Nafasi Ya Matangazo

October 05, 2024

Na Mwandishi Wetu, Morogoro
Klabu ya Michezo ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imetwaa ubingwa wa mpira wa miguu wa michuano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala za Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI) baada ya kuwafunga Wizara ya Maji kwa mikwaju ya penati 3-2 katika mchezo wa fainali uliofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri Mkoani Morogoro.

Timu hizo zilitoshana nguvu kwa kutofungana katika dakika za kawaida, ambapo ikafuata hatua ya kupigiana mikwaju ya penati na Utumishi wakashinda baada ya kipa wake kupangua mikwaju miwili na moja mpigaji akipaisha juu.

Katika mchezo wa fainali wa mpira wa netiboli timu ya Ofisi ya Rais Ikulu imedhihirisha ni malkia kwa kutwaa ubingwa kwa mara ya 10 mfululizo ambapo leo wamewachapa Wizara ya Afya kwa magoli 51-25. Katika mchezo huo uliochezwa kwa robo nne, washindi waliongoza zote kwa magoli 13-7; 27-12 na 40-19.

Kocha Haleluya Kavalambi wa Ikulu, amesema siri ya mafanikio yao ni kujituma na kufanya mazoezi kwa bidii, na ameahidi kuendeleza ubabe kwa wapinzani katika mashindano yote wanayoshiriki.

Naye kocha Micky Mollel wa timu ya Wizara ya Afya amesema mchezo ulikuwa mzuri na anawapongeza waamuzi wamechezesha vizuri, pamoja na kwamba alitarajia kutwaa ubingwa lakini bahati haikuwa yao na anakwenda kujipanga kwa mwakani.




Posted by MROKI On Saturday, October 05, 2024 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo