Nafasi Ya Matangazo

April 23, 2026










Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Imeelezwa kwamba Serikali kupitia Wizara ya Madini na Taasisi zake itaendelea kuwawezesha kwa kuwajengea uwezo  wanawake, vijana na watu wenye uhitaji maalum kwa kuwapatia  vifaa vya uchimbaji , mitambo ya uchorongaji miamba na kuwapatia maeneo ya leseni yaliyofanyiwa utafiti wa kina ili kuwaendeleza na uchimbaji bora na wenye tija bila kupoteza mitaji na muda.

Rai hiyo imetolewa leo Aprili 23, 2026 na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati akikabidhi  Pampu 10 za kutolea maji mgodini kwa Chama cha Wanawake wachimbaji Madini Tanzania (TAWOMA) kwenye Kongamano la fursa na mageuzi kwa wanawake katika  sekta ya madini nchini liliofanyika jijini Dodoma.

Waziri Mavunde amesema kwamba, kupitia Program wezeshi ya _Mining For A Brighter Tommorrow_ (MBT), itaendelea kuwawezesha wanakimama na vijana kwa kuwapatia leseni  zilizofanyiwa utafiti wa kina wa jiosayansi na mitambo ya kusaga mawe ili kuendelea kuwawezesha kuchimba kwa tija na uhakika.

Waziri Mavunde amesema kuwa, mpaka sasa wachimbaji wadogo wanachangia asilimia 40 katika makusanyo kwenye sekta ya madini ambayo ni mpaka mwezi April trilioni 1.1 

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) Dkt.Venance Mwase amesema , STAMICO itaendelea kuwawezesha wachimbaji wadogo katika makundi yote kwa kuwapatia mashine , 
kuwafanyia utafiti  lengo ni kufikia Dira ya 2030  inayosema Madini ni Maisha na Utajiri.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa TAWOMA Bi.Semeni Malale ameeleza kuwa kupitia mradi wa kimkakati wa Malkia wa Madini unaendelea kuwaunganisha wanawake na vijana nchini kwa kufungua fursa za uwezeshaji katika mikoa mbalimbali hususan katika suluhisho la kuongeza tija na kipato.

Malale ameongeza kuwa 
mpaka sasa mradi wa malkia wa madini umefanikiwa kuwaendeleza  kiuchumi wanawake 7000 katika mikoa 21 na vijana 120.

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Jabiri Shekimweri akimwakilisha Mkuu wa Mkoa ameipongeza  TAWOMA kwa kuwaingiza vijana wengi katika mnyororo wa thamani madini ambapo kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 ilionyesha idadi ya vijana katika taifa  kuwa na  asilimia 21 ya wakazi wote.

Washiriki wengine katika kongamano hilo ni pamoja na Tume ya Madini,Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) Benki ya CRDB, Azani , GF Truck.
Posted by MROKI On Thursday, April 23, 2026 No comments




Na Mwandishi Wetu, Kahama
Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuwawezesha Wakaguzi Wakuu wa Migodi pamoja na wachimbaji wadogo nchini ili kuimarisha usalama kazini, kulinda mazingira na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Wito huo umetolewa leo Aprili 23, 2026 wilayani Kahama, mkoani Shinyanga na Mkurugenzi wa Huduma za Leseni wa Tume ya Madini, Mhandisi Aziza Swedi, alipokuwa akifungua mafunzo kwa mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo.

Mafunzo hayo yanawakutanisha washiriki kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga yakilenga kuimarisha uelewa wa kitaalam, usimamizi bora wa migodi, uzingatiaji wa sheria na kanuni pamoja na kukuza uchimbaji salama na endelevu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Mhandisi Swedi amesema Wakaguzi Wakuu wa Migodi wanapaswa kupewa ushirikiano na mazingira wezeshi ili waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu, hatua itakayosaidia kuzuia ajali migodini, kulinda afya za wachimbaji na kuhifadhi mazingira yanayozunguka maeneo ya uchimbaji.

Amesema mafanikio ya jitihada za Serikali katika kuwawezesha wachimbaji wadogo yanategemea ushirikiano wa wadau wote, hususan mameneja na wakaguzi wa migodi ambao ni nguzo muhimu katika kusimamia uzingatiaji wa sheria, kanuni na viwango vya usalama.

“Serikali inalenga kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinaendelea kuchangia maendeleo ya Taifa huku zikifanyika kwa njia salama zisizoathiri mazingira, afya za wachimbaji na ustawi wa jamii,” amesema.

Aidha, amesema kupitia usimamizi madhubuti, nchi inaweza kufikia azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuongeza mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa kutoka asilimia 10 ya sasa hadi asilimia 12.5 ifikapo mwaka 2030.

Ameeleza kuwa wachimbaji wadogo tayari wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato yatokanayo na shughuli za madini, hali inayoonesha umuhimu wao katika uchumi wa Taifa, huku akiwataka wamiliki wa migodi kuhakikisha taarifa za uzalishaji na kumbukumbu muhimu zinatunzwa ipasavyo ili Serikali ipate mapato stahiki kwa wakati.

Mhandisi Swedi pia ameonya kuhusu athari za uchimbaji usiozingatia taratibu, akitaja matumizi holela ya kemikali hatarishi kama zebaki na sayanaidi pamoja na vumbi la silica kuwa chanzo cha magonjwa hatari ikiwemo silicosis, kifua kikuu na saratani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kutoka Tume ya Madini, Mhandisi Hamisi Kamando, amesema Wakaguzi Wakuu wa Migodi wanapaswa kuwasilisha taarifa za ukaguzi mara kwa mara ili kuiwezesha Serikali kubaini mapema vihatarishi vinavyoweza kusababisha ajali na kuchukua hatua za kinga kwa wakati.

Amesema bado kuna changamoto katika baadhi ya maeneo ya migodi ikiwemo ukiukwaji wa sheria, ukosefu wa kumbukumbu sahihi za uzalishaji, ukwepaji wa kodi na utoroshaji wa madini, hivyo mafunzo hayo yanalenga kuwajengea washiriki uwezo wa kuwa mabalozi wa uzingatiaji wa sheria na taratibu za sekta hiyo.

“Tunataka kuona wachimbaji wanaingia migodini salama na kurejea majumbani mwao salama kila siku. Uhai wa binadamu una thamani kubwa kuliko madini,” amesema Mhandisi Kamando.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini Mkoa wa Shinyanga (SHIREMA), Hamza Tandiko, amesisitiza umuhimu wa weledi kwa wachimbaji na utoaji wa taarifa sahihi za shughuli za uchimbaji, huku akipongeza mchango wa wakaguzi katika kupunguza ajali na madhara migodini.






Posted by MROKI On Thursday, April 23, 2026 No comments



Na Mwandishi wetu, Dodoma
Wanawake nchini Tanzania wanaojishughulisha na mnyororo wa thamani madini wameshauriwa kufanya shughuli za madini katika mwamvuli mmoja utakaowatambulisha kulingana na huduma zitolewazo ndani ya Sekta ya Madini ikiwemo Uchimbaji, Uchenjuaji, Uongezaji thamani.

Rai hiyo imetolewa leo Aprili 22, 2026 na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati akizungumza na wanawake wanaojihusisha za shughuli za madini katika mnyororo mzima wa thamani madini nchini.

Waziri Mavunde amesema kuwa, ni wakati sasa wa kutengeneza jukwaa moja litakalobeba  vyama vyote ambapo itakuwa rahisi kuwafikia kwa pamoja na kwa wakati mmoja tofauti na ilivyosasa.

Waziri Mavunde amesema, katika nyanja ya uongezaji thamani madini ,  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan ametoa shilingi bilioni 30 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Kituo cha mafunzo ya  Uongezaji thamani madini (TGC) ambacho ni fursa kwa Wanawake walio katika mstari wa uongezaji thaman madini.

Aidha, Waziri Mavunde ameeleza kuwa, Mpango wa  Ushirikishwaji kwa Wazawa (Local Content) una fursa mbalimbali ambapo kila mwaka utengwa kiasi cha trilioni 5.1 kwa ajili ya manunuzi na huduma za migodini , hivyo kupitia jukwaa moja ndani ya vyama husika ni rahisi kuingia katika mnyororo huo.

Waziri Mavunde amefafanua kuwa kupitia Programu maalum ya (MBT) , inakuja na mpango maalum wa kuwawezesha Wanawake, Vijana na Watu wenye uhitaji maalum kwa kuwapatia leseni , vifaa na mashine na  kuwapatia mafunzo maalum ya  uchimbaji na uchenjuaji madini.

Pamoja na mambo mengine , Waziri amewapongeza wachimbaji wanawake na wachimbaji wadogo wote  kwa mchango wanatoa katika sekta ya madini, ambapo  umepelekea kuchangia  Pato la Taifa kwa asilimia 10.1.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini Wanawake Tanzania(TAWOMA) Semeni Malale ameipongeza Wizara ya Madini na taasisi zake kwa Juhudi mbalimbali inazofanya za kuwawezesha wachimbaji wanawake nchini.

Vyama vilivyoshiriki mkutano  huo ni pamoja na  TAWOMA, Chama cha Wanawake Wachimbaji Madini ya Viwanda (TWIMMI), Muungano wa  Wanawake wanaojihusisha na Uchimbaji Madini(WIMA) na Chama cha Wanawake Wachimbaji na Waongezaji thamani ya madini Tanzania (WIMO).







Posted by MROKI On Thursday, April 23, 2026 No comments
Posted by MROKI On Thursday, April 23, 2026 No comments

April 22, 2026

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius J. Ndejembi (Mb.), akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 22 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Serikali imesema itaendelea kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa mafuta nchini licha ya changamoto za kimataifa zinazoathiri mnyororo wa usambazaji wa nishati hiyo , ikiwemo vita inayoendelea katika Ukanda wa Mashariki ya Kati.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma wakati wa uwasilishaji wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/27 ,Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Deogratius Ndejembi, alisema kuwa Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa za mafuta ya petroli kwa uhakika.

“Sambamba na kuimarika kwa upatikanaji wa umeme, nchi yetu pia imeendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa bidhaa za mafuta ya petroli licha ya changamoto za kimataifa zilizotokana na vita baina ya Marekani, Israel na Iran,” alisema Mhe. Ndejembi.

Alifafanua kuwa vita hiyo imesababisha athari kubwa katika usambazaji wa mafuta duniani, ikiwemo kufungwa kwa Mlango Bahari wa Hormuz ambao hupitisha zaidi ya asilimia 20 ya mafuta yote duniani, pamoja na kuathiri miundombinu ya uzalishaji na uhifadhi wa mafuta.

“Hali hii imeathiri kwa kiasi kikubwa nchi za Mashariki ya Kati ambako Tanzania inaagiza takribani asilimia 59 ya mafuta yake, huku asilimia 41 ikitoka India ambayo nayo hutegemea mafuta ghafi kutoka ukanda huo huo,” aliongeza.

Kutokana na hali hiyo, Waziri Ndejembi alisema Serikali imechukua hatua za haraka na za kimkakati ili kulinda usalama wa nishati nchini. Moja ya hatua hizo ni kuliwezesha Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuagiza mafuta ya kutosha kwa kipindi cha miezi mitatu ijayo.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa soko la mafuta duniani na iko tayari kuchukua hatua zaidi kulingana na mabadiliko yatakayotokea.
Posted by MROKI On Wednesday, April 22, 2026 No comments






Dodoma
Serikali imeendelea kuimarisha usimamizi wa utekelezaji wa wajibu wa kampuni kwa jamii (Corporate Social Responsibility – CSR) katika Sekta ya Madini, kufuatia kuwepo kwa mfumo maalum wa kisheria uliowekwa kupitia Kanuni za CSR za mwaka 2023 zinazolenga kuongeza uwazi, uwajibikaji na ushirikiano miongoni mwa wadau.

Akifungua kikao kazi cha wataalam kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI (OWM-TAMISEMI) kilichofanyika leo Aprili 22, 2026 jijini Dodoma kwa lengo la kujadili masuala mtambuka ya utekelezaji wa CSR, Kamishna wa Tume ya Madini, Dkt. Theresia Numbi, amesema kanuni hizo zilibuniwa mahsusi kupunguza migogoro iliyokuwa ikijitokeza kati ya Serikali za Mitaa na wamiliki wa leseni za madini kuhusu utekelezaji wa miradi ya CSR.

Dkt. Numbi amesema kuwa pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2018 hadi 2025, bado kuna changamoto zinazoathiri utekelezaji wa kanuni hizo, zikiwemo matarajio makubwa ya jamii zinazozunguka migodi kulinganisha na uwezo wa wachimbaji, uelewa mdogo wa kanuni kwa baadhi ya wamiliki wa leseni, pamoja na mivutano ya wadau mbalimbali wakiwemo wanasiasa na watendaji wa halmashauri.

Amesema kuna umuhimu wa kuandaliwa kwa jukwaa pana la kitaifa litakalowakutanisha wadau wote ili kujadili mafanikio, changamoto na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha utekelezaji wa miradi ya CSR nchini.

“Jukwaa hilo litawakutanisha wamiliki wa leseni za madini, watendaji wa halmashauri, waratibu wa CSR wa mikoa, Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa, pamoja na wadau kutoka OWM-TAMISEMI na Wizara ya Fedha,” amesema Dkt. Numbi.

Amesisitiza kuwa madini ni rasilimali isiyorejea, hivyo usimamizi madhubuti wa miradi ya CSR ni muhimu ili kuhakikisha jamii zinazozunguka migodi zinapata manufaa stahiki na kuchangia maendeleo ya taifa.

“Tusipojipanga vizuri kama taasisi za Serikali kusimamia utekelezaji wa miradi ya CSR, jamii hazitanufaika ipasavyo na hatimaye taifa litapoteza fursa muhimu za maendeleo,” ameongeza.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Serikali za Mitaa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Alfao Sanga, amesema uwepo wa Kanuni na Miongozo ya CSR umeleta mafanikio makubwa katika uratibu wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenye halmashauri mbalimbali nchini.

Ameeleza kuwa kwa mwaka wa fedha 2025/2026, hadi kufikia mwezi Februari 2026, miradi ya CSR yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 28 ilikuwa imetekelezwa katika sekta mbalimbali, ambapo Sekta ya Madini pekee imechangia takribani Shilingi bilioni 19.7.

Amesema mafanikio hayo yanaonesha mchango mkubwa wa Sekta ya Madini katika maendeleo ya jamii na ustawi wa wananchi wanaoishi maeneo yanayozunguka shughuli za uchimbaji.
Posted by MROKI On Wednesday, April 22, 2026 No comments






Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Eng. Ramadhani Lwamo, amesisitiza umuhimu wa kuongeza ufanisi katika uthaminishaji wa madini ya vito kupitia ushirikiano wa karibu kati ya Tume na wadau wa sekta ya madini, hususan katika upangaji na uhuishaji wa bei elekezi za madini hayo.

Hatua hiyo inalenga kuimarisha uwazi, kuongeza tija pamoja na kuboresha mazingira ya biashara ya madini nchini.

Akizungumza katika kikao  kazi cha Wajimolojia na Wathaminishaji wa Madini kilichofanyika leo Aprili 22, 2026, Makao Makuu ya Tume ya Madini jijini Dodoma, Eng. Lwamo amesema kuwa ushirikiano huo tayari umeanza kuleta matokeo chanya.

Amesema mafanikio yaliyopatikana ni pamoja na kuboreshwa kwa mifumo ya uthaminishaji wa madini ya vito na kuongezeka kwa mapato ya Serikali yatokanayo na biashara ya madini ya vito na almasi.

Eng. Lwamo ameeleza kuwa juhudi hizo zinaendana na lengo la Tume ya Madini la kukusanya shilingi trilioni 1.2 katika mwaka wa fedha 2025/2026, huku taasisi ikiendelea kuimarisha upatikanaji wa wataalam wa uthaminishaji pamoja na vitendea kazi muhimu ili kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa majukumu hayo.

Aidha, amewapongeza watumishi wa Tume ya Madini kwa juhudi wanazoendelea kuzionesha na kusisitiza umuhimu wa kuongeza bidii ili kufikia na kuvuka malengo yaliyowekwa.

Kikao hicho kinatarajia kufuatiwa na vikao maalum vya kupitia na kuhuisha bei elekezi za madini ya vito kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta hiyo, wakiwemo FEMATA, TAMIDA, TAWOMA na CHAMATA.
Posted by MROKI On Wednesday, April 22, 2026 No comments

April 21, 2026










Na Mwandishi Wetu, Dodoma 
Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa kushirikiana na Chemba ya Migodi Tanzania (TCM) imejadili na kuweka mikakati wa kuifanya Sekta ya Madini kuwa mhimili mkuu wa kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ya kuifanya Tanzania kufikia uchumi wa thamani ya dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050, kwa kusisitiza utafiti wa madini, usimamizi madhubuti na ushirikiano na sekta binafsi kama nguzo kuu za mafanikio hayo.

Akizungumza katika kikao na Chemba ya Migodi kilichofanyika katika ukumbi wa Tume ya Madini jijini Dodoma, leo Aprili 21, 2026, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amesema kuwa hatua hiyo haiwezekani bila kuwekeza kwa nguvu katika utafiti wa kina wa rasilimali madini kwa kushirikiana na sekta binafsi.

Ameeleza kuwa utafiti wa madini unapaswa kupewa kipaumbele kwani ndio unaofungua milango ya uwekezaji, kuongeza tija na kuhakikisha nchi inanufaika ipasavyo na rasilimali zake.

Katika kikao hicho, Waziri Mavunde amepokea changamoto, maoni na mapendekezo kutoka kwa wadau wa Sekta ya Madini kupitia TCM, akiahidi kuwa Serikali itayafanyia kazi kwa lengo la kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wanachama wa TCM kupitisha hoja zao kupitia umoja wao ili kuwa na sauti moja yenye nguvu na kurahisisha mawasiliano kati ya Serikali na sekta binafsi.

Kwa upande wa usimamizi, Waziri Mavunde ameelekeza kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya Ofisi ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini na taasisi za kiserikali ili kuhakikisha utekelezaji wa Sera na Sheria unakuwa na ufanisi zaidi bila kuingilia na kuleta usumbufu kwa wawekezaji.

Akizungumzia changamoto ya uvamizi wa maeneo yenye leseni halali za uchimbaji, Mavunde amesisitiza kuwa vitendo hivyo havitavumiliwa na tayari maelekezo yametolewa kwa Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa, kupitia Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini, kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kuwaondoa mara moja wavamizi wote na ametumia nafasi kueleza msimamo wa serikali wa kufuta  leseni ambazo hazifanyi kazi zinazomilikiwa na wawekezaji hao.

Amefafanua kuwa Serikali inakamilisha mfumo wa kidijitali unaohakikisha kuwa leseni za utafiti zinazoisha muda wake zinarejeshwa moja kwa moja Serikalini, hatua inayolenga kudhibiti tabia ya watu kushikilia maeneo makubwa kwa matarajio ya kuvutia wawekezaji baadaye.

Katika kuimarisha ajenda ya Ushirikiwa wa Watanzania kwenye sekta ya madini, Waziri Mavunde ameeleza kuwa, kuanzishwa kwa maeneo maalum ya uwekezaji wa viwanda vinavyozalisha vifaa na vipuri vya migodini, akitaja eneo la mgodi wa uliofungwa wa Buzwagi kama kitovu kinachoweza kuendelezwa kuwa ukanda maalum wa uchumi kwa shughuli hizo.

Pia, amekazia kuwa orodha ya bidhaa na huduma 20 zilizotengwa kwa Watanzania pekee katika migodi itaendelea kulindwa bila mabadiliko, akibainisha kuwa Serikali inalenga kulinda maslahi ya wazawa kwa kuzingatia sheria zilizopo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Steven Kiruswa amesema kuwa pamoja na juhudi za kuvutia wawekezaji, Serikali inaweka mkazo katika madini muhimu na ya kimkakati ambayo yanaendelea kuwa na soko kubwa katika zama za mabadiliko ya teknolojia na mazingira duniani.

Naye, Katibu Mkuu wa TCM, Eng. Benjamin Mchwampaka, ameipongeza Serikali kwa hatua zake za kushughulikia changamoto za sekta hiyo na kudumisha ushirikiano thabiti na sekta binafsi, ameshauri kuwa Serikali inapaswa kudumisha uthabiti wa Sera, Sheria na moiongozo ya Sekta ya Madini, kwani mabadiliko ya mara kwa mara kwani huchelewesha maamuzi ya uwekezaji na kwamba mazingira ya kisheria yanayotabirika yanaongeza ushindani wa nchi, huvutia uwekezaji wa muda mrefu, na kuhakikisha rasilimali za madini zinachangia kikamilifu ukuaji endelevu wa uchumi.

Kwa upande wa Serikali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Eng. Yahya Samamba amebainisha kuwa mpango maalum unaandaliwa kufadhili wataalamu wa Kitanzania kujifunza katika fani za kisasa kama uchumi wa madini (Mineral Economy), ili kuendana na mahitaji pamoja na  mabadiliko ya kimataifa na kuongeza ushindani wa nchi.

Kwa ujumla, kikao hicho kimeonesha dhamira ya dhati ya Serikali na wadau wa Sekta ya Madini kujenga msingi imara utakaowezesha sekta hiyo kuwa moja ya injini ya uchumi wa Tanzania kuelekea 2050.
Posted by MROKI On Tuesday, April 21, 2026 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo