Nafasi Ya Matangazo

January 16, 2026


Na: OWM (KAM) – Dodoma
Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano imetangaza vijana 5,746 kujiunga na mafunzo ya uanagenzi ambayo yatawawezesha kupata ujuzi wa vitendo utakao wasaidia kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi kwa kujiajiri na kuajiri wenzao.
 
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Clement Sangu wakati wa Mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika leo Januari 16, 2026, Jijini Dodoma ukilenga kuelezea vijana waliochaguliwa kushiriki mafunzo ya Uanagenzi kwa mwaka 2025/2026.
 
Aidha, amesema mafunzo hayo yanafadhiliwa na Serikali kwa asilimia 100.
 
Mhe. Sangu amesema, mafunzo hayo ya ufundi stadi yatatolewa katika vyuo 47 nchini kupitia fani za ubunifu wa mitindo na ushonaji nguo, ufundi bomba, uashi, useremala, uchomeleaji na uungaji vyuma, upakaji rangi na maandishi ya alama, upishi, utengenezaji wa vipuri vya mitambo, ufundi magari na mitambo, umeme wa majumbani na viwandani, umeme wa magari, huduma za hoteli na utalii, ukataji madini na ufundi vyuma.
 
“Fani hizi ni muhimu sana kwa vijana wetu, kwa kuwa zitawawezesha kupata ujuzi ambao utawawezesha kuajiriwa au kujiajiri,” amesema
 
Vilevile amesema kuwa, Serikali inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuweka mikakati na kutekeleza afua mbalimbali zitakazowezesha kuwa na jamii yenye ustawi na kujenga nguvu kazi yenye ujuzi utakao wawezesha kushindana katika soko la ajira ndani na nje ya nchi.
 
Amesema, afua hizo ni pamoja na utekelezaji wa Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi kwa njia ya Uanagenzi inayolenga kuimarisha nguvukazi ya taifa ili kumudu ushindani katika soko la ajira la ndani na nje ya nchi kwa kupata ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira na hatimaye kuweza kuajiriwa au kujiajiri.
 
Kadhalika, Waziri Sangu amevitaka vyuo vilivyopata dhamana ya kutoa mafunzo hayo, kutoa ushirikiano kwa vijana waliochaguliwa, kuwafundisha na kuwasimamia vyema kipindi chote cha mafunzo yao. Pia, ametoa wito kwa vijana waliochaguliwa kushiriki mafunzo kusoma kwa bidii, kuwa na nidhamu na kufuata sheria na taratibu za vyuo. 
Posted by MROKI On Friday, January 16, 2026 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo