Nafasi Ya Matangazo

March 15, 2016

RAIS wa Rwanda, Paul Kagame amelaumu Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kwa kutumia pesa ‘kiholela’ kutokana na mawaziri kufanya ziara za mara kwa mara kuhudhuria mikutano.

Amesema mawaziri wa nchi yake wanatumia chombo hicho kama njia ya kujinufaisha kwa kufanya ziara na kuhudhuria mikutano ya jumuiya hiyo isiyo muhimu.

Rais Kagame ameahidi kuiga mfano wa Rais John Magufuli wa Tanzania  kutokomeza ufisadi huo kwa kusitisha ziara za mawaziri alizotaja kuwa za kufuja mali ya taifa.

Akiongea katika mkutano wa faragha wa viongozi wa taasisi zote za serikali nchini Rwanda, Rais Kagame amesema suala la ufisadi nchini humo linachukua mwelekeo mpya na kasi ya ajabu na kwamba hawezi kuendelea kuvumilia.

Rais Kagame alisema  EAC imeanza kuwa ghali na mzigo kwa taifa lake akisema mawaziri katika mataifa wanachama wanatumia jumuiya hiyo kama chombo cha kuchota pesa kwa kubuni mikutano ya kila siku baadhi akiitaja kuwa haina umuhimu wowote.

Alisema mawaziri wake wasiopungua watano wanasafiri kama mara tatu kwa wiki kushiriki mikutano ya EAC popote inapotokea katika nchi wanachama na kwamba ziara hizo zinaigharimu serikali fedha nyingi.

“Ni kama mawaziri wa nchi hizi walikubaliana kushinikiza serikali zao kuwa lazima wahudhurie kila aina ya vikao vya jumuia hii kwa kisingizio kuwa waziri anayeshindwa kuhudhuria nchi yake inachukuliwa hatua ama inaonekana kupinga juhudi na mikakati ya jumuiya,” alisema Rais Kagame.

Moja ya njia alizosema anaweza kutumia ni kumpa waziri wake wa masuala ya EAC, Valentine Rugwabiza jukumu la kushughulikia masuala yote yanayohusu jumuiya hiyo.

Amepongeza juhudi za Rais wa Tanzania John Magufuli za kukomesha ufisadi uliokuwa umekithiri katika taasisi za serikali, akisema lazima na yeye afuate nyayo za Rais Magufuli katika suala zima la kukomesha ufisadi na ufujaji wa mali ya serikali.

Rwanda inaorodheshwa ya kwanza katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki katika kupambana na rushwa na ufisadi.


Mwandishi wa BBC Yves Bucyana anasema miaka ya nyuma viongozi kadhaa wa wilaya na taasisi nyingine za serikali walipoteza kazi zao na kutupwa jela kwa makosa ya kuhusika na rushwa na ufisadi.
Posted by MROKI On Tuesday, March 15, 2016 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo