Nafasi Ya Matangazo

June 01, 2026

Na Mwandishi Wetu
Waandishi wa Habari watakaoshiriki Tuzo za Uandishi wa Habari na Makala za Maendeleo (Samia Kalamu Awards - SKA) 2026 wamelazimika kukidhi sharti la kuwa na ithibati kutoka Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), hatua inayolenga kuimarisha weledi, uwajibikaji na ushindani wa haki katika taaluma hiyo.

Akizindua rasmi mchakato wa kupokea kazi za kushindanishwa, Jumapili Tarehe 31 Mei, 2026, jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa SKA, Mha. Peter Mwasalyanda, amesema maandalizi ya mwaka huu yanazingatia maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kutambua mchango wa Waandishi wa Habari za maendeleo nchini.
Mwasalyanda amesema ili kuhakikisha uadilifu, uwazi na ushindani wa haki, maandalizi ya tuzo hizo yanahusisha pia Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kama mdau muhimu katika kusimamia weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari.

“Tuzo hizi zinalenga kutambua, kuthamini na kuhamasisha uzalishaji wa maudhui ya ndani yenye ubora, yanayochangia kuelimisha, kuhabarisha na kuburudisha, na kuimarisha taswira chanya ya Taifa kupitia habari za maendeleo,” amesema.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema tofauti na msimu wa kwanza wa tuzo hizo, mwaka huu washiriki wanapaswa kuhakikisha wamekidhi sharti la ithibati.

“Mtakumbuka Msimu wa kwanza wa Samia Kalamu mambo ya JAB hayakuwepo, kwa hiyo waandishi walishiriki wote bila kujali vigezo vya Ithibati lakini mwaka huu kuna hiki kigezo cha kuwa na ithibati kwa hiyo niwashauri basi wote wanaoshiriki kwenye hizi tuzo wahakikishe wanakuwa na ithibati, wamethibitishwa na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari.” Amesema Wakili Kipangula na kuongeza;
“Ni muhimu sana kwa sababu ni takwa la kisheria na kitu ambacho hatuwezi kukikwepa. Nawahamasisha tushiriki wote kwa sababu isionekane ni tuzo za watu fulani tu, kila mmoja awasilishe kazi zake,” amesema Kipangula.

Kwa mujibu wa vigezo vya ushiriki vilivyotangazwa, Waandishi wa Habari wa Tanzania Bara wanatakiwa kuwa wamethibitishwa na JAB, huku kwa Zanzibar washiriki wakitakiwa kuwa na kitambulisho cha Mwandishi wa Habari (Press Card).

Tuzo hizo zimeanza kupokea kazi kuanzia Mei 31 hadi Juni 30, 2026 na zinatarajiwa kutolewa kati ya Oktoba na Desemba mwaka huu.

Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments
Wananchi wa Kijiji cha Mkungugu jimbo la Ismani katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa wakiwa katika foleni ya kupiga kura ya kumchagua Mbunge wao katuika uchaguzi mdogo uliyofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwananchi Mkazi wa wa Kijiji cha Kihongorota katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa, Angelista Mwenda akipiga kura katika uchaguzi mdogo wa Ubunge jimbo la Ismani uliofanyika leo Juni 01, 2026.  
Mwananchi Mkazi wa wa Kijiji cha Kihongorota katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa, Angelista Mwenda akipiga kura katika uchaguzi mdogo wa Ubunge jimbo la Ismani uliofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akipita kuingia katika kituo cha Kura cha Ofisi ya Kijiji Mtera katika jimbo la Ismani Wilaya ya Iringa mkoani Iringa kukagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Ismani lililofanyika leo Juni 01, 2026. 
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akizungumza na Mawakala katika moja ya vituo alivyotembelea.
MWENYEKITI wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele amesema zoezi la upigaji Kura wa Ubunge katika jimbo la Isman  katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara limekwenda vizuri.
 
Mwenyekiti huyo wa Tume Jaji Mwambegele amesema hayo leo Juni 01,2026 akiwa katika ofisi za Kijiji Igingilanyi Wilayani Iringa mara baada ya kutembelea na kukagua zoezi la upigaji Kura linavyoendelea katika vituo vya kupigia Kura vya jimbo la Isimani ambako kunafanyika uchaguzi mdogo wa ubunge.
 
Amesema mwitikio wa wananchi wa Ismani katika kujitokeza kupiga kura umekua mkubwa na hata katika Kata nyingine 12 ambazo nazo zinachagua Madiwani hii leo wamejitokeza kwa Wingi.
 
Mwenyekiti huyo wa Tume Jaji Mwambegele ameshudia upigaji kura kwa baadhi yavituo vilivyopo katika vijiji vya   Igingilanyi, Mkungugu, Kihongorota na Migori.
 
Kata 12 zilofanya uchaguzi leo ni Mzimuni iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Halmashauri ya Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji Kasulu.
 
Nyingine ni Kata ya Kala iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akikagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Iringa mkoani Iringa hii leo Juni 01,2026. 

Wananchi wakiwa katika mistari tayari kuingia vituoni kupiga Kura. 

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akikagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Iringa mkoani Iringa hii leo Juni 01,2026. 

Wananchi wakiwa katika mistari tayari kuingia vituoni kupiga Kura. 

Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe 


Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema jumla ya wanafunzi 246,197 wakiwemo wasichana 114,102 na wavulana 132,095 waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano mwaka 2026 wanatakiwa kuripoti shuleni kuanzia Julai 04, 2026 hadi Julai 31, 2026 kwakuwa muhula wa kwanza wa masomo utaanza Julai 06, 2026. 

Prof. Shemdoe amesema hayo leo Juni 01, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi Ndogo ya Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Magogoni Jijini Dar es Salaam, wakati akitoa taarifa kwa umma kuhusu wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya elimu ya ufundi kwa mwaka 2026.

“Wanafunzi 172,114 sawa na asilimia 69.9 wakiwemo wasichana 85,987 na wavulana 86,127 wenye sifa wamechaguliwa kujiunga na kidato cha tano katika shule  za sekondari za Serikali 856 zikiwemo shule za bweni 825, kutwa 25 na kutwa na bweni sita (06),” amefafanua Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amesema jumla ya wanafunzi 74,083 sawa na asilimia 30.1  wakiwemo wasichana 28,115 na wavulana 45,968 wamechaguliwa kujiunga na vyuo vya Ufundi.

“Wanafunzi 3,144 wakiwemo wasichana 1,170 na wavulana 1,974 wamechaguliwa kujiunga na fani mbalimbali katika vyuo 04 vya elimu ya ufundi, vyuo hivyo ni Chuo cha Ufundi cha Arusha (ATC), Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT), Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST) na Chuo cha Maendeleo ya Maji (WMDI),” ameeleza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amesisitiza kwamba, uchaguzi wa wanafunzi wa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya elimu ya ufundi umefanyika kwa kuzingatia ufaulu na nafasi zilizopo katika shule; hivyo, hakutakuwa na fursa ya kufanya mabadiliko yoyote ya Shule kutokana na ukosefu wa nafasi.  

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi zilizotumika kujenga miundombinu bora ya shule za kidato cha tano na vyuo vya kati ambayo itatumika kuwahudumia wanafunzi 246,197 waliochaguliwa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya elimu ya ufundi mwaka 2026.
Posted by MROKI On Monday, June 01, 2026 No comments

May 31, 2026






Mpwapwa
Mkoa wa Dodoma leo umepokea Mwenge wa Uhuru 2026 katika Uwanja wa Shule ya Msingi Mtera iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa, ukitokea Mkoa wa Iringa.

Akizungumza katika hafla ya mapokezi hayo, Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma, Dkt. Khatibu Kazungu, amesema Mwenge wa Uhuru utakimbizwa umbali wa kilomita 1,595.3 katika wilaya zote saba (7) na halmashauri nane (8) za Mkoa wa Dodoma, ambapo utapitia, kuzindua, kuweka mawe ya msingi na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo yenye thamani ya jumla ya Shilingi 23,243,056,418.58.

Dkt. Kazungu alipokea Mwenge huo kutoka kwa Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Bi. Doris Kalasa, na kueleza kuwa Mkoa wa Dodoma una miradi mikubwa ya kimkakati itakayopitiwa na Mwenge wa Uhuru mwaka huu.

Amesema mafanikio hayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ameendelea kuuletea Mkoa wa Dodoma fedha nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali.

“Tunamshukuru na kumpongeza Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuupatia Mkoa wa Dodoma rasilimali za kutosha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Miradi hii ya kimkakati imeendelea kuufungua Mkoa wa Dodoma kiuchumi, kuimarisha huduma za kijamii na kuufanya kuwa kivutio muhimu kwa uwekezaji na utalii,” amesema Dkt. Kazungu.

Aidha, ameeleza kuwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma wanathamini mchango wa Mwenge wa Uhuru katika kuhamasisha umoja, mshikamano na uzalendo miongoni mwa Watanzania.

“Katika mazingira ya amani na umoja wa kitaifa, Taifa letu linaendelea kustawi, kuvutia wawekezaji na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Hakuna Taifa linaloweza kufanikiwa kiuchumi bila kuwepo kwa amani na mshikamano wa Wananchi wake,” alisisitiza.

Dkt. Kazungu ameongeza kuwa wananchi pamoja na viongozi wa Mkoa wa Dodoma wameendelea kuzingatia na kutekeleza ujumbe wa kudumu wa Mwenge wa Uhuru unaohimiza uzalendo, uwajibikaji na ushiriki wa wananchi katika maendeleo ya Taifa, sambamba na kaulimbiu ya mwaka huu isemayo:

“Tanzania ni yetu sote, tushikamane kwa pamoja kuleta maendeleo.” 
Posted by MROKI On Sunday, May 31, 2026 No comments
Na Mwandishi wetu, Iringa
Wapiga Kura 222,218 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki kwenye uchaguzi mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Isimani lililopo Halamashauri ya Wilaya ya Iringa Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara.
 
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele ameyasema hayo leo Mei 31, 2026 Mkoani Iringa wakati akisoma risala maalum kuhusu uchaguzi katika jimbo na kata husika utakao fanyika kesho Juni 01, 2026 na kusema kuwa jumla ya vituo 628 vya Kupigia Kura vitatumika.
 
“wapiga kura 89,753 wapo kwenye Jimbo la Ismani na wapiga kura 132,465 wapo kwenye kata 12 zitakazofanya uchaguzi mdogo na vituo 277 vipo kwenye Jimbo la Ismani na vituo 351 vipo kwenye kata 12 zitakazofanya uchaguzi mdogo.,”amesema Jaji Mwambegele.
 
Aidha, amesema Katika Uchaguzi huu, jumla ya wagombea 108 kutoka katika vyama vya siasa 17 wanawania nafasi wazi ya ubunge na udiwani katika maeneo niliyoyataja.

“Jimbo la Ismani lina wagombea 17 wa nafasi ya Ubunge ambapo kati ya wagombea hao wagombea nane (08) sawa na asilimia 47.06 ni wanaume na wagombea tisa (09) sawa na asilimia 52.94 ni wanawake. Kata 12 zinazofanya uchaguzi mdogo wa udiwani zina jumla ya wagombea 91 ambapo kati ya hao wagombea 61 sawa na asilimia 67.03 ni wanaume na wagombea 30 sawa na asilimia 32.97 ni wanawake.” alisema Jaji Mwambegele.

“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho Juni 01, 2026 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Jimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.
 
Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.
 
Jaji Mwambegele amesema vituo vitafunguliwa saa 01:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni na kwamba ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapiga kura bado wapo kwenye mistari, mlinzi wa kituo atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapiga kura walio kwenye mstari watakapomalizika.
 
“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpiga kura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura; na Mpiga kura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapiga kura,”amesema Jaji Mwambegele.
 
Kwa mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi yake au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga Kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, Leseni ya udereva au Pasi ya kusafiria (Passport).

Kata 12 zitakazo fanya uchaguzi ni Mzimuni iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Halmashauri ya Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji Kasulu. 

Nyingine ni Kata ya Kala iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.
Posted by MROKI On Sunday, May 31, 2026 No comments

May 30, 2026

 
Sehemu ya Wafanyakazi wa Mradi wa C-SDTP wakiwa kwenye banda la maonesho wakati wa Wiki ya Maziwa Kitaifa Mkoani Iringa.

Na Kadama Malunde - Iringa

Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia mradi wa Tasnia ya Maziwa na Mabadiliko ya Tabianchi (C-SDTP), kwa kushirikiana na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), imeungana na wadau wengine wa kitaifa maadhimisho ya Wiki ya Maziwa kitaifa katika viwanja vya Mwembe Togwa, mkoani Iringa kuanzia 25 Mei hadi 1 Juni 2026 kwa lengo la kuhamasisha ufugaji wa ng'ombe na uzalishaji wa maziwa unaozingatia mabadiliko ya tabianchi.

Maadhimisho hayo yameandaliwa na Bodi ya Maziwa Tanzania (TDB), na kuwaleta pamoja wadau muhimu katika mnyororo wa thamani wa maziwa, ikiwa ni pamoja na wakulima, wachakataji, taasisi za Serikali, taasisi za kifedha, washirika wa maendeleo,na maafisa wa Serikali ili kujadili fursa za uwekezaji, viwango vya ubora, na teknolojia bunifu kwa maendeleo ya sekta ya maziwa.

Katika maadhimisho haya, mradi wa C-SDTP unaonesha jitihada zake katika kufanya mabadiliko katika sekta ya maziwa kwa kuimarisha uzalishaji maziwa kwa wakulima wadogo katika mikoa nane inayotekeleza mradi huu ikiwemo mikoa ya Iringa, Mbeya, Morogoro, Arusha, Kilimanjaro, Tanga, na Pwani; pamoja na Zanzibar (Pemba na Unguja).

Mratibu wa Taifa wa Mradi wa Tasnia ya Maziwa na Mabadiliko ya Tabianchi (C-SDTP) Dkt. Lazaro Kapella ameeleza,"C-SDTP, chini ya mwongozo wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, inaendelea kusaidia wazalishaji wadogo wa maziwa kwa kuimarisha ushiriki wao katika mnyororo wa thamani wa maziwa, kuongeza mapato ya kaya, kuboresha usalama wa chakula na lishe, na kupunguza athari za kimazingira zitokanazo na mifumo ya uzalishaji wa maziwa".

Katika maadhimisho haya ya Wiki ya Maziwa, mradi wa C-SDTP unaongeza uelewa wa umma kuhusu umuhimu wa unywaji wa maziwa na kukuza mbinu bora katika ufugaji wa ng’ombe, zikiwemo ufugaji wa mbari bora za ng'ombe wa maziwa, upandikizaji wa mbegu za ng’ombe (Artificial Insemination), uzalishaji wa malisho, huduma za afya ya wanyama, usimamizi wa samadi ya ng‘ombe, na teknolojia nyingine za mabadiliko ya tabianchi zinazolenga kuongeza tija ya maziwa, kuimarisha ustahimilivu na kupunguza athari za mazingira zitokanazo na uzalishaji wa maziwa.

Mradi pia unaongeza uelewa wa wananchi kuhusu mnyororo wa thamani wa maziwa kwa kuonyesha jinsi mradi unavyosaidia kutoa maarifa, ujuzi, na vifaa vinavyoongeza usalama na ubora wa maziwa. Uelewa huu utahusisha mnyororo mzima wa kushughulikia maziwa.

Kuhusu C- SDTP

Mradi wa Tasnia ya Maziwa na Mabadiliko ya Tabianchi ni juhudi ya pamoja ya miaka kumi (2024-2034) kati ya Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zenye lengo la kuboresha maisha na ustahimilivu wa jamii za vijijini kupitia mabadiliko endelevu ya sekta ya maziwa.

Mradi unalenga kuwezesha wazalishaji wadogo wa maziwa kupitia uwekezaji unaojali mabadiliko ya tabianchi na unaolenga masoko na kuongeza ushiriki katika mnyororo wa thamani wa maziwa, kuongeza mapato ya kaya, kuboresha usalama wa chakula na lishe, na kukuza mifumo endelevu ya utengenezaji wa maziwa inayojali uhifadhi wa mazingira.

Mradi huu unafadhiliwa na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Mfuko wa OPEC wa Maendeleo ya Kimataifa (OFID), Mfuko wa Hali ya Hewa ya Kijani (GCF) na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB).
Posted by MROKI On Saturday, May 30, 2026 No comments







Ruangwa, Lindi
Waziri wa Madini, Mhe Anthony Mavunde (Mb) ameielekeza Timu ya Majadiliano ya Serikali kwenye Sekta ya Madini (GNT) kuwaita na kufanya nao majadiliano wamiliki wote wa leseni za uchimbaji madini kinywe nchini Tanzania kujadiliana kuhusu ubia wa serikali katika Kampuni hizo na kuwataka kuanza utekelezaji wa uchimbaji kwa mujibu wa masharti ya leseni na Sheria ya Madini Sura ya 123.

Ameyasema hayo leo tarehe 30 Mei, 2026 Wilayani Ruangwa aliposhiriki zoezi la utiaji saini na Kampuni za Grafica Resources na Eminent Minerals Limited zenye ubia wa  uwekezaji wa hisa asilimia 83 na Serikali asilimia 17 kwa kila kampuni. 

"Sisi sekta ya madini tunamshukuru kwa dhati Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyotupa maelekezo na kutuwezesha kusimamia sekta kikamilifu kwa maendeleo ya Taifa letu"

"Na ndiyo maana Kampuni zote ambazo hazijaanza uzalishaji kwa mujibu wa masharti ya leseni zao tumeziandikia hati ya makosa (Default Notice) kwa mujibu wa Sheria ya Madini Sura ya 123. Kusaini kwetu mikataba siku ya leo, hakutoi unafuu kwa wawekezaji hawa kutotekeleza uwekezaji wao kwa mujibu wa Sheria yetu ya madini" alisisitiza Mhe. Mavunde.

Waziri Mavunde alisema hatua ya Timu ya GNT kuwaita na kuwataka wamiliki wa leseni za uchimbaji madini kinywe kufuata masharti ya Sheria na kuanza uzalishaji kutapelekea ufikiaji wa lengo la kuifanya Tanzania kuwa mzalishaji wa kwanza duniani wa madini kinywe ifikapo mwaka 2030.

Vilevile, Waziri Mavunde alitoa wito kwa wawekezaji wa miradi hiyo kutoa fursa ya kipaumbele cha ajira kwa watanzania hususan wanaozunguka miradi hiyo. Kwa kufanya hivyo kutachochea uchumi wa Vijiji, Wilaya ya Ruangwa hususan kupitia wajibu wa uwekezaji kwa jamii (CSR) na kupelekea maendeleo ya uchumi wa Nchi yetu.

Aidha, Waziri Mavunde alibainisha kuwa miradi hiyo itakapoanza kuzalisha kikamilifu, itakuwa na  uwezo wa kuzalisha tani 101,048 za kinywe kila mwaka kwa upande wa mradi wa Grafica na tani 15,930 za kinywe kila mwaka kwa upande wa mradi wa Eminent mtawalia, hali inayoifanya Ruangwa sasa kuwa sehemu ya mnyororo wa thamani wa teknolojia za kisasa duniani.

Waziri Mavunde pia alieleza kuwa bado Tanzania ina nafasi kubwa ya kufanya vizuri katika uzalishaji wa madini mbalimbali duniani, na ndiyo maana tunaendelea kuweka mkazo kwenye ufanyaji wa utafiti wa kina ili kubaini mashapo zaidi yatakayoongeza uchimbaji hususan kupitia wachimbaji wadogo wenye mchango mkubwa katika uchumi wetu.

Awali, akieleza mchakato wa kufikia makubaliano hayo, Mwenyekiti wa Timu ya Majadiliano ya Serikali kwenye sekta ya Madini, Prof. Sifuni Mchome alibainisha kuwa majadiliano hayo yalifanyika kwa kuzingatia maslahi mapana ya nchi yetu na hayakuwa na lengo la kutafuta mshindi, hali iliyopelekea Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupata hisa zisizofifishwa za asilimia 17 kwenye kila mradi wa ubia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni ya Grafica Resources, Bw. Vikas Bardiya alieleza kuwa kampuni yao inaishukuru Serikali kwa ushirikiano iliyowapa mpaka kufikia makubaliano ya kuwekeza na kuahidi kwamba watahakikisha wanatekeleza uwekezaji huo kwa mujibu wa mkataba ili uweze kuleta manufaa kwa wananchi wa Ruangwa na Taifa kwa ujumla.

Pia, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Eminent Minerals Limited, Bw. Shafiqali Khakialieleza kufarijika kwao kuwa kampuni ya kizawa kuingia ubia na Serikali katika uwekezaji kwenye mradi huo wa uchimbaji madini kinywe na kwamba wao kama wazawa watahakikisha sehemu kubwa ya zaidi ya ajira 250 zitakazozalishwa katika uwekezaji huo zinachukuliwa na watanzania ili kuinua uchumi wa Taifa letu. 

Naye Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mh Zainab Telack alimshukuru Mhe. Rais kwa kuwa kiongozi mahiri katika kusimamia uchumi na kuhakikisha rasilimali zetu zinanufaisha watanzania. Aidha, alisisitiza kuwa Serikali ya Mkoa wa Lindi itaendelea kuwapa ushirikiano wawekezaji hao ili waweze kuendesha shughuli zao kwa kasi na kunufaisha wananchi wa Lindi na Taifa kwa ujumla.
Posted by MROKI On Saturday, May 30, 2026 No comments

Na Mwandishi Wetu, Pwani
Hifadhi ya Msitu wa Asili ya Pugu Kazimzumbwi mkoani Pwani imeendelea kujidhihirisha kuwa moja ya hazina kubwa za utalii wa ikolojia nchini baada ya kuvutia wahifadhi kutoka Shamba la Miti Sao Hill waliotembelea eneo hilo kujifunza mbinu za uhifadhi, usimamizi wa bioanuai na maendeleo ya utalii endelevu.

Ziara hiyo imekuja wakati Tanzania ikiendelea kuimarisha juhudi za kuhifadhi rasilimali za misitu na kuendeleza utalii wa asili kama sehemu ya kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa, huku Pugu Kazimzumbwi ikitajwa kuwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa kuhifadhi urithi wa kihistoria na mazingira ya kipekee karibu na Jiji la Dar es Salaam.

Wakati wa ziara hiyo, wahifadhi hao walitembelea vivutio mbalimbali vinavyopatikana ndani ya hifadhi hiyo ikiwemo misitu ya asili yenye bioanuai adimu, njia za utalii wa kutembea msituni, maeneo ya kihistoria pamoja na vivutio vya kiikolojia vinavyovutia watalii wa ndani na nje ya nchi.

Maofisa wa hifadhi hiyo waliwaeleza wageni hao kuhusu hatua zinazochukuliwa kulinda mazingira, kudhibiti shughuli zinazohatarisha misitu na kuendeleza utalii wa ikolojia unaochochea maendeleo ya jamii na kuongeza mapato ya taifa bila kuathiri mfumo wa ikolojia.

Akizungumza baada ya kutembelea vivutio hivyo, Kiongozi wa Msafara huo, CO I Donald Makupa, alisema uzoefu walioupata katika Hifadhi ya Msitu wa Asili ya Pugu Kazimzumbwi utakuwa chachu ya kuboresha mikakati ya uhifadhi katika maeneo wanayoyasimamia.

“Tumeshuhudia namna ambavyo uhifadhi wa misitu unaweza kwenda sambamba na maendeleo ya utalii. Maarifa haya yatatusaidia kuimarisha usimamizi wa rasilimali za misitu na kuongeza thamani ya maeneo yetu ya uhifadhi,” alisema Makupa.

Aliongeza kuwa ushirikiano na kubadilishana uzoefu kati ya taasisi na maeneo mbalimbali ya uhifadhi ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha sekta ya misitu na utalii inaendelea kukua kwa manufaa ya taifa.

Kwa upande wake, Afisa Utalii wa Hifadhi ya Msitu wa Asili ya Pugu Kazimzumbwi, Mbaruku Sinon, alisema ujio wa wahifadhi hao unaonesha namna maeneo ya uhifadhi yanavyozidi kuwa vituo vya kujifunzia na kubadilishana uzoefu kuhusu mbinu bora za kulinda mazingira na kuendeleza utalii.

Alisema kuimarika kwa ushirikiano kati ya wahifadhi kutoka maeneo mbalimbali kutasaidia kuongeza ubunifu katika usimamizi wa rasilimali za misitu, kukuza idadi ya watalii na kuhakikisha bioanuai inayopatikana nchini inalindwa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

“Pugu Kazimzumbwi ni zaidi ya hifadhi ya misitu. Ni darasa la uhifadhi, kituo cha utalii wa ikolojia na sehemu inayobeba historia muhimu ya nchi yetu. Tunahitaji kuendelea kushirikiana ili kuitangaza zaidi ndani na nje ya Tanzania,” alisema Sinon.

Katika ziara hiyo, wahifadhi hao walikumbushwa umuhimu wa kushiriki kampeni ya kuhamasisha wananchi kupigia kura vivutio vya utalii vinavyosimamiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), hususan Pugu Kazimzumbwi Nature Forest Reserve na Amani Nature Forest Reserve, ambavyo vimeingia katika kinyang’anyiro cha Tuzo za Kimataifa za Utalii.

Wadau wa uhifadhi wanaamini kuwa mafanikio ya maeneo hayo katika tuzo hizo yataongeza mwonekano wa Tanzania katika soko la utalii duniani, kuvutia wageni wengi zaidi na kuchochea uwekezaji katika utalii wa asili unaozingatia uhifadhi wa mazingira.

Kwa miaka ya karibuni, Pugu Kazimzumbwi imeendelea kuwa kivutio muhimu kwa watalii, wanafunzi, watafiti na wadau wa mazingira kutokana na utajiri wake wa bioanuai, historia ya kipekee na ukaribu wake na Jiji la Dar es Salaam, hali inayoiweka katika nafasi ya kuwa moja ya nguzo muhimu za utalii wa ikolojia nchini.







Posted by MROKI On Saturday, May 30, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo