Nafasi Ya Matangazo

April 24, 2023

Naibu Waziri wa Ujenzi, Eng. Godfrey Kasekenya, akihutubia wananchi wakati wa utiaji saini mkataba wa ujenzi wa barabara ya Sengerema - Nyehunge (km 54.4) kwa kiwango cha lami na ujenzi wa Kivuko kipya cha Buyagu – Mbalika, wilayani Sengerema, mkoani Mwanza.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara (TANROADS), Eng. Rogatus Mativila, akisaini mkataba wa ujenzi wa barabara ya Sengerema - Nyehunge (km 54.4) kwa kiwango cha lami na Mwakilishi kutoka kampuni ya AVM - Dilingham kwa gharama takribani Bilioni 73. mkoani Mwanza. Barabara hiyo ni sehemu ya mtandao wa barabara inayounganisha Mkoa wa Mwanza na Mikoa ya Geita, Kagera na Kigoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Bw. Lazaro Kilahala na Meneja wa Kampuni Songoro Marine, Major Songoro wakionesha mkataba wa ujenzi wa kivuko kipya cha Buyagu – Mbaika mara baada ya kutiliana saini kitakachogharimu kiasi cha Bil 3.8 wilayani Sengerema mkoani Mwanza. Kivuko hicho kipya kitakuwa na uwezo wa kubeba uzito wa tani 50 ikijumuisha abiria 100 (waliokaa 50 na waliosimama 50) pamoja na magari madogo 6.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara (TANROADS), Eng. Rogatus Mativila, akitoa taarifa ya ujenzi wa barabara ya Sengerema - Nyehunge (km 54.4) kwa kiwango cha lami wakati wa utiaji saini wa mkataba huo na Mwakilishi kutoka kampuni ya AVM - Dilingham kwa gharama takribani Bilioni 73. mkoani Mwanza. Barabara hiyo ni sehemu ya mtandao wa barabara inayounganisha Mkoa wa Mwanza na Mikoa ya Geita, Kagera na Kigoma.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Bw. Lazaro Kilahala, akitoa taarifa ya ujenzi wa kivuko kipya kitachotoa huduma kati ya Buyagu – Mbalika, mkoani Mwanza. Kivuko hicho kitakuwa na uwezo wa kubeba uzito wa tani 50 ikijumuisha abiria 100 (waliokaa 50 na waliosimama 50) pamoja na magari madogo 6.
Wananchi wakifatilia hotuba ya mgeni rasmi Naibu Waziri wa Ujenzi, Eng. Godfrey Kasekenya, wakati wa utiaji saini mkataba wa ujenzi wa barabara ya Sengerema - Nyehunge (km 54.4) kwa kiwango cha lami na ujenzi wa Kivuko kipya cha Buyagu – Mbalika, wilayani Sengerema, mkoani Mwanza.
*************
Serikali imesaini mikataba miwili ya ujenzi wa miundombinu ya barabara ya Sengerema - Nyehunge (km 54 4), kwa kiwango cha lami na ujenzi wa kivuko kipya kitakachotoa huduma kati ya maeneo ya Buyagu - Mbalika katika wilaya ya Sengerema na Misungwi kwa gharama ya takriban kiasi cha Bilioni 77 mkoani Mwanza.

Mkataba wa barabara umesainiwa kati ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), na kampuni ya AVM - Dilingham ya Uturuki kwa gharama ya shilingi Bilioni 73 na mkataba wa kivuko kipya umesainiwa kati ya Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) na kampuni ya Songoro Marine kwa gharama ya Bilioni 3.8.

Akishuhudia utiaji saini mikataba hiyo mkoani humo, Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya, amesema kuwa miradi hiyo itakapokamilika itaimarisha shughuli za kiuchumi kwa wananchi waishio maeneo ya Wilaya ya Sengerema hasa Halmashauri ya Buchosa.

Aidha, amesema miradi hiyo itasaidia kutengeneza ajira kwa wananchi wa Wilaya hiiyo wakati wa utekelezaji wa ujenzi.

Eng. Kasekenya ameziagiza TANROADS na TEMESA kuisimamia vyema miradi yote hiyo ili thamani ya fedha ipatikane na kukamilika kwa wakati.

Ameeleza kuwa ujenzi wa barabara na kivuko hicho utatekelezwa kwa kutumia fedha za ndani kwa asilimia 100 ikiwa ni moja ya juhudi na mikakati ya Serikali chini ya Uongozi thabiti wa Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kuboresha maisha ya wananchi wake hususan wana Sengerema.

Akiongelea kuhusu barabara Eng. Kasekenya ameeleza kuwa barabara hiyo ni sehemu ya mtandao wa barabara muhimu za nchi yetu ambayo inaunganisha Mkoa wa Mwanza na Mikoa ya Geita, Kagera na Kigoma.

"Barabara hii itakapokamilika itachochea shughuli za kiuchumi kama vile usafirishaji wa bidhaa mbalimbali na abiria, bidhaa za uvuvi, mazao ya chakula, mazao ya biashara mazao ya misitu na shughuli za kijamii kwa ujumla", amesema Eng. Kasekenya.

Eng. Kasekenya ametaja miradi mingine ya madaraja na barabara ambayo ujenzi/ukarabati wake unaendelea kwa kugharamiwa na Serikali ni ujenzi wa Daraja la Kigongo-Busisi lenye urefu (mita 3,000) pamoja na barabara unganishi zenye urefu wa km 1.66, barabara ya Tarime – Mugumu, sehemu ya Tarime hadi Nyamwaga (km 25), barabara ya Bugene hadi Burigi Chato National Park (km 60), Daraja la Kitengule lenye urefu wa mita 140 pamoja na barabara unganishi zenye urefu wa km 18, barabara ya Nyamuswa - Bunda - Kisorya hadi Nansio sehemu ya Nyamuswa – Bunda hadi Bulamba (km 56.4), na barabara ya Makutano – Nyamuswa hadi Ikoma Gate sehemu ya Sanzate hadi Natta (km 40).

Kwa upande wa ujenzi wa kivuko kipya Eng. Kasekenya amesema kuwa kivuko hicho kitatoa huduma Buyagu na Mbalika katika Wilaya ya Sengerema na Misungwi lengo likiwa ni kuwapatia usafiri ulio salama na wenye uhakika wananchi wa maeneo hayo ambayo wamekuwa wakitumia mitumbwi kwenye eneo hilo lenye umbali wa takribani kilometa saba.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Eng. Rogatus Mativila, amesema kuwa zabuni za ujenzi wa barabara hiyo zilitangazwa tarehe 13 Juni, 2022 na kufunguliwa tarehe 30 Agosti, 2022 ambapo jumla ya zabuni12 zilipokelewa na kufanyiwa tathmini na Mkandarasi aliyeshinda tuzo ni Kampuni ya AVM-Dilingham Construction International Inc. ya nchini Uturuki kwa muda wa miezi 28.

Naye Mtendaji Mkuu wa TEMESA, Lazaro Kilahala, amesema kuwa kivuko kipya cha Buyagu - Mbalika baada ya ujenzi kukamilika kitakuwa na uwezo wa kubeba uzito wa tani 50 zikijumuisha; abiria 100 (waliokaa 50 na waliosimama 50) pamoja na magari madogo 6.

Kilahala ameongeza kuwa mbali na ujenzi wa kivuko hicho wanaendelea na utekelezaji wa vivuko vingine ambapo jumla ya miradi mitano ya ujenzi wa vivuko vipya, miradi 18 ya ukarabati wa vivuko na miradi ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya vivuko imekwishasainiwa na inatekelezwa kwa gharama ya Shilingi bilioni 60.72.

Miradi hiyo iliyosainiwa ni moja ya mkakati wa Serikali ya kuwaondolea wananchi kero ya usafiri wa kivuko na kuboresha mtandao wa barabara na madaraja ili kuongeza ufanisi katika sekta ya usafiri na usafirishaji hapa nchini.

Posted by MROKI On Monday, April 24, 2023 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo