Nafasi Ya Matangazo

March 05, 2026


Na Mwandishi Wetu-Wizara ya Madini
Katika juhudi za Tanzania kuendelea kujidhihirisha kimataifa kupitia Sekta ya Madini, wanawake wa Kitanzania wameendelea kung’ara katika majukwaa ya madini barani Afrika na duniani. 

Hivi karibuni, katika Kongamano la African Mining Indaba nchini Afrika Kusini, Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wanawake Afrika (AWIMA) lilitoa tuzo kwa wanawake hodari wa sekta ya madini barani Afrika, ambapo wanawake wawili wa Tanzania walishinda vipengele tofauti. 

Mshindi mwingine ni Eng. Rose Mayembe, aliyeibuka mshindi wa pili katika kipengele cha Leading Woman in Large-Scale Mining akitanguliwa na mshindi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na wa tatu kutoka Afrika Kusini.

 Eng. Rose Mayembe  ni nani na ametoka wapi?

Akizungumza katika mahojiano maalum na Madini Diary, Rose anasema yeye ni mhandisi na mtaalamu mwelekezi wa masuala ya kimazingira na jamii, uchimbaji endelevu, na mabadiliko ya tabianchi. 

Safari yake katika madini ilianza takribani miaka 12 iliyopita aliposhiriki katika utekelezaji wa hatua za kufunga na baada ya kufunga mgodi mkubwa wa uchimbaji dhahabu wa Golden Pride Project (GPP) uliokuwa unamilikiwa na kampuni ya Resolute Mining Wilayani Nzega, Tabora. 

Uzoefu huo ulimfundisha umuhimu wa kuzingatia mipango ya kimazingira na kijamii mapema, ili kupunguza madhara kwa jamii na mazingira. 

“Hapo ndipo niliona umuhimu wa kuingiza fikra za mabadiliko ya tabianchi na ubunifu tangu mwanzo wa mradi,” anasema Rose.

Tuzo ya African  Mining Indaba na GGA
Katika Mining Indaba, Rose alitambuliwa mshindi wa pili wa Leading Woman in Large-Scale Mining in Africa. Anasema tuzo hiyo ni heshima kubwa, kwani majukwaa kama hayo hujumuisha Serikali, wawekezaji, kampuni kubwa, na wataalamu kutoka duniani kote. Anasema  ushindi huo unaonyesha uwezo wa wanawake wa kitanzania kushindana na kuongoza katika shughuli za uchimbaji mkubwa. Rose anasisitiza, “kwa wanawake, tuzo hii ni ishara ya kuvunja glass ceiling na kuthibitisha tunaweza kuwa mezani pa maamuzi, kusukuma mbele ajenda ya madini yenye uwajibikaji, ushindani wa kimataifa, na ushiriki wa wanawake na vijana,” anasema.

Mbali na tuzo hiyo, mwaka 2025, Rose alipata tuzo ya Global Advocacy Award (GAA) katika kipengele cha Nishati Safi na Uchimbaji Endelevu (Clean Energy & Sustainable Mining), ikitambua mchango wake katika SDG 7 (Affordable and Clean Energy)  iliyotolewa wakati wa Global Advocacy Forum Awards (GAF 2025) London, Uingereza.

Safari ya Kazi na mchango wake Sekta ya Madini

Kwa sasa, Rose anafanya kazi katika miradi ya kitaifa na kimataifa, akichangia uzoefu wake katika hatua zote za maisha ya mgodi: usanifu wa migodi, uendeshaji migodi, kufunga mgodi na baada ya kufungwa (post-closure). Lengo lake ni kuhakikisha sekta ya madini inaleta mapato, inalinda mazingira, inaheshimu haki za binadamu, na kuchangia maendeleo endelevu ya jamii.

 “Nilipoanza kuzungumza kwa takwimu na maandalizi ya kitaalamu, niliona nafasi ya uongozi si cheo bali ni uwezo wa kuathiri maamuzi na tangu hapo sikuwahi tena kujiona kama mshiriki wa pembeni bali kama sehemu ya mwelekeo wa Sekta,’’ anasema.


Nini kilimfikisha  alipo?
Anapoulizwa kilichomfikisha alipo anasema ilikuwa ni uamuzi wa ndani na aliamini kutokusubiri ili kuthibitishwa na wengine katika sekta ambayo imezoea sauti flani na kwamba aligundua ubora wa hoja unazidi sauti ya anayezungumza.  

Nini kilichomfanya atambulike?
Anasema anaamini kinachomtofautisha ni uwezo wake wa kuunganisha taaluma tofauti katika mtazamo mmoja wa kimkakati, akiangalia Sekta ya Madini si tu kama shughuli za uchimbaji bali kama mfumo unaogusa uhandisi, mazingira, jamii, fedha, na sera. “Uzoefu wangu katika hatua zote za maisha ya mgodi kuanzia feasibility, design, operations hadi closure na post-closure na umenipa  uwezo wa kuona picha kubwa na kutoa mwelekeo unaozingatia uendelevu tangu mwanzo wa mradi,’’anasisitiza.

Anasema zaidi, mtazamo wa mabadiliko ya tabianchi na haki za binadamu kama sehemu ya maamuzi ya kimkakati, umemfanya kuunganisha uchumi, mazingira, na jamii katika mfumo mmoja unaotekelezeka.

Wanawake Wachimbaji Tanzania

Mhandisi Rose anasema  wanawake katika Sekta ya madini wakiwemo  wachimbaji na wataalamu wanaofanya kazi na sekta, wanahitaji zaidi kuaminiwa na kupewa nafasi ya kuongoza. Anasema changamoto si  uwezo ni nafasi. ‘’Tunahitaji kushirikishwa katika maamuzi ya kimkakati, bodi na sera, si kubaki katika utekelezaji pekee,’’ anaeleza.


Anaizungumziaje Sekta ya Uchimbaji   Mdogo?

Mhandisi Rose anashauri kuanza na uwezeshaji wa wachimbaji wadogo, kuwarasimisha, kuwezesha upatikanaji wa mitaji, elimu ya biashara, na mafunzo ya lazima ya mazingira na usalama. Anasisitiza mwongozo rahisi wa EIA na ufuatiliaji wa kitaalamu ambao anasema unaweza kuboresha sekta hiyo bila kuongeza mzigo wa kisheria. Anasema lengo ni kujenga sekta ya uchimbaji mdogo endelevu, salama, na yenye ushindani wa muda mrefu.

Wito kwa Watanzania, wanawake na Wasichana.

Anatoa wito kwa watanzania, hususan wasichana na wanawake, akisema sekta ya madini ni fursa ya ubunifu na uongozi, si sekta ya jinsia. “Jiwekezeni katika elimu, jengeni ujuzi, na msijitenge katika meza za maamuzi. 

Uwezo hauna jinsia. Madini ni chachu ya maendeleo, lakini maendeleo ya kweli yanakuja pale tunaposhirikisha wanawake na vijana kikamilifu. 

"Naamini kizazi kijacho cha wanawake hakitaomba nafasi, kitakuwa sehemu ya mwelekeo wa sekta hii,” anasema Rose.
Posted by MROKI On Thursday, March 05, 2026 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo