Naibu Waziri Ofisi ya Makamu
wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa amesema suala la uhifadhi
wa mazingira ni mtambuka linahitaji ushirikiano wa sekta zote.
Amesema hayo wakati akizungumzia
katika kipindi cha ‘Kumekucha’ kinachorushwa na kituo cha runinga cha ITV leo
Juni 04, 2026 jijini Dodoma ambapo alisisitiza kuwa Serikali itaendelea
kusimamia sekta hiyo ili ilete maendeleo endelevu.
Mhe. Kwagilwa alieleza kuwa
kwa kutambua umuhimu huo Serikali imelipambanua suala la mazingira na mabadiliko
ya tabianchi kuwa ni mojawapo ya nguzo tatu zilizopo kwenye Dira ya Taifa ya
Maendeleo 2050.
“Tunatambua shughulI zote za
kiuchumi zinafanyika kwenye mazingira yetu hivyo tunao wajibu wa kuyatunza kwa
vizazi vya sasa na vijavyo kwani inakadiriwa kuwa ifikapo mwaka 2050 idadi ya
Watanzania itakuwa watu milioni 118 mara mbili ya idadi ya sasa hivyo shughuli
zinazoathiri mazingira zitakuwa nyingi Zaidi,” alisema.
Mhe. Kwagilwa alifafanua kuwa katika
miaka ijayo uchumi utakua na kwamba sekta mbalimbali zikiwemo za kilimo, uchimbaji
wa madini zitaathiri mazingira hivyo lazima kama nchi iwe na mkakati madhubuti
wa kuhakikisha kuwa mazingira yanahifadhiwa bila kuwathiriwa.
Aidha, akizungumzia
Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayoendelea hapa nchini, alisema
kuwa pamoja na mambo mbalimbali Ofisi ya Makamu wa Rais imeandaa maonesho
yanayohusisha takriban taasisi za Serikali zisizo za Serikali takriban 80.
Alisema maonesho hayo ni katika
kuhakikisha Serikali inaweka jitihada madhubuti za kusimamia mazingira kwa kuwashirikisha
na kuwakaribisha wadau mbalimbali kuonesha na kutoa elimu ya ubunifu na
teknolojia ya usimamizi wa taka.
“Tukiwa katika wiki hii ya
kuelekea kilele cha Siku ya Mazingira Duniani tunayo mabanda ya wadau
wanaoonesha namna ya kuchakata taka, kuzirejeleza au kuzitumia tena, wananchi
wanapata elimu hatua itakayosaidia kupunguza taka zinazozogaa na kuchangia
uzalushaii wa gesijoto,” alisema.
Kwa upande mwingine Naibu
Waziri hiyo alisema Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC)
likiwa Mamlaka kamili itaweza kutekeleza majukumu kwa nguvu zote bila uonevu
Alisema hivi sasa kuna sheria
mbalimbali zenye mnasaba na mazingira lakini ziko kwenye sekta tofauti tofauti
zikiwemo ya Maji, Usafi na Usafi na Mazingira ambazo NEMC haina meno ya
kuziingilia hivyo, ikiwe Mamlaka kamili itakuwa na nguvu ya kuwawajibisha
wanaokiuka sheria.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)







0 comments:
Post a Comment