Nafasi Ya Matangazo

September 21, 2023

 
Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa  ameutaka Uongozi wa Mgodi wa Tembo Nickel kuandaa na kuwasilisha Serikalini Mpango Mkakati unaoonyesha namna wanavyoenda kushughulikia eneo lote la leseni ili kuhakikisha wanaepuka migogoro na wananchi wanaozunguka eneo hilo.

Alisema hayo Septemba 20, 2023 wakati akizungumza na uongozi wa mradi wa Tembo Nickel unaomilikiwa kwa ubia kati ya Serikali ya Tanzania na Kampuni ya Kabanga Nickel, uliopo Wilaya ya Ngara Mkoani Kagera akiwa katika ziara ya kukagua shughuli za Sekta ya Madini katika Mikoa ya Kagera na Geita. 

“Mradi huu tunataka uwe wa mfano hapa nchini, hatutaki kurudia makosa yaliyotokea huko nyuma kutokana na miradi kuingia kwenye migogoro na wananchi wanaozunguka maeneo yao, nyie muwe mfano katika kuepuka hili kupitia mpango kazi wenu” alisema Dkt. Kiruswa.

Aliwataka kuratibu suala la kuwalipa fidia na kuwahamisha wananchi ili kuepuka usumbufu na kwamba wahakikishe wanawalipa fidia kwa awamu ili kusiwe na usumbufu wakati bado hawajahamia katika nyumba wanazojengewa, ili kila mguswa ahamie kwenye nyumba yake akiwa na fedha za kujikimu na kuendeleza maisha yake.

“Tunaomba mkamilishe haraka utaratibu wa malipo ya fidia na yaende sambamba na uhamishaji wa wananchi na mlete hizo taarifa wizarani. Pia tunataka tujue ujenzi wa hizo nyumba unaanza lini na unaisha lini” alisema Dkt. Kiruswa. 

Alisema kuwa Rais Samia anatamani kuona utekelezaji wa mradi huo ukiendelea kwa kasi ili kutimiza lengo la kuanzishwa kwake, kwakuwa mgodi huo unazalisha miongoni mwa  madini ya kimkakati ambayo kwasasa mahitaji yake ni makubwa duniani.

Aliutaka mgodi huo kupeleka huduma zote muhimu kama shule, barabara na   maji,  katika maeneo utakaohamishia watu ili wapate huduma zote muhimu kwani ni haki za msingi. 






Posted by MROKI On Thursday, September 21, 2023 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo