Nafasi Ya Matangazo

June 17, 2025




Mradi wa Kuimarisha Ustahimilivu wa Bioanuwai ya Misitu ya Mazingira Asilia dhidi ya Matishio ya Mabadiliko ya Tabianchi, unaotekelezwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), umeendelea kuimarisha miundombinu ya uhifadhi katika Hifadhi ya Pindiro, wilayani Kilwa.
 
Katika ziara ya ukaguzi iliyofanywa na Kamati ya Utekelezaji ya mradi huo, maendeleo ya ujenzi wa majengo muhimu ya hifadhi hiyo yalionekana kufikia asilimia 46. Ujenzi huo unahusisha jengo la utalii, vyoo, jengo la walinzi na geti la kuingilia, kwa gharama ya Sh milioni 297. Mkandarasi anayetekeleza kazi hiyo ni kampuni ya Strider Engineering Ltd, huku mradi ukitarajiwa kukamilika Oktoba 2025.
 
Akizungumza wakati wa ukaguzi huo, Mhandisi Hendry Sanga kutoka kampuni ya Strider Engineering alisema kuwa kazi inaendelea vizuri na kwamba wanazingatia viwango vya ubora pamoja na muda wa utekelezaji kama ilivyokubaliwa.
 
“Tunaendelea na kazi kwa kasi nzuri, tukizingatia viwango vilivyokubaliwa. Lengo ni kuhakikisha tunakamilisha mradi kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa,” alisema Sanga.
 
Naye Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi kutoka TFS, Bw. Fridolin Matembo, alieleza kuridhishwa na mwenendo wa utekelezaji wa mradi huo.
 
“Mkandarasi anafanya kazi nzuri. Kasi ya utekelezaji ni ya kuridhisha, lakini tunasisitiza umuhimu wa kukamilika kwa wakati na kwa ubora wa hali ya juu,” alisema Matembo.
 
Katika hatua nyingine, hifadhi ya Pindiro imekabidhiwa pikipiki mbili mpya kwa ajili ya kusaidia kazi za uhifadhi. Vifaa hivyo ni sehemu ya mchango wa UNDP ulioainishwa wakati wa uzinduzi rasmi wa mradi huo katika Hifadhi ya Kazimzumbwi, mkoani Pwani.
 
Akikabidhi vifaa hivyo, Mratibu wa Mradi, Bw. Mteleka Someni Lusugu alisema:
 
“Pikipiki hizi ni sehemu ya vifaa muhimu tulivyopokea kupitia UNDP. Zitatumika kuongeza ufanisi katika shughuli za uhifadhi, hasa maeneo yenye changamoto za miundombinu ya usafiri,” alisema Lusugu.
 
Mradi wa Bioanuwai unatekelezwa kwa kipindi cha miaka sita katika maeneo mbalimbali ya misitu ya asili nchini. Lengo kuu ni kuimarisha usimamizi wa rasilimali misitu, kuongeza ustahimilivu wa jamii dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi, pamoja na kuboresha miundombinu na huduma za uhifadhi kwa maendeleo endelevu ya wananchi na taifa kwa ujumla.

Posted by MROKI On Tuesday, June 17, 2025 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo