Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan
ametangaza kuwa katika kuzidi kuleta ustawi kwa wafanyakazi nchini, Serikali
imefanya maamuzi ya kupandisha kima cha chini cha mishahara kwa watumishi wa
umma kwa 35.1%.
Rais Dkt. Samia ameyasema hayo leo katika viwanja vya Bombadia katika Maadhimisho
ya Sherehe za Wafanyakazi Dunia (Mei Mosi) ambazo kitaifa zimefanyika mkoani
Singida.
Aidha, Rais Dkt. Samia amesema maamuzi ya Serikali kupandisha mishahara
yamewezeshwa na kasi ya ukuaji wa uchumi kupanda hadi kufikia 5.5% kwa mwaka,
hali iliyochangiwa na wafanyakazi kujituma na kufanya kazi kwa bidii.
Aidha, kwa upande wa wafanyakazi wa sekta binafsi, Rais Dkt. Samia
amesema Bodi ya Kima cha Chini cha Mshahara inaendelea na tathmini kwa lengo la
kuboresha viwango vya mishahara kwa sekta binafsi.
Aidha, Rais Dkt. Samia amebainisha kuwa Serikali itaendelea kushirikiana
na wafanyakazi kuzifanyia kazi changamoto zinazowakabili.
“Ahadi yetu,
tutaendelea kuboresha mazingira ya wafanyakazi ikiwemo maslahi ya wafanyakazi
kwa kadiri hali itakavyoruhusu... Kujenga nchi yetu ni jukumu letu sote, hivyo
hatuna budi kuimarisha umoja na mshikamano wetu.
Ili tuweze kujenga vyema Taifa
letu ni lazima tulinde amani na utulivu nchini. Kwa namna yoyote ile, tusitoe
fursa kwa vyama vya wafanyakazi kutumika kuichafua nchi yetu. Historia ya vyama
vya wafanyakazi ni vyama vilivyoleta vuguvugu la uhuru wetu, tusitumike
kusaliti uhuru wetu.” amesisitiza Rais Dkt. Samia.
Rais Dkt. Samia amepongeza Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania
(TUCTA) kwa namna kinavyolinda maslahi ya wafanyakazi kwa weledi kupitia
mazungumzo ya utatu ya Serikali, mfanyakazi na mwajiri na ameitaka TUCTA
kuimarisha mifumo ya utatuzi wa migogoro baina ya vyama vilivyopo kwenye
shirikisho.
Kuhusu Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani kwa mwaka huu, Rais
Dkt. Samia ameeleza haja ya wafanyakazi kutumia haki yao ya kikatiba ya
kushiriki uchaguzi na kuwachagua viongozi bora watakaolinda na kutetea maslahi
yao.
0 comments:
Post a Comment