Nafasi Ya Matangazo

September 19, 2024

Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, akizungumza wakati akifungua mkutano maalum ukihusisha viongozi wa mkoa huo, wakuu wa wilaya, baadhi ya wafanyakazi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kutoka Makao Makuu jijini Dodoma na Kituo cha Tanga pamoja na wavuvi, kujadili namna bora ya kudhibiti uvuvi haramu na kukuza rasilimali za uvuvi. Kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi mkutano huo umewakilishwa na Naibu Katibu Mkuu Sekta ya Uvuvi Dkt. Edwin Mhede (hayupo pichani). 
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede akizungumza wakati wa mkutano uliofanyika jijini Tanga kwa kuhusisha viongozi wa mkoa huo, wakuu wa wilaya, baadhi ya wafanyakazi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kutoka Makao Makuu jijini Dodoma na Kituo cha Tanga pamoja na wavuvi, kwenye mkutano maalum kujadili namna bora ya kukukuza rasilimali za uvuvi na kudhibiti uvuvi haramu.
Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohamed Sheikh (aliyesimama), akitoa taarifa juu ya hali ya uvuvi haramu nchini, wakati wa mkutano uliohusisha viongozi wa mkoa huo, wakuu wa wilaya, baadhi ya wafanyakazi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kutoka Makao Makuu jijini Dodoma na Kituo cha Tanga pamoja na wavuvi. Mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga.
Baadhi ya washiriki wa mkutano wa kukuza rasilimali za uvuvi na kudhibiti uvuvi haramu uliofanyika jijini Tanga. Mkutano huo ulifunguliwa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian ambapo Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede aliiwakilisha wizara katika mkutano huo.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede akitoa salaam za wizara kwa Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, mara baada ya kufika katika ofisi ya mkuu wa mkoa huo, kabla mkutano uliohusisha viongozi wa mkoa huo, wakuu wa wilaya, baadhi ya wafanyakazi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kutoka Makao Makuu jijini Dodoma na Kituo cha Tanga pamoja na wavuvi. 
Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede (kulia kwake) na baadhi ya viongozi kutoka katika wizara hiyo na ofisi ya mkuu wa mkoa huo, baada ya Mhe. Balozi Dkt. Burian kutembelewa ofisini kwake na Naibu Katibu Mkuu Dkt. Mhede, kabla ya kushiriki mkutano wakujadili namna ya kukuza rasilimali za uvuvi na kudhibiti uvuvi haramu, kilichohusisha baadhi ya viongozi na wadau wa Sekta ya Uvuvi Mkoa wa Tanga. 
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede (aliyesimama katikati, mstari wa kwanza) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya viongozi kutoka wizara hiyo makao makuu jijini Dodoma na Kituo cha Tanga, baada ya kikao kifupi cha awali kujadili mikakati ya namna bora ya kushiriki vyema kwenye mkutano uliofanyika katika Ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Tanga uliohusisha baadhi ya viongozi wa mkoa na wadau wa Sekta ya Uvuvi katika kukukuza rasilimali za uvuvi na kudhibiti uvuvi haramu. 
***************
Na.Mwandishi Wetu
Mkoa wa Tanga unajikita kuongeza kiwango cha uzalishaji wa samaki na mazao mengine ya baharini, ili kuzinufaisha jamii zake kupitia shughuli hizo zinazohusiana na Uchumi wa Buluu.

Mkuu wa Mkoa huo, Mhe Balozi Dkt. Batilda Burian, ameyasema hayo (18.09.2024) kwenye mkutano ulioandaliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, kwa ajili ya kujadili masuala ya uhifadhi wa bahari kwa vizazi na maendeleo ya sekta hiyo Mkoani Tanga.

Amesema uvuvi ni moja ya sekta muhimu mkoani humo, hususan kwenye wilaya za Tanga, Pangani, Mkinga na Muheza ambapo takwimu zinaonesha kuwepo jumla ya wavuvi 13,336 na vyombo vya uvuvi vilivyosajiliwa 1,922.

Mhe Balozi Dkt. Burian ametoa mfano kuwa, mwaka 2023/2024 samaki waliouzwa mkoani humo walikuwa na thamani ya Shilingi Bilioni 47.208, zilizowezesha ukusanyaji ushuru uliofikia takriban Shilingi Milioni 951.7 huku wakulima wa mwani wakifikia 5,300.

Ameongeza kuwa uzalishaji wa zao hilo la baharini umefikia tani 3,000 kwa thamani ya takribani Shilingi bilioni 5, kiasi kinachotarajiwa kuongezeka kufikia tani tani 5,000.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia uvuvi, Dkt. Edwin Mhede, amemtaja Mhe Balozi Dkt. Batilda Burian kuwa ni ‘Champion’ wa ulinzi wa rasilimali za bahari na mazao yake, kutokana na jitihada mbalimbali anazozifanya katika sekta hiyo Mkoani Tanga.

Amebainisha kuwa mkuu huyo wa mkoa amekuwa akifanya kampeni mbalimbali za kuhakikisha rasilimali za bahari hususan samaki wanazaliana kwa wingi kwa kupiga marufuku na kusimamia matukio ambayo yanaashiria uvunjifu wa sheria katika Sekta ya Uvuvi.

Aidha, amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi itaendelea kutoa elimu na kuhakikisha wadau wa sekta hiyo wanaendelea kufanya shughuli kwa misingi ya sheria, kanuni na taratibu za nchi lengo likiwa kuhakikisha ukuaji wa pato la taifa kupitia Sekta ya Uvuvi.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Mohamed Sheikh ametoa wito kwa Sekretarieti za Mikoa kusimamia halmashauri kutekeleza sheria, kanuni na miongozo ya uvuvi, kupitia sera, sheria na kanuni za uvuvi, kuandaa miongozo ya usimamizi wa rasilimali za uvuvi na mazingira yake, kupanga na kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya uvuvi.

Amesema endapo hayo yatasimamiwa vyema rasilimali za uvuvi zitakuwa na tija kwa mwananchi mmoja mmoja na taifa kwa ujumla na kuifanya Sekta ya Uvuvi kuwa endelevu na kubadili mtazamo juu ya jamii ya wavuvi na wote wanaojishughulisha na mazao ya uvuvi. 

Baadhi ya washiriki wa mkutano huo wametoa maoni yao juu ya kuendeleza rasilimali za uvuvi wakitaka elimu zaidi kutolewa kwa wadau wa uvuvi ya namna ya kutunza rasilimali za uvuvi na mazao ya uvuvi kwa ujumla na kuendelezwa kwa kampeni mbalimbali za kudhibiti uvuvi haramu.
Posted by MROKI On Thursday, September 19, 2024 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo