Nafasi Ya Matangazo

July 28, 2026

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, akiongoza Kikao cha Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kilichofanyika katika Afisi Kuu ya CCM, Kisiwandui, Zanzibar, leo Jumanne, tarehe 28 Julai 2026.






Posted by MROKI On Tuesday, July 28, 2026 No comments




Wananchi zaidi ya 500 kutoka Kata za Chanji, Msua, Kantalamba na Kizwite zilizopo Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa wamenufaika na huduma mbalimbali za afya zilizotolewa bure na Jeshi la Polisi Mkoa wa Rukwa kupitia Zahanati ya Polisi Mkoa wa Rukwa, ikiwa ni sehemu ya kusogeza huduma za afya karibu na wananchi na kuimarisha ustawi wa jamii.


Huduma hizo zilitolewa Julai 28, 2026 katika Zahanati ya Serikali Kizwite, ambapo wananchi walipatiwa vipimo vya kisasa vya Ultrasound, uchunguzi wa magonjwa mbalimbali, ushauri wa kitaalamu pamoja na dawa bila malipo. Huduma hizo ni miongoni mwa huduma ambazo kwa kawaida hazipatikani katika zahanati hiyo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa zoezi hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Shadrack Masija, alisema Jeshi la Polisi linaendelea kutekeleza dhana ya Polisi Jamii kwa vitendo kupitia ushiriki wake katika shughuli za maendeleo na utoaji wa huduma zinazogusa maisha ya wananchi.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Manispaa ya Sumbawanga, Dkt. Robert Lwebangila, aliipongeza Zahanati ya Polisi Mkoa wa Rukwa kwa kushirikiana na Halmashauri ya Manispaa katika kusogeza huduma za afya karibu na wananchi, akisema ushirikiano huo unaimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya.

Naye Mkuu wa Kikosi cha Afya Polisi Mkoa wa Rukwa, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Edgar Ullaya, alisema lengo la zoezi hilo ni kuwapatia wananchi huduma za uchunguzi na matibabu bila gharama pamoja na kugundua mapema changamoto za kiafya ili kutoa tiba stahiki.

Mganga Mfawidhi wa Zahanati ya Serikali Kizwite, Dkt. Simon Mjema, alisema huduma za Ultrasound zimeongeza uwezo wa zahanati hiyo kuwahudumia wananchi waliokuwa wakilazimika kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo katika vituo vingine vya afya.

Kwa upande wake, Kaimu Mtendaji wa Kata ya Chanji, Dominica Mwaipopo, aliishukuru Serikali na Jeshi la Polisi kwa kuandaa huduma hiyo, akisema imepunguza gharama na muda ambao wananchi walikuwa wakitumia kutafuta matibabu.

Baadhi ya wananchi waliopata huduma hizo walieleza kufurahishwa na hatua ya Jeshi la Polisi kusogeza huduma za afya karibu na makazi yao na kuomba zoezi hilo liendelee ili wananchi wengi zaidi wanufaike.

Zoezi hilo ni sehemu ya juhudi za Jeshi la Polisi Mkoa wa Rukwa za kuimarisha ushirikiano na jamii kupitia utoaji wa huduma za kijamii zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.
Posted by MROKI On Tuesday, July 28, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia wakati wa ufunguzi wa Semina Elekezi kwa Mawaziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Mawasiliano Serikalini, tarehe 28 Julai, 2026, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amefungua Semina Elekezi ya Mawaziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Mawasiliano Serikalini, katika Ikulu ya Tunguu, Zanzibar.

Semina hiyo ya siku mbili imewakutanisha, kwa mara ya kwanza, viongozi waandamizi wa Serikali kutoka pande zote mbili za Muungano, kwa lengo la kujenga uelewa na msimamo wa pamoja kuhusu mawasiliano ya Serikali na umma.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Rais Dkt. Samia amesema mawasiliano ya Serikali yanahitaji uratibu, weledi na mwelekeo wa kimkakati ili kujenga imani ya wananchi kwa Serikali na kulinda maslahi ya Taifa. 

“Mawasiliano ni sehemu ya uongozi na nyenzo ya kimkakati ya kulinda maslahi ya Taifa,” amesema Rais Dkt. Samia.

Ameeleza kuwa mawasiliano yanapotumika vizuri hujenga ushirikishwaji na imani ya wananchi kwa Serikali, huku taarifa sahihi zikiwawezesha kuelewa na kushiriki katika mipango ya maendeleo.

“Taarifa za Serikali zinapaswa kutolewa kwa wakati, kwa lugha inayoeleweka na kwa takwimu zilizothibitishwa,” amesema.

Rais Dkt. Samia amesema Serikali zote mbili zimepata mafanikio katika sekta za elimu, afya, miundombinu, nishati na maeneo mengine ya maendeleo, ambayo yanapaswa kuelezwa kwa wananchi kwa ufasaha.

Kuhusu Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, amesema Serikali zote mbili zimeanza kutekeleza mageuzi makubwa ya uchumi na huduma zinazowagusa wananchi moja kwa moja. 

Amesema takribani asilimia 70 ya utekelezaji wa Dira 2050 inategemea ushiriki wa sekta binafsi, hivyo mafanikio yake yanahitaji mawasiliano na ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na sekta hiyo.

Awali, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Mpogole Kusiluka, amesema semina hiyo ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais Dkt. Samia ya kuwajengea viongozi uwezo katika mawasiliano ya Serikali na umma.

Amesema mafunzo hayo yatahusu utoaji wa taarifa kwa ufasaha na kwa wakati, pamoja na matumizi sahihi ya vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.
Viongozi mbalimbali wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa Semina Elekezi kwa Mawaziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Mawasiliano Serikalini, tarehe 28 Julai, 2026, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar
Viongozi mbalimbali wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa Semina Elekezi kwa Mawaziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Mawasiliano Serikalini, tarehe 28 Julai, 2026, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu Prof. Palamagamba A. Kabudi akitoa mada inayohusu Muungano na Mawasiliano; Msingi, Muundo na Umuhimu wake wakati wa ufunguzi wa Semina Elekezi kwa Mawaziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Mawasiliano Serikalini, tarehe 28 Julai, 2026, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar.

Viongozi mbalimbali wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa Semina Elekezi kwa Mawaziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Mawasiliano Serikalini, tarehe 28 Julai, 2026, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar

Viongozi mbalimbali wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa Semina Elekezi kwa Mawaziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Mawasiliano Serikalini, tarehe 28 Julai, 2026, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar

Viongozi mbalimbali wakifuatilia mada wakati wa Semina Elekezi kwa Mawaziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Mawasiliano Serikalini, tarehe 28 Julai, 2026, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar
Viongozi mbalimbali wakifuatilia mada wakati wa Semina Elekezi kwa Mawaziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Mawasiliano Serikalini, tarehe 28 Julai, 2026, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar



Posted by MROKI On Tuesday, July 28, 2026 No comments

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Salaam Maalum kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Mhe Xi Jinping iliyokabidhiwa kwake na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania ni Mhe. Chen Mingjian, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar tarehe 28 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania ni Mhe. Chen Mingjian, Ikulu ya Tunguu, Zanzibar tarehe 28 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania ni Mhe. Chen Mingjian mara baada ya kumaliza mazungumzo yaliyofanyika Ikulu ya Tunguu, Zanzibar tarehe 28 Julai, 2026.

Posted by MROKI On Tuesday, July 28, 2026 No comments
Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Elias Magosi, akizungumza wakati wa ufunguzi wa Wiki ya Tisa ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026), inayoadhimishwa katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini. Mkutano huo unawakutanisha viongozi wa serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo kujadili mikakati ya kuharakisha maendeleo ya viwanda na biashara ya kikanda.
Washiriki wa Wiki ya Tisa ya Viwanda kutoka nchi wanachama wa SADC wakifuatilia hotuba ya Mgeni Rasmi, Katibu Mtendaji wa SADC, Elias Magosi, wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), Durban, Afrika Kusini.
Meneja wa Utafiti na Biashara Dkt.Hilderbrand Shayo na Meneja wa Mawasiliano, Masoko na Mahusiano Bw. Allan Chonjo, kutoka Benki ya Maendeleo - TIB wakitoa maelezo kuhusu bidhaa na huduma zinazotolewa na Benki hiyo kwa mdau aliyetembelea banda la Tanzania, pembezoni mwa Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.
Meneja wa Mawasiliano, Masoko na Mahusiano wa Benki ya Maendeleo - TIB, Bw. Allan Chonjo akitoa maelezo kuhusu bidhaa na huduma zinazotolewa na Benki hiyo kwa baadhi ya wadau waliotembelea Banda la Tanzania, pembezoni mwa Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.
********************
 Na Ramadhani Kissimba, Durban
Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) imezitaka nchi wanachama kuongeza kasi ya utekelezaji wa ajenda ya maendeleo ya viwanda kwa kuwekeza katika kuongeza thamani ya malighafi na kuimarisha miundombinu ili kukuza biashara, ajira na ustawi wa wananchi wa Jumuiya ya hiyo.

Wito huo umetolewa na Katibu Mtendaji wa SADC, Bw. Elias Magosi, wakati akifungua rasmi Wiki ya Tisa (9) ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) inayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Durban, Afrika Kusini.

Alisema kuwa ukanda wa SADC una rasilimali nyingi za kilimo, madini na nishati ambazo zinapaswa kutumika kama msingi wa kujenga uchumi wa viwanda badala ya kuendelea kuuza malighafi bila kuziongezea thamani.

Alisisitiza kuwa maendeleo ya viwanda hayawezi kufikiwa bila ushirikiano wa karibu kati ya serikali, sekta binafsi, taasisi za fedha na wadau wa maendeleo. 

“Ushirikiano utasaidia kuvutia uwekezaji, kuongeza ushindani wa bidhaa za ukanda na kuimarisha biashara ndani ya SADC, hatua itakayochochea ukuaji wa uchumi jumuishi na wenye manufaa kwa wananchi wote” alisema Bw. Magosi.

Aidha, alizihimiza nchi wanachama kuwekeza katika miundombinu ya nishati, usafirishaji, TEHAMA na ubunifu, pamoja na kuwawezesha wanawake na vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na ujasiriamali wa viwanda.

Wiki ya Viwanda ya SADC imebeba kaulimbiu isemayo: "Kukuza Viwanda Imara, Endelevu na Jumuishi kupitia Maendeleo ya Miundombinu, Mageuzi ya Kilimo na Madini kwa Ajili ya Dunia Yenye Haki." Ikihimiza matumizi ya rasilimali zilizopo katika nchi wanachama katika kujenga uchumi wenye ushindani, unaostahimili changamoto za kiuchumi na mabadiliko ya tabianchi. 

Mkutano huo wa siku tano unaowakutanisha Viongozi wa Serikali, sekta binafsi, wawekezaji, wataalamu na wadau wa maendeleo kutoka nchi wanachama wa SADC unatarajiwa kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuimarisha ushindani wa viwanda kwa nchi za SADC, kuvutia uwekezaji mpya na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo pamoja na madini, ukiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea Mkutano wa 46 wa kawaida wa  Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC utakaofanyika tarehe 17 Agosti, 2026 Jijini Durban, Afrika ya Kusini. 
Meneja wa Utafiti na Biashara kutoka Benki ya Maendeleo - TIB, Dkt.Hilderbrand Shayo akimkabidhi zawadi Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani Tanzania (FCC), Bi. Khadija Juma Ngasongwa alipotembelea Banda la Tanzania katika maonesho yanayofanyika sambamba na Wiki ya Tisa ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), Durban, Afrika Kusini.
Posted by MROKI On Tuesday, July 28, 2026 No comments

Dar es Salaam,
Kufuatia kuimarishwa kwa mfumo wa udhibiti wa biashara haramu ya madini unaofanywa na Wizara ya Madini kupitia Kikosi Kazi (Taskforce), madini aina ya dhahabu Gramu 4,402.20 yenye thamani ya 1,238,458,594.42 yamekatwa yakitoroshwa.

Hayo yamesemwa tarehe 27 Julai, 2026 na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde  Jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na vyombo vya habari.

Serikali kupitia Wizara ya Madini iliunda Kikosi kazi ambacho kinahusisha vyombo vya dola ili kudhibiti biashara haramu ya madini na utoroshaji. Hii ni sehemu tu ya kazi ambazo zimeendelea kufanywa na Kikosi kazi hicho katika kuimarisha mfumo wa ufanyaji biashara ya madini.

"Ndugu zangu, dhahabu hii yenye zaidi ya thamani ya bilioni 1.2 haikupitia katika mfumo rasmi wa ufanyaji biashara ya madini na hivyo kupelekea Serikali kukosa mapato ambayo yangeisaidia kuimarisha utoaji wa huduma mbalimbali kwa wananchi," amesisitiza  Mhe. Mavunde.

Aidha, Waziri Mavunde amebainisha kuwa dhahabu hiyo iliyokamatwa imetaifishwa kwa mujibu wa taratibu za Sheria na imehifadhiwa Benki Kuu ya Tanzania.

Vilevile, Mhe. Mavunde amekielekeza Kikosi Kazi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola kumhoji vizuri mtuhumiwa aliyekamatwa na dhahabu hizo kufahamu alikotoka na alikuwa anapeleka wapi, ili kuweza kutibu kabisa mzizi wa vitendo hivyo na kuvunja mnyororo wa wote wa utoroshaji.

Mhe. Mavunde amesisitiza kuwa, iwapo mtuhumiwa aliyekamatwa alikuwa na leseni ya ufanyaji biashara ya madini kufutiwa leseni hiyo mara moja na kuingizwa kwenye orodha maalum ya wenye makosa (blacklisted) ili asiruhusiwe tena kufanya biashara ya madini nchini.

Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde ametoa rai kwa wananchi wote kuzingatia na kufuata sheria na mifumo ya ufanyaji biashara ya madini ambayo tumejiwekea kupitia masoko ya madini na vituo vya ununuzi ambavyo vimesambaa Nchi nzima.
Posted by MROKI On Tuesday, July 28, 2026 No comments









Na Neema Chalila Mbuja
NAIBU Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii Bw. Nkoba Mabula leo Julai 27, 2026 amefungua rasmi Kikao Kazi cha Wadau wa Sekta ya Utalii kujadili Rasimu ya Mpango Mkakati wa Miaka Mitano wa wizara hiyo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2030, wenye lengo la kutoa mwelekeo  wa utekelezaji wa pamoja wa malengo yaliyowekwa na vipaumbele vyake.

Akizungumza kwenye kikao hicho kilichojumuisha wadau wa Sekta ya Utalii wakiwemo Wakurugenzi wa Idara za Wanyamapori, Utalii na Malikale, Bw. Mabula amesema mchango wa wadau wa sekta hiyo ni muhimu kwani wao ndio watekelezaji wa mipango, mikakati na vipaumbele mbalimbali vilivyowekwa na Wizara na ndio maana wamealikwa ili kutoa maoni yao juu ya Mpango Mkakati huo ili kufikia malengo yaliyowekwa.

“Kuelekea lengo la kufikia watalii milioni 8 ifikapo mwaka 2030 niwaombe wadau kushirikiana na Wizara ili kuhakikisha malengo yanafikiwa na kuongeza pato la Taifa,” amesema Bw. Mabula.

Akiwasilisha Rasimu ya Mpango Mkakati huo wa Wizara,   Mkurugenzi wa Sera na Mipango kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii,  Bw. Abdullah Mvungi amesema Rasimu ya Mpango Mkakati huo wa Wizara imeainisha ni nini Wizara inataka kufanya, ni vipaumbele gani vya utekelezaji na ni malengo yapi yanapimika sambamba na viashiria vya utekelezaji ili kufikia malengo mahususi. 

Amesema Rasimu ya Mpango Mkakati wa Wizara imeandaliwa kwa kuangalia vipaumbele vya utekelezaji kwa upande wa Serikali ikiwemo mapambano dhidi ya rushwa na Ukimwi, uelekeo wa Dira 2050 ambayo inaitaka Wizara kuhakikisha idadi ya watalii na mapato yatokanayo na utalii vinaongezeka, sambamba na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya Mwaka 2025.

Kwa upande wa wadau waliotoa maoni ya utekelezaji wa Mpango Mkakati huo wameipongeza wizara kwa kuandaa rasimu iliyogusa maeneo yote ya utekelezaji na kuahidi kushirikiana bega kwa bega na Wizara ili malengo mahususi hayo yaweze kufikiwa.

Miongoni kwa maeneo yaliyopewa kipaumbele ni pamoja na kuongeza nguvu ya kutangaza vivutio vya utalii, kutunza urithi wa malikale na kushirikisha zaidi jamii kwenye shughuli za uhifadhi.
Posted by MROKI On Tuesday, July 28, 2026 No comments

July 27, 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Ndugu Prisca Burton Lwangili kuwa Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Tunguu Zanzibar, tarehe 27 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Dkt. LatifaMohammed Khamis kuwa Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais – Muungano kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Tunguu Zanzibar, tarehe 27 Julai, 2026.

Viongozi  Wateule wakiapa kiapo cha uadilifu kwa Viongozi wa Umma kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Tunguu Zanzibar, tarehe 27 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka viongozi wateule kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, ushirikiano na bila upendeleo, wakitanguliza huduma kwa wananchi na maslahi ya Taifa. Rai hiyo ameitoa leo Ikulu, Tunguu, Zanzibar, baada ya kuwaapisha Naibu Makatibu Wakuu wawili na kushuhudia viongozi wengine wanne wakila Kiapo cha Uadilifu kwa Viongozi wa Umma. Amesema uteuzi huo unaonesha imani ya Serikali kwa viongozi hao, hivyo wanapaswa kufanya kazi kwa bidii, weledi na kuwahudumia wananchi kwa ufanisi.

Rais Dkt. Samia pia ameiagiza Ofisi ya Makamu wa Rais kuimarisha usimamizi wa masuala ya Muungano na kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinatatuliwa kwa ushirikiano ili kuendelea kuulinda na kuuimarisha Muungano. Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha usimamizi wa mazingira kwa kushirikiana katika utekelezaji wa programu za uhifadhi na kukabiliana na changamoto zinazotishia mazingira na ustawi wa Taifa.

Katika kuimarisha utendaji wa Serikali, Rais ameitaka Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kuweka mazingira bora yatakayowawezesha watumishi wa umma kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi. Kwa upande wa sekta ya uchukuzi, ameelekeza kuongeza kasi ya ujenzi na usimamizi wa miradi ya reli, barabara, bandari na meli, sambamba na kutathmini fursa za kupanua biashara ya anga ya Shirika la Ndege la Tanzania.

Vilevile, Rais Dkt. Samia ameitaka Wizara ya Katiba na Sheria kuendelea kuimarisha upatikanaji wa haki nchini kwa kuongeza kasi ya utekelezaji wa kampeni za msaada wa kisheria ili huduma hizo ziwafikie wananchi wengi zaidi na kuwawezesha kupata haki zao kwa wakati. Aidha, ameitaka Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) kuimarisha ukuzaji wa biashara pamoja na usimamizi wa maonesho ya biashara nchini.

Kwa upande wa uhifadhi wa maliasili, Rais ameliagiza Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kuimarisha usimamizi na ulinzi wa hifadhi za wanyamapori na rasilimali za utalii, akisisitiza kuwa taasisi hiyo ina nafasi muhimu katika kulinda na kukuza sekta ya utalii nchini. Pia amelitaka Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kuendelea kuimarisha nafasi yake kama chombo cha Serikali na sauti ya Taifa kwa kuboresha maudhui, kuongeza ufanisi wa utendaji na kuendeleza weledi wa watumishi wake.

Walioapishwa ni Dkt. Latifa Mohammed Khamis, aliyeteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia masuala ya Muungano, na Bi. Prisca Burton Lwangili, aliyeteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Viongozi wengine walioapa Kiapo cha Uadilifu kwa Viongozi wa Umma ni Bw. Ephraim Balozi Mafuru, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE); Bw. Salum Nassor Mnuna, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA); Bw. Massana Gibril Mwishawa, Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA); na Bi. Asha Dachi Mbaruk, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).









Posted by MROKI On Monday, July 27, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo