Nafasi Ya Matangazo

February 06, 2026



WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Februari 6, 2026 ameahirisha Mkutano wa Pili wa Bunge la 13 jijini Dodoma na kutumia fursa hiyo kuwaasa Watanzania wote kuwa na matumizi chanya ya mitandao ya kijamii na kuifanya kuwa nyenzo muhimu ya kujielimisha, kuendeleza biashara na kueneza ujumbe wa mshikamano.

Pia, Mheshimiwa Dkt. Nchemba ameiagiza Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum iweke kipaumbele cha kutoa elimu ya malezi bora katika kijamii kwa kushirikiana wadau mbalimbali wakiwemo Viongozi wa Asasi za Kiraia na Mashirika yasiyo ya Kiserikali.

Waziri Mkuu amesema suala la amani, usalama na utulivu ni jukumu la kila Mtanzania na linahitaji juhudi za pamoja katika nyanja mbalimbali, hivyo wote wanawajibika kuepuka masuala yote yanayochochea uvunjifu wa amani ikiwemo matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii.

Aidha, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa rai kwa Watanzania wote kuendelea kulinda Tunu za Taifa kwa kuwa ni wajibu wa kila raia kuziheshimu na kuziendeleza ili kuleta mshikamano na kuimarisha heshima ya Taifa.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuwawezesha wananchi kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuongeza upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya biashara ndogo za kati na kampuni changa.

“Tarehe 05 Februari, 2026 nilishiriki kwenye tukio muhimu la uzinduzi wa utoaji mitaji yenye thamani ya shilingi bilioni 200 ili kuwawezesha wakulima, wafugaji, wavuvi, wafanyabiashara, maafisa usafirishaji, wasanii na kampuni changa za vijana kuongeza mitaji, kukuza biashara na kuchangia ajira na ukuaji wa uchumi.”

Pia, Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kutoa mikopo mingine yenye masharti nafuu kupitia mifuko mbalimbali na kunufaisha wafanyabiashara wadogo, wajasiriamali na kampuni changa kwa kuwatambua na kuwasajili wafanyabiashara wadogo zaidi ya milioni moja na kuwapatia mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 707.4 kutoka taasisi za fedha za NMB, DCB na TCB.

Vilevile, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa rai kwa Watanzania kuendelea kutumia taasisi za kifedha zilizo rasmi na kuepuka taasisi zisizokuwa na usajili . “Hakuna benki yenye masharti mabaya kuliko yale ambayo baadhi ya Watanzania wanayapata kwenye kausha damu. Tusiziogope taasisi rasmi ili kujiepusha na matatizo ambayo yamekuwa yakijitokeza kwenye baadhi ya taasisi ambazo hazijasajiliwa.”
Posted by MROKI On Friday, February 06, 2026 No comments

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa ahadi za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan zimeendelea kutekelezwa kikamilifu ikiwemo ya kugharimia kwa asilimia 100 matibabu ya vipimo vya kibingwa kwa magonjwa sugu yasiyoambukiza kama saratani, figo, moyo, sukari, mifupa na mishipa ya fahamu.

Waziri Mkuu amesisitiza kuwa uamuzi huo ni sehemu ya dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kulinda afya za Watanzania, kuimarisha mfumo wa huduma za afya na kuhakikisha hakuna mwananchi atakayeshindwa kupata matibabu muhimu kutokana na ukosefu wa uwezo wa kifedha.

Ameyasema hayo leo Ijumaa, Februari 6, 2026 wakati wa kuahirisha Mkutano wa Pili wa Bunge la 13 jijini Dodoma, ambapo amesisitiza kuwa Serikali imepata mafanikio makubwa katika sekta ya afya ikiwemo kuongeza wigo wa upatikanaji na ufanisi wa utoaji wa huduma za afya nchini.

 

“Sote tunakumbuka kuwa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania alitoa ahadi mbalimbali kwa wananchi. Ahadi hizo ni pamoja na zile zitakazotekelezwa ndani ya siku 100 baada ya Serikali kuingia madarakani.”

 

Waziri Mkuu ametaja mafanikio mengine yaliyopatikana katika sekta ya afya ni pamoja na kuendelea kuratibu utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote kwa awamu ya majaribio ambao unahusisha makundi maalum ya watoto, wajawazito na wenye ulemavu.

Pia, Waziri Mkuu amesema Serikali imeondoa zuio la kuchukua miili ya marehemu katika vituo vya umma vya kutolea huduma za afya kwa kigezo cha madeni ya matibabu, imeajiri watumishi wa afya 5,000 na kuwapangia vituo vya kazi kote nchini na imefanya uwekezaji mkubwa wa miundombinu ya afya.

”Serikali imetoa zaidi ya shilingi bilioni 39 ili kuboresha huduma za uzazi na watoto wachanga katika vituo 89 vya kutolea huduma za afya na imeongeza vituo vya upasuaji wa dharura kutoka vituo 523 Oktoba, 2025 hadi vituo 578 Januari, 2026.”

Kadhalika, Waziri Mkuu amesema Serikali imeongeza uwezo wa Taifa kukabiliana na athari za VVU na UKIMWI kwa kuhakikisha utoshelevu wa dawa za kufubaza makali ya UKIMWI kwa kufufua Kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Industries (TPI) kilichopo mkoani Arusha na kuongeza fedha za ndani kupitia Mfuko wa Udhamini wa Afua za UKIMWI.
Posted by MROKI On Friday, February 06, 2026 No comments


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema mipango inayoandaliwa na Serikali inalenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha usafiri na usafirishaji wa bidhaa, viwanda na biashara katika ukanda wa Afrika.

Amesema Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027 – 2030/2031 una dhima ya mageuzi kwa ajili ya ukuaji wa uchumi jumuishi na uzalishaji wa ajira na kwamba unatarajiwa kuweka msukumo wa kipekee na kuleta mageuzi yatakayobadilisha mifumo, mitazamo na mwenendo katika utendaji.

“Hatua hii itachochea tija katika uzalishaji, kuongeza uwezo wa nchi katika kushindana kikanda na kimataifa, na kuchochea muunganiko wa sekta mbalimbali. Lengo ni kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha usafiri na usafirishaji wa bidhaa, viwanda na biashara katika ukanda wa Afrika,” amesema.

Ametoa kauli hiyo bungeni leo (Ijumaa, Februari 6, 2026) katika hotuba ya kuhitimisha mkutano wa pili wa Bunge wakati akielezea Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali katika muda wa Kati wa 2026/2027 – 2028/2029 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka 2026/2027. Bunge limeahirishwa hadi Machi 31, 2026.

Akielezea mapendekezo ya mwongozo wa maandalizi ya mpango huo, Waziri Mkuu amesema Serikali itatekeleza vipaumbele katika miradi inayoendelea, iliyosainiwa pamoja na vipaumbele vilivyoainishwa katika Mpango wa Kwanza wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano. 

“Maeneo mahsusi ya kipaumbele katika matumizi ni kugharimia miradi ya kielelezo na kimkakati inayoendelea, deni la taifa, mishahara ya watumishi wa umma na huduma za jamii,” amesema.

Akitoa maelekezo katika maandalizi ya Mpango na Bajeti kwa mwaka 2026/2027, Waziri Mkuu amewataka Maafisa Masuuli waweke msukumo kwenye maeneo sita yakiwemo ya kusimamia kusimamia nyongeza ya asilimia tano kwenye mikopo ya wanawake, vijana na wenye ulemavu inayotokana na mapato ya ndani ya halmashauri.

“Ninaelekeza Ofisi za Wakuu wa Mikoa zisimamie Mamlaka za Serikali za Mitaa kutumia kwa pamoja asilimia tano kati ya asilimia 15 ya mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa ajili ya uwekezaji kwenye miradi ya kuboresha mazingira ya biashara na ujasiriamali ili kuvutia na kuongeza fursa za ajira kwa makundi haya,” amesema.

Amewataka Maafisa Masuuli wazingatie mkakati wa kulinda wawekezaji wa ndani kwa kutoa kipaumbele cha kwanza katika zabuni, masharti ya mikataba na malipo ya hati za madai. Aidha amewataka waandae mikakati ya kuzalisha, kulea na kukuza wajasiriamali wadogo, wa kati na wakubwa kupitia dhana ya ushirikishaji wa wananchi katika utekelezaji, uwezeshaji na upatikanaji wa mikopo ya gharama nafuu ili kuwezesha uibuaji wa fursa za ajira kwa vijana.

Pia amezitaka taasisi na mashirika ya umma yanayojiendesha kibiashara yaweke mikakati ya kuondokana na utegemezi wa ruzuku kutoka Serikali Kuu ifikapo Juni, 2029 ili kutoa fursa kwa serikali kuendelea kutekeleza miradi ya maendeleo inayowahusu wananchi.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu ameziagiza Mamlaka za Serikali za Mitaa ziongeze uwazi katika utekelezaji wa miradi kwenye halmashauri nchini. “Mapato yote yajulikane kwa Waheshimiwa Wabunge na Madiwani. Kila wakati, Katibu Tawala Mkoa anapotuma fedha kwenye halmashauri atoe nakala kwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Ofisi ya Mbunge, ofisi ya Meya, kwa Wenyeviti wa Halmashauri na Madiwani na aainishe aina ya miradi inayoenda kutekelezwa,” amesisitiza.

Amesisitiza kuwa ratiba za vikao vya Baraza la Madiwani zizingatie ratiba za vikao vya Bunge ili kutoa fursa kwa wabunge kushiriki vikao kwani vikao vya Bunge si vya dharura na ratiba yake inajulikana mapema. “Miradi yote ambayo ipo kwenye hatua za utekelezaji gharama zake zisiwe siri, taarifa zake zijulikane kwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Wabunge, Meya, Wenyeviti wa Halmashauri na Madiwani. Lengo la kuweka uwazi ni kuwarahisishia Waheshimiwa Wabunge kufuatilia miradi inayotekelezwa kwenye maeneo yao,” amesema 

Ili kufanikisha utekelezaji wa maelekezo hayo, Waziri Mkuu amewaomba wabunge wanaporejea majimboni kwao, wafuatilie kwa karibu utekelezaji wa miradi ya maendeleo, waweke mawe ya msingi na kuzindua miradi ambayo imekamilika. Vilevile, hakikisheni mnapata taarifa za utekelezaji wa kila mradi na maeneo ambayo mna ushauri, tumieni fursa zote zikiwemo vikao vya halmashauri, vikao vya baraza la ushauri la wilaya (DCC), vikao vya Baraza la Ushauri la Mkoa (RCC), wizara za kisekta au hata Ofisi ya Waziri Mkuu,” amesema.

Amewataka viongozi na watendaji wote wa serikali waithamini na kuishirikisha sekta binafsi katika hatua mbalimbali za kupanga na kutekeleza miradi yote ya maendeleo kwa kuwa mchango wa sekta binafsi katika utekelezaji Dira ya Taifa ni mkubwa. “Sekta binafsi ipewe heshima ili kuhakikisha mchango wao unaonekana.”
Posted by MROKI On Friday, February 06, 2026 No comments
Mkurugenzi wa Hospitali ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Dkt. Tulizo Shemu akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya hospitali hiyo kwa mwaka 2025 leo wakati wa mkutano huo uliofanyika katika hospitali hiyo iliyopo Tazara jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group wakisikiliza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya hospitali hiyo kwa mwaka 2025 uliofanyika leo JKCI Hospitali ya Dar Group iliyopo Tazara jijini Dar es Salaam. Picha na: JKCI
Baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group wakisikiliza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya hospitali hiyo kwa mwaka 2025 uliofanyika leo JKCI Hospitali ya Dar Group iliyopo Tazara jijini Dar es Salaam.
**************
Na Mwandishi Maalumu – Dar es Salaam
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group imetoa huduma za upimaji na matibabu ya magonjwa mbalimbali kwa watu 138,699 kwa mwaka 2025. 

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Hospitali ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Dkt. Tulizo Shemu alisema watu wazima 124,959 na watoto 13,740 walipatiwa matibabu mwaka 2025 huku wagonjwa 4,144 kulazwa katika hospitali hiyo kwaajili ya matibabu.

Dkt. Shemu alisema ukilinganisha na mwaka 2024 Hospitali hiyo ilitoa huduma kwa wagonjwa 133,756 kati yao watu wazima walikuwa 109,931 na watoto 23,825 hivyo kuwa na ongezeko la wagonjwa 4,943 huku idadi ya watoto ikipungua na idadi ya watu wazima ikiongezeka.
 
“Huduma zilizotolewa kwa wagonjwa zilikuwa ni za matibabu ya moyo, matibabu ya kinywa na meno, kliniki ya magonjwa ya ngozi, matibabu ya magonjwa yanayoambukiza ikiwemo malaria, huduma za magonjwa ya dharura, kliniki ya wanawake na wajawazito, kliniki ya macho, kliniki ya pua, masikio na koo”,

“Huduma nyingine zilikuwa ni kliniki ya mfumo wa mkojo, kliniki ya magonjwa ya tumbo na ini, kliniki ya magonjwa ya figo, upasuaji mkubwa na mdogo, huduma za fiziotherapia (mazoezi tiba) na huduma za maabara”, alisema Dkt. Shemu.

Aidha Dkt. Shemu alisema kwa mwaka 2025 JKCI Hospitali ya Dar Group ilitoa huduma mpya ambazo hapo awali zilikuwa hazitolewi ikiwemo kuangalia shinikizo la damu kwa masaa 24 (ambulatory blood pressure monitoring), matibabu ya kuangalia umeme wa moyo kwa masaa 24 (ECG Halter Monitoring) na kipimo cha kuchunguza mishipa ya damu ya moyo na mfumo wa umeme wa moyo katika hali ya mazoezi kwa kutumia mashine ya treadmill (Treadmill stress test).

Kwa upande mwingine Dkt. Shemu alisema watu 251 walifanyiwa uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali yakiwemo magonjwa ya moyo, ngiri, vidonda sugu, matatizo ya mifupa na mgongo pamoja na tiba ya kinywa na meno kupitia huduma za tiba mkoba zijulikanazo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services zilizofanyika katika viwanja vya Mbagala wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam.

“Kupitia kambi hiyo jumla ya watu 198 walikutwa na magonjwa mbalimbali na hivyo kupewa rufaa ya kufika JKCI Hospitali ya Dar Group kwaajili ya vipimo zaidi na kuanzishiwa matibabu”, alisema Dkt. Shemu.

Dkt. Shemu alisema mwaka 2025 JKCI Hospitali ya Dar Group ilifanya upasuaji kwa wagonjwa 1,874 ikiwemo upasuaji wa mfumo wa mkojo, upasuaji wa mifupa, Upasuaji wa uzazi, Upasuaji wa pua, masikio na koo, Upasuaji wa matatizo mbalimbali ya wanawake na upasuaji wa jumla.
 
“Hospitali hii imeongeza urahisi wa upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi waishio Temeke, Tabata, Mbagala, Chanika, Gongo la Mboto na maeneo mengine ya ukanda huu”, alisema Dkt. Shemu
 
Upande wa ajira Dkt. Shemu alisema Serikali kupitia Tume ya Ajira katika Utumishi wa Umma kwa mwaka 2025 ilitoa ajira mpya kwa wafanyakazi 149 katika kada mbalimbali zikiwemo za afya, utawala, uhasibu, ugavi, ICT, na nyinginezo.
Posted by MROKI On Friday, February 06, 2026 No comments
Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara akizungumza na wananachi na wanachama wa CCM Wilaya Bunda leo februari 05 katika Sherehe za Maazimisho ya  Miaka 49 ya Kuzaliwa kwa CCM, Mkoani Mara katika Viwanja Vya Stendi ya Zamani
Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara akizungumza na wananachi na wanachama wa CCM Wilaya Bunda leo februari 05 katika Sherehe za Maazimisho ya  Miaka 49 ya Kuzaliwa kwa CCM, Mkoani Mara katika Viwanja Vya Stendi ya Zamani.
***************
Na Mwandishi Wetu, Bunda
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira, amesisitiza umoja wa wanachama ndiyo uliokiwezesha Chama kufanya mambo makubwa.

Wasira alisema hayo leo mjini Bunda katika sherehe za kilele cha maadhimisho ya miaka 49 ya kuzaliwa kwa CCM.

“Niwaambie kwamba umoja ni nguvu na msingi wa CCM, hakuna CCM kama hakuna umoja, nguvu yetu ni wanachama wetu wa CCM na wanachama hao nguvu yao ni umoja wao, na umoja huo ndiyo umetufikisha hapa, kwa muda mfupi wa siku nane tumechangisha sh. milioni 400,” alisema.

Aidha, Wasira alisema kwa miaka 49 Chama kimefanikiwa kubaki imara na kukubalika kwa wananchi kwa kinasikiliza mahitaji ya Watanzania.

“Mwaka 1962 baada ya kujitawala Mwalimu Julius Nyerere alilitangazia taifa kwamba kuna maadui watatu ambao tunatakiwa kupambana nao (ujinga, maradhi na umaskini), kauli hiyo ilichukuliwa na TANU na kauli hiyo inatekelezwa CCM,” alisema na kusisitiza kuwa, huo ni msingi wa Chama kuwahudumia wananchi wakati wote.

Katika mkutano huo, Wasira aliongoza uchangiaji wa kufanikisha ujenzi wa ofisi ya CCM ya wilaya ya Bunda Mkoa wa Mara na kufanikisha kupatikana zaidi ya sh milioni 400. 
Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara akikagua athari za uharibifu wa Ofisi ya CCM Wilaya Bunda leo februari 05 akita wilayani humo kwa ajili ya Maazimisho ya Cherche za Miaka 49 ya Kuzaliwa kwa CCM.
Posted by MROKI On Friday, February 06, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu, Geita
SERIKALI imewahimiza wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza katika viwanda vya uchenjuaji na uchakataji wa madini ya dhahabu mkoani Geita ili kuongeza thamani ya madini, kuimarisha ajira, kulinda mazingira na kukuza mapato ya Taifa.

Wito huo umetolewa na Mjiolojia kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Geita, John Maganga, wakati wa ziara ya kutembelea masoko ya madini mkoani humo, ambapo amesema Geita ina fursa kubwa ya uwekezaji kutokana na uzalishaji mkubwa wa dhahabu unaofanywa na wachimbaji wadogo na wa kati.

Amesema licha ya uzalishaji huo, bado kuna upungufu wa viwanda vya uchenjuaji na uchakataji wa dhahabu, hali inayosababisha madini mengi kuuzwa yakiwa ghafi bila kuongeza thamani, jambo linalonyima wananchi na Serikali mapato makubwa.

“Ni wakati sasa kwa wawekezaji kuchangamkia fursa zilizopo Geita kwa kujenga viwanda vya uchenjuaji na uchakataji wa dhahabu, hatua itakayopunguza matumizi ya zebaki, kulinda afya za wananchi na mazingira, pamoja na kuongeza mapato ya Serikali,” amesema.

Ameeleza kuwa uanzishwaji wa viwanda hivyo utaenda sambamba na uwepo wa masoko rasmi ya madini, ambayo yameimarisha uwazi, usalama na ufanisi katika biashara ya dhahabu, na kudhibiti vitendo vya magendo vilivyokuwa vikisababisha upotevu wa mapato ya Serikali.

Ameongeza kuwa masoko ya dhahabu yamekuwa kichocheo cha ukuaji wa uchumi wa mkoa wa Geita kwa kuongeza ajira, biashara na mzunguko wa fedha, huku wachimbaji wakinufaika kwa kuuza madini yao kwa bei ya soko na kwa mifumo rasmi ya Serikali.

Kwa upande wake, Afisa Mthaminishaji wa Madini, Peter Jamhuri, amesema mifumo ya kidigitali inayotumika katika masoko ya madini imeongeza uwazi na ufanisi kwa kuwezesha ukusanyaji wa takwimu sahihi za mauzo, jambo linalosaidia wafanyabiashara kupata mikopo kutoka taasisi za fedha.

Amesema mifumo hiyo imeimarisha uwazi na kuondoa magendo, huku akimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kusimamia sera na mifumo bora inayochochea maendeleo ya sekta ya madini na uchumi wa Taifa kwa ujumla.

“Kwa sasa wafanyabiashara wanapata ripoti za mauzo zinazotumika kama vielelezo muhimu katika taasisi za kifedha, hali inayochochea upanuzi wa biashara na uwekezaji zaidi,” amesema.

Naye mfanyabiashara wa dhahabu na mmiliki wa Gambo Mining Ltd, Magambo Magambo, amesema kuanzishwa kwa masoko rasmi ya madini kumeleta mapinduzi makubwa katika sekta hiyo na kusaidia kukuza wafanyabiashara wazawa.






Posted by MROKI On Friday, February 06, 2026 No comments


Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana,  imesaini Hati ya Makubaliano (MoU) na Benki ya CRDB kupitia CRDB Bank Foundation kwa ajili ya uendeshaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, hatua inayolenga kuimarisha uwezeshaji wa vijana kiuchumi, kijamii na kitaaluma nchini.

Hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo imefanyika katika Ofisi za Wizara ya Maendeleo ya Vijana zilizopo Mtumba, jijini Dodoma, na kushuhudiwa na Mheshimiwa Joel Arthur Nanauka, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana.

Katika hatua muhimu ya utekelezaji wa mfuko huo, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameidhinisha na kutoa jumla ya Shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kuanza rasmi kwa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana. Fedha hizo zinalenga kuwawezesha vijana kunufaika na fursa za mikopo nafuu, ujasiriamali, ubunifu, ajira pamoja na miradi ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Hundi ya fedha hizo imekabidhiwa rasmi na Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, kwa niaba ya Mheshimiwa Rais, kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Mheshimiwa Joel Arthur Nanauka, katika hafla iliyofanyika kwenye Ofisi za Waziri Mkuu, Mji wa Serikali, jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri wa Maendeleo ya Vijana amesema kuwa kuanzishwa kwa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ni uthibitisho wa dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais, ya kuwawezesha vijana kiuchumi, kuwaandaa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya taifa, na kujenga msingi imara wa kizazi chenye tija kwa sasa na baadaye


Posted by MROKI On Friday, February 06, 2026 No comments

February 05, 2026









WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amekabidhi hundi ya shilingi bilioni 200 kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka ikiwa ni utekelezaji wa vitendo wa ahadi ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, ya kutenga na kutoa mitaji kwa ajili ya kuwawezesha vijana na wanawake.
 
Pia, Waziri Mkuu amesema uwezeshaji wananchi kiuchumi ni mhimili wa kukuza uzalishaji, biashara, uwekezaji na ustawi wa maisha ya wananchi, hasa vijana na wanawake ambapo amezitaka wizara, taasisi na mamlaka za kisekta zinazoendelea kutekeleza mpango huo kuhakikisha fedha hizo zinawafikia walengwa wote na program zilizokusudiwa na kutoa tija tarajiwa.
 
“Utoaji wa Hundi ya Shilingi Bilioni 200 unaonesha kwa vitendo kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inatekeleza ahadi zake kwa vitendo, si kwa maneno. Tukio hili linaweka msingi mpya wa kuimarisha ushiriki wa vijana na wanawake katika uchumi wa Taifa na kuharakisha safari ya Tanzania kuelekea uchumi jumuishi na endelevu.”
 
Amekabidhi hundi hiyo leo Alhamisi, Februari 5, 2026 katika ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma, ambapo pamoja na mambo mengine amesisitiza kuwa mafanikio hayo hayatapimwa kwa kiasi cha fedha kilichotolewa, bali kwa mabadiliko halisi ya maisha ya wananchi, hususan vijana na wanawake.
 
“Wizara, Taasisi na Mamlaka zote zinazoshiriki katika utekelezaji wa uwezeshaji kiuchumi lazima zibadilishe mtazamo kutoka katika kutoa fedha kwenda katika kusimamia matokeo na kwamba kila taasisi ijiwekee malengo yanayopimika, viashiria vya utendaji na ratiba za utekelezaji, ili kuhakikisha mitaji hiyo inazalisha ajira, kipato na biashara endelevu.”

Waziri Mkuu amesisitiza kwamba uwezeshaji huo usiwe zoezi la kawaida la kiofisi bali uwe chombo cha mageuzi ya kiuchumi, hivyo utekelezaji wa Shilingi Bilioni 200 lazima uendeshwe kwa uwazi na uwajibikaji. “Taarifa za maendeleo zitolewe mara kwa mara, na hatua zichukuliwe dhidi ya matumizi mabaya. Serikali haitasita kuchukua hatua kwa yeyote atakayekiuka dhamira ya uwezeshaji huu.”

Kadhalika, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema katika kipindi kifupi cha Novemba 2024 hadi Januari 2025, Serikali kupitia mifuko na programu za kuwawezesha wananchi kuichumi imetoa mikopo na dhamana zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 66.9 kwa wanufaika zaidi ya 13,000, wakiwemo vijana na wanawake katika sekta mbalimbali.

Kwa upande wakeWaziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu); William Lukuvi amemshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwa kinara katika kukuza uwezeshaji kiuchumi pamoja na jitihada mbalimbali anazofanya katika kuhakikisha vijana na wanawake wanashiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuwawezesha mitaji.

Waziri Lukuvi amesema hata hivyo, changamoto ya upatikanaji wa mitaji ikiwemo mikopo, vifaa, mashine na mitambo bado imekuwa kikwazo kikubwa cha ukuaji wa shughuli za kiuchumi zinazotekelezwa na vijana na wanawake. ”Kutokana na changamoto hiyo, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameongeza fedha shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kuwawezesha vijana na wanawake.
 
Amesema uwezeshaji huo wa shilingi bilioni 200 ni uthibitisho wa maono na dhamira aliyonayo Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inayolenga kupanua wigo wa upatikanaji wa mitaji ya gharama nafuu kwa vijana na wanawake ili waweze kuwa shindani kitaifa, kikanda na kimataifa.
Posted by MROKI On Thursday, February 05, 2026 No comments
Dar es Salaam — Kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia kinywaji chake cha kifahari cha Tanzanite Royal Gin imezindua rasmi kampeni maalum ya msimu wa Siku ya Wapendanao (Valentine’s Day) ijulikanayo kama “Tanzanite Royal Gin – Royal Love Challenge 2026”, yenye lengo la kuimarisha uhusiano na wateja pamoja na kusherehekea mapenzi kwa njia ya kipekee.

Akizungumza kuhusu kampeni hiyo, Izack Piganio, Meneja wa Chapa Mati Super Brands, alisema, "Royal Love Challenge ni njia yetu ya kuwapa wateja uzoefu wa kipekee wa kusherehekea Valentine’s Day, huku tukijenga uhusiano wa karibu na wapenzi na wanandoa kupitia chapa ya Tanzanite Royal Gin. Tunataka mapenzi yashehereke kwa hadhi ya kifalme, na washiriki washindwe kwa ubunifu na upendo wao."
Shindano hili la mtandaoni litafanyika kupitia mtandao wa kijamii wa Instagram, likiwalenga wapenzi, couples na wanandoa. Washiriki wanatakiwa kupiga picha wakionyesha upendo wao pamoja na chupa halisi ya Tanzanite Royal Gin, kisha kuipakia kwenye akaunti zao za Instagram. Ili kushiriki kikamilifu, washiriki wanapaswa kutag ukurasa rasmi wa @TanzaniteRoyalGin, kutumia hashtag #RoyalLoveChallenge, na kufanya collaboration na ukurasa wa kampeni.

Kwa upande wake, Meneja wa hoteli ya Asmorain, Amina Mrutu, alisema: "Tunakufariji kuwa sehemu ya kampeni hii ya Royal Love Challenge. Tunatarajia mshindi atapata zawadi za kipekee zenye mchanganyiko wa mapenzi na burudani, ikiwemo usiku mmoja katika hoteli yetu, chakula cha jioni cha kimapenzi na safari ya kupumzika Hifadhi ya Taifa ya Tarangire."
Mshindi wa Royal Love Challenge 2026 atatangazwa Februari 12, 2026, huku zawadi zote zikitolewa rasmi Februari 14, siku ya Valentine’s Day. Kampeni hii inatarajiwa kuleta burudani, ushindani chanya, na kuendeleza utamaduni wa kusherehekea mapenzi kwa hadhi ya kifalme.
Posted by MROKI On Thursday, February 05, 2026 No comments

Waziri wa Fedha, Mhe Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) akieleza kuhusu maeneo ya uwekezaji wakati wa mkutano na  Kiongozi wa Timu ya Wataalamu kutoka Taasisi ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya nchi kukopesheka katika masoko ya mitaji ya kimataifa ya Moody’s Investor Service, ikiongozwa na  Bw. John Walsh (hayupo pichani), kilichofanyika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) akiongoza Kikao na  Timu ya Wataalamu kutoka Taasisi ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya nchi kukopesheka katika masoko ya mitaji ya kimataifa  ikiongozwa na  Bw. John Walsh (wa kwanza kulia), kilichofanyika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Kiongozi wa Timu ya Wataalamu kutoka Taasisi ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya nchi kukopesheka katika masoko ya mitaji ya kimataifa (Sovereign Credit Rating) Moody’s Investor Service, Bw. John Walsh,  akielezea  kuhusu ujio wa Timu yake nchini ili kufanya tathimini mpya ya uwezo wa Tanzania kukopesheka katika Soko la Kimataifa la mitaji, wakati wa kikao na Waziri wa Fedha, Mhe Balozi Khamis Mussa Omar (Mb),  kilichofanyika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Kiongozi wa Timu ya Wataalamu kutoka Taasisi ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya nchi kukopesheka katika masoko ya mitaji ya kimataifa (Sovereign Credit Rating) Moody’s Investor Service, Bw. John Walsh,  akielezea  kuhusu ujio wa Timu yake nchini ili kufanya tathimini mpya ya uwezo wa Tanzania kukopesheka katika Soko la Kimataifa la mitaji, wakati wa kikao na Waziri wa Fedha, Mhe Balozi Khamis Mussa Omar (Mb),  kilichofanyika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Timu ya Wataalamu wa Wizara ya Fedha wakifuatilia maelezo ya Waziri wa Fedha, Mhe Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati wa Kikao na   Timu ya Wataalamu kutoka Taasisi ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya nchi kukopesheka katika masoko ya mitaji ya kimataifa (Sovereign Credit Rating) Moody’s Investor Service (Moody’s) ikiongozwa na Bw. John Walsh (hawapo pichani), kilichofanyika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Timu ya Wataalamu kutoka Taasisi ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya nchi kukopesheka katika masoko ya mitaji ya kimataifa (Sovereign Credit Rating) Moody’s Investor Service (Moody’s) ikiongozwa na Bw. John Walsh (kulia), wakisikiliza maelezo ya Waziri wa Fedha, Mhe Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa Bajeti, Bw. Meshack Anyingisye (kushoto) na Kamishna Msaidizi wa Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama, wakifuatilia kikao kati ya Waziri wa Fedha, Mhe Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) na Kiongozi wa Timu ya Wataalamu kutoka Taasisi ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya nchi kukopesheka katika masoko ya mitaji ya kimataifa (Sovereign Credit Rating) Moody’s Investor Service (Moody’s), Bw. John Walsh (hawapo pichani), Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.

***************

Na. Peter Haule. na Jordan Mbwambo, WF, Dodoma

Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesema kuwa mageuzi ya uchumi yataendelea kuwa ajenda ya muda mrefu yakilenga si tu kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi bali kuhakikisha ukuaji huo unachangia katika upatikanaji wa ajira na ustawi wa wananachi kwa ujumla.

Amebainisha hayo wakati wa kikao na Timu ya Wataalamu kutoka Taasisi ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya nchi kukopesheka katika masoko ya mitaji ya kimataifa ya Moody’s Investor Service ikiongozwa na  Bw. John Walsh, kilichofanyika Ofisi za Treasury Square, jijini Dodoma.

 

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa uchumi wa nchi umeendelea kuimarika licha ya matukio kadhaa yaliyokwaza ustawi wa uchumi wa dunia ukiwemo uviko 19 ambapo katika kipindi cha mwaka jana uchumi ulikua kwa asilimia 5.4 na unatarajiwa kukua zaidi mwaka huu wa fedha 2025/26 hadi kufikia asilimia 6.

 

Aidha, alibainisha kuwa mahitaji ya uwekezaji yanaendelea kuwa makubwa hususani kwenye miundombinu ya kimkakati kama Bandari, Viwanja vya Ndege, Reli na mtandao wa Barabara ili kuchochea maendeleo.

 

Alieleza kuwa nchi inaendelea kuwekeza katika ujenzi wa miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Reli iendayo Kasi -SGR, Bwawa la uzalishaji wa umeme la Julius Nyerere na uimarishaji wa sekta nyingine za kijamii na kiuchumi hatua itakayochochea zaidi ukuaji na uimara wa uchumi wa nchi na maendeleo ya jamii.

 

Akizungumzia Mfumuko wa bei amesema kuwa, hali imeendelea kuwa tulivu ambapo kiwango cha mfumuko wa bei kimeendelea kubaki chini ya asilimia tano kwa miaka kadhaa, kikiwa kati ya asilimia 2.9 na 3.4.

 

Kwa upande wake Kiongozi wa Timu ya Wataalamu kutoka Taasisi ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya nchi kukopesheka katika masoko ya mitaji ya kimataifa Moody’s,  Bw. John Walsh, alisema kuwa uamuzi wa kupandisha hadhi ya uwezo wa nchi kukopesheka na kuipa alama B1 yenye mtazamo thabiti ulitokana na uthabiti wa kiuchumi na kifedha ambao nchi imeuonesha licha ya changamoto za uchumi za dunia katika miaka ya karibuni.


Alisema kuwa Tanzania iliendelea kurekodi ukuaji thabiti wa uchumi licha ya athari za janga la UVIKO-19, mfumuko wa bei wa kimataifa na kupanda kwa viwango vya riba duniani.


“Uamuzi wa kupandisha hadhi kwa kiwango cha B1 ulitokana na uthabiti wa sera za uchumi jumla na mageuzi ya Serikali yanayotekelezwa chini ya Mpango wa Shirika la Fedha la Kimatafa (IMF), unaokaribia kukamilika”, alisema Bw. Walsh.


Alisema kuwa Serikali imepiga hatua muhimu katika kushughulikia changamoto za muda mrefu, ikiwemo ukusanyaji mdogo wa mapato ya ndani na mapungufu ya utekelezaji wa sera, hivyo Tathmini ya sasa inalenga kufuatilia mafanikio, changamoto zilizopo, na mwelekeo wa mageuzi katika kipindi cha miaka miwili iliyopita.


Aidha alieleza kuwa tathmini hiyo inalenga kupata taswira ya kina ya hali ya sasa ya uchumi wa Tanzania, mafanikio yaliyopatikana, pamoja na hatua zinazochukuliwa kuhakikisha ukuaji endelevu na uthabiti wa kifedha kwa muda mrefu.

Matokeo ya mapitio ya hivi karibuni ya Kampuni za Moody’s na Fitch ziliipa Tanzania daraja la B1 (stable outlook) na B+ (stable outlook), mtawalia ambayo yanaonesha kwamba Tanzania ni nchi salama kwa wawekezaji.

Posted by MROKI On Thursday, February 05, 2026 No comments
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza jambo wakati wa Kikao chake na Uongozi wa Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania, ulioongozwa na Mwenyekiti wa Bodi wa Kampuni hiyo Bw. David Tarimo (hayupo pichani), ambapo walijadiliana masuala mbalimbali ya kukuza sekta ya mawasiliano na masuala ya kidigitali katika maendeleo ya uchumi wa jamii, ambacho kilifanyika katika Ofisi ya Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania, Bw. Philip Besiimire, akizungumza jambo wakati wa kikao cha Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani) na Kampuni hiyo kilichofanyika katika Ofisi ya Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma, ambapo walijadiliana masuala mbalimbali ya kukuza sekta ya mawasiliano na masuala ya kidigitali katika maendeleo ya Uchumi wa jamii, ambacho kilifanyika katika Ofisi ya Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiongoza kikao chake na Uongozi wa Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania, ulioongozwa na Mwenyekiti wa Bodi wa Kampuni hiyo Bw. David Tarimo (hayupo pichani), ambapo walijadiliana masuala mbalimbali ya kukuza sekta ya mawasiliano na masuala ya kidigitali katika maendeleo ya Uchumi wa jamii, ambacho kilichofanyika katika Ofisi ya Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania, Bw. David Tarimo (Kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao cha Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani) na Kampuni hiyo kilichofanyika katika Ofisi ya Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma, ambapo walijadiliana masuala mbalimbali ya kukuza sekta ya mawasiliano na masuala ya kidigitali katika maendeleo ya uchumi wa jamii, ambacho kilifanyika katika Ofisi ya Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma. Kushoto ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania, Bw. Philip Besiimire.
**************
Na Benny Mwaipaja, Dodoma
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesema kuwa Serikali inatambua mchango mkubwa wa sekta ya mawasiliano katika kukuza uchumi jumuishi wa nchi kupitia mageuzi makubwa ya uchumi wa kidigitali, ulipaji kodi na uboreshaji wa huduma za jamii.

Mhe. Balozi Omar amesema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na Uongozi wa Kampuni ya Simu ya Vodacom ikiongozwa na Mwenyekiti wake wa Bodi, Bw. David Tarimo, katika Ofisi za Hazina-Treasury Square, Jijini Dodoma.

Aliishauri sekta ya mawasiliano nchini itumie fursa ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050 iliyozinduliwa hivi karibuni, kuchangia zaidi maendeleo ya nchi Kupitia matumizi ya teknolojia ambayo itachangia kuongeza ukwasi kwa makundi mbalimbali wakiwemo vijana.

Mhe. Balozi Omar aliahidi kuwa Serikali kwa uopande wake itaendelea kuboresha na kuweka mazingira bora ya uwekezaji ili kuchochea na kukuza mchango wa sekta ya mawasiliano nchini katika kuboresha maisha ya wananchi na kuwawezesha wawekezaji kupata faida.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa VODACOM, Bw. David Tarimo, aliishukuru Serikali kwa kuweka mazingira mazuri ya ufanyaji biashara kwa wawekezaji hali iliyoifanya sekta ya mawasiliano kuchangia kodi ya zaidi ya shilingi trilioni 1.1 katika mwaka wa fedha 2024/2025, huku Vodacom ikichangia zaidi ya shilingi bilioni 621 hadi ilipofikia mwezi Machi, 2025.

Aidha, Bw. Tarimo alieleza kuwa tangu Kampuni yake izinduliwe imewekeza zaidi ya shilingi trilioni 4.5 kwa ajili ya Kujenga miundombinu ya mawasiliano na na mwaka jana 2025 imesaidia jamii zaidi ya shilingi bilioni 3.7 kwa kufadhili miradi mbalimbali ikiwemo sekta za afya, elimu, mazingira na kuwawezesha vijana kiuchumi.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), Kaimu Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha, Bi. Dionisia Mjema, Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania, Bw. Philip Besiimire, Mkurugenzi wa Masuala ya Nje wa Vodacom Tanzania, Bi. Zuweina Farah, na maafisa wengine waandamizi wa Wizara ya Fedha na Vodacom.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb)(kulia), akiagana na Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania, Bw. David Tarimo, baada ya Kikao chake na uongozi wa Kampuni hiyo, kilichojadili masuala mbalimbali ya kukuza sekta ya mawasiliano na masuala ya kidigitali katika maendeleo ya uchumi wa jamii, ambacho kilifanyika katika Ofisi ya Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (wa tatu kushoto), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania, Bw. David Tarimo (wa tatu kulia), Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania, Bw. Philip Besiimire (wa pili kushoto), Mkurugenzi wa Masuala ya Nje wa Vodacom Tanzania, Bi. Zuweina Farah (kushoto) na maafisa wengine waandamizi wa kampuni hiyo, wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kikao chao kilichojadili masuala mbalimbali ya kukuza sekta ya mawasiliano na masuala ya kidigitali katika maendeleo ya uchumi wa jamii, ambacho kilifanyika katika Ofisi ya Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.

Posted by MROKI On Thursday, February 05, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo