Nafasi Ya Matangazo

December 10, 2025

Jeshi la Polisi lingependa kuwajulisha kuwa, kama tulivyo wapa taarifa iliyokuwa na ahadi ndani yake majira ya saa 6 usiku tarehe 9.12.2025 kuamkia leo tarehe 10.12.2025 kuwa, kwa ushirikiano na Vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama tutaendelea kuimarisha hali ya usalama nchini na kwamba tutaendelea kulinda maisha ya wananchi na mali zao, nitumie fursa hii kuwajulisha kuwa, kazi hiyo tumeifanya vizuri na kwa ufanisi mkubwa na hali ya usalama wa nchi yetu imeamka ikiwa shwari.
 
Aidha, kama tulivyo waeleza tarehe 3 na 5 Disemba 2025 kwenye taarifa ya Jeshi la Polisi kuwa, wanaohamasisha maandamano wanayoyaita ya amani na yasiyo na kikomo kuwa, miongoni mwa mbinu za kihalifu 13 walizo kuwa wanahamasishana na kupanga kutumia kupitia klabu za mitandaoni na njia zingine ni kuhakikisha wanasimamisha shughuli zote za kiuchumi na kijamii nchini zisiendelee.
 
Tumewafuatilia kwa karibu na kwa muda mrefu toka jana tarehe 9.12.2025 kwenye klabu hizo za mitandaoni na njia zingine walizokuwa wana tumia kuwasiliana wakipanga na kuhamasishana kwa vile jana tarehe 9.12.2025 walishindwa kufanya maandamano yao hayo yaliyo kinyume na Katiba ya nchi ya Mwaka 1977 na Sheria ya Polisi na Polisi Wasaidizi wajitokeze mitaani leo tarehe 10.12.2025 kufanya maandamano hayo haramu.
 
Jeshi la Polisi linaendelea kuwakumbusha, kuwasisitiza na kuwaonya wasifanye hivyo kwani wanacho kiita maandamano ya amani yasiyo na kikomo yalipigwa marufuku toka tarehe 5.12.2025 kwa sababu yamekosa sifa kulingana na matakwa ya Sheria mama Katiba ya nchi ya 1977 na Sheria ya Polisi na Polisi Wasaidizi Sura 322.
 
Jeshi la Polisi kwa ushirikiano na Vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama tuna wahakikishia wananchi tutaendelea kulinda usalama wa nchi yetu, sambamba na maisha na mali zenu ili muweze kuendelea na shughuli zenu kama kawaida.
 
Aidha, kama kuna ambaye atajitokeza na kukaidi kutii sheria za nchi kwa lengo la kuhatarisha usalama wa nchi ili kusimamisha shughuli za kiuchumi na kijamii zisiendelee kama wanavyo hamasishana na kudanganyana tutawadhibiti ili nchi ibaki salama na Watanzania wema na wapenda amani wabaki salama.
 
Tungependa kutoa wito kwa wananchi waendelee kufanya shughuli zao na kufuata maelekezo watakayo kuwa wanapewa na Vyombo vya Ulinzi na Usalama maeneo yote nchini sambamba na kutii sheria za nchi.
 
Hayo yote yanafanyika ili Taifa letu liendelee kuwa salama na sisi sote Watanzania wapenda amani tuendelee kuwa salama wakati wote.
Posted by MROKI On Wednesday, December 10, 2025 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo