On Friday, July 24, 2026 No comments

July 22, 2026

Na.Mwandishi wetu - Dar es Salaam
Kamati ya Kitaifa ya Wataalamu ya Usimamizi wa Maafa imeidhinisha Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El Niño na kuzielekeza Wizara, Idara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri kuongeza kasi ya maandalizi ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na mvua za El Niño zinazotabiriwa kudumu hadi mwisho wa mwaka 2026.

Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, ambaye pia ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, ameelekeza kila sekta kutenga rasilimali zitakazowezesha hatua za kuzuia, kujiandaa, kukabili na kurejesha hali katika eneo lake na pia kuandaa mipango ya dharura ya manunuzi. Pia amesisitiza umuhimu wa kutambua mapema maeneo hatarishi, kufanya tathmini za vihatarishi na kuwahamasisha wananchi wanaoishi katika maeneo hayo kuhamia maeneo salama.

Aidha, Dkt. Yonazi ameelekeza wananchi kupewa elimu kuhusu namna ya kupunguza madhara ya mvua hizo kwa kuweka akiba ya chakula, kulima mazao yanayostahimili mvua nyingi na kutumia fursa zitokanazo na mvua katika kilimo, uvunaji wa maji, ufugaji na uvuvi. Vilevile, amezitaka taasisi husika kuandaa mipango ya kuzuia milipuko ya magonjwa kwa binadamu, mifugo na mimea.

Kamati hiyo pia imeagiza ukaguzi na uboreshaji wa miundombinu muhimu ikiwemo barabara, maji na umeme, kuimarisha usimamizi wa mazingira, kuhakikisha vifaa vya uokoaji, huduma za dharura na mifumo ya mawasiliano vinakuwa tayari wakati wote, pamoja na kuhuisha mipango ya utekelezaji katika maeneo hatarishi. 

Aidha, Wizara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri zimeelekezwa kufuatilia kwa karibu utabiri na maelekezo ya kitaalamu kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ili hatua zote za maandalizi na kukabiliana na athari za El Niño zichukuliwe kwa wakati.











Posted by MROKI On Wednesday, July 22, 2026 No comments






Na Mwandishi Wetu, Kisarawe
Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), imefaya ziara ya mafunzo katika Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Julai 21, 2026, wilayani Kisarawe mkoani Pwani.

Ujumbe huo uliongozwa na Mwenyekiti wa UWT Taifa, Mary Chatanda. Katika ziara hiyo, Wajumbe wa Kamati hiyo, walitembelea kiwanda cha Rafiki Briquettes, kinachochakata makaa ya mawe kuwa nishati safi ya kupikia ambayo ni rafiki wa afya na utunzaji mazingira.

Katika ziara hiyo, Chatanda amesema, wanawake wana mchango mkubwa katika kufanikisha kampeni ya nishati safi ya kupikia kutokana na ukweli kuwa kazi hiyo inafanywa kwa kiwango kikubwa na wanawake.

"Tunamuunga mkono Rais wetu, Dk. Samia Suluhu Hassan, katika kampeni ya kuhimiza matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kutunza afya na mazingira. Sisi UWT tunahimiza jamii itumie nishati safi," amesema Chatanda.

Aidha, amesema UWT wapo tayari kuwa mabalozi na kushirikiana na STAMICO katika kutoa elimu kwa wanawake na jamii kwa ujumla ili kuongeza idadi ya watumiaji wa nishati safi nchini.

"UWT tuna vikao na mikutano mingi inayotukutanisha na wanawake na wananchi, hivyo niwaombe wenzetu wa STAMICO watupe wataalamu wa kuja kutoa elimu katika mikusanyiko yetu, ili elimu hiyo iwafikie wananchi wengi zaidi," ameongeza.

Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati hiyo na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Subira Mgallu, ameipongeza STAMICO kwa kusimamia kikamilifu sera ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ambayo ni muhimu katika dunia ya sasa ya maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Petro Magoti, aliwashukuru Wajumbe wa Baraza hilo, kufanya ziara ya mafunzo kwani agenda ya nishati safi ni ya kitaifa na kimataifa, hivyo wakawe mabalozi wa kuelimisha wengine watumie nishati hiyo.
Posted by MROKI On Wednesday, July 22, 2026 No comments

July 20, 2026








Chato, Geita
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, ameanza ziara rasmi ya kikazi mkoani Geita kwa lengo la kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuhamasisha shughuli za kiuchumi na kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Serikali yanayolenga kuboresha maisha ya wananchi.

Mhe. Mavunde, ambaye pia ni Mlezi wa shughuli za maendeleo mkoani Geita, anatarajiwa kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya kimkakati inayotekelezwa katika halmashauri na wilaya za mkoa huo, sambamba na kuzungumza na wananchi kuhusu fursa za maendeleo na mchango wa sekta ya madini katika kukuza uchumi wa Taifa.

Katika siku ya kwanza ya ziara hiyo, Waziri Mavunde amekagua mradi mkubwa wa maji wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 40, unaotarajiwa kunufaisha zaidi ya wananchi 185,000 kwa kuwapatia huduma ya maji safi na salama. Ameeleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza katika miradi ya maji ili kuboresha afya, ustawi wa jamii na kuongeza tija katika shughuli za uzalishaji.

Akizungumza baada ya kukagua mradi huo, Mhe. Mavunde amesema upatikanaji wa maji ni msingi muhimu wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi, huku akiwataka wakandarasi kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyokidhi thamani ya fedha za umma.

Katika kuendelea kuhamasisha maendeleo ya sekta ya madini, Waziri Mavunde pia ametembelea mradi wa vijana wa ujenzi wa kiwanda cha kuchenjua madini, akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uchimbaji na uongezaji thamani wa madini.

Amesema uwekezaji katika viwanda vya uchakataji na uchenjuaji wa madini utaongeza thamani ya rasilimali za madini nchini, kufungua ajira kwa vijana na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Aidha, Waziri Mavunde ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa Daraja la Rwantaba, mradi unaotarajiwa kuboresha miundombinu ya usafiri na usafirishaji, kurahisisha shughuli za biashara, kuunganisha maeneo ya uzalishaji na masoko pamoja na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa Mkoa wa Geita.

Mkuu wa Mkoa wa Geita Mh. Martin Shigela amesema utekelezaji wa shughuli za maendeleo mkoani Geita unajibu changamoto za wa wananchi kivitendo na kwamba serikali ya mkoa imejipanga kuhakikisha miradi yote ya maendeleo inakamilika kwa wakati.
Posted by MROKI On Monday, July 20, 2026 No comments

July 18, 2026



📍Bagamoyo - PWANI
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani inaendelea kutekeleza majukumu yake ya kusimamia sheria za Forodha kwa lengo la kuhakikisha kunakuwepo ushindani wa haki katika biashara na kulinda mapato ya Serikali.

Katika operesheni iliyofanyika tarehe 16 Julai 2026 wilayani Bagamoyo, TRA imekamata Jahazi likiwa na katoni 50 za sabuni aina ya Malaika Brown Soap, zilizoingizwa nchini kinyume na taratibu za Forodha. Hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa sheria unaolenga kuimarisha biashara halali.

TRA Mkoa wa Pwani inaendelea kuwahimiza wafanyabiashara kuzingatia sheria na taratibu za Forodha, huku ikiahidi kuendelea kutoa huduma kwa weledi, kulinda ushindani wa haki na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Posted by MROKI On Saturday, July 18, 2026 No comments

July 16, 2026

Katibu Mkuu Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Dkt. Asha-Rose Migiro, amefanya mazungumzo na Balozi wa Norway nchini Tanzania, Mhe. Tone Tinnes, katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba, Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Julai 15,2026, viongozi hao walijadiliana kuhusu uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania na Ufalme wa Norway, pamoja na maeneo ya ushirikiano yanayohusu maendeleo ya kidemokrasia, utawala bora, ujenzi wa taasisi na maendeleo endelevu.





Posted by MROKI On Thursday, July 16, 2026 No comments

July 15, 2026





Dodoma
Kufuatia utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa maabara ya kisasa ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), hatua hiyo inakwenda kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha utoaji wa huduma za maabara ya madini kusini mwa Jangwa la Sahara.

Hayo yamesemwa leo tarehe 15 Julai, 2026 na Waziri wa Madini, *Mh.Anthony Mavunde (Mb)* alipotembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa maabara ya GST uliopo Kizota, Jijini Dodoma.

"Tunamshukuru Rais wetu Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kukubali kutoa fedha za utekelezaji wa mradi huu wa kisasa, unaokwenda kuifanya Nchi yetu kuwa kinara na mahiri katika utoaji wa huduma za maabara za madini"

"Mradi huu pia unakwenda kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha utoaji wa huduma za maabara kwa Nchi za Afrika ya Mashariki na Kati, kutokana na ubora wa huduma hizo kuwa za kimataifa" alieleza Waziri Mavunde.

Aidha, Waziri Mavunde alibainisha kuwa kwa muda mrefu wachimbaji wadogo wamekuwa wakipata changamoto ya upimaji wa sampuli zao kwenye maabara, hali iliyopelekea kushindwa kufanya shughuli zao kiufanisi.

Mavunde alisisitiza kuwa ujio wa maabara hiyo ya kisasa unakwenda kuwa mwarobaini wa changamoto za wachimbaji ikiwa ni pamoja na kuhudumia wachimbaji wengi zaidi kwa ubora wa kimataifa.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Madini Tanzania, *Mhandisi Ally Samaje* alieleza kuwa ujenzi wa mradi huo wa maabara unagharimu shilingi bilioni 14.3 na upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji ambapo unataraji kukamilika ifikapo Mwezi Septemba, 2027. 

Aidha, aliongeza kuwa maabara hiyo ikikamilika itakuwa ni ya kisasa na inakwenda kuhudumia wateja wengi wa ndani na nje ya Nchi.
Posted by MROKI On Wednesday, July 15, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo