Nafasi Ya Matangazo

August 20, 2026




Na, Mwandishi wetu – Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu–Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi, amewataka wananchi kuzingatia tahadhari na maelekezo yanayotolewa na wataalamu na mamlaka husika ili kupunguza madhara yanayotokana na majanga na maafa.

Prof. Kabudi ametoa wito huo tarehe 19 Agosti, 2026 wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Watoa Huduma za Misaada ya Kibinadamu Duniani yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

“Ushiriki wa wananchi ni muhimu katika kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya majanga, huku akiwataka kuendelea kufuata taarifa na maelekezo rasmi kutoka kwa wataalamu na mamlaka zinazohusika na masuala ya maafa.”

Katika hatua nyingine, alisema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema na kujenga ustahimilivu wa jamii ili kuongeza uwezo wa wananchi kukabiliana na majanga na kupunguza madhara yanayotokana na matukio hayo.

Alisema uwezo wa nchi katika kukabiliana na majanga kwa ufanisi unategemea uwepo wa mifumo madhubuti, uratibu na ushirikiano wa karibu na wenye tija kati ya Serikali na wadau wa huduma za kibinadamu.

Prof. Kabudi pia alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake katika kusimamia masuala ya kibinadamu na ustawi wa wananchi.

“Kupitia uongozi wa Rais Dkt. Samia, Serikali imeendelea kuhakikisha wananchi wanaokumbwa na changamoto za majanga wanapata msaada na faraja wakati wa dharura.”

Prof. Kabudi aliwataka watoa huduma za kibinadamu kuwekeza zaidi katika kuwawezesha wananchi kwa elimu na taarifa sahihi kuhusu vihatarishi vinavyowazunguka, pamoja na hatua za kuchukua kabla, wakati na baada ya janga.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Dkt. James Kilabuko, amesema maadhimisho ya siku hiyo yanatoa fursa ya kutambua na kuthamini mchango wa watoa huduma za kibinadamu ambao hujitolea kwa moyo wa huruma, ujasiri na mshikamano katika kuokoa maisha na kupunguza madhara.

Alisema ni muhimu kuendelea kuimarisha ushirikiano na mshikamano miongoni mwa Serikali, wadau wa huduma za kibinadamu na jamii katika kuhakikisha kuwa msaada unapatikana kwa wakati na unawafikia wale wanaouhitaji.

“Ni muhimu kuhakikisha kuwa katika kila hatua ya utoaji wa huduma za kibinadamu, maisha, usalama na utu wa mwanadamu vinaendelea kuwa kiini cha hatua tunazochukua.”
=MWISHO=
Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments

August 19, 2026






Na. Mwandishi Wetu - Shinyanga
SERIKALI imesema itaendelea kuongeza nguvu katika mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU), kwa kuboresha vituo vya huduma, kuwezesha vikundi na kuimarisha ushirikiano na wadau, ili kuhakikisha Tanzania inafikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dk. Jim Yonazi, wakati wa ziara yake mkoani Shinyanga, ambapo alitembelea vikundi mbalimbali vya vijana vinaoishi na Maambukizi ya VVU pamoja na Kituo cha Maarifa Kahama kilichopo Kagongwa mkoani humo.

Dk. Yonazi amesema juhudi zinazofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau zimeanza kuzaa matunda, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza kasi katika utoaji wa elimu, upimaji, ushauri nasaha, pamoja na huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.

“Lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma karibu nao, lakini vilevile wanapata elimu inayowasaidia katika mapambano dhidi ya UKIMWI
na maambukizi ya UKIMWIi,” amesema.

Amesema Serikali imeendelea kuboresha huduma hizo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa wakati, huku akiwataka wadau kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha afua za kukabiliana na VVU.

Dkt. Yonazi amepongeza Mkoa wa Shinyanga kwa kufikia malengo ya kimataifa ya 95-95-95, akisema hatua hiyo ni ishara ya mafanikio katika jitihada za kupunguza maambukizi mapya na madhara yatokanayo na VVU.

“Serikali imeamua kwa makusudi kabisa kuongeza nguvu yake. Ndiyo maana imeanzisha Mfuko wa Mfadhili, na asilimia 70 ya fedha hiyo inakwenda katika Mfuko wa UKIMWI ili kusaidia afua mbalimbali na kuondokana na utegemezi,” amesema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Mhe. Mbona Mahita, alisema mkoa huo bado una kiwango cha maambukizi ya VVU kilicho juu ya wastani wa kitaifa, ambapo Shinyanga ina asilimia 5.6 ikilinganishwa na asilimia 4.4 ya kitaifa.

Mahita alisema Serikali imeendelea kuongeza elimu kuhusu VVU katika ngazi mbalimbali, kuanzia kaya hadi jamii, ili wananchi wawe na uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kujikinga na maambukizi.

“Shinyanga ni business hub kwa Kanda ya Ziwa. Movement za watu mara kwa mara ni kubwa. Watu wanaoingia na kutoka ni wengi, ndiyo maana tumeshuka mpaka kwenye ngazi za kijamii katika utoaji wa elimu,” alisema.

Awali, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Dk. Honoratha Rutatinisibwa, alisema mkoa huo una vituo 374 vinavyotoa huduma za afya, ambapo vituo 120, sawa na asilimia 32, vinatoa huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.

Dkt. Rutatinisibwa amesema, kwa mujibu wa utafiti wa maambukizi ya VVU uliofanyika mwaka 2023, kiwango cha maambukizi mkoani Shinyanga ni asilimia 5.6, ikilinganishwa na wastani wa kitaifa wa asilimia 4.4.

Akizungumzia huduma zinazotolewa katika Kituo cha Maarifa Kahama kilichopo Kagongwa, Mratibu wa Kudhibiti Maambukizi ya VVU, Homa ya Ini na Magonjwa ya Ngono Kahama, Dkt. Herry Silvester, amesema kituo hicho kinatoa huduma za tiba na matunzo, pamoja na huduma maalumu kwa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi.

Amesema makundi hayo ni pamoja na madereva wa masafa marefu, mabinti na wanawake vijana, ambao wamekuwa wakifikiwa kupitia huduma za upimaji, elimu na ushauri nasaha.
Posted by MROKI On Wednesday, August 19, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu
Ushirikiano baina ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), umeelezwa kuwa na manufaa mengi yenye mchango wa kukuza maendeleo baina ya nchi hizo mbili. 

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu (MCC), Mary Chatanda, Agosti 18, 2026.

Chatanda amesema, ziara ya siku mbili ya Rais Felix Tshisekedi wa DRC Kongo nchini Tanzania ni kielelezo cha uhusiano mzuri ambao hauishii kuwa urafiki wa kawaida bali nyenzo ya kushirikiana katika kukuza uchumi na maendeleo.

"Rais Dk. Samia na mwenzake Tshisekedi wamekubaliana kushirikiana katika kuboresha sekta za uchukuzi, madini, nishati, uwekezaji, biashara, barabara, bandari, usafiri wa majini, jambo linaloongeza kasi ya ukuaji uchumi," amesema.

Aidha, Chatanda amehimiza uzingatiaji wa maslahi ya wananchi katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa nchi zote.

"Wananchi wetu wanapaswa kunufaika na fursa za uchumi katika sekta za ushirikiano, ili maendeleo yawe jumuishi kwa serikali na wananchi wake," amesisitiza.

Katika hatua nyingine, Chatanda amempongeza Rais Dk. Samia kwa kuendelea kuifungua nchi kwa kuhimiza diplomasia ya kiuchumi kwa kushirikiana na mataifa mbalimbali duniani.

"Nampongeza Rais wetu Dk. Samia kwa namna anavyoshirikiana na mataifa mengine, kwa kufanya hivyo, tunaongeza wigo wa kupata fursa za biashara na uwekezaji," ameongeza.
Posted by MROKI On Wednesday, August 19, 2026 No comments

August 18, 2026








Na. Mwandishi Wetu, Mwanza
Serikali imedhamiria kuendelea kuimarisha afua za masuala ya UKIMWI nchini kwa kuboresha mazingira ya utekelezaji wa shughuli hizo, huku ikihimiza ushirikiano na wadau mbalimbali katika kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, alipotembelea na kujionea utekelezaji wa shughuli zinazotekelezwa na vikundi vya watu wanaoishi na Maambukuzi ya Virusi vya UKIMWI katika Wilaya ya Nyamagana, Jijini Mwanza.

Akiwa katika ziara hiyo, Dkt. Yonazi amesema Serikali imeendelea kuboresha mazingira na kutenga bajeti inayosaidia kuratibu na kutekeleza afua za masuala ya UKIMWI nchini, huku ikishirikiana na wadau mbalimbali.

“Ushirikiano ni muhimu sana kwani, tunaamini unauwezo wa kutuvusha katika mapambano dhidi ya VVU, ambapo tumeendelea kuunganisha nguvu pamoja katika mapambano hayo,” alisema Dkt. Yonazi.

Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu, yenye dhamana ya kuratibu shughuli zote za Serikali, ikiwemo masuala ya UKIMWI, itaendelea kuhakikisha vifaa na huduma zinatolewa kwa wakati na ubora kwa WAVIU, huku kanuni na taratibu za afya zikizingatiwa.

Dkt. Yonazi Ametumia jukwaa hilo kuiasa jamii kuendelea kupima afya ili kujitambua na kuchukua hatua za mapema endapo mtu atabainika kuwa na maambukizi ya VVU, ili aweze kuishi kwa tahadhari na kuwalinda wengine.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Ndugu Balandya Elikana, amesema kuwa mkoa umechukuwa hatua madhubuti kuimarisha mapambano dhidi ya UKIMWI kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya afya na kamati za utekelezaji wa mikakati ya kuzuia maambukizi, huku wakihimiza upatikanaji wa huduma bora na elimu kwa jamii. 

“Jamii inaendelea kuhamasishwa kuhusu upimaji wa afya kwa hiari na matumizi sahihi ya njia za kujikinga na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI pamoja na kuendelea kushirikiana kwa karibu na mashirika na wadau wa afya ili kuboresha huduma za kinga na tiba,” alisema Elikana

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dkt. Kheri Kagya, akiwasilisha taarifa ya hali ya UKIMWI mkoani humo, amesema Mkoa wa Mwanza una kiwango cha maambukizi ya VVU cha asilimia 4.7, ikilinganishwa na kiwango cha kitaifa cha asilimia 4.4, kwa mujibu wa matokeo ya Utafiti wa Kitaifa wa THIS 2022/2023.

Alisema kwa mujibu wa taarifa ya DHIS2 Annual Report ya mwaka 2025/2026, Mkoa wa Mwanza unakadiriwa kuwa na idadi ya watu wanaoishi na VVU (WAVIU) 112,685.

“Mkoa, kwa kushirikiana na wadau, umeendelea kutoa elimu ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya VVU kwa kuhamasisha matumizi sahihi ya kondomu. Katika kipindi cha mwaka 2025/2026, Mkoa ulisambaza jumla ya kondomu 2,265,772 katika jamii, hususani sehemu za kulala wageni, sehemu za kuuzia vileo (baa), kumbi za starehe na kwenye mikusanyiko mbalimbali,” alisema.
Posted by MROKI On Tuesday, August 18, 2026 No comments

August 16, 2026

Na: Dk. Reubeni Lumbagala 
Katika maisha ya kawaida ya mwanadamu, kuna kuweka malengo ili kufikia mafanikio. Inapotokea malengo yametimia, moyo hujaa furaha kwani mlango wa kufanikiwa unakuwa umefunguka.

Haya ndiyo yaliyotokea kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Kwa TRA, mwaka wa fedha 2026/2027 umeanza vizuri. Hii ni kufuatia Mamlaka hiyo kukusanya shilingi trilioni 3.245 kwa mwezi Julai, 2026, ambapo makusanyo hayo ni sawa na asilimia 109 ya lengo la kukusanya trilioni 2.971 kwa mwezi huo.

Ni kwamba; mwaka mpya wa fedha huanza Julai 1 ya kila mwaka. Hivyo mwezi wa kwanza wa mwaka mpya wa fedha ni kuanzia Julai 1 hadi 31. Kwa malengo ambayo TRA ilijiwekea, ni kukusanya shilingi trilioni 2.971, lakini lengo hilo limetimia na kuzidi, ambapo zimekusanywa shilingi trilioni 3.245. 

Kimsingi, bajeti iliyopitishwa na bunge kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ni shilingi trilioni 62.33, ambapo asilimia 74 ya fedha hizo zinategemewa kukusanywa kupitia mapato ya ndani (own sources).

Katika fedha hizo, TRA inawajibika kukusanya shilingi trilioni 41.08, sawa na asilimia 67 ya bajeti nzima katika kipindi cha Julai 1, 2026 hadi Juni 30, 2027.

Akiwa katika hafla ya Uwekezaji wa Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya TRA, Kizimkazi, Zanzibar, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Omar, ameipongeza TRA kwa kufanikiwa kukusanya shilingi trilioni 3.245 kwa mwezi Julai, 2026.

Naye, Kamishna Mkuu wa TRA, CPA Yusuph Mwenda, amesema wanaendelea kuwahudumia vyema walipakodi na kutatua changamoto zao ili Mamlaka ifanikishe malengo.

"Kutokana na usimamizi wako mzuri Mheshimiwa Waziri wa Fedha na ushirikiano na walipakodi, tunakuhakikishia tutavuka lengo hilo na kupitia, ishara inaonyesha kwamba tumeanza mwaka wa fedha kwa nguvu kubwa na tuna imani tutafikia na kuvuka malengo tuliyowekewa," amesema CPA Mwenda.

MAMBO YA KUZINGATIA KATIKA SAFARI YA UKUSANYAJI MAPATO WENYE TIJA

Mosi, kufanya malipo kwa njia za kieletroniki. Moja ya mabadiliko ya sheria za kodi ni pamoja na kuhimiza malipo ya kieletroniki ili kuendana na uchumi wa kidijitali unaoachana na matumizi ya fedha taslimu (cashless economy). Ni muhimu kufanya malipo kwa njia za kieletroniki kama simu na benki.

Pili, kudai na kutoa risiti halali ya kieletroniki. Ni muhimu kwa mnunuaji kudai risiti pale anapofanya malipo na muuzaji nae atoe risiti halali ya kieletroniki (EFD), ili serikali ipate kodi yake halali. Mmoja kati ya hawa wawili au wote wawili wasipotimiza wajibu wao, serikali itakosa mapato, na hivyo kushindwa kutimiza kikamilifu malengo ya kuwahudumia wananchi.

Tatu, kuwa waaminifu katika kurekodi taarifa za mauzo. Muuzaji anapaswa kuandika taarifa sahihi za mauzo ili Mamlaka iwe na taarifa sahihi za mwelekeo wa biashara au shughuli za uzalishaji zinazofanyika. Kwa mabadiliko ya sheria za kodi yaliyofanyika, udanganyifu katika uandishi wa taarifa za mauzo, adhabu yake ni mhusika kulipa mara mbili ya kiwango kilichofanyiwa udanganyifu.

Nne, kuboresha uhusiano baina ya walipakodi na TRA. Pamoja na mafanikio katika eneo la uhusiano, bado suala hili linapaswa kuhimizwa kwani walipakodi ndiyo waliobeba hatma ya maendeleo ya nchi yetu. Namna yeyote ya kuwapuuza, ni kuikosesha serikali mapato na kuua shughuli zao za uzalishaji ambazo zinachangia kutoa ajira na kuongeza mapato ya nchi.

Tano, kutoa makadirio ya kodi yanayoendana na kiwango cha biashara. Wakati mwingine, mfanyabiashara anaweza kufunga baishara pale anapokadiriwa kiwango kikubwa zaidi ya uwezo wa biashara yake. Hivyo basi, ukadiriaji kodi unapaswa kumwezesha mfanyabiashara kukua na si kumrudisha nyuma.

Sita, ajenda ya kujitegemea iwe ni ajenda ya kitaifa na si ya viongozi. Mwelekeo wa serikali ni kujitegemea kibajeti. Ajenda hii imefungamanishwa na ulipaji kodi wa hiari na wa kizalendo. Katika safari ya maendeleo ya nchi yetu wananchi na walipakodi kwa ujumla, tuone fahari kulipa kodi kwani kodi hizo ndizo zitakazotujengea heshima ya kujitegemea na kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na ya kimkakati nchini.

Saba, kutoa elimu endelevu ya kodi kwa walipakodi na wananchi. Elimu ya kodi izidi kutolewa ikizingatiwa serikali imefanya mabadiliko makubwa ya sheria za kodi. Elimu ya kodi itolewe kwa wanafunzi wa shule za msingi, sekondari na vyuo. Klabu za kodi ziimarishwe katika taasisi za elimu nchini. Pia, elimu hiyo itolewe sehemu za wazi kama sokoni, vituo vya mabasi ili kujenga uelewa mkubwa kwa wananchi. Pia, TRA iwafuate wafanyabiashara kule walipo kuwapa elimu ya kodi.

Ni faraja kuona mwaka mpya wa fedha umeanza kwa kishindo cha makusanyo yaliyozidi malengo yaliyowekwa. Nchi yetu itaendelea kupiga hatua kubwa za maendeleo endapo wananchi tutalipa kodi kwa uaminifu. Hakuna mwingine wa kutuletea maendeleo katika nchi yetu - ni sisi wenyewe tunawajibika, hivyo kodi zetu zitaamua maendeleo yetu. 

Mungu Ibariki Tanzania.

0620800462.
Posted by MROKI On Sunday, August 16, 2026 No comments

August 14, 2026







Na Mwandishi Wetu, Tanga
Katika kuhakikisha wafanyabiashara wanakuwa na uelewa wa kutosha kuhusiana na mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka 2026/2027, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Tanga, imetoa mafunzo kwa wafanyabiashara mkoani humo.

Mafunzo hayo yametolewa Agosti 12, 2026, katika Ukumbi wa YDCP Jijini Tanga. Katika mafunzo hayo, wafanyabiashara wamejengewa uwezo juu ya mabadiliko mbalimbali ya sheria za kodi yaliyofanyika ili kuiwezesha TRA kutekeleza majukumu waliyopangiwa na serikali kuu.

Akifungua mafunzo hayo, Meneja wa TRA mkoa wa Tanga, CPA. Castro John, amesema sheria zaidi ya 15 za kodi zimefanyiwa mabadiliko, hivyo wanalo jukumu la kutoa elimu kwa wafanyabiashara.

"Niwashukuru wafanyabiashara wa Tanga kwa kujitokeza kupata elimu hii muhimu kwani wafanyabiashara wanapokuwa na uelewa wa mabadiliko haya, basi utekelezaji wa ulipaji kodi utakuwa mwepesi," amesema CPA John.

Maofisa mbalimbali kutoka TRA Makao Makuu waliwaelimisha wafanyabiashara hao mabadiliko ya sheria mbalimbali za kodi ambazo utekelezaji wake una mchango wa moja kwa moja katika kufanikisha mipango mbalimbali ya kodi.

Naye, Afisa Elimu ya Mlipakodi na Mawasiliano kutoka TRA Makao Makuu, Hamisi Sanze, alitoa mada juu ya Sheria ya Kodi ya Mapato, amesema, serikali imedhamiria kuinua sekta ya madini ili iendelee kuchangia pato la taifa. 

Amesema, katika sura ya 332, serikali imetoa msamaha wa kodi ya mapato kwa mmiliki wa leseni ya uchimbaji wa madini (Mining licence) au leseni maalum ya uchimbaji madini.

Pia amesema, katika kuendelea kuweka mazingira wezeshi kwa sekta hiyo, Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) Sura 148 imeeleza kuwa, bidhaa na huduma zinazoangizwa au kununuliwa na mwenye leseni ya madini au leseni maalum ya madini zitapata msamaha wa kodi.

Aidha, msamaha huo utatumika kwa bidhaa na huduma zinazotumika katika ujenzi wa mradi wa madini na utakoma uzalishaji wa madini utakapoanza.

Katika hatua nyingine, Sanze amesema, kwa mujibu wa Sheria ya Ushuru wa Bidhaa, Sura 147; inafafanua kuwa, watoa huduma za mitandao wasio wakazi, wanatakiwa kujisajili, kupata TIN, kutoza, kuwasilisha ritani na kulipa ushuru wa bidhaa kwa huduma zinazotolewa.

Kwa upande wake, Afisa Mkuu Msimamizi wa Kodi, Salim Bakari, amesema kwa mujibu wa Sheria za Usimamizi wa Kodi, Sura ya 438 ni kwamba, mtu anayepaswa kulipa kodi kutokana na ajira, biashara na uwekezaji anatakiwa kuomba Namba ya Utambulisho wa Mlipakodi (TIN) ndani ya siku 15 tangu aanze shughuli hizo. 

Aidha, kifungu cha 73(4) kinaeleza, Kamishna Mkuu wa TRA, amepewa mamlaka ya kuuza bidhaa zilizokamatwa ambazo zinaharibika haraka kwa njia ya mnada au mauzo ya moja kwa moja

Sambamba na hilo, amesema kifungu cha 95, kinatoa onyo kwa mtu anayehusika kurekodi taarifa za uongo au zisizo sahihi kwenye vitabu vya hesabu, rejesta au mifumo, kwani kwa kufanya hivyo, atapaswa kulipa adhabu mara mbili ya kodi aliyokwepa au aliyopunguza kulipa.

Halikadhalika, Bakari, amewakumbusha wafanyabiashara wa Jiji la Tanga kuwa, serikali imetoa msamaha wa kodi kwa kipindi cha mwaka mmoja kwa mfanyabiashara anayeanza biashara kwa mtaji usiozidi milioni 200.

Pia, amewakumbusha, malipo ya ada za shule, utalii, tozo, bidhaa, huduma, ununuzi wa magari, mashamba, viwanja, yafanyike kieletroniki ili kuongeza ufanisi wa ukusanyaji mapato ya serikali.

Akihitimisha mafunzo hayo, Meneja Msaidizi Ukaguzi na Ufuatiliaji TRA mkoa wa Tanga, Daniel Ramadhani, amewasisitiza wafanyabiashara kulipa kodi kwa uaminifu mkubwa kwani ndizo zinazowezesha serikali kutoa huduma nzuri kama elimu, afya, maji, miundombinu, umeme kwa wananchi wake.

Pia, ametoa wito kwa wafanyabiashara na walipakodi kwa ujumla, kuwasilisha changamoto zao ili zifanyiwe kazi kwani wapo kwa ajili ya kuwahudumia.

Ikumbukwe kuwa, bajeti ya mwaka 2026/2027, TRA inapaswa kukusanya shilingi trilioni 41.80 ambayo ni sawa na asilimia 67 ya bajeti nzima ya shilingi trilioni 62.33. Bajeti hii ndiyo bajeti ya kwanza kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.
Posted by MROKI On Friday, August 14, 2026 No comments

August 13, 2026

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemjulia hali, Mama Fatma Karume,Mjane wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, ambaye anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Lumumba Zanzibar. Tarehe 13 Agosti 2026.


Posted by MROKI On Thursday, August 13, 2026 No comments
Mwenyekiti wa TASWA, Amir Mhando.
CHAMA cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), kimeandaa kampeni maalumu ijulikanayo kama ‘AFCON Kitaa 2027’, ambayo itazinduliwa rasmi Oktoba 30, 2026 jijini Dar es Salaam.

Kampeni hiyo ni mahususi kwa wanataaluma ya habari kwa ajili ya Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON), zitakazofanyika nchini mwaka 2027 na itahusisha matukio ambayo TASWA itayafanya kuelekea fainali hizo, ambazo Tanzania itaandaa kwa ubia na nchi za Kenya na Uganda.

Taarifa iliyotolewa na TASWA leo Agosti 13, 2026 na kusainiwa na Mwenyekiti wa wake, Amir Mhando imesema,Kampeni ya AFCON Kitaa 2027 itawafikia makundi yote katika jamii ili kuwapa hamasa ya kuchangamkia fursa za kufanyika ka
Wa michusno hiyo nchini.

"Kampeni ya AFCON Kitaa 2027 inatarajia kufikia makundi mbalimbali kuanzia wanahabari, wanamichezo, wanasiasa, wafanyabiashara, watumishi wa umma, wajasiriamali, vijana, wanawake na wanafunzi kuyataja kwa uchache, lengo Watanzania wote tuimbe wimbo mmoja kwamba AFCON 2027 ni fursa ya kitaifa," imesema sehemu ya taarifa hiyo.

Pia kuelekea uzinduzi rasmi wa AFCON Kitaa 2027, TASWA itaendesha warsha na makundi ya wanahabari kwa awamu tofauti, ikiwa ni mwendelezo wa mpango wake iliouanzisha Aprili, 2026 jijini Dar es Salaam ujulikanayo kama Mustakabali wa Uandishi wa Habari za Michezo 'The Future Of Sports Journalism’.

Makundi hayo ni waandishi wa habari chipukizi, waandishi wa habari waandamizi, wachambuzi wa habari za michezo, wahariri wa habari za michezo. Pia itakutana na viongozi wa michezo wa sasa na wa zamani, lengo ikiwa ni kutazama mwelekeo wa uandishi wa habari za michezo na pia ujio wa AFCON Kitaa 2027.

Aprili 24, 2026 TASWA ilianza Awamu ya Kwanza ya Mpango wa Mustakabali wa Uandishi wa Habari za Michezo kwa kuendesha warsha iliyohusisha wanahabari chipukizi, wahariri wa habari za michezo na waandishi magwiji wa habari za michezo, ambapo mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwemo masuala ya rushwa kwenye michezo iliyotolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Posted by MROKI On Thursday, August 13, 2026 No comments

August 12, 2026

 

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Asha-Rose Migiro, amefungua rasmi Tawi la CCM Kibuteni, Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja, leo tarehe 12 Agosti 2026.

Tawi hili lina historia kubwa tangu nyakati za ASP na TANU, na ni jambo la kujivunia kuona sasa lina sura mpya inayokwenda sambamba na mahitaji na hadhi ya Chama.

Dkt. Migiro amewahimiza viongozi na wanachama kuhakikisha Tawi hilo linakuwa kituo cha uhai wa Chama, mshikamano, mafunzo, vikao na utekelezaji wa shughuli za Chama.

Pia, Katibu Mkuu amewashukuru wana-CCM wa Kibuteni kwa mapokezi mazuri, upendo na zawadi.




Posted by MROKI On Wednesday, August 12, 2026 No comments


Dodoma
Jaribio la kwanza la Mbegu ya viazi mviringo lililotafitiwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) limeonesha mafanikio makubwa mkoani Dodoma katika shamba la Makamu wa Rais Mstaafu  Mhe. Dkt Philip Mpango lililopo Kijiji cha Mayamaya, Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.

Jaribio hilo lililochukua  siku 104 za majaribio shambani hadi kuvuna limedhihirisha kuwa zao la viazi mviringo linaweza kustawi katika mazingira ya  Mkoa wa Dodoma na kuufanya Mkoa huo kuwa na fursa mpya ya zao la chakula na biashara ambalo linaweza kuwasaidia wananchi wa mkoa huo kuondokana na umasikini.

Akiongelea  kuhusu jaribio hilo na matokeo yake,  Makamu wa Rais  Mstaafu Mhe. Dkt. Philip Mpango, ameishukuru TARI kwa kusimamia jaribio hilo ambalo kwa mara ya kwanza limeonyesha mafanikio  katika Kijiji cha Mayamaya na kuwataka wakazi wa Mkoa wa Dodoma kuchangamkia fursa ya kulima zao hilo pindi utafiti utakapokamilika.

“ Wakazi wa  Dodoma sasa tuanze kuchangamkia hii fursa na TARI wako tayari kutusaidia kwa kutupatia mbegu bora zinazofaa zaidi na hii itatusaidia chakula na kipato kwa ajili ya kusaidia watoto wetu kwenda shule. Dodoma sio nusu jangwa, ni maarifa tu ya kupata na kuvuna maji kwa ajili ya kuendeleza kilimo chetu, hatuwezi kuendelea kwa kutegemea mtama, mahindi, zabibu au alizeti pekee lazima tuongeze na mazao mengine” alisema Mhe. Dkt. Mpango.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TARI, Dkt. Thomas Bwana amemshukuru Mhe. Dkt. Mpango kwa kukubali TARI kuweka jaribio  la viazi mviringo katika shamba lake  lililopo katika Kijiji cha Mayamaya na kueleza kuwa  kwa sasa TARI imepanga kuweka majaribio ya zao hilo kwa wakulima wadogo wanaolima kwa kutegemea mvua.

Katika hatua nyingine Dkt. Bwane ameongeza kuwa  TARI itaendelea na majaribio ya utafiti wa mazao katika maeneo mbalimbali nchini  ili kuondoa dhana iliyojengeka ya  ikolojia  hii ni ya mazao Fulani pekee na kuwaomba wananchi hususan wakulima  kuwakaribisha TARI kuweka majaribio ya utafiti katika mashamba yao.

Kwa mujibu wa Mtafiti Kiongozi  wa zao la viazi mviringo kutoka kituo cha TARI - Uyole Dkt. Owekisha Kwigizila, mbegu hiyo  mpya ya TARI ina sifa ya kukomaa kwa muda mfupi wa takribani siku 90, kustahimili ukame na baadhi ya magonjwa pamoja na kuwa na uwezo wa kuzalisha tani 35 hadi 40 kwa hekta moja.

Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Mayamaya walioshiriki katika zoezi la uvunaji wa viazi hivyo wameonesha kustaajabishwa na kustawi kwa zao hilo katika Kijiji hicho cha Mayamaya na kueleza kuwa hiyo ni mara yao ya kwanza kuona zao hilo la viazi likilimwa  na kustawi Mkoani Dodoma na kuonyesha shauku kubwa ya kujaribu kulima zao hilo katika mashamba yao,

Utafiti huo wa zao la viazi Mkoani Dodoma bado unaendelea ili kukamilisha hatua zote muhimu kabla ya mbegu hiyo kuingizwa rasmi sokoni. Mafanikio hayo yanaendelea kuthibitisha kuwa Dodoma inaweza kuzalisha mazao mbalimbali ya chakula na biashara kupitia nguvu ya utafiti, ubunifu na teknolojia za kilimo  na kubadilisha maisha ya wakulima wa Mkoa wa Dodoma.
Posted by MROKI On Wednesday, August 12, 2026 No comments


 

Posted by MROKI On Wednesday, August 12, 2026 No comments

August 10, 2026



Kuelekea Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii nchini, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limewataka Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lyoto kutoa taarifa za uhalifu.

Wito huo umetolewa Agosti 10, 2026 na Polisi Kata ya Ilemi Mkaguzi wa Polisi Elibariki Mambuye wakati akizungumza na Walimu na Wanafunzi hao na kuwahimiza kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za uhalifu ili kuzuia vitendo hivyo katika jamii.

Aidha, Mkaguzi wa Polisi Mambuye amewaeleza Walimu na Wanafunzi wa Shule hiyo kuhusu Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii ambayo yatafanyika kitaifa Mkoani Mbeya yakiwa yamebeba kauli mbiu inayosema, Miaka 20 ya Polisi Jamii: Tushirikiane kuimarisha Amani, Usalama na Umoja wa Kitaifa.
Posted by MROKI On Monday, August 10, 2026 No comments

Timu ya mpira wa miguu ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya imeibuka bingwa wa mashindano ya mpira wa miguu kanda ya nyanda za juu kusini baada ya kuwafunga goli moja kwa bila Polisi Mkoa wa Songwe.


Akizungumza mara baada ya fainali hiyo iliyochezwa Agosti 10, 2026 Mkoani Rukwa, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Benjamin Kuzaga amesema kuwa ushindi huo umetokana na maandalizi mazuri ya timu, umoja na mshikamano.

Aidha, Kamanda Kuzaga amewapongeza wachezaji, benchi la ufundi na vikundi vya hamasa kwa kila mmoja kutimiza wajibu wake hadi kupata matokeo mazuri na kusisitiza nidhamu kuelekea maandalizi ya Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii ambapo timu hiyo itashindana na timu kutoka kanda nyingine.

Mashindano hayo ya kikanda yalifunguliwa rasmi Agosti 09, 2026 yalishirikisha timu za mpira wa miguu, mpira wa pete, riadha, kuvuta kamba na michezo mingine ya jadi ikijumuisha mikoa ya Rukwa (Mwenyeji), Mbeya, Songwe na Katavi ikiwa ni maandalizi ya Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii yatakayofanyika Agosti 25, 2026 Mkoani Mbeya yakibeba kauli mbiu inayosema, Miaka 20 ya Polisi Jamii: Tushirikiane kuimarisha Amani, Usalama na Umoja wa Kitaifa.






 

Posted by MROKI On Monday, August 10, 2026 No comments

Fundi Mussa Malale akielekeza jambo kwa msimamizi wake katika mradi wa ujenzi wa Uwanjha wa Ndege wa Kimataifa wa  Msalato Mkoani Dodoma.

Na Ssgt Mawazo Mtondo - DODOMA
Jeshi la Magereza linaendelea kutoa Programu mbalimbali za Urekebishaji kwa Wafungwa ili kuwapa ujuzi utakaowasaidia kujitegemea kwa kujiajiri au kuajiriwa pindi wamalizapo vifungo magerezani.

Magereza Tanzania Habari, tumefanya mahojiano na aliyekuwa mfungwa, Ndugu Mussa Malale, ambaye ni miongoni mwa wanufaika wa programu za urekebishaji zinazotekelezwa na Jeshi la Magereza.

Akizungumza katika mahojiano hayo, Ndg. Malale amesema kipindi chote alichokuwa gerezani alipewa mafunzo mbalimbali ya ufundi stadi, ikiwemo ufundi wa viyoyozi (Air Conditioning – AC), yaliyotolewa na wakufunzi wenye uzoefu na kumjengea ujuzi uliokuwa msingi wa mafanikio yake baada ya kumaliza kifungo.

Amesema baada ya kuachiliwa huru alianza kufanya kazi ya kuendesha gari la kubeba mchanga, lakini shughuli hiyo ilisimama baada ya gari kuharibika. Baadaye, rafiki yake alimshauri kutafuta kibarua katika mradi wa ujenzi wa Uwanja wa Ndege Mpya wa Msalato jijini Dodoma.

Malale, amesema alifanyiwa majaribio ya vitendo na kufanikiwa kuonesha uwezo wake, hatua iliyomwezesha kupata kibarua na kushiriki katika kazi za ufungaji wa viyoyozi katika mradi huo mkubwa, ambapo ametoa shukrani kwa Jeshi la Magereza kwa kumpatia ujuzi ambao hakuwa nao kabla ya kuingia gerezani.

Ushuhuda wa aliyekuwa Mfungwa, Ndg. Mussa Malale ni ushahidi wa mafanikio ya programu za urekebishaji zinazotekelezwa na Jeshi la Magereza, zinazowapa wafungwa elimu, mafunzo ya ufundi stadi na stadi za maisha zinazowawezesha kujitegemea, kupata ajira na kurejea katika jamii wakiwa raia wema wenye mchango chanya kwa maendeleo ya Taifa.

Usikose kufuatilia kampeni ya "MAGEREZA NURU YA MABADILIKO" kupitia kipindi cha Jambo Tanzania kinachorushwa na TBC kila siku kuanzia saa 12:00 asubuhi hadi saa 3:00 asubuhi, ili upate simulizi na ushuhuda wa mafanikio ya shughuli za urekebishaji zinazotekelezwa na Jeshi la Magereza.
Posted by MROKI On Monday, August 10, 2026 No comments

August 09, 2026



Na WMA - DODOMA.
Wakala wa Vipimo (WMA) umemhakikishia Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Mhe. Selemani Mwendwa kuwa utaongeza kasi ya utendaji kazi wa masuala ya vipimo katika wilaya hiyo ili kulinda uchumi wa wakulima na wafugaji.

Hakikisho hilo limetolewa jana Agosti 8, 2026 alipotembelea banda la WMA kwenye Maonesho ya 33 ya Wakulima Nane Nane, Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Dodoma, na kupatiwa elimu ya vipimo.

Meneja wa WMA Mkoa wa Singida, Bw.  Willie Amosi alisema kuwa "WMA itashirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya kuratibu na kutoa elimu ya vipimo katika maeneo mbalimbali ya Iramba kwa  lengo la kufikia wakulima wa mahindi, alizeti na pamba pamoja na wafugaji kwenye minada na masoko.

Aidha,  alimjulisha  Mkuu wa Wilaya kuwa WMA  itajipanga ili  kuanzisha Klabu za Vipimo (Vipimo Clubs) katika shule mbalimbali  za msingi na sekondari ikiwa ni mikakati ya kufika Tanzania nzima, hususan Tanzania Bara ambao ndiyo uwanda wa WMA. 

Vilevile, Meneja Amosi alisema kuwa WMA itaendelea  kushirikiana na ofisi ya Mkuu wa Wilaya ili wananchi wa Iramba waweze kuripoti moja kwa moja matumizi ya vipimo visivyo rasmi vinavyotumika katika masoko  na kwamba hatua za kisheria zitachukuliwa kwa uharaka

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya alisema:  
“Nimefurahishwa sana. Kama Serikali ya Wilaya tuko tayari kushirikiana na WMA ili kuhakikisha vipimo sahihi vinatumika na wananchi waweze kupata stahiki ya jitihada zao. Ningetamani Iramba iwe miongoni mwa   Wilaya zinazotumia vipimo sahihi katika sekta za kilimo.uvuvi pamoja na ufugaji.”

Wataalamu wa WMA walimkabidhi pia vipeperushi vyenye elimu ya vipimo ili vimsaidie kuendelea kujenga uelewa wa elimu ya vipimo.
Posted by MROKI On Sunday, August 09, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo