Nafasi Ya Matangazo

October 13, 2017


Meneja wa Shamba la Kahawa, Aviv, linalomilikiwa na kampuni ya Olam Tanzania Limited lililoko kijiji cha Lipokela, kilomita 45 kutoka Songea mjini Bw.Hamza Kassim, (katikati), akizungumzia mradi wa umeme wa Makambako-Songea ambao utaunganishwa kwenye kiwanda chake, mbele ya wahariri wa vyombo vya habari waliofika kiwandani hapo ili kujionea manufaa yatokanayo na mradi huo katika uwekezaji mkubwa, Oktoba 12, 2017.
Meneja wa Shirika la Umeme Tanzania, 9TANESCO), Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Patrick Lwesya, (wakwanza kulia), akizungumza kwenye eneo la Shamba la Aviv, kuhusu hatua iliyofikiwa na TANESCO kupeleka umeme wa kutosha kwenye shamba hilo ifikapo Desemba mwaka huu wa 2017. Wengine pichani kutoka kushoto mstari wa mbele, ni pamoja na Meneja Mradi wa umeme Makambako-Songea, Mhandisi Didas Lyamuya, na Meneja wa Shamba hilo, Bw. Hamza Kassim, (katikati).
 ****************
Na K-VIS Blog/Khalfan Said, Songea
UONGZI wa Shamba la Kahawa la Aviv, lililoko kijiji cha Lipokela, kilomita 45 kutoka Songea mjini, umesema Mradi wa umeme wa Makambako-Songea utaleta nafuu kubwa ya kupunguza gharama za kuendesha majenereta ya kufua umeme kwenye shamba hilo kwa asilimia 70,  Meneja wa shamba Bw.Hamza Kassim amesema.
Akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari waliotembelea shamba hilo ili kupata maoni ya wamiliki kuhusiana na mradi mkubwa wa umeme wa 220kV, Makambako- Songea  Oktoba 12, 2017, Bw. Kassim alisemamahitaji ya umeme kwenye shamba hilo ni  Megawati 2.25 hadi 2.5 na zote hizo zinazalishwa na umeme wa kutumia mafuta (Jenereta). 


shamba hilo linalo ilikiwa na kampuni ya Olam Tanzania Limited yenye makao yake makuu nchini Songapo, lina ukubwa wa Hekta 1,012 kati ya hizo, Hekta 1,000,000 zimepandwa mazao.


“Mimea ya Kahawa ambayo imefikia hatua ya kupevuka (matured), ni Hekta 800, huku Hekta 200 bado ni Kahawa changa, tunatumia nishati ya umeme kwa shughuli za umwagiliaji na ubanguaji wa Kahawa ambapo kwa siku tunatumia lita 4,000 za dizeli kuendesha jenereta hizo.” Alifafanua Bw. Kassim.



Ujio wa mradi huu ni faraja kubwa kwetu na tunashukuru mradi huu utakapokamilika utatupunguzia gharama za uendeshaji kwa asilimia 70 na hivyo kutupa fursa ya kufanya upanuzi zaidi wa kilimo cha kahawa, Alibainisha Meneja huyo.


Kwa upande wake Meneja wa Shirika la Umeme Nchini, (TANESCO), Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Patrick Lwesya alisema, Shamba la Aviv, ni moja kati ya wateja wake elfu kumi, (10,000),  ambao wataunganishiwa umeme, Desemba mwaka huu 2017 baada ya kukamilika kwa ujenzi wa mfumo wa usambazaji umeme wa kilovolti 33 pamoja na kuunganisha wateja 22,700, katika mikoa ya Songea na Njombe.

“Shamba hili ndio wateja wetu wakubwa kabisa, na tunamuhakikishia muwekezaji huyu kumpatia umeme zaidi endapo atauhitaji kwani kwa sasa tunazalisha umeme kwa asilimia 99.75, lakini mradi ukikamilika tutazalisha kwa asilimia 100 na umeme utakuwa bora na wa uhakika.” Alisema Mhandisi Lwesya.

Alisema, pamoja na mteja huyo wa shamba la Kahawa la Aviv, pia wateja wengine watakaofikishiwa umeme chini ya mradi huo ni pamoja na wale wa Mji wa Songea, vijiji vilivyo katika wilaya za Mbinga, Namtumbo na Halmashauri ya Madaba.

“Nitoe wito kwa wawekezaji kuja kuwekeza mkoani kwetu kwani tunao umeme wa kutosha kutokana na uzalishaji wake ambapo tunazalisha jumla ya Megawati 6.3 huku mahitaji halisi ya Mkoa ni Megawati 5.3.” Alisema.

Hata hivyo kumekuwepo vitendo vya uharibifu wa miundombinu hiyo mipya iliyojengwa chini ya mradi huu vinavyofanywa na baadhi ya wananchi wanaochoma misitu kwa ajili hya kuandaa mashamba.

Wahariri walishuhudia nguzo mbili moja ikiwa imeungua vibaya huku nyingine ikiwa imeungua kabisa na kubaki nyaya zikining’inia kandokando ya barara ya Songea-Mbinga kwenye kijiji cha Lipokela.

“Vitendo hivi vinasikitisha sana, niwaombe wananchi waache tabia hiyo kwani mradi huu unakwenda kubadilisha maisha yao na kwa kufanya uharibifu huu ni kuhujumu jitihada za Shirika la Umeme TANESCO kwa niaba ya Serikali, kutatua changamoto ya upatikanaji umeme wa uhakika kwa wananchi.” Alisema Meneja wa Mradi wa umeme wa Makambako-Songea Mhandisi Didas Lyamuya.

Maneno ya Meneja huyo yaliungwa mkono na Meneja wa Shamba la Aviv ambalo liko jirani na eneo ambako nguzo hizo zilichomwa moto na kutaka utamaduni wa wananchi wa mkoa wa Ruvuma wa kuchoma moto nyasi na misitu kwa nia ya kutayarisha maeneo ya kilimo waache.

“Nilifurahi ni hivi majuzi tu Mkuu wa Mkoa alizunguzia vitendo hivi na kuwaagiza viongozi wa serikali kwenye kata na vijiji kuwaelimisha wananchi kuhusu madhara ya vitendo hivyo, na kwa uoande etu sisi tumejenga mifumo ya kuzima moto kuzunguka eneo letu la shamba.” Alibainisha.
Posted by MROKI On Friday, October 13, 2017 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo