Nafasi Ya Matangazo

October 21, 2024










Na Mwandishi wetu, Kondoa
Watumishi wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) mkoa wa Dodoma wametakiwa kufanya kazi kwa bidii na upendo ili kuweza kutekeleza mpango kazi wa Taasisi.

Hayo yamesema na Meneja wa TARURA mkoa wa Dodoma, Mhandisi Edward Lomelo wakati wa mafunzo ya VVU/UKIMWI na Magonjwa Sugu Yasiyoambukiza yaliyofanyika Eneo la Michoro ya Miambani Kolo wilayani Kondoa.

“Tunafanya kazi kubwa za kuboresha barabara na tunapokea mrejesho mzuri toka kwa wananchi hivyo nawataka watumishi wote tufanye kazi kwa ushirikiano na upendo”.

Kuhusiana na mada walizofundishwa na wataalam wa afya alisema watumishi kama wazazi wanapaswa kuwalinda watoto wa kiume na wa kike ili wawe  na maadili katika makuzi yao wakati wao wanaendelea kujenga nchini.

Naye, Muelimishaji Rika ambaye  ni Meneja wa Wilaya ya Chamwino, Mhandisi Nelson Maganga alisema lengo kubwa la mwaka huu ni afya ya akili mahali pa kazi kwani afya ya akili ndiyo kitu pekee kinachomfanya mtumishi akafanikisha utendaji kazi vizuri na kupitia mafunzo waliyoyapata kila mtu amekiri kuelewa na itawasaidia kufanikiwa katika utendaji kazi wao kazini.

Wakati huo huo, Mratibu wa VVU/UKIMWI TARURA Mkoa ambaye pia ni Afisa Utumishi, Bi. Anna Baigana alisema utaratibu wa kupima afya ni utekelezaji wa mpango wa Taasisi hivyo ni nafasi nzuri kwa watumishi kupata elimu na kupima afya ili kulinda afya mahali pa kazi.

Aliongeza kusema kwamba katika mafunzo hayo wameongeza kitu kikubwa hususan upande wa kulinda watoto ana imani wameongeza kitu kikubwa hususan eneo la kuwapa nafasi watoto baada ya kazi kwani muda mwingi wanakuwa kazini na hivyo kama wazazi wanapaswa kuwapa ulinzi watoto katika familia zao.

TARURA Mkoa wa Dodoma umefanya mafunzo hayo ambapo watumishi wa ofisi ya mkoa na wilaya zake ikiwa ni kutekeleza mpango kazi wa Taasisi.
Posted by MROKI On Monday, October 21, 2024 No comments

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb) akiwa na Wajumbe wa Kamati hiyo pamoja na Viongozi wa Wizara wakiongozwa na Naibu Waziri Viwanda na Biashara Mhe. Exaud Kigahe pamoja na Viongozi wa Mkoa wa Morogoro wakiangalia miche iliyopo katika kitalu cha kuotesha miche ya Kakao, Karafuu na Chikichi kilichopo katika kijiji cha Kichangani, Kata ya Mhonda, Tarafa ya Tuliani wilayani Mvomero.
**********
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imetoa rai kwa wananchi kuutumia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa kutunza na kuuza mazao yao kwa bei halisi ili kupata manufaa na kujenga uchumi kwa ujumla

Aidha, ametoa wito kwa Wananchi hao na kutoa ushirikiano ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa kwa Viongozi wa Wilaya au Mkoa husika mara wanapoona watu wachache wenye lengo nia ovu yala kuharibu na kudhoofisha Mfumo huo ili kuuimarisha na kuuwezesha kufanya kazi kikamilifu.ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.

Hayo yamesemwa Oktoba 20, 2024 na Kamati hiyo ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Deodatus Mwanyika ( Mb) wakati wa ziara ya Kamati hiyo katika Mkoa wa Morogoro kwa lengo la kuona maendeleo katika zao la Kakao na jinsi Mfumo wa Stakabadhi za Ghala unavyowanufaisha wakulima Mkoani Morogoro

Aidha amefafanua kuwa nia ya Serikali na Kamati hiyo ni kuhakikisha kuwa Mkulima anapata bei halisi na faida kutokana na Mazao yao kama vile zao la Kakao ambalo lililoongezeka bei kutoka Tsh 4,200 mwaka 2021 hadi Tsh 29,595 mwaka 2024

Vilevile, Mwenyekiti huyo imeielekeza Bodi ya Stakabadhi za Ghala (WRRB) kueneza Mfumo huo katika mikoa yote Nchini pamoja na kuongeza aina idadi ya nyingi za mazao yatakayohifadhiwamazao yanatotumia mfumo huo katika maghala kama vile Karafuu na mengineyo ili kuendelea kuwanufaisha Wakulima.

"Nawapongeza WRRB kwa kufanya kazi vizuri na nawataka muendelee kufanya kazi kwa bidii na ubunifu ili kuwawezesha Wakulima kupata thamani ya Mazao yao. Bodi hii ndio tegemeo katika kumnyanyua Mkulima"

Naye Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Exaud Kigahe akijibu hoja mbalimbali za Wananchi wa Mvomero amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imedhamiria kuwakomboa Wakulima kwa kuhakikisha kuwa wanaongeza tija kwenye uzalishaji kwenye eneo dogo, kuongeza thamani na kuwatafutia masoko ya mazao hayo.

Aidha, alitoa wito kwa Wakulima hao kuendelee kujituma, kufanya kazi kwa bidii na kitumia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa manufaa yao huku akiwaasa wasidanganyike kwa Madali wanaonunua mazao kwa bei ya chini bali wawe wavumilivu kwa muda wa siku tatu hadi tano wakisubiri fedha zao baada ya kuuza mazao kupitia Mfumo huo

Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima amewashauri wakulima kuutumia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa kuwa Mkoa wake unalima mazao mengi kujipanga kuongeza uzalishaji wa mazao mengi ya kibiashara hususani zao la Karafuu ambapo umepanga kugawa kila kaya kuwa na miche 40 ya karafuu ikiwa ni mpango wa kuongeza uzalishaji wa zao hilo Mkoani humo

Naye Naye Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB Bw. Asangye Bangu amesema Bodi hiyo imepokea maelekezo wajumbe na ameahidi kuwa Bodi hiyo itaendelea kuusimamia Mfumo huo ili kuhakikisha kuwa unawanufaisha wakulima wa mazao yanayopita katika mfumo.

Nao Wananchi wa Mvomero kata ya Turiani wakiongea na Kamati hiyo wamekiri kuwa Mfumo huo ni mzuri na wamefanikiwa kuuza Kakao kwa bei ya tsh 29,000 na 17,000 kwa kilo mwaka 2024 wakati kabla ya kutumia Mfumo huo waliuza Kakao hiyo kwa Tsh 2500 na wameiomba Serikali kuwachukulia hatua wale wote wanaodhoofisha Mfumo huo ili uendelee kuwawezesha kunufaika na bei za ushindani zilizoko sokoni.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb) akiwa na Wajumbe wa Kamati hiyo pamoja na Viongozi wa Wizara wakiongozwa na Naibu Waziri Viwanda na Biashara Mhe. Exaud Kigahe pamoja na Viongozi wa Mkoa wa Morogoro wakiangalia miche iliyopo katika kitalu cha kuotesha miche ya Kakao, Karafuu na Chikichi kilichopo katika kijiji cha Kichangani, Kata ya Mhonda, Tarafa ya Tuliani wilayani Mvomero.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima akisalimiana na akiongea na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo walipowasili Ofisini kwake kwa ajili ya ziara Mkoani humo kwa lengo la kuona maendeleo katika zao la Kakao na jinsi Mfumo wa Stakabadhi za Ghala unavyowanufaisha wakulima Mkoani Morogoro.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Exaud Kigahe akijibu hoja mbalimbali za Wananchi wa Mvomero wakati wa Ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo Mkoa wa Morogoro kwa lengo la kuona maendeleo katika zao la Kakao na jinsi Mfumo wa Stakabadhi za Ghala unavyowanufaisha wakulima Mkoani humo.
Posted by MROKI On Monday, October 21, 2024 No comments


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa, Frank Chonya ahakikishe mkandarasi anayejenga mabweni, madarasa na vyoo katika shule ya sekondari Mandawa awe ameanza kazi ifikapo Oktoba 24, mwaka huu.

Akizungumza na walimu na wanafunzi wa shule hiyo pamoja na viongozi wa Wilaya hiyo, leo (Jumatatu, Oktoba 21, 2024) mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu hiyo, Waziri Mkuu amesema kuwa Serikali imeamua kuipandisha hadhi shule hiyo kwa kuamua kuifanya iwe na madarasa ya kidato cha tano na sita. 

Waziri Mkuu Majaliwa ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ruangwa, yupo wilayani Ruangwa kwa ziara ya kikazi ya siku nne, amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alitoa sh. milioni 545 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni matatu, madarasa sita na matundu ya vyoo 12 katika shule hiyo, iliyopo kata ya Mandawa, wilayani Ruangwa, mkoani Lindi.

Waziri Mkuu amekemea tabia ya watumishi kupokea fedha za miradi na kukaa nazo huku wakifanya vikao bila kufikia maamuzi yanayosaidia kuanza kwa utekelezaji wa miradi husika.

“Mmesaini mkataba Oktoba 8, mwaka huu, lakini mpaka sasa hakuna kazi yoyote iliyofanyika, hivi kweli tutamaliza majengo haya kwa wakati? Msingi wa bweni upo wapi? Tunataka ifikapo Desemba mwaka huu, majengo yawe yamekamilika ili Februari, 2025 tuweze kuisajili,” amesisitiza.

Waziri Mkuu amesema kuwa msisitizo wa Serikali ni kuona miradi yote inayoletewa fedha inakamilika na inaanza kutumika. “Wananchi wanapoona mradi unajengwa, wanataka kuona mradi huo unakwenda kwa haraka na kwa ubora ili ulete matokeo pale unapoanza kutumika.”

Akizungumza kwa nyakati tofauti na wananchi kwenye mikutano ya hadhara iliyofanyika katika kata za Mandawa, Namichiga na Matambarale, Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa kazi kubwa inaendelea kufanyika katika sekta za elimu, afya, maji, umeme na barabara.

“Leo katika wilaya hii vijiji vyote tumemaliza kuweka umeme na na sasa tunakwenda katika vitongoji. Tumemaliza kujenga shule za msingi, huko hatuna shida. Kwa upande wa sekondari, tumepiga hatua kubwa, kwani mwaka 2010 nilipoingia madarakani tulikuwa na shule tatu tu za sekondari, lakini leo 2024 tuna shule 30 za sekondari, lengo ni kuona watoto wa Ruangwa wanapata elimu mahali walipo.”

Akizungumzia kuhusu miundombinu ya barabara, Waziri Mkuu amesema kuwa kwa sasa kuna mtandao wa lami wa kilomita 24 Ruangwa mjini. “Pia tuna mpango wa kujenga kilomita 100 za barabara za vijijini kuelekea kwenye maeneo ya uzalishaji, ili kuongeza urahisi wa kufikisha mazao sokoni; zote hizi tunaziweka lami.”

Kwa ujumla, Waziri Mkuu amewaomba wakazi wa kata hizo waendelee kuwa watulivu na waendelee kuiamini Serikali yao.

Akizungumza kwa niaba ya wanafunzi wenzake, Kaka Mkuu wa shule ya sekondari Mandawa, Saidi Mohammed Mkowola ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia kwa kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa mabweni, matundu vya vyoo, vyumba vya madarasa pamoja na ujenzi wa maabara ya kemia na bailojia na ununuzi wa vifaa vingi vya maabara.

Pia aliishukuru Serikali kwa kutoa fedha kiasi cha sh. milioni 30 kwa ajili ya ukamilishaji wa maabara ya fizikia.
Posted by MROKI On Monday, October 21, 2024 No comments











Kongamano la 10 la Jotoardhi Afrika (ARGeo-C10) limeanza kwa mafanikio jijini Dar es Salaam ambapo Wataalam takriban 800 kutoka 21 duniani wameshiriki.

Hayo yameelezwa na Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga wakati akifungua mafunzo kuhusu masuala mbalimbali ya Jotoardhi kwa niaba ya Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Khatibu Kazungu ikiwa ni sehemu ya programu ya siku saba za Kongamano hilo.

“Katika Kongamano hili washiriki watafaidika na masuala mbalimbali ikiwemo kupata ufahamu wa kina kuhusu maendeleo ya rasilimali za jotoardhi kupitia mazungumzo na warsha za kiufundi, Kubadilishana uzoefu, kutembelea na kujifunza kwa vitendo katika maeneo ya miradi ya jotoardhi, kujadili athari za masoko ya kaboni (carbon markets) na kukuza Uwezo kupitia kozi fupi za kiufundi (Pannel and Parallel Sessions).” Amesema Mhandisi Luoga

Ameongeza kuwa, Tanzania imekuwa mwenyeji wa kongamano hilo kutokana na juhudi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika uendelezaji wa Sekta ya Nishati ikiwemo Jotoardhi.

“ Ili tuweze kuwa na umeme wa uhakika na usalama wa nishati nchini lazima umeme uzalishwe kutoka vyanzo mbalimbali ikiwemo Maji, Gesi, Jua, Upepo na Jotoardhi yenyewe na lengo la Serikali ni kuachana na utegemezi vyanzo vichache vya umeme.” Amesema Mhandisi Luoga

Ametanabaisha kuwa, Tanzania ina maeneo takriban 52 yaliyoainishwa kwa ajili ya uendelezaji wa  nishati ya Jotoardhi ambapo maeneo matano tayari yanaendelezwa, ikiwemo Ngozi, Kiejo-Mbaka, Ruhoi, Natron na Songwe.

Ameeleza kuwa, Kongamano hilo la Kimataifa la Jotoardhi linaamsha ari mpya katika uendelezaji wa Jotoardhi Tanzania kwani litasaidia pia kuongeza fursa za uwekezaji kwenye sekta hiyo.

Amesema Kongamano la ARGeo- C10 litafunguliwa na Makamu wa Rais, Mhe.Dkt.Philip Isdor Mpango ambapo nchi mbalimbali duniani zinazoshirikiana na Tanzania katika kuendeleza rasilimali ya Jotoardhi zinashiriki.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Kampuni ya Uendelezaji wa Jotoardhi Tanzania (TGDC), Mathew Mwangomba amesema Kongamano hilo linahusisha wadau mbalimbali duniani ikiwemo watalam wa jotoardhi ambapo kongamano litaangazia masuala mbalimbali ikiwemo masoko ya gesi ya ukaa na upunguzaji wa gesi ya ukaa.

Ametaja Kauli mbiu ya Kongamano hilo kuwa ni, Kuharakisha Maendeleo ya Rasilimali za Jotoardhi katika Afrika, Masoko ya Gesi ya Ukaa na Upunguzaji wa Gesi ya Ukaa. 

Ametaja faida za ARGeo- C10 kuwa ni pamoja na kufungua fursa zinazotokana na jotoardhi na kuharakisha maendeleo ya nishati hiyo Tazania hali itakayoongeza pia pato la Taifa na kuongeza kiasi cha umeme.

Amesema Kongamano kama hilo  lilifanyika mwaka 2014 nchini Tanzania na kuleta matokeo chanya ikiwemo uanzishwaji wa kampuni ya Jotoardhi Tanzania, Wataalam wa Kitanzania kupata mafunzo nje ya nchi na kuongeza mchango wa wadau wa maendeleo katika Jotoardhi ikiwemo Japan (JICA), Iceland, New Zealand na Marekani.

Naye, Mkuu wa Ofisi ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maziringira (UNEP) katika nchi za Kusini mwa Afrika, Meseret Teklemarian ameipongeza Tanzania kwa kuandaa Kongamano hilo kwa mafanikio makubwa.


Pia ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kulipa umuhimu mkubwa Kongamano hilo kwani maandalizi ya Kongamano husika yameshirikisha Watalam kutoka Sekta mbalimbali huku Watalam wengi kutoka Taasisi mbalimbali na mashirika binafsi wakihudhuria mafunzo yanayoendelea katka kongamano hilo.
Posted by MROKI On Monday, October 21, 2024 No comments
 Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa Serikali inawakaribisha wawekezaji katika sekta ya nishati ili kuongeza kasi ya usambazaji, uzalishaji na unganishwaji wa nishati nchini Tanzania.

Dkt. Biteko amesema hayo leo Oktoba 21, 2023 nchini Singapore wakati akishiriki mjadala kuhusu nishati akiwa pamoja na Waziri wa Madini na Nishati  kutoka nchini Cambodia, Mhe. Keo Rottanak na Waziri wa Maliasili kutoka nchini  New Zeland Mhe. Shane Jones wakati wa ufunguzi wa Wiki ya Kimataifa ya Nishati ya nchini Singapore.

“ Serikali haziwezi kufanya kila kitu zenyewe hivyo ni muhimu kushirikiana na sekta binafsi. Sisi Tanzania tunawaalika sekta binafsi ije kuwekeza katika sekta ya nishati kwa ajili ya kuimarisha uzalishaji, upatikanaji na usambazaji nishati na kuboresha maisha ya watu kwa ujumla,” amesema Dkt. Biteko.

Akizungunzia, ajenda ya nishati safi ya kupikia nchini amesema kuwa ni matokeo ya utafiti uliofanywa na kubaini kuwa idadi kubwa ya Watanzania wanatumia kuni na mkaa kwa ajili ya kupikia hali inayosababisha magonjwa ya mfumo wa upumuaji na uharibifu wa mazingira.

Ili kupunguza athari hizo, Dkt. Biteko amesema kuwa Serikali imeandaa mkakati unaolenga kuhakikisha Watanzania asilimia 80 wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

“ Serikali imeendelea  kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia pamoja na kuhakikisha nishati safi inapatikana kwa urahisi na bei nafuu na hivyo tunawakaribisha wawekezaji kuja kuwekeza katika hili kwa sababu soko lipo,” amesema Dkt. Biteko.

Kuhusu jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya nishati nchini, Dkt. Biteko ametaja miradi mbalimbali inayofanywa na Serikali ikiwemo mradi wa kufua umeme wa  Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP) wenye uwezo wa kuzalisha megawati 2115.

“ Serikali inaendeleza vyanzo vipya vya nishati mfano umeme wa jua, upepo na gesi, aidha kwa sasa asilimia 51 ya umeme unazalishwa kwa maji. Tanzania tumeendelea na maandalizi ya  kuziuzia umeme nchi za Kenya, Rwanda, Burundi na sasa tunaendelea na mradi kwa ajili ya kuunganisha na nchi ya Zambia, kupitia Umoja wa Mauzio ya Umeme wa pamoja katika nchi za Afrika Mashiriki na Jumuiya za Kusini mwa Afrika (SADC) tuna soko la uhakika na hivyo tunawakaribisha wawekezaji kuja kushirikiana nasi,” amesisitiza Dkt. Biteko.

Naye, Waziri wa Madini na Nishati  kutoka nchini Cambodia, Mhe. Keo Rottanak amesema kuwa mwaka 1998 nchi yake ilifanya mageuzi makubwa katika sekta ya nishati na kuwa sasa asilimia 99 ya vijiji ina umeme.

“ Tutahakikisha tunafikisha umeme katika nyumba za watu na malengo yetu ni ifikapo mwaka 2030 umeme unaozalishwa kwa jua kuwa mbadala wa umeme unaozalishwa na maji, amesema Mhe. Rottanak.

Kwa upande wake, Waziri wa Maliasili na kutoka nchini  New Zeland, Mhe. Shane Jones amesema kuwa nchi yake imeendelea kutoa fedha kwa ajili ya kusambaza umeme na kuwa inajikita katika kuwekeza katika vyanzo mbadala vya kuzalisha nishati.

Awali akifungua mkutano huo, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Viwanda na Biashara wa Singapore Mhe. Gan Kim Yong amesema kuwa mahitaji ya nishati duniani yanazidi kuongezeka siku hadi siku hivyo nchi zinapaswa  kubuni vyanzo mbadala na kupunguza madhara yatokanayo na gesi ya ukaa ifikapo mwaka 2050.

Akitoa uzoefu wa nchi yake kwenye kuongeza vyanzo mbadala vya nishati amesema  “ Kwa sasa tuko kwenye mkakati wa kuzalisha umeme kwa kutumia haidrojeni na nyuklia ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kuongezeka kwa ushiriki wa Kampuni  za Google na Amazon ambazo zimeonesha nia ya kuwekeza kwenye miradi ya nishati jadidifu.” Amesema Mhe. Kim Yong.

Aidha,katika mkutano huo pia umefanyika uzinduzi wa tawi la ofisi ya kanda ya Shirika la  Kimataifa  la Nishati (IEA) nchini Singapore.




Posted by MROKI On Monday, October 21, 2024 No comments

October 20, 2024


MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na Mbunge wa Ruangwa, Kassim Majaliwa mwishoni mwa wiki hii, ameshuhudia madiwani wawili na Katibu Kata kutoka vyama vya CUF na ACT-Wazalendo wakirejea Chama cha Mapinduzi.

Akiwa kwenye kijiji cha Milola katika siku ya kwanza ya ziara yake, Mheshimiwa Majaliwa alishuhudia madiwani wa Kata za Milola na Rutamba wakitambulishwa na Mbunge wa Jimbo la Mchinga, Mama Salma Kikwete katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye senta ya Milola, Kata ya Milola, Manispaa ya Lindi.

Viongozi waliorejea CCM ni Diwani wa Milola, Bw. Hussein Kimbyoko kutoka Chama cha Wananchi (CUF) na Diwani wa Rutambi, Bw. Athumani Mmaije kutoka Chama cha ACT – Wazalendo.

Akiwa katika siku ya pili ya ziara yake jimboni Ruangwa, Mheshimiwa Majaliwa alishuhudia wanachama wengine wawili wakikabidhi kadi zao kwa Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya ya Ruangwa, Mzee Ibrahim Issa Ndoro katika mkutano uliofanyika kwenye viwanja vya Wandorwa, wilayani Ruangwa, mkoani Lindi.

Wanachama hao ni Alhaji Abasi Abdallah Chinguwile kutoka ACT WAZALENDO ambaye alikuwa mwanachama katika kijiji cha Mmawa, Kata ya Likunja, wilaya ya Ruangwa. Mwingine ni Bw. Jafari Juma Nang’anda kutoka CUF ambaye pia alikuwa ni Mkurugenzi wa Uchaguzi na Katibu Kata wa Kata ya Nachingwea, wilayani humo.

Akizungumza baada ya kupokewa na viongozi wa CCM, Bw. Jafari Nang’anda alisema ana imani na viongozi wa CCM wa mkoa na wilaya na akawaomba watambue kuwa anaweza kufanya kazi saa yoyote na mahali popote.



Posted by MROKI On Sunday, October 20, 2024 No comments

October 19, 2024








Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde ameeleza kuhusu umuhimu wa Madini Bonanza na kueleza kuwa limelenga kuimarisha umoja, mshikamano na ushirikiano baina ya  Watumishi wa Wizara na Taasisi zake ili kuifanya Wizara kuwa familia moja.

Amesema hayo leo Oktoba 19, 2024 katika Viwanja vya Shule ya Sekondari John Merlin – Miyuji jijini Dodoma, wakati akizungumza katika Madini Bonanza lililowajumuisha Watumishi wa Wizara ya Madini na Taasisi zake. 

" Ninawapongeza kwa bonanza hili kwasababu linatusaidia kukaa  pamoja, kufurahi na kufahamiana zaidi," amesema.

Aidha, amewasisitiza watumishi  kujenga utamaduni  wa kufanya mazoezi ili kuimarisha afya zao, na kuongeza," kama mnavyofahamu hivi sasa takwimu  zinaonesha kuna changamoto kubwa ya magonjwa yasiyoambukiza hivyo kuna umuhimu mkubwa wa kufanya mazoezi,".

Katika hatua nyingine, Mhe. Mavunde amewahamasisha watumishi wa Wizara kujishiriki katika zoezi linaloendelea hivi sasa la kujiandikisha kwa ajili ya uchaguzi wa Viongozi wa Serikali za Mitaa unaotarajia kufanyika mwezi Novemba mwaka huu.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Terence Ngole ameeleza kuhusu  mashindano ya michezo mbalimbali yaliyofanyika yakihusisha mpira ya miguu, pete, kamba, mbio za mita 100 na mita 400 ambapo  washindi mbalimbali wamepatikana kutoka Wizara na Taasisi zake huku Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania ( GST)  ikiondoka na medali  lukuki na makombe.
Posted by MROKI On Saturday, October 19, 2024 No comments

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Bw. Kailima Ramadhani  amejiandikisha kwenye daftari la wakazi katika mtaa wa Chimuli II kwenye kituo cha Shule ya Msingi Chadulu jijini Dodoma leo Oktoba 19, 2024.

Akizungumza baada ya kujiandikisha, Bw. Kailima aliwasisitiza wananchi umuhimu wa kujitokeza kwa wingi kuandikishwa katika maeneo yao ili watimize haki yao ya kikatiba ya kupiga kura.

"Nimetoka kujiandikisha katika orodha ya wakazi ambayo itazaa daftarinla orodha ya wapiga kura kwaajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa, niwaombe na kuwasihi wananchi wote wenye umri wa miaka 18 na wenye sifa za kuandikishwa wajitokeze kuandikishwa ili watumie haki yao ya kikatiba ya kupiga kura.

Kailima amesema watu wa makundi yote, Wazee, wakina mama na vijana wenye sifa wajitokeze kwani imesalia siku moja ili kuhitimisha zoezi hilo kwaajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa. 

Aidha amesema vituo vipo katika maeneo mbalimbali yaliyo karibu na makazi ya wananchi hasa katika mashule na ofisi za mitaa.

Uandikishaji wa wapiga kura wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, kwenye daftari la wakaazi, ulianza tarehe 11 Oktoba, 2024 na utamalizika tarehe 20 Oktoba 2024.

Wananchi waliojiandikisha watapiga kura kuchagua viongozi wa mitaa na vijiji Novemba 27, 2024 katika uchaguzi wa serikali za mitaa.
Posted by MROKI On Saturday, October 19, 2024 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo