Wizara ya Madini imekutana katika Bonanza la Michezo lililowashirikisha watumishi wa Wizara pamoja na taasisi zake zote, ikiwa ni utaratibu wa kawaida wa kukutana kila Robo Mwaka kwa lengo la kuimarisha ushirikiano, mshikamano na kufahamiana zaidi miongoni mwa watumishi.
Akizungumza katika bonanza hilo, lililofanyika Juni 6, 2026 katika Viwanja vya Shule ya Sekondari John Merlin, Mipango jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, ameeleza umuhimu wa michezo na manufaa yake katika maisha ya kila siku, akibainisha kuwa michezo ni afya, burudani na ajira.
“Michezo ni afya kwa sababu inasaidia kujenga mwili imara na kukinga dhidi ya maradhi mbalimbali yasiyoambukiza. Afya inapokuwa imara, manufaa yake ni makubwa kwa mtu binafsi na taifa kwa ujumla,” amesema Dkt. Kiruswa.
Ameongeza kuwa michezo ni burudani kwa kuwa huwapa watu furaha, huondoa msongo wa mawazo na kuongeza amani ya moyo, hali inayochangia kuongeza ubora wa maisha na umri wa kuishi.
Kuhusu ajira, Dkt. Kiruswa amesema katika nyakati za sasa michezo imekuwa sekta muhimu inayotoa ajira kwa wananchi wengi na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.
Vile vile, amependekeza katika mabonanza mengine Wizara kuangalia namna ambavyo michezo hiyo itawashirikisha watoto wa watumishi kama familia ya madini.
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri amewapongeza watumishi wa Wizara ya Madini na taasisi zake kwa utendaji wao mzuri ulioiwezesha Wizara kuwa miongoni mwa wizara zenye utulivu na matokeo chanya katika utekelezaji wa majukumu yake.
Amesema hadi kufikia tarehe 5 Juni 2026, Wizara ilikuwa tayari imekusanya shilingi trilioni 1.27, na hivyo kuvuka lengo la shilingi trilioni 1.2 lililowekwa kwa Mwaka wa Fedha 2025/26.
Awali, akizungumza katika bonanza hilo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, amesema bonanza hilo ni mwendelezo wa maelekezo ya viongozi wa Wizara ya kuhakikisha watumishi wanakutana mara kwa mara kwa ajili ya kuimarisha afya zao na kujikinga dhidi ya maradhi yasiyoambukiza.
“Siku za karibuni tumeshuhudia ongezeko la maradhi yasiyoambukiza ambayo yamekuwa na athari kubwa kwa wananchi. Hivyo, michezo ni sehemu muhimu ya kujenga afya bora,” amesema Eng. Samamba.
Ameongeza kuwa, Wizara inatambua watumishi wake kuwa ndiyo nguvu kazi kuu ya taasisi hiyo, hivyo itaendelea kuimarisha shughuli za michezo mahali pa kazi ili kukuza mshikamano, umoja na upendo miongoni mwa watumishi na kuongeza hatua hiyo itasaidia kuongeza ufanisi wa kazi na kuifanya Sekta ya Madini kuendelea kuchangia katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya nchi.
Watumishi wameshiriki katika michezo mbalimbali ikiwemo jogging, mpira wa miguu, Pete, riadha kufukuza Kuku, kukimbia na mayai, kukimbia na magunia, basketball, kuvuta kamba ambapo washindi wamepokea tuzo mbalimbali na medali.
Pia, wanamichezo walioshiriki Mashindano ya Mei Mosi wamekabidhi vikombe viwili kufuatia ushindi walioupata wa mbio na pool table na hivyo kuishukuru Wizara kwa kuwapatia fursa ya kushiriki katika mashindano hayo.






































.jpg)
















