Nafasi Ya Matangazo

September 18, 2026

Ni Sekunde, Dakika, Saa, Siku, Wiki, Mwezi, Mwaka na hatimaye mika 19 sasa imetimia tangu Mzee S. T Nathan (18/08/1925 – 18/09/2007) ututangulie Mbele za haki kama ulivyotutangulia kuja duniani.

Nimajonzi sana kwetu na pengo lako halijazibika hadi hivi leo.

Unakumbukwa na wengi sana maana ulikuwa ni mhimili mkuu katika familia, kipekee unakunbukwa na Mke wako, watoto wako wote, wakwe zako, wajukuu  na vitukuu.

Aidha, unakumbukwa na Ndugu zako, Wananchi na majirani zako wa pale Kijiji cha Kinyenze,Kata na Tarafa ya Mlali , Wilayani Mvomero mkoani Morogoro, Same na Ugweno mkoani Kilimanjaro pia wanakukumbuka sana na kukuombea kila lililo jema katika mapumziko yako.
 
Tunakumbuka maneno yako ya Mwisho uliyotuachia watoto wako kuwa TUPENDANE, TUSAIDIANE na TUSHIRIKIANE, baba hakika hili linatendeka na tupo na umoja uliotujengea na tunajivunia hilo daima.

Tunazidi kukuombea Baraka na pumziko jema maana sote uliotuacha tutakufuata kama tulivyo kufuata hapa duniani.
PUMZIKA KWA AMANI MZEE S.T NATHAN
Jina la Bwana Lihimidiwe Amina.
Posted by MROKI On Friday, September 18, 2026 No comments


Na Neema Mbuja
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe.Dennis Londo, amewataka wafanyabiashara wa Tanzania  kutumia fursa kubwa kupitia Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na Soko Huru la Afrika, kuuza bidhaa  zao.

Mhe. Londo ameyasema hayo wakati alipokuwa akifunga hafla ya utoaji tuzo za jukwaa la 4 la biashara na uwekezaji kwa Watendaji Wakuu na Wakurugenzi wa makampuni 200 ambalo linawakutanisha wadau kujadili namna ya kufungua fursa kwa watanzania, wajasiriamali kufanya  biashara nje ya Tanzania.

Mhe Londo amesema kuwa uwepo wa jukwaa hili kunasaidia kuwakutanisha Wakurugenzi   Makampuni kubadilishana uzoefu  ma kuchangamkia fursa zilizopo.

Aliongeza kuwa Tanzania ni mwanachama wa EAC na SADC na sasa inaelekea kwenye Itifaki ya Soko Huru la Afrika, hivyo maandalizi ni sehemu muhimu ya kuhakikisha Watanzania wanashiriki na kunufaika na jumuiya hizo.

Amesema Wizara ya viwanda na Biashara itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya wafanyabiashara kufungua fursa zaidi kwa kushirikiana na sekta binafsi ili kukuza uchumi wa nchi.
Posted by MROKI On Friday, September 18, 2026 No comments

September 17, 2026

Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Tan Communication Media Ltd, inayomiliki na kuendesha kituo cha redio cha Redio 5 cha jijini Arusha, Robert Lowassa, amesema mshikamano baina ya Marekani na Tanzania yaongeze fursa zaidi za uwekezaji nchini.

Lowassa ameyasema hayo leo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Msemaji na Afisa Habari wa Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, Nice Cole ofisini kwake Arusha.
 
Amesema Marekani imekuwa mshirika muhimu kwa Tanzania katika maeneo mbalimbali, ikiwemo utalii, biashara, uwekezaji na miradi ya maendeleo.
 
Lowassa amesema ni matumaini yake kuwa mshikamano huo utaendelea kuwa imara zaidi ili kufungua fursa nyingi zaidi za uwekezaji na maendeleo kwa manufaa ya pande zote mbili.
 
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TanMedia, Angela Maina, amekaribisha ushirikiano huo, akisema Arusha na Tanzania kwa ujumla vina nafasi kubwa ya kunufaika zaidi kupitia mafunzo kwa vijana na waandishi wa habari, pamoja na programu za kubadilishana uzoefu (exchange programs) zitakazosaidia kukuza taaluma ya habari na uendeshaji bora wa vipindi.

Akizungumza na Radio 5, Msemaji na Afisa Habari wa Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, Nice Cole, amesema ushirikiano kati ya Tanzania na Marekani kwa miaka mingi umechangia maendeleo na ustawi wa wananchi wa pande zote mbili, pamoja na kuimarisha usalama katika ukanda wa Afrika Mashariki.
 
Amesema, Marekani inaendelea kuthamini uhusiano wake wa muda mrefu na Tanzania, huku ushirikiano katika sekta za usalama, biashara na uwekezaji, afya pamoja na maendeleo ukiendelea kuwa miongoni mwa maeneo muhimu katika mahusiano ya nchi hizo mbili.
 
Katika mahojiano hayo, Cole pia amesema Tanzania inaweza kuwa na nafasi muhimu katika kujenga minyororo ya usambazaji wa bidhaa na malighafi duniani, kutokana na upatikanaji wa madini muhimu yanayotumika katika sekta mbalimbali.
 
Amesema Marekani kwa sasa inaangalia kwa karibu suala la critical minerals, akieleza kuwa baadhi ya madini yanayopatikana Tanzania yanaweza kutumika katika sekta ya usafirishaji, ikiwemo uzalishaji wa betri za magari ya umeme.

Posted by MROKI On Thursday, September 17, 2026 No comments

September 16, 2026






Na. Zawadi Msalla
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), ipo mbioni kuzindua mwongozo wa tathmini ya misingi ya utawala nchini.

 Mwongozo huo umelenga kuangalia hali ya uzingatiwaji wa misingi ya utawala bora na kuweka mfumo unaoweza kutumika kupima namna taasisi za umma, binafsi na mifumo ya utawala inavyotekeleza misingi ya utawala bora.

 Mwongozo huo pia imelenga kuwa nyenzo muhimu katika kubaini mafanikio yaliyofikiwa, changamoto zilizopo na maeneo yanayohitaji maboresho katika nyanja ya utawala bora.

Akizungumza katika kikao kazi cha kupitia rasimu hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa Mkuu wa Mkoa Jijini Dodoma leo, Kaimu Katibu Mtendaji wa THBUB, Bi. Suzan Ndeona amesema kazi ya uandaaji wa nyaraka hiyo muhimu kwa nchi, ilianza rasmi mwaka 2023 kwa kuangalia vigezo mbalimbali na uhitaji wa nchi wa kuwepo mwongozo na nyenzo itakayotumika katika kufanya tathmini ya Utawala Bora nchini. 

Bi. Suzan amesema mwongozo huo umeweka vigezo vyote muhimu vya upimaji wa uwepo wa utawala bora katika Taasisi.  Aidha ameeleza mwongozo huo utaendelea kuboreshwa ili kuhakikisha unaenda sambamba na mabadiliko mbalimbali ya kimfumo yanayoendelea nchini  kama vile upimaji wa Watumishi wa Umma (PEPMIS).

“Bado mwongozo huu ni rasimu, utakapokamilika utawekwa mezani kupata maoni ya taasisi za umma, binafsi, na mashirika mbalimbali ambayo yanahusika na masuala ya utawala bora”.   Amesema Bi. Suzan.

Miongoni mwa misingi muhimu itakayoangaliwa na kufanyiwa tathimini ni pamoja na uwazi, uwajibikaji, usawa, utawala wa sheria, ushirikishwaji, ufanisi na tija, maridhiano, mwitikio na uadilifu.

 Akieleza kuhusu misingi ya utawala bora, Bi. Suzan alisema   misingi hiyo ina uhusiano wa moja kwa moja na jamii kwa kuwa utawala bora huonekana kupitia taasisi zinavyotoa huduma, kusikiliza wananchi, kutumia rasilimali na kutekeleza majukumu kwa mujibu wa sheria.

Naye Bi Hellen Siriwa kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wakati wa kutoa wasilisho la rasimu hiyo, amesema NBS imeshirikiana kikamilifu na THBUB katika kuandaa nyenzo za kufanyia tathmini kwa kuangalia namna ambavyo nchi itafaidika na mwongozo huo ulioandaliwa. Aliongeza kuwa NBS itaendelea kushirikiana na THBUB katika kuhakikisha kuwa mwongozo huo unakamilika na kuweza kuzinduliwa rasmi Kitaifa.  

Mwongozo huo utakuwa nyenzo ya kujenga utamaduni wa uwajibikaji katika taasisi za umma na binafsi kwa kutambua mapema maeneo yenye changamoto na kuchukua hatua za maboresho kabla ya kutokea kwa madhara.
Posted by MROKI On Wednesday, September 16, 2026 No comments






Na OWM – TAMISEMI, Lindi
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amesema hajaridhishwa na kasi ya utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na Mkandarasi KIKIM Contractors Limited kwa kushirikiana na mbia wake AMACO Enterprises katika Manispaa ya Lindi.

Miradi hiyo inahusisha ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilomita 5.3, Stendi ya Mabasi Mitwero, Soko Kuu la Matopeni na Ofisi ya Mradi, inayotekelezwa na Serikali kupitia Mradi wa Ustawishaji Miji Tanzania (TACTIC).

Prof. Shemdoe ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji wa miradi hiyo Septemba 15, 2026, mara baada ya kutembelea na kukagua ujenzi wa Stendi ya Mabasi ya Mitwero na Soko Kuu la Matopeni, ambapo alibaini kuwa utekelezaji wake umefikia asilimia 23, huku ikiwa imesalia miezi mitano kabla ya muda wa kukamilisha na kukabidhi miradi hiyo.

Akizungumza baada ya kukagua miradi hiyo, Prof. Shemdoe amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, kuhakikisha suala la utekelezaji wa mikataba hiyo linashughulikiwa kwa mujibu wa masharti ya mikataba, ili kuharakisha utekelezaji na kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati.

“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, hawa wanaotukwamisha ni wakandarasi wazawa ambao usipowapa kazi wanalalamika. Hivyo, Mheshimiwa RC, hawa wana mikataba, shughulikia suala hili kwa mujibu wa mkataba, kwani wakandarasi hawa wanaonekana ni wababaishaji,” amesema Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi kukutana na wakandarasi hao ili wampe mpango mkakati wa kukamilisha miradi hiyo haraka iwezekanavyo, na kuwasilisha kwake mpango kazi huo ifikapo Septemba 23, 2026.Vilevile, ameelekeza kuwa kila baada ya wiki mbili apatiwe mrejesho wa utekelezaji wa mpango huo, ili kufahamu hatua zinazochukuliwa na maendeleo ya miradi hiyo.

Akieleza chanzo cha kasi ndogo ya utekelezaji wa miradi hiyo, Mwakilishi wa Mhandisi Mshauri kutoka kampuni ya Interconsult Ltd, ambaye pia ni Mhandisi Mkazi, Mhandisi Rashidi Abdallah, amesema changamoto hiyo imetokana na mkandarasi kutokuwa amejipanga vyema kiutendaji, kutokuwa na rasilimaliwatu ya kutosha na kutumia vibaya fedha za awali alizolipwa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi.

Naye mmoja wa Wakurugenzi wa kampuni zilizopewa kandarasi hizo, John Daniel, amekiri kuwa wamechelewa kutekeleza miradi hiyo kutokana na uzembe, huku akieleza kuwa wamejipanga kufanya kazi usiku na mchana baada ya kuzifanyia kazi changamoto zilizokuwa zikikwamisha utekelezaji. 

Bw. Daniel ameomba kukutana na Mkuu wa Mkoa wa Lindi ili kuwasilisha mpango kazi wao, huku akimuomba Mkuu wa Mkoa kuwawekea malengo ya muda mfupi yatakayowawezesha kukamilisha kandarasi yao kwa wakati.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, amesema atakutana na wakandarasi hao ili wamueleze mkakati wanaokuja nao wa kukamilisha miradi yote ndani ya miezi mitano iliyobaki.

Mhe. Malima amewataka wakandarasi hao, wakati wa kikao hicho, kuwa tayari kuridhia kutoa mkataba mdogo (sub-contract) kwa mkandarasi mwingine kutekeleza sehemu ya mradi endapo wataona hawana uwezo wa kuikamilisha kwa wakati.

Katika ziara yake ya Septemba 15, 2026, Prof. Shemdoe alitembelea na kukagua pia utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa Daraja la Ng’uni katika Kata ya Nanganga, ujenzi wa shule mpya ya msingi eneo la Shule ya Sekondari Kitandi, ujenzi wa Kituo cha Afya Chiola Nachingwea, pamoja na kufanya mkutano wa hadhara katika Kijiji cha Mtuha, Nachingwea DC.
Posted by MROKI On Wednesday, September 16, 2026 No comments


Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amewasili mkoani Arusha leo Jumatano, Septemba 16, 2026, ambapo amepokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Arusha na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, CPA Amos Makalla, pamoja na viongozi wengine wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali.

Dkt. Mwigulu yupo mkoani Arusha kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kikazi, ikiwemo kufungua rasmi Kongamano la Kitaifa la Wanamipango, litakalofanyika kesho Alhamisi, Septemba 17, 2026, katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC).
Posted by MROKI On Wednesday, September 16, 2026 No comments


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi amefanya mikutano miwili ya pande mbili (bilateral meetings) pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa 70 wa Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu (IAEA) Jijini Vienna, Austria, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Tanzania kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika maeneo mbalimbali ya maendeleo.
 
Katika mkutano wake na Mkurugenzi Mkuu wa IAEA, Bw. Rafael Mariano Grossi, mazungumzo yalijikita katika kuimarisha ushirikiano katika matumizi ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kwa madhumuni ya amani na maendeleo, hususan matibabu ya saratani, kilimo na usalama wa chakula, lishe, maendeleo ya wataalamu pamoja na maandalizi ya Tanzania kuelekea matumizi ya nishati ya nyuklia kama nyongeza ya vyanzo vya uzalishaji umeme nchini siku zijazo.
 
Aidha, Makamu wa Rais amefanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa Vienna (UNOV) na Mkurugenzi Mtendaji wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Dawa za Kulevya na Uhalifu (UNODC), Dkt. Monica Juma. Mazungumzo yaliyolenga kuendeleza ushirikiano baina ya Tanzania na UNODC katika juhudi za kudhibiti dawa za kulevya.
 
Makamu wa Rais, Mhe. Ndejembi, yuko Jijini Vienna, Austria, akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano Mkuu wa 70 wa Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu (IAEA), unaowakutanisha Viongozi na Wawakilishi wa Nchi wanachama kujadili masuala mbalimbali yanayohusu matumizi salama na ya amani ya sayansi na teknolojia ya nyuklia.





Posted by MROKI On Wednesday, September 16, 2026 No comments


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) itaanza kuchukua hatua za kuwasajili na kuwatambua watoto walio chini ya umri wa miaka 18, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha mfumo wa utambulisho wa Taifa.

Dkt. Mwigulu amesema hatua hiyo itamuwezesha kila Mtanzania kutambulika kuanzia hatua za mwanzo za maisha yake pamoja na kuondoa pengo lililokuwepo katika mfumo wa utambulisho kati ya mtoto anapozaliwa na anapofikisha umri wa miaka 18.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo, Jumatano, Septemba 16, 2026, wakati akiwa Mgeni Rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Utambulisho Duniani, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.

“Mfumo huu utasaidia kupunguza usumbufu wa kutumia nyaraka au vitambulisho vingi wakati wa kupata huduma mbalimbali, kwa kuwa taarifa muhimu za mwananchi zitaendelea kutambulika na kuhifadhiwa katika mfumo mkuu wa Taifa wa utambuzi” amesema.

Aidha, Dkt. Mwigulu amewataka Watanzania ambao tayari wamesajiliwa na vitambulisho vyao vya Taifa vimekamilika kwenda kuvichukua, akisisitiza kuwa utambulisho ni msingi muhimu wa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

“Kitambulisho chenyewe kama nchi tumeingia gharama, tumeahirisha baadhi ya shughuli za maendeleo ili tutoe vitambulisho. Lakini tunapokuwa tumetoa kitambulisho, halafu mhusika haendi kuchukua, haya ni mambo ambayo yanakwamisha malengo mapana,” amesema.

Amesema kwa sasa NIDA imeboresha utaratibu wa kuwafahamisha wananchi pale vitambulisho vyao vinapokuwa tayari, ikiwemo kupitia ujumbe mfupi wa simu (SMS), hivyo hakuna sababu kwa wananchi waliokwishaandikishwa kuacha vitambulisho vyao kwa muda mrefu bila kuvichukua.

“Niendelee kusisitiza wananchi wote ambao wako tayari na vitambulisho vyao, basi waende kuvichukua. Lengo letu ni kuona kuwa hakuna Mtanzania anayeachwa nyuma katika kupata vitambulisho vya Taifa,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeendelea kufanya maboresho katika mfumo wa utambulisho wa Taifa ili kuhakikisha unakidhi mahitaji ya sasa ya kiteknolojia, usalama wa taarifa na utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Serikali imeendelea kuboresha mfumo wa utambulisho ili kupunguza utegemezi wa vitambulisho vingi kwa huduma mbalimbali na kuelekea katika mfumo ambao taarifa muhimu za mwananchi zinapatikana kupitia mfumo mkuu wa Taifa wa utambuzi,” amesema.

Naye, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi, amesema NIDA imefanya mapitio ya jumla ya vitambulisho vilivyotolewa katika ofisi zake na vituo 10 vya usajili vilivyopo katika kila wilaya, bila kuhusisha vituo 156 vilivyotajwa awali.

Amesema hadi sasa jumla ya watu 27,520,835 wamesajiliwa, ambapo watu 23,515,667 wamekwishapatiwa Namba za Utambulisho wa Taifa. Aidha, vitambulisho 21,526,635 vimezalishwa, huku bado kukiwa na idadi ya vitambulisho ambavyo havijachukuliwa na wananchi waliostahili kuvipata.

Kwa Upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, James Kaji, amesema jamii inapaswa kuacha dhana kwamba NIDA ni taasisi inayotoa kadi pekee, kwa kuwa utambulisho wa Taifa ni msingi wa upatikanaji wa huduma na utambulisho wa mwananchi katika maisha yake yote.

Amesema NIDA inaendelea kuboresha kitambulisho cha Taifa ili kiwe cha kidijitali na kiweze kuhusisha taarifa muhimu za huduma mbalimbali za kijamii, ikiwemo cheti cha kuzaliwa, bima ya afya, TIN, leseni ya udereva na taarifa nyingine muhimu, huku taarifa za kiafya kama kundi la damu zikitarajiwa kusaidia wakati wa dharura, kwa kuzingatia uthibitisho wa kitabibu.

Kanji amesema usajili wa watoto tangu wanapozaliwa ni muhimu kwa sababu utamwezesha kila mtoto kutambulika na kupata huduma za kijamii kwa urahisi katika hatua zote za maisha. Amesema zoezi hilo litaanza kwa majaribio katika wilaya za Kilolo, Lungu na Kusini Unguja, kabla ya kupanuliwa katika maeneo mengine nchini.
Posted by MROKI On Wednesday, September 16, 2026 No comments


Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, leo Jumatano, Septemba 16, 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na uongozi wa kampuni ya Barrick kuhusu namna bora ya uendelezaji wa migodi nchini.

Ujumbe wa Barrick uliongozwa na Afisa Mkuu wa Masuala ya Kimataifa wa Barrick, Bw. Woo Lee, ambaye aliambatana na Makamu wa Rais wa Masuala ya Kimataifa wa Barrick, Bw. James Ratchford, pamoja na Meneja wa Barrick nchini Tanzania, Bw. Melkiory Ngido.

Mazungumzo hayo yalilenga kujadili namna bora ya kuendeleza shughuli za uchimbaji madini, pamoja na kuangalia fursa za kuimarisha ushirikiano na kuongeza manufaa yatokanayo na sekta ya madini kwa uchumi wa Tanzania.
Posted by MROKI On Wednesday, September 16, 2026 No comments





Na Neema Thomas Chalila Mbuja
WAZIRI wa Viwanda na Biashara Mhe.Judith Kapinga (Mb), amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa nchi anayeshughulikia Shirikisho la Ulaya na Kimataifa mwenye dhamana ya kuratibu tatatibu za kiutawala jimbo la Hessen kutoka shirikisho la nchi ya Ujerumani Mhe. Manfred Pentz aliyeambatana na wafanyabiashara na wawekezaji takribani 30 kutoka nchini humo.

Akizungumza wakati wa mazungumzo na Ujumbe huo wa wafanyabiashara na wawekezaji kutoka ujerumani Mhe Kapinga amesema, kwa sasa Tanzania imejikita kwenye kuongeza mnyororo wa thamanini kwa mazao mbalimbali ikiwemo yale ya usindikaji kwenye mazao ya kilimo, mbolea, madawa, hapa nchini ili kuongeza thamani.

Aidha Mhe Kapinga aliongeza kuwa, chini uongozi wa Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, nchi ya Tanzania imejipanga kufikia uchumi wa Dola Trilioni 1 ifikapo mwaka 2050 na kuhakikisha mauzo ya nje yanaongezeka.

Kwa upande wake Waziri wa nchi anayeshughulikia shirikisho la Ulaya na kimataifa mwenye dhamana ya kuratibu taratibu za kiutawala Jimbo la Hessen Mhe. Manfred Pentz amesema, Tanzania ina fursa nyingi na maeneo ya kuwekeza kwenye sekta ya Kilimo, Madawa Utalii na gesi na mafuta na ujerumani iko tayari kushirikiana nayo kwenye maeneo hiyo kutokana na uwepo wa sera rafiki za Uwekezaji.

Ameitaka Tanzania kutumia fursa kwenye mkutano wa jukwaa la kibiashara itakaofanyika mwezi Februari mwakani kushiriki na kunadi fursa za nchi ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi kutoka nchini ujerumani.

Jumla ya wawekezaji takribani 30 kutoka nchini ujerumani wako hapa nchini kuangalia fursa za uwekezaji kwa Afrika Mashariki ikiwemo Tanzania na kuimarisha ushirikiano baina ya pande hizi mbili Kati ya Tanzania na Ujerumani.

Mkutano huo pia ulihudhuriwa na Naibu katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Aristides Mbwasi, Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani na Wakurugenzi kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara na wawakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki.



Posted by MROKI On Wednesday, September 16, 2026 No comments
Naibu Kamishna wa Uhifadhi anayesimamia Kurugenzi ya Huduma Saidizi na Utawala katika Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), DCC Emmanuel Wilfred Kiboko akitoa mada. 
Naibu Kamishna wa Uhifadhi anayesimamia Kurugenzi ya Huduma Saidizi na Utawala katika Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), DCC Emmanuel Wilfred Kiboko, amewaonya watumishi wapya 328 kutokuondoka katika vituo vyao vya kazi bila kufuata utaratibu, akisema kufanya hivyo kunaweza kusababisha kuchukuliwa hatua za kinidhamu.
 
DCC Kiboko ametoa kauli hiyo leo, Jumanne, Septemba 15, 2026, wakati akiwasilisha mada katika siku ya pili ya programu ya mafunzo elekezi kwa watumishi hao inayofanyika Dodoma. 

Amesema baada ya kukabidhiwa barua za ajira, watumishi hao wanatakiwa kuripoti katika vituo vyao vya kazi ndani ya siku saba, huku wakuu wa vituo wakitakiwa kuthibitisha kuripoti kwao na kuwapatia majukumu.
 
“Ukiondoka kwenye kituo cha kazi kwa utaratibu wowote ule, ina maana utapaswa kuchukuliwa hatua za kinidhamu kwa utoro kazini,” amesema DCC Kiboko, akiwataka watumishi hao kuchukulia kwa uzito masharti ya ajira na taratibu za utumishi wa umma.
 
Amesema pia watumishi hao hawataruhusiwa kuondoka vituoni kwenda kumalizia masomo bila kufuata taratibu na kupata kibali cha Kamishna wa Uhifadhi. Amesema TFS imebaini baadhi ya wakuu wa vituo wamekuwa wakiwaruhusu watumishi kwenda kumalizia masomo kinyume na taratibu, na kuwa hatua zinaweza kuwahusu viongozi watakaofanya hivyo bila kibali.
 
Akizungumzia mafunzo na maendeleo ya kielimu, DCC Kiboko amesema TFS hutumia Training Needs Assessment (TNA) kubaini maeneo ambayo taasisi inahitaji kuwekeza katika mafunzo, huku Training Programme ikibainisha mahitaji ya kila mtumishi na muda wa mafunzo kulingana na mahitaji ya taasisi na uwezo wa bajeti.
 
Amesema ajira za watumishi hao 328 zinalenga kuongeza nguvu kazi katika maeneo ya utekelezaji wa majukumu ya TFS, hivyo watumishi wanapaswa kutimiza wajibu wao katika vituo walivyopangiwa ili kufikia matarajio ya Serikali ya kuongeza ufanisi na mapato.
 
Aidha, amewataka watumishi hao kujiunga na vyama vya kitaaluma vinavyohusiana na kada zao, akitolea mfano Tanzania Association of Foresters (TAF) kwa wataalamu wa misitu, huku akisisitiza kuwa utumishi wa umma ni safari inayoendelea inayohitaji kujifunza na kukumbushana kuhusu maadili kila siku.
 
Akihitimisha, DCC Kiboko amewataka watumishi hao kuzingatia nidhamu, uadilifu na taratibu za utumishi, akisisitiza kuwa wanapaswa kulinda heshima ya TFS, Utumishi wa Umma, wao wenyewe na familia zao katika kipindi chote cha utumishi wao.





Posted by MROKI On Wednesday, September 16, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo