Nafasi Ya Matangazo

September 20, 2016



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ametuma salamu za rambirambi kwa familia zilipatwa na msiba kufuatia ajali ya basi la Kampuni ya New Force iliyotokea jana tarehe 19 Septemba, 2016 majira ya saa 2:00 Usiku katika Kijiji cha Lilombwi, Kata ya Kifanya, Tarafa ya Igominyi Mkoani Njombe ambapo watu 12 wamepoteza maisha na wengine 28 kujeruhiwa.

Basi hilo limepinduka katika kona ya barabara wakati likisafiri kutoka Dar es Salaam kwenda Songea Mkoani Ruvuma.

Katika salamu hizo kupitia kwa Mkuu wa Mkoa wa Njombe Dkt. Rehema Nchimbi, Rais Magufuli amesema amepokea taarifa za ajali hiyo kwa masikitiko makubwa na kwamba anaungana na familia, ndugu, jamaa na marafiki wote waliopatwa na msiba katika kipindi kigumu cha majonzi.

"Ndugu Mkuu wa Mkoa wa Njombe Dkt. Rehema Nchimbi naomba unifikishie pole nyingi kwa wote walipatwa na msiba, wamewapoteza wapendwa wao, wamewapoteza watu waliowategemea na hakika familia zimetikisika.

"Sote tuwaombee wote waliofikwa na msiba wawe na moyo wa subira, uvumilivu na ustahimilivu na pia tuwaombee Marehemu wote wapumzishwe mahali pema peponi, Amina" Amesema Rais Magufuli. 

Rais Magufuli pia amewapa pole majeruhi wote na amewaombea wapone haraka ili waweze kuungana na familia zao na kuendelea na shughuli zao za kila siku.
Posted by MROKI On Tuesday, September 20, 2016 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo