Nafasi Ya Matangazo

June 09, 2026




Dodoma
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inatarajia kuadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake kwa hafla maalum itakayofanyika Julai 1, 2026, sambamba na utoaji wa Tuzo za Rais kwa Walipakodi Bora wa Mwaka wa Fedha 2024/2025.

Akizungumza jijini Dodoma kwa niaba ya Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Yusuph Juma Mwenda, Mkurugenzi wa Elimu kwa Mlipakodi na Mawasiliano wa TRA, Bw. Richard Kayombo, amesema maadhimisho hayo yatafanyika chini ya kaulimbiu isemayo, “_*Miongo Mitatu ya TRA, Mlipakodi Shujaa, Tanzania Inayojitegemea*_.”

Bw. Kayombo amesema maadhimisho hayo yanalenga kuenzi mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 30 tangu TRA ianzishwe mwaka 1996, pamoja na kuendelea kuhamasisha ulipaji kodi kwa hiari na kuimarisha ushirikiano kati ya TRA na walipakodi.

Ameeleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atatoa Tuzo za Walipakodi Bora wa Mwaka wa Fedha 2024/2025 kwa walipakodi walioonyesha uadilifu, uwajibikaji na mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa kupitia ulipaji wa kodi.

Aidha, amesema tuzo hizo ni njia ya kutambua na kuthamini mchango wa walipakodi katika kugharamia huduma za kijamii, utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kukuza uchumi wa nchi katika nyanja mbalimbali. Amebainisha kuwa maendeleo yanayoonekana katika sekta za afya, elimu, miundombinu na huduma nyingine za umma yanategemea kwa kiasi kikubwa mapato yatokanayo na kodi.

TRA imewataka walipakodi na Watanzania kwa ujumla kuendelea kutimiza wajibu wao wa kodi kwa hiari na kwa wakati ili kuendelea kuchochea maendeleo ya Taifa na kujenga Tanzania yenye uchumi imara na endelevu.
Posted by MROKI On Tuesday, June 09, 2026 No comments




Dar es Salaam
Waziri wa Madini, Mh. Anthony Mavunde (Mb) amewataka Wanazuoni kuwa sehemu ya upatikanaji wa suluhu ya utatuzi wa changamoto za kusaidia kuendeleza sekta ya madini ili iweze kukua zaidi na kuleta manufaa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Ameyasema hayo leo tarehe 09 Juni, 2026 Jijini Dar es Salaam alipokuwa akifungua Wiki ya 11 ya Ubunifu na Utafiti iliyoandaliwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

"Ninawashukuru sana kwa kunialika kuja mahali hapa kushuhudia miradi na programu mbalimbali ambazo zimekuwa chachu ya kusaidia si tu ajira kwa wahitimu, bali suluhisho ya changamoto mnalimbali kwenye sekta yetu ya madini"

"Mheshimiwa Rais ametuelekeza kuweka mkazo katika kusaidia upatikanaji wa ajira kwa vijana. Sisi sekta ya madini tunapoona jitihada hizi mnazofanya hapa Chuoni tunapata faraja kubwa na tupo tayari kuwaunga mkono ili ziwe na tija zaidi" amesisitiza Mhe. Mavunde.

Aidha, Waziri Mavunde amebainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi thabiti wa Mhe. Rais Dkt. Samia imeweka kipaumbele kwenye utafiti wa kina wa madini, ambapo kupitia Vision 2030 Madini ni Maisha na Utajiri tumejipanga kuhakikisha tunaongeza eneo lililofanyiwa utafiti wa kina kutoka asilimia 16 hadi asilimia 50 ifikapo mwaka 2030.

Vilevile, Mhe. Mavunde amepongeza programu ya Chuo kikuu cha Dar es salaam(UDSM) ya ubunifu na utafiti ambayo imewezesha vijana wengi kujiajiri na kusisitiza kwamba Vyuo Vikuu kupitia taaluma yao vinaweza kuwa ni kichocheo kikubwa cha ukuaji wa sekta ya madini kupitia tafiti zenye lengo la kutafuta suluhu za changamoto za sekta hiyo.

Pia, Mavunde amebainisha kwamba pamoja na kuwa zipo bado changamoto kadhaa kwenye sekta, lakini ni ukweli usiopingika kuwa tumepiga hatua kubwa na kutoa mfano wa mchango wa sekta ya madini kwenye pato la taifa umeongezeka na kufikia asilimia 10.1 mwaka 2024, mwaka mmoja kabla ya mwaka wa lengo wa 2025.

Awali, akitoa maelezo kuhusiana na Wiki ya 11 ya Ubunifu na Utafiti, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam anayeshughulikia Utafiti, Prof. Nelson Boniface alibainisha kuwa maonesho hayo ni ya 11 kufanyika tangu walipoanza mwaka 2015 na yameweza kuibua mawazo bunifu mengi kwa wanafunzi yanayopelekea kujiajiri na kujipatia kipato pasipo kutegemea kuajiriwa.

Akieleza kwa kifupi kuhusiana na MoU waliyosaini na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Meneja Mkazi wa Kampuni ya Barrick Tanzania, Dkt. Melkiory Ngido ameishukuru Serikali kwa namna inavyoendelea kushirikiana na Kampuni yao na kusisitiza kwamba Barrick itaendelea kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ili bunifu na tafiti mbalimbali ziweze kufanyika na kuleta tija kwenye sekta ya madini nchini.

Naye, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Prof. William Anangisye ameeleza kuwa tangu kuanzishwa kwake, Wiki ya Ubuntu na Utafiti imeendelea kuchochea ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, Sekta binafsi kupitia wadau kama kampuni, taasisi za fedha na wadau wengine. 

Aidha, amebainisha kuwa kupitia kauli mbiu ya Mwaka huu wanataraji kuhakikisha taaluma inayozalishwa chuoni hapo inaingia kwenye sera na kupelekea matumizi ya teknolojia katika uvunaji wa rasilimali zetu kwa maslahi ya kizazi cha sasa na cha baadae.
Posted by MROKI On Tuesday, June 09, 2026 No comments









Mke wa Rais wa Singapore, Mheshimiwa Mama Jane Ittogi Shanmugaratnam, ametembelea kituo cha uzalishaji nguo za pamba zinazotengenezwa kwa mikono Msasani jijini Dar es Salaam na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanyika katika eneo hilo. 

Akiwa katika kituo hicho, Mheshimiwa Mama Jane Ittogi Shanmugaratnam alitembelea maeneo tofauti ya uzalishaji na kushuhudia hatua mbalimbali za uchakataji wa pamba hadi kufikia utengenezaji wa nguo bora zinazozingatia ubora wa hali ya juu na utunzaji wa mazingira.

Akiwa katika kituo hicho, alielezwa namna wafanyakazi wa kiwanda hicho wanavyotumia ujuzi wa jadi pamoja na teknolojia za kisasa kuzalisha bidhaa za pamba zinazokidhi mahitaji ya masoko ya ndani na kimataifa. 

Mheshimiwa Mama Jane alionesha kufurahishwa na ubunifu, ustadi na juhudi zinazofanywa na watumishi wa kiwanda hicho kidogo na wanavyotumia malighafi za ndani na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa kimataifa unaolenga kukuza biashara, uwekezaji na maendeleo endelevu.

Rais wa Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam na mwenza wake wako nchini kwa ziara ya siku tatu ya kitaifa ikilenga kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Singapore.
Posted by MROKI On Tuesday, June 09, 2026 No comments
Katika kuhakikisha usafi wa mazingira unaimarishwa nchini, Serikali imeendelea kuhamasisha uwekezaji katika sekta ya usimamizi wa taka hususan taka ozo zinazozalishwa katika vyanzo mbalimbali kama hoteli, masokoni na majumbani.

Akijibu maswali bungeni jijini Dodoma leo Juni 09, 2026, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa amesema hadi kufikia Aprili, 2026 jumla ya viwanda sita vimeanzishwa kwa ajili ya kuchakata na kurejelesha taka ozo.

Mhe. Reuben Kwagilwa amesema katika kufanikisha hatua hiyo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) zimeendelea kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya uhifadhi wa mazingira ikiwemo udhibiti wa taka.
 
Amesema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Lucy Edward Mwakyembe aliyetaka kujua Serikali kwa kushirikiana na Majukwaa ya Kimataifa (COP) na kamati za Kimataifa (NDC) itasimamiaje uchakataji wa taka na matumizi ya nishati kwenye hoteli.

Akiendelea kujibu swali hilo, Mhe. Kwagilwa alisema Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi mwanachama wa Mikataba mbalimbali ya kuhifadhi mazingira na mabadiliko ya tabinchi ambapo kupitia mikataba hii, Tanzania imekuwa ikishiriki katika mikutano ya Kimataifa ya Nchi Wanachama (COP).
Alifafanua kuwa Serikali inaendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Usimamizi wa Taka wa miaka mitano (2025 – 2030) wenye lengo la kuimarisha mfumo wa usimamizi wa taka kwa dhana ya uchumi rejeshi ambapo taka zinazozalishwa zinaweza kutumika tena kama malighafi viwandani.

Aidha, Mhe. Kwagilwa alilieleza Bunge kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi mwanachama wa Mikataba mbalimbali ya kuhifadhi mazingira na mabadiliko ya tabinchi ambapo kupitia mikataba hii, Tanzania imekuwa ikishiriki katika mikutano ya Kimataifa ya Nchi wanachama (COP).

Alisema kuwa kupitia mikutano hiyo ya kimataifa, Tanzania imeendelea kuchangamkia fursa kwa kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya uhifadhi wa mazingira ikiwemo udhibiti wa taka zinazozalishwa katika maeneo mbalimbali nchini hatua inayosaidia pia kusafisha mazingira.

Sanjari na hilo, aliongeza kuwa kupitia makubaliano ya Paris, Tanzania imeandaa Mchango wa Taifa wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (Nationally Determined Contribution, NDC) ambao umebadilisha eneo la udhibiti wa taka kama mojawapo ya vipaumbele vya kupunguza uzalishaji wa hewa ya Kaboni.

Kadhalika, Naibu Waziri huyo amebainisha kuwa SJMT na SMZ pia zinashirikiana katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwenye taasisi zinazohudumia watu zaidi ya 100 ikiwemo ya gesi ili kuachana na kuni na mkaa ambao unatokana na ukataji wa miti kwa wingi.
 
Alisema hamasa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia imemfanya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassn kuwa ni kinara wa nishati safi na uhifadhi wa mazingira ndani ya nchi, Afrika Mashariki na duniani.
 
Hivyo, tayari Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira (ZEMA) zilisaini makubalinao ya ushirikiano katika masuala mbalimbali ikiwemo uchakataji wa taka.
 
Posted by MROKI On Tuesday, June 09, 2026 No comments



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mhe. Tharman Shanmugaratnam akisaini Kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mhe Tharman Shanmugaratnam akizungumza na Waandishi wa Habari kufuatia Ziara yake ya Kitaifa Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.




Posted by MROKI On Tuesday, June 09, 2026 No comments
Kaimu Kamishna, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, Wizara ya Fedha, ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo, Bw. Bashiru Taratibu, akizungumza wakati akifungua mafunzo kuhusu Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne 2023-2030, yaliyoandaliwa na Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu ,Wizara ya Fedha, yaliyofanyika katika ukumbi wa Hazina Ndogo, jijini Arusha.
Mkaguzi Mkuu wa Ndani, Wizara ya Fedha, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo, Bw. Evaristo Mwalongo (katikati) akiwa na Kaimu Kamishna, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, Wizara ya Fedha, na mjumbe wa Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo, Bw. Bashiru Taratibu (kulia) na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Utawala, Wizara ya Fedha, na katibu wa Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo, Bw. Simbani Liganga, wakifuatilia mada wakati wa mafunzo kuhusu Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne 2023-2030, yaliyoandaliwa na Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu, Wizara ya Fedha, yaliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Hazina Ndogo, jijini Arusha.
Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Utawala, Wizara ya Fedha, na Katibu wa Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo, Bw. Simbani Liganga, akifafanua jambo wakati wa mafunzo kuhusu Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne 2023-2030, yaliyoandaliwa na Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu, Wizara ya Fedha, yaliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Hazina Ndogo, jijini Arusha.
Afisa Uchunguzi Kiongozi Msaidizi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Bw. John Shija, akiwasilisha mada kuhusu Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne 2023-2030, katika mafunzo ya Kamati ya Uadilifu ya Wizara ya Wizara ya Fedha, yaliyoandaliwa na Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu, Wizara hiyo, yaliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Hazina Ndogo, jijini Arusha.

Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Utawala, Wizara ya Fedha, na Katibu wa Kamati ya Uadilifu, Bw. Simbani Liganga (kushoto) na Kaimu Kamishna, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, Wizara ya Fedha, na mjumbe Kamati ya Uadilifu ya Wizara, Bw. Bashiru Taratibu, wakifuatilia mada wakati wa mafunzo kuhusu Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne 2023-2030, yaliyoandaliwa na Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu, Wizara ya Fedha, yaliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Hazina Ndogo, jijini Arusha.
Baadhi ya maafisa kutoka Wizara ya Fedha, wakifuatilia mada wakati wa mafunzo ya Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo kuhusu Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne 2023-2030, yaliyoandaliwa na Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu, Wizara ya Fedha, yaliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Hazina Ndogo, jijini Arusha.
Baadhi ya maafisa kutoka Wizara ya Fedha, wakifuatilia mada wakati wa mafunzo ya Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo kuhusu Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne 2023-2030, yaliyoandaliwa na Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu, Wizara ya Fedha, yaliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Hazina Ndogo, jijini Arusha.
Kaimu Kamishna, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, Wizara ya Fedha, na mjumbe wa Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo, Bw. Bashiru Taratibu (mstari wa mbele katikati), Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Utawala, Wizara ya Fedha, na Katibu wa Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo, Bw. Simbani Liganga (kulia) na Afisa Uchunguzi Kiongozi Msaidizi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Bw. John Shija (kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na washiriki, baada ya mafunzo kuhusu Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne 2023-2030, yaliyoandaliwa na Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu, Wizara ya Fedha, yaliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Hazina Ndogo, jijini Arusha.
**************
Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu Wizara ya Fedha, imeendesha mafunzo kwa Kamati ya Uadilifu ya Wizara hiyo kuhusu Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne (2023– 2030), ambayo yatasaidia kuwapa washiriki uelewa wa kusimamia Mpango wa utekelezaji wa Mkakati huo wa Wizara.

Mkakati wa Taifa Dhidi ya Rushwa na Mpango wa Utekelezaji Awamu ya Nne - NACSAP IV (2023– 2030) unaweka mfumo wa kitaifa unawaongoza watekelezaji wote wanaohusika na ukunzaji wa uadilifu na juhudi dhidi ya rushwa ili kujenga jamii yenye uadilifu na isiyovumilia vitendo vya rushwa.

Akizungumza wakati akiwakaribisha washiriki katika mafunzo hayo, Kaimu Kamishna, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi kutoka Wizara ya Fedha, ambaye pia ni mjumbe wa kamati hiyo, Bw. Bashiru Taratibu, alisema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kujengewa uwezo kwenye masuala yanayohusiana na mpango wa utekelezaji wa mkakati, kukuza uadilifu, kuzuia na kupambana na vitendo vya rushwa katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara.

Aliwasisitiza washiriki kuzingatia mada mbalimbali zitakazowasilishwa wakati wa mafunzo hayo ambayo matokeo yake yanatarajiwa kuwa nyenzo muhimu katika kutekeleza majukumu yao.

Mafunzo hayo yaliyohusisha watumishi wa Wizara ya Fedha kutoka Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali watu, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani pamoja na Idara ya Mifumo ya Usimamizi wa Fedha na Huduma za Tehama, yamefanyika katika ukumbi wa mikutano wa Hazina Ndogo, jijini Arusha.
Posted by MROKI On Tuesday, June 09, 2026 No comments

June 08, 2026








Na, mwandishi wetu – Dar es Salaam
SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imeingia Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) na Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) yenye lengo la kuimarisha usimamizi wa maafa nchini kwa kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu.

Akizungumza mapema hii leo (08 Juni, 2026) katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Dkt. Jim Yonazi, amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa  Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kujenga mifumo madhubuti ya kiutendaji inayoongozwa na maarifa, sayansi na teknolojia ikiwemo matumizi ya Akili Unde (AI) katika kukabiliana na maafa.

Amesema makubaliano hayo yanatekeleza pia mapendekezo ya Mkutano wa Nane wa Umoja wa Mataifa wa Jukwaa la Dunia la Upunguzaji wa Vihatarishi vya Maafa uliofanyika Geneva, Uswisi, mwezi Juni 2025, na yanaashiria mabadiliko ya kimkakati katika namna Serikali inavyoshughulikia changamoto za maafa kutoka mfumo wa kusubiri majanga hadi mfumo wa kujikita katika kinga, maandalizi na tahadhari.

“Vyuo vikuu na taasisi za utafiti, ikiwemo Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam, zina jukumu muhimu la kuzalisha maarifa na suluhisho za kisayansi zitakazosaidia kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini,”amesema.

Ameongeza kuwa ili kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa makubaliano hayo, Serikali itaandaa Mpango Kazi wa utekelezaji pamoja na Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Usimamizi wa Maafa itakayobainisha maeneo ya kipaumbele yanayohitaji ufumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia.

Dkt. Yonazi amesisitiza kuwa mafanikio ya makubaliano hayo yatapimwa kwa matokeo halisi yatakayochangia kuongeza usalama wa wananchi, kulinda rasilimali za taifa na kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa.

Ushirikiano huo unaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoweka msisitizo katika matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nguzo kuu ya maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii.

Kwa upande wake Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam Prof.Preksedis Marco Ndomba amesema kuwa taasisi imeandika historia kwa kusaini hati ya ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu ambapo ameeleza kuwa mchakato huu ulianza muda mrefu na matunda yake yameanza kuonekana jambo ambalo ni mafanikio makubwa.

“Tunaahidi juu ya kufanikisha  makubaliano hayo kwa kuwa, uwezo huo tunao, utalaam upo wa kutosha kwa kushirikiana kwenye masuala ya viatarishi kitaifa ili kufanikisha adhima hii ya Serikali,” Alisema Profesa Ndomba.
Posted by MROKI On Monday, June 08, 2026 No comments
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu (mwenye suti), akiwa na Kiongozi Mkuu wa Buddha hapa nchini, Mchungaji Dkt.  Ilukuptiye  (kushoto) na Mchungani Xianhong, wakielekea eneo la sherehe za kuachimisha siku ya kuzaliwa ya dini hiyo, na uzinduzi wa Sanamu ya Golden Buddha Upanga jijini Dar es Salaam Juni 7, 2026.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu (mwenye suti), akiwa na Kiongozi Mkuu wa Buddha hapa nchini, Mchungaji Dkt.  Ilukuptiye  Pannasekara na viongozi wengine, wakati akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Sanamu ya Buddha kwenye temple la dini hiyo Upanga jijini Dar es Salaam, Juni 7, 2026.a



Na: Mwandishi wetu - Dar es Salaam, Juni 7, 2026
Kiongozi Mkuu wa dini ya Buddha nchini, Mchungaji Dkt. Ilukuptiye Pannasekara, amesifu ushirikiano ambao wanaupata sio tu kutoka katika dini zingine bali pia serikalini kwa ujumla.

Ametoa kauli hiyo wakati wa kusherehekea siku ya kuzaliwa kwa kiongozi wa dhehebu la Buddha duniani na uzinduzi wa sanamu ya dhahabu ya Buddha (Golden Buddha Statue) eneo la Upanga jijini Dar es Salaam Juni 7, 2026, ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu, akimwakilisha Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba.

Alisema, amekuwa akipata ushirikiano mkubwa kutoka dini nyingine hapa nchini na hivyo kuwafanya waumuni wa Buddha kujisikia furaha.

“Kutokana na mazingira hayo mazuri, tuna jumla ya miradi mitano  kwenye sekta za elimu, utalii na afya, miradin hii tayari mingine imeanza na mingine iko katika hatua mbalimbali.” Alisema.

“Hatuhitaji usaidizi wa fedha kutoka serikalini, tunahitaji ushirikiano, miradi hii mitano ni ya uhakika, italeta zaidi ya dola za kimarekani milioni 100 kwenye uchumi wa Tanzania, alisema Mchungaji Dkt. Pannasekara.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amewahakikishia kuwa Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wake, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kutoa ushirikiano kwa dini zote bila kuwepo kwa ubaguzi.

Amesema Muelekeo wa serikali inapoanza utekelezaji wa dira ya Maendeleo ya 2050 imefungua milango ya kidiplomasia ili kuwaalika wawekezaji kuwekeza hapa nchini.

“Kama serikali tumewahakikishia kuwa kupitia Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji tumewahakikishia kwamba watakapokuwa tayari tutawepeleka kwenye maeneo ya kimkakati ili kutekeleza miradi yao katika sekta za Utalii, Afya na Elimu.” Alisema.
Posted by MROKI On Monday, June 08, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo