Nafasi Ya Matangazo

May 22, 2026







Arusha
Tume ya Madini imeanza rasmi kutumia Mfumo Jumuishi wa Kodi za Ndani (IDRAS) unaolenga kurahisisha utoaji wa huduma, kuongeza ufanisi wa utendaji na kuongeza ukusanyaji wa mapato ya Serikali katika sekta ya madini.

Akizungumza wakati wa kufunga kikao kazi cha wahasibu na wachumi wa Tume ya Madini kilichomalizika leo mkoani Arusha kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa Tume, Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Nsajigwa Kabigi, amesema mfumo huo utawawezesha wateja kujihudumia saa 24 popote walipo na kuharakisha utoaji wa huduma.

Amesema matumizi ya IDRAS yataongeza ufanisi katika usimamizi wa mapato huku yakirahisisha huduma kwa wananchi na wadau wa sekta ya madini.

“Tunatarajia mfumo huu kuongeza mapato ya Serikali na kuwapa wateja huduma kwa haraka na urahisi zaidi,” amesema Kabigi.

Kabigi pia amewataka wahasibu na wachumi kuwa makini katika matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) kwa kuzingatia usalama wa taarifa na nyaraka zinazotumika kupitia mfumo huo.

Aidha, amesema Serikali imeiwekea Tume ya Madini lengo la kukusanya shilingi trilioni 1.4 katika mwaka wa fedha 2026/2027 baada ya kufikia makusanyo ya shilingi trilioni 1.2 hadi Mei 18 mwaka huu kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Fedha na Mipango wa Tume ya Madini, CPA Idfonce Masoud, amesema mafunzo hayo yamewajengea uwezo wahasibu na wachumi kuhusu matumizi ya mfumo mpya pamoja na utekelezaji wa sheria za kodi.

Amesema washiriki wamepata uelewa kuhusu ukokotoaji wa kodi ya zuio, PAYE na namna ya kuwasilisha taarifa za kodi kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Masoud ameongeza kuwa wahasibu wanapaswa kuendana na viwango vya kimataifa vya uandaaji wa hesabu ili kuhakikisha taasisi zinaandaa taarifa za fedha kwa viwango vinavyokubalika kimataifa.
Posted by MROKI On Friday, May 22, 2026 No comments




 

Posted by MROKI On Friday, May 22, 2026 No comments







Arusha
Wahasibu na wachumi wametakiwa kujijengea nidhamu ya kitaaluma kwa kufuata sheria, taratibu na kanuni zilizowekwa ili kujiepusha na vitendo vya udukuzi wa mifumo ya kielektroniki na kulinda taarifa za Serikali.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Fedha na Mipango, CPA Idfonce Masoud, baada ya mawasilisho kuhusu faida za Mfumo Jumuishi wa Kodi za Ndani (IDRAS), mifumo mipya ya ukusanyaji wa mapato na usalama wa mifumo yaliyofanyika jijini Arusha.

CPA Masoud amesema usiri wa taarifa mahala pa kazi ni jambo muhimu katika taaluma ya uhasibu na uchumi, huku akisisitiza kuwa maadili na uwajibikaji vinapaswa kupewa kipaumbele ili kuongeza ufanisi wa kazi na kulinda taswira ya taasisi.

“Maadili ni muhimu katika maeneo ya kazi; bila kuwa na maadili hata kazi zetu hazitaheshimiwa na kuharibu taswira ya taasisi,” amesema.

Kwa upande wake, Meneja wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Jastin Chankani, amesema wahasibu, wachumi na watumishi wengine wanapaswa kutumia mifumo ya kielektroniki kwa usalama ili kulinda taarifa za Serikali na rasilimali za umma.

Amesema wahasibu ni kundi muhimu kwa kuwa hushughulikia taarifa za mapato na matumizi ya Tume, hivyo wanapaswa kuwa makini dhidi ya wadukuzi wenye nia mbaya.

“Ulinzi wa taarifa ni muhimu ili kuhifadhi usalama wa mitandao ya ofisi na kuzuia uvunjaji wa faragha pamoja na matumizi mabaya ya rasilimali za umma,” amesema Chankani.

Naye Afisa Kodi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania, Deogratius Mrosso, ameeleza kuwa Mfumo Jumuishi wa Kodi za Ndani (IDRAS) utawezesha utoaji wa huduma za kodi kwa saa 24 kila siku, kuhifadhi kumbukumbu za kodi, kutoa risiti za kielektroniki bila kutumia mashine, kuthibitisha nyaraka za kodi na kuonesha taarifa za kikodi za waajiriwa.

Amesema mfumo huo utaongeza uwazi, ufanisi na urahisi katika utoaji wa huduma za kodi nchini.

Aidha, Meneja wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Frank Mbele, amewataka wahasibu na wachumi kufanya kazi kwa bidii na kujitathmini katika utekelezaji wa majukumu yao kwa kuzingatia Mpango Mkakati wa Tume pamoja na viashiria vya utendaji ili kufikia malengo waliyojiwekea.

Washiriki wa kikao hicho wamehimizwa kuendelea kuimarisha usalama wa mifumo ya kielektroniki na kushirikiana katika kuboresha miundombinu ya teknolojia kwa lengo la kuongeza uwazi, ulinzi wa taarifa na ufanisi wa ukusanyaji wa mapato kwa manufaa ya umma.
Posted by MROKI On Friday, May 22, 2026 No comments









Mwanza
WAKAGUZI wa Migodi na Baruti nchini wametakiwa kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuimarisha usimamizi wa usalama migodini ili kudhibiti ajali, kulinda maisha ya wafanyakazi, mazingira na rasilimali za Taifa.

Kauli hiyo imetolewa jijini Mwanza na Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Tano wa Mwaka wa Wakaguzi wa Migodi na Baruti.

Dkt. Lekashingo amesema wakaguzi hao wana nafasi muhimu katika kuhakikisha shughuli za uchimbaji wa madini zinafanyika kwa usalama, ufanisi na kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Amesema shughuli za uchimbaji madini ni miongoni mwa kazi zenye hatari kubwa hivyo zinahitaji usimamizi madhubuti ili kuhakikisha uchimbaji endelevu unafanyika bila kuhatarisha maisha ya watu na mazingira.

Katika hatua nyingine, Dkt. Lekashingo amepongeza viongozi na watumishi wa Tume ya Madini kwa kuvuka lengo la makusanyo ya mwaka wa fedha 2025/2026 kabla ya muda.

Amesema lengo la makusanyo kwa mwaka huo lilikuwa Shilingi trilioni 1.2, huku hadi Mei 18, 2026 makusanyo yakifikia Shilingi trilioni 1.203 sawa na asilimia 100.31 ya lengo lililowekwa.

“Mafanikio haya ni uthibitisho wa usimamizi madhubuti, uwajibikaji, uzalendo na juhudi kubwa mnazozifanya katika kusimamia Sekta ya Madini,” amesema Dkt. Lekashingo.

Aidha, amesema Serikali kupitia Tume ya Madini itaendelea kuboresha mazingira na vitendea kazi kwa wakaguzi wa migodi na baruti ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Akimwakilisha Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, Mkurugenzi wa Leseni wa Tume, Eng. Aziza Swedi, amewataka wakaguzi wa migodi kuwa wabunifu na kutumia taaluma zao ipasavyo katika kusimamia ukaguzi wa migodi nchini.

Eng. Swedi amesema ni muhimu kwa wakaguzi hao kujiendeleza kitaaluma ili kwenda sambamba na kasi ya mabadiliko ya teknolojia pamoja na matumizi ya mbinu za kisasa za ukaguzi migodini.

Pia amesisitiza umuhimu wa kuzingatia maadili ya kazi na kutoa huduma kwa haki bila kuwaonea wadau wa sekta ya madini.

“Mkaguzi yeyote atakayesababisha sifa hii kuharibika, hatua kali za kimaadili zitachukuliwa dhidi yake na uteuzi wake kufutwa mara moja,” amesema Eng. Swedi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira, Eng. Hamisi Kamando, amesema idara hiyo ina jukumu la kuhakikisha shughuli za uchimbaji madini zinafanyika kwa kuanzia hatua za awali za uendeshaji wa mgodi hadi kufungwa kwake.

Amesema idara hiyo pia inasimamia usalama, afya, mazingira pamoja na utekelezaji wa sheria na taratibu zote za uchimbaji ili kuhakikisha migodi inaleta manufaa kwa Taifa bila kuathiri mazingira na jamii zinazozunguka maeneo ya uchimbaji.
Posted by MROKI On Friday, May 22, 2026 No comments

May 21, 2026


 

Posted by MROKI On Thursday, May 21, 2026 No comments

Njombe
Mkoa wa Njombe unatarajiwa kuwa kitovu kipya cha uchumi wa madini nchini kufuatia uwekezaji mkubwa katika miradi ya uchimbaji na uchakataji wa madini ya chuma inayolenga kufungua maelfu ya ajira, kukuza biashara za ndani na kuongeza mapato kwa wananchi wa Wilaya ya Ludewa.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Mhandisi Lucas Mlekwa, amesema tayari moja ya miradi mikubwa inayosimamiwa na Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) kwa kushirikiana na kampuni ya kigeni imepata Leseni Kubwa ya Uchimbaji wa Madini baada ya utafiti wa kina uliofanyika kati ya mwaka 2012 na 2013 kubaini uwepo wa zaidi ya tani milioni 126 za madini ya chuma.

Amesema tafiti hizo pia zimeonesha uwepo wa madini mengine yenye thamani kubwa yanayoambatana na chuma ikiwemo titanium na vanadium, hatua inayoongeza thamani ya kiuchumi ya mradi huo kwa Taifa.

“Kwa sasa tupo katika hatua za mwisho za kukamilisha makubaliano kati ya Serikali na wawekezaji, na tunatarajia ndani ya mwaka mmoja utekelezaji rasmi wa mradi utaanza,” amesema Mlekwa.

Kwa mujibu wa Mlekwa, mradi huo utahusisha shughuli kuu mbili ambazo ni uchimbaji wa madini pamoja na ujenzi wa kiwanda cha kisasa cha kuchakata chuma kitakachozalisha bidhaa mbalimbali zitakazotumika katika sekta ya ujenzi na viwanda nchini.

Ameeleza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo utaongeza ushiriki wa wazawa kupitia utekelezaji wa sera ya  Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini, ambapo wananchi watanufaika na fursa za ajira na biashara zikiwemo huduma za ulinzi, usafirishaji, ugavi wa vifaa vya ujenzi, huduma za migodini pamoja na shughuli nyingine za kiuchumi zinazozunguka miradi hiyo.

Aidha, amesema mradi wa chuma wa Maganga Matitu unaosimamiwa pia na NDC kwa ubia na kampuni ya kigeni umefikia hatua za mwisho za maandalizi baada ya mwekezaji kulipa zaidi ya Shilingi bilioni 4.2 kama fidia kwa wananchi waliopisha eneo la mradi huo, ambao una akiba inayokadiriwa kufikia tani milioni 45 za madini ya chuma.

Mlekwa ameongeza kuwa pamoja na miradi hiyo, Wilaya ya Ludewa itanufaika na utekelezaji wa mradi wa  Mchuchuma   wenye zaidi ya tani milioni 428 za makaa ya mawe kwa ajili ya uzalishaji wa umeme, unaotarajiwa kuimarisha upatikanaji wa nishati kwa shughuli za uchimbaji na viwanda vya chuma vitakavyojengwa wilayani Ludewa.

Amesema maendeleo hayo yataifanya Njombe kuwa miongoni mwa maeneo muhimu zaidi nchini katika sekta za madini, viwanda na nishati, huku yakitarajiwa kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa Taifa na maendeleo ya wananchi wa eneo hilo.
Posted by MROKI On Thursday, May 21, 2026 No comments
Mzee Peter Morisi Shirima akitia saini Hati ya Haki Miliki ya Kimila ya eneo alilofidiwa baada ya timu ya wataalamu kutoka iliyotumwa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba  kumaliza kwa njia ya maridhiano mgogoro wa ardhi  uliodumu kwa miaka 51 kati ya  Mzee huyo na Kanisa Katoliki Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, Mei 19, 2026. Wengine  kutoka kushoto ni Mkewe Juliana Anatoli, Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Rombo, Charles Daudi Mganga, Msaidizi wa Waziri Mkuu - Ardhi, Senso Magesa, Msaidizi wa Waziri Mkuu, Mahusiano, Asasi za Kiraia na Mashirika yasiyo ya  Kiserikali, Tryphone Mkorokoti na kulia ni Kamishina Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Kilimanjaro, Rehema Mdeedee. Tukio hilo lilifanyika kwenye ofisi ya kijiji cha Msaranga, Rombo. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Padri Amedeus Mtui, Wakili wa Askofu Rombo, Jimbo Katoliki Moshi akitia saini Hati ya Haki Miliki ya Kimila ya eneo la Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo baada ya timu ya wataalamu iliyotumwa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba kumaliza kwa njia ya maridhiano mgogoro  wa ardhi uliodumu kwa miaka 51 kati ya  Mzee Peter Morisi Shirima na Kanisa Katoliki Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, Mei 19, 2026. Wengine kutoka kushoto ni Paroko Parokia ya Mtimhoo, Padri Benedict Mwacha, Mke wa Mzee Peter,  Juliana Anatoli, Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Wilaya ya Rombo, Charles Daudi Mganga, Msaidizi wa Waziri Mkuu - Ardhi, Senso Magesa, Msaidizi wa Waziri Mkuu, Uhusiano wa rami na Taasisi za Dini i, Tryphone Mkorokoti na kulia ni Kamishina Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Kilimanjaro, Rehema Mdee.Tukio hilo lilifanyika  katika Ofisi ya kijiji cha Msaranga wilayani Rombo.
Mzee Peter Morisi Shrima akipokea kutoka kwa Msaidizi wa Waziri Mkuu- Ardhi, Senso Magesa, Hati ya Haki Miliki ya Kimila  ya eneo alilofidiwa baada ya timu ya wataalamu iliyotumwa na Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kumaliza kwa njia ya maridhiano mgogoro  wa ardhiuliodumu kwa miaka 51 kati ya  Mzee huyo na Kanisa Katoliki Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, Mei 19, 2026.  Wengine kutoka kushoto ni Diwani wa Kata ya Kisale Msaranga, Aloyce Assenga, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilay ya Rombo, Charle Daudi Mganga na kulia ni Mwenyekiti wa Kijiji cha Msaranga, Fratei Shirima. Tukio hilo lilifanyika  katika Ofisi ya kijiji cha Msaranga wilayani Rombo.
Paroko wa Parokia ya Mtimhoo ya Jimbo Katoliki la Moshi wilayani Rombo, Padri Benedict Mwacha (kushoto) na WaKili wa Askofu Rombo, Jimbo Katoliki Moshi, Pandri  Amedeus Mtui wakipokea  kutoka kwa Msaidizi wa Waziri Mkuu - Ardhi, Senso Magesa, Hati ya Haki Miliki ya Kimila  ya eneo la Parokia hiyo baada ya timu ya wataalamu iliyotumwa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba  kumaliza kwa njia ya maridhiano mgogoro  wa ardhi uliodumu kwa miaka 51 kati ya  Mzee Peter Morisi Shirima na Kanisa Katoliki Parokia ya Mtimhoo wilayani Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, Mei 19, 2026.  Wa pili kulia ni Diwani wa Kata ya  Kisale Msaranga, Aloyce Assenga. Tukio hilo lilifanyika  katika Ofisi ya kijiji cha Msaranga wilayani Rombo.
Mzee Peter Morisi Shirima   na Paroko wa Parokia ya Mtimhoo wa Jimbo Katoliki la Moshi, Padri Benedict Mwacha wakifurahia baada ya timu ya wataalamu iliyotumwa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba  kumaliza kwa njia ya maridhiano mğogoro wa ardhi  uliodumu kwa miaka 51 kati ya Mzee Peter Morisi Shirima na Parokia hiyo, kwenye Ofisi ya kijiji cha Msaranga wilayani Rombo,  Mei 19, 2026.
******************
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba ametatua mgogoro wa ardhi kati ya Parokia ya Mtimhoo ya Kanisa Katoliki Jimbo la Moshi na Mzee Peter Morisi wa Kijiji cha Msaranga, Wilaya ya Rombo Mkoa wa Kilimanjaro, uliodumu kwa kipindi cha miaka 51.
 
Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokea malalamiko ya Mzee Peter Morisi alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Halmashauri ya Wilaya ya Rombo wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Kilimanjaro tarehe 17 Februari 2026 ambapo aliahidi kuwa Serikali ingetuma wataalamu wilayani humo kwa ajili ya kuchunguza na kutatua mgogoro huo.
 
Kufuatia maelekezo hayo, Waziri Mkuu alituma timu ya wataalamu kutoka Ofisi yake ambao walifika mkoani Kilimanjaro na kushirikiana na viongozi wa Mkoa pamoja na viongozi wa Kijiji cha Msaranga kutembelea eneo la mgogoro. Aidha, timu hiyo ilifanya vikao na familia iliyokuwa katika mgogoro, viongozi wa kijiji, viongozi wa Parokia ya Mtimhoo pamoja na viongozi wa Jimbo Katoliki la Moshi ambapo pande zote zilikubaliana kuwa maridhiano ndiyo njia sahihi ya kumaliza mgogoro huo.
 
Katika madai yake, Mzee Peter Morisi alieleza kuwa eneo lake lilichukuliwa kwa nguvu na Kanisa Katoliki na kwamba fidia aliyolipwa ilikuwa ndogo ikilinganishwa na ukubwa wa eneo lililotwaliwa. Kutokana na kutopata suluhisho kwa muda mrefu, aliamua kuwasilisha malalamiko yake kwa Waziri Mkuu wakati wa mkutano wa hadhara.
 
Timu ya wataalamu ilipitia nyaraka zote zilizowasilishwa na pande husika na kubaini kuwa Mzee Peter Morisi alipokea fidia ya shilingi 3,935.50 tarehe 16 Aprili 1980. Aidha, alipewa eneo jingine katika Kitongoji cha Kirachi, Kijiji cha Msaranga ili kupisha ujenzi wa shule na kanisa katika eneo lake la awali.
 
Katika hatua nyingine, timu hiyo ilikutana na Askofu wa Jimbo Katoliki la Moshi, Askofu Ludovick Minde ambaye alisisitiza kuwa Kanisa Katoliki lina utamaduni wa kutatua migogoro kwa njia ya maridhiano na kuwataka wahusika kuendelea na mazungumzo ya amani.
 
Askofu Minde alitoa shilingi milioni tano kama kifuta machozi kwa madhara ambayo Mzee Peter Morisi na familia yake wameyapitia katika kipindi chote cha kutafuta suluhisho la mgogoro huo. Aidha, alisema Kanisa halina kinyongo na mlalamikaji na litaendelea kushirikiana naye wakati wote.
 
Vilevile, Askofu Minde alimshukuru Waziri Mkuu kwa kutuma timu ya wataalamu kutoka Ofisini kwake na kumtakia heri katika utekelezaji wa majukumu yake ya uongozi.
 
Kwa upande wake, Mheshimiwa Waziri Mkuu naye alitoa shilingi milioni tano na kufanya jumla ya fedha zilizotolewa kwa Mzee Peter Morisi kuwa shilingi milioni kumi kwa lengo la kujenga maridhiano na kuimarisha mshikamano katika jamii.
 
Baada ya kufikiwa kwa maridhiano hayo, pande zote zilitia saini nyaraka za makubaliano zikikiri kuwa mgogoro huo umemalizika kwa njia ya maridhiano na kuahidi kusameheana pamoja na kuendelea kuishi kwa amani. Kila upande pia ulikabidhiwa Hati za Hatimiliki za Kimila kwa maeneo husika.
 
Akizungumza baada ya kukabidhiwa hati hizo na kusaini nyaraka za maridhiano, Mzee Peter Morisi aliishukuru Serikali kwa kumaliza mgogoro huo uliodumu kwa muda mrefu na kuahidi kushirikiana na Kanisa pamoja na wanakijiji wenzake bila kinyongo.
 
Naye Diwani wa Kata ya Kisale Msaranga, Mhandisi Mathias Assenga alisema mgogoro huo uliathiri mshikamano wa wananchi pamoja na uhuru wa kuabudu kwa kuwa ulihusisha eneo la kanisa linalotumiwa na waumini kwa ibada na shughuli nyingine za kidini.
 
Kwa upande wake, Padri Amadeus Mtui ambaye ni Wakili wa Baba Askofu wa Jimbo Katoliki la Moshi alimshukuru Waziri Mkuu kwa kutuma timu ya wataalamu ambayo imekuwa chachu ya kumalizika kwa mgogoro huo.
 
Baadhi ya viongozi walioshiriki katika mchakato wa maridhiano hayo ni pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Rombo, Charles Daudi Mganga, Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Kilimanjaro, Rehema Mdee pamoja na Diwani wa Kata ya Kisale Msaranga, Mhandisi Mathias Assenga.

Mzee wa Kijiji cha Msaranga, Andrea Peter Mkenda alisema kumalizika kwa mgogoro huo kutaleta amani, utulivu na kuimarisha mshikamano miongoni mwa wananchi hali itakayowapa nafasi nzuri ya kuendelea na shughuli zao za maendeleo.
Posted by MROKI On Thursday, May 21, 2026 No comments

May 20, 2026










MKuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila ametoa ahadi ya milioni 50 kwa Dar City Basket Team endapo itafunzu mtanange huko Rwanda kufikia hatua ya nusu fainali.

RC Chalamila ameyasema hayo leo Mei 20, 2026 katika uwanja wa ndege wa Mwalimu JK Nyerere Terminal 3 wakati akiiaga team hiyo kuelekea Kigali Rwanda kwenye mashindano.

Aidha RC Chalamila ametoa rai kwa wakazi wa Mkoa huo endapo watabaini kuna kijana anakipaji cha basket ball,wamlete ofisini kwake ili aweze kuendelezwa kipaji hicho pamoja na kumuunganisha na wachezaji nguli wa Dar City Basket Ball.

Vilevile RC Chalamila amesema Rais wa team hiyo Ndg Hashimu Thabit akirudi toka Rwanda uandaliwe utaratibu wa kukutana na Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wote wa Mkoa huo kuona namna ya kuwa na uwanja mkubwa wa kisasa wa Basket Ball  katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Kwa upande wa Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe Edward Mpogolo amesema Dar City ni team ya kimataifa na inafanya vizuri ni ya kihistoria toka Tanzania ipate uhuru hivyo anaitakia kila kheri.

Mwisho RC Chalamila amemshukuru Rais Dkt Samia kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya michezo kwa kuwa michezo ni afya lakini pia michezo ni uchumi.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments



Freetown- Sierra Leone
Tanzania imesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa Kikanda katika kuongeza thamani Madini ya Almasi, uwazi katika usimamizi wa rasilimali madini na kuimarisha mchango wa Sekta ya Madini katika maendeleo ya uchumi wa nchi wanachama Zinazozalisha Madini ya Almasi Afrika (ADPA).

Hayo yalibainishwa  Mei 19, 2026   mjini Freetown, Sierra Leone, na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo, ambaye anaongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki  katika Mkutano wa 11 wa Kawaida  wa Kamati ya  Wataalam  wa umoja huo.

Mkutano huo unawakutanisha wataalam kutoka nchi wanachama wa ADPA kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha usimamizi, biashara na maendeleo ya sekta ya almasi barani Afrika.

 Aidha, katika mkutano huo, wajumbe walijadili taarifa ya mwaka ya Mkurugenzi Mtendaji wa ADPA ya mwaka 2025, utekelezaji wa bajeti na taarifa za fedha za mwaka 2025 pamoja na taarifa ya ukaguzi wa nje wa hesabu kwa kipindi cha 2023–2024. Aidha, masuala ya msamaha wa madeni, daftari la hatari, maendeleo ya uwezo wa taasisi na uanachama wa ADPA katika Shirika la Viwango Duniani (ISO) yalipata nafasi ya kujadiliwa kwa lengo la kuimarisha ufanisi wa taasisi hiyo.

Vilevile, mkutano ulipokea taarifa za maendeleo kuhusu maandalizi ya Mkutano wa Almasi na maadhimisho ya miaka 20 ya ADPA, mapitio ya mkakati wa mawasiliano na masoko, utekelezaji wa ukaguzi wa ndani wa miaka 2023–2025 pamoja na mapendekezo ya sera ya usimamizi wa utendaji kazi.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing pamoja na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing pamoja na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing, Ujumbe Maalumu kwenda kwa Rais wa China Mhe. Xi Jinping mara baada ya mazungumzo, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi wa Chama cha Mapinduzi  (CCM) na Serikali kwenye picha na Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing pamoja na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.
Posted by MROKI On Wednesday, May 20, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo