Nafasi Ya Matangazo

August 26, 2026

CHAMA cha Mapinduzi CCM kimependekeza jina la mwanachama wake Ndg. Deogratius John Ndejembi kua Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 

Akitangaza uamuzi huo wa Halmashauri Kuu ya CCM iliyokugana leo jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro amesema hivi sasa zonasubiriwa taratibu za kikatiba ili kukamilisha mchakato huo.

Hatua hiyo imekuja siku moja baada ya Makamu wa Rais aliyepo madarakani Balizi Dkt.Emmanuel Nchimbi kumwandikia barua Rais ya kutaka kujiuzulu na Rais Samia Suluhu Hassan siku hiyo hiyo ya Agosti 25, 2026 kuridhia barua hiyo.

Ndejembi (43) ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Chamwino Mkoni Dodoma na Waziri wa Nishati atalazimika kuachia nafasi hizo na kushika wadhifa wake mpya wa Makamu wa Rais pindi Bunge likimuidhinisha. 

Ni msomi wa Shahada ya International Relations katika Chuo Kikuu cha Lincoln cha Nchini Uingereza.

Ndejembi alianza elimu ya msingi  Cannon Andrea kuanzia mwaka 1988-1995, kisha akasoma sekondari ya Kigurunyembe mkoani Morogoro mwaka 1996-1998 na Merton College 2002-2004.

Deo Ndejembi ni miongoni mwa wanasiasa ambao wamepanda hatua kwa hatua katika uongozi wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Ndejembi alianza kujijenga kisiasa kupitia UVCCM, kabla ya kuingia kwenye nafasi za uongozi wa Serikali.

Kada huyo wa Chama cha Mapinduzi nyota yake ilianza kushamiri mwaka 2016, alipoteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma na Rais Dkt John Magufuli.

Baadae alijitosa kuwania Ubunge 2020 na kushika nafasi mbalimbali ikiwa na Unaibu Waziri Ofisi ya Rais, (Utumishi na Utawala Bora).

Julai 2024, Rais Samia alimteua Ndejembi kuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na baadae Waziri wa Nishati
Aidha, katika hatua nyingine Chama cha Mapinduzi kimetangaza kumvua uanachama Ndugu. Dkt Emmanuel Nchimbi aliyekua Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tamzania.






Posted by MROKI On Wednesday, August 26, 2026 No comments

August 25, 2026


 

Posted by MROKI On Tuesday, August 25, 2026 No comments




Posted by MROKI On Tuesday, August 25, 2026 No comments


Na: Mwandishi Wetu, Tanga 
Janga la moto lililowakumba wafanyabiashara wa Stendi ya Ngamiani iliyoko Barabara ya 12, Jijini Tanga, limewagusa wadau mbalimbali ambao wamejitolea kuwapa pole na kuwapatia kifuta machozi.

Ajali hiyo iliyotokea usiku wa Agosti 14, 2026, imeleta hasara kubwa kwa wafanyabiashara hao kutokana na bidhaa zao kuteketea kabisa.

Akihitimisha Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu, Agosti 24, 2026, katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, Jijini humo, Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, kipekee alizipongeza Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga chini ya uongozi wa Balozi Dk. Batilda Buriani na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Tanga chini ya uongozi wa CPA. Castro John.

Dk. Mwigulu amesema, alipata taarifa ya janga la moto kutoka kwa Mbunge wa Jimbo la Tanga Mjini, Kassim Amar, hivyo anaungana nao katika kuwapa pole wafanyabiashara hao.

"Nikupongeze Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa na timu yako, mlienda mkawafuta machozi kidogo wananchi wale waliopatwa na madhila hayo. Niliambiwa umeshawapatia kiasi, basi nitadouble (kuongeza mara mbili ya fedha zilizotolewa) huo mkono uliowashika," amesema Dk. Mwigulu.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa imekabidhi shilingi milioni 14 kwa wafanyabiashara 12 na familia mbili zilizounguliwa, huku kila mmoja akipata shilingi milioni moja katika mgao huo.

Vilevile, Dk. Mwigulu amewapongeza TRA kwa kuwashika mkono wafanyabiashara hao. "Nawapongeza pia TRA kwa kutoa kifuta machozi, nitoe wito kwa wadau wengine na sekta binafsi kuwaunga mkono TRA," amesema.

Katika salamu za pole, Agosti 18, 2026, Meneja TRA mkoa, CPA John, alisisitiza pamoja na kuwapatia kiasi cha fedha lakini pia watakaa na wafanyabiashara ili kuwasaidia katika kuwapa unafuu wa kodi.
Posted by MROKI On Tuesday, August 25, 2026 No comments

Na: Mwandishi Wetu 
Wazazi na walezi waishio wilayani Pangani mkoani Tanga, wamehimizwa kuwapeleka watoto wao walio chini ya umri wa miaka kumi katika vituo vya kutolea huduma ili wakapate chanjo ya ugonjwa wa Polio.

Hayo yameelezwa na Mbunge wa Jimbo la Pangani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, Agosti 25, 2026.

Amesema, chanjo hiyo ni muhimu kwani inawapa watoto hao kinga dhidi ya kupooza katika ukuaji wao na hivyo kuwaimarisha kiafya.

"Nitoe rai kwa wazazi na walezi, kuhakikisha wanawapeleka watoto wao kupata chanjo ya Polio kuanzia Agosti 27 hadi 30, 2026. Hii itawasaidia watoto wao kuwa na afya na ukuaji bora," amesema Aweso.

Ameongeza kuwa, serikali inaandaa taifa la watu wenye afya bora, ndiyo maana inagharamia chanjo za magonjwa mbalimbali na kutoa bure kwa wananchi wake.

"Serikali inataka raia wake wawe na afya njema, ndiyo maana inasimamia kikamilifu utoaji wa chanjo za magonjwa mbalimbali ukiwemo ugonjwa wa Polio. Chanjo hii inawalinda watoto dhidi ya kupooza, ulemavu na hata kupoteza maisha," amesema.

Kimsingi, Halmashauri ya wilaya ya Pangani imejipanga kutoa chanjo katika vituo vyote vya afya, shule za msingi na awali, maeneo ya mikusanyiko pamoja na kaya kwa kaya.

Kampeni ya utoaji chanjo inaratibiwa na Wizara ya Afya ambapo kwa awamu hii itatolewa katika mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Kilimanjaro, Manyara, Mara, Pwani na Tanga kuanzia Agosti 27 hadi 30, 2026.

Kampeni hiyo inachagizwa na kaulimbiu isemayo "Mpe Chanjo, Zuia Polio," ikihimiza watoto kupewa chanjo ili kujikinga na ugonjwa huo.

 

Posted by MROKI On Tuesday, August 25, 2026 No comments

August 24, 2026








Mirerani, Manyara. 
Serikali kupitia Wizara ya Madini imeanza kuchukua hatua za kuboresha mfumo wa biashara na uchimbaji wa madini ya Tanzanite nchini, kwa kufikia maamuzi yaliyotokana na taarifa za Tume na Kamati zilizoundwa kuchunguza changamoto za sekta hiyo, kwa ajili ya kuboresha mazingira ya biashara, kuimarisha usimamizi na kuongeza uzalishaji wa madini hayo adimu duniani sambamba na kuongeza thamani. 

Mhe. Mavunde ametoa maelekezo hayo leo, Agosti 24, 2026, wakati wa ziara ya kukagua shughuli za uchimbaji na biashara ya Tanzanite Mirerani, Wilaya ya Simanjiro, ambapo ametembelea migodi inayomilikiwa na Franone Mining & Gems Co. Ltd. Na Chusa Mining Limited,soko dogo la madini,eneo la uthaminishaji na jengo la biashara ya madini ya Tanzanite.

Aidha Waziri  Mavunde, ametoa wiki mbili kwa wachimbaji wa kati wa madini ya Tanzanite Mirerani kuwasilisha taarifa ya hatua wanazochukua katika kutumia teknolojia za kisasa za utafiti, akisisitiza kuwa sayansi na teknolojia ni muhimu katika kubaini mashapo yaliyopo na kuongeza uzalishaji wa madini hayo adimu duniani sambamba na kuacha uchimbaji wa kubahatisha kwa kukosa taarifa sahihi.

“Wekezeni kwenye teknolojia ya kisasa ya utafiti, wekezeni kwenye sayansi ili kubaini mashapo yaliyopo. Ndani ya wiki mbili kuanzia leo, nataka kupata taarifa ya juhudi zenu za uwekezaji katika teknolojia ya kisasa ya utafiti,” amesema Mhe. Mavunde.

Aidha, Waziri Mavunde amempongeza na kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa maelekezo ya kutenga asilimia 10 ya mapato yatokanayo na Sekta ya Madini kwa ajili ya utafiti, akisema uamuzi huo utaongeza kasi ya utafiti wa kina wa rasilimali za madini nchini.

Amesema Mirerani na Mkoa wa Manyara ni miongoni mwa maeneo ya kipaumbele katika mpango huo wa utafiti, hatua inayolenga kuongeza uelewa wa rasilimali zilizopo na kuwezesha shughuli za uchimbaji kufanyika kwa ufanisi zaidi.

Akizungumzia upatikanaji wa mitaji, Mhe. Mavunde amesema wachimbaji wanaweza kunufaika na mikopo nafuu kupitia taasisi za fedha, huku Serikali ikiendelea kuimarisha mifumo ya dhamana za mikopo.

Amesema Shirika la Mfuko wa Dhamana za Mikopo (Credit Guarantee Scheme Corporation) kupitia Benki Kuu ya Tanzania tayari umeundwa na kusajiliwa, na unatarajiwa kusaidia wachimbaji kupata mitaji kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao.

Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde, ametangaza kuanza kutumika kwa kofia ngumu yenye kamera katika migodi ya Mirerani, teknolojia itakayowezesha ufuatiliaji wa shughuli za uchimbaji hata chini ya mgodi kwa kuanza na Mgodi wa Franone Mining & Gems Co. Ltd na kuelekeza migodi mingine kutumia teknolojia hiyo ili kuongeza ufanisi katika usimamizi na ufuatiliaji wa shughuli za uchimbaji.

Kuhusu changamoto ya nishati ya umeme, Mhe. Mavunde amesema Wizara ya Madini na Wizara ya Nishati zimeweka mkakati wa pamoja wa kuhakikisha upatikanaji wa nishati unaendana na mahitaji ya Sekta ya Madini, ili shughuli za uchimbaji na shughuli zingine zinazoambatana na Sekta ya Madini ziendelee bila vikwazo.

Aidha, Mhe. Mavunde amewapongeza wadau wa Mirerani kwa kushiriki minada ya madini pamoja na kuchangia huduma za kijamii, ikiwemo ujenzi wa zahanati, akisisitiza umuhimu wa Sekta ya Madini kuendelea kuwa na manufaa kwa jamii.

Aidha, amepiga marufuku wafanyabiashara wa madini (dealers) kutumia wageni kufanya biashara kinyume na utaratibu, akionya kuwa Serikali itachukua hatua kali dhidi ya watakaokiuka sheria. Sambamba na hilo, amemuelekeza Afisa Madini Mkazi wa Mirerani kukutana na kampuni za uchimbaji na wadau wengine ili kuboresha mazingira ya kazi kwa wanaapolo, huku Ofisi hiyo ikitakiwa kukaa na wadau wote kuangalia namna bora ya kuboresha mazingira ya biashara katika soko lililopo ndani ya migodi.

Waziri Mavunde pia ameiagiza Kituo cha Jemolojia Tanzania  (TGC) kutembelea wanawake wanaojihusisha na shughuli za magonga katika eneo la Mirerani na kutathmini namna ya kuwawezesha zaidi. Aidha, ameiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro kuangalia uwezekano wa kutoa mikopo ya asilimia 10 kwa wananchi kwa kuzingatia shughuli za uchimbaji wa madini ambazo ndizo shughuli kuu za kiuchumi katika eneo hilo.

Kwa upande wake, Mbunge wa Simanjiro na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Mhe. James Kinyasi Ole Millya, amemshukuru Waziri Mavunde kwa kutembelea Mirerani na kuchukua hatua za kushughulikia changamoto zinazowakabili wachimbaji na wananchi wa eneo hilo.

Naye Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Simanjiro, Kiria Laizer, ameipongeza Serikali kwa utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, akisema hatua zinazochukuliwa zinaendelea kuimarisha shughuli za madini na maendeleo ya wananchi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mkurugenzi wa Franone Mining, Onesmo Mbise, na Mkurugenzi wa Chusa Mining, Joseph Mwakipesile, wametoa ahadi mbele ya Waziri Mavunde kutekeleza maelekezo hayo kwa kufanya utafiti wa kisasa wa mashapo ya Tanzanite na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji ndani ya muda uliowekwa.
Posted by MROKI On Monday, August 24, 2026 No comments
1.    Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akishiriki Mkutano wa Kumi na Saba wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kupambana na Kuenea kwa Hali ya Jangwa na na Ukame (UNCCD COP 17) unaofanyika katika Jiji la Ulaanbaatar nchini Mongolia, Agosti 24, 2026.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (kushoto) akizungumza na Waziri wa Kilimo na Usalama wa Chakula nchini Sudani Kusini Mhe, Clement Juma walipokutana katika Mkutano wa Kumi na Saba wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kupambana na Kuenea kwa Hali ya Jangwa na na Ukame (UNCCD COP 17) unaofanyika katika Jiji la Ulaanbaatar nchini Mongolia, Agosti 24, 2026.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akishiriki Mkutano wa Kumi na Saba wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kupambana na Kuenea kwa Hali ya Jangwa na na Ukame (UNCCD COP 17) unaofanyika katika Jiji la Ulaanbaatar nchini Mongolia, Agosti 24, 2026.
*****************
Na, Mwandishi Wetu, Ulaanbaatar, Mongolia
Tanzania inashiriki Mkutano wa Kumi na Saba wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kupambana na Kuenea kwa Hali ya Jangwa na Ukame (UNCCD COP 17) unaofanyika katika Jiji la Ulaanbaatar nchini Mongolia.
 
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akiambata na Ujumbe wa Tanzania wameshiriki Mkutano huo uliofunguliwa na Rais wa Mongolia Mhe. Khurelsukh Ukhnaa, Agosti 24, 2026.
 
Mhe. Masauni amesema Mkutano huo umeweka msisitizo kupitia kaulimbiu yake ya “Ongoa Ardhi, Ongoa Matumaini”, kaliuambiu ambayo inasisitiza kuongeza uwekezaji katika urejeshaji wa ardhi, ustahimilivu dhidi ya kuenea kwa hali ya jangwa, ukame na usimamizi endelevu wa maeneo ya malisho.
 
Aidha, Mwaka 2026 pia umetangazwa kuwa Mwaka wa Wafugaji na nyanda za Malisho jambo linalofanya ajenda ya Tanzania kuhusu uhifadhi wa malisho na ustawi wa wafugaji kuwa muhimu zaidi katika mkutano huu.
 
“Kwa Tanzania, changamoto ya uharibifu wa ardhi inahusishwa na sababu mbalimbali, zikiwemo ukataji na uharibifu wa misitu, upanuzi wa mashamba kwaajili ya kilimo, uchomaji moto usiodhibitiwa, mmomonyoko wa udongo, matumizi yasiyo endelevu ya ardhi na uendelezaji wa makazi.”
 
“Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huu unatoa fursa ya kupata uzoefu, teknolojia, ushirikiano na rasilimali za kifedha kwa ajili ya kuimarisha usimamizi endelevu wa malisho, urejeshaji wa ardhi iliyoharibika, uhifadhi wa misitu, vyanzo vya maji na bioanuwai, pamoja na kuongeza ustahimilivu wa jamii za wakulima na wafugaji katika kupambana na kuenea kwa hali ya Jangwa na Ukame.” Amesema Mhe. Masauni.
 
Kwa upande wake, Afisa Kiungo wa Mkataba huo kutoka Tanzania Bw. Thimoth Mande amesema Ushirikiano huu unawezesha Tanzania kushughulikia kwa pamoja changamoto za uharibifu wa ardhi, upotevu wa bioanuwai na mabadiliko ya tabianchi, badala ya kuzishughulikia kama changamoto zinazojitegemea.
 
Amesema, ushiriki wa Tanzania si wa kuhudhuria mkutano pekee, bali ni fursa ya kuonesha hatua ambazo tayari Tanzania inachukua katika kupambana na changamoto hii, huku ikiomba kuongezewa uwekezaji na teknolojia.
 
Tanzania inaweza kutumia matokeo ya mkutano huu kuhamasisha rasilimali zaidi kutoka katika mifuko ya kifedha za mazingira kama vile GEF, IFAD, UNDP, FAO, UNEP, sekta binafsi na mifumo bunifu ya fedha, ili kuongeza miradi hii kutoka kiwango cha maeneo maalum kwenda maeneo makubwa zaidi.
 
Naye, Meneja wa Kanda ya Mashariki Kusini,  Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Bi. Aminata Kirama amesema Baraza hilo linalowajibu wa kufanya kupitia maeneo ambayo yamebainishwa hasa katika kufanya tafiti.
 
Posted by MROKI On Monday, August 24, 2026 No comments

August 23, 2026

Kampuni ya Azam Marine imeanza maandalizi ya kuimarisha huduma za usafiri wa majini kuelekea michuano ya AFCON 2027, ikiwamo kuongeza meli mpya ya Kilimanjaro 9 iliyowasili Januari mwaka huu.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Azam Marine, Bw. Abubakari Aziz Salim, amesema hatua hiyo inalenga kuongeza uwezo wa kusafirisha mashabiki, wachezaji na viongozi kati ya Dar es Salaam na Zanzibar wakati wa michuano hiyo.

Bw. Salim amesema kampuni hiyo ina uwezo wa kusafirisha hadi abiria 15,000 kwa siku, huku ikijivunia uzoefu wa miaka 33 katika sekta ya usafiri wa majini.

Aidha, amesema Azam Marine itatoa ajira za muda mfupi ili kukidhi ongezeko la mahitaji ya wasafiri wakati wa AFCON 2027.

Amewataka Watanzania kutumia fursa hiyo kuitangaza Tanzania kwa ukarimu na huduma bora, akisisitiza kuwa urithi wa michuano hiyo utategemea namna nchi itakavyojiandaa na kutumia fursa zitakazojitokeza.

“Tutumie platform hii ya AFCON 2027 kuiweka Tanzania katika mioyo ya wageni,” amesisitiza Bw. Salim.
Posted by MROKI On Sunday, August 23, 2026 No comments

August 22, 2026









Na. Mwandishi Wetu -  Kazuramimba Kigoma
Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, Amewaasa vijana kulinda afya zao na kuepuka tabia hatarishi ili kupunguza maambukizi mapya ya VVU, kwa kuzingatia kuwa ni kundi linaloongoza kuwa hatarini zaidi nchini Tanzania.

Dkt. Yonazi ameyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Afua za UKIMWI Wilaya ya Uvinza Mkoa wa Kigoma alipoambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania, Dkt. Adam Mrisho, timu ya wataalam kutoka Ofisi yake, Wizara ya Afya, TAMISEMI na Ofisi ya Mkoa huo.

Aidha amepata wasaa kutembelea Kituo cha Maarifa Kata ya Kazuramimba mkoani humo kinachotoa huduma za masuala ya VVU na UKIMWI, na kukutana na vijana wanaotekeleza afua za UKIMWI kupitia vikundi vya uzalishaji mali kwa lengo la kujiinua kiuchumi na kujiletea maendeleo yao.

Akiwa katika kituo hicho, Dkt. Yonazi amepokea taarifa kutoka kwa mwenyekiti wa kikundi, Billy Sekibaha, kuhusu shughuli zinazofanywa na kikundi hicho ikiwemo za biashara ndogondogo za kuuza dagaa pamoja na shunguli za ushonaji wa nguo kwa lengo la kujikwamua kiuchumi na kuondokana na dhana ya utegemezi.

Amesisitiza kuwa, kundi la vijana linategemewa na Taifa katika shughuli za uzalishaji mali na kujiletea maendeleo yao na Taifa kwa ujumla hivyo ni vyema vijana wakaendelea kujilinda na kulinda wengine kwa kutambua hali zao na endapo wakagundulika kuwa na maambukizi ya VVU inashauriwa kuanza kutumia dawa mapema.

"Mnafanya kazi nzuri sana, endeleeni kuchangamkia uwepo wa mitandao ya kijamii kutangaza bidhaa zenu ili kuwafikia wateja wengi zaidi na kujitangaza kitaifa na kimataifa," alisisitiza Dkt. Yonazi

Kwa upande wake Mtendaji  wa TACAIDS, Dkt. Adam Mrisho amewapongeza vijana hao kwa kazi nzuri wanazofanya na kusisitiza kuwa Tume itaendelea kuwawezesha vijana kiuchumi na kuwajengea uwezo ili kuendeleza mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya VVU na kufikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.
Posted by MROKI On Saturday, August 22, 2026 No comments

August 21, 2026




Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Benjamin Kuzaga amewaongoza Maafisa, Wakaguzi na Askari wa vyeo mbalimbali wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia Mbeya kutoa msaada wa mahitaji mbalimbali kwa akina mama waliolazwa Kituo cha Afya Ruanda Mwanjelwa Jijini Mbeya.

Akizungumza Agosti 21, 2026 mara baada ya kutembelea Kituo hicho, Kamanda Kuzaga amesema kuwa lengo la kufika katika kituo hicho ni kutoa msaada kwa akina mama ambao wamelazwa, kuwapatia vitu mbalimbali kama vile Sukari, Maziwa, Sabuni, Soda, Pampasi ili viweze kuwasaidia katika kipindi ambacho watakuwa Kituoni hapo.

Aidha, Mkuu wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia Mkoa wa Mbeya Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Ibrahim Mhando kwa niaba ya Askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia ameeleza kuwa wao kama Askari wa Kikosi hicho waliona ni vema kufika Katika Kituo cha Afya Ruanda kwa ajili ya kuwashika mkono kwa kuwapatia vitu mbalimbali wagonjwa ambao wamelazwa ili viweze kuwasaidia.

Naye, Bi. Adelina Amnaaye Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Ruanda - Mwanjelwa Mbeya amelishukuru Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kwa kuchagua kutembelea Kituo hicho na kwa msaada walioutoa kwani vitu hivyo vitawasaidia wagonjwa ambao wamelazwa Hospitalini hapo.

Kwa upande wake, Witness Kiberenge kwa niaba ya akina mama waliolazwa Hospitalini hapo amelishukuru Jeshi la Polisi kwa msaada wa vitu mbalimbali huku akitoa wito kwa jamii kuwakumbuka wagonjwa na watu wenye mahitaji maalum.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kuelekea Maadhimisho ya miaka ishirini (20) ya Polisi Jamii, linaendelea kuyafikia makundi mbalimbali yenye uhitaji lengo likiwa ni kutoa elimu, misaada mbalimbali kwa makundi ya kijamii yenye mahitaji maalum.






Posted by MROKI On Friday, August 21, 2026 No comments
Katika sekta ya usafiri wa anga, kuna wataalamu mbalimbali wanaoshiriki kuhakikisha ndege zinafanya safari kwa usalama na ufanisi. Miongoni mwa wataalamu ambao mara nyingi huchanganywa ni Waongozaji wa Ndege, wanaojulikana kama Air Traffic Controllers, na Waegeshaji wa Ndege, wanaojulikana kitaalamu kama Aircraft Marshallers.
Waegeshaji wa ndege ni wataalamu wanaofanya kazi katika maeneo ya maegesho ya ndege viwanjani. Mara nyingi huonekana wakiwa wamevaa mavazi maalum ya usalama na kutumia vijiti vya mwanga au ishara za mikono kumwelekeza rubani wakati ndege inapokaribia sehemu ya maegesho au inapojiandaa kuondoka.

Jukumu lao ni kuhakikisha ndege inaelekezwa kwa usahihi katika eneo lililotengwa bila kuhatarisha usalama wa ndege, vifaa vya uwanja, majengo au watu waliopo katika mazingira ya karibu. Ishara wanazotumia hutambulika kimataifa na humsaidia rubani kufanya maamuzi sahihi hasa katika maeneo ambayo mwonekano kutoka ndani ya ndege unaweza kuwa na mipaka.

Historia ya kazi ya uegeshaji wa ndege inaanzia katika miaka ya mwanzo ya maendeleo ya usafiri wa anga, ambapo mawasiliano kati ya marubani na wahudumu wa ardhini yalitegemea zaidi ishara za mikono. Pamoja na maendeleo ya teknolojia katika viwanja vya ndege, kazi ya Aircraft Marshaller bado inaendelea kuwa sehemu muhimu ya shughuli salama za ndege ardhini.

Kwa upande mwingine, Waongozaji wa Ndege, au Air Traffic Controllers, wana jukumu la kusimamia na kuratibu mwendo wa ndege angani na katika maeneo maalum ya viwanja vya ndege. Hutumia mifumo ya mawasiliano, ufuatiliaji na taratibu za uongozaji wa ndege kuhakikisha ndege zinatenganishwa kwa umbali salama na kupewa maelekezo wakati wa kuruka, kutua na kujiendesha katika maeneo wanayoyasimamia.

Tofauti kubwa kati ya wataalamu hawa ni kwamba Air Traffic Controllers huongoza na kuratibu mwendo wa ndege kupitia mawasiliano ya redio na mifumo ya uongozaji, wakati Aircraft Marshallers humwelekeza rubani kwa ishara za kuona katika eneo la maegesho ya ndege.

Pamoja na tofauti hiyo ya majukumu, wataalamu hawa wote ni sehemu muhimu ya mfumo wa usalama wa usafiri wa anga na huchangia kuhakikisha shughuli za ndege zinafanyika kwa mpangilio, usalama na ufanisi.
Nchini Tanzania, Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) ina jukumu la kusimamia na kudhibiti usalama wa usafiri wa anga kwa kuzingatia sheria, kanuni na viwango vinavyotambuliwa kitaifa na kimataifa, ikiwemo miongozo ya Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga, ICAO.

 Chanzo- TCAA

Posted by MROKI On Friday, August 21, 2026 No comments

August 20, 2026






Na Mwandishi Wetu – Iringa
MUFINDI: Wananchi wa vijiji vinavyopakana na Shamba la Miti Sao Hill wilayani Mufindi wameahidi kushirikiana na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika kuzuia na kudhibiti moto wa misitu, baada ya kupatiwa elimu kuhusu matumizi salama ya moto.

Ahadi hiyo imetolewa leo, Agosti 20, 2026, katika mikutano ya uhamasishaji iliyofanyika vijiji vya Bumilayinga na Kisada, Kata ya Bumilayinga, ikiwa sehemu ya kampeni za kila mwaka za kuelimisha jamii kuhusu madhara ya moto na umuhimu wa kulinda misitu na mazingira.

Akizungumza katika mikutano hiyo, Mwakilishi wa Mhifadhi Mkuu wa Tarafa ya Pili ya Shamba Ihefu, SCO Frank Milanzi, amesema wananchi wanaoishi karibu na shamba la miti wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha moto unaotokana na shughuli za kibinadamu hauingii katika misitu.

“Moto unaweza kusababisha madhara makubwa kwa misitu, mali na maisha. Ni muhimu kila mmoja kuhakikisha moto unaotumika kwa shughuli mbalimbali unadhibitiwa na kuzimwa kabisa baada ya matumizi,” amesema.

Mkuu wa Kitengo cha Ulinzi wa Msitu Dhidi ya Moto wa Shamba la Miti Sao Hill, CO I Murya Sawa, amewataka wananchi kuacha kuwasha moto kiholela na kutoa taarifa mapema wanapoona dalili za moto katika maeneo ya misitu.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Bumilayinga, Mhe. Dorian Lyanzile, amesema viongozi wa vijiji na wananchi wanapaswa kuimarisha ushirikiano wao na TFS ili kuhakikisha matumizi ya moto hayahatarishi misitu na mazingira.

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Kisada, Lidia Mwenda, amesema wananchi wamepokea elimu hiyo kwa umuhimu na wako tayari kushirikiana na TFS katika kulinda misitu, akieleza kuwa mikutano hiyo huwasaidia kutambua madhara ya matumizi yasiyo sahihi ya moto.

Mikutano hiyo ni sehemu ya mpango wa TFS kupitia Shamba la Miti Sao Hill kuimarisha ushirikiano na jamii zinazozunguka shamba hilo, ikiwemo vijiji 60 vinavyopakana nalo wilayani Mufindi, kwa kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi katika kuzuia na kudhibiti moto, hasa wakati wa kiangazi.
Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments
NnnMkuu wa Wilaya ya Kiteto akagua miradi ya elimu yenye thamani ya Shilingi bilioni 1.37

Mkuu wa Wilaya ya Kiteto, Mhe. Remidius Mwema,tarehe 17 Agosti 2026  alifanya ziara ya ukaguzi wa miradi mbalimbali katika sekta ya elimu yenye thamani ya jumla ya Shilingi bilioni 1.37, katika Kata za Partimbo, Engusero na Laiseri.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mwema pia alizungumza na wananchi kwa kusikiliza na kutatua kero mbalimbali,akiwa katika Kata ya Laiseri, Mhe. Mwema alishuhudia mapokezi makubwa na bashasha kutoka kwa wananchi kufuatia hatua ya Serikali kutegua kitendawili cha muda mrefu cha ukosefu wa shule ya sekondari katika kata hiyo.

Serikali tayari imeanza ujenzi wa Shule Mpya ya Sekondari Laiseri, ambayo itakuwa shule ya kwanza ya sekondari katika kata hiyo.Mapema akizungumza na wananchi, Mhe. Mwema alisema:

_“Serikali imekata kiu kwa wananchi wa Kata ya Laiseri kufuatia hitaji la shule ya sekondari. Tambueni kwamba vijiji na kata zote zina usawa kimtazamo linapokuja suala la maendeleo ya wananchi, sasa Serikali imetekeleza kwa vitendo. Wito wetu kwenu ni kuendelea kutoa ushirikiano katika kipindi chote cha utekelezaji wa mradi huu,”Alisema.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mwema alitembelea na kukagua maendeleo ya miradi ifuatayo:

Ujenzi wa Shule Mpya ya Sekondari Mbeli – Kata ya Partimbo, wenye thamani ya Shilingi milioni 584.

Ujenzi wa Bweni katika Shule ya Sekondari Engusero, wenye thamani ya Shilingi milioni 204.

Ujenzi wa Shule Mpya ya Sekondari Laiseri, wenye thamani ya Shilingi milioni 584.

Miradi hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuhakikisha wananchi wa maeneo yote wanapata huduma bora za elimu.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Wilaya amesema hakuna Kijiji au kata ambayo inasahaulika linapokuja suala la maendeleo, Ujenzi wa Sekondari Laiseri ilikuwa ni hitaji muhimu na muda mrefu kwa wananchi wa kata  Laiseri, leo Serikali imetekeleza hitaji hili kubwa na itaendelea kugusa maisha ya Wananchi wote Wilayani Kiteto.






 


Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo