Nafasi Ya Matangazo

August 01, 2016

 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akisisitiza jambo katika ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo Wilayani humo
  Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akielekezwa jambo na muwekezaji wa miche ya miti Wikayani humo Mr Choi
 Viongozi mbalimbali wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi wakikagua ujenzi wa matundu ya choo
  Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akipokea maelekezo ya namna ya kuitumia miche iliyooteshwa na muwekezaji Mr Choi. BOFYA HAPA KUSOMA ZAIDI.
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu alipata nafasi ya kukutana na Club inayopambana na maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi na UKIMWI kwenye Shule ya Sekondari ya Issuna
 ***************
Na Mathias Canal, Singida
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu Leo amekagua miradi ya maendeleo katika kijiji cha Utaho A ambapo inajengwa shule mpya ili kupunguza adha ya watoto kwenda umbali mrefu na kuvuka barabara ambapo pamoja na kupatiwa mafunzo ya usalama barabarani lakini bado ni Hatari kwao. 

Mtaturu amewapongeza wananchi kwa kazi nzuri wakishirikiana na Mbunge wa Jimbo la Singida Magharibi Mhe Elibariki kingu na Diwani wa Kata ya Kituntu kusimamia vyema shughuli za maendeleo na hatimaye kufanikiwa kupaua madarasa mawili na ofisi ya walimu.

Sawia na pongezi hizo Mkuu huyo wa Wilaya amewapongeza viongozi wote katika Wilaya hiyo kwa kusimamia ujenzi wa choo cha wanafunzi ambacho kina jumla ya matundu 12.

Dc Mtaturu amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo kuhakikisha serikali inaunga mkono juhudi za wananchi ili kuwasaidie kujenga nyumba za walimu ili kufikia Januari 2017 shule ianze kupokea wanafunzi wa darasa la kwanza.

Mkuu huyo wa Wilaya pia ametembelea vikundi viwili vilivyopo katika Kijiji cha Makyungu, kikundi cha Muungano ambacho kinatarajia kutotolesha vifaranga baada ya Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kuwanunulia mashine(Equbator )kwa thamani ya shilingi 8,700,000/- na kikundi cha pili kinaitwa Wajefia kinachotarajia kutengeneza chakula cha kuku kwa kutumia mashine maalumu waliyoinunua toka Shirika la Viwanda vidogo SIDO cha Mkoani Mbeya.

Sawia na hayo Mtaturu pia amebaini Changamoto waliyonayo ikiwa ni pamoja na elimu ya kuendesha Shuguli zao kibiashara na mtaji ambapo amewapa nafasi ya kupeleka wajumbe watatu kwa kila kikundi kwenye viwanja vya nane nane mjini Dodoma kwa ajili ya kupata mafunzo na mtaji wa shilingi milioni moja kwa ajili ya kuwasaidia kuanza ununuzi wa vifaa vya kusaga chakula cha kuku na mayai ili waanze uzalishaji wa vifaranga.

Dc Mtaturu pia amemtembelea Mr Choi raia wa Korea aliyeamua kuanzisha kitalu cha miche ya miti na matunda kwa ajili ya utunzaji wa mazingira katika kijiji cha Kimbwi na pia amewekeza katika elimu ambapo anajenga shule ya Awali hadi kidato cha Sita.

Aidha Dc Mtaturu amempongeza muwekezaji huyo na kuwaalika wawekezaji wengine kwa ajili ya kuwekeza wilayani Ikungi katika sekta mbalimbali kwani kuna ardhi ya kutosha ambapo pia amemwagiza Mkurugenzi wa Halmshauri kuwaelekeza watendaji wa Kata kwa ajili ya kuchukua miche ya miti na matunda kwa Mr Choi ambaye ameamua kuungana na serikali katika kampeni ya kutunza mazingira kwa kugawa miche bure.

"Naomba mfahamu kuwa Gharama za mashine ya kusagia chakula cha kuku ni shilingi milioni 9.1 zilizotolewa na Halmashauri na wananchi walichangia kujenga majengo" Alisema Mtaturu

Mtaturu pia amekagua ujenzi wa maabara uliokwama katika Sekondari ya Mkiwa hadi umeanza kubomoka hivyo amemuagiza Diwani kukaa na Kamati ya maendeleo ya Kata yake kuweka mikakati ya kuwashirikisha wananchi katika Kata wapatao 2009 ili serikali iwaunge mkono kupaua na hatimaye ifikapo Januari mwakani maabara ianze kazi.

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu anatekeleza kauli ya serikali ya awamu ya tano kwa vitendo ya Hapa Kazi Tu ambapo ametenga Siku ya Jumapili kuwa Maalumu kwa ajili ya kukagua shughuli za maendeleo.

Katika kutembelea shughuli za maendeleo Wilayani humo pia Mtaturu alipata nafasi ya kukutana na Club inayopambana na maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi na UKIMWI kwenye Shule ya Sekondari ya Issuna ambayo kitaaluma matokeo ya kidato cha nne mwaka jana ilishika nafasi ya 10 bora.
Posted by MROKI On Monday, August 01, 2016 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo