Nafasi Ya Matangazo

April 11, 2018

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina (katika) akizungumza na Mkurugenzi wa Kiwanda cha kuchinjia Punda Fang Hua, Lifang Yu, kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Uzalishaji wa Masoko wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Assimwe Lovince.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina akiangalia zizi la Punda na Mkurugenzi wa Kiwanda cha kuchinjia Punda Fang Hua, Lifang Yu aliye kushoto kwake.
Punda kwenye zizi la Kiwanda cha kuchinjia Punda Fang Hua mjini Shinyanga.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina (mwenye miwani) katika picha ya pamoja na watumishi wa Kiwanda cha kuchinjia Punda Fang Hua. Picha na John Mapepele.
****************************
Na John Mapepele, Shinyanga
WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amewahakikishia wenye viwanda nchini kuwa hakuna mali ya mifugo ya Tanzania itakayotoroshwa tena kwenda nje ya nchi kimagendo kwani Tanzania haiwezi kukubali kugeuzwa kuwa machungio ya mifugo hiyo.

Waziri Mpina ametoa kauli hiyo jana mjini Shinyanga baada ya kutembelea Kiwanda cha Fang Hua kinachojishughulisha na uchinjaji wa Punda ambapo alielezea kuridhishwa kwake na juhudi kubwa zilizofanywa na mwekezaji huyo kuwezesha kuwepo soko la uhakika la mifugo hiyo.

Mkurugenzi wa Kiwanda cha Fang Hua, Lifang Yu alimweleza Waziri Mpina kwamba kiwanda chake kimeshaingia ubia na wafugaji wadogo wapatao 27 ili kuongeza uzalishaji ambapo kinatarajia kuwashilikisha wafugaji wengi zaidi katika mikoa mbalimbali nchini

Waziri Mpina aliwahakikishia wawekezaji wenye viwanda katika sekta ya mifugo kuwa malighafi hiyo itakuwepo ya kutosha kwani Serikali ya awamu ya tano chini ya Dk. John Pombe Magufuli haitakubali tena mifugo hiyo kuendelea kutoroshwa nje ya nchi na kunufaisha viwanda vya nchi hizo.

Hivyo Waziri Mpina alisema uwekezaji wa aina hiyo wa kuongeza thamani ya mazao ya mifugo ni moja ya vipaumbele vya wizara yake kwa sasa ili kuchochea kwa kasi kufanikisha azma ya Tanzania ya viwanda.

Alisema kiwanda hicho mbali na kuongeza soko la punda pia kimechangia kuchochea uchumi wa Mkoa wa Shinyanga pamoja na kutatua changamoto ya ajira ambapo hadi sasa kimeajiri wafanyakazi 100 hivyo alimhakikishia mwekezaji huyo kuwa changamoto ya punda wengi kutoroshwa nchini Kenya haitakuwepo tena.

Alisema kwa sasa kuna viwanda viwili vya kuchakata nyama ya punda na kuuza nchini China, ambapo wastani wa mauzo ya nyama hiyo nje ya nchi yalifikia tani 2000 mwaka 216/17

Mpina aliwahimiza wawekezaji hao kuhakikisha wanawasaidia wafugaji katika kuongeza uzalishaji, kupambana na maradhi, upatikanaji wa maji na malisho kwa mifugo.

Aliwataka kuanzisha ranchi ya mifugo na maeneo yakupumzishia mifugo hiyo kabla ya kuchinjwa.

Alisema idadi ya punda waliopo nchini ni 520,000 tu hivyo juhudi za makusudi zinahitajika kuongeza uzalishaji.

Kaimu Mkurugenzi wa Uzalishaji Mifugo na Masoko wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Lovince Assimwe aliwataka wafugaji kuongeza soko la uhakika.

Alipongeza uongozi wa kiwanda hicho kwa kubuni mbinu za kuwasaidia wafugaji kwa kuwapatia shilingi elfu tano kila mwezi kwa ajili ya matibabu ya punda.
Posted by MROKI On Wednesday, April 11, 2018 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo