Nafasi Ya Matangazo

March 18, 2024

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi (kushoto) kwenye picha ya pamoja na Katibu Mkuu wa Chama cha SWAPO (Namibia) Komredi Sophia Shaningwa (katikati) na Katibu Mkuu wa Chama cha ANC (Afrika Kusini), Komredi Fikile Mbalula (kulia), wakionesha alama ya salaam za CCM, Chama cha ANC na Chama cha SWAPO, leo Jumatatu, Machi 18, 2024, pembezoni mwa siku ya kwanza ya Mkutano wa 11 wa Makatibu Wakuu wa Vyama Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika, unaofanyika katika Mji wa Victoria Falls, nchini Zimbabwe. Makatibu Wakuu  wa Vyama wengine wanaoshiriki mkutano huo ni pamoja na Komredi Roque Silva Samuel (FRELIMO - Msumbiji), Komredi Paulo Pombolo (MPLA - Angola), Komredi Kavis Kario (BDP – Botswana) na Komredi Albert Mpofu (ZANU – PF - Zimbabwe), ambaye ni mwenyeji wa mkutano huo.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi akijadiliana jambo na wajumbe wa msafara wake aliombatana nao kushiriki Mkutano wa 11 wa Makatibu Wakuu wa Vyama Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika (FLMS), leo Jumatatu, Machi 18, 2024. Kutoka kushoto ni Gilbert Kalima (Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wazazi), Fack Lulandala (Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM – UVCCM), akifuatiwa na Tunu Juma Kondo (Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake – UWT – Zanzibar). Mkutano huo unaofanyika katika Mji wa Victoria Fall, nchini Zimbabwe, umewakutanisha Makatibu Wakuu wengine wa vyama hivyo rafiki, ambao ni pamoja na Katibu Mkuu wa Chama cha SWAPO (Namibia) Komredi Sophia Shaningwa, Katibu Mkuu wa Chama cha ANC (Afrika Kusini), Komredi Fikile Mbalula, Komredi Roque Silva Samuel (FRELIMO - Msumbiji), Komredi Paulo Pombolo (MPLA - Angola), Komredi Kavis Kario (BDP – Botswana) na Komredi Albert Mpofu (ZANU – PF - Zimbabwe), ambaye ni mwenyeji na mwenyekiti wa mkutano huo.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi akizungumza wakati wa kutoa salaam za CCM za mshikamano kwenye Mkutano wa 11 wa Makatibu Wakuu wa Vyama Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika (FLMS), leo Jumatatu, Machi 18, 2024. Mkutano huo unaofanyika katika Mji wa Victoria Falls, nchini Zimbabwe, umewakutanisha Makatibu Wakuu wengine wa vyama hivyo rafiki, ambao ni pamoja na Katibu Mkuu wa Chama cha SWAPO (Namibia) Komredi Sophia Shaningwa, Katibu Mkuu wa Chama cha ANC (Afrika Kusini), Komredi Fikile Mbalula, Komredi Roque Silva Samuel (FRELIMO - Msumbiji), Komredi Paulo Pombolo (MPLA - Angola), Komredi Kavis Kario (BDP – Botswana) na Komredi Albert Mpofu (ZANU – PF - Zimbabwe), ambaye ni mwenyeji na mwenyekiti wa mkutano huo.
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi akizungumza wakati wa kutoa salaam za CCM za mshikamano kwenye Mkutano wa 11 wa Makatibu Wakuu wa Vyama Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika (FLMS), leo Jumatatu, Machi 18, 2024. Mkutano huo unaofanyika katika Mji wa Victoria Falls, nchini Zimbabwe, umewakutanisha Makatibu Wakuu wengine wa vyama hivyo rafiki, ambao ni pamoja na Katibu Mkuu wa Chama cha SWAPO (Namibia) Komredi Sophia Shaningwa, Katibu Mkuu wa Chama cha ANC (Afrika Kusini), Komredi Fikile Mbalula, Komredi Roque Silva Samuel (FRELIMO - Msumbiji), Komredi Paulo Pombolo (MPLA - Angola), Komredi Kavis Kario (BDP – Botswana) na Komredi Albert Mpofu (ZANU – PF - Zimbabwe), ambaye ni mwenyeji na mwenyekiti wa mkutano huo.
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi (wa pili kutoka kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja, leo Jumatatu, Machi 18, 2024, pembezoni mwa siku ya kwanza ya Mkutano wa 11 wa Makatibu Wakuu wa Vyama Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika, unaofanyika katika Mji wa Victoria Falls, nchini Zimbabwe. Makatibu Wakuu wengine pichani, (kutoka kulia) ni Komredi Roque Silva Samuel (FRELIMO - Msumbiji), Komredi Paulo Pombolo (MPLA - Angola), Komredi Albert Mpofu (ZANU – PF - Zimbabwe, mwenye suti), Komredi Sophia Shaningwa (SWAPO – Namibia) na Komredi Fikile Mbalula (ANC – ANC).

Mkutano wa 11 wa vyama rafiki vya Ukombozi Kusini Mwa Afrika (FLMS), unaowakutanisha wajumbe wake, ambao ni pamoja na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi, Katibu Mkuu wa Chama cha SWAPO (Namibia), Komredi Sophia Shaningwa, Katibu Mkuu wa Chama cha ANC (Afrika Kusini), Komredi Fikile Mbalula, Katibu Mkuu wa Chama cha FRELIMO (Msumbiji), Komredi Roque Silva Samuel, Katibu Mkuu wa Chama cha MPLA (Angola), Komredi Paulo Pombolo, Katibu Mkuu wa Chama cha BDP (Botswana), Komredi Kavis Kario na Katibu Mkuu wa Chama cha ZANU – PF (Zimbabwe), Komredi Albert Mpofu, (mwenyeji na mwenyekiti wa mkutano), ukiendelea kujadili agenda, leo Jumatatu, Machi 18, 2024, katika ukumbi ulioko Mji wa Victoria Falls, nchini Zimbabwe, unakofanyikia.
Posted by MROKI On Monday, March 18, 2024 No comments
Waziri Mavunde na CEO wa Barrick wakikata utepe kuzindua chuo, katikati ni mkuu wa wilaya ya Kahama, Mboni Mhita
***********
Waziri wa Madini, Mhe. Antony Mavunde, ameipongeza Kampuni ya Dhahabu ya Barrick ambayo inaendesha shughuli zake nchini kwa ubia na Serikali kupitia kampuni ya Twiga Minerals, kwa kufanya uwekezaji unaoendelea kuchangia kukuza uchumi na kufanikisha miradi ya kijamii ambayo inaendelea koboresha maisha ya wananchi.

Mh. Mavunde, ametoa pongezi hizo leo Jumatatu Machi 18,2024 wilayani Kahama wakati wa uzinduzi wa Chuo cha mafunzo cha Barrick chenye hadhi ya kimataifa kijulikanacho kama Barrick Academy, katika mgodi wa zamani wa Buzwagi wilayani Kahama ambao umefungwa ambacho kitakuwa kinatoa mafunzo kwa wafanyakazi wa Barrick wa nchini na nje ya nchi kupata utaalamu wa kuendesha shughuli zao kwa weledi.

Waziri Mavunde amesema ulimwengu wa sasa ni wa sayansi na teknolojia hivyo chuo hicho kimeanzishwa katika wakati muafaka ambapo sekta ya madini nchini inakua kwa kasi sana na kuhitaji wataalamu wa kutosha.

Ametoa wito kwa uongozi wa Barrick kuangalia uwezekano wa kuanzisha kozi za kuwasaidia wachimbaji wadogowadogo nao wapate maarifa ya kuendesha kazi zao kwa maarifa.

“Barrick mmeanza kwa kufungua chuo katika eneo hili la Ukanda Maalum wa Kiuchumi la Buzwagi la Serikali, nina imani wawekezaji wengi watajitokeza kujenga viwanda ili kuziba athari za kiuchumi zilizotokana na kufungwa kwa mgodi wa Buzwagi”,amesisitiza.

Kwa upande Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow, amesema Barrick itaendelea kufanya kazi na Serikali kuhakikisha ubia wake unanufaisha pande zote na kuchangia kukuza uchimi wa nchi,

Bristow amesema Barrick, inalipa umuhimu kubwa suala la elimu na itaendelea kuwekeza katika sekta hiyo ili kuhakikisha watanzania wanapata elimu na ndio maana imeamua kufungua chuo kikubwa cha kimataifa cha Barrick Academy nchini.

“Tutaendelea kuhakikisha kuwa ubia wetu na Serikali ya Tanzania unakuwa wa kuigwa katika sehemu mbalimbali duniani kwa kufanikisha kuleta mafanikio na maendeleo chanya kwa wananchi”, alisisitiza Dkt. Bristow.

Bristow amesema Chuo cha Barrick kimebuniwa na Barrick ili kutoa programu maalumu za mafunzo zinazoandaliwa kulingana na mahitaji zinazolenga kuandaa mameneja wa mstari wa mbele wa Barrick ili wakue kama watu binafsi na viongozi katika nyanja zao huku kozi hizo zikiwapa ujuzi wa kusimamia timu zao kwa ufanisi zaidi na kuboresha utendaji.

“Chuo cha Barrick kitakuwa kikitoa mafunzo kwa mafomeni, wasimamizi na warakibu zaidi ya 2,000 kutoka Kannda ya Afrika Mashariki na Kati katika kipindi cha miezi 24 ijayo. Tukiwa na maono ya mbele, tunajitayarisha pia kuwajumuisha Wakandarasi wetu na kupanua mtaala ili kufikia taaluma nyingi zaidi ikiwa ni pamoja na kutoa kozi za uongozi katika masuala ya fedha, ujuzi wa ngazi ya juu wa Kompyuta na katika masuala ya usalama”,ameongeza Bristow.

Ameeleza kuwa, ufunguzi wa chuo cha Barrick unafuatia ujenzi wa jengo la abiria katika uwanja wa ndege wa Buzwagi Kahama mnamo mwezi Januari 2024 lililofungua fursa kwa ajili ya huduma za ndege zilizopangwa ambalo linaweza kuhudumia zaidi ya abiria 200 kwa wakati mmoja ambapo jengo hilo linatarajiwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji uchumi katika Manispaa ya Kahama.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Afisa Mkuu wa Uendeshaji wa Barrick katika Kanda ya Afrika Mashariki na Kati, Sebastiaan Bock amesema uwanja wa ndege na Chuo katika mgodi uliofungwa wa Buzwagi ni sehemu ya mpango wa Barrick wa kuibadili Buzwagi kuwa Ukanda Maalum wa kiuchumi.

“Upembuzi yakinifu uliofanyika mwaka 2021 ulionesha kuwa uundwaji wa Kanda maalumu ya kiuchumi ulikuwa na uwezo wa kuchukua nafasi ya mgodi wa Buzwagi kama kichocheo cha uchumi wa eneo hili na unaweza kutengeneza ajira zipatazo 3,000 kila mwaka, kuzalisha zaidi ya dola 150,000 kila mwaka kutokana na tozo za huduma kwa Manispaa ya Kahama na kutoa takribani dola milioni 4.5 kwa mwaka kama kodi ya ajira”,amesema Sebastiaan.

Amesema Serikali ya Tanzania iliidhinisha ubadilishaji wa mgodi wa Buzwagi kuwa ukanda maalum wa kiuchumi (SEZ) kupitia tangazo la Serikali ilitolewa mwezi Februari 2024 na tayari Wawekezaji wameanza mchakato wa kuanzisha viwanda katika eneo hilo.

“Namna tunavyofunga migodi yetu ni muhimu kwetu kama ambavyo tunaijenga na kuiendesha. Mgodi wetu wa Buzwagi ulikuwa kitovu cha uchumi katika ukanda huu kwa takribani miaka 15 kabla ya kutoa dhahabu yake ya mwisho mwaka 2021. Hata hivyo, mtazamo wetu huo siyo mwisho wa hadithi hii kwa Buzwagi tunapoibadilisha kuwa mali mbadala yenye tija ambayo itahudumia jamii kwa miongo kadhaa ijayo”,amesema Bock.

Naye Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maeneo Maalum ya Uwekezaji kwa Mauzo ya Nje (EPZA) Charles Itembe, ameipongeza Kampuni ya Barrick kwa kubuni wazo la kuanzisha Chuo cha Barrick huku akiwaomba wawekezaji mbalimbali kujitokeza kuwekeza katika eneo hilo ili kuongeza thamani ya madini na vitu vingine kwenye eneo la Buzwagi ambako kutakuwa na viwanda zaidi ya 100 na mpaka sasa kuna wawekezaji wanane.

Mkuu wa Wilaya ya Kahama Mhe. Mboni Mhita amesema kuanzishwa kwa Chuo cha Barrick ni matokeo mazuri ya ushirikiano baina ya Serikali ya Tanzania na Kampuni ya Barrick ili kukuza uwekezaji nchini.
Mbunge wa Jimbo la Kaham Mjini Mhe. Jumanne Kishimba amewapongeza Barrick kuwa wawekezaji wa kwanza katika Mgodi uliofungwa wa Barrick huku akiomba chuo hicho pia kitumike kutoa mafunzo ya madini kwa wachimbaji wadogo na jinsi ya kufanya biashara ya madini huku Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kahama Thomas Myonga akisema uwekezaji unaofanyika katika eneo hilo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM katika kukuza uwekezaji nchini.

Waziri wa Madini, Mhe. Antony Mavunde
Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow
Afisa Mkuu wa Uendeshaji wa Barrick katika Kanda ya Afrika Mashariki na Kati, Sebastiaan Bock
Meneja wa Barrick nchini, Melkiory Ngido
Waziri wa Madini Antony Mavunde na CEO wa Barrick wakibadilishana mawazo wakati wa hafla hiyo
Sehemu ya wageni waalikwa
Wanafunzi wa awamu ya kwanza katiika chuo katika picha ya pamoja na Waziri Mavunde na Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow na viongozi wengine wa mkoa wa Shinyanga.
Posted by MROKI On Monday, March 18, 2024 No comments
 






Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Biteko ameagiza Watendaji wa Wizara ya Nishati kuanzisha Kitengo maalum cha usimamizi wa Nishati Safi ya Kupikia ili kutekeleza kwa ufanisi ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia na siyo tu kuishia kwenye kuandaa na kushiriki makongamano kisha masuala yote yanaishia hapo.

Amesema hayo tarehe 18 Machi, 2024 jijini Mwanza wakati akifungua Mkutano wa Tano wa Baraza la Wafanyakazi la Wizara  ya Nishati wenye lengo mahsusi la kupitia na kupitisha rasimu ya Bajeti ya Wizara ya Nishati kwa mwaka 2024/2025.

 “Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ndiye kinara wa utekelezaji wa ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia Afrika hivyo wizara lazima iweke mkakati wa kitaasisi na kimfumo ili kufanikisha ajenda hiyo ili utekelezaji wa suala hili usiwe ni jambo la zimamoto.” Amesema Dkt. Biteko

Vilevile, Dkt.Biteko amesema kuwa, Wizara ya Nishati ina jukumu la kuihamisha nchi kutoka matumizi ya mafuta na kuhamia kwenye matumizi ya gesi (CNG) kwa kutengeneza mazingira ambayo yatapunguza utegemezi wa mafuta na hivyo kufanya nchi kujiendesha kwa kutumia CNG hivyo, ameagiza Watendaji wa Wizara kusimamia pia utekelezaji wa suala hilo.

Kuhusu Watumishi wa Wizara ya Nishati, Dkt. Biteko  amewakumbusha Watumishi kufanya kazi kwa bidii huku wizara ikiangalia stahiki zao ikiwemo motisha.

Amesema kuwa, Watumishi wa Wizara ya Nishati wana deni la kuwatumikia Watanzania kwani ndio waliopewa dhamana ya kusimamia Sekta ya Nishati kwa niaba yao hivyo watimize wajibu huo.

Vilevile, ametoa wito kwa  Wizara ya Nishati kuwa na utaratibu wa kuwapa motisha watumishi wanaofanya vizuri katika kazi na wale wazembe na wasiotumikia wananchi kwa weledi na kwa wakati watambuliwe pia na kuchukuliwa hatua stahiki.

Aidha, ametoa angalizo kwa wenye mamlaka ndani ya Wizara na Taasisi zake kutoona fahari ya kutumia vyeo vyao kwa ajili ya kuabudiwa na kutukuzwa kwani nafasi walizonazo ni za muda tu, hivyo wajijengee marafiki zaidi kuliko maadui na kujikita katika kuhudumia wananchi na hivyo kuepuka kuchafua utendaji wa Wizara ya Nishati na Taasisi zake.

Pia, amewataka Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi Wizara ya Nishati kupitia bajeti hiyo kwa umakini kabla haijafika katika ngazi ya Kamati ya Bunge na baadaye  katika Bunge la Bajeti.

Ameongeza kuwa, kama kuna changamoto zozote ambazo Baraza hilo wanaona kuwa zipo katika Sekta basi wazijadili na kutoa njia mbadala ya kutatua changamoto hizo.

“Mfano, pamoja na mradi wa Julius Nyerere kuanza kuzalisha umeme lakini bado tunapaswa kuendeleza miradi mingine kwani JNHPP ni holiday ya muda mfupi, kama tunafikiria miaka 50 mbele lazima tutambue kuwa lazima tuendeleze vyanzo vingine vya umeme ili kuwa na umeme wa ziada., hivyo mna wajibu wa kuja na njia mbadala” Amesema Dkt. Biteko

Awali Mwenyekiti wa Baraza hilo  ambaye ni Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba, alisema kuwa baada ya Baraza hilo kupitisha Bajeti ya Wizara kwa mwaka 2024/ 2025 hatua inayofuata ni kupitishwa kwenye Kamati za Bunge na baadaye Waziri wa Nishati ataisoma bungeni kwa ajili ya kupitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kuhusu bajeti ya mwaka 2023/2024, Mhandisi Mramba amesema kuwa masuala yaliyopangwa kufanyika kwenye bajeti hiyo yametekelezwa kwa kiasi kikubwa na hii ikitoa mwanga kuwa bajeti ijayo pia itatekelezwa vizuri. 

Ameongeza kuwa, kwa sasa Sekta ya Nishati inatazamwa upya kwa kuangalia mchango wa nishati jadidifu katika Sekta, nishati bora ya kupikia, uhifadhi way nishati na matumizi bora ya nishati lengo likiwa ni kuiboresha zaidi Sekta husika kwenye nyanja mbalimbali.
Posted by MROKI On Monday, March 18, 2024 No comments







Na Mwandishi wetu, Dodoma
Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba amesema kuwa Serikali kupitia  Tume  ya Madini itaendelea kuweka mazingira mazuri kwa wachimbaji wadogo wa madini nchini  kama mkakati wa kuhakikisha mchango wao kwenye Sekta ya Madini unaendelea kukua sambamba na kuzalisha ajira zaidi.

Mhandisi Samamba ameyasema hayo leo Machi 18, 2024 kwenye kikao cha sita cha Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Madini kilichofanyika jijini Dodoma ambacho kimeshirikisha Wakurugenzi, Mameneja, Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa, watumishi na wageni waalikwa kutoka TUGHE, na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).

Amesema kuwa, mchango wa wachimbaji wadogo kwenye mapato yatokanayo na Sekta ya Madini umeendelea kukua kutoka asilimia tano (5) hadi asilimia arobaini (40) Mwaka 2022/2023 na kusisitiza kuwa Tume ya Madini itaendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji kwa wachimbaji wadogo sambamba na kutatua changamoto mbalimbali.

Akielezea mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa Tume ya Madini, Mhandisi Samamba amesema kuwa ni pamoja na ongezeko la ukusanyaji wa maduhuli kutoka shilingi bilioni 213.3 katika kipindi cha mwaka wa fedha  2016/17 hadi shilingi bilioni 677.7 katika kipindi cha mwaka wa fedha 2022/2023.

“Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2022/2023 kama Tume ya Madini tulipewa lengo la kukusanya kiasi cha shilingi bilioni  822 na kufanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 677.7  ikiwa ni (82.45%) na katika kipindi cha mwaka wa fedha 2023/2024 tumepewa lengo la kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 882 ambalo ninaamini kabisa tutalivuka,” amesema Mhandisi Samamba.
 
Mhandisi Samamba ameendelea kusema kuwa  siri ya mafaniko kwenye ukusanyaji wa maduhuli ni pamoja na uzalendo na ubunifu wa  watumishi wa Tume ya Madini Makao Makuu, Ofisi za Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa, Maafisa Migodi Wakazi na ushirikiano mkubwa kutoka kwa viongozi wa Wizara ya Madini.

Ameendelea kueleza mafanikio mengine kuwa ni pamoja na uanzishwaji wa  masoko ya madini 42 na vituo vya ununuzi wa madini 100 nchini,  ongezeko la utoaji wa leseni za madini  kutoka leseni 5094 katika mwaka wa fedha 2018/2019 hadi leseni 9642 katika mwaka wa fedha 2022/2023, kudhibiti utoroshaji wa madini na kupungua kwa ajali kwenye migodi ya madini kutokana na kaguzi zinazofanywa mara kwa mara kwenye shughuli za uchimbaji wa madini sambamba na kutolewa kwa elimu.

Amefafanua mafanikio mengine kuwa ni pamoja na ongezeko la ushiriki wa kampuni za kitanzania kwenye utoaji wa huduma kwenye migodi kutokana na maboresho ya kanuni za ushirikishwaji wa watanzania katika Sekta ya Madini ambapo hadi  kufikia mwaka 2022 asilimia 86 ya bidhaa na huduma zinatolewa na kampuni za kitanzania kwenye kampuni kubwa za uchimbaji wa madini huku asilimia 14 zikitolewa na kampuni za nje ya nchi kupitia kibali maalum kinachotolewa na Tume ya Madini na kwa upande wa ajira katika migodi ya madini asilimia 97 ni watanzania huku raia wa kigeni wakiwa ni asilimia (3) tatu.

“Mchango wa Sekta ya Madini kweye Pato la Taifa uliongezeka kutoka asilimia 4.4 mwaka 2017 hadi asilimia 9.1 mwaka 2022; tumejipanga kuhakikisha tunavuka lengo lililowekwa la asilimia 10 kabla ya mwaka 2025,” amesema Mhandisi Samamba.

Katika kikao hicho mbali na kujadili, kutatua changamoto mbalimbali katika Sekta ya Madini na kuweka mikakati ya baadaye, wajumbe wamepata fursa ya kupata elimu kutoka kwa wataalam kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Posted by MROKI On Monday, March 18, 2024 No comments

March 17, 2024

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi, akisalimiana na Mjumbe wa Kamati Kuu na Katibu wa Idara ya Mambo ya Nje ya Chama Tawala cha Zimbabwe (ZANU – PF), Komredi Simbarashe Simbanenduku Mumbengegwi (aliyevaa suti nyeusi kushoto), baada ya Dk. Nchimbi na msafara wa baadhi ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) Taifa, kuwasili mapema leo mchana, Machi 17, 2024, katika Uwanja wa Victoria Falls, nchini Zimbabwe kushiriki Mkutano wa 11 wa Vyama Marafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika.
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi, akisalimiana na kuzungumza jambo na Katibu Mkuu wa Chama cha SWAPO (Namibia), Komredi Mama Sophia Shaningwa walipokutana mara baada ya kuwasili nchini Zimbabwe, leo mchana Machi 17, 2024, kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 11 wa Makatibu Wakuu wa Vyama Marafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika, utakaofanyika nchini humo.




**********
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi, akiambatana na baadhi ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu CCM ya CCM ya Taifa (NEC), amewasili nchini Zimbabwe kushiriki Mkutano wa 11 wa Makatibu Wakuu wa Vyama Marafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika (FLMS), ambao pamoja na masuala mengine utajadili maendeleo ya mshikamano wao na kuuendelea kuuimarisha zaidi.

Mkutano huo ambao pia utashirikisha watendaji wakuu wa Jumuiya za Wazazi, Wanawake na Vijana wa vyama hivyo, utafanyika kwa siku tatu, kuanzia Machi 17 hadi 20, 2024, katika Mji wa Victoria Falls, kwa ajili ya kujadili agenda mbalimbali zinazohusu urafiki na uhusiano wa vyama hivyo ambavyo vyote viko madarakani, vikiongoza Serikali na Nchi husika.

Katika msafara wake, Katibu Mkuu Balozi Dk. Nchimbi ameambatana na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wazazi ya CCM, Komredi Gilbert Kalima, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Vijana wa CCM (UVCCM), Komredi Fack Raphael Lulandala, na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT) Zanzibar, Komredi Tunu Juma Kondo.

Mbali ya Chama Cha Mapinduzi, vyama vingine vinavyoshiriki mkutano huo ni pamoja na mwenyeji ZANU – PF (Zimbabwe), MPLA (Angola), SWAPO (Namibia), FRELIMO (Msumbiji), ANC (Afrika Kusini) na Botswana Democratic Party (BDP – cha Botswana).
Posted by MROKI On Sunday, March 17, 2024 No comments









Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko leo amejumuika na viongozi na wananchi mbalimbali katika misa Takatifu ya kumwombea Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli iliyofanyika katika Kanisa  Katoliki, Parokia ya Mt. Yohana Maria Muzeyi, wilayani Chato mkoani Geita.

Akitoa Salaam za Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Dkt. Biteko amesema kuwa, Dkt. Samia na Serikali yake inaendelea kumkumbuka  Hayati Dkt. John Pombe Magufuli si tu kama Rais katika Serikali Awamu ya Tano, bali pia kama kiongozi aliyeweka misingi mbalimbali ambayo Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kuitekeleza.

Ametaja miradi mbalimbali ambayo ilianzishwa katika Serikali ya Awamu ya Tano ambayo inaendelea kutekelezwa kwa kasi kubwa na Serikali ya Awamu ya Sita, ni pamoja na mradi wa umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) ambao sasa umeshaanza kuzalisha megawati 235, mradi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kutoka Dar es Salaam ambao tayari umeshaanza kufanyiwa  majaribio na ujenzi wa Daraja kubwa la Kigongo-Busisi mkoani Mwanza ambao umefikia asilimia 80.

Dkt. Biteko amewahakikishia Watanzania kuwa, masuala yaliyobuniwa na Hayati Magufuli yanaendelea na yataendelea kutekelezwa kwa kasi kubwa na Serikali ya Awamu ya Sita ili kuendelea kumuenzi kwa vitendo.

“Hayati Magufuli anasifika kote duniani kwa uwezo wake wa kiongozi, karama ya kutatua matatizo ya wananchi, kuwasikiliza wananchi, kuondoa kero, uzembe, ubadhirifu, rushwa na kuhimiza uwajibikaji serikalini, nataka niwahakikishie kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita inayasukuma masuala yote hayo ili kutoa huduma kwa ufanisi kwa watanzania.” Amesisitiza Dkt. Biteko

Vilevile, amempongeza, Mjane wa Hayati Magufuli, Mama Janet Magufuli kwa kuendelea kusimama kama mhimili wa familia na kuendelea kuunganisha na kuiongoza familia hiyo. 

Kwa upande wake, Mjane wa Hayati Magufuli, Mama Janeth Magufuli amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa pamoja na familia hiyo tangu kifo cha Hayati Magufuli ambapo pia amewashukuru viongozi waliojumuika na familia katika adhimisho hilo la misa Takatifu, akieleza kuwa hiyo ni alama ya upendo kwa familia hiyo.

Naye Mbunge wa Chato, Mhe. Dkt. Medard Kalemani amemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuijali wilaya ya Chato kwani pamoja kuitembelea Chato mara kwa mara, ameendelea kutoa fedha zinazotekeleza miradi mbalimbali kama ya maji, shule, afya ( hospitali ya kanda), barabara n.k

Aidha, amemshukuru Dkt. Samia kwa kuendelea kumuenzi Hayati Dkt. John Pombe Magufuli kwa namna mbalimbali ikiwemo kujenga makumbusho ya Hayati Magufuli wilayani Chato ambayo itafanya historia yake na kazi alizofanya kuendelea kujulikana ndani na nje ya nchi, kizazi cha sasa na cha baadaye

Huu ni mwaka wa Tatu tangu Hayati, Dkt. John Pombe Magufuli afariki dunia tarehe 17 Machi, 2021.

Misa hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigella, Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa na Mbunge wa Chato, Mhe. Dkt. Medard Kalemani.
Posted by MROKI On Sunday, March 17, 2024 No comments
Wagombea wa vyama mbalimbali wakiangalia fomu za uteuzi wa wagombea walioteuliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kugombea nafasi ya udiwani Kata ya Kimbiji iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni, Dar es Salaam.

********""" 
Na Mroki Mroki
TUME ya Taifa ya Uchaguzi imetangaza Machi 20,2024 kuwa ni siku ya kupiga kura katika Uchaguzi Mdogo wa udiwani katika Kata 23 za Tanzania Bara.
 
Tume ilitangaza uchaguzi huo baada ya kuketi katika kikao chake cha Februari 15 mwaka huu na siku hiyohiyo, Mkurugenzi wa Uchaguzi, Bw. Kailima, R. K  akatoa taarifa kwa umma juu ya uwepo wa uchaguzi huo mdogo.
 
Tayari mchakato wa Uchaguzi huo umeshaanza ambapo Februari 27 hadi Machi 4, 2024 wagombea walichukua fomu za uteuzi, uteuzi ulifanyika Machi 4,2024 na kampeni za uchaguzi zilianza Machi 5,2024 na zinaendelea hadi tarehe 19 Machi, 2024.
 
Hata hivyo, baada ya hatua ya uteuzi, Kata ya Nkokwa iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Kyela ilipata mgombea mmoja tu aliyeteuliwa bila kupingwa hivyo hakutakuwa na kampeni kwenye Kata hiyo. Hivyo, uchaguzi utafanyika kwenye kata 22 zilizobakia.
 
Kata zitakazofanya uchaguzi huo mdogo ni Kimbiji (Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni), Kasingirima (Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma/Ujiji), Ndevelwa (Halmashauri ya Manispaa ya Tabora), Msangani (Halmashauri ya Mji Kibaha), Fukayosi(Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo), Mlanzi (Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti), Utiri (Halmashauri ya Mji Mbinga) na Mbingamhalule (Halmashauri ya Wilaya ya Songea).

Nyingine ni  Isebya (Halmashauri ya Wilaya ya  Mbogwe), Kibata (Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa), Mshikamano (Halmashauri ya Manispaa ya Musoma), Busegwe (Halmashauri ya Wilaya ya Butiama), Kamwene (Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba), Chipuputa (Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu), Buzilasoga (Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema), Mhande (Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba), Kabwe (Halmashauri ya Nkasi), Bukundi (Halmashauri ya Wilaya ya Meatu) Mkuzi (Halmashauri ya Wilaya ya Muheza) na Boma, Mtimbwani na Mayomboni (Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga).
 
Katika Uchaguzi huu wa Kata 22, Vyama vya siasa 18 vimesimamisha wagombea 127 kati ya hao wanaume ni 89 na wanawake ni 38. Wagombea kutoka kwenye vyama hivyo walichukua fomu za uteuzi na kuzirejesha na hatimaye wakateuliwa kuwania nafasi hiyo.
 
Wagombea wa vyama mbalimbali wakiangalia fomu za uteuzi wa wagombea walioteuliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kugombea nafasi ya udiwani Kata ya Kimbiji iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni, Dar es Salaam. 

Wagombea wote wameaminiwa na kupewa ridhaa na vyama vyao vya siasa kuwania nafasi zilizowazi,  kwa kufanya hivyo, vyama hivyo vya siasa  vimewatendea haki wanachama wao na wananchi kwa ujumla kwa kuwa wamepata haki ya kikatiba ya kugombea lakini pia wanachama na wananchi, watapata haki yao ya kikatiba ya kupiga kura na kuwachagua viongozi wanaowataka.
 
Wagombea walioteuliwa na Tume ni wale waliopendekezwa na vyama vyao vya siasa kugombea kiti cha udiwani ambapo pia walijaza na kuwasilisha fomu za uteuzi katika Ofisi za Uchguzi katika Kata husika.
 
Wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi ngazi ya kata walisimamia vyema majukumu yao ya kutoa fomu za uteuzi. Fomu za uteuzi za wagombea wote ziliwasilishwa siku ya uteuzi kabla ya saa kumi kamili (10:00) jioni.
 
Wagombea hawa wote siku ya uteuzi walijaza na kusaini mbele ya Msimamizi wa Uchaguzi Fomu Na. 10 ya maadili ya uchaguzi.
 
Wagombea hawa walijaza fomu hizo   kukiri kuheshimu na kuyazingatia maadili ya uchaguzi yaliyosainiwa na  viongozi wa vyama vyao mwaka 2020 wakati wa uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Madiwani kwa Tanzania Bara.
 
Uwepo wa maadili ya Uchaguzi unalenga hasa kuwa na uchaguzi huru, wa haki, uwazi na wa kuaminika. Na kwamba amani, ustawi wa nchi, usalama wa raia, uhuru wa vyama vya siasa na utii wa sheria , kanuni na taratibu za uchaguzi ndio msingi wa uchaguzi ulio huru, haki na wenye kuzingatia ushiriki wa makundi yote ya jamii katika uchaguzi.
 
Vyama vya Siasa, Serikali na Tume walikubaliana kuwajibika kuyatekeleza Maadili hayo yanayotokana na kifungu cha 124A cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343. Viongozi hao kwa pamoja walisema “Tutafanya jitihada za wazi kuhakikisha Maadili haya yanajulikana na kuheshimiwa na wagombea pamoja na wanachama wote wa vyama vya siasa”.
 
Sheria, Kanuni na miongozo yote iliyotumika katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 bado inatumika na kufuatwa na vyama vya siasa, Tume ya Taifa ya Uchagzi na Serikali katika chaguzi hizi ndogo za udiwani.
 
Tayari Kampeni za uchaguzi zimeanza tangu siku moja baada ya uteuzi na zitaendelea hadi siku moja kabla ya siku ya kupiga kura.
 
Wakati wote wa kampeni wagombea wanatakiwa kuzingatia sheria, kanuni za uchaguzi, Maadili ya Uchaguzi na ratiba za kampeni.
 
Uzingatiaji wa Sheria, Kanuni, Maadili ya Uchaguzi na ratiba za kampeni utasaidia katika kuweka uwanja sawa katika kipindi chote cha kampeni na siku ya uchguzi.
 
Vyama vya Siasa na wagombea pamoja na wafuasi wao wanapaswa kuepuka kufanya siasa za fujo na za vitisho dhidi ya upande mwingine.
 
Aidha, Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa mujibu wa kifungu cha 4C cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343, imepewa jukumu la kutoa elimu ya mpiga kura nchi nzima, kuratibu na kusimamia taasisi au asasi za kiraia zinazotoa elimu hiyo.
 
Tume itatoa elimu kwa wananchi katika maeneo yote ambayo yanafanya uchaguzi mdogo. Lakini pia zipo asasi ambazo zimepewa kibali na Tume kutoa elimu hiyo kwa baadhi ya maeneo.
 
Elimu hiyo inayotolewa ni ile ya kumuwezesha Mpiga Kura kutambua sheria, kanuni na taratibu za uchaguzi ikiwa ni pamoja na utaratibu mzima wa kufunguliwa na kufungwa kwa vituo vya kupigia kura. 
 
Lakini pia elimu hiyo itasaidia kutoa hamasa kwa wananchi kutumia haki yao ya kikatiba katika kujitokeza kupiga kura na kuchagua viongozi wanaowataka.
 
Ni muhimu wananchi katika maeneo yote yanayofanya uchaguzi mdogo wakajitokeza kwa wingi kusikiliza sera za vyama na wagombea kisha kwa utashi wao wachague viongozi wanaowafaa kujaza nafasi zilizowazi katika Kata 23 za Tanzania Bara.
 
Mwandishi wa Makala haya ni Afisa Habari Msaidizi Mwandamizi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi.


Posted by MROKI On Sunday, March 17, 2024 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo