September 16, 2026

WATUMISHI 328 WAPYA TFS WAPATIWA MISINGI YA UTUMISHI BORA

Naibu Kamishna wa Uhifadhi anayesimamia Kurugenzi ya Huduma Saidizi na Utawala katika Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), DCC Emmanuel Wilfred Kiboko akitoa mada. 
Naibu Kamishna wa Uhifadhi anayesimamia Kurugenzi ya Huduma Saidizi na Utawala katika Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), DCC Emmanuel Wilfred Kiboko, amewaonya watumishi wapya 328 kutokuondoka katika vituo vyao vya kazi bila kufuata utaratibu, akisema kufanya hivyo kunaweza kusababisha kuchukuliwa hatua za kinidhamu.
 
DCC Kiboko ametoa kauli hiyo leo, Jumanne, Septemba 15, 2026, wakati akiwasilisha mada katika siku ya pili ya programu ya mafunzo elekezi kwa watumishi hao inayofanyika Dodoma. 

Amesema baada ya kukabidhiwa barua za ajira, watumishi hao wanatakiwa kuripoti katika vituo vyao vya kazi ndani ya siku saba, huku wakuu wa vituo wakitakiwa kuthibitisha kuripoti kwao na kuwapatia majukumu.
 
“Ukiondoka kwenye kituo cha kazi kwa utaratibu wowote ule, ina maana utapaswa kuchukuliwa hatua za kinidhamu kwa utoro kazini,” amesema DCC Kiboko, akiwataka watumishi hao kuchukulia kwa uzito masharti ya ajira na taratibu za utumishi wa umma.
 
Amesema pia watumishi hao hawataruhusiwa kuondoka vituoni kwenda kumalizia masomo bila kufuata taratibu na kupata kibali cha Kamishna wa Uhifadhi. Amesema TFS imebaini baadhi ya wakuu wa vituo wamekuwa wakiwaruhusu watumishi kwenda kumalizia masomo kinyume na taratibu, na kuwa hatua zinaweza kuwahusu viongozi watakaofanya hivyo bila kibali.
 
Akizungumzia mafunzo na maendeleo ya kielimu, DCC Kiboko amesema TFS hutumia Training Needs Assessment (TNA) kubaini maeneo ambayo taasisi inahitaji kuwekeza katika mafunzo, huku Training Programme ikibainisha mahitaji ya kila mtumishi na muda wa mafunzo kulingana na mahitaji ya taasisi na uwezo wa bajeti.
 
Amesema ajira za watumishi hao 328 zinalenga kuongeza nguvu kazi katika maeneo ya utekelezaji wa majukumu ya TFS, hivyo watumishi wanapaswa kutimiza wajibu wao katika vituo walivyopangiwa ili kufikia matarajio ya Serikali ya kuongeza ufanisi na mapato.
 
Aidha, amewataka watumishi hao kujiunga na vyama vya kitaaluma vinavyohusiana na kada zao, akitolea mfano Tanzania Association of Foresters (TAF) kwa wataalamu wa misitu, huku akisisitiza kuwa utumishi wa umma ni safari inayoendelea inayohitaji kujifunza na kukumbushana kuhusu maadili kila siku.
 
Akihitimisha, DCC Kiboko amewataka watumishi hao kuzingatia nidhamu, uadilifu na taratibu za utumishi, akisisitiza kuwa wanapaswa kulinda heshima ya TFS, Utumishi wa Umma, wao wenyewe na familia zao katika kipindi chote cha utumishi wao.





No comments:

Post a Comment