Nafasi Ya Matangazo

October 07, 2014

SURUA na rubella ni magonjwa hatari yanayoenezwa haraka kwa njia ya hewa, kutoka kwa mtu mwenye vimelea vya ugonjwa huo kwenda kwa mwingine.

Wataalamu wa afya wanaeleza kuwa dalili za magonjwa haya mawili zinafanana, hivyo ni vigumu kutofautisha. Wataalamu hao wanasema dalili kuu ni homa na vipele vidogovidogo.

Chanjo ya surua-rubella hutoa kinga kamili dhidi ya magonjwa haya. Dozi ya kwanza hutolewa kwa mtoto anapofikia umri wa miezi 9 na dozi ya pili akiwa na mwaka mmoja na nusu (miezi 18).

Serikali kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, imekutana na wadau wake wa masuala ya chanjo jijini Dar es Salaam jana, kuzungumzia mkakati wa kampeni za chanjo ulio na lengo la kuwafikia walengwa wengi zaidi ili kuongeza idadi ya watu wenye kinga dhidi ya magonjwa ya surua na rubella.

Akizungumza katika mkutano huo wa wadau wa chanjo, Meneja Mpango wa Chanjo wa Taifa, Dk Dafrossa Lyimo, alisema kampeni hii itajumuisha watoto wenye umri wa miezi tisa hadi chini ya miaka 15.

Dk Lyimo alitoa mwito kwa wadau wote kushiriki kikamilifu katika kampeni hii nchini kote, kwa kujitokeza na kuwapeleka watoto wetu katika chanjo kwa tarehe ambazo zimepangwa.

Kampeni hiyo imepangwa kufanyika kuanzia Oktoba 18 hadi 24 mwaka huu katika vituo mbalimbali vya afya nchini ambavyo hutoa huduma ya chanjo.

Mimi kama mzazi kwanza napenda kuwasihi sana wazazi wenzangu tuwapeleke watoto wetu kupata chanjo hii maana mara kwa mara tumekuwa tukiwapa tiba watoto wetu ya surua kumbe kinachowasibu si surua ni rubella na matokeo yake ni madhara makubwa.

Ugonjwa wa rubella kwa watoto huja na dalili za vipele vidogo vidogo, homa, macho kuwa mekundu, uchovu wa mwili, vidonda kooni na uvimbe wa matezi na mafua.

Wataalamu wanasema madhara ya ugonjwa huu ukimpata mama mjamzito, unaweza kusababisha kuharibika kwa mimba, kuzaa mtoto njiti, au mfu. Pia mtoto akizaliwa anaweza kupata madhara kama mtoto wa jicho, matatizo ya moyo, kutokusikia vizuri, mtindio wa ubongo, kuvimba kwa ini na bandama na mengineyo kama ukuaji.

Surua yenyewe husababisha watoto kuzaliwa na upofu, nimonia, utapiamlo, pia kifo kinaweza kutokea endapo mgonjwa hatapata matibabu mapema.

Kama mwandishi, pia natumia fursa hii kutumia kalamu yangu kuuelimisha umma juu ya utofauti wa magonjwa haya mawili ambayo baadhi yetu katika jamii tunazotoka tumekuwa tukitumia mitishamba kama kuwaogesha watoto walio na homa kali maji ya mchunga au mwarobaini.

Rubella mara nyingi huwapata watoto wadogo na huenezwa kwa njia ya hewa, lakini watu wazima pia wanaweza kupata.

Shime wazazi na walezi hebu tujitokeze na tusaidiane kwa pamoja kueneza elimu hii juu ya hiyo chanjo inayokuja hapo baadae mwezi huu.

Ni wakati muafaka sasa wa kutokomeza kabisa magonjwa haya katika jamii zetu na hili litawezekana tu pindi tutakapowapeleka watoto wetu katika chanjo hii.

Katika mkutano huo wa wadau ikaelezwa kuwa hata ile chanjo ya vitamin A pamoja na minyoo nazo zitatolewa pamoja na chanjo hii.

Tunahimizwa na wataalamu wa chanjo na afya kwa ujumla kuwa wazazi tuwapeleke watoto wetu kupata dozi mbili za chanjo hii ya surua-rubella akitimiza umri wa miezi tisa na miezi 18.

Aidha, inaelezwa kuwa pasije pakatokea mtu awaye yote akapotosha kuwa chanjo hii ina madhara. Chanjo ya Surua-rubella ni salama na imethibitishwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na Shirika la Afya Duniani (WHO).

Lakini kubwa zaidi ambalo wengi huweza kuhofia kujitokeza kupata chanjo hii wakidhani ina malipo, la hasha chanjo hii haina malipo na itatolewa bure hivyo kila mwananchi aliye na mtoto wa umri huo ajitokeze kumpeleka mtoto wake.

*Porojo hii ya Anko Kidevu pia imetoka katika gazeti la Habarileo Toleo la Oktoba 7,2014 . 
Posted by MROKI On Tuesday, October 07, 2014 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo