Nafasi Ya Matangazo

March 16, 2024













Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde akiambatana na uongozi wa Tume ya Madini ameongoza Iftar iliyofanyika jijini Dodoma. Viongozi wengine walioshiriki katika Iftar hiyo ni pamoja na Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini,  Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu, Festus Mbwilo, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula, Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Eng. Yahya Samamba, Wakurugenzi, Mameneja, Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa na watumishi wa Tume ya Madini.

Akizungumza kwenye Iftar hiyo iliyoambatana na kuwaaga Makamishna wa Tume ya Madini wanaomaliza muda wao wakiongozwa na Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula Waziri Mavunde amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uteuzi wa Mwenyekiti wa Tume ya Madini na Makamishna walioleta mageuzi makubwa kwenye Sekta ya Madini, ikiwa ni pamoja na ongezeko la makusanyo ya maduhuli la kila mwaka pamoja na kuwa na vyanzo vile vile vya makusanyo.

" Tunawashukuru sana kwa mageuzi makubwa ambayo yamefanyika katika Sekta ya Madini, majina yenu tutayaandika kwa wino wa dhahabu," amesema Waziri Mavunde.

Katika hatua nyingine sambamba na kuwapongeza watumishi wa Tume ya Madini kwa mchango mkubwa kwenye uchumi wa madini amewataka kuendelea kuimarisha umoja, kufanya kazi kwa uzalendo na ubunifu ili kuendelea kuinua Sekta ya Madini.

Amesema kuwa Wizara ya Madini itaendelea kutoa ushirikiano na kutatua changamoto mbalimbali kwenye Sekta ya Madini.

Wakati huo huo Mwenyekiti wa Tume ya Madini Profesa Idris Kikula amepongeza kwa ushirikiano mkubwa ambao umekuwa ukitolewa na Wizara ya Madini kwenye usimamizi wa Sekta ya Madini sambamba na kutatua changamoto mbalimbali.

Katika hatua nyingine, Profesa Kikula amewataka Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na ubunifu ili Sekta ya Madini iendelee kuwa na mchango mkubwa kwenye ukuaji wa Pato la Taifa.

Naye  Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Eng. Yahya Samamba amempongeza Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula kwa usimamizi mzuri wa Tume hali iliyopelekea kuteuliwa kwa awamu ya Pili na Rais Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Amesema kuwa, chini ya uongozi wa Profesa Kikula mabadiliko makubwa yalipatikana ikiwa ni pamoja na ongezeko la ukusanyaji wa maduhuli kwa kila mwaka, mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa kuendelea kukua, ukuaji wa Sekta ya Madini kukua, uanzishwaji wa masoko ya madini na vituo vya ununuzi wa madini na ongezeko la ushiriki wa watanzania katika Sekta ya Madini kupitia maboresho ya Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini.

Amesisitiza kuwa Tume itaendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa ujenzi wa ofisi mpya, usambazaji wa vitendea kazi na uboreshaji wa maslahi ya watumishi.

Pia, zimetolewa zawadi kwa viongozi wa Kamisheni wanaomaliza muda wao. Awali kabla ya kuanza kwa Iftar, yamefanyika mafunzo kuhusu namna ya kujiandaa na maisha baada ya kustaafu kwa watumishi wa Tume.
Posted by MROKI On Saturday, March 16, 2024 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo