Nafasi Ya Matangazo

August 21, 2026




Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Benjamin Kuzaga amewaongoza Maafisa, Wakaguzi na Askari wa vyeo mbalimbali wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia Mbeya kutoa msaada wa mahitaji mbalimbali kwa akina mama waliolazwa Kituo cha Afya Ruanda Mwanjelwa Jijini Mbeya.

Akizungumza Agosti 21, 2026 mara baada ya kutembelea Kituo hicho, Kamanda Kuzaga amesema kuwa lengo la kufika katika kituo hicho ni kutoa msaada kwa akina mama ambao wamelazwa, kuwapatia vitu mbalimbali kama vile Sukari, Maziwa, Sabuni, Soda, Pampasi ili viweze kuwasaidia katika kipindi ambacho watakuwa Kituoni hapo.

Aidha, Mkuu wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia Mkoa wa Mbeya Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Ibrahim Mhando kwa niaba ya Askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia ameeleza kuwa wao kama Askari wa Kikosi hicho waliona ni vema kufika Katika Kituo cha Afya Ruanda kwa ajili ya kuwashika mkono kwa kuwapatia vitu mbalimbali wagonjwa ambao wamelazwa ili viweze kuwasaidia.

Naye, Bi. Adelina Amnaaye Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Ruanda - Mwanjelwa Mbeya amelishukuru Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kwa kuchagua kutembelea Kituo hicho na kwa msaada walioutoa kwani vitu hivyo vitawasaidia wagonjwa ambao wamelazwa Hospitalini hapo.

Kwa upande wake, Witness Kiberenge kwa niaba ya akina mama waliolazwa Hospitalini hapo amelishukuru Jeshi la Polisi kwa msaada wa vitu mbalimbali huku akitoa wito kwa jamii kuwakumbuka wagonjwa na watu wenye mahitaji maalum.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kuelekea Maadhimisho ya miaka ishirini (20) ya Polisi Jamii, linaendelea kuyafikia makundi mbalimbali yenye uhitaji lengo likiwa ni kutoa elimu, misaada mbalimbali kwa makundi ya kijamii yenye mahitaji maalum.






Posted by MROKI On Friday, August 21, 2026 No comments
Katika sekta ya usafiri wa anga, kuna wataalamu mbalimbali wanaoshiriki kuhakikisha ndege zinafanya safari kwa usalama na ufanisi. Miongoni mwa wataalamu ambao mara nyingi huchanganywa ni Waongozaji wa Ndege, wanaojulikana kama Air Traffic Controllers, na Waegeshaji wa Ndege, wanaojulikana kitaalamu kama Aircraft Marshallers.
Waegeshaji wa ndege ni wataalamu wanaofanya kazi katika maeneo ya maegesho ya ndege viwanjani. Mara nyingi huonekana wakiwa wamevaa mavazi maalum ya usalama na kutumia vijiti vya mwanga au ishara za mikono kumwelekeza rubani wakati ndege inapokaribia sehemu ya maegesho au inapojiandaa kuondoka.

Jukumu lao ni kuhakikisha ndege inaelekezwa kwa usahihi katika eneo lililotengwa bila kuhatarisha usalama wa ndege, vifaa vya uwanja, majengo au watu waliopo katika mazingira ya karibu. Ishara wanazotumia hutambulika kimataifa na humsaidia rubani kufanya maamuzi sahihi hasa katika maeneo ambayo mwonekano kutoka ndani ya ndege unaweza kuwa na mipaka.

Historia ya kazi ya uegeshaji wa ndege inaanzia katika miaka ya mwanzo ya maendeleo ya usafiri wa anga, ambapo mawasiliano kati ya marubani na wahudumu wa ardhini yalitegemea zaidi ishara za mikono. Pamoja na maendeleo ya teknolojia katika viwanja vya ndege, kazi ya Aircraft Marshaller bado inaendelea kuwa sehemu muhimu ya shughuli salama za ndege ardhini.

Kwa upande mwingine, Waongozaji wa Ndege, au Air Traffic Controllers, wana jukumu la kusimamia na kuratibu mwendo wa ndege angani na katika maeneo maalum ya viwanja vya ndege. Hutumia mifumo ya mawasiliano, ufuatiliaji na taratibu za uongozaji wa ndege kuhakikisha ndege zinatenganishwa kwa umbali salama na kupewa maelekezo wakati wa kuruka, kutua na kujiendesha katika maeneo wanayoyasimamia.

Tofauti kubwa kati ya wataalamu hawa ni kwamba Air Traffic Controllers huongoza na kuratibu mwendo wa ndege kupitia mawasiliano ya redio na mifumo ya uongozaji, wakati Aircraft Marshallers humwelekeza rubani kwa ishara za kuona katika eneo la maegesho ya ndege.

Pamoja na tofauti hiyo ya majukumu, wataalamu hawa wote ni sehemu muhimu ya mfumo wa usalama wa usafiri wa anga na huchangia kuhakikisha shughuli za ndege zinafanyika kwa mpangilio, usalama na ufanisi.
Nchini Tanzania, Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) ina jukumu la kusimamia na kudhibiti usalama wa usafiri wa anga kwa kuzingatia sheria, kanuni na viwango vinavyotambuliwa kitaifa na kimataifa, ikiwemo miongozo ya Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga, ICAO.

 Chanzo- TCAA

Posted by MROKI On Friday, August 21, 2026 No comments

August 20, 2026






Na Mwandishi Wetu – Iringa
MUFINDI: Wananchi wa vijiji vinavyopakana na Shamba la Miti Sao Hill wilayani Mufindi wameahidi kushirikiana na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika kuzuia na kudhibiti moto wa misitu, baada ya kupatiwa elimu kuhusu matumizi salama ya moto.

Ahadi hiyo imetolewa leo, Agosti 20, 2026, katika mikutano ya uhamasishaji iliyofanyika vijiji vya Bumilayinga na Kisada, Kata ya Bumilayinga, ikiwa sehemu ya kampeni za kila mwaka za kuelimisha jamii kuhusu madhara ya moto na umuhimu wa kulinda misitu na mazingira.

Akizungumza katika mikutano hiyo, Mwakilishi wa Mhifadhi Mkuu wa Tarafa ya Pili ya Shamba Ihefu, SCO Frank Milanzi, amesema wananchi wanaoishi karibu na shamba la miti wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha moto unaotokana na shughuli za kibinadamu hauingii katika misitu.

“Moto unaweza kusababisha madhara makubwa kwa misitu, mali na maisha. Ni muhimu kila mmoja kuhakikisha moto unaotumika kwa shughuli mbalimbali unadhibitiwa na kuzimwa kabisa baada ya matumizi,” amesema.

Mkuu wa Kitengo cha Ulinzi wa Msitu Dhidi ya Moto wa Shamba la Miti Sao Hill, CO I Murya Sawa, amewataka wananchi kuacha kuwasha moto kiholela na kutoa taarifa mapema wanapoona dalili za moto katika maeneo ya misitu.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Bumilayinga, Mhe. Dorian Lyanzile, amesema viongozi wa vijiji na wananchi wanapaswa kuimarisha ushirikiano wao na TFS ili kuhakikisha matumizi ya moto hayahatarishi misitu na mazingira.

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Kisada, Lidia Mwenda, amesema wananchi wamepokea elimu hiyo kwa umuhimu na wako tayari kushirikiana na TFS katika kulinda misitu, akieleza kuwa mikutano hiyo huwasaidia kutambua madhara ya matumizi yasiyo sahihi ya moto.

Mikutano hiyo ni sehemu ya mpango wa TFS kupitia Shamba la Miti Sao Hill kuimarisha ushirikiano na jamii zinazozunguka shamba hilo, ikiwemo vijiji 60 vinavyopakana nalo wilayani Mufindi, kwa kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi katika kuzuia na kudhibiti moto, hasa wakati wa kiangazi.
Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments
NnnMkuu wa Wilaya ya Kiteto akagua miradi ya elimu yenye thamani ya Shilingi bilioni 1.37

Mkuu wa Wilaya ya Kiteto, Mhe. Remidius Mwema,tarehe 17 Agosti 2026  alifanya ziara ya ukaguzi wa miradi mbalimbali katika sekta ya elimu yenye thamani ya jumla ya Shilingi bilioni 1.37, katika Kata za Partimbo, Engusero na Laiseri.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mwema pia alizungumza na wananchi kwa kusikiliza na kutatua kero mbalimbali,akiwa katika Kata ya Laiseri, Mhe. Mwema alishuhudia mapokezi makubwa na bashasha kutoka kwa wananchi kufuatia hatua ya Serikali kutegua kitendawili cha muda mrefu cha ukosefu wa shule ya sekondari katika kata hiyo.

Serikali tayari imeanza ujenzi wa Shule Mpya ya Sekondari Laiseri, ambayo itakuwa shule ya kwanza ya sekondari katika kata hiyo.Mapema akizungumza na wananchi, Mhe. Mwema alisema:

_“Serikali imekata kiu kwa wananchi wa Kata ya Laiseri kufuatia hitaji la shule ya sekondari. Tambueni kwamba vijiji na kata zote zina usawa kimtazamo linapokuja suala la maendeleo ya wananchi, sasa Serikali imetekeleza kwa vitendo. Wito wetu kwenu ni kuendelea kutoa ushirikiano katika kipindi chote cha utekelezaji wa mradi huu,”Alisema.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mwema alitembelea na kukagua maendeleo ya miradi ifuatayo:

Ujenzi wa Shule Mpya ya Sekondari Mbeli – Kata ya Partimbo, wenye thamani ya Shilingi milioni 584.

Ujenzi wa Bweni katika Shule ya Sekondari Engusero, wenye thamani ya Shilingi milioni 204.

Ujenzi wa Shule Mpya ya Sekondari Laiseri, wenye thamani ya Shilingi milioni 584.

Miradi hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuhakikisha wananchi wa maeneo yote wanapata huduma bora za elimu.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Wilaya amesema hakuna Kijiji au kata ambayo inasahaulika linapokuja suala la maendeleo, Ujenzi wa Sekondari Laiseri ilikuwa ni hitaji muhimu na muda mrefu kwa wananchi wa kata  Laiseri, leo Serikali imetekeleza hitaji hili kubwa na itaendelea kugusa maisha ya Wananchi wote Wilayani Kiteto.






 


Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Tanga.
Ajali ya moto iliyotokea usiku wa Agosti 14, 2026, Barabara ya 12, Jijini Tanga, ambayo iliteketeza maduka 12 ya wafanyabiashara, imewaibua Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani humo, ambapo wamefika eneo la ajali na kuwapa mkono wa pole wafanyabiashara hao.

Akizungumzia suala hilo, Agosti 18, 2026, Meneja TRA mkoa wa Tanga, CPA Castro John, amesema wameguswa na tukio hilo la moto kwani wafanyabiashara ni wadau muhimu katika ulipaji kodi nchini.

"Wafanyabiashara wameunguliwa karibu vitu vyao vyote, tumekuja kuwapa pole na kuonyesha mshikamano, pia tumekuja kuwapa kiasi cha fedha kidogo kama kianzio kutokana na wengi wao kupoteza mali zao zote," amesema CPA John.

Ameongeza kuwa, TRA inawajibika si tu kukusanya kodi lakini pia kuwalea wafanyabiashara waweze kustawi na kukua kibiashara, hivyo, wanapopata majanga ya aina hiyo, wanalo jukumu la kuwashika mkono.

"TRA ina jukumu la kukusanya kodi lakini pia kuhakikisha wafanyabiashara wanastawi. Tutawaita waje ofisini tuongee nao na kuona tunawasaidiaje ili wapate unafuu wa kodi," amesema.

Katika hatua nyingine, Katibu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara mkoani humo, Ismail Masoud, amempongeza Meneje TRA mkoa na Kamishna Mkuu kwa kuthibitisha kwa vitendo kuwa wafanyabiashara ni familia moja na TRA.

Pia, ameatoa wito kwa wafanyabiashara wote wa Mkoa wa Tanga kuendelea kulipa kodi kwani kodi hizo ndizo zimesaidia hata kupata misaada hiyo.

Kwa upande wa wafanyabiashara hao, wameushukuru uongozi wa TRA kwa kuwafariji na kuwapa mkono wa pole kwani wapo katika kipindi kigumu kutokana na wengi wao kupoteza mali zao zote.
Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments




Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Ndugu Aggrey Mwanri, amekutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi wa Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) nchini Tanzania, Ndugu Xu Sujiang, huku akisisitiza dhamira ya CCM ya kuendelea kuimarisha uhusiano wa kihistoria na wa kimkakati kati ya vyama hivyo viwili.

Kikao hicho kimefanyika leo Agosti 20,2026 katika Makao Makuu ya CCM, Dodoma, ambapo Ndugu Xu ametumia nafasi hiyo kuaga rasmi kabla ya kuhitimisha majukumu yake nchini Tanzania
Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments



Na, Mwandishi wetu – Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu–Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi, amewataka wananchi kuzingatia tahadhari na maelekezo yanayotolewa na wataalamu na mamlaka husika ili kupunguza madhara yanayotokana na majanga na maafa.

Prof. Kabudi ametoa wito huo tarehe 19 Agosti, 2026 wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Watoa Huduma za Misaada ya Kibinadamu Duniani yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

“Ushiriki wa wananchi ni muhimu katika kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya majanga, huku akiwataka kuendelea kufuata taarifa na maelekezo rasmi kutoka kwa wataalamu na mamlaka zinazohusika na masuala ya maafa.”

Katika hatua nyingine, alisema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema na kujenga ustahimilivu wa jamii ili kuongeza uwezo wa wananchi kukabiliana na majanga na kupunguza madhara yanayotokana na matukio hayo.

Alisema uwezo wa nchi katika kukabiliana na majanga kwa ufanisi unategemea uwepo wa mifumo madhubuti, uratibu na ushirikiano wa karibu na wenye tija kati ya Serikali na wadau wa huduma za kibinadamu.

Prof. Kabudi pia alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake katika kusimamia masuala ya kibinadamu na ustawi wa wananchi.

“Kupitia uongozi wa Rais Dkt. Samia, Serikali imeendelea kuhakikisha wananchi wanaokumbwa na changamoto za majanga wanapata msaada na faraja wakati wa dharura.”

Prof. Kabudi aliwataka watoa huduma za kibinadamu kuwekeza zaidi katika kuwawezesha wananchi kwa elimu na taarifa sahihi kuhusu vihatarishi vinavyowazunguka, pamoja na hatua za kuchukua kabla, wakati na baada ya janga.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Dkt. James Kilabuko, amesema maadhimisho ya siku hiyo yanatoa fursa ya kutambua na kuthamini mchango wa watoa huduma za kibinadamu ambao hujitolea kwa moyo wa huruma, ujasiri na mshikamano katika kuokoa maisha na kupunguza madhara.

Alisema ni muhimu kuendelea kuimarisha ushirikiano na mshikamano miongoni mwa Serikali, wadau wa huduma za kibinadamu na jamii katika kuhakikisha kuwa msaada unapatikana kwa wakati na unawafikia wale wanaouhitaji.

“Ni muhimu kuhakikisha kuwa katika kila hatua ya utoaji wa huduma za kibinadamu, maisha, usalama na utu wa mwanadamu vinaendelea kuwa kiini cha hatua tunazochukua.”
=MWISHO=
Posted by MROKI On Thursday, August 20, 2026 No comments

August 19, 2026






Na. Mwandishi Wetu - Shinyanga
SERIKALI imesema itaendelea kuongeza nguvu katika mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU), kwa kuboresha vituo vya huduma, kuwezesha vikundi na kuimarisha ushirikiano na wadau, ili kuhakikisha Tanzania inafikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dk. Jim Yonazi, wakati wa ziara yake mkoani Shinyanga, ambapo alitembelea vikundi mbalimbali vya vijana vinaoishi na Maambukizi ya VVU pamoja na Kituo cha Maarifa Kahama kilichopo Kagongwa mkoani humo.

Dk. Yonazi amesema juhudi zinazofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau zimeanza kuzaa matunda, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza kasi katika utoaji wa elimu, upimaji, ushauri nasaha, pamoja na huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.

“Lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma karibu nao, lakini vilevile wanapata elimu inayowasaidia katika mapambano dhidi ya UKIMWI
na maambukizi ya UKIMWIi,” amesema.

Amesema Serikali imeendelea kuboresha huduma hizo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa wakati, huku akiwataka wadau kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha afua za kukabiliana na VVU.

Dkt. Yonazi amepongeza Mkoa wa Shinyanga kwa kufikia malengo ya kimataifa ya 95-95-95, akisema hatua hiyo ni ishara ya mafanikio katika jitihada za kupunguza maambukizi mapya na madhara yatokanayo na VVU.

“Serikali imeamua kwa makusudi kabisa kuongeza nguvu yake. Ndiyo maana imeanzisha Mfuko wa Mfadhili, na asilimia 70 ya fedha hiyo inakwenda katika Mfuko wa UKIMWI ili kusaidia afua mbalimbali na kuondokana na utegemezi,” amesema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Mhe. Mbona Mahita, alisema mkoa huo bado una kiwango cha maambukizi ya VVU kilicho juu ya wastani wa kitaifa, ambapo Shinyanga ina asilimia 5.6 ikilinganishwa na asilimia 4.4 ya kitaifa.

Mahita alisema Serikali imeendelea kuongeza elimu kuhusu VVU katika ngazi mbalimbali, kuanzia kaya hadi jamii, ili wananchi wawe na uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kujikinga na maambukizi.

“Shinyanga ni business hub kwa Kanda ya Ziwa. Movement za watu mara kwa mara ni kubwa. Watu wanaoingia na kutoka ni wengi, ndiyo maana tumeshuka mpaka kwenye ngazi za kijamii katika utoaji wa elimu,” alisema.

Awali, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Dk. Honoratha Rutatinisibwa, alisema mkoa huo una vituo 374 vinavyotoa huduma za afya, ambapo vituo 120, sawa na asilimia 32, vinatoa huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.

Dkt. Rutatinisibwa amesema, kwa mujibu wa utafiti wa maambukizi ya VVU uliofanyika mwaka 2023, kiwango cha maambukizi mkoani Shinyanga ni asilimia 5.6, ikilinganishwa na wastani wa kitaifa wa asilimia 4.4.

Akizungumzia huduma zinazotolewa katika Kituo cha Maarifa Kahama kilichopo Kagongwa, Mratibu wa Kudhibiti Maambukizi ya VVU, Homa ya Ini na Magonjwa ya Ngono Kahama, Dkt. Herry Silvester, amesema kituo hicho kinatoa huduma za tiba na matunzo, pamoja na huduma maalumu kwa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi.

Amesema makundi hayo ni pamoja na madereva wa masafa marefu, mabinti na wanawake vijana, ambao wamekuwa wakifikiwa kupitia huduma za upimaji, elimu na ushauri nasaha.
Posted by MROKI On Wednesday, August 19, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu
Ushirikiano baina ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), umeelezwa kuwa na manufaa mengi yenye mchango wa kukuza maendeleo baina ya nchi hizo mbili. 

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu (MCC), Mary Chatanda, Agosti 18, 2026.

Chatanda amesema, ziara ya siku mbili ya Rais Felix Tshisekedi wa DRC Kongo nchini Tanzania ni kielelezo cha uhusiano mzuri ambao hauishii kuwa urafiki wa kawaida bali nyenzo ya kushirikiana katika kukuza uchumi na maendeleo.

"Rais Dk. Samia na mwenzake Tshisekedi wamekubaliana kushirikiana katika kuboresha sekta za uchukuzi, madini, nishati, uwekezaji, biashara, barabara, bandari, usafiri wa majini, jambo linaloongeza kasi ya ukuaji uchumi," amesema.

Aidha, Chatanda amehimiza uzingatiaji wa maslahi ya wananchi katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa nchi zote.

"Wananchi wetu wanapaswa kunufaika na fursa za uchumi katika sekta za ushirikiano, ili maendeleo yawe jumuishi kwa serikali na wananchi wake," amesisitiza.

Katika hatua nyingine, Chatanda amempongeza Rais Dk. Samia kwa kuendelea kuifungua nchi kwa kuhimiza diplomasia ya kiuchumi kwa kushirikiana na mataifa mbalimbali duniani.

"Nampongeza Rais wetu Dk. Samia kwa namna anavyoshirikiana na mataifa mengine, kwa kufanya hivyo, tunaongeza wigo wa kupata fursa za biashara na uwekezaji," ameongeza.
Posted by MROKI On Wednesday, August 19, 2026 No comments

August 18, 2026








Na. Mwandishi Wetu, Mwanza
Serikali imedhamiria kuendelea kuimarisha afua za masuala ya UKIMWI nchini kwa kuboresha mazingira ya utekelezaji wa shughuli hizo, huku ikihimiza ushirikiano na wadau mbalimbali katika kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, alipotembelea na kujionea utekelezaji wa shughuli zinazotekelezwa na vikundi vya watu wanaoishi na Maambukuzi ya Virusi vya UKIMWI katika Wilaya ya Nyamagana, Jijini Mwanza.

Akiwa katika ziara hiyo, Dkt. Yonazi amesema Serikali imeendelea kuboresha mazingira na kutenga bajeti inayosaidia kuratibu na kutekeleza afua za masuala ya UKIMWI nchini, huku ikishirikiana na wadau mbalimbali.

“Ushirikiano ni muhimu sana kwani, tunaamini unauwezo wa kutuvusha katika mapambano dhidi ya VVU, ambapo tumeendelea kuunganisha nguvu pamoja katika mapambano hayo,” alisema Dkt. Yonazi.

Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu, yenye dhamana ya kuratibu shughuli zote za Serikali, ikiwemo masuala ya UKIMWI, itaendelea kuhakikisha vifaa na huduma zinatolewa kwa wakati na ubora kwa WAVIU, huku kanuni na taratibu za afya zikizingatiwa.

Dkt. Yonazi Ametumia jukwaa hilo kuiasa jamii kuendelea kupima afya ili kujitambua na kuchukua hatua za mapema endapo mtu atabainika kuwa na maambukizi ya VVU, ili aweze kuishi kwa tahadhari na kuwalinda wengine.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Ndugu Balandya Elikana, amesema kuwa mkoa umechukuwa hatua madhubuti kuimarisha mapambano dhidi ya UKIMWI kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya afya na kamati za utekelezaji wa mikakati ya kuzuia maambukizi, huku wakihimiza upatikanaji wa huduma bora na elimu kwa jamii. 

“Jamii inaendelea kuhamasishwa kuhusu upimaji wa afya kwa hiari na matumizi sahihi ya njia za kujikinga na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI pamoja na kuendelea kushirikiana kwa karibu na mashirika na wadau wa afya ili kuboresha huduma za kinga na tiba,” alisema Elikana

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dkt. Kheri Kagya, akiwasilisha taarifa ya hali ya UKIMWI mkoani humo, amesema Mkoa wa Mwanza una kiwango cha maambukizi ya VVU cha asilimia 4.7, ikilinganishwa na kiwango cha kitaifa cha asilimia 4.4, kwa mujibu wa matokeo ya Utafiti wa Kitaifa wa THIS 2022/2023.

Alisema kwa mujibu wa taarifa ya DHIS2 Annual Report ya mwaka 2025/2026, Mkoa wa Mwanza unakadiriwa kuwa na idadi ya watu wanaoishi na VVU (WAVIU) 112,685.

“Mkoa, kwa kushirikiana na wadau, umeendelea kutoa elimu ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya VVU kwa kuhamasisha matumizi sahihi ya kondomu. Katika kipindi cha mwaka 2025/2026, Mkoa ulisambaza jumla ya kondomu 2,265,772 katika jamii, hususani sehemu za kulala wageni, sehemu za kuuzia vileo (baa), kumbi za starehe na kwenye mikusanyiko mbalimbali,” alisema.
Posted by MROKI On Tuesday, August 18, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo