Mkoa wa Shinyanga umeendelea kuimarisha nafasi yake kama kitovu muhimu cha sekta ya madini nchini, huku uchimbaji wa dhahabu na almasi ukitajwa kuwa nguzo kuu ya ukuaji wa uchumi wa mkoa huo na chanzo kipya cha fursa za uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani ya madini.
Akizungumza mkoani Shinyanga, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa huo, Mhandisi Noel Odera, amesema mkoa umebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi za madini zikiwemo dhahabu, almasi, madini ya ujenzi pamoja na madini ya viwandani kama chokaa, hali inayochochea shughuli za kiuchumi, ajira kwa wananchi na ongezeko la mapato ya Serikali.
Amesema shughuli za uchimbaji zinaendelea kwa kasi katika maeneo mbalimbali ya mkoa, zikihusisha wachimbaji wadogo, wa kati na migodi mikubwa, ikiwemo migodi ya El-Illari na Williamson Diamond iliyopo Wilaya ya Kishapu katika eneo la kimbaritiki linalozalisha sehemu kubwa ya almasi nchini.
Kwa mujibu wa Mhandisi Odera, utafiti mpya umeibua matumaini ya ongezeko la uzalishaji baada ya wachimbaji wadogo kugundua almasi katika eneo la Ng’wapangabule kwenye mwamba unaofanana na kimbaritiki, hatua inayofungua fursa mpya za uwekezaji na utafiti wa kina wa kijiolojia.
Ameeleza kuwa uzalishaji wa dhahabu unaendelea kuimarika katika maeneo ya Mwakitoryo, Nyandolwa, Mwanubi, Ishinabulandi na Mwazezema ambapo wachimbaji wadogo na wa kati wameendelea kuchangia ukuaji wa sekta hiyo kupitia ajira, kipato binafsi na mapato ya Serikali.
Mbali na uchimbaji, amesema Shinyanga ina mazingira rafiki kwa uwekezaji katika viwanda vya kisasa vya uchenjuaji wa dhahabu vinavyotumia teknolojia za Carbon in Pulp (CIP) na Carbon in Leach (CIL), vitakavyosaidia kuongeza thamani ya madini kabla ya kuuzwa na kuwapa wachimbaji huduma bora za uchenjuaji.
Aidha, amesema mkoa una fursa kubwa za uwekezaji katika viwanda vya utengenezaji wa bidhaa zitokanazo na almasi ikiwemo vito vya thamani na mapambo, hatua itakayoongeza thamani ya madini ndani ya nchi na kuimarisha uchumi wa viwanda.
Mhandisi Odera ameongeza kuwa uwepo wa malighafi za kutosha kama chokaa umeifanya Shinyanga kuwa eneo lenye uwezo mkubwa wa uwekezaji katika viwanda vya saruji, vitakavyosaidia kukuza sekta ya ujenzi, kuongeza ajira na kuimarisha maendeleo ya kijamii.
Amesema masoko ya madini yanaendelea kuimarika ambapo kwa sasa kuna wanunuzi wakubwa 19 wa dhahabu na almasi wanaofanya biashara mkoani humo, hali inayorahisisha biashara ya madini kwa wachimbaji na kuongeza uwazi wa biashara hiyo.
Amehitimisha kwa kuwahimiza wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kutumia fursa zilizopo Shinyanga kwa kuwekeza katika uchimbaji, utafiti wa madini na viwanda vya kuongeza thamani, akisisitiza kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki ili sekta ya madini ichangie zaidi maendeleo endelevu ya taifa na ustawi wa wananchi.










0 comments:
Post a Comment