Na John Mapepele
Waziri wa Afya, Mohammed Mchengerwa, amesema
kuwa ushirikiano madhubuti kati ya Serikali na Washirika wa Mfuko wa Pamoja wa
Afya (Health Basket Fund) umeendelea kuwa chachu ya maboresho makubwa katika
utoaji wa huduma za afya nchini.
Akizungumza katika mkutano wa nchi washirika
wa Mfuko huo Machi 2, 2026 jijini Dar es Salaam Mhe. Mchengerwa alianza kwa
kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuiwezesha Tanzania kufikia hatua ya kufanya
majadiliano muhimu kuhusu mustakabali wa sekta ya afya. Alisisitiza kuwa pale
washirika wa sekta ya afya wanapoungana kwa uwazi, dhamira na malengo ya
pamoja, maisha ya wananchi huboreshwa kwa haraka zaidi.
“Mkutano huu si wa kawaida. Ni wakati wa
kimkakati wa kuimarisha ushirikiano na kuthibitisha upya wajibu wetu wa pamoja
wa kutoa huduma bora za afya kwa Watanzania,” alifafanua.
Mfuko wa Pamoja wa Afya Waimarisha Huduma za
Msingi nchini
Waziri Mchengerwa alieleza kuwa tangu
kuanzishwa kwa Mfuko wa Pamoja wa Afya mwaka 1999, zaidi ya dola za Marekani
bilioni 1.3 zimechangishwa kusaidia utekelezaji wa mipango ya kimkakati ya
sekta ya afya. Asilimia 90 ya fedha hizo zimeelekezwa katika huduma za Afya ya
Msingi zinazosimamiwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Alibainisha kuwa kuanzia mwaka 2017, fedha za
Mfuko zilianza kupelekwa moja kwa moja katika zaidi ya vituo 7,345 vya afya
kupitia utaratibu wa ufadhili wa moja kwa moja kwa Vituo vya Afya, hatua
iliyoongeza uwazi na ufanisi katika matumizi ya rasilimali.
“Kwa pamoja tumeimarisha upatikanaji wa dawa
na vifaa tiba muhimu, tumepunguza vifo, na kuongeza uzazi salama katika Vituo
vya Afya. Mageuzi haya yameweka msingi imara wa mfumo wa afya wenye
ustahimilivu,” alisisitiza.
Katika hatua nyingine, Mhe. Mchengerwa
alisema Tanzania ipo katika kipindi cha mageuzi makubwa, huku lengo kuu likiwa
utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote. Alifafanua kuwa wakati bima
hiyo ikipanua ulinzi wa kifedha kwa wananchi, Mfuko wa Pamoja wa Afya unabaki
kuwa mhimili wa kuhakikisha huduma bora na zenye usawa zinapatikana kwa wote.
Aidha, Waziri huyo alitoa wito kwa washirika
kuunga mkono utekelezaji wa Mkakati wa Kitaifa wa Afya Kidijitali
uliounganishwa, akisisitiza umuhimu wa kuwa na mfumo mmoja wa kitaifa
unaounganisha taarifa zote za afya.
“Huwezi kusimamia usichokiona, na huwezi
kuboresha usichokipima. Mfumo wa kidijitali uliounganishwa ni mageuzi ya
utawala, ufanisi na uaminifu,” alisema.
Akizungumzia dira ya muda mrefu, Mhe.
Mchengerwa alisema Tanzania inalenga kupunguza utegemezi mkubwa wa bidhaa za
afya kutoka nje kwa kuwekeza katika uzalishaji wa ndani wa dawa, vifaa tiba na
teknolojia za afya.
“Hili si suala la uchumi pekee, bali ni suala
la usalama wa afya ya taifa. Mfumo imara wa afya lazima uunganishe ustahimilivu
wa kifedha, kidijitali, rasilimali watu pamoja na uzalishaji na ugavi,”
alifafanua.
Waziri huyo alieleza kuwa mandhari ya
maendeleo duniani yanabadilika, huku nchi zikielekea kwenye ushirikiano wa
thamani ya pande zote na uendelevu wa muda mrefu.
“Tunaamini mustakabali wa ushirikiano
haujengwi juu ya utegemezi, bali ubunifu wa pamoja na uwekezaji. Ushirikiano
wenye busara haufiche changamoto; hujifunza kutoka kwake na hubuni mifumo bora
zaidi,” alisema.
Alikiri kuwepo kwa changamoto ya upatikanaji
wa fedha kwa wakati, akieleza kuwa Serikali inafanya kazi kwa karibu na Wizara
nyingine ikiwa ni pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI na Wizara ya Fedha ili kuondoa vikwazo vya
kiutendaji na kuimarisha uwazi katika usimamizi wa fedha.
Akizungumza
kwa niaba ya timu ya mabalozi walioshiriki katika kikao hicho,
Mheshimiwa Elke Wisch, Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia
Watoto (UNICEF) na Mratibu wa Wadau wa Mfuko wa Pamoja wa Afya alimshukuru Rais
Samia kwa kazi kubwa katika kuokoa vifo vya mama wajawazito na mtoto wakati wa
kujifungua.
Mhe. Wisch aliihakikishia Serikali ya
Tanzania kuendelea kuchangia katika sekta ya afya.
Aidha, walisifu juhudi zilizofikiwa katika kuimarisha huduma bora za afya katika
kipindi kifupi cha Serikali chini ya Rais Samia.
0 comments:
Post a Comment