Nafasi Ya Matangazo

November 09, 2016



MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imeanzisha vituo vinavyohama katika jitihada za kukabiliana na msongamano wa wananchi wanao hakiki na kuboresha taarifa za Namba ya Utambulisho wa Mlipakodi (TIN) katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Pamoja na kutumia vituo vinavyohama, TRA pia inaendelea kuongeza idadi ya vituo na vifaa vya utendaji ili kuhakikisha wananchi ambao hawajahakiki na kuboresha taarifa zao wanafanya hivyo kabla ya tarehe ya mwisho ya uhakiki ambayo ni 30 Novemba 2016 

Kituo kimojawapo kilichoongezwa ni cha Kimara Mwisho ambapo pamoja na kufanya shughuli za uhakiki kituo cha Ofisi ya Kimara ambacho kimefunguliwa rasmi hivi karibuni kitatoa huduma zingine za kodi ikiwa ni pamoja na usajili wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), malipo ya kodi za magari, malipo ya kodi za mapato ikiwemo Kodi za Kampuni, kodi za watu binafsi, kodi za mishahara, kodi za uendelezaji ufundi stadi na ushuru wa stempu.

TRA inawasihi wananchi wanaohakiki taarifa zao kuwa makini kwani TRA imebaini kuibuka wananchi wasiowaaminifu ‘vishoka’ ambao wanatumia mwanya wa msongamano wa wanachi katika vituo vya uhakiki kuwalaghai na kusababisha usumbufu usio wa lazima. 

Katika kuhakikisha kuwa wafanyabiashara wanatendewa haki wanapopata huduma TRA hasa wakati wa makadirio, TRA inawaasa kutambua kwamba wanayo haki ya msingi kukata rufaa katika ngazi mbalimbali kwa kuanzia na Meneja wa Mkoa husika au kwa Kamishna kutegemea na aina ya kodi na hatimaye kwa Kamishna Mkuu endapo wataona haki haijatendeka.

Katika hatua nyingine TRA  imeendelea na jukumu la ukusanyaji wa mapato ambapo imekusanya jumla ya shilingi Trilioni  1.150 kipindi cha mwezi Oktoba 2016 na kufanya makusanyo yote ambayo TRA imekusanya kwa mwaka wa fedha 2016/17 kufikia shilingi Trilioni 4.752 hadi sasa.

Pamoja na mafanikio hayo ya makusanyo ya kodi TRA pia imepata mafanikio katika rufaa za kesi zinazowasilishwa kwa uamuzi zaidi katika baraza ra Rufani za kodi katika kipindi cha mwezi Oktoba baada ya kushinda kesi tisa zenye thamani ya kodi ya shilingi billioni 16.941.
 
Jumla ya kesi 27 zinazohusu masuala mbalimbali ya kodi ziliwasilishwa katika Baraza la Rufani za Kodi kwa uamuzi ambapo kesi kumi zimeamuliwa na kati ya hizo ni kesi moja tu ambayo mlipakodi alishinda. Kesi nyingine bado zinaendelea kusikilizwa.

Ushindi huu wa kesi unadhihirisha jinsi TRA inavyofanya makadirio ya kodi kwa umakini haki na weledi bila kumuonea mtu yeyote.

‘Pamoja Tunajenga Taifa Letu’
 
Richard M. Kayombo
MKURUGENZI HUDUMA NA ELIMU KWA MLIPAKODI
Posted by MROKI On Wednesday, November 09, 2016 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo