Nafasi Ya Matangazo

July 08, 2025

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy akiwasili kwenye Banda la REA katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam Julai 7, 2025
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (kushoto) akipata maelezo kuhusiana na bidhaa za Nishati Safi ya Kupikia zinazosambazwa na Kampuni ya Jicho Chanya kutoka kwa Afisa Masoko wa kampuni hiyo, Ibrahim Kikoti kwenye Banda la REA katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam Julai 7, 2025.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (kushoto) akiwa amebeba bidhaa ya kuni poa inayozalishwa kutokana na mabaki ya  miwa na Kampuni ya Hanny G Investment ya Arusha wakati akipata maelezo kuhusiana na kuni hiyo kutoka kwa Afisa Masoko wa kampuni, Neema Chiva kwenye Banda la REA katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam Julai 7, 2025.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (kulia) akipata maelezo kuhusiana na bidhaa mbalimbali za nishati safi ya kupikia zilizoandaliwa kwa teknolojia iliyoboreshwa katika Banda la REA kwenye Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam Julai 7, 2025.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Mratibu wa Miradi wa Kampuni ya TaTEDO-SESO inayojihusisha na Uendelezaji wa Teknolojia na Huduma za Nishati Endelevu, Shima Sago kuhusiana na bidhaa za Nishati Safi ya Kupikia zinazozalishwa na kampuni hiyo wakati wa Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam katika Banda la REA Julai 7, 2025


Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy amesema Wakala umejizatiti kuhakikisha 80% ya Watanzania wanatumia Nishati Safi ya Kupikia ifikapo mwaka 2034 kama ilivyoelekezwa katika Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.

Amebainisha hayo Julai 07, 2025 katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam ndani ya Banda la Maonesho la Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

“REA inalo jukumu la kuhakikisha maeneo yote ya vijijini yanapata aina zote za nishati safi zinazotumika nchini ikiwemo; umeme, nishati safi ya kupikia pamoja na bidhaa za mafuta ya petroli na dizeli na hili linafanyika kupitia miradi mbalimbali ambayo baadhi imekamilika na mingine ipo katika hatua tofauti tofauti za utekelezaji,” amebainisha Mha. Saidy.

Alisema Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia umeelekeza ifikapo mwaka 2034; angalau 80% ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia na REA ni miongoni mwa taasisi zilizopewa jukumu la kuhakikisha lengo hilo linafikiwa.

Alibainisha kuwa kwa sasa takriban asilimia 96 ya wananchi maeneo ya vijijini wanatumia kuni na mkaa kupikia na kwamba jukumu lililopo ni kuhakikisha wananchi hao wanaachana na matumizi ya nishati zisizo salama na kuanza kutumia nishati safi na salama.

Alitaja hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na REA ikiwemo uhamasishaji na uelimishaji wananchi kufahamu athari za kutumia nishati isio salama pamoja na kuwafahamisha faida za kutumia nishati safi ya kupikia, kuwarahisishia wananchi upatikanaji wa bidhaa za nishati safi jirani na maeneo yao na kuwezesha teknolojia za nishati yenyewe.

“Kuna dhana imejengeka kwamba nishati safi ya kupikia ni gharama kuliko nishati zingine dhana ambayo haina ukweli kwa 100% kwani kwa sasa kuna teknolojia zilizoboreshwa ambazo zinazuia upotevu wa nishati wakati wa kupika hivyo kuwapunguzia gharama watumiaji," alifafanua Mha. Saidy.

Aliongeza kuwa watu wengi hawaangalii gharama nyingine kama muda wanaotumia kusaka kuni na madhila mengine wanayokutana nayo huko porini wakati wakisaka kuni.

Alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha REA kutekeleza jukumu la kusimamia upatikanaji wa nishati safi ya kupikia hasa ikizingitiwa kuwa yeye ni kinara wa nishati safi ya kupikia.

Alibainisha baadhi ya mafanikio ambayo yamepatikana tangu kuanza kutekeleza mkakati huo wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ambayo ni pamoja na kuwezesha wananchi maeneo mbalimbali vijijini kuhama kupitia ruzuku iliyotolewa ya asilimia 50 kwenye majiko ya gesi ya kilo 6 na vichomeo vyake.

“Serikali inayoongozwa na Mhe. Rais Samia ilitoa ruzuku ya 50% kwenye mitungi ya gesi ya kupikia ipatayo 452,000 ambayo imeshaanza kusambazwa kwenye mikoa yote Tanzania Bara na zoezi linaendelea; sambamba na mitungi 110,000 ambayo ilisambazwa mwaka juzi kupitia Wabunge kwenye majimbo yao,” alisema Mhandisi Saidy.

Sambamba na hilo, Mha. Saidy alibainisha kuwa REA imewezesha Jeshi la Magereza ambapo kwa sasa magereza zote 129 zimehama kutoka kwenye matumizi ya nishati zisizo salama, na hivi karibuni REA imekuja na mpango wa kuwezesha Maafisa wa Jeshi la Magereza nao kutumia nishati safi ya kupikia katika familia zao.

“Kama mtakumbuka Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alielekeza taasisi zinazohudumia zaidi ya watu 100 zianze kutumia nishati safi ya kupikia na hili tunatekeleza na tunatarajia kuzifikia zaidi ya taasisi 400 katika mwaka huu wa fedha. Tulianza na Jeshi la Magereza, Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na takriban shule 53,” alibainisha Mha. Saidy.

Mhandisi Saidy vilevile alibainisha mradi wa mikopo nafuu wa kuwezesha ujenzi na uendeshaji wa vituo vya mafuta ya petroli na dizeli ulioanzishwa na REA ambao umelenga kuwasogezea wananchi wa vijijini huduma kwa gharama nafuu na ubora unaokubalika.
Posted by MROKI On Tuesday, July 08, 2025 No comments

July 07, 2025






Rais wa Zanzibar na mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Hussein Ali Mwinyi leo 7 Julai, 2025 ametembelea banda la Wizara ya Nishati  kwenye maonesho ya biashara ya kimataifa maarufu kama sabasaba jijini Dar es salaam

Akiwa kwenye banda la Wizara ya Nishati Mhe Mwinyi alipokelewa na Mkuu wa kitengo cha  Mawasiliano Serikalini Bi Neema Chalila Mbuja, ambapo alimweleza juu ya hatua za utekelezaji zilizofikiwa kwenye utekelezaji wa mkakati wa Taifa wa nishati safi ya kupikia na kuongeza kuwa ajenda hiyo ni utekelezaji wa azimio la Mhe Rais Samia kama kinara wa nishati safi ya kupikia.

Amesema Wizara ya Nishati kupitia taasisi zilizopo chini ya Wizara zimekuwa zikitekeleza kwa vitendo ajenda hiyo kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ambae ni kinara wa nishati safi ya kupikia kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2034 asilimia 80 ya watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia.

Wizara ya nishati tayari imezindua mikakati miwili ya nishati safi ya kupikia na ule wa mawasiliano ili kuwezesha utekelezaji wa ajenda ya nishati safi ya kupikia kwa vitendo
Posted by MROKI On Monday, July 07, 2025 No comments

 BOFYA LINK HII KUONA MATOKEO 
Posted by MROKI On Monday, July 07, 2025 No comments





Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Dkt. Venance Mwasse, ameipongeza Tume ya Madini kwa mafanikio makubwa ya kuvuka lengo la makusanyo ya mapato kwa mwaka wa fedha 2024/2025, ambapo imekusanya kiasi cha shilingi trilioni 1.071 dhidi ya lengo la shilingi trilioni 1.

Akizungumza wakati wa ziara yake katika banda la Tume ya Madini kwenye Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba), yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu J.K. Nyerere, Dar es Salaam, Dkt. Mwasse amesema mafanikio hayo ni matokeo ya usimamizi makini, matumizi ya teknolojia, na ubunifu unaoendelea ndani ya Tume.

“Mafanikio haya ni uthibitisho kuwa sekta ya madini ni nguzo imara ya uchumi wa nchi. Kama alivyosema Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, madini siyo nyanya tuziache zioze – yanapaswa kuchimbwa kwa weledi na kwa kutumia wataalamu wa ndani. Tume ya Madini imetekeleza hilo kwa vitendo,” amesisitiza Dkt. Mwasse.

Aidha, ameeleza kuwa utekelezaji wa mabadiliko ya sheria ya madini umechangia kwa kiasi kikubwa mafanikio haya, hususan kupitia sera ya Ushiriki wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), inayotoa fursa kwa wazawa kushiriki kikamilifu katika huduma, ajira na biashara zinazohusiana na sekta ya madini. 

Amebainisha kuwa STAMICO ni miongoni mwa mashirika yaliyonufaika moja kwa moja na utekelezaji wa sera hiyo.

Kwa upande wake, Afisa Sheria Mwandamizi kutoka Tume ya Madini, Bw. Damian Kaseko, ameeleza kuwa Tume ilianzishwa rasmi mwaka 2017 chini ya Sheria ya Madini Na. 7, ikiwa na jukumu la kusimamia kikamilifu shughuli zote za madini nchini. Tangu kuanzishwa kwake, Tume imeendelea kuimarika na kuwa chombo madhubuti katika kusimamia rasilimali za madini kwa manufaa ya Taifa.

Makusanyo haya ya kihistoria ni kielelezo cha mafanikio ya kimkakati katika sekta ya madini na mchango wake mkubwa katika kukuza uchumi wa Taifa, huku yakionesha uwezekano mkubwa wa sekta hiyo kuwa chachu ya maendeleo endelevu kwa Watanzania wote.
Posted by MROKI On Monday, July 07, 2025 No comments

July 06, 2025





Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhandisi Cyprian Luhemeja, ameipongeza Tume ya Madini kwa hatua yake ya kutoa leseni za uchimbaji wa madini kwa wachimbaji wadogo huku ikizingatia vigezo vya utunzaji wa mazingira. 

Ameitaka Tume kusimamia kikamilifu utekelezaji wa masharti ya leseni ili kuhakikisha mazingira yanalindwa ipasavyo.

Akizungumza wakati wa ziara yake katika Banda la Tume ya Madini katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, jijini Dar es Salaam, Mhandisi Luhemeja amesema hatua hiyo ni muhimu katika kuondoa uchimbaji holela na kupunguza uharibifu wa mazingira.

“Zamani wachimbaji wadogo wa madini walikuwa wanaingia kwa nguvu kwenye maeneo ya uchimbaji bila kufuata utaratibu wowote, na mara nyingi kuchimba bila kuwa na leseni. Hali hii ilisababisha uharibifu mkubwa wa mazingira,” amesema Mhandisi Luhemeja.

Kwa upande wake, Afisa Sheria Mwandamizi wa Tume ya Madini, Bw. Damian Kaseko, amesema Tume inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Madini, ikiwa ni pamoja na kutoa leseni za uchimbaji, kusimamia biashara ya madini nchini, pamoja na kusuluhisha migogoro ya ardhi  katika maeneo ya uchimbaji wa madini.

Bw. Kaseko ameeleza kuwa utoaji wa leseni  za madini kwa wachimbaji wadogo unazingatia taratibu madhubuti, ikiwemo kuwasilisha Mpango wa Utunzaji na Uendelezaji wa Mazingira (Environmental Protection Plan - EPP) kabla ya kuidhinishiwa leseni ya uchimbaji katika eneo husika.
Posted by MROKI On Sunday, July 06, 2025 No comments

July 05, 2025











Wizara ya Madini kwa kushirikiana na taasisi zake inaendelea kutoa elimu ya kina kuhusu shughuli za madini katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.

Kupitia banda la Wizara hiyo, wananchi, wawekezaji na wanafunzi wanapata fursa adhimu ya kujifunza kwa undani kuhusu sekta ya madini nchini, kuanzia shughuli za uchimbaji, uchenjuaji, usimamizi wa mazingira, hadi masuala ya usafirishaji wa madini na masoko ya madini.

Akizungumza katika maonesho hayo, Mjolojia kutoka Wizara ya Madini, Neema Masinde, amesema kuwa lengo la ushiriki wa Wizara na taasisi zake ni kuhakikisha wananchi wanaelewa mchango mkubwa wa sekta ya madini katika kukuza uchumi wa nchi pamoja na kuwapa maarifa sahihi kuhusu fursa zilizopo ili waweze kushiriki kikamilifu katika shughuli za sekta hiyo.

“Tunatoa elimu ili kuwahamasisha wananchi washiriki kwa tija katika sekta hii muhimu, kwani ni miongoni mwa sekta zinazochangia kwa kiasi kikubwa katika Pato la Taifa (GDP) pamoja na kutoa ajira kwa Watanzania,” amesema Masinde.

Maonesho ya Sabasaba mwaka huu yamevutia washiriki kutoka zaidi ya nchi 40, huku banda la Wizara ya Madini likitajwa kuwa miongoni mwa mabanda yaliyovutia idadi kubwa ya wageni kutokana na mvuto wa sampuli mbalimbali za madini na elimu ya moja kwa moja inayotolewa na wataalam waliobobea.
Posted by MROKI On Saturday, July 05, 2025 No comments
Posted by MROKI On Saturday, July 05, 2025 No comments






WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa leo Julai 05, 2025 ameshiriki katika mbio za Great Ruaha Marathon (GRUMA 2025) zilizoanzia na kuishia kwenye eneo la Ibuguziwa, ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Ruaha.

Akizungumza katika tukio hilo, Mheshimiwa Majaliwa ameto wito kwa waratibu wa mbio hizo kuweka mikakati ya kuzifanya ziwe za kimataifa ili ziweze kukutanisha raia wa mataifa mbalimbali duniani.

Lengo la Mbio hizo ni kuhamasisha uhifadhi wa mazingira  wa Mto Ruaha Mkuu ambao ni uti wa mgongo wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha na kuifanya jamii kuona umuhimu wa kulinda vyanzo vya maji na kuhimiza matumizi endelevu ya rasilimali za asili.
Posted by MROKI On Saturday, July 05, 2025 No comments






WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema kuwa huduma za fidia kwa wafanyakazi si suala la hiari bali ni haki ya msingi ya mfanyakazi, inayopaswa kulindwa, kuendelezwa na kusimamiwa kwa weledi na uwajibikaji wa hali ya juu.
 
Amesema kuwa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuendelea kuhakikisha kuwa maendeleo ya nchi yanakwenda sambamba na ulinzi wa haki na ustawi wa wafanyakazi wake.
 
Amesema hayo leo (Ijumaa, Julai 05, 2025) alipomwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika ufunguzi wa maadhimisho ya miaka kumi ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), katika kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
 
“Waajiri, wafanyakazi na Serikali tunapaswa kuendelea kushirikiana kwa dhati katika kuhakikisha kuwa kazi inaendelea kwa tija, na wakati huo huo, wafanyakazi wanalindwa dhidi ya madhila yanayotokana na kazi wanazozifanya kila siku.”
 
Aidha, Mheshimiwa Majaliwa ametoa wito kwa waajiri wote nchini kuhakikisha wanazingatia kikamilifu matakwa ya Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi ikiwa ni pamoja na kujisajili katika Mfuko, kuwasilisha michango kwa wakati, na kutoa taarifa mapema pale wafanyakazi wanapopata madhila yanayotokana na kazi. ” Kutotimiza wajibu huu ni kutotendea haki ustawi wa wafanyakazi na kulemaza ufanisi wa Mfuko.”
 
Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Rais Dkt. Samia wakati wote ametoa miongozo ya kuhakikisha Serikali inaboresha maslahi ya watumishi wa umma, kuboresha mazingira yakufanyia kazi na Utumishi wa umma kuendeshwa kwa kuzingatia misingi ya utawala bora.
 
Kwa Upande wake Waziri wa Nchi- Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Ridhiwani Kikwete amesema kuwa katika jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita kuendelea kuboresha ustawi wa Wafanyakazi walioumia kazini, Serikali imekwishatangaza kwenye Gazeti la Serikali Ongezeko la malipo ya fidia ya kila mwezi kwa wanufaika wa Mfuko wa WCF kwa kati ya asilimia 3 hadi asilimia 31 kutegemea mnufaika alistahili kulipwa kuanzia lini.
 
Ameongeza kuwa WCF imeishi falsafa ya 4R ya Rais Samia Suluhu Hassan ambapo utendaji mzuri wa mfuko huo umeleta mageuzi chanya ya kiuchumi kwa wafanyakazi na kuleta maelewano kati ya wafanyakazi na waajiri. “Kwa kiasi kikubwa hii imewajengea ari ya kufanya kazi kwa bidii na kuongeza uzalishaji hasa tunapoendelea kujenga uchumi wa viwanda”.
 
Kwa Upande wake Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma ameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupunguza kiwango cha uchangiaji kwa waajiri wa sekta binafsi kutoka asilimia moja wakati Mfuko unaanzishwa hadi asilimia sifuri nukta tano (0.5%) hivi sasa. Hiki kilikuwa ni kilio cha waajiri cha muda mrefu
 
“Tunaipongeza Serikali pia kwa kuwezesha kupunguza kiwango cha riba ya ucheleweshaji wa michango kwa waajiri kutoka asilimia kumi hadi asilimia mbili kwa mwezi. Hatua hii imeongeza imani ya wawekezaji kwa WCF na Serikali kwa ujumla”.
 
Naye Mwakilishi mkazi wa Kanda ya Afrika Mashariki wa Shirika la Kazi (ILO) Bi. Caroline Mugalla amesema kuwa katika maadhimisho ya miaka 10 ya WCF, jamii inapaswa kukumbuka kuwa kinga ya jamii sio matumizi yasiyo na tija bali ni uwekezaji katika haki, uzalishaji wenye tija unaolifanya Taifa kuwa thabiti. “Tuendelee kujenga Tanzania ambayo kila mfanyakazi anapata huduma stahiki”
 
Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) Suzanne Ndomba-Doran amesema kuwa Chama hicho kwa kushirikiana na WCF wamekuwa wakitoa mafunzo na kuhamasisha waajiri kuhusu fidia kwa wafanyakazi.
 
“Mafunzo haya yameongeza uelewa na kuchangia kupunguza ajali na magonjwa au vifo vinavyotokana nakazi. Tangu mwaka 2016-2024, ATE kwa kushirikiana na WCF tumefanikiwa kutoa mafunzo mara 21 katika Maudhui Kuhusu Sheria ya Fidia kwa Wafanyakaziya mwaka 2008 na kanuni zake, Fidia Mahali pa Kazi, Ajali na Magonjwa.“
 
Naye, Naibu Katibu Mkuu wa TUCTA Rehema Ludanga ameipongeza WCF kwa kuimarisha matumizi ya mifumo ya teknolojia ya habari na Mawasiliano ambayo imeweza kuongeza ufanisi na kuhudumia wanachama wake.
 
“Tunaipongeza sana Serikali kwa kuendelea kuipa nguvu WCF sisi TUCTA tunaahi
di kuendelea kushiriana nao ili mafanikio yazidi kwenda mbele na tunaipongeza kwa kufikia miaka 10 ya faida”
 
Katika hafla hiyo Mheshimiwa Majaliwa alizindua fao la utengamao ambalo litamuwezesha mfanyakazi aliyepata madhara kazini kurejeshwa ofisini na kupatiwa kazi mbadala inayoendana na hali yake.
Posted by MROKI On Saturday, July 05, 2025 No comments









Naibu katibu Mkuu Wizara ya Nishati anayeshughulikia umeme na nishati Jadidifu, Dkt Khatibu Kazungu leo 04 Julai, 2025 amepokea magari mawili yatakayotumika kwa ajili ya kampeni ya kuhamasisha na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia chini ya kampeni ya nishati safi ya kupikia Okoa Maisha na Mazingira itakayoendeshwa nchi nzima na Wizara ya nishati kwa kushirikiana na UNCDF.

‘’ Ajenda ya Nishati safi ya kupikia ni ajenda ya Dunia na sisi Wizara ya Nishati tuko tayari kwa utekelezaji ili kumuunga mkono Mhe. Rais Samia’’ Amesema Dkt. Kazungu

Aidha, ameishukuru Umoja wa Ulaya, na UNCDF kwa kutekeleza mradi wa nishati safi ya kupikia chini ya mfuko wa Cook fund kwa kuwa umesaidia kubadili maisha na mitazamo ya wananchi kuhusu  utekelezaji wa miradi ya Nishati safi.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo,  Balozi wa Umoja wa Ulaya Mhe. Balozi Christine Grau amesema umoja wa Ulaya uko tayari kuendelea kuisaidia Tanzania kwenye utekelezaji wa Nishati safi ya kupikia na tayari EU imetoa kiasi cha Euro Milioni 19.4 sawa na shilingi Bilioni 59 kutekeleza miradi ya nishati safi ya kupikia kwa mikoa ya Dar es salaam, Dodoma, Pwani, Morogoro  na Mwanza. 

Kuhusu magari amesema magari hayo mawili yana thamani ya Euro 130,000 na amewataka wizara ya Nishati kuhakikisha wananchi wa vijijini wanafikiwa na nishati safi ya kupikia

Tanzania inajipanga kutekeleza kwa vitendo mkakati wa Taifa wa Nishati safi ya kupikia chini ya mkakati wa Mawasiliano wa Taifa ili kutoa elimu kwa wananchi na kufikia lengo la Serikali la asilimia 80 ya watanzania kuanza kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.
Posted by MROKI On Saturday, July 05, 2025 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo