Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima ametambuliwa kuwa mmoja wa viongozi wanawake mashuhuri kutoka Tanzania kati Wanawake 100 Wanaoheshimiwa wa Asili ya Kiafrika waliotambuliwa kwa mwaka 2026.
Tuzo ya Wanawake Wenye Sifa ya Juu wa Asili ya Afrika ni Heshima Maalum inayotolewa na Kongamano la Wanawake wa Afrika (Africa Women Summit) kwa Wanawake 100 waliodhihirisha uongozi wa kipekee, uadilifu wa hali ya juu na mchango mkubwa katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kisiasa barani Afrika na katika jumuiya ya kimataifa.
Orodha hii inalenga kutambua na kuenzi wanawake wanaobadilisha simulizi, kuvunja vikwazo, na kuhamasisha kizazi kijacho cha viongozi wanawake.
Katika toleo la mwaka 2026, orodha hii inajumuisha wanawake mashuhuri kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika ambapo, kwa upande wa Tanzania, orodha ya mwaka 2026 imemtambua Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, kwa mchango wake katika kuendeleza usawa wa kijinsia, uwezeshaji wa wanawake, ulinzi wa watoto, na ujumuishaji wa makundi maalum.
Naye Waziri Dkt. Gwajima amepokea utambuzi huo kwa moyo wa shukrani na kutoa shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ndiye kinara duniani wa uwezeshaji wanawake katika Nyanja mbali ikiwemo uchumi na uongozi hivyo, moja kwa moja utambuzi wake ni juhudi na mchango mkubwa wa Rais Dkt. Samia katika kumuamini na kumpa nafasi na kumlea hadi hatua aliyofikia sasa.
“Namshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutekeleza dhamira yake ya kutupa nafasi wanawake na kutulea ili, tutoe mchango wetu kwenye maendeleo na ustawi wa nchi yetu. Mimi na timu yangu, heshima hii ni yetu sote hivyo, tutaendelea kuchochea Kazi na Utu kwa kujituma kwa bidii ili kuwagusa wananchi wote kwa wakati na hususan, wenye mahitaji maalum ili kutimiza maono ya Mhe. Rais wa JMT Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuenzi heshima hii’ amesema Dkt. Gwajima.
Dkt. Gwajima anaongoza juhudi za kitaifa katika kukuza usawa wa kijinsia, uwezeshaji wa wanawake, ulinzi wa watoto, pamoja na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia. Pia amekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha makundi maalum ikiwemo watu yanajumuishwa kikamilifu katika mipango ya maendeleo ya taifa.





0 comments:
Post a Comment