Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo, amewasilisha Taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya chama cha Mapinduzi CCM ya Desemba 2025 mpaka FEBRUARY 2026 kwa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya ccm wilaya ya Ilala.
Akiwasilisha taarifa hiyo Mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo, amesema Halmashauri hiyo imejipanga kujenga vyumba vya madarasa kwa ajili ya kupokea wanafunzi 65000 ambapo Halmashauri hiyo imeweka fedha nyingi sekta ya Elimu.
Alisema miradi yote Ilala imekamilika kwa asilimia 89 changamoto ilikuwa katika vyumba vya madarasa kwa sasa wanaenda kuitatua changamoto ndani ya wilaya Ilala.
"Leo nimewasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani katika taarifa hii tumeelekeza shilingi bilioni 80 kuelekezwa katika miradi mbalimbali ya maendeleo katika fedha shilingi bilioni 347 zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan ambapo natumia fursa hii kumpongeza Rais kwa kushusha Neema Ilala inaenda kuwa ya kisasa" amesema Mpogolo .
Katika hatua nyingine aliagiza viongozi wa ngazi ya kata kusimamia vikundi vya mikopo ya Serikali ya asilimia kumi ambayo inatolewa ngazi ya Halmashauri wakishirikiana Umoja wanawake UWT Wilaya ya Ilala katika kuratibu vikundi hivyo .
Akizungumzia migogoro ya ardhi ndani ya wilaya Ilala ameagiza viongozi wa chama na Serikali kushirikiana pamoja katika kutatua changamoto hizo.
Alitumia fursa hiyo kuwapongeza Wajumbe wa Halmashauri Kuu wilaya ya Ilala wakiongozwa na Madiwani na Wabunge kwa kufanya kazi kwa kushirikiana
Wakati huohuo Mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo amesema Wenyeviti wa Serikali za mitaa 159 wa Wilaya ya Ilala hivi karibuni wanatarajia kukabidhiwa Vitamburisho vyao vya kazi hivyo aliwataka wavute subira taratibu zote zimekamilika
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Ilala Said Sidde alitumia fursa hiyo kumpongeza mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo pamoja na Katibu Tawala Wilaya Charangwa Selemani na Watendaji wote kwa kuleta maendeleo makubwa Ilala.
Mwenyekiti Side alisema Ilala wana mahusiano mazuri kati ya chama na Serikali katika utendaji wao wa kazi kila jambo wanashirikiana pamoja kujenga Serikali.
Meya wa Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam Nurudini sheta ameomba Wajumbe wa Halmashauri Kuu wilaya waweze kupatiwa mafunzo kwa ajili ya kuwajengea uwelewa kila mjumbe aweze kufanya kazi kwa Weledi.
























































