Nafasi Ya Matangazo

June 20, 2025


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema kukamilika kwa Daraja la John Pombe Magufuli (Kigongo–Busisi) sio tu ni ndoto ya mtangulizi wake iliyotimia, bali pia ni alama ya uhuru wa kiuchumi wa Tanzania na chachu ya maendeleo kwa mikoa ya Kanda ya Ziwa na nchi jirani.





 
Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa daraja hilo, Rais Dkt. Samia amesema daraja la J.P. Magufuli ni mkombozi mkubwa kwa wananchi waliokuwa wakikabiliwa na changamoto ya vivuko kwa miongo kadhaa, na sasa wamepata suluhu ya kudumu kwa usafirishaji wa watu, bidhaa na huduma.
 
Daraja hilo kubwa lenye urefu wa kilomita 3.0 na barabara unganishi ya kilomita 1.66 limejengwa kwa gharama ya zaidi ya Shilingi Bilioni 700 ambazo ni fedha za ndani na ni daraja refu zaidi Afrika Mashariki na la sita kwa urefu barani Afrika.
 
Rais Dkt. Samia ameeleza ujenzi wa daraja hilo kama kielelezo cha uwezo wa Taifa kupanga na kutekeleza miradi mikubwa kwa kutumia rasilimali zake na ni hatua ya kujivunia kama nchi inayojitegemea.
 
Aidha, Rais Dkt. Samia amesema daraja hilo ni kiungo muhimu kwa Kanda ya Ziwa na kuzifikia nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Burundi, Rwanda na Uganda, huku akiwaasa wananchi kuhakikisha wananufaika nalo kwa kuongeza uzalishaji, kusafirisha bidhaa, pembejeo na kufikia masoko kwa urahisi.
 
Rais Dkt. Samia pia amepongeza juhudi za vijana Watanzania waliopata fursa ya kushiriki katika ujenzi wa daraja hilo, akiwataka kutumia ujuzi na maarifa waliyoyapata katika ujenzi wa miradi mingine ya kimkakati nchini.
 
Vilevile, Rais Dkt. Samia ametoa rai kwa wananchi kulitunza daraja hilo na kulitumia kwa uangalifu kwa kuwa ni rasilimali kubwa ya Taifa, huku akizielekeza Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na vyombo vya ulinzi na usalama kuhakikisha linafanyiwa ukaguzi wa mara kwa mara na kuimarishwa ulinzi dhidi ya vitendo vya uharibifu.
 
Hali kadhalika, Rais Dkt. Samia amesema Serikali imekamilisha madaraja mengine makubwa tisa kote nchini tangu mwaka 2021, na ipo katika hatua mbalimbali za kukamilisha miradi mingine saba katika maeneo tofauti nchini, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa barabara zinazounganisha maeneo muhimu ya kiuchumi.
 
Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia alizindua rasmi Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira wa Mji wa Lamadi katika Wilaya ya Busega, sambamba na kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi mkoani Simiyu.
 
Mradi wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi unahusisha sekta za maji, kilimo, mifugo na uhifadhi wa mazingira, ukiwa na lengo la kuiwezesha jamii kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
 
Rais Dkt. Samia amewapongeza wananchi waliotoa maeneo yao kwa hiari ili kupisha utekelezaji wa mradi wa maji, na kuhimiza wananchi kuendelea kutoa ushirikiano katika awamu inayofuata ya utekelezaji wa miradi kama hiyo katika miji ya Maswa na Meatu.
Posted by MROKI On Friday, June 20, 2025 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo