Nafasi Ya Matangazo

April 08, 2024

Kuanzia Aprili 1,2024 hadi Aprili 7,2024 watu 15 wamefariki dunia kutokana na kusombwa na maji ya mvua zinazoendelea kunyesha, wengine wakiwa wanaogelea, wengine wakiwa wanavuka maeneo ambayo maji yanatiririka kwa kasi na wengine kutokana na kutumbukia kwenye mashimo/madimbwi yaliyojaa maji. Miongoni mwa watu hao watoto ni 12 na watu wazima ni 3.
 
Matukio hayo yametokea katika Wilaya  mbalimbali hapa nchini. Wilaya ya Kalambo Mkoa wa Rukwa mtu mmoja mwanaume miaka 18, alisombwa na maji ya mvua yaliyokuwa yakitokea milimani wakati akijaribu kuvuka daraja Aprili 1,2024. 

Tarehe hiyo hiyo katika Wilaya ya Kilwa Mkoa wa Lindi watoto 2 wote wakiwa na miaka 12 walikufa maji baada ya kusombwa na maji ya mvua.
 
Aprili 2,2024 mwanaume mmoja wa miaka 28, huko katika Wilaya ya Ludewa Mkoa wa Njombe alikufa baada ya kufukiwa na udongo ulioporomoka kutokana na mvua kubwa zilizokuwa zinanyesha.
 
Aprili 3,2024 huko Wilayani Muheza Mkoa wa Tanga, mtoto wa miaka 8 alikufa maji wakati akiogelea.
 
Mkoani Pwani Aprili 3,2024 Wilaya ya Mkuranga mtoto mmoja wa miaka 10 alifariki Dunia akiogelea mto Mzinga na Wilaya ya Kibaha mtoto wa miaka 12 alikufa maji yaliyokuwa yamejaa katika bonde la mpunga.
 
Aprili 5,2024 mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 55 huko Wilayani Babati moani Manyara alikufa maji baada ya kutumbukia kwenye shimo lenye maji.
 
Aidha, Aprili 7,2024 huko katika Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya watoto 5 wenye umri kati ya miaka 5 na 6 walifariki dunia baada ya kuzama kwenye dimbwi lilojaa maji ya mvua wakiwa wanaogelea.

 Pia tarehe hiyo hiyo huko Mkoani Geita watoto 2 wenye umri wa miaka 9 na 14 walifariki dunia baada ya kusombwa na maji ya mvua yaliyokuwa yanatiririka kutoka milimani wakitoka kuokota kuni.
 
Jeshi la Polisi kutokana na mtiririko wa matukio haya kwa mwezi huu na  katika kipindi kifupi na uzoefu wa matukio mengine kama haya ya siku za nyuma linaendelea kutoa wito na tahadhari kwa watu wote hususani wazazi na walezi kuwalinda watoto kwa karibu sana na kuwapa maelekezo sahihi kutokana na mvua hizi zinazoendelea kunyesha. 

Pia Viongozi wa Serikali za Mitaa, Waalimu mashuleni, Viongozi wa Dini tuendelee kuelimisha watoto wetu kujihadhari na maji yaliyotuama au yanayotembea na wala wasishindane na maji ya mvua yanayotiririka kwani ni hatari kwa maisha yao. Kila mmoja wetu kwa nafasi yake akemee anapoona watoto wakicheza, wakipita au kuogelea kwenye maeneo hatarishi. 

Sehemu ambazo zinastahili kuwekwa alama za tahadhari ziwekwe au kufunikwa mfano mashimo yaliyochimbwa kwa ajili ya visima vya maji majumbani na sehemu zingine.


Posted by MROKI On Monday, April 08, 2024 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo