Nafasi Ya Matangazo

July 25, 2026

SONGWE
Wananchi wa Kata ya Mkwajuni, Wilaya na Mkoa wa Songwe, wametakiwa kufuata sheria za usalama barabarani, ili kupunguza ajali za barabarani katika eneo  hilo.

Akizungumza na wananchi Julai 25, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mheshimiwa Jabiri Makame alisema wakati wa ziara yake katika kampeni ya Serikali Nyumbani Kwako iliyofanyika katika kata hiyo. amepita katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo na kujionea namna wananchi wanavyothamini kazi nzuri inayofanywa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe, huku akisisitiza kuwa ni wajibu wa kila mtumiaji wa barabara kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani ili kulinda maisha na mali za wananchi.

Aidha Mh. Makame aliwataka askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani kuendelea kusimamia sheria kwa weledi, uadilifu na bila upendeleo, huku wakichukua hatua za kisheria dhidi ya wote watakaobainika kukiuka sheria na kanuni za usalama barabarani.

Pia Mh Makame alisema kuna mambo matatu ya msingi yatakayosaidia kupunguza ajali za barabarani ambazo ni kuzingatia alama za usalama barabarani, kuendelea kutoa elimu kwa madereva wa bodaboda na watumiaji wengine wa barabara kuzingatia matumizi salama ya  barabara, pamoja na kuchukua hatua za kisheria dhidi ya wote wanaokiuka sheria na taratibu za usalama barabarani.

Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Augustino Senga, aliwataka wasafirishaji wote kuzingatia sheria za usalama barabarani kwa kuvaa kofia ngumu (helmet) wakati wote, kuepuka kubeba mizigo au abiria kinyume cha sheria, pamoja na kuendesha kwa mwendo unaoruhusiwa, hususan katika maeneo ya makazi, akibainisha kuwa kufanya hivyo kunalinda maisha yao, familia na jamii kwa ujumla.

Akihitimisha, Kamanda Senga aliwataka madereva wote kuachana na tabia ya kuendesha vyombo vya moto wakiwa wametumia pombe au vilevi vya aina yoyote, akieleza kuwa vitendo hivyo ni hatari kwa maisha ya dereva na watumiaji wengine wa barabara, huku akisisitiza kuwa kila mmoja anapaswa kuchukua tahadhari ili kulinda usalama wake na wa vizazi vijavyo.










Posted by MROKI On Saturday, July 25, 2026 No comments





RUKWA
Wananchi, Wafugaji pamoja na Wafanyabiashara wa Mifugo katika mnada wa mifugo uliopo katika Kijiji cha Kisumba, Kata ya Matanga, Wilaya ya Sumbawanga mjini Mkoani Rukwa wametakiwa kuacha vitendo vya kujichukulia sheria mkononi wakiaswa kuwa hiyo sio njia ya kumaliza migogoro baina yao.

Hayo yameelezwa leo Julai 25, 2026 na Kamanda wa Polisi Kikosi cha Kuzuia Wizi wa Mifugo Nchini (STPU) Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Simon Pasua ambapo amewataka Wananchi hao kuripoti matukio ya uhalifu katika vituo vya Polisi kuanzia ngazi ya Kata na sio kujichukulia sheria mkononi, kwani kwa kufanya hivyo kunachangia kuongezeka kwa matukio hayo.

Aidha Kamanda Pasua amewataka Wananchi hao kuonyesha ushirikiano katika vyombo vya sheria ili kufanikisha kesi za uhalifu, huku akiwaagiza wenyeviti wa Vijiji kuwapa Wafugaji, barua za utambulsho wa uhalali wa umiliki mifugo pindi wapelekapo mifugo yao katika minada.

Naye Mkaguzi Kata wa Kata hiyo (INSP) Fatuma Mkumbo amesema Jeshi la Polisi katika Kata hiyo litaendelea kuimarisha ulinzi katika minada yote ya Mifugo, huku akitoa rai kwa Wafugaji kuacha kuwatumia watoto katika shughuli za uchungaji mifugo.
Posted by MROKI On Saturday, July 25, 2026 No comments

Mkuu wa Kikosi cha usalama barabarani Mkoa wa Mbeya Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Notker Kilewa ameitaka jamii kuwakumbuka watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu.

Hayo amezungumza Julai 25, 2026 alipowaongoza Maafisa, Wakaguzi na Askari wa Kikosi cha usalama barabarani Mkoani humo kutembelea na kutoa msaada wa vitu mbalimbali kwa watoto wanaolelewa katika kituo cha Nuru Orphans Center kilichopo Uyole Jijini Mbeya.

Aidha SSP Kilewa alisema kuwa, Jeshi la Polisi kama sehemu ya jamii limekuwa likifanya kazi zake kwa kushirikiana na jamii ili kuzuia uhalifu na ajali za barabarani, limetembelea kituo hicho na kutoa vitu mbalimbali kama sehemu ya kurejesha kwa jamii na kama sehemu ya kuguswa na watoto yatima.

"Nalaani vitendo vya baadhi ya wazazi kutupa na kutelekeza watoto na kusababisha wengine kupoteza maisha, wengine kuishi katika mazingira magumu na hata kukosa mahitaji muhimu, haki zao za msingi, nitoe wito kwa jamii kutembelea kituo hiki na kutoa msaada wa mahitaji kwa watoto" alisema SSP Kilewa.

Naye, Meneja wa Kituo hicho Bi. Mary Emily amesema kuwa kituo hicho kilianza mwaka 2006 na kinapokea watoto kuanzia umri wa mwaka 0 na kuendelea, kituo kinapata watoto kutoka Ustawi wa Jamii na hadi sasa kituo kina jumla ya watoto 39.

Vilevile, Bi. Mary amelishukuru Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kwa kuwafikiria na kutoa msaada wa vitu mbalimbali ambavyo vimegusa mahitaji yao. Pia Bi. Mary ametoa wito kwa jamii kuendelea kuwakumbuka watoto wanaoishi katika mazingira magumu na yatima.

Kwa upande wake, mmoja wa watoto wanaolelewa katika kituo hicho tangu mwaka 2006 Melania Nuru amelishukuru Jeshi la Polisi kwa msaada na ameiomba jamii kuwasaidia watoto wenye mahitaji. Kwa sasa amemaliza kidato cha nne na anatarajia kuendelea na masomo ya elimu ya juu, hivyo anaiomba jamii kumsaidia mahitaji yatakayomsaidia kukidhi masomo yake.










Posted by MROKI On Saturday, July 25, 2026 No comments






Bukombe, Geita
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, ameendelea na ziara yake ya kukagua na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo mkoani Geita kwa kutembelea miradi mbalimbali katika Wilaya ya Bukombe, huku akisisitiza umuhimu wa kukamilika kwa miradi hiyo kwa wakati ili wananchi waanze kunufaika na huduma zinazotarajiwa.

Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara, Waziri Mavunde amesema serikali chini ya uongozi wa  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Dkt. Samia Suluhu Hassan  imedhamiria kuleta miradi mingi ya maendeleo ili kupeleka huduma za msingi kwa wananchi.


Awali, Waziri Mavunde alikagua mradi wa maji katika Kijiji cha Businda, Kata ya Bulangwa, wenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 963.7. Mradi huo unatarajiwa kuhudumia zaidi ya wananchi 9,949 na kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama katika eneo hilo.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mavunde ametembelea na kukagua ujenzi wa soko na standi kuu ya kisasa ya mabasi katika Kata ya Katente, Ushirombo, mradi wenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 22 na kumpongeza Mbunge wa Bukombe Mh. Dkt. Doto M. Biteko kwa kusaidia upatikanaji wa miradi hii ya kimkakati kupitia serikali kuu na pia kutoa rai kwa mkandarasi kuongeza kasi ya utekelezaji ili mradi ukamilike kwa wakati na kuwawezesha wananchi, hususan waliopisha ujenzi wa mradi huo, kurejea katika shughuli zao za kiuchumi.

Wachimbaji wadogo wa Bukombe wamemshukuru Rais Mh. Dkt. Samia S. Hassan kwa kuweka mazingira rafiki ya uchimbaji na kuruhusu ufutwaji wa Leseni kubwa za madini na kupewa wachimbaji wadogo.


Aidha Waziri Mavunde ametoa katazo kwa  wachimbaji wadogo kuvamia maeneo yenye leseni za utafiti na kuagiza kufuatwa kwa sheria na taratibu zilizowekwa ili kuepusha migogoro na ugumu wa usimamizi wa leseni za madini,kwa kuwa serikali sasa inaweka mpango mzuri wa ugawaji wa Leseni kwa wananchi wake.

Waziri Mavunde amekagua ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami nyepesi yenye urefu wa kilomita 1.2 kutoka Uyovu hadi Namonge katika Kata ya Runzewe, mradi unaogharimu zaidi ya Shilingi milioni 917.6. Amesema kukamilika kwa barabara hiyo kutachochea biashara, kuboresha usafiri na kuongeza usalama wa wananchi wakati wa mchana na usiku.

Katika eneo la machimbo ya Msasa, Waziri Mavunde pia amekagua ujenzi wa kituo cha polisi na zahanati vinavyojengwa kwa ufadhili wa wachimbaji wadogo kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR). Amepongeza wachimbaji hao kwa kurejesha sehemu ya faida wanazopata kwa kuwekeza katika huduma muhimu za kijamii.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martin Shigella, amesema miradi inayotekelezwa katika Wilaya ya Bukombe ni mkombozi kwa wananchi na itachochea ukuaji wa uchumi wa eneo hilo.

Shigella pia amemuomba Waziri Mavunde kumfikishia Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan salamu za shukrani kutoka kwa wananchi wa Bukombe kwa kutoa fedha za ujenzi wa soko la kisasa la Ushirombo.

Amesema kukamilika kwa soko hilo kutatoa mazingira bora ya biashara, kuongeza mapato ya wananchi na Halmashauri, pamoja na kuhudumia wakazi wa Ushirombo na maeneo jirani.
Posted by MROKI On Saturday, July 25, 2026 No comments




Abidjan, Côte d’Ivoire
Nchi za Afrika zimekubaliana kuweka kipaumbele katika ufadhili wa viwanda vinavyotegemea rasilimali za ndani, hususan madini, pamoja na kuharakisha uongezaji thamani wa bidhaa na kuimarisha biashara ya ndani ya bara ili kujenga uchumi jumuishi, endelevu na wenye ushindani.

Makubaliano hayo yamefikiwa katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini uliofanyika jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.

Akizungumza baada ya kuhitimishwa kwa mkutano huo, Naibu Waziri wa Fedha, Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), alisema nchi wanachama zimekubaliana kuongeza uwekezaji katika viwanda vinavyoongeza thamani ya rasilimali za Afrika, kuimarisha biashara ya kikanda na kupunguza utegemezi wa misaada na ufadhili kutoka nje ya bara na kusisitiza Afrika inapaswa kutumia ipasavyo utajiri wake wa rasilimali pamoja na nguvu kazi ya vijana kwa kuwekeza katika elimu, ujuzi na teknolojia za kisasa ili kuchochea maendeleo ya viwanda, huku ikiondoa vikwazo vya biashara na kuimarisha utekelezaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).

*Kiruswa: Afrika iongeze thamani ya madini yake*

Akichangia mjadala katika mkutano huo, Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, alisisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kushirikiana katika kutekeleza mikakati ya uongezaji thamani wa madini ndani ya bara badala ya kuendelea kuuza malighafi.

Alisema Afrika imejaaliwa kuwa na utajiri mkubwa wa madini, yakiwemo madini mkakati (Strategic Minerals) na madini muhimu (Critical Minerals) yanayohitajika duniani kwa ajili ya maendeleo ya teknolojia za kisasa, uzalishaji wa nishati safi na maendeleo ya viwanda.

“Ni wakati wa Afrika kunufaika kikamilifu na rasilimali zake kwa kuwekeza katika uchakataji na uongezaji thamani wa madini ndani ya bara. Ushirikiano wa nchi zetu utasaidia kuongeza ajira, mapato, uhamishaji wa teknolojia na kuifanya Afrika kuwa kitovu cha maendeleo ya viwanda vinavyotokana na madini,” alisema Dkt. Kiruswa.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, alisema ili kuharakisha mageuzi ya kiuchumi Afrika ni muhimu kuimarisha ujumuishaji wa kifedha, kuboresha miundombinu ya kimkakati na kuondoa vikwazo vya biashara ili kuongeza ushindani wa bidhaa za Afrika katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Mkutano huo wa siku mbili uliokuwa na kaulimbiu “Financing Africa’s Industrialization for Sustainable Development” ulilenga kuweka mikakati ya kuharakisha maendeleo ya viwanda vinavyotegemea rasilimali za Afrika, hususan madini, na kuimarisha biashara na ushirikiano wa kiuchumi miongoni mwa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika.
Posted by MROKI On Saturday, July 25, 2026 No comments





Dodoma
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, amekutana na Wabunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) kutoka Tanzania Makao Makuu ya CCM, Dodoma, na kuwapongeza kwa dhamana ya kuiwakilisha nchi katika chombo hicho cha kikanda.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika leo Julai 24,2026, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro,amewahimiza kuendelea kutanguliza maslahi ya Taifa na Jumuiya kwa kudumisha mshikamano, kujenga ushirikiano na wabunge kutoka nchi wanachama katika kuimarisha mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao Tanzania inajivunia kuwa moja wa waasisi wake. 

Katibu Mkuu amesisitiza kuwa Chama kina matarajio makubwa kwao na kitaendelea kuwapa ushirikiano wanapotekeleza wajibu wao wa kitaifa na kikanda.
Posted by MROKI On Saturday, July 25, 2026 No comments

July 24, 2026








Na. Mwandishi wetu - Dar es Salaam
Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu na Kusimamia Fedha za Mfuko wa Dunia nchini Tanzania (Tanzania National Coordinating Mechanism – TNCM), imeidhinisha rasmi Ombi la Tanzania la Ufadhili wa Mzunguko wa Nane wa Mfuko wa Dunia (Global Fund Grant Cycle 8 – GC8) kiasi cha dola za Marekani milioni 538.6 kwa ajili ya kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI, Kifua Kikuu (TB) na Malaria, pamoja na kuimarisha Mifumo Thabiti na Endelevu ya Afya (RSSH), katika kipindi cha utekelezaji kuanzia Januari 2027 hadi Desemba 2029.

Uidhinishaji huo umefanyika jijini Dar es Salaam katika kikao maalum cha TNCM kilichoongozwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa TNCM.

Dkt. Yonazi amesema kuwa, mchakato wa maandalizi ya Ombi la GC8 ulianza rasmi tarehe 13 Machi, 2026 na umeendelea kwa zaidi ya miezi minne, ukihusisha mashauriano ya kina, majadiliano ya kitaifa, upangaji wa vipaumbele, uandishi wa andiko, mapitio ya kitaalamu na uhakiki wa nyaraka za maombi. 

Aidha, alifafanua kuwa, mchakato huu umejengwa katika msingi wa ushirikishwaji mpana wa wadau, uwazi, uwajibikaji na umiliki wa kitaifa ambapo zaidi ya wadau 270 walishiriki kwa uwakilishi wa makundi mbalimbali, yakiwemo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara, Idara na Taasisi zake; Washirika wa Maendeleo, Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mashirika ya Kimataifa, Asasi za Kiraia, Sekta Binafsi, Mashirika ya Dini, watu wanaoishi na VVU, jamii zilizo katika hatari kubwa ya maambukizi na zilizoathiriwa na magonjwa hayo; pamoja na wataalamu wa sekta ya afya.

Dkt. Yonazi ameeleza kuwa uwekezaji wa Mfuko wa Dunia umeendelea kutoa mchango mkubwa katika juhudi za Serikali za kuboresha afya na ustawi wa Watanzania, na kusema utekelezaji wa GC8 utatoa fursa kwa Nchi kuendela kuzuia maambukizi mapya ya VVU, kuongeza upatikanaji wa dawa za kufubaza makali ya VVU (ARV), kuimarisha kinga, uchunguzi na matibabu ya Malaria, pamoja na kuboresha ugunduzi wa mapema na matibabu ya Kifua Kikuu.

“Kuidhinishwa kwa Ombi hili la Ufadhili ni matokeo ya kazi kubwa na ushirikiano wa wadau wetu ambao wamewekeza muda, utaalamu na rasilimali kuhakikisha kuwa vipaumbele vilivyoainishwa vinazingatia mahitaji ya nchi pamoja na sauti za jamii na makundi yanayoathiriwa na magonjwa hayo”.Alisema Dkt. Yonazi.

Aliongezea kuwa,hatua hiyo ni mafanikio muhimu yanayoonesha dhamira ya Tanzania ya kuendeleza mapambano dhidi ya magonjwa hayo matatu, sambamba na kujenga mfumo wa afya ulio imara, jumuishi na endelevu.

Dkt. Yonazi ameshukuru Sekretarieti ya Mfuko wa Dunia iliyopo Geneva (Global Fund Country Team), wajumbe wa TNCM pamoja na wadau wote walioshiriki katika maandalizi na ukamilishaji wa maombi hayo, amepongeza jitihada zao akisema zimekuwa na mchango muhimu kuwezesha kufikia hatua hii.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TNCM, Bw. Kent Pius, ametoa shukrani maalum kwa Mwenyekiti wa TNCM, Mfuko wa Dunia, wajumbe na wadau wote kwa ushirikiano na uwajibikaji mkubwa katika kuhakikisha kuwa zoezi hili limefanyika kwa ufanisi na ubora uliokusudiwa na kusema kuwa, hatua hii ni matokeo ya dhamira ya dhati na juhudi za pamoja. 

“TNCM itaendelea kuratibu ushirikiano kati ya Serikali, jamii, Asasi za Kiraia, Washirika wa Maendeleo, Sekta Binafsi na wadau wa kimataifa katika kuhakikisha uwekezaji wa Mfuko wa Dunia unachangia katika kufikia malengo ya Kitaifa na Kimataifa ya kutokomeza UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria kama vitisho vya afya ya jamii,” alisema Kent.
Posted by MROKI On Friday, July 24, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo