Nafasi Ya Matangazo

July 07, 2026

Na Dk. Reubeni Lumbagala 
Kuna umuhimu mkubwa kwa Watanzania kubadili mtizamo kuhusiana na lugha ya Kiswahili. Hii ina maana kuwa, tusiiangalie lugha ya Kiswahili katika muktadha wa mawasiliano pekee. Hapana. 

Ni kwamba, twende mbele zaidi, yaani tukifanye Kiswahili kuwa bidhaa ya kuuza na kuingiza fedha, kuongeza ajira, hatimaye kukuza uchumi na maendeleo ya mama Tanzania badala ya Kiswahili kubaki kama chombo cha mawasiliano na kupiga soga.

Kiswahili kimepiga hatua kubwa sana na kupata heshima kubwa ulimwenguni. Tuna kila sababu ya kujivunia lugha hii adhimu na adimu, ambayo tunapaswa kuifungamanisha na mikakati ya ukuzaji uchumi kwa maendeleo endelevu.

Ni hivi: Lugha ya Kiswahili imevuka mipaka. Kwa sasa, Kiswahili si lugha ya Tanzania au Afrika Mashariki pekee bali ni lugha ya Afrika na ya dunia. 

Kiswahili sasa kimepata heshima kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO). UNESCO imeichagua Julai 7, ya kila mwaka, kuwa "Siku ya Kiswahili Duniani".

Na kwa mwaka huu, maadhimisho hayo, yanafanyika Jijini Paris, nchini Ufaransa, yalipo makao makuu ya UNESCO, ambapo Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amehudhuria maadhimisho hayo, kumuwakilisha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Kwa hakika, kuna mwamko mkubwa wa watu kujifunza Kiswahili ulimwenguni. Aidha, Kiswahili sasa kinafundishwa katika shule na vyuo mbalimbali ulimwenguni, jambo linaloendelea kuongeza thamani yake. Kukibidhaisha Kiswahili kunahusisha  kuingiza fedha kupitia lugha hiyo. Sasa, tunawezaje kutengeneza fedha kupitia lugha ya Kiswahili?

Kwanza, kupitia ajira ya kufundisha Kiswahili. Wapo vijana wengi wahitimu wa vyuo na vyuo vikuu waliosomea somo la Kiswahili. Hawa wanaweza kutumika kufundisha Kiswahili kwa wageni wanaopenda kujifunza lugha hii.

Aidha, kupitia shughuli hiyo, vijana hao wataingiza fedha na serikali kunufaika kupitia kuongeza fursa za ajira kwa wananchi wake na kupata kodi kupitia mishahara ya walimu hao, jambo litakalochangia katika kukuza uchumi.

Pili, kuuza matini za Kiswahili. Wataalamu wa Kiswahili wanaweza kuingiza fedha kupitia kuandika na kuuza vitabu vya Kiswahili vilivyo katika muundo wa nakala laini na nakala ngumu (soft and hard copies). Mauzo hayo, yatawezesha kujenga uchumi wa nchi yetu na kukuza maendeleo.

Tatu, kukifungamanisha Kiswahili na sanaa ya filamu na tamthiliya za nje. Serikali ishirikiane na wandaaji wa filamu na tamthiliya za nje kama Korea, Uturuki, India na wengineo katika kutafsiri filamu na tamthiliya hizo kwa kutumia Kiswahili. 

Hii itaongeza fursa za ajira kwa 'waingizaji wa sauti za Kiswahili' katika tamthiliya hizo na hivyo kuwezesha wahusika hao kupata kipato. Jambo hili natamani liendelee kufanyika kwa ukubwa zaidi ya linavyofanyika sasa.

Jambo muhimu, ni wataalamu wetu wa Kiswahili kuwa na umahiri katika lugha nyingine za kimataifa kama Kiingereza, Kifaransa, Kichina, Kijerumani, Kiarabu, Kikorea, kutaja kwa uchache ili waweze kuwa walimu mahiri wa kufundisha wanafunzi wa kigeni na kuongeza mawanda ya kupata fursa za kufundisha lugha hiyo ulimwenguni.

Kimsingi, hata safari ya miaka 25 ijayo, kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050, Kiswahili kina nafasi ya kuchangia kufanikisha mipango mingi ya kiuchumi kwa kutumia fursa zilizopo katika kukibidhaisha kama nilivyoeleza katika nyanja ya uchumi.
Mungu Ibariki Tanzania.
Maoni: 0620 800 462.

Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments




Na Dk. Reubeni Lumbagala 
Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, anatambulika kimataifa katika nyanja mbalimbali kutokana na utendajikazi wake uliotukuka. Miongoni mwa maeneo yanayomtambulisha kwa upekee ni pamoja na kuwa Kinara wa Afya ya Uzazi ya Mama na Mtoto barani Afrika.

Ni heshima ya kipekee aliyoipata kutokana na mageuzi makubwa yaliyofanyika katika sekta ya afya, ambapo matunda yake yameonekana hasa katika kupungua kwa vifo vya mama na mtoto wakati wa kujifungua.

Kwa wadhifa huu, Rais Dk. Samia anao wajibu wa kuhakikisha nchi zote 54 za barani Afrika na Tanzania ikiwemo, zinaendea kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa kiwango kikubwa.

Hii inatokana na ukweli kuwa, kundi la mama na mtoto ni wadau muhimu katika juhudi za maendeleo. Ni kundi ambalo linapaswa kuhakikishiwa usalama wa maisha na kamwe uzazi usio tishio la usalama wao.

Juhudi za kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa sehemu kubwa zinahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali hasa katika kubadilishana uzoefu, teknolojia na uwekezaji wa miundombinu bora ya afya na vifaa tiba vya kisasa.

Kwa kutumia ushirikiano baina ya sekta ya umma na binafsi (Public and Private Partnership - PPP), juhudi na mapambano ya kupunguza vifo vya mama na mtoto zitafanikiwa kwa kiwango kikubwa.

Ili jambo hili liwe halisi, Julai 02, 2026, Rais Dk. Samia alifanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Sera, Uhusiano na Ushirikiano na Serikali (PGRP), Divisheni ya Afrika na India kutoka Taasisi ya Gates, Bi. Caty Fall Sow ambaye aliambatana na ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam. 

Haya yamefanyika ikiwa ni mwendelezo wa harakati chanya za uboreshaji wa afya ya uzazi ya mama na mtoto Tanzania na Afrika kwa ujumla.

"Bi. Sow alimpongeza Rais Samia kwa kuteuliwa kwake kuwa Bingwa wa Umoja wa Afrika wa Afya ya Mama, Mtoto Mchanga na Mtoto, na akathibitisha upya dhamira ya Taasisi ya Gates ya kuunga mkono juhudi zinazoongozwa na Waafrika za kumaliza vifo vinavyoweza kuzuilika vya akina mama na watoto," ilieleza Taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu.

Aidha, taarifa imesisitiza kuwa pande zote mbili zimejadili namna ya kuimarisha ushirikiano zaidi katika maeneo ya afya ya mama na mtoto, chanjo, lishe, kuimarisha mifumo ya huduma na kudhibiti magonjwa.

Naye, Rais Dk. Samia amesema, "Dhamira yetu ni kuhakikisha kila mama na kila mtoto anapata huduma bora za afya na nafasi ya kuishi maisha yenye afya na matumaini".

Taasisi ya Gates ni mdau mkubwa wa uimarishaji wa masuala ya afya barani Afrika, jambo linalosaidia kuimarika kwa huduma za afya na kuwezesha kufanikiwa kwa mipango ya serikali ya kuwahudumia wananchi wake.

Kutokana na kazi kubwa aliyonayo Rais Dk. Samia ya kusaidia mafanikio ya masuala ya afya ya uzazi ya mama na mtoto barani Afrika, Juni 02, 2026, alimteua Bi. Ummy Mwalimu kuwa Mshauri wa Rais - Masuala ya Afya ya Uzazi ya Mama na Mtoto.

Maoni: 0620 800 462.
Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments
Na Dk. Reubeni Lumbagala 
Malezi bora ya watoto yanapaswa kutiliwa mkazo ili kujenga jamii yenye watu wenye maadili, nidhamu, uzalendo na uwajibikaji katika maisha yao.

Wazazi wamepata baraka ya kupata watoto kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Watoto hao wanapaswa kuendelea kuwa baraka kwa kuhakikisha wanapata malezi na matunzo muhimu.

Katika miaka ya karibuni, kumekuwa na kulegalega malezi ya watoto. Baadhi ya wazazi na walezi ambao ndiyo wadau wa kwanza wa kusimamia malezi ya watoto wamekuwa walipambana na matunzo ya watoto huku wakisahau malezi yao.

Wazazi na walezi wanahangaika kutafuta fedha za kuwapatia watoto wao mahitaji muhimu kama vyakula, mavazi, mahitaji ya shule ili wafurahie maisha. Hili ni jambo zuri na la kupongezwa na kila mtu.

Changamoto inayokuja ni pale wazazi na walezi wanapojitahidi kutoa matunzo na kusahau suala la malezi ambalo ni la muhimu sana.

Julai 02, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dk. Batilda Buriani alitoa somo zuri la malezi kwa wazazi na walezi. 

Ni kwamba, Dk. Buriani alitoa somo hilo alipomwakilisha Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dk. Dorothy Gwajima, katika kilele cha Maadhimisho ya Mtoto wa Afrika na Kampeni ya Kitaifa ya Maadili na Malezi Chanya Kwa Watoto yenye kaulimbiu isemayo "Mtoto ni Malezi; Msingi wa Familia Bora kwa Taifa Imara".

Katika hafla hiyo, Balozi Dk. Buriani alisema, "Wazazi wanatakiwa kutenga muda kuwafuatilia watoto, kuwapa malezi bora, malezi si hiari bali ni wajibu kwa wazazi na walezi".

Kimsingi, Dk. Buriani alihimiza juu ya wazazi na walezi kutenga muda wa kufuatilia watoto wao na kuwalea watoto kwa misingi ya imani za dini zao.

Hivyo basi, wazazi na walezi wazingatie ushauri huu chanya uliotolewa. Wazungumze na watoto wao kutambua changamoto zao ili kuzitafutia ufumbuzi kwa ustawi wao. Pia, wafuatilie maendeleo ya kitaaluma ya watoto wao shuleni ili wafanye vizuri zaidi katika masomo yao.

Sanjari na hilo, wazazi na walezi wasimamie suala la mafundisho ya dini kwa watoto wao ili wawe na hofu ya Mungu na mwenendo mwema unaokubalika katika jamii na mbele za Mungu.

Naamini, haya yakifanyiwa kazi, tutajenga kizazi chenye maadili mazuri ambayo ni chachu ya maendeleo kuanzia ngazi ya familia, jamii na taifa kwa ujumla, na hili litafanya hata utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya mwaka 2050 kuwa rahisi.

Maoni: 0620 800 462.
Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments
Na Dk. Reubeni Lumbagala
Miongoni mwa haki za msingi za mfanyakazi serikalini au sekta binafsi ni pamoja na kulipwa mafao yake kwa wakati pindi anapostaafu utumishi wake.

Mafao hayo yanatokana na michango aliyochangia katika mifuko ya hifadhi ya jamii kutoka kwenye makato ya mshahara wake pamoja na michango ya mwajiri wake.

Kwahiyo, mfanyakazi anapomaliza muda wa utumishi wake eidha kwa kustaafu kwa hiari au kwa lazima, mifuko ya hifadhi ya jamii inapaswa kumlipa mafao yake ili kuendeleza maisha mengine, kwani maisha lazima yaendelee hata baada ya kustaafu.

Kwa muda mrefu, kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya wastaafu kucheleweshewa kulipwa mafao yao, ambayo kama nilivyoeleza awali ni haki yao ya msingi na si hisani. Kwa ufupi, wanastahili kulipwa bila usumbufu wowote.

Kucheleweshewa mafao ya wastaafu kumesababisha usumbufu mkubwa kwa wastaafu, na hata kuwasababishia msongo wa mawazo kwa kujiuliza kwani kustaafu ni kosa la jinai hadi kusumbuka kiasi hicho? 

Ni faraja kuona kuwa, sasa kero hiyo ya kuchelewa kulipwa kwa mafao ya wastaafu inakuwa historia nchini.

Mwezi Aprili, 2026, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeanzisha kaulimbiu isemayo "Tunalipa Jana" yenye malengo ya kuharakisha malipo ya mafao ya wastaafu kwa wakati mara tu mfanyakazi anapostaafu.

Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Fortunatus Magambo, amesema mfuko huo umejizatiti kuhakikisha wastaafu wanalipwa mafao yao kwa wakati ili kufurahia utumishi wao.

"Tunapoanza kumsajili mwanachama, tunahakikisha taarifa zake zinakuwa sahihi na zinahuishwa kila inapobidi. Lengo letu ni kwamba anapofikia umri wa kustaafu asiwe na changamoto yoyote ya malipo. Tunataka alipwe siku ya kustaafu. Hiyo ndiyo tafsiri halisi ya kaulimbiu yetu ya Tunalipa Jana, amesema Magambo.

Katika hatua nyingine, Magambo ameishukuru serikali chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kulipa deni la shilingi trilioni nne kwa Mfuko huo, jambo lililoimarisha ukwasi na uendelevu wa kulipa mafao.

Kwa hakika, mkakati wa PSSSF wa kulipa mafao ya wastaafu mara tu wanapostaafu ni jambo la kupongezwa. 

Wapo baadhi ya wastaafu kwa kuchelewa kulipwa mafao yao, wamejiingiza katika mikopo yenye riba kubwa, jambo linaloathiri mafao yao kwani wanapokuja kulipwa, hujikuta wakilipa deni kubwa linalochukua asilimia kubwa mafao yao. 

Kwa hili la kumlipa mstaafu kwa wakati, kutaleta utulivu wa akili, kustamwezesha mstaafu kutumia fedha zake kadri ya mipango yake aliyonayo na kufurahia utumishi wake na kuona kustaafu ni heshima na si mateso au adhabu. Sitakosea kusema PSSSF mmeutendea haki msemo wenu wa "Kesho Yako, Kipaumbele Chetu".

Maoni : 0620 800 462.
Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments





Na Mwandishi Wetu, Afrika Kusini
Waziri wa Maji, Jumaa Aweso pamoja na ugeni wake, wapo nchini Afrika Kusini, ikiwa ni ziara ya kikazi yenye lengo la kushirikiana na wadau mbalimbali katika kufanikisha udhibiti wa upotevu wa maji ili kuongeza kasi ya usambazaji wa huduma ya maji kwa wananchi.

Ziara hiyo iliyoanza Julai 6, 2026, imelenga kushiriki kikao kazi na wataalamu wa masuala ya teknolojia zenye uwezo wa kudhibiti upotevu wa maji, ili wananchi waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza kwa matumizi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.

Ikumbukwe kuwa, upotevu wa maji ni miongoni mwa changamoto inayoikabili Wizara ya Maji, ambayo imesababisha kupotea kwa maji mengi na kuzikosesha mapato mamlaka za maji katika wilaya mbalimbali nchini. 

Kimsingi, moja ya kipaumbele cha Wizara ya Maji kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ni kupambana na upotevu wa maji. Hivyo ziara hiyo, ni mkakati wa kufanikisha kipaumbele hicho.

Katika ziara hiyo, Aweso ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara, Mhandisi Mwajuma Waziri, Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, James Bwana pamoja na wataalamu wengine wa wizara hiyo.

Pamoja na masuala ya maji, Julai 7, akiwa nchini humo, Aweso pamoja na ugeni wake wameshiriki kikamilifu hafla ya maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani. 

Katika hafla hiyo, amezindua Kituo cha Utamaduni wa Kiswahili Tanzania (Tanzania Kiswahili Cultural Center) ikiwa ni mkakati wa kufundisha lugha ya Kiswahili kwa wageni ili kuendelea kukuza lugha hiyo na utamaduni wa Kitanzania ulimwenguni.
Posted by MROKI On Tuesday, July 07, 2026 No comments

July 06, 2026

 


Posted by MROKI On Monday, July 06, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akimjulia hali Sheikh Rashid Hamad Othman, Kaka mkubwa wa Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha ACT Wazalendo, Mhe. Othman Masoud Othman, anayepatiwa matibabu katika Hospitali ya Aga Khan Jijini Dar es Salaam. Akiwa hospitalini hapo Mhe. Rais Dkt. Samia pia alijulishwa kuhusu kuwepo kwa Mchezaji wa Timu ya Yanga Pacome Zouzoua katika chumba jirani, ambapo alipata muda wa kumtembelea na kumpa pole kufuatia majeraha aliyopata katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya JKT Tanzania katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo hivi karibuni.



 

Posted by MROKI On Monday, July 06, 2026 No comments

July 05, 2026





Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo leo Julai 5, 2026 ametembelea na kuzungumza na wataalam waliopo kwenye banda la Wakala wa Nishati Vijijini (REA) wakati wa maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es salaam 

Akiwa katika banda la REA, Mbibo alielezwa kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya nishati safi ya kupikia na umeme vitongojini iliyotekelezwa na inayotekelezwa na REA katika maeneo hayo.
Posted by MROKI On Sunday, July 05, 2026 No comments


Katika siku ya nane (08) ya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa maarufu kama SabaSaba, yanayoendelea jijini Dar es Salaam, Wakala wa Vipimo (WMA) imeendeleza mkakati wake wa kuwatembelea wajasiriamali na kuwapatia elimu kuhusu matumizi sahihi ya vipimo. 

Zoezi la utoaji elimu ya vipimo kwa wajasiriamali linaenda sambamba na kuhudumia wadau mbalimbali wanaotembelea banda la WMA katika Maonesho hayo ya SabaSaba. 

Lengo ni kuhakikisha elimu na huduma mbalimbali za ki-vipimo zinafikishwa kwa wadau wengi kadri iwezekanavyo.

Pichani ni matukio mbalimbali kuhusu utoaji elimu na huduma za ki-vipimo kwa wananchi na wadau, leo Julai 05, 2026.
Posted by MROKI On Sunday, July 05, 2026 No comments

July 04, 2026






Posted by MROKI On Saturday, July 04, 2026 No comments

July 03, 2026

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.
Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeendelea kutumia Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake, huduma mbalimbali na umuhimu wa ithibati katika kuimarisha taaluma ya uandishi wa habari nchini.

Hatua hiyo imejidhihirisha leo baada ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, kuungana na maafisa wa Bodi katika banda la JAB lililopo Kijiji cha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kutoa elimu kwa wananchi, kujibu maswali mbalimbali na kuzungumza na waandishi wa habari waliotembelea banda hilo.

Akizungumza katika maonesho hayo, Wakili Kipangula alisema JAB imejipanga kuhakikisha wananchi na wadau wa sekta ya habari wanapata uelewa sahihi kuhusu majukumu ya Bodi pamoja na huduma zinazotolewa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari.

Alisema ushiriki wa JAB katika maonesho ya Sabasaba unalenga kusogeza huduma karibu na wananchi, kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa ithibati kwa waandishi wa habari na kuhamasisha uzingatiaji wa maadili, weledi na uwajibikaji katika taaluma ya uandishi wa habari.

Mbali na kutoa elimu, JAB inaendelea kutoa huduma mbalimbali katika banda lake ikiwemo usajili wa waandishi wa habari, utoaji wa vitambulisho vya ithibati kwa waliokidhi vigezo, marekebisho ya taarifa za usajili pamoja na ushauri kuhusu huduma zinazotolewa na Bodi.

JAB imewahimiza waandishi wa habari, wadau wa sekta hiyo na wananchi kwa ujumla kutumia fursa ya Maonesho ya Sabasaba kutembelea banda lake ili kupata huduma, elimu na ufafanuzi kuhusu shughuli zake, huku ikisisitiza kuwa ithibati ni nyenzo muhimu katika kujenga taaluma ya uandishi wa habari yenye weledi, uwajibikaji na kuaminika.

Posted by MROKI On Friday, July 03, 2026 No comments








Na. Mwandishi Wetu - Arusha
Tanzania ipo tayari kwa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) ikiwa mwenyeji kwa kushirikiana na Kenya na Uganda ambapo maandalizi yamefikia hatua nzuri kwa kuzingatia viwango vya Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF) vinavyotakiwa.

Akizungumza hii leo Julai 3, 2026 Jijini Arusha kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Makatibu Wakuu ya Maandalizi ya Michuano hiyo, Dkt. Jim Yonazi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbasi amesema Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha michuano hiyo inafana kwa kuzingatia mipango na mikakati thabiti iliyopo.

Dkt. Abbasi ameiongoza Kamati hiyo iliyotembelea viwanja vitakavyotumika wakati wa michuano hiyo ikiwemo Kiwanja cha Mazoezi cha Mgambo, kiwanja cha mazoezi cha Engutoto, Kiwanja cha mazoezi Magereza, uwanja Mpya wa Arusha pamoja na ukaguzi wa barabara za mjini zinazosimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania-TANROADS pamoja na zinasosimamiwa na Wakala wa Barabara za mjini na vijijni -TARURA zitakazoingia na Kutoka Katika uwanja wa Arusha, kujionea maendeleo ya ukarabati na maboresho mbalimbali kuelekea michuano hiyo.

Aidha amesema kuwa, michuano hiyo itakuwa ya kihistoria kwa kukutanisha na kuvutia mamilioni ya watu barani Afrika na duniani kote, ambapo ni kwa mara ya kwanza mashindano hayo kuandaliwa kwa pamoja na Mataifa matatu ya Afrika Mashariki.

Aliongezea kuwa, Tanzania imejipanga kupokea Maelfu ya mashabiki, wachezaji, na viongozi wa soka wanatarajiwa kukusanyika na kuleta mwamko mkubwa kupitia Mashindano Makubwa ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027).

"Ni wakati wetu sasa, kuipa nchi heshima yake kuelekea Michuano hiyo ya AFCON, kila mmoja akae tayari katika eneo lake na kujua kuwa anajukumu la kuifanikisha michuano hii na kwa viwango vya kimataifa," alisema Dkt. Abbasi.

Pia alisisistiza Wakandarasi kwenye miradi mbalimbali ya kuboresha miundombinu kuongeza kasi ili kumaliza kazi hizo kwa wakati bila kukwamisha maandalizi hayo.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha Dkt. Toba Nguvila amesema kuwa mkoa umeendelea na maandalizi yote muhimu ikiwemo ya ukarabati wa miundombinu itakayotumika, kuhakikisha upatikanaji wa huduma za maji, kuboresha maeneo ya utoaji wa huduma za kiafya ikiwemo hospitali, masuala ya mawasiliano, pamoja na umeme na kuhakikisha vinapatikana kwa ubora na viwango.

“Jiji linaimarisha miundombinu ya barabara, huku kukiwa na ujenzi na ukarabati wa hoteli za kutosha zitakazotoa huduma pamoja na uboreshwaji wa vituo vya afya vya kutolea huduma za afya ikiwemo hospitali ya Mount Meru, JKCI pamoja na NSK ambazo zitatoa huduma za kiafya kwa ubora na viwango,” alisema Dkt. Nguvila.
Posted by MROKI On Friday, July 03, 2026 No comments







DAR ES SALAAM
Madini ya Tanzanite yameendelea kuwa kivutio kikubwa katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), huku mamia ya wananchi wakifurika katika Banda la Tume ya Madini kujionea kwa karibu jiwe hilo la thamani linalopatikana Tanzania pekee duniani pamoja na kupata elimu kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya madini.

Maonesho hayo yenye kaulimbiu ya “Fahari ya Tanzania” yalianza rasmi Juni 28, 2026 na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13 2026, sambamba na maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa maonesho hayo makubwa ya biashara nchini.

Miongoni mwa wananchi waliotembelea banda hilo ni Nuru Maliki, ambaye amesema ameridhishwa na elimu na huduma alizopata pamoja na nafasi ya kujionea madini mbalimbali ambayo awali alikuwa akiyasikia kupitia historia na simulizi pekee.

“Nimepata huduma nzuri sana na fursa ya kujionea madini mbalimbali, hususan Tanzanite na madini mengine yanayopatikana hapa nchini. Kuna baadhi nilikuwa nikiyasikia tu katika historia, lakini leo nimeyaona kwa macho yangu,” amesema.

Kwa upande wake, Eveline Natai amesema maonesho hayo yameongeza uelewa wake kuhusu fursa za uwekezaji katika sekta ya madini na kumhamasisha kuanza kupanga namna ya kushiriki katika shughuli za sekta hiyo.

“Nimefurahishwa kuona madini mbalimbali na kupata taarifa kuhusu fursa za uwekezaji zilizopo. Nitajipanga kuingia katika sekta hii. Serikali iendelee kutoa elimu kwa Watanzania ili watu wengi zaidi wajifunze na kunufaika na fursa zinazotokana na rasilimali za madini,” amesema.

Akitoa elimu kwa wananchi, Mjiolojia kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Abbas Mruma, amesema maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwaelimisha wananchi kuhusu rasilimali za madini, matumizi yake pamoja na fursa mbalimbali za kiuchumi zinazotokana na sekta hiyo.

Naye Mjiolojia Mwandamizi kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mirerani, Seleman Khamis, amesema thamani ya madini ya Tanzanite hupimwa kwa kuzingatia vigezo vinne muhimu ambavyo ni rangi, uzito, ubora na umbo.

Amefafanua kuwa rangi kuu za Tanzanite ni bluu na zambarau, huku akibainisha kuwa madini hayo yanapatikana Tanzania pekee katika eneo la Mirerani, Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, jambo linaloyafanya kuwa miongoni mwa madini ya vito yenye upekee na thamani kubwa zaidi katika soko la kimataifa.

Mvuto mkubwa wa Tanzanite katika maonesho hayo umeendelea kuthibitisha nafasi ya Tanzania kama kitovu cha madini ya vito duniani, huku wananchi wakizidi kuhamasika kufahamu zaidi kuhusu sekta ya madini na fursa zake za uwekezaji na maendeleo ya kiuchumi.

Wakati huohuo, viongozi mbalimbali wametembelea banda la Tume ya Madini, akiwemo Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Dkt. Venance Mwasse.

Viongozi hao wamepongeza kazi kubwa ya utoaji elimu na uhamasishaji kuhusu sekta ya madini inayotekelezwa na Tume ya Madini, wakieleza kuwa imechangia kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu fursa zilizopo katika sekta hiyo na mchango wake kwa maendeleo ya uchumi wa taifa.
Posted by MROKI On Friday, July 03, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo