Nafasi Ya Matangazo

October 13, 2024








Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, ametoa wito kwa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) pamoja na jumuiya nyingine za chama hicho kuendelea kushindana kwa hoja na kuwa mfano bora wanapojadili masuala mbalimbali ya kitaifa. 

Akizungumza katika hafla ya kumaliza matembezi ya vijana kuadhimisha kumbukumbu ya Mwalimu Julius Nyerere, Balozi Nchimbi aliweka wazi kuwa nafasi ya CCM kushinda katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwezi Novemba inategemea sana juhudi za vijana hao.

Balozi Nchimbi, aliyekuwa akizungumza mbele ya vijana takriban 2,156 waliotembea kutoka Butiama, Mkoa wa Mara, hadi Nyamagana, Jijini Mwanza, alisisitiza umuhimu wa vijana wa CCM kuwa mstari wa mbele katika kutafuta kura kwa bidii.

Alieleza kuwa ushindi wa CCM hautapatikana kwa kubahatisha, bali kwa juhudi za makusudi na mipango ya kimkakati, huku akiwataka vijana hao kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha chama kinapata ushindi mkubwa.

“Vijana wa UVCCM, ninyi ni nguzo muhimu katika chama hiki. Ushindi wa CCM uko mikononi mwenu. Mnapaswa kushindana kwa hoja na kuhakikisha mnatafuta kura za CCM usiku na mchana. Tunataka ushindi wa aina ambayo wapinzani wetu hawajawahi kushindwa tangu chaguzi hizi zianze. Na baada ya hapo, tutawashukuru kwa ushiriki wao mzuri kwenye mchakato wa uchaguzi,” alisema Balozi Nchimbi.

Pamoja na kutoa wito huo kwa vijana, Nchimbi alitoa pongezi kwa UVCCM kwa kuandaa matembezi hayo, ambayo alisema yamekuwa na maana kubwa kwa Chama na Taifa zima.

Alieleza kuwa matembezi ya vijana yaliyoanza tarehe 9 Oktoba 2024 hadi 13 Oktoba 2024, yameleta faraja kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM. 

Alisema Rais Samia ni muumini wa falsafa za Mwalimu Nyerere, na hivyo matembezi hayo yamemgusa kwa namna ya kipekee.

“Nimefurahi sana kuona vijana wa UVCCM mmekuwa na ujasiri wa kuandaa matembezi haya. Mwalimu Nyerere alikuwa mfuasi wa falsafa zake mwenyewe, na mara ya kwanza alitembea kwa miguu kuunga mkono Azimio la Arusha. Kuanzia hapo, matembezi ya miguu yamekuwa ishara ya imani thabiti kwa jambo fulani. Kwa hatua hii, UVCCM mmefanya jambo kubwa sana ambalo limeleta faraja kwa Rais Samia na kwa wote tunaopenda historia ya nchi hii,” aliongeza.

Aidha, Balozi Nchimbi alisisitiza kuwa chini ya uongozi wa Rais Samia, Muungano wa Tanzania umekuwa na ustawi mkubwa, na amani imeendelea kudumu.

Alisema ni jukumu la vijana kuendeleza falsafa za Baba wa Taifa na kuhakikisha wanaendeleza mshikamano ndani ya chama na katika jamii kwa ujumla.

Katika ujumbe wake wa mwisho, aliwataka vijana hao kuzingatia wajibu wao wa kuhakikisha CCM inapata ushindi katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. 

Alisema kwa jitihada na ushirikiano kati ya vijana na wazee wa chama, ushindi wa chama hicho utakuwa wa kihistoria na wa kipekee.

“CCM ni chama cha wazee na vijana. Wazee ndio waanzilishi wa chama, lakini sasa nyinyi vijana ndio mna jukumu la kuhakikisha chama kinaendelea kushinda. Lazima tushirikiane kwa karibu kuhakikisha tunaleta ushindi mkubwa wa CCM kwenye uchaguzi huu ujao. Nina uhakika tutaweza kufanya hivyo,” alihitimisha Balozi Nchimbi.
Posted by MROKI On Sunday, October 13, 2024 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo