Nafasi Ya Matangazo

December 11, 2013

BENDI ya muziki wa dansi ya Mashujaa Musica 'Wazee wa Kibega' inatarajia kupamba uzinduzi wa albamu ya 'Chuki ya Nini' ya bendi ya FM Academia utakaofanyika Desemba 21 mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Hayo yalisemwa jana Rais wa bendi hiyo, Nyoshi El-Saadat alipokuwa akizungumza na waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari kuhusu
maandalizi ya uzinduzi huo aliodai kuwa utakuwa wa kishindo. 

"Hii ni albamu yetu ya kumi ambayo imeandaliwa kwa ubora wa kimataifa  na sasa iko tayari kuzinduliwa Desemba 21 tukisindikizwa na bendi ya Mashujaa Musica," alisema Nyoshi. 

Nyoshi alitaja nyimbo za albamu hiyo kuwa ni 'Fataki', 'Otilia', 'Ndoa ya Kisasa', 'Neema', 'Dai Chako Ulaumiwe', 'Maisha', 'Madudu', 'Miraessa' na 'Intro' ambazo zote zimeshaingizwa kwenye video.

Aliongeza kusema kuwa katika uzinduzi huo watawakumbuka pia kwa kuwaombea watu wawili maarufu waliofariki dunia ambao ni Rais wa zamani wa Afrika Kusini mzee Nelson Mandela na mwanamuziki mkongwe wa Kongo, Tabu Ley.

Bendi ya FM Academia ilizindua albamu ya kwanza ya 'Hadija' mwaka 1998 kisha ikafuatia ya pili iitwayo 'Atomic' iliyozinduliwa mwaka 1999 na baadaye mwaka uliofuata wa 2000 bendi hiyo ilizindua albamu ya tatu iliyopewa jina la 'Prison'.

'Wazee wa Ngwasuma' hawakuishia hapo, mwaka 2001 walizindua albamu ya nne iitwayo Freedom na kufuatiwa na ya tano ya 'Mpambe Nuksi' iliyozinduliwa mwaka 2001 na kisha ikafuata ya sita iitwayo 'Dotnata' mwaka 2003 kabla ya 'Dunia Kigeugeu' iliyozinduliwa mwaka 2006.

Baada ya hapo bendi hiyo ilikaa kidogo hadi mwaka 2010 ilipozindua albamu mbili kwa mpigo ambazo ni 'Vuta Nikuvute' na 'Heshima kwa Wanawake'  na sasa mwaka huu wa 2013 unaumalizia kwa kuzindua albamu ya 'Chuki ya Nini'.
Posted by MROKI On Wednesday, December 11, 2013 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo