Nafasi Ya Matangazo

June 14, 2023

Mkurugugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Ramadhan Kailima, akizungumza jijini Dodoma leo Juni 14,2023 wakati akitangaza taarifa ya uchaguzi mdogo wa Udiwani katika Kata 14 za Tanzania bara. 
*************
Na Mwandishi Maalum, Dodoma
Tume ya Taifa ya Uchaguzi imetangaza Uchaguzi Mdogo wa Udiwani katika Kata 14 za Tanzania Bara utakaofanyika tarehe 13 Julai mwaka 2023.
 
Akitangaza Uchaguzi huo mdogo jijini Dodoma leo, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Ramadhani Kailima amesema uchaguzi huo unafanyika baada ya kupokea taarifa kutoka kwa waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa.
 
Amefafanua kuwa Waziri ametoa taarifa hiyo kwa kuzingatia matakwa ya Kifungu cha 13(1) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292.
 
“Kutokana na taarifa hiyo, Tume kwa kuzingatia matakwa ya kifungu cha 13(3) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292, inatoa taarifa kwa Umma kuhusu uwepo wa uchaguzi mdogo wa  adiwanikatika kata 14 za Tanzania Bara”alisema Kailima.
 
Kailima amezitaja kata hizo kuwa ni Kata ya Ngoywa iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, Kata ya Kalola iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Uyui zote za Mkoani Tabora na Kata Sindeni Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Kata ya Potwe Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Kata ya Kwashemshi Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe na Kata ya Bosha Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga zote za Mkoa wa Tanga.
 
Kata zingine ni Kata ya Mahege katika Halmashauri ya Kibiti mkoa wa Pwani, Kata ya Bunamhala katika Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu, Kata ya Njoro na Kalemawe katika Halmashauri ya Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro, Kata ya Mnavira katika Halmashauri ya Wilaya ya Masasi mkoa wa Mtwara, Kataya Kinyika katika Halmashauri ya Wilaya ya mkoa wa Njombe.
 
Kailima ametaja Kata zingine zitakazo fanya uchaguzi ni Kata ya Magubike katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro na Kata ya Mbede katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe ya mkoa wa Katavi.
 
Amesema ratiba ya uchaguzi huo itaanza na utoaji wa fomu za uchaguzi kwa wagombea kuanzia tarehe 24 hadi 30 Juni , 2023 huku uteuzi wa wagombea watakao wania nafasi hizo ukifanyika Juni 30  mwaka huu.
 
Kailima amesema vyama vitakavyopata uteuzi vitaanza kampeni za Uchaguzi tarehe 01 hadi 12 Julai na siku ya kupiga kura itakuwa tarehe 13 Julai mwaka 2023.
 
“Tume inatumia nafasi hii kuvikumbusha vyama vya siasa, wagombea na wadau wote wa uchaguzi  uzingatia Sheria, Kanuni, Maadili ya Uchaguzi, Taratibu, Miongozo na maelekezo katika kipindi cha uchaguzi huu mdogo” alisema Kailima.
Posted by MROKI On Wednesday, June 14, 2023 2 comments

2 comments:

  1. AnonymousJune 14, 2023

    NEC endelea kusimamia Sheria, Kanuni na Taratibu kwani ndiyo msingi wa Uchaguzi huru, haki na wa kuaminika

    ReplyDelete
  2. AnonymousJune 14, 2023

    Kura ni haki ya kila raia aliyejiandikisha kuwa mpiga kura, tujitokeze kutimiza wajibu huo.

    ReplyDelete

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo