Nafasi Ya Matangazo

February 23, 2026

 
Uwepo wa Tume ya Ushindani Tanzania (FCC) umetajwa kuwa chachu ya kupungua kwa uingizaji na usambazaji wa bidhaa bandia katika maeneo mbalimbali ya nchi, hususan bandarini na mipakani. Hatua hiyo imeelezwa kuimarisha ulinzi wa watumiaji na kuweka mazingira rafiki ya ushindani wa haki sokoni.

Serikali imeipongeza FCC kwa juhudi zake za kuimarisha usimamizi na ukaguzi wa bidhaa, ikisisitiza kuwa kazi hiyo ina mchango mkubwa katika kulinda afya za wananchi na kukuza uchumi wenye misingi ya ushindani sawa.

Pongezi hizo zimetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, alipokuwa akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, katika ufunguzi wa kikao kazi kati ya FCC na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) kilichofanyika jijini Dar es Salaam.

Mpogolo amesema mafanikio hayo yanaonyesha wazi umuhimu wa ushirikiano kati ya taasisi za serikali na wadau mbalimbali, hususan wanahabari, katika vita dhidi ya bidhaa bandia. Ameeleza kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa katika kuibua na kufichua vitendo vinavyohatarisha afya na uchumi wa wananchi.

Hata hivyo, ameihimiza FCC kuongeza kasi ya operesheni zake, hasa katika maeneo yenye shughuli kubwa za kibiashara kama Soko Kuu la Kariakoo na maeneo mengine ya jiji, ambako bado kuna changamoto ya uwepo wa bidhaa zisizo halali sokoni.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa FCC, Amina Ngasongwa, amepongeza mchango wa vyombo vya habari katika kuelimisha umma kuhusu madhara ya bidhaa bandia na kusisitiza umuhimu wa watumiaji kuwa makini kabla ya kufanya maamuzi ya ununuzi.

Kikao kazi hicho kililenga kuimarisha ushirikiano kati ya FCC na wahariri wa vyombo vya habari, kwa lengo la kuongeza uelewa wa umma na kuendeleza mapambano dhidi ya bidhaa bandia nchini. 
Source: Madelemonews Blog. 

Posted by MROKI On Monday, February 23, 2026 No comments


Posted by MROKI On Monday, February 23, 2026 No comments



WAZIRI MKUU Dkt Mwigulu Nchemba amezindua shule mpya ya sekondari ya Sinya ambayo ni ya bweni iliyojengwa katika kijiji cha Leremeta, wilayani Longido, Arusha kwa gharama ya sh. bilioni 1.23.
 
Akizungumza na wakazi wa kata ya Sinya na viongozi mbalimbali waliofika kushuhudia uzinduzi huo leo (Jumatatu, Februari 23, 2026), Waziri Mkuu ameelekeza suala la ujenzi wa uzio wa shule lifanyiwe kazi haraka kutokana uwepo wa wanyama wakali.
 
“Nimeridhishwa na ujenzi wa hii shule; taarifa nilizonazo zinaonesha ujenzi wake umezingatia thamani halisi ya fedha kwa ubora. Ombi la kuwekwa uzio hapa shuleni ni jambo la maana kwa sababu kuna wanyama wakali. Mkurugenzi angalia ndani ya mapato ya Halmashauri mnaweza kupata kiasi gani ili kazi hiyo ifanywe kwa haraka. Mkuu wa Mkoa simamia jambo hili ili liwe moja ya kipaumbele.”
 
“Nyumba za walimu kama alivyoomba Mkuu wa shule, Naibu Waziri wa TAMISEMI kaa nao muangalie uwezekano. Na mabweni yaliyoombwa ni muhimu yajengwe,” amesisitiza Waziri Mkuu.
 
Mapema, akitoa taarifa ya ujenzi, Mkuu wa shule hiyo, Mwalimu Andrew Emmanuel alisema shule hiyo ina wanafunzi 387 wa kidato cha kwanza hadi cha tatu na walimu 12 ambao kati yao tisa ni wa kiume na watatu ni wa kike.
 
Alisema bweni la wanafunzi wa kike limekamilika na linatumika na akaomba mabweni zaidi na nyumba za walimu kwani iliyopo ni moja inayoweza kutumika kwa familia mbili. Alisema nguvu ya wananchi ya sh. milioni 34 ilitumika kununua meza 140 na vitanda 80.
 
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu amekagua ujenzi wa mradi wa majisafi wa Sinya–Namanga ambao pia unatekelezwa katika kijiji cha Sinya, wilayani Longido, mkoani Arusha kwa gharama ya sh. bilioni 13.5.
 
Akitoa maelezo mafupi, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso alisema kupatikana kwa maji kwenye eneo hilo kulitoka na uwepo wa mitambo ya kupimia maji chini ya ardhi iliyonunuliwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo iligawanywa kwenye kanda tofauti.
 
“Wananchi wa huku walikuwa wanategemea chanzo cha mto Simba ambacho hakitoshelezi lakini utafiti uliofanywa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Arusha (AUWSA) ulibaini eneo la Ildonyo (Sinya) linafaa kuwa na kisima chenye uwezo wa kuzalisha lita milioni 2.4 kwa siku.”
 
Alisema uzalishaji wa sasa ni wastani wa lita milioni 1.7 kwa siku wakati mahitaji ni lita milioni 3.8 na kwamba mradi ukikamilika utaweza kuongeza uzalishaji hadi lita milioni 4.1 kwa siku, hivyo kuboresha huduma ya maji safi kwa wananchi na mifugo.
Posted by MROKI On Monday, February 23, 2026 No comments

 

Katika Picha hii ya Maktaba inamuonesha Rais Jakaya Kikwete akiongea na Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam. Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, aliyekwenda kumjulia hali na kumpa pole Ikulu jijini Dar es Salaam Disemba 23, 2014.

Posted by MROKI On Monday, February 23, 2026 No comments
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele leo Februari 23, 2026 ametembelea mafunzo ya Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma na kuzungumza nao ambapo amewasisitiza kutekeleza majukumu yao kwa weledi kwa kufuata Sheria, Kanuni na maelekezo ya Tume.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele leo Februari 23, 2026 ametembelea mafunzo ya Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma na kuzungumza nao ambapo amewasisitiza kutekeleza majukumu yao kwa weledi kwa kufuata Sheria, Kanuni na maelekezo ya Tume.

Mafunzo hayo ya siku mbili yalifanyika katika Kumbi tatu tofauti za Seminari Kuu Peramiho, Maposeni Sekondari na Ukumbi wa Josephat Mkuwa ni maandalizi ya Uchaguzi Mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Peramiho ambao unatarajiwa kufanyika Februari 26, 2026 na utashirikisha vyama vya siasa 15.

Wajumbe wengine wa Tume walitembelea vituo hivyo vya mafunzo na kuzungumza na washiriki hao. 


Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi walipotembelewa katika kituo cha mafunzo kilichopo Ukumbi wa Seminari Kuu Peramiho.  
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uchaguzi kutoka INEC ambaye pia ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kisheria Ndg. Cyprian Mbugano akizungumza jambo. 
Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi walipotembelewa katika kituo cha mafunzo kilichopo Ukumbi wa Seminari Kuu Peramiho. 
Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Peramiho, wilayani Songea mkoani Ruvuma Ndg. Exavery Luyagaza akizungumza jambo wakati wa mafunzo hayo kituo cha Seminari Kuu Peramiho.

Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi walipotembelewa katika kituo cha mafunzo kilichopo Ukumbi wa Seminari Kuu Peramiho. 
Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) Mhe. Balozi Omar Ramadhan Mapuri, leo Februari 23, 2026 ametembelea na kukagua Mafunzo kwa Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi wa Vituo vya Kupiga Kura katika jimbo la Peramiho, Songea mkoani Ruvuma. 

Mjumbe huyo wa Tume amewapongeza washiriki wa mafunzo na kuwataka kuzingatia weledi na kuwakumbusha kuepuka vitendo vinavyoweza kusababisha matatizo kama yaliyojitokeza katika uchaguzi mkuu uliopita uliofanyika Oktoba 29, 2025.

Balozi Mapuri amewasisitiza washiriki wa mafunzo hayo kuwa mafanikio ya uchaguzi yatatokana na wao kuzingatia mafunzo waliyoyapata ili kufanikisha uchaguzi huu mdogo unaotarajiwa kufanyika Februari 26, 2026 kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo la Peramiho Jenista Mhagama.

Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma waliokua katika kituo cha mafunzo cha Maposeni Sekondari wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi. 
Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Magdalena Rwebangira leo tarehe 23 Februari, 2026 ametembelea na kukagua mafunzo kwa makarani wasimamizi na wasimamizi wasaudizi wa vituo vya kupugia kura yaliyofanyika katika ukumbi wa Josephat Mkuwa uliyopo halmashauri ya wilaya Songea Mkoani Ruvuma ikiwa ni maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Peramiho utakaofanyika siku ya Alhamisi tarehe 26 Februari, 2026.

Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma waliokua katika kituo cha mafunzo cha Josephat Mokuwa wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi. 
Posted by MROKI On Monday, February 23, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam 
Katika hatua ya kihistoria na mageuzi ya Sekta ya Madini nchini, Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini leo Februari 23, 2026 imesaini Makubaliano Maalum na Benki ya CRDB yatakayorahisisha upatikanaji wa huduma za fedha kwa wachimbaji wadogo wa madini. 

Akizungumza katika hafla hiyo ya kihistoria iliyofanyika katika Hoteli ya Johari Rotana, jijini Dar es Salaam, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde (Mb) ambaye pia alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa utashi na uongozi thabiti unaoendelea kuibadilisha Sekta ya Madini kuendelea kuwavutia wawekezaji .

Waziri Mavunde amesisitiza kuwa hatua hiyo ni mwendelezo wa juhudi za makusudi za Serikali kujenga mazingira rafiki kwa wachimbaji wadogo wa madini kwa kuimarisha uchimbaji, biashara, kuongeza ufanisi, na kuimarisha mchango wa sekta katika Pato la Taifa (GDP).
“Tunawapongeza CRDB kwa kwenda “field”, kujionea uhalisia wa shughuli za uchimbaji, na kufanya maamuzi kupata taarifa sahihi na sio zilizopikwa. Nawapongeza kwa kuwa mmeanza kuielewa Sekta ya Madini, na hili litaongeza tija ya uwekezaji wenu, maendeleo ya sekta, na mapato ya taifa,” amesisitiza Mavunde. 

Mhe. Mavunde ameeleza kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi chache barani Afrika zinazowatambua wachimbaji wadogo kisheria, na kwamba Serikali inaendelea; kutoa leseni za uchimbaji kwa wachimbaji wadogo, kufuta leseni za utafiti zisizoendelezwa na kugawa maeneo kwa wachimbaji wadogo, na kujenga mazingira ya uwezeshaji ili wachimbaji wadogo waongeze uzalishaji, tija, na mchango wao kwa uchumi.

Hatua ya Kihistoria: Mkopo wa Shilingi Bilioni 50
Waziri Mavunde ameeleza kuwa katika hatua ya kihistoria Kikundi cha Wachimbaji Wadogo cha Songwe Gold Family kitakuwa cha kwanza kupata mkopo wa shilingi bilioni 50 kwa wakati mmoja, jambo ambalo halijawahi kutokea nchini, akiitaja hatua hiyo kuwa ya uthubutu wa kipekee kutoka Benki ya CRDB. 

Pia, amebainisha kuwa, Serikali  iko katika hatua za mwisho za kuanzisha Mfuko wa Dhamana kwa ajili ya kukopesha wachimbaji wadogo, ili kupunguza vikwazo vya upatikanaji wa mitaji na kuongeza kasi ya urasimishaji wa shughuli za uchimbaji.
Benki CRDB Yasema ni Mfumo Bunifu, Dhamana Rafiki
Akizungumza katika hafla hiyo , Mkurugenzi Mtendaji, Dkt. Abdulmajid Nsekela, amesema mpango huu ni historia kwa benki na kwa Sekta ya Madini, kwani unaweka mfumo wa kisasa na shirikishi unaoendana na uhalisia wa wachimbaji wadogo kwa kuwa wanabeba sehemu kubwa ya sekta inayokua kwa kasi kwa miaka mitano mfululizo kuliko sekta nyingine.

“Changamoto tulizoona kwa wachimbaji ni ukosefu wa mitaji, teknolojia, na ushauri wa kitaalamu. Uwezeshaji wa sekta ndiyo msingi wa mapato ya taifa. Huu ni mpango wa mkakati wa kitaifa unaojumuisha elimu ya kifedha, urasimishaji wa shughuli, na kuimarisha mchango wa sekta kwenye GDP,” amesema Nsekela. 

Kwa mujibu wa Dkt. Nsekela, tayari benki imeshatoa shilingi bilioni 186 kwa Sekta ya Madini, kati ya hizo bilioni 136 kwa wachimbaji wakubwa na bilioni 50 kwa wachimbaji wadogo.

“Tofauti kubwa ya mpango huu ni aina ya dhamana, si lazima kutumia mali zisizohamishika, dhamana zitajumuisha leseni halali za uchimbaji, leseni ya biashara ya dhahabu, hifadhi ya dhahabu ya mkopaji, pamoja na mikataba maalum” amesisitiza Nsekela.

Kwa upande wake,  Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo, amempongeza Waziri Mavunde kwa kuhakikisha mageuzi haya yanafikiwa katika kipindi cha uongozi wake kwa kushawishi Taasisi za Fedha kuwekeza katika Sekta ya Madini na leo ni ishara ya mafanikio ya jitihada hizo.
Naye, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi CRDB, Dkt. Donald Mmari, ameeleza kuwa Sekta ya Madini inachochea na kufungamanisha sekta nyingine, na kwamba ni miongoni mwa sekta za vipaumbele katika Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050. Ameongeza kuwa mpango huu utaleta mageuzi ya kimkakati na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi.

Akizungumza kwa niaba ya wachimbaji wadogo, Rais wa FEMATA, John Bina, amesema wachimbaji watakwenda kumshukuru Rais Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kulifanikisha jambo hilo la kihistoria, akisisitiza kuwa mpango huo ulikuwa kilio cha muda mrefu cha wachimbaji wadogo na sasa unafungua ukurasa mpya wa maendeleo kwa sekta hiyo.
Posted by MROKI On Monday, February 23, 2026 No comments

 Mwenyekiti Mtendaji wa Taifa Gas, Hamis Ramadhan na Meneja Mkuu,Devis Deogratius wakikata utepe kuwakaribisha mawakala wakubwa (Super Dealers) wa kampuni kwenye kiwanda cha kutengeneza mitungi Kibaha.

Mwenyekiti Mtendaji wa Taifa Gas, Hamis Ramadhan akiongea na mawakala wakuu wa kampuni wakati wa hafla hiyo iliyofanyika katika kiwanda cha kutengeneza mitungi kilichopo Kibaha mkoani Pwani.
Katika hafla hiyo mawakala walitunukiwa vyeti kwa kutambua mchango wao
Baadhi ya mawakala katika hafla hiyo
Baadhi ya mawakala katika picha ya pamoja na viongozi wa kampuni ya Taifa Gas
**********************
Viongozi, wafanyakazi na mawakala wakuu wa kampuni ya kusambaza nishati bora ya gesi nchini ya Taifa Gas,wamekutana katika kiwanda kipya cha kutengeneza mitungi kilichopo Kibaha mkoani Pwani kwa ajili ya kuweka mikakati ya kuendelea kutoa huduma kwa wateja kwendana na kukua kwa biashara ya matumizi ya nishati safi ya gesi nchini sambamba na kupongezana kwa mafanikio yaliyopatikana kipindi kilichopita.

Akiongea kuhusiana na tukio hilo, Mwenyekiti Mtendaji wa Taifa Gas, Hamis Ramadhani amewapongeza wateja, mawakala wakuu wa kampuni, wafanyakazi na wadau wote kwa kuendelea kufanya kazi kwa pamoja na kufanikisha kupata mafanikio yaliyopatikana hadi kufikia sasa.

Kwa upande wake Meneja Mkuu wa kampuni hiyo , Deogratias David amesema Taifa Gas itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha inatoa huduma bora zaidi kwa wateja ili kuzidi kupata mafanikio sambamba na kuhakikisha Tanzania inaendelea kua kinara katika maendeleo endelevu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia duniani.

“Dhamira ya Taifa gas ni kuunga mkono agenda ya nishati safi inayoongozwa na Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan kwa lengo la kuwarahisishia Watanzania maisha kutokana na matumizi ya nishati safi kwa ajili ya kupikia ili kuchochea ukuaji wa biashara zao na uchumi kwa ujumla sambamba na kulinda mazingira”, amesema Devis.

Amesema kuwa kampuni itaendelea kuwekeza ili kufanikisha mkakati wa kutoa huduma bora kwa wateja na kuwasogezea huduma kwa karibu katika maeneo yote nchini kupitia kwa mawakala wake wakuu.

Kwa upande wao mawakala wakuu wa kampuni hiyo wamepata fursa ya kutoa maoni yao kuhusiana na jinsi gani ya kufanikisha mkakati wa masoko wa kampuni ambapo pia walitoa pongezi kwa uongozi na wafanyakazi wa Taifa Gas kwa kuendesha shughuli zake kwa ubunifu na weledi kwa lengo la kuhakikisha watanzania wananufaika na matumizi ya nishati ya Gesi.

Mawakala hao pia wameweza kuona uwekezaji mkubwa uliofanywa na kampuni kwa kujenga kiwanda kipya na cha kisasa cha kutengeneza mitungi ya gesi ambacho ni moja ya utekelezaji wa kimkakati wa kampuni wa kuhakikisha mapinduzi ya kijana yanafanikiwa kwa watanzania wengi zaidi kwa kutumia nishati safi kwa ajili ya kupikia.



Posted by MROKI On Monday, February 23, 2026 No comments
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo.
*********
Na Mwandishi Wetu
Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imekanusha malalamiko ya Taasisi ya Al-Malid kuhusiana na umiliki wa kiwanja Na 8 Kitalu A kilichopo Nzuguni jijini Dodoma.

Akizungumza jijini Dodoma leo tarehe 23 Februari 2026, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo amesema, malalamiko ya taasisi hiyo yalishughulikiwa kikamilifu na walalamikaji kujibiwa kwa maandishi kupitia barua yenye kumbukumbu namba BA 97/171/01L/28 ya tarehe 9/01/2026.

Kwa mujibu wa Dkt Akwilapo, kumbukumbu za umiliki zinaonesha Al-Malid iliwahi kumilikishwa kiwanja namba 1 Kitalu H Ihumwa jijini Dodoma wakati wa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) tarehe 21 Machi 2009 kikiwa na ukubwa wa mita za mraba 181,700 kwa matumizi  ya taasisi.
Hata hivyo, amesema taasisi ya Al-Mallid ilikiuza kiwanja hicho kwa Kampuni ya Elishadai Centre for Academic Limited kupitia mkataba uliosainiwa tarehe 25 Julai 2009, na Wizara ilipatiwa nakala ya mauziano hayo.

Ameongeza kuwa, taasisi ya Al-Mallid ilianza kulalamika kuhusu kiwanja hicho tajwa mnamo mwaka 2019 na wataalamu wa Wizara waliomba kuoneshwa eneo linalolalamikiwa ambapo taasisi hiyo ilionesha maeneo tofauti kwa nyakati tofauti, ambayo ufuatiliaji uliofanyika ulibaini kuwa, maeneo hayo yana miliki halali za Taasisi nyingine na wao Al-Mallid hawakuwa na nyaraka zozote za kuthibitisha umiliki wao kwenye maeneo hayo.

Kupitia kumbukumbu za Wizara eneo lenye Kiwanja Na. 1 Kitalu ’H’, ni eneo ambalo taasisi ya Al- Mallid ililiuza kwa Kampuni ya Elishadai Centre for Academic Limited. Aidha, Wizara imekuwa ikiwafahamisha ukweli wa suala hili mara zote ambazo walifika kupata huduma.

Waziri huyo wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ameutaarifu umma kuwa upatikanaji na umiliki wa ardhi unasimamiwa kwa mujibu wa Sheria za Ardhi pamoja na kanuni zake. Sheria na Kanuni zimewekwa makusudi ili kuondoa migogoro kama hii na vilevile kuimarisha usimamizi bora wa rasilimali ardhi.

Amesisitiza kuwa, ni umuhimu kuzingatia Kanuni na Taratibu zilizowekwa kwa mujibu wa sharia ili kuondoa mgongano isiyo ya lazima katika jamii.

Tarehe 18 Februari 2026 Taasisi ya kiislamu ya Al-Mallid ya mkoani Dodoma iliilalamikia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa madai ya kusababisha sintofahamu ya umiliki wa kiwamja namba 8 Kitalu A Nzuguni C,  malalamiko ambayo yalisambaa katika mitandao mbalimbali ya kijamii.
Posted by MROKI On Monday, February 23, 2026 No comments

February 22, 2026


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele akizungumza leo Februari 22, 2026 na washiriki wa mafunzo ya makarani waongozaji wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Peramiho unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026. 

Na Waandishi wetu, Ruvuma na Songwe
Tume huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imewataka Makarani Waongozaji wapiga kura katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma kutekeleza majukumu yao bila woga kwa kufuata Sheria, Kanuni, maelekezo ya Tume.
 
Wito huo umetolewa na  Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele leo Februari 22, 2026 wakati akizungumza na washiriki wa mafunzo ya makarani waongozaji wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Peramiho unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026. 

“Nawasihi mnapokwenda kufanya kazi yenu mkawe wakarimu na wanyenyekevu katika kutekeleza shughuli zenu... .” amesema Jaji Mwambegele.

Jaji Mwambegele amewataka washiriki hao kutoa kipaumbele kwa wapiga kura wenye mahitaji maalum wakiwemo watu wenye ulemavu, wazee, wagonjwa, wajawazito na akina mama wanaonyonyesha watakaokwenda na watoto wao vituoni.

“Jambo lingine nawasihi mkatende kazi yenu bila kumuogopa mtu yeyote bali mkatekeleze majukumu yenu kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo ya Tume,” amesema Mhe. Jaji Mwambegele.
 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura klatika Jimbo la Peramiho 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura klatika Jimbo la Peramiho 
Katika hatua nyingine Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama Kuu Mhe. Asina Omari leo tarege 22 Februari, 2026 ametembelea mafunzo ya Makarani Waongozaji Wapiga Kura kwa ajili ya Uchaguzi mdogo wa Udiwani Kata ya Shiwinga, iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, Mkoani Songwe.
 
Mhe. Asina amewataka washiriki wa mafunzo hayo kufanya kazi kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo ya Tume kwani wao ndio taswira ya Tume katika kufanikisha uchaguzi huo.
 
Amesema pamoja na jukumu lao la kuwaongoza wapiga kura kutekeleza haki yao ya kupiga kura kwa urahisi, wanapaswa kutoa elimu ya mpiga kura kwa wapiga kura ambao hawatambui utaratibu wa kupiga kura kituoni.
 
“Mafunzo haya yana lengo la kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yenu. Hivyo, niwakumbushe mkatekeleze majukumu yenu kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo ya Tume” amesema Mhe. Asina na kuongeza….
 
“Kabla ya mafunzo mmeapa, viapo vyenu maana yake ni kwenda kutekeleza majukumu kwa uadilifu na kuzingatia weledi na kazi yenu ni zaidi ya kuwaongoza wapiga kura kwani mna jukumu la kutoa elimu ya mpiga kura”
 
Amesema katika kutekeleza majukumu yao wanapaswa kushirikiana na watendaji wa uchaguzi na wasimamizi wa vituo vya kupigia kura ili kuhakikisha wanatatua changamoto wanazokutana nazo wakati wa kutekeleza majukumu yao.
 
Akifungua mafunzo hayo, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Mbozi, Ndg. Danny Tweve amewakumbusha washiriki hao kuwa wamechaguliwa kutekeleza jukumu hilo la kitaifa kwa niaba ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi. Hivyo, wanapaswa kutoa huduma kwa wapiga kura kwa uaminifu na weledi mkubwa na kwa kuzingatia sheria za uchaguzi ili kufanikisha uchaguzi huo na kuwasaidia wapiga kura kutekeleza haki yao bila usumbufu.
 
Uchaguzi katika Jimbo la Peramiho, Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma na Udiwani katika Kata ya Shiwinga, Halmashauri ya Mbozi Mkoani Songwe umeapangwa kufanyika Februari 26,2026.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura katika Kata ya Shiwinga. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura katika Kata ya Shiwinga. 

Posted by MROKI On Sunday, February 22, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo