Nafasi Ya Matangazo

September 21, 2018




 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akizungumza wananchi wa Kata ya Mauno wilayani Kondoa, akiwa kwenye ziara yake ya kikazi Mkoani Dodoma, Septemba 20, 2018.Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu
……………………..

*Akerwa na tabia ya kupokea fedha na kutopeleka vifaa, dawa

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema hataki kuona tabia ya kupokea fedha na kuchelewa kupeleka vifaa inayofanywa na Bohari ya Madawa (MSD) ikiendelea.

“MSD ninawatahadharisha wasirudie kosa la kupokea fedha na kutopeleka dawa na vifaa tiba. Ofisi zao ziko hapo Dodoma mjini, ni kwa nini mnachelewa kuleta vifaa hivyo,” amehoji.Ametoa onyo hilo leo mchana (Alhamisi, Septemba 20, 2018) wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Mauno, wilayani Kondoa ambako alienda kukagua ujenzi wa kituo cha afya na kuelezwa kuwa MSD imekuwa ikichelewa kuleta dawa. Waziri Mkuu jana ameanza ziara ya kikazi ya siku saba katika mkoa wa Dodoma.

Amesema Serikali ilitoa sh. milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya na kwamba baada ya ukaguzi ameridhika na kazi inayofanyika. Hata hivyo, amemtaka Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo pamoja na madiwani wahakikishe wanatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa wodi mbili za wagonjwa wa kawaida wa kike na wa kiume.

“Hapa mna kituo cha afya, hospitali ya wilaya iko Kondoa mjini ambako ni km.62 kutoka hapa. Tengeni fedha za kujenga hizo wodi ili watu walazwe hapahapa. Halmashauri mnao uwezo wa kujenga hizo wodi mbili. Nataka nione mnaanza na nipate taarifa kuwa mmeanza ujenzi huo,” 
amesisitiza.

“Mwenyekiti wa Halmashauri na madiwani kaeni na mfanye hiyo kazi. Nikisema muanze maana yake ni kuanza. Tunataka wana-Mauno watibiwe hukuhuku na hakuna haja ya kuwasumbua wananchi kwenda hadi Kondoa mjini. Mkimaliza ujenzi, mtuambie, tutaleta sh. milioni 250 za kununua vifaa vya ndani.”

Amesema Serikali inaimarisha huduma za afya kwa kujenga zahanati na kuimarisha vituo vya afya ambapo hadi kufikia Agosti mwaka huu, jumla ya vituo vya afya 209 vilikuwa vimekwishajengwa hapa nchini.Amesema kila mwezi, Serikali inapeleka wilayani humo sh. milioni 25 kwa ajili ya ununuzi wa dawa kuanzia hospitali ya wilaya, vituo vya afya na zahanati na akawaonya waganga na wauguzi wasiziguse dawa hizo kwa sababu zimelenga kuwasaidia wananchi.

Mapema, akizungumza na wananchi hao, Naibu Waziri wa Fedha, Dk. Ashatu Kijaji ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Kondoa, aliishukuru Serikali ya awamu ya tano kwa kuimarisha huduma za afya wilayani humo ambapo katika kipindi cha miaka mitatu, wameweza kuwa na vituop vya afya vitano.

“Katika kipindi cha miaka 40, tulikuwa na vituo vya afya vitatu tu lakini ndani ya miaka mitatu, tumefikisha vituo vya afya vitano. Alivitaja vituo hivyo kuwa ni Mauno, Busi, Bereko, Kalamba na Thawi.Waziri Mkuu anaendelea na ziara yake wilayani Kondoa ambako atazungumza na wananchi.
Posted by MROKI On Friday, September 21, 2018 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo