Nafasi Ya Matangazo

July 04, 2026






Posted by MROKI On Saturday, July 04, 2026 No comments

July 03, 2026

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.
Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeendelea kutumia Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake, huduma mbalimbali na umuhimu wa ithibati katika kuimarisha taaluma ya uandishi wa habari nchini.

Hatua hiyo imejidhihirisha leo baada ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, kuungana na maafisa wa Bodi katika banda la JAB lililopo Kijiji cha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kutoa elimu kwa wananchi, kujibu maswali mbalimbali na kuzungumza na waandishi wa habari waliotembelea banda hilo.

Akizungumza katika maonesho hayo, Wakili Kipangula alisema JAB imejipanga kuhakikisha wananchi na wadau wa sekta ya habari wanapata uelewa sahihi kuhusu majukumu ya Bodi pamoja na huduma zinazotolewa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari.

Alisema ushiriki wa JAB katika maonesho ya Sabasaba unalenga kusogeza huduma karibu na wananchi, kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa ithibati kwa waandishi wa habari na kuhamasisha uzingatiaji wa maadili, weledi na uwajibikaji katika taaluma ya uandishi wa habari.

Mbali na kutoa elimu, JAB inaendelea kutoa huduma mbalimbali katika banda lake ikiwemo usajili wa waandishi wa habari, utoaji wa vitambulisho vya ithibati kwa waliokidhi vigezo, marekebisho ya taarifa za usajili pamoja na ushauri kuhusu huduma zinazotolewa na Bodi.

JAB imewahimiza waandishi wa habari, wadau wa sekta hiyo na wananchi kwa ujumla kutumia fursa ya Maonesho ya Sabasaba kutembelea banda lake ili kupata huduma, elimu na ufafanuzi kuhusu shughuli zake, huku ikisisitiza kuwa ithibati ni nyenzo muhimu katika kujenga taaluma ya uandishi wa habari yenye weledi, uwajibikaji na kuaminika.

Posted by MROKI On Friday, July 03, 2026 No comments








Na. Mwandishi Wetu - Arusha
Tanzania ipo tayari kwa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) ikiwa mwenyeji kwa kushirikiana na Kenya na Uganda ambapo maandalizi yamefikia hatua nzuri kwa kuzingatia viwango vya Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF) vinavyotakiwa.

Akizungumza hii leo Julai 3, 2026 Jijini Arusha kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Makatibu Wakuu ya Maandalizi ya Michuano hiyo, Dkt. Jim Yonazi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbasi amesema Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha michuano hiyo inafana kwa kuzingatia mipango na mikakati thabiti iliyopo.

Dkt. Abbasi ameiongoza Kamati hiyo iliyotembelea viwanja vitakavyotumika wakati wa michuano hiyo ikiwemo Kiwanja cha Mazoezi cha Mgambo, kiwanja cha mazoezi cha Engutoto, Kiwanja cha mazoezi Magereza, uwanja Mpya wa Arusha pamoja na ukaguzi wa barabara za mjini zinazosimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania-TANROADS pamoja na zinasosimamiwa na Wakala wa Barabara za mjini na vijijni -TARURA zitakazoingia na Kutoka Katika uwanja wa Arusha, kujionea maendeleo ya ukarabati na maboresho mbalimbali kuelekea michuano hiyo.

Aidha amesema kuwa, michuano hiyo itakuwa ya kihistoria kwa kukutanisha na kuvutia mamilioni ya watu barani Afrika na duniani kote, ambapo ni kwa mara ya kwanza mashindano hayo kuandaliwa kwa pamoja na Mataifa matatu ya Afrika Mashariki.

Aliongezea kuwa, Tanzania imejipanga kupokea Maelfu ya mashabiki, wachezaji, na viongozi wa soka wanatarajiwa kukusanyika na kuleta mwamko mkubwa kupitia Mashindano Makubwa ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027).

"Ni wakati wetu sasa, kuipa nchi heshima yake kuelekea Michuano hiyo ya AFCON, kila mmoja akae tayari katika eneo lake na kujua kuwa anajukumu la kuifanikisha michuano hii na kwa viwango vya kimataifa," alisema Dkt. Abbasi.

Pia alisisistiza Wakandarasi kwenye miradi mbalimbali ya kuboresha miundombinu kuongeza kasi ili kumaliza kazi hizo kwa wakati bila kukwamisha maandalizi hayo.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha Dkt. Toba Nguvila amesema kuwa mkoa umeendelea na maandalizi yote muhimu ikiwemo ya ukarabati wa miundombinu itakayotumika, kuhakikisha upatikanaji wa huduma za maji, kuboresha maeneo ya utoaji wa huduma za kiafya ikiwemo hospitali, masuala ya mawasiliano, pamoja na umeme na kuhakikisha vinapatikana kwa ubora na viwango.

“Jiji linaimarisha miundombinu ya barabara, huku kukiwa na ujenzi na ukarabati wa hoteli za kutosha zitakazotoa huduma pamoja na uboreshwaji wa vituo vya afya vya kutolea huduma za afya ikiwemo hospitali ya Mount Meru, JKCI pamoja na NSK ambazo zitatoa huduma za kiafya kwa ubora na viwango,” alisema Dkt. Nguvila.
Posted by MROKI On Friday, July 03, 2026 No comments







DAR ES SALAAM
Madini ya Tanzanite yameendelea kuwa kivutio kikubwa katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), huku mamia ya wananchi wakifurika katika Banda la Tume ya Madini kujionea kwa karibu jiwe hilo la thamani linalopatikana Tanzania pekee duniani pamoja na kupata elimu kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya madini.

Maonesho hayo yenye kaulimbiu ya “Fahari ya Tanzania” yalianza rasmi Juni 28, 2026 na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13 2026, sambamba na maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa maonesho hayo makubwa ya biashara nchini.

Miongoni mwa wananchi waliotembelea banda hilo ni Nuru Maliki, ambaye amesema ameridhishwa na elimu na huduma alizopata pamoja na nafasi ya kujionea madini mbalimbali ambayo awali alikuwa akiyasikia kupitia historia na simulizi pekee.

“Nimepata huduma nzuri sana na fursa ya kujionea madini mbalimbali, hususan Tanzanite na madini mengine yanayopatikana hapa nchini. Kuna baadhi nilikuwa nikiyasikia tu katika historia, lakini leo nimeyaona kwa macho yangu,” amesema.

Kwa upande wake, Eveline Natai amesema maonesho hayo yameongeza uelewa wake kuhusu fursa za uwekezaji katika sekta ya madini na kumhamasisha kuanza kupanga namna ya kushiriki katika shughuli za sekta hiyo.

“Nimefurahishwa kuona madini mbalimbali na kupata taarifa kuhusu fursa za uwekezaji zilizopo. Nitajipanga kuingia katika sekta hii. Serikali iendelee kutoa elimu kwa Watanzania ili watu wengi zaidi wajifunze na kunufaika na fursa zinazotokana na rasilimali za madini,” amesema.

Akitoa elimu kwa wananchi, Mjiolojia kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Abbas Mruma, amesema maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwaelimisha wananchi kuhusu rasilimali za madini, matumizi yake pamoja na fursa mbalimbali za kiuchumi zinazotokana na sekta hiyo.

Naye Mjiolojia Mwandamizi kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mirerani, Seleman Khamis, amesema thamani ya madini ya Tanzanite hupimwa kwa kuzingatia vigezo vinne muhimu ambavyo ni rangi, uzito, ubora na umbo.

Amefafanua kuwa rangi kuu za Tanzanite ni bluu na zambarau, huku akibainisha kuwa madini hayo yanapatikana Tanzania pekee katika eneo la Mirerani, Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, jambo linaloyafanya kuwa miongoni mwa madini ya vito yenye upekee na thamani kubwa zaidi katika soko la kimataifa.

Mvuto mkubwa wa Tanzanite katika maonesho hayo umeendelea kuthibitisha nafasi ya Tanzania kama kitovu cha madini ya vito duniani, huku wananchi wakizidi kuhamasika kufahamu zaidi kuhusu sekta ya madini na fursa zake za uwekezaji na maendeleo ya kiuchumi.

Wakati huohuo, viongozi mbalimbali wametembelea banda la Tume ya Madini, akiwemo Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Dkt. Venance Mwasse.

Viongozi hao wamepongeza kazi kubwa ya utoaji elimu na uhamasishaji kuhusu sekta ya madini inayotekelezwa na Tume ya Madini, wakieleza kuwa imechangia kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu fursa zilizopo katika sekta hiyo na mchango wake kwa maendeleo ya uchumi wa taifa.
Posted by MROKI On Friday, July 03, 2026 No comments

 

Bohari ya Dawa (MSD) imezipingeza Hospitali za tufaa mkoa wa Morogoro, Hospitali ya Rufaa Temeke ya mkoani Dar es Salaam na Halmashauri ya Wilaya ya Mafia kwa kuvuka mwaka wa Fedha wa 2025/,2026 bila kuwa na deni MSD. 

MSD imetuma pongezi hizo kwa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Morogoro, Dkt. Daniel Joseph Nkungu, Mganga Mkuu wa Hospitali ya Temeke, Dkt. Mfaume Kibwana na kwa Mkurugenzi wa Wilaya ya Mafia Ndg. Mussa Kitungi.



Posted by MROKI On Friday, July 03, 2026 No comments





Na Dk. Reubeni Lumbagala
Waasisi wa taifa letu walipambana na wakoloni ili kujinasua kutoka kwenye makucha ya kutawaliwa na kuamuliwa nini cha kufanya ili hali uwezo wa kufanya hivyo tulikuwa nao.

Disemba 09, 1961, tukapata uhuru kamili wa kisiasa lakini tukiwa hoi kiuchumi, hivyo kuwa na wajibu wa kujenga uchumi imara wa kutufanyia tuheshimike kwa wengine.

Wenye wajibu wa kujenga uchumi ni wananchi wenyewe wa nchi husika. Mathalani, kwa Tanzania, ni sisi Watanzania wenyewe ambao tunawajibika kuijenga nchi yetu kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Ni hivi: Hatuna mjomba wala shangazi wa kuja kuijenga Tanzania yetu. Ni sisi Watanzania wenyewe ndiyo wahusika wa kuijenga nchi yetu, kuhakikisha tunatatua changamoto zilizopo na kukuza ustawi wetu kwa maendeleo endelevu.

Kazi kubwa ya kujenga uchumi imara na uboreshaji wa huduma za kijamii, inategemea sana uwepo wa raslimali fedha za kufanikisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo. 

Swali linakuja, tunapata wapi fedha za kutekeleza miradi na mipango ya maendeleo? Majibu yanaweza kuwa mengi, lakini jibu la msingi ni kupitia ukusanyaji wa kodi kutoka kwa wananchi wenyewe.

UMUHIMU WA TRA KATIKA KUFANIKISHA MIPANGO YA MAENDELEO

Julai 1, 1996, serikali ikaanzisha Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambapo hadi kufikia Julai 1, 2026, Mamlaka hiyo imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake. 

Pamoja na majukumu mengi ya TRA, moja kubwa ni kukusanya kodi kutoka kwa wadau kama vile wafanyabiashara, wafanyakazi, wajasiriamali, wawekezaji na wananchi kwa ujumla wenye sifa za kulipa kodi.

Kwa hakika, mageuzi makubwa yaliyofanywa, imeiwezesha TRA kuongeza mapato kutoka shilingi bilioni 531 mwaka wa fedha 1996/1997 hadi trilioni 32 mwaka 2025/2026.

Maono ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ni kuifanya Tanzania kujitegemea kwa asilimia kubwa badala ya kutegemea misaada na mikopo ya wahisani, ambayo wakati mwingine imejaa masharti magumu, kutunyima uhuru wetu na hata kutweza utu wetu.

Aidha, kutokana na maono hayo, mapema mwezi Aprili 2021, Rais Dk. Samia alitoa maelekezo mahsusi kwa TRA kuongeza makusanyo ya kodi lakini kodi hizo zisiwe za dhulma, uonevu, ubabe na mabavu.

Ukweli ni kuwa, Rais alikuwa tayari mapato ya nchi yashuke hata kwa miezi miwili au mitatu, lakini kujengwe misingi imara na rafiki katika ukusanyaji kodi bila kuwaumiza walipakodi na wananchi ambao ndiyo nyenzo ya ujenzi wa taifa.

Leo, TRA inapoadhimisha miaka 30 na taifa letu linaloelekea maadhimisho ya miaka 65 ya uhuru wake, tuna kila sababu ya kusema "Tumeupiga mwingi katika makusanyo ya kodi, lakini tusibweteke, tuna kazi kubwa ya kujenga taifa linalojitegemea".

Nasema haya kwa sababu, bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027, asilimia 74.2 ni mapato ya ndani. Ni matunda ya Watanzania kusema tunaweza tutajenga nchi kwa nguvu zetu, kama kusaidiwa basi tusaidiwe katikati ya safari ya ujenzi wa Taifa letu, tena tusaidiwe kwa heshima kwa kuzingatia Tanzania imeimarisha sana diplomasia hasa ya kiuchumi na mataifa mengi ulimwenguni.

Hivyo, niwapongeze walipakodi na wananchi ambao wameipa heshima nchi yetu kwa kuongeza makusanyo ya kodi kwa mafanikio makubwa. Mwelekeo wa kujitegemea kibajeti utafanikiwa zaidi ya tulivyo sasa endapo kila mwenye sifa ya kulipa kodi atatimiza wajibu wake wa kulipa kodi tena kwa hiari.

Julai 01, 2026, Rais Dk. Samia alihudhuria hafla ya Tuzo za Rais kwa Walipakodi katika Ukumbi wa Mlimani City, Jijini Dar es Salaam. Katika hafla hiyo, Rais alikemea "Kodi ya dhulma na dhulma ya kodi".

Alifafanua kuwa, kodi ya dhulma ni kumlipisha mlipakodi zaidi ya kiwango kinachopaswa kulipwa na dhulma ya kodi ni kulipa kiwango cha chini cha kile kinachopaswa kulipwa.

Kimsingi, msisitizo wa Rais ni kuwa, kila anayepaswa kulipa kodi alipe kiwango kinachopaswa kulipwa ili kujenga uchumi imara, shindani na jumuishi kwa maendeleo endelevu ya kizazi cha sasa na kijacho.

Maoni: 0620 800 462.
Posted by MROKI On Friday, July 03, 2026 No comments

July 02, 2026



Na. Mwandishi Wetu – Dar es Salaam
Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Makatibu Wakuu ya Maandalizi ya Michuano ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027),  Dkt. Jim Yonazi, amesema michuano ya AFCON ni fursa adhimu ya kuitangaza Tanzania Kimataifa kupitia sekta mbalimbali ikiwemo ya utalii na uwekezaji hivyo ni jukumu la kila sekta kuhakikisha inachangamkia na kushiriki kikamilifu katika kufanikisha michuano hiyo.

Ameyasema hayo hii leo 01 Julai 2026 wakati wa ziara ya Kamati hiyo inayojumuisha Makatibu Wakuu wa kisekta na baadhi ya wakuu wa Taasisi walipotembelea na kukagua maendeleo ya maandalizi kuelekea michuano hiyo ikiwemo kuangalia miundombinu na vituo vya michezo vitakavyotumika katika michuano ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027) ili kufanikisha mashindano hayo makubwa ya soka barani Afrika.

Katika ziara hiyo, Kamati imekagua maendeleo ya maboresho katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Uwanja wa Mazoezi wa Shule ya Sheria (Law School Grounds), Uwanja wa Mazoezi wa Leaders Club, Uwanja wa Mazoezi wa Gymkhana (Gymkhana Club), Uwanja wa Mazoezi wa Farasi pamoja na Uwanja wa Taifa wa Benjamin Mkapa ili kujionea utayari wa miundombinu itakayotumika wakati wa mashindano hayo.

Dkt. Yonazi amesema ili kufanikisha AFCON 2027 kila sekta inapaswa kuweka nguvu ya pamoja katika kuelekea kwenye michuano hiyo kwa kuzingatia faida zake ikiwemo ya kukuza uchumi wa jamii na Nchi kwa ujumla  

"AFCON 2027 ni zaidi ya mashindano ya soka; ni jukwaa la kuitangaza Tanzania Duniani hivyo kila taasisi inapaswa kutekeleza wajibu wake ili kuhakikisha nchi inanufaika ipasavyo na fursa hii," amesema Dkt. Yonazi.

Aidha, ameielekeza Bodi ya Utaliii Tanzania (TTB) kuandaa mkakati mahsusi wa kuitangaza Tanzania kupitia mashindano hayo kwa kuonesha vivutio vya utalii, utamaduni na fursa za uwekezaji kwa wageni watakaofika nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Maendeelo ya Michezo kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Boniface Tamba, amesema maboresho ya miundombinu yanaendelea vizuri na kwamba ujenzi wa barabara zinazoingia na kutoka katika vituo pamoja na viwanja vya michezo umefikia hatua za mwisho za ukamilishaji.

"Maandalizi yanaendelea kwa kasi na miundombinu muhimu ipo katika hatua za mwisho ili kuhakikisha Tanzania inakuwa tayari kuandaa AFCON 2027 kwa viwango vinavyotakiwa," amesema Bw. Tamba.

Kamati ya Makatibu Wakuu inaendelea na ziara ya ukaguzi wa miundombinu ya AFCON 2027, ambapo baada ya kukamilisha ukaguzi katika Mkoa wa Dar es Salaam itatembelea Zanzibar kabla ya kuhitimisha ziara hiyo itatembelea katika viwanja vilivyopo  Jijini Arusha.





Posted by MROKI On Thursday, July 02, 2026 No comments
Na Dk. Reubeni Lumbagala 
Mwelekeo wa serikali ni kuhakikisha nchi yetu inapiga hatua kubwa za kimaendeleo kupitia sekta mbalimbali za kiuchumi ikiwemo sekta ya viwanda.

Viwanda ni miongoni mwa nyenzo muhimu kufikia matarajio ya serikali ya kukuza uchumi na maendeleo ya nchi. Viwanda vina mnyororo mkubwa wa thamani ambapo mafanikio yake yanawezesha ukuaji wa sekta nyingine muhimu za kijamii na kiuchumi ili kukuza maendeleo.

Mipango ya serikali ni kuhakikisha kila wilaya inakuwa na kongani za viwanda ili kuhakikisha ukuaji uchumi unakuwa jumuishi katika maeneo yote ya nchi.

Katika wilaya ya Pangani mkoani Tanga, upo mradi wa mashamba makubwa ya miwa pamoja na ujenzi wa kiwanda kikubwa cha sukari. 
Mradi huo ni mpango wa serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan wa kukuza uchumi na kuchochea ukuaji wa maendeleo.

Februari 26, 2025, akiwa katika ziara ya kikazi wilayani Pangani, Rais Dk. Samia alieleza dhamira ya serikali ya kuanzisha kilimo cha mashamba makubwa ya miwa na kujenga kiwanda cha sukari ili kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, ajira na kuurejesha mkoa wa Tanga katika sifa yake ya kuwa na maendeleo ya viwanda.

Aidha, mradi huo unasimamiwa na Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) ambapo katika mwezi Juni, 2026, zoezi la ulipaji fidia kwa wananchi wapatao 474 kutoka vijiji vya Mseko na Kigurusimba, Kata ya Masaika wilayani humo, limeanza.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dk. Batilda Buriani, amepongeza zoezi hilo la ulipaji fidia wananchi kwani ni hatua nzuri kuelekea utekelezaji wa mradi huo ambao una tija kubwa katika kukuza maendeleo ya mkoa wa Tanga na taifa kwa ujumla.

"Tayari zaidi ya wananchi 400 wameshakamilisha kusaini nyaraka zinazohitajika. Wale waliojitokeza mapema watapewa kipaumbele, huku wengine wakiendelea kuhudumiwa kadri zoezi linavyoendelea," amesema Balozi Dk. Buriani.

Kimsingi, mradi huo utagharimu dola za kimarekani milioni 350, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 900 za Kitanzania, huku ekari 22,000 zikitarajiwa kutumika kufanikisha utekelezaji wa mradi huo kabambe wilayani Pangani.

Kwahiyo, utekelezaji wa mradi huu utasaidia kuongeza fursa za ajira nchini hasa kwa vijana huku ukichangia uzalishaji wa sukari kwani dhamira ya serikali ni kuhakikisha nchi yetu inajitosheleza kwa mahitaji ya sukari na kuuza ziada nje ya nchi.

Pia, sekta ya kilimo wilayani Pangani itakua kwani wakulima wataongeza kasi ya uzalishaji wa miwa kutokana na uhakika wa soko katika kiwanda hicho.

Sambamba na hilo, mapato ya ndani wilayani humo pamoja na ongezeko la makusanyo ya kodi yataongezeka kupitia uwepo wa mradi huo. Haya yote yatachechemua uchumi na maendeleo ya wilaya ya Pangani, mkoa wa Tanga na taifa kwa ujumla.
Posted by MROKI On Thursday, July 02, 2026 No comments






Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Asha-Rose Migiro, amefanya mazungumzo na Mheshimiwa Christine Grau, Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, katika Ofisi ya Katibu Mkuu wa CCM, Lumumba, Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yamefanyika ikiwa ni sehemu ya ziara ya kumuaga Balozi Grau anayehitimisha kipindi chake cha uwakilishi nchini Tanzania. Viongozi hao walitathmini ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya na kujadili namna ya kuuendeleza kwa manufaa ya pande zote mbili.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao walibadilishana mawazo kuhusu umuhimu wa kuimarisha misingi ya utawala bora, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa kama nguzo ya maendeleo endelevu ya Taifa. Katika muktadha huo, CCM ilisisitiza dhamira yake ya kuendelea kujenga Taifa linaloongozwa kwa misingi ya haki, uwajibikaji na utulivu wa kisiasa.

Pia, ilitambua changamoto zilizojitokeza nchini katika kipindi cha Uchaguzi Mkuu uliopita na umuhimu wa hatua ambazo Serikali inaendelea kuzichukua katika kuimarisha imani ya wananchi, ikiwemo kuundwa kwa Tume ya Uchunguzi, Tume ya Upelelezi wa Jinai na hatua nyingine za kisheria zinazolenga kuhakikisha ukweli, uwajibikaji na haki vinaendelea kutawala katika kulinda amani na mshikamano wa Taifa.

Aidha, ilielezwa kuwa ajenda ya kuendelea kuimarisha demokrasia nchini, ikiwemo mchakato wa Katiba Mpya ambao umeainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2025–2030, inabaki kuwa sehemu muhimu ya maono ya muda mrefu ya kuimarisha utawala bora na mshikamano wa Taifa.

Viongozi hao pia walitambua nafasi ya vijana katika mustakabali wa maendeleo ya Tanzania na umuhimu wa kuhakikisha kizazi hicho kinaendelea kuwa sehemu ya safari ya Taifa kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na ujenzi wa uchumi wenye ushindani na maendeleo jumuishi.

CCM inathamini ushirikiano wake na Umoja wa Ulaya na inaamini kuwa ushirikiano huo utaendelea kuimarika kwa kuzingatia misingi ya kuheshimiana, maslahi ya pamoja na dhamira ya pamoja ya kuendeleza maendeleo endelevu ya Tanzania.
Posted by MROKI On Thursday, July 02, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo