Nafasi Ya Matangazo

August 05, 2026









Na Neema Chalila Mbuja, Dodoma
WAGENI mbalimbali wameendelea kumiminika kwenye Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii kwenye Maonesho ya Maadhimisho ya Siku ya Wakulima Duniani (NANE NANE), kujionea shughuli mbalimbali za uhifadhi na wanyamapori zinazofanywa na Wizara.

Miongoni mwa wageni waliotembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii ni pamoja na Wakuu wa Wilaya na Makatibu Tawala mbalimbali ambapo waliipongeza Wizara kwa ushiriki wa Maonesho hayo ya NANE NANE kwani wamekuwa wakichagiza uwepo wa wananchi wengi wanaokuja kufanya utalii wa ndani wa kuona wanyamapori.

Makatibu Tawala hao ni pamoja na Katibu Tawala wa Wilaya ya Kongwa Sozi Ngate, Katibu Tawala wa Wilaya ya Dodoma Mjini Sakina Mbugi, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kondoa Christina Kalekezi na Wakuu  wa Wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri na Mpwapwa Dkt. Sophia Kizigo.

Viongozi hao wamesema kila mwaka Wizara ya Maliasili na Utalii imekuwa ikipokea wageni wengi hususani wananchi na wanafunzi wanaotembelea banda lake kujifunza elimu kuhusu uhifadhi, wanyamapori, malikale, misitu na nyuki.

Katika hatua nyingine Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii Imepokea wananfunzi zaidi ya elfu moja waliofika kwa ajili ya kupata wa elimu na kuona wanyamapori hai ambapo wengi wao wamevutiwa na mnyama  Ngiri maarufu kama Kasongoyeye ambaye  ana umaarufu mkubwa kutokana na tabia yake na kutokuwa na woga.
Posted by MROKI On Wednesday, August 05, 2026 No comments






Na Neema Chalila Mbuja, Dodoma
BALOZI wa Tanzania nchini Italia na Mwakilishi Mkazi  wa Shirika la Chakula na Kilimo la  Umoja wa Mataifa (FAO), Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) na Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa (WFP),  Mhe. Mbarouk  Nassoro Mbarouk leo Agosti 04, 2026,  ametembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii  na kusema kuwa nchi ya Italia ina nafasi kubwa ya kuleta watalii wengi nchini.

Mhe. Balozi Mbarouk amesema Tanzania inafanya vizuri kwenye kutangaza utalii na vivutio vyake  na kuipongeza Wizara kwa kazi nzuri inayoifanya.

Katika hatua nyingine Wizara ya Maliasili na Utalii  imepokea ugeni wa Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Rajab Mruma ambaye ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kubuni mbinu za kutafuta utatuzi wa  changamoto za wanyamapori hai kuingia kwenye makazi ya wananchi kwa kujenga  uzio ili kuzuia uharibifu unaoweza kutokea.

Aidha, Mhe Jaji Mruma ametembelea bustani ya wanyamapori  hai iliyoko kwenye Maonesho ya Nane  Nane yanayoendelea Jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya kutangaza utalii wa ndani kwa wananchi.
Posted by MROKI On Wednesday, August 05, 2026 No comments

August 04, 2026






Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe kupitia programu ya Polisi Jamii limeendelea kuonesha mshikamano na jamii baada ya kuwatembelea wakina mama waliojifungua, watoto na wagonjwa mbalimbali katika kituo cha afya cha Tnduma kilichopo Wilaya ya Momba, ambapo walikabidhi mahitaji mbalimbali na kuwasaidia kulipia gharama ndogo za matibabu. Hatua hiyo imelenga kuimarisha mahusiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi pamoja na kuhamasisha ushirikiano katika kudumisha amani, usalama na malezi bora ya watoto.

Akiongoza ziara hiyo Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Songwe, Kamishna Msaidizi wa Polisi Maria Kway, tarehe 04 Agosti 2026, alisema kuwa malezi bora ndiyo msingi wa kujenga taifa lenye maadili na usalama, hivyo aliwataka wakina mama kuhakikisha watoto wanapata haki zao za msingi, uangalizi unaostahili na kulindwa dhidi ya aina zote za ukatili, ikiwemo unyanyasaji wa kimwili, kisaikolojia na kijinsia. 

Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuzuia uhalifu na kulinda ustawi wa jamii.

Mwisho wananchi wamehimizwa kutumia elimu hiyo kwa kuwalea watoto katika mazingira salama, kuripoti matukio ya ukatili na uhalifu kwa wakati kwenye vyombo vya dola, pamoja na kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kudumisha amani, usalama na maendeleo ya jamii kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Posted by MROKI On Tuesday, August 04, 2026 No comments







DODOMA
Vijana nchini wamehimizwa kutumia nguvu kazi, maarifa na ubunifu wao kuchangamkia fursa zinazotolewa na Sekta ya Madini badala ya kusubiri misaada au mitaji kutoka serikalini, huku wakitakiwa kuanza na rasilimali walizonazo ili kujenga mafanikio ya kiuchumi.

Wito huo umetolewa  kwenye Maonesho ya Nane Nane yanayoendelea Kitaifa jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Xinda Energy Resources Technology Import and Export Trade Co. Ltd, Abia Mafie, aliyesema Serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa vijana kupitia mafunzo, warsha na programu mbalimbali za uwezeshaji, lakini baadhi yao hushindwa kutumia maarifa hayo kwa vitendo.

“Vijana tusisubiri Serikali itupatie kila kitu. Unaweza kuanza na kidogo ulichonacho na ukakua hatua kwa hatua. Watu wengi waliofanikiwa walianza hivyo,” amesema Mafie.

Amesema Sekta ya Madini ni miongoni mwa maeneo yenye fursa kubwa za ajira, ujasiriamali na uwekezaji, hususan katika uchakataji na uongezaji thamani wa madini, hatua inayochochea ukuaji wa uchumi wa viwanda na kuongeza mapato ya taifa.

Mafie amesema kampuni yake imewekeza katika uchakataji wa shaba na kuzalisha copper cathode yenye kiwango cha ubora cha asilimia 99.99 kinachokidhi viwango vya soko la kimataifa, hatua inayounga mkono juhudi za Serikali za kuongeza thamani ya rasilimali za madini nchini.

Ameeleza kuwa Xinda Precious Metal Resources Co. Ltd ilianza kujenga kiwanda chake mwaka 2024 na kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha tani 50 za copper cathode kwa mwezi, huku bidhaa zake zikipata soko kutokana na ubora wake.

Kwa mujibu wa Mafie, kampuni hiyo inapanga kujenga viwanda vingine viwili vya uchakataji mkoani Dodoma ili kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za usafirishaji wa malighafi na kuongeza mchango wa Sekta ya Madini katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Amesema uwekezaji huo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, huku ukionesha nafasi muhimu ya sekta binafsi na ushiriki wa Watanzania katika kuongeza thamani ya madini na kuimarisha uchumi unaotegemea viwanda.
Posted by MROKI On Tuesday, August 04, 2026 No comments







Na.WMA-DODOMA
WANANCHI  wametakiwa kuhakikisha wanapima mitungi ya gesi kabla ya kuinunua ili kujiridhisha kuwa wanapata kipimo cha gesi kinacholingana na fedha wanazolipa, huku wafanyabiashara wote wa gesi wakikumbushwa kutimiza matakwa ya kisheria ya kuwa na mizani iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo (WMA).

Rai hiyo imetolewa na Meneja wa Wakala wa Vipimo (WMA) Mkoa wa Singida, Willie Amosi, wakati wa Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma ambapo amesema matumizi ya gesi ya kupikia yameongezeka kwa kasi kufuatia jitihada za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi.

Amesema jukumu la Wakala wa Vipimo ni kuhakikisha kila mtungi wa gesi unaouzwa kwa wananchi unakuwa na kipimo sahihi cha gesi kama kilivyoainishwa na mzalishaji, ili kumlinda mlaji dhidi ya hasara inayoweza kusababishwa na vipimo visivyo sahihi.

"Wananchi wana haki ya kujiridhisha kuwa gesi wanayonunua ina uzito sahihi. Ndiyo maana sheria inamtaka muuzaji wa mwisho kuwa na mizani iliyohakikiwa na WMA ili kila mnunuzi aweze kupima mtungi wake kabla ya kuuchukua," amesema Amosi.

Ameeleza kuwa kila mtungi wa gesi hubeba taarifa zinazoonyesha uzito wa mtungi wenyewe pamoja na kipimo cha gesi kilichomo ndani, hivyo mnunuzi anapaswa kulinganisha taarifa hizo kwa kupima mtungi kwenye mizani iliyothibitishwa.

Amosi amesema WMA inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwa wazalishaji, wafungashaji na wauzaji wa gesi nchini ili kuhakikisha vipimo sahihi vinazingatiwa, huku akibainisha kuwa malalamiko kuhusu upungufu wa gesi katika mitungi ya matumizi ya majumbani yamepungua kwa kiasi kikubwa kutokana na kuimarika kwa usimamizi.

Hata hivyo, amewataka wananchi kutoridhika na kupokea mitungi bila kupimwa, akisema ushiriki wao katika kuhakiki uzito wa gesi ni njia muhimu ya kulinda haki zao kama walaji na kuchangia uwajibikaji kwa wafanyabiashara.

Aidha, amewatahadharisha wauzaji wa gesi ambao hawana mizani inayotakiwa kisheria kuhakikisha wanaipata haraka, akisisitiza kuwa ukaguzi wa WMA unaendelea nchini kote na hatua za kisheria zitachukuliwa kwa watakaobainika kukiuka sheria.

Ametoa wito kwa wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nane Nane kutembelea banda la Wakala wa Vipimo ili kupata elimu kuhusu haki zao katika ununuzi wa gesi na bidhaa nyingine zinazouzwa kwa kutumia vipimo, akisisitiza kuwa usahihi wa vipimo ni msingi wa biashara ya haki na ulinzi wa maslahi ya mlaji.
Posted by MROKI On Tuesday, August 04, 2026 No comments







Na Mwandishi Wetu, Dodoma
DODOMA — Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeonesha namna sekta ya misitu na nyuki inavyoweza kuwa chanzo kikubwa cha ajira, kipato na ukuaji wa uchumi kupitia mnyororo wa thamani wa mazao yake.

Hayo yamebainika katika Maonesho ya Nane Nane 2026 yanayoendelea Dodoma, baada ya Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa SUMA JKT, Brigedia Jenerali Shija Lupi, kutembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii na kujionea ubunifu unaofanywa na TFS katika kuibua fursa hizo.

Brigedia Jenerali Lupi, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maonesho ya Nane Nane Kitaifa upande wa JKT, alielezwa kuhusu safari ya mazao ya misitu na nyuki kutoka uzalishaji, uchakataji, uongezaji thamani hadi kufikia masoko ya ndani na nje.

Amesema ubunifu huo unaonesha kuwa rasilimali za misitu zinaweza kutumika zaidi ya uhifadhi, bali pia kuwa kichocheo cha maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi.

“Nimeona mnyororo mzima wa thamani unaoonesha namna mazao ya misitu na nyuki yanavyoweza kuongeza ajira, kipato na kuchangia uhifadhi wa mazingira,” amesema.

Katika banda hilo, Brigedia Jenerali Lupi pia alishuhudia huduma ya tiba nyuki (Apitherapy), inayotumia bidhaa za nyuki pamoja na kudungishwa na nyuki chini ya uangalizi wa wataalamu.

Alielezwa kuwa tiba hiyo imekuwa ikitumika kusaidia kupunguza baadhi ya maumivu ya viungo na changamoto nyingine zinazohusishwa na afya, huku wataalamu wakisisitiza matumizi sahihi na salama ya huduma hiyo.
Posted by MROKI On Tuesday, August 04, 2026 No comments



Na WMA   - DODOMA.
Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Bw. Needpeace Wambuya leo Agosti 2, 2026 ametembelea banda la Wakala wa Vipimo (WMA) katika Maonesho ya Wakulima, Mifugo na Uvuvi (Nane Nane)  yanayofanyika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela Nzuguni jijini Dodoma.

Katika ziara hiyo aliyomwakilisha Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, Mkurugenzi Wambuya alipongeza juhudi za WMA za kutoa elimu kwa wakulima, wafugaji na wajasiriamali kuhusu umuhimu wa vipimo sahihi. Hata hivyo aliwataka watumishi kuongeza bidii, juhudi na maarifa katika utoaji wa huduma ili kuhakikisha huduma za uhakiki wa vipimo zinafikia wadau wote wa sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.

 “Kazi yenu ni muhimu katika kulinda haki za wazalishaji na walaji. Niwahimize muendelee na kasi hii kwa kutumia teknolojia ili kila mkulima na mfanyabiashara apate uelewa na kushawishika kutumia vipimo sahihi” alisema.

Pia Mkurugenzi Wambuya alitoa wito kwa Wakala kuharakisha michakato ya utekelezaji wa huduma mpya za kivipimo zilizopangwa na Serikali ili zianze kutoa manufaa kwa wananchi mara moja. 

Alisisitiza kuwa Serikali imeweka nguvu katika kuboresha sekta ya vipimo ili kuongeza tija na ushindani wa bidhaa za Kitanzania sokoni ndani na nje ya nchi.
Posted by MROKI On Tuesday, August 04, 2026 No comments
Na Neema Chalila Mbuja, Dodoma
NAIBU Mkurugenzi Mtendaji wa SUMA JKT  Brigedia Jenerali  Shija Lupi leo Agosti 03, 2026 ametembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii kujionea wadau mbalimbali wanaoshirikiana na wizara kwenye uzalishaji wa bidhaa za misitu na asali na kuipongeza wizara kwa kushirikiana na wadau hao.

Brigedia Jenerali Shija amesema wadau hao wamekuwa wakifanya kazi nzuri katika kuhakikisha mazao hayo ya bidhaa za nyuki ikiwemo asali, miche ya miti na mazao ya misitu yanakuwa na soko ndani na nje ya nchi.

Brigedia Jenerali Shija alipata wasaa wa kutembelea wanyamapori hai waliopo kwenye Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii kama njia mojawapo ya kuutangaza utalii wa ndani.









Posted by MROKI On Tuesday, August 04, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo