Nafasi Ya Matangazo

February 25, 2016

Wafanyakazi wa Kampuni ya TARMAL ya jijini Dar es Salaam inayofanya kazi za PSI katika ghala lake la kuhifadhia dawa na vifaa mbalimbali kama Condomu za kike na kiume wakiimba wakiwa na mabango wakimtaka Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kusimama na kusikiliza kilio chao. Baadae Waziri Mkuu alisimama na kuwasikiliza. 
KUNDI la watumishi wa kampuni ya TARMAL inayofanya kazi katika ghala la PSI katika bohari ya vifaa tiba lililopo Ubungo jijini Dar es Salaam leo waliuzuia msafara wa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa dakika kadhaa ili wampe kilio chao. Mwandishi wa Father Kidevu Blog anaandika zaidi.

Watumishi hao wengi wao wakiwa ni wanawake walipaza sauti zao wakati Waziri Mkuu akipita alipokuwa akitokea Bohari ya  Dawa (MSD) katika Ghala la vifaa tiba kupokea msaada wa vifaa tiba vyenye thamani ya Sh Bilioni 10 kutoka kampuni za Uzalishaji vinywaji Baridi nchini vya Coca Cola, Pepsi na Azam.

Waziri Mkuu Majaliwa baada ya kuona kundi hilo la watumishi aliamua kuteremka katika gari na kuzungumza kidogo na wasaidizi wake kasha kuwasalimu watanzania hao na kupokea kilio chao kilicho wasilishwa kwake na kiongozi wao Amin Athumani.

Athumani alisema kubwa linalowaumiza ni wao kudumu kama vibarua kwazaidi ya miaka saba, huku wakipewa ujira wa sh 5,550/= kwa siku sawa na Sh 27,500 kwa wiki au 110,000 kwa mwezi.

Kilio kingine ni kukosa huduma za afya pindi wanapoumwa, kutopelekewa makato ya PPF au NSSF, kukosa ajira na kupewa mikataba ya ajira ambayo haina kikomo na ambayo haina maslahi yoyote ili mradi kuzidanganya mamlaka za serikali.

Aidha kilio kingine ni kukosa malipo pindi mama akiwa katika likizo ya uzazi, manyanyaso ya mwajiri wao TARMAL, pamoja na malipo hayo ya 5,500 ambayo wakati mwingine hulipwa pungufu.

“Tunakuomba  Waziri Mkuu, Serikali yako imeonesha nia ya dhati kuwasaidia wanyonge, kwahiyo maombi yetu tunakuomba walau mshahara wetu uwe sh 10,000 kwa siku na tulipwe kwa mwezi,”alisema Athumani kwa niaba ya wenzake.

Baada ya kusikia kilio chao hicho kutoka kwa wafanya kazi hao katika ghala la PSI na kazi yao kubwa ni kupaki bidhaa mbalimbali za PSI Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aliwasihi kuendelea na kazi lakini kesho Ijumaa, February 26,mwaka huu majira ya Saa 2:00 asubuhi Waziri mwenye dhamana ya Kazi atafika na kuzungumza nao.

Waziri Mkuu aliwaeleza haya katika kujibu hoja zao …”Nimeyasikia malalamiko yenu na tunakutana leo kwa mara ya kwanza, lakini serikali hii inasimamia pale pote ambapo pana matatizo na wizara yangu ndio inahusika na mambo ya ajira, kazi na maeneo yote yale yanayohitaji kutatuliwa matatizo haya, na mimi nina waziri anaeshughulikia jambo hilo mheshimiwa Jenista Mhagama.

Nawasihi wote kesho mje kazini asubuhi, Saa mbili mama Jenista Mhagama atakuwa hapa,… kwakua mmelalamikia hata makato ya PPF hayakatwi atakuja na Mtendaji wa PPF hapa ili aje amthibitishie mheshimiwa Mhagama kwamba hakuna makato yanakuja kwake, kwahiyo na wasihi sana Yule kiongozi ayaandike vizuri yale matatizo ili kesho akija ayasome vizuri, ayasikie na atazungumza na Management kesho hiyo hiyo na utatuzi utaoata njia kesho hiyo hiyo.

Kwahiyo na wasihi sasa kwakua jambo lenu mmeliwasilisha kwa mara ya kwanza, wala msigomee kazi mmesha yaleta serikalini, Waziri mwenye dhamana anakuja atawasikiliza na atashughulikia kikamilifu na atawapa ufumbuzi naomba mniruhusu nipite!,” alimaliza kuzungumza na kuingia katika gari na kuondoka katika eneo hilo.


Wafanyakazi hao wa kampuni ya TARMAL walibaki wakiimba na kufurahi huku kesho wakimsubiri kwa hamu  Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Jenista Mhagama akiambatana na  Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Pensheni wa PPF, William Erio kwenda kuwasikiliza kama Waziri Mkuu alivyo elekeza.
Posted by MROKI On Thursday, February 25, 2016 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo