Nafasi Ya Matangazo

April 05, 2012

IDADI kubwa ya wagonjwa waliokwenda kutafuta tiba kwa Mchungaji mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambilikile Mwaisapile, Loliondo wamepoteza maisha.

Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ambayo sasa itatangaza matokeo ya utafiti wa tiba hiyo ya ‘Kikombe cha Babu’ imesema wengi ni wale wenye Ukimwi walioacha matumizi ya dawa za kurefusha maisha (ARVs).


Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Regina Kikuli, aliiambia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) jana Dar es Salaam, kwamba hadi sasa Serikali inafanyia utafiti watu 206 ambao walipata kikombe hicho.


Utafiti unaofanywa na Wizara hiyo inataka kubaini kama kweli dawa hiyo ina uwezo wa kuponya Ukimwi, kisukari, saratani na magonjwa mengine sugu. Wanaofanyiwa utafiti huo walipata ‘kikombe’ hicho baada ya kuugua kisukari na Ukimwi.


“Kwa sasa ni vigumu kusema dawa hiyo inaponya au haiponyi, tusubiri utafiti wa kitaalamu. “Baada ya miezi miwili tutatangaza matokeo kwa umma,” alisema Kikuli na kuongeza kuwa utafiti huo unafanywa katika hospitali mbalimbali nchini chini ya usimamizi wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR).


Utafiti huo unafanywa katika hospitali za Bugando, Mwanza; Mbeya; Mount Meru, Arusha; Hydom, Manyara na KCMC, Kilimanjaro. Hospitali hizo ziko maeneo ambayo wananchi wengi walijitokeza kupata ‘kikombe’ Loliondo. Kikuli pia alisema kwa sasa idadi ya Watanzania wanaokwenda Loliondo kupata tiba hiyo imepungua; lakini bado wananchi wa kutoka Kenya na nchi zingine wanaendelea kwenda kupata ‘kikombe’ hicho.


Hata hivyo, Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali, Donan Mmbando, alikiri kuwa wagonjwa wengi wa Ukimwi waliokwenda kupata tiba hiyo na kuachana na ARVs wamepoteza maisha. Mbunge wa Nkasi, Ali Kessy Mohamed (CCM), aliishauri Wizara hiyo kuacha siasa badala yake iwaambie wananchi kwamba dawa ya Babu wa Loliondo haina madhara kwa binadamu, lakini pia haina uwezo wa kuponya magonjwa.


“Msiogope kusema kama wanasiasa, ninyi ni wataalamu, ni kweli kuwa ile dawa haina madhara kama yalivyo maji, lakini tusidanganyane, haitibu, kwa nini mnaendelea kudanganya wananchi?” Alihoji Mbunge huyo. Makamu Mwenyekiti wa PAC, Zainab Vullu, ndiye aliyetaka Wizara itoe taarifa ya utafiti wa tiba ya ‘kikombe cha Babu’. 
SOURCE: HABARILEO
Posted by MROKI On Thursday, April 05, 2012 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo