Nafasi Ya Matangazo

July 20, 2026








Chato, Geita
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, ameanza ziara rasmi ya kikazi mkoani Geita kwa lengo la kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuhamasisha shughuli za kiuchumi na kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Serikali yanayolenga kuboresha maisha ya wananchi.

Mhe. Mavunde, ambaye pia ni Mlezi wa shughuli za maendeleo mkoani Geita, anatarajiwa kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya kimkakati inayotekelezwa katika halmashauri na wilaya za mkoa huo, sambamba na kuzungumza na wananchi kuhusu fursa za maendeleo na mchango wa sekta ya madini katika kukuza uchumi wa Taifa.

Katika siku ya kwanza ya ziara hiyo, Waziri Mavunde amekagua mradi mkubwa wa maji wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 40, unaotarajiwa kunufaisha zaidi ya wananchi 185,000 kwa kuwapatia huduma ya maji safi na salama. Ameeleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza katika miradi ya maji ili kuboresha afya, ustawi wa jamii na kuongeza tija katika shughuli za uzalishaji.

Akizungumza baada ya kukagua mradi huo, Mhe. Mavunde amesema upatikanaji wa maji ni msingi muhimu wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi, huku akiwataka wakandarasi kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyokidhi thamani ya fedha za umma.

Katika kuendelea kuhamasisha maendeleo ya sekta ya madini, Waziri Mavunde pia ametembelea mradi wa vijana wa ujenzi wa kiwanda cha kuchenjua madini, akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uchimbaji na uongezaji thamani wa madini.

Amesema uwekezaji katika viwanda vya uchakataji na uchenjuaji wa madini utaongeza thamani ya rasilimali za madini nchini, kufungua ajira kwa vijana na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Aidha, Waziri Mavunde ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa Daraja la Rwantaba, mradi unaotarajiwa kuboresha miundombinu ya usafiri na usafirishaji, kurahisisha shughuli za biashara, kuunganisha maeneo ya uzalishaji na masoko pamoja na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa Mkoa wa Geita.

Mkuu wa Mkoa wa Geita Mh. Martin Shigela amesema utekelezaji wa shughuli za maendeleo mkoani Geita unajibu changamoto za wa wananchi kivitendo na kwamba serikali ya mkoa imejipanga kuhakikisha miradi yote ya maendeleo inakamilika kwa wakati.
Posted by MROKI On Monday, July 20, 2026 No comments

July 18, 2026



📍Bagamoyo - PWANI
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani inaendelea kutekeleza majukumu yake ya kusimamia sheria za Forodha kwa lengo la kuhakikisha kunakuwepo ushindani wa haki katika biashara na kulinda mapato ya Serikali.

Katika operesheni iliyofanyika tarehe 16 Julai 2026 wilayani Bagamoyo, TRA imekamata Jahazi likiwa na katoni 50 za sabuni aina ya Malaika Brown Soap, zilizoingizwa nchini kinyume na taratibu za Forodha. Hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa sheria unaolenga kuimarisha biashara halali.

TRA Mkoa wa Pwani inaendelea kuwahimiza wafanyabiashara kuzingatia sheria na taratibu za Forodha, huku ikiahidi kuendelea kutoa huduma kwa weledi, kulinda ushindani wa haki na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Posted by MROKI On Saturday, July 18, 2026 No comments

July 16, 2026

Katibu Mkuu Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Dkt. Asha-Rose Migiro, amefanya mazungumzo na Balozi wa Norway nchini Tanzania, Mhe. Tone Tinnes, katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba, Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Julai 15,2026, viongozi hao walijadiliana kuhusu uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania na Ufalme wa Norway, pamoja na maeneo ya ushirikiano yanayohusu maendeleo ya kidemokrasia, utawala bora, ujenzi wa taasisi na maendeleo endelevu.





Posted by MROKI On Thursday, July 16, 2026 No comments

July 15, 2026





Dodoma
Kufuatia utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa maabara ya kisasa ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), hatua hiyo inakwenda kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha utoaji wa huduma za maabara ya madini kusini mwa Jangwa la Sahara.

Hayo yamesemwa leo tarehe 15 Julai, 2026 na Waziri wa Madini, *Mh.Anthony Mavunde (Mb)* alipotembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa maabara ya GST uliopo Kizota, Jijini Dodoma.

"Tunamshukuru Rais wetu Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kukubali kutoa fedha za utekelezaji wa mradi huu wa kisasa, unaokwenda kuifanya Nchi yetu kuwa kinara na mahiri katika utoaji wa huduma za maabara za madini"

"Mradi huu pia unakwenda kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha utoaji wa huduma za maabara kwa Nchi za Afrika ya Mashariki na Kati, kutokana na ubora wa huduma hizo kuwa za kimataifa" alieleza Waziri Mavunde.

Aidha, Waziri Mavunde alibainisha kuwa kwa muda mrefu wachimbaji wadogo wamekuwa wakipata changamoto ya upimaji wa sampuli zao kwenye maabara, hali iliyopelekea kushindwa kufanya shughuli zao kiufanisi.

Mavunde alisisitiza kuwa ujio wa maabara hiyo ya kisasa unakwenda kuwa mwarobaini wa changamoto za wachimbaji ikiwa ni pamoja na kuhudumia wachimbaji wengi zaidi kwa ubora wa kimataifa.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Madini Tanzania, *Mhandisi Ally Samaje* alieleza kuwa ujenzi wa mradi huo wa maabara unagharimu shilingi bilioni 14.3 na upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji ambapo unataraji kukamilika ifikapo Mwezi Septemba, 2027. 

Aidha, aliongeza kuwa maabara hiyo ikikamilika itakuwa ni ya kisasa na inakwenda kuhudumia wateja wengi wa ndani na nje ya Nchi.
Posted by MROKI On Wednesday, July 15, 2026 No comments
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekuletea mashindano ya Wazo Bunifu yanayolenga kupata suluhisho za kibunifu zitakazochangia kuboresha mfumo wa kodi nchini. Hii ni fursa yako ya kuwasilisha wazo lenye tija na kushindania zawadi ya hadi Shilingi Milioni 50.

Mawazo yatakayowasilishwa yanapaswa kulenga eneo moja au zaidi kati ya yafuatayo ; kupanua wigo wa kodi, kurahisisha ukadiriaji na ulipaji wa kodi kwa biashara ndogo ndogo, kuimarisha huduma za kodi za kidijitali, kupunguza gharama za ukusanyaji wa mapato, kutumia teknolojia za kisasa kama AI, Big Data na Blockchain katika usimamizi wa kodi, pamoja na kuboresha utatuzi wa migogoro ya kodi ili kuwa wa haraka, wazi na wenye kuaminika zaidi.

Kutuma Wazo lako ingia tovuti ya TRA, Bonyeza kitufe cha innovation portal fuata hatua zinazofuata, Mwisho wa kutuma wazo lako bunifu ni julai 31, 2026.  

@tratanzania #WazobunifuTRA2026 #Buniwazoushinde
Posted by MROKI On Wednesday, July 15, 2026 No comments

July 13, 2026

Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Thabit Ramadhani akumueleza Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Mhe. Fatma Almasi Nyangasa namna moyo unavyofanya kazi alipotembelea banda la Taasisi hiyo lililopo katika maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Idd Kimario akimpima Shinikizo la damu Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Mhe. Fatma Almasi Nyangasa alipotembelea banda la Taasisi hiyo wakati wa maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Mhe. Fatma Almasi Nyangasa akitazama mfano wa saani ya makundi ya chakula alipotembelea banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) lililopo katika maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Mhe. Fatma Almasi Nyangasa akipokea zawadi kutoka kwa daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mohamed Aloyce alipotembelea banda la Taasisi hiyo wakati wa maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Mhe. Fatma Almasi Nyangasa akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) mara baada ya kutembelea banda la Taasisi hiyo lililopo katika maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa jijini.
*************
Mwandishi Maalumu – Dar es Salaam
Wananchi wametakiwa kutumia fursa ya Maonesh ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) kutembelea banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ili kupima afya zao na kutambua mapema vihatarishi vya magonjwa ya moyo na magonjwa mengine yasiyoambukiza kupitia kampeni ya Jua Namba Zako.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Mhe. Fatma Almasi Nyangasa alipotembelea banda la  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) lililopo katika maonesho hayo na kuweza kujua namba zake.

Mhe. Fatma alisema JKCI imewaletea wananchi huduma muhimu zinazowawezesha kufanya uchunguzi wa afya, lakini pia kupata elimu ya kujikinga na magonjwa ya moyo.

“Kuna vitu vingi vya faida katika banda hili kuna huduma zote za msingi zinazohusiana na masuala ya moyo, lakini pia huduma nyingine muhimu za afya zinazopatikana kwa urahisi”, alisema Mhe. Fatma

Aidha Mhe. Fatma alisema kampeni ya Jua Namba Zako ni ya muhimu kwa kuwa inawahamasisha wananchi kujenga utamaduni wa kupima afya mara kwa mara badala ya kusubiri hadi wanapoumwa.

“Mimi tayari nimezijua namba zangu, fika kwenye banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete upime urefu, uzito, shinikizo la damu na vipimo vingine muhimu ili ujue hali yako ya afya”, alisema Mhe. Fatma

Vile vile Mhe. Fatma aliipongeza Serikali kwa uwekezaji mkubwa uliofanywa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na kuifanya  Taasisi hiyo kuwa miongoni mwa vituo vinavyotoa huduma za kisasa za matibabu ya moyo.

Mbali na kampeni ya Jua Namba Zako, Mhe. Fatma aliwahamasisha wananchi kuendelea kushiriki katika kampeni ya Kutoa ni Moyo inayolenga kuchangisha fedha za kuwasaidia watoto wenye matatizo ya moyo kupata matibabu katika Taasisi hiyo.
Posted by MROKI On Monday, July 13, 2026 No comments
 
Na Mwandishi Wetu
Rai imetolewa kwa wadau mbalimbali kujitoa kwa hali na mali kuchangia fedha kwa ajili ya mfuko unaohudumia wagonjwa wa figo na upandikizaji uloto kwa watoto wenye selimundu (sickle cell) wanaopatiwa matibabu katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) ya jijini Dodoma.

Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti Taifa wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mary Chatanda, Julai 13, 2026, jijini Dodoma.

Chatanda amesema, kutokana na gharama kubwa za matibabu ya magonjwa hayo, viongozi, taasisi binafsi, asasi za kiraia na wananchi kwa ujumla hawana budi kuunganisha nguvu ya pamoja, kuwezesha upatikanaji wa shilingi bilioni saba, ili wagonjwa wasio na uwezo, waweze kunufaika na mfuko huo na hatimaye kuokoa maisha yao.

"Wenzetu Hospitali ya Benjamin Mkapa, wamekuja na mpango kabambe wa kukusanya shilingi bilioni saba za kugharamia wagonjwa wa figo na selimundu, na UWT tuliposhirikishwa tuliona ni jambo jema kwani linagusa uhai wa watu, hivyo basi, niwaombe wadau na wananchi kwa ujumla kuchangia kuwezesha kuokoa maisha ya wagonjwa hao," amesema Chatanda.

Aidha, amesema upatikanaji wa fedha hizo utawezesha kuleta matumaini ya wagonjwa hao kuishi tena na ndiyo maana hafla hiyo imepewa jina la "Okoa Maisha Gala".

"Hata jina la tukio hili linajieleza wazi, yaani Okoa Maisha Gala, na sisi UWT tuko sambamba na serikali yetu ambayo imewekeza fedha nyingi katika uboreshaji wa sekta ya afya ili kuokoa maisha ya wananchi kwani wananchi wanapokuwa na afya njema, wanakuwa na uwezo wa kufanya shughuli zao za kujiingizia kipato na kujenga uchumi wa nchi," ameongeza.

Katika kuadhimisha miaka kumi ya utoaji huduma, BMH wameratibu hafla ya uchangiaji ili kupata fedha za kutibu wagonjwa wa figo na selimundu. Hafla hiyo inatarajiwa kuongozwa na Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, Julai 16, 2026, katika Ukumbi wa Mabeyo wa jijini Dodoma.
Posted by MROKI On Monday, July 13, 2026 No comments

July 12, 2026



 

Posted by MROKI On Sunday, July 12, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu.
Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imezindua rasmi Mwongozo wa Kisheria wa Utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa Waandishi wa Habari Wakongwe, hatua inayolenga kutambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari waliolitumikia Taifa kwa muda mrefu na kwa utumishi uliotukuka katika maendeleo ya sekta ya habari nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo, Julai 11, 2026, wakati wa maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika katika Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Kupitia hotuba yake iliyosomwa na Dkt. Egbert Mkoko, Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Bw. Tido Mhando, alisema mwongozo huo umeandaliwa kwa kuzingatia mamlaka iliyopewa Bodi chini ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 pamoja na Kanuni zake, ili kuweka utaratibu wa utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa waandishi wa habari wakongwe waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya taaluma hiyo.

Alisema mwongozo huo unawahusu waandishi wa habari ambao wakati Sheria ya Huduma za Habari ilipoanza kutumika mwaka 2016 walikuwa na umri wa miaka 50 au zaidi na walikuwa tayari wametoa mchango mkubwa katika sekta ya habari, lakini hawakupata fursa ya kujiendeleza hadi kufikia sifa za kitaaluma zinazohitajika kwa mujibu wa sheria.

"Mwongozo huu unalenga kuhifadhi historia ya tasnia ya habari, kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe na kuhakikisha uzoefu wao unaendelea kuwa sehemu ya urithi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini," ilieleza sehemu ya hotuba ya Mwenyekiti.

Bw. Mhando alisisitiza kuwa mwongozo huo hauondoi wala haupunguzi masharti ya msingi yaliyowekwa na Sheria ya Huduma za Habari kuhusu sifa za kupata ithibati kwa waandishi wa habari, bali unaweka utaratibu wa kutekeleza mamlaka ambayo sheria imeipa Bodi kuhusu utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa watu wenye utumishi uliotukuka na waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya sekta ya habari.

Aidha, aliipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuendelea kuiwezesha Bodi kutekeleza majukumu yake na kuimarisha ushirikiano unaolenga kukuza weledi, uwajibikaji na maadili katika taaluma ya uandishi wa habari.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alisema uzinduzi wa mwongozo huo ni hatua muhimu katika utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari na unaonesha dhamira ya Bodi ya kuimarisha viwango vya taaluma huku ikitambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe waliolitumikia Taifa kwa uaminifu, uzalendo na weledi.

Sambamba na uzinduzi huo, JAB iliendesha mdahalo uliowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya habari kujadili maendeleo ya sekta ya habari nchini, utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari pamoja na mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mwaka mmoja wa utekelezaji wa mfumo wa utoaji wa ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo vya sheria.

Posted by MROKI On Sunday, July 12, 2026 No comments

July 11, 2026

Mkurugenzi wa Sera na Mipango kutoka Wizara ya Nishati,Petro Lyatuu ametembelea banda la Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA ) katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba)leo  Julai 11 2026.



Posted by MROKI On Saturday, July 11, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Mkurugenzi Mtendaji wa Wasafi Media, Nasib Abdul maarufu Diamond Platnumz, amesema utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari unaweka mazingira bora ya kukuza uwekezaji katika sekta ya habari kwa kuhakikisha vyombo vya habari vinaendeshwa kwa kuzingatia sheria, weledi na viwango vya taaluma.

Diamond alitoa kauli hiyo tarehe 11 Juni, 2026 alipotembelea Banda la Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), kufuatia mwaliko wa Bodi hiyo ili kujionea huduma na elimu inayotolewa kwa waandishi wa habari pamoja na wananchi.

Alisema uwekezaji katika sekta ya habari unahitaji nidhamu, maono, subira na uongozi unaozingatia sheria, akibainisha kuwa usimamizi unaofanywa na JAB unasaidia wawekezaji kuelewa matakwa ya kisheria na namna ya kuyazingatia bila kuhisi kuwa biashara zao zinakwamishwa.

"Utekelezaji na usimamizi wa Sheria ya Huduma za Habari unaonesha ni kwa kiwango gani Serikali inaunga mkono uwekezaji wa vijana katika sekta ya habari. Kazi ya Bodi si kuzuia watu kufanya biashara, bali kuwaelekeza kufuata matakwa ya sheria na kuwahamasisha kuongeza elimu na kukidhi vigezo vinavyotakiwa," alisema Diamond.

Aliongeza kuwa utekelezaji wa sheria unahitaji busara, maarifa na uwezo wa kuwaelimisha wadau ili waelewe mabadiliko ya taratibu bila kujenga hofu au kuona kuwa wanawekewa vikwazo.

"Kazi hii inahitaji busara na maarifa ya kuwafundisha watu, kuwaelekeza na kuwafanya waelewe taratibu mpya pasipo kuona kwamba wameharibiwa biashara zao. Nimeona Bodi ina timu nzuri inayounga mkono maono ya uongozi wake katika kusimamia sekta hii," alisema Diamond.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alimpongeza Diamond kwa uwekezaji wake katika sekta ya habari na kwa Wasafi Media kuendelea kuzingatia matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari.

Alisema JAB itaendelea kushirikiana na wamiliki wa vyombo vya habari na wadau wengine kuhakikisha sheria inatekelezwa kwa njia inayokuza weledi, uwajibikaji na maendeleo ya sekta ya habari, huku ikitoa elimu na ushauri unaowawezesha wadau kutekeleza matakwa ya sheria kwa ufanisi.

Ziara ya Diamond katika Banda la JAB ilikuwa sehemu ya maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika ndani ya Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, ambapo Bodi imekuwa ikitoa huduma za ithibati, elimu kuhusu Sheria ya Huduma za Habari na ushauri kwa waandishi wa habari, wamiliki wa vyombo vya habari na wananchi.
Posted by MROKI On Saturday, July 11, 2026 No comments
 



Dar es Salaam
Mjiolojia kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Abbas Mruma, amesema Tanzania inaendelea kujijengea nafasi muhimu duniani kutokana na kuwa na hifadhi kubwa ya madini muhimu ya kimkakati, yakiwemo graphite, lithium na rare earth elements, ambayo ni nguzo muhimu katika maendeleo ya teknolojia za kisasa na nishati safi.

Mruma ameyasema hayo wakati akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Stanslaus Muyungi, alipotembelea banda la Tume ya Madini katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Amesema mahitaji ya madini ya lithium yanaendelea kuongezeka kwa kasi duniani kutokana na matumizi yake katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, simu za mkononi, kompyuta mpakato (laptops) na vifaa vingine vya kisasa vya kielektroniki.

Amefafanua kuwa nchini Tanzania, madini ya lithium yanapatikana zaidi katika maeneo ya Dodoma na Ikungi, mkoani Singida.

Akizungumzia madini ya graphite, Mruma amesema Tanzania ndiyo nchi inayoongoza barani Afrika kwa kuwa na hifadhi kubwa ya madini hayo, ambayo ni malighafi muhimu katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme pamoja na matumizi mengine mbalimbali ya viwandani.

Aidha, amesema Tanzania pia ina hifadhi kubwa ya madini ya rare earth elements katika Ukanda wa Afrika Mashariki, yanayopatikana katika eneo la Ngualla mkoani Songwe na Wigu mkoani Morogoro.

Baada ya kupokea maelezo hayo, Dkt. Richard Stanslaus Muyungi ameipongeza Tume ya Madini kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu rasilimali za madini na fursa zilizopo katika sekta hiyo.

Amesema elimu hiyo ina mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa rasilimali za madini, fursa za uwekezaji na nafasi ya sekta ya madini katika kukuza uchumi na maendeleo endelevu ya Taifa.
Posted by MROKI On Saturday, July 11, 2026 No comments

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe, akitoa maelekezo kwa watumishi wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali wakati alipotembelea banda la Mamlaka katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) Julai 8,2026.
Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Aretas Lyimo, akisaini kitabu cha wageni wakati aipotembelea banda la Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) Julai 8,2026.
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe, akisaini kitabu cha wageni wakati aipotembelea banda la Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) Julai 8,2026.
*********
Na. Judith Meingarai
Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Aretas Lyimo, ameipongeza Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) kwa mchango wake mkubwa katika kuimarisha mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini kupitia uchunguzi wa kitaalamu wa sampuli, matumizi ya teknolojia za kisasa pamoja na utoaji wa ushahidi wa kisayansi unaosaidia kuimarisha ushindi wa kesi mahakamani.

Akizungumza wakati alipotembelea banda la GCLA katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Kamishna Jenerali Lyimo alisema ushirikiano kati ya DCEA na GCLA umeendelea kuimarika na kuwa nguzo muhimu katika kutekeleza majukumu ya taasisi hizo kwa ufanisi.

Alisema sampuli zote zinazowasilishwa GCLA kwa ajili ya uchunguzi hupimwa kwa wakati na kwa usahihi, jambo linalowezesha wataalamu wa Mamlaka hiyo kutoa ushahidi wenye weledi mahakamani na hivyo kuongeza kiwango cha mafanikio katika kesi zinazohusu dawa za kulevya.

"Ushirikiano wetu na GCLA ni wa mfano. Majibu ya uchunguzi tunayapata kwa wakati pamoja na ushahidi wa kitaalamu unaotolewa na Wakemia mahakamani umechangia kwa kiwango kikubwa kushinda kesi mbalimbali zinazohusu dawa za kulevya," alisema Lyimo.

Aidha, aliipongeza GCLA kwa kuendelea kuwekeza katika vifaa na teknolojia za kisasa zinazowezesha kubaini aina mbalimbali za dawa za kulevya na kemikali husika, akieleza kuwa uwezo huo umeifanya Tanzania kuwa na mfumo imara wa uchunguzi wa kisayansi unaokidhi mahitaji ya sasa.

Alibainisha kuwa duniani kuna zaidi ya aina 1,430 za dawa za kulevya na kwamba uwezo wa GCLA wa kuzitambua na kuzichunguza kwa usahihi ni mchango mkubwa katika kuimarisha utekelezaji wa sheria na utoaji wa haki.

Kamishna Jenerali Lyimo pia aliwataka wafanyabiashara na wananchi kuhakikisha wanajiridhisha kuhusu kemikali zilizomo kwenye bidhaa wanazoingiza au kuuza nchini kwa kushirikiana na GCLA, pamoja na taasisi nyingine za udhibiti, ili kuepuka kujikuta wakikiuka sheria bila kufahamu.

"Baadhi ya wafanyabiashara wamejikuta wakikamatwa kwa kuuza bidhaa walizodhani ni salama, lakini baadaye kubainika kuwa zina kemikali zinazohusiana na dawa za kulevya. Ni muhimu kupata ushauri na uhakiki wa kitaalamu kabla ya kuingiza au kusambaza bidhaa hizo," alisisitiza.

Wakati huo huo, mmoja wa wananchi waliotembelea banda la GCLA, Pasehsi Anthony mkazi wa Mbezi, Dar es Salaam, alisema elimu aliyoipata imemsaidia kuelewa kwa undani mchango wa Mamlaka hiyo katika mfumo wa haki jinai nchini.

Alisema kabla ya kutembelea banda hilo hakuwa akifahamu kuwa dawa zote za kulevya zinazokamatwa nchini lazima zipitie uchunguzi wa kisayansi katika maabara za GCLA ili kuthibitisha aina ya dawa husika kabla ya ushahidi huo kutumika mahakamani.

"Leo nimegundua kuwa GCLA ina jukumu kubwa zaidi kuliko nilivyokuwa nikifahamu. Uchunguzi wake wa kisayansi unasaidia kuthibitisha ukweli mahakamani na kuhakikisha haki inatendeka. Nawahamasisha wananchi wote watembelee banda hili ili wapate elimu muhimu kuhusu huduma zinazotolewa na taasisi hii," alisema Anthony.

Kupitia ushiriki wake katika Maonesho ya Sabasaba, GCLA inaendelea kutumia jukwaa hilo kutoa elimu kwa wananchi kuhusu huduma zake mbalimbali, ikiwemo uchunguzi wa kisayansi wa dawa za kulevya, kemikali, bidhaa, mazingira na vielelezo vya jinai, sambamba na kuhamasisha matumizi salama ya kemikali kwa maendeleo na usalama wa taifa.


Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kuthibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Aretas Lyimo (Katikati), akiwa na Mkurugenzi wa Huduma za Taasisi, Evaclotida Kapinga (wa nne kutoka kushoto) pamoja na watumishi wa Mamlaka katika maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) Julai 8,2026.
Posted by MROKI On Saturday, July 11, 2026 No comments

July 10, 2026


Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia Mradi wa Urejeshaji Endelevu wa Mazingira na Hifadhi ya Bayoanuai Tanzania imewezesha urejeshaji wa hekta milioni 3.3 za ardhi na misitu iliyoharibiwa hadi kufikia mwezi Desemba 2024.
 
Hayo yamebainishwa Julai 9, 2026 Mkoani Morogoro na Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais, Abdllah Hassan Mitawi wakati ufunguzi wa warsha ya kujenga uwezo kikosi-kazi cha taifa cha urejeshaji wa mazingira ya ardhi na misitu iliyoharibika.
 
Amebainisha kuwa Tanzania imebarikiwa utajiri mkubwa wa mifumo ikolojia ambapo takribani hekta milioni 48 ni misitu, ambapo hata hivyo pamoja na wingi wa rasimali hizo kumekuwepo na changamoto za uharibifu wa mazingira, ambapo tafiti zimeonesha kuwa takribani hekari 469,000 za misitu hupotea kila mwaka.
 
Mitawi amesema urejeshaji wa Ardhi ya Misitu iliyoharibiwa ni sehemu ya ajenda muhimu ya maendeleo endelevu ya Tanzania, kutokana na hatua hiyo Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kisera na kimkakati kwa kushirikiana na wadau.
 
Amesema mwa juhudi hizo ni utekelezaji wa Mkakati wa AFR100, unaolenga kurejesha hekta milioni 100 za ardhi  na misitu iliyoharibika barani Afrika kufikia mwaka 2030 ambapo mkakati huo unachangia malengo ya kidunia ya kurejesha hekari milioni 350 za ardhi na misitu duniani kote.
 
Amefafanua kuwa katika kuchangia jitihada za kimataifa na malengo ya uhifadhi mazingira kitaifa, mwaka 2018, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliahidi kurejesha hekta milioni 5.2 za maeneo ya ardhi na misitu iliyoharibika kufikia mwaka 2030 chini ya mkakati wa AFRI100.
 
Kwa mujibu wa Mitawi amesema mwaka 2024 Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia mradi wa Urejeshaji Endelevu wa Mazingira na Hifadhi ya Bayoanuai Tanzania (SLR) ilikamisheni Kituo cha Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC) kufanya tathmini ya utekelezaji wa ahadi hiyo ili kubaini hatua iliyofikiwa.
 
Ameeleza utekelezaji wa ahadi hiyo inaongozwa na na Mkakati wa Taifa wa Urejeshaji wa Ardhi na Misitu iliyoharibiwa (2023–2033); Mpango Kabambe wa Taifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022 – 2032); Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024 -2034) na Programu ya Mageuzi ya Usimamizi wa Mazingira kuelekea Dira2050.
 
”Nichukue fursa hii kuwajulisha wajumbe wa kikosi-kazi hiki mchukue jambo hili kwa umakini na uzito unaostahili, kwakuwa Serikali na wadau wote wa masuala ya urejeshaji na hifadhi wa mazingira watategemea sana maoni, ushauri na mapendekezo yenu” amesema Mitawi.
Kaimu Meneja wa Vyanzo vya Mbegu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Dk Fortunata Senya alisema Serikali imeandaa Mkakati wa Taifa wa Urejeshaji wa Mandhari ya Misitu wa mwaka 2023–2030 ili kuhakikisha lengo la kurejesha hekta milioni 5.2 linafikiwa.
 
Alisema mafanikio ya mpango huo hayawezi kupatikana kwa juhudi za Serikali pekee, bali yanahitaji ushiriki mpana wa wadau mbalimbali wakiwamo taasisi za utafiti, sekta binafsi, mashirika ya maendeleo na wananchi.
 
Kwa upande wake, Mtafiti wa Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI), Joshua Maguzu alisema taasisi hiyo inaendelea kufanya tafiti zinazolenga kubaini aina sahihi za miti zinazofaa kupandwa katika maeneo mbalimbali ya nchi kulingana na hali ya udongo na tabianchi.
 
 
Alisema matokeo ya tafiti hizo yanawasaidia wataalamu na wananchi kuchagua miche inayostawi vizuri katika maeneo husika, hatua inayoongeza mafanikio ya urejeshaji wa mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.




Posted by MROKI On Friday, July 10, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo