Nafasi Ya Matangazo

July 08, 2017





Muonekano wa Daraja la Kavuu lenye urefu wa Mita 89 linalounganisha Halmashauri ya  Wilaya ya Mlele na Halmashauri ya Wilaya ya Mpwimbwe Mkoani Katavi ambalo ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 99.

 Meneja Wa Wakala Wa Barabara nchini (TANROADS), Eng. Abdon Maregesi (kulia), akitoa maelezo kwa Naibu Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani (Katikati) juu ya hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa Daraja la Kivuu wakati Naibu Waziri huyo alipokagua, Mkoani Katavi.
Naibu Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani (Wa kwanza kushoto), akikagua ujenzi wa Nyumba za viongozi zinazojengwa na Wakala Wa Majengo nchini (TBA) Mkoani Katavi, Kulia kwake ni Mkuu wa Wilaya ya Mlele Bi. Rachel Kassanda.



Naibu Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akiongea na wananchi wa kata ya MajiMoto Wilaya ya Mlele Mkoani Katavi mara baada ya kukagua Daraja la Kavuu ambalo ujenzi wake umekamilika na linatarajiwa kuanza kutumika mwishoni mwa mwezi huu. BOFYA HAPA KWA PICHA ZAIDI.


 Naibu Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akisalimiana na wakazi wa kata ya MajiMoto Wilaya ya Mlele Mkoani Katavi mara baada ya kuongea nao.

Naibu Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani (Kulia) akiongea na Mbunge wa Jimbo la Manyoni Magharibi, Omary Yahya Massare (Kulia), Wakati Waziri Ngonyani alipotembelea Jimboni kwake mwishoni mwa wiki.
******************
Ujenzi wa Daraja la Kavuu lenye urefu wa Mita 89 linalounganisha Halmashauri ya  Wilaya ya Mlele na Halmashauri ya Wilaya ya Mpwimbwe Mkoani Katavi ujenzi wake umekamilika na litaanza kutumika ifikapo mwishoni mwa mwezi Julai mwaka huu.

Akizungumza mara baada ya kukagua ujenzi wa Daraja hilo Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani amesema kukamilika kwa ujenzi huo kutarahisisha usafirishaji wa abiria na  Mizigo kutoka Mkoa wa katavi kwenda mikoa ya jirani.

“Serikali iliona kero kubwa wanazozipata wananchi wa mkoa huu hasa kwenye usafirishaji wa abiria na mizigo kwenye kipindi cha mavuno, hivyo baada ya kukamilisha Daraja hili wananchi wataweza kupita vipindi vyote vya Mwaka,” alisema Naibu Waziri Eng. Ngonyani.
Aidha, Eng. Ngonyani amemuagiza Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), Mkoa wa Katavi Eng. Abdon Maregesi Kuhakikisha Mzani unaohamishika unawekwa ili kudhibiti magari yatakayozidisha Tani 36.

Kwa upande wake Meneja wa Wakala wa Barabara Mkoa wa Katavi Eng. Abdon Maregesi amemuhakikisha Naibu Waziri, Eng. Ngonyani kuwa wakala utaweka mzani huo ili kutoruhusu magari yaliyozidisha Uzito wa Mzigo kupita kwenye Daraja hilo.

Wakati huo huo, Naibu Waziri Eng. Ngonyani amekagua ujenzi wa Nyumba za Viongozi Mkoani humo na kuuagiza Wakala wa Majengo nchini (TBA), kuhakikisha  ujenzi wa nyumba hizo unakamilika ifikapo Novemba mwaka huu.

“Serikali imeshatoa fedha za kukamilisha ujenzi wa nyumba hizi, ujenzi huu ulisimama kwa takribani miezi minne kwa sasa hakuna sababu ya ujenzi kusuasua wakati fedha zipo, ninakuhakikishia Mkuu wa Wilaya nyumba hizi zitakamilika kwa wakati ili zianze kutumika,” alisisitiza Naibu Waziri Eng. Ngonyani.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Eng. Nyonyani amekagua ujenzi wa Barabara ya Sitalike-Mpanda yenye urefu wa kilomita 36.9 ambao ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 99, barabara hii ni sehemu ya barabara kuu inayoanzia Tunduma kupitia Sumbawanga, Mpanda, Uvinza, Kibondo, Nyakanazazi hadi Mutukula. 

Naibu Waziri Eng. Ngonyani yupo katika Ziara ya kukagua Miundombinu ya barabara, Viwanja vya Ndege, Ujenzi wa Nyumba za viongozi na Madaraja katika Mkoa wa Katavi.
Posted by MROKI On Saturday, July 08, 2017 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo