October 12, 2023

SAGCOT SAIDIENI KUTIMIZA NDOTO YA SAMIA KULISHA AFRIKA IFIKAPO 2030

Mkuu wa Mkoa wa Njombe Antony Mtaka akisisitiza jambo kwa wadau wa kilimo katika  mikoa ya nyanda za juu kusini mwa Tanzania pamoja na mambo mengine amewahimiza  kuwa karibu sana na Kituo cha Kuendeleza Kilimo Nyanda za Juu Kusini mwa Tanzania (SAGCOT) ili mikakati ya kuzalisha mazao ya kilimo na biashara itekelezwe kwa ufanisi na ndoto ya Rais Samia Hassan ya Tanzania kulilisha Bara la Afrika 

Na Mwandishi Wetu,  Njombe
Wadau wa kilimo katika  mikoa ya nyanda za juu kusini mwa Tanzania wamehimizwa  kuwa karibu sana na Kituo cha Kuendeleza Kilimo Nyanda za Juu Kusini mwa Tanzania (SAGCOT) ili mikakati ya kuzalisha mazao ya kilimo na biashara itekelezwe kwa ufanisi na ndoto ya Rais Samia Hassan ya Tanzania kulilisha Bara la Afrika itimie.
 
SAGCOT ndiyo taasisi inayotambua  wadau wa kilimo katika ushoroba wa kusini mwa Tanzania na kuratibu ushirikiano baina yao ili uzalishaji  wa mazao ya kilimo na biashara uwe wenye tija na kuboresha maisha ya wakulima wadogo kwa kutumia sayansi na teknolojia katika kulima mazao.
 
Akiongea katika mkutano wa siku mbili wa wadau wa kilimo kutoka taasisi za sekta binafsi na umma zilizomo katika Kongani ya Ihemi,  Mkuu wa Mkoa wa Njombe Antony Mtaka amewataka wadau hao kushirikiana na SAGCOT katika kuhamasisha wakulima kuzalisha kwa wingi mazao ya chakula na biashara ili ziada ya mazao ya chakula iwe  kubwa  na  ilishe Bara la Afrika ifikiapo 2030.  Aidha ameishauri SAGCOT ielewe ndoto ya Rais Samia kwani ina uzoefu mkubwa katika kuwaingiza Watanzania katika kilimo.
 
Mtaka alisema  kuzalisha ziada kubwa ya chakula kwa kutumia mikakati iliyo, ikiwemo utoaji wa mbolea ya ruzuku,  ni dhamira ya serikali ya kulisha Afrika ifikapo 2030. “Kulisha Afrika ni ndoto ya Rais Samia na ni dhamira ya serikali anayoiongoiza,” alisema, na kuongeza kuwa dhamira ya serikali inaonekana kwa kuwawezesha wakulima kwa kutumia mikakati mbalimbali ikiwemo utoaji wa mbolea za ruzuku.
 
‘’Political will (dhamira ya kisiasa) sasa hivi ya kukuza kilimo ni ya rais mwenyewe na ni kubwa mno. Mnaona ameishasema visima eflu 68 vichimbwe kwabajili ya umwagiliaji lakini pia mabwawa yachimbwe; na pesa zimeisha tolewa kwa ajili kuanza uchimbaji.  Haya ni matamanio makubwa ya kiongozi wa nchi na sisi SAGCOT ni lazima tumulewe vizuri Rais, tusaidie matamanio haya kufikiwa,’’alieleza Mtaka. 
 
 
Alisema SAGCOT wamesaidia watu wengi kuingia katika shughuli za kilimo na kwamba kuongezeka kwa uzalishaji wa maparachichi na viazi mviringo ni ushahidi wa kuongezeka kwa uzalishaji  tangu SAGCOT walipoanza kuwahudumia wakulima mwaka 2015.
 
 
Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wadau hao kutafuta  majawabu ya changamoto zilizopo kwenye sekta za kilimo na ufugaji na kusema dhamira ya kukuza kilimo  inajitokeza katika kuwawezeha wakulima kuhusu mbolea, uchimbaji wa visima na utengenezaji wa mabwawa ya kumwagilia mazao na mradi wa Jenga Kesho iliyo Bora (BBT).  BBT inawalenga vijana wengi ili wazalishe kisasa  na kupunguza changamoto ya ajira kwa vijana.
 
Aidha amewataka viongozi kuunganisha taasisi binafsi nawakulima na viongozi wa serikali  kuhamasisha shughuli za kilimo.
 
‘’Zamani wakilima walikua wanapata gunia 40 za viazi mbatata.  Lakini sasa watu wanavuna mpaka gunia 200. Hii ni kazi nzuri  inayofanywa na ninyi wenzetu Sagcot. Hii ni tija kubwa na hongereni, ’’alisema Mtaka
 
Awali Mkuu wa Maendeleo ya Kongani na Ubia wa SAGCOT, Bi Maria Ijumba akiwasilisha taarifa ya makubaliano yaliyofanyIka mwaka 2022 alisema kuwa ndani ya mwaka mmoja limekuweko ongezeko kubwa katika nyanja za ajira, uzalishaji na uwekezaji, na kuwa sekta ya kilimo imesaidia kundi kubwa la Watanzania wameshinda  umasikini baada ya kuingia kwenye kilimo na ufugaji.
 
Amesema tathimini ya mwaka 2022 inaonyesha kuwa wakulima wadogo wa mazao ya biashara wameongezeka mara 8 kutoka laki moja mpaka kufikia  847,385.

No comments:

Post a Comment