Nafasi Ya Matangazo

January 26, 2018

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Wizara hiyo Mjini Dodoma leo. Kulia kwake ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk. Aloyce Nzuki.
**************
Na Hamza Temba - Dodoma
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla leo Januari 25, 2018 mjini Dodoma ametaja majina ya watuhumiwa wa ujangili ambao wengi wao ni wamiliki na washirika wa Kampuni za uwindaji wa kitalii na kuwapa siku saba wawe wamefika kwa hiari yao wenyewe katika ofisi za Wizara hiyo Mjini Dodoma, Swagaswaga House kwa ajili kutoa maelezo kwanini wasichukuliwe hatua za kisheria ikiwemo kujibu tuhuma hiyo na nyingine nyingi zinazowakabili mbele ya kamati atakayoiunda.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, Dk. Kigwangalla ametaja baadhi ya tuhuma hizo ambazo ziko kinyume cha sheria na taratibu za uwindaji wa kitalii kuwa ni uwindaji haramu, uhawilishaji wa umiliki wa vitalu vya uwindaji pasipo kufuata sheria, udanganyifu kwenye kujaza fomu za uangalizi,  rushwa, uhalifu dhidi ya rasilimali za wanyamapori na uhujumu uchumi.

Alitaja tuhuma zingine kuwa ni ukiukwaji wa kanuni za uwindaji (kupiga wanyama usiku, kuwinda wanyama bila kujali umri, kupiga wanyama nje ya maeneo waliyopewa), kukutolipa tozo mbalimbali za maendeleo za jamii kwenye vijiji jirani na maeneo wanaoendesha biashara ya uwindaji, kushindwa kuendesha ipasavyo shughuli za kuzuia ujangili.

Dk. Kigwangalla aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni ndugu Pasanis na wenzake ambao wanamilikia kampuni ya Berlette Safari Corporation Ltd na Ngugu Shein Ralgi na wakurugenzi wenzake wa kampuni ya Game Frontiers of Tanzania Ltd.

Wengine ni Ndugu Howel na wakurugenzi wenzake wa kampuni ya Mkwawa Hunting Sfaris Tanzania Ltd, Ndugu Thomas Fredikin na wenzake wa Kampuni ya Mwiba Holdings Ltd, Wengert Windrose Safaris Tanzania  Ltd na Tanzania Game Trackers Safaris Ltd, na Ndugu Awadh na wenzake ambao wanamiliki kampuni ya Uwindaji wa Greenmiles Safaris Ltd.

Aliwataja washirika wengine kuwa ni Ndugu ni Kwizema, Ndugu Robert, Ndugu Solomon Makulu, Ndugu Siasa Shaban, Ndugu Hamis Abdul Ligagabile na mtumishi wa Wizara Wizara ya Maliasili na Utalii, Alex Aguma.

Katika hatua nyingine Dk. Kigwangalla ametoa Ilani ya siku 30 kwa watu mbalimbali ikiwemo Mawaziri Wakuu Wastaafu waliovamia kiwanja chenye hati namba 4091 kilichopo Njiro Jijini Arusha wafike kwa Kamishna Mkuu wa Ardhi waweze kuhakikiwa na kuthibitisha umiliki wao halali ama sivyo wavirejeshe Serikalini viweze kumilikishwa kwa mmiliki wake halali.

“Natoa ilani ya siku 30 kwa mtu yeyote ambaye anajua alivamia kiwanja katika eneo hili ambalo lina hati namba 4091 kilichopo Njiro, Arusha, haraka sana ajipange kupeleka taarifa zake mbele ya Kamishna wa Ardhi kabla hatujachukua hatua nyingine za kisheria, hati iliyoko pale ipo katika jina la Bodi ya Utalii Tanzania japo wao wanadai wana hati nyingine.

“Wengi wao wamejenga nyumba za kudumu katika eneo lile, na wengine ni viongozi waliokuwa mawaziri wakuu wastaafu nao wana viwanja katika eneo hilo na wamejenga nyumba zao katika eneo hilo,” alisema Dk. Kigwangalla.

Alisema kiwanja hicho kilichokuwa na ekari zaidi ya 40 kilikuwa kinamilikiwa na taasisi ya Serikali ambayo ni kampuni tanzu ya Bodi ya Utalii Tanzania iliyokuwa inajulikana kama Serengeti Safari Lodges na baadae kikauzwa kwa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro.

Wakati huo huo, Dk. Kigwangalla ametoa siku saba kwa Jeshi la Polisi nchini kuchukua hatua dhidi ya watuhumiwa wanne wanaojihusisha na mtandao wa ujangili pamoja na kupanga njama zilizopelekea mauaji ya Mhifadhi wa Wanyamapori Ndugu Wayne Lotter, raia wa Afrika ya Kusini ambaye alikuwa Mkurugenzi wa Kampuni Pams Foundation, aliyeuawawa eneo la Chole Masaki Jijini Dar es Salaam mwezi Agosti mwaka jana.

“Natoa siku saba kwa wenzetu wa jeshi la Polisi wachukue hatua dhidi ya watu wanne, ambao mimi majina yao ninayafahamu ambao miongoni mwao watatu wanahusika na kuendesha biashara ya ujangili, na ni watu wakubwa, ni matajiri wakubwa na wana mitandao mikubwa ya ujangili.

“Ninafahamu taarifa hizi polisi wanazo lakini hawajachukua hatua za kuwakamata watu hawa na kuwafikisha kwenye macho ya sheria, muda ni mrefu  na sisi wenye taarifa hizi sasa tumeanza kuchoka kusubiri.

“Hawa watu wanne walihusika kupanga njama ambazo zilipelekea kusababisha mauaji ya kikatili ya Mkurugenzi wa Kampuni ya Palm Foundation, Ndugu Wayle Lotter mwezi Agosti mwaka jana eneo la Chole Masaki mwezi Agosti mwaka jana.

“Nataka ndani ya siku hizi saba wawe wamechukua hatua na kama hawatochukua hatua manaake tutajua wana vested interest (maslahi) kwahivo tutaenda kuripoti kwa Amiri Jeshi mkuu ambaye ni Mhe. Rais aliyetutuma kazi ya kusimamia sekta hii,”. Alisema Dk. Kigwangalla.
 Dk. Kigwangalla akizungumza katika mkutano huo leo mjini Dodoma.
Posted by MROKI On Friday, January 26, 2018 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo