Nafasi Ya Matangazo

January 27, 2017

 Meneja Mifumo ya Kielektroniki ya  Forodha kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)  Bw. Tinkasimile Felix (kushoto) akipokea tuzo ya ubunifu wamfumo wa TANCIS kutoka kwa Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Nchi na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Mindi Kasiga. Mfumo huu wa TANCIA umeundwa kwa kuzingatia kanuni za hali ya juu za kiteknolojia kwa lengo la kuongeza ufanisi, uharaka, uwazi na uhakika katika usimamizi wa masuala ya forodha.
 *****************
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imepata tuzo kutoka Umoja wa Afrika (AU) kutokana na mfumo wa Uondoaji Mizigo Bandarini (TANCIS) ambao unafanya kazi kwa ufanisi na uharaka zaidi pamoja na kudhibiti mianya ya rushwa.

Tuzo hiyo imetolewa na Umoja wa Nchi za Afrika jijini Addis Ababa Ethiopia,   baada ya kufanyika shindano la Taasisi za Serikali za Umoja wa Nchi hizo kutokana na kuboresha mifumo ya utendaji kazi katika taasisi zao.

Akizungumza kwa niaba ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Mindi Kisiga amesema kuwa TRA na Mamlaka ya Usimamizi wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) ndiyo taasisi pekee za Serikali zilizoweza kufanya vizuri katika ubunifu katika utendaji wa taasisi hizo.

“Tuzo hizi zinatolewa na nchi za Umoja wa Afrika kwa taasisi za Serikali ambapo hushindanishwa katika masuala ya ubunifu katika utendaji kazi wa taasisi husika,” alisema Bi. Mindi.

Akizungumza kwa niaba ya Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Alphayo Kidata,  Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi toka Mamlaka ya Mapato Tanzania Bw. Richard Kayombo alisema TRA imeshinda tuzo hiyo kutokana na ubunifu wa mfumo wa TANCIS ambao umeundwa kwa kuzingatia kanuni za hali ya juu za kiteknolojia kwa lengo la kuongeza ufanisi, uharaka, uwazi na uhakika katika usimamizi wa masuala ya forodha. 

Alisema mfumo huu umeunganishwa na mifumo mingine ya TRA na ya wadau muhimu ambao wanahusika katika uondoshaji wa bidhaa katika udhibiti wa forodha .

“Mfumo wa TANCIS humwezesha mwagizaji wa bidhaa kufuatilia hatua iliyofikiwa  katika kuondosha bidhaa zake kwa kutumia simu ya kiganjani au kifaa kingine chochote cha kielektroniki hivyo mfumo huu unarahisisha utoaji huduma na kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato,” alisema Bw. Kayombo.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano toka Mamlaka ya Udhibiti wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) Bi. Sarah Kibonde alisema kuwa taasisi yake imepokea tuzo hiyo  ya ubunifu kwa kupitia mfumo wa kanzidata ya Taifa ya Sekta ya Hifadhi ya Jamii.

Alisema TRA iliwawezesha kupata taarifa zilizohusu walipajikodi wa (PAYE) ambazo zilifanikisha uchambuzi wa waajiri wasiochangia Mifuko ya Jamii.

TRA na SSRA wameahidi kuendelea na ubunifu zaidi ili kuhakikisha wanaendelea kubaki katika nafasi ya ushindi na kufanya vizuri zaidi katika mashindano yajayo.
Posted by MROKI On Friday, January 27, 2017 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo