Nafasi Ya Matangazo

April 23, 2025

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisaini Tamko la kuzindua Toleo la Sheria za Tanzania zilizofanyiwa urekebu la mwaka 2023 kwa mujibu wa kifungu cha 12 cha Sheria ya urekebu wa sheria, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 23 Aprili, 2025. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisaini nakala 3 za Sheria za Tanzania zilizofanyiwa urekebu kwa mujibu wa kifungu cha 17 cha Sheria ya urekebu wa sheria, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 23 Aprili, 2025. 
***************
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kukamilisha zoezi la kutafsiri Sheria za Tanzania kwa lugha ya Kiswahili, ikiwemo Toleo la Sheria za Tanzania la Mwaka 2023.
 
Rais Dkt. Samia ametoa agizo hilo leo wakati wa uzinduzi wa Toleo la Sheria za Tanzania zilizofanyiwa Urekebu la Mwaka 2023 katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino.
 
Aidha, Rais Dkt. Samia ameelekeza uwekwe utaratibu utakaowezesha kupatikana kwa nakala za Toleo la Sheria zilizofanyiwa Urekebu la Mwaka 2023 ikiwemo kutumia TEHAMA ili wananchi wazipate kwa urahisi kwenye mitandao kwa minajili ya kujifunza na  kuzijua haki zao.
 
Sheria ni kioo cha ustaarabu wa Taifa, bila sheria zilizowekwa wazi haki haiwezi kupatikana, bila sheria kuwa wazi uhakika wa ulinzi wa haki ya raia unatoweka na kusababisha uvunjifu wa amani na shughuli za kiuchumi zinafanyika kwa mashaka,” amesema Rais Dkt. Samia.
 
Rais Dkt. Samia amebainisha kuwa kutokuwepo kwa Juzuu za Sheria zilizorekebishwa kwa wakati huchangia kunyima haki za raia, kwa sababu wanaotumia kutolea maamuzi hawana uelewa wa uwepo wa sheria mpya. Hivyo, kukamilika kwa Toleo la Sheria zilizofanyiwa Urekebu litarahisisha upatikanaji wa haki kwa wananchi kwa kuwa Sheria zote kuu 446 zimehuishwa, zinapatikana kwa pamoja na kwa urahisi na zimepangwa vizuri.  
 
Vilevile, Rais Dkt. Samia ameeleza kuwa upatikanaji wa Toleo lililozinduliwa utasaidia kupunguza muda wa Mahakama kufanya utafiti kabla ya kufanya maamuzi, kuongeza uwazi na kuwajengea wananchi imani kwa Serikali, kupunguza matumizi mabaya ya madaraka kwa kuziba ombwe la kisheria linalochochea mianya ya rushwa, kuimarisha utawala wa sheria na kuongeza hadhi ya nchi kiuchumi, kisiasa na kijamii.
 
Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia ameagiza zoezi la Urekebu wa Sheria lifanyike kila baada ya miaka 10 badala ya sasa ambapo limefanyika baada ya miaka 20 tangu zoezi kama hilo kufanyika miaka 23 iliyopita mnamo mwaka 2002. 
 
Pamoja na hayo, Rais Dkt. Samia amebainisha kuwa mbali ya kusubiri zoezi hilo la miaka 10, kila mara Sheria zinaporekebishwa, marekebisho hayo yajumuishwe kila mwaka na yapatikane kwa urahisi kwa kutumia TEHAMA.
 
Uzinduzi wa Toleo la Sheria za Tanzania zilizofanyiwa Urekebu la Mwaka 2023 unadhihirisha dhamira ya dhati ya Serikali kujenga Taifa linalosimamia utawala wa sheria kwa kuwa na sheria zilizowekwa wazi, zilizo sahihi na zinazoeleweka.



Matukio mbalimbali wakati wa uzinduzi wa toleo la Sheria za Tanzania zilizofanyiwa urekebu la mwaka 2023, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 23 Aprili, 2025.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia viongozi pamoja na wageni mbalimbali mara baada ya toleo la Sheria za Tanzania zilizofanyiwa urekebu la mwaka 2023, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 23 Aprili, 2025.




Matukio mbalimbali wakati wa uzinduzi wa toleo la Sheria za Tanzania zilizofanyiwa urekebu la mwaka 2023, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 23 Aprili, 2025.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Profesa Ibrahim Hamis Juma pamoja na Mwakilishi wa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Joseph Kizito Mhagama mara baada ya kuwakabidhi nakala 3 za Sheria za Tanzania zilizofanyiwa urekebu kwa mujibu wa kifungu cha 17 cha Sheria ya urekebu wa sheria kwa ajili ya kumbukumbu, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 23 Aprili, 2025.


Posted by MROKI On Wednesday, April 23, 2025 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo