Nafasi Ya Matangazo

November 14, 2025


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika hafla iliyofanyika Chamwino Ikulu jijini Dodoma Novemba 14, 2025.






Posted by MROKI On Friday, November 14, 2025 No comments

November 13, 2025

Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini MHE. DANIEL BARAN SILLO amechaguliwa na Wabunge kushika nafasi ya Naibu Spika wa Bunge.

Uchaguzi wa Mhe. Sillo ulifanyika muda mfupi baada ya kuthibitishwa na Bunge kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mwigulu Nchemba.

Sillo amechaguliwa kwa kura za ndio 371 kati ya kura 371 zilizopigwa na Wabunge. 

Tayari Naibu Spika ameshakula Kiapo cha kushika nafasi hiyo na anataraji kufanya mahojiano na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kuahirishwa kwa kikao cha Bunge hii leo Novemba 13, 2025 katika lango kuu la kuingilia bungeni. 

Posted by MROKI On Thursday, November 13, 2025 No comments

BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lkimemthibitisha kwa kauli moja Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu Mbunge wa Jimbo la Iramba Magharibi kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 
Mwigulu, mtaalamu wa uchumi wa Tanzania na mwanasiasa wa Chama cha Mapinduzi (CCM), ambaye amehudumu katika nyadhifa mbalimbali serikalini ikiwepo kuwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Waziri wa Sheria na Katiba na Waziri wa Fedha nafasi aliyoishika hadi anateuliwa kuwa Waziri Mkuu.

Aidha kwa upande wa siasa katika Chama chake cha Mapinduzi alipata kuwa Katibu wa Uchumi na Fedha wa CCM Taifa, na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara.

Dkt. Mwigulu aliingia Bungeni kwa mara ya kwanza 2010 akimtoa mtangulizi wake Mhe. Juma Hassan Killimbah na kuendelea kuchaguliwa na wananchi Iramba Magharibi katika chaguzi zote zinazofuata ukiwepo wa mwaka 2025. 

Aliwahi kuwa miongoni mwa wanachama wa Chama cha Mapinduzi walioonesha nia na kuchukua fomu za kuwania nafasi ya kugombea nafasi ya Rais kupitia Chama hicho.

Mwigulu anakuwa Waziri wa 12 tangu kupatikana kwa uhuru wa Tanzania na anakua mrithi wa Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Majaliwa Kasim Majaliwa. 
Waziri Mkuu Mteule, Dkt. Mwigulu Nchemba akitoa neno la shukurani baada ya kuthibitishwa na Bunge kwa Waziri Mkuu, Novemba 13, 2025. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Meteule, Dkt. Mwigulu Nchemba akipokea maua kutoka kwa mtumishi wa Ofisi Binafsı ya Waziri Mkuu, Tecla Kilangi  alipowasili kwenye Makazi ya Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma na kupokelewa na watumishi Ofisi ya Waziri Mkuu, Novemba 13, 2025. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).
Waziri Mkuu Mteule, Dkt. Mwigulu Nchemba akisalimiana na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Dkt. Jim Yonaz alipowasili kwenye Makazi ya Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma, Novemba 13, 2025. Kushoto ni Naibu Katibu, Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Dkt.  James Kilabuko.


Waziri Mkuu Mteule, Dkt. Mwigulu Nchemba akipongezwa na wabunge baada ya kuthibitishwa  na Bunge kuwa Waziri Mkuu, Novemba 13, 2025.

Posted by MROKI On Thursday, November 13, 2025 No comments





Na Mwandishi Wetu, Simiyu
Serikali imesema itaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) inayotekelezwa na kampuni za uchimbaji madini nchini, ili kuhakikisha wananchi wanaoishi jirani na migodi wananufaika moja kwa moja na shughuli za uchimbaji madini.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Simiyu, Mayigi Makolobela, alisema hayo hivi karibuni alipokagua utekelezaji wa miradi ya CSR inayofanywa na kampuni za uchimbaji madini katika mkoa huo, akibainisha kuwa miradi hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa kuboresha huduma za kijamii ikiwemo elimu, afya na miundombinu ya umeme.

“Serikali inatambua mchango mkubwa wa sekta ya madini katika kukuza uchumi wa nchi na kuboresha maisha ya wananchi. Ndiyo maana tunasisitiza kampuni zote za uchimbaji, zikiwemo zinazomilikiwa na wachimbaji wadogo, kutekeleza wajibu wao wa kijamii kupitia miradi ya CSR ili jamii inayoishi jirani na migodi inufaike moja kwa moja na rasilimali hizo,” alisema Makolobela.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni ya EMJ Mining iliyopo eneo la Dutwa mkoani Simiyu, Masanga Silanga, alisema kampuni hiyo inajihusisha na uchimbaji wa dhahabu kwa ushirikiano na wawekezaji kutoka China, jambo lililoongeza ufanisi na teknolojia katika shughuli zao za uchimbaji.

Alisema kampuni hiyo huzalisha wastani wa kilo 10 za dhahabu kwa mwezi endapo kuna upatikanaji mzuri wa mwamba wenye madini (mbale), ingawa wakati mwingine hukumbwa na changamoto ya upatikanaji wa mwamba kutokana na baadhi ya maeneo kuwa na mishororo midogo ya dhahabu (narrow vein).

Silanga alibainisha kuwa kampuni yake imetekeleza miradi kadhaa ya CSR ikiwemo kutoa madawati 50 na matofali 2,000 kwa Shule ya Msingi Dutwa, mashine za kuchapisha (printer) na nakala (photocopy) kwa taasisi za elimu, pamoja na mchango wa matofali 2,000 kwa Hospitali ya Nguno.

“Tayari tumewekeza zaidi ya Dola 50,000 katika miradi ya CSR, ikiwemo mradi wa kuvuta umeme kutoka Dutwa hadi vijiji vya jirani ambavyo awali havikuwa na huduma ya umeme,” alisema Silanga.

Naye Meneja wa Mgodi huo, Noah Wang, alisema changamoto kubwa wanayokabiliana nayo kwa sasa ni upungufu wa mwamba wenye madini (mbale), hali inayosababisha baadhi ya mitambo kusimama na kupunguza uzalishaji.

“Mitambo yetu ina uwezo wa kuchakata hadi tani 500 za mwamba kwa siku, lakini kwa sasa hatupati kiwango hicho, jambo linalolazimisha baadhi ya mitambo kuzimwa mara kwa mara. Kwa sasa shaft moja pekee ndiyo inaendelea na kazi, hivyo uzalishaji umeshuka kwa kiasi kikubwa,” alisema Wang.

Aliongeza kuwa kampuni hiyo imeajiri jumla ya wafanyakazi 48, wakiwemo 30 wazawa na 18 raia wa China, wanaofanya kazi kwa mfumo wa kupokezana (shift system).
Posted by MROKI On Thursday, November 13, 2025 No comments

November 12, 2025

 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akikata utepe wakati wa uzinduzi wa kitengo cha usafishaji damu (dialysis unit) ambacho kinatoa huduma kwa wagonjwa wa moyo wenye matatizo ya figo wanaotibiwa katika taasisi hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na wafanyakazi wa kitengo cha kusafisha damu (dialysis unit) ambacho kinatoa huduma kwa wagonjwa wa moyo wenye matatizo ya figo wanaotibiwa katika taasisi hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa taasisi hiyo mara baada kuzindia kitengo cha kusafisha damu (dialysis unit) kinachotoa huduma kwa wagonjwa wa moyo wenye matatizo ya figo wanaotibiwa katika taasisi hiyo.
Picha na JKCI
******************
Na Mwandishi Maalumu – Dar es Salaam
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imezindua rasmi kitengo kipya cha kusafisha damu (dialysis unit) kwa wagonjwa wa moyo wanaopata matatizo ya figo hatua inayolenga kuboresha huduma za tiba jumuishi kwa wagonjwa hao.
Kitengo hicho chenye mashine za kisasa zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 200 kilichozinduliwa jana kimeanza kutoa huduma mara moja baada ya kuzinduliwa huku kikiwa na uwezo wa kusafisha damu kwa zaidi ya wagonjwa nane kwa siku.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema uanzishwaji wa kitengo hicho umetokana na ongezeko la wagonjwa wa moyo wanaokabiliwa na matatizo ya figo hali iliyokuwa ikiwalazimu kwenda kupata huduma hiyo katika hospitali nyingine.
“Wagonjwa wengi wa moyo hupata matatizo ya figo kutokana na hali zao za kiafya au matibabu wanayopata. Awali walikuwa wanachelewa kupata huduma kwa sababu ya wingi wa wagonjwa katika hospitali nyingine, lakini sasa huduma hiyo itapatikana hapa hapa JKCI”, alisema Dkt. Kisenge.
Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo aliongeza kuwa kuanzishwa kwa kitengo hicho ni sehemu ya mpango wa JKCI wa kuhakikisha huduma zote muhimu kwa wagonjwa wa moyo zinapatikana chini ya paa moja, hatua itakayoongeza ufanisi na kurahisisha matibabu.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alisema awamu ya kwanza ya kitengo hicho ina vitanda viwili huku mpango wa muda mrefu ukiwa ni kuongeza hadi zaidi ya vitanda 20 ili kuhudumia wagonjwa wengi zaidi.
“Tunafurahia kuona huduma hii inaanza rasmi JKCI. Wagonjwa wetu sasa watapata huduma za moyo na figo mahali pamoja jambo litakalopunguza usumbufu na kuboresha matokeo ya matibabu”, alisema Dkt. Angela ambaye pia ni daktari bingwa wa usingizi na wagonjwa mahututi.
Naye Daktari bingwa wa figo kutoka Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) Daniel Msilanga ambaye anatoa huduma za matibabu ya figo kwa wagonjwa wanaotibiwa katika taasisi hiyo  alisema kufunguliwa kwa kitengo hicho kutarahisisha upatikanaji wa huduma za figo kwa wagonjwa wa moyo ambao awali walikuwa wakihangaika kupata huduma hiyo nje ya taasisi.
“Tumeona ongezeko kubwa la wagonjwa wenye matatizo ya moyo na figo. Kitengo hiki kitasaidia kupunguza msongamano katika hospitali nyingine na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma”, alisema Dkt. Msilanga.
Kwa upande wake msimamizi wa kitengo hicho cha figo Daktari bingwa wa usingizi na wagonjwa mahututi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Nai Kipuyo alisema kitengo hicho kinaendeshwa na timu ya wataalamu waliobobea wakiwemo madaktari, wauguzi na mafundi sanifu waliopata mafunzo maalum ndani na nje ya nchi kwa ushirikiano na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Uzinduzi wa kitengo hicho umeenda sambamba na maadhimisho ya wiki ya magonjwa yasiyoambukiza ambapo JKCI imetoa wito kwa wananchi kufanya uchunguzi wa mara kwa mara wa afya zao, hasa magonjwa ya moyo na figo ambayo yanaendelea kuongezeka kwa kasi duniani.
Posted by MROKI On Wednesday, November 12, 2025 No comments
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi akizungumza katika Mkutano wa 26 wa Baraza Kuu la Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism) Novemba 9, 2025, jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Katibu Mkuu wa Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism) anayemaliza muda wake, Zurab Pololikashvili akizungumza katika Mkutano wa 26 wa Baraza Kuu la Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism) Novemba 9, 2025, jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Baadhi ya wajumbe kutoka nchi mbalimbali wakimsikiliza Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza katika Mkutano wa 26 wa Baraza Kuu la Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism) Novemba 9, 2025, jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, akiongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa 26 wa Baraza Kuu la Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism) kilichoanza leo Novemba 9, 2025, jijini Riyadh, Saudi Arabia, ameihakikishia dunia kuwa hali ya utalii na amani viko imara nchini Tanzania kufuatia machafuko yaliyotokea wakati na baada ya uchaguzi katika baadhi ya maeneo.
 
Dkt. Abbasi ameyasema hayo leo wakati akichangia Taarifa ya Utekelezaji ya Mwaka ya Taasisi hiyo ambapo pia Tanzania ilinufaika na programu mbalimbali ikiwemo kuandaa Mkutano wa Dunia Kanda ya Afrika wa Utalii wa Vyakula uliofanyika Arusha April mwaka huu na kufadhiliwa baadhi ya programu za utunzaji wa mazingira katika maeneo ya Safu za Milima ya Usambara.
 
“Mheshimiwa Mwenyekiti wa Baraza hili baada ya kumpongeza Katibu Mkuu na  Sekretarieti ya UN Tourism kwa utekelezaji ambao Tanzania pia imenufaika, naomba kutumia fursa hii kutoa taarifa kuwa Tanzania ni salama baada ya kadhia iliyojitokeza wakati wa uchaguzi.
 
“Serikali imefanya jitihada na kurejesha nchi yetu katika hali ya utulivu na hivyo kuendelea kuwa salama kwa watalii na vivutio vyetu vyote mnavyovijua viko salama. Nawakaribisha wajumbe wa Mkutano huu na wadau wengine wa utalii kuja na kuendelea  kutembelea nchi hii ambayo ni kivutio bora Afrika kwa utalii wa safari,” alisema Dkt. Abbasi.
 
Aidha, mbali ya Tanzania kuwa miongoni mwa  nchi 32 pekee kati ya wanachama wa Umoja huo wanaofikia 160 kuwa Mjumbe wa Kamati ya Utendaji (Executive Committe), leo pia Baraza Kuu hilo limeipitisha Tanzania kuwa Mjumbe wa Kamati ya Kuhakiki wanachama (UN Tourism Credentials Committe).
 
Mkutano huo unaendelea jijini hapa na pamoja na mambo mengine utajadili kuhusu matumizi ya akili mnemba katika kutangaza utalii na pia jioni hii umemthibitisha Sheikha Nasser Al Nowais kutoka UAE kuwa Katibu Mtendaji mpya wa taasisi hiyo muhimu kwa sekta ya utalii duniani.
Katibu Mkuu wa Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism) anayemaliza muda wake Zurab Pololikashvili (wa tano kutoka kushoto mstari wa mbele) katika picha ya pamoja na wajumbe nchi wanachama wa Shirika la Utalii Duniani mara baada ya kufungua Mkutano wa 26 wa Baraza Kuu la Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism) Novemba 9, 2025, jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Posted by MROKI On Wednesday, November 12, 2025 No comments

Na Mwandishi Wetu, Simiyu
WACHIMBAJI Wadogo wa Madini wa Mkoa wa Simiyu wameiomba Serikali pamoja na taasisi za kifedha kuwaunga mkono kwa kuwapatia umeme wa kudumu na mikopo yenye masharti nafuu, wakisema changamoto hizo zimekuwa kikwazo kikubwa katika kuongeza uzalishaji wa madini, hususan dhahabu.

Mmoja wa wachimbaji wanawake kupitia Chama cha Wachimba Madini Wanawake Tanzania (TAWOMA) mkoani humo, Anisia Japhet, amesema wamekuwa wakitumia gharama kubwa kuendesha mitambo kutokana na kutegemea nishati ya dizeli.

“Tunatumia dizeli ambayo ni ghali. Lita 80 zinamalizika ndani ya saa 24. Tungepata umeme wa kudumu, tungepunguza gharama na kuongeza tija,” amesema Anisia.

Ameongeza kuwa uchimbaji si kazi ya wanaume pekee bali ni fursa yenye manufaa makubwa kwa wanawake wanaojituma.

“Nikiwa mwanamke, nimefanikiwa kusomesha watoto na kuendesha maisha yangu kupitia uchimbaji. Kila mwezi tunapata wastani wa viroba 100 vya mawe, na kila kiroba kinaweza kutoa gramu moja au zaidi za dhahabu,” ameongeza.

Kwa upande wake, Meneja wa Mgodi wa TAWOMA, Paul Ntalima, amesema wanamiliki maduara 24 ya uzalishaji, lakini ni maduara 14 pekee yanayoendelea na kazi kutokana na gharama kubwa za uendeshaji.

“Wachimbaji wadogo wana uwezo wa kuongeza tija mara mbili zaidi endapo watapatiwa mikopo yenye riba nafuu. Tunatengeneza ajira kwa vijana na wanawake zaidi ya 400. Sekta hii si tu inaleta kipato, bali pia inaimarisha maisha ya wananchi. Tukipata umeme wa gridi, uzalishaji utaongezeka mara mbili hadi tatu,” amesema Ntalima.

Naye Mussa Kazidijshi, Mtendaji wa Mgodi wa Ludovic Mlalo & Partners, amesema mgodi wao unaajiri zaidi ya wafanyakazi 200 na umeendelea kurejesha kwa jamii kupitia miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa barabara.

“Jamii inanufaika hasa wakati wa mvua ambapo barabara huboreshwa na milipuko ya magonjwa hupungua. Tukipatiwa mikopo ya riba nafuu na nishati ya kudumu ya umeme, uzalishaji wetu utaongezeka mara tatu,” amesema Kazidijshi.

Akizungumzia changamoto hizo, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Simiyu, Mayigi Makolobela, amesema Serikali kupitia Tume ya Madini kwa kushirikiana na TANESCO inaendelea na mazungumzo kuhakikisha maeneo yote ya wachimbaji wadogo mkoani humo yanapatiwa umeme wa kudumu.

“TANESCO wameahidi kufikisha umeme katika maeneo yote ya wachimbaji wadogo mkoani Simiyu ili kuongeza uzalishaji na kupunguza gharama za uendeshaji,” amesema Makolobela.

Ameongeza kuwa Serikali inaendelea na mpango wa kufanya tafiti zaidi katika maeneo ya madini ili kuwasaidia wachimbaji wadogo kufanya uchimbaji wenye tija.

“Wito wangu kwa taasisi za kifedha ni kuangalia upya namna ya kuwakopesha wachimbaji wadogo, kwa kuwa wana bidhaa halisi, masoko yapo, na taarifa zao za kifedha zinajulikana. Wana uwezo wa kurejesha mikopo,” amesisitiza Makolobela.

Amebainisha kuwa kwa sasa Mkoa wa Simiyu una vituo vitano vya ununuzi wa madini na soko kuu moja lililopo Bariadi Mjini, ambako shughuli kubwa za biashara ya madini hufanyika.

Makolobela pia amewapongeza wachimbaji kwa kuendelea kushiriki katika shughuli za kijamii kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), akitaja mfano wa vikundi vya TAWOMA na EMJ vilivyotoa zaidi ya madawati 90 kwa Shule ya Majengo kama sehemu ya kurudisha kwa jamii.







Posted by MROKI On Wednesday, November 12, 2025 No comments

November 11, 2025









Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amewataka watumishi wa Tume kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi ya mwili mara kwa mara na kuepuka tabia zinazoweza kusababisha magonjwa sugu na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU).

Mhandisi Lwamo ametoa wito huo Novemba 10, 2025, wakati akifungua mafunzo ya waelimisha rika wa Tume ya Madini yanayofanyika jijini Dodoma.

Amesema lengo la mafunzo hayo ni kuongeza uelewa miongoni mwa watumishi kuhusu VVU, Ukimwi na magonjwa yasiyoambukizwa, ili kulinda afya zao na kuboresha ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

“Afya bora ya mwili na akili ni nguzo muhimu ya utendaji kazi wenye tija. Magonjwa mengi tunayokabiliana nayo leo yanatokana na mitindo ya maisha, ulaji usio sahihi, kutofanya mazoezi na tabia hatarishi za ngono. Ni jukumu letu kila mmoja kuhakikisha tunajilinda na kuishi kwa afya,” amesema Mhandisi Lwamo.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa waajiri kujumuisha mikakati ya afya kazini kwenye mipango ya kila mwaka ya taasisi, sambamba na kujengeana uwezo wa kukabiliana na changamoto za kiafya katika maeneo ya kazi.

Ameongeza kuwa Tume ya Madini imeendelea kuwa mfano wa kuigwa kwa kuhimiza mazoezi ya viungo kupitia mabonanza, pamoja na kuhakikisha watumishi wenye magonjwa sugu wanapata lishe bora na huduma stahiki.

Akizungumza kuhusu usiri wa taarifa za kiafya, Mhandisi Lwamo amewataka watumishi kuheshimu faragha ya wagonjwa na kuhakikisha taarifa za afya zinatolewa kwa ridhaa ya mhusika pekee, ili kuepuka usambazaji wa taarifa zisizo sahihi.

“Ni muhimu wale walioathirika kutoa taarifa kwa hiari yao ili waweze kusaidiwa ipasavyo. Tunapaswa kuwa na moyo wa huruma na uelewa katika kushughulikia masuala haya,” ameongeza Mhandisi Lwamo.

Kwa upande wake, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo ambaye pia ni Fundi Sanifu wa Migodi kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi -Kahama, Jackson Mumanyi, ameishukuru Tume ya Madini kwa kuandaa mafunzo hayo muhimu, akisema yatasaidia kuongeza uelewa na kubadili mitazamo ya watumishi kuhusu kujikinga na magonjwa hayo.

Mafunzo hayo ya siku mbili yanafanyika katika ofisi za Tume ya Madini mkoani Dodoma, yakiwa na lengo la kuandaa waelimisha rika watakaosaidia kusambaza elimu ya afya kazini na kuhimiza tabia za kufanya mazoezi kwa watumishi wote wa Tume.
Posted by MROKI On Tuesday, November 11, 2025 No comments



Na Mwandishi wetu, Simiyu
AFISA Madini Mkazi wa Mkoa wa Simiyu, Mayigi Makolobela, amesema mkoa huo umeendelea kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato yatokanayo na Sekta ya Madini, ambapo makusanyo ya robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2025/2026 yamevuka malengo kwa kufikia zaidi ya asilimia 103 ya lengo lililowekwa kwa kipindi husika.

Akizungumza mkoani Simiyu, Makolobela amesema kwa mwaka wa fedha uliopita, ofisi yake ilipewa lengo la kukusanya Shilingi bilioni 4, lakini walifanikiwa kukusanya zaidi ya Shilingi bilioni 4.5.

 “Kwa mwaka huu wa fedha tumewekewa lengo la kukusanya Shilingi bilioni 4.76, na hadi kufikia robo ya kwanza tayari tumekusanya zaidi ya Shilingi bilioni 1.23, sawa na asilimia 103 ya lengo la robo mwaka,” amesema Makolobela.

Ameongeza kuwa tangu kuanza kwa Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, makusanyo ya madini kupitia wachimbaji wadogo mkoani humo yamefikia zaidi ya Shilingi bilioni 17, hatua inayodhihirisha ukuaji na uimara wa sekta hiyo katika Mkoa wa Simiyu.

Aidha, Makolobela amesema Simiyu ni miongoni mwa mikoa yenye utajiri mkubwa wa madini mbalimbali ikiwemo dhahabu, shaba, madini ya ujenzi, vito aina ya Amethyst na Nikeli yanayopatikana katika  wilaya za Bariadi na Busega.

Hata hivyo, amebainisha kuwa tafiti za kina bado hazijafanyika ipasavyo katika maeneo yote ya mkoa huo, jambo linaloweza kusababisha baadhi ya maeneo yenye rasilimali kutobainika mapema.

“Kama Mkoa huu utafanyiwa utafiti wa kina, kuna uwezekano mkubwa wa kugundulika mashapo mengine, hususan madini ya metali yanayoweza kuchimbwa kwa kiwango cha kati na kikubwa, hivyo kuinufaisha Serikali na wananchi kwa ujumla,” amesema Makolobela.

Katika hatua nyingine, ameeleza kuwa Mkoa wa Simiyu una vituo vitano vya ununuzi wa madini pamoja na Soko Kuu la Madini lililopo Bariadi Mjini, ambapo shughuli kuu za biashara ya madini zinafanyika kwa ufanisi mkubwa.
Posted by MROKI On Tuesday, November 11, 2025 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo