Nafasi Ya Matangazo

November 21, 2019

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 21 Novemba, 2019 ametunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari wa Falsafa katika Sayansi (Doctor of Science Honoris Causa) ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).
Mhe. Rais Magufuli aliyeongozana na Mkewe Mama Janeth Magufuli ametunukiwa shahada hiyo na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma Mhe. Benjamin William Mkapa (Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu) katika sherehe za mahafali ya 10 ya chuo hicho zilizofanyika katika ukumbi wa Chimwaga Jijini Dodoma.
Sherehe hizo zimehudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa aliyeongozana na Mkewe Mama Mary Majaliwa, Mawaziri, Wabunge, Mabalozi wa nchi mbalimbali, Viongozi Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Wakuu wa Mikoa, viongozi wa Dini, viongozi wa siasa na wasomi.
Wasifu wa Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli uliosomwa na Prof. Davis George Mwamfupe umeeleza kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kimeamua kumtunuku Shahada ya Heshima ya Udaktari wa Falsafa Mhe. Rais Magufuli kwa kutambua mchango wake mkubwa katika maendeleo ya Tanzania kwa kipindi kifupi cha miaka 4 ya uongozi wake kwenye sekta za elimu, nishati, miundombinu, uchukuzi, maji, mawasiliano, maliasili, utalii, afya, madini na kilimo.
UDOM imeeleza kuwa kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mhe. Rais Magufuli katika kutekeleza Dira ya Maendeleo ya 2025 inayoelekeza Tanzania kuingia katika uchumi wa kati imefanywa kwa mafanikio makubwa na imetaja baadhi ya maeneo ya mafanikio kuwa ni utoaji wa elimu bila malipo kwa shule za msingi na sekondari, kujenga miundombinu na kuongeza mikopo ya wanafunzi wa vyuo vikuu, kuongeza uzalishaji wa nishati ya umeme na kuanza ujenzi wa Bwawa la Nyerere, kujenga barabara, reli ya kisasa (SGR), bandari na viwanja vya ndege.
Maeneo mengine ni kuongeza upatikanaji wa maji ambapo hadi Februari 2019 miradi 65 ya maji iliyowanufaisha Watanzania Milioni 25.36 imetekelezwa, kuunganisha Zanzibar na mkongo wa Taifa na kuweka mfumo wa kusimamia mawasiliano (TTMS), kununua ndege 11 kwa ajili ya kuimarisha usafiri wa anga na kukuza utalii, kudhibiti ujangili, kuboresha sekta ya afya (kwa kujenga hospitali 69, vituo vya 352, kuongeza bajeti ya dawa kutoka Shilingi Bilioni 31 hadi Bilioni 270 na kununua vifaa tiba), kusimama na kuongeza mapato ya madini na kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula hali iliyoweza kuwepo chakula cha kutosha na cha ziada.
Akizungumza baada ya kutunukiwa shahada hiyo, Mhe. Rais Magufuli amekishukuru Chuo Kikuu cha Dodoma kwa kumtunuku shahada hiyo na amebainisha kuwa awali haikuwa rahisi kwake kukubali kutunukiwa shahada ya Udaktari wa Falsafa pasipo kuisomea darasani, lakini baadaye alikubali kwa kuwa anaamini shahada hiyo imetolewa kwa kutambua kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wake.
“Kutokana na maisha niliyokulia sikuwahi kuzoea vitu vya burebure (dezo), na hapa dunia nimejifunza kuwa hakuna kitu cha bure, hata hivyo nimetambua kuwa shahada hii imetolewa kwa kutambua mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano kwa miaka 4, hivyo hii ni heshima kwa Watanzania wote, wafanyakazi, wakulima, wafugaji na wavuvi hasa wanaolipa kodi” amesema Mhe. Rais Magufuli.
Mhe. Rais Magufuli amewashukuru viongozi wote nchini, Chama Cha Mapinduzi (CCM), vyombo vya Ulinzi na Usalama, viongozi wa Dini, viongozi wa Siasa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano wao mkubwa katika kuhakikisha nchi inakua na amani na utulivu, na miradi ya maendeleo inatakelezwa kwa mafanikio makubwa.
Pamoja na kueleza mafanikio yaliyopatikana katika maeneo mbalimbali ambayo Serikali ya Awamu ya Tano imetilia mkazo, Mhe. Rais Magufuli amewataka Watanzania wote kuendelea kushikamana katika kujenga nchi na kutokubali kuyumbishwa na changamoto za mabeberu na vibaraka wao waliopo ndani ya nchi, ambao wamekuwa wakitumika kukwamisha juhudi za Serikali katika maendeleo na safari ya kuufikia uchumi wa kati ifakapo mwaka 2025.
Amewapongeza wahitimu wa UDOM wa mwaka huu na ametoa wito kwa wasomi hapa nchini kuendelea kufanya tafiti mbalimbali zinazojielekeza kutatua changamoto za Watanzania, na kwamba tafiti hizo zisiwe tegemezi kwa watu wa nje ambao ndio huchagua ajenda za utafiti huku akibainisha kuwa Serikali itaendelea kuchangia mfuko wa utafiti.

Kesho tarehe 22 Novemba, 2019 Mhe. Rais Magufuli ataweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Uhuru katika eneo la Maduka Chamwino, ataweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa nyumba 118 za askari polisi katika eneo la Nzuguni, ataweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi cha Dodoma katika eneo la Nzuguni, ataweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa Soko Kuu la Dodoma katika eneo la Nzuguni na kisha atazungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara.
Posted by MROKI On Thursday, November 21, 2019 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo