WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Deogratius Ndejembi amemuelekeza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mhandisi Anthony Sanga kumsimamisha kazi na kumchukulia hatua za kinidhamu, Afisa Ardhi wa Halmashauri ya Mji Handeni kwa kuwa chanzo cha migogoro ya ardhi kwenye halmashauri hiyo.
Mhe. Ndejembi ametoa agizo hilo Januari 20, 2025 alipofanya ziara ya kikazi katika Wilaya ya Handeni Mkoani Tanga ambapo alitembelea eneo la Kwanjugo Kitalu A ambalo wananchi wake wamekua wakilalamika kwa muda mrefu kuchukuliwa mashamba yao bila kulipwa fidia.
“Hapa kiasili pana historia yake, palikua pana umiliki wa wenyewe sasa haiwezekani watu hawa kuonewa na migogoro yote hii ni kwa sababu hatusikilizi wananchi wetu. Sasa ninamuelekeza Katibu Mkuu kumsimamisha kazi mara moja Mkuu wa Idara ya Ardhi wa Halmashauri na haraka sana aletwe mtu mwingine atakayetatua migogoro ya ardhi Handeni.'
'Lakini pia ninaelekeza kuundwa kwa Timu ya uchunguzi itakayokua chini ya Kamishna wa Ardhi, ije hapa Handeni ndani ya wiki moja ili tuangalie umiliki wa viwanja vya sasa ni akina nani, na kama ni watumishi wa ardhi tuchukue hatua kali. Kwa sababu hatuwezi kuruhusu watumishi wa ardhi kunyang’anya ardhi ya wananchi,” amesema Mhe. Ndejembi.
0 comments:
Post a Comment