Sehemu ya Mahakimu na Watumishi wengine wa Mahakama mpya za Wilaya 18 wakifuatilia kwa makini mada iliyokuwa ikitolewa na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt (hayupo katika picha) aliyekuwa akitoa mada ya wajibu na Majukumu ya Mahakama ya Wilaya. Mada hiyo ametoa jana tarehe 29 Novemba, 2022 kwenye Ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro.
Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt (aliyesimama) akiwasilisha Mada ya wajibu na Majukumu ya Mahakama ya Wilaya kwa Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya 18.
Mkurugenzi wa Idara ya Nyaraka na Kumbukumbu- Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula akitoa mada ya Utunzaji na matumizi sahihi ya Kumbukumbu na matumizi ya ofisi mtandao ‘e-office’ kwa Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya 18 zilizozinduliwa hivi karibuni.
Washiriki wakimsikiliza mtoa mada (hayupo katika picha).
Washiriki wakimsikiliza mtoa mada (hayupo katika picha).
Mchumi Mwandamizi kutoka Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Bi. Felister Fatukubonye akiwasilisha mada ya Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama kwa Washiriki wa Mafunzo ya Huduma kwa Mteja yanayofanyika kwenye Ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro.
Mkurugenzi Msaidizi kutoka Kitengo cha Maboresho-Mahakama ya Tanzania, Bw. Daniel Msangi akichangia mada ya Mradi wa uboreshaji wa huduma za Mahakama iliyotolewa na Bi. Felister.**********
Na Mary Gwera,
Mahakama-Morogoro
Watumishi wa Mahakama mpya za
Wilaya 18 zilizozinduliwa hivi karibuni wanaendelea kupatiwa mada mbalimbali za
kuboresha utendaji kazi wao katika Mafunzo yanayoendelea kutolewa kwenye Ukumbi
wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro.
Ikiwa ni siku ya pili ya
mafunzo hayo, jana tarehe 29 Novemba, 2022 mada zilizotolewa ni pamoja na;
Wajibu na Majukumu ya Mahakama za Wilaya, Utunzaji na matumizi sahihi ya
Kumbukumbu na matumizi ya ofisi mtandao ‘e-office’, Mradi wa Uboreshaji wa
Huduma za Mahakama.
Akiwasilisha Mada ya Wajibu na
Majukumu ya Mahakama ya Wilaya, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe.
Sharmillah Sarwatt amewataka Watumishi wa Mahakama hizo kuwathamini wananchi
ambao ndio wateja wanaosababisha wao kuwa kazi, hivyo huduma zitakazotolewa ziwe
za viwango.
“Nadhani hapa wote mnafahamu
majukumu ya Mahakama mnazofanyia kazi, hivyo tuko hapa kwa ajili ya
kukumbushana ili kutoa huduma bora zaidi, ni matumaini yangu na Mahakama kwa
ujumla kuwa mtaboreshaji utendaji kazi wenu kwa kufanya kazi kwa bidii ili
kutimiza jukumu kuu la Mahakama la kutoa haki,” amesema Mhe. Sarwatt.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa
Idara ya Nyaraka na Kumbukumbu- Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula
amewaasa Watumishi hao kuzingatia utunzaji sahihi wa nyaraka mbalimbali za
ofisi na kuwaasa kutunza siri za ofisi na za wateja.
Akiwasilisha mada ya Mradi wa
Uboreshaji wa Huduma za Mahakama, naye Mchumi Mwandamizi kutoka Kitengo cha
Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Bi. Felister Fatukubonye amewaeleza
washiriki wa Mafunzo hayo kuwa Mahakama ya Tanzania inatekeleza Mpango Mkakati
wake wa mwaka 2020/2021-2024-2025, ambapo amewaeleza Watumishi hao kuwa
Mahakama ya Tanzania bado inaendelea na uboreshaji wa huduma mbalimbali zenye
lengo la kuhakikisha kuwa huduma ya utoaji haki inamfikia mwananchi kwa
urahisi.
Aidha, Bi. Felister amesema
kuwa, ili jitihada za Mahakama, Serikali na Wafadhili ziweze kuzaa matunda
kunahitajika ushirikiano wa pamoja ikiwemo watumishi kubadili mtazamo na fikra
ili uboreshaji za miundombinu na kadhalika viweze kwenda sambamba na utoaji
huduma bora kwa wananchi.
Mafunzo haya ya Huduma kwa
mteja yanaendelea kutolewa na Watumishi hao mpaka tarehe 02 Desemba, 2022 na
mada nyingine zitatolewa ikiwemo Jinsi ya kukabiliana na msongo (Stress
Management) na kadhalika.
Tarehe 25 Novemba, 2022 Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alizindua Mahakama ya Wilaya
Busega iliyowakilisha Mahakama nyingine mpya za Wilaya mpya 17, Mahakama hizo
zilizojengwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia ni pamoja na; Butiama, Rorya,
Songwe, Gairo, Mkinga, Mvomero, Kilombero, Mbogwe, Nyang'hwale, Kyerwa,
Itilima, Missenyi, Kaliua, Uvinza, Buhingwe, Kakonko na Tanganyika.
0 comments:
Post a Comment