Nafasi Ya Matangazo

April 12, 2026





Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, amekutana na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kiarabu ya Sahara (SADR), Mhe. Brahim Ghali. Katika mazungumzo hayo, aliwasilisha salaam za Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mazungumzo hayo yalifanyika tarehe 9 Aprili 2026 katika makazi rasmi ya Mhe. Ghali, Kambi ya Ausserd, Tindouf, Algeria. Balozi Migiro alisisitiza kuwa msimamo wa Tanzania na CCM wa kuunga mkono haki ya watu wa Saharawi kujitawala ni wa muda mrefu. Alieleza kuwa msingi wake uliwekwa tangu enzi za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Kwa upande wake, Mhe. Ghali alimshukuru Rais Dkt. Samia kwa salaam na kwa kutuma uwakilishi kwenye maadhimisho ya miaka 50 ya SADR yaliyofanyika tarehe 8 Aprili 2026 katika Kambi ya Ausserd. Pia aliomba salamu zake zifikishwe kwa Rais, CCM na Watanzania.

Aliongeza kuwa watu wa Saharawi wanathamini mchango wa Mwalimu Nyerere katika kuhamasisha mshikamano wa Afrika na dunia. Alisema mshikamano huo umeendelea kuimarisha harakati za SADR, chini ya uongozi wa Chama cha Polisario, katika kudai haki ya kujitawala.
Posted by MROKI On Sunday, April 12, 2026 No comments





Na Mwandishi wetu, Dodoma
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imepatiwa mafunzo maalum kuhusu Sheria, Kanuni na Miongozo ya Sekta ya Madini, kwa lengo la kuongeza uelewa hususan juu ya tofauti kati ya Haki ya Ardhi na Haki ya Madini.

Mafunzo hayo yamefanyika katika Ukumbi wa Tanzanite, Makao Makuu ya Tume ya Madini, jijini Dodoma.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema kuwa umiliki wa haki ya madini na haki ya ardhi ni mambo mawili tofauti kisheria, na kwamba mwenye leseni ya madini haruhusiwi kuanza shughuli za uchimbaji bila kufikia makubaliano na mmiliki wa ardhi husika.

Amefafanua kuwa, kwa mujibu wa Sheria, leseni ya madini inaweza kutolewa katika eneo lolote, lakini utekelezaji wake unahitaji ridhaa au makubaliano na mwenye haki ya ardhi. Hata hivyo, iwapo makubaliano hayatapatikana, Waziri ana mamlaka ya kuruhusu shughuli za uchimbaji kuendelea kwa kuzingatia sheria.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgalu, ameipongeza Wizara ya Madini kwa kuandaa mafunzo hayo, akieleza kuwa yameongeza uelewa na kuwajengea wabunge uwezo wa kusimamia vyema sekta hiyo.

Wasilisho kuhusu haki ya madini na haki ya ardhi limetolewa na Mkurugenzi wa Huduma za Sheria kutoka Wizara ya Madini, Dkt. Arnold Gisase, ambaye ameeleza kuwa mtu anaweza kumiliki haki ya madini bila kuwa mmiliki wa ardhi, na kwamba umiliki wa ardhi pekee haumruhusu mtu kufanya shughuli za madini bila leseni husika.

Dkt. Gisase pia amebainisha changamoto zinazojitokeza, ikiwemo uelewa mdogo wa wananchi kuhusu haki na wajibu wao, kutokuelewa taratibu za uthamini na fidia, ucheleweshaji wa malipo ya fidia, pamoja na baadhi ya wamiliki wa ardhi kudai kuwa sehemu ya umiliki wa leseni za madini.

Naye, Mwanasheria kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Method Akilimali, amesisitiza kuwa fidia kwa mmiliki wa ardhi lazima ilipwe kabla ya kuanza kwa shughuli za utafiti au uchimbaji.

Ameongeza kuwa sheria inamtaka mmiliki wa leseni kurejesha eneo katika hali yake ya awali baada ya shughuli za madini kukamilika. Aidha, ameeleza kuwa ardhi yote nchini ni mali ya umma chini ya usimamizi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama mdhamini.

Amesema pia fidia inapaswa kulipwa ndani ya miezi sita; kuchelewa hulazimu kulipwa riba, na endapo itazidi miaka miwili tangu uthamini kufanyika, tathmini hiyo hupoteza uhalali.

Akizungumzia muundo wa leseni, Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amesema zipo aina kuu tatu za leseni ambazo ni leseni ya utafiti, uchimbaji mdogo na uchimbaji mkubwa ambapo kwa leseni ya uchimbaji mdogo Mtanzania pekee mwenye umri wa kuanzia miaka 18 ndiyo anaruhusiwa kuomba.

Mhandisi Lwamo amesema leseni kubwa na ya kati inaruhusiwa kuombwa na mtu yoyote na kwa sasa kuna mfumo wa kuomba leseni bila kufika ofisi za madini.

Mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha wabunge kuelewa kwa kina masuala ya kisheria na kiutendaji katika sekta ya madini ili kuboresha usimamizi na maamuzi yenye tija kwa maendeleo ya taifa.
Posted by MROKI On Sunday, April 12, 2026 No comments

April 11, 2026

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko (wapili kulia) akishiriki kuimba Wimbo wa Wafanyakazi wakati wa ufunguzi wa Barala la Wafanyakazi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi lililokutana leo Aprili 11, 2026 mkoani Morogoro. Wengine pichani ni Mwenyekiti wa Baraza hilo na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa INEC, Ramadhani Kailima (wapili kushoto), Katibu wa Baraza, Livini Avith (kulia) na Kulia ni mtumishi wa Tume, Rose Tengu. 
Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi wakishiriki kuimba Wimbo wa Wafanyakazi wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Barala la Wafanyakazi  INEC lililokutana leo Aprili 11, 2026 mkoani Morogoro. 
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko akizungumza wakati wa kufungua baraza la Wafanyakazi la INEC. 
Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi INEC ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume, Ndg. Ramadhani Kailima akizungumza katika kikao hicho cha Baraza. 
****************
Na Mwandishi Wetu, Morogoro
Watumishi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia katiba, sheria, kanuni  na taratibu na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania.
 
Hayo yamesemwa leo Aprili 11, 2026 na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt Jimmy Yonaz wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, katika kikao kilichoketi Mkoani Morogoro.
 
“Napenda kuwaasa, kuzingatia katiba, sheria, kanuni  na taratibu mnapotekeleza majukumu ya Tume na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania,”alisema Dkt Kilabuko.
 
Dkt. Kilabuko amesema, taasisi ina malengo yake, upo uwezakano wa kuepusha migogoro ya ndani na nje ya taasisi inayoweza kuathiri utekelezaji wa majukumu ya Tume kwa ufanisi.
  
Mapema akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi INEC ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume, Ndg. Ramadhani Kailima alisema kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025.
 
“Tume imekamilisha Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 ambao ulifanyika tarehe 29 Oktoba, 2025.  Kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025. Taarifa hiyo baada ya kukamilika, itawasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,”alisema Kailima.
 
Aidha, amesema Tume ipo katika maandalizi ya uchaguzi mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Isimani mkoani Iringa kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Mhe. William Lukuvi pamoja na uchaguzi wa udiwani katika Kata mbalimbali nchini ambazo madiwani wake walifariki.
 
Katika Kikao hicho cha siku moja pia kilitumika kwa kufanya uchaguzi wa Katibu wa Baraza hilo ambapo wajumbe walimchagua Ndg. Mwitaru Keboya kuwa Katibu mpya wa Baraza akichukua nafasi ya Ndg. Livini Avith ambaye amemaliza muda wake.
Katibu Mpya wa baraza la Wafanyakazi INEC, Ndg. Mwitaru Keboya akizungumza. 
Katibu wa Baraza aliyemaliza muda wake, Ndg. Livini Avith akizungumza. 

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi INEC wakifuatilia agenda mbalimbali katika mkutano huo. 

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi INEC wakifuatilia agenda mbalimbali katika mkutano huo. 

Mwenyekiti wa TUGHE tawi la INEC, Ndg. Juvenile Kaiza akizungumza.

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi INEC wakifuatilia agenda mbalimbali katika mkutano huo. 
Posted by MROKI On Saturday, April 11, 2026 No comments

April 10, 2026




Na Shaban Juma, WAF – Dodoma
Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Florence Samizi, amesema Serikali inatarajia kujenga upya Hospitali ya Taifa Muhimbili kupitia mkopo wa shilingi trilioni 1.2, badala ya kufanya ukarabati wa majengo yaliyopo sasa.

Dkt. Samizi ametoa ufafanuzi huo bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu hoja ya Mbunge wa Sumbawanga, Mhe. Aeshi Hillary, aliyehoji kuhusu matumizi ya mkopo huo uliotengwa kwa ajili ya hospitali hiyo.

Amesema uamuzi wa kujenga hospitali mpya unatokana na hali ya majengo ya sasa kuwa yamechoka na kusambaa katika maeneo mbalimbali, hali inayopunguza ufanisi wa utoaji huduma na kushindwa kukidhi viwango vinavyohitajika kwa hospitali ya taifa.

Ameeleza kuwa kupitia mkopo huo, Serikali itatekeleza ujenzi wa hospitali ya kisasa pamoja na usimikaji wa mitambo ya tiba ya kisasa, hatua itakayoongeza ubora wa huduma za afya na kuwahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi.

Aidha, amebainisha kuwa mradi huo utahusisha ujenzi wa majengo mapya ya hospitali yenye jumla ya vitanda 1,301 pamoja na vitanda 100 vya watoto wachanga (bay cots), ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa, pamoja na uwekaji wa Mfumo wa Kisasa wa Taarifa za Afya (Health Information System – HIS).

Pia, mradi huo unaendana na vipaumbele vya maendeleo ya taifa katika kuimarisha huduma za afya za ubingwa na ubingwa bobezi, sambamba na kuimarisha mafunzo na utafiti katika sekta ya afya.

Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kuchukua takribani miaka nane, huku huduma za kila siku katika hospitali hiyo zikiendelea kutolewa bila kusitishwa.

Aidha, mradi huo ni hatua muhimu ya Serikali katika kuboresha miundombinu ya afya na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora ndani ya nchi bila kulazimika kusafiri nje kwa matibabu.
Posted by MROKI On Friday, April 10, 2026 No comments

April 09, 2026

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema hakuna zuio la kisheria wala la kikanuni linalosababisha kutokuanza utekelezaji wa Mradi wa Kuchakata na Kusindika Gesi Asilia kuwa Kimiminika (LNG) wenye thamani shilingi trilioni 100 bali Serikali inaendelea na majadiliano na wawekezaji ili kuhakikisha inalinda maslahi ya Taifa.
 
“Kinachofanyika ni masuala ya majadiliano na kwa kutambua ukubwa wa mradi huo na nchi yetu haijawahi kuingia kwenye uwekezaji mkubwa kama huo na ili kuweza kuitendea haki nchi yetu na rasilimali zake tukaona ni vema Serikali ikawa makini katika kila kipengele ili kuweza kulinda maslahi mapana ya nchi.”

Ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Aprili 9, 2026 wakati akijibu swali la Arif Premji, Mbunge wa Mtwara Vijijini katika kipindi cha Maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu. Mbunge huyo alitaka kujua ni zuio lipi la kisheria au la kisera linalosababisha kutokutekelezwa kwa mradi huo ambao ni kipaumbele cha Taifa ulioanza mwaka 2014.

Waziri Mkuu amesema majadiliano yanaendelea na yako kwenye hatua nzuri na ni vipengele vichache vinaendelea kukamilishwa ili kuweza kuanza utekelezaji, ambavyo ni pamoja na uwepo wa asilimia tatu ama zaidi ya gesi inayozalishwa itumike nchini kwani awali ilikuwa iende nje baada ya kufanyika uwekezaji. “Nchi iliona lazima kuwe na gesi itakayotumika nchini.”

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kipengele kingine ni ulazima wa uwepo wa ushiriki wa makampuni ya wazawa katika utekelezaji wa mradi huo ili kujenga uchumi ulio imara. “Mara zote Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa akielekeza ili tujenge uchumi ulio imara lazima tuyajengee uwezo makampuni ya wazawa”.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu amesema Serikali imefungua dirisha  la kutoa dhamana kwa vijana wanaokosa dhamana litakaloanza mwaka huu ambapo tayari kupitia Benku Kuu ya Tanzania (BoT) imetenga shilingi bilioni 280.

Pia, amesema yamefunguliwa madirisha ambayo vijana wanaweza kupata fursa likiwemo dirisha la kuwaunganisha katika masuala ya viwanda, masoko na taasisi za kifedha jambo ambalo lilikuwa likiwakwamisha vijana wengi.

Amesema Serikali inaendelea utaratibu wa kuandaa mazingira bora yatakayowawezesha vijana kupata vijana ajira ndani ya sekta ya umma na kwa wingi katika sekta binafsi na tayari imeshapitisha sheria ya uwekezaji ambapo wanaweza kunufaika na vivutio wanavyovipata wawekezaji wakubwa ikiwemo kupata ardhi, mapunguzo kwenye kodi, ushuru pamoja na tozo mbalimbali.

Waziri Mkuu ameyasema hayo wakati akijibu swali la mbunge wa Viti Maalumu, Timida Fyandomo aliyetaka kujua mkakati wa Serikali katika kuwawezesha vijana kuwekeza kwa kuwaunganisha na wawekezaji mbalimbali wa ndani na nje ya nchi ili kuweza kukuza wigo wa ajira.
Posted by MROKI On Thursday, April 09, 2026 No comments
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuboresha bajeti ya elimu wakati ikitekeleza mtaala mpya wa elimu ili kuziba mianya ya mahitaji shuleni.
 
“Kwa kuwa tunaenda katika mtaala mpya wa elimu, tutaendelea kuboresha bajeti. Tutaendelea kuboresha bajeti kwa sababu mahitaji yanaongezeka kila wakati katika kumfanya mtoto asome vizuri,” amesema.
 
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo Bungeni jijini Dodoma, leo (Alhamisi, Aprili 9, 2026) wakati akijibu swali la Mbunge wa Segerea, Agnesta Lambert Kaiza, kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu ambaye alitaka kujua kauli ya Serikali juu ya kukomesha michango holela inayotozwa shuleni.
 
Dkt. Mwigulu amesema Serikali haina shida na michango ya chakula ambayo imekuwa ikitolewa shuleni lakini akasisitiza kuwa endapo kutatokea michango mingine yoyote, ni lazima ifuate miongozo ya serikali na ipate baraka za Wakuu wa Mikoa husika.
 
Akitoa mfano wa michango ambayo haikubaliki, Waziri Mkuu amesema akiwa ziarani mkoani Katavi, alipokea malalamiko ya Mama mmoja ambaye mwanaye alizuiwa kujiunga na shule ya sekondari hadi atoe sh. 50,000/- ya dawati.
 
“Nilielekeza yule mtoto arudishwe shuleni na nimpongeze Mkuu wa Mkoa ambaye amenijulisha kuwa yule mtoto amesharudi shuleni. Lakini pia nilielekeza yule mwalimu mkuu naye aitwe na mamlaka za nidhamu, ahojiwe kwa uzembe wa kuona mtoto anakosa masomo kwa miezi miwili na wao wakaendelea na maisha kana kwamba hakuna jambo lililotokea,” amesema.
 
Mbali na changamoto hiyo, Waziri Mkuu amewapongeza walimu nchini kwa kujitoa bila kuchoka ili kuhakikisha watoto wa Kitanzania wanapata elimu bora. “Sote tunatambua kuwa walimu wengi wamejitoa sana katika baadhi ya maeneo. Licha ya wingi watoto na uchache wa walimu, kwa juhudi zao wamehakikisha wanakamilisha syllabus zao ili watoto wetu wapate elimu bora.”
 
Akielezea kuhusu uwepo wa walimu wa kujitolea katika baadhi ya shule, Waziri Mkuu amesema alishatoa maelekezo kwamba malipo ya walimu wa aina hiyo yatoke kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri husika badala ya kuwataka wazazi wachangie malipo yao.
 
“Wazo la kuwa na walimu wa kujitolea ni jema, na sisi wakati tunasoma tulipata mafunzo ya ziada (tuition) kwa walimu wa aina hii. Wazo la kuwa na walimu wanaojitolea ni jema lakini malipo yao yasilipwe na wazazi, badala ya kwenda kwenye michango, Mamlaka za Serikali za Mitaa watumie mapato ya ndani.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuimarisha vitengo vya tathmini na ufuatiliaji katika kila wizara ili viweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi. “Kwenye kila wizara, kuna hivi vitengo vya ufuatiliaji na tathmini. Tunapanga kuongeza bajeti zao ili viweze kutimiza wajibu wao katika ufuatiliaji wa miradi na shughuli zote za Serikali.
 
Alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Monduli, Isack Joseph Copriano aliyetaka kujua  Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha timu ya tathmini na ufuatiliaji ili kuharakisha majibu ya wananchi na hususan kero zao.
 
Alisema katika kuimarisha mawasiliano na wananchi, Serikali imeanzisha kituo cha kupokea simu (Call Centre) yenye namba 190 ambapo mwananchi mwenye shida yoyote anaweza kupiga simu na kutoa kero yake na kwamba atajulishwa majibu yake kupitia kituo hicho.
 
Amesema Serikali inataka kurejesha utaratibu wa kila kiongozi kubeba hoja za wananchi kupitia rejesta ambazo zitakuwa zinatumika kwenye ofisi za viongozi kurekodi kero za wananchi na kutoa mrejesho serikalini kila mwisho wa mwezi.
 
“Utaratibu wa kupokea kero siyo wa kwenye ziara tu, kila mwezi viongozi watapaswa kutoa taarifa ya idadi ya wananchi waliowahudumia na majibu waliyowapa wakionesha hoja zipi walipokea, namba za simu za wananchi waliohudumiwa na hizo hoja zimetatuliwa vipi.”
 
“Tunataka kurejesha utaratibu wa kila kiongozi kubeba hoja za wananchi na siyo kuacha wananchi waende kutafuta majibu kwa viongozi,” alisisitiza.
Posted by MROKI On Thursday, April 09, 2026 No comments
 
Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Reuben Kwagilwa (kushoto), akipokelewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi, alipowasili Ofisi ya Makamu wa Rais zilizopo, Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma, Aprili 9, 2026 mara baada ya kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Aprili 8, 2026.
Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Reuben Kwagilwa (kushoto) akizungumza na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi (wa pili kutoka kushoto) mara baada ya kuwasili ofisini Aprili 8, 2026. Wengine katika picha ni Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Luvanda (kulia) na Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Mitawi.
Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Reuben Kwagilwa, akipokea ua mara baada ya kuwasili Ofisi ya Makamu wa Rais zilizopo, Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma, Aprili 9, 2026.

Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Reuben Kwagilwa (Kushoto) akipokelewa na Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Luvanda, mara baada ya kuwasili Ofisi hiyo, Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma, Aprili 9, 2026.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Reuben Kwagilwa (Kushoto) akipokelewa na Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais Bw. Abdallah Mitawi mara baada ya kuwasili Ofisi hiyo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma, Aprili 9, 2026.

Posted by MROKI On Thursday, April 09, 2026 No comments

April 08, 2026

 


Na Shaban Juma, WAF – Dodoma
Serikali ya Tanzania inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kukuza utalii wa tiba, ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kuongeza uchumi wa sekta ya afya na mchango wake wa pato la Taifa.

Hayo yamesemwa leo Aprili 08, 2026, na Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Florence Samizi, bungeni jijini Dodoma, akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Dkt. Catherine Canute Joachim, katika Bunge la Kumi na Tatu, Mkutano wa Tatu, Kikao cha Nne.

Akijibu swali kwa niaba ya Waziri wa Afya,.Mhe. Mohamed Mchengerwa, Dkt. Samizi amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imewekeza zaidi kwenye uboreshaji wa miundombinu ya hospitali, ikiwemo kujenga majengo mapya na kukarabati yale yaliyochakaa.

Aidha, amesema Serikali inaendeleza upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa kama PET/CT Scan, Angio Suite, Cathlab, na CT Scan, sambamba na kuendeleza mafunzo ya kitaaluma kwa wataalamu wa afya ili kuhakikisha huduma zinakuwa za ubora wa kimataifa.

“Serikali pia inaanzisha huduma mpya za ubingwa bobezi na kuhakikisha hospitali zinapata ithibati za kimataifa, na kuzitangaza katika masoko ya kimataifa ili kuvutia wagonjwa kutoka nje ya nchi,” amesema Dkt. Samizi.

Takwimu zinaonyesha ukuaji wa utalii wa tiba: katika kipindi cha Julai 2025 hadi Februari 2026, wagonjwa 3,018 kutoka nje ya nchi walipatiwa huduma za ubingwa bobezi katika hospitali za rufaa za mikoa, kanda, maalum na taifa.

Aidha, Dkt. Samizi ameongeza kuwa Serikali inaendelea kuwekeza katika rasilimali watu kupitia Samia Health Super-specialization Program, ambapo wataalamu 1,483 wanafadhiliwa kusomea fani za ubingwa na ubingwa bobezi ndani na nje ya nchi, hatua inayolenga kuongeza ubora na uwezo wa hospitali zetu.



Posted by MROKI On Wednesday, April 08, 2026 No comments

April 07, 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum mbele ya kaburi la aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake, Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum mbele ya kaburi la aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake, Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akiweka Shada la Maua katika Kaburi la Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume mara baada ya Dua iliyofanyika katika Afisi Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kisiwandui Zanzibar leo tarehe 07 Aprili 2026, katika Siku ya Kumbukumbu ya (Karume Day).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akiweka Shada la Maua katika Kaburi la Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume mara baada ya Dua iliyofanyika katika Afisi Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kisiwandui Zanzibar leo tarehe 07 Aprili 2026, katika Siku ya Kumbukumbu ya (Karume Day).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum ya kumuombea aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake. Dua hiyo maalum imefanyika Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum ya kumuombea aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake. Dua hiyo maalum imefanyika Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.




Posted by MROKI On Tuesday, April 07, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo