Nafasi Ya Matangazo

May 27, 2025






Na Mwandishi wetu,Dar Es Salaam
Mkoa wa Dar es Salaam umeendelea kufanya vizuri katika ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali kupitia Sekta ya Madini kwa mwaka wa fedha 2024/2025, baada ya kufanikisha makusanyo ya Shilingi Bilioni 23.02 kufikia mwezi Mei, sawa na asilimia 125 ya lengo la mwaka.

Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa huo ilipangiwa kukusanya Shilingi Bilioni 18.36, lakini hadi kufikia Machi mwaka huu tayari ilikuwa imetimiza lengo hilo, na sasa imevuka kwa kiasi kikubwa.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa huo, Mjiolojia Lameck Gabote amesema mafanikio hayo yametokana na usimamizi thabiti wa vyanzo mbalimbali vya maduhuli ikiwemo mrabaha, ada na tozo mbalimbali.

“Mwaka ujao wa fedha 2025/2026 tumepangiwa kukusanya Shilingi Bilioni 24. Tuna imani kubwa kwamba tutafikia na kuvuka lengo hilo. Mkoa wa Dar es Salaam uko ‘active’ kukusanya maduhuli, hatulali,” amesema Gabote kwa msisitizo.

Ameeleza kuwa licha ya Dar es Salaam kutokuwa na shughuli kubwa za uchimbaji wa madini, imekuwa kitovu muhimu cha biashara ya madini kutokana na uwepo wa Soko la Kimataifa la Madini, bandari na uwanja wa ndege wa kimataifa ambavyo hurahisisha biashara ya madini ndani na nje ya nchi.

Aidha, Gabote amebainisha kuwa ofisi yake pia inasimamia mgodi mdogo wa dhahabu uliopo kijiji cha Kibindu, Handeni mkoani Tanga, ambao uzalishaji wake ni mdogo – ukitoa wastani wa gramu 12 hadi 25 kwa mwezi.

Kwa mujibu wa Gabote, mikoa ya Dar es Salaam na Pwani imejaliwa kuwa na aina mbili za madini: madini ya ujenzi na madini ya viwandani, ambayo yamechangia kwa kiasi kikubwa makusanyo ya maduhuli. Madini haya yamekuwa yakitumika katika miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa barabara ya BRT unaoendelea jijini Dar es Salaam.

Takwimu hizi zinaonesha ukuaji chanya wa Sekta ya Madini katika maeneo yasiyokuwa ya uchimbaji wa moja kwa moja, na kuonesha umuhimu wa miundombinu ya biashara kama masoko, bandari na viwanja vya ndege katika kuchochea maendeleo ya sekta hiyo.
Posted by MROKI On Tuesday, May 27, 2025 No comments

May 26, 2025









WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali itaendelea na mikakati ya kuwaunganisha wafanyabiashara wa Tanzania na wa Mataifa mbalimbali duniani ikiwemo Japan ili kuwawezesha kunufaika na fursa mbalimbali zilizopo katika mataifa hayo.

Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Serikali imekuwa ikifanya hivyo kwa kushiriki katika makongamano mbalimbali ya kimataifa ambayo yamekuwa yakiwakutanisha wafanyabiashara na wawekezaji ili kuongeza tija kubwa kwenye masuala ya biashara na uwekezaji.

Amesema hayo leo (Jumatatu, Mei 26, 2025) alipofungua kongamano la Biashara, Uwekezaji na Utalii lililowakutanisha wafanyabiashara wa Tanzania na wafanyabiashara na wawekezaji wa Japan katika ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Westin, Osaka, Japan ikiwa ni sehemu ya  ushiriki wa Tanzania katika maonersho ya World Expo Osaka 2025.

“Tumewaeleza wafanyabaishara na wawekezaji hawa wa Japan fursa ambazo zipo nchini, hii ni mara ya tatu tunakutana na wafanyabara na wawekezaji kutoka Japan, tayari tumeanza kuona manufaa ya makongamano haya kutokana na kuongezeka kwa biashara kati ya mataifa haya mawili.”

Waziri Mkuu amesema hadi Machi 2025 jumla ya makampuni 24 kutoka Japan yamewekeza nchini Tanzania katika miradi mbalimbali yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 42.70 nchini na kuwawezesha jumla ya Watanzania wapatao 1,182 kupata ajira.

Mheshimiwa Majaliwa amesema licha ya uwekezaji wa makampuni hayo, Serikali ya Tanzania imeendelea kunufaika na ushirikiano wake na Serikali ya Japan kwa kupata misaada katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenye sekta mbalimbali ikiwemo ya kilimo na miundombinu.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameshuhudia utiaji saini wa hati sita za ushirikiano ikiwemo ya ushirikiano katika kuendeleza sekta ya mafuta baina ya Serikali ya Tanzania na Shirika la JGC la Japan, hati nyingine ni baina ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) na Axcel Afrika kwa ajili ya kukuza uwekezaji nchini.

Hati nyingine zilizosainiwa ni kati ya Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA) na Axcel Afrika kwa ajili ya kukuza uwekezaji Zanzibar, hati nyingine iliyosainiwa ni kati ya Kampuni ya Uendelezaji wa Jotoardhi Tanzania (TGDC) na Shirika la Nishati la Toshiba, hati nyingine ni kati ya Shirika la Tiba la TOKUSHUKAI na Chuo Kikuu cha Dodoma na Hospitali ya Benjamin Mkapa.

Hati nyingine iliyosainiwa ni kati ya ushirikiano kati Chuo Kikuu cha Dodoma na Hospitali ya Benjamin Mkapa na Chama cha Maendeleo na Uchumi Afrika cha Japan (AFRECO)

Kwa upande wake, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Suleimani Jafo amesema dhamira ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uwekezaji inazindi kufunguka hivyo amewaomba Watanzania kuhakikisha wanachangamkia fursa hizo kwa ajili ya maendeleo yao binafsi na Taifa.

Amesema lengo la Serikali la kuendelea kutafuta fursa hizo za biashara, uwekezaji na utalii ni kukuza uchumi pamoja na kuwezesha upatikanaji wa ajira nchini, na kwamba kipaumbele kimewekwa katika sekta za biashara, miundombinu, utalii, uchumi wa buluu, uwekezaji kwa kuwa Japan imepiga hatua kubwa katika sekta hizo.

Dkt. Jafo amesema kipaumbele kingine ni kutafuta wawekezaji watakaoshirikiana nao katika kuendeleza sekta ya kilimo ili kuwa na viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, kuendeleza kilimo cha umwagiliaji kwa kujenga miundombinu ya kisasa, katika sekta ya madini ni kuoyaongezea thamani madini ya kimkakati.

Naye, Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Omar Said Shaaban amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imejipanga katika kutumia fursa za uwekezaji zinazotokana na ushirikiano kati ya Tanzania na Japan.

Waziri Shaaban amesema tayari Serikali hiyo imeshaanza utekelezaji wa ujenzi wa miundombinu ya uwekezaji ikiwemo ujenzi wa mitaa ya viwanda ambapo mmoja umejengwa mtaa wa Duga Zuze visiwani Zanzibar pamoja na eneo la Chamanangwe visiwani Pemba.

Mbali na miradi ya ujenzi wa mitaa ya viwanda, pia Waziri Shaaban amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kushirikiana na Chama cha Wafanyabiashara Zanzibar wameandaa jarida linaloeleza fursa za uwekezaji Zanzibar ambalo limezinduliwa na Waziri Mkuu na kugawiwa kwa wafanyabiashara na wawekezaji wa Japan.

Amesema eneo jingine ambalo Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imejipanga kutafuta wawekezaji ni  uchumi wa Buluu kupitia mazao ya bahari ikiwemo usindikaji wa samaki ili kuhakikisha unafanyika kisasa zaidi kwa faida ya wananchi na serikali.

Awali, Kamishina Jenerali wa World Expo Osaka 2025 kwa Tanzania na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade), Latifa Khamis amesema kongamano hilo ambalo ni sehemu ya ushiriki wa Tanzania katika maonesho ya World Expo Osaka 2025 linalenga kuwakutanisha wafanyabiashara wa Tanzania na Japan.

Mkurugenzi huyo alisema maeneo ambayo yamepewa kipaumbele katika kongamano hilo ni kwenye sekta ya nishati, madini, kilimo, huduma za kibenki, utalii, uwekezaji, afya ambapo wafanyabiashara wa Tanzania wanakutana na wafanyabiashara wa Japan kujadiliana namna ya kushirikiana katika kukuza biashara na uwekezaji.
Posted by MROKI On Monday, May 26, 2025 No comments
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe Judith Kapinga amesema Serikali imefikisha  umeme kwenye mitaa 58 ya Mji wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime kati ya mitaa 81 ya Halmashauri hiyo.

Mhe. Kapinga ameyasema hayo leo Mei 26, 2025 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la la Mbunge wa Tarime Mjini, Mhe. Michael Kembaki aliyeuliza Serikali itapeleka lini umeme katika mitaa 18 ya Halmashauri ya Mji wa Tarime. 
 
"Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji wa Tarime ina mitaa 81, kati ya hiyo mitaa 58 tayari  imefikiwa na umeme, na mitaa 23 bado haijafikiwa na umeme."  Amesema  Kapinga

Ameongeza kuwa, mitaa 13 inapelekewa umeme kupitia mradi wa Hamlets Electrification Project - IIA (HEP IIA) unaotekelezwa na Mkandarasi Dyname Construction Engineering,  na mitaa 10 iliyobaki itafikishiwa umeme katika miradi inayofuata.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu Wanawake (UWT), Mhe. Zaytuni Swai aliyeuliza kuhusu jinsi  Serikali ilivyojipanga  kupeleka umeme maeneo ya pembezoni mwa mji wa Arusha hususan kwenye Kata ya Telat, Mhe. Kapinga ameeleza kuwa, Serikali inatekeleza miradi mbalimbali katika maeneo ya pembezoni  (Peri Urban)  kupitia Wakala wa Nishati Vijijini  (REA) ambayo lengo lake ni kusambaza  umeme maeneo ya pembezoni mwa mji.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Cecilia Pareso alyeuliza kuhusu Vitongoji vya Wilaya ya Karatu kutokuwa na umeme na vichache vilivyo kwenye mradi kupelekewa nguzo 40 ambazo hazitoshelezi mahutaji na kuiomba Serikali  kuongeza idadi hiyo, Mhe. Kapinga amesema kuwa kwa kawaida miradi ya Vitongoji inawigo kulingana na kazi aliyopewa  Mkandarasi, hata hivyo amesema  kuwa Wilaya ya Karatu ipo katika mradi wa Vitongoji 9,000 ambao utaanza kutekelezwa hivi karibuni na kusisitiza kuwa, miradi ya kupeleka umeme kwenye Vitongoji ni endelevu.
Posted by MROKI On Monday, May 26, 2025 No comments

May 25, 2025


WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema ushirikiano wa Tanzania na Japan umezidi kukua katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kidiplomasia umezidi kuimarika siku hadi siku, ambapo mauzo ya biashara kati ya nchi hizo yameongezeka kutoka dola za Marekani bilioni saba mwaka 2023 hadi bilioni 37 kwa mwaka 2024.

Mheshimiwa Majaliwa ameyasema hayo leo (Jumapili, Mei 25, 2025) alipomwakilisha Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa maadhimisho ya Siku ya Tanzania kwenye Maonesho ya Kimataifa ya Osaka (World Expo Osaka 2025) yanayoendelea nchini Japan.

Amesema Wajapan wanapenda sana bidhaa kutoka Tanzania zikiwemo za kilimo kama chai, kahawa, ufuta, tumbaku, tingatinga, vinyago, katani, viungo kama karafuu pamoja na madini mbalimbali yanayopatikana nchini.

Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji na wafanyabiashara wa Japan na duniani kote waje kuwekeza katika maeneo mbalimbali nchini yakiwemo ya elimu, afya, miundombinu, nishati, kilimo, utalii kwani Tanzania imeweka mazingitra mazuri ya uwekezaji na pia ina amani na utulivu.

“…Tanzania licha ya kuwa na fursa nyingi za uwekezaji ikiwemo ardhi yenye rutuba, amani na mazingira tulivu, pia ni kitovu cha biashara katika Ukanda wa Afrika Mashariki, Kusini na Kati kwa kuwa inapakana na nchi saba ambazo ni Uganda, Rwanda, Burundi, Jamuhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Zambia, Malawi na Msumbuji hivyo kuwawezesha wawekezaji kupata masoko ya uhakika katika mataifa hayo.”

Waziri Mkuu amesema Serikali ipo katika mchakato wa kuvifanyia maboresho viwanja vya Maonesho vya Mwalimu Julius Nyerere maarufu sabasaba ili viwe na hadhi ya kimataifa na kuwezesha kufanyika mikutano na maonesho ya biashara ya kikanda na kimataifa.

Monesho hayo yamehudhuriwa na viongozi mbalimbali kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanziba wakiwemo Mawaziri, Manaibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na Wakuu wa Taasisi mbalimbali.

Maonesho hayo yalianza tangu Aprili 13, 2025 na yanatarajia kumalizika Oktoba 13, 2025, hii ni mara ya pili kwa Japan (Osaka) kuwa mwenyeji wa maonesho hayo ya kimataifa, ambapo mara ya mwisho yalifanyika 1970 (EXPO 1970).

Kesho (Jumatatu, Mei 26, 2026), Mheshimiwa Majaliwa anatarajiwa kushiriki katika kongamano la biashara, uwekezaji na utalii ambalo litahusisha wafanyabiashara kutoka Tanzania na Japan. Pia, Waziri Mkuu atashiriki katika Mikutano ya Uwili na viongozi wa Serikali ya Japan, mashirika ya maendeleo na watendaji wakuu wa makampuni mbalimbali kwa lengo la kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Japan.











Posted by MROKI On Sunday, May 25, 2025 No comments









Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imeridhishwa na kazi ya upangaji matumizi ya ardhi katika Kijiji cha Msungua kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi mkoani Singida.

Akizungumza na wananchi wa Kijiji hicho katika mkutano wa hadhara, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Mhe. Timotheo Mzava amesema, kamati yake imeridhishwa na kazi ya upangaji matumizi katika kijiji cha Msungua ambapo anaamini kukamilika kwake kutawezesha  wananchi kupata hati za maeneo yao.

“Sisi kama kamati, tumeridhika na kwa kazi nzuri inayofanywa, wananchi wanaijua hii ni kazi yao, wameshiriki vizuri. Tumeridhika na kasi ya kutekeleza kazi ya upangaji wa matumizi ya ardhi” amesema Mhe. Mzava.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Mhe. Geophrey Pinda amesema, utekelezaji wa kazi hiyo unasaidia wananchi kuondokana na migogoro ya mipaka ya vijiji, Jirani na Jirani katika maeneo yao na kuwataka kuheshimu mkakati na mipango waliojiwekea ya matumizi ya ardhi.

“Lindeni maeneo haya ili fedha za serikali zikiletwa kuwe na maeneo ya kutekeleza miradi ya maendeleo, maeneo yaliyopangwa kwa huduma za jamii mkayatunze na mkipata hati tambueni, hati ni mtaji zitasaidia kustawisha Maisha ya wananchi” amesema Naibu Waziri Pinda.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa kazi hiyo kwa Kamati kwa kamati ya Bunge mkoani Singida, Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi Bw. Joseph Mafuru ameeleza kuwa, hadi Mei 2025 jumla ya vijiji 224 sawa na asilimia 67.27 vimeandaliwa mipango ya matumizi ya ardhi katika halmashauri za wilaya 14 huku vijiji 109 kati ya 333 mipango yake ya matumizi ikitarajiwa kukamilika ifikapo Juni 2025.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii imefanya ziara mkoani Singida kwa lengo la kukagua utekelezaji wa kazi ya upangaji wa matumizi ya ardhi katika Kijiji cha Msungua, kazi  inayotekelezwa na Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi.

Itakumbukwa Machi 2025 Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi ilipokea fedha kiasi cha Sh. Bilioni tano kwa ajili ya kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi katika vijiji 333 kikiwemo Kijiji cha Msungua.

Ili kukamilisha kazi hiyo kikamilifu Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge wameitaka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi kukamilisha kazi hiyo katika Kijiji cha Msungua kwa kuwapatia wananchi Hati za maeneo yao.
Posted by MROKI On Sunday, May 25, 2025 No comments

May 24, 2025







WANANCHI wa Mkoa wa Lindi wametakiwa kuacha uvivu na badala yake wachangamkie fursa zilizopo kwenye sekta ya  madini hususani katika mgodi wa kati  wa Elianje uliopo kitongoji cha Namungo, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.

Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti  wa  Kijiji  cha  Chingumbwa, kilichopo Kata ya Namungo, Abdallah Rashid akielezea fursa zilizopo mkoani humo kupitia Sekta ya Madini.

“Fursa zipo nyingi ni uvivu tu wa wananchi wetu, ukiangalia kwenye mgodi huu unaotuzunguka wa Elianje Genesis kuna fursa ya usambazaji vyakula, vinywaji, usafi, kupika, kusambaza vifaa vya usalama migodini, uchimbaji na uchenjuaji lakini ndio hivyo,”amesema Abdallah

Aidha, Mwenyekiti huyo amesema uwepo wa mgodi huo umetoa manufaa makubwa kwa wananchi kwa kuchimbiwa kisima cha maji ambacho kwa sasa kinahudumia kaya 918, awali kulikuwa na shida ya maji na wananchi walilazimika kutembea umbali mrefu kuchota maji.

“Pia, mwekezaji ametujengea shule ambayo kwa sasa ina wanafunzi 79, awali watoto walitembea umbali mrefu zaidi ya kilomita tatu kufuata shule vijiji vya jirani hali iliyopelekea baadhi yao kuacha shule. Pia mwekezaji amekua akitoa chakula kwa wanafunzi kipindi cha mitihani, kuwaletea vifaa vya michezo vya mpira  wa miguu kwa wanaume na netball kwa  wanawake na yupo mbioni kununua basi la shule,”amesema.

Kwa upande wa Mkuu wa shule ya msingi Chingumbwa iliyopo kata ya Mbekenyela mkoani humo, Joseph Raymond amesema mgodi wa Elianje umejenga ofisi za Walimu, kuwawekea umeme  kwa ajili ya kambi kwa darasa la saba na la nne itakayoanza mwenzi ujao wa sita  wakijiandaa na mitihani ya taifa.


Naye, Meneja wa Mgodi wa Elianje, Philibert Masawe akizungumzia mgodi huo amesema wanajishughulisha na  uchenjuaji wa madini ya dhahabu na uchimbaji wa ‘green garnet’,

Amesisitiza pia Kampuni ya Elianje imejenga  kituo cha mfano cha uchenjuaji wa madini ya dhahabu kinachotumia teknolojia ya CIP ambacho kina uwezo wa wa kuchenjua mbale (mwamba) ya dhahabu kiasi cha tani 500 kwa siku.

Amesema pia kiwanda hicho kimeajiri watanzania 300 na kuipongeza Serikali kuweka sera rafiki na sheria nzuri ambazo zinavutia uwekezaji.
Posted by MROKI On Saturday, May 24, 2025 No comments

May 23, 2025


Na Mwandishi Wetu,Ruvuma
Kampuni za uchimbaji wa madini ya makaa ya mawe katika Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma zimeendelea kusaidia jamii ambapo wananchi wanaoishi jirani na migodi wameendelea kunufaika na ajira huku migodi ikiendelea kuboresha huduma za jamii ikiwa ni pamoja na kuchangia ujenzi wa zahanati hali iliyopunguza adha ya wananchi kufuata huduma za afya katika maeneo ya mbali. 

Akizungumza katika mahojiano, Msimamizi wa Kituo cha Mauzo cha Kampuni ya Makaa ya Mawe ya Jitegemee (Jitegemee Holdings Company Limited), Mark Tarimo ameeleza kuwa katika miradi  iliyotekelezwa na kampuni hiyo kwa jamii ni pamoja na ujenzi wa vyoo vya shule katika kijiji cha Luagala pamoja na kutoa ajira kwa vijana zaidi ya 200 wanaozunguka maeneo ya mgodini kama mkakati wa kuwawezesha  kujikwamua kiuchumi na kupata unafuu wa maisha.

“ Vijana hawa tumeweza kuwapatia ajira  katika shughuli za udereva na kufunga maturubai kwenye magari yanayofika kupakia makaa,” amesema Tarimo.

Ameendelea kusema kuwa  kampuni ya Jitegemee imeweza kuboresha miundombinu ya mgodi ambapo kwa siku inaweza kuzalisha zaidi ya tani 3000 za makaa, ambayo huchakatwa na kuwauzia wananchi  huku wateja wao wakubwa ni kutoka nchi za Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi.

Kwa upande wake Meneja wa kampuni ya Ruvuma Coal Limited, Sanzeh Ntikwa  akielezea namna mgodi ulivyoboresha huduma za jamii amesema  kuwa  mgodi umefanikiwa kujenga madarasa mawili kwenye kijiji cha Paradiso, zahanati na kuboresha ujenzi wa Soko la Paradiso pamoja na kununua vifaa vya michezo kwa vijana.

“Kwenye kijiji cha Sara tumeweza kujenga madarasa mawili, Ofisi ya walimu na zahanati kubwa, kwa sasa tumejipanga kujenga shule ya VETA kwenye kijiji cha Paradiso, ambapo tunasubiri vibali kutoka Serikalini pamoja na michoro ili tuanze ujenzi, vilevile tumenunua basi kwa ajili ya kuwabeba wanafunzi kutoka kijiji cha Paradiso kwenda kwenye shule iliyopo Luagala katika Wilaya ya Mbinga,” amesema Ntikwa.

Naye, Mjiolojia wa kampuni ya Ruvuma Coal Limited, Penina Rububula  ambaye ni mmoja wa wananchi walioajiriwa na mgodi huo akielezea manufaa ya ajira yake amesema  kupitia ajira yake ameweza  kusomesha watoto, kununua kiwanja pamoja na kuendesha maisha yake ya kila siku.





Posted by MROKI On Friday, May 23, 2025 No comments
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe Judith Kapinga amesema Serikali imetoa ruzuku ya asilimia 20 hadi 50 kwenye mitungi ya gesi ya LPG takribani 452,445 kwa watumiaji wa mwisho ikiwa ni jjtihada za kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.

Mhe. Kapinga ameyasema hayo leo Mei 23, 2025 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Grace Tendega aliyetaka kufahamu Serikali ina mkakati gani wa muda mfupi wa kuhakikisha Wananchi wa Vijijini wanatumia Nishati Safi ya kupikia badala ya Kuni na Mkaa.
 
"Mheshimiwa Mwenyekiti Serikali kupitia REA pia  itasambaza majiko banifu 200,000 yenye bei ya punguzo la hadi asilimia 75 pamoja na kuwezesha ufungaji wa mifumo ya nishati safi ya kupikia katika Taasisi za Umma zinazohudumia watu zaidi ya 100."  Amesema  Kapinga

Aidha, amesema Serikali imekamilisha kazi ya usambazaji umeme katika vijiji vyote hivyo kwa sasa inaendelea kuhimiza matumizi ya majiko ya kupikia yanayotumia umeme ikiwa ni njia mojawapo ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa wananchi wa vijijini badala ya kutumia kuni na mkaa.

Mhe. Kapinga ametanabaisha  kuwa, Mkakati wa Taifa wa  Nishati Safi ya Kupikia ni wa miaka kumi lakini Serikali inao mkakati wa matumizi bora ya nishati ambao unahusisha pia sekta binafsi kwa ajili ya kusaidia kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Akijibu swali la Mbunge wa Mbulu, Mhe. Zacharia Isaay aliyeuliza Serikali imejipangaje kuhakikisha Vitongoji vyote vilivyokusudiwa katika mwaka huu wa bajeti kufikiwa  na umeme katika kipindi cha mwezi mmoja uliobaki, Mhe. Kapinga amesema Serikali inayo mikakati na miradi mbalimbali ya kupeleka umeme katika Vitongoji. 

Amesema kuwa, moja ya mikakati hiyo ni kupeleka umeme katika Vitongoji 15 kwa kila Jimbo, na pia  Serikali imekuja na mkakati wa kupeleka umeme katika Vitongoji 20,000 ambapo   awamu ya kwanza inaanza kupeleka umeme katika Vitongoji 9000 na hatua iliyopo ni utafutajj wa wakandarasi.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Anatropia Theonest aliyeuliza bei ya Serikali ya ruzuku imeanza kutumika lini kutokana na mitungi ya gesi kuendelea kuuzwa kati ya 22,000/- na 25,000 na kwa mitungi mikubwa ya kilo 15 shilingi 50,000/- na 60,000/-,  Mhe. Kapinga ameeleza kuwa kwa maeneo ya mjini Serikali imepeleka ruzuku hadi asilimia 25 na maeneo ya Vijijini ni kati ya asilimia 50 hadi 75 na kutolea mfano iwapo mtungi ulikuwa unauzwa shilingi 45,000/- kwa bei ya ruzuku inapatikana kwa shilingi 17,000/- hadi 21,000/- na kusema ni zaidi ya nusu ya bei yake.

Ameongeza kuwa, katika kila Wilaya kuna takribani mitungi 3,255 inayopatikana kwa ruzuku na kuongeza kuwa ndio kwanza mkakati umeanza.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Yustina Rahhi alieuliza mpango wa Serikali kuwapelekea jamii ya wafugaji teknolojia ya biogas au kuwajengea majiko yanayotumia samadi ya gesi ambayo ni rahisi, Mhe. Kapinga amesema Serikali inatekeleza mradi huo kupitia umoja wa Ulaya (mfuko wa UNCDF) ambao unateknolojia alizozitaja Mhe. Mbunge.

Akijibu swali la Mbunge wa Nyang’wale, Mhe. Hussein Amar aliyeuliza kuhusu mpango wa Serikali kuzipelekea nishati safi ya kupikia  Shule za Sekondari 19 na Sekondari 12 za bweni zilizo Wilaya ya Nyang’wale ili kulinda mazingira,  Mhe. Kapinga amesema Wizara ya Nishati inaompango wa kuzipelekea nishati safi ya kupikia Taasisi za umma kwa kushirikiana na TAMISEMI.

Katika hatua nyingine Mhe. Kapinga amezishauri Halmashauri  kufunga mifumo ya nishati safi ya kupikia  katika Taasisi zilizopo katika Halmashauri wanazoziongoza kwa kutumia mapato ya ndani.
Posted by MROKI On Friday, May 23, 2025 No comments

May 22, 2025

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Ramadhani Kailima (kulia) akimkabidhi kadi ya mpiga kura Mkazi wa Ipagala, jijini Dodoma, Lomalisa Palahi, mwenye umri wa miaka 125, baada ya kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, Mkoani Dodoma, Mei 21, 2025. Picha na INEC
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Ramadhani Kailima (kulia) akimkabidhi kadi ya mpiga kura Mkazi wa Ipagala, jijini Dodoma, Lomalisa Palahi, mwenye umri wa miaka 125, baada ya kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, Mkoani Dodoma, Mei 21, 2025.
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Ramadhani Kailima akitoka kukagua zoezi la uandikishaji wapiga kura katika daftari la Kudumu la Wapiga Kura, awamu ya pili, Ofisi ya Serikali ya Mtaa wa Chang’ombe, Kata ya Ihumwa leo Mei 21, 2025, jijini Dodoma. Kulia ni Afisa uandikishaji Jimbo la Dodoma Mjini na Mtumba, Dickson Kimaro. 

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Ramadhani Kailima (kulia) akizungumza na Mwandishi wa zoezi la uandikishaji wapiga kura katika daftari la kudumu la wapiga kura, awamu ya pili, katika Ofisi ya Mtendaji Kilimani, jijini Dodoma, leo Mei 21, 2025.
******************
Na Mwandishi Wetu, Dodoma.
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Ndg.Ramadhani Kailima, amewataka Watanzania kuitumia siku ya kesho Mei 22, 2025 ambayo ni ya mwisho kujiandikisha katika vituo mbalimbali vya wapiga kura ili waweze kupata haki zao za kupiga kura katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu 2025.

Kailima ameyasema hayo wakati alipokuwa anatembelea vituo vya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na uwekaji wazi wa daftari la awali la wapiga kura  katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, katika Jimbo la Dodoma Mjini Mkoani Dodoma, leo Mei 21, 2025, akikagua zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya pili, akiangalia zoezi linavyoendelea kufanyika vituoni pamoja na kujua kama kuna changamoto mbalimbali katika vituo hivyo.

‘’Tume inahakikisha kuwa kila Mtanzania mwenye sifa anapata fursa ya kuandikishwa kwa usahihi bila kukosea, licha ya kuwa kuna kituo kuna mtu amekosea majina yake wakati anajiandikisha, hii ni kosa, lazima tuwe makini wakati unahakiki au kujiandikisha vituoni,’’ alisema Kailima.

Kwa upande wake Afisa Mwandikishaji wa Jimbo la Dodoma Mjini, Dickson Kimaro amesema zoezi lilikua la siku saba, kuanzia Mei 16 hadi 22, idadi ya wananchi wanaofika vituoni ni kubwa hivyo amewataka wananchi waendelee kujitokeza siku ya kesho ambapo zoezi litahitimishwa.

Naye Mwananchi aliyefika kujiandikisha katika Kituo cha Kilimani Ofisi ya Mtendaji, amesema amefanikisha kujiandikisha ikiwa ni haki yake ya msingi, na amesema Tume imejipanga vema kufanikisha wananchi wanajiankisha kwa utulivu bila usumbufu naye amefanikisha hilo.
Posted by MROKI On Thursday, May 22, 2025 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo