Ushirikiano baina ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), umeelezwa kuwa na manufaa mengi yenye mchango wa kukuza maendeleo baina ya nchi hizo mbili.
Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu (MCC), Mary Chatanda, Agosti 18, 2026.
Chatanda amesema, ziara ya siku mbili ya Rais Felix Tshisekedi wa DRC Kongo nchini Tanzania ni kielelezo cha uhusiano mzuri ambao hauishii kuwa urafiki wa kawaida bali nyenzo ya kushirikiana katika kukuza uchumi na maendeleo.
"Rais Dk. Samia na mwenzake Tshisekedi wamekubaliana kushirikiana katika kuboresha sekta za uchukuzi, madini, nishati, uwekezaji, biashara, barabara, bandari, usafiri wa majini, jambo linaloongeza kasi ya ukuaji uchumi," amesema.
Aidha, Chatanda amehimiza uzingatiaji wa maslahi ya wananchi katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa nchi zote.
"Wananchi wetu wanapaswa kunufaika na fursa za uchumi katika sekta za ushirikiano, ili maendeleo yawe jumuishi kwa serikali na wananchi wake," amesisitiza.
Katika hatua nyingine, Chatanda amempongeza Rais Dk. Samia kwa kuendelea kuifungua nchi kwa kuhimiza diplomasia ya kiuchumi kwa kushirikiana na mataifa mbalimbali duniani.
"Nampongeza Rais wetu Dk. Samia kwa namna anavyoshirikiana na mataifa mengine, kwa kufanya hivyo, tunaongeza wigo wa kupata fursa za biashara na uwekezaji," ameongeza.







0 comments:
Post a Comment