Nafasi Ya Matangazo

April 02, 2026

DODOMA
Kuelekea sikukuu ya Pasaka, Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, Bw. Pendolake Elinisafi, ameongoza ziara ya kutembelea kaya za watu wenye ulemavu wa macho wilayani Chamwino (Matembebora), akiongozana na Meneja Msaidizi Huduma kwa Walipa Kodi, Bw. John Njau, pamoja na watumishi wengine wa TRA Mkoa wa Dodoma, kwa lengo la kutoa faraja, upendo na kuwajengea matumaini, akisisitiza kuwa wao ni sehemu muhimu ya jamii inayothaminiwa.

Akizungumza kwa niaba ya wanakaya hao, Mwenyekiti Bw. Yeledi Cheleso ameishukuru TRA Dodoma kwa moyo wa kujali na msaada walioutoa, akieleza kuwa hatua hiyo imeongeza faraja na kuwapa nguvu mpya ya kuendelea na maisha.

Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii, Bi. Elizabeth, ameipongeza TRA kwa kuendeleza mshikamano na jamii, akibainisha kuwa juhudi hizo zinaimarisha ushirikiano kati ya taasisi na wananchi, hususan kwa makundi yenye uhitaji maalum.

Ziara hiyo imeacha ujumbe wa upendo na mshikamano, ikionesha dhamira ya TRA ya kuendelea kugusa maisha ya jamii sambamba na majukumu yake ya ukusanyaji wa mapato.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments




Na Saidi Saidi WMJJWM - Dodoma 
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe.Dkt. Dorothy Gwajima, ametoa wito kwa jamii na wazazi kushiriki kikamilifu katika malezi na ulinzi wa watoto, ili kuzuia ongezeko la watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani. 

Akizungumza na waandishi wa habari Aprili 01, 2026 jijini Dodoma kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mtoto anayeishi na kufanya kazi mtaani, yatakayofanyika Aprili 12, 2026 Jijini Dar Es Salaam yakiwa na Kaulimbiu isemayo “Malezi na Ulinzi wa Mtoto, Wajibu wetu Sote”.

Amesema ushiriki wa pamoja ni muhimu ili kuhakikisha watoto wanakua katika mazingira salama na yenye maadili mema huku akisisitiza jukumu la malezi si la wazazi pekee, bali ni la jamii nzima. 

Aidha, Waziri Gwajima ameeleza kuwa changamoto kama umasikini, migogoro ya kifamilia, na ukatili dhidi ya watoto zimekuwa zikichangia watoto wengi kukimbilia mitaani.

Ameibainisha pia mafanikio ya juhudi za Serikali katika kuwaokoa watoto wa mitaani kuwa zaidi ya watoto 5,000 wameunganishwa na familia zao tangu kuanza kwa kampeni ya kuwaokoa watoto wa mitaani mwaka 2025.

Vilevile, Serikali imeanzisha mifumo mbalimbali, ikiwemo madawati ya ustawi wa jamii katika vituo vya usafiri na makao ya watoto, ili kuhakikisha watoto waliookolewa wanapata huduma muhimu kama elimu, afya, na malezi bora.

Waziri Gwajima ametoa wito kwa Watanzania kushirikiana na Serikali kwa kutoa taarifa za ukatili dhidi ya watoto na kuhakikisha wanapata malezi bora. Amesisitiza kuwa watoto wa mitaani wanapaswa kulindwa na kupewa fursa sawa za maendeleo, akihitimisha kwa kusema kuwa ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha hakuna mtoto anayelazimika kuishi au kufanya kazi mitaani.

Waziri Gwajima ametumia nafasi hiyo pia kuwashukuru wadau wote wanaoshirikiana na Serikali katika kuhakikisha malezi ya watoto yanaimarishwa hususani shirika SoS Village na Railway Children.

Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Dodoma, mkuu wa wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wadau wote katika kukabiliana na changamoto ya watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani, akieleza hatua mbalimbali zilizofikiwa na mkoa wa Dodoma.

Shekimweri amesema mwaka 2024 hadi 2026 Serikali ya mkoa imewaunganisha watoto 293 na familia zao.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments


Na Mwandishi wa OMH,Dar es Salaam. 
Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH) imeanza zoezi la uchambuzi wa mipango na bajeti za taasisi na mashirika ya umma, likilenga kuimarisha mchango wa taasisi hizo katika utekelezaji wa Dira 2050.

Akizungumza kuhusu zoezi hilo, Alhamis, Aprili 2, 2026, Bw. Joseph Mwaisemba, Mkurugenzi Msaidizi wa Tathmini ya Mashirika yasiyo ya kibiashara (kwa upande wa mamlaka za udhibiti), alisema jumla ya watumishi 50 wa OMH wamekutana katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere kwa ajili ya kuchambua bajeti za taasisi na mashirika ya umma 252.

Alisema uchambuzi huo unalenga kuangalia namna taasisi hizo zilivyojipanga katika kutekeleza Dira 2050 sambamba na Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (FYDP IV).

“Tunachofanya hapa ni kuangalia kwa kina mipango ya taasisi na mashirika ya umma ili kuona namna inavyochangia utekelezaji wa Dira 2050 na mipango ya maendeleo ya taifa kwa ujumla,” alisema.

Aidha, alieleza kuwa zoezi hilo pia linahusisha uchambuzi wa mikakati ya taasisi hizo katika kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kutekeleza bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27.

Kwa mujibu wake, OMH inasimamia jumla ya taasisi 308, kati ya hizo 252 zinamilikiwa na serikali kwa hisa nyingi na 56 zinamilikiwa na serikali kwa hisa chache, huku jumla ya uwekezaji ukiwa ni Sh92.3 trilioni.

OMH pamoja na mashirika yake yaliyo chini yake yanatarajiwa kukusanya Sh1.8 trilioni kama mapato yasiyo ya kodi katika mwaka wa fedha 2026/27, ikiwa ni sehemu ya bajeti ya Serikali inayokadiriwa kufikia Sh62 trilioni.

“Hivyo basi, unaweza kuona namna ambavyo zoezi hili lilivyo muhimu katika kuhakikisha malengo ya Serikali yanafikiwa,” alisisitiza.

Kisheria, utekelezaji wa zoezi hilo la uchambuzi unaongozwa na matakwa ya kifungu cha 10(2)(c) cha Sheria ya Msajili wa Hazina, Sura ya 370, pamoja na kifungu cha 17(a) cha Sheria ya Bajeti, Sura ya 439, vinavyoitaka OMH kufanya uchambuzi wa mipango na bajeti za taasisi na mashirika ya umma yaliyo chini yake.

Kwa kuzingatia msingi huo wa kisheria, lengo la uchambuzi huo ni kuidhinisha mikakati na mipango ya mwaka ya taasisi na mashirika ya umma, na kuijumuisha katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo kwa ajili ya usimamizi madhubuti wa utekelezaji pamoja na upatikanaji wa rasilimali za kugharamia mipango hiyo.

Aliongeza kuwa katika uchambuzi huo, wataalamu wanapitia mipango ya matumizi ya rasilimali kwa kuangalia mgawanyo kati ya matumizi ya kawaida, miradi ya maendeleo, pamoja na michango ya taasisi katika bajeti kuu ya Serikali.

Maeneo makuu yanayopewa kipaumbele ni pamoja na tathmini ya namna taasisi zilivyojipanga kutekeleza miradi ya maendeleo kwa kutumia fedha za Serikali na zile zinazotokana na vyanzo vya ndani vya mashirika husika.

Baada ya kukamilika kwa uchambuzi huo, bajeti zitaingizwa katika mfumo wa mipango na bajeti wa Serikali (PlanRep), kabla ya OMH kuendelea na jukumu la kufuatilia utekelezaji wake kwa kila robo mwaka ili kuhakikisha malengo yaliyokubaliwa yanafikiwa.

Bw. Mwaisemba alitoa wito kwa taasisi na mashirika ya umma kushirikiana kikamilifu katika kuhakikisha rasilimali chache zilizopo zinatumika kwa ufanisi katika upangaji na usimamizi wa mipango.

“Ufanisi wa kila shirika katika kutekeleza majukumu yake utaakisi moja kwa moja mafanikio ya utekelezaji wa Dira 2050 pamoja na mipango ya maendeleo ya taifa,” alisisitiza.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akijibu maswali, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026.
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akisikiliza swali kutoka kwa Mbunge wa Viti Maalum Rose Tweve katika kipindi cha Masalı kwa Waziri Mkuu, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026. 
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba  akisikiliza swali kutoka kwa Mbunge wa Tunduru Kakazini, Ado Shaibu katika kipindi cha Maswalı kwa Waziri Mkuu, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akijibu maswali, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akijibu maswali, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026.
Mbunge wa Nachingwea, Fadhili Liwaka akimuuliza swali Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba katika Kipindi cha Masalı kwa Waziri Mkuu, Bungeni jijini Dodoma, Aprili 2, 2026. 
*********************
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amemuelekeza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) Profesa Riziki Shemdoe ahakikishe halmashauri zote ambazo bado hazijachukua viuadudu kwa ajili ya kutokomeza ugonjwa wa malaria ifikapo mwezi Mei zote ziwe zimeshakusanya dawa hizo ili ifikapo mwezi Juni waweze kutekeleza zoezi hilo.
 
Ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Aprili 2, 2026 wakati akijibu swali la Rose Tweve, Mbunge wa Viti Maalum katika kipindi cha Maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu. Mbunge huyo alitaka kujua tamko ya Serikali kuhusu baadhi ya halmashauri ambazo bado hazijatekeleza agizo la chukua viuadudu na kusababisha adha kwa Watanzania.
Kwa mujibu wa mbunge huyo Mwaka wa fedha 2025/2026 Serikali ilitoa kiasi cha shilingi bilioni 6.5 kwa ajili ya ununuzi wa lita 541,666 za viuadudu  ili ziweze kusambazwa katika halmashauri zote nchini, ambapo hadi sasa kuna baadhi hazijachukua dawa hizo huku wananchi wakiendelea kupoteza maisha kutokana na ugonjwa wa malaria.
 
“…Cha kusikitisha Mheshimiwa Waziri Mkuu kuna baadhi ya halmashauri hazijatekeleza agizo hilo na kusababisha adha kwa Watanzania kwani tatizo la maralia bado linaendelea kupoteza maisha ya Watanzania kwa sababisha vifo hususani kwa wanawake na watoto. Je nini tamko la Serikali kwa halmashauri hizi ambazo bado hazijatekeleza agizo hili?” alihoji.
 
“Ni kweli kumekuwepo agizo hilo la Serikali katika jitihada za kupambana na maralia kuhakikisha kwamba kunakuwepo na dawa hizo ambazo Serikali imezinunua kwa lengo la kupelekwa kwenye halmashauri zote nchini ili ziweze kuchukua hatua za kukabiliana na ugonjwa huo.”
 
Amesema suala hilo lilishajadiliwa ndani ya Serikali na kwamba ilihitajika yafanyike mafunzo katika ngazi za halmashauri kuhusu utekelezaji wa jambo hilo, kulikuwepo na angalizo la ratiba kwamba jambo hilo liweze kutekelezwa kuanzia mwezi Juni na kuendelea kwa kuwa ni kipindi ambacho maeneo mengi ya nchi yanakuwa hayana mvua.
 
Wakati huo huo, Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Sita imefanya jitihada kubwa za kuweza kuhakikisha kwamba mikoa ambayo haijaunganishwa kwa barabara za lami inaunganishwa ili kuweza kuhakikisha mawasiliano pamoja na biashara zinafanyika.
 
Waziri Mkuu amesema hadi sasa kuna mikoa michache ambayo bado kazi hiyo haijakamilika.  “Natambua kutoka Katavi kwenda Rukwa kulikuwa bado kuna eneo ambalo bado halijaunganishwa kwa lami lakini mkandarasi yuko site kwa ajili ya kuunganisha mkoa wa Rukwa na Katavi, Katavi kwenda Kigoma kulikuwa na sehemu bado haijaunganiishwa kwa lami fedha zipo zoezi hilo litakamilika.”
 
Ameyasema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Kisesa, Mussa Mbuga aliyetaka kujua ni upi mpango wa Serikali katika kuhakikisha barabara zote zinazounganisha mikoa nchini zinajengwa kwa kiwango cha lami ili kurahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa mbalimbali kwa ajili ya kuchochea ukuaji wa uchumi.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeandika historia nyingine ya mafanikio baada ya kuvuka malengo ya ukusanyaji mapato katika robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26, ikiashiria uimara wa mifumo ya kodi na juhudi za dhati za mageuzi ya kiutendaji.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamishna Mkuu wa Mamlaka hiyo Yusuf Mwenda, TRA imefanikiwa kukusanya jumla ya shilingi trilioni 9.31 katika kipindi cha Januari hadi Machi 2026, kiwango kinachozidi lengo la shilingi trilioni 8.75. 

“Hii ni sawa na ufanisi wa asilimia 106.4, ikiwa ni ishara tosha ya nidhamu ya ukusanyaji na kuimarika kwa mifumo ya usimamizi wa kodi nchini,”anasema Kamishna Mwenda kwenye taarifa hiyo.

Taarifa inasema kwa mwezi Machi pekee, TRA ilikusanya shilingi trilioni 3.58 dhidi ya lengo la trilioni 3.32, sawa na ufanisi wa asilimia 107.6. 

Takwimu hizi zinaonesha kasi ya kipekee ya ukusanyaji mapato, huku zikionesha pia mwitikio mzuri wa walipa kodi pamoja na juhudi za mamlaka katika kuziba mianya ya ukwepaji kodi.

Ukuaji wa mapato pia umeonekana kuwa wa kuridhisha, ambapo katika robo ya tatu ya mwaka huu wa fedha, TRA imepata ongezeko la asilimia 23.6 ikilinganishwa na makusanyo ya shilingi trilioni 7.53 katika kipindi kama hicho mwaka wa fedha 2024/25. 

Huu ni ushahidi wa wazi kuwa mageuzi yanayoendelea ndani ya mamlaka hiyo yanaanza kuzaa matunda yanayoonekana.

Uchambuzi wa mwenendo wa kila mwezi unaonesha kuwa Januari 2026 TRA ilikusanya trilioni 3.04 kwa ufanisi wa asilimia 106.7, Februari trilioni 2.69 kwa ufanisi wa asilimia 104.4, huku Machi ikiongoza kwa trilioni 3.58. Hali hii inaashiria uthabiti wa makusanyo kwa miezi yote mitatu ya robo ya tatu, bila kuyumba.

Wachambuzi wa masuala ya uchumi wanaeleza kuwa mafanikio haya yanachangiwa kwa kiasi kikubwa na matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa kodi, kuimarika kwa ushirikiano kati ya TRA na walipa kodi, pamoja na hatua kali dhidi ya wakwepa kodi. 

Aidha, elimu kwa walipa kodi imeendelea kusaidia kuongeza uelewa wa umuhimu wa kulipa kodi kwa hiari.

Mbali na mafanikio ya robo ya tatu, takwimu za kipindi cha miezi tisa kuanzia Julai 2025 hadi Machi 2026 zinaonesha kuwa TRA imekusanya jumla ya shilingi trilioni 28.005 dhidi ya lengo la trilioni 26.773, sawa na ukuaji wa asilimia 16.5. 

Hii inaashiria kuwa mamlaka ipo kwenye mstari sahihi wa kufikia na hata kuzidi malengo ya mwaka mzima wa fedha.

Katika hatua nyingine, ufanisi wa usimamizi wa sheria za kodi umeendelea kuimarika, ambapo uwiano wa gharama za ukusanyaji umebaki kuwa mdogo katika asilimia 2.41. 

Hii ina maana kuwa TRA inaendelea kutumia rasilimali chache kukusanya mapato makubwa zaidi, jambo linaloonesha ufanisi wa hali ya juu wa kiutendaji.

Aidha, mchango wa kodi katika pato la taifa umeongezeka hadi kufikia asilimia 14.1 kutoka asilimia 13.7, hatua inayodhihirisha jinsi mapato ya ndani yanavyozidi kuwa mhimili muhimu wa maendeleo ya uchumi wa nchi.
Wadau wa maendeleo wamepongeza mafanikio haya wakieleza kuwa yanaongeza imani kwa wawekezaji na washirika wa maendeleo, kwani yanaonesha uthabiti wa mifumo ya kifedha ya nchi.

Pia, mafanikio haya yanatarajiwa kusaidia serikali katika kugharamia miradi ya kimkakati bila kutegemea sana mikopo ya nje.

Hata hivyo, wataalam wanashauri kuwa pamoja na mafanikio haya, TRA inapaswa kuendelea kuboresha huduma kwa walipa kodi, kupunguza urasimu, na kuimarisha mifumo ya kidigitali ili kuongeza zaidi wigo wa walipa kodi na kuhakikisha uendelevu wa mafanikio haya.
Kwa ujumla, matokeo ya robo ya tatu yanaweka wazi kuwa TRA imepiga hatua kubwa katika ukusanyaji wa mapato, na kuifanya kuwa taasisi muhimu katika kuimarisha uchumi wa Tanzania. 

Kasi hii ikiendelezwa, basi matarajio ya kufikia malengo ya mwaka mzima wa fedha yanaonekana kuwa si ndoto bali ni jambo linalowezekana kwa asilimia kubwa.

Wachambuzi wa Masuala ya Kiuchumi wanashauri kuwa huu ni wakati muafaka kwa wadau wote kushirikiana zaidi na TRA ili kujenga taifa linalojitegemea kwa mapato yake ya ndani. 

Mafanikio haya si ya TRA pekee, bali ni ushindi wa kila Mtanzania anayetekeleza wajibu wake wa kulipa kodi kwa hiari na kwa wakati.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments
Ushirikiano baina ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Walipakodi umetajwa kuwezesha Mamlaka hiyo kuandika historia mpya kwa kukusanya kiasi cha shilingi trilioni 9.31 kwa kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26 sawa na ufanisi wa asilimia 106.4 ya lengo la kukusanya shilingi trilioni 8.75.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda April 1, 2026 imeeleza kuwa kwa mwezi Machi pekee TRA imekusanya shilingi trilioni 3.58 sawa na ufanisi wa asilimia 107.6 ya lengo la kukusanya shilingi trilioni 3.32.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa makusanyo hayo ya kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26, ni sawa na ukuaji wa asilimia 23.6 ikilinganishwa na kiasi cha shilingi trilioni 7.53 kilichokusanywa katika kipindi kama hicho mwaka wa fedha 2024/25. 

Kwa mujibu wa taarifa hiyo Ufanisi wa makusanyo kwa mwezi Machi unapelekea TRA kuweza kuandika rekodi mpya za kipekee katika ukusanyaji wa mapato nchini Wastani wa Makusanyo kwa mwezi katika kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26 umefikia shilingi trilioni 3.10 ambacho ni kiasi cha juu kabisa ukilinganisha na wastani wa shilingi trilioni 2.51  kwa kipindi kama hicho mwaka 2024/25.

TRA imeweza kurekodi Ukuaji chanya wa asilimia 23.6 katika kipindi cha Januari -Machi 2026, na imeweza kulifikia na kuvuka lengo la makusanyo kwa miezi 21 mfululizo kuanzia mwezi Julai 2024, mafanikio ambayo Mamlaka haijawahi yafikia toka ianzishwe hali ambayo imechagizwa na makusanyo ambayo yamechangiwa na ukaribu uliopo baina ya Mamlaka hiyo na Walipakodi.

Imeeleza kuwa Makusanyo yaliyokusanywa kwenye robo ya tatu ya Mwaka wa Fedha 2025/26 ni sawa na ukuaji wa asilimia 114.1 ukilinganisha na kiasi cha shilingi trilioni 4.35 kilichokusanywa katika kipindi kama hicho wakati Serikali ya Awamu ya Sita ilipoingia madarakani, mwaka 2020/21. 

Ushirikiano baina ya TRA na walipakodi umeiwezesha katika kipindi cha Julai, 2025 hadi Machi, 2026, kusajili walipakodi waруа 900,755 ambao ni ufanisi wa asilimia 131.36 wa kusajili walipakodi wapya 685,706 kufikia tarehe 31 Machi, 2026.

Pia imeelezwa kuwa katika kipindi cha robo ya tatu mahusiano na Viongozi wa vyama vya wafanyabiashara pamoja na wafanyabiashara wenyewe yaliimarishwa kwa kufanya mikutano na kuwasikiliza ili kutatua changamoto zao za kikodi ambapo TRA itaendelea kuboresha mahusiano na walipakodi kwenye Shughuli zote za Kiuchumi ili kuhamasisha ulipaji kodi wa hiari nchini.

Aidha TRA inapenda kuwahakikishia wananchi wote kuwa itaendelea kushirikiana na wananchi wote kwa ukaribu ili kuhakikisha kuwa lengo la makusanyo kwa mwaka huu wa fedha 2025/26 linafikiwa lote na hivyo kuiwezesha Serikali kuweza tekeleza mipango ya maendeleo kwa manufaa ya Taifa zima.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akifurahi jambo na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, wakati wakiagana mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican Aprili mosi, 2026.




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akisalimiana na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican,  April mosi, 2026.

Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kusimamia na kuratibu ushiriki wa Tanzania katika michezo ya kimataifa sambamba na kuharakisha maandalizi ya mashindano ya AFCON 2027 kwa lengo la kujenga urithi endelevu wa michezo, uchumi na heshima ya Taifa.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatano, Aprili 1, 2026) wakati akiwasilisha hotuba yake kuhusu Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma.

Amesema Tanzania inaendelea na maandalizi ya kuwa mwenyeji katika mashindano ya AFCON 2027, ambayo yanahusisha ujenzi na ukarabati wa viwanja pamoja na miundombinu wezeshi ikiwemo ujenzi wa Uwanja wa Arusha uliofikia asilimia 75.

“Ukarabati wa Uwanja wa Benjamin Mkapa umefikia asilimia 95; na ujenzi wa Uwanja wa Dodoma umefikia asilimia nne. Vilevile, Serikali imekamilisha ujenzi na ukarabati wa viwanja vya Meja Jenerali Isamuhyo, Gymkhana Club na Shule ya Sheria Tanzania kwa ajili ya mazoezi”.
 
Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea na ujenzi wa Viwanja vya Farasi, Gymkhana Annex na Leaders Club ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kuimarisha miundombinu ya michezo nchini.
 
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema mafanikio yanayoendelea kushuhudiwa katika sekta ya michezo yanatokana na uwekezaji wa kimkakati na uongozi thabiti wa Serikali.

“…Ninapenda kutumia fursa hii pia, kulipongeza Shirikisho la Mchezo wa Mpira wa Miguu Tanzania kwa uongozi, uratibu na usimamizi mzuri wa mchezo huo hapa nchini. Kupitia uongozi huo, kwa mara ya kwanza Tanzania imefanikiwa kuingiza vilabu vinne kwa pamoja katika hatua ya makundi ya mashindano ya Klabu Bingwa na Shirikisho Barani Afrika”.
 
Waziri Mkuu amevitaja vilabu hivyo kuwa ni Klabu ya Michezo Yanga (wananchi), Klabu ya Michezo Simba (wenye nchi), Klabu ya Michezo Azam (wana lambalamba) na Klabu ya Michezo Singida (wana kilemankundi).

Amesema kuwa mafanikio katika mchezo wa mpira wa miguu na michezo mingine kwa ujumla ni matokeo ya uwekezaji na hamasa inayotolewa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Mafanikio hayo, siyo tu yanaleta burudani kwa mashabiki, bali yanatoa fursa ya ajira na uwekezaji hapa nchini”.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha ushiriki wa wanafunzi katika michezo ili kuibua na kukuza vipaji vyao, ikiwa ni mkakati wa muda mrefu wa kujenga kizazi cha wanamichezo wenye ushindani kimataifa. 
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete leo April 1, 2026 akitia saini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Rais wa zamani wa Algeria, Jenerali Mstaafu Liamine Zeroual,  aliyefariki dunia mnamo Machi 28, 2026 akiwa na umri wa miaka 84 baada ya kuugua kwa muda mrefu. Pamoja naye ni Balozi wa Algeria nchini Mheshimiwa Ghalib Zermane.  Kitabu hicho kimefunguliwa nyumbani kwa Balozi Oysterbay jijini Dar es salaam.

Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete leo April 1, 2026 ametia saini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Rais wa zamani wa Algeria, Jenerali Mstaafu Liamine Zeroual,  aliyefariki dunia mnamo Machi 28, 2026 akiwa na umri wa miaka 84 baada ya kuugua kwa muda mrefu.
 
Jenerali Zeroual, aliyependwa na kuheshimikka sana, alichaguliwa kuwa rais mwaka 1995 katika kipindi kigumu cha vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Algeria. 

Alianzisha mageuzi ya kisiasa, ikiwa ni pamoja na kuratibu uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi.
 
Hata hivyo alijiuzulu mapema mwaka 1998 kabla ya kumaliza muhula wake wa miaka mitano ili kutoa nafasi kwa mpito wa kisiasa, na tangu hapo aliishi maisha ya faragha bila kujihusisha sana na siasa.
 
Hadi leo anakumbukwa kama kiongozi aliyetoa mchango muhimu katika kuiongoza Algeria katika kipindi cha mpito na changamoto kubwa za kisiasa na kiusalama.
 
Akiongea na Balozi wa Algeria nchini Mheshimiwa Ghalib Zermane, Dkt Kikwete alisema Algeria na Tanzania imekuwa rafiki wa karibu kwa muda mrefu, na kwamba viongozi wake wote waliopita wamefanya kazi kwa karibu na viongozi wa Tanzania kuanzia Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, hususan katika  ukombozi wa bara la Afrika, akiwataja viongozi hao kama Ahmed Ben Bella, Houari Boumédiène, Chadli Bendjedid,  Liamine Zéroual na Abdelaziz Bouteflika.
Posted by MROKI On Thursday, April 02, 2026 No comments

April 01, 2026


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameziagiza 
Wizara za Kisekta, Taasisi na Mamlaka za Serika za Mitaa zihakikishe zinalipa fidia kwa wananchi wanaopisha maeneo kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya Serikali kabla ya kutwaliwa kwa maeneo yao kwa kuzingatia taratibu zilizopo.
“Baadhi ya maeneo unakuta mwananchi mnyonge, mwananchi wa kawaida ametoa eneo limejenga kituo cha afya, limejenga shule na anachodai ni kidogo tu miaka yote ameendelea kudai hajalipwa. Mheshimiwa Rais alishaelekeza pamoja ya kuwa tunataka miradi ya maendeleo, tunataka uwekezaji tusipore maeneo ya wananchi kwa vigezo hivyo bila ya kuwalipa fidia.”
Pia, Waziri Mkuu amewataka wakandarasi wote wanaotekeleza miradi ya Serikali watimize wajibu wao kwa mujibu wa mikataba waliyoingia ikiwa ni pamoja na kuwalipa watoa huduma walioshiriki kwenye utekelezaji wa mradi husika.
Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo (Jumatano, Aprili 1, 2026) wakati akiwasilisha hotuba yake kuhusu Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma.
Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo kufuatia malalamiko mbalimbali ya wananchi wanaodai kuchukuliwa maeneo yao kwa ajili ya kupisha ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali bila ya kulipwa fidia.
Kuhusu wakandarasi amesisitiza ubora wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa uwiane na thamani ya fedha iliyotolewa, pia Waziri Mkuu amewataka maafisa masuuli wahakikishe wazabuni na watoa huduma wanalipwa kwa wakati kwa mujibu wa makubaliano na huduma iliyotolewa.
Pia, Waziri Mkuu ameziagiza mamlaka zinazohusika na masuala ya wakandarasi kuwawajibisha baadhi ya wakandarasi kutoka nje ya nchi ambao wanashindwa kuwalipa kwa wakati wakandarasi wa ndani.
…fedha zinazoelekezwa na Serikali kwenye miradi hiyo zitumike kama ilivyokusudiwa. Vilevile, wakandarasi wa ndani wawe wazalendo kwa kutumia ipasavyo fursa inayotolewa ya ushiriki wa kampuni zilizosajiliwa ndani kutekeleza miradi mikubwa.”
Vilevile, Waziri Mkuu amezielekeza taasisi zote za umma kuimarisha ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Serikali ikiwemo mipango, programu na miradi ili kuongeza tija ya utendaji kazi na kuboresha huduma kwa wananchi.
Aidha, Waziri Mkuu amezitaka Wizara, Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Taasisi, Wakala na Idara zinazojitegemea kuanza kutekeleza mapendekezo ya Tume ya Rais ya Kutathmini Maboresho ya Mfumo wa Kodi kama alivyoelekeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi trilioni 12.50 kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 8.73 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi trilioni 3.76 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Fedha hizo ni kwa ajili ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake kwa mwaka 2026/2027.
Vilevile, Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi 225,021,780,000 kwa ajili ya Mfuko wa Bunge. Kati ya fedha hizo, shilingi 207,992,798,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi 17,028,982,000 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.
Posted by MROKI On Wednesday, April 01, 2026 No comments



JUMLA ya sh. trilioni 1.77 zinahitajika kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, maabara, ajira mpya za walimu, ruzuku ya mitihani, ya vitabu na uendeshaji kwa wanafunzi zaidi ya milioni tatu wanaotarajiwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka 2028.
 
Hayo yamesemwa Bungeni, jijini Dodoma leo (Jumatano, Aprili Mosi, 2026) na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba wakati akiwasilisha Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027.
 
“Tathmini inaonesha kuwa wanafunzi 3,021,177 wanatarajiwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka 2028. Jumla ya gharama zinazohitajika ni shilingi trilioni 1.77 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 23,226; matundu ya vyoo 46,632; maabara 9,366; ajira mpya za walimu 40,192; ruzuku ya vitabu na uendeshaji pamoja na ruzuku ya mitihani na upimaji,” amesema.
 
Amesema mahitaji hayo yanatokana na uamuzi wa Serikali kuimarisha sekta ya elimu kwa kuzingatia Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 (Toleo la 2023), mitaala iliyoboreshwa, mipango na mikakati mbalimbali ikiwa na lengo la kuzalisha rasilimaliwatu wenye ujuzi na maarifa stahiki yatakayowezesha kumudu ushindani wa ajira na uwezo wa kujiajiri ndani na nje ya nchi.
 
Amewataka Wakuu wa Mikoa yote nchini wasimamie kikamilifu maandalizi na mapokezi ya wanafunzi wa elimumsingi ya lazima ya miaka 10 watakaojiunga na kidato cha kwanza mwaka 2028 kwa kukamilisha miundombinu na huduma zote muhimu.
 
“Tunaposema elimu ya lazima kuwa miaka 10, kimsingi tunasema tulikuwa na sekondari kila kata, sasa tunaongelea kuwa na shule ya sekondari kila kijiji. Lazima tujiandae kwa miundombinu pamoja na maoteo ya mahitaji yote ya kutekeleza mpango huo.”
 
Amesema ili kuhakikisha wanafunzi wote wanapata nafasi ya kuendelea na masomo, katika mwaka wa fedha ujao, Serikali imetenga sh. bilioni 139.28 kupitia mapato ya ndani ya halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 4,193 na matundu ya vyoo 13,943. Na kupitia Serikali Kuu, Waziri Mkuu amesema, zimetengwa sh. bilioni saba kwa ajili ya ujenzi wa maabara 233.
 
Alielezea kuhusu ujenzi wa shule mpya za sekondari za amali, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imetoa sh. bilioni 88.84 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya 103 za amali. “Kati ya hizo, ujenzi wa shule 27 umekamilika na zinatumika. “Hadi kufikia Februari, 2026 shule 158 za sekondari ya chini (O’ level) zinatekeleza mkondo wa amali wa mitaala iliyoboreshwa ikilinganishwa na shule 41 zilizoanza mwaka 2024,” amesema.
 
“Ili kuboresha ufundishaji wa masomo ya amali, Serikali imepeleka walimu 150 kwenye mafunzo ya muda mfupi nchini India. Aidha, walimu 156,948 kati 172,609 kutoka shule za msingi 17,111 pia walishiriki mafunzo endelevu kazini.”
 
Akielezea utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2025/2026, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kutekeleza miradi ya ujenzi wa shule mpya za msingi 277. “Serikali imeongeza miundombinu katika shule za msingi na sekondari zilizopo kwa kujenga madarasa 5,439, majengo ya utawala saba, mabweni 21, hosteli 26, nyumba za walimu 69, maabara 46, mabwalo matano na vituo vya walimu 70.
 
Akifafanua kuhusu ukarabati wa shule, Waziri Mkuu amesema Serikali imekamilisha ukarabati wa shule za msingi 228 na ujenzi wa miundombinu iliyojengwa kwa nguvu za wananchi ikiwemo maboma 132 ya mabweni ya shule za sekondari, vyumba vya madarasa 697 katika shule za msingi na vyumba vya maabara 175 katika shule za sekondari.
 
Waziri Mkuu ametua fursa hizo kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupeleka vifaa vya maabara katika shule za sekondari 231 zikiwemo shule mpya 26 maalumu za kitaifa za sayansi za wasichana.
 
Mbali na hilo, Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kutekeleza Mpango wa Elimu Bila Ada kwa kugharimia elimu ya awali hadi elimu ya sekondari ya juu ambapo hadi kufikia Februari, 2026 shi. bilioni 383.22 kati ya sh. bilioni 510.96 sawa na asilimia 75 zilikuwa zimetolewa kwa shule za msingi 18,119 na shule za sekondari 5,179.
 
Kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe sh. trilioni 12.5 kwa ajili ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake ambapo kati ya fedha hizo, sh. trilioni 8.73 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na sh. trilioni 3.76 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.
 
Vilevile, Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe sh. bilioni 225 kwa ajili ya Mfuko wa Bunge ambapo kati ya fedha hizo, sh. bilioni 207.99 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na sh. bilioni 17.02 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.
Posted by MROKI On Wednesday, April 01, 2026 No comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Wagombea wa nafasi ya Urais wa Vyama vya Siasa 16 vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Oktoba, 2025 mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 31 Machi, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Wagombea wa Nafasi ya Urais na Wagombea Wenza kutoka vyama vya Siasa 16 vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Oktoba, 2025. Mazungumzo hayo yalifanyika Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 31 Machi, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Wagombea wa Nafasi ya Urais na Wagombea Wenza kutoka vyama vya Siasa 16 vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Oktoba, 2025. Mazungumzo hayo yalifanyika Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 31 Machi, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Wagombea Wanawake katika nafasi ya Urais pamoja na Wagombea Wenza wa Vyama vya Siasa 16 vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Oktoba, 2025 mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 31 Machi, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Wagombea wa nafasi ya Urais pamoja na Wagombea Wenza wa Vyama vya Siasa 16 vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Oktoba, 2025 mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 31 Machi, 2026.

Posted by MROKI On Wednesday, April 01, 2026 No comments

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akiwasilisha Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali naMakadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027, Bungeni jijini Dodoma Aprili 1, 2026. PICHA NA OFISI YA WAZIRI MKUU
**************
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza kuanza utekelezaji wa Dira 2050 kupitia Mpango na Bajeti iliyoandaliwa na kuendelea kuishirikisha sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kuharakisha utekelezaji wake ili kujenga uchumi jumuishi, shindani na unaotegemea uzalishaji wenye tija.

Aidha, Waziri Mkuu ameilekeza Tume ya Mipango kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu Dira 2050 ili kuwezesha kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake kwa sababu suala hilo litawezekana ikiwa wadau wote watakuwa na ufahamu wa kutosha kuhusu vipaumbele vilivyoainishwa katika Dira 2050.

Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo (Jumatano, Aprili 1, 2026) wakati akiwasilisha hotuba yake kuhusu Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma.

Amesema Dira 2050 iliyozinduliwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mnamo tarehe 17 Julai, 2025, itaongoza mipango ya maendeleo katika miaka 25 ijayo inalenga kujenga Taifa jumuishi, lenye ustawi kwa wote, lenye haki na linalojitegemea.

 “Nitoe rai kwa viongozi wa Serikali, Dini, Sekta Binafsi, Asasi za Kiraia na Wadau wa Maendeleo kuhakikisha kwamba mipango yao inawiana na vipaumbele vya Dira 2050 na kuiunga mkono katika utekelezaji wake”.

Amesema utekelezaji wa Dira hiyo, utawezesha Taifa kuwa na uchumi wenye thamani ya dola za Marekani trilioni moja na wastani wa pato la mtu mmoja mmoja kuwa dola za Marekani 7,000 kwa mwaka ifikapo 2050. “Nguzo muhimu za kutuwezesha kufikia malengo hayo ni pamoja na utawala bora, amani, usalama na utulivu.”

Vilevile, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewaagiza viongozi wa kila sekta wahakikishe rasilimali zote za Taifa zinaelekezwa katika maeneo yenye tija na matokeo makubwa ili kupunguza utegemezi kutoka nje.

Amesema kuwa Dira 2050 imejengwa na nguzo kuu tatu ambazo ni uchumi imara jumuishi na shindani; uwezo wa watu na maendeleo ya jamii; na uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi.

Amesema katika hatua za kutekeleza Dira hiyo kwa vitendo, Serikali kwa kushirikiana na wadau imeweka mikakati mbalimbali ya utekelezaji, ambayo ni pamoja na kuchagiza ubia kati ya sekta ya umma na binafsi.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa mikakati mingine ni pamoja na matumizi yenye tija ya rasilimali za Taifa kupitia utekelezaji wa programu za kimkakati na kukuza utamaduni wa kuweka akiba kwa ajili ya uwekezaji.

Amesema Mpango na Bajeti itakayopitishwa na Bunge hilo ni hatua ya kwanza ya utekelezaji wa Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027 - 2030/2031 na Dira 2050,huku dhima ya mpango huo ni “Mageuzi katika Kukuza Uchumi na Kuzalisha Ajira.”

Amesema mipango hiyo inawezesha Taifa kuelekeza rasilimali katika vipaumbele vya kimkakati vyenye matokeo makubwa kwa ajili ya ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi.

Aidha, Waziri Mkuu amesema kwa kutambua umuhimu wa Dira hiyo, Serikali itaendelea kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji na tathmini pamoja na kuhimiza uwajibikaji, ili kuhakikisha tunafikia malengo tuliyojiwekea.

Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi trilioni 12.50 kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 8.73 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi trilioni 3.76 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Fedha hizo ni kwa ajili ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake kwa mwaka 2026/2027.

Vilevile, Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi 225,021,780,000 kwa ajili ya Mfuko wa Bunge. Kati ya fedha hizo, shilingi 207,992,798,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi 17,028,982,000 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.


Posted by MROKI On Wednesday, April 01, 2026 No comments

March 31, 2026





Na Mwandishi wetu, Dodoma
Wizara ya Madini imekutana na ujumbe wa wawekezaji kutoka Jamhuri ya Watu wa China unaotoka katika Kampuni ya Kimataifa ya Liaoning Fangda Group, kwa lengo la kujadili na kubaini maeneo ya kimkakati ya ushirikiano katika kuendeleza Sekta ya Madini nchini Tanzania.

Ujumbe huo uliongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Kampuni hiyo, Bw. Ao Xinhua, ambaye ameambatana na wataalamu mbalimbali kutoka Sekta za Viwanda, Madini na Teknolojia.

Kikao hicho kilifanyika Machi 30, 2026 katika Ukumbi wa Tume ya Madini jijini Dodoma, kikiongozwa na Kamishna wa Madini, Dkt. AbdulRahman Mwanga.

Katika majadiliano hayo, pande zote mbili zilijikita katika kuchambua fursa mbalimbali zilizopo katika mnyororo mzima wa thamani wa Sekta ya Madini, ikiwemo utafiti wa madini, uchimbaji, uongezaji thamani (beneficiation), pamoja na uwekezaji katika teknolojia za kisasa za uchakataji wa madini.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Dkt. Mwanga alieleza kuwa Tanzania ina mazingira rafiki ya uwekezaji, sera thabiti na mifumo ya kisheria inayolenga kuvutia wawekezaji wa ndani na nje, huku akisisitiza dhamira ya Serikali katika kuhakikisha rasilimali za madini zinatumika kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo ya viwanda.

Kwa upande wake, Bw. Ao Xinhua alieleza kuridhishwa na fursa zilizopo nchini na kuonesha nia ya dhati ya Kampuni yake kuwekeza na kushirikiana na Tanzania katika maeneo ya kimkakati, hususan katika miradi ya madini na viwanda vinavyoongeza thamani ya rasilimali hizo.

Kampuni ya Liaoning Fangda Group ni miongoni mwa Kampuni kubwa duniani yenye uwekezaji katika madini ya chuma, madini mengine, usafiri wa anga na uzalishaji dawa, jambo linaloifanya kuwa mshirika muhimu katika juhudi za Tanzania za kukuza uchumi wa viwanda.

Kikao hicho ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuendelea kufungua milango ya ushirikiano wa kimataifa na kuvutia uwekezaji wenye tija katika sekta ya madini, ambayo inaendelea kuwa mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Posted by MROKI On Tuesday, March 31, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo