Ushirikiano baina ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Walipakodi umetajwa kuwezesha Mamlaka hiyo kuandika historia mpya kwa kukusanya kiasi cha shilingi trilioni 9.31 kwa kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26 sawa na ufanisi wa asilimia 106.4 ya lengo la kukusanya shilingi trilioni 8.75.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda April 1, 2026 imeeleza kuwa kwa mwezi Machi pekee TRA imekusanya shilingi trilioni 3.58 sawa na ufanisi wa asilimia 107.6 ya lengo la kukusanya shilingi trilioni 3.32.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa makusanyo hayo ya kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/26, ni sawa na ukuaji wa asilimia 23.6 ikilinganishwa na kiasi cha shilingi trilioni 7.53 kilichokusanywa katika kipindi kama hicho mwaka wa fedha 2024/25.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo Ufanisi wa makusanyo kwa mwezi Machi unapelekea TRA kuweza kuandika rekodi mpya za kipekee katika ukusanyaji wa mapato nchini Wastani wa Makusanyo kwa mwezi katika kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26 umefikia shilingi trilioni 3.10 ambacho ni kiasi cha juu kabisa ukilinganisha na wastani wa shilingi trilioni 2.51 kwa kipindi kama hicho mwaka 2024/25.
TRA imeweza kurekodi Ukuaji chanya wa asilimia 23.6 katika kipindi cha Januari -Machi 2026, na imeweza kulifikia na kuvuka lengo la makusanyo kwa miezi 21 mfululizo kuanzia mwezi Julai 2024, mafanikio ambayo Mamlaka haijawahi yafikia toka ianzishwe hali ambayo imechagizwa na makusanyo ambayo yamechangiwa na ukaribu uliopo baina ya Mamlaka hiyo na Walipakodi.
Imeeleza kuwa Makusanyo yaliyokusanywa kwenye robo ya tatu ya Mwaka wa Fedha 2025/26 ni sawa na ukuaji wa asilimia 114.1 ukilinganisha na kiasi cha shilingi trilioni 4.35 kilichokusanywa katika kipindi kama hicho wakati Serikali ya Awamu ya Sita ilipoingia madarakani, mwaka 2020/21.
Ushirikiano baina ya TRA na walipakodi umeiwezesha katika kipindi cha Julai, 2025 hadi Machi, 2026, kusajili walipakodi waруа 900,755 ambao ni ufanisi wa asilimia 131.36 wa kusajili walipakodi wapya 685,706 kufikia tarehe 31 Machi, 2026.
Pia imeelezwa kuwa katika kipindi cha robo ya tatu mahusiano na Viongozi wa vyama vya wafanyabiashara pamoja na wafanyabiashara wenyewe yaliimarishwa kwa kufanya mikutano na kuwasikiliza ili kutatua changamoto zao za kikodi ambapo TRA itaendelea kuboresha mahusiano na walipakodi kwenye Shughuli zote za Kiuchumi ili kuhamasisha ulipaji kodi wa hiari nchini.
Aidha TRA inapenda kuwahakikishia wananchi wote kuwa itaendelea kushirikiana na wananchi wote kwa ukaribu ili kuhakikisha kuwa lengo la makusanyo kwa mwaka huu wa fedha 2025/26 linafikiwa lote na hivyo kuiwezesha Serikali kuweza tekeleza mipango ya maendeleo kwa manufaa ya Taifa zima.



.jpeg)



0 comments:
Post a Comment