Nafasi Ya Matangazo

March 31, 2022


Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipata maelezo kutoka kwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Shaka Hamdu Shaka kuhusu matayarisho ya Mkutano Mkuu Maalum wa CCM unaotarajiwa kufanyika kesho alipotembelea ukumbi wa Jakaya Kikwete Jijini Dodoma leo tarehe 31 Machi, 2022.
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipata maelezo kutoka kwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Shaka Hamdu Shaka kuhusu matayarisho ya Mkutano Mkuu Maalum wa CCM unaotarajiwa kufanyika kesho alipotembelea ukumbi wa Jakaya Kikwete Jijini Dodoma leo tarehe 31 Machi, 2022.
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipata maelezo kutoka kwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Shaka Hamdu Shaka kuhusu matayarisho ya Mkutano Mkuu Maalum wa CCM unaotarajiwa kufanyika kesho alipotembelea ukumbi wa Jakaya Kikwete Jijini Dodoma leo tarehe 31 Machi, 2022.
Posted by MROKI On Thursday, March 31, 2022 No comments

March 30, 2022


MAREHEMU BALOZI EMMANUEL OLE NAIKO
24/07/1951 - 30/03/22

Familia ya Emmanuel Ole Naiko inasikitika kutangaza kifo cha BABA YAO, BALOZI EMMANUEL OLE NAIKO kilichotokea leo 30/03/22, nyumbani kwake Bahari Beach, Dar es Salaam. Habari ziwafikie wana familia waliopo Dar es Salaam, Monduli-Arusha na kwengine kote. 

Balozi Ole-Naiko amewahi kushika nyadhifa mbali mbali kwenye serikali ikiwemo Mkurugenzi mkuu wa kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC).

Wakati wa mauti unamfika alikuwa ni balozi wa Heshima wa Botswana.

Mipango ya mazishi inaendelea nyumbani kwake Utulivu Road, Bahari Beach, Dar es salaam.

Bwana ametoa na bwana ametwaa, jina lake lihimidiwe.

2 Timotheo 4; 7
Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda
Posted by MROKI On Wednesday, March 30, 2022 No comments

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea Taarifa ya Taasisi ya TAKUKURU kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo CP Salum Hamduni katika hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino Jijini Dodoma leo tarehe 30 Machi, 2022.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi mbalimbali mara baada ya kupokea Taarifa ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali kwa mwaka 2020/2021 pamoja na Taarifa ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU, katika hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino Jijini Dodoma leo tarehe 30 Machi, 2022.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amewataka Mawaziri, Wabunge na viongozi mbalimbali wa Kisekta nchini kuzungumza na wananchi kuhusu kero zinazowakabili.

Rais Samia aliongea hayo leo Machi 30, Ikulu Chamwino Jijini Dodoma wakati akipokea Ripoti ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali kwa mwaka 2020/2021 kutoka kwa Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na Ripoti ya TAKUKURU.

Rais Samia alisema kwamba kumekuweko na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi kuhusu kupanda kwa bei za bidhaa mbalimbali sokoni hasa mafuta ya kula pamoja na mafuta ya petrol na diseli ambapo ni matokea ya mlipuko wa Ugonjwa wa COVID 19 duniani.

“Wabunge na Viongozi mnaosimamia Sekta waambieni wananchi ukweli waelewe yanayoendelea duniani, vita ya Russia na Ukraine imepandisha sana bei ya mafuta na kupelekea bei ya bidhaa zote kupanda kutokana na gharama za usafiri kupanda”, alisema Rais Samia

 Aliongeza, mlipuko wa ugonjwa wa COVID 19 duniani pia umechochea mfumuko wa bei za bidhaa kwa kuwa bidhaa zote zilizohifadhiwa kwenye maghala zilitumika kwa vile uzalishaji ulisimama kwa kipindi chote ambacho hofu ya COVID 19 ilikuwa juu zaidi.

“Ukiangalia kwenye ukanda wa Afrika Mashariki na kati, Tanzania ndio nchi yenye bei ya chini zaidi ya mafuta ambapo Serikali ilichukua hatua mbalimbali za kupunguza ikiwemo kuondoa tozo lakini bado bei iliendelea kupanda kwenye soko la dunia, viongozi waelezeni haya wanachi waelewe”, aliongeza Rais Samia.

Kuhusu suala la kupanda bei ya mafuta ya kula Rais Samia aliwaagiza viongozi wenye Sekta husika kuchukua hatua stahiki kwa suala hilo ili kuhakikisha wananchi hawakosi bidhaa hiyo sokoni.

“Nawaagiza viongozi waangalie suluhu ya changamoto ya mafuta ya kula, tulisimamisha kuingiza mafuta kutoka nje ili kulinda viwanda vya ndani, lakini hivi sasa viwanda vyote vya ndani vimesimamisha uzalishaji, nataka viongozi wangalie kama tunaweza kuyaruhusu sasa ili wananchi wasikose bidhaa sokoni”.

Kwa upande mwingine Rais Samia alitoa maelekezo kwa taasisi mbalimbali za Serikali ikiwemo Bohari Kuu ya Madawa (MSD) kujichunguza na kujirekebisha ili kuhakikisha majukumu ya kila Sekta yanatekelezwa kwa wakati na kwa weliedi ambapo alisema viongozi wanaohusika na kutoa maamuzi wafanye hivyo bila kupoteza muda.

“Bohari Kuu ya Madawa naitaka ifanyiwe mabadiliko makubwa kuanzia ngazi ya uongozi wa juu mpaka kwenye vitengo vyake ili tuweze kwenda mbele, huko nyuma ilishafika hatua ya kupata tenda kutoka Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), lakini hatua iliyofikiwa sasa hata ndani watu wanalalamika hawapati huduma, kwa vile SADC bado wana imani nasi turekebishe ili twende mbele”, alisema Rais Samia.

Taasisi nyingine zilizoguswa na ripoti hiyo ni pamoja Mfuko wa Barabara Vijijini na Mjini (TARURA), Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Sekta ya  Afya na Maji ambapo Rais Samia aliwataka wabunge kufanyia kazi hoja zote zilizowasilishwa kwenye ripoti hiyo kwa haraka na kutoa majibu kwa wananchi pindi watakapoenda bungeni.

Posted by MROKI On Wednesday, March 30, 2022 No comments

March 27, 2022

Mwenyekiti Kamati ya Kuduma ya Bunge Uwekezaji wa Mitaji ya Umma(PIC), Jerry Slaa akiongozana na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi(Ujenzi), Ludovick Nduhiye, Mtendaji Mkuu wa TANROADS Eng. Rogatus Mativila na Barakaeli Mmari Mhandisi wa Miradi ya BRT wakati kamati hiyo ilipokagua ujenzi wa mradi wa Usafiri wa Haraka wa Mabasi(BRT) Awamu ya Pili Kariakoo-Mbagala leo jijini Dar es Salaam.
Barakaeli Mmari Mhandisi wa Miradi ya BRT akitoa maelezo kwa Mh. Jerry Slaa Mwenyekiti wa  Kamati ya Kudumu ya Bunge Uwekezaji wa Mitaji ya Umma(PIC) katikati  na wajumbe wake,  wa tatu kutoka kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi(Ujenzi), Ludovick Nduhiye na wa pili kutoka kushoto ni Mtendaji Mkuu wa TANROADS Eng. Rogatus Mativila 
Moja ya Daraja linalojengwa eneo la BP ambapo magari yatapita juu na treni itapita chini katika barabara ya Kilwa jijini Dar Es Salaam.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi(Ujenzi), Ludovick Nduhiye akimsikilia mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Temeke Mh. Dorothy Kilave alipokuwa akiuliza swali.
Baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo
Mtendaji Mkuu wa TANROADS Eng. Rogatus Mativila akiwasilisha taarifa ya ujenzi wa mradi huo kwa kamati.
********
Mwenyekiti Kamati ya Kudumu ya Bunge  Uwekezaji wa Mitaji ya Umma(PIC), Jerry Slaa amesema TANROADS imeendelea kufanya kazi kubwa kwa taifa na kusimamia kikamilifu  ujenzi wa miundombinu kwa sababu wamepewa dhamana kubwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Samia Samia Suluhu Hassan kufanya kazi kwa bidii.

Jerry Slaa ameyasema hayo wakati Kamati ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma, ikipokea taarifa ya mradi wa Usafiri wa Haraka wa Mabasi(BRT) Awamu ya Pili, ambao unasuasua kukamilika tofauti na muda wa ukamilishaji wa mradi huo.

Ameitaka TANROARDS kuendelea kumsimamia kwa ukamilifu mkandarasi anayejenga miundombinu ya barabara ya Usafiri wa Haraka Awamu ya Pili kutoka Gerezani hadi Mbagala ili kuhakikisha serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan inatekeleza azma yake ya kufanya kazi kwa kasi kubwa.

Amebainisha kwamba  mradi huo ni muhimu na ndio maana Rais Samia alitoa maagizo ya kutaka mradi kumalizika kwa haraka ili wananchi waweze kunufaika na huduma ya usafiri ya mradi huo, ambao kumalizika kwake utakuwa na faida kubwa.

''TANROADS mnafanya kazi nzuri lakini mwenendo wa makandarasi sio mzuri, mnapaswa kumfuatilia kwa karibu ili amalize mradi huu kwa wakati na kwa ufanisi mkubwa. Kwa kuwa kuchelewa kwake kunasababisha sintofahamu kwa wananchi,'' amesema Jerry Slaa.

Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati hiyo, Augustine Vuma, naye aliitaka TANROADS kuhakikisha wanawasimamia wakandarasi mbalimbali nchini na kuwachukulia hatua wale wanaochelewesha utekelezaji wa miradi mbalimbali.

Katika mradi huo, kazi za ujenzi wa majengo ikiwemo karakana 1, vituo vikuu 2 na vituo mlisho vinne imeshakamilika toka Julai 31, 2021 na sasa sehemu hiyo iko katika muda wa uangalizi wa mwaka mmoja kama mkataba unavyotaka.

TANROADS imeshakaa na mkandarasi na kuzungumza naye, ambaye kuchelewa kwake kulitokana na matatizo ya Uviko-19, hivyo Machi 27, 2023 mradi huo utamalizika.

Wakati huo huo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi(Ujenzi), Ludovick Nduhiye, alisema ushauri wote ulitolewa na Bunge kupitia kwa Kamati hiyo utafanyiwa kazi ikiwemo kuusimamia mradi huo na kumalizika kwa wakati.
Posted by MROKI On Sunday, March 27, 2022 No comments

March 21, 2022

 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea Taarifa ya Kikosi Kazi cha kuratibu Maoni ya Wadau wa Demokrasia ya Vyama vingi vya Siasa kutoka kwa Mwenyekiti wa Kikosi Kazi hicho Profesa Rwekaza Mukandala Ikulu Jijini Dar es Salaam leo tarehe 21 Machi, 2022.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wajumbe wa Kikosi Kazi cha kuratibu Maoni ya Wadau wa Demokrasia ya Vyama vingi vya Siasa mara baada ya kupokea Taarifa yao Ikulu Jijini Dar es Salaam leo tarehe 21 Machi, 2022.
Wajumbe wa Kikosi Kazi cha kuratibu Maoni ya Wadau wa Demokrasia ya Vyama vingi vya Siasa wakimsikiliza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan alipokua akizungumza nao mara baada ya kupokea Taarifa yao Ikulu Jijini Dar es Salaam leo tarehe 21 Machi, 2022.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Kikosi Kazi cha kuratibu Maoni ya Wadau wa Demokrasia ya Vyama vingi vya Siasa mara baada ya kupokea Taarifa yao Ikulu Jijini Dar es Salaam leo tarehe 21 Machi, 2022. 
Posted by MROKI On Monday, March 21, 2022 No comments
Sheha wa Kojani, Hamad Ali Bakari akizungumza wahariri kutoka Jukwaa la Wahariri waliozuru kisiwa cha Kojani hivi karibuni
“Ndiyo tumesikia. Kuna watu wa serikali wamefika hapa. Kuna ofisa hapa anafanya   kuratibu tupo  wavuvi wangapi.
Wanatuambia serikali italeta nyenzo.

Kojani ni kisiwa cha wavuvi. Hatufanyi shughuli nyingine hapa. Ni uvuvi miaka nenda, miaka rudi. Maisha yetu ni samaki, watoto wanasoma shule na tunajitibu kwa mapato ya samaki. Tunasubiri kuona wataleta nini.

Nasikia kuna vyombo vitakuja. Tutaweza kwenda kwenye bahari kubwa. Tunasubiri, wakati wao ukifika tutaambiwa. Tukipata yote hayo kama ambavyo wanasema, patakuwa na mabadiliko makubwa ya maisha ya hapa.

Hapa kama mlivyoona maisha ni pesa. Ukitaka embe, kama ambazo mmekula kule ng’ambo, ni pesa. Kojani hakuna mashamba, kila kitu kinaletwa, utakila kama una pesa. Kama serikali itatufanya tuondokane na uvuvi huu mdogo itakuwa imetusaidia sana”.

Nukuu hizi ni za Sheha wa Kojani,    Hamad Ali Bakari. Kisiwa cha Kojani, kiko pembeni mwa kisiwa kikubwa cha Pemba. Kina Shehia mbili, Kojani anakoongoza Bakari na Mpambani kwa Sheha Omary Ali Omary. 

Bakari  alikuwa akijibu swali kama amepata kusikia/anaujua mpango mkubwa wa Uchumi wa Buluu, wa Rais Dk. Hussein Mwinyi na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, unaolenga  kubadili maisha ya Wazanzibar kwa kuifanya Bahari na mazingira yake kuwa chanzo kikubwa cha mapato ya nchi.

Ni wavuvi kama hawa wa Kojani walioenea katika maeneo mbalimbali ya nchi ambao Dk. Mwinyi na timu yake wamedhamiria kuwafikia na kubadili maisha yao.

Serikali ya Dk. Mwinyi imetenga shilingi bilioni 36.5 zitakazotumika kuwezesha makundi mbalimbali ndani ya jamii kushiriki katika mpango mzima wa Uchumi wa Buluu.

Na kwa wavuvi kama Sheha huyu, yaani wale wavuvi wadogowadogo wapatao 5,770, watapatiwa maboti yapatayo 577 na nyenzo mbalimbali za uvuvi ili kuwawezesha badala ya kuvua kilo chache tu za samaki kama walivyozowea, wakipata vyombo sasa waende kwenye kina kikubwa zaidi cha bahari  na wavue samaki kwa tani na tani.

Anasema Dk. Mwinyi kwamba wamekusudia kuitumia Bahari kujenga Uchumi wa Buluu ulio endelevu kuwafanya wavuvi na makundi mengine kama ya Wanawake kushiriki katikia kujiletea maendeleo.

“Badala ya mvuvi kupata kilo mbili kwa sababu hawezi kufika kwenye kina kirefu, sasa awezeshwe kwanza kwenda kwenye kina kirefu cha bahari na awe na nyavu stahiki za kuvua samaki.

Tunasema shughuli hii iwe endelevu kwa maana kwamba ule uvuvi wa nyavu zisizostahiki au wa kupiga mabomu unaoharibu mazingira unaachwa," anasema Dk. Mwinyi.

Katibu Mkuu, Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi, Dk. Aboud Jumbe
Mmoja wa walioko msitari wa mbele na gwiji katika masuala ya Uchumi wa Bluu ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi  Dk. Aboud Jumbe, ambaye anaamini kwamba Uchumi wa Bluu ulioendelevu unafaida nyingi za kijamii na kiuchumi kwa watu wa Zanzibar.


“Unaleta faida za kijamii na kiuchumi kwa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo kwa kuchangia katika upatikanaji wa chakula, kuondoa umasikini, kuongeza ajira, kuimarisha afya, kuleta usawa na utulivu wa kisiasa, ” anasema Dk. Jumbe kwenye sehemu ya mada yake ya Uchumi wa Buluu aliyowasilisha katika Mkutano Mkuu wa Jukwaa la Wahariri, mwezi huu, Zanzibar.
Kwa mujibu wa Dk. Jumbe, ukiacha wavuvi wadogowadogo watakaofikiwa, Mpango huu unawalenga pia Wanawake wapatao 5,000 ambao hushiriki kwenye ukulima au ufugaji wa mazao ya baharini kama Mwani. Kundi hili nalo litanufaika na maboti yapatayo 500 na nyenzo zake.

Dk. Jumbe anasema kwa ujumla kwa Zanzibar Uchumi wa Buluu utakuwa ni shirikishi ukilenga kupata ushiriki wa kila mmoja.
 
“Uchumi wa Buluu unahusu pia Ushirikishwaji wa Jamii na masuala ya haki Sawa. Zaidi ya asilimia 54 ya washiriki katika Uchumi wa Bluu ni Wanawake. Lakini hatuoni Wanawake wengi katika sekta kama za Utalii, Uvuvi na Ufugaji wa mazao ya baharini. Tutaangazia pia Mabadiliko ya Tabia nchi, masuala ya uelewa, kujenga uwezo, ubunifu, utafutaji mitaji na masoko na uongezaji thamani ya bidhaa.
Ziara ya kisiwani Kojani imeisha, Wahariri wanarudi Chakechake, Pemba.
Dk. Jumbe anasema katika ujumla wake Sera ya Uchumi wa Buluu ya Zanzibar imeweka maeneo kadhaa ya kipaumbele ambayo ni pamoja na Uvuvi na Kilimo cha mazao ya baharini, Mafuta na Gesi, Utaalii Endelevu, Nishati Mbadala, Uwezeshaji wa Wanawake na Usafi/utunzaji wa Mazingira.
Posted by MROKI On Monday, March 21, 2022 No comments
 
Na Mwandishi Wetu
WATANZANIA wametakiwa kuzingatia afya ya kinywa na meno kwa kuwa ndio ufunguo wa kuwa na siha njema.

Kauli hiyo imetolewa na mtaalamu wa masuala ya afya ya kinywa na meno, Dk Donna Williams- Ngirwa (pichani) wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Afya ya Kinywa na Meno.

Alisema ipo haja ya watanzania kuhakikisha kwamba wanashughulika na afya ya kinywa na meno kwa kuwa ndio mlango wa uhai na afya bora katika maisha yao.

 Alisema katika mahojiano leo kuwa mtu akizimbea kushughulikia afya ya kinywa anakaribisha maradhi mbalimbali yakiwemo yaliyo sugu.

Dk Donna  wa Afya Bora Complete Dentistry  Ltd alisema kwamba maadhimisho ya mwaka huu yenye kauli mbiu ya kimataifa ya ‘jivunia kinywa chako’ yana maana kubwa  kwa kuwa kuzuia maradhi ya kinywa kwa kumtembelea daktari wa meno angalau mara mbili kwa mwaka husaidia sana.

 “Magonjwa mengi ya kinywa na meno hayajitambulishi mpaka yamefikia hatua mbaya hivyo ni vyema kuwahi kuyagundua, ili uwe na siha njema”  alisema.

 Hata hivyo alitaja kuwepo na kampeni kubwa ya  afya ya kinywa ili kujiweka sawa kama ufanyaji wa mazoezi unavyotumika kuweka sawa mwili.

 “Kuna haja ya kuanzisha kampeni ya kuelimisha umma umuhimu wa afya ya kinywa kwa kuwa ndio mlango wa afya,”  alisema na kuongeza kwamba ni watu  waone umuhimu  wa kujua wanachokula na madhara yake kwani ndio msingi wa afya njema ya meno na kinywa.

 Anasema watu hawafikirii kuhusu uhusiano uliopo kati ya afya ya kinywa na afya yao kwa ujumla, kwani kinywa ndio ukuta wa kuzuia maradhi katika mwili.
Anasema maradhi ya kinywa yanapokuwa katika hatua za mwanzo ni rahisi kutibika lakini yanapokuwa katika hatua kubwa yanakuwa changamoto.

"Mtu anapokuwa na tatizo la kinywani huongeza hatari , kwa mfano ugonjwa wa rheumatoid arologist, atherosulinosis, shinikizo la damu, ugonjwa wa Alzheimers, ugonjwa wa sukari, na matatizo wakati wa kujifungua."
Alisema watu wanaougua matatizo ya kinywani , huwa na sababu tofauti zinazoweza kusababisha magonjwa mengine.

Kwa mfano, idadi kuu ya molekuli zinazozalishwa na seli za binadamu na kusababisha uvimbe katika ufizi zinaweza kufikia viungo vingine vya mwili na kusababisha athari katika maeneo hayo. Kumtembelea daktari wa meno ili kutibu matatizo hayo ya kinywa ni muhimu.

Dk Donna   amesema kwa sasa wataalamu wa afya ya kinywa wamekuwa na vifaa vya kisasa zaidi hivyo ni rahisi kubaini matatizo kabla hayajawa sugu.
“Kwa mfano ninapofanya shughuli zangu tunafuata misingi ya kimataifa ya utoaji huduma kutokana na umuhimu wake,” alisema na kuongeza kuwa sekta hiyo ina teknolojia mpya.

Dk Donna  ambaye pia alishiriki kuanzisha  kliniki ya afya ya kinywa ya  Morningside Dental Care, ya New York, Marekani mwaka 1995, alisema njia nzuri ya kuwezesha afya ya kinywa na meno ni kuhakikisha kwamba unamuona daktari wa meno ili aweze kukusaidia.
Posted by MROKI On Monday, March 21, 2022 No comments

March 17, 2022

 
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Tulia Ackson (Mb), amemuelezea hayati Magufuli kuwa ni miongoni mwa  viongozi bora waliowahi kutokea Barani Afrika kwa namna alivyokuwa mtu mwema, mbunifu na mwenye moyo wa kulijenga taifa lake kwa upendo na kwa usawa.

Mhe. Spika ameyasema hayo wakati wa maadhimisho ya mwaka mmoja wa kifo cha aliyekuwa Rais wa Tanzania awamu ya tano hayati Dkt. John Pombe Magufuli, yaliyofanyika Wilayani Chato Mkoani Geita leo machi 17, 2022.

Aidha, Mhe. Dkt. Tulia amemshukuru na kumpongeza Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuyaendeleza mambo mazuri ikiwemo miradi mbalimbali ya maendeleo iliyoanzishwa na hayati Magufuli kitendo alichokieleza kuwa ni kuwafuta machozi ya watanzania walio wengi.

 “Mheshimiwa Rais, siku ya leo ni siku ya kukumbuka mtangulizi wako alipoiaga dunia lakini tunafurahi kwamba kumbukizi hii haiji na majonzi tena bali inakuja na ushindi mkubwa ambao Mheshimiwa Rais umetufikisha hapa kwa kuyafanya mambo makubwa yakiwemo yale ambayo unayaendeleza kutoka kwa mtangulizi wako na zaidi yale ambayo unayafanya kwa utashi wako.” Amesisitiza Spika. Dkt. Tulia.

Maadhimisho hayo yaliyoongozwa na Rais wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, yamehudhuriwa pia na Viongozi mbalimbali wa serikali, dini na wananchi mbalimbali kutoka maeneo tofauti nchini.
Posted by MROKI On Thursday, March 17, 2022 No comments
Na Mwandishi Wetu- Dar es salama
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Mhe.Balozi Dkt.Pindi Chana amewataka waraibu wa dawa za kulevya kutumia fursa za kliniki za kuponya zilizopo katika maeneo mbalimbali nchini ili waweze kurejea katika hali ya kawaida kushiriki katika shughuli mbalimbali za ujenzi wa Taifa.
 
Mheshimiwa Pindi ametoa rai hiyo Jijini Dar es salam baada ya kufanya ziara katika Kliniki ya Methadone iliyopo katika Hospitali ya Mkoa ya Rufaa Mwananyamala ambapo inasimamiwa na Serikali kupitia Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA).
 
Pia aliishauri idara hiyo kushirikiana bega kwa bega na idara nyingine vikiwemo vitengo vilivyopo halmashauri kama Mwanasheria wa Halmashauri ili pale ambapo kuna uhitaji aweze kushiriki kikamilifu kutoa huduma.
 
“Niwasishi  watu wote mnapata dawa hizi saidizi hususani methadone muendelee kuzitumia kadri mnavyoelekezwa ili kuepuka changamoto ya kurejea katika hali za awali iwapo mtasistisha kuzituma kwa sababu Serikali inatamani kuona kila mwananchi anafanya kazi halali kujiingizia kipato maana kuendelea kuzitumia unaharibu afya yako na kupunguza nguvu kazi ambayo ni vijana,” alisema Mhe. Pindi.
 
Pia aliwataka maafisa ustawi wa jamii kuwahamasisha vijana hao kujiunga katika vikundi ili waweze kunufaika kupitia fursa mbalimbali za kiuchumi zinazotolewa na Serikali pamoja na wadau wengine nchini baada ya kupona kwani  Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa, vijana wote wananufaika kupitia mikopo ya asilimia 10 inayotokana na mapato ya ndani ya Halmashauri.
 
"Hata wale wenye changamoto, waraibu wanayo haki ya kujiunga katika vikundi wakapata fursa hii, na mikopo hii inatolewa pasipokuwa na riba ya aina yoyote. Hizi ni jitihada za Serikali yetu za kuwasaidia wanawake na vijana, hivyo fursa hizi zinatolewa katika vikundi, ni muhimu sana vijana wakajiunga katika vikundi, kwani umoja ni nguvu. Kikundi chenye ndiyo dhamana, ya kurudisha fedha hizo ili wengine wapate.

Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala, Dkt. Zavery Benela alieleza kwamba , Kliniki ya MAT, Mwananyamala inahudumia wateja zaidi ya 1,350 kila siku ambao wanafika kupata huduma.
 
Kwa upande wake Kamishina wa Kinga na Tiba wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA), Dkt. Peter Mfisi alifafanua kwamba hadi Desemba mwaka jana zaidi ya waraibu 10,600 walikuwa wamehudumiwa kupitia vituo vya tiba saidizi kwa waraibu, vikubwa kwa vidogo vilivopo hapa nchini.
 
“Kwa  sasa tuna vituo 15 ambapo kuna vinne vidogo huku 11 vikiwa vikubwa kwa ajili ya kutoa tiba saidizi kwa waraibu kwa kutumia dawa.Vituo hivi husimamiwa na Serikali na huhudumia waathirika wa dawa ya kulevya aina ya afyuni kama vile heroin na baadhi ya dawa tiba zenye asili ya kulevya na waathirika wanatakiwa kuhudhuria matibabu kila siku mpaka watakapomaliza matibabu,” Alifafanua Dkt.Mfisi.
 
Akieleza baadhi ya sababu zinazisababisha vijana wengi kujiingiza katika matumizi ya dawa za kulevya Afisa Ustawi wa Jamii anayesimamia kliniki hiyo, Hafsa Mtwange alitaja kuwa ni pamoja na  makundi, hali ya maisha na ndoa.
 
Vilevile Mtaalamu kutoka Kliniki ya MAT Mwananyamala, Dkt. Miriam Kabanywanyi alibainisha kuwa, wamekuwa na jukumu kubwa la kuwajenga kisaikolojia waraibu hao wa dawa za kulevya, kwani kila anayefika kituoni hapo ana changamoto zake kubwa ikiwa ni kuathirika kisaikolojia.
 
"Hivyo, tunatumia muda mwingi kuwajengea uwezo kwa kuwaandaa kisaikolojia ili waweze kuyakubali mazingira ya kupatiwa tiba na baada ya kuhitimu waweze kuwa watu mwema katika jamii na kushiriki kikamilifu katika maendeleo yao na jamii kwa ujumla,"alieleza Dkt. Miriam.

Aidha baadhi ya  waraibu walieeleza kuwa, changamoto kubwa ambazo wanakabiliana nazo baada ya kuhitimu hatua hiyo ya kupatiwa dawa na kurudi katika hali ya kawaida ni pamoja na kukosa kazi za kufanya, hivyo kujikuta wanajiingiza tena kwenye makundi mabaya.

Posted by MROKI On Thursday, March 17, 2022 No comments

March 16, 2022

NAIBU Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Ridhiwani Kikwete amewahakikishia Watanzania kuwa Serikali imejipanga kutatua migogoro ya ardhi ikiwemo ile ya mipaka ya Wakulima na wafugaji.

Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema hayo mapema Machi 15,2022 wakati akishiriki uzinduzi wa Wiki ya Maji Simanjiro Mkoani Manyara ambapo mgeni rasmi alikuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango.

Akitoa salamu za Wizara ya Ardhi, Mhe Ridhiwani Kikwete amempongeza na kumshukuru Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutenga bajeti itakayowezesha utekelezaji wa majukumu ikiwemo kuondoa migogoro ya wakulima na wafugaji, mipaka baina ya Wilaya, Mikoa na Hifadhi na Usalama wa Ardhi.

"Wizara ya Ardhi imejipanga kuleta amani na utulivu kwa kutatua changamoto kwenye mipaka ya ardhi." Alisema Mhe. Ridhiwani Kikwete.

Posted by MROKI On Wednesday, March 16, 2022 No comments
Na Mwandishi wetu -Dodoma
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe.  Balozi. Dkt. Pindi Chana amewataka wadau wa chaneli ya utalii Tanzania Safari, kuhakikisha wanatanua wigo wa vipindi vya utalii viweze kuonekana katika mitandao ya kijamii.

Waziri Dkt. Pindi alitoa agizo hilo jijini Dodoma wakati akizungumza na wadau wa chaneli hiyo na Manaibu Mawaziri kwa lengo la kujadili mikakati na  maboresho ya channeli  ili kufanikisha malengo ya kuanzishwa kwake.

Alisema kwamba baada ya uzinduzi wa Chaneli hiyo  uliofanywa na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa  Disemba , 2015 iliundwa  kamati ya watendaji wa wizara  kujadili na kutoa mapendekezo yatakayoboresha  uendeshaji wake  kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini kimataifa.

“Moja ya mapendekezo ilikuwa ni kuhakikisha inapatikana katika visimbuzi vyote  na majukwaa mengine nchini  na hapa kuna wataalamu mtatuambia  hii haitoshi tuweke na kwenye simu, mitandao ya kijamii  ndiyo maana kikao cha leo kina wabobezi hivyo ni lazima tufikiri nje ya boksi  kama tunazungumzia utalii siyo lazima mtu afike nyumbani ndipo awashe luninga yake zionekane hata katika vyombo vya usafiri,”alisema Mhe. Pindi.

Kuhusu athahari ya UVIKO -19 katika sekta ya utalii Mhe. Pindi alisema pato linalotokana na utalii lilishuka kutoka dola za Kimarekani Bilioni 2.532 mwaka 2019 hadi Bilioni 1.107 mwaka 2021 lakini bado inatajwa kama sekta muhimu kwa uchumi wa Nchi.

Hata hivyo Waziri Pindi alibainisha  kwamba chaneli hiyo inapaswa kuwa endelevu na vipindi vinavyoandaliwa  viwe vyenye  ushawishi kwa wananchi kuvutiwa kutembelea vivutio vilivyopo nchini hata mataifa ya nje kutembelea vivutio hivyo.

“Vivile  kikao hiki kitoe mapendekezo ya namna ya kupata fedha za dharula kwa jili ya kushughulikia uandaaji wa vipindi vipya na kuweka mikakati ya kuhakikisha uendelevu wa chaneli hii  na kamati ya Mheshimwa Waziri Mkuu ilikutana Disemba 27, 2018 kuweka mikakati ya uendelevu wa chaneli ikiwemo ubora unaozingatia viwango vya kimataifa, uhitaji wa mafunzo, upatikanaji wa vifaa vya kisasa na kuwezesha chaneli kupatikana  katika majukwaa yote,”alisisitiza Mhe. Pindi.

Alihitimisha kwa kusema masuala ya utalii ni mtambuka yanayoshirikisha sekta mbalimbali kama sekta ya utalii, sekta ya uchukuzi, sekta ya habari na mawasiliano na  sekta ya fedha hivyo kama wasimamizi wa sera katika Wizara husika ipo haja ya kuifahamu chaneli hiyo, lengo la kuanzishwa na umuhimu wake kwa sekta ya utaliii na uchumi kwa Nchi.

Akieleza mapendekezo yaliyofikiwa na wataalamu wa sekta hiyo mara baada ya kikao Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Bw. Kaspar Mmuya alieleza maazimio yaliyofikiwa kwamba ni pamoja na Mawaziri kuendelea kupewa nafasi ya kuwasilisha mawazo yao, wanaochangia kwa kujitolea kuwezesha chaneli watambuliwe  na kila taasisi kuweka utaratibu utakaowezesha uchangiaji wa Safari Chaneli.

Aidha Mkurugenzi wa Shirika la Utangazaji (TBC) Dkt. Ayoub Ryoba akaeleza mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa chaneli hiyo ambayo ni ununuzi na ufungaji wa mitambo ya kidigitali, kurusha matangazo kote Duniani, kurushwa vipindi vyake kupitia visimbuzi vyote nchini, kuboresha vifaa, kutoa elimu ya utalii kwa watanzania kuptia vivutio vya kiutamaduni, hifadhi za wanyama na utalii wa Ikolojia.

Posted by MROKI On Wednesday, March 16, 2022 No comments


Sehemu ya Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wakifuatilia wasilisho la Mradi wa Jengo la Kuhifadhia kumbukumbu. Wasilisho hilo limetolewa leo tarehe 15 Machi, 2022 na Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji wa Mahakama, Bw. Erasmus Uisso (hayupo katika picha) wakati Wanakamati hao walipokagua Mradi huo.


 Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akifafanua jambo kwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria walipokuwa wakikagua Jengo la kuhifadhia Kumbukumbu za Mahakama lililopo Mahakama Kuu Tanga.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Ole Gabriel akionyesha moja ya maboksi maalum yanayotumika kuhifadhia majalada mbalimbali yanayohifadhiwa katika jengo hilo.

Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji wa Mahakama, Bw. Erasmus Uisso akiwasilisha mada kwa Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria (hawapo katika picha).
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akiwaongoza Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kukagua Jengo la kuhifadhia Kumbukumbu za Mahakama lililopo Mahakama Kuu Tanga. Kushoto (mwenye suti ya bluu) ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Geofrey Pinda na katikati ni Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Emmanuel Mwakasaka na waliopo nyuma ni sehemu ya Wajumbe wa Kamati hiyo. Kamati hiyo imeanza ziara ya kukagua Miradi mbalimbali ya Mahakama leo tarehe 15 Machi, 2022.
Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Emmanuel Mwakasaka akizungumza jambo katika hafla hiyo.
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria imeupongeza Mhimili wa Mahakama ya Tanzania kwa kuboresha huduma zake ikiwa ni pamoja na kupiga hatua katika uboreshaji wa miundombinu ya majengo yake na matumizi ya TEHAMA.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo tarehe 15 Machi, 2022 katika jengo la Mahakama Kuu Tanga, Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Emmanuel Mwakasaka (Mb.) amesema kwa niaba ya Kamati hiyo kuwa huduma mbalimbali za Mahakama zimeendelea kuboreshwa hali ambayo inaleta faraja kwa Serikali kuona tija ya fedha inazotoa kwa Mhimili huo.

“Napenda pia kumshukuru Mhe. Rais Samia kwa kuujali hasa huu Mhimili wa Mahakama kwa kuendelea kutoa fedha katika kuwezesha kuboresha huduma za utoaji haki na haki kuonekana kutendeka kwa wananchi, na ninaomba nikiri wazi kuwa Mahakama imepiga hatua kubwa sana katika matumizi ya TEHAMA na  kwa sasa inaongoza kwa Tanzania kwa sababu inakwenda kidijitali zaidi,” alisema Mhe. Mwakasaka.

Mhe. Mwakasaka sambamba na Wabunge wenzake wa Kamati hiyo, leo wameaanza ziara ya kukagua Miradi ya Mahakama ambapo wameanza rasmi kwa kukagua Jengo jipya la kuhifadhi Kumbukumbu za Mahakama lililopo Mahakama Kuu-Kanda ya Tanga.

Mhe. Mwakasaka ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maadili, Madaraka na Haki za Bunge alikiri wazi kuridhishwa na muonekano wa jengo hilo baada ya kulikagua na Wanakamati wenzake na kusema kuwa jengo ni zuri na litasaidia katika kuhifadhi vizuri kumbukumbu za Mahakama katika Kanda hiyo.

“Leo tumekuja kutembelea jengo hili ya kuhifadhi kumbukumbu, kwakweli jengo hili kwa kiasi kikubwa linaridhisha ukiachia mbali mambo madogo madogo ambayo Viongozi wameahidi watayafanyia kazi. Na nikiri wazi kuwa Mahakama mnaendelea vizuri,” aliongeza Mbunge huyo.

Naye Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Geofrey Pinda ameeleza kuwa wajibu wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria ni kupitia/kukagua Miradi iliyopo chini ya mwamvuli wa Wizara hiyo ambamo ndani yake imo pia Mahakama ya Tanzania inayotekeleza Miradi mingi.

Kwa mujibu wa Mhe. Pinda, alisema hadi kufikia 2025 Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa inaendelea kusogeza huduma za miundombinu ya majengo huku akieleza kuwa Wilaya zote zitakuwa na Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo kwa kila Tarafa.

“Tunao uhaba mkubwa wa majengo ya Mahakama, ukiangalia katika ngazi ya Mahakama za Mwanzo, kati ya Kata karibia 3800 ni Kata 960 pekee zenye Mahakama za Mwanzo, hivyo lengo lililopo ni kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2025 kila Wilaya iwe na Mahakama na kwa upande wa Mahakama za Mwanzo angalau kila makao makuu ya Tarafa kuwe na Mahakama,” alieleza Mhe. Pinda.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel ameishukuru Kamati hiyo kwa ushirikiano na vilevile kuishukuru Serikali kwa kuendelea kutoa rasilimali fedha zinazowezesha kuendesha miradi na shughuli mbalimbali za kimahakama akiongeza kuwa Mahakama ipo katika hatua za mwisho kukamilisha ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga na kuwezesha mkoa huo kuwa na Mahakama za Wilaya kwa wilaya zake zote.

“Kwa niaba ya Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania napenda kutoa shukrani zangu kwenu ninyi Wahe. Wabunge kwa kuendelea kutoa ushirikiano kwa Mhimili huu unaotuwezesha kusonga mbele, vilevile pokeeni shukrani hizi kutoka kwa Mhe. Jaji Mkuu ambaye anatambua ziara hii ambayo mmeianza leo na ninaomba kuwahakikishia kuwa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Mkinga utakamilika mwisho mwa mwezi Aprili mwaka huu,” alisema Prof. Ole Gabriel.

Jengo hilo la kisasa la Kuhifadhi kumbukumbu za Mahakama lililokaguliwa limegharimu kiasi cha fedha za Kitanzania 139, 411,376/= na imeelezwa kuwa litasaidia kuongeza ufanisi katika kazi kwa kuokoa muda mrefu wa kutafuta majalada ambayo awali hayakuwa katika mpangilio mzuri, vilevile litasaidia kuleta uwazi na kuimarisha usalama wa kumbukumbu hizo muhimu.

Kamati hiyo inatarajia kufanya ukaguzi pia kwenye Mradi wa Ujenzi wa Bweni la Wavulana katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) -Lushoto, Mradi wa Ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Same, Mradi wa Ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Mwanga na Ukarabati wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi-Kilimanjaro na mwisho Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC)-Arusha.

Posted by MROKI On Wednesday, March 16, 2022 No comments
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Mhe. Vita Kawawa akizungumza wakati kamati hiyo ilipotembelea Chuo Cha Diplomasia Jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula.
*******
Na Waandishi Wetu, Dar 
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) imeipongeza Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa juhudi ilizozichukua hadi kufanikisha zoezi la kuwarejesha salama wanafunzi waliokuwa nchini Ukraine.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Vita Kawawa (Mb) Jijini Dar es Salaam wakati Kamati hiyo ilipotembelea Chuo cha Diplomasia (CFR).

Katika Kikao hicho ambacho pia kilihudhuriwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula pamoja na Naibu Katibu Mkuu Mhe. Balozi Fatma Rajab.
“Nichukue nafasi hii kutoa pongezi nyingi kwa Wizara kwa jinsi mlivyoshughulikia suala zima la kuhakikisha wanafunzi wa Kitanzania walioko nchini Ukraine wanarejea salama nchini,” amesema Mhe. Kawawa.

‘’Mhe. Waziri tunawapa pongezi nyingi, kwa kazi  na hatua kubwa mlizochukua  na jinsi mlivyoshirikiana na wazazi wenye wanafunzi waliokuwa wanasom nchini Ukraine hasa ikizingatiwa kuwa wazazi hao waliwapeleka watoto wao binafsi bila ya kuishirikisha Serikali,’’ ameongeza Mhe. Kawawa.

Amesema kamati imeridhishwa na jinsi ambavyo Wizara ilivyosimama imara na kuwasaidia Watanzania wote waliokuwepo nchini Ukraine na kuhakikisha wanarejea nyumbani salama.

Mhe. Kawawa ametoa wito kwa Watanzania wanapokuwa nje ya nchi kujiandikisha katika Balozi za Tanzania ili kuwa rahisi kuwaratibu pale inapotokea athari yoyote kule wanapokuwepo.

Mhe. Kawawa amewapongeza vongozi wa wizara, mabalozi na watumishi wa wizara ambao kwa namna moja au nyingine wamefanikisha uondoaji wa watanzania waliokuwepo nchini Ukraine.
Akizungumza katika kikao hicho Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula ameihakikishia kamati hiyo kwamba Uongozi wake utaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuhakikisha inasimamiwa ili ikamilike kwa wakati na kuendana na thamani halisi ya fedha iliyotolewa na Serikali.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula akimkaribisha Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Mhe. Vita Kawawa katika Chuo cha Diplomasia (CFR) Jijini Dar es Salaam
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula wakikagua mradi wa ujenzi wa vyumba vya mihadhara ya Chuo cha Diplomasia (CFR) Jijini Dar es Salaam
 
Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Mhe. Alexander Mnyeti akizungumza wakati kamati hiyo ilipotembelea Chuo Cha Diplomasia Jijini Dar es Salaam
Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Mhe. Stella Ikupa akizungumza wakati kamati hiyo ilipotembelea Chuo Cha Diplomasia Jijini Dar es Salaam
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU)  katika picha ya pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula, Naibu Katibu Mkuu Balozi Fatma Rajab pamoja na viongozi wa Chuo  Cha Diplomasia Jijini Dar es Salaam
Posted by MROKI On Wednesday, March 16, 2022 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo