Nafasi Ya Matangazo

August 31, 2026

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) Mhe. Deus Sangu akiteta jambo na  Sheikh Mkuu wa Jumuiya ya Waithna’ashariyyah Tanzania (TIC) Sheikh Hemed Jalala (Kushoto) Pamoja na Mwenyekiti wa Taifa wa Jumuiyah ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) Sheikh Alhad Mussa Salum (Kulia) katika hafla ya kumbukizi ya mazazi ya Mtume Muhammad (Sallallahu Alayhi Wasallam) iliyofanyika Agosti 30,2026 katika uwanja wa Kigogo Posti, Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) Mhe. Deus Sangu akiteta jambo na  Sheikh Mkuu wa Jumuiya ya Waithna’ashariyyah Tanzania (TIC) Sheikh Hemed Jalala (Kushoto) Pamoja na Mbunge wa Jimbo la Kinondoni Mhe. Abbas Tarimba (Kulia) katika hafla ya kumbukizi ya mazazi ya Mtume Muhammad (Sallallahu Alayhi Wasallam) iliyofanyika Agosti 30,2026 katika uwanja wa Kigogo Posti, Jijini Dar es Salaam.
**************
Na: OWM (KAM), Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu ametoa wito kwa wananchi na Taasisi za dini kuendelee kushirikiana na Serikali katika kudumisha amani, upendo, umoja na mshikamano, akisisitiza kuwa misingi hiyo ni nguzo muhimu katika kujenga Taifa imara.

Aidha, pia amewasihi kuhusu suala la malezi bora na uadilifu kwa watoto na vijana ili kuepuka athari za mmomonyoko wa maadili pamoja na kutokomeza ukatili dhidi ya watoto, kwa lengo la kujenga kizazi kijacho chenye maadili na upendo.
 
Mhe. Sangu ametoa wito huo (Jumapili, Agosti 30, 2026) alipomwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba katika hafla ya kumbukizi ya mazazi ya Mtume Muhammad (Sallallahu Alayhi Wasallam) iliyofanyika katika uwanja wa Kigogo Posti, Jijini Dar es Salaam.

Amesema Serikali inatambua mchango wa Taasisi za Dini katika kuimarisha mshikamano wa kijamii; kukuza maadili ya uadilifu, uwajibikaji na upendo; kutoa huduma za kijamii kama vile elimu, afya na msaada wa kijamii pamoja na kuelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa amani na mshikamano wa kitaifa.

“Serikali inatambua nafasi ya Jumuiya ya Waithna’ashariyyah Tanzania (TIC), ikiongozwa na Sheikh Mkuu wa TIC Maulana Sheikh Hemed Jalala na taasisi zote za dini katika kuimarisha mahusiano mema, amani na utuivu,” amesema

Kadhalika, ametoa wito kwa waumini wa dini ya kiislamu kuyashika na kuyaishi kwa vitendo mafundisho na Maisha ya Mtume Mohammad (S.A.W) dini hususan katika kuimarisha maadili, upendo, amani na mshikamano katika jamii ili kujenga Taifa lente maadili mema na uwajibikaji.

Kwa upande mwengine, Waziri Sangu amewasilisha salamu za Sikukuu ya Maulid kutoka kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba na pia kuwapongeza kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kudumisha Amani, mshikamano na umoja wa kitaifa.

Pia, Sheikh Mkuu wa Jumuiya ya Waithna’ashariyyah Tanzania (TIC) Sheikh Hemed Jalala,ameishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa nia njema ya kushiriki katika Sherehe za Maulid, akisema ushiriki huo ni ishara ya ushirikiano mzuri kati ya Serikali na jamii. Aidha, upendo na Huruma ndo Mafunzo ya Mtume Muhammad (S.W.W) ampapo amezitaka taasisi zote za dini kuendeleza juhudi za kuwaleta pamoja waumini na wasiokuwa waumini kupitia mihadhara na shughuli mbalimbali za kidini zinazolenga kumuenzi na kumsifia Mtume Muhammad (S.W.W), huku akisisitiza umuhimu wa mshikamano na umoja katika jamii.
Posted by MROKI On Monday, August 31, 2026 No comments
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi, pamoja na familia yake wameungana na waumini mbalimbali katika kushiriki Ibada ya Misa Takatifu ya Jumapili, katika Kanisa Katoliki, Parokia ya Paulo wa Msalaba Jimbo Kuu Katoliki Dodoma. Tarehe 30 Agosti 2026.











Posted by MROKI On Monday, August 31, 2026 No comments
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akimpongeza Askofu Jimbo la Mpanda Eusebius Nzigilwa baada ya kuzungumza katika Ibada ya Misa ya Jubilei ya miaka 25 ya Jimbo hilo leo tarehe 30 Agosti, 2026. 
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza katika Jubilee ya miaka 25 ya Jimbo Katoliki la Mpanda zilizofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari Saint Mary’s  mjini Mpanda, Agosti 30, 2026.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza katika Jubilee ya miaka 25 ya Jimbo Katoliki la Mpanda zilizofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari Saint Mary’s  mjini Mpanda, Agosti 30, 2026.
******************
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu taasisi za dini likiwemo kanisa Katoliki katika kuimarisha huduma za kijamii, maendeleo na ustawi wa wananchi, akisisitiza kuwa mchango wa taasisi za dini ni sehemu muhimu ya safari ya maendeleo ya Tanzania.

Dkt. Mwigulu ameyasema hayo leo Jumapili, Agosti 30, 2026, katika maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 25 ya Jimbo Katoliki la Mpanda, yaliyofanyika mkoani Katavi, ambapo amesema Serikali inatambua mchango wa Kanisa Katoliki katika maendeleo ya nchi, hususan katika sekta za elimu, afya na huduma za kiroho.

 “Serikali inatambua mchango wa Kanisa na baba Askofu. Kila tunapotaja maendeleo ya nchi yetu, kuanzia mwanzo mpaka hapa tulipofika, hatuwezi kuyataja kwa kina maendeleo hayo bila kutaja mchango wa Kanisa.”

Amesema ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa umeendelea kuwa muhimu katika kuhakikisha huduma za kijamii na shughuli za maendeleo zinaimarika, akisisitiza kuwa milango ya Serikali itaendelea kuwa wazi kwa Kanisa na taasisi nyingine za dini katika masuala yanayolenga ustawi wa wananchi.

 “Niwahakikishie Serikali itaendelea kushirikiana na Kanisa na popote pale mlipo na jambo msisite, milango yetu iko wazi ili tuweze kuhakikisha kwamba tufanye jambo lolote linalotufurahisha.”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ametoa maelekezo kwa viongozi wa Mkoa wa Katavi na mamlaka husika kuharakisha utekelezaji wa miradi ya barabara, maji na umeme, akisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kupata huduma hizo kwa wakati.

Amesema maandalizi ya kukabiliana na uwezekano wa kutokea kwa El Niño yanapaswa kwenda sambamba na hatua za vitendo, ikiwemo ujenzi na uboreshaji wa mifereji na madaraja ili kupunguza athari za mafuriko.

Kuhusu huduma za maji, Waziri Mkuu ameitaka Wizara ya Maji na wahusika wa mradi wa maji Mpanda kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo ifikapo Desemba 2026, huku akisisitiza pia kuharakishwa kwa miradi ya barabara inayounganisha Katavi na mikoa jirani.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua za kuboresha mazingira ya haki kwa wananchi, akitangaza kuwa Serikali inaelekea kufuta sheria inayohusu utaifishaji wa mifugo, akieleza kuwa hatua hiyo inalenga kuondoa changamoto za wananchi kunyang’anywa mifugo yao.

 “Katika Bunge hili linaloendelea tunakwenda kufuta sheria ya utaifishaji wa mifugo... kumekuwepo na majeraha makubwa ya watu kunyang’anywa katika baadhi ya maeneo. Tunataka tuondoe hayo ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanaepukana na hayo.”

Pia ametoa maelekezo kwa wasimamizi wa sheria kuacha kukamata vitendea kazi vya wananchi kama pikipiki, bajaji na magari katika utekelezaji wa sheria za makosa mbalimbali, akisisitiza umuhimu wa kutumia utaratibu wa kisheria wa adhabu na faini.

Kwa upande wake, Askofu wa Jimbo Katoliki la Mpanda, Mhashamu Baba Askofu Eusebius Nzigilwa, amemshukuru Waziri Mkuu kwa kutenga muda na kushiriki katika maadhimisho hayo, akisema uwepo wake umeonesha heshima na kuthaminiwa kwa Jimbo la Mpanda na Kanisa Katoliki Tanzania.

 “Ninakushukuru sana. Tunaona hiyo ni heshima kwa Jimbo letu na kwa Kanisa Katoliki Tanzania, na hivyo tunaomba Mwenyezi Mungu azidi kuwaongoza na kuwajalia neema na hekima katika kutuongoza sisi raia na wananchi wenu.”

Naye Balozi wa Baba Mtakatifu nchini Tanzania anayemaliza muda wake, Mhashamu Askofu Mkuu Angelo Accattino, amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa Katoliki, akisema ushiriki wa viongozi wa Serikali na viongozi wa dini mbalimbali katika maadhimisho hayo ni ishara ya mahusiano mema kwa ajili ya ustawi wa jamii.

Maadhimisho hayo yamefanyika katika kuadhimisha miaka 25 tangu kuanzishwa kwa Jimbo Katoliki la Mpanda mwaka 2001, huku viongozi wa Kanisa wakieleza kuwa katika kipindi hicho Jimbo limepiga hatua katika huduma za kichungaji, elimu, afya na ujenzi wa miundombinu kwa ajili ya jamii.

Waziri Mkuu amewapongeza viongozi wa Kanisa, waamini na wananchi wa Jimbo Katoliki la Mpanda kwa kufanikisha Jubilee hiyo, akiwataka kuendelea kushirikiana na Serikali katika kujenga jamii yenye amani, mshikamano na maendeleo.

Watoto wa Shirika la Mtakatifu PMS Jimbo Katoliki Mpanda wakiimba katika Ibada ya Misa ya Jubilee ya miaka 25 ya Jimbo hilo kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari ST.  Mary’s mjini Mpanda, Agosti 30, 2026. 
 Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akimtuza mtoto Ritha Msangama aliyekuwa akiimba pamoja na Watoto wa Shirika la Mtakatifu PMS jimbo la Mpanda ikiwa ni moja ya shamrashamra za Jubilee ya miaka 25 ya Jimbo Katoliki Mpanda kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari  ST. Mary’s mjini Mpanda, agosti  30, 2026.



Posted by MROKI On Monday, August 31, 2026 No comments

August 30, 2026





Na WMA  -  Mwanza
Banda la Wakala wa Vipimo (WMA) limeendelea kuvutia makundi mbalimbali ya wananchi katika Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yanayoendelea katika Viwanja vya Furahisha jijini Mwanza, ikiwa ni siku ya tatu, Agosti 30, 2026.

Makundi hayo yameonesha kuvutiwa na elimu ya vipimo tofauti tofauti.

Wakiwa bandani hapo, wengi wa wanafunzi na vijana wameonesha kuvutiwa zaidi na elimu ya matumizi  ya mizani za kielektroniki na pampu za kupimia mafuta.

 Wamesema elimu hiyo inawapa uelewa wa kuwa mabalozi wa vipimo shuleni na majumbani mwao huku wengine wakidai ndoto yao ni kuwa Maafisa Vipimo wa baadae.

Kwa upande wa akina mama wajasiriamali, wengi  wamejikita kujifunza kuhusu matumizi sahihi ya mizani  inayotumika masokoni na waliuliza maswali mengi kuhusu namna ya kutambua ujazo wa mtungi wa gesi ya kupikia wanapoenda kununua.

 Wengi wameipongeza WMA kwa kuwaelimisha jinsi ya kuepuka hasara na kuhakikisha mteja anapata haki yake.

Askari na wazee waliotembelea Banda la WMA wameonesha kuvutiwa na elimu ya vipimo katika sekta ya mafuta ya petroli, saruji na bidhaa nyingine za ujenzi. Askari wamesema elimu hiyo itawasaidia katika doria za kuhakikisha biashara inafanyika kwa haki, wakati wazee wamesema wamepata uelewa mpya wa kulinda familia zao dhidi ya udanganyifu.

Wananchi wote waliotembelea banda hilo wamepongeza Serikali kwa kuona umuhimu wa kuwa na Wakala wa Vipimo nchini. Wamesema uwepo wa WMA umesaidia kulinda haki za walaji na kuweka mazingira bora ya biashara yanayosadifu kaulimbiu ya maonesho isemayo “Usalama na  Amani ni Kichocheo cha Biashara na Uwekezaji".
Posted by MROKI On Sunday, August 30, 2026 No comments

August 28, 2026

Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali inaendelea kutoa elimu kuhusu majukumu mbalimbali yanayotekelezwa na Mamlaka hiyo hususan katika uchunguzi wa kimaabara wa Dawa Asili kwa wadau wa Tiba Asili katika maadhimisho ya wiki ya Tiba Asili ya Mwafrika yanayofanyika katika viwanja vya Uhindini mkoani Mbeya.








Posted by MROKI On Friday, August 28, 2026 No comments
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imejipanga vema kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza wakati wa mvua kubwa za El Niño zinazotarajiwa kuanza mwezi ujao hasa katika maeneo yanayopata mvua nyingi.

 

Ametoa kauli hiyo Bungeni jijini Dodoma, leo (Alhamisi, Agosti 27, 2026) wakati akijibu swali la Mbunge wa Bukoba Mjini, Mha. Johnston Mutasingwa, kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu aliyetaka kujua Serikali imejipangaje kukabiliana na changamoto ya uharibifu wa miundombinu ya barabara na makazi ya wananchi kulingana na tahadhari ambayo imetolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini (TMA) juu ya uwepo wa El-Nino yenye nguvu.

 

“Ni kweli tumepata tahadhari kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini juu ya uwepo wa mvua kubwa za El-Nino na hasa kwenye mikoa ya Kanda ya Ziwa ambako mvua hizo zinatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi Septemba ama Oktoba mwanzoni. Serikali imejipanga kwa kuandaa mifereji katika maeneo hayo ili kuondoa uwezekano wa maji kurundikana.”

 

Waziri Mkuu amesema Serikali imeelekeza TANROADS na TARURA zifanye ukaguzi wa barabara, madaraja, makalavati na mifereji ya maji ili kubaini mapema maeneo korofi yanayoweza kuathiriwa ili kuhakikisha wananchi hawakosi miundombinu kutokana na mafuriko.

 

“Bunge lako tukufu lilielekeza fedha za mifuko ya barabara ziwe zinakwenda moja kwa moja kwenye mifuko ya barabara badala ya Serikali kuu. Nimpongeze Waziri wa Fedha pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa kuanza kutekeleza uamuzi huo ambapo kwa mwezi zaidi ya sh. bilioni 320 zinaenda moja kwa moja kweye mifuko na kuiwezesha kukabiliana na mambo kama haya,” amesema.

 

Amewataka Watanzania wachukue tahadhari kwa kila mmoja kufanya tathmini ya mahali wanapoishi kwa kuangalia mazingira ya mahali walipo kwani wanajua ni wapi maji huwa yanapita au yanatuama. “Tuendelee kuchukua hizo tahadhari ili maafa yasitokee ilhali tumeshatahadharishwa,” amesisitiza.

 

 

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amempongeza Deogratius John Ndejembi kwa kuaminiwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Kamati Kuu ya CCM na Halmashauri Kuu ya CCM na kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

 

Dkt. Mwigulu ameitumia nafasi hiyo pia kumpongeza Rais Samia kwa kuwa na jicho la kipekee hadi akamuona Mheshimiwa Ndejembi. Amesema kiongozi huyo anazo sifa zinazomfanya astahili kupewa dhamana hiyo kubwa ya kitaifa.

 

“Mheshimiwa Naibu Spika, Deogratius Ndejembi ni kiongozi mahiri sana, ni kiongozi makini, ni kiongozi mchapakazi anayefanya kazi bila kuchoka ili Watanzania waweze kupata manufaa. Ndejembi pia ana sifa za unyenyekevu na upole, ni mtu rahimu asiye na hiana ndani yake,” amesema.

 

Waziri Mkuu amemhakikishia Mheshimiwa Ndejembi kuwa yeye pamoja na mawaziri wenzake wako tayari kushirikiana naye wakati akitekeleza majukumu yake mapya katika kuijenga Tanzania.

Posted by MROKI On Friday, August 28, 2026 No comments
Posted by MROKI On Friday, August 28, 2026 No comments
Posted by MROKI On Friday, August 28, 2026 No comments
Wanachama waliohitimu pamoja na familia zao kwenye mahafali ya Awamu ya Pili, Mapigano, Ulyankulu, tarehe 21 Agosti 2026.

Mradi wa DREAMS Tanzania ulianza ukiwa na lengo la kuthibitisha kwamba kaya maskini zaidi zinaweza kujenga biashara zinazodumu. Ndani ya siku nne za mwezi Agosti, kaya 1,356 zilizohitimu zilitoa ushahidi.


ULYANKULU, MKOA WA TABORA, TANZANIA · AGOSTI 2026.

Mwezi Februari 2025, maafisa wa mradi walipita nyumba kwa nyumba katika vijiji vinne vya eneo hili la mkoa wa Tabora. Walikuta kwamba asilimia 14 tu ya kaya maskini zaidi zilikuwa zinaishi kwa zaidi ya dola tatu kwa siku. Baada ya miezi 12 ya utelekelezaji wa mradi, idadi hiyo ilikuwa imefika asilimia 82.75.

Mahafali mawili yaliyotenganishwa na siku tatu yalionesha mabadiliko hayo. Chini ya hema pale Mapigano siku ya Ijumaa tarehe 21 Agosti, kaya 762 kutoka Mbeta, Mapigano na Taba zilipokea vyeti vyao kutoka kwa Jumanne Singani, mkuu wa makazi ya Ulyankulu. Pale Sasu siku ya Jumatatu tarehe 24 Agosti, kaya nyingine 594 zilipokea vyao, huku Mkuu wa Wilaya ya Kaliua akiwa mgeni rasmi. Viongozi wa vikundi walipanda mmoja mmoja kupeana mikono mezani kuu, kuchukua cheti na kusimama kwa ajili ya picha. Kwaya ziliimba, vikundi vya biashara vilitandika mazao, kuku na mchele uliokobolewa, na kila mradi ulipotajwa umati ulijibu jambo lilelile: ongeza kipato cha familia.

Jumanne Singani, mkuu wa makazi ya Ulyankulu na mgeni rasmi, akizungumza na wahitimu kutoka meza kuu pale Mapigano.

Kwa pamoja kaya hizo 1,356 ndio Awamu ya Pili, na zote ziliingia kwenye mradi zikiwa miongoni mwa kaya maskini zaidi ndani ya makazi. Mradi huu unaitwa DREAMS Tanzania, na upo ili kujibu swali ambalo mashirika ya maendeleo yameshughilika nalo kwa miongo mingi: je, familia zilizo kwenye umaskini uliokithiri zinaweza kuingizwa kwenye uchumi wa kudumu, au msaada huishia kupotea tu mara mradi unapoondoka?

DREAMS, au Delivering Resilient Enterprises and Market Systems, unaongozwa na Mercy Corps kwa kushirikiana na Village Enterprise, Caritas Tabora na shirika la msaada wa kisheria la Dignity Kwanza. Utaendelea hadi Desemba 2027, unalenga kujenga uwezo wa kujitegemea kwa watu 150,000 katika makazi ya Ulyankulu, Mishamo na Katumba pamoja na vijiji vinavyozunguka hayo makazi, ambako Watanzania waliopewa uraia na vijiji vinavyowazunguka wanaishi bega kwa bega. Hadi sasa umewafikia watu 140,414.

JINSI MRADI UNAVYOFANYA KAZI

Mbinu yenyewe ni ya polepole kwa makusudi. Hakuna anayekabidhiwa pesa siku ya kwanza. Maafisa hupita kwanza kila kaya katika kijiji kilichochaguliwa wakiwa na dodoso la kupima hali ya umaskini, Poverty Probability Index (PPI), na majibu ndiyo yanayoamua nani anastahili. "Hatukai chini ya mti na mwenyekiti tukamuuliza nani maskini hapa," anasema January Julius Nyanda, anayesimamia timu za uwandani kwa upande wa Caritas Tabora. "Angetutajia majina ya ndugu zake wote."

Katika Awamu ya Pili, kaya 1,670 zilikidhi vigezo na kaya 1,356 zikajiunga. Zilipitia mada tisa za mafunzo kuhusu uendeshaji wa vikundi, elimu ya fedha na ujasiriamali, kisha zikaunda vikundi vya kuweka akiba na kukopeshana vya wanachama thelathini hadi arobaini na tano, pamoja na vikundi vya biashara vya kaya tatu tatu. Ndipo pesa ilipofika: shilingi 533,820 kwa kila kikundi, na mgao wa pili wa shilingi 228,720 baada ya miezi sita, jumla ya shilingi milioni 344.4 katika biashara 452.

Kikundi cha biashara kikionesha bidhaa zake kwenye mahafali: miche ya sabuni, sahani zilizopangwa, nyanya na kabichi.

Fredrick Kumbule Modestus, aliyewashauri takribani washiriki 150, anakumbuka waziwazi walipoanzia. "Mtu alikuwa anapata shilingi elfu kumi bila kuwa na wazo kwamba angeweza kutumia elfu saba na kubakiza elfu tatu," anasema. "Wazo la biashara halikuwepo kabisa."

Si kila mtu alijiunga mwanzoni. Zilienea tetesi kwamba mtaji ungerudishwa baadaye, kwa ardhi au kwa mifugo, na baadhi walikaa pembeni mpaka walipoona vikundi vya kwanza vikinufaika.

MWAKA MMOJA UMEZAA NINI

Utafiti wa mwisho, uliofanywa na Caritas Tabora awamu ilipomalizika, ulionesha wastani wa mali za kaya umepanda kutoka dola 260 hadi dola 955, na matumizi kwa kila mtu kutoka dola 164 hadi dola 453. Kaya zinazoweka akiba mara kwa mara zilipanda kutoka asilimia 3.5 hadi asilimia 99.7, na asilimia 91.8 ya biashara zilipimwa kuwa zenye afya wakati wa kuhitimu.

John Brighton Mwangolela ni mkulima wa kitongoji cha Itagwa, kilichoko Sasu. Kwenye mahafali ya Jumatatu alizungumzia mafanikio waliyopata katika kikundi chao;

"Tulianza na mbuzi wanne. Mwisho wa mwaka tukawa na mbuzi kumi na sita. Tukagawana mbuzi mmoja mwenye mimba kila mmoja, na wale kumi na watatu waliobaki tukawauza tukanunua ng'ombe jike mwenye mimba. Hivi ninavyosimama hapa, ana wiki tangu amezaa, na sasa tunakunywa maziwa yake."
John Brighton Mwangolela
Mhitimu, kitongoji cha Itagwa, Sasu

Antonet Yohana ni mwenyekiti wa kikundi cha kuweka akiba cha Muungano kilichoko Taba, ambacho hununua mpunga, hukikoboa na kuuza mchele kwa kupima. Mwezi aliouchagua ni Januari, wakati ada za shule zinapofika na wazazi walipokuwa wanakopa kwa wenye pesa kwa riba aliyoiita nusu kwa nusu. Sasa kikundi chake kinawakopesha wanachama wake wenyewe kwa riba nafuu.

SHERIA ILIBADILISHA NINI

Pesa huleta matatizo yake yenyewe, na ndiyo maana shirika la msaada wa kisheria lipo ndani ya muungano huu wa mashirika. Ulyankulu ni ardhi tengefu na haiwezi kununuliwa wala kuuzwa ndani ya makazi, hivyo kipato kinapopanda ni lazima kiambatane na uelewa wa mahali ambapo ardhi inaweza kununuliwa kihalali. Masala Johnson, afisa wa masuala ya kisheria wa mradi, pia amewasaidia wanachama kupata vyeti vya kuzaliwa kwa watoto wanaojiunga na kidato cha tano, na namba za utambulisho wa taifa, ambazo bila hivyo hakuna akaunti ya benki inaweza kufunguliwa.

Timu yake ilifanya kazi kwenye mazingira magumu. "Awali tulipoingia kwenye mradi huu, kulikuwa na matukio mengi ya ukatili wa kijinsia yakiripotiwa ndani ya nyumba, ikiwemo wanaume kutowaruhusu wake zao kuhudhuria mafunzo ya biashara," anasema. "Sasa wapo wanaume wanaotoa ushuhuda kwamba wamewaruhusu wake zao kufanya biashara."

Kwa Mwangolela, masomo ya sheria yalibadilisha namna kijiji chake kinavyozungumzia mabinti.

"Akizaliwa mtoto wa kiume tulisema tumepata mchungaji wa mifugo, na akizaliwa wa kike tulisema tumepata mahari kubwa. DREAMS walitufundisha sheria na wakatufundisha madhara yake. Nenda Itagwa sasa. Shule yetu imejaa watoto kwa sababu ya DREAMS."
John Brighton Mwangolela

MASOKO YENYE SABABU ZAKE ZA KUBAKI

Kinachotofautisha DREAMS na mradi wa kugawa ruzuku ni kinachotokea pale biashara zinapokuwa zimeshaanza. CRDB Bank Foundation ilihamisha pesa kutoka kwenye masanduku na kuiingiza kwenye akaunti takribani 708 katika eneo la Ulyankulu pekee, KickStart International inasambaza pampu za umwagiliaji, SimuSolar inatoa mashine za kusaga na za umwagiliaji zinazotumia nishati ya jua kwa mkopo usio na riba, na AKM Glitters inatoa vifaranga vya siku moja. Mgarang'ombe Traders, wanaokoboa mpunga, walijiunga ili kuimarisha mnyororo wa thamani wa zao la mpunga, nao wakapata kitu.

"Mimi ni mfanyabiashara wa muda mrefu, lakini nilikuwa sina elimu ya biashara. DREAMS walitufundisha, na wakatuomba tuwafikishie wakulima tunaowanunulia mazao. Sasa wanazalisha mchele bora kabisa wa grade A na grade B."
Peter Maganga Mapembe
Wakala, Mgarang'ombe Traders, kata ya Makingi

Kwa mradi mzima, kila dola moja ambayo DREAMS inawekeza imeambatana na dola 4.83 za mtaji wa sekta binafsi.

Kikundi bora cha kuweka akiba katika kila kijiji kilipewa viti hamsini vya plastiki badala ya pesa taslimu, kwa sababu katika vijiji, kila harusi na kila msiba unahitaji viti, viti vinaweza kukodishwa.

KINACHODUMU

Hata zawadi zilibeba mantiki ya mradi. Ili kikundi kistahili kupata viti, kila mwanachama alipaswa kuwa ameweka akiba isiyopungua shilingi 250,000 katika mzunguko wa wiki 52. Pale Sasu zawadi ilikwenda kwa kikundi cha Maboresho, kilichokuwa kimeweka shilingi 12,882,000.

Vyeti vina uzito zaidi. DREAMS hufanya kazi kupitia viongozi wa wilaya badala ya kuwazunguka, na pale Sasu Mkuu wa Wilaya ya Kaliua aliwaambia wahitimu kwamba halmashauri hutenga asilimia kumi ya mapato yake kwa ajili ya mikopo ya vikundi, akiwaagiza watumishi wake kuvipa kipaumbele vikundi vyenye vyeti vya DREAMS. "Cheti hicho kimesajiliwa na halmashauri na kinatambulika nayo," Martin Mgallah, meneja msaidizi wa mradi, aliwaambia. "Wenyeviti, kitunzeni. Ndiyo uhai wa kikundi chenu."

Martin Mgallah, meneja msaidizi wa mradi wa DREAMS Tanzania.

Sehemu nyingine za mpangilio wa mradi zinaelekea upande huohuo. Vikundi vya kuweka akiba vinamilikiwa na wanachama wenyewe na havihitaji pesa kutoka nje ili viendelee kufanya kazi, kila biashara ni mali ya kaya tatu badala ya kaya moja, na maafisa wa wilaya wanashikilia kumbukumbu za kila kikundi.

Awamu ya Kwanza ndiyo mtihani halisi wa kwanza. "Tuliwaaga mwaka mmoja uliopita," alisema Mgallah. "Tumetembelea biashara zao jana. Bado wanafanya biashara na wanaendelea kufanikiwa." Mmoja wao ni Abraham Mgaywa wa Makingi, aliyekuwa na familia kubwa na hakuwa na kipato cha kukidhi mahitaji yake wakati dodoso lilipomfikia. Sasa anajiita Mabala the Farmer, na mwezi huu amesafirisha maroli mawili ya matikiti kwenda Dodoma wakati bei ilipokuwa juu kabisa.

Awamu nyingine nne zinaendelea na mafunzo nyuma ya Awamu ya Pili, jumla ya kaya 5,245, na mwakani maafisa watakuwa milangoni Mkindo, Makonge, Kaswa, Usigara, Keza na Ikonongo. Obed Method Bujoro, mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Mapigano, anataka warudi kijijini kwake. Ameona jambo ambalo hakuna utafiti ungeliweza kuligundua: watoto wa kaya zenye shida walikuwa wakitokea milangoni kwa majirani wakati wa chakula, na hilo limekoma.

Wahitimu na watumishi wa DREAMS wakicheza mwishoni mwa mahafali.

Anastazia Paulo Makula alisoma risala ya wahitimu pale Sasu. Alijiunga bila mtaji wowote, akajiwekea lengo la kuweka akiba kwa muda wa miezi mitatu, na kwa pesa iliyopatikana akafungua duka la nguo za watoto. Muhtasari wake ndio uliokuwa mfupi kuliko yote siku hiyo.

"Tulikuwa na maisha ya chini sana. Leo nina imani sisi wana Sasu tuko vizuri."
Anastazia Paulo Makula
Kikundi cha kuweka akiba cha Maboresho, Sasu Centre

Mradi wa DREAMS Tanzania unatekelezwa na Mercy Corps kwa kushirikiana na Village Enterprise, Caritas Tabora na Dignity Kwanza, pamoja na wadau wa sekta binafsi wakiwemo CRDB Bank Foundation, Mgarang'ombe Traders, AKM Glitters, SimuSolar na KickStart International.



Posted by MROKI On Friday, August 28, 2026 No comments

August 27, 2026


Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) inatoa mafunzo kwa Wachunguzi wa Maabara za Sayansi Jinai na Vinasaba vya Binadamu yanayofanyika katika Jengo la Mkemia, Dar es Salaam, kuanzia tarehe 26–28 Agosti 2026.

Mafunzo hayo yanalenga kuongeza uelewa, weledi na umahiri wa wachunguzi katika utekelezaji wa majukumu ya uchunguzi wa Vinasaba vya Binadamu, kwa kuzingatia sheria, kanuni, viwango vya kitaalamu, maadili na usiri wa taarifa za vinasaba.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Huduma za Sayansi Jinai, David Elias, amesisitiza umuhimu wa mafunzo endelevu katika kuhakikisha uchunguzi wa vinasaba unafanyika kwa usahihi, uadilifu na viwango vinavyokubalika, huku haki na usiri wa taarifa za wahusika vikilindwa.







Posted by MROKI On Thursday, August 27, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo