Nafasi Ya Matangazo

April 02, 2012

WABUNGE wawili wa Chadema wamejeruhiwa vibaya kwa mapanga na mashoka huko Mwanza katika tukio lililotokea saa nane usiku katika eneo la Ibanda Kabuhoro baada ya kuvamiwa na watu wanaosadikiwa kuwa ni wafuasi wa CCM usiku wa kuamkia uchaguzi wa diwani Kata ya Kirumba.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow alisema jana kwamba mbali na wabunge hao, Samson Highness Kiwia wa Ilemela na Salvatory Machemuli wa Ukerewe, wengine walioshambuliwa ni pamoja na Ahmed Waziri ambaye inasemekana kuwa ni kada wa UVCCM aliyekatwa kiganja chake cha mkono wa kulia.

Wengine ni Haji Mkweda (21), ambaye alijeruhiwa mguu wa kulia, Judhith Madaraka (26), aliyechomwa kisu kwenye titi lake la kushoto na mkono wa kushoto, Ivory Mchimba (26), aliyejeruhiwa kichwani na mdomoni. Majeruhi wote ukiondoa wabunge hao na Waziri, wamelazwa katika Hospitali ya Mkoa ya Sekou Toure.

Majeraha aliyopata kichwani mh.Highness

Awali, wabunge hao walilazwa katika Hospitali ya Rafaa Bugando lakini baadaye walisafirishwa kwa ndege kupelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Dar es Salaam. Kwa upande wake, Waziri amelazwa Bugando.

Mbali ya Mwanza, katika uchaguzi mwingine wa udiwani Kata ya Kiwira, Mbeya nako damu ilimwagika baada ya watu kadhaa kushambuliwa kwa mapanga na nodo. Katika tukio hilo polisi imewatia mbaroni watu 10.

Kamanda Barlow alisema katika vurugu hizo magari matatu likiwemo la Kiwia yaliharibiwa.

Alisema polisi ilipata mapema taarifa za tukio hilo lakini ilichelewa kufika kutokana na eneo hilo kuwa lenye mawe na milima hivyo kufika wakati tayari wabunge wameshajeruhiwa vibaya na mali hizo kuharibiwa.

“Kiwia alionekana kushambuliwa kichwani na kitu chenye ncha kali na magari nayo yakiwa yameharibiwa vibaya. Kwa mazingira hayo ya usiku na hali ilivyotokea, jeshi langu linafanya uchunguzi wa kina kuweza kujua kiini cha vurugu hizo, lakini tumewaelekeza wenzetu wa Takukuru kufuatilia kujua kama mazingira ya wabunge hao kutembea usiku huo yalikuwa na uhusiano wowote na masuala ya rushwa,” alisema.

Bunge latoa tamko
Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai alithibitisha taarifa za kuvamiwa kwa wabunge hao na kusema wamepelekwa Dar es Salaam kwa matibabu zaidi.

Ndugai alisema utaratibu ulivyo ni kwamba mbunge yeyote akiumia, Bunge ndilo linaloshughulikia matibabu yake na ni katika hospitali za Serikali tu.

“Nimepata taarifa hizo na tumetuma timu yetu ya Bunge kwenda kushughulika suala hilo. Mara ya kwanza nilisikia ni mbunge mmoja tu ndiye aliyepelekwa Dar es Salaam, lakini baadaye nikaambiwa ni wote wawili hivyo tunafuatilia kujua hali zao,” alisema Ndugai

Soma zaidi katika Chanzo cha habari hii hapa>>>> MWANANCHI
Posted by MROKI On Monday, April 02, 2012 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo