Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Ndugu Aggrey Mwanri, akiwa ameambatana na wajumbe wengine wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, amepokelewa Makao Makuu ya CCM, jijini Dodoma, leo tarehe 6 Agosti 2026. Mapokezi hayo yaliyoandaliwa na CCM Mkoa wa Dodoma, yamehudhuriwa na wanachama, makada na viongozi mbalimbali wa CCM, akiwemo Makamu Mwenyekiti Mstaafu wa CCM (Bara), Mzee Philip Japhet Mangula.
August 06, 2026
Tume ya Madini imeendelea kuimarisha ukaguzi wa migodi nchini ili kuhakikisha shughuli zote za uchimbaji zinafanyika kwa kuzingatia sheria, usalama wa wafanyakazi, afya kazini na utunzaji wa mazingira, hatua inayolenga kujenga sekta ya madini yenye tija na endelevu.
Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma, Mjiolojia na Mkaguzi wa Migodi kutoka Tume ya Madini, Paschal Juma, amesema Kurugenzi ya Ukaguzi wa Migodi na Mazingira chini ya Mkurugenzi wake, Mhandisi Hamisi Kamando, ina jukumu la kusimamia na kufuatilia shughuli zote za uchimbaji ili kuhakikisha zinazingatia Sheria ya Madini, kanuni, sera na miongozo mbalimbali ya sekta hiyo.
Amesema Kurugenzi hiyo hufanya ukaguzi wa usalama na afya mahali pa kazi, hufuatilia utekelezaji wa mipango ya usimamizi wa mazingira, urejeshaji wa maeneo yaliyochimbwa pamoja na mipango ya ufungaji migodi kwa kuzingatia viwango vinavyolinda mazingira na kuhakikisha rasilimali za madini zinatumika kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Aidha, amesema Kurugenzi hiyo hupitia na kuidhinisha mipango ya uchimbaji, taarifa za utendaji wa migodi na usanifu wa miundombinu ya migodi, huku ikisimamia matumizi salama ya baruti kwa mujibu wa Sheria ya Baruti, Sura ya 45, na kanuni zake.
Paschal amesema Tume ya Madini inatumia Maonesho ya Nanenane kama jukwaa la kutoa elimu kwa wananchi, wachimbaji na wadau wa sekta kuhusu matumizi sahihi ya vifaa vya kujikinga, mbinu salama za uchimbaji, utunzaji wa mazingira pamoja na uhifadhi na matumizi salama ya baruti.
Amesisitiza kuwa elimu hiyo inalenga kuongeza uelewa wa wadau, kuimarisha uzingatiaji wa sheria na viwango vya usalama, kupunguza ajali migodini na kuendeleza sekta ya madini inayochangia ukuaji wa uchumi wa taifa kwa njia endelevu.
August 05, 2026
Kampuni ya CDICD Group Limited imeendelea kuimarisha mnyororo wa thamani katika Sekta ya Madini kwa kuchakata madini ya black granite na kuzalisha bidhaa mbalimbali za ujenzi zinazouzwa katika soko la ndani na nje ya nchi, hatua inayochochea ukuaji wa viwanda, kuongeza ajira na kukuza mauzo ya bidhaa zenye thamani.
Akizungumza jijini Dodoma kwenye Maonesho ya Nane Nane, Meneja wa CDICD, Shija Shimba, amesema kampuni hiyo imewekeza katika kiwanda cha kisasa cha uchakataji wa black granite kinachobadilisha mawe ghafi kuwa bidhaa mbalimbali zikiwemo countertops za majiko, paving stones, slabs za ujenzi na headstones zinazotumika katika makaburi.
Amesema shughuli za uchimbaji na uchakataji zinafanyika katika kijiji cha Manyemba, wilayani Chamwino mkoani Dodoma, ambapo kampuni imejikita katika kuongeza thamani ya madini kabla ya kuyapeleka sokoni.
Kwa mujibu wa Shimba, uwekezaji huo umeiwezesha CDICD kupanua masoko yake ndani na nje ya Tanzania. Mbali na kuuza bidhaa zilizochakatwa nchini, kampuni pia husafirisha black granite blocks kwenda China na nchi nyingine kwa ajili ya uchakataji zaidi katika viwanda vya nchi hizo.
Amesema kampuni huzalisha wastani wa tani 270 za black granite kwa wiki, huku bidhaa zake zikisambazwa kupitia vituo vya mauzo vilivyopo Dodoma na Victoria, Kinondoni jijini Dar es Salaam, pamoja na mikoa mbalimbali nchini.
Shimba amesema uwekezaji huo pia umefungua fursa za ajira kwa vijana kati ya 90 na 100 wanaofanya kazi katika maeneo mbalimbali, ikiwemo uendeshaji wa mitambo, udereva, uchomeleaji na shughuli nyingine za uzalishaji.
Ameongeza kuwa CDICD ilianza shughuli zake mwaka 2014 na imeendelea kupanua shughuli za uchimbaji wa black granite katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Chamwino, kabla ya kuhamishia shughuli zake Manyemba, ambako inaendelea na uzalishaji na uchakataji wa madini hayo kwa sasa.
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, ameipongeza Halmashauri ya wilaya ya Songwe kwa kufanikisha miradi mingi ya maendeleo yenye tija kwa wananchi.
Chatanda ametoa pongezi hizo, Agosti 3, wilayani Songwe, katika ziara maalum ya viongozi wa UWT Taifa kukagua shughuli mbalimbali mkoani Songwe.
Amesema kuwa, serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, imejikita katika kutatua kero za wananchi kupitia miradi ya maendeleo.
"Nimejionea kwa macho kazi nzuri zimefanyika Songwe, mmegusa maisha ya wananchi, fedha za mikopo ya asilimia kumi zinafika kwa vijana, wanawake na wenye mahitaji maalum, hakika Songwe mmeonyesha mfano mzuri wa kuigwa," amesema Chatanda.
Akiwa Songwe, Chatanda na wajumbe wa Jumuiya hiyo, walipata fursa ya kutembelea kikundi cha wanawake cha 'Mama ni Nguzo' kinachojishughulisha na uchimbaji na uchenjuaji wa madini ya dhahabu. Kikundi hiki kimenufaika na mkopo wa shilingi milioni 100.
Aidha, walitembelea kikundi cha waponda kokoto Saza ambacho kimeonyesha uaminifu wa kurejesha mkopo wote wa shilingi milioni 23 waliokopeshwa awali huku uongozi wa Halmashauri ukijipanga kuwakopesha gari aina ya fuso ili kubeba mawe na hatimaye waweze kukuza mradi wao.
Katika hatua nyingine, wajumbe hao walitembelea mradi wa ujenzi wa Soko la Madini la CPA. Cecilia Kavishe, ambapo ujenzi wake umefikia asilimia 99.
Sanjari na hilo, wametembelea mradi wa ujenzi wa nyumba ya Katibu wa UWT wilaya, huku wakipongeza hatua nzuri iliyofikiwa.
Ziara hiyo ya siku tatu mkoani humo ni mahsusi kwa ajili ya kukagua uhai wa Chama, Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025-2030.
Vilevile, kufanya mikutano ya ndani, kuongea na wanachama na wananchi kuwapongeza kwa kuendelea kuwa na imani na Chama hicho katika kuwatumikia.
Katika ziara hiyo, Chatanda ameambatana na viongozi wengine wakiwemo Ellen Bogohe (MNEC), Mjumbe wa Baraza Kuu la UWT Taifa Flora Magambe na Mbunge wa Viti Maalum, Dk. Catherine Joakim.
WAGENI mbalimbali wameendelea kumiminika kwenye Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii kwenye Maonesho ya Maadhimisho ya Siku ya Wakulima Duniani (NANE NANE), kujionea shughuli mbalimbali za uhifadhi na wanyamapori zinazofanywa na Wizara.
Miongoni mwa wageni waliotembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii ni pamoja na Wakuu wa Wilaya na Makatibu Tawala mbalimbali ambapo waliipongeza Wizara kwa ushiriki wa Maonesho hayo ya NANE NANE kwani wamekuwa wakichagiza uwepo wa wananchi wengi wanaokuja kufanya utalii wa ndani wa kuona wanyamapori.
Makatibu Tawala hao ni pamoja na Katibu Tawala wa Wilaya ya Kongwa Sozi Ngate, Katibu Tawala wa Wilaya ya Dodoma Mjini Sakina Mbugi, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kondoa Christina Kalekezi na Wakuu wa Wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri na Mpwapwa Dkt. Sophia Kizigo.
Viongozi hao wamesema kila mwaka Wizara ya Maliasili na Utalii imekuwa ikipokea wageni wengi hususani wananchi na wanafunzi wanaotembelea banda lake kujifunza elimu kuhusu uhifadhi, wanyamapori, malikale, misitu na nyuki.
Katika hatua nyingine Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii Imepokea wananfunzi zaidi ya elfu moja waliofika kwa ajili ya kupata wa elimu na kuona wanyamapori hai ambapo wengi wao wamevutiwa na mnyama Ngiri maarufu kama Kasongoyeye ambaye ana umaarufu mkubwa kutokana na tabia yake na kutokuwa na woga.
BALOZI wa Tanzania nchini Italia na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) na Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa (WFP), Mhe. Mbarouk Nassoro Mbarouk leo Agosti 04, 2026, ametembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii na kusema kuwa nchi ya Italia ina nafasi kubwa ya kuleta watalii wengi nchini.
Mhe. Balozi Mbarouk amesema Tanzania inafanya vizuri kwenye kutangaza utalii na vivutio vyake na kuipongeza Wizara kwa kazi nzuri inayoifanya.
Katika hatua nyingine Wizara ya Maliasili na Utalii imepokea ugeni wa Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Rajab Mruma ambaye ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kubuni mbinu za kutafuta utatuzi wa changamoto za wanyamapori hai kuingia kwenye makazi ya wananchi kwa kujenga uzio ili kuzuia uharibifu unaoweza kutokea.
Aidha, Mhe Jaji Mruma ametembelea bustani ya wanyamapori hai iliyoko kwenye Maonesho ya Nane Nane yanayoendelea Jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya kutangaza utalii wa ndani kwa wananchi.
August 04, 2026
Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe kupitia programu ya Polisi Jamii limeendelea kuonesha mshikamano na jamii baada ya kuwatembelea wakina mama waliojifungua, watoto na wagonjwa mbalimbali katika kituo cha afya cha Tnduma kilichopo Wilaya ya Momba, ambapo walikabidhi mahitaji mbalimbali na kuwasaidia kulipia gharama ndogo za matibabu. Hatua hiyo imelenga kuimarisha mahusiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi pamoja na kuhamasisha ushirikiano katika kudumisha amani, usalama na malezi bora ya watoto.
Akiongoza ziara hiyo Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Songwe, Kamishna Msaidizi wa Polisi Maria Kway, tarehe 04 Agosti 2026, alisema kuwa malezi bora ndiyo msingi wa kujenga taifa lenye maadili na usalama, hivyo aliwataka wakina mama kuhakikisha watoto wanapata haki zao za msingi, uangalizi unaostahili na kulindwa dhidi ya aina zote za ukatili, ikiwemo unyanyasaji wa kimwili, kisaikolojia na kijinsia.
Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuzuia uhalifu na kulinda ustawi wa jamii.
Mwisho wananchi wamehimizwa kutumia elimu hiyo kwa kuwalea watoto katika mazingira salama, kuripoti matukio ya ukatili na uhalifu kwa wakati kwenye vyombo vya dola, pamoja na kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kudumisha amani, usalama na maendeleo ya jamii kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Vijana nchini wamehimizwa kutumia nguvu kazi, maarifa na ubunifu wao kuchangamkia fursa zinazotolewa na Sekta ya Madini badala ya kusubiri misaada au mitaji kutoka serikalini, huku wakitakiwa kuanza na rasilimali walizonazo ili kujenga mafanikio ya kiuchumi.
Wito huo umetolewa kwenye Maonesho ya Nane Nane yanayoendelea Kitaifa jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Xinda Energy Resources Technology Import and Export Trade Co. Ltd, Abia Mafie, aliyesema Serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa vijana kupitia mafunzo, warsha na programu mbalimbali za uwezeshaji, lakini baadhi yao hushindwa kutumia maarifa hayo kwa vitendo.
“Vijana tusisubiri Serikali itupatie kila kitu. Unaweza kuanza na kidogo ulichonacho na ukakua hatua kwa hatua. Watu wengi waliofanikiwa walianza hivyo,” amesema Mafie.
Amesema Sekta ya Madini ni miongoni mwa maeneo yenye fursa kubwa za ajira, ujasiriamali na uwekezaji, hususan katika uchakataji na uongezaji thamani wa madini, hatua inayochochea ukuaji wa uchumi wa viwanda na kuongeza mapato ya taifa.
Mafie amesema kampuni yake imewekeza katika uchakataji wa shaba na kuzalisha copper cathode yenye kiwango cha ubora cha asilimia 99.99 kinachokidhi viwango vya soko la kimataifa, hatua inayounga mkono juhudi za Serikali za kuongeza thamani ya rasilimali za madini nchini.
Ameeleza kuwa Xinda Precious Metal Resources Co. Ltd ilianza kujenga kiwanda chake mwaka 2024 na kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha tani 50 za copper cathode kwa mwezi, huku bidhaa zake zikipata soko kutokana na ubora wake.
Kwa mujibu wa Mafie, kampuni hiyo inapanga kujenga viwanda vingine viwili vya uchakataji mkoani Dodoma ili kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za usafirishaji wa malighafi na kuongeza mchango wa Sekta ya Madini katika maendeleo ya uchumi wa taifa.
Amesema uwekezaji huo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, huku ukionesha nafasi muhimu ya sekta binafsi na ushiriki wa Watanzania katika kuongeza thamani ya madini na kuimarisha uchumi unaotegemea viwanda.
Subscribe to:
Posts (Atom)
























































