Nafasi Ya Matangazo

March 04, 2026

Spinel ni miongoni mwa madini ya vito yenye thamani kubwa sana duniani, yanayoendelea kupata umaarufu mkubwa katika masoko ya kimataifa kutokana na ubora wake wa kipekee, rangi adimu na uimara wa hali ya juu. 

Tanzania ni miongoni mwa nchi chache duniani zilizojaaliwa rasilimali hii adimu, hususan katika eneo la Mahenge, Kijiji cha Epanko, Wilaya ya Ulanga, mkoani Morogoro, eneo ambalo limejijengea sifa ya kuwa chanzo cha spinel bora zaidi duniani.

Spinel ni jiwe la vito lenye rangi mbalimbali ikiwemo nyekundu, pinki, zambarau, bluu na machungwa. Umaarufu wake unatokana na sifa kadhaa muhimu ikiwemo uwazi wake wa hali ya juu (high clarity), rangi kali na ya kuvutia inayopendwa sana katika soko la vito, pamoja na uimara mkubwa unaoufanya kudumu kwa muda mrefu. Aidha, spinel nyingi hupatikana bila kuhitaji matibabu ya joto (heat treatment), jambo linaloongeza thamani yake sokoni.

Kwa miaka mingi, spinel nyekundu ilichanganywa na ruby hadi pale sayansi ya madini ilipobaini tofauti zake. Leo hii, spinel imesimama kama jiwe la vito lenye hadhi yake binafsi na thamani inayozidi kuongezeka mwaka hadi mwaka.

Mahenge, iliyopo Wilaya ya Ulanga mkoani Morogoro, ni eneo lenye umuhimu mkubwa katika ramani ya madini ya vito duniani. Spinel inayopatikana Mahenge inajulikana kwa rangi yake ya pinki na nyekundu yenye mwanga wa kipekee (neon-like glow), sifa inayofanya spinel ya Mahenge kutafutwa sana na wafanyabiashara wa vito duniani.

Ugunduzi wa spinel katika eneo hili umeifanya Mahenge kutambulika kimataifa na kuiweka Tanzania miongoni mwa nchi muhimu katika biashara ya madini ya vito. Spinel ya Mahenge imekuwa ikitajwa mara kwa mara katika maonesho makubwa ya vito ya kimataifa ikiwemo Tucson Gem Show nchini Marekani, Hong Kong Jewellery Fair, pamoja na maonesho ya vito ya Bangkok, Thailand, hatua inayoongeza hadhi ya Tanzania katika soko la kimataifa la madini ya vito.

Uchimbaji wa spinel Mahenge unaongozwa na kampuni za Kitanzania, zikiwemo Ruby International Limited na Franone Mining, ambazo ndizo wawekezaji wakuu katika uchimbaji wa madini haya katika eneo hilo. Kampuni hizi, ambazo ni mali ya Watanzania, zimeonesha mfano mzuri wa jinsi wawekezaji wa ndani wanavyoweza kuendeleza rasilimali za taifa kwa ufanisi, uwajibikaji na uzingatiaji wa Sheria.

Akizungumza kuhusu umuhimu wa spinel ya Mahenge na mchango wake kwa jamii, Msimamizi wa Ruby International Mining, Mhandisi


 Penina Mtego, katika mgodi wa Epanko, Mahenge, anasema:
“Spinel ya Mahenge ni rasilimali adimu yenye ubora wa kipekee duniani. Kama kampuni ya Kitanzania, tumedhamiria kuhakikisha uchimbaji wake unazingatia viwango vya kitaalamu huku manufaa yake yakirudi moja kwa moja kwa taifa na kwa wananchi wa Mahenge. Kipaumbele chetu ni kutoa ajira, kuchangia maendeleo ya jamii na kulinda mazingira.”

Msimamo wa Serikali
Serikali ya Tanzania inaendelea kusisitiza umuhimu wa kusimamia rasilimali za madini kwa tija na uwazi ili ziwe chachu ya maendeleo ya wananchi. Akizungumzia mchango wa madini ya vito, hususan spinel ya Mahenge, Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, anasema:

“Madini ya vito kama spinel ya Mahenge ni utajiri mkubwa wa taifa letu. Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji wazawa ili kuhakikisha rasilimali hizi zinachimbwa kwa kuzingatia Sheria, zinawanufaisha wananchi, na kuongeza mapato ya serikali kwa maendeleo ya nchi.”

Kauli hiyo inaakisi dhamira ya serikali ya kuimarisha ushiriki wa Watanzania katika sekta ya madini na kuongeza thamani ya rasilimali kabla ya kuingia kwenye masoko ya kimataifa.

Uwepo wa migodi ya spinel Mahenge unaleta mabadiliko makubwa ya kijamii na kiuchumi kwa wakazi wa eneo hilo. Vijana wengi pamoja na kina mama wamepata ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja katika shughuli za uchimbaji, ulinzi, usafirishaji na huduma mbalimbali.
Dkt. Kiruswa anasisitiza kuwa, ajira hizi zimekuwa chanzo muhimu cha kipato kwa familia nyingi, hivyo kusaidia kupunguza umaskini na kuboresha hali ya maisha ya wakazi wa Mahenge na maeneo ya jirani.

Mbali na kutoa ajira, Dkt. Kiruswa anazipongeza Kampuni za Ruby International Limited na Franone Mining kuwa kuendelea kutekeleza wajibu wao kwa kijamii kwa kuchangia maendeleo ya jamii inayozunguka migodi yao ambapo mchango huo unajumuisha: Ujenzi wa zahanati, ujenzi na ukarabati wa shule na madarasa, ujenzi wa ofisi za serikali za mitaa, kuboresha miundombinu ya barabara, kuchangia ustawi wa vijana na wanawake na ushirikiana kwa karibu na viongozi wa eneo katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya Mahenge.

Hatua hizi zinaonesha dhamira ya dhati ya kampuni hizi katika kuhakikisha rasilimali za madini zinaleta manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi.

Utalii wa Madini na Fursa Mpya za Kiuchumi
Uwepo wa madini ya spinel Mahenge umechochea pia kukua kwa utalii wa madini, ambapo wadau wa ndani na nje ya nchi wanafika Mahenge kujifunza, kuona na kushuhudia shughuli za uchimbaji wa madini ya vito.

Utalii wa madini Mahenge umeanza kuchangia kukua kwa uchumi wa eneo hilo kwa kuleta fursa mpya katika sekta za malazi, usafiri, uuzaji wa vito pamoja na kukuza utamaduni wa wenyeji.

Spinel ni hazina kubwa ya taifa ambayo imeipa Tanzania heshima na nafasi ya kipekee katika soko la madini ya vito duniani. Mahenge, Wilaya ya Ulanga mkoani Morogoro, imekuwa mfano bora wa namna rasilimali asili zinavyoweza kuleta maendeleo endapo zitasimamiwa kwa uwazi, uzalendo na uwajibikaji.

Kupitia uwekezaji wa kampuni za Kitanzania kama Ruby International Limited na Franone Mining, spinel imekuwa chanzo cha ajira, mapato na maendeleo ya kijamii, kuthibitisha kuwa uwekezaji wa wazawa katika rasilimali za taifa ni nguzo muhimu ya maendeleo endelevu ya nchi.

Kutokana na ubora wa madini hayo, rasilimali hii bado inahitaji uwekezaji wa kutafiti, kuchimba, biashara  na kuongezwa thamani fursa hizi bado zipo na ikizingatiwa kwa mujibu wa wataalam kwa vito ni aina 25 tu vinazochimbwa Tanzania huku kukiwa na zaidi ya aina 100 za  madini ya vito ambayo nchi hii imebarikiwa kuwa nazo. Kwa wageni Sheria inaruhusu kuingia mkataba wa usaidizi kupitia teknolojia na mitaji.

Posted by MROKI On Wednesday, March 04, 2026 No comments

March 03, 2026




Na Mwandishi wetu, Dodoma
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amekutana na Mkurugenzi wa Go Plant Tanzania Bw. Emmanuel Likida kwa lengo la kujadili namna ya kushirikiana katika maandalizi ya Mjadala (Debate) wa Clean Cooking Solutions utakaowahusisha wanafunzi wa shule za Sekondari katika Halmashauri za Mkoa wa Dodoma. 

Katika kikao hicho, pande zote mbili zimejadili umuhimu wa kuwajengea vijana uelewa wa mapema kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia, athari za matumizi ya nishati zisizo safi kwa afya na mazingira, pamoja na fursa zilizopo katika ubunifu na ujasiriamali wa suluhisho za upishi safi.

Mjadala huo unatarajiwa kuwa jukwaa la kielimu na kimkakati la kukuza uelewa, kuchochea fikra bunifu, na kuibua mabalozi vijana wa Nishati Safi katika jamii.

Kikao hicho kimefanyika leo Machi 03,2026 katika Ofisi za Wizara ya Nishati zilizopo Mtumba, jijini Dodoma.
Posted by MROKI On Tuesday, March 03, 2026 No comments




Na Mwandishi wetu, Bagamoyo
Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Mhe. Subira Mgalu leo Machi 03, 2026 amekabidhi magari mapya kwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani kwa lengo la kuimarisha huduma kwa wateja na kuongeza ufanisi wa utendaji kazi katika kuwahudumia Wateja wilayani Bagamoyo.

Akizungumza katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika Ofisi ya TANESCO Bagamoyo, Mhe. Mgalu amesema kuwa hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme kwa wakati, kwa ubora na kwa uhakika zaidi.

“Magari haya yatawezesha mafundi na wahandisi wa TANESCO kuwafikia wananchi kwa haraka pale panapotokea hitilafu au changamoto za umeme. Tunataka kuona muda wa kushughulikia matatizo unapungua na huduma inaboreshwa,” amesema Mhe. Mgalu.

Amesisitiza kuwa, hivi sasa TANESCO imeimarika katika utoaji wa huduma ikiwa ni pamoja na kutoka katika kutengeneza hasara na linajiendesha bila kupata ruzuku kutoka Serikalini.

Aidha, amesema baada ya kukamilika bwawa la Julius Nyerere linalozalisha megawati 2115 na kupelekea Nchi kuwa na uwezo wa takribani wa megawati 4,000 huku mahitaji yakiwa takribani megawati 2,000 hivyo kuitaka TANESCO kuongeza kasi ya kuwaunganishia wateja.

Mkurugenzi wa TANESCO Kanda ya Mashariki,Mha. Kenneth Boymanda amesema  TANESCO inatekeleza miradi mingi ya maendeleo Wilaya ya Bagamoyo ikiwemo ya umeme Vijijini hivyo upatikanaji wa magari hayo kutarahisisha utekelezaji wa miradi hiyo.

“Bagamoyo tunao mpango mkubwa wa kuhakikisha kila nyumba inafikishiwa nishati ya  umeme nak ama Nchi mpaka mwaka 2030 kuunganisha nyumba milioni nane na laki tatu na nyumba Milioni Moja na Laki Saba kwa mwaka”, amesema Mha. Boymanda

Ameongeza kuwa, majukumu hayo yanahitaji uwepo wa vitendea kazi na kusisitiza kuwa TANESCO itafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa na Serikali kupitia mpango wa mission 300.

Serikali imeendelea kuweka mkazo katika kuboresha miundombinu ya umemme kama msingi wa maendeleo ya viwanda, biashara na ustawi wa jamii.

 Hatua ya TANESCO kununua magari hayo ni sehemu ya juhudi za kuimarisha huduma kwa wateja  na kuongeza ubora wa huduma kwa wananchi.
Posted by MROKI On Tuesday, March 03, 2026 No comments

 





Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imesogeza karibu huduma za Sekta ya Ardhi kwa wanawake nchini nchini kupitia Kliniki ya Ardhi Maalumu "Samia Ardhi Kliniki"

Mkoa wa Simiyu ni miongoni mwa mikoa ambayo Kliniki hiyo inaendeshwa ambapo inatarajiwa kuzinduliwa rasmi Machi 4, 2026 na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anamringi Macha katika Viwanja vya Sabasaba vilivyopo katika mji wa Bariadi.

Katika kufanikisha Kliniki hiyo, Wizara na Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Simiyu inashirikiana na team ya wataalamu wa Sheria kutoka Mama Samia Legal Aid kutoa huduma za Sekta ya Ardhi ikiwemo upimaji wa ardhi, utoaji wa Hati Miliki, uhamishaji wa umiliki, uthamini wa ardhi, kusikiliza changamoto mbalimbbali za sekta ya ardhi na kutoa ushauri wa kitaalamu kuhusu matumizi bora ya ardhi.

Kliniki hiyo inalenga kutoa huduma za ardhi kwa wanawake nchi nzima kuelekea Siku wa Kimataifa ya Wanawake kuanzia tarehe 2 hadi 7 Machi 2026 ikiongozwa na Kaulimbiu "Haki sawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kifikia Dira 2050"
Posted by MROKI On Tuesday, March 03, 2026 No comments

March 02, 2026


WAZIRI MKUU Dkt Mwigulu Nchemba amepokea kero na hoja mbalimbali 305 kutoka kwa wananchi wa Wilaya ya Mbulu akiwa kwenye mkutano wa hadhara ambao ni wa mwisho katika ziara ya kikazi ya siku tatu ya Mkoa wa Manyara.

Akizungumza na wananchi na viongozi mbalimbali leo jioni (Jumatatu, Machi 2, 2026) katika uwanja wa mpira wa Mbulu Mjini, Waziri Mkuu amesema anataka kuona utaratibu wa kulundika kero za wananchi unaisha mara moja. 

“Kila mtu aliyeko ofisini anapaswa ajishughulishe na mambo yanayowahusu wananchi. Ninaandaa utaratibu, kila mwisho wa mwezi kila mtu atapaswa kutoa taarifa ametatua kero ipi na ipi imeshindikana kuanzia kijiji na mtaa, kata, tarafa, wilaya hadi mkoa. Tutafuatilia utekelezaji wake,” amesema. 

Dkt. Mwiguliu amesisitiza kuwa hilo siyo la suala la ziara tu bali anataka wananchi wakifika kwenye ofisi za viongozi wapewe vitabu vya wageni na waandike hoja zao ili iwe rahisi kufuatilia utekelezaji wake.

Amesema kuwa mambo ya kupuuza na kuzoea shida za wananchi siyo makusudi ya kuanzishwa kwa ofisi za umma. “Tunataka watumishi wajihusishe na matatizo ya wananchi. Tulianzisha ofisi siyo kwa ajili ya kugawana madaraka, bali watafute ufumbuzi wa matatizo ya wananchi. Tunataka mambo ambayo yanaweza kufika ukomo yaishe,” amesisitiza.

Akiwa njiani kuelekea Mbulu mjini, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba alikagua ujenzi wa barabara ya km 25 kutoka Mbulu hadi Garbabi ambayo ni sehemu ya barabara kuu inayojengwa kwa kiwango cha lami kutoka Karatu – Mbulu – Haydom – Sibiti River – Lalago – Maswa yenye urefu wa km 389.

Utekelezaji wa mradi huo umefikia asilimia 41.7 ambapo sh. bilioni 36.3 zitatumika kukamilisha ujenzi. Hadi sasa, sh. bilioni 12.5 tayari zimeshalipwa.

Mradi huo unaotekelezwa na Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) unalenga kuboresha mawasiliano ya barabara, kuimarisha usafirishaji wa watu na bidhaa, na kuchochea ukuaji wa uchumi katika maeneo husika.

Mapema, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga alisema kwa mara ya kwanza wameandika historia ya kushika namba mbili kitaifa kwenye matokeo ya kidato cha nne ya mwaka jana. “Hii ni historia, haijapata kutokea,” alisema. 

“Huu si muujiza bali ni majibu ya jitihada za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwekeza katika elimu kwa kujenga shule za msingi na sekondari, madarasa mapya na mabweni ili kupunguza umbali kwa watoto hasa wanaotoka kwenye jamii za wafugaji,” alisema.
Posted by MROKI On Monday, March 02, 2026 No comments







WAZIRI MKUU Dkt Mwigulu Nchemba amewaomba Wabunge wa Mbulu na uongozi wa wilaya hiyo waendelee kutoa elimu kwa wananchi juu ya kuendeleza amani na kuishi kindugu.

Ametoa wito huo leo (Jumatatu, Machi 2, 2026) wakati akizungumza na wananchi waliojitokeza kwenye hospitali ya Lutheran ya Haydom, wilayani Mbulu, mkoani Manyara mara baada ya kukagua ujenzi wa jengo la afya ya mama na mtoto.

“Nimepata taarifa ya kuwepo kwa mizozo kule Yaeda Chini. Waheshimiwa Wabunge wa majimbo haya mawili na viongozi wa Halmashauri kaeni na wananchi muwaelimishe kuwa ardhi haiongezeki. Kaeni na wananchi muwaeleze kuwa suluhisho ni kupanga matumizi bora ya ardhi.”

“Endeleeni kuwaelimisha wananchi kuwa hata wakipigana ardhi haiongezeki. Hata mkiwaondoa kabila fulani, bado ardhi haiongezeki kwa sababu watu wanaendelea kuzaa.”

Akizungumzia kuhusu ujenzi wa jengo hilo, Waziri Mkuu amesifu kazi nzuri iliyofanywa na akamshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya hospitali zinazoendeshwa na taasisi za dini ili kuboresha utoaji huduma kwenye hospitali hizo. 

“Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alielekeza taasisi zinazotoa huduma kwa jamii (charitable organisations) zipewe nafuu ya kikodi. Hii ni kwa sababu hizi taasisi hazifanyi biashara na serikali inatambua mchango mkubwa unaofanywa na hizo taasisi,” amesema. 

Akitoa maelezo kuhusu fedha zinazotolewa na serikali kwenye hospitali hiyo, Naibu Waziri – OWM-TAMISEMI (Elimu), Reuben Kwagilwa alisema kumekuwa na ushirikiano wa mrefua ambapo kila mwezi, Serikali imekuwa ikilipa sh. milioni 188 kwa ajili ya watumishi 128 wa hospitali hiyo.

“Serikali pia imekuwa ikitoa ruzuku ya sh. milioni 545 kila mwaka ambazo hupitia MSD kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba. Vilevile, imekuwa ikitoa sh. milioni 57 kila mwaka kwa ajili ya uendeshaji wa hospitali,” amesema.

Mapema, Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Dayosisi ya Mbulu, Askofu John Nade alimweleza Waziri Mkuu kwamba wanashukuru kwa ushirikiano uliopo baina ya Serikali na kanisa kwenye utoaji wa huduma za jamii.

Alisema mbali na hospitali, wana Taasisi ya Afya ya Haydom ambayo inatoa mafunzo kwenye kozi tano ambazo ni Radiolojia, Famasia, Afisa Tabibu, Maabara na Uuguzi.

Akitoa taarifa ya ujenzi wa mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Haydom, Dkt. Paschal Mdoe alisema ujenzi wa jengo hilo umegharimu sh. bilioni 6.3 ambazo zimetokana na vyanzo vya ndani na marafiki wa Haydom Norway.

Alisema hospitali hiyo ya Kanisa imekuwa mdau mkubwa na wa muda mrefu katika sekta ya afya, ikitoa huduma za rufaa na kibingwa kwa wananchi wa Mkoa wa Manyara na mikoa jirani, pamoja na kushirikiana na Serikali katika kuboresha huduma za afya ya jamii.
Posted by MROKI On Monday, March 02, 2026 No comments
Na Mwandishi wetu, Kilimanjaro
MKAKATI wa uongezaji thamani katika Sekta ya Madini umeanza kuzaa matunda mkoani Kilimanjaro, baada ya kampuni ya Mega Copper Co Ltd kujikita katika uongezaji wa kiwango cha ubora wa madini ya shaba kutoka asilimia moja hadi kufikia kati ya asilimia 20 na 25.

Akizungumza katika kijiji cha Kiruru, wilayani Mwanga, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Ally Ng’anzo, amesema maboresho hayo yameongeza ushindani wa kampuni katika soko la kimataifa, huku China ikiwa soko kuu la sasa la mauzo ya madini hayo.

Amesema pamoja na kampuni kufikia hatua hiyo ya uongezaji thamani ili kuzalisha makinikia ya shaba, matarajio yao ni kufanya uwekezaji zaidi kwa kufunga mitambo maalum ya uongezaji thamani, ili kufikia ubora wa hadi asilimia 99. Hatua hiyo inatarajiwa kuongeza thamani ya bidhaa hiyo, kupanua wigo wa masoko na kuimarisha upatikanaji wa malighafi ya kutengeneza bidhaa za shaba kwa viwanda vya ndani.

Kwa mujibu wa Ng’anzo, kampuni hiyo ina wafanyakazi 65, wakiwemo 20 wa kiwandani na 45 wa migodini, hali inayochangia ajira kwa vijana wa Mwanga na maeneo ya jirani, sambamba na kukuza uchumi wa jamii inayozunguka mgodi huo.

Kwa upande wake, Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhandisi Abel Madaha, amesema mgodi huo unaomilikiwa kwa asilimia 100 na Watanzania umeendelea kuwa chanzo muhimu cha mapato, ukichangia  zaidi ya Shilingi milioni 500 katika kipindi cha miaka miwili iliyopita kupitia tozo ya mrabaha pekee.

Amesisitiza kuwa mgodi huo ni mfano halisi wa utekelezaji wa sera ya Serikali ya kuhimiza uongezaji thamani wa madini kabla ya kusafirishwa nje ya nchi, hatua inayolenga kuongeza mapato ya taifa, ajira na uhamishaji wa teknolojia.

Mhandisi Madaha amewahimiza wawekezaji wengine kutumia fursa zilizopo mkoani humo, akieleza kuwa Kilimanjaro ina rasilimali za madini ya metali na viwandani ambazo bado hazijaendelezwa kikamilifu.

“Ofisi ya Madini itaendelea kutoa ushirikiano kwa wawekezaji wote ili kuhakikisha Sekta ya Madini inakua kwa kasi na kuchangia ipasavyo maendeleo ya mkoa na taifa kwa ujumla,” amesema.



Posted by MROKI On Monday, March 02, 2026 No comments
Mwanasheria Mkuu na Waziri wa Katiba wa Ghana Dominic Akuritinga Ayine akipokea Tuzo kwa niaba ya Rais John Mahama wa Ghana
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akikabidhi Tuzo kwa Waziri Mkuu wa Lesotho, Samuel Matekane
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia  wakati wa Hafla hiyo ya kukabidhi Tuzo kwa Viongozi Bora wa Mwaka wa Afrika kwa Mwaka 2026.
********
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amekabidhi Tuzo za Viongozi Bora barani Afrika kwa Mwaka 2026 katika Hafla iliyofanyika Accra, Ghana tarehe 28 Februari 2026.

Tuzo hizo zinatolewa na Jarida la Africa Leadership Magazine linaloandaliwa na Taasisi ya Uongozi Afrika (Africa Leadership Organisation) ambayo Rais Mstaafu Dkt. Kikwete ni Mwenyekiti wa Bodi yake ya Ushauri.

Mshindi wa Jumla wa Tuzo hizo ni Rais John Dramani Mahama wa Ghana, ambaye ametunukiwa Tuzo ya Mwafrika wa Mwaka kwa Mwaka 2026 kwa kutambua mchango wake katika kukuza demokrasia na uchumi nchini Ghana pamoja na kuwa kinara katika kuimarisha utengamano wa kikanda kupitia Eneo Huru la Biashara Afrika (AfCFTA).

Akihutubia kabla ya kukabidhi Tuzo hiyo ya mshindi wa jumla, Rais Mstaafu Dkt. Kikwete ameeleza kuwa "kila kizazi za uongozi hukutana na changamoto za kipekee za wakati wake na hivyo hulazimika kubuni njia za kipekee za kuzitatua". Akaongeza kuwa "kipimo mojawapo cha mafanikio katika uongozi ni kuweza kukuza kipato cha mtu mmoja mmoja na kuboresha hali ya jumla ya kimaisha kwa watu unaowaongoza kutoka hali ya chini kwenda hali ya juu zaidi".

Mbali na Rais Mahama, miongoni mwa watu mashuhuri waliiopata Tuzo hizo ni pamoja na Waziri Mkuu wa Ufalme wa Lesotho, Samuel Matekane aliyepata tuzo kwa kutambua mchango wake katika kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na Sekta Binafsi nchini Lesotho pamoja na Mkuu wa Majeshi wa Uganda, Jenerali Muhoozi Kainerugaba aliyepata tuzo kwa kutambua mchango wake katika kuliimarisha jeshi la Uganda na kukuza diplomasia ya kijeshi katika ukanda wa maziwa makuu.

Rais wa Namibia Netumbo Nandi-Ndaitwah alipata Tuzo ya Kiongozi Bora wa Kisiasa Afrika huku Makamu wa Rais wa Angola Esperança da Costa, Makamu wa Rais wa Angola akioata Tuzo ya Kiongozi Bora Mwanamke barani Afrika.

Tuzo ya Rais Mahama ilipokelewa kwa niaba yake na Mwanasheria Mkuu wa Ghana, ambaye pia ni Waziri wa Sheria wa Ghana, Dominic Akuritinga Ayine wakati tuzo ya Jenerali Kainerugaba ilipokelewa na Msemaji wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Uganda, Kanali Chris Magezi.

Kila mwaka Jarida la Africa Leadership Magazine huratibu mchakato wa wazi unaojumuisha kupokea mapendekezo ya viongozi mbalimbali wenye sifa ambao hupigiwa kura kwa njia ya mtandao ili kupata washindi. 

Viongozi wa tasnia mbalimbali zikiwemo uongozi wa kisiasa, diplomasia, biashara na uwekezaji, ujasiriamali, habari, ulinzi na usalama, nk., wanaoshinda hupokea Tuzo hizo kwa kutambua mchango wao katika kusimamia vizuri tasnia zao pamoja na kulea na kuwaandaa vijana wanaowaongoza ili kuja kuwa viongozi bora wa baadaye.

Katika hafla hiyo, jumla ya Tuzo 36 zilitolewa.

Jarida la Africa Leadership Magazine linaloandaliwa na Taasisi ya Uongozi Afrika (Africa Leadership Organisation) ambayo Rais Mstaafu Dkt. Kikwete ni Mwenyekiti wa Bodi yake ya Ushauri.

Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akisalimiana na mwigizaji maarufu wa kimataifa wa Ghana Bw. Moses Nyarko aliyeshiriki katika Hafla hiyo ya utoaji wa Tuzo kwa Viongozi Bora barani Afrika kwa Mwaka 2026.
Kanali Chris Magezi, Msemaji wa Jeshi la Wananchi la Uganda akipokea Tuzo kwa niaba ya Mkuu wa Majeshi wa Uganda, Jenerali Muhoozi Kainerugaba
Posted by MROKI On Monday, March 02, 2026 No comments

March 01, 2026

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba leo tarehe 1 Machi, 2026 akiweka jiwe la msingi la uzinduzi wa stendi ya mabasi iitwayo Dkt. Samia Suluhu Hassan iliyopo Kateshi mkoani Manyara. Mradi huo umegharimu kiasi cha Shilingi Bilion 5.69 hadi kukamilika kwake. 
 
Muonekano mradi wa stendi ya mabasi iitwayo Dkt. Samia Suluhu Hassan iliyopo Kateshi mkoani Manyara ambayo imezinduliwa leo tarehe 1 Machi, 2026. Mradi huo umegharimu kiasi cha Shilingi Bilion 5.69 hadi kukamilika kwake.


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amezindua Stendi ya Mabasi ya Dkt. Samia Suluhu Hassan iliyopo Katesh, wilayani Hanang, mkoani Manyara ambayo imejengwa kwa gharama ya sh. bilioni 5.69.

Stendi hiyo ambayo ujenzi wake umekamilika na imeanza kutumika, imelenga kuboresha utoaji huduma za usafiri na usafirishaji. Miundombinu iliyopo ni pamoja na jengo kuu la kituo cha mabasi, maduka 116, maeneo ya wauza vyakula, vyoo matundu 21, vituo saba vya kukusanyia taka na vituo viwili vya ukaguzi na ulinzi. Hakuna kituo cha polisi. 

Akizungumza na wakazi wa Hanang waliofika kushuhudia uzinduzi huo leo (Jumapili, Machi Mosi, 2026), Waziri Mkuu amesema ameridhishwa na ujenzi wa stendi hiyo ambao ni sehemu ya miradi ya kimkakati ya kuboresha miundombinu ya usafiri na kuongeza mapato ya ndani.

Dkt. Mwigulu ametumia fursa hiyo kumwagiza Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya awasiliane na Waziri wa Ujenzi na Mtendaji Mkuu wa TANROADS ili watafute fedha za kuitengeneza barabara ya Katesh – Babati kutokana na uchakavu ilionao.

Amesema barabara za wilayani za mkoa wa Manyara ziangaliwe na kujengwa haraka kwani mkoa wa Manyara ni miongoni mwa mikoa ambayo haina barabara za lami za wilaya. “Ukiondoa barabara kuu ya Arusha - Dodoma na hii ya Babati – Singida kupitia Katesh, hawana barabara nyingine.”

Kuhusu tabia ya kuwanyang'anya wajasiriamali zana zao za kazi, Waziri Mkuu amekemea tabia hiyo na kuwataka watendaji wanaofanya hivyo waache mara moja. “Acheni watu wafanye kazi, bakuli, sahani, bajaji au pikipiki ni vitendea kazi vyao. Msikamate vitendea kazi vyao,” amesisitiza.

“Tusichukue bidhaa za watu, tusitupe bidhaa za watu hiyo ni mitaji yao. Tuna kazi kubwa ya kutekeleza Dira 2050, tunahitaji fedha nyingi kutekeleza miradi iliyopo. Msichukue bidhaa zao, kama kuna jambo tuongee nao, tuwaeleweshe,” amesisitiza.


Kuhusu kesi zilizoko mahakamani au zilizotolewa maamuzi na mahakama, Waziri Mkuu amewataka wananchi wafuate taratibu za kisheria kwa vile Serikali ni mhimili mwingine na unaheshimu maamuzi yanayotolewa na na mhimili wa mahakama. Amesema maamuzi ya kimahakama hayabatilishwi na matamko ya viongozi kama Makamu wa Rais, Waziri Mkuu au Mkuu wa Mkoa.

“Jambo likishaenda mahakamani Mkuu wa Mkoa wala Waziri Mkuu hawawezi kuweka neno hapo. Sisi ni lazima tuheshimu utaratibu wa kisheria. Kama mwananchi hajaridhika na maamuzi ya awali, ipo njia. Ipo milango ya kufuata, lakini sisi hatuwezi kuingilia maamuzi ya mhimili wa sheria,” amesisitiza.

Waziri Mkuu ambaye amekuwa akisikiliza kero za wananchi kwenye mikutano yake ya hadhara, leo kwenye mkutano huo amepokea hoja nyingi zilizohusu kesi za madai na mirathi, migogoro ya ardhi, familia kudhulumiana na mipaka ya mashamba.
Posted by MROKI On Sunday, March 01, 2026 No comments





Na Mwandishi Wetu, Same
SHUGHULI za uchimbaji wa madini ya Jasi katika vijiji vya Ruvu Jiungeni na Makanya, wilayani Same mkoani Kilimanjaro, zimeendelea kushika kasi huku wachimbaji wadogo wenye leseni zaidi ya 200 wakiungana kuimarisha uzalishaji na usimamizi wa rasilimali hiyo muhimu kwa viwanda vya saruji na bidhaa nyingine za viwandani.

Wachimbaji hao wameanzisha chama chao kwa lengo la kusimamia maslahi na kuratibu uendeshaji wa shughuli za uchimbaji, hatua inayotajwa kuongeza tija, uwajibikaji na mchango wa sekta hiyo kwa wanachama pamoja na jamii inayowazunguka. Katika kipindi cha takribani mwaka mmoja, wamefanikiwa kuweka mifumo ya pamoja ya usimamizi na udhibiti wa mapato.

Akizungumza wilayani humo, Mhandisi Abel Madaha, Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kilimanjaro anayesimamia wilaya za Same, Mwanga, Hai, Rombo, Siha na Moshi, amesema pamoja na fursa za kiuchumi zinazotokana na madini hayo, sheria inazitaka leseni zote kuhakikisha kunakuwa na urejeshaji wa mazingira mara baada ya uchimbaji kukoma.

Amesema kwa kutambua wajibu huo, wachimbaji wameanzisha mfuko maalum wa Ukarabati wa Mazingira (Rehabilitation Fund) wenye akaunti ya pamoja, ambapo kila gari la madini linalotoka eneo la uchimbaji linachangia kiasi maalum cha fedha kwa ajili ya kurekebisha maeneo yaliyoathirika, badala ya kumwachia mchimbaji mmoja mmoja jukumu hilo.

“Mfuko huu unasimamiwa kwa pamoja chini ya Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ili kuhakikisha fedha zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa,” amesema Mhandisi Madaha.

Aidha, ametoa wito kwa wawekezaji kuchangamkia fursa zilizopo katika kuongeza thamani ya madini ya Jasi badala ya kutegemea soko la viwanda vya saruji pekee, akieleza kuwa madini hayo yanaweza kuzalisha bidhaa mbalimbali zikiwemo gypsum powder, gypsum board, mikanda zinazotumika katika ujenzi na bidhaa nyingine kama chaki nk.

Kwa mujibu wa Mhandisi Madaha, Mkoa wa Kilimanjaro umejipanga kukusanya Shilingi bilioni 4.2 katika mwaka wa fedha 2025/2026 na tayari umevuka zaidi ya asilimia 60 ya lengo hilo, huku madini ya Jasi yakichangia kati ya asilimia 45 hadi 50 ya mapato yote ya Sekta ya Madini mkoani humo.

Ameongeza kuwa katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, jumla ya Shilingi bilioni 2.6 zimekusanywa kutoka shughuli za uchimbaji wa Jasi, jambo linalodhihirisha ukuaji wa sekta hiyo na mchango wake kwa mapato ya Serikali.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji wa Jasi Mkoa wa Kilimanjaro, Emmanuel Mbwambo, amesema lengo la chama hicho ni kuwaunganisha wachimbaji wadogo, kuongeza uzalishaji na faida, pamoja na kuhakikisha wanatekeleza wajibu wao kwa mujibu wa sheria.

Amesema chama kimeweka mkakati wa kuwa na kiwanda chao wenyewe kitakachotengeneza bidhaa zinazotokana na jasi na kuomba Serikali kuwaunga mkono ili waweze kufikia malengo yao.

Ameongea kuwa chama hicho pia kimejikita katika utekelezaji wa miradi ya uwajibikaji kwa jamii (CSR), ikiwamo kuchangia huduma za kijamii kwa wananchi wanaoishi jirani na maeneo ya uchimbaji, hatua inayolenga kuimarisha mahusiano mema kati ya wachimbaji na jamii.
Posted by MROKI On Sunday, March 01, 2026 No comments

February 28, 2026








Na Mwandishi Wetu, Rombo
MGODI wa Rock Block uliopo Wilayani Rombo, mkoani Kilimanjaro, umeendelea kuwa kichocheo cha mageuzi katika Sekta ya Madini ya Ujenzi kwa kuzalisha ajira 122 na kuiingizia Serikali zaidi ya Shilingi milioni 400 katika kipindi cha miaka mitatu ya uendeshaji wake.

Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhandisi Abel Madaha, amesema hayo kupitia mahojiano maalum Wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro na kuongeza kuwa uchimbaji na uchongaji wa miamba kwa ajili ya kutengeneza matofali na bidhaa nyingine za ujenzi ikiwa ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kusimamia na kuendeleza madini ya ujenzi ili kuongeza thamani na mapato ya taifa.

Amesema mgodi huo umeendelea kuchangia mapato ya Serikali kupitia ada, mrabaha na kodi mbalimbali zinazolipwa kwa taasisi ikiwemo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na Halmashauri ya Wilaya, hali inayochochea maendeleo ya kiuchumi katika eneo la Rombo na mkoa wa Kilimanjaro kwa ujumla.

Mhandisi Madaha amefafanua kuwa miamba inayochimbwa katika eneo la Holili ilitokana na milipuko ya lava kutoka Mlima Kilimanjaro, jambo linalolifanya eneo hilo kuwa na malighafi adimu na ya kipekee inayopatikana Rombo pekee nchini.

Amesema bidhaa zinazozalishwa na mgodi huo ni pamoja na matofali ya miamba, paving blocks, vigae, coblestone, wall cladding, kerbstone zinazotumika katika utengenezaji wa kingo za barabara, pozolana — mchanga maalum mweusi unaotumika katika uzalishaji wa Saruji na kazi nyingine za ujenzi.

Kwa mujibu wa Mhandisi Madaha, matofali ya miamba yana uimara mara tatu zaidi ya matofali ya kawaida, hayaathiriwi na fangasi wala ukungu na hudumu kwa muda mrefu, jambo linaloyafanya kuwa chaguo sahihi kwa miradi ya kisasa ya ujenzi. 

Amewahimiza wawekezaji kujitokeza kuwekeza katika Sekta ya Madini ya ujenzi kwa kuwa ina fursa kubwa ya kukuza uchumi na ajira.

Naye Mkurugenzi wa Rock Block Limited, Fabian Woisso, amesema kampuni hiyo imeajiri wafanyakazi 72 wa kudumu na vibarua 50, hatua inayochangia kupunguza changamoto ya ajira kwa vijana katika eneo hilo.

Amesema soko la bidhaa zao ni la ndani ya nchi, hususan katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Tanga, Dodoma na Dar es Salaam, ambapo mahitaji ya vifaa vya ujenzi yamekuwa yakiongezeka kufuatia kukua kwa miradi ya miundombinu na makazi.

Aidha, Woisso amesema kampuni imewekeza katika miradi ya uwajibikaji kwa jamii (CSR), ikiwemo ujenzi wa barabara ya kilomita tisa kutoka Holili hadi Kidondoni, ujenzi wa darasa katika Shule ya Msingi Kidondoni na uchangiaji wa matofali kwa shule na vituo vya polisi.

Amehitimisha kwa kuwataka vijana kuchangamkia fursa zilizopo katika Sekta ya Madini ya Ujenzi, akisisitiza kuwa sekta hiyo ina uwezo wa kuongeza ajira, mapato ya taifa na kuimarisha maendeleo ya mtu mmoja mmoja na jamii kwa ujumla.
Posted by MROKI On Saturday, February 28, 2026 No comments

February 27, 2026



On August noon in forty-four, beneath Tanganyika’s sky,
In Mwazye’s quiet parish land, a child began to cry.
The sixth of nine, yet heaven-marked before the world could see,
A shepherd chosen long before he bent his first small knee.

His sister saw the spark in him and made a solemn vow,
To guard his dream with sacrifice, though trials pressed her brow.
Her youth she gave, her wages too, his schooling to defend,
So he might serve the Lord of Life until his journey’s end.

Through Karema’s halls and Kaengesa’s rising gleam,
Through Kipalapala’s sacred books and nights of ceaseless stream,
His mind grew luminous, his spirit ardent, his purpose living beam,
A leader formed by discipline, by prayer, by sacred theme.

Ordained a priest in seventy-one, still humble, still afraid,
Yet faithful to the call of God, whatever price was paid.
In Rome he drank from ancient wells of moral truth and grace,
Then hastened home to serve his land, not seek a higher place.

A bishop young in Nachingwea, in Tunduru he stood,
To build where little yet was formed, to plant where none yet could.
Though fear would knock upon his heart whenever roles were new,
His answer was obedience, God’s will he would pursue.

In Dar he rose to guide the flock where giants once had been,
A Cardinal in scarlet red, yet simple still within.
He asked, “Why beg for distant grain when ours can fill the bowl?”
And taught the Church to stand upright in dignity of soul.

From twenty parishes he dreamed of one hundred in their place,
They doubted such a vision vast could ever run that race.
But when he laid the crozier down and passed the charge along,
One hundred eighteen stood in faith, his vision proved them wrong.

For death to him was not defeat, nor darkness, nor despair,
But simply door to promised glory beyond all earthly care.
The pilgrim laid his labors down where saints and angels sing,
And entered joy no mortal tongue could fully name or bring.

Though on 19 February he left this earthly state,
On 28 February, in solemn farewell we congregate.
Not stripped of honor, nor lost to sight,
But clothed in dignity, in hallowed rite.

A priest for decades he faithfully stood,
A guide in truth, in strength, in good.
A bishop, archbishop, cardinal upright,
A conscience steady in nation’s sight.

Eternal rest, O Lord, bestow,
Let endless light upon him glow.
May he who led with faithful hand
Now dwell within God’s promised land.

And when the final trumpet rings,
And time surrenders all its kings,
May the shepherd, his flock, and the Church above,
Rejoice in resurrected love.

His spirit whispers still,
Through every heart he touched, through every faithful will.
Though tears may fall, his love will never fade,
A shepherd, father, guide, forever ours to aid.

Thank you.

Written by Christopher Makwaia
Tel: +255 789 242 396


- The writer, is a University of West London graduate (formerly Thames Valley University) and an expert in Management, Leadership, International Business, Foreign Affairs, Global Marketing, Diplomacy, International Relations, Conflict Resolution, Negotiations, Security, Arms Control, Political Scientist, and a self-taught Computer Programmer and Web Developer.


Posted by MROKI On Friday, February 27, 2026 No comments





🔴DC atoa siku tatu watoto wa bweni warejeshwe makwao

ZIARA ya Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba jijini Arusha imewazindua watendaji na kujikuta wakibaini ujenzi wa shule ya ghorofa usio na vibali na watoto kulazwa katika bweni wakati ujenzi ukiendelea kwenye ghorofa hizo.

Hayo yamebainika leo (Ijumaa, Februari 27, 2026) wakati Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Joseph Mkude na Kamati ya Usalama ya Wilaya walipofanya ziara kwenye shule ya Nariva Hill na kufanya ukaguzi katika madarasa, mabweni, jikoni na eneo wanalojenga ghorofa juu ya bweni lililokuwa linatumika.

Katika ziara hiyo shuleni hapo ambayo ilikuwa ni utekelezaji wa maagizo ya Waziri Mkuu, viongozi hao walibaini kuwepo kwa msongamano wa wanafunzi wa kike wanaolala katika bweni la muda ilhali hawana vyoo wala mabafu kwenye ghorofa yao. Pia walibaini baadhi ya watoto wanalala wawiliwawili kwenye kitanda kimoja.

“Yale mabweni sikuona standards za Wizara ya Elimu, kuanzia leo natoa muda wa siku tatu tu kwa sababu hawa watoto wana kwao; kwa hiyo wazazi wao lazima wajulishwe. Natoa siku tatu mabweni haya yawe yamefungwa. Tumepewa tahadhari ya magonjwa ya kipindupindu na mfumo wa hewa, hali iliyopo mabwenini haipo sawa, yafungwe warudi kusoma shule ya kutwa,” amesema Mkuu huyo wa Wilaya.

Pia amesitisha ujenzi unaoendelea shuleni hapo kwa kuwa hawana vibali vya ujenzi licha ya kuwa walishapewa stop order tangu Oktoba 13, 2025 lakini wakakaidi na kuendelea na ujenzi. “Stop order ilitolewa tangu mwezi wa Oktoba na haikuzingatiwa. Kwa hiyo, kuanzia leo, ianze kutekelezwa hadi vibali kamili vitakapotolewa,” amesema.

Vilevile amemwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Jiji la Arusha na Mkaguzi wa Elimu wafuatilie barua halisi zilizoruhusu usajili wa shule hiyo ikiwemo nakala za vibali vya kuruhusu kulaza watoto shuleni.

 “Walete nakala za vibali kutoka wizara ya elimu na haraka viwasilishwe kwenye ofisi ya TAKUKURU ya Wilaya ili wafanye uchunguzi zaidi,” amesisitiza.

Mkuu huyo wa Wilaya amesema hali ya jikoni shuleni hapo ni chafu, hakuna bwalo na watoto waliopo shuleni ni zaidi 1,700. Amewataka wamiliki wa shule hiyo wazingatie viwango vya wizara ya elimu vya ujenzi wa jiko.

Kuhusu maji yanayotumiwa na wanafunzi, Mkude amesema eneo la maji ya kunywa ni finyu na watoto wanapokezana vikombe vya kunywea maji kutoka kwenye tenki. 

Amewataka waweke mifumo ya mabomba kama ilivyoelekezwa na wizara ya elimu ambapo mabomba mengi huwekwa kwa pamoja na watoto wanaweza kunywa bila kupanga foleni.

Mapema, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Javelin Gaspar alisema shule hiyo ambayo ilianzishwa mwaka 2016, ina wanafunzi 1,726 wanaosoma kuanzia shule ya awali hadi darasa la saba. “Shule ina madarasa 55, walimu 42, mabweni mawili ambapo wanafunzi wanaolala shuleni ni 162.

Alipoulizwa kuhusu uwepo wa vibali vya ujenzi, mmiliki wa shule hiyo, Emmanuel Saanya na mshauri wa ujenzi wa shule hiyo, Emmanuel Rajab walikiri kutokuwa na vibali vya ujenzi.

Mkuu wa Wilaya hiyo alimwagiza Kamanda wa Polisi wa Wilaya, Georgina Matagi aende nao polisi wakatoe maelezo yao leo hii hii. 
Posted by MROKI On Friday, February 27, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo