Nafasi Ya Matangazo

October 26, 2024


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema kuwa mapambano dhidi ya rushwa si jukumu la TAKUKURU pekee bali kila Mtanzania anapaswa kushiriki kikamilifu kusimamia maadili na kupinga vitendo vya rushwa.
 
Amesema kuwa rushwa inaweza kusababisha kutofikiwa kwa jukumu la Serikali la kuleta ustawi wa wananchi linalotamkwa katika Ibara ya 8(1)[b] ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 
Amesema hayo leo (Jumamosi, Oktoba 26, 2024) alipomwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika hafla ya ufungaji wa mafunzo ya awali ya uchunguzi ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini (TAKUKURU), yaliyofanyika kwenye Shule ya Polisi Tanzania, Moshi mkoani Kilimanjaro.
 
“hili ni jukumu la kila Mtanzania na wadau wote muhimu hapa nchini, rushwa ni adui wa haki na maendeleo katika jamii, Vitendo vya rushwa rushwa vinasababisha uchepushaji wa rasilimali kutoka kwenye matumizi sahihi na kuathiri haki za kiraia. Katika utumishi wa umma, rushwa inavuruga ushindani wenye usawa na inaathiri rasilimaliwatu ya nchi”
 
Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Rais Dkt. Samia anawategemea watumishi wa TAKUKURU katika mapambano dhidi ya rushwa nchini na kuhakikisha wanaimaliza kabisa vitendo vyote vya rushwa “Ameniambia niwaambie kuwa hatawaangusha kamwe” 
 
Amesema kuwa rushwa ni changamoto ya kidunia ambayo kwa nchi zinazoendelea linachochewa na umaskini uliokithiri, ujinga na mmomonyoko wa maadili. “Rushwa ni changamoto inayotokana na kuahidi, kutoa, kupokea au kushawishi moja kwa moja au kupitia wakala, Sisi kama Taifa eneo hili lazima tulisimamie”
 
Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amewaeleza wahitimu hao kuwa wanapaswa kwenda mpaka vijijini kuelimisha umma kuhusu athari za rushwa  “Kamanda wa TAKUKURU unapaswa kulisisitiza hili, badala ya kukuta watumishi wapo ofisini kuanzia asubuhi mpaka jioni, tunatarajia mpite huko muone na muwasisitize waende field”
 
Pia, Mheshimiwa Majaliwa ameagiza TAKUKURU iongeze kasi na mikakati ya kudhibiti rushwa hasa katika maeneo ya ukusanyaji mapato, manunuzi wa umma, michakato ya ajira katika utumishi wa umma, mifumo ya ugawaji wa ardhi, utoaji wa huduma za jamii. “Pia Endeleeni kuongoza ufuatiliaji na usimamizi wa karibu wa fedha zinazotolewa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo”.
 
Kwa Upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mheshimiwa George Simbachawene amemshukuru Rais Dkt. Samia kwa uwekezaji mkubwa alioufanya ikiwemo ununuzi wa magari, ujenzi wa majengo katika ofisi za TAKURURU wilaya na mikoa ajira za maafisa uchunguzi ambao wataongeza nguvu katika mapambano dhidi ya rushwa nchini.
 
“Kazi kubwa aliyoifanya Rais Dkt. Samia inatufanya tukose kisingizio, ni  lazima tulipe dhamani ya uwekezaji huu katika kupambana na rushwa usiku na mchana kwa vitendo na kuhakikisha rushwa hailitafuni  Taifa, Mimi na Wenzangu Wizarani tutahakikisha uwekezaji huu unaleta tija katika mapambano dhidi ya Rushwa nchini”
 
Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Crispin Chalamila amemweleza Waziri Mkuu kuwa katika kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan madarakani, TAKUKURU imepatiwa jumla ya Shilingi bilioni 30 za kununulia magari 195 ambapo 88 yameshanunuliwa.
 
“Magari haya mapya 10 uliyokabidhi ikiwa ni ishara ya kukabidhi magari 88 ni sehemu ya magari hayo, Mchakato wa kununua magari 107 yaliyobakia unaendelea na tunatarajia kuyapata hivi karibuni, tunaahidi kutatunza magari haya ili kuongeza tija katika utendaji wetu” Amesema  Bw. Crispin
 
Waziri Mkuu amekabidhi magari hayo wakati anafunga mafunzo ya awali ya uchunguzi ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini (TAKUKURU), hafla inayofanyika kwenye Shule ya Polisi Tanzania, Moshi mkoani Kilimanjaro.
 
Akitoa taarifa kuhusu mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu TAKUKURU Bw. Ayoub Akida amesema kuwa jumla ya washiriki waliohitimu mafunzo hayo ni 436, ambapo wanawake ni 175 na wanaume 261. “Washiriki hawa wamegawanyika katika makundi mawili ambapo kundi la kwanza ni la Maafisa Uchunguzi 323, wanaume wakiwa ni 182 na wanawake 141, na kundi la pili ni la Wachunguzi Wasaidizi 113, wanaume wakiwa ni 79 na wanawake ni 34”
 
Ameongeza kuwa Lengo la mafunzo hayo ni kuwaandaa wahitimu hao ambao ni waajiriwa wapya wa TAKUKURU, kutekeleza majukumu ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa.








Posted by MROKI On Saturday, October 26, 2024 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo