Nafasi Ya Matangazo

November 24, 2013

Na Mwandishi Wetu
BINGWA wa dunia wa mbio za marathon, Edna Ngeringwony Kiplagat (pichani ) wa Kenya amejitokeza kushiriki zile za Uhuru Marathon zinazotarajiwa kufanyika jijini Dar ers Salaam Desemba 8, mwaka huu.
 
Katibu wa Kamati ya Uhuru Marathon, Innocent Melleck alisema, wamefarijika kwa kiasi kikubwa kwa Edna mwenye sifa lukuki katika mbio za marathon kujitokeza kushiriki.
 
“Kwetu tumefarijika mno kutokana na ushiriki wa Edna, kwani ni mwanariadha wa kimataifa mwenye rekodi nyingi za kuvutia na hasa hii ya ubingwa wa dunia kwa upande wa wanawake,” alisema.
 
Edna,34, alitwaa ubingwa wa dunia kwa upande wa marathon mwaka 2011 katika mashindano yaliyofanyika Daegu, Korea Kusini na akafanya hivyo tena mwaka huu katika mashindano ya dunia yaliyofanyika Moscow, Urusi.
 
Pia alishinda katika mbio za Los Angeles Marathon na New York Marathon zilizofanyika mwaka 2010 na muda bora zaidi kupata kuuweka katika mbio hizo ni wa saa 2:19:50 katika mbio za London Marathon mwaka jana.
 
Pia ametwaa medali mbalimbali katika mashindano ya vijana wakati anaanza kukimbia mwaka 1996, pale alipoonyesha uwezo wake katika mashindano ya dunia kwa vijana.
 
Melleck alisema, umuhimu wa mbio hizo unaonekana zaidi kwani watu wengi wanazidi kujitokeza kushiriki nab ado fomu za usajili zinaendelea kutolewa.
 
Alisema, katika usajili huo, mshiriki wa kilomita 3 atalipa Sh 100,000 yule wa kilomita 5 Sh 2,000 na washiriki wa kilomita 21 na 42 watalipia Sh 6,000.
 
“Pia tunapenda kuchukua fursa hii kuziomba kampuni au taasisi mbalimbali zinazotaka kudhamini mbio hizo zijitokeze na kufanya hivyo, kwani nafasi bado ipo na tukumbuke bila amani hakuna chochote kinachoweza kuendelea, hivyo hata wao pia wanatakiwa kuipigania amani kwa nguvu zote.”
 
Mbio hizo zinatarajiwa kuanza na kumalizikia katika Viwanja vya Leaders, vilivyopo Kinondoni.
Posted by MROKI On Sunday, November 24, 2013 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo