Nafasi Ya Matangazo

September 08, 2026

 Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi Tiba na Uhakiki Ubora wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Hemed Myanza akiwaeleza wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi hatua zilizofikiwa na taasisi hiyo katika mchakato wa kupata ithibati ya ubora wa huduma  wakati wa kikao cha sita cha baraza hilo kilichofanyika hivi karibuni katika Hoteli ya Stella Maris iliyopo Bagamoyo mkoani Pwani. Picha na ORCI
Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) wakimsikiliza Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi Tiba na Uhakiki Ubora, Hemed Myanza wakati akiwaeleza hatua zilizofikiwa katika mchakato wa kupata ithibati ya ubora wa huduma wakati wa kikao cha sita cha baraza hilo kilichofanyika hivi karibuni katika Hoteli ya Stella Maris, Bagamoyo mkoani Pwani.


Na Mwandishi Maalumu – Bagamoyo
Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) imeanza maandalizi ya kupata ithibati ya ubora wa huduma ikiwa tayari imefanya tathmini katika maeneo mbalimbali na kubaini mapungufu yanayohitaji kufanyiwa kazi ili kufikia viwango vya ubora vinavyotambulika kimataifa.

Hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za ORCI za kuimarisha mifumo ya utoaji huduma, kuongeza usalama wa wagonjwa na kuhakikisha huduma zinazotolewa katika taasisi hiyo zinaendana na viwango vya ubora vinavyokubalika kimataifa.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi Tiba na Uhakiki Ubora wa ORCI, Hemed Myanza wakati akieleza hatua zilizofikiwa katika mchakato wa kupata ithibati, alipokuwa akizungumza na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi katika kikao cha sita cha baraza hilo kilichofanyika hivi karibuni katika Hoteli ya Stella Maris wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani.

Myanza alisema  katika maandalizi hayo ORCI imeweka mkazo katika kuhakikisha Taratibu za Kawaida za Uendeshaji (Standard Operating Procedures – SOPs) zinawekwa na kutumika katika maeneo yote ya taasisi ili kuwepo kwa mifumo na viwango vinavyofanana katika utoaji wa huduma.

Alisema hatua hiyo inalenga kuhakikisha kila eneo la huduma linafanya kazi kwa kuzingatia taratibu na viwango vilivyowekwa jambo litakalosaidia kuongeza ufanisi, usalama na ubora wa huduma zinazotolewa kwa wagonjwa.

Aidha Myanza alisema  ORCI tayari imefanya mazungumzo na bodi zinazohusika na ithibati za kimataifa hatua inayolenga kusaidia taasisi kubaini chombo cha ithibati itakachoshirikiana nacho pamoja na kuelekezwa hatua zinazopaswa kuchukuliwa ili kufikia kiwango cha kupata ithibati ya kimataifa.

“Tumeshatoa elimu kwa wafanyakazi na tumeweza kuona maeneo ambayo tunahitaji kuyafanyia maboresho. Tumekwenda katika maeneo yote ya kitabibu na yasiyo ya kitabibu ili kuhakikisha watumishi wanakuwa na uelewa mmoja kuhusu viwango vinavyotakiwa kimataifa katika utoaji wa huduma”,  alisema Myanza.

Alisema mchakato huo haujajikita katika maeneo ya kitabibu pekee bali unahusisha pia maeneo yasiyo ya kitabibu ili kuhakikisha watumishi wote wanakuwa na uelewa wa pamoja kuhusu viwango vinavyopaswa kuzingatiwa katika utoaji wa huduma.

Myanza alisema  huduma kwa wateja (customer care) ni miongoni mwa maeneo yanayopewa kipaumbele katika mchakato huo, ambapo ORCI inalenga kuhakikisha watumishi wanakuwa na uelewa na uwezo wa kutoa huduma bora, salama na zenye viwango vya juu vinavyoweza kuendana na viwango vya kimataifa.

Alisema  tathmini zilizofanyika katika maeneo mbalimbali ya taasisi zimewezesha kubaini mapungufu yanayohitaji kufanyiwa kazi huku hatua za maboresho zikiendelea ili ORCI iweze kufikia viwango vinavyohitajika.

“Lengo la ithibati ni kuhakikisha taasisi inatambuliwa kwa kuzingatia viwango vya ubora vinavyotakiwa. Tumefanya tathmini na kubaini maeneo ambayo tunahitaji kuyafanyia maboresho ili kufikia viwango hivyo vya kimataifa”,  alisema.

Myanza alisema kupata ithibati hiyo kutasaidia kuongeza imani na uaminifu wa wagonjwa kwa ORCI kwa kuwa utambuzi huo utaonesha kuwa taasisi inatoa huduma kwa kuzingatia viwango vinavyotambulika vya ubora na usalama.

“Tunatarajia ithibati hii itaongeza imani na uaminifu wa wagonjwa kwa sababu watakuwa na uhakika na kuthamini zaidi huduma wanazozipata katika taasisi yetu”, alisema.

Kwa upande wao wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi waliupongeza uongozi wa ORCI kwa hatua mbalimbali za maboresho yanayolenga kuongeza ubora wa huduma na kuimarisha mazingira ya kazi huku wakisisitiza umuhimu wa kuunganisha uwekezaji katika miundombinu na vifaa vya kisasa na mifumo madhubuti ya utoaji wa huduma bora.

Naye Wamoja Mbonde ambaye ni Msimamizi wa Kumbukumbu za Afya na Mjumbe wa Baraza hilo alisema  kupata ithibati kutakuwa hatua muhimu katika kuimarisha ubora wa huduma zinazotolewa na ORCI kwa kuwa kutaiwezesha taasisi kuwa na mifumo na viwango vinavyofanana katika maeneo mbalimbali ya utoaji huduma.

Alisema  ithibati hiyo pia itasaidia kuimarisha uwajibikaji wa watumishi, kuzingatia taratibu na viwango vilivyowekwa pamoja na kuhakikisha huduma zinazotolewa kwa wagonjwa zinaendelea kuboreshwa kwa kuzingatia mahitaji na usalama wao.

“Uwepo wa ithibati utasaidia kuhakikisha tunafanya kazi kwa kuzingatia viwango vilivyowekwa kwani kila mfanyakazi atavituata kwa vitendo, wagonjwa wataona tofauti katika huduma wanazopata. Hii itaongeza imani yao na kuifanya ORCI kuwa taasisi inayozingatia ubora katika kila hatua ya huduma”, alisema Mbonde.

Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani na Mjumbe wa Baraza hilo Faraja Kiwanga alisema mchakato wa kupata ithibati unapaswa kwenda sambamba na maboresho ya miundombinu, vifaa na mashine za kisasa yanayoendelea katika  taasisi hiyo ili uwekezaji unaofanyika uweze kuleta matokeo yanayotarajiwa kwa wananchi.

Dkt. Faraja alisema  maboresho hayo yakitekelezwa sambamba na mifumo madhubuti ya ubora na watumishi kuzingatia viwango vilivyowekwa, yataendelea kuongeza uwezo wa ORCI katika kutoa huduma bora, salama na zenye ufanisi kwa wagonjwa kutoka ndani na nje ya nchi.

Kupatikana kwa Ithibati kutaifanya  ORCI kuwa na mifumo thabiti ya ubora katika maeneo yote ya utoaji wa huduma,  kuongeza uwajibikaji wa watumishi, usalama wa wagonjwa na imani ya wananchi katika huduma zinazotolewa na taasisi hiyo.
Posted by MROKI On Tuesday, September 08, 2026 No comments




Na Mwandishi Maalumu - Dar es Salaam 
Watoto 100 wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kuchangiwa gharama za matibabu kupitia marathon iliyoandaliwa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) msimu wa tatu inayotarajiwa kufanyika mwezi Novemba mwaka huu.

Marathon hiyo yenye kauli mbiu “Hatua Yako Inaokoa Maisha” ni ishara ya mshikamano wa jamii katika kulinda na kuokoa maisha ya watoto wanaotoka katika familia zisizokuwa na uwezo wa kugharamia matibabu ya moyo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa marathon hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema zaidi ya watoto 1,500 wenye magonjwa ya moyo wako katika foleni ya kusubiria huduma za upasuaji wa moyo huku wengi wao wakitoka katika familia zenye uwezo mdogo wa kumudu gharama za matibabu.

Dkt. Kisenge alisema hali hiyo imeifanya taasisi hiyo kuitegemea Serikali na wadau mbalimbali ili kuhakikisha watoto wenye matatizo ya moyo wanapata matibabu kwa wakati na kuokoa maisha yao.

“Tunapokea watoto wengi wenye matatizo ya moyo. Takwimu zinaonesha kuwa kati ya watoto 100 wanaozaliwa, takribani wawili huzaliwa wakiwa na matatizo ya moyo”, alisema Dkt. Kisenge.

Dkt Kisenge alisema Serikali imeendelea kutoa msaada kwa watoto wenye magonjwa ya moyo hasa kwa kuzingatia kuwa sehemu kubwa ya wagonjwa hao hutoka katika familia zenye uwezo mdogo wa kifedha na hivyo kushindwa kumudu gharama za matibabu.

“Tunaishukuru TPDC kwa kuendelea kushiriki katika kusaidia gharama zamatibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo kupitia mpango wake wa kuchangisha fedha, mwaka 2022 TPDC ilichangia shilingi milioni 100 kwa ajili ya matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo, huku mwaka 2025 ikichangia shilingi milioni 50”,

“Tunawaomba wananchi wajitokeze kwa wingi kushiriki mbio hizi. Zaidi ya kusaidia watoto wenye magonjwa ya moyo, kushiriki mbio hizi ni sehemu ya kufanya mazoezi, kujenga afya bora na hatimaye kuokoa maisha”, alisema Dkt. Kisenge.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Derick Moshi alisema afya ni miongoni mwa nguzo muhimu katika utekelezaji wa majukumu ya kampuni hiyo, hivyo ushiriki wao katika kusaidia sekta ya afya ni sehemu ya wajibu wao kwa jamii.

“Kaulimbiu ya TPDC marathon msimu wa tatu inatukumbusha kuchukua hatua, kuunganisha nguvu na kutumia nafasi tulizonazo kujali maisha ya wengine”, alisema Moshi.

Moshi alisema mbio hizo zitakuwa jukwaa la kuunganisha nguvu ya michezo, dhamira ya kijamii na ushiriki wa wadau mbalimbali katika kuchangisha fedha za kuboresha huduma za matibabu kwa watoto wenye magonjwa ya moyo.

“Tunathamini kuona watu wanakuwa na afya njema na wanaishi, jambo la afya linalowezekana kufanyika leo lifanyike leo lisubiri kesho”, alisema Moshi.

Moshi alisema ushiriki wa TPDC katika kusaidia watoto wenye matatizo ya moyo si jambo jipya bali ni mwendelezo wa jitihada za kampuni hiyo za kuirudishia jamii kupitia shughuli za uwajibikaji kwa jamii.

Naye Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati Mussa Mussa aliwataka waandishi wa habari kutumia nafasi yao kuelimisha na kuhamasisha jamii kuhusu TPDC Marathon 2026 ili kuongeza ushiriki wa wananchi na hatimaye kufanikisha lengo la kuwasaidia watoto wenye magonjwa ya moyo.

Mussa alisema kushiriki katika mbio hizo kuna faida mbili ikiwemo kuchangia katika kuokoa maisha ya watoto wenye matatizo ya moyo na kuimarisha afya za washiriki wenyewe.

“Naipongeza TPDC kwa kuanzisha na kuendeleza mpango huo, Wizara ya Nishati inafurahia kuona kampuni hii ikishiriki katika jambo lenye manufaa kwa jamii, tunatamani mpango huu uwe uendelevu”, alisema Mussa.
Posted by MROKI On Tuesday, September 08, 2026 No comments

September 07, 2026

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi ameshiriki maziko ya Marehemu Hafidh Ameir Hassan, ambaye ni mwenza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yaliyofanyika Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, leo tarehe 07 Septemba 2026.
 
Maziko hayo yamehudhuriwa na Viongozi Wakuu, Viongozi Wakuu Wastaafu, Viongozi wa Serikali, Dini, Vyama vya Siasa, Viongozi wa Mahakama, Bunge, Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Familia, Marafiki pamoja na waombolezaji kutoka maeneo mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.
 
Marehemu Hafidh Ameir Hassan amefariki leo, tarehe 07 Septemba 2026 katika Hospitali ya kumbukumbu ya Emilio Mzena, Zanzibar alipokuwa anapatiwa matibabu.










Posted by MROKI On Monday, September 07, 2026 No comments







Dodoma
‎Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) umeanza kutumia teknolojia ya kisasa kufanya uchunguzi wa kina wa udongo kabla ya ujenzi wa miradi ya barabara, madaraja na miundombinu mingine hatua inayolenga kuongeza usalama, ubora na uimara wa miradi ili iweze kudumu kwa muda mrefu ikiwemo kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
‎Hatua hiyo inawawezesha wataalamu kupata taarifa za kina kuhusu tabaka za udongo na miamba zilizopo chini ya ardhi hivyo kusaidia kubaini aina ya msingi na mbinu za ujenzi zinazofaa kulingana na mazingira ya eneo husika.
‎Akizungumza jijini Dodoma wakati wa ziara ya waandishi wa habari katika maabara za TARURA, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Tafiti na Udhibiti Ubora wa Wakala huo, Mhandisi Vincent Lwanda amesema uchunguzi wa udongo ni miongoni mwa hatua muhimu katika kuhakikisha miundombinu inayojengwa inakuwa salama, imara na yenye uwezo wa kudumu kwa muda mrefu.
‎Amesema TARURA imekuwa ikifanya tafiti kuhusu udongo pamoja na vifaa mbalimbali vinavyotumika katika ujenzi huku taarifa zinazopatikana kupitia vipimo hivyo zikitumika kuwawezesha wataalamu kufanya maamuzi sahihi wakati wa kupanga na kutekeleza miradi.
‎Ameeleza kuwa TARURA imewekeza takribani zaidi ya shilingi bilioni 2 katika mtambo maalumu unaotumika kuchimba ardhi na kuchukua sampuli za udongo na miamba kutoka kwenye kina cha chini ya uso wa ardhi kwa ajili ya uchunguzi wa kitaalamu.
‎"Maabara hizi hazitumiki kwa ajili ya barabara pekee, tunawakaribisha wananchi wanaofanya ujenzi waweze kuleta malighafi zao kwa ajili ya kupima ubora",  amesema.
‎Amesema matumizi ya maabara yamechangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha ubora wa barabara zinazotekelezwa na TARURA tofauti na awali ambapo baadhi ya barabara ziliharibika muda mfupi kutokana na kutofanyika kwa uchunguzi wa kutosha wa udongo na vifaa.
‎Amesema kuwa TARURA ina maabara kuu jijini Dodoma pamoja na maabara nyingine 16 katika maeneo mbalimbali nchini ambazo pia zinatoa huduma kwa wananchi, taasisi, wakandarasi na watu binafsi wanaotekeleza shughuli za ujenzi. 
‎Vilevile, amesema wakandarasi wanaotekeleza miradi ya TARURA wanatakiwa kutumia maabara katika hatua mbalimbali za ujenzi huku matokeo ya vipimo yakitumika kama sehemu muhimu ya kuthibitisha ubora wa kazi kabla ya malipo.
‎Ameongeza kuwa maabara za TARURA zimekuwa na mchango katika kukuza ujuzi wa kizazi kijacho cha wahandisi kwa kutoa fursa kwa wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali nchini kupata mafunzo kwa vitendo.
‎Kwa upande wake, Mhandisi wa Vifaa Kitengo cha Tafiti na Udhibiti wa Ubora TARURA Makao Makuu, Emmanuel Kilasi amesema TARURA imepata mtambo mpya "drilling rig" ambao unatumika kuchimba na kutoa sampuli za udongo kwa ajili ya uchunguzi wa hali ya ardhi.
‎Amesema mtambo huo una uwezo wa kuchukua sampuli za udongo kutoka kina cha mita 200 hadi 300 chini ya uso wa ardhi taarifa zinazopatikana kupitia sampuli hizo husaidia kubaini uwezo wa udongo kubeba mzigo jambo ambalo ni muhimu katika kupanga misingi ya miundombinu mikubwa kama madaraja, barabara na majengo.
‎Amesisitiza kuwa upatikanaji wa taarifa sahihi kuhusu hali ya ardhi kabla ya ujenzi ni hatua muhimu katika kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa utekelezaji au baada ya kukamilika kwa miradi huku wataalamu wakiwa na uwezo wa kuchagua teknolojia na aina ya ujenzi inayolingana na mazingira ya eneo.
‎Naye, mwanafunzi wa mwaka wa pili wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST), Vivian Mwakabaja amesema mafunzo aliyoyapata katika maabara za TARURA yamemsaidia kuunganisha maarifa anayopata darasani na utekelezaji halisi wa kazi za uhandisi ambapo mafunzo hayo yamemwezesha kujifunza namna ya kupima ubora wa udongo na kubaini uwezo wake wa kubeba mizigo.
Posted by MROKI On Monday, September 07, 2026 No comments

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi akimfariji Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kufuatia kufiwa na Mume wake, Hafidh Ameir Hassan, wakati alipofika katika makazi yake, Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, leo tarehe 07 Septemba 2026.
Posted by MROKI On Monday, September 07, 2026 No comments

Mwenza wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, Hafidh Ameir Hassan, amefariki dunia Septemba 7, 2026.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mhe. Deogratius Ndejembi, Hafidh Ameir Hassan amefariki wakati akipatiwa matibabu ya ugonjwa wa moyo Zanzibar.

Ndejembi amesema Mzee Hafidh amefikwa na umauti leo Saa mbili asubuhi akipatiwa matibabu katika Hospitlai ya Kumbukumbu ya Emilio Mzena visiwani Zanzibar.

“kwa masikitiko makubwa, nawajulisha taarifa ya kifo cha Mheshimiwa Hafidh Ameir Hassan, Mume wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kilichotokea leo tarehe saba Septemba 2026, majira ya saa mbili ya asubuhi, katika Hospitali ya kumbukumbu ya Emilio Mzena Zanzibar, alipokuwa akipatiwa matibabu ya ugonjwa wa moyo,”

“Ninatoa pole kwa Mheshimiwa Rais, familia, ndugu, jamaa na marafiki, na Watanzania wote kwa msiba huu, mpango wa mazishi unaendelea kufanyika Kizimkazi, Zanzibar,”

Marehemu Hafidh Amir Hassan na Rais Samia walifunga ndoa mwaka 1978 na kufanikiwa kupata watoto kadhaa akiwepo Naibu Waziri wa Elimu, Wanu Hafidh Amir. 

Aidha mipango ya mazishi inafanyika Kizimkazi Zanzibar nyumbani kwa marehemu ambapo taarifa zinaarifu kuwa maziko yanataraji kufanyika hii leo Septemba 7, 2026 Saa 10:00 alasiri. 

Posted by MROKI On Monday, September 07, 2026 No comments
Waziri wa Ujenzi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Abdallah Ulega amewaasa wanafunzi nchini kusoma kwa bidii, kuipenda nchi yao na kujituma ila kufikia malengo yao.

Ulega ameyasema hayo wakati akizungumza na wanafunzi hao kwa njia ya simu wakati wa uterkelezaji wa programu ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi Temeke ya kuwakutanisha watu mashuhuri waliosoma katika shule za msingi na sekondari nchini.

Ulega aliwakilishwa na Mke wake ambaye ni Mbunge wa Viti maalum Pwani, Mhe. Mariam Ulega na kuzungumza na  walimu na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Karibu ambayo zamani ilikua shule ya Msinhgi Muungano.

Akizungumza na hadhara hiyo kwa njia ya simu, Waziri Ulega amelipongeza Jeshi la Polisi Mkoa wa Temeke kwa kubuni program hiyo ambayo inatoa hamasa kwa wanafunzi kujibidisha katika masomo ili watimize ndoto zao kitaaluma.

Aidha ameishukuru Shule ya Msingi Muungano na sasa Karibuni Sekondari kwa kumjenga vyema huku akiwaasa wa wanafunzi wa shule ya Sekondari Karibuni kusoma kwa bidi ili kuwa watendaji bora.

“Lakini niseme tu kwa wanafunzi,   wafanye jitihada ya kusoma ili kuwa watenda kazi wema katika taifa na watambue kuwa nchi hii ni yao na waanze kujifunza kuwa na tabia njema,”alisema Ulega.

Ulega amesema wanafunzi wanapaswa kutambua kuwa nchi hii ina fursa kwa kila mmoja wao, bila kujali anatoka wapi katika kila pande ya nchi hii na kinachohitajika ni kujifunza kwa bidi, kuipenda nchi na kujituma.  
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Kamishna Msaidizi mwandamizi wa Polisi (SACP) Kungu John Malulu pamoja na Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP. Emma Foya ndio walioongoza programu hiyo shuleni hapo.

Lengo la Programu hiyo inayotekelezwa nchi nzima  ni kushawishi wanafunzi kusoma kwa bidii ili wafikie malengo yao na kufikia malengo kama ya watangulizi wao au kuwazidi watu hao maarufu ambao walisoma katika shule zao.

Posted by MROKI On Monday, September 07, 2026 No comments

September 06, 2026


Na: Dk. Reubeni Lumbagala 
Malazi, chakula na mavazi ni mahitaji ya msingi ya binadamu. Mwanadamu anapoyapata mahitaji haya kwa ukamilifu wake, hujenga utulivu wa akili, moyo na ari ya kufanya kazi kwa bidii.

Chama Cha Mapinduzi (CCM) nchini kinatekeleza mpango mkakati wake wa kuhakikisha watumishi wa Chama wanajengewa makazi ya kudumu kwani makazi ni hitaji la msingi la binadamu.

Kupatikana kwa makazi hayo, kunachochea uwajibikaji na uchapakazi wa watumishi hao, ambao wapo nchi nzima kwa madhumuni ya kuwatumikia wananchi.

CCM mkoani Tanga, chini ya uongozi wa Mwenyekiti wake, Rajab Abdallah, maarufu "Ustadhi Rajab," ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (MCC), umedhamiria kuhakikisha ujenzi wa nyumba 36 unakamilika kwa wakati katika wilaya zote tisa za mkoa wa Tanga. 

Kila wilaya zitajengwa nyumba nne za makatibu wa Chama wilaya, na za makatibu wa jumuiya ya vijana, wanawake na wazazi. Jumla ya gharama za nyumba zote 36 ni shilingi bilioni 2.5. 

Ikumbukwe kuwa, katika Uchaguzi Mkuu wa Chama wa mwaka 2022, Ustadhi Rajab aliahidi endapo atachagukiwa katika nafasi ya Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tanga, atahakikisha anasimamia na kuwezesha ujenzi wa nyumba hizo.

Ujenzi wa nyumba hizo unaendelea vizuri na ni faraja kuona, Mei 31, 2026, Ustadhi Rajab alikabidhi hundi ya shilingi milioni 500 kwa Katibu wa CCM mkoa wa Tanga, Mfaume Kizigo, ili ziwezeshe shughuli za ujenzi wa nyumba hizo ambazo malengo ni kukamilika ifikapo mwezi Disemba mwaka huu.

Ustadhi Rajab amekuwa na ubunifu wa kuwashirikisha marafiki zake na wadau mbalimbali katika shughuli za maendeleo ndani ya mkoa wa Tanga, jambo linalosaidia utatuzi wa changamoto kwa haraka.

Kwa hakika, Ustadhi Rajab amefanya kazi kubwa na ya kupongezwa katika mradi huu kabambe wa ujenzi wa nyumba 36 za watumishi wa Chama mkoani humo. Ahadi ni deni na sasa deni hilo linalipwa.
Posted by MROKI On Sunday, September 06, 2026 No comments

September 03, 2026


DODOMA
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Subira Mgalu (Mb.) imepatiwa mafunzo kuhusu usimamizi wa mikataba ya msaada wa kiufundi katika Sekta ya Madini, ikiwa ni pamoja na masharti ya kisheria yanayohusu umiliki wa leseni ndogo za uchimbaji wa madini.

Akizungumza kupitia mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye Ofisi za Makao Makuu ya Tume ya Madini jijini Dodoma mapema leo Mkurugenzi wa Huduma za Sheria wa Tume ya Madini, Francis Kayichile, kwa Niaba ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini amesisitiza kuwa mtu ambaye si raia wa Tanzania kupewa leseni ndogo ya uchimbaji madini ni kosa kwa mujibu wa Sheria ya Madini, Sura ya 123, kwa kuwa fursa ya kuomba na kumiliki leseni hizo imetengwa kwa Watanzania pekee.

Kayichile amesema Kifungu cha 64 kikisomwa pamoja na kifungu cha 9 (3) cha Sheria ya Madini, Sura ya 123, kinatoa fursa kwa Watanzania pekee kuwasilisha maombi ya leseni ndogo za uchimbaji madini, hivyo mtu asiye raia wa Tanzania hanufaiki na fursa hiyo.

Amesema pamoja na umiliki wa leseni kuwa kwa Watanzania, wamiliki wa leseni ndogo wanaweza kupata msaada wa kiufundi kutoka kwa wawezeshaji kwa kuzingatia sheria na kanuni zilizopo.


Aidha ameeleza kuwa kwa mujibu wa kanuni hizo mwenye leseni yenye msaada wa kiufundi amepatiwa  asilimia 30 ya faida baada ya kuondoa tozo zote za Serikali, bila kuzingatia gharama za uendeshaji wa mradi alizobeba mwezeshaji.

Ameongeza kuwa usimamizi wa mgodi, uingizaji wa vifaa na mitambo pamoja na ulinzi wa eneo na mali ni majukumu ya pamoja ya wahusika wa mkataba.

Kayichile amesema mkataba wa msaada wa kiufundi huwa na muda wa awali wa miaka mitatu na unaweza kuhuishwa, lakini kwa jumla muda wake haupaswi kuzidi miaka 12 au uhai wa mgodi unapoisha.

“Mikataba hiyo husajiliwa na Tume ya Madini na wahusika wana haki ya kufanya marekebisho  wakati wowote na pindi kunapofanyika marekebisho ya sheria  yanayoathiri masharti ya mkataba au pale inapobainika uwepo wa madini mapya katika eneo lenye leseni yenye msaada wa kiufundi” amesema.

Amesema Tume ya Madini inaendelea kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa mikataba hiyo, huku akisisitiza kuwa ukiukwaji wa masharti unaweza kusababisha hatua kuchukuliwa kwa mujibu wa Kifungu cha 74 cha Sheria ya Madini, Sura ya 123, ikiwemo kusitishwa au kufutwa kwa leseni.

Aidha, Kayichile amesema Serikali imefanya marekebisho ya Kanuni za Haki Madini kwa lengo la kulinda haki za wenye maduara waliopo ndani ya maeneo yenye leseni ndogo za uchimbaji madini.

Amesema kupitia Kanuni za Madini (Msaada wa Kiufundi) za mwaka 2025, hususan Kanuni ya 8(1)(h), mwenye leseni analazimika, kabla ya kuingia mkataba wa msaada wa kiufundi, kufanya makubaliano na wenye maduara au kuwalipa fidia kwa uwekezaji walioufanya katika eneo lenye leseni hiyo.

Kwa mujibu wa Kayichile, hatua hiyo inalenga kuhakikisha haki za Watanzania wanaomiliki leseni na wenye maduara zinalindwa, huku ikiweka mazingira ya ushirikiano katika shughuli za uchimbaji madini yanayozingatia sheria na kuhakikisha rasilimali za madini zinawanufaisha Watanzania wote.

Kikao hicho kilichoongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu (Mb.) kimeshirikisha pia watendaji wa taasisi zilizopo chini ya Wizara ya Madini.










Posted by MROKI On Thursday, September 03, 2026 No comments



Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Naibu Wasajili wa Mahakama nchini kuendelea kutekeleza majukumu yao ipasavyo huku wakilinda maslahi ya haki (Interest of Justice).

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 31 Agosti, 2026 alipokuwa akifungua Mafunzo Elekezi kwa Naibu Wasajili wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Tuna wajibu wa kuendelea kutekeleza majukumu yetu kwa kulinda maslahi ya haki, kwa kutokufungwa kwa masharti ya kiufundi kupita kiasi hadi kukwamisha upatikanaji haki,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema kuwa, Wasajili wa Mahakama ndio 'injini' ya Mahakama. Hivyo, wana nafasi kubwa katika maendeleo ya Mhimili huo ambao mamlaka yake kwa mujibu wa Ibara ya 4 ni kutekeleza jukumu la utoaji haki.

“Kwa mujibu wa Ibara ya 107A(1), Mahakama ndio yenye kauli ya mwisho kwenye masuala ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano. Na ukiwa unaongozwa na kanuni kadhaa: mojawapo, kutenda haki kwa wote bila kujali hali ya mtu kiuchumi au kijamii, kutochelewesha haki bila kuwepo sababu ya msingi na kwamba itakuwa huru, italazimika tu kuzingatia sheria za nchi na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kama ambavyo Ibara ya 107A inavyoelekeza,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema, shughuli zote za umma huongozwa na kusimamiwa na sheria; hakuna shughuli yoyote ya umma ambayo haiongozwi na kusimamiwa na sheria. Na kwa sababu hiyo, Katiba inakuwa pia sheria, kwa mujibu wa ile Sheria ya Tafsiri za Sheria, sura ya kwanza ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Jaji Mkuu amewakumbusha Naibu Wasajili hao kuwa waadilifu ili wanapofanya maamuzi, watu waone kweli kwamba haki imetendeka. Amesisitiza, “Na katika hilo lazima tuwe waadilifu, tunapoacha kuwa waadilifu, tukiwa wazembe, tukiwa wavivu, uwezo wetu ukiwa mdogo, watu hawatatuheshimu.”

Vilevile, Mhe. Masaju amekemea vikali tabia ya baadhi ya watu kuingilia uhuru na maamuzi ya Mahakama huku akibainisha kuwa, Katiba imeiwekea ulinzi kwa Mahakama kupitia Ibara ya 30(2)(c) inayoelekeza kuhakikisha utekelezaji wa hukumu au amri ya Mahakama iliyotolewa katika shauri lolote la madai au la jinai.

Aidha, Ibara ya 30(2)(d) inatamka kulinda heshima, haki na uhuru wa watu wengine au faragha ya watu wanaohusika katika shauri lolote mahakamani, kuzuia kutoa habari za siri, au kulinda heshima na uhuru wa Mahakama.

“Ni lazima hukumu na amri za Mahakama zitekelezwe, ni Mahakama gani hiyo inaweza ikafanya maamuzi halafu yasitekelezwe, halafu ikabaki kuwa Mahakama?” amehoji Jaji Mkuu.

Ameongeza kuwa, Katiba hiyo pia inaelekeza kwamba lazima Mahakama iheshimike; uhuru wake, mamlaka, na hadhi yake lazima vilindwe na viheshimiwe. Kwa hiyo, lazima kulinda sifa na haki au uhuru wa watu wengine, au maisha binafsi ya watu wanaohusika katika mashauri mahakamani, kuzuia kutoa habari za siri, kutunza heshima, mamlaka, na uhuru wa Mahakama.
Posted by MROKI On Thursday, September 03, 2026 No comments

September 02, 2026

Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC, Kenneth Simbaya (katikati) akiwa na Mwenyekiti wa Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA. Richard Mwaikenda pamoja na Makamu Mwenyekiti wa jukwa hilo, Sylivester Ngombaniza baada ya kufanya kikao cha pande hizo mbili.
Kutoka kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa JUWATA,Ngombaniza, Kaimu Afisa wa Fedha, Winfrida Madeni, Mwenyekiti wa JUWATA, Mwaikenda, Mkurugenzi Mtendaji wa UTPC, Simbaya na Afisa wa Programu UfutiliajiRasilimali, Andrew Malawiti.
Viongozi wa JUWATA na UTPC wakiwa katika kikao hicho.

Mwaikenda akimsikiliza kwa makini Simbaya wakati wa kikao hicho.
Mwaikenda akizungumza wakati wa kikao hicho.
Simbaya akiagana na viongozi wa JUWATA.
 ***************
JUKWAA Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) wamekubaliana kuimarisha ushirikiano katika kulinda uhuru wa vyombo vya habari, kutetea haki na maslahi ya waandishi wa habari pamoja na kuhakikisha jamii inapata habari sahihi na kwa wakati.

‎Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao cha pamoja cha viongozi wa JUWATA na UTPC kilichofanyika katika ofisi za UTPC zilizopo Barabara ya Aboud Jumbe, Mtaa wa Kazembo, eneo la Uzunguni jijini Dodoma.

Katika kikao hicho, viongozi hao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya habari, ikiwemo umuhimu wa kuwa na mshikamano miongoni mwa wadau wa habari katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili waandishi wa habari na vyombo vya habari nchini.

Aidha, walisisitiza umuhimu wa taasisi hizo kushirikiana katika kutetea uhuru wa vyombo vya habari, haki za waandishi wa habari na maslahi yao, huku wakitambua nafasi muhimu ya wanahabari katika kuhabarisha, kuelimisha na kuwajibika katika jamii.

Ushirikiano huo pia unalenga kuongeza nguvu katika kushughulikia changamoto zinazohusu mazingira ya kazi ya waandishi wa habari, pamoja na kujenga mahusiano mazuri kati ya wadau wa habari na taasisi mbalimbali zinazohusika na maendeleo ya sekta hiyo.

UTPC ina jumla ya Klabu 28 za Waandishi wa Habari zinazowakilisha waandishi wa habari kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, hivyo kuwa na mtandao mpana wa kuwafikia wanahabari katika maeneo mbalimbali nchini.

Kwa upande wa JUWATA, ujumbe uliongozwa na Mwenyekiti wake, Richard Mwaikenda, akifuatana na Makamu Mwenyekiti, Sylivester Ngombaniza, pamoja.

UTPC iliwakilishwa na Mkurugenzi Mtendaji, Kenneth Simbaya, pamoja na Afisa wa Programu wa Ufuatiliaji Rasilimali, Andrew Malawiti, Kaimu Afisa wa Fedha Winfrida Madeni na Afisa Msaidizi wa Programu, Edmund Kapungu.

Viongozi hao wameeleza umuhimu wa kuendeleza mawasiliano na ushirikiano wa karibu baina ya taasisi hizo kwa manufaa ya waandishi wa habari, vyombo vya habari na jamii kwa ujumla.

Wamesisitiza kuwa mshikamano wa wadau wa habari ni muhimu katika kujenga sekta imara, yenye weledi na inayoweza kutekeleza kwa ufanisi wajibu wake wa kuhabarisha umma na kulinda maslahi mapana ya jamii.
************
‎Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) limeanzishwa kihalali kwa kuzingatia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, likiwa na lengo la kupanua wigo kwa Wahariri wanaotimiza vigezo kuwa huru kujiunga na jukwaa hilo, ili kuongeza nguvu, umoja na ushirikiano katika kutetea na kulinda haki na maslahi ya Waandishi wa Habari pamoja na jamii kwa ujumla.

Katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku, JUWATA itazingatia Katiba na kanuni zake, sambamba na kufuata na kuheshimu Sheria za Nchi pamoja na taratibu zinazotawala tasnia ya Habari.

‎Kwa ufupi, JUWATA haijaasisiwa kwa lengo la kupambana, kushindana au kusigana na taasisi nyingine za Habari.

Badala yake, inalenga kujenga ushirikiano, mshikamano na mahusiano mema na taasisi za Habari za ndani na nje ya nchi, kwa manufaa ya Wahariri, Waandishi wa Habari na jamii kwa ujumla.

JUWATA inaamini kuwa umoja, ushirikiano na kuheshimiana ndiyo msingi wa kujenga tasnia imara, huru, yenye uwajibikaji na inayoweza kusimamia kwa ufanisi haki na maslahi ya Wadau wa Habari.
Posted by MROKI On Wednesday, September 02, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo