Waziri Mkuu Kassim Majaliwa,
akizungumza wananchi wa Kata ya Mauno wilayani Kondoa, akiwa kwenye
ziara yake ya kikazi Mkoani Dodoma, Septemba 20, 2018.Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu
……………………..
*Akerwa na tabia ya kupokea fedha na kutopeleka vifaa, dawa
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa
amesema hataki kuona tabia ya kupokea fedha na kuchelewa kupeleka vifaa
inayofanywa na Bohari ya Madawa (MSD) ikiendelea.
“MSD ninawatahadharisha
wasirudie kosa la kupokea fedha na kutopeleka dawa na vifaa tiba. Ofisi
zao ziko hapo Dodoma mjini, ni kwa nini mnachelewa kuleta vifaa hivyo,”
amehoji.Ametoa onyo hilo leo mchana
(Alhamisi, Septemba 20, 2018) wakati akizungumza na wakazi wa kata ya
Mauno, wilayani Kondoa ambako alienda kukagua ujenzi wa kituo cha afya
na kuelezwa kuwa MSD imekuwa ikichelewa kuleta dawa. Waziri Mkuu jana ameanza ziara ya kikazi ya siku saba katika mkoa wa Dodoma.
Amesema Serikali ilitoa sh.
milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya na kwamba baada
ya ukaguzi ameridhika na kazi inayofanyika. Hata hivyo, amemtaka
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo pamoja na madiwani wahakikishe wanatenga
fedha kwa ajili ya ujenzi wa wodi mbili za wagonjwa wa kawaida wa kike
na wa kiume.
“Hapa mna kituo cha afya,
hospitali ya wilaya iko Kondoa mjini ambako ni km.62 kutoka hapa.
Tengeni fedha za kujenga hizo wodi ili watu walazwe hapahapa.
Halmashauri mnao uwezo wa kujenga hizo wodi mbili. Nataka nione mnaanza
na nipate taarifa kuwa mmeanza ujenzi huo,”
amesisitiza.
“Mwenyekiti wa Halmashauri na
madiwani kaeni na mfanye hiyo kazi. Nikisema muanze maana yake ni
kuanza. Tunataka wana-Mauno watibiwe hukuhuku na hakuna haja ya
kuwasumbua wananchi kwenda hadi Kondoa mjini. Mkimaliza ujenzi,
mtuambie, tutaleta sh. milioni 250 za kununua vifaa vya ndani.”
Amesema Serikali inaimarisha
huduma za afya kwa kujenga zahanati na kuimarisha vituo vya afya ambapo
hadi kufikia Agosti mwaka huu, jumla ya vituo vya afya 209 vilikuwa
vimekwishajengwa hapa nchini.Amesema kila mwezi, Serikali
inapeleka wilayani humo sh. milioni 25 kwa ajili ya ununuzi wa dawa
kuanzia hospitali ya wilaya, vituo vya afya na zahanati na akawaonya
waganga na wauguzi wasiziguse dawa hizo kwa sababu zimelenga kuwasaidia
wananchi.
Mapema, akizungumza na
wananchi hao, Naibu Waziri wa Fedha, Dk. Ashatu Kijaji ambaye pia ni
mbunge wa jimbo la Kondoa, aliishukuru Serikali ya awamu ya tano kwa
kuimarisha huduma za afya wilayani humo ambapo katika kipindi cha miaka
mitatu, wameweza kuwa na vituop vya afya vitano.
“Katika kipindi cha miaka 40,
tulikuwa na vituo vya afya vitatu tu lakini ndani ya miaka mitatu,
tumefikisha vituo vya afya vitano. Alivitaja vituo hivyo kuwa ni Mauno,
Busi, Bereko, Kalamba na Thawi.Waziri Mkuu anaendelea na ziara yake wilayani Kondoa ambako atazungumza na wananchi.
0 comments:
Post a Comment