Nafasi Ya Matangazo

June 19, 2026




Na Adelina Johnbosco - MAELEZO
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, amesema benki hiyo itaendelea kuwa mdau mkubwa wa maendeleo ya michezo nchini kwa kushiriki kikamilifu kufanikisha mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) yanayotarajiwa kufanyika nchini Tanzania mwaka 2027.

Dkt. Nsekela ametoa kauli hiyo Juni 19, 2026, alipotembelea banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea kwenye viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.

Amesema CRDB iko tayari kushirikiana kwa karibu na wizara hiyo katika kuhakikisha maandalizi na utekelezaji wa AFCON 2027 unafanikiwa kwa kiwango kikubwa.

"Sisi CRDB tunaahidi kuwa na wizara hii bega kwa bega kila hatua pale tutakapohitajika. Ni wadau wakubwa wa michezo na sekta nyingine zilizo chini ya wizara hii, hivyo nawahakikishia kwamba tutashiriki kwa nguvu zote kuifanikisha AFCON 2027," amesema Dkt. Nsekela.

Mbali na ahadi hiyo, Dkt. Nsekela ameipongeza Wizara kwa namna ilivyojipanga katika kutoa huduma na elimu kwa wananchi kupitia maonesho hayo, akieleza kuwa ushiriki wa taasisi zote chini ya wizara hiyo umeongeza ufanisi wa utoaji huduma.

"Hii ni wizara inayogusa sekta nyingi muhimu. Mmefanya vizuri kushiriki maonesho haya pamoja na taasisi zenu zote ili mwananchi anapohitaji msaada asikwame, bali apate suluhisho kwa haraka na urahisi," ameongeza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu wa Wizara hiyo, Bi. Savera Salvatory, ameishukuru Benki ya CRDB kwa ahadi ya ushirikiano na kuipongeza kwa mchango wake katika maendeleo ya sekta ya michezo na maeneo mengine ya kijamii.

Bi. Savera amesema wizara itaendelea kuboresha huduma zake kwa wananchi na kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha sekta zilizo chini yake zinapiga hatua zaidi.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026.
Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments




Dodoma
Tume ya Madini imeendelea kuimarisha ukaguzi wa migodi nchini kupitia Kurugenzi ya Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kwa lengo la kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinafanyika kwa usalama, ufanisi na kwa kuzingatia uhifadhi wa mazingira, hatua inayolenga kuhakikisha rasilimali za madini zinanufaisha kizazi cha sasa na kijacho.

Akizungumza Juni 19, 2026, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, Afisa Mkaguzi wa Migodi wa Tume ya Madini, Rose Mika, amesema ukaguzi wa mara kwa mara unaofanyika katika migodi mikubwa, ya kati na midogo unalenga kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinaendeshwa kwa kuzingatia Sheria ya Madini pamoja na Kanuni za Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira za mwaka 2010.

Amesema ukaguzi huo husaidia kubaini mapema changamoto zinazoweza kuhatarisha usalama wa wafanyakazi na wananchi wanaoishi jirani na maeneo ya migodi, hivyo kuwezesha hatua stahiki kuchukuliwa kabla ya kutokea kwa madhara.

Rose amesema Tume ya Madini pia inaendelea kusimamia utekelezaji wa mipango ya usimamizi wa mazingira, ikiwemo kudhibiti uchafuzi wa maji, hewa na ardhi pamoja na kuhakikisha taka zinazotokana na shughuli za uchimbaji zinahifadhiwa na kushughulikiwa kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa.

Aidha, amesema Tume inafuatilia utekelezaji wa mipango ya kufunga migodi (Mine Closure Plans) ili kuhakikisha maeneo yaliyokwishafanyiwa uchimbaji yanarejeshwa katika hali salama na yenye tija baada ya shughuli hizo kukamilika.

Kwa mujibu wa Rose, hatua hiyo ni muhimu katika kuhakikisha ukuaji wa sekta ya madini unaenda sambamba na uhifadhi wa mazingira na ustawi wa jamii zinazozunguka maeneo ya migodi.

Mbali na ukaguzi wa migodi, Tume ya Madini inaendelea kusimamia matumizi ya baruti katika shughuli za uchimbaji, ikiwemo utengenezaji, uingizaji, usafirishaji na biashara yake kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizopo.

Katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, Tume ya Madini inaendelea kutoa elimu kwa wananchi na wadau kuhusu fursa mbalimbali zilizopo katika sekta hiyo na kuwahamasisha kushiriki katika shughuli za utafiti, uchimbaji, uchenjuaji, biashara ya madini pamoja na utoaji wa huduma kwenye migodi ya madini kwa kuzingatia matakwa ya sheria, ili kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments

Na Oscar Nkembo
Msimamizi wa Dawati la Ukaguzi wa Kemikali wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali Ofisi ya Kanda ya Kati, Suitbert Sinduhije amesema Mamlaka imedhibiti Kemikali ya Sulphur iliyomwagika eneo la Mikumi na amewataka Madereva kuzingatia mafunzo wanayopata huku akiwasihi Wananchi kutoa taarifa kwa Mamlaka pindi ajali za Kemikali zinapotokea.

Sinduhije amesema hayo Juni 18, 2026 baada ya kukamilisha zoezi la kuiondoa Kemikali iliyomwagika ikiwa inasafirishwa kwa njia ya barabara ambapo alisema.

“Tumepata Taarifa kuhusu Kemikali hii iliyomwagika tumefika kwaajili ya kudhibiti na hali ni shwari athari ndogo ndogo zilizosababishwa na vumbi la Kemikali hiyo ni kusikia muwasho mwishili na usoni ambapo kunywa maji mengi na kuosha eneo lililofikiwa na Kemikali inamuweka mwananchi salama kabisa, nawasihi Madereva kuzingatia mafunzo ambayo Mkemia Mkuu amewapa, pia nawaomba wananchi waendelee kutupa taarifa pindi matukio haya yanapotokea ili yakabiliwe kwa wakati bila madhara kwa wananchi” alisema Sinduhije.

Aggrey Kinzilizi na Yusta Komba ni wakazi wa Mikumi wanaofanya Biashara kando ya Barabara wamesema wamesikia muwasho sehemu zao za mwili baada ya vumbi la Kemikali hiyo kuwafikia.

“Magari yanapopita yanatibua ile Kemikali inakuja huku kiukweli ni kuwashwa mwanzo mwisho, Mkemia amefika akatueleza tunawe kwa maji mengi kwa sasa hamna tena ule muwasho, tunaomba hawa wanaosafirisha Kemikali wasiwe peke yao Mkemia wa Serikali awe anawafuatilia kwa nyuma ili changamoto hizi zisitukute” walisema wakazi hao wa Mikumi.
 
Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments

 

Posted by MROKI On Friday, June 19, 2026 No comments

June 18, 2026

Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, akizungumza wakati akifungua Kikao cha Jukwaa la Taifa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa kilicholenga kupitia na kuthibitisha Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa, Mwongozo wa Uendeshaji na Uratibu wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa, pamoja na Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS) jijini Dodoma.







Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SERIKALI imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kuongeza uwezo wa kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa, kufuatia kuongezeka kwa matukio yanayochochewa na mabadiliko ya tabianchi pamoja na vihatarishi vingine vya asili na kijamii.

Hayo yameelezwa leo Juni 18, 2026 jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, wakati akifungua Kikao cha Jukwaa la Taifa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa kilicholenga kupitia na kuthibitisha Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa, Mwongozo wa Uendeshaji na Uratibu wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa, pamoja na Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS).

Brigedia Jenerali Ndagala amesema kuwa katika miaka ya hivi karibuni Tanzania imekumbwa na matukio mbalimbali ya maafa yakiwemo mafuriko, ukame, maporomoko ya ardhi, upepo mkali, magonjwa ya mlipuko na ajali mbalimbali, hali ambayo imeathiri maisha ya wananchi, miundombinu, mazingira na shughuli za kiuchumi.

“Kwa kuzingatia hali hiyo, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu imeendelea kuimarisha sera, mifumo, mikakati, mipango na nyenzo mbalimbali za usimamizi wa maafa ili kuhakikisha hatua zote za kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali baada ya maafa zinafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya Mwaka 2022,” amesema.

Amesema kikao hicho ni hatua muhimu katika kuimarisha uratibu wa kitaifa wa usimamizi wa maafa kwa kuwa kinahusisha uthibitishaji wa nyenzo tatu muhimu zitakazochangia uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi wakati wa maafa na baada ya maafa.

Kwa mujibu wa Brigedia Jenerali Ndagala, Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa utaweka mfumo wa pamoja wa kitaifa wa kupanga na kuratibu shughuli za urejeshaji baada ya maafa, huku Mwongozo wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa ukiboresha utaratibu wa utoaji wa misaada ya fedha kwa waathirika. Aidha, Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS) utaimarisha ukusanyaji, uchambuzi, uhifadhi na matumizi ya taarifa za maafa kwa ajili ya kufanya maamuzi sahihi na kwa wakati.

“Nyenzo hizi zina mchango mkubwa katika utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya Mwaka 2022 kwa kuimarisha usimamizi wa taarifa, uratibu wa wadau, utoaji wa misaada na shughuli za urejeshaji hali baada ya maafa. Vilevile, zinachangia utekelezaji wa Mfumo wa Sendai wa Kupunguza Hatari za Maafa kwa kuimarisha uelewa wa hatari za maafa, usimamizi wa vihatarishi, uwekezaji katika ustahimilivu na kuimarisha hatua za kujiandaa na kujenga upya kwa ubora zaidi baada ya maafa,” amesisitiza.

Ameeleza kuwa mafanikio yanayoendelea kupatikana katika sekta ya usimamizi wa maafa nchini yanatokana na ushirikiano madhubuti kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, mashirika ya Umoja wa Mataifa, sekta binafsi na asasi za kiraia.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), Bi. Judith Bihondwa, amesema shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha uwezo wa jamii kukabiliana na maafa pamoja na kujenga ustahimilivu dhidi ya majanga mbalimbali.

Amesema ushirikiano huo utaendelea kulenga kuimarisha mifumo ya maandalizi, mwitikio na urejeshaji hali baada ya maafa kwa kuzingatia makundi yote ya jamii, hususan watoto na watu walio katika mazingira hatarishi.

Kikao hicho kimewakutanisha wadau mbalimbali wa usimamizi wa maafa kutoka taasisi za Serikali, mashirika ya Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na wadau wa maendeleo kwa lengo la kujadili na kuthibitisha nyenzo zitakazochangia kuimarisha usimamizi wa maafa na kuongeza ustahimilivu wa jamii nchini.
Posted by MROKI On Thursday, June 18, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Bw. Ramadhan Kailima, amepongeza ufanisi na uwazi wa Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja unaosimamiwa na Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja, akieleza kuwa mfumo huo umechangia kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya Serikali na kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini.

Bw. Kailima alitoa pongezi hizo Juni 18, 2026 alipotembelea banda la PBPA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.

Akizungumza baada ya kupata maelezo kuhusu utekelezaji wa mfumo huo, alisema kuwa umejengwa katika misingi ya uwazi na ushindani, jambo linalosaidia kupunguza gharama za uagizaji wa mafuta na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa sekta hiyo muhimu kwa uchumi wa nchi.

Akitoa ufafanuzi kwa mgeni huyo, Mkaguzi wa Mafuta wa PBPA, Bw. Issa Mwitazy, alisema kuwa katika mfumo wa uagizaji mafuta kwa pamoja, ushindani hujikita katika gharama za usafirishaji wa mafuta (Premium).

Alieleza kuwa wazabuni hushindanishwa kwa kuwasilisha bei za usafirishaji wa bidhaa za petroli, dizeli na mafuta ya taa, ambapo mzabuni mwenye gharama nafuu zaidi hupatiwa zabuni husika.

“Utaratibu huu umetuwezesha kuhakikisha upatikanaji wa mafuta ya kutosha nchini wakati wote na wakati huohuo kuipa Serikali taarifa sahihi za kiasi cha mafuta na hivyo kuwezesha ukusanyaji wa mapato yatokanayo na biashara ya mafuta,” alisema.

Aliongeza kuwa mikataba ya uagizaji wa mafuta husainiwa mapema kabla ya bidhaa kuwasili nchini, jambo linaloiwezesha Serikali kufanya makadirio sahihi ya mapato yatokanayo na sekta hiyo.

Kwa mujibu wa Mwitazy, mafanikio ya mfumo huo yameifanya PBPA kuwa kitovu cha huduma za uagizaji mafuta kwa nchi kadhaa za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, zikiwemo Malawi, Rwanda, Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ambazo huleta mahitaji yao kupitia mfumo wa uagizaji wa mafuta kwa pamoja.

Ziara ya Bw. Kailima katika banda la PBPA ni sehemu ya shughuli za Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayolenga kuonesha mafanikio, huduma na ubunifu unaotekelezwa na taasisi za umma katika kuwahudumia wananchi na kuchangia maendeleo ya taifa.

Posted by MROKI On Thursday, June 18, 2026 No comments

Afisa Mwandamizi wa Idara ya Usimamizi wa Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Bi. Anne Swila, akitoa elimu kwa wananchi kuhusu Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025, walipotembelea Banda la Maonesho la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yenye Kaulimbiu ya “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu”, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.

Msimamizi wa Fedha Mkuu, Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha, Bi. Grace Samwel, akitoa elimu kwa mwananchi kuhusuusimamizi wa fedha binafsi, walipotembelea Banda la Maonesho la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yenye Kaulimbiu ya “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu”, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.

Mchumi Mkuu wa Idara ya Ubia Kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, Wizara ya Fedha, Bi. Josephina Buhili, na Mchumi Daraja la Kwanza wa Idara ya Ubia Kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, Bi. Anastazia Amandi, wakitoa elimu kwa wananchi kuhusu, majukumu, mipango na malengo pia miradi mbalimbali iliyotekelezwa na Idara hiyo, walipotembelea Banda la Maonesho la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yenye Kaulimbiu ya “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu”, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.



Mchumi Mwandamizi wa Idara ya Bajeti, Wizara ya Fedha, Bi. Consolatha Komba, akifafanua kwa wananchi kuhusu, vipaumbele na utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, walipotembelea Banda la Maonesho la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yenye Kaulimbiu ya “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu”, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.

Maafisa wa Wizara ya Fedha wakiendelea kutoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, kuhusu majukumu yanayotekelezwa na wizara, wakati wananchi hao walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, yenye kauli mbiu ‘Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Maendeleo Endelevu’, yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.
**************
Na. Jordan Mbwambo, WF, Dodoma.
Serikali imeanza kutumia Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025, hatua inayolenga kufungamanisha na kuboresha usimamizi wa shughuli za Mnyororo wa Ugavi nchini ili kuongeza ufanisi, matumizi bora ya rasilimali na kupata thamani halisi ya fedha za umma.

Hayo yalibainishwa na Afisa Mwandamizi wa Idara ya Usimamizi wa Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Bi. Anne Swila, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Maonesho la Wizara ya Fedha, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026, yenye Kaulimbiu ya “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu”, yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.

Alisema kuwa Sera hiyo inalenga maeneo sita makuu, yakiwemo Ununuzi wa Umma, Ugomboaji na Uondoshaji wa Mizigo ya Serikali, Upokeaji na Urejeshaji, Utunzaji na Uhifadhi, Usambazaji, pamoja na uhifadhi wa Mazingira na Utawala Bora.

‘‘Kwa miaka mingi tumekuwa na sheria nzuri za ununuzi, lakini hazikuwa zimeunganishwa kwa msingi mmoja wa kisera, Sera hii sasa inakwenda kuziba pengo hilo na kuhakikisha kila shilingi ya umma inatumika kwa thamani yake halisi, kwa kuhakikisha mikakati ya utekelezaji inajumuisha kuimarisha udhibiti wa bei, uchaguzi wa wazabuni, na kuendeleza Kada ya Ununuzi na Ugavi Serikalini " alieleza Bi. Swila.

Alisisitiza kuwa ushiriki wa wananchi katika utekelezaji wa Sera hii itaongeza ushindani na kuwapa fursa wazabuni wazawa, sekta binafsi na makundi maalum ya kijamii, hatua itakayowezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika uchumi na kuchochea ukuaji wa ajira.

Bi. Swila alisema Sera hiyo pia inatarajiwa kuimarisha matumizi ya mifumo ya kielektroniki na rasilimali za ndani, kuvutia uwekezaji katika miundombinu ya uhifadhi na usambazaji, na hivyo kuifanya sekta ya mnyororo wa ugavi kuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

‘‘Miongoni mwa mafanikio yanayotarajiwa ni kuongezeka kwa ufanisi, udhibiti bora wa gharama, kuimarika kwa ubora wa huduma kwa wananchi, ongezeko la ajira, uzingatiaji wa uhifadhi wa mazingira, na kuwa na mfumo jumuishi wa ufuatiliaji na tathmini utakaohakikisha utekelezaji wa sera unaleta tija iliyokusudiwa’’, alifafanua Bi Swila.

Aidha, alisema kuwa Sera hiyo itawezesha kuwepo kwa mfumo jumuishi wa ufuatiliaji na tathmini, hatua itakayoifanya sekta ya mnyororo wa ugavi kuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii na kuchangia kupunguza umasikini nchini.

Sera hiyo inatarajiwa kutekelezwa kwa kipindi cha miaka 10 kuanzia mwaka 2026 hadi 2036 na tathmini ya utekelezaji itafanyika kila baada ya miaka mitano ya utekelezaji.
Posted by MROKI On Thursday, June 18, 2026 No comments




Tume ya Madini imesema kuanzishwa kwa masoko ya madini na vituo vya ununuzi wa madini nchini kumeongeza uwazi katika biashara ya madini na kusaidia kudhibiti utoroshaji wa rasilimali hiyo, hatua iliyochangia kuongezeka kwa mapato ya Serikali.

Akizungumza leo katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, Afisa wa Tume ya Madini kutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Biashara ya Madini, Ibrahim Akyoo, amesema mfumo huo umewezesha wachimbaji na wafanyabiashara kuuza madini kupitia njia rasmi na hivyo kuimarisha usimamizi wa sekta hiyo.

Amesema kwa sasa nchini kuna masoko ya madini 44 na vituo vya ununuzi wa madini 120 vinavyorahisisha biashara ya madini na kuhakikisha Serikali inapata mapato stahiki yatokanayo na rasilimali hizo.

Akyoo amesema miongoni mwa majukumu ya Kurugenzi ya Ukaguzi na Biashara ya Madini ni kusimamia biashara ya madini nchini, kuhakikisha ushiriki wa Watanzania katika sekta hiyo unaongezeka, kudhibiti utoroshaji wa madini, kufanya ukaguzi wa fedha na kodi pamoja na kutoa huduma za kimaabara kwa wadau wa sekta hiyo.

Amesema kupitia maonesho hayo, Tume ya Madini inaendelea kutoa elimu kwa wananchi na wadau kuhusu fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya madini, zikiwemo biashara ya madini, uchimbaji, uongezaji thamani, utoaji wa huduma na shughuli nyingine katika mnyororo wa thamani wa sekta hiyo.

Amesema hatua hizo zinaendelea kuifanya sekta ya madini kuwa miongoni mwa sekta muhimu zinazochangia ukuaji wa uchumi na maendeleo ya taifa.




Posted by MROKI On Thursday, June 18, 2026 No comments



Dodoma – “Sasa najua ni nini ninapaswa kuangalia ninapojaza mafuta, kununua sukari au hata ninaponunua gesi ya kupikia.” Ni kauli ya Bw. Bilson Vedastus, mmoja wa wananchi waliotembelea banda la Wakala wa Vipimo (WMA) katika Maonesho ya Kitaifa ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea Viwanja vya Chinangali Park, Dodoma.

Banda hilo limekuwa kitovu cha msongamano siku ya tatu ya maonesho, Juni 18, 2026 huku wananchi wakijitokeza kwa wingi kujifunza jinsi Serikali kupitia WMA inavyohakikisha kila kipimo kinachotumika kibiashara na katika huduma ni sahihi. Maonesho yalianza tarehe 16 Juni na yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 23 Juni 2026.

Baada ya kupata maelezo ya hatua kwa hatua kutoka kwa wataalamu, wengi wameahidi kuwa mabalozi wa Wakala wa Vipimo katika maeneo yao. 
“Tumeona jinsi pampu, mizani na vifaa vingine vinavyohakikiwa kuhakikisha vinapima kwa usahihi. Sasa hatuwezi kukaa kimya tukiona mteja anadhulumiwa. Tutawaeleza jirani zetu na kuripoti udanganyifu popote tutakapouona,” alisema Bi. Asha Siyaya.

Wataalamu wa WMA, Albogast Kajungu, Mbwana Amani na Said Ibrahim waliwaeleza wananchi kuwa uhakiki wa vipimo unagusa sekta zote zinazowahusu moja kwa moja kila siku. Katika sekta ya mafuta, pampu zote huhakikiwa na kuwekewa stika ya uthibitisho. Sokoni na madukani, mizani inayotumika kupimia sukari, mchele na mboga hufanyiwa ukaguzi ili mteja asipoteze pesa.

Sekta ya maji na umeme nayo haikuachwa nyuma. Mita za maji na umeme zinazotumika nyumbani na kwenye biashara ndogo huhakikiwa na kuthibitishwa ili kuhakikisha mteja analipia matumizi halisi na si makadirio au idadi isiyo sahihi. Vile vile mitungi ya gesi ya kupikia, bidhaa zilizofungashwa kama unga na sabuni, pamoja na mizani  za barabarani zote huhakikiwa mara kwa mara.

Akizungumza na Waandishi wa Habari, Meneja Mawasiliano wa Wakala wa Vipimo, Bi Veronica Simba amesema lengo ni moja: kuhakikisha mwananchi anapata thamani kamili ya kila shilingi anayolipa, na amewahamasisha wananchi wengi zaidi kutembelea banda hilo kabla ya maonesho kuhitimishwa.
Posted by MROKI On Thursday, June 18, 2026 No comments

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka watendaji wa Wizara ya Maji pamoja na Wakuu wa Mikoa wasimamie vizuri mitambo ya uchimbaji visima ili iweze kufanya kazi iliyokusudiwa.

Amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alinunua mitambo ya uchimbaji wa visima hivyo watendaji wachukue hatua na waache kufanya kazi kwa mazoea.

"Nielekeze Wakuu wa Mikoa yote pamoja na wizara, kusimamia ili mitambo ile iweze kufanya kazi iliyokusudiwa, ni kweli kuna baadhi ya maeneo ya tunaendelea endelea na ile tabia ya business as usual, sasa ili kufikia matokeo ya Dira 2050, ni lazima tufanye kazi business unusual, tuache kufanya kazi kwa kuchukulia vitu kimazoea mazoea", Ameelekeza Waziri Mkuu.

Dkt. Mwigulu ametoa maelekezo hayo leo (Alhamisi Juni 18, 2026) Bungeni jijini Dodoma katika kipindi cha Maswali kwa Waziri Mkuu wakati akijibu swali la Mbunge wa Kwimba, Cosmas Bullala.

Mbunge huyo alitaka kujua kauli ya Serikali kuhusu ufanisi wa mitambo hiyo, ambapo Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema mitambo hiyo inaendelea kuchimba visima katika maeneo mbalimbali nchini. Ambapo kwa sasa unatekelezwa mpango wa uchimbaji visima 900.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Mwigulu amesema Serikali inatarajia kuanza kuwalipa kifuta jasho askari waliojitolea katika vita dhidi ya Idd Amin wa Uganda mwaka 1978-79.

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu ameeleza hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Njombe, Deodatus Mwanyika aliyetaka kujua ni lini Serikali itawalipa kifuta jasho askari hao, ambapo Waziri Mkuu Mwigulu amesema tayari Serikali imefanya mabadiliko ya Sheria ambapo sasa askari hao wanatambulika kisheria kutokana na hapo mwanzo kutotambuliwa.

“Mheshimiwa Spika, Sheria za zamani zilikuwa haziwatambui wapiganaji wale, hasa hasa wapiganaji waliopata mafunzo ya muda mfupi, hivi tunavyoongea, kupitia tangazo la Serikali la mwezi wa 6, mwaka 2025, kuhusu mabadiliko ya Sheria ya mafao ya veterani, sasa imeshawatambua wapiganaji hao”, Amesema Dkt. Mwigulu.

“Mheshimiwa Spika, wapiganaji hao wataanza kulipwa na watalipwa kwa kuwa sasa hakuna kikwazo cha kisheria ambacho kilikuwa kinawakwamisha, na kile cha uhakiki, kwani wapiganaji hao wameshahakikiwa”, Amesisitiza Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu.

Posted by MROKI On Thursday, June 18, 2026 No comments
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge na Kiongozi wa kamati ya ukaguzi wa mradi wa ujenzi kutoka Jamhuri ya Watu wa China Yang Ling wakionesha hati ya makubaliano ya ujenzi wa hospitali mpya moyo mara baada ya kusaini hati hiyo jana katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge na Kiongozi wa kamati ya ukaguzi wa mradi wa ujenzi kutoka Jamhuri ya Watu wa China Yang Ling wakisaini hati ya makubaliano ya ujenzi wa hospitali mpya moyo jana katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na wafanyakazi wa JKCI pamoja na wataalamu wa mradi wa ujenzi kutoka Jamhuri ya Watu wa China wakati wa hafla fupi ya kusaini hati ya makubaliano ya ujenzi wa hospitali mpya moyo jana katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wataalamu wa mradi wa ujenzi kutoka Jamhuri ya Watu wa China wakisikiliza wakati wa hafla fupi ya kusaini hati ya makubaliano ya ujenzi wa hospitali ya moyo iliyofanyika jana  katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akipokea zawadi kutoka kwa Kiongozi wa kamati ya ukaguzi wa mradi kutoka Jamhuri ya Watu wa China Yang Ling mara baada ya hafla fupi ya kusaini hati ya makubaliano ya ujenzi wa hospitali mpya moyo iliyofanyika jana katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimkabidhi zawadi Mkurugenzi wa Kitengo cha Afrika ya Kusini na Mashariki, Wakala wa Ushirikiano wa Kimataifa wa Kiuchumi (AIEC) chini ya Wizara ya Biashara ya China Li Qing wakati wa hafla fupi ya kusaini hati ya makubaliano ya ujenzi wa hospitali mpya ya moyo iliyofanyika jana katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Kitengo cha Afrika ya Kusini na Mashariki, Wakala wa Ushirikiano wa Kimataifa wa Kiuchumi (AIEC) na wataalamu wa mradi wa ujenzi kutoka Jamhuri ya Watu wa China  wakati wa hafla fupi ya kusaini  hati ya makubaliano ya ujenzi wa hospitali mpya moyo iliyofanyika jana katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
***************
Na Mwandishi maalum – Dar es Salaam
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Wataalamu kutoka China wasaini hati ya makubaliano ujenzi wa hospitali mpya ya moyo itakayoleta mabadiliko makubwa katika utoaji wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi kwa wagonjwa wa moyo nchini.
 
Hati hiyo imesainiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge pamoja na Kiongozi wa Kamati ya Ukaguzi wa Mradi kutoka Jamhuri ya Watu wa China Yang Ling na kuahidi kuanza mchakato wa ujenzi huo mara baada ya taratibu kukamilika.
 
Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji wa saini Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema hospitali hiyo itasaidia kuongeza upatikanaji wa huduma za uchunguzi na matibabu ya kibingwa, pamoja na kuimarisha mazingira ya kazi kwa wataalamu wa afya wanaofanya kazi katika Taasisi hiyo.
 
“Mradi huu ni hatua muhimu sana katika kuimarisha uwezo wetu wa kutoa huduma za matibabu ya moyo kwa viwango vya juu zaidi na kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma bora kwa wakati”, alisema Dkt. Kisenge
 
Dkt. Kisenge alisema mradi huo ni sehemu ya juhudi ya Serikali ya awamu ya sita ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha sekta ya afya na kupunguza vifo vinavyotokana na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo.
 
******************************************************************************************
 
Caption
 
Picha 1: 
 
 
 
Picha 5: 
Posted by MROKI On Thursday, June 18, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo