Nafasi Ya Matangazo

September 21, 2016

Mkurugenzi wa Mawasiliano na Masuala ya Nje  wa TBL Group, Georgia Mutagahywa, (kulia)   na Mkurugenzi Mkazi wa AMREF Health Afrika Tanzania Dk.Florence Temu. wakionyesha waandishi wa habari (hawapo pichani) hati  za mkataba wa  makubaliano ya kuchimba Kisima cha  maji  katika Wilaya ya Muleba  mkoa wa Kagera.Hafla ilifanyika katika Ofisi za AMREF jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mkazi wa Amref Health Afrika Tanzania Dk.Florence Temu (katikati) na Mtaalamu  wa Maji,Afya na Usafi wa Mazingira wa Amref Health Afrika- Tanzania Mhandisi Charles Mlingi (kushoto) wakimsikiliza  Mkurugenzi wa Mawasiliano na Masuala ya Nje wa TBL Group, Georgia Mutagahywa, (kulia)  jijini Dar es Salaam muda mfupi   baada ya kusaini mkataba wa makubaliano na Amref Health Africa –Tanzania  wa kuchimba kisima cha  maji  katika Wilaya ya Muleba  mkoa wa Kagera.



Mkurugenzi wa Mawasiliano na Masuala ya Nje wa TBL Group, Georgia Mutagahywa, (kushoto)  akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani)  baada ya kusaini mkataba wa makubaliano na AMREF Health Africa –Tanzania  wa kuchimba visima virefu vya  maji safi  katika Wilaya ya Muleba  mkoani  Kagera.Kushoto ni Mkurugenzi Mkazi wa AMREF Health Africa Tanzania Dk.Florence Temu.
************
 

KAMPUNI ya TBL Group imesaini mkataba mkataba na Shirika lisilo la Kiserikali la AMREF Tanzania  kwa ajili ya kuchimba kisima cha maji chenye kina kirefu katika  kijiji cha Busole Wilayani Muleba,mradi wenye thamani  ya zaidi ya milioni 67 ambao ukikamilika utanufaisha wananchi wa kijiji hicho na vijiji jirani.

Akiongea wakati wa hafla ya kusaini mkataba huo jijini Dar es Salaam jana,Mkurugenzi wa Mambo  ya Nje wa TBL Group,Georgia Mutagahywa alisema kuwa msaada huo  ni utekelezaji wa moja ya sera ya kampuni ya kutumia sehemu ya faida inayopata baada ya kulipa kodi kusaidia huduma za kijamii.

Alisema kampuni  imeingia ubia na AMREF Tanzania katika utekelezaji wa mradi huu kwa kuwa ni moja ya taasisi ambao inao utaalamu wa kutekeleza miradi ya maji vijijini ambayo imeonekana kunufaisha jamii katika sehemu mbalimbali za nchini.

“Tunafurahi kushirikiana na AMREF katika mradi huu unaotarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha mwaka mmoja,tuna uhakika utawapunguzia wanawake adha ya kutembea mwendo mrefu kutafuta maji,kupunguza utoro wa wasichana mashuleni pia utawezesha wakazi wa maeneo hayo kupata maji safi na kupunguza uwezekano wa kupata maradhi yatokanayo na matumizi ya maji yasio salama”.Alisema Mutagahywa.

Alisema  TBL Group ikiwa kampuni inayotegemea malighafi ya maji kwa asilimia kubwa katika viwanda vyake inaelewa changamoto iliyopo ya upungufu wa maji katika sehemu mbalimbali na ndio maana imekuwa ikisaidia kufanikisha miradi ya kuwapunguzia wananchi adha ya maji kwa kusaidia kuwachimbia visima kama ambavyo imefanya katika mradi huu “Tunaelewa tatizo la maji ni  changamoto kubwa na tutaendelea kushirikiana na serikali na wadau wengine kufanikisha miradi ya maji katika sehemu mbalimbali nchini”.Alisema.

Kwa  upande wake Mkurugenzi Mkazi wa AMREF Tanzania,Dk.Florence Temu,aliishukuru TBL Group kwa kuamua kushirikiana na taasisi yake kutekeleza mradi wa maji wa kuboresha maisha ya wananchi wa wilaya ya Muleba.

“Tunashukuru kushirikiana na TBL Group katika mradi huu na tutahakikisha tunaufanikisha na unaleta manufaa kwa  wananchi  kama ilivyokusudiwa kwa kuwa tunao  utaalamu na uzoefu wa muda mrefu wa kuendesha miradi ya uchimbaji wa visima vya maji katika maeneo ya vijijini na tumefanikisha uazishwaji wa miradi shirikishi ya maji sehemu mbalimbali vijijini”.Alisema Dk. Temu.

Aliongeza kuwa katika  hatua ya awali kampuni itafanya utafiti ili kubaini sehemu ya kuchimba kisima hicho na baada ya kufanikisha zoezi na kuufanya mradi huo kuwa endelevu  itatoa elimu kwa wananchi  ili wauone mradi huu kuwa ni wa kwao hata baada ya kukamilika.

Posted by MROKI On Wednesday, September 21, 2016 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo