Waziri wa Madini, Mhe. Anthony P. Mavunde, amekutana na wawakilishi wa Chama cha Mabroka Tanzania (CHAMATA) katika kikao maalum kilicholenga kujadili changamoto na fursa zilizopo katika sekta ya madini pamoja na kuimarisha uwazi katika biashara ya madini nchini.
Kikao hicho kimefanyika leo Aprili 21, 2026, katika Ofisi za Tume ya Madini jijini Dodoma, ambapo pande zote mbili zilijadiliana kwa kina masuala ya usimamizi wa leseni za udalali, uwazi wa biashara ya madini na namna mabroka wanavyoweza kuongeza mchango wao katika kukuza uchumi wa taifa.
Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Mavunde amesisitiza umuhimu wa kuimarisha uwazi, kuzingatia sheria na taratibu pamoja na matumizi ya mifumo rasmi ya biashara ili kuongeza ufanisi na tija katika sekta ya madini.
Amebainisha kuwa Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha mazingira ya biashara ya madini kwa lengo la kuvutia uwekezaji zaidi na kuongeza mapato ya Taifa.
“Serikali itaendelea kusikiliza maoni ya wadau na kufanya maboresho yatakayochochea ukuaji endelevu wa sekta ya madini nchini.
Hatuwezi kupuuza mapendekezo na ushauri wa wadau wenye lengo zuri la kuboresha mazingira ya biashara, hivyo Tume ya madini fanyieni kazi kwa haraka baadhi ya mapendekezo ya kimfumo ambayo hayagusi sheria na taratibu” amesema Mavunde.
Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde ameonesha utayari wa serikali kufanya utafiti wa kina eneo la Lemshuku ambapo kuna madini mengi ya vito ili kuongeza fursa zaidi ya uchimbaji wa madini ya vito mkoani Manyara badala ya kutegemea madini ya Tanzanite pekee, akisisitiza kuwa kuna fursa nyingi za madini mengine ambazo zinapaswa kuendelezwa ili kupanua wigo wa biashara na kuongeza thamani ya sekta hiyo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Mabroka Tanzania, Jeremia Kituyo, amependekeza kuanzishwa kwa gulio maalum la madini litakalofanya kazi kwa mfumo wa mnada, likiwahusisha wafanyabiashara wa madini, wanunuzi wa ndani na nje ya nchi pamoja na wadau wengine wa sekta hiyo.
Amesema mfumo huo utasaidia kuongeza uwazi wa bei, kupanua masoko ya madini na kuhakikisha mabroka wanapata fursa sawa katika biashara ya madini nchini.

































.jpg)
.jpg)
.jpeg)

.jpeg)


















