Nafasi Ya Matangazo

March 09, 2026

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa Serikali itachukua hatua kali ikiwemo kufilisiwa kwa yeyote anatakayebainika kuhujumu wakulima kwa kuwauzia pembejeo zisizokuwa na ubora zikiwemo mbegu.
 
Ameyasema hayo leo Jumapili, Machi 08, 2026 alipozungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Laela A wilayani Sumbawanga, Rukwa. Amesisitiza kuwa watu hawatovumiliwa kwa kuwa wana lengo la kuliingiza Taifa katika njaa.
 
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo baada ya Mbunge wa Viti Maalumu, Sylvia Sigula kuishukuru Serikali kwa kuwapatia ruzuku ya pembejeo ila ameiomba Serikali kuwatatulia changamoto ya kuuziwa mbegu zisizokuwa na ubora jambo linalosababisha wakulima kupata hasara kwani kilimo ndio uchumi wa Rukwa.

ameiagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufanya uchunguzi wa kina kuhusu matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo katika baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Rukwa kufuatia taarifa za kuchelewa kwa utekelezaji wa miradi hiyo.

Ametoa agizo hilo leo Jumapili (Machi 8, 2026) wakati akizungumza na mamia ya wananchi wa Laela mkoani Rukwa baada ya kupokea taarifa za utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika eneo hilo.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali haitavumilia kuona miradi ya maendeleo ikicheleweshwa wakati fedha zake tayari zimetolewa kwa ajili ya kuwahudumia wananchi.

 “Kamanda wa TAKUKURU nifanyie uchunguzi wa kina, senti mpaka senti, yeyote aliyehusika kwenye hii fedha hapa nipe taarifa hiyo ili niweze kufanya maamuzi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameonesha kutoridhishwa na kuchelewa kwa utekelezaji wa baadhi ya miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa shule za sekondari, madarasa pamoja na miundombinu mingine ya elimu katika eneo hilo.
 
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde amesema wizara amekuwa ikifanya uchunguzi na kuchukua hatua pale inapobaini kuwepo kwa pembejeo zisizokuwa na ubora na tayari kuna mtu mmoja amekamatwa mkoani humo.
Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu,Pwani
Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) wameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kusambaza miundombinu ya gesi asilia kwenye kaya takribani 1000 na shule moja  ambapo mradi huo umefadhiliwa na Serikali kwa asilimia 100 kupitia REA.

Hayo yamezungumzwa leo Machi 8, 2026 na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF)  Bw. Deodatus Balile wakati wa Ziara ya TEF Kutembelea mradi uliofadhiliwa na REA wa ujenzi wa miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia kwenye nyumba za makazi mkoa wa Pwani

Bw. Balile amesema kupitia mradi huo Serikali imepunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa Nishati nyingine kama mkaa wa kawaida, kuni, na mafuta ya taa na nishati gesi asilia sasa inakua ni chanzo cha nishati ya kupikia.

"REA imefanya kazi kubwa sana ya kufadhili mradi huu, hivyo basi mradi huu utaboresha kiwango cha maisha ya walengwa wa mradi kwa kuokoa gharama na muda wa kupika, mazingira safi afya bora na uwezeshaji wa wanawake kuongezeka, " Amesema Bw. Balile.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Mradi kutoka REA,  Mha. Emmanuel Yessaya amesema kuwa Wakala ulitenga Fedha kwa ajili ya kufadhili mradi ya usambazaji wa gesi asilia kupitia Mfuko wa Nishati Vijijini (REF) ambapo takribani kaya 1000 pamoja na taasisi moja zimenufaika kwa kusambaziwa miundombinu ya gesi asilia kwa ajili ya kupikia majumbani katika mkoa wa Lindi na Pwani.

Mha.Yessaya ameongeza kuwa, Mradi huo ni wa kimkakati kwa ajili ya kupunguza gharama za nishati ya kupikia, kulinda afya za wananchi na kupunguza athari za kimazingira zitokanazo na ukataji wa misitu kwa ajili ya nishati ya kupikia kwa wananchi wanaoishi Vijijini na kwenye vijiji miji.

Kwa upande wake Mhandisi wa mradi huo kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Mha. Anthony Karomba, amesema kuwa mradi huo wa kuunganisha wateja wa majumbani kwenye mtandao wa gesi asilia umegharamikiwa kwa fedha nyingi na Serikali kupitia REA na hivyo amewasihi wananchi kuendelea kuilinda miundombinu hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi wa Kata ya Kisemvule wameishukuru Serikali kupitia REA kwa kusambaza miundombinu ya gesi asilia ya kupikia katika miji yao. Wameeleza kuwa mradi umenufaisha kaya zao kwa kuokoa gharama, kuongeza muda wa kufanya shughuli za kuzalisha mali, imelinda mazingira, imeboresha afya zao na kuimarisha usawa wa kijinsia kwenye shughuli za kiuchumi.



Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments
Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu akiwa anamfariji mtoto wa yatima wa kituo cha Caring from Childhood to Youth kilichopo katika kijiji cha Bumilayinga,wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu akiwa akikabidhi zawadi  katika kituo cha watoto yatima cha Caring from Childhood to Youth kilichopo katika kijiji cha Bumilayinga,wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake.
Na Fredy Mgunda, Mufindi
Wanawake wahifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kutoka Shamba la Miti Sao Hill wametembelea na kuwafariji watoto wanaolelewa katika Kituo cha Kulelea Watoto Yatima cha Caring from Childhood to Youth kilichopo katika kijiji cha Bumilayinga, wilayani Mufindi mkoani Iringa.

Ziara hiyo imefanyika ikiwa ni sehemu ya shughuli za kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, ambapo wanawake hao walionyesha upendo na mshikamano kwa watoto hao kwa kutumia muda kuzungumza nao pamoja na walezi wao na kusikiliza changamoto wanazokabiliana nazo.

Akizungumza kwa niaba ya wanawake hao, Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu, alisema licha ya majukumu yao ya kulinda na kuhifadhi rasilimali za misitu, wanatambua pia umuhimu wa kushiriki katika shughuli za kijamii zinazogusa maisha ya watu moja kwa moja.

Alisema vitendo hivyo vinasaidia kuimarisha upendo, mshikamano na ushirikiano ndani ya jamii, huku vikiwapa watoto walioko katika mazingira magumu matumaini na ari ya kuendelea kupambana ili kufikia malengo yao ya maisha.

Kwa upande wake, Meneja wa Kituo cha Caring from Childhood to Youth, Bw. Ponsiano Mfikwa, aliwashukuru wanawake hao kwa kuwatembelea na kuwakumbuka watoto hao, akisema ujio wao umeleta faraja kubwa kwa watoto pamoja na walezi wao.

Alisema msaada huo ni ishara ya moyo wa upendo na unatoa mfano mzuri kwa jamii kuendelea kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu ili waweze kukua katika malezi bora.

Naye Diwani wa Kata ya Sao Hill ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga, Mhe. Stephen Msigwa, aliwapongeza wanawake wahifadhi kwa juhudi zao katika kulinda na kuhifadhi rasilimali za misitu pamoja na kushiriki katika shughuli za kijamii.

Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba akizungumza katika Mji wa Laela, Halmashauri ya wilaya ya Sumbawanga wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba iliyoanza jana mkoani Rukwa.
***************
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema wananchi wa Mkoa wa Rukwa wataanza kupata umeme wa gridi kuanzia mwezi mei mwaka huu mara utakapokamilika mradi wa usafirishaji umeme wa msongo wa kV 400 kutokea mkoani Iringa.

Ameyasema hayo tarehe 8 Machi 2026, katika Mji wa Laela, Halmashauri ya wilaya ya Sumbawanga wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba iliyoanza jana mkoani Rukwa.

“Kwa maelekezo ya Rais, Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan na maelekezo yako, tunaendelea kuhakikisha inapofika mei 2026 tunawasha umeme kupitia mradi wa TAZA. Hali ya mradi inaenda vizuri na kama kila kitu kitakwenda kama kilivyo, itakapofika mwezi wa tano mwaka huu hatimaye Mkoa huu wa Rukwa utanufaika na umeme wa gridi.” Amesema Mhe.Salome

Ameeleza kuwa, kwa sasa mkoa wa Rukwa unapata umeme kutoka nchini Zambia kupitia mashirikiano ya biashara ya umeme katika nchi za Ukanda wa Kusini mwa Afrika (Southern Africa Power Pool) ambayo yanawezesha nchi wanachama kuuza au kununua umeme pale kunapokuwa na uhitaji ili kukidhi mahitaji ya wananchi.

 Ameongeza kuwa, kutokana na nchi kuwa na umeme wa kutosha, kazi zinazoendelea ili kuweza kuutumia umeme huo ipasavyo ni ujenzi wa miundombinu imara ya usafirishaji na usambazaji umeme itakayowezesha kufikisha huduma hiyo kwa wananchi wengi.

Kuhusu Nishati Safi ya Kupikia, amesema jitihada mbalimbali zinaendelea ili kuweza kufikia asilimia 80 ya wananchi wanaotumia Nishati Safi ya Kupikia ifikapo 2034 ikiwemo ya kusambaza majiko banifu na mitungi ya gesi kwa bei ya ruzuku.

Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Palamagamba J. Kabudi, ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa 26 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Jumuiya ya Madola (CFAMM) uliofanyika Machi 8, 2026 jijini London, Uingereza akimwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.).

Akichangia mjadala, Prof. Kabudi amesema Jumuiya ya Madola inapaswa kubaki kuwa jukwaa muhimu la kushughulikia changamoto za maendeleo na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa (multilateralism) katika kipindi cha sasa chenye changamoto za kisiasa, kiuchumi na kimazingira.

Katika masuala ya uchumi, Prof. Kabudi amesisitiza umuhimu wa kuimarisha biashara na uwekezaji kati ya nchi wanachama kwa kujifunza kutoka mifano ya ushirikiano wa kikanda kama Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA). 

Amesema jukwaa la biashara na uwekezaji la Jumuiya ya Madola litasaidia kupunguza vikwazo vya biashara na kuongeza biashara kati ya nchi wanachama.

Vilevile amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika madini muhimu na kuimarisha miundombinu ya kidijitali ili kuhamasisha uwekezaji, uhamishaji wa teknolojia na matumizi ya huduma za serikali mtandaoni. Hatua hizo, amesema zitasaidia kupunguza pengo la kidijitali na kuongeza fursa za kiuchumi kwa vijana.

Kwa upande wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Shirley Ayorkor Botchwey, amewaimiza nchi wanachama kuimarisha ushirikiano kukabiliana na mabadiliko ya mazingira ya kimataifa. 

Amesema mkutano huo ni fursa ya kujadili mikakati ya kukuza biashara, uwekezaji na kukabiliana na changamoto kama mabadiliko ya tabianchi na changamoto za kiuchumi.

Mkutano wa CFAMM unawakutanisha Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka nchi 56 za Jumuiya ya Madola ikiwa ni jukwaa muhimu la kujadiliana masuala ya kimataifa yanayoathiri maendeleo ya nchi wanachama.
Posted by MROKI On Monday, March 09, 2026 No comments

March 08, 2026

Wanawake kutoka Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Leo tarehe 08 Machi, 2026 wameshiriki katika maadhimisho ya siku wanawake duniani ambayo kimkoa yamefanyika katika uwanja wa shule ya msingi Mbande iliyopo katika halmashauri ya wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma.








Posted by MROKI On Sunday, March 08, 2026 No comments



Na Mwandishi wetu, Dodoma
Wanawake kutoka Tume ya Madini Makao Makuu pamoja na Ofisi ya Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Dodoma wameungana na wanawake wengine duniani kusherehekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, yaliyofanyika katika Shule ya Msingi Mbande, Wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma.

Maadhimisho hayo yamewakutanisha wanawake kutoka taasisi mbalimbali za serikali na binafsi, yakilenga kuadhimisha mchango wa wanawake katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Maadhimisho ya mwaka huu yanafanyika chini ya kauli mbiu isemayo: “Haki kwa wanawake na wasichana ni msingi wa maendeleo jumuishi kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”

Kauli mbiu hiyo inalenga kuhamasisha jamii kutambua umuhimu wa kuhakikisha wanawake na wasichana wanapata haki na fursa sawa katika elimu, uchumi na uongozi, hatua inayochangia kwa kiasi kikubwa katika kufanikisha maendeleo endelevu ya taifa.

Kupitia maadhimisho hayo, washiriki wamepata fursa ya kujadili namna ya kuendelea kuimarisha usawa wa kijinsia na kuhamasisha jamii kushiriki katika kuondoa vikwazo vinavyoweza kuzuia maendeleo ya wanawake na wasichana nchini.
Posted by MROKI On Sunday, March 08, 2026 No comments

March 07, 2026

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba  akizungumza na wananchi mara baada ya kuhudhuria mashindano ya kuhifadhi qur’an Tukufu yaliyofanyika katika Kijiji cha Bukulu, Kondoa mkoani Dodoma, Machi 7, 2026 
 Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akionesha tuzo aliyokabidhiwa kwa kutambua mchango wake mkubwa katika kukuza vipaji na kuendeleza Mashindano ya kuhifadhi Qur'an Tukufu wilayani Kondoa. Tuzo hiyo imetolewa na Ofisi ya Mbunge wakati wa mashindano ya kuhifadhi Qur’an Tukufu yaliyofanyika katika kijiji cha Bukulu, Wilayani Kondoa mkoani Dodoma Machi 7, 2026
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akiitika Dua wakati wa mashindano ya kuhifadhi qur’an Tukufu yaliyofanyika katika Kijiji cha Bukulu, Kondoa mkoani Dodoma,Machi 7, 2026
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba  akizungumza na Mbunge wa Kondoa ambaye pia ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji wakati wa mashindano ya kuhifadhi qur’an Tukufu yaliyofanyika katika Kijiji cha Bukulu, Kondoa mkoani Dodoma, Machi 7, 2026.
************
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema ni muhimu wa kuendeleza maadili, elimu ya dini na mshikamano wa jamii kupitia mashindano ya kuhifadhi Qur’an tukufu.

Ameyasema hayo leo (Jumamosi, Machi 7, 2026) wakati akizungumza na wananchi waliohudhuria mashindano hayo yaliyofanyika uwanja wa Kambi ya Fisi kwenye kijiji cha Bukulu, kata ya Soera, wilayani Kondoa, mkoani Dodoma.

Amesema mashindano ya aina hiyo yana mchango mkubwa katika kukuza malezi bora kwa vijana pamoja na kuimarisha misingi ya maadili mema katika jamii.

“Serikali inaunga mkono juhudi za taasisi za dini katika kuimarisha elimu ya kiroho na maadili kwa vijana. Malezi ya kidini yana nafasi muhimu katika kujenga jamii yenye amani, uvumilivu na mshikamano,” amesema Waziri Mkuu ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mashindano hayo.

Akielezea umuhimu wa mashindano hayo, Waziri Mkuu amesema katika Qur’an sura ya pili aya ya 185, imeelezwa kuwa Qur’an imeshushwa ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhan. “Mwezi wa Ramadhan ni mwezi wa kuisoma sana Qur’an kwa namna mbalimbali. Hongereni sana kwa kutekeleza agizo hili,” amesema. 

“Nilikuwa nawaangalia usoni watoto wetu hawa, nikawa naona siyo tu kwamba wanashindana mbele yetu, niliona ni kweli wamehifadhi Qur’an. Nilishangaa kuona tunaanza na juzuu tano, zikaja 10, halafu juzuu 20 na kisha juzuu 30.”

Amewataka washiriki waendelee kuyatumia majukwaa ya mashindano ya Qur’an kuhamasisha mapenzi ya Qur’an na si ushindani peke yake. “Katika mashindano yetu haya ya leo, hakuna mshiriki ambaye amepoteza au ameshindwa, washiriki wote ni washindi kwa sababu mmejifunza, mmebeba Qur’an katika nyoyo zenu na mnaiendeleza Qur’an.” 

Vilevile, Waziri Mkuu amewataka waumini wa dini hiyo watambue kuwa kuhifadhi Qur’an kichwani kunapaswa kuendane na kuiishi Qur’an kwa vitendo. “Majukwaa yote ya mashindano ya Qur’an, walimu wa Qur’an, wazazi na walezi mnawajibika kuwafundisha kwa vitendo vijana wetu kuhusu ucha-Mungu, maadili mema, uadilifu, kuhudumia na kuunganisha makundi mbalimbali katika jamii. Tusipowafundisha kuwa wachaMungu na watu wa ibada, ndivyo watakavyokuwa wakiwa watu wazima,” amesisitiza.

Mapema, Waziri wa Maliasili na Utalii ambaye pia ni Mbunge wa Kondoa Vijijini, Dkt. Ashatu Kijaji alisema mashindano hayo yamekuwa yakifanyika wilayani humo kwa miaka tisa mfululizo na yamelenga kuandaa kizazi ambacho kinamcha Mungu.

“Wana-Kondoa tunatamani kuona tunaandaa kizazi kilicho bora chenye kumjua Mungu. Kondoa tumeamua kuandaa Watanzania wenye hofu ya Mungu kwa kuwafundisha kitabu cha Mwenyezi Mungu na niahidi kwamba ofisi ya Mbunge haitachoka kuandaa kazi hii,” amesema.
Posted by MROKI On Saturday, March 07, 2026 No comments
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba leo amekagua utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa Malagarasi (MW 49.5) unaotekelezwa katika Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma ambapo ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji.

Akiwa katika Kijiji cha Mazungwe wilayani Uvinza Mhe Salome amekagua sehemu mbalimbali za mradi ikiwemo ujenzi wa tuta na uchepushaji mto, ujenzi wa jengo la kuendeshea  mitambo na kambi za wafanyakazi ambapo hakukuta wafanyakazi wa kutosha kama ambavyo mkataba unaelekeza.

Kutokana na hilo, Naibu Waziri wa Nishati amemuagiza mkandarasi kampuni ya Dongfang ya China kuhakikisha kuwa anaongeza wafanyakazi,  vifaa vya kazi na ndani ya mwezi mmoia awe amejenga kambi ya wafanyakazi.

Aidha,  amemtaka Mkandarasi kuwasilisha ratiba mpya  ya utekelezaji wa kazi.

Vilevile, ameagiza wasimamizi wa mradi wa Malagarasi kutoka Kampuni ya Mkandarasi  Mshaurii na TANESCO kuhamia katika eneo la mradi ndani ya mwezi  mmoja ili kuweza kuusimamia mradi huo kwa ukaribu.

"Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Wizara ya Nishati kuzalisha megawati 8000 za umeme ifikapo 2030, hatutakubali mtu atukwamishe katika kufikia malengo haya. Mkandarasi hakikisha unakamilisha kazi ifikapo Oktoba 2027 kama mkataba unavyoelekeza." Amesisitiza Mhe.Salome

Aidha, amemtaka Mkandarasi  Mshauri kampuni ya Multiconsult Norge AS ya Norway na Norplan kutoka Tanzania kuhakikisha kuwa wanamsimamia mkandarasi ipasavyo ili mradi ukamilike kwa wakati na kwa viwango stahiki.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Dinah Mathamani ameeleza kuwa uongozi wa wilaya hiyo utasimamia kwa karibu maelekezo yanayotolewa na Wizara ili mkandarasi atekeleze kazi kulingana na.mkataba.

Naye, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amesema utekelezaji wa mradi wa Malagarasi kwa saaa ulipaswa kuwa kwenye asilimia 28 ila  umefikia asilimia 23.

Amesema Wizara ya Nishati itaendelea  kumsimamia kwa karibu mkandarasi  ili amalize kazi kwa wakati.

Sehemu nyingne zinazohusisha mradi wa Malagarasi ni upelekaji umeme katika vijiji saba vyenye vitongoji 18 ambapo mradi huo umekamilika kwa asilimia 100.

Pia ujenzi wa njia ya msongo wa kV 132 kutoka eneo la mradi hadi Kidahwe ambao umekamilika kwa asilimia 100.











Posted by MROKI On Saturday, March 07, 2026 No comments




WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa majibu ya mgogoro wa ardhi baina ya wakazi wa Wilaya ya Monduli na Jeshi la Wananchi ambao umedumu tangu mwaka 2004 baada ya kumpigia simu Mkuu wa Majeshi nchini na kumweleza kilio cha wanaMonduli.

Waziri Mkuu alichukua hatua hiyo jana jioni (Ijumaa, Machi 6, 2026) wakati akizungumza na wananchi na viongozi mbalimbali kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Barafu Mto wa Mbu, wilayani Monduli, mkoani Arusha. 

Akitoa majibu baada ya maongezi yao, Dkt. Mwigulu aliwaeleza wananchi hao kwamba Mkuu wa Majeshi nchini ameridhia hoja yao iliyotolewa na Mbunge wa Monduli, Isack Joseph pamoja na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Namelok Sokoine ambao waliomba suala la fidia lisiwepo bali wananchi waachiwe kuendelea kushirikiana na jeshi kama ilivyokuwa zamani.

“Mkuu wa Majeshi ameridhia kwamba hakuna jambo la fidia. Makubaliano mliyokuwa nayo awali ya mafunzo na malisho yaendelee vilevile. Bali ametoa angalizo kwamba watu wasijenge makazi ya kudumu kama mlivyokubaliana awali,” alisema na kuamsha nderemo na shangwe kutoka kwa wananchi hao.

Waziri Mkuu alitoa rai kwa watendaji wa Halmashauri nchini akiwataka waheshimu na kulinda maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya malisho ya mifugo ili kuepusha migogoro na kuhakikisha shughuli za ufugaji zinaendelea kwa tija. “Maeneo yanayohusu wafugaji tusiyadokoe, tusiyachanganye. Tuendelee kulinda maeneo ya wafugaji bila kuyachanganya na matumizi mengine.”

Mapema, Mbunge wa Monduli, Isack Joseph alimuomba Waziri Mkuu afuatilie suala hilo ili wanaotaka kumilikishwa eneo hilo kwa kudai fidia, wasipatiwe hiyo fursa bali libakishwe kuwa eneo huru kwa Jeshi la Wananchi na kwa wafugaji. Eneo hilo lina kilometa za mraba 870 ambazo ni sawa na ekari 214,981.68

Pia alimuomba afuatilie suala la malipo ya mabomba ya maji kwenye kiwanda cha Pipes Industries ambacho kinatengeneza mabomba kwa ajili mradi wa maji wa vijiji 13 vya Monduli wenye thamani ya sh. bilioni 20.3. Mradi huo unatarajiwa kutoa maji umbali wa km. 45 kutoka Ngaramtoni hadi Monduli mjini.

Vilevile, mbunge huyo alieleza changamoto zinazoikabili sekta ya utalii katika eneo la Mto wa Mbu kwamba licha ya kuwa eneo hilo lina vivutio vikubwa vya utalii, bado linasimamiwa kama Game Controlled Area, jambo linalosababisha watalii wengi kukwepa kulitembelea na hivyo kudhoofisha uchumi wa wilaya hiyo.

Naye, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Namelok Sokoine akisisitiza kuhusu eneo hilo alisema anakubaliana na maelezo ya Mbunge wake, Bw. Isack Joseph kwa vile anatambua kuwa wafugaji hawana mbadala zaidi ya mifugo yao. “Kitu pekee ambacho wazazi wetu wanaweza kutuachia kama urithi ni mifugo na ardhi yetu,” alisema.

Alisema kwamba marehemu baba yake (hayati Edward Moringe Sokoine) alitambua umuhimu wa ardhi na malisho ndipo aliamua kutenga eneo la jeshi kufanyia mafunzo lakini pia ambalo wafugaji wangeweza kulisha mifugo yao pale.

 “Nia yake kubwa ni ili maeneo yale yasiweze kuuzwa kwa watu wengine, njia pekeee ilikuwa ni kuwapa jeshi walitumie kwa mafunzo lakini pia wafugaji walitumie wakati hakuna mafunzo.”

Alisema kuwa mwaka jana kupitia kwa mbunge wao mstaafu, Fredrick Lowassa, walikuwa na vikao virefu na Waziri wa Ulinzi kuhusu suala hilo na wakaazimia kuwa hawako tayari kufidiwa kwa kuwa hawana mahali pengine pa kwenda. 

“Sisi wafugaji hatuna pa kupeleka mifugo yetu. Tunajua kuwa ardhi haiongezeki licha kuwa watu na wanyama wanaongezeka; na kokote mtakapotupeleka, tunatambua kuwa migogoro ya ardhi haiishi. Ndiyo maana tulisema tulisema tungependa kubaki katika eneo letu. 

Serikali itambue tunatamani tubaki pale. Wana Monduli tunasema hatuko tayari kufidiwa, tunaomba tuendelee kubaki katika ardhi yetu na tuko tayari kubakia na Jeshi,” alisisitiza.
Posted by MROKI On Saturday, March 07, 2026 No comments

March 06, 2026


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amelipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa kusimamia na kukamilisha mradi wa kupeleka umeme wa gridi mkoani Kigoma na hivyo kuokoa takribani shilingi bilioni 58 zilizokuwa zikitumika kila mwaka kwa ajili ya ununuzi wa mafuta na matengenezo ya vipuri vya majenereta ya kuzalisha umeme.

Mhe. Salome ametoa pongezi hizo tarehe 6 Machi 2026 mara baada ya kutembelea mradi wa ujenzi wa kituo kikubwa cha Kupoza umeme cha Kidahwe kilichopo mkoani Kigoma pamoja na kituo cha kupoza umeme cha kigoma mjini na kituo cha muda cha Kidahwe.

“Niwapongeze TANESCO kwa kufikisha umeme wa gridi Kigoma hasa baada ya kukamilisha mradi  kutoka Nyakanazi hadi Kigoma na kwa kuamua kutumia fedha zenu za ndani shilingi bilioni tano kukamilisha kituo cha muda cha Kidahwe ambacho kwa sasa kinapeleka umeme Kigoma wakati ujenzi wa kituo kikubwa cha umeme Kidahwe ukiendelea,” amesema Mhe. Salome

Amesema kituo kipya cha umeme cha Kidahwe kitakuwa na uwezo wa megawati 192 na hivyo kitaimarisha zaidi hali ya upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Kigoma ambao kwa sasa unapata takribani megawati 30.

Ameongeza kuwa kituo hicho kinatarajiwa kukamilika mwezi Novemba mwaka huu na kitasaidia pia kuimarisha hali ya umeme katika mikoa ya Magharibi, kuendesha Treni ya Mwendo Kasi (SGR) pamoja na kuchochea biashara ya umeme na nchi jirani za Magharibi mwa Tanzania.

Kutokana na uwepo wa umeme wa kutosha mkoani Kigoma, Mhe. Salome amewakaribisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza katika mkoa huo.

 Aidha, amewaasa wananchi kulinda miundombinu ya umeme akieleza kuwa Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anaendelea kutoa fedha nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya nishati nchini hivyo wananchi wanao wajibu wa kuilinda na kuithamini.

Awali, Mratibu wa Mradi wa Kusafirisha umeme wa msongo wa kilovolti 400 kutoka Nyakanazi hadi Kigoma, Mhandisi Ramadhan Uwessu, alisema kuwa ujenzi wa kituo kipya cha Kidahwe unaenda sambamba na upanuzi wa kituo cha Nyakanazi ili kukiwezesha kusafirisha umeme wa msongo wa kV 400 kutoka Nyakanazi hadi Kidahwe.

Ameongeza kuwa kituo hicho pia kitapokea umeme kutoka njia ya Tabora kwa msongo wa kV 132, kutoka Sumbawanga kwa msongo wa kV 400 pamoja na umeme utakaozalishwa kutoka mradi wa Malagarasi.

Amesema mradi huo umefikia asilimia 47 ya utekelezaji na unagharimu takribani shilingi bilioni 434 zilizotolewa na Serikali ya Tanzania, Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) pamoja na Mfuko wa Maendeleo wa Watu wa Korea Kusini (EDCF).







Posted by MROKI On Friday, March 06, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo