Nafasi Ya Matangazo

April 21, 2026










Na Mwandishi Wetu, Dodoma 
Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa kushirikiana na Chemba ya Migodi Tanzania (TCM) imejadili na kuweka mikakati wa kuifanya Sekta ya Madini kuwa mhimili mkuu wa kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ya kuifanya Tanzania kufikia uchumi wa thamani ya dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050, kwa kusisitiza utafiti wa madini, usimamizi madhubuti na ushirikiano na sekta binafsi kama nguzo kuu za mafanikio hayo.

Akizungumza katika kikao na Chemba ya Migodi kilichofanyika katika ukumbi wa Tume ya Madini jijini Dodoma, leo Aprili 21, 2026, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amesema kuwa hatua hiyo haiwezekani bila kuwekeza kwa nguvu katika utafiti wa kina wa rasilimali madini kwa kushirikiana na sekta binafsi.

Ameeleza kuwa utafiti wa madini unapaswa kupewa kipaumbele kwani ndio unaofungua milango ya uwekezaji, kuongeza tija na kuhakikisha nchi inanufaika ipasavyo na rasilimali zake.

Katika kikao hicho, Waziri Mavunde amepokea changamoto, maoni na mapendekezo kutoka kwa wadau wa Sekta ya Madini kupitia TCM, akiahidi kuwa Serikali itayafanyia kazi kwa lengo la kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wanachama wa TCM kupitisha hoja zao kupitia umoja wao ili kuwa na sauti moja yenye nguvu na kurahisisha mawasiliano kati ya Serikali na sekta binafsi.

Kwa upande wa usimamizi, Waziri Mavunde ameelekeza kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya Ofisi ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini na taasisi za kiserikali ili kuhakikisha utekelezaji wa Sera na Sheria unakuwa na ufanisi zaidi bila kuingilia na kuleta usumbufu kwa wawekezaji.

Akizungumzia changamoto ya uvamizi wa maeneo yenye leseni halali za uchimbaji, Mavunde amesisitiza kuwa vitendo hivyo havitavumiliwa na tayari maelekezo yametolewa kwa Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa, kupitia Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini, kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kuwaondoa mara moja wavamizi wote na ametumia nafasi kueleza msimamo wa serikali wa kufuta  leseni ambazo hazifanyi kazi zinazomilikiwa na wawekezaji hao.

Amefafanua kuwa Serikali inakamilisha mfumo wa kidijitali unaohakikisha kuwa leseni za utafiti zinazoisha muda wake zinarejeshwa moja kwa moja Serikalini, hatua inayolenga kudhibiti tabia ya watu kushikilia maeneo makubwa kwa matarajio ya kuvutia wawekezaji baadaye.

Katika kuimarisha ajenda ya Ushirikiwa wa Watanzania kwenye sekta ya madini, Waziri Mavunde ameeleza kuwa, kuanzishwa kwa maeneo maalum ya uwekezaji wa viwanda vinavyozalisha vifaa na vipuri vya migodini, akitaja eneo la mgodi wa uliofungwa wa Buzwagi kama kitovu kinachoweza kuendelezwa kuwa ukanda maalum wa uchumi kwa shughuli hizo.

Pia, amekazia kuwa orodha ya bidhaa na huduma 20 zilizotengwa kwa Watanzania pekee katika migodi itaendelea kulindwa bila mabadiliko, akibainisha kuwa Serikali inalenga kulinda maslahi ya wazawa kwa kuzingatia sheria zilizopo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Steven Kiruswa amesema kuwa pamoja na juhudi za kuvutia wawekezaji, Serikali inaweka mkazo katika madini muhimu na ya kimkakati ambayo yanaendelea kuwa na soko kubwa katika zama za mabadiliko ya teknolojia na mazingira duniani.

Naye, Katibu Mkuu wa TCM, Eng. Benjamin Mchwampaka, ameipongeza Serikali kwa hatua zake za kushughulikia changamoto za sekta hiyo na kudumisha ushirikiano thabiti na sekta binafsi, ameshauri kuwa Serikali inapaswa kudumisha uthabiti wa Sera, Sheria na moiongozo ya Sekta ya Madini, kwani mabadiliko ya mara kwa mara kwani huchelewesha maamuzi ya uwekezaji na kwamba mazingira ya kisheria yanayotabirika yanaongeza ushindani wa nchi, huvutia uwekezaji wa muda mrefu, na kuhakikisha rasilimali za madini zinachangia kikamilifu ukuaji endelevu wa uchumi.

Kwa upande wa Serikali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Eng. Yahya Samamba amebainisha kuwa mpango maalum unaandaliwa kufadhili wataalamu wa Kitanzania kujifunza katika fani za kisasa kama uchumi wa madini (Mineral Economy), ili kuendana na mahitaji pamoja na  mabadiliko ya kimataifa na kuongeza ushindani wa nchi.

Kwa ujumla, kikao hicho kimeonesha dhamira ya dhati ya Serikali na wadau wa Sekta ya Madini kujenga msingi imara utakaowezesha sekta hiyo kuwa moja ya injini ya uchumi wa Tanzania kuelekea 2050.
Posted by MROKI On Tuesday, April 21, 2026 No comments



Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndg. Asha-Rose Migiro, leo tarehe 21 Aprili 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Mtandao wa Viongozi Wanawake wa Afrika (African Women Leaders Network - AWLN), ulioongozwa na Marais wastaafu wa Jamhuri ya Liberia, Mhe. Ellen Johnson Sirleaf, na Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia ya Ethiopia, Mhe. Sahle-Work Zewde, jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalijikita katika hali ya kisiasa nchini pamoja na matukio ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, yakihusisha pia umuhimu wa kudumisha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa.

Ujumbe huo upo nchini Tanzania kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kufanya mashauriano na viongozi mbalimbali wa kitaifa kuhusu maendeleo ya kisiasa na juhudi zinazoendelea za kuimarisha demokrasia na utawala bora, ikiwa ni sehemu ya mchango wa wanawake viongozi wa Afrika katika kulinda amani na utulivu barani.
Posted by MROKI On Tuesday, April 21, 2026 No comments






Na Mwandishi wetu, Dodoma
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony P. Mavunde, amekutana na wawakilishi wa Chama cha Mabroka Tanzania (CHAMATA) katika kikao maalum kilicholenga kujadili changamoto na fursa zilizopo katika sekta ya madini pamoja na kuimarisha uwazi katika biashara ya madini nchini.

Kikao hicho kimefanyika leo Aprili 21, 2026, katika Ofisi za Tume ya Madini jijini Dodoma, ambapo pande zote mbili zilijadiliana kwa kina masuala ya usimamizi wa leseni za udalali, uwazi wa biashara ya madini na namna mabroka wanavyoweza kuongeza mchango wao katika kukuza uchumi wa taifa.

Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Mavunde amesisitiza umuhimu wa kuimarisha uwazi, kuzingatia sheria na taratibu pamoja na matumizi ya mifumo rasmi ya biashara ili kuongeza ufanisi na tija katika sekta ya madini.

Amebainisha kuwa Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha mazingira ya biashara ya madini kwa lengo la kuvutia uwekezaji zaidi na kuongeza mapato ya Taifa.

“Serikali itaendelea kusikiliza maoni ya wadau na kufanya maboresho yatakayochochea ukuaji endelevu wa sekta ya madini nchini.

Hatuwezi kupuuza mapendekezo na ushauri wa wadau wenye lengo zuri la kuboresha mazingira ya biashara, hivyo Tume ya madini fanyieni kazi kwa haraka baadhi ya mapendekezo ya kimfumo ambayo hayagusi sheria na taratibu” amesema Mavunde.

Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde ameonesha utayari wa serikali kufanya utafiti wa kina eneo la Lemshuku ambapo kuna madini mengi ya vito ili kuongeza fursa zaidi ya uchimbaji wa madini ya vito mkoani Manyara badala ya kutegemea madini ya Tanzanite pekee, akisisitiza kuwa kuna fursa nyingi za madini mengine ambazo zinapaswa kuendelezwa ili kupanua wigo wa biashara na kuongeza thamani ya sekta hiyo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Mabroka Tanzania, Jeremia Kituyo, amependekeza kuanzishwa kwa gulio maalum la madini litakalofanya kazi kwa mfumo wa mnada, likiwahusisha wafanyabiashara wa madini, wanunuzi wa ndani na nje ya nchi pamoja na wadau wengine wa sekta hiyo.

Amesema mfumo huo utasaidia kuongeza uwazi wa bei, kupanua masoko ya madini na kuhakikisha mabroka wanapata fursa sawa katika biashara ya madini nchini.
Posted by MROKI On Tuesday, April 21, 2026 No comments

April 20, 2026





Posted by MROKI On Monday, April 20, 2026 No comments








Na Mwandishi wetu, Dodoma
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amewataka wadau wa madini ya metali (base metals) kujipanga kimkakati na kuifanya sekta hiyo kuwa kichocheo kipya cha ukuaji wa uchumi wa viwanda nchini, akisisitiza kuwa usimamizi madhubuti wa rasilimali, uwekezaji katika teknolojia za kisasa, uongezaji thamani, pamoja na kuzingatia misingi ya uwajibikaji na uwazi ni nguzo kuu za kuongeza tija, thamani na ushindani wa madini hayo katika soko la madini hayo. 

Amesema kuwa kupitia mbinu hizo, sekta ndogo ya madini ya metali ina uwezo mkubwa wa kufungua fursa za ajira, kuongeza mapato ya Taifa na kuimarisha mnyororo wa thamani wa viwanda, hivyo kuchangia kwa kiwango kikubwa katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi shindani na wa viwanda endelevu.

Amesema hayo leo Aprili 20, 2026 wakati akizungumza katika kikao na wadau wa Tanzania Base Metal Association (TBMA) kilichofanyika katika Ukumbi wa Tume ya Madini Jijini Dodoma, ambako amesema Serikali ina dhamira ya dhati ya kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji ili sekta hiyo iweze kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya Taifa.

“Mwelekeo wetu ni kuhakikisha sekta ndogo ya madini ya metali inakuwa na mchango mkubwa zaidi katika uchumi. Tutahakikisha changamoto zinazowakabili wadau zinapatiwa ufumbuzi wa haraka na wa kudumu,” amesisitiza Mhe. Mavunde.

Mhe. Mavunde ametumia kikao hicho kusikiliza na kupokea changamoto mbalimbali zinazowakabili wachimbaji wa madini ya metali, ikiwemo masuala ya miundombinu na masoko, huku akiagiza uanzishwaji wa Kituo cha Madini eneo la Mlongo-Kyerwa mahususi kwa ajili ya wachimbaji wa madini bati (tin) huku akiahidi kuzifanyia kazi kwa haraka ili kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji katika sekta hiyo.

Katika kuimarisha ubora wa huduma za kitaalamu za upimaji wa sampuli za madini, Waziri Mavunde amesema kuwa, Serikali inaendelea na ujenzi wa maabara ya kisasa ya uchunguzi wa sampuli za madini katika eneo la Kizota, jijini Dodoma, mradi unaotarajiwa kuongeza ufanisi wa uchambuzi wa madini na kupunguza gharama kwa wachimbaji na wawekezaji.

Katika hatua ya kuongeza upatikanaji wa mitaji, Waziri Mavunde ameelekeza kuanzishwa kwa mfuko wa dhamana (Export credit guarantee scheme) utakaowezesha wachimbaji wadogo kupata mikopo yenye masharti nafuu, hatua inayotarajiwa kuongeza uzalishaji na ushindani katika soko la kimataifa.

Aidha, ameagiza Tume ya Madini kuanzisha jukwaa la kudumu kwa kushirikiana na wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini, litakalokuwa likikutana mara kwa mara kujadili changamoto na kupendekeza maboresho ya kisera na kiutendaji kwa lengo la kukuza sekta hiyo kwa ufanisi zaidi.

Pia, Mhe. Mavunde amesisitiza Serikali inaendelea kuboresha miundombinu katika maeneo yote yenye shughuli za madini, ikiwemo barabara na huduma za nishati, ili kuwezesha usafirishaji wa madini na kupunguza gharama za uzalishaji.

Mhe. Mavunde amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kukutana na wadau mara kwa mara ili kuimarisha ushirikiano, akibainisha kuwa mafanikio ya Sekta ya Madini yategemea mshikamano na uwazi kati ya Serikali na sekta binafsi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa TBMA Godfrey Kente, ameipongeza Serikali kwa kuendelea kushirikiana nao katika kutatua changamoto za sekta hiyo, akiahidi kuongeza uwekezaji na uzalishaji ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza mapato ya Taifa.
Posted by MROKI On Monday, April 20, 2026 No comments

April 18, 2026

Uamuzi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC),kuongeza safari za treni za SGR kutoka safari mbili  hadi nne kati ya Dar es Salaam na Morogoro si jambo la kawaida tu la ratiba bali ni ishara kubwa ya mabadiliko ya kiuchumi, kimkakati na kiutendaji.
 
Mosi,  Ongezeko la mahitaji ya abiria (Demand-driven decision), kuongeza safari maana yake ni kwamba, Idadi ya abiria imeongezeka sana na huduma ya SGR imekubalika na wananchi. Kwa mfano, tayari SGR imeonyesha mafanikio makubwa kwa kubeba mamilioni ya abiria na kurahisisha usafiri

Tafsiri yake ni kwamba, TRC haiongezi safari bila sababu bali ni muitikio wake kwa soko.

Pili, Kuboresha upatikanaji wa huduma (Service accessibility), awali safari mbili zilikuwa hazimpi nafasi abiria kuwa na machaguo ya safari   hivyo ilikuwa kwamba

abiria akikosa  treni ya asubuhi ama jioni basi atasubiri muda mrefu.
Kuongeza treni hizo kufikia nne, kunampa machaguo mengi zaidi kwa abiria,  ikiwemo urahisi wa kupanga safari kulingana na muda wa kazi/shughuli husika.

Aidha, hii inaifanya reli, kuwa rafiki kwa wafanyakazi na kuwa  mbadala halisi wa mabasi na magari binafsi

Tatu, kuongezeka kwa ufanisi wa matumizi ya miundombinu, kama inavyofahamika, SGR ni uwekezaji mkubwa wa serikali (mabilioni ya fedha), hivyo kuuongeza safari za treni kati ya Jiji la Dar Es Salaam na Mkoa wa Morgoro, kunamaanisha kwamba, treni zinatumika muda mwingi zaidi na kwamba miundombinu haikai muda mwingi bila kutumika (idle)

Nne, athari chanya kiuchumi, kuwa na Safari nyingi zaidi  ni sawasawa na harakati nyingi zaidi za watu na hii  inasabaisha biashara kuongezeka kati ya Dar es salaam na Morogoro. Aidha ni fursa za ajira (moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja), Ukuaji wa miji, wakati tunaangalia matokeo ya kuongeza treni kati ya maeneo hayo mawili, SGR tayari inachochea biashara, ajira na utalii

Tano,. Kupunguza msongamano wa barabara na gharama za usafiri, kuwa na Safari nyingi za treni kuna maana kubwa sana kufanya barabaara kupumua kwa maana kwamba zinapunguza mabasi barabarani, zinapunguza ajali na uchakavu wa barabara lakini pia zinatoa usafiri wa haraka na wa gharama nafuu. Treni hubeba maelfu ya watu kwa safari moja tofauti na mabasi.

Sita, hatua kuelekea huduma ya “high-frequency rail system”, kuongeza safari ni hatua ya kuelekea mfumo wa kisasa wa reli (kama metro/intercity advanced systems).

Ratiba zinazokaribiana ni ishara kuwa: TRC inaelekea kwenye mfumo wa reli wa kisasa unaofanana na nchi zilizoendelea.
 
Kuongezeka kwa safari kutoka mbili  hadi nne,  kunamaanisha kuwa Mahitaji ya huduma yameongezeka, wananchi wana imani na SGR, uchumi unaanza kunufaika, na huduma inakuwa ya kisasa zaidi na rafiki kwa mtumiaji.


Posted by MROKI On Saturday, April 18, 2026 No comments
Na Mwandishi Wetu.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula , amesema uandishi wa habari usiozingatia maadili unaweza kuhatarisha umoja wa kitaifa, amani na utulivu wa jamii.

Akizungumza na waandishi wa habari  ambao ni wanachama wa JUMIKITA, TADIO na TBN, leo Ijumaa Aprili 17, 2026 jijini Dar es Salaam, Kipangula alisema waandishi wa habari wanapaswa kutambua uzito wa nafasi yao katika jamii, hasa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya kijamii, kisiasa na kiuchumi, ambapo taarifa wanazozitoa zina athari kubwa kwa mwenendo wa jamii.

Alifafanua kuwa amani ni hali ya kutokuwepo kwa migogoro au vurugu, huku utulivu ukimaanisha usalama na uhakika wa maisha ya wananchi bila hofu, akibainisha kuwa hali hizi mbili haziwezi kudumu bila uwepo wa umoja wa kitaifa unaojengwa juu ya mshikamano wa wananchi bila kujali tofauti zao.
“Pale ambapo uandishi hauzingatii maadili, unaweza kuchochea migawanyiko, kupotosha ukweli na hatimaye kuvuruga mshikamano wa kitaifa. Hivyo, ni muhimu kwa waandishi wa habari kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji,” alisema Kipangula.

Alibainisha kuwa waandishi wa habari wana wajibu wa msingi wa kukusanya, kuchakata na kusambaza taarifa sahihi, pamoja na kusaidia kuunda mitazamo ya wananchi kwa njia inayochangia maridhiano na maendeleo ya jamii.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia Kanuni za Maadili ya Taaluma ya Uandishi wa Habari, akibainisha kuwa maadili hayo yanahimiza ukweli, usawa, uwazi na heshima kwa haki za binadamu, mambo ambayo ni msingi wa kulinda amani, kuimarisha utulivu na kukuza umoja wa kitaifa.
Posted by MROKI On Saturday, April 18, 2026 No comments

April 17, 2026

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa akijibu maswali bungeni jijini Dodoma leo Aprili 17, 2026.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa akisalimiana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) Mhe. Ridhiwani Kikwete bungeni jijini Dodoma leo Aprili 17, 2026. Kulia ni Naibu Waziri wa Maji Mhe. Mhandisi Kundo Mathew.
******************
Serikali imesema itaendelea kuimarisha juhudi za kuhakikisha wananchi wanapata uelewa wa kutosha na kushiriki kikamilifu katika biashara ya kaboni ili kunufaika kiuchumi huku wakichangia uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
 
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa amesema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu Mhe. Josephine Kapoma aliyetaka kujua Serikali ina mkakati gani wa kufikisha elimu kwa wananchi kuhusu biashara ya kaboni.
 
Akijibu swali hilo bungeni jijini Dodoma leo Aprili 17, 2026, Mhe. Kwagilwa alisema Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais na Kituo cha Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC) zimeweka mikakati mbalimbali ya kufikisha elimu kwa wananchi.
 
Alitaja mikakati hiyo kuwa ni kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu dhana, faida na fursa zilizopo katika biashara hiyo kupitia vyombo vya habari na kutoa mafunzo kwa viongozi wa ngazi za mikoa, halmashauri na vijiji ili waweze kuwa mabalozi wa elimu kwa jamii zao kuhusu utekelezaji wa miradi ya kaboni na manufaa yake.
 
“Tangu kupitishwa kwa Kanuni na Mwongozo wa Biashara ya Kaboni tumetoa elimu kwa viongozi mbalimbali pamoja na kushirikiana na wadau wa maendeleo, asasi za kiraia na sekta binafsi katika kutoa elimu na kujenga uwezo kwa jamii kuhusu namna ya kuanzisha na kunufaika na miradi ya kaboni,” alisema Mhe. Kwagilwa.
 
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Kwagilwa alisema kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinashirikiana katika kutekeleza miradi ya mazingira na kunufaisha wananchi wa pande zote mbili za Muungano.
 
Alisema hayo wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Jimbo la Amani Mhe. Abdul Yussuf Maalim aliyetaka kufahamu Zanzibar inanufaika vipi na biashara ya kaboni.
 
Akiendelea kujibu swali hilo, Mhe. Kwagilwa alisema pamoja na kushirikiana katika biashara ya kaboni pia Serikali zote mbili zinashirikiana katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
 
Ikumbukwe kuwa biashara ya kaboni ni mfumo wa kifedha unaoruhusu nchi, taasisi au miradi kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kupata faida kwa kuuza au kubadilishana hati za kaboni ambazo hutolewa unapofanikiwa kupunguza au kufyonza hewa ya kaboni.
Posted by MROKI On Friday, April 17, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Arusha
WANANCHI wa Kijiji cha Losimingor, wilayani Monduli mkoani Arusha, wanatarajiwa kunufaika kiuchumi na kijamii kupitia utekelezaji wa Mradi wa Kujenga Ustahimilivu wa Bioanuai za Misitu ya Mazingira Asilia dhidi ya Athari za Mabadiliko ya Tabianchi (BUREFOBI), unaolenga kuunganisha uhifadhi wa mazingira na maendeleo ya wananchi.

Mradi huo unatekelezwa katika vijiji vinavyopakana na Msitu wa Hifadhi ya Mazingira Asilia Essimingor, ukiwa na lengo la kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi huku ukiboresha maisha ya jamii kupitia miradi ya maendeleo endelevu.

Losimingor ni miongoni mwa vijiji sita vinavyonufaika na mradi huo, ambapo utekelezaji wake unatarajiwa kuleta mageuzi ya kiuchumi kupitia shughuli mbalimbali ikiwamo uimarishaji wa majosho ya mifugo, sekta inayobeba maisha ya wananchi wengi wa eneo hilo.

Mbali na ufugaji, mradi huo pia unafungua fursa mpya za kipato kupitia utalii shirikishi, ambapo jamii itanufaika moja kwa moja kwa kushiriki katika shughuli za utalii, ikiwemo kuanzishwa kwa kituo cha jamii cha kuuza bidhaa za utalii. Hatua hiyo inalenga kupanua wigo wa ajira na kupunguza utegemezi wa moja kwa moja wa rasilimali za misitu.

Akizungumza Aprili 16,2026 wakati wa ziara ya timu ya mradi wilayani Monduli, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Mwalimu Happiness Laizer, alisema halmashauri imejipanga kikamilifu kuhakikisha utekelezaji wa mradi unakuwa na tija kwa wananchi.

“Halmashauri ya Monduli inajivunia kuwa miongoni mwa wanufaika wa mradi huu. Tunaahidi tutatimiza wajibu wetu kikamilifu kadri tutakavyoelekezwa na wasimamizi wa mradi,” alisema.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Someni Mteleka, alisema ziara hiyo inalenga kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa miradi na kuhakikisha manufaa yaliyokusudiwa yanawafikia wananchi.

Alisisitiza kuwa TFS itaendelea kushirikiana na halmashauri za wilaya ili kuhakikisha miradi hiyo inaleta matokeo chanya kwa jamii, huku ikiimarisha uhifadhi endelevu wa misitu.

Naye mwakilishi wa Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Getrude Lyatuu, alisema ushirikiano kati ya taasisi hiyo na TFS utaendelea kuimarishwa ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa ufanisi na ushirikishwaji mpana wa jamii.

Alibainisha kuwa lengo kuu ni kuhakikisha makundi yote ya wananchi, wakiwemo wanawake na vijana, yanapata fursa sawa za kunufaika na miradi hiyo.

Ziara ya timu ya mradi inaendelea katika Mkoa wa Manyara, ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo pamoja na tathmini ya athari zake kwa wananchi na mazingira

Posted by MROKI On Friday, April 17, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo