October 19, 2023

DODOMA YAENDELEA NA JITIHADA ZA KUTOKOMEZA MIGOGORO YA ARDHI

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe.Rosemary Senyamule   amesema Serikali ya Mkoa  wa Dodoma inaendelea na jitihada mbalimbali za kuhakikisha inatokomeza migogoro ya ardhi ambapo Jiji la Dodoma limeanzisha kliniki ya kutatua migogoro hiyo.





Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe.Rosemary Senyamule   amesema Serikali ya Mkoa  wa Dodoma inaendelea na jitihada mbalimbali za kuhakikisha inatokomeza migogoro ya ardhi ambapo Jiji la Dodoma limeanzisha kliniki ya kutatua migogoro hiyo, kusikiliza kero na malalamiko ya wananchi kuhusu ardhi pamoja na kuwapatia hati zao wale wote wanaokidhi vigezo vinavyohitajika.

 Ameyasema hayo Oktoba 19,2023 wakati wa ziara yake ya kikazi katika Kata  ya Ihumwa  jijini Dodoma ikiwa na dhamira ya kusikiliza na kuzitatua kero mbalimbali za wananchi pamoja na kuwaeleza wananchi Mambo  mbalimbali yanayofanywa na kutekelezwa na Serikali.

Aidha,  Mhe. Senyamule ametumia fursa hiyo kuwahimiza wakazi wa Kata hiyo  kutumia fursa ya miradi ya kimkakati inayotekelezwa na serikali ikiwemo  reli ya kisasa (SGR) pamoja na Barabara ya Mzunguko ( Ringroad) kama fursa ya kujiongezea na kujipatia vipato vya kukidhi mahitaji yao  ya kila siku.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mhe.Jabir Shekimweri amesema hali ya usalama katika maeneo ya kata hiyo kwa sasa ni  shwari ukilinganisha na hapo awali pia amebainisha vyanzo vya matukio ya kiuhalifu katika Kata hiyo kuwa ni pamoja na visasi  baina ya ndugu, wivu wa kimapenzi pamoja na wananchi kujichukulia Sheria Mikononi.

Naye, Diwani wa Kata hiyo Bw.Edward Magawa  amesema, kwa sasa wameshaanza Ujenzi wa kituo cha polisi ili kuhakikisha hali ya ulinzi na usalama inaendelea kuimarika na kuepukana na vitendo vya kiuhalifu vinavyojitokeza mara kwa mara katika maeneo yao.

No comments:

Post a Comment