Nafasi Ya Matangazo

February 16, 2026




WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza wajumbe wa Kamati Mapokezi na Kamati za Ujenzi za mradi wa ujenzi wa ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Muheza wakamatwe na kuhojiwa mara moja ili watoe taarifa juu ya upotevu wa vifaa vya mradi huo.

“Kuna nondo 700, Marine boards 500 na matofali 2,000... hivi vifaa havijulikani viko wapi. Wahusika kila siku mnaripoti kazini, na mishahara mnalipwa wakati ujenzi umesimama na hakuna hatua zinazochukuliwa,” amesema wakati akimhoji Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Dkt. Jumaa Mhina.

Ametoa agizo hilo leo (Jumatatu, Februari 16, 2026) wakati akizungumza na wananchi wa Lusanga, kata ya Mgomeni, wilayani Muheza waliofika kushuhudia uwekaji wa jiwe la msingi la ofisi hiyo itakayokuwa na ghorofa moja pindi ikikamilika.

“Kamanda wa TAKUKURU ninahitaji hii taarifa kwa kina kabla sijamaliza ziara yangu mkoani Tanga. OCD fuatilieni kwa kina ushiriki wa watumishi wa hii Halmashauri. Kila mmoja ahojiwe hadi tujue vifaa vilipoteaje.”

Amesema kuwa anazo taarifa kwamba timu ya manunuzi imenunua vifaa ambavyo vimewekwa stoo wakati hatua yake ya ujenzi haijafikiwa. “Nimeambiwa vifaa vingine vimekuja lakini vimekaa stoo tu. Ni kwa nini mmenunua wakati hamjamaliza hatua ya kwanza? Mshauri mwelekezi wa mradi yupo lakini hamsikilizi ushauri anaotoa,” alisema. 

Jengo hilo ndiyo limemalizika kujengwa ghorofa ya chini, na linasubiri kuanza kuwekewa linta kwenye ghorofa ya kwanza. 

Waziri Mkuu amekemea tabia ya kutochukua hatua masuala kama hayo yanapojitokeza hasa ikizingatiwa kwamba Halmashauri nyingine ambazo walipewa fedha kwa wakati mmoja wao wameshakamilisha kazi ya ujenzi.

Mapema, akitoa taarifa ya ujenzi wa mradi huo, Kaimu Mkuu wa Idara ya Miundombinu na Maendeleo Mijini na Vijijini, Mhandisi Abdalla Jaha alisema mradi huo ambao umefikia asilimia 68, ulianza kujengwa Septemba 29, 2023 na wanatarajia ifikapo mwishoni mwa Juni, 2026 sakafu ya chini ianze kutumika.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ametoa pongezi kwa kiwanda cha vifungashio cha Yogi PolyPack ambacho kiko Pongwe, nje kidogo ya Manispaa ya Tanga.

Akizungumza na viongozi na watumishi wa kiwanda hicho, Waziri Mkuu amesema uwekezaji uliofanywa ni mkubwa na kwamba serikali itaendelea kuhakikisha inatengeneza mazingira mazuri ya uzalishaji.

“Nimetembelea kiwanda, nimeona kazi nzuri ikiendelea na inatumia teknolojia ya kisasa. Haya ndiyo mambo Mheshimiwa Rais anataka kuyaona. Unatengeneza ajira, unazalisha bidhaa ambazo ni malighafi kwa viwanda vyetu hapa nchini na unatoa kipato kwa wafanyakazi wako,” amesema.

Mapema leo, Waziri Mkuu alitembelea bandari ya Tanga na kukagua shughuli za bandari hiyo na kisha kuzungumza na watumishi. 

Akiwa bandarini hapo, alipokea maelezo ya uboreshaji wa bandari hiyo kisha akatembelea eneo ambalo zitajengwa gati mbili mpya, katika bandari ya Tanga ikiwa ni mkakati wa Serikali ya kuiongezea uwezo bandari ya Tanga wa kutoa huduma shindani na za ufanisi.

Akizungumza na watumishi wa bandari ya Tanga, Waziri Mkuu aliahidi kwamba Serikali itahakikisha inaendelea kufanyia kazi changamoto zote za kiutumishi zinazowahusu watumishi hao.

“Serikali itaendelea kufanya maboresho katika bandari hii ili iweze kuhudumia idadi ya meli nyingi kwa kadiri inavyowezekana. Tunatambua ushindani wa kibiashara uliopo lakini tutaendelea kufanya maboresho ili tunufaike na nafasi ya kijiografia ya mkoa wetu,” alisema.

Pia ameiagiza Mamlaka ya Bandari ifanyia kazi changamoto ya uhaba wa vifaa vya kupakulia mizigo ili kuendana sambamba na maboresho hayo. 
Posted by MROKI On Monday, February 16, 2026 No comments

February 15, 2026









Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imetumia siku ya Valentine kwa kupeka tabasamu kwa wananachi wa mkoa wa Mwanza kwa kutoa Hatimiliki za Ardhi kwa watu ambao wamekamilisha taratibu zote za umiliki wa ardhi. 

Akizindua Kliniki ya Ardhi inayoendelea katika viwanja vya Ofisi ya Kata ya Igoma jijini Mwanza Februari 14, 2026, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya amesema wizara hiyo imepeleka tabasamu kwa wananchi wa Mwanza ambao wamekamilisha mchakato wa kupata Hati kwa kufuata taratibu zote za umiliki na eneo lake halina mgogoro na kupelekea kupata hati kwa muda mfupi.

“Inawezekana hati kutoka, hakuna madalali katika kupata hati, Watanzania tusigombanishwe na madalali katika mchakato wa kupata Hatimiliki ya Ardhi. Katika mchakato wa kupata hati hayupo dalali, huu ni muda wa kuwaletea wananchi tabasamu, tabasamu la wananchi wa Mwanza ni kupata hati” amesema Naibu Waziri Mmuya.

Ameongeza kuwa Kliniki ya Ardhi ni utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwaletea wananchi tabasamu.

Katika hatua nyingine, amewataka watendaji wa Sekta ya Ardhi kuwafuata watumishi wa sekta mbalimbali katika ofisi zao na kutumia fursa ya matukio yanayoendeshwa ndani ya maeneo yao kwa kutoa huduma za ardhi hatua inayowarahisishia wananchi hao kujisajili katika mfumo wa e-Ardhi ili kuwarahisishia mchakato wa kupata hati.

Katika kuendelea kuwapelekea tabasamu watanzania, Naibu Waziri Mmuya. amesisitiza kuwa Waziri ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo ameelekeza watumishi wa Ardhi mikoa yote Tanzania Bara kuendesha Kliniki ya Ardhi Maalum kwa wananwake kuanzia tarehe 2 – 7 Machi 2026 kuelekea maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake ambayo hufanyika kila tarehe 8 Machi kila mwaka ili kuendelea kuwaletea tabasamu watanzania katika maeneo mbalimbali nchini. 

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Amina Makilagi amesema Ofisi yake Pamoja na Mkuu wa Mkoa huo, wametenga siku za Jumanne na Alhamisi kila wiki kushughulikia changamoto mbalimbali na kuhakikisha wanamaliza migogoro iliyopo na kutokuzalisha migogoro mipya.

Naye mwananchi wa Kata ya Igoma jijini Mwanza ambaye amepokea hati ya kiwanja chake Bi. Zuwena Soudy amesema furaha yake ni kupokea hati ya kiwanja chake ambayo ataitumsaidia kiuchumi na sasa ana uhakika wa eneo lake lipo salama.

Naibu Waziri Mhe. Kaspar Mmuya yupo katika ziara ya kikazi mkoani Mwanza kuanzia tarehe 13 hadi 18 Machi 2026 ambapo atashiriki zoezi la Kiliniki ya Ardhi Igoma jijini Mwanza, Wilaya ya Ukerewe pamoja na halmashauri ya Buchosa katika Kijiji cha Kasisa.
Posted by MROKI On Sunday, February 15, 2026 No comments

February 14, 2026






Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amemwagiza Kamanda wa TAKUKURU Mkoa wa Tanga, Bw. Ramadhani Ndwatah afuatilie suala la gharama ya miradi kuongezeka na saruji kuganda kwa kisingizio cha kununuliwa kutoka mbali ili kubaini kama kuna mianya ya wizi.

"Kamanda wa TAKUKURU fanyia kazi hili eneo, hiki kichaka cha gharama kuongezeka kwa sababu ya umbali kinazidi kukua. Wanaomba nyongeza ya fedha wakati ilishatolewa yote. Hatuwezi kupoteza juhudi za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutafuta fedha za miradi halafu ninyi mnakuja kuzichezea," amesema. 

Ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Februari 14, 2026) wakati akizungumza na wananchi wa Kilindi mara baada ya kuweka jiwe la msingi la Hospitali ya Wilaya Kilindi iliyojengwa kwa gharama ya sh. bilioni 2.64.

Waziri Mkuu amesema kuna michezo inachezwa na watumishi wa umma ili kuhalalisha upotevu wa fedha ambapo watumishi wanadai kuwa vifaa vinaagizwa kutoka mbali. "Jana nikiwa Handeni nilisema kuhusu ujenzi wa VETA ambao umekwama kwa sababu mifuko ya saruji zaidi ya 1,200 imeganda. Tanga kuna kiwanda cha saruji lakini wao wananunua kutoka Dar es Salaam na Mbeya. Kuna miradi inajengwa Njombe nao wananunua saruji Dar es Salaam badala ya Mbeya ambako ni jirani zaidi. Kamanda fuatilia, nipate taarifa haraka."

Akielezea ujenzi wa hospitali hiyo, Waziri Mkuu amesema hospitali hiyo inatakiwa iwe na hadhi ya Mkoa ili ijitegemee kwani mgonjwa akipata dharura atapaswa kupelekwa Tanga mjini ambako ni mbali. Kilindi iko umbali wa kilometa 219 kutoka Tanga mjini.

Waziri Mkuu amesema ameridhishwa na ubora wa majengo katika hospitali hiyo, lakini akahoji ni kwa nini kuna upungufu wa majengo ikilinganishwa na idadi ya majengo tisa yaliyokuwa yamebajetiwa tangu awali.

"Majengo yaliyopo ni machache kuliko yaliyokusudiwa ikiwa fedha yote ya utekelezaji wa mradi ilitoka. Majengo yapo kwenye viwango vizuri, ila fedha iliyokuja ilikuwa ijenge majengo mengi zaidi lakini mmejenga pungufu, fedha nyingine ipo wapi? Michezo ya upotevu wa fedha za Serikali hatuwezi kuivumilia”

Alipoulizwa ni kwa nini idadi ya majengo haijatimia, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi, Bw. Kulwa Mgalula alisema walishindwa kupata majengo yote tisa kwa sababu gharama za manunuzi ziliongezeka kutokana na umbali wa eneo hilo. 

Mapema, akitoa taarifa ya ujenzi wa mradi huo, Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo, Dkt. Pendo Mang'ombe alisema gharama za mradi hadi sasa ni sh. bilioni 2.64 ambapo kati ya fedha hizo sh. bilioni 2.51 zimetoka Serikali Kuu, sh. milioni 50 ni za mapato ya ndani ya Halmashauri na sh. milioni 89.9 zimetoka Benki ya Dunia.

Alisema ujenzi wa hospitali hiyo umesaidia kuwapunguzia wananchi adha na gharama kubwa za matibabu ambazo walilazimika kuzifuata katika wilaya za jirani.
Posted by MROKI On Saturday, February 14, 2026 No comments

February 13, 2026

Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo (katikati) akiwa na viongozi wengine wa wa Serikali, Bunge, na Benki ya CRDB wakipata maelezo kutoka mwanzilishi wa kampuni ya Aquafresh iliyoshiriki katika maonesho ya biashara changa bunifu za vijana katika hafla ya uzinduzi wa programu ya Go Green Na IMBEJU inayolenga kuwezesha biashara na bunifu za kijani za vijana kama sehemu ya kuchochea uchumi wa kijani kuelekea Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050.
Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo (katikati) akipokelewa na kikundi cha ngoma za asili vacati alipowasili katika uzinduzi wa programu ya Go Green Na IMBEJU inayolenga kuwezesha biashara na bunifu za kijani za vijana kama sehemu ya kuchochea uchumi wa kijani kuelekea Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050. Wengine pichana ni kushoto kwake ni Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa, kulia kwake ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela.
Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo (wapili kushoto) akipata maelezo kutoka kampuni ya Kana Wine iliyoshiriki katika maonesho ya biashara changa bunifu za vijana katika hafla ya uzinduzi wa programu ya Go Green Na IMBEJU inayolenga kuwezesha biashara na bunifu za kijani za vijana kama sehemu ya kuchochea uchumi wa kijani kuelekea Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050. Wengine pichani ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori (watatu kulia), Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya CRDB, Dkt. Donald Mmari (wapili kulia), Mwenyekiti wa CRDB Bank Foundation, CPA Osward Urassa (wakwanza kulia), na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa.
Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo (wapili kushoto) akiwasili katika katika hafla ya uzinduzi wa programu ya Go Green Na IMBEJU inayolenga kuwezesha biashara na bunifu za kijani za vijana kama sehemu ya kuchochea uchumi wa kijani kuelekea Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050. Alioongozana nao ni Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, (katikati), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori (wapili kulia), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (wakwanza kushoto), na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Kitila Mkumbo, ameipongeza CRDB Bank Foundation pamoja na CRDB Bank kwa kuanzisha programu ya Go Green na IMBEJU, akisema ni hatua ya kimkakati inayounganisha ajenda ya Serikali ya uchumi wa kijani na uwezeshaji wa vijana nchini.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika katika ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Centre jijini Dodoma, Profesa Mkumbo alisema mpango huo unaendana na Dira ya Taifa 2050 inayolenga kujenga uchumi jumuishi, shindani na himilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, huku vijana wakitambuliwa kuwa nguvu kazi kuu ya maendeleo.

Alisema Serikali imeweka mkazo katika kukuza ubunifu wa vijana, uchumi wa kijani na ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi, akibainisha kuwa miradi ya vijana inayolinda mazingira ni utekelezaji wa moja kwa moja wa dira ya maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, alisema Go Green na IMBEJU ni daraja linalounganisha fedha za kimataifa za tabianchi na vijana wabunifu wanaokosa dhamana au historia ya mikopo katika mifumo ya kawaida ya kifedha. Alieleza kuwa kupitia programu ya TACATDP yenye thamani ya dola milioni 200 kwa ushirikiano na Green Climate Fund, zaidi ya Sh bilioni 100 tayari zimetolewa kufikia takribani wanufaika 600,000 kote nchini.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo, Tully Esther Mwambapa, alisema maombi ya programu yatafanyika kidijitali kupitia jukwaa la FursaHub kuanzia Februari 12 hadi Machi 11, 2026, yakilenga kuchuja miradi yenye uwezo wa kujiendesha kibiashara na kurejesha mitaji nafuu. Alibainisha kuwa mitaji itatolewa kuanzia Sh 500,000 hadi Sh milioni 500, huku miradi bora zaidi ikipata ruzuku ya kati ya Sh 500,000 hadi Sh milioni 10 kuongeza kasi ya ukuaji.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Naibu Spika wa Bunge, Daniel Sillo, alisema Bunge limeweka msingi wa kisheria unaounga mkono ulinzi wa mazingira na uchumi wa kijani, akitaja programu hiyo kuwa mfano halisi wa kuunganisha sera, mitaji na ubunifu wa vijana.

Kwa niaba ya vijana wanufaika, Irene Vambi, mwanzilishi wa Mrembo Naturals, alisema programu ya IMBEJU imemwezesha kubadili wazo la biashara kuwa uzalishaji unaokua na kutoa ajira kwa vijana wengine, akiwahimiza vijana nchini kutumia fursa hiyo kujenga mustakabali wao kiuchumi.

Uzinduzi wa Go Green na IMBEJU unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa mitaji nafuu, kuimarisha biashara bunifu za vijana na kuchochea uchumi wa kijani nchini, huku ukiongeza mchango wa sekta binafsi katika maendeleo endelevu ya taifa.

Ukitaka, naweza pia kukuandalia kichwa cha habari kikali cha ukurasa wa mbele, au toleo fupi la mtandaoni.
Posted by MROKI On Friday, February 13, 2026 No comments
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amekagua ujenzi wa mradi wa kupoza umeme uliopo Mkata, wilayani Handeni na kuweka jiwe la msingi la kituo hicho pamoja na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 132 kutoka Mkata kwenda Kilindi. mkoani Tanga

Waziri Mkuu ambaye yuko mkoani Tanga kwa ziara ya kikazi, amezindua pia ujenzi wa njia za kusambaza umeme msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 45 kutoka kituo cha Mkata kwenda kijiji cha Kwamsisi.

Akizungumza na wakazi wa Mkata waliofika kushuhudia tukio hilo leo (Ijumaa, Februari 13, 2026), Waziri Mkuu amemuagiza Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi afuatilie malipo ya hati ya madai ya zaidi ya sh. bilioni moja ya wakandarasi wa mradi huo ili ukamilike kwa wakati. 

Amesisitiza kuwa fedha ya Serikali inapotolewa inapaswa iende kufanya kazi iliyokusudiwa na akataka viongozi wasimamie matumizi ya fedha hizo. “Wakandarasi wote nchini wanapaswa kuhakikisha kuwa kiasi cha fedha kilipokelewa kiendane na kazi inayofanyika,” amesisitiza.

“Waziri wa Nishati fuatilia fedha hizo za wakandarasi ili zije haraka. Tunataka mradi wa umeme ukamilike, uende kule Kwamsisi ili viwanda vilivyopo kule vifanye kazi,” amesema.

Mapema, Waziri wa Nishati alisema ujenzi wa kituo hicho unatarajiwa kugharimu sh. bilioni 44 ambazo zitatumika kujenga kituo hicho cha kupoza umeme na kuweka tranforma mbili. 

Alisema Serikali imetoa sh. bilioni 73 kwa ajili ya mradi wa umeme wa REA katika vitongoji 559 kote nchini. “Hii ni awamu ya kwanza kwani tayari kuna vitongoji 4,553 nchini kote ambavyo tayari vina umeme sawa na asilimia 64 ya lengo la serikali.”

Naye Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Lazaro Twange alimweleza Waziri mkuu kwamba ujenzi wa mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa miradi ya kuimarisha gridi ya Taifa (maarufu kama Gridi Imara) ambapo serikali imetoa sh. bilioni 1.97 kugharimia miradi 27 ya aina hiyo kote nchini.

“Mradi huu ni miongoni mwa miradi ya uimarishaji wa Gridi ya Taifa wenye lengo la kuimarisha upatikanaji wa umeme katika wilaya za Handeni na Kilindi pamoja na kuimairisha hali ya upatikanaji wa umeme katika migodi ya graphite katika kijiji cha Kwamsisi,” alisema.

Akielezea faida za mradi huo, Bw. Twange alisema kukamilika kwa mradi huo kutaimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika Wilaya za Handeni na Kilindi; kutawezesha upatikanaji wa umeme kwenye eneo la migodi ya graphite hivyo kuongeza uzalishaji na kuchochea uchumi na kuongeza mapato kwa shirika hilo kupitia wateja wakubwa wanaotarajiwa kupatiwa huduma hiyo.

Mradi huo unafadhiliwa na Serikali ambapo sh. bilioni 44.14 ni kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha kupoza umeme na shilingi bilioni 5.75 ni kwa ajili ya ujenzi wa njia ya kusambaza umeme.
Posted by MROKI On Friday, February 13, 2026 No comments

February 12, 2026









Na WMJJWM – Arusha
‎Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mheshimiwa Dkt. Dorothy Gwajima, amepongeza mchango wa sekta binafsi na mashirika yasiyo ya kiserikali katika kuimarisha ustawi wa jamii, hususan watoto, vijana na familia, wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi ya SOS Children’s Villages Tanzania iliyofanyika Ngaramtoni, wilayani Arumeru mkoani Arusha.
‎Dkt. Gwajima amesema ameridhishwa na utekelezaji wa programu zinazolenga malezi chanya, ulinzi wa mtoto, maendeleo ya awali ya mtoto (ECD) na uwezeshaji wa kiuchumi kwa vijana na familia, akisisitiza kuwa jitihada hizo zinaendana na sera na miongozo ya Taifa. Amesema malezi bora na mazingira salama kwa watoto ni msingi wa kujenga Taifa imara.
‎Aidha, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali, mashirika ya kiraia na jamii katika kuhakikisha utekelezaji wa programu za maendeleo una matokeo endelevu, huku akiwataka wadau kuendelea kuzingatia mipango ya Taifa, hususan katika kukomesha ukatili dhidi ya wanawake na watoto.
‎Katika ziara hiyo, Waziri Gwajima ameshiriki kukabidhi pikipiki 15 zenye thamani ya shilingi milioni 40 kwa vijana wanufaika wa miradi ya SOS Children’s Villages Tanzania, akibainisha kuwa hatua hiyo inalenga kuwawezesha vijana kujitegemea kiuchumi kupitia ajira binafsi na ujasiriamali.
‎Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Mhe. Seleman Msumi, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuimarisha ustawi wa watoto, vijana na familia, akipongeza mchango wa SOS Children’s Villages Tanzania katika malezi, ulinzi wa mtoto na uwezeshaji wa vijana wilayani humo.
‎Naye Mkurugenzi wa SOS Children’s Villages Tanzania,  Thomas Kipng’ili, amesema kupitia Mradi wa Arusha Re-Innovation uliotekelezwa kwa miaka minne, shirika limewafikia vijana zaidi ya 1,000, ambapo 229 waliwezeshwa mitaji. Amesema mradi huo pia umewezesha walezi wa malezi mbadala 450, watoto 3,538 na familia 1,211 katika Halmashauri za Jiji la Arusha, Arusha DC, Meru na Karatu. Jumla ya shilingi milioni 173.5 zilitolewa kuwawezesha wanufaika 121, hatua iliyosaidia kuboresha ustawi wa watoto 346 waliokuwa katika mazingira hatarishi.
Posted by MROKI On Thursday, February 12, 2026 No comments



Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt.Asha-Rose Migiro, leo, Alhamis, Februari 12, 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Namibia hapa nchini, Mheshimiwa Gabriel Pandureni Sinimbo.

Mazungumzo hayo yamefanyika katika Ofisi Ndogo ya CCM, Lumumba, jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo yao, wamejadili masuala mbalimbali yenye lengo la kuendelea kuimarisha uhusiano wa kihistoria na urafiki wa kidugu kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha SWAPO, pamoja na uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Namibia.
Posted by MROKI On Thursday, February 12, 2026 No comments

February 11, 2026







Mtuhumiwa wa makosa nane ya kikodi Bw. Matondo Kilugala Malanda, mmiliki wa kampuni ya Matondo Breweries Investment Limited, iliyopo Wilaya ya Bukombe amefikishwa katika Mahakama Kuu mkoani Geita na kusomewa mashtaka nane ya kikodi yanayomkabili.

Mtuhumiwa huyo alifikishwa mbele ya Mahakama kuu Geita tarehe 10 Februari, 2026, ambapo shauri lake lilisikilizwa  na hakimu Mkazi Mhe. Cleofas Waane.

Akizungumza kuhusu shauri hilo, Wakili wa Serikali Bw. Emmanuel Cheneko amesema mtuhumiwa huyo anakabiliwa na makosa nane ya kikodi, ikiwemo kuanza uzalishaji bila kuwa na leseni halali, matumizi ya stempu bandia, kukutwa na bidhaa zinazopaswa kulipiwa ushuru wa bidhaa bila kulipiwa ushuru huo, pamoja na kushindwa kuandaa na kuwasilisha ritani za ushuru wa bidhaa kama inavyotakiwa kisheria.

Aidha, Meneja wa Idara ya Upelelezi wa Kodi Kanda ya Ziwa, Bw. Joel Mbilinyi, amewakumbusha wazalishaji wa pombe kali kuwa pamoja na kupata usajili kutoka BRELA, wanapaswa pia kupata leseni ya uzalishaji kutoka TRA kwa mujibu wa sheria, ili kuepuka kuchukuliwa hatua za kisheria.
Posted by MROKI On Wednesday, February 11, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Dennis Londo akizungumza na wafanyakazi wa FCC wakati alipotembelea Taasisi hiyo kwa ajili ya kujua majukumu ,jijini Dar es Salaam.
**************
Na Mwandishi Wetu 
Waziri wa Viwanda na Biashara Dennis Londo amesema Tume ya Ushindani (FCC) iendelee na majukumu  ya kusimamia ushindani katika kujenga imani ya walaji kwani sehemu ya huduma ndio wananchi wanapokutana na serikali

Londo aliyasema hayo wakati alipotembelea Tume ya Ushindani Jijini Dar es Salaam,amesema kuwa ushindani katika soko unajenga imani ya walaji kupata huduma zilizo bora na kufanya kuchangia uchumi wa nchi.

Amesema imani ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ni kuona Taasisi ya  FCC inaendelea kulinda ushindani nchini kwa taratibu na sheria zilizowekwa katika kuhakikisha walaji wanakuwa wa kwanza kutoa taarifa sahihi za huduma wanazozipata.

Aidha amesema kuwa katika kuhakikisha  wanalinda soko za bidhaa za ndani kwani Tanzania inafikiwa na mataifa mbalimbali hivyo bidhaa hizo zikitoka zikawa chini ya viwango kunafanya nchi kuathirika na kushindwa kupata fedha za kigeni.

Hata hivyo amesema kuwa wafanyakazi FCC kuendelea kutoa huduma bora ambazo zitachochea uwekezaji wa viwanda vitavyofanya kuendelea kuongeza ajira kwa vijana wa kitanzania.

Amesema matamanio ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kuona tija inaendelea kuongezeka katika malengo ya kukua kiuchumi na Dira ya Taifa 2050.

"Nina imani na FCC na Wizara tutaendelea kushirikiana katika kuwafikisha watanzania kwenye kupata huduma bora katika ushindani wa soko wenye uwazi bidhaa za ndani na nje ya nchi".amesema Londo 

Nae Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC) Khadija Ngasongwa amesema FCC imejipanga vyema kuendelea kushirikiana na  katika kutekeleza majukumu kwa mujibu wa sheria ili kuendelea kutoa huduma zenye tija kwa mlaji na Taifa kwa ujumla hususan katika masuala ya Ushindani, Udhibiti wa Bidhaa Bandia na Kumlinda Mlaji kwa lengo la kukuza ustawi wa uchumi jumuishi.

Khadija anesema  katika kutekeleza majukumu yetu kwa mujibu wa mamlaka tuliyopewa kisheria, Tume ya Ushindani (FCC) hufanya kazi kwa karibu na Wizara ya Viwanda na Biashara, Idara, Taasisi za Serikali, Wadau wa Maendeleo na Sekta Binafsi kwa kuzingatia dira na miongozo mbalimbali ya kisera, kitaifa na kimataifa ili kuhakikisha inatekeleza jukumu lake kama chombo cha usimamizi wa utendaji wa ufanisi wa uchumi wa soko kwa kulinda na kushajiisha uzingatiwaji wa misingi ya ushindani wa haki, kumlinda mlaji na kudhibiti bidhaa bandia katika soko la Tanzania Bara. 

Majukumu haya kwa pamoja yanalenga kulifanya soko kuwa shindani, salama na walaji wanajenga uaminifu katika bidhaa zinazoletwa sokoni na hivyo mazingira ya biashara kuchangia ukuaji endelevu na jumuifu katika uchumi na ustawi wa mtu mmoja mmoja.

Amesema FCC ina jukumu la kusimamia Ushindani katika Soko la Tanzania Bara kwa kuhakikisha kuwa inadhibiti makubaliano yanayofifisha Ushindani, matumizi mabaya ya nguvu ya soko na miungano ya kampuni inayolenga kuimarisha hodhi ya soko. Tume imepewa mamlaka ya kisheria ya kufanya uchunguzi endelevu (Inquisitorial Procedure) katika kushughulikia ukiukwaji wa Sheria ya Ushindani ambapo huweza kutoa maamuzi dhidi ya ukiukwaji huo, ikihusisha pia masuala ya kumlinda mlaji.

Aidha, FCC imepata mafanikio makubwa baada ya Marekebisho ya Sheria ya Ushindani  ambapo sasa Sheria hiyo inaweza kufanya maamuzi dhidi ya ukiukwaji wa mashauri yanayohusiana na masuala ya kumlinda mlaji badala ya masuala hayo kufanywa na mahakama pekee.

Aidha amesema  majukumu mengine wanayotekeleza ni pamoja na kuchunguza na kuchukua hatua kwa wafanyabiashara wanaobainika kujihusisha na uingizaji nchini, uuzaji, uzalishaji, usafirishaji na uhifadhi wa bidhaa bandia.

 Amesema FCC inatoa elimu au uraghibishi wa Ushindani  kushajiisha utekelezaji wa Sheria ya Ushindani kwa njia ya mashauriano na maelekezo kwa Taasisi za Umma bila kutumia taratibu za kisheria zenye adhabu mbalimbali. 

Hata hivyo Kaimu Mkurugenzi Mkuu amesema FCC inajukumu la kumlinda mlaji dhidi ya mbinu na mienendo kandamizi na hadaifu katika soko, na hivyo kutoa elimu kuhusu haki na wajibu wa mlaji kupitia vyombo vya habari, tovuti na mitandao yake ya kijamii, kutathmini na kusajili mikataba ya walaji inayoandaliwa na upande mmoja na hushughulikia malalamiko ya walaji wa bidhaa na huduma katika soko.

 Amesema  FCC imewezesha na kuimarisha uwekezaji baada ya kuongeza kizingiti cha ulazima wa kuiarifu FCC kuhusu kusudio la kuunganisha shughuli za kibiashara kutoka Shilingi milioni 800 hadi bilioni 3.5 ambapo kampuni za wajasiriamali wadogo na wa kati ambazo thamani ya jumla ya rasilimali zao haifiki kizingiti hicho cha Shilingi bilioni 3.5, zinaweza kuunganisha shughuli zao za kibiashara bila ulazima wa kuomba kibali kutoka FCC. 

Kwa hatua hiyo FCC tumewezesha ukuaji wa biashara ndogo na za kati ambazo zimeweza kuunganisha shughuli zao na kukuza kiwango cha mitaji ya SMEs na kuziwezesha kukopesheka na utafutaji wa teknolojia zaidi, ili kuweza kushiriki zaidi katika uwekezaji na biashara nchini.

 Katika hatua hiyo FCC ya Miungano ya kampuni  imekuwa ikileta faida kubwa katika uchumi wa soko ikiwa ni pamoja na kukuza mitaji ya kampuni husika, kuingia sokoni kwa wawekezaji wapya, kupatikana kwa teknolojia bora za uzalishaji, kuongezeka kwa uzalishaji na tija, kuwezesha upatikanaji wa uchaguzi wa bidhaa na huduma na hivyo kuwezesha bidhaa kupatikana kwa bei za ushindani na kuongeza mapato ya Serikali kwa njia ya kodi.

 Khadija amesema FCC imesogeza huduma karibu kwa kufungua Ofisi za Kanda katika Kanda ya Ziwa (Mwanza), Kanda ya Kaskazini (Arusha) na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini (Mbeya) pamoja na Ofisi ya Tanga.  Baada ya kufungua Ofisi hizo, FCC sasa tuna jumla ya Ofisi sita ikiwa ni pamoja na Dar es Salaam na Dodoma. Ofisi hizi zinawezesha usimamizi madhubuti wa Sheria ya Ushindani pamoja na Sheria ya Alama za Bidhaa kwa ufanisi zaidi.

Khadija amesema FCC imepata Cheti cha Ithibati ya utoaji wa huduma zenye viwango kimataifa, “ISO CERTIFIED 9001:2015” na usimamizi mzuri wa misingi ya Ushindani, kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara na uwekezaji ni jambo tunaloliangalia kwa karibu sana na kuliimarisha na kuwapa wawekezaji imani ya kuwekeza nchini kutokana na FCC kuaminika na kuwa miongoni mwa vyombo vya kusimamia uchumi wa soko, kwa kuhakikisha urahisi wa wawekezaji kuingia na kutoka sokoni bila vikwazo, na kwa kuhakikisha sheria, taratibu na kanuni za ushindani, kumlinda mlaji na kudhibiti bidhaa bandia zinasimamiwa vyema katika soko.

Mwenyekiti wa FCC Dkt.Aggrey Mlimuka akizungumza kuhusiana na majukumu yao kuishauri Taasisi yao katika utoaji huduma ,jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu FCC Khadija Ngasongwa akitoa maelezo kuhusisiana na Majukumu ya Taasisi hiyo kwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara  Dennis Londo wakati alipotembelea Taasisi hiyo jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Wafanyakazi  wakimsikiliza Naibu Waziri wakati alipotembelea ofisi hiyo jijini Dar es Salaam. 
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Dennis Londo akiwa katika picha ya pamoja na makundi ya muundo wa FCC ,jijini Dar es Salaam.

Posted by MROKI On Wednesday, February 11, 2026 No comments

February 10, 2026



Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi amesema kuwa Serikali inatambua jitihada za wabunifu wa nyenzo mbalimbali zinazosaidia kupunguza gesijoto inayotokana na matumizi ya mafuta kwenye vyombo vya moto.
 
Amesema hayo wakati mkutano na wadau kutoka Jumuiya ya Vyombo vya Moto vitumiavyo Umeme Tanzania (TAEMA) pamoja na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) jijini Dar es Salaam kwa lengo la kujadiliana na kuweka mikakati ya namna bora ya kuifanyia huduma hiyo iwe endelevu.
 
Dkt. Muyungi alitoa wito kwa wadau hao kuendelea kuongeza wigo wa huduma ya usafirishaji kwa kutumia magari ya umeme kwa kuwa hivi sasa Tanzania imeanza kuzalisha umeme wa kutosha hususan kutoka Bwawa la Nyerere. 
 
“Tunawahitaji sana ninyi wadau wa sekta hii ya usafirishaji wa vyombo vya moto vya umeme, mtumie fursa ya upatikanaji wa umeme wa uhakika kwani mtasaidia katika kupunguza uzalishaji wa gesijoto,” alisisitiza.
 
Aidha, Dkt. Muyungi alipongeza mchango wa COSTECH katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi hususan kupitia tafiti zake ikiwemo Programu ya Utafiti wa Mabadiliko ya Tabianchi.
 
Pamoja na hayo alitoa wito kwa Tume hiyo kuwekeza kwenye teknolojia ya kukabiliana na maabdiliko ya tabianchi kuhakikisha inakuwa chanzo cha maarifa ya kukabiliana na changamoto hiyo.
Posted by MROKI On Tuesday, February 10, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo