Nafasi Ya Matangazo

June 14, 2026









Na, mwandishi wetu – Arusha
Mgongano wa maslahi kwa watumishi wa umma umetajwa kuathiri ufanisi kwenye utendaji na majukumu ya Serikali kutokana na matokeo hasi ya vitendo hivyo vinavyopelekea kuchochea mazingira ya rushwa na kujinufaisha binafsi badala ya ofisi na kukwamisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi. 

Hayo yameelezwa mapema mwishoni mwa wiki Jijini Arusha na Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Stella Mwaiswaga wakati akifunga mafunzo kwa wajumbe wa Kamati Maalum ya Menejimenti ya ofisi hiyo yaliyolenga kuwajengea uwezo wajumbe hao katika kusimamia masuala ya uadilifu sehemu za kazi .

Aliongezea kuwa ni muhimu kuendelea kuzingatia taratibu, kanuni na sheria za utumishi wa umma ili kuepuka vitendo vinavyoathiri utendaji wa watumishi hasa katika kujali maslahi binafsi yanayochochea kukosekana kwa huduma bora kwa wananchi.

Alisema kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuwa Ofisi ya mfano katika masuala ya Uratibu wa Shughuli za Serikali hivyo ni wajibu wa kila mtumishi kuendelea kuzingatia masuala ya uadilifu ikiwemo la kujilinda na vitendo vyote vinavyoweza kuharibu taswira ya ofisi hiyo.

Akiwasilisha mada kuhusu masuala ya dhana ya Mgongano wa Maslahi, Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Kaskazini Bw. Gerald Mwaitebele amesema ni vyema kuzingatia na kuepuka masuala ya mgongano wa maslahi katika maeneo ya kazi kwani yameendelea kuwa chachu ya kuondoa ufanisi na uwazi wa ofisi zetu.

Aliongezea kuwa,kiongozi anayetekeleza majukumu kwa kujali maslahi binafsi humpelekea kutokuwa na maamuzi sahihi na kusababisha kuharibu utendaji wa taasisi na ofisi anayoihudumia hivyo kuondoa uaminifu kwa jamii, hadi ngazi ya Taifa. 

"Mgongano wa maslahi hutokea pale ambapo maslahi yako binafsi (kifedha, kijamii au kindugu) yanapokinzana na majukumu yako ya kikazi. Hali hii inapaswa kuepukwa kwani inaharibu uadilifu, inasababisha upendeleo, na inaweza kuondoa uaminifu wa umma au wa taasisi tunazofanyia kazi," alisisitiza Mwaitebele

Akitoa neno la shukran kwa niaba ya wajumbe wa kamati hiyo, Bi.Ngole Keya, Naibu Katibu wa Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshukuru mafunzo hayo yenye lengo la kuwajengea uelewa na kuendelea kuwakumbusha masuala ya msingi katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

“Kipekee tunawapongeza watoa mada wametujenga na kutupa maarifa zaidi katika kuendelea kuboresha utendaji wetu ili kuendelea kutoa huduma bora na kuhakikisha tunaendelea vyema na majukumu yetu ikiwemo la kuratibu shughuli za Serikali kwa kuzingatia misingi na kanuni za kiutumishi zinavyoelekeza,” alisema Bi.Ngole.
Posted by MROKI On Sunday, June 14, 2026 No comments

June 13, 2026






Dar Es Salaam
Serikali imesisitiza kufanyia kazi kwa haraka Mapendekezo yaliyotolewa na Timu ya Wataalamu iliyoundwa Kuishauri Wizara ya Madini kuhusu namna ya Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo Kiuchumi na kueleza kuwa, utatuzi wa changamoto za Mitaji, Teknolojia na upatikanaji wa taarifa sahihi za Kijiolojia kwa Wachimbaji Wadogo wa Madini ni hatua muhimu ya kuongeza ajira kwa watanzania, kupunguza umaskini na kukuza uchumi wa Taifa kuelekea Dira 2050.

Hayo yamebainishwa Juni 13, 2026 jijini Dar Es Salaam  na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, wakati wa hafla ya Kupokea Mapendekezo ya Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo Nchini na kusisitiza kwamba, maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha mipango ya maendeleo inajibu changamoto tatu kuu za taifa ambazo ni kuongeza mitaji kwa wananchi, kuzalisha ajira na kupunguza umaskini.

Amesema kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata mitaji na teknolojia, kunafungua fursa za kuongeza uzalishaji, ajira na kipato cha wananchi na kuongeza kuwa hiyo ndiyo njia mojawapo ya kupambana na umaskini.

‘’Kazi kubwa ya Waziri ni kutoa mwelekeo wa kisera wa taasisi au wizara anayoiongoza. Kwa muda niliokaa kwenye Wizara yangu, Mhe. Mavunde amekua akijua kipaumbele anachokitaka na jinsi ya kukipata,’’amesisitiza Prof. Mkumbo.

Ameongeza kwamba, hali ya umaskini nchini  bado ipo kwa kiwango cha juu na kutolea mfano wa Mkoa wa Geita ambao unaoongoza kwa shughuli za uchimbaji madini ya dhahabu nchini ambapo  hali ya umaskini inafikia asilimia 38 na kusisitiza kwamba, wachimbaji wadogo wanapowezeshwa wanasaida kutatua changamoto kama hizo na kuongeza kuwa, Sekta ya Madini imewekwa kama moja ya sekta muhimu za kimageuzi  inayotarajiwa kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi na ajira ambapo awali haikuwa ikibeba watu wengi.

Naye, Waziri wa Madini Anthony Mavunde akizungumza katika halfa hiyo, amesema Serikali iliamua kuunda kamati hiyo kutokana na mchango mkubwa unaotolewa na wachimbaji wadogo katika Sekta ya Madini, licha ya kukabiliwa na changamoto za mitaji, teknolojia na upatikanaji wa huduma za kifedha , hivi sasa wanachangia asilimia 40 ya makusnyo ya maduhuli ya Serikali.

Ameongeza kwamba, kuwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika Sekta ya Madini ndani ya miaka ya hivi karibuni yanaonyesha umuhimu wa kuwawezesha zaidi wachimbaji wadogo ili waongeze mchango wao katika uchumi wa taifa.

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, Mwaka wa Fedha  2015/16 Sekta ya Madini katika mwaka mmoja iliingiza shilingi bilioni 161 pekee katika Mfuko Mkuu wa Serikali. 

Hata hivyo, kufuatia mageuzi mbalimbali yaliyofanyika ikiwemo mabadiliko ya sheria, kuanzishwa kwa masoko ya madini na udhibiti wa biashara haramu ya madini, makusanyo yameongezeka kwa kiwango kikubwa kufikia Shilingi trilioni 1.107 mwaka 204/25 na mpaka kufikia  tarehe 13, Juni, tayari Serikali imekusanya shilingi trilioni 1.3.

Amesisitiza kuwa jukumu la Serikali yoyote duniani ni kuwawezesha wananchi wake kufanya shughuli za uzalishaji kwa tija zaidi sababu ambayo ilipelekea  Serikali kuweka mkakati maalum wa kuwawezesha wachimbaji wadogo ili waweze kukua na kuwa wachimbaji wa kati na baadaye wakubwa.

Kuhusu changamoto ya mitaji, Waziri Mavunde  amesema Serikali imeanza utekelezaji wa Kampuni ya dhamana ya mikopo (Credit Guarantee Corporation) itakayosaidia  wachimbaji kupata mikopo kutoka taasisi za fedha mbalimbali.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo  Dkt. Victor Tesha  amesema suluhu ya changamoto hizo ni kujenga mfumo jumuishi wa kuwawezesha wachimbaji wadogo kupitia upatikanaji wa mitaji, teknolojia za kisasa, taarifa za kijiolojia na uratibu wa taasisi zinazohusika na sekta hiyo huku akipendekeza kuanzishwa kwa Mfuko wa Madini Tanzania utakaowezesha miradi yenye sifa kupata fedha za kuendeleza uzalishaji, kununua mitambo na kuboresha shughuli za uchimbaji, na kuongeza kwamba, mfuko huo utasaidia kugharamia tafiti na taarifa za kijiolojia kwa wachimbaji.

Ameongeza kuwa, baada ya mfuko huo kukua na kuimarika, hatua itakayofuata itakuwa ni kuanzisha Benki ya Wachimbaji itakayotoa huduma maalumu za kifedha kwa sekta ya madini kwa masharti yanayoendana na mazingira ya wachimbaji.

‘’Kamati pia imependekeza mikopo ielekezwe zaidi katika ununuzi wa mitambo na teknolojia badala ya fedha taslimu pekee, ili kuongeza tija, uzalishaji na usalama katika shughuli za uchimbaji,’’ amesema Tesha.

 Naye, rais wa Shirikisho la Vyama Vya Wachimbaji Wadogo John Bina, ameipongeza Serikali kwa ripoti hiyo na kueleza imetokana  na Serikali kusikiliza na kuyafanyia kazi maoni na changamoto za wachimbaji wadogo, pamoja na kuipongeza kwa kutenga asilimia 10 ya mapato yanayotokana na shughuli za madini kwa ajili ya utafiti.
Posted by MROKI On Saturday, June 13, 2026 No comments








Na, Mwandishi Wetu - Dar es Salaam
Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Taasisi OpenMap Development Tanzania (OMDTZ), kupitia mradi wa Ramani Zetu, Sauti Zetu imeendesha warsha ya kupitia na kuthibitisha Mipango ya Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa kwa kata tano za Makurumula, Mabibo, Keko, Ubungo na Tabata jijini Dar es Salaam.

Warsha hiyo imewakutanisha viongozi wa serikali za mitaa, Kamati za Usimamizi wa Maafa za Kata, wataalamu wa usimamizi wa maafa, waratibu wa maafa wa mkoa na wilaya pamoja na wadau mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha mipango hiyo inakidhi mahitaji halisi ya jamii zinazokabiliwa na hatari ya mafuriko Dar es Salaam.

Akifungua warsha hiyo Mkurugenzi Msaidizi wa Operesheni za Maafa kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Kanali Selestine Masalamado amesema kuwa ubora wa mpango wa maafa hupimwa kwa uwezo wake wa kutekelezeka na kuleta matokeo chanya kwa wananchi, huku akisisitiza umuhimu wa mipango hiyo kuzingatia mazingira halisi, rasilimali zilizopo na uwezo wa taasisi husika.

“Mradi huu unaofadhiliwa na Zayed Sustainability Prize kupitia Taasisi ya Open Map Development Tanzania (OMDTZ), kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – Idara ya Usimamizi wa Maafa, umekuja wakati sahihi na tunamatarajio makubwa katika kuleta matokeo chanya kuhakikisha tunaimarisha masuala ya usimamizi wa maafa nchini, ”alisema Kanali Masalamado

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa OMDTZ, Bw. Innocent Maholi, alisema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa kupitia matumizi ya teknolojia, uchoraji ramani shirikishi na uwekezaji katika mifumo ya tahadhari ya mapema katika maeneo hatarishi.

Naye Mratibu wa Maafa wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Gerald Sondo, amepongeza ushirikiano huo akieleza kuwa mipango hiyo itasaidia kuongeza utayari wa jamii, kuboresha uratibu wa mwitikio wa dharura na kupunguza athari za mafuriko katika Jiji la Dar es Salaam.

“Kwa kipindi cha miezi mitatu iliyopita, kamati za usimamizi wa maafa katika kata husika zimefanya tathmini ya vihatarishi, kubainisha njia za uokoaji na maeneo salama, kuandaa mifumo ya mawasiliano na uratibu pamoja na kupendekeza hatua za tahadhari ya mapema zinazoshirikisha jamii,”alisema Bw. Sondo.

Aliongezea kuwa, Mipango iliyothibitishwa itatumika kama mwongozo wa vitendo kwa jamii kabla, wakati na baada ya maafa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha usalama wa wananchi na ustahimilivu dhidi ya mafuriko na majanga mengine.
Posted by MROKI On Saturday, June 13, 2026 No comments

June 12, 2026








Na, mwandishi wetu - Arusha
SERIKALI imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuzingatia misingi ya uadilifu katika utumishi wa umma ili kuhakikisha utekelezaji wa majukumu na mipango ya maendeleo unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia maadili ya kazi.

Hayo yamesemwa hii leo (12 Juni, 2026) na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, wakati akifungua Mafunzo ya Kamati ya Uadilifu yaliyolenga kuwajengea uwezo wajumbe wa Kamati Maalum ya Menejimenti katika kusimamia masuala ya uadilifu katika ofisi hiyo.

“Uadilifu ni nguzo muhimu katika ufanikishaji wa majukumu na utekelezaji wa mipango ya maendeleo katika sehemu za kazi,” amesema Dkt. Yonazi.

Dkt. Yonazi amesema kuwa ni wajibu wa kila mtumishi wa umma kuhakikisha anazingatia maadili ya kazi na kulinda misingi ya uadilifu ili kuimarisha utendaji na kuongeza imani ya wananchi kwa Serikali.

Aidha, Dkt. Yonazi amesema mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha wajumbe kusimamia utekelezaji wa Mkakati wa Uadilifu kwa kuhakikisha unaingizwa katika mipango kazi na bajeti za mwaka za taasisi.

Vilevile, amebainisha kuwa Kamati za Uadilifu zina jukumu la kusimamia utekelezaji wa sera dhidi ya rushwa na kuhakikisha watumishi wanazingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma. 

“Kuna umuhimu wa kuimarisha uwazi na uwajibikaji pamoja na kuanzisha mifumo madhubuti ya kupokea na kushughulikia malalamiko ya wananchi kwa kuzingatia usiri.

Akiwasilisha mada ya masuala ya Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji (NACSAP IV) 2023-2030 Mkurugenzi kutoka Ofisi ya Rais Ikulu Bw. Andrew Massawe amesema, ni wajibu wa watumishi kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na kupinga vitendo vyote vinavyoashiria mazingira ya rushwa ili kuendelea kuhudumia wananchi, na Taifa kwa ujumla katika misingi sahihi ya utumishi wa umma.

“Tufanye kazi kwa uadilifu na kuzingatia masuala ya huduma bora kwa wateja, tusihudumie watu kama favor bali tutoe huduma kwa viwango bora vinavyotakiwa,”alisema Bw. Massawe
Posted by MROKI On Friday, June 12, 2026 No comments








Na Oscar Nkembo
Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Mhe. Naitapwaki Tukai, amewataka wachimbaji wa dhahabu kuzingatia usimamizi na matumizi salama ya Kemikali ili kuepukana na madhara ya kemikali yanayoweza kuathiri afya za wananchi na mazingira.

Mkuu wa Wilaya, Tukai amesema hayo Juni 12, 2026 wakati akifungua mafunzo ya usimamizi na matumizi salama ya Kemikali kwa wachimbaji wadogo wa Nzega na tabora yaliyoandaliwa na Ofisi ya Kanda ya Kati ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na kufanyika wilayani Nzega Mkoa wa Tabora.

“Inaumiza sana kupoteza nguvu kazi kwa uzembe wa kutozingatia mafunzo haya, Afya ni mtaji namba moja, tufanye uchimbaji tutumie kemikali kwa kuzingatia yale tunayoelekezwa na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ili tuweze kulinda afya za watu na mazingira” alisema Tukai.

Naye Meneja wa Kanda ya Kati ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Magdalena Mtenga, amesema Mamlaka inahakikisha inawawezesha wananchi kwenye shughuli zao wakiwa salama kiafya pamoja na Mazingira yao kwa kuhakikisha taratibu na kanuni za matumizi salama ya kemikali yanazingatiwa.

“Mamlaka imekuwa rafiki na taasisi wezeshi kwa wananchi ili kufanikisha shughuli zao huku wakiwa salama na kuayaacha mazingira yakiwa salama, Kemikali ni muhimu zinatusaidia kuingiza kipato binafsi na pato la Taifa lakini lazima tuzingatia usimamizi na matumizi salama ya hizo Kemikali ili zisilete madhara” alisema Mtenga.

Aidha, Wadau wa Kemikali wameipongeza Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kwa kuwekeza katika teknolojia ikiwemo mfumo wa wa usajili wa wadau wa kemikali kwani mfumo huo umekuwa mkombozi mkubwa kwao kwenye shughuli mbalimbali za usajili na upatikanaji wa vibali vya Kemikali.

“Mfumo wa usajili wa wateja wa kemikali umerahisisha sana kazi na kuokoa muda na fedha, kwa sababu huhitaji kwenda ofisini, bali kwa njia ya mtandao tu unaweka nyaraka
Posted by MROKI On Friday, June 12, 2026 No comments

June 11, 2026



Na, Mwandishi Wetu - Dodoma
KATIKA kuendelea kuimarika kwa sekta ya usimamizi wa maafa nchini na kuongezeka kwa hamasa ya kujifunza mifumo ya usimamizi wa maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura, wanafunzi wa Shahada ya Usimamizi wa Hatari za Maafa kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wamefanya ziara ya mafunzo kupitia Idara ya Usimamizi wa Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu).

Ziara hiyo imefanyika tarehe 10 na 11 Juni, 2026 iliyolenga kuwajengea uelewa kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa, ufuatiliaji wa vihatarishi mbalimbali, utoaji wa taarifa za tahadhari ya mapema pamoja na uratibu wa operesheni za dharura nchini.

Katika ziara hiyo, wanafunzi walitembelea Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kilichopo Ngome, Chumba cha Ufuatiliaji wa Mienendo ya Majanga na Tahadhari za Mapema kilichopo Mtumba pamoja na eneo la ujenzi wa Kituo Kikuu cha Taifa cha Usimamizi wa Maafa na Maghala ya Kuhifadhi Vifaa vya Dharura kilichopo Nzughuni, jijini Dodoma.

Akizungumza na wanafunzi hao, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Dkt. Jim Yonazi, aliwapongeza kwa uamuzi wao wa kujifunza kwa vitendo kuhusu masuala ya usimamizi wa maafa na kuonesha dhamira ya kuchangia maendeleo ya sekta hiyo nchini.

Dkt. Yonazi aliwahimiza wanafunzi kuendelea kujiongezea maarifa kupitia tafiti, ubunifu na uandishi wa machapisho mbalimbali kuhusu usimamizi wa hatari za maafa ili kuchangia katika kuimarisha uwezo wa Taifa wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa. 

Aidha, aliwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za elimu ya juu katika kukuza taaluma ya usimamizi wa maafa na kuahidi kutembelea Chuo Kikuu cha Dodoma siku zijazo kwa ajili ya kutoa mihadhara na kushiriki katika mijadala ya kitaaluma.

“Ziara yenu ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu ya juu na Serikali katika kujenga kizazi cha wataalamu wenye uelewa wa kina kuhusu usimamizi wa hatari za maafa, tahadhari ya mapema na uratibu wa dharura. Aidha, inaonesha mafanikio ya uwekezaji uliofanywa na Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa, jambo ambalo limeendelea kuvutia wadau mbalimbali, watafiti na wanafunzi kutoka ndani na nje ya nchi kujifunza na kubadilishana uzoefu,”alisema Dkt. Yonazi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, aliwaeleza wanafunzi hao kuwa wamefanya jambo la msingi kwa kutenga muda wa kujifunza na kushuhudia kwa vitendo namna Serikali inavyotekeleza majukumu yake ya usimamizi wa maafa nchini.

Alisema kuwa mifumo iliyowekwa na Serikali katika ufuatiliaji wa vihatarishi, utoaji wa tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao dhidi ya madhara yatokanayo na maafa mbalimbali.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Bi. Jane Alfred Kikunya, ambaye aliongoza mafunzo hayo, alisema ameridhishwa na hamasa na ari kubwa iliyooneshwa na wanafunzi katika kujifunza masuala ya usimamizi wa maafa na tahadhari ya mapema.

Bi. Jane alieleza kuwa ujio wa wanafunzi hao unaonesha namna sekta ya usimamizi wa maafa inavyoendelea kupata umuhimu katika jamii na taasisi za elimu ya juu. Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kufungua milango kwa wanafunzi, watafiti na wadau mbalimbali wanaotaka kujifunza kuhusu mifumo ya ufuatiliaji wa majanga, uchambuzi wa vihatarishi, tahadhari za mapema na uratibu wa operesheni za dharura kutembelea ofisi hiyo.

Kwa upande wake, Dkt. Japhet Ringo kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma ambaye aliambatana na wanafunzi hao, aliishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuwapatia wanafunzi fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu mifumo ya usimamizi wa maafa nchini.

Dkt. Ringo alisema kuwa ziara hiyo imekuwa darasa muhimu lililowawezesha wanafunzi kuunganisha maarifa ya kinadharia wanayojifunza darasani na utekelezaji halisi wa shughuli za usimamizi wa maafa katika ngazi ya Taifa.

Aliongeza kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kukuza tafiti, ubunifu na maendeleo ya taaluma ya usimamizi wa hatari za maafa ili kusaidia juhudi za Taifa za kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.


Posted by MROKI On Thursday, June 11, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akifuatilia Hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/2027, kupitia Televisheni ya Taifa (TBC1), Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 11 Juni, 2026. Bajeti hiyo ilikuwa ikisomwa Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, kwenye Bunge la 13, Mkutano wa tatu katika Kikao cha 48 Jijini Dodoma. 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipiga makofi pamoja na Wasaidizi wake mara baada ya Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar kumaliza kuwasilisha Hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/2027 kwenye Bunge la 13, Mkutano wa tatu katika Kikao cha 48 Jijini Dodoma. Rais Dkt. Samia alikuwa akifuatilia Hotuba ya Bajeti hiyo Kuu ya Serikali kupitia Televisheni ya Taifa (TBC1), Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 11 Juni, 2026.






Posted by MROKI On Thursday, June 11, 2026 No comments



Dodoma
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, amefanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Marvel Gold ya Australia, Timothy Strong, jijini Dodoma ambapo amepokea taarifa kuhusu maendeleo ya hatua za awali za mradi wa mgodi wa dhahabu unaoendelezwa katika Wilaya ya Hanang’, Mkoa wa Manyara.

Akizungumza katika kikao hicho, Strong amesema kuwa kampuni hiyo inaishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi yaliyowezesha kufanikisha uwekezaji huo.

Ameeleza kuwa baada ya kukamilisha hatua ya awali ya utafiti kwa kutumia teknolojia ya ndege nyuki (drones), kampuni imeingia katika hatua ya pili ya uchorongaji, huku awamu ya kwanza ya shughuli hizo ikitarajiwa kukamilika mwishoni mwa Julai 2026.

“Shabaha yetu ni kuanza mara moja shughuli za uchimbaji pindi ambapo taratibu zote zitakapokamilika kwa mafanikio,” amesema Strong.

Kwa upande wake, Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira bora na kuvutia uwekezaji unaochochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Waziri Mavunde ameipongeza Kampuni ya Marvel Gold kwa kasi ya utekelezaji wa mradi huo mpya wa dhahabu katika Mkoa wa Manyara, akieleza kuwa kukamilika kwake kutachochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika Wilaya ya Hanang’, Mkoa wa Manyara na Tanzania kwa ujumla.

“Ni matarajio yetu kwamba mradi huu utakuwa chachu ya maendeleo kwa wananchi wa Hanang’ na Mkoa wa Manyara, sambamba na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa Taifa. Serikali itaendelea kushirikiana na wawekezaji mbalimbali ili kuhakikisha sekta ya madini inaendelea kutoa mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa Tanzania,” amesema Waziri Mavunde.
Posted by MROKI On Thursday, June 11, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo