Nafasi Ya Matangazo

January 03, 2016

Dereva Tukae Ngonyani akiwa kwenye usukani kwenye moja ya lori la kusambaza vinywaji analoliendesha 
Dereva Tukae Ngonyani akiwa amesimama katika moja ya lori la kusambaza vinywaji analoliendesha
Dereva Tukai Ngonyani akishuka kwenye Folk Lift anayoendesha baada ya kuchapa kazi
.  Dereva Tukae Ngonyani akiendesha  Folk Lift  katika kiwanda cha TBL kilichopo Ilala jijini Dar es Salaam
********
  • Atoa ushauri kwa wanawake wenzake kuzingatia  falsafa ya ‘Hapa Kazi’

“Wanawake wa Tanzania tunakabiliwa na changamoto mbalimbali kutokana na kukandamizwa na mfumo dume kwa muda mrefu. Moja ya changamoto kubwa ni  kuachwa nje ya mfumo wa ajira rasmi na  zisizo rasmi”.Anasema Tukae Ngonyani ambaye ni dereva wa magari makubwa ya kusambaza vinywaji ya kampuni ya Tanzania Breweries Limited katika kiwanda cha Ilala jijini Dar es Salaam.

Pamoja na ukosefu wa ajira kuwa moja ya changamoto kubwa inayowakabili wanawake ,Tukae anasema kuwa wanawake wengi nao wana tatizo la kushindwa kujiamini na kuwa na kasumba ya kuchagua kazi na kudhani kuwa baadhi ya kazi ni kwa ajili ya wanaume tu wakati hakuna kitu kama hicho.

“Inafurahisha hivi sasa akina mama wameweza kuwa na mwamko wa kufanya kazi mbalimbali zinazofanywa kwa wingi na wanaume,hata hivyo bado idadi yao ni asilimia ndogo na kuna haja ya kujitokeza  zaidi ili kupunguza idadi kubwa ya wanawake wasio na kazi.”Anasema. SOMA ZAIDI BOFYA HAPA

  Akielezea historia  yake ya kazi alisema kuwa tangu alipokuwa na umri mdogo alikuwa anatamani kufanya kazi za ufundi na alipomaliza elimu yake ya msingi alijifunza ufundi umeme wa majumbani.

“Nilijifunza ufundi wa umeme wa majumbani nikawa nafanya wiring na kazi nyinginezo za ufundi wa umeme kwenye nyumba mbalimbali mitaani nikiwa na mafundi wa kiume kwa kuwa kwenye fani ya ufundi pia akina mama ni wachache.”Anasema.

Tukae alisema kuwa mnamo mwaka 1987 aliomba kazi ya ufundi umeme katika kampuni ya Tanzania Breweries Limited (TBL) kwa bahati  mbaya hakufanikiwa kuipata  badala yake alipata kazi ya kuwa Mhudumu wa ofisini (Messenger) ambapo  hata hivyo hakusita kuifanya kazi hiyo.

“Nikiwa nafanya kazi ya uhudumu nilivutiwa na jinsi nilivyokuwa nikiwaona wanaume wakiendesha vifaa mbalimbali vinavyosaidia katika uzalishaji kiwandani na nilipomueleza bosi wangu kuwa nilitaka kujifunza kuendesha magari madogo ya kupakia na kushusha mizigo (Fork Lifts) hakunikatisha tamaa bali nilipatiwa fursa hiyo na kupatiwa mafunzo ya ndani na baada ya muda mfupi nikamudu kazi hiyo na kufanikiwa kubadilisha kazi kutoka kuwa mhudumu wa ofisi hadi kuwa dereva wa Folk Lifts”.

Anasema baada ya kuendesha magari hayo kwa kipindi cha miaka mitano ndani ya kiwanda alitamani  kujifunza udereva wa magari makubwa baada ya kuvutiwa na madereva aliokuwa akiwaona kiwandani hapo na barabarani wakiwa wanaendesha magari makubwa ya mizigo.

“Nashukuru mume wangu aliyenitia moyo wa kufanikisha ndoto yangu ambaye pia anafanya kazi ya udereva bila kusahau mabosi wangu wa TBL  kwa kuniwezesha kuhudhuria kozi ya udereva katika chuo cha VETA kilichopo jijini Dar es Salaam na kufanikiwa kufuzu vizuri kozi ya udereva wa magari makubwa na kupata leseni inayostahili kwa kazi hiyo”

Kuhusu changamoto anazokabiliana nazo katika kazi yake alisema zipo changamoto za kawaida kama zilizopo kwenye kazi nyingine . “Naipenda kazi yangu na nafurahi kuona watu wengi kwenye jamii wakifurahi na kunipongeza wanapoona naendesha lori kubwa la mizigo na hii inatokana na sababu kuwa wamezoea kuona kazi hizi zikifanywa na wanaume pekee”.

Tukae ambaye ni mama mwenye mume, watoto na wajukuu anasema kuwa anafurahi kufanya kazi katika kampuni kubwa ya TBL kwa kuwa ina mifumo mizuri ya ajira yenye maslahi mazuri ikiwemo taratibu za kuwapatia mafunzo ya mara kwa mara wafanyakazi wake  na anakiri kuwa ajira yake imemwezesha kupata mafanikio kimaisha.

 Kuhusu mipago yake ya baadaye alisema kwa sasa hana mpango wa kubadilisha kazi na alimalizia kwa kuwataka akina mama wajitokeze na kujiamini kufanya kazi zote bila kuchagua kwa kuwa hakuna kazi kwa ajili ya wanaume peke yao au wanawake peke yao.


“Akina mama tuzingatie kauli mbiu ya Rais wetu wa Tanzania Mh.John Magufuli isemayo ‘Hapa Kazi tu’ tufanye kazi na kuacha kuwa wategemezi tutafanikiwa”.Alisisitiza.
Posted by MROKI On Sunday, January 03, 2016 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo