Katibu
Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi, akiwa katika mazungumzo na Bw.
Lorenzo Guadagno wa Sekretarieti ya Santiago Network pamoja na ujumbe
ulioambatana nao, pembeni mwa mkutano wa SB64 mjini Bonn, Ujerumani.
Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mtaalamu wa Ushirikishwaji wa Wanachama wa Sekretarieti ya Santiago Network, Bw. Lorenzo Guadagno baada ya mazungumzo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano na kuhakikisha Ofisi ya Kanda ya Santiago Network kwa Afrika iliyopo Dar es Salaam inatekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kufikia malengo yaliyowekwa.
*************
Wadau wa mazingira kutoka
Taasisi ya Hanns R. Neumann Stiftung (HRNS) ya Ujerumani wameonesha nia ya
kuwekeza na kushirikiana na Tanzania katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya
maendeleo endelevu ikiwemo uhifadhi wa mazingira, nishati safi, biashara ya
kaboni, maendeleo ya vijana na kilimo.
Nia hiyo imebainishwa katika
mazungumzo kati ya Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi
na Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini wa HRNS, Bw. Olaf Tschimpke, yaliyolenga
kutafuta maeneo mapya ya ushirikiano kati ya taasisi hiyo na Serikali ya
Tanzania.
Kikao hicho kimefanyika pembezoni
mwa Mkutano wa 64 wa Wataalam wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko
ya Tabianchi (SB64) unaofanyika Bonn, Ujerumani.
Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Muyungi
aliwasilisha vipaumbele vya Taifa vilivyomo katika Dira ya Taifa ya Maendeleo
2050, ikiwemo maendeleo ya masoko ya kaboni, nishati jadidifu, uchumi wa buluu,
nishati safi ya kupikia na ushiriki wa vijana katika uhifadhi wa mazingira.
Aidha, Dkt. Muyungi alieleza umuhimu wa kupata
wadau wa kusaidia kuendesha Kituo cha Vijana cha Afrika cha Majadiliano ya
Mabadiliko ya Tabianchi kilichopo Dar es Salaam.
Kwa upande wake, Bw. Tschimpke alisema HRNS ina
uzoefu wa kusaidia wakulima wadogo wa kahawa, kulinda mazingira na kuwawezesha
vijana katika nchi mbalimbali za Afrika, ikiwemo Tanzania, Uganda na Ethiopia.
Maeneo yaliyotajwa kuwa na fursa za ushirikiano ni
pamoja na kusaidia wakulima wadogo wa kahawa, kuanzisha Muungano wa Kudhibiti
Uchafuzi wa Plastiki nchini, kuendeleza masoko ya kaboni, uwekezaji katika
nishati ya jua, programu za michezo kwa vijana, mafunzo ya mazingira na
ujasiriamali kwa vijana pamoja na uwekezaji katika teknolojia za usafiri wa
umeme (e-mobility).
Pia, pande hizo mbili zimekubaliana kuendelea na
mazungumzo kupitia kikao cha ufuatiliaji kitakachofanyika mwezi Julai mjini
Bonn, Ujerumani, pamoja na kuandaa Hati ya Makubaliano (MoU) itakayobainisha
maeneo ya ushirikiano na utekelezaji wake.
Vilevile, imekubaliwa kuandaliwa kwa mkutano wa
wadau utakaowakutanisha washirika wa HRNS na Serikali ya Tanzania nchini
Tanzania ili kujadili kwa kina fursa za ushirikiano, uwekezaji na utekelezaji
wa maeneo yaliyobainishwa kuwa na maslahi ya pamoja.
Katika hatua nyingine, Dkt. Muyungi,
amekutana na Mwakilishi wa Sekretarieti
ya Santiago Network, Bw. Lorenzo Guadagno
kwa lengo la Lengo kuu la mazungumzo hayo kuimarisha ushirikiano kati ya
Ofisi ya Makamu wa Rais na Santiago Network, pamoja na kujadili
namna ya kuhakikisha kuwa Ofisi ya
Kanda ya Santiago Network kwa Afrika iliyopo Dar es Salaam.
Tanzania,
inatekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kufikia malengo yaliyokusudiwa katika kusaidia nchi za Afrika kukabiliana
na athari za mabadiliko ya tabianchi, hususan Hasara na Uharibifu (Loss and Damage).
Dkt. Muyungi alisisitiza dhamira ya Serikali ya
Tanzania ya kuendelea kushirikiana na Santiago Network ili kuhakikisha kuwa
ofisi hiyo ya kikanda inakuwa kitovu muhimu cha uratibu, ujenzi wa uwezo,
kubadilishana uzoefu na utoaji wa msaada wa kiufundi kwa nchi za Afrika.
Alieleza kuwa Tanzania iko tayari kutoa ushirikiano unaohitajika ili kuwezesha
utekelezaji wa majukumu ya ofisi hiyo kwa manufaa ya bara la Afrika.
Kwa upande wake, Bw. Guadagno alieleza dhamira ya
Sekretarieti ya Santiago Network ya kuimarisha ushirikiano na Tanzania na wadau
wengine wa kikanda ili kuhakikisha kuwa huduma na msaada wa kiufundi unaotolewa
kupitia ofisi ya Dar es Salaam unawafikia walengwa kwa wakati na kwa ufanisi,
sambamba na malengo ya Santiago Network ya kusaidia nchi zinazoendelea
kukabiliana na changamoto za hasara na uharibifu unaotokana na mabadiliko ya
tabianchi.
Pande zote mbili zilikubaliana kuendelea
kuimarisha mawasiliano na ushirikiano wa karibu ili kuhakikisha kuwa Ofisi ya
Kanda ya Santiago Network kwa Afrika inakuwa chombo madhubuti cha kusaidia nchi
za bara hilo katika kujenga ustahimilivu na kuimarisha uwezo wa kukabiliana na
athari za mabadiliko ya tabianchi.